• Anza
  • Iliyopita
  • 6 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 7956 / Pakua: 1967
Kiwango Kiwango Kiwango
UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA IMAM HUSEN

Mwandishi:
Swahili

UTENZI WA IMAM HUSEN

MWANDISHI: HEMED BIN ABDALLAH BIN SAID

UTENZI WA KISA CHA SAYYIDNA HUSSEIN

1. Bismillahi Aziza, ArRahmani Mweneza, Ndiye wa Kwanza na kwanza, Wa milele na abadi

2. Ndiye Huyu 'lKayumu, Wa milele na dawamu, Ndiye muumba Adamu, Na wote wake waladi

3. Ndiye muumba 'ssamai, Na wote anbiai, Thumma na auliai, Wote ni wake ibadi

4. Jamii ni wake waja, Wala hawati mmoja, Kula atakae haja, Apata wake mradi

5. Kuumba kwake Jalali, Nabiu na Mursali, Aliyeumbwa awali, Tumwa wetu Muhammadi

6. Huyo alitangulia, Kisijawa vitu pia, Vyote vilivyobakia, Vijile yake baadi

7. Nuru yake yalidanda, Na sifaze zikenenda, Jina aketwa Kipendwa, Kipendo chake 'sSamadi

8. Baada ya kudhukuri, Sifa za Mola Jabari, Na za tumwa Mukhtari, Penda nitunge ishadi

9. Natanga tunga utenzi, Usipate nusu mwezi, Ama kwandika siwezi, Macho yametasawadi

10. Macho yamesawidika, Sioni vema kwandika, Kwa kula siku kushika, Karatasi na midadi

11. Macho yangu wanakwetu, Hayafafanui mtu, Natendea kazi yetu, Ya tangu jadi na jadi

12. Na kuiwacha si vema, Taja dhuriwa nakoma, Hata kwamba si mzima, Afadhali jitihadi

13. Na hadithiye kwambile, Nitakayo nitongole, Bajani moyo mkale, Tena mtuze fuadi

14. Mtoe na wasiwasi, Niwatulie nafusi, Baada ya kujilisi, Na roho kutabaradi

15. Ndipo niweleze shani, Ya Maulana Huseni, Dhuria wake Amini, Vita vyao na Yazidi

16. Huyu Yazidi sikia, Babaye ni Muawia, Kutawafukwe Nabia, Na arubaa Sayyidi

17. Wa kwanza Abubakari, Na Maulana Omari, Na Ally Haidari, Na mmoja taradidi

18. Maulana Athumani, Watu hao sikiani, Kuondoka duniyani, Ndipo hayo yakabidi

19. Kuondoka kwao pia, Kutawala Muawia, Miji yote kuzuia, Asibakie biladi

20. Akashika ufalume, Wala pasiwe muume, Na dhuriaze Mtume, Pendo likenda ahadi

21. Akampenda Huseni, Na watotowe nyumbani, Na angawa sultani, Asiweze kutaadi

22. Kakithiri Muawia, Heshima kamwekea, Na pendo kamzidia, Atakalo lisirudi

23. Akazidi muheshimu, Na wote bani Hashimu, Jamii kawakirimu, Akajifanya abidi

24. Baada hayo rafiki, Akenenda Dimishiki, Na dhuriaze sadiki, Asibakie wahidi

25. Kamtukua Huseni, Na dhuriaze Amini, Rijali na nisiwani, Wakubwa hata waladi

26. Dimishiki kenda nao, Muawia kawa nao, Akawaweka kikao, Kizuri kisikyo budi

27. Baada suu wuadhi, Akapatwa ni maradhi, Muawia kiaridhi, Akajua ni ahadi

28. Akajua ni ajali, Ya roho kunakali, Akamwita tasihili, Mtoto wake Yazidi

29. Akamuweka usoni, Wali wao faraghani, Muawia kabaini, Akamba ewe waladi

30. Ewe Yazidi mwanangu, Nitazama hali yangu, Muwili wote matungu, Na uzito wa jasadi

