• Anza
  • Iliyopita
  • 6 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 8070 / Pakua: 2060
Kiwango Kiwango Kiwango
UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA IMAM HUSEN

Mwandishi:
Swahili

1

UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA KISA CHA SAYYIDNA HUSSEIN

263. Na Huseni kuwasili, Hasha haya hakubali, Ya dhuluma na batili, Zote tungetabaradi

264. Angeitengeza haki, Tangu Kofu na Iraki, Hata huko Dimishiki, Ikafika yake yadi

265. Jamii sote raia, Roho zingefurahia, Angehukumu sharia, Yake Muungu Wadudi

266. Nasi tungekuwa naye, Tukafuata eziye, Tukaola asemaye, Jamii tukamrudi

267. Hayo wakisha yasema, Jamii watu wazima, Wakaona kuwa mema, Kuwa kheri na suudi

268. Jamii wakatamka, Na twandikeni waraka, Na mtu wa kwenda Maka, Tumuarifu Sayyidi

269. Wakataka karatasi, Ikaja hima upesi, Na kalamu ya nukhasi, Na wino mtasawadi

270. Wakatafuta katibu, Fasihi wa kiarabu, Khati wakaikutubu, Maneno wakaradidi

271. Bismillahi Jalali, Ila mtoto wa Ali, Mjukuu wa Rasuli, Tumwa wetu Muhammadi

272. Ila Sayyidi Huseni, Bun binti Amini, Twakuarifu yakini, Kwetu yanayotubidi

273. Ajile mtu kabihi, Jinale Abidallahi, Miji ameifusahi, Kwa hali ya kufisadi

274. Na aliyetuletea, Ni ibunu Muawiya, Mambo yametuzidia, Hatuwezi kujimudi

275. Ameingia 'lKofu, Kwa mambo yake dhaifu, Sote tumetawakafu, Kama tunao baridi

276. Kaziye kula haramu, Na watu kuwadhulumu, Hapana mwenye makamu, Awezaye kuradid

277. Ataka badili dini, Ya babu yako Amini, Sote tuwe taghiyani, Tusujudie Yazidi

278. Mwenye mke si mkewe, Mwenye mwana si mwanawe, Ni kama kuku kwa mwewe, Hali alivyotushidi

279. Na sasa twakuarifu, Twakutaka uje Kofu, Wala usitawakafu, Alla Alla ya Sayyidi

280. Maana ndiwe Khalifa, Wa babuyo Mustafa, Na wasaliao Kofa, Wote ni wako abidi

281. Hima ni kutujilia, Utamalaki raia, Ambaye hakuridhia, Juu yetu kumrudi

282. Tukusalimu eziyo, Ya babuyo na babayo, Na mwenye kufanya payo, Tumuonyeshe hadidi

283. Na Yazidi akitaka, Harubati na shabuka, I juu yetu daraka, Kuwana nae Yazidi

284. Vita vyake twavikifu, Jamii tulio Kofu, Wala usitie khofu, Wajapokuja juradi

285. Twavitosha vita vyake, Yeye na kaumu yake, Bora ni wewe ufike, Uje tukupe biladi

286. Ni hayo maneno yetu, Tafadhali bwana wetu, Twakutaka kuja kwetu, Na haiba tusirudi

287. Wakaukunda waraka, Roho zilifurahika, Tena wakaupeleka, Kwa upesi na juhudi

288. Basi risala akenda, Akizikata ya nanda, Pa milima akipanda, Majimbo yote na wadi

289. Hata akafika Maka, Kwake Huseni pulika, Na rukhusa akitaka, Hodi wenye nyumba hodi

290. Tena kataka idhini, Kuonana na Huseni, Akambiwa pita ndani, Ndiko kunako Sayyidi

291. Yule risala kangia, Kwa Huseni kangukia, Kampa akapokea, Waraka kaufaridi

292. Akayasoma Huseni, Yaliyomo warakani, Kuyaonakwe yuani, Risala kamtwaridi

293. Kautwaa warakawe, Akatowa mkonowe, Akampiga usowe, Khati ikamjalidi

294. Akampiga mateke, Yeye na waraka wake, Yule risala anguka, Toba na toba Sayyidi

295. Akampiga mabawa, Kwa hali ya kutukiwa, Yule risala kaawa, Kakimbia asirudi

296. Kakimbia kenda zake, Yeye na waraka wake, Hata akifika kwake, Wenziwe kawaradidi

297. Faraghani kiwataka, Akawambia hakika, Yaliyompata Maka, Sikuupata muradi

298. Kwa jamii wakanena, Twandike waraka tena, Maana mambo twaona, Kula siku kutuzidi

299. Wakawandika wa pili, Na maneno wakakuli, Bwana wetu tafadhali, Tulitakalo tubidi

