• Anza
  • Iliyopita
  • 6 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 8073 / Pakua: 2060
Kiwango Kiwango Kiwango
UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA IMAM HUSEN

Mwandishi:
Swahili

2

UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA KISA CHA SAYYIDNA HUSSEIN

544. Nimtazame ambaye, Huseni ampendaye, Nimuangushe rasiye, Na wote wake waladi

545. Na jamii mali yake, Niyatwae niyateke, Dimishiki nipeleke, Ni huo yangu mradi

546. Basi semani upesi, Nijue yenu jinsi, Wote wakenika rasi, Wa khofu nyingi fuadi

547. Jamii wakiolana, Khatimaye wakanena, Aliye bwana ni bwana, Huseni au Yazidi

548. Kwa kula atawalaye, Tutafuata eziye, Hatuna tukataaye, Ali yoyote Sayyidi

549. Kusikiakwe adui, Akaruka kama chui, Kawambia hamjui, Kwamba nyinyi mu abidi

550. Na Yazidi bwana wenu, Aliyemiliki kwenu, Ni haba akili zenu, Ujinga unawazidi

551. Kwamba mmemridhia, Zidi bunu Muawia, Afadhali kutulia, Make mtabaradi

552. Ambaye hakumtaka, Yuwatafuta hilaka, Mimbarini akishuka, Hayo akisha radidi

553. Kitoka msikitini, Akenda kwa Nuamani, Akampa anuwani, Itokayo kwa Yazidi

554. Alipokwisha ijua, Nuamani kamkua, Sisi hatuna uluwa, Wala hatu maSayyidi

555. Ila sisi tu raia, Twawapenda wote pia, Wala hatutakimbia, Kwa amri ya Wadudi

556. Kusikiakwe makali, Abidallahi jahili, Akamnyang'anya mali, Mangi yasiyo idadi

557. Beti asimbakiye, Ila ni yeye rohoye, Sababu asimwambie, Nimpendaye Yazidi

558. Kashukuru Nuamani, Na kuhimidi Manani, Baada sayo yuani, Abidallahi karudi

559. Kenda nyumba ya hukumu, Akawatoa kaumu, Katafuta Mselemu, Katika yote biladi

560. Na Mselemu sikia, Kipindi kilipongia, Ajili kukimbilia, Beti 'l masjidi

561. Akenda akaadhini, Kakaa msikitini, Wote walio mjini, Asimuone wahidi

562. Kasali yeye pekee, Hapo amfuataye, Kataajabu rohoye, Ajabu kubwa shadidi

563. Kwisha kusali yuani, Katoka msikitini, Kamuona ghulimani, Karibu amekaidi

573. Allahumma niauni, Unitie nusurani, Na jeshi ya maluuni, Bi shufaa Muhamadi

564. Mselemu akanena, Nambia ewe kijana, Leo mji nauona, Jamii wote baridi

565. Watu wametaharaki, Gharibi na mashariki, Kusali hawakutaki, Kijana akaradidi

566. Kijana akakalimu, Wailaka Mselemu, Huoni hawa kaumu, Walivyo kujizadidi

567. Jamii wamekuhuni, Hawakutaki mjini, Wala nduguyo Huseni, Hawapendi mshahidi

568. Akamwambia asahi, Mambo ya Abidallahi, Na roho zao kutahi, Na warakawe Yazidi

569. Na wewe wakutafuta, Na pindi wakikukuta, Kitwa chako kitakatwa, Kuuwawa huna budi

570. Ukae ukitambua, Huna budi kuuwawa, Mselemu kamkuwa, Subhana ya Wadudi

571. Akitazama yamini, Asimuone auni, Akiola shimalini, Asione msaadi

572. La haula akasema, Illa billahi Karima, Kamkua Allahumma, Ya Allahu ya Samadi

574. Mara ile kenda zake, Katwaa upanga wake, Ilihamu roho yake, Na matozi yakabidi

575. Silaha kajizaini, Roho haina makini, Akatembea mjini, Makusudi kusharidi

576. Azima ni kukimbia, Hanapo pa kuawia, Mumule katika nyia, Pana nyumba msafidi

577. Na nyumba hiyo yuani, Mwenyewe akitwa Khani, Ali mzee zamani, Wa tangu jadi na jadi

578. Lakini ni Islamu, Yu dini ya Muungamu, Na wote bani Hashimu, Kiwapenda jitihadi

579. Akiwapenda sikia, Dhuria wake Nabia, Na wote 'l Hashimia, Pendo lisilo idadi

580. Kenda kwake Mselemu, Mlangoni akakumu, Kamuuliza khadimu, Yu wapi wako Sayyidi

581. Na kwamba yu humo ndani, Mwambie pana mgeni, Kenda hima ghulumani, Khani akamradidi

582. Mzee Khani kajibu, Na'pite hima gharibu, Akapita Muarabu, Mlango kaukaidi

583. Wakenda wakaonana, Khabari wakauzana, Mselemu akanena, Kama yaliyombidi

584. Khabari akamweleza, Tokea mwanzo wa kwanza, Na jamii miujiza, Hata ya bunu Ziadi

585. Na hivi sasa rijali, Wa kati kunidalili, Wapate kunikutuli, Kwetu Maka nisirudi

586. Kisha sayo kutamka, Khani akaghadhabika, Kwa hayo yalofanyika, Ghadhabu kubwa shadidi

587. Kanena mzee Khani, Na kwamba yali zamani, Sasa ningejizaini, Henda hawa na jihadi

588. Kama banii Hashimu, Huwaje kuwalaumu, Ukataka wadhulumu, Huo ndio wa hasidi

589. Lakini sasa pulika, Hapa umesitirika, Kwa amri ya Rabuka, Watakwisha usitadi

590. Na huyo akutakaye, Rafiki yake ni miye, Labuda asisikiye, Kwamba siwezi jasadi

591. Lakini asikiapo, Hana budi kuja papo, Na pindi hapa ajapo, Kumuua huna budi

592. Ajapo akiwasili, Taja kuweka mahali, Na upangao mkali, Ungoje akikaidi

593. Taja muwekea kiti, Hata akisha keleti, Umuonyeshe mauti, Ahimari na suwedi

594. Akisha kusema hayo, Mselemu kamba ndiyo, Akafurahika moyo, Kwa Khani aloradidi

595. Abidallahi hakika, Siku mbili zikifika, Roho akatia shaka, Khani hajamshahidi

596. Kauliza barazani, Yu wapi mzee Khani?, Kambiwa yuko nyumbani, Ana maradhi shadidi

597. Mara kondoka kitini, Kusudi kwenda kwa Khani, Akipata mlangoni, Kamba wenye nyumba hodi

598. Kisikia sautiye, Wakajua kwamba ndiye, Tena Khani amwambie, Mselemu jizadidi

599. Shika sefu na turusi, Ukae pia nafasi, Hata akisha jilisi, Sikawe kumhusudi,

600. Mselemu kajifita, Paziani akapita, Na sefu kaitafuta, Isiyo shaka na budi

601. Akiweka na siriri, Akitengeza vizuri, Tena kapewa amri, Kupita bun Ziadi

602. Basi akapita ndani, Akaonana na Khani, Mselemu faraghani, Seifi kaikalidi

603. Tena kampa maungo, Khani akamba Muungu, Leo atakata shingo, Ipukane na jasadi

604. Kakaa muda mzima, Khani akaona kimya, Kafazaika mtima, Mbona kimya kinazidi?

605. Basi akatoa fumbo, Kama aimbae wimbo, Akamba mambo si mambo, Si ya jadi na jududi