31. Muwili umezuiwa, Sijiwezi kujinua, Na sisi waja twajua, Mauti hatuna budi

32. Twaijua kwa hakika, Ni faradhi kutoweka, Yazidi akatamka, Maneno akaradidi

33. Baba utakapokufa, Nnani nyuma Khalifa, Mtamalaki taifa, Na ezi ikambidi?

34. Akinena Muawia, Khalifa wewe dhuria, Lakini nakuusia, Usije ukafisidi

35. Sikia ewe mwanangu, Ushike wosia wangu, Wepukane na matungu, Hiyo siku ya mnadi

36. Kwanza nikuusiayo, Ezi ni kutunza moyo, Ujue na marikayo, Na walio kukuzidi

37. Na wote raia wako, Ukae nao kitako, Usikithiri vituko, Utakuja jihusudi

38. Na tena uwashauri, Ijiriapo amri, Ukae nao vizuri, Roho zao ziburudi

39. Pindi hayo ukitenda, Tambua watakupenda, Utakalo utatenda, Neno lako halirudi

40. Baada hayo yakini, Nakusikia Huseni, Na watotowe nyumbani, Alla Alla ya Yazidi

41. Alla Alla uwashike, Tangu waume na wake, Na jambo lisitendeke, Shati apende Sayyidi

42. Jambo asilolipenda, Usije ukalitenda, Tambua umejivunda, Hata kwa Mola Wadudi

43. Wala usimkasiri, Hata kwa jambo saghiri, Mpe kuti na uzari, Kabla wote junudi

44. Alla Alla muheshimu, Umzidie makamu, Kwani sisi tu hadimu, Walidio masayidi

45. Ewe Yazidi yashike, Yule asikasirike, Sisi tu watumwa wake, Na babuye Muhamadi

46. Na ukhalifa si wetu, Wala si wa baba zetu, Wake yeye bwana wetu, Sisi kwao tu abidi

47. Pindi atakapokuwa, Siwate kumtukuwa, Umsalimu ulua, Kuko kwao na urudi

48. Alla Alla ewe mwana, Akuapo Maulana, Enenda naye Madina, Na wote wake waladi

49. Umsalimu eziye, Kwamba atatwaa yeye, Au mtu atakaye, Ushike ndiya urudi

50. Atakalo mfanyie, Wala simzuilie, Na kadiri amriye, Ndiyo itayokufidi

51. Umtie mahabani, Dhahiri na faraghani, Siwe na kitu moyoni, Roho yako isafidi

52. Na pindi umpendapo, Hapana budi na pepo, Utakwenda kaa papo, Pa babuye Muhammadi

53. Pindi usipompenda, Kesho huna la kutenda, Ndia utakayokwenda, Na Majusi na Yahudi

54. Muawia kamaliza, Yazidi asikiliza, Maneno kamrudiza, Manenoyo hayarudi

55. Yote uloniusia, Baba nimeyasikia, Si mwenye kuyawatia, Yote uliyoradidi,

56. Baada hayo nakuli, Isipate siku mbili, Akapatwa na ajali, Mauti yakambidi

57. Alipokwisha toweka, Yazidi kafadhaika, Kasimama akazika, Na kuchawanya nakidi

58. Akaliweka tanzia, La babaye Muawiya, Na vitu vikangamia, Vingi visivyo idadi

59. Akavihasiri vitu, Akawakusanya watu, Si siku mbili si tatu, Ikawa hiyo abadi

60. Akawatinda ghanamu, Na wingi wa bahayumu, Na zakula tamtamu, Na sharubati waridi

61. Matanga akiondoa, Nguo mbaya kazivua, Akavaa za uluwa, Nzuri za kusafidi

62. Akajivika na taji, Lawaka kama siraji, Na wengi watundamaji, Majaria na abidi

63. Akajivika libasi, Hudhuri na sandusi, Zawaka kama shamsi, Rihi ambari na udi

64. Akavaa burukhuti, Akakikalia kiti, Cha lulu na yakuuti, Chema cha zabarijudi

65. Akatungika johari, Na thoria mnawari, Vyandarua vya hariri, Siriri na l'wasidi

66. Sayo yakisha tendeka, Akakutubu nyaraka, Kula nti kapeleka, Akamkua junudi

67. Akaweta asibaki, Kula panapo muluki, Wakutane Dimishiki, Wamkiri usayidi

68. Barua zisibakie, Na kula asikiaye, Akaja na kaumuye, Na nyingi mno zawadi

69. Wakaitika amri, Jamii ya ansari, Wakakutana jifiri, Kuja kwake makusudi

70. Walipokwenda timia, Yazidi akawambia, Jambo alilowetia, Ya maishara junudi

71. Mimi nimetamalaki, Aridhi ya Dimishiki, Na jamii ya muluki, Mje kwangu musujudi

72. Mimi ndimi sultani, Niwetapo nitikani, Pasiwe na ushindani, Wala mwenye kukaidi

73. Mimi ni wenu amiri, Ambaye amenikiri, Tamjaza utajiri, Na kula siku nizidi

74. Ambaye amekubali, Tamjaza mangi mali, Yeye na wake ayali, Na wakewe na abidi

75. Ambaye hakuridhika, Kuwa mimi mamlika, Rasiye itaondoka, Kwa saifi ya hadidi

76. Tamkata yake rasi, Nimwangue kama sisi, Semani hima upesi, Nipate kuyafanidi

77. Jamii wakabaini, Wewe ndiwe sultani, Akubishaye nnani?, Hapo mwenye kukaidi

78. Wewe ndiwe bwana wetu, Uliyemiliki watu, Wala hazumbuki mtu, Kuja kwako na taadi

79. Na ambaye atakuja, Kwa harubu au huja, Shauri letu ni moja, Tambua tutakufidi

80. Haya wakishatamka, Yazidi kafurahika, Akawapa twika twika, Jeshi yote ikarudi

81. Kabaki yeye pekee, Na mjini kaumuye, Akampa ampaye, Wengine akawazidi

82. Akaweka mawaziri, Na aribabu amri, Akadirika hamri, Barazani ikabidi

83. Kinyang'anya masikini, Wenye kupita ndiani, Na wajao barazani, Wengine kiwahusudi

84. Kawakataa tariki, Sipitike Dimishiki, Watu wakataharuki, Kwa mambo yake Yazidi

85. Akaitenda jeuri, Kubwa isiyo kadiri, Raia na mawaziri, Wote wakasitajidi

86. Na kula mtu ambaye, Alipendwa na babaye, Yeye kawa hasimuye, Akija kimtaridi

87. Ali akiwasukuma, Wenye haya na huruma, Akakithiri dhuluma, Na kila siku kuzidi

88. Akautupa wosia, Wa babaye Muawiya, Ukazidi utaghia, Mno akatamaridi

89. Na Maulana Huseni, Asimpe nufaani, Wala kwenda barazani, Asipende mshahidi

90. Na mtu amtajaye, Alosimama mbeleye, Yuamkata nyamaye, Na kumpiga jalidi

91. Kamzia Maulana, Asitake kumuona, Pasiwe neno kunena, Ila la kumuhusudi

92. Akashirabu khamri, Na jilasi ikajiri, Na nyama ya hinziri, Akila na kurajidi

93. Kuonakwe Maulana, Vitendo vyake laana, Na babaye alonena, Yote hayakusuudi

94. Kuonakwe tafauti, Kondoka suu wakati, Kenda kwa wake ukhti, Ili kwenda muradidi

95. Akifika akalia, Nduguye akangalia, Sakina akamwambia, Waliza nini Sayyidi?

96. Akatamka Sakina, Una nini Maulana, Ambalo ni kubwa sana, Jambo lililokuzidi?

97. Kilio chako Huseni, Kitawaliza majini, Na malaika mbinguni, Na baharini swayyidi

98. Na nyama wote barani, Watangia kilioni, Hata maji baharini, Pia yatatujamidi

99. Usilie Maulana, Na uliyo nayo nena, Kwa amriye Rabana, Neo lako halirudi

100. Huseni akamwambia, Ewe Sakina sikia, Yaliyonipa kulia, Ni mambo yake Huseni

101. Ametukiwa na siye, Hapendi atusikie, Ni kheri tumuukiye, Si naye tuwe baidi

102. Sikia ewe Sakina, Twenende zetu Madina, Hapa sipataki tena, Hata kwa saa wahidi

103. Twende zetu Yathiribu, Kunako nyumba za Babu, Tumwondokee harabu, Atakayetuhusudi

104. Ni hayo maneno yangu, Nitakayo roho yangu, Wanenaje nduu yangu, Katika suu mradi?

105. Kamaliza Maulana, Akatamka Sakina, Sayyidi unayonena, Mimi ni bora zaidi

106. Huyu ametakabari, Na kumuasi Jabari, Na kushirabu khamri, Na watu kuwajalidi

107. Na babaye Muawiya, Pia alomuusia, Yote hayakutimia, Hata kwa jambo wahidi

108. Afadhali twende zetu, Kunako majumba yetu, Kwani Yazidi si kitu, Amekwisha tamaridi

109. Walakini kamjibu, Umuarifu kitabu, Nenda zangu Yathiribu, Wala huku sitarudi

110. Mpelekee khabari, Ya kumuaga safari, Tusikize madhukuri, Atakayo kuradidi

111. Kwani tutokapo Kofu, Tusipo kumuarifu, Atasema tuna khofu, Haya atayafanidi

112. Sakina kwisha kalimu, Mara Huseni kakumu, Akaagiza kalamu, Na lauhi na midadi

113. Akawandika waraka, Tasihili kwa kikaka, Ila muhibu pulika, Sikia ewe Yazidi

114. Rohoni nimeazimu, Kwenda Madina kukimu, Au kunako Haramu, Hakae nitaabidi

115. Napenda kwenenda Maka, Au Madina hifika, Hatake pa kuniweka, Katika mbili biladi

116. Nami siwezi safiri, Ila unipe amri, Na ambapo hukukiri, Takaa nitabaradi

117. Nipe rukhusa ya kwenda, Au niambie Vunda, Kula utakalopenda, Siwezi kukukaidi

118. Kashilia Maulana, Kaukunda iyo hina, Kamsalimu kijana, Kenda nao kwa Yazidi

119. Ikiwasili barua, Yazidi kaufungua, Jamii makutubua, Yote akayaadidi

120. Hata akisha usoma, Kaupindua kwa nyuma, Aketa kalamu hima, Kumuarifu Sayyidi

121. Maneno akabaini, Akamba ewe Huseni, Kwangu wataka idhini, Ndiyo uliyoradidi

122. Tumia khiari wewe, Hayo ni yako mwenyewe, Mimi sina haja nawe, Sipendi kukushahidi

123. Ukenenda sikutaki, Wala hu wangu rafiki, Na uwapo Dimishiki, Sikupi hata nakidi

124. Sipendi kushuhudia, Kwamba Rabi ajalia, Kuigauza dunia, Ikawa zabarijudi

125. Ningewapa insani, Watu wote duniani, Wewe ukaitamani, Ujapo kujitahidi

126. Kwangu hupati mahaba, Wala kula ukashiba, Nakuwazia msiba, Na 'ladhabu shadidi

127. Na Maka ukiwasili, Majumba yangu ya mali, Nenda kayakae mbali, Usende ukarajidi

128. Sende ukapanda ngazi, Majumba yangu ya ezi, Akimaa matongozi, Waraka kaujadili

129. Kamsalimu risali, Kenda nao tasihili, Hata alipowasili, Kwa Maulana sayyidi

130. Kausoma kauona, Kenda nao kwa Sakina, Akamba tazama mwana, Maneno yake Yazidi

131. Amesema ni khiari, Kukaa na kusafiri, Wanambiaje shauri?, Mwanamke karadidi

132. Mwanamke kadhukuri, Hapana tena usiri, Na watengeze bairi, Wa kuja panda waladi

133. Hima twandame tariki, Tuitoke Dimishiki, Huseni akasabiki, Kamzaini jawadi

134. Twika kazitengeneza, Ngamia akawatwisa, Kula ambaye apasa, Waungwana na abidi

135. Wakalekea safari, Wakamuomba Jabari, Wakaikabili bari, Yenye nondo na asadi

136. Rabi akawanusuru, Kwenda kheri wa sururu, Pasiwe la kuwadhuru, Dhuria za Muhammadi

137. Kawanusuru Rabuka, Kwa maafa na shabuka, Nondo wote na majoka, Wakuja wakisuudi

138. Jamii watu wazima, Hata watoto yatima, Wakiwasili salama, Badari 'lmakusudi

139. Walipofika Madina, Watu walipowaona, Wakafurahika sana, Furaha kubwa shadidi

140. Wakatelea rikabu, Wakangia Yathiribu, Jamii ya Waarabu, Wakamlaki sayyidi

141. Akafikilia dari, Ya babaye Haidari, Ndiyo aliyokhiari, Kuwatia auladi

142. Baada ya kuwasili, Akenenda tasihili, Kaburini kwa rasuli, Kumzuru wake jadi

143. Kimaa yake zuari, Kaburi iketa nuri, Hata juu ya kamari, Nuru hiyo ikazidi

144. Kwishakwe zuru nabia, Roho ikafurahia, Nyumbani akarejea, Nyumbani kwake kurudi

145. Ali yeye na nduguye, Alokwenda zuru naye, Mtakapo ismuye, Jina ketwa Muhammadi

146. Ni mwana wa Shekhe Ali, Kazawa nyumba ya pili, Naye katika kitali, Kama umeme na radi

147. Jamii zote taifa, Wamwita bunu Khanifa, Wala hafikiri kufa, Atokeapo jihadi

148. Ali simba maalumu, Katika nchi ya Shamu, Ambapo ataranamu, Utamboni akabidi

149. Hakiwa akizumbuka, Awezaye kumfika, Wote wenye kutajika, Kwake wakasitajidi

150. Basi wakarejeea, Na Maulana pamoya, Nyumbani wakenda ngia, Kwa baba yao asadi

151. Na wote 'lAnsari, Na jamii Muhajiri, Pasibakie saghiri, Msifurahi fuadi

152. Wale wakamkirimu, Kwa zakula tamtamu, Wakamuweka makamu, Na pendo likashitadi

153. Jamii wakalingana, Kumwambia Maulana, Kula utakalonena, Kwani ni yako biladi

154. Sisitahi bwana wetu, Roho ikataka kitu, Nafasi na mali zetu, Ni yako wewe Sayyidi

155. Sote tumefurahika, Madina unavyofika, Hatupendi kuondoka, Katika zetu fuadi

156. Basi wakasimulia, Hata kiza kikangia, Wakenenda zao pia, Pasibakie wahidi

157. Ila ni wao theneni, Wao wawili nyumbani, Akatamka Huseni, Kamba Ewe Muhammadi

158. Sababu ya kuja zangu, Ni ghadhabu na matungu, Ya hayo asi wa Mungu, Abdullahi Yazidi

159. Alipokufa babaye, Hamtazama haliye, Sikuweza kaa naye, Kwa jeuri na taadi

160. Yote aliyousiwa, Hata moja halikuwa, Aliposhika ulua, Kangia na kufisidi

161. Nami kanizia sana, Asitake kuniona, Haona sina maana, Kukaa yake biladi

162. Haradhiwa kuondoka, Kuja Madina na Maka, Muhammadi katamka, Ahsanta Sayyidi

163. Hasanta bun Ali, Kuja zako afadhali, Mtu kukaa muhali, Wala asipo mradi

164. Miji yao maghasiki, 'lKofu na Dimishiki, kukaa wewe ni dhiki, mashaka hayana budi

165. Na Yazidi bardhuli, Kuwania udawali, Wala si yao asili, Si ya jadi na jududi

166. Huu ulua ni wetu, Wa baba na babu zetu, Wala hazumbuki mtu, Ambaye ametuzidi

167. Wenyewe tukiutaka, Twenenda tukaushika, Na afanyapo dhihaka, Tukamuonya hadidi

168. Na kwamba hatuutaki, Ya nini kwenda jidhiki?, Kheri kufuata haki, Ya Mola wetu Wadudi

169. Nawe sasa Maulana, Keleti hapa Madina, Kula utakalo nena, Neno lako halirudi

170. Na utakapo Makati, Enenda zako kaketi, Na kwamba wataka nti, Takuwali sina budi

171. Utakapo ukhalifa, Sema niwete taifa, Ahadi ni mimi kufa, Ndipo uone taadi

172. Takawali hivi sasa, Utamalaki kabisa, Pasiwe mtenda kisa, Ukate utabaridi

173. Huseni kamrudia, Ya 'lakhi nisikia, Hayo sikupendelea, Kutamalaki junudi

174. Roho yangu naazimu, Nenende hasitakimu, Maka kunako Haramu, Nimuabudu Wadudi

175. Niabudu Subhana, Kwa usiku na mchana, Nitazame kwa Rabana, Atakalo kunibidi

176. Ezi sina haja nayo, Haimo katika moyo, Wakisha kusema hayo, Wakenda wakarajidi

177. Akaketi Maulana, Siku ashara Madina, Khatima wakandamana, Nduguye akamuwadi

178. Maulana akatoka, Akakusudia Maka, Siku haba zikifika, Akawasili biladi

179. Alipokwisha wasili, Wakatoka kabaili, Wanawake na rijali, Kwenda mlaki Sayyidi

180. Katoka bun Zuberi, Abdalla mashihuri, Pasibakie saghiri, Waungwana na abidi

181. Na Abdalla yuani, Ni ndugu yake Huseni, Wa katika ridhaani, Zamani wali wabidi

182. Ni nduguye hana huja, Walinyonya ziwa moja, Akenda akimngoja, Bara katika 'lwadi

183. Na Abdalla pulika, Zamani hizo hakika, Ndiye khalifa wa Maka, Mtamalaki junudi

184. Wakamlaki Huseni, Na ndugu yake Sakini, Wakamtia mjini, Na furaha za fuadi

185. Abdalla akanena, Twende kwangu Maulana, Kwenda pengine hapana, Kwangu ni bora zaidi

186. Kuwasilikwe fahamu, Ikafanyiwa karamu, Ya hubuzi na lahamu, Na vitu vya kusafidi

187. Twenende kwangu nyumbani, Ukae uje makini, Akatikia Huseni, Asiweze kumrudi

188. Kasimama Abdalla, Akafanyiza vyakula, Na wengine kabaila, Wote wakajitahidi

189. Kula mtu katamani, Kumkirimu Huseni, Vitu launi launi, Vya moto na vya baridi

190. Karamu zikafanyiwa, Na kuliwa zikasazwa, Hata kukangia kiza, Usiku ukasawidi

191. Watu wote barazani, Wakarejea nyumbani, Kabaki yeye Huseni, Na mtoto wa asadi

192. Huseni akatamka, Ya Abdalla pulika, Kisa cha kungia Maka, Na Dimishiki kurudi

193. Ni ibnu Muawia, Mambo alonifanyia, Uasi na utaghia, Jeuri na uhasidi

194. Amekithiri jeuri, Uasi na ujabari, Si mwenye kutafakari, Na kwamba yuko Wadudi

195. Amekithiri uasi, Kupita hao Majusi, Nilipoona jinsi, Hushika ndia harudi

196. Babaye akifariki, Akaushika muluki, Yote hakuyasadiki, Aliyokumradidi

197. Yote alomuusia, Jamii hakuridhia, Sikuweza vumilia, Mji wake kurakidi

198. Nimekuja zangu kwetu, Kuliko majumba yetu, Niabudu Mola wetu, Rakaa na kusujudi

199. Abdalla akanena, Hasanta Maulana, Yamenipendeza sana, Kuja Maka kukaidi

200. Kama wewe kuja Maka, Utakalo ni kutaka, Inshalla litatendeka, Kula utaloradidi

201. Ulitakalo twambie, Hapana alibishaye, Twajua bwana ni wewe, Tangu jadi na jududi

202. Utakapo khalafati, Sasa takitoa kiti, Utamalaki Makati, Na jamii ya biladi

203. Nikuwali ukhalifa, Wa babuyo Musitafa, Na mweye kutaka kufa, Ni mwenye kukukayidi

204. Na asemaye hataki, Sharuti tamuhiliki, Na Yazidi Dimishiki, Tapanda mimi jawadi

205. Nitukue farisani, Wazoefu wa vitani, Kama simba ghadhibani, Walio kama asadi

206. Dimishiki nirikabu, Niuonyeshe barabu, Hadi ni kutaadabu, Yeye na wake juhudi

207. Ningie na bildiye, Nitafute asemaye, Nimuondoshe rasiye, Kula aliye hasidi

208. Pasibaki kabaili, Ambaye hatakubali, Huseni kamba ni kweli, Yote unayoradidi

209. Walakini ndugu yangu, Siupendi ulimwengu, Taka abudu Muungu, Ni huu wangu mradi

210. Sitaki usultani, Taka niwe masikini, Wala hayo sitamani, Kwenda wapiga jihadi

211. Nataka niketi Maka, Nimuabudu Rabuka, Wala sipendi kwondoka, Hata ifike ahadi

212. Hapano Maka sondoki, Na ukhalifa sitaki, Kisha sayo kunatiki, Wakenda wakarakidi

213. Baada hayo yuani, Kaketi Make Huseni, Wote walio mjini, Kupenda wakamzidi

214. Wakampenda sikia, Yeye na wake dhuria, Kula siku kuzidia, Mahaba mangi shadidi

215. Wote wakamjamili, Yeye na wake tifili, Na wake namarijali, Wakubwa na auladi

216. Wasitambike nufaa, Wala nguo za kuvaa, Wala nyumba ya kukaa, Tena akataabadi

217. Roho akaituliza, Akaabudu Aziza, Hata usiku wa kiza, Haramuni kisujudi

218. Kaabudu Mola pweke, Kwa kusafi moyo wake, Yeye na msala wake, Pasiwe na kurakidi

219. Akakithiri saumu, Na yake masitakimu, Yali ndani Haramu, Ikwa hiyo abadi

220. Asitake neno tena, Ila dini ya Rabana, Baada sayo nanena, Mambo baidi baidi

221. Nataka niyakutubu, Niyaweke babubabu, Nisije nikaharibu, Haja hambiwa kusudi

222. Nataka nielekeze, Kula kwa sifaze, Na utenzi upendeze, Nilio kuufanidi

223. Baada kupita hayo, Maneno niwambiayo, Sasa ni kutuza moyo, Niwakhubiri Yazidi

224. Kwondoka kwake Huseni, Kashika usultani, Kamiliki buldani, Kwa nguvu na uhasidi

225. Akawadhiki wenziwe, Wageni raiawe, Jamii wasitongoe, Pasi mwenye kuradidi

226. Watu akiwadhulumu, Na kula mna haramu, Na nguzo za Islamu, Zote asitaamidi

227. Wangine kiwadhurubu, Wala pasipo sababu, Akawa mnoa harabu, Kushinda hao Yahudi

228. Ndia zikafungamana, Pasiwe safari tena, Na ambaye amuona, Humwegema kwa hadidi

229. Kiwapoka watu mali, Wangine kiwakutuli, Ndia zote kazidhili, Za karibu na baidi

230. Pasiwe asafririye, Ala mtu enendaye, Kwa vitendo na haliye, Awatendavyo junudi

231. Kisha sayo nitamke, Katika kaumu yake, Mli mtu jina lake, Akitwa bun Ziadi

232. Jinale Abidallahi, Ali adui asahi, Dhuluma na ukabihi, Apita huyo Yazidi

233. Akichecha watu damu, Kwa jeuri na dhulumu, Hali akisha karimu, Ali jabari anidi

234. Yazidi kumuonakwe, Jeuri na hali yakwe, Kampenda yakwe, Pendo lisilo idadi

235. Kawa mtu maarufu, Tena akamsharifu, Akenda muweka Kofu, Akampa na biladi

236. Kampa katamalaki, Tangu Kofu na Iraki, Neno ambalo hataki, Pasiwe mwinua yadi

237. Akenda akaishika, Kakusa watu mashaka, Viumbe wakadhilika, Ikiwa kheri abidi

238. Jamii watu wa Kofu, Roho zikangia khofu, Kwa mambo yake dhaifu, Aliyo kutaahidi

239. Pasiwe mtu mzima, Wala naye heshima, Na mabaye uasema, Mara yamkaidi

240. Hunyang'anywa mali zao, Huuliwa wana wao, Hutwaliwa nyumba zao, Hali ya nguvu shadidi

241. Mali zao hutwaliwa, Na wao wakauawa, Na wasemalo haliwa, Wa sawa na 'kurudi

242. Wakakeleti mjini, Wakawa kama manyani, Mashekhe na madiwani, Nyuso zikawa sawidi

243. Pasiwe mwenye shauri, Wala anye amri, Kwa kushitadi jeuri, Akaptia Namrudi

244. Wa Kofu wakiyatunza, Dhuluma na miujiza, Wakamba hatutawaza, Dhuluma inatuzidi

245. Wakakutana kabili, Wote wazele wazele, Na mashaibu wa kale, Wasizo na 'lmuridi

246. Mashekhe na madiwani, Wakangia faraghani, Wakauzana yakini, Mwaionaje biladi?

247. Mwaonaje wenye nti, Na hakimu mwenye kiti, Tutaweza kuiketi, 'lKofu tukakhalidi?

248. Mwaonaje wenye kaya, Na huyo mwenye ulaya, Na mambo yake ni haya, Atutendayo abadi?

249. Kwa jamii wamwambie, Bunu Ziadi mamboye, Hapana ayawezaye, Yanatuchoma fuadi

250. Hatuwezi siku moja, Kuvumilia miuja, Kupigwa pasipo huja, Kama tunao jihadi

251. Kupigwa kama watoto, Kwa bakora na makoto, Haya ni mambo mazito, Hatuwenepo abadi

252. Kupigwa tukiuawa, Na mali yakitwaliwa, Wala hakutaadiwa, Si kwamba tuna taadi

253. Katungia kwa batili, Akatunyang'anya mali, Kuno akatukutuli, Mambo yanatupa hadi

254. Shauri na tufanyeni, Tuli hapa faraghani, Wangine wakabaini, Walio wana mradi

255. Wangine wakatamka, Yote yaliyotungika, Ya adhabu na mashaka, Tunayataka kusudi

256. Maana tuna yakini, Ezi na usultani, Si wake huyu laini, Wala babaye Ziadi

257. Wala si ya Muawia, Hawa wanajitwalia, Kutamalaki raia, Kampasaje Yazidi?

258. Sisi tu makabaili, Kutoka majitu mbali, Yakaja na ufedhuli, Katika zetu biladi

259. Wakatenda watakayo, Nasi tukaona ndiyo, Twabasa ni kama hayo, Hata yajapo tuzidi

260. Ezi si ya Marijani, Babuye huyo laini, Wala si ya Sufiyani, Babuye huyo Yazidi

261. Twayajua kwa makini, Ezi mwenyewe Huseni, Kwa babu yake Amini, Na baba yake Asadi

262. Twayajua maarufu, Jamii tulio Kofu, Kwondoka kwake Sharifu, Ezi ya wake waladi