300. Ukenda tena waraka, Huseni kaghadhibika, Na watatu wakandika, Kwa shauku za fuadi

301. Mwaka haujatimia, Khati wakamwandikia, Idadi yake sikia, Khati alufu idadi

302. Zote za kumuarifu, Twakutaka uje Kofu, Na Maulana hashufu, Hajali hata wahidi

303. Kula waupelekao, Hupiga risala wao, Katwa wasipate shuo, Wala kukidhi mradi

304. Walipojua yakini, Hataki kuja Huseni, Khati wakaizaini, Maneno wakasanidi

305. Wakawandika waraka, Kumtisha kwa Rabuka, Na kumpa maalaka, Kesho mbele ya Wadudi

306. Barua wakayandika, Ewe Huseni pulika, Khati tumezipeleka, Nyingi hazina idadi

307. Khati haziidadiki, Twakwita uje Iraki, Na wewe kuja hutaki, Na sasa twakuradidi

308. Kesho mbele ya Khaliki, Tutakwenda kushitaki, Ukatupe zetu haki, Hapo mbele ya Wadudi

309. Tutamwambia Manani, Twalimwambia Huseni, Tuli hali duniani, Asitake kutufidi

310. Yote twalimkalimu, Ya kwamba tu madhulumu, Asitake tuhukumu, Akakataa kusudi

311. Nasi leo Mola wetu, Twazitaka haki zetu, Shaurilo bwana wetu, Lipi utaloradidi?

312. Haki zote utatoa, Za wenye kudhulumiwa, Ukae ukitambua, Na kwamba hayana budi

313. Wala huna la kusema, La kumjibu Karima, Hiyo siku ya kiama, Ila kulipa junudi

314. Utawalipa khaliki, Wa Kofu na wa Iraki, Huna utakakobaki, Ibada uloabidi

315. Kwisha kwandika barua, Risala wakamtoa, Barua kaitukua, Kenda hata kwa Sayyidi

316. Alipowasili Maka, Kwa Huseni akafika, Barua akaishika, Kusoma akiadidi

317. Alipokwisha isoma, Muwili ukatetema, Mfano anaye homa, Au la nyingi baridi

318. Huseni katetemeka, Kwa kumkhofu Rabuka, Na matozi kumtoka, Ndia mbele yakabidi

319. Matozi yakamuawa, Kwa kucha kushitakiwa, Na haki kwenda zitowa, Za jamii ya junudi

320. Akalia Maulana, Na kufazaika sana, Kwa kumkhofu Rabana, Watu kwenda mjalidi

321. Akisha kulia mno, Keta dawati na wino, Akayandika maneno, Kwa lafudhi tajididi

322. Waraka kaukutubu, Ila kafa 'lmuhibu, Maneno mulonijibu, Yamenichoma fuadi

323. Khati zalotangulia, Maneno mulonambia, Yote sikuyaridhia, Zote nalizitaridi

324. Wa ama khati ya mwisho, Imekithiri matisho, Kwenda nishitaki kesho, Kwa Mola wetu Wadudi

325. Nami sasa sina huja, Wala sina jambo moja, Litaloniasa kuja, Tasafiri sina budi

326. Nimemleta fahamu, Ndugu yangu Mselemu, Aje akae makamu, Ya sala na kusujudi

327. Akae msikitini, Na kadhi ni Nuamani, Awahukumu mjini, Kula mwenye kutaadi

328. Mselemu na asali, Na Nuamani ni wali, Na karibu tawasili, Kwa amri ya Wadudi

329. Kwisha kwandika fahamu, Kaufunga marukumu, Akamwita Mselemu, Ndoo hima bunu jadi

330. Mselemu kawasili, Maulana akakuli, Ewe ibni Akili, Sikia nakuradidi

331. Nenda ukatwae sefu, Uje nikutume Kofu, Na wendapo tawakafu, Uwasalishe junudi

332. Nenda kasalishe wewe, Nuamani aamuwe, Wala mangine yasiwe, Na mimi najizadidi

333. Nawakusanya ghulamu, Na tweka za bahaimu, Siku haba hazitimu, Ndio yangu makusudi

334. Mselemu ketikia, Marahaba mara mia, Hali ya kufurahia, Utumwa wake Sayyidi

335. Akanena Inshalla, Ewe aba Abdalla, Mimi naona fadhila, Nenolo tajitahidi

336. Hivi sasa nenda kwangu, Nenda twaa uda zangu, Niwaage na wanangu, Farasi tamjalidi

337. Akenenda Mselemu, Kaaga wake ghulamu, Akakaa na hasamu, Sefuye kaikalidi

338. Kamzaini farasi, Akampanda upesi, Roho ina wasiwasi, Kandamana na abidi

339. Wakenda pasi muhula, Yeye na yule risala, Wala pasiwe kulala, Hata kunako biladi

340. 'lKofu wakiwasili, Jamii ya kabaili, Wakafurahi kwa kweli, Furaha kubwa shadidi

341. Wote wakafurahika, Na roho zikasafika, Wakajua ni hakika, Atawasili Sayyidi

342. Hata kukicha yuani, Wakenda kwa Nuamani, Na waraka mkononi, Kapewa kaufaridi

343. Waraka kuusomake, Kafurahi roho yake, Na maneno atamke, Tahukumu sina budi

344. Namshukuru Rabana, Kuwasili Maulana, Tena adhabu hapana, Hana budi kutufidi

345. Akaketi Mselemu, Na watu kumkirimu, Kina wakimuheshimu, Heshima kubwa shadidi

346. Kasali msikitini, Na wote ajmaini, Asubuhi na jioni, Nahari na tasaridi

347. Ali akiwasalisha, Kwa magharibi na isha, Asubuhi huwamsha, Wakenda wakaabidi

348. Wote wakasali naye, Pasiwe akataaye, Akayakini rohoye, Dini watajitahidi

349. Na huyule Nuamani, Akahukumu mjini, Jamii ya khasimani, Kufunga na kujalidi

350. Sasa nyuma turudini, Niwakhubiri Huseni, Kuwatiakwe ndiani, Mselemu na abidi

351. Kimaa kutangulia, Na khati kuwandikia, Asinyamaze kulia, Kula mara akazidi

352. Akondoka hiyo hina, Kenda hata kwa Sakina, Na matozi kumpuna, Usoni yakajamidi

353. Akamwambia mwenzangu, Waliza nini ndu yangu, Huseni hwishi matungu, Daima zote abadi?

354. Huseni akatamka, Nimeletewa nyaraka, Alufu zenye kwandikwa, 'Lhaji hata 'Lkadi

355. Zote hazipurukusha, Ila hino ya kiisha, Ndio iliyonitisha, Kwa mambo yaloradidi

356. Wa Kofu wamenambia, Kesho mbele ya Jalia, Hawatakwenda ridhia, Watakwenda nijalidi

357. Wanitake haki zao, Hao wadhulumi wao, Au niwasili kwao, Hawondolee Yazidi

358. Na sasa tuwasafiri, Na tupandane bairi, Pasiwe tena usiri, Tutawakali Wadudi

359. Tupandeni twende zetu, Na wote watoto wetu, Waama haki za watu, Kesho zitaziadidi

360. Sakina akanatiki, Safari hiyo sitaki, Kwenda Kofu na Iraki, Wakwita kukuhusudi

361. Safari na ivundike, Wala usihadaike, Maneno yao sishike, Wale ni watu fisadi

362. Maneno yao kidhabu, Ndimi zao makilubu, Waweza wapi harubu, Asili yao Hunudi

363. Huseni akatamka, Safari haina shaka, Wala haitavundika, Kwenda zangu sina budi

364. Sakina akakalimu, Na kwamba umeazimu, Na tupishe Muharamu, Hata ingie Jamadi

365. Kwani Tumwa Muungamu, Alisema yako damu, Shahari 'l Muharamu, Ndipo itapomadidi

366. Nae Huseni anene, Sakina tusishindane, Kenda Huseni mwengine, Babu aliyeradidi

367. Na Sakina akakuli, Siku moja Jibrili, Alikuja kwa Rasuli, Na mchanga msafidi

368. Alitukua mchanga, Mzuri uketa anga, Rasuli akiufunga, Kitambaani jadidi

369. Jibrili kabaini, Mtanga wake Huseni, Siku zote uwoleni, Hata ukitasawadi

370. Muuonapo na damu, Tambuani imetimu, Ajali yake ghulamu, Kautwaa Muhamadi

371. Kampa mama Fatuma, Akenda uweka vema, Ningoja tautazama, Sasa hivi tutarudi

372. Sakina akaondoka, Akenda akaushika, Wote umehamirika, Tena umetasawidi

373. Kaja nao hima hima, Akamwambia tazama, Huseni katakalama, Subhana ya Wadudi

374. Huseni akadhukuri, Sina budi tasafiri, Rabi alilokadiri, Siwezi litabaidi

375. Kuona kwake Sakina, Hana budi Maulana, Akondoka iyo hina, Na matozi yakabidi

376. Kenda kwa bunu Zuberi, Akamweleza khabari, Na kushitadi safari, Wala nyuma hairudi

377. Abdalla akondoka, Kwa upesi na haraka, Kwa Maulana kifika, Kalia akaradidi

378. Abdalla akanena, Huseni utatupona, Wala usipo maana, Ya kwenda zako Sayyidi

379. Keti usende Iraki, Wala usitaharaki, Kwamba ni huo muluki, Utakapo maujudi

380. Ulitakalo twambie, Upesi tukufanyie, Huseni amrudie, Tasafiri sina budi

381. Wala sitazuilika, Msijikuse mashaka, Hivino sasa natoka, Nawe Abdalla rudi

382. Abdalla katongoa, Kheri nami nitukuwa, Kula litakalokuwa, Niwepo nilishahidi

383. Kwamba hapano hutaki, Maka kuitamalaki, Shati wenende Iraki, Twenende sote Sayyidi

384. Kwani watuwe jahili, Wala haya si ya kweli, Wakitwa kwenda kudhili, Ndio yao makusudi

385. Tawatukua kaumu, Wana wa bani Hashimu, Wavundao jiwe gumu, Na wenginewe junudi

386. Nende na watu alufu, Wa rumuhi na suyufu, Nende haipande Kofu, Kwa jeuri na taadi

387. Nitukuwe panga kali, Nende mimi hakuwali, Na asemaye si kweli, Nimtoe uritadi

388. Hakusalimishe nti, Pasi kuwa harubati, Niwete makubarati, Na ahali 'l biladi

389. Niwausie maneno, Shekhe Huseni huyuno, Pasiwe na mnong'ono, Wala mwenye kutaadi

390. Nisikize asemaye, Nimuangushe rasiye, Hata nti ituliye, Nishike ndia nirudi

391. Huseni akamjibu, Hasanta ya muhibu, Ama siyo matulubu, Wala si wangu mradi

392. Tatawakali Muungu, Nende mimi peke yangu, Na hawa watoto wangu, Sitaki mtu wahidi

393. Abdalla akalia, Kina akiombolea, Khatima akarejea, Asiweze mkaidi

394. Basi akazipakia, Twika twika za ngamia, Na watu wake dhuria,Katawakali Wadudi

395. Katukua panga kali, Watu sitini rijali, Wasio kucha mahali, Wangiapo hawarudi

396. Na sabaati ashara, Watoto wa watu bora, Sabuini anfara, Na sabaati zaidi

397. Asikari ni sitini, Na watoto wa Hasani, Na wake yeye Huseni, Saba ashara idadi

398. Wali vijana pulika, Wa ithnaashara Maka, Ila panapo shabuka, Wapita hao asadi

399. Kwisha sayo pakhubiri, Huseni akasafiri, Madinati munawiri, Ndipo alipokasidi

400. Sikuhaba kawasili, Madinati ya Rasuli, Akanenda tasihili, Kwa nduguye Muhamadi

401. Akiwasili nyumbani, Nduguye yu kitandani, Yuna maradhi zamani, Hawezi yote jasadi

402. Kumuonakwe nduguye, Akashituka rohoye, Kamba Huseni ni weye, Wenda wapi niradidi

403. Mbona una atifali, Na wake na marijali, Kama wendaye mahali, Tena kuliko baidi

404. Huseni akatamka, Ni kweli hayo hakika, 'l Kofu napenda fika, Ndiyo yangu makusudi

405. Kamwambia moja moja, Na khati zilizokuja, Na jamii ya miuja, Asibakie wahidi

406. Na khati ya kwishilia, Na waliyomwandikia, Nduguye akasikia, Akanena Muhamadi

407. Akanena La Haula, Illa billahi taala, Ewe aba Abdalla, Safari ya Kofu rudi

408. 'lKofu waisa nini, Ewe 'lakhi Huseni, Au kuna haja gani, Ni upi huko mradi?

409. Wa Kofu wakuhadaa, Na wewe yakakutwaa, Huwajui kwamba baa, Tangu jadi na jududi

410. Khasa sisi nyumba yetu, Jamii mauti yetu, Kula atokaye kwetu, Akenda Kofu harudi

411. Wameua baba yako, Na Hasani ndugu yako, Na wewe wenenda huko, Ili kwenda jihusudi

412. Na kwamba wataka kwenda, Safari huwezi vunda, Ngoja Rabi akipenda, Nione vema jasadi

413. Twandamane mimi nawe, Kula mtu upangawe, Tungie Kofu tuawe, Kwa amri ya Wadudi

414. Twenendapo panga mbili, Za wana wa Shekhe Ali, 'lKofu twaikabili, Kuingia na kurudi

415. Ila kwenenda pekeyo, Haunipi wangu moyo, Akisha kusema hayo, Huseni akamrudi

416. Takwenda mimi natosha, Sihitaji mshawasha, Wala sitaki juyusha, Kwandamana na junudi

417. Muhamadi akalia, Kwa kuto amridhia, Abdalla kaawiya, Bun Abbasi Sayyidi

418. Kamuuliza Huseni, Mbona una kharisani, Na wewe waliza nini, Ya 'lakhi Muhamadi

419. Huseni akadhukuri, Yakhi napenda safari, Akamweleza khabari, Kama yaliyo kubidi

420. Kamweleza tangu mwanzo, Khati apelekewazo, Khabari alizo nazo, Abdalla kiadidi

421. Huseni akimaliza, Abdalla akiwaza, Tena akimkataza, Kina akimradidi

422. Kamwambia tawakafu, Sende Iraki na Kofu, Kwa mambo yao dhaifu, Waliyo nayo abadi

423. Wa Kofu ni wanafiki, Uongo hawakutaki, Wala walio Iraki, Hao ndio mahasidi

424. Kwamba umependa moyo, Kusafiri ndia hiyo, Ngoja apoe nduguyo, Mtukue na junudi

425. Nami ningiye ndiyani, Nitukue farisani, Kama watu alufeni, Watambuao hadidi

426. Nende Kofu maridhiwa, Niingie na kuawa, Na ambae ajinuwa, Nimrudishe arudi

427. Nikakuweke Iraki, Hisha handame tariki, Nende zangu Dimishiki, Hamrakidhi Yazidi

428. Wendapo upanga wako, Na wangu ukawa huko, Thama nao ndugu yako, Upangawe Muhamadi

429. Zenendapo panga tatu, Tena hizi panga zetu, Tambua hakuna mtu, Awezaye tujalidi

430. Huseni akatamka, Abdalla pumzika, Hivino sasa natoka, Niombeani Wadudi

431. Sihitaji upangao, Wala huo usemao, Watosha nilio nao, Wa kula litalobidi

432. Akalia Abdalla, Bun Abbasi Fadhila, Na kusema La-Haula, Pamoja na Muhamadi

433. Na watu wote Madina, Jamii wakalizana, Kwa kwondoka Maulana, Yali msiba shadidi

434. Huseni asiridhike, Akenda kwa babu yake, Kenda zuru yeye peke, Khatimaye akarudi

435. Alipokwisha zuari, Kaitengeza safari, Katawakali Jabari, Kamwelekea Samadi

436. Hata bara akifika, Wakashuka malaika, Wana panga wameshika, Na silaha za jihadi

437. Wakamwambia Huseni, Tumeletwa ni Manani, Ili kwenda kuawini, Kwa kula litalobidi

438. Kwamba wataka twambie, Safari yako tungie, Hutaki turejeee, Huseni akaradidi

439. Huseni akawambia, Ni kheri kurejeea, Na apendalo Jalia, Amriye hairudi

440. Malaka wote yakini, Wakarejea mbinguni, Akenda zake Huseni, Hata kafika baidi

441. Akawaona majini, Ambao ni waumini, Wote wamejizaini, Kwa silaha za hadidi

442. Amiri wao kwa mbele, Fijaadumu jinale, Kaja kasimama mbele, Usoni kwake Sayyidi

443. Yule jini akakuli, Ewe ibnu Batuli, Kwenda peke sikubali, Nami nenda sina budi

444. Taichukuwa kaumu, Wenye silaha za sumu, Nende haingie Rumu, Niwachawanye junudi

445. Tawatukua watoto, Wenye dharuba nzito, Na marumuhi ya moto, Na silaha kama radi

446. Nikae usoni kwako, Kwa kula adui yako, Nimuonyeshe vituko, Atakaye tamaridi

447. Huseni akakalimu, Marahaba Fijadumu, Sitaki hata kaumu, Rudi na watuo rudi

448. Natawakali Jalia, Sitaki mtu mmoya, Majini wakarejea, Na matozi yakabidi

449. Katawakali Jabari, Mle katika safari, Akawaona namiri, Na ukuba wa asadi

450. Kaona chui na simba, Na kucha kama vigumba, Usonikwe wamewamba, Jamii wakaradidi

451. Wote kauli walete, Maulana twende sote, Adui tukawakate, Tule nyama tufaidi

452. Wala usitukataze, Sayyidi tutangulize, 'l Kofu tukailaze, Jamii iwe baridi

453. Huseni akawambia, Nyote ni kurejeea, Siwezi kulizuia, Alipendalo Wadudi

454. Hata mbele akifika, Akawaona majoka, Mbele yamejitandika, Wanao sumu shadidi

455. Kaona wamesimama, Majoka kama milima, Wote wakatakalama, Wakamwambia Sayyidi

456. Sayyidi situkataze, Twataka tukawameze, 'l Kofu tusiisaze, Jamii tuisafidi

457. Tutangulie usoni, Tukawatie tumboni, Uje kule na amani, Hakuna tena hasidi

458. Huseni akawajibu, Siyo yangu matulubu, Natawakali Wahabu, Aliye pweke Wahidi

459. Kwisha sayo pakhubiri, Wakamjilia tiri, Mbao wamezinashiri, Sanguri na kanfadi

460. Madege yenye midomo, Wala yasiyo ukomo, Wakaja kwa kitetemo, Akanena hodi hodi

461. Hodi hodi atongoe, Sayyidi wetu ni wewe, Twataka tukawambue, Kufari na mayahudi

462. Twataka tutangulie, 'lKofu tukaingie, Hata ukifika weye, Wote wamesitajidi

463. Maulana kadhukuri, Endani zenu tairi, Sitaki jeshi kathiri, Wa kwenenda nisaidi

464. Huseni asikubali, Wote niliowakuli, Akataka tawakali, Katika yake fuadi

465. Wote asiwaridhie, Pia walosema nae, Kataka yeye pekee, Kutawakali Wadudi

466. Katawakali Rabana, Mwenye ezi Subhana, Kwa usiku na mchana, Kenda akajitahidi

467. Baada hayo kukoma, Ya dhuria wake Tumwa, Natamani rudi nyuma, Niwakhubiri Yazidi

468. Mambo yasichanganyike, Moja moja niliweke, Yazidi kusikiakwe, 'lKofu yanayobidi

469. Akasikia hakika, Wa Kofu wamekwandika, Barua za kwenda Maka, Kumwamkua Sayyidi

470. Khati wamemuarifu, Idadi khati alufu, Wamtaka aje Kofu, Waje wampe biladi

471. Huseni hakuridhia, Na khati ya kwishilia, Yote waliyomwambia, Kesho mbele ya Wadudi

472. Na hivi sasa fahamu, Amekuja Mselemu, Kuwasalisha kaumu, Juu yake Masijidi

473. Na kadhi ni Nuamani, Ahukumuye mjini, Na Huseni yu ndiani, Na akali ya junudi

474. Nao wametangamana, Wa Kofu na Maulana, Na ukitaka pigana, Wao watamsaidi

475. Wakunyang'anye na ezi, Wakutwae wakuhizi, Usitambue makazi, Wala pa kwenda rajidi

476. Wakunyang'anye eziyo, Na jamii ya maliyo, Yazidi kupata hayo, Akili zikasharidi

477. Hayo akiyafasili, Zikamruka akili, Keta wino tasihili, Na lohi njema jadidi,

478. Waraka kaunasihi, Kwa khati njema malihi, Ya akhi Abidillahi, Sikia bun Ziadi

479. Khabari nimepulika, Kofu yanayotendeka, Huseni wamemtaka, Kwa shime na jitihadi

480. Wa Kofu na wa Iraki, Wamwita kutamalaki, Na mimi hawanitaki, Katika zao fuadi

481. Wametukiwa na miye, Watamani nangamiye, Ezi isinijuzie, Ni huo wao mradi

482. Na wote shauri moja, Huseni akisha kuja, Harubu hapana hoja, Na vita hapana budi

483. Na hivi sasa Huseni, Ametoka yu ndiani, Na kadhi ni Nuamani, Ndie kadhi maujudi

484. Na aliye tangulia, Ni Mselemu sikia, Naye wamemridhia, Kuwasalisha junudi

485. Aliyekuja fahamu, Jina lake Mselemu, Mwana wa bani Hashimu, Yumo katika biladi

486. Hayo nilipokwambia, Roho yakinishitua, Na kwamba nawe wajua, Basi u wangu hasidi

487. Kwamba unazo khabari, Hukuwa mtu wa kheri, Labuda mu mashauri, Wewe na hao junudi

488. Kwamba hunazo dalili, Basi enda tasihili, Ukifika kamdhili, Huyo mwenye masijidi

489. Kamuue Mselemu, Ajili mchache damu, Na rasi yake fahamu, Na ije huko baidi

490. Rasi yake niletea, Alla Alla nakwambia, Baada hayo sikia, Kwa Nuamani ubidi

491. Kamwambie Nuamani, Angie mwangu taani, Afanyapo ushindani, Ajili kumuhusudi

492. Umkate rasi yake, Utwae na mali yake, Na mjini uzunguke, Jamii wote junudi

493. Utenze anitakaye, Mali yake muwatie, Na mtu akataaye, Mkutuli asirudi

494. Umngoje na Huseni, Umtiye mautini, Na rasiye iyo hini, Ije na wake waladi

495. Huseni umuuapo, Rasiye na ije papo, Na jamii kilichopo, Wana na wake abidi

496. Ajili kuyafanyiza, Yote nilokuagiza, Nami najua waweza, Hayo na hayo zaidi

497. Najua yatafanyika, Pasipo kuharibika, Nisingali kukuweka, Hakupa na uSayyidi

498. Ni kukujua mamboyo, Waweza kufanya hayo, Na kadiri nitakayo, Wanikidhia mradi

499. Waraka kaukhitimu, Kaufunga marikumu, Kamsalimu hadimu, Kwenda kwa bun Ziadi

500. Akenda hima mtumwa, Pasi kuwa kasimama, Siku haba zikikoma, Kafika kwa jitihadi

501. Kuwasilikwe asahi, Akatoa mansahi, Kampa Abidillahi, Usoni kausujudi

502. Akisha kusujudia, Khati akiangalia, Yaliyokwandikwa pia, Jamii kayaadidi

503. Alipokwisha yaona, Maneno ya wake bwana, Akafurahika sana, Furaha kubwa shadidi

504. Akajua ni hakika, Yazidi ameniweka, Nitakalo lafanyika, Kwa pendo lake Yazidi

505. Baada sayo fahamu, Akaagiza kalamu, Na lohi njema ya Shamu, Khati akaimadidi

506. Ila bunu Muawia, Maneno ulonambia, Na mimi nalisikia, Na watu mtasharidi

507. Haona ni upumbavu, Nisiyashike kwa nguvu, Na kwamba sasa mapevu, Takwenenda sina budi

508. Bwana takutumikia, Kama uliyonambia, Jamii yatatimia, Uyatakayo Sayyidi

Tuliza nafusi yako, Sasa hivi nenda kuko, Najua ezi ni yako, Tangu jadi na jududi

510. Twajua bwana u wewe, Wala hako mwenginewe, Na asemaye welewe, Yuataka jihusudi

511. Rasi mbili utakazo, Naona kama matezo, Na jamii maagizo, Hata moja halirudi

512. Baada ya kuyandika, Kampa tume waraka, Akenda hima haraka, Kama kuvuma baridi

513. Kwa Yazidi kiwasili, Khati akaifasili, Akafurahi kwa kweli, Na mahaba akazidi

514. Baada sayo asahi, Kondoka Abidillahi, Akazipiga siyahi, Kawakusanya junudi

515. Akamba Ya maishara, Mlo mji wa Basara, Ajilini mwa hadhara, Mje tuole taadi

516. Wakakutana sufufu, Sitaashara alufu, Ambao ni mausufu, Watambuao hadidi

517. Wakafika wakasema, Ni wapi penye nakama, Aula penye kilema?, Tukirudishe kirudi

518. Naye akawaarifu, Naweta twende 'lKofu, Ndiko kwenye hitilafu, Wamuasio Yazidi

519. Wakayandama darubu, Kama rihi ya shabubu, Hali ya kutaghadhabu, Na roho kutasawidi

520. 'lKofu wakikaribu, Abidallahi kajibu, Akawambia sahibu, Taka nifanye mradi

521. Ngojani nitangulie, Wa Kofu niwangilie, Kwamba wanipenda mie, Tawaona sina budi

522. Akazifanya hadaa, Nguo nyeupe kavaa, Na ngamia kamtwaa, Na bakora msafidi

523. Kaiwata kaumuye, Akenda yeye pekee, Wa Kofu kumuonaye, Wakadhani ni Sayyidi

524. Wa Kofu na wa Iraki, Wakenda wakamlaki, Na furaha kusabiki, Katika zao fuadi

525. Jamii watu mjini, Wakadhani ni Huseni, Wakangia furahani, Iliyo kubwa shadidi

526. Pasiwe mtu kukaa, Wakatoka kwa fazaa, Kusudi kwenda mtwaa, Waje wampe biladi

527. Kufika wakamuona, Abidallahi laana, Kwa jamii wakanena, Hima upesi nirudi

528. Kumbe ni Abidallahi, Amekwisha tufedhehi, Roho zao zikatwahi, Kwa mara hiyo wahidi

529. Wakambiana ajabu, Mambo tumeyaharibu, Hatukwenda taratibu, Ndipo saya yakabidi

530. Abidallahi kangia, Na watuwe wote pia, Usiku kujilalia, Na wote wake junudi

531. Kulipokucha yuani, Kaamuru maluuni, Kulia mbiu mjini, Wakutane masijidi

532. Basi mbiu ikalia, Mwatakwa jote jamia, Basi jeshi ikangia, Waungwana na abidi

533. Wakenda msikitini, Ma Shekhe na Madiwani, Na wakubwa wa mjini, Na jamii ya muridi

534. Kimaa kukutanika, Abidallahi katoka, Msikitini kifika, Mimbarini akanadi

535. Kwa kweleza mimbari, Kanadi akidhukuri, Ya Maishara jifiri, Sikizani niradidi

536. Tumesikia yakini, Kwamba wenu Sultani, Mmemkiri Huseni, Hamumtaki Yazidi

537. Basi semani sadiki, Wa Kofu na wa Iraki, Yazidi hamumtaki, Kweli mmemtaridi?

538. Kimaa kuwauliza, Jamii wakanyamaza, Na tena likawataza, Neno watakalorudi

539. Jamii wakasakiti, Pasi mtoa sauti, Tena akatoa khati, Itokayo kwa Yazidi

540. Akausoma waraka, Jamii wakapulika, Yote yaliyo kwandika, Wakasikia junudi

541. Tena sapo akakuli, Nambiani tasihili, Maneno haya ni kweli, Nambieni maujudi?

542. Kimya wakanyamazana, Pasiwe mwenye kunena, Abidallahi laana, Kuwambia akazidi

543. Akawambia wa Kofu, Ili kuwatia khofu, Yazidi kaniarifu, Nije kwenu makusudi