606. Hino ndiyo kazi yenu, Mliyozoea kwenu, Si kazi yao sununu, Katika zote abadi

607. Kutuka akamuonya, Ni kazi yenu mwafanya, Wala sikukudanganya, Niliyokupa ahadi

608. Nakwambia mara zote, Simama ukiokote, Na lijirilo tu sote, Kwa amri ya Wadudi

609. Khani akisha yasoza, Fumbo la kumuhimiza, Mselemu kanyamaza, Hata saa ikabidi

610. Kasema mara ya pili, Mselemu katwawili, Abidallahi kakuli, Naona mwataradidi

611. Unani mzee Khani, Kwondoa taji kitwani, Ukabanja kitandani, Khatima ukalirudi?

612. Mara wavua kilemba, Na mara nyimbo ukimba, Unani katika nyumba, Jambo lililokuzidi?

613. Mzee Khani kakuli, Ni jua liwapo kali, Hunipungua akili, Na ndwele ikashitadi

614. Ndipo hivi hafanyiza, Fiili na miujiza, Ni ndwele imenikaza, Na akili msharidi

615. Abidallahi kasema, Kwa kheri narudi nyuma, Nijile kukutazama, Khani akenda muwadi

616. Aliporudi nyumbani, Kasema mzee Khani, Mselemu jinsi gani, Usitimize ahadi?

617. Mselemu akakuli, Sefu yali masiluli, Hataka kumkutuli, Hazuiwa yangu yadi

618. Hitaka mwandika sefu, Nimpasue nusufu, Nikasikia khatifu, Na mnada ukanadi

619. Mnada ukatongoa, Usende ukamuua, Na muili hazuiwa, Kujondoa sijimudi

620. Ndipo saya yakajiri, Na zohali na usiri, Na Khani akadhukuri, Kheri ni yake Wadudi

621. Baada sayo asahi, Kondoka Abidallahi, Akili katanabahi, Kuzichawanya nakidi

622. Roho yake kaazimu, Azitoe darahimu, Atafute Mselemu, Kwa akili na juhudi

623. Kamwamkua rijali, Jina lake Muakali, Ubazazi na khitali, Apita wote junudi

624. Dinari kazihesabu, Alufu tatu dhahabu, Na maneno kamjibu, Shime yakhe jitahidi

625. Mtafute Mselemu, Kwa akili na fahamu, Ukampe darahimu, Ukisha mpa urudi

626. Ujue nyumba aliyo, Kwa rai na akiliyo, Muakali kamba ndiyo, Inshallah tajitahidi

627. Akondoka Muakali, Akayatukua mali, Akenda akadalili, Katokea masijidi

628. Akaona msikiti, Kaingia akaketi, Ilipofika salati, Akaja mtu wahidi

629. Jina kitwa Mselemu, Bun Ghaushi fahamu, Kaja kampa salamu, Na heshima kamzidi

630. Kamwambia ndugu yangu, Takupa faragha yangu, Maana humu si mwangu, Mimi natoka baidi

631. Mimi ni mtu wa Maka, Huseni kanipeleka, Nitukuzie waraka, Na mali yaso idadi

632. Nijile na darahimu, Kuja mpa Mselemu, Na alipo sifahamu, Nimekwisha usitadi

633. Na kuuliza siwezi, Mji unavyo makonzi, Na mimi ni mwanagenzi, Sijui mtu wahidi

634. Na wewe kukubaini, Ni kwamba natumaini, Yakhi fanyiza hisani, Na haiba nisirudi

635. Twende ukanipeleke, Hampe amana yake, Hima upesi nitoke, Humu siwezi rajidi

636. Kanionyeshe upesi, Hapo alipojilisi, Roho ina wasiwasi, Mselemu karadidi

637. Kanena bunu Ghausha, Takwenenda kuonyesha, Lakini niaminisha, Kwa mithaki na ahadi

638. Muakali kabaini, Nakuapia yamini, Nami ni msikitini, Ni katika masijidi

639. Kisha apa sura mia, Mara iyo kamwambia, Nyumba alokimbilia, Ya banii 'l Asadi

640. Mselemu yu nyumbani, Huko kwa mzee Khani, Muakali kibaini, Kenda hima na juhudi

641. Alipofika nyumbani, Kabisha kangia ndani, Akamwambia yakini, Nijile nina zawadi

642. Kamtaka Mselemu, Kwa wema na tabasamu, Akampa darahimu, Akisha kamradidi

643. Akamwambia Huseni, Ametoka yu ndiani, Atakuja kuawini, Kama yaliyo kubidi

644. Amenipa diinari, Utakako ushitiri, Kula kipasacho shari, Chombo kilicho jadidi

645. Nami hivi nenda zangu, Nina khofu roho yangu, Nakuhongea mwenzangu, Nawe kujificha zidi

646. Kaamini Mselemu, Kapokea darahimu, Akampa na salamu, Nisalimia Sayyidi

647. Muakali akatoka, Kwa upesi na haraka, Barazani akifika, Kwake ibnu Ziadi

648. Muakali akanena, Kamwambia wake bwana, Umekwisha patikana, Uliotaka mradi

649. Khani bin Ghuruata, Ndiye aliyemfita, Hivi tukimtafuta, Anaye zote abadi

650. Kwambiwa kwake juhali, Kawamkua rijali, Majina yao nakuli, Wa kwanza ni Muhamadi

651. Wa pili etwa asema, Na Omari kawatuma, Akamba nendani hima, Khani mukamkaidi

652. Wakenda na furisani, Wakenda mtwaa Khani, Akifika barazani, Salamu akaradidi

653. Jamii wakanyamaza, Kwa hali ya kutukiza, Abidallahi kauza, Kwani Khani kutaadi?

654. Wamficha Mselemu, Nasi ni wetu khasimu, Wewe u mwenda wazimu, Akili umesharidi

655. Naye Khani atongoe, Mwenda wazimu u wewe, Utakae umuuwe, Bin ami Muhamadi

656. U wewe mwenda wazimu, Utakaye Mselemu, Nikupe umdhulumu, Upate kumhusudi

657. Mara akaghadhibika, Abidallahi karuka, Bakora akaishika, Kitaka kumjalidi

658. Khani alipomshufu, Akaikabili sefu, Kamwegema asikhofu, Kama umeme na radi

659. Dharuba kamsukuma, Akazikata kwa nyuma, Kofia mbili za chuma, Na dirii za hadidi

660. Abidallahi kanguka, Kwa kiwewe kumshika, Roho ikafazaika, Akawambia junudi

661. Kawambia tasihili, Mshikeni mumdhili, Asijesha wakutuli, Khani akaiadidi

662. Akaishika hasama, Jeshini akajitoma, Mithili wimbi la joma, Livumalo na baridi

663. Kawangusha iyo hini, Khamsa wa ishirini, Bi tarafati aini, Kaumu wakamzidi

664. Wakampiga asira, Akafungwa kwa kambara, Na kumpiga bakora, Na dharuba za hadidi

665. Kashahadia Karimu, Kafa ali Islamu, Fi'l janati naimu, Akenda akarajidi,

666. Khabari zilipofika, Nyumani kwake hakika, Mselemu akatoka, Na jitimai shadidi

667. Katoka na jitimai, Hana hila wala rai, Ali katika sarai, Kaona nyumba baidi

668. Nyumba hiyo nitamke, Kamwona mwanamke, Kamuuza hali yake, Yote akamradidi

669. Kasikia nisiwani, Akamba pita nyumbani, Kwani adui mjini, Wa kati kukuadidi

670. Akapita Mselemu, Harume kamuheshimu, Ali na wake ghulamu, Yeye mmoja waladi

671. Kumuonakwe mamaye, Ana fazaa rohoye, Akamuuza haliye, Mama umetasawidi

672. Ni kungia ukatoka, Kitu gani umeweka, Mamaye akatamka, Sikia ewe waladi

673. Nyumbani mna ghulamu, Jina lake Mselemu, Min bani Hashimu, Bin amu Muhamadi

674. Na mimi nimemsiri, Ahadi ni kusafiri, Kijana akadhukuri, Mama kumficha zidi

675. Mara ile akatoka, Barazani akafika, Watu wamekutanika, Kamwita bun Ziadi

676. Yule kijana kasema, Mselemu yu kwa mama, Wapeleke watu hima, Mimi nimemshahidi

677. Kwa mama ndiko aliko, Na mimi natoka huko, Adui keta kacheko, Na kufurahi shadidi

678. Mara ile kasimama, Akawataka kauma, Akamba nendani hima, Na amiri Muhamadi

679. Bun Shiati amiri, Akampa asikari, Khamsamia jifiri, Walio kama asadi

680. Kamwambia tangulia, Mselemu niletea, Basi akashika ndia, Kandamana na junudi

681. Mselemu pakhubiri, Kasikia hawafiri, Na kishindo cha bairi, Kajua ndio hasidi

682. Kamwambia nisiwani, Kanipe maji kuzini, Nisali rakaateni, Nipate omba Wadudi

683 Kasali rakaateni, Akamuomba Manani, Baada sayo yuani, Kamrakibu jawadi

684. Akampanda farasi, Na upanga na turusi, Akamuomba Kudusi, Kawakabili junudi

685. Mbele yao kasimama, Kawauza akasema, Ajili semani hima, Nijue wenu mradi

686. Lililowaleta nini, Msikawe nambiani, Na ambalo mwatamani, Mutafutalo kusudi

687. Mara walipomshufu, Wakamwegema kwa sefu, Wapate kumtilifu, Afungwe kama abidi

688. Kajitia katikati, Akawonesa mauti, Watu khamsamiati, Watu kumi wakarudi

689. Kawapiga kama huwa, Kukata na kuangua, Kama radi ilotia, Shajaria 'l jadidi

690. Akawatawanya damu, Ikenenda milizamu, Wakarejea kaumu, Hata kwa bun Ziadi

691. Wakenda wakimwambia, Kama yaliyo jiria, Sote hatukubakia, Tumebadia suudi

692. Kusikiakwe yuani, Kawatoa shujaani, Idadiye alufeni, Wasioweza taadi

693. Akawambia nendeni, Mselemu mleteni, Msishindwe ni mgeni, Aliyetoka baidi

694. Endani mkamtwae, Upesi muniletee, Tupate hiyo rasiye, Apelekewe Yazidi

695. Wakenenda asikari, Kama rihi na matari, Na kula mtu tayari, Kwa silaha za hadidi

696. Walipomkaribia, Mselemu kawangia, Jeshini kajipakia, Na farasiwe najidi

697. Akamrusha kimatu, Akaja ndani ya watu, Isipate saa tatu, Wote akawasafidi

698. Akaishika hasamu, Mwana wa bani Hashimu, Akawatawanya damu, Nchi yote ikabidi

699. Akinga simba dharia, Damu ikenda milia, Na watu wakangamia, Wangi wasio idadi

700. Yamini kajipeleka, Wanguka kama mataka, Hata akizungumka, Kupigana akazidi

701. Kawatia mautini, Wote watu alufeni, Wakabaki thelathini, Wasihimili hadidi

702. Wakenda kwa bwana wao, Wakampa hali yao, Wakamba siku ya leo, Adui katuhusudi

703. Tulipowasili kando, Katungia kama nondo, Akitutenda kitendo, Hatuwezi kuradidi

704. Katungia kwa upanga, Jeshi yote kaizinga, Pasi muweza kukinga, Wala mkaa baidi

705. Bwana fanyiza shauri, Adui katuhasiri, Kwambiya siyo khabari, Kawakusanya junudi

706. Kawakusanya sufufu, Ambao ni mausufu, Ithnashara alufu, Akaja kawaradidi

707. Akawambia kaumu, Endani kwa Mselemu, Na mrudipo haramu, Mauti yatawabidi

708. Ambapo mwarejeea, Msipo kuniletea, Tawataka vitwa pia, Hayo nimewaahidi

709. Basi ikenenda jeshi, Kama dharuba ya tushi, Na kutaharaki nchi, Kwa hafiri za jawadi

710. Wakamfika alipo, Wakenda muona yupo, Mselemu iwenepo, Ghadhabu akashitadi

711. Upanga kauzungusha, Farasi akamwegesha, Ukinga mwamba kuusha, Na wingu kubwa na radi

712. Muili ukanafiri, Kwa ghadhabu kukithiri, Kiruka kama namiri, Ghadhabu kinga asadi

713. Dharuba akizitoa, Kama umeme na kuwa, Na kipovu kumuawa, Likachemka zubadi

714. Alikikabili mbele, Kusibakie kisele, Akileneza fumole, Watu hamadi hamadi

715. Muili ukamvimba, Kimatu akinga simba, Mara moja kawaramba, Watu mia wakarudi

716. Barazani wakifika, Mtangani wakanguka, Maneno wakitamka, Sikia bun Ziadi

717. Leo tuwene harubu, Iliyo kubwa ajabu, Vita vyake Muarabu, Ataitwaa biladi

718. 'l Kofu itatwaliwa, Ukae ukitambua, Na wewe utauwawa, Ni huyo mtu wahidi

719. Harubu apiganavyo, Hatuwene kama hivyo, Jamii vita twandavyo, Hatuwenepo abadi

720. Muarifu mwenye nchi, Atudirikiye jeshi, Ila sisi hatutoshi, Kupata huo mradi

721. Fisa khati Dimishiki, Watuletee khaliki, Na Basara na Iraki, Na wakutane junudi

722. Na ufanyapo dhihaka, Usipeleke waraka, Tambua unamtoka, Ulua wake Yazidi

723. Kwambiwa hayo asahi, Keta wino na lauhi, Kandika Abidallahi, Sikia ewe Sayyidi

724. Akaikutubu khati, Ya Yazidi mwenye nti, Tu katika harubati, Na vita vimetuzidi

725. Vita vyake Mselemu, Vyapita jabali gumu, Turidikie kaumu, Hima wapate tufidi

726. Wote watu maarufu, Katika nti ya Kofu, Jamii wametilifu, Watambuao hadidi

727. Mselemu atashinda, Na nti ataivunda, Atakalo atatenda, Ni hayo nakuradidi

728. Ulipokwenda waraka, Kwa Yazidi ukafika, Maneno akipulika, Uso ukamsawidi

729. Kanena akitukana, Watu wa Kofu naona, Hawawezi kupigana, Tokea jadi na jadi

730. Huwaje mtu mmoja, Akajirisha vioja, Tena wakatoa hoja, Kwamba avunja biladi

731. Tapeleka farisani, Kama simba ghadhibani, Mselemu na Huseni, Wakawatoe taadi

732. Kawakusanya sufufu, Watu sitini alufu, Ambao ni mausufu, Wasio shaka na budi

733. Kawambia enendani, Mkifika washikeni, Mselemu na Huseni, Upesi hima murudi

734. Basi jeshi ikatoka, Wakapanda wakishuka, Siku haba zikafika, 'l Kofu wakaibidi

735. 'l Kofu wakiwasili, Jamii wote rijali, Wakafurahi kwa kweli, Kwa kuwasili junudi

736. Wakelezana khabari, Za awali na akheri, Na kama yaliyojiri, Wasibakie wahid

737. Hata kukipambazuka, Basi jeshi ikatoka, Kusudi kwenda mshika, Bun amu Muhamadi

738. Alipokwisha waona, Mselemu kakazana, Meno akajitafuna, Mfano kama asadi

739. Kuionakwe shabuka, Mshipa ukamwinuka, Na tauka na tauka, Na kukazana jasadi

740. Jasadi ikahariki, Akinuka na uruki, Wote wakataharuki, Wasiweze mjalidi

741. Kizinga kama umeme, Kushotoni na kulume, Wali papo wasimeme, Na khofu kubwa shadidi

742. Akaipiga siahi, Ikavuma kama rihi, Zikawapuna silahi, Zilizo katika yadi

743. Akamzinga rikabu, Alisimika dhanubu, Na jamii ya ghadhabu, Siku hiyo akazidi

744. Uso ukaghadhibika, Mato yakahamirika, Na kipovu kumtoka, Yeye na wake jawadi

745. Akajitia jeshini, Akawachenga laini, Ali akenda usoni, Na kinyume akarudi

746. Akanenda kwa shimali, Akawachenga rijali, Kija upande wa pili, Ikiwa hivyo abadi

747. Mselemu kiwangua, Kama matone ya mvua, Pasi muweza jinua, Wala enuaye yadi

748. Na ambaye akabili, Mara huwa mbali mbali, Kushotoni na kuvuli, Wote wakatabaadi

749. Wakatamani kimbia, Hapana pa kuawia, Hali ya kuwazuia, Pasiwe muweza rudi

750. Mselemu akawesha, Kuwaua kiwangusha, Wote akawababusha, Wakawa kama rimadi

751. Siku hiyo maarufu, Arubaini alufu, Aliyo kuwatilifu, Wasazao wakarudi

752. Jamii wakakubali, Kuvushwa nchi ni kweli, Wala hataki wa pili, Kutunyang'anya biladi

753. Mashauri wakanena, Na tutoeni vijana, Twende nao mbali sana, Tukawafiche baidi

754. Hana budi Mselemu, Ataimiliki Rumu, Awaue na kaumu, Ashike ndia arudi

755. Wakawatoa kabili, Wana na wao wavyele, Na walio na uwele, Vipofu na makaidi

756. Wakawatoa viwete, Na wenye madonda wote, Mmoja wasimuate, Ila walio jadidi

757. Wakenenda ughaibu, Hata ipite harubu, Baada sayo najibu, Wakakutana junudi

758. Wakakutana kaumu, Thamaanini timamu, Alufu zilizotimu, Isipungue wahidi

759. Basi shauri waseme, Twendeni tukamwegeme, Mmoja asisimame, Ataghumiwa jawadi

760. Farasi akighumiwa, Mara moja atajiwa, Basi sapo wakaawa, Wote wakajizadidi

761. Hata walipomfika, Jeshini kajichomeka, Kupita zote shabuka, Wote wakamsharidi

762. Kawachawanya khumra, Ikenea zote bara, Na mafisi waking'ara, Kwa hali ya kufaidi

763. Akawatenda kitendo, Kuwachawanya uvundo, Kiwopoa kama nondo, Amezaye 'lkurudi

764. Farasiwe apitapo, Hapabaki aliyepo, Kama wingu na upepo, Na dharuba na baridi

765. Akiwangamiza watu, Idadiye wanakwetu, Alufu kumi na tatu, Waliokufa junudi

766. Wote waliobakia, Jamii wakakimbia, Mselemu kawendea, Na sefuye ya hadidi

767. Kiwapiga kwa hasamu, Akawachanganya damu, Wakawa kama ghanamu, Walio katika nadi

768. Kapiga kiwangamiza, Kuno akiwafukuza, Wote wakijelemeza, Masaharati na wadi

769. Wakenda mtashatiti, Kwa kuyakhofu mauti, Wakaikimbia nti, Wote ahali biladi

770. Mselemu akazinga, Akampita kipanga, Mji wote akatanga, Asimuone wahidi

771. Akaizuia Kofu, Thuluthani na nusufu, Na majumba maarufu, Yakawa katika yadi

772. Nusu ya mji baadhi, Yote kaitakabidhi, Pasiwe mtaaradhi, Wala mwenye kutaadi

773. Katamalaki majumba, Mazuri yaliyopambwa, Mwana wa simba na simba, Ni kazi yao abadi

774. Na jamii ya rijali, Kukionakwe kitali, Wakakutanika mbali, Wasiiweze biladi

775. Jamii wakakimbia, Mji wakamuatia, Walipokwisha tulia, Shauri wakafanidi

776. Shauri wakelekeza, Jawabu la kufanyiza, 'lKofu tukakweleza, tukamwondoa hasidi

777. Pana mmoja kanena, Hapana shauri tena, Mji unasha tupona, Na kufa hatuna budi

778. Hawa ni asili yao, Kuwana ni kazi yao, Na ushujaa wa kwao, Jadi zao na jududi

779. Ndio simba wa Mungu, Wanywesa watu matungu, Na katika ulimwengu, Hako aliyewazidi

780. Na roho yangu hiwaza, Yule hatutamuweza, Shauri la kufanyiza, Hapana ila wahidi

781. Na tutimbeni handaki, Ajapo akisabiki, Tufanye kutaharuki, Kinyumenyume turudi

782. Atangia handakini, Tumtie mikononi, Jamii wakayakini, Shauri linalobidi

783. Wakaichimba rijali, Yali usiku laili, Na shimo likenda mbali, Tena wakalisafidi

784. Juu wakalifinika, Farasi akija ruka, Hana budi kuanguka, Kumshika hana budi

785. Kulipokucha sikiza, Wakaitaka baraza, Mselemu katokeza, Mtamboni akanadi

786. Alipokuwatokea, Jamii wakakimbia, Mbele akiwandamia, Na sefuye ya hadidi

787. Kupata punde usoni, Farasi kanguka tini, Akangia handakini, Akaumia jawadi

788. Farasi akavundika, Na Mselemu kanguka, Wakaja wakamshika, Jamii wote junudi

789. Wakakutana asahi, Wakazipiga siahi, Na roho zilifurahi, Furaha kubwa shadidi

3

UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA KISA CHA SAYYIDNA HUSSEIN

790. Wakamfunga kwa kweli, Mikono yote miwili, Wasimbaki pahali, Wasipo kumkaidi

791. Mselemu kamkuwa, La haula wala kuwa, Aladi qalu Molewa, Kujiri halina budi

792. Wakenda naye hakika, Wote walifurahika, Barazani wakifika, Mbele ya bun Ziadi

793. Wakamuweka usoni, Mbele yake maluuni, Abidallahi yuani, Maneno akaradidi

794. Kamwambia Mselemu, Enyi banii Hashimu, Mtakao jidhulumu, Mwatezea maSayyidi

795. Hivi kwenu mkitoka, Kuja Kofu na shabuka, Makusudi kumpoka, Ulua wake Yazidi

796. Mpate usultani, Wewe na huyo Huseni, Mukaishi duniani, Muwe watu maadudi

797. Mtamalaki Iraki, Na Kofu na Dimishiki, Na Yazidi mumdhiki, Ndiyo yenu makusudi

798. Mjile taka matata, Na vitwa vyenu kukatwa, Hayo hamtayapata, Hata mkajitahidi

799. Mselemu kabaini, Wayy-laka maluuni, Wadharauje Huseni, Ukamsifu Yazidi

800. Sakiti ulimi wako, Kwamba si hadaa zako, Ningekuonya vituko, Vikubwa visivyo budi

801. Na kwamba si kunitenga, Nti ningalizipinga, Haziwata nyonganyonga, Hamngojea Sayyidi

802. Hata akija Huseni, Akaikuta amani, Na ambaye mshindani, Akija hamhusudi

803. Mtu wa pili sitaki, Wa 'l Kofu na Iraki, Peke yangu nawadhiki, Mkaitoka biladi

804. Na sasa matungu yangu, Sijutii roho yangu, Nakumbuka ndugu yangu, Yatakayo kumbidi

805. Namkumbuka Huseni, Na jeshi ya maluuni, Wala hanayo yakini, Kwamba wametamaradi

806. Baada sayo nanena, Abidallahi laana, Akawambia watwana, Endani naye baidi

807. Mkamkate rasiye, Ajili mniletee, Watumwa wakenda naye, Wakenda kumuhusudi

808. Akenda akauwawa, Shahada akamkuwa, Ya Rabi wake Molewa, Na Mtume Muhamadi

809. Kashahadia Jalali, Na Mtume Murisali, Wakisha kumkutuli, Roho yake naradidi

810. Roho yake Mselemu, Ikenda fi 'nnaimu, Hurri 'l aini fahamu, Wote wakashua yadi

811. Mikono wakashuua, Rohoye ikapokewa, Fi'l jana ikatiwa, Kunako njema baridi

812. Kisha sayo niwambie, Wakaitwaa rasiye, Na ya Khani rafikiye, Zote wakazijalidi

813. Kitwa chake muumini, Na kile kitwa cha Khani, Vikenda kwa Sultani, Hakimu wao Yazidi

814. Kifika vikatolewa, Yazidi kafurahiwa, Na kaumu kaitoa, Nyingi isiyo idadi

815. Akawambia endani, Mkamngoje Huseni, Mkifika simamani, Nyinyi na bun Ziadi

816. Huseni akiwasili, Upesi kumkutuli, Na rasiye tasihili, Na ije pasipo budi

817. Basi wakenda khaliki, Wana panga kwa mikuki, Wakiwasili Iraki, Na Kofu wakakhalidi

818. Wakaketi kusikiza, Na watu kupeleleza, Kula ndia wakitunza, Kumtazama Sayyidi

819. Hata sikuye kwa mbele, Khabari wazisikile, Kwamba Huseni ajile, Hayuko tena baidi

820. Kaja aba Abdalla, Inshaallah taala, Naye yupo Karabala, Hapo shatii' l wadi

821. Karabala amefika, Na kesho atakondoka, Siku haba zikifika, Aja miliki biladi

822. Abidallahi pulika, Kuipatakwe hakika, Mno akafurahika, Na kutengeza junudi

823. Katengeza asikari, Bi yamini wa yasari, Na kula penye khatari, Kapatengeza jadidi

824. Akazizuia ndia, Mjini za kungilia, Pasiwe pa kupitia, Kwa majiwe kujamidi

825. Tena mbiu ikalia, Katika zote karia, Maneno akiwambia, Abidallahi kanadi

826. Akamba ya farisani, Nnani keno nnani, Mwenda vita vya Huseni, Hamsalimu junudi

827. Nnani aviwezaye, Akenda twaa rasiye, Enzi akapewa yeye, Kwa myaka kumi idadi

828. Akapewa uhakimu, Kwa myaka kumi timamu, Kwisha sayo kukalimu, Pana mmoja hasidi

829. Hayo akayakubali, Huseni kumkutuli, Na jina lake nakuli, Omari bun Saidi

830. Akamba mimi takwenda, Huseni kwenda mtinda, Na utakalo tatenda, Nitimilize ahadi

831. Basi kapewa kaumu, Kuwa yeye mkadamu, Na maamiri fahamu, Majina tawaradidi

832. Wa kwanza bun Hasini, Akapewa alufeni, Kamba simba ghadhibani, Ukali kama asadi

833. Bun Rabia wa pili, Aliopewa rijali, Alufu kumi na mbili, Kandamana na junudi

834. Bun Shiati sikia, Akapewa zikwi mia, Kaambiwa tangulia, Akatoka Muhamadi

835. Alipewa farisani, Watu wa kwenda vitani, Idadi arubaini, Elfu zisizo budi

836. Tena akapewa Hari, Sita alfu jifiri, Walio kama namiri, Akenda bun Yazidi

837. Na Hajari tabaini, Akapewa farasani, Theneni wa ishirini, Alufu wenye hadidi

838. Wakaamrisha mwendo, Na kwenda tenda kitendo, Wakenenda kama nondo, Majimbo yote na wadi

839. Amiri akadhukuri, Endani enyi jifiri, Na amri kwa Omari, Jamii yote junudi

840. Sikizani amriye, Pasiwe ambishaye, Kwa jamii wetikie, Inshallahu Sayyidi

841. Basi wakafuatana, Pasi kuona mchana, Kwa ghubari kufungana, Mchana ukasawidi

842. Wakafika Karabala, Wakazitoa kafila, Wasibakie mahala, Bara yote wakabidi

843. Mito wakaizuia, Ya maji ya kutumia, Pasiwe kuona ndia, Hali ya jeshi kuzidi

844. Wakazuia mitoni, Na maji ya visimani, Kumzuia Huseni, Yeye na wake waladi

845. Huseni akitazama, Kushuka wangi kauma, Na kuzuiwa visima, Na watu kama juradi

846. Kashika yake hasadi, Kawakabili kaumu, Mbele yao akakumu, Kasimama akanadi

847. Akatamka Huseni, Ya kaumu sikiani, Mwanijua ndimi nani, Na baba yangu na jadi

848. Au la jina la mama, Mwalijua ni kusema, Wakatamka kauma, Wakamjibu Sayyidi

849. Ndiwe Huseni rijali, Na babayo Shekhe Ali, Na mama yako Batuli, Na babuyo Muhamadi

850. Huseni akawambia, Kumbe hayo yawelea, Kisa cha kunizuia, Maji na wangu waladi

851. Mwanizuia sharabu, Kesho mbele ya Wahabu, Ndombezi wenu ni babu, Hiyo siku ya mnadi

852. Au maji hamtaki, Siku ya kutaharaki, Jamii wakanatiki, Jamii wakamrudi

853. Twayajua kama hayo, Ndombezi kuwa babuyo, Waama leo rohoyo, Kutoka haina budi

854. Na mngawanya haudhi, Ni babuyo muritadhi, Waama kufa faradhi, Katwaa Maka hurudi

855. Majambo yake babuyo, Yanatupata na moyo, Hayeshi tukili nayo, Yanatuchoma fuadi

856. Kusikiakwe Huseni, La haula kabaini, Illa billahi Manani, Kashika ndia karudi

857. Akarudi akilia, Kwa mambo kumzingia, Hemani alipongia, Wote wakamshahidi

858. Kulia kwake Huseni, Wakalia nisiwani, Na vijana mikononi, Na rijali na abidi

859. Tena wakanyamazana, Basi Huseni kanena, Hema ijengeni sana, Na boma liwe jadidi

860. Basi hema zikakita, Pasi mahali kupita, Na boma kama ukuta, Likawa gumu shadidi

861. Boma lilipotulia, Usiku ulipongia, Huseni akawambia, Wenziwe kawaradidi

862. Wenziwe kawabaini, Afadhali kimbieni, Mtukue nisiwani, Hivi sasa msharidi

863. Tokani hivi laili, Hata kukicha mmbali, Maana hiki kitali, Ni changu mimi wahidi

864. Tokeni enyi wenzangu, Mniwate peke yangu, Na rehema kwa Muungu, Nusura kwake Wadudi

865. Aliposema akesha, Wote wakanena hasha, Ya nini hayo maisha, Ufapo wewe Sayyidi?

866. Twaradhiwa tuyayuke, Ndipo nawe upatike, Ila kukuwata pweke, Sio yetu makusudi

867. Ufapo wewe Huseni, Maisha hayo ya nini?, Twafanyani duniani, Uondokapo Sayyidi?

868. Hayo wakisha mwambia, Huseni kafurahia, Na kumwomba Jalia, Na dua njema kazidi

869. Wakalala ni laili, Wakisoma na kusali, Kabiri na tahalili, Na salatu Muhamadi

870. Hata kukipambazuka, Wakamuomba Rabuka, Kwa kiu ilowashika, Wanawake na waladi

871. Wataka maji ya kunywa, Wayatafuta hawana, Akondoka Maulana, Akawendea junudi

872. Akatamka Huseni, Akamba ya Farisani, Nataka maji nipani, Kwa upesi na juhudi

873. Maji musiyazuie, Nayataka nitumie, Kwani sina nikhofuye, Wala aliyenizidi

874. Nipani maji haraka, Msifanyike dhihaka, Mkatafuta hilaka, Na kwangamia kusudi

875. Na hayo muazimuyo, Yote nayaona siyo, Maneno niwambiayo, Nipani maji nirudi

876. Wakatamka kaumu, Sikia bani Hashimu, Twakuwazia kuzimu, Katika zetu fuadi

877. Wala hapo hatwondoki, Wala maji huyateki, Ahadi ni kuhiliki, Wewe na wako junudi

878. Ewe Aba Abdalla, Katwaa hwendi pahala, Utakufa Karabala, Huna budi huna budi

879. Huseni akipulika, Mno akaghadhibika, Na upanga kaushika, Kawakabili junudi

880. Walipomuona aja, Wasende mbio pamoja, Ila mmoja mmoja, Kwa khofu kuu shadidi

881. Kukimbiakwe kauma, Huseni karudi nyuma, Akenda kunako hema, Na kaumu wakarudi

882. Na jamii watu wake, Wataka maji wateke, Wana waume na wake, Kiu inawashitadi

883. Watoto wamedhikika, Kwa roho kuwakauka, Asimamaye hwanguka, Hapo muweza jasadi

884. Kuyaonakwe yakini, Akondoka farasini, Akamwambia Huseni, Kanena ewe Sayyidi

885. Sayyidi nipa idhini, Nende hangie jeshini, Rabbi ataniauni, Kwa nusuraye Wadudi

886. Na Huseni akakuli, Baraka 'Llahu rijali, Takunusuru Jalali, Bi shufaa Muhamadi

887. Kwambia siyo jinsi, Akenda hima upesi, Dereya kajilabisi, Kanzu mbili za hadidi

888. Na upanga kaushika, Na fumo likigeuka, Farasi kamtandika, Kamkalia jawadi

889. Akajitia jeshini, Kama wingu na tufani, Bi shimali wa yamini, Kwenda huko na kurudi

890. Kiwakata vyao vichwa, Kiwaua kiwangusha, Ukinga mwamba kuosha, Wenye wingu na baridi

891. Kawatia mautini, Alufu na miateni, Kauwawa muumini, Rahema 'Llahu Wadudi

892. Akanguka Islamu, Kashahadia Karimu, Na Mtume Muungamu, Swala 'Llahu wa Sayyidi

893. Roho yake Muumini, Ikenda fi'l janani, Kuona sayo Huseni, Kawakabili junudi

894. Kawangia katikati, Akawanyesha mauti, Yamini na shimalati, Wote wakamsharidi

895. Akawaua Huseni, Jumlaye alufeni, Kampata Muumini, Waliye kumuhusudi

896. Kamfika maitiwe, Kamshika mkonowe, Huseni kapiga yowe, Kulia na kuradidi

897. Akalia akinena, U wapi babu Amina, Leo kwamba waniona, Wanitendavyo junudi?

898. Na baba yangu Alii, Na kwamba leo uhai, Ingalishuka samai, Kwa hurubu kushitadi

899. U wapi baba Sharifu?, Ukaja ukawashufu, Wa Iraki na wa Kofu, Watakavyo nihusudi

900. Akawasili hemani, Kamuweka pale tini, Wakalia nisiwani, Na jamii ya junudi

901. Kulia wakiomboa, Na mikono wakinua, Na kuomba njema dua, Kwa Mola wetu Wadudi

902. Kimaa kunyamazana, Pana mmoja kanena, Nirukhusu Maulana, Nende hawane jihadi

903. Akamba katawakali, Ukamuombe Jalali, Akajifunga kwa kweli, Seifuye ya hadidi

904. Kimaa kushika sefu, Akawangia wa Kofu, Kaua watu alufu, Kama umeme na radi

905. Na yeye wakamuuwa, Kashahadia Molewa, Na Tume wake Rasuwa, Fi'l janna akabidi

906. Akangia Maulana, Akenda akapigana, Hata akenda muona, Kamtwaa akarudi

907. Akatoka na wa tatu, Akenda jeshi ya watu, Yali hivyo wanakwetu, Kwenda wahidi wahidi

908. Na kadiri atokaye, Yuapigana pekeye, Akaua auaye, Alufu au zaidi

909. Na pindi akiuawa, Huseni amtukuwa, Tena akirehemewa, Na Mola wetu Wadudi

910. Kiuawa Muumina, Huseni yuapigana, Hata akenda muona, Hapo alipo shahidi

911. Wakangia mautini, Jamii watu sitini, Kabaki yeye Huseni, Na wale wake waladi

912. Watu sitini fahamu, Wote wakenda kuzimu, Wakabakia ghulamu, Na baba yao Sayyidi

913. Na kiu imekithiri, Watoto wataghayari, Wala hawana shauri, Kupata maji baridi

914. Watoto wamedhikika, Kwa kiu ilowashika, Na maji wakiyataka, Wanazuia junudi

915. Wanawake na vijana, Wapita povu la kanywa, Kazi yao hulizana, Na sala na kusujudi

916. Wamsabihi Jalali, Na sala na tahalili, Kwa mtana na laili, Wa katika kuabidi

917. Huseni akibusiri, Kamtwaa nakhubiri, Mwanawe Ali saghiri, Kijana fi'l mahidi

918. Kijana hajaachishwa, Bado akalinyonyeshwa, Mwana mchanga kabisa, Hazidi mwaka wahidi

919. Kamtukuwa Huseni, Kamuweka mkononi, Akenda naye jeshini, Maneno akaradidi

920. Huseni akabaini, Nataka maji nipani, Kwani huyu ghulimani, Atishi imemzidi

921. Ngawa fanyani huruma, Kwa huyu mwana yatima, Hakumaliza kusema, Mshare ukambidi

922. Mshare ukaja hima, Kapiga yule ghulama, Huseni akitazama, Wanakwisha muhusudi

923. Mshare ukaja mbio, Ukamkata shikio, Kijana keta kilio, Na damu kutamaridi

924. Kijana kafazaika, Kina akipapatika, Kwa shikio kukatika, Naye kijana waladi

925. Babaye akamshika, Kifuani kamuweka, Keno akasikitika, Na kilio akazidi

926. Kenda nayo iyo hina, Akafika kwa Sakina, Ikiwa ni kulizana, Kwa msiba kuwashidi

927. Wakalizana kabili, Wote wana na wavyele, Kwa siaha na kelele, Waungwana na abidi

928. Wakinyamaza yuani, Kondoka katabayani, Mtoto wake Huseni, Jina ketwa Muhamadi

929. Akamwambia amuye, Nipa rukhusa ningie, Naradhiwa nangamie, Kama kuona taadi

940. Alufu wa thamanini, Kawatia mautini, Ndipo akanguka tini, Wakampiga hadidi

931. Akaumba Murisali, Kuwa yeye afadhali, Wa akheri na awali, Bora wao Muhamadi

932. Bora ya watu babuyo, Alomzaa babayo, Akaumbwa na babayo, Akawa yeye asadi

933. Kapewa dhu' l Fukari, Akawapiga kufari, Hata wakataghayari, Pasiwe mwinua yadi

934. Na pepo alowekewa, Ni babu yako Rasuwa, Babayo enda tukuwa, Hiuliwa 'l hamdi

935. Na sisi tu wana wao, Tuzawa ni watu hao, Nnani watupitao, Katika wote junudi

936. Na haya ni makutubu, Yandishiwe ni Wahabu, Kula litalotusibu, Ni amri ya Wadudi

937. Na sasa nipa idhini, Nikaingie jeshini, Huseni akabaini, Naamu wangu waladi

938. Naamu uliyonena, Siwezi kurudi tena, Mtawakali Rabana, Kijana kajizadidi

939. Kajifunga upangawe, Akapanda farasiwe, Kawapoa kama mwewe, Harubu ikashitadi

930. Maana Rabi Molewa, Alimuomba Rasuwa, Kampa haja na kuwa, Kupita wote ibadi

941. Akapiga ukelele, Huseni njoo uole, Hawana wako wavyele, Na babuyo Muhamadi

942. Huyu bibiyo Khadija, Na muombezi wa waja, Na Hasani wa pamoja, Na Fatuma wangu Jadi

943. Na babayo Shekhe Ali, Njoo hima tasihili, Kusikiakwe makali, Sefu kaitakaladi

944. Akaushika upanga, Mwana wa anga kwa anga, Kangia akawachenga, Kama fisi na asadi

945. Hata akamdirika, Miongoni kimweleka, Matozi yakimwaika, Kilio kikashitadi

946. Kufika kunako hema, Huseni kashika tama, Ali papo usimama, Kalia mno Sayyidi

947. Zainabu na Sakina, Zaina 'l abidina, Jamii wakalizana, Pasibakie wahidi

948. Na 'l Umi Kulithumu, Kalia mno fahamu, Na jamii ya ghulamu, Kilio wakaamidi

949. Na Fatuma na Rukia, Wakashitadi kulia, Keno wakipindukia, Kwa kilio kuwazidi

950. Wakashukuru Taala, Akatoka Abdalla, Bin Huseni Fadhila, Kawakabili junudi

951. Jeshini akjitia, Muda wa saa kungia, Alufu wa sita mia, Kawaua asibudi

952. Ndipo naye kauwawa, Kashahadia Molewa, Pepo zimefunguliwa, Mola wetu akanadi

953. Akatamka Manani, Enyi mahuru 'l aini, Simamani simamani, Kwa shime na jitihadi

954. Mpokee roho zao, Viumbe niwapendao, Ni laula baba yao, Kusinge kitu abadi

955. Roho zao zitwaeni, Zisanguke mtangani, Wakaja huru 'l aini, Hapo panapo jihadi

956. Kwa kila auawaye, Wakapokea rohoye, Pasibaki abakiye, Jamii wote waladi

957. Wana sabaa ashara, Wote wakenda akhera, Kwa uwezo wa kudura, Yake Muungu Wadudi

958. Kabaki pweke Huseni, Na upanga mkononi, Akitazama yamini, Asione msaadi

959. Akitazama yasiri, Asione mshauri, Kalia akakithiri, Hata akapita budi

960. Baada kulia kwake, Wakalia wanawake, Kwa Huseni kuwa pweke, Na vita vimeshitadi

961. Junudi yangalizana, Kwa usiku na mtana, Hapana kusikizana, Kwa wangi junudi

962. Ni kamkam malaki, Walioko wanafiki, Hawana walipobaki, Majimbo yote na wadi

963. Wamekutana sufufu, Kamkam maalufu, Kwa mafumo na suyufu, Walizo kutakaladi

964. Kuona bun Imamu, Kuzidi mno kaumu, Kondoka kutayamumu, Kasali akisujudi

965. Akamuomba Rabana, Mwenye ezi Subhana, Baada sayo nanena, Kandoka kajizadidi

966. Kangia kajiwadaa, Pambo ambalo lafaa, Na kofia akavaa, Isiyo shaka na budi

967. Kofia yake kitwani, Ya hadidi mbayani, Ya tokea Adnani, Ya tangu jadi na jadi

968. Akajivika kilemba, Cha maidani kutamba, Ghadhabu akinga simba, Na uso kama asadi

969. Akaishika na sefu, Ka'l bariku khatifu, Ya Abdi 'l Manafu, Izoelee jihad

970. Akalishika fumole, Ukali likinga ghule, Likitisha mlekule, Aliye mbali baidi

971. Akaishika turusi, Ya chuma kingi suwesi, Hata akavuma kusi, Haimpati baridi

972. Dereya sita za chuma, Muili wote mzima, Asiosaze alama, Wote wenele hadidi

973. Na thelatha suruali, Za chuma kingi thakili, Jini na simba wakali, Wote wakamsharidi

974. Kamkali farasi, Kinga umeme wa kusi, Na wingu nene jeusi, Lenye kiza na baridi

975. Akasimama Huseni, Kawaaga nisiwani, Kwa kherini kwa kherini, Nenda zangu sitarudi

976. Kwa kherini wanakwetu, Namuomba Mola wetu, Nasi makutano yetu, Kesho mbele ya Wadudi

977. Kwa kheri ewe Sakina, Zaina 'l abidina, Wake wote na vijana, Na jamii ya waladi

978. Kwa kherini ndugu zangu, Na jamii ya wanangu, Nawaaga nenda zangu, Tena nendako baidi

979. Msikithiri kilio, Tulizani yenu moyo, Kwani Rabi andikayo, Kujiri hayana budi

980. Kwishakwe sema yuani, Wakalia nisiwani, Na jamii ghulmani, Kilio kikashitadi

981. Wakalia na majini, Na nyama wote yakini, Wa bara na baharini, Hata ndege na asadi

982. Kwisha sayo kukalimu, Kamzinza bahaimu, Kaelekea kaumu, Kasimama akanadi

983. Anaa mwana wa enzi, Mwana wa jua na mwezi, Ndiswi waliza walinzi, Na waliotabaradi

984. Ndiswi watenda vitendo, Ndiswi wamwanga uvundo, Ndiswi tumezao nondo, Kula panapo jihadi

985. Ndiswi wavunda milima, Ndiswi wondoa nakama, Ndiswi wondosha kilima, Ndiswi wavunda junudi

986. Kaumu wakisikia, Jamii wakakimbia, Pasi mtu kubakia, Wote wakamsharidi

987. Kwa kumuona haliye, Kifungo na libasiye, Na hayale manenoye, Wakamkaa baidi

988. Huseni akawambia, Haifai kukimbia, Hamna pa kungilia, Hata mahali wahidi

989. Kukimbia hakufai, Kwani zimekwisha rai, Hapana tena uhai, Mimi na nyinyi junudi

990. Basi akajelemeza, Katika wimbi na kiza, Subhana ya Aziza, Ajua yeye Wadudi

991. Akajitia jeshini, Kama wingu baharini, Watu wangukao tini, Huwezi kuwaadidi

992. Sefu ikatenda kazi, Na farasi kanywa wazi, Na awezapo pumzi, Zawalika kama radi

993. Farasi ni Maimuni, Wa Shekhe Aba Huseni, Mzoea upigani, Vita vyote vya jihadi

994. Farasi kaghadhibika, Hako muweza mshika, Yuaruka akiruka, Na kwelemea junudi

995. Farasi akinga simba, Na kivumi kama mwamba, Na maiti wamewamba, Majimbo yote na wadi

996. Akawana Muarabu, Vita vikubwa ajabu, Na uso kutaghadhabu, Ghadhabu kubwa shadidi

997. Pakondoka tushitushi, Kama dharuba ya moshi, Kwa kuwazuia jeshi, Na ghadhabu kumzidi

998. Sefu ikatenda kazi, Kama wembe wa kinyozi, Kumpiga hawawezi, Kwa nguvu aliwazidi

999. Nchi ikafunga kiza, Na damu ikifuaza, Pasiwe na kusikiza, Kwa vita kupita hadi

1000. Dunia ikahamiri, Wakaliona ghubari, Watu walio Misiri, Na walio Baghadadi

1001. Na wa Maka na Madina, Ghubari wakiliona, Wakafazaika sana, Kwa nahari kusawidi

1002. Kharisani na Hijazi, Ghubari li waziwazi, Kwa mwana kutenda kazