MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)0%

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S) Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Imam Husein (A.S)

  • Anza
  • Iliyopita
  • 7 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 8297 / Pakua: 1957
Kiwango Kiwango Kiwango
MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

Mwandishi:
Swahili

2

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN(A.S)

MAJLISI YA TISA

IMAM HUSEIN(A.S) AAZIMIA SAFARI YA IRAQ

Imam Husein (a.s.) alipoazimia kwenda Iraq alisimama akatoa hatuba akasema; "Hamu yangu ya kukutana na wazazi na ndugu zangu waliotangulia (kufariki) ni kama shauku aliyokuwa nayo Yaaqub kwa mwanawe Yusuf (alipopotea) na kifo kitakchonifika kwangu ni jambo bora, kwani naona viungo vya mwili wangu vitakatwakatwa na maadui zangu hapo katika jangwa lililo baina ya Nawasiisi na Karbala.

Wakisha kinuia, lengo lao litakuwa limetimia na hamu yao dhidi yangu itakamilika. Hakuna njia ya kuwepa siku ambayo imekwisha kuandikwa. Alitakalo Mwenyezi Mungu liwe, kwetu sisi watu wa nyumba ya Mtume huwa tumeridhia pia liwe. Jamii ya Mtume wa Mwenyezi Mungu haitatenganishwa naye, bali itakusanywa iwe pamoja naye kesho Akhera mahali patukufu.

Mtume atawakaribisha jamii yake kwa wema na furaha na atawatimizia yote aliyowaahidi. Fahamuni enyi watu ya kwamba, ye yote atakayejitolea roho yake kwa ajili yetu, na akawa amejiandaa kukutana na Mwenyezi Mungu kwa wema, basi na asafiri pamoja nasi, kwani nitaondoka asubuhi pindi apendapo Mwenyezi Mungu Mtukufu."

Usiku wa kuamkia safari, alikuja Muhammad Al-Hanafiyyah ambaye ni mdogo wa Imam Husein (kwa mama mwingine) akamwambia Imam Husein(a.s) "Ewe ndugu yangu bila shaka watu wa Al-Kufah ndiyo wao ambao wewe unafahamu khiyana waliyomfanyia baba yako na nduguyo (Hasan a.s.), nami nachelea kwamba yatakufika yaliyowafika waliokutangulia, basi iwapo utaona ni vema bora ubakie hapa Makkah, kwani wewe ni kiumbe bora mno katika Haram hii ya Makkah nawe ndiyo mlinzi wake".

Imam(a.s) akajibu kwa kusema "Ewe ndugu yangu hakika nachelea Yazid asije ndani ya eneo hili takatifu, nami nikawa ndiyo kiumbe wa kwanza kuhusishwa na uvunjwaji wa heshima ya nyumba hii."

Muhammad AI-Hanafiyya akasema, "Basi ikiwa unachelea hilo, nenda Yemen au sehemu nyingine za nchi, kwani huko utapata hifadhi wala hakuna atakayeweza tena kukusbambulia ukiwa huko".

Imam Husein akasema, "Nitaitafakari rai yako". Kulipokucha alfajiri mapema, Imam Husein(a.s) alifungasha akaondoka.

Khabari zikamfikia Muhammad Al-Hanafiyya kwamba Imam Husein(a.s) ameondoka, akamfuatia, na alipompata akazishika hatamu za ngamia aliyekuwa kapanda Imam Husein(a.s) kisha akasema, "Ewe ndugu yangu hukuniahidi kwamba utalitafakari ombi langu?"

Imam akasema, "Bila shaka nilikuahidi".

Muhammad Al-Hanafiyyah akasema, "Basi jambo gani limekufanya utoke haraka namna hii?"

Imam akajibu, "Ulipoondoka Mtume wa Mwenyezi Mungu alinijia akaniambia, "Ewe Husein toka (wende Iraq) bila shaka Mwenyezi Mungu amekwisha taka kukuona wewe umeuawa".

Akasema Muhammad Al-Hanafiyya, "Hakika sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na bila shaka kwake tutarejea, lakini nini maana yako kuwachukuwa wanawake hawa pamoja nawe ikiwa hali yenyewe ndiyo hii uliyoniambia?"

Imam akajibu "Mtume ameniambia kwamba Mwenyezi Mungu amekwisha kutaka vile vile kuwaona wakiwa ni mateka".

Kadhalika kabla Imam(a.s) hajatoka kuelekea Iraq, alikutana na Mabwana Abu Muhammad Ar-Raaqdiy na Zurarah bin Khalaj, na walimjulisha udhaifu wa watu wa Al-Kufah, na kwamba nyoyo zao ziko pamoja naye na wakati huo huo panga zao ziko juu ya shingo yake.

Imam Husein (a.s.) alinyoosha mkono wake juu mbinguni, ikafunguliwa milango ya mbingu na wakateremka malaika wengi mno, idadi yao aijuaye ni Mwenyezi Mungu kisha akasema, "Lau isingekuwa vitu viko karibu karibu na kama muda wa kifo changu ungekuwa bado Wallahi ningepigana na maadui zangu kwa jeshi na Malaika hawa, lakini nafahamu wazi kabisa kwamba huko niendako ndiko kwenye kifo changu na vifo vya wafuasi wangu, hataokoka yeyote isipokuwa Mwanangu".(Ali bin Husein Zainul-Abidina(a.s) .

Imam Husein(a.s) akawa ameondoka Makkah siku ya Jumanne tarehe nane mfungo tatu mwaka wa sitini. A.H.

Amesema Bwana Maamar katika kitabu kiitwacho "Maqtalul- Husain) kwamba: Ilipokuwa siku ya nane mfungo tatu, Omar bin Saad bin Abi Waqas alifika Makkah akiwa na idadi kubwa ya askari ili kumshambulia Imam Husein hapo Makkah kutokana na amri ya Yazid, na ikiwezekana amuuwe kabisa.

Kumbe Imam naye akawa ametoka siku hiyo hiyo ya tarehe nane mfungo tatu, kwani hakuweza kukamilisha Hija yake kwa kuchelea kuuwa kwake hapo Makkah na itakuwa heshima ya nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu imevunjwa, akafungua Ihram yake na akaifanya kuwa ni Umra "Mufradah".

Imepokewa kutoka kwa Imam Jaafar As-Sadiq(a.s) katika mapokezi ya Sheikh Mufid amesema, "Alipoondoka Imam Husein(a.s) Makkah kwenda Iraq, alikutana na makundi ya malaika waliokuwa na mikuki wamepanda ngamia wakamtolea salamu na wakasema, "Ewe uliye muongozo wa Mwenyezi Mungu kwa viumbe wake baada ya Babu yako na Baba yako na nduguyo, bila shaka Mwenyezi Mungu alimsaidia Babu yako kwa kututumia sisi mahala pengi, na hapana shaka Mwenyezi Mungu amekupa msaada wewe kwa kupitia kwetu".

Imam(a.s) akawaambia, "Makutano yawe katika uwanja wa kaburi langu, mahali ambapo nitapata shahada (nitauwa) napo ni Kar-bala, basi nikishafika hapo njooni ".

Wale Malaika wakamjibu wakasema, "Ewe uliye muongozo utokao kwa Mwenyezi Mungu, hakika Mwenyezi Mungu ametuamuru kukusikiliza na kukutii, je unayo khofu kutokana na adui kwamba atakutana nawe (njiani) ili tuwe nawe pamoja (tukusaidie)"?

Imam Husein(a.s) akasema, "Hawana uwezo kama huo juu yangu, na wala hawatanifanya lolote la ubaya mpaka nifike kwenye kiwanja changu".

Pia walimjia Imam(a.s) makundi ya majini waumini wakamwambia, "Ewe kiongozi wetu sisi ni wafuasi wako na ni wasaidizi wako, tuamuru chochote ukitakacho (tutakufanyia), na lau utatuamuru kumuuwa adui yako nawe ukiwa hapo ulipo tutakutelezea jambo hilo".

Imam Husein(a.s) akawajibu akasema, "Je hamujasoma kitabu cha Mwenyezi Mungu kilichoteremshwa kwa Babu yangu Mtume wa Allah pale aliposema Mwenyezi Mungu, "Waambie hata kama mngelikuwa majumbani mwenu, wangelitoka wale ambao wameandikiwa kufa wakaenda mahali pao pa kuangukia kifo". Kwa hiyo ikiwa mimi nitabaki hapa basi kwa kitu gani atatahiniwa mja huyu muovu, na ni kwa jambo lipi watu hawa (waovu) watajaribiwa, basi ni nani pia atakayengia katika kaburi langu, kaburi ambalo Mwenyezi Mungu alinichagulia siku aliyoumba ardhi na akapafanya kuwa ni mategemeo ya wafuasi wetu na wanaotupenda, mahala hapo hupokelewa matendo yao na sala zao, na hukubaliwa maombi yao, na wafuasi wetu watakujaishi hapo, basi watapata amani duniani na akhera, lakini pamoja na yote niliyosema njooni siku ya "ASHURA" ambayo nitauawa mwishoni mwa siku hiyo, hatabakia baada yangu mwenye kutafutwa katika watu wangu na ukoo wangu na ndugu zangu na watu wa nyumba yangu, na watatekwa wapelekwe pamoja na kichwa changu kwa Yazid bin Muawiyya.

MAJLISI YA KUMI

IMAM HUSEIN SAFARINI KWENDA IRAQ

Siku aliyotoka Imam Husein(a.s) kuelekea Al-Kufah ndiyo siku ambayo Muslim bin Aqiil alikuwa yumo katika mapambano na askari wa Ibn Ziyad, nayo ilikuwa ndiyo siku ya tarehe nane Dhil-Hija, na Muslim aliuawa siku ya nane tangu Imam Husein(a.s) atoke Makkah, na siku hiyo ilikuwa ni siku ya "ARAFAH".

Kwa hiyo, siku ya kuondoka kwake Imam hapo Makkah, walikusanyika watu mbali mbali kutoka Hijaz na Basra wakaungana na watu wa nyumba ya Imam(a.s) na wafuasi wake.

Wakati akitaka kwenda Iraq Imam Husein(a.s) alitufu na kufanya Saayi, kisha alifungua Ihram yake na akaifanya kuwa Umra Mufradah, ndipo alipoondoka na watu wake na wanawe pia watu ambao walioungana naye miongoni mwa wafuasi wake.

Imepokewa kutoka kwa Farzadaq amesema kwamba, "Nilikwenda Hija pamoja na Mama yangu mwaka wa sitini Hijriya, wakati nilipokuwa namuongoza ngamia wa mama kuingia Al-Haram nilikutana na Husein(a.s) anatoka Makkah akiwa na panga na ngao zake nikasema, msafara huu ni wa nani? Pakasemwa kuwa ni wa Husein bin Ali(a.s) , basi nikamuendea na nikamsalimia kisha nikasema, "Mwenyezi Munga akupe maombi na matarajio yako katika mambo uyapendayo ewe mjukuu wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni jambo gani likufanyalo uache Hija kwa haraka namna hiyo?"

Imam Husein(a.s) akasema. "Lau sitafanya haraka nitakamatwa nikiwa hapa hapa, kwani wewe uniulizaye ni nani ?"

Nikasema "Mimi ni mtu miongoni mwa Waarabu, basi Wallahi Husein(a.s) hakunidadisi zaidi ya hivyo nilivyomwambia".

Kisha Imam Husein akasema kuniuliza "Hebu nifahamishe hali ya watu huko utokako ?"

Nikasema "Hakika umemuuliza mtu anayefahamu hali halisi nayo ni kuwa, nyoyo za watu ziko nawe, panga zao ziko juu ya shingo yako na maamuzi yote yanashuka kutoka mbinguni ".

Imam Husein akasema: "Usemavyo ni kweli kabisa, mambo yote ataamua Mwenyezi Mungu, iwapo uamuzi wake utashuka kwa yale tuyapendayo basi tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema zake, naye ndiye mwenye kuombwa msaada ili kuitekeleza shukurani tunayo mshukuru, na ikiwa uamuzi wake utakuwa kinyume cha matarajio hatajitenga yeyote ambaye niya yake ilikuwa kutafuta haki, na ucha Mungu ndilo lengo lake ".

Basi nikamwambia Imam Husein(a.s) , "Basi vema, namuomba Mwenyezi Mungu akutimizie yale uyapendayo na atakulinda kutokana na yale unayoyachelea, kisha nilimuuliza baadhi ya mambo ikiwa ni pamoja na nadhiri na ibada mbali mbali nikataka aniambie, Imam(a.s) alimtikisa mnyama aliyekuwa kapanda (Ishara ya kuondoka) na akaniambia amani iwe juu yako na hapo tukaachana".

Wakati Imam Husein(a.s) anaondoka, Yahya bin Said na kikundi cha watu waliokuwa wametumwa na Amri bin Said bin Al-As (Gavana wa Yazid) walijaribu kumzuia Imam Husein(a.s) .

Imam alikataa katakata yeye na wafuasi wake, jambo ambalo lilipelekea kuzuka mashambulizi ya fimbo baina ya pande mbili hizi.

Basi Imam(a.s) aliendelea na safari yake mpaka akafika mahali paitwapo Tan-im, hapa alikutana na msafara fulani unatoka Yemen akanunua kwa watu wa msafara huo ngamia kwa ajili ya matumizi ya safari yake na wafuasi wake. Naye Bwana Abdallah bin Jaafar aliwatuma wanawe wawili Aun na Muhammad wamfuate Imam Husein(a.s) , kisha akawapa na barua ambayo ndani yake alisema kama ifuatavyo:

Ama baad, bila shaka mimi nakuomba kwa Jina la Mwenyezi Mungu (Basi kubali maombi yangu) utapoiona barua yangu usiende rudi, kwa hakika nakuhurumia kutokana na upande unaoelekea, kwani huenda huko kukawa kuna kifo chako na watu wa Nyumba yako kutawanyika ovyo. Na iwapo wewe utauawa leo hii, basi Nuru ya ulimwengu itakuwa imezimika kwani wewe ndiyo bendera ya wenye kuongoka na ndiyo matumaini ya Waumini.

Basi tafadhali usifanye haraka kwenda katika safari yako, bila shaka mimi nitakuja kukufuatia baada ya barua yangu hii.

Wasalaam.

Huyu Bwana Abdallah aliondoka mpaka kwa Amri bin Said (Gavana wa Makkah) akamuomba kwamba amuandikie Imam Husein maandishi ya kumpa hifadhi na amani ili arudi asiendelee na safari yake aliyokusudia.

Amri akamuandikia Imam Husein kama alivyoombwa, na akaituma barua hiyo kwa Imam Husein, na ikapelekwa na Yahya ambaye ni ndugu wa Amri akiwa pamoja na AbdaIIah bin Jaafar, nao wakampa barua hiyo Imam Husein na wakajitahidi kumfanya arudi lakini akasema;

"Hakika mimi nimemuona Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) usingizini na ameniamuru kama hivi ambavyo ninafinya ."

Abdallah alipokwisha kila namna kumrai Imam(a.s) abadili msimamo, alikata tamaa na pale pale akawaamuru wanawe wafuatane na Imam Husein(a.s) katika safari hiyo na wapigane upande wake itapobidi mapambano, naye Bwana Abdallah na Yahya wakarudi Makkah.

Imam Husein(a.s) akaendelea na safari yake kwenda Iraq bila kupinda kushoto wala kulia mpaka akafika mahali paitwapo "Dhat-Irqi". Hapo alikutana na Bwana Bishri bin Ghalib akitokea Iraq, Imam akamuuliza hali ya watu ilivyo huko Bwana Bishri akasema "Huko nimeacha nyoyo za watu zikiwa pamoja nawe, na panga zao ziko pamoja na bani Umayya ".

Imam(a.s) akasema: "Amesema kweli ndugu wa Bani Asad, bila shaka Mwenyezi Mungu anafanya ayatakayo na anaamua mambo ayapendayo yawe ".

Habari zilipomfikia Ibn Ziyad kwamba Husein anakuja (huko al-Kufah) kutoka Makkah, alimtuma kamanda wake aliyekuwa akiitwa Al-Hasin Bin Numair akaja mpaka Qadisiyya na akalipanga jeshi lake kuanzia Qadisiyya mpaka Khifaan na pia kuanzia Qadisiyya hadi Al-Qatqataniyya.

Imam Husein(a.s) alipofika katika kijia cha Batnu-Rumah, alimtuma Bwana Qais bin Mas-har As-Saidawiy- baadhi ya wanahistoria wanasema alimtuma ndugu wa kunyonya Abdallah bin Yaqtar- kwenda al-Kufah.

Wakati Imam anatuma ujumbe huo alikuwa bado hajafahamu yaliyompata Muslim bin Aqiil.

Katika ujumbe huo aliandika bauua ifuatayo:

BISMILLAHI RAHMAN RAHIM

Barua toka kwa Husein bin Ali, kwenda kwa nduguze Waumini wa Waislamu:

Amani ya Mwenyezi Mungu ikushukieni, bila shaka mimi ninaowajibu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwenu nyinyi, Mwenyezi Mungu ambaye hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye tu.

Ama baad.

Hakika barua ya Muslim bin Aqiil imenifikia ikiwa na maelezo yanayoonyesha uzuri wa rai yenu, na kukubaliana kwenu juu ya kutusaidia na pia kuitetea haki yetu.

Basi mimi nimemuomba Mwenyezi Mungu ayafanye mema mambo yenu na akulipeni kwa yote ya wema mnayokusudia kututendea, wema ulio mkubwa kabisa. Kwa hakika mimi nimeondoka Makkah kuja huko siku ya Jumanne tarehe nane mfungo tatu.

Basi atapokufikieni mjumbe wangu mujizatiti katika maamuzi yenu bila shaka mimi nitafika hivi karibuni.

Wasalaam.

Kabla Muslim hajauawa kwa siku ishirini na saba, alikuwa kamuandikia barua Imam(a.s) .

Watu wa Al-Kufah nao walimuandikia Imam Husein(a.s) katika kipindi hicho wakimjulisha kwamba, "Wapo wapiganaji laki moja hapa kwa ajili ya kukusaidia usichelewe kuja".

Qais bin Mas-har alielekea Al-Kufah akiwa na barua ya Imam Husein(a.s) mpaka alipofika Al-Qadisiyya akakumbana na Al- Hasin bin Numeir (Askari wa Ibn Ziyad) akampokonya barua hiyo na akampeleka yeye pamoja na barua mpaka kwa Ibn Ziyad.

Alipofikishwa hapo, lbn Ziyad akamuamrisha Qais apande kwenye mimbar amtukane Husein na baba yake na nduguye. Qais akapanda juu ya mimbar kisha akamshukuru Mwenyezi Mungu na akamtukuza halafu akasema, "Enyi watu bila shaka huyu Husein bin Ali Iii miongoni mwa viumbe vya Mwenyezi Mungu vilivyo bora mno, naye ni mwana wa Fatma binti ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , nami ni Mjumbe wake amenituma kwenu, basi muitikieni muungeni mkono."

Kisha Qais akamlaani Ibn Ziyad na Baba yake na akamuombea msamaha Ali bin Abi talib na akamtakia Rehma na Amani.

Kuona hivyo, lbn ziyad akaamuru Qais atupwe kutoka juu ya jumba la Ibn Ziyad, akakamatwa kisha akatupwa kama ilivyoamuriwa mpaka chini akakatika vipande vipande.

Baadhi ya wanahistoria wanasema alifungwa mikono kisha akarushwa kutoka juu na alipoanguka chini akawa bado hajafa, lakini mtu moja aitwaye Abdul-Malik bin Umair Al-Lakhmi akaja akammalizia kwa kumchinja.

Imam Husein(a.s) aliendelea na safari yake kutoka hapo Batnu-Rumah kuelekea Al-Kufah mpaka alifika sehemu fulani iliyokuwa na maji, hapo akakutana na Bwana Abdallah bin Mutii Al-Adawi.

Bwana huyu alipomuona Imam(a.s) alisimama kisha akamwambia "Ewe mwana wa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu ni jambo gani lililokuleta huku?" Imam Husein(a.s) akasema, "Bila shaka habari za kifo cha Muawiyya zimekwisha kukufikia, basi kwa kifo hicho cha Muawiyya watu wa Iraq waliniandikia barua wakiniita niende kwao."

Ibn Mutii akasema "Nakukumbusha Mwenyezi Mungu Ewe mjukuu wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, pia ikumbuke heshima ya Uislamu (uliyonayo) nachelea itavunjika (kwa safari yako hii)".

Aliendelea Ibn Mutii kumwambia Imam Husein(a.s) "Wallahi iwapo utakitaka kilichomo mikononi mwa bani Umayya watakuua, na wakisha kukuuwa wewe hawatamuogopa yeyote baada yako, (kumfanyia uovu) Wallahi heshima ya Uislamu itaporomoka na heshima ya Maquraish na Waarabu kwa jumla, basi usiende huko Al-Kufah na wala usiitoe nafsi yako kuwapa Bani Umayya".

Imam Husein(a.s) alikataa rai ya Bwana Mutii na akaamua kutimiza lengo lake tukufu katika kuunusuru Uislam.

Kwa upande wake Ibn Ziyad alikuwa ameweka askari wake kuanzia Waqisa hadi kwenye njia iendayo Shamu na ile iendayo Basra, na akawamuru wasimruhusu yeyote kuingia wala kutoka.

Imam(a.s) akaendelea na safari yake, njiani akakutana na mabedui akawauliza khabari za huko Iraq, wakamjibu, "Sisi hatuna tukijuacho lakini uwezekano wa mtu kuingia huko au kutoka hakuna".

Hata baada ya kufahamu hilo Imam(a.s) hakukata tamaa bali aliendelea na safari kama alivyokusudia.

Kuna kikundi cha watu kutoka Fizarah na Bajiila walisimulia wakasema, "Wakati tulipokuwa tunatoka Makkah, msafara wetu ulikuwa jirani na msafara wa Husein(a.s) na Zuheri bin Al- Qain alikuwa nasi, lakini tulikuwa tunachukizwa mno kuweka kambi mahali alipoweka Husein(a.s) , cha ajabu ni kwamba kila Imam Husein alipoweka kituo kupumzika nasi tulijikuta tunalazimika kuweka kituo chetu tupumzike, ingawaje tulikuwa tukipumzika upande usiokuwa ule aliyoko Imam Husein(a.s) .

Jamaa wanaendelea kusimulia, "Basi kipindi fulani tulipokuwa tumepumzika tunakula chakula chetu ghafla alitufikia Mjumbe wa Imam Husein(a.s) akatusalimia kisha akasema, "Ewe Zuheri hakika Abu Abdillah Husein(a.s) amenituma kwako anakuita".

Baada ya maneno ya Mjumbe huyu kusemwa kila mmoja wetu alidondosha chakula alichokuwa nacho mkononi hata tukajikuta kama kwamba vichwani mwetu kumetuwa ndege (aliyesababisha mshituko)."

Mkewe Zuheri akamwambia Zuheri (akiitwa Dailam bint Omar) "Sub-hanallah. Mjukuu wa Mtume anakutumia ujumbe nawe hutaki kumuitika basi afadhali uende ukamsikilize maneno yake". (atakayo kukuambia)

Basi Zuheri akaondoka kwenda kwa Husein(a.s) , na wala hakukaa sana akarudi hali ya kuwa mwenye furaha na uso wake unapendeza, pale pale akaamuru hema lake likunjwe na mizigo yake akafunga akahamia kwa Imam Husein(a.s) .

Wakati akiondoka alimwambia mkewe 'Wewe sasa hivi umeachika hivyo basi rejea kwenu, hakika sipendi upate taabu kwa sababu yangu bali nakutakia kheri, na sasa nimeazimia kufuatana na Husein(a.s) na roho yangu nitaitoa iwe ni fidia kwake na nitamlinda kwa nafsi yangu".

Kisha Zuheri akampa mkewe mali zake na akamkabidhi kwa baadhi ya watoto wa Ammi zake wamrejeshe kwao.

Yule mama alisimama kisha akalia na kumuaga mumewe akasema. "Mwenyezi Mungu amekugeuzia (mwelekeo) basi nakuomba unikumbuke mbele ya Babu yake Husein(a.s) siku ya Kiyama".

Kisha Zuheri akawaambia jamaa zake, "Mwenye kupenda kunifuata miongoni mwenu anifuate, vinginevyo hapa ndiyo mwisho wa mahusiano kwangu mimi, lakini sina budi kuwasimulieni hadithi: Hakika tulipata kupigana vita iitwayo Al-Bahr, na Mwenyezi Mungu akatupa ushindi pia tulipata ngawira, Salman Al-Farisi akatuambia, je mmefurahi kwa ushindi aliokupeni Mwenyezi Mugnu na ngawira mlizopata? Tukasema "Ndiyo".

Salman akasema "Iwapo mtakutana na Bwana wa vijana wa kizazi cha Muhammad(s.a.w.w) , furahini mno kupigana mkiwa pamoja naye kutokana na haya mliyoyapata leo". Kisha Zuheri akaondoka na akafaulu kuwa miongoni mwa waliomsaidia Imam Husein(a.s) .

Wamesema Abdallah bin Suleiman na Mundhir bin Mash-al (Mabwana katika kabila la Asadi) "Tulipomaliza Hija yetu hatukuwa na jambo lolote la muhimu ila tulikusudia tumpate Imam Husein(a.s) njiani ili tuone ni jambo gani litamtokea, basi tukaelekea aliko kwa haraka mpaka tukamkuta amefika Zuruud, na tulipomsogelea mara tukamuona mtu katika watu wanaotoka Al-Kufa amegeuza njia baada ya kumuona Husein(a.s) , naye Imam(a.s) akasimama kama kwamba anataka kumfuata mtu yule, lakini akabadili niya na akamuacha aende zake naye akaendelea na safari yake".

Wale mabwana wanaendelea kusimulia wanasema, "Sisi tulipoona hivyo tukamfuata mtu yule mpaka tukampata tukamsalimia "Asalamu Alaika" akaitika "Waa laikumus-Salaam" tukamwambia: "Wewe ni nani?"

Akasema: "Mimi ni katika kabila la Asad".

Tukasema: "Nasi pia ni katika Asadi, basi jina lako nani"?

Akasema: "Mimi naitwa Bakri Bin fulan, kisha nasi tukamtajia nasaba zetu, kisha tukamwambia, "Hebu tupe khabari za watu walivyo huko utokako?"

Akasema: "Bila shaka sikutoka Al-Kufa mpaka alipokuwa Muslim bin Aqiil ameuawa yeye na Hani bin Ur-wah na nimewaona wawili hawa baada ya kuuawa wanakokotwa kwa miguu yao kuzungushwa sokoni" (waonekane kwa kila mtu).

Wale mabwana wanaendelea kueleza kisa chao wanasema, "(Tukamuacha mtu yule) na tukauelekea msafara wa Imam Husein(a.s) , tukaenda naye mpaka alipotua mahala paitwapo Tha-alabiya ikiwa ni jioni. Sisi tukamwendea hapo alipokuwa tukamsalimia naye akaitikia."

Tukamwambia "Tunamuomba Mwenyezi Mungu akupe Rehma, bila shaka sisi tunayo mazungumzo, iwapo utapenda tukuzungumze wazi au kwa siri."

Imam(a.s) akatutazama sisi kisha akawatazama watu wake akasema, "Hakuna siri kwa hawa waliopo hapa."

Basi tukamwambia "Je ulimuona yule msafiri uliyepishana naye jana jioni?"

Akasema, "Ndiyo, na nilitaka kumuuliza khabari fulani."

Sisi tukamwambia Husein(a.s) "Bila shaka Wallahi sisi tutakutosheleza habari zake, na tumemuuliza mambo yake kwa niyaba yako, na mtu huyo ni katika watu wa kabila letu kisha ni mwenye mawazo mazuri tena mkweli mwenye akili timamu".

Wakaendelea kusema, Na yeye ametuzungumza kwamba ametoka Al-Kufah baada ya kuuawa Muslim na Hani, na amewaona wakikokotwa kwa miguu yao wakipitishwa sokoni."

Imam Husein(a.s) akasema, Inna lillahi waina ilaihi Raajiuna - bila shaka sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na hakika kwake tutarudi, Rehma za Mwenyezi Mungu ziwashukie Muslim na Hani, akarudia kusema hivyo mara nyingine".

Baada ya Imam(a.s) kupata habari hizo alikaa akasubiri mpaka kulipokucha, akawaambia vijana wake ongezeni akiba ya maji nanyi mnywe vya kutosha munyanyuke tuendelee na safaari.

Imam akaondoka kuendelea na safari, akaenda mpaka akafika mahali paitwapo "Zubalah", hapo zikamfikia habari za Abdallah bin Yaqtar na yote yaliyomfika, na ndipo alipotoa barua mbele za watu aliokuwa nao na akawaomea kama ifuatavyo:- Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehma Mwenye Kurehemu, ama baad - kwa yakini zimetufikia khabari za kusikitisha, kwamba Muslim bin Aqiil na Hani bin Ur-wa na Abdallah bin Yaq-tar wameuawa, na wafuasi wetu huko Iraq wamtutupa mkono hakuna watakalo tusaidia, basi yeyote miongoni mwenu apendaye kuondoka (kuanchana nasi) basi na aondoke bila ya taabu na wala hatakuwa na lawama.

Basi baada ya tangazo hili, watu wengi wakamkimbia Imam Husein(a.s) wakawa wanakimbia kuelekea kila upande, wengine kulia na wengine kushoto.

Ikawa hapakubaki ila watu wale wale aliondoka nao Madina na wachache katika watu waliomfuata baadae.

Imam alifanya hivyo kwa sababu alifahamu kwamba, Mabedui waliokuwa wamemfuata walifanya hivyo kwa kutaraji kwamba Nchi anayoelekea Imam ataikuta ikiwa na watu wanaomtii yeye Imam Husein(a.s) ndiyo maana Imam(a.s) akaona vibaya kwenda nao hivi bila kuwajulisha hali halisi bali akawatangazia bayana wafahamu ni kitu gani watakachokutana nacho.

Baada ya hapo Imam akasafiri hadi akapita sehemu iitwayo "BAT-NUL-UQBAH akatua hapo.

Mahali hapa alikutana na mzee mmoja katika Bani Ik-Rimah aitwaye Omar bin Luwadhan, na huyu mzee akamuuliza Imam: "Unakusudia kwenda wapi?"

Imam akasema: "Al-Kufah."

Yule mzee akasema "Nakunasihi tafadhali usiende, Wallahi huko hutakutana isipokuwa na mikuki na mapanga, na hawa waliokuita lau wengekuwa ni wenyekukusaidia kwa vita na wakakuanalia mapokezi mazuri, hapo ilikuwa na busara kwako wewe kwenda kwao, lakini kutkana na hali hii unayozungumza mimi naona si vema kwako kuenda."

Imam(a.s) akamwambia yule mzee, "Ewe mtumwa wa Mwenyezi Mungu, kwangu mimi halijifichi lipi la kufanya na lipi la kuacha, lakini fahamu kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu anapoamua jambo hakuna wa kupinga ."

Kisha Imam(a.s) akasema, "Wallahi naapa kwamba, maadui zangu hawataniacha mpaka wahakikishe wanautoa uhai wangu, na wakisha fanya hivyo Mwenyezi Mungu atawapambanisha na watu watakaowanyanyasa mpaka wawe wao ndiyo viumbe dhalili mno katika makundi ya Umma" (Duniyani).

MAJLISI YA KUMI NA MOJA

IMAM HUSEIN(A.S) AWASILI KARBALA

Imam Husein aliendelea na safari yake mpaka ikabaki kiasi cha safari ya siku moja kutoka Al-Kufah hadi hapo alipokuwa.

Mara ghafla alitokea Bwana Huru bin Yazid akiwa na Askari alfu moja wenye farasi na Imam(a.s) akamwambia Huru, "Je hapa nitasalimika au tutaangamia ".

Huru akajibu "Lililopo hapa ni kuangamia tu ewe Abu Abdullahi."

Imam akisema: Lla haula wala Quwwata ma billahi l-aliyyiladhiim" Kisha wakawa wanazungumza baina yao (Imam na Huru) hatimaye Imam Husein(a.s) akasema "Basi iwapo ninyi mmekuwa na mawazo tofauti na zile barua zilizonifikia, pia vile ambavyo wajumbe wenu mlivyowatuma kwangu, basi niacheni nirudi nilikotoka.

Huru na jamaa zake wakamzuia Imam karudi Makkah, bali Huru akamwambia Imam(a.s) "Ewe mjukuu wa Mtume pita njia nyingine yoyote ambayo haitakufikisha Al-Kufah wala Madina, ili nami nipate kisingizio cha kumwambia Ibn Ziyad kwamba wewe umenikwepa njiani ".

Imam Husein(a.s) akaelekea upande wa kushoto, na alipofika mahali paitwapo Udhaibul-Hajanaat, Ubaidullah bin Ziyad (Mwenyezi Mungu Amlaani) akatuma barua kwa Huru akamlaumu kutokana na tendo lake la kumuachia Imam Husein ashike njia nyingine na akamuamuru kuanzia hapo amsonge Imam Husein(a.s) .

Huru na wale askari wake wakamfuata Imam na kumzuia.

Imam Husein(a.s) akamwambia Huru, "Je siyo wewe uliyetuamrisha tubadilishe njia "?

Huru akamjibu Imam(a.s) akasema, "Hakika ni mimi, lakini imenifikia barua ya Amiri (Ibn Ziyad) ananiamrisha nikusonge nisikupe nafasi, na ameniwekea mtu wa kunipeleleza iwapo ninatekeleza jambo hilo au hapana ".

Imam Husein(a.s) akasimama kuwahutubia watu wake, akamshukuru Mwenyezi Mungu na kumsifu, kisha akamtaja Babu yake (Mtume Muhammad(s.a.w.w) na akamswaIia kisha akasema: "Bila shaka yamekwisha kutufika mambo ambayo mnayaona wazi wazi, na kwamba duniya imebadilika na imeyakataa na kuyapa mgongo mema yake, na imeimarika kutenda yasiyokuwa na busara, na hakuna kilichobakia katika dunia isipokuwa ni kama maji kidogo ndani ya chombo, na maisha duni mfano wa malisho yasiyofaa, je hamuoni kwamba ukweli sasa hivi hautumiki na kwamba uovu haukemewi? Basi aliye Muumini na atarajie kukutana na Mola wake kwa kuuawa (na madhalimu) kwani mimi mimi naona kifo (katika njia ya haki) ni mafanikio na kuishi pamoja na watu dhalimu ni unyonge".

Baada ya hotuba ya Imam(a.s) alisimama Bwana Zuhair bin Al-Qain akasema, "Tumesikia usemi wako ewe mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, lau dunia ingekuwa ni yenye kudumu kwa ajili yetu nasi tukawa ni wenye kuishi humo milele, Wallahi tungethamini mno kupambana na udhalimu tukiwa pamoja nawe ili kuitetea haki".

Kisha alisimama Hilal bin Nafii Al-Bajali akasema, "Wallahi hatuchukii kufa ili tukutane na Mola wetu, nasi katika niya zetu na tunavyofahamu ni kwamba tutamtawalisha anayekutawalisha wewe na tutampinga anayekupinga".

Naye Burair bin Khudhair alisimama akasema, "Wallahi Ewe Mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, bila shaka Mwenyezi Mungu ametuneemesha kwa kupitia kwako pale alipo tujaalia kuwa tutauawa mbele yako na viungo vyetu vitakatwakatwa kwa ajili yako, kisha siku ya Qiyama Babu yako (Muhammad s.a.w.w) atakuwa ndiyo muombezi wetu".

Baada ya hapo Imam Husein aliondoka kuendelea na safari yake, lakini ikawa kila alipotaka kuelekea upande fulani Huru na askari wake humzuia na wakati mwingine humsonga wakawa ubavuni mwa msafara wake.

Kutokana na hali hiyo ya kusongwa na majeshi hayo, wanawake waliokuwa pamoja na Imam(a.s) wakaingiwa na woga na watoto nao wakawa na khofu isiyokuwa na kipimo.

Huru na Askari wake walimsonga Imam(a.s) mpaka wakamfikisha Kar-bala ikiwa ni tarehe mbili mfungo nne (Muharram). Walipofika hapo Imam Husein(a.s) akauliza Jina la Ardhi hiyo na akaambiwa, "hapa ni Kar-bala".

Imam(a.s) akasema, "Ewe Mola najilinda kwako kutokana na huzuni na tabu ". (Karb-balaa).

Kisha akasema tena, hapa ndipo mahali penye huzuni na taabu, basi teremkeni kwa kuwa ndicho kituo cha msafara wetu, na ndipo mahali ambapo damu zetu zitamwagika, na ni sehemu itakayokuwa na makaburi yetu, mahali hapa alinisimulia Babu yangu Mjumbe wa Mwenyezi Mungu kwa yote niliyoyaeleza".

Watu wote waliokuwa na Imam Husein(a.s) wakashuka kando ya Imam Husein(a.s) .

Imam Husein(a.s) aliketi akawa anauandaa upanga wake huku akisema mashairi yaliyokuwa yanabashiri kifo chake.

Dada yake Imam(a.s) aliyekuwa akiitwa Zainab aliposikia maneno ya nduguye akasema: "Ewe kaka yangu maneno haya usemayo ni ya mtu ambaye tayari amekwisha thibitisha kwamba atauawa ".

Imam akasema: "Hivi ndivyo ilivyo kwangu ewe dada yangu ".

Bibi Zainab akasema: "Aa! hasara iliyoje. Husein anaomboleza mbele yangu kifo chake mwenyewe "!

Kilio cha bi Zainab na maneno aliyoyasema yaliwafanya wanawake wote walie na wakawa wanapiga nyuso zao na kukata mikufu yao. Naye Ummu Kul-thuum akawa anaomboleza kwa kusema "Ewe Muhammad wangu(s.a.w.w) ewe Ali wangu(a.s) Ewe Mama yangu (Fatma a.s) Ewe ndugu yangu Ewe Hasani wangu(a.s) , tumeangamia baada yako ewe Abaa-Abdillah".

Imam Husein(a.s) aliposikia maombolezo ya Ummu Kulthuum akamtaka awe na subira akamwambia, "Ewe dada yangu vumilia ufarijike kwa Mwenyezi Mungu, kwani viumbe vya mbinguni vitakufa, na viumbe wa ardhini nao watakufa, kadhalika viumbe wote watakufa ".

Imepokewa katika mapokezi mengine kwamba Bibi Ummu Kul-thuum alipofahamu madhumuni ya beti za mashairi aliyokuwa akiyasoma Imam(a.s) alitoka kwa uchungu mkubwa huku akikokota nguo zake mpaka akaenda kusimama mbele ya Imam Husein(a.s) akasema, "Ooo! Hasara iliyoje laiti mauti yangenichukua (leo), kwani leo ni sawa na kifo cha mama yangu Fatma, na Baba yangu Ali na ndugu yangu Hasan(a.s) . Ewe uliyebaki baada ya hao waliokutangulia, wewe ulikuwa ndiyo nguzo ya sisi tuliobakia".

Imam Husein(a.s) alimtazama dada yake kisha akasema: "Ewe dada yangu angalia shetani asije akauchukua uvumilivu na subira yako katika machungu yako kwangu ".

Imam Husein(a.s) akashikwa na huzuni kubwa machozi yakawa yanamlengalenga kisha akasema, "Sina njia ya kufanya kuepuka mauti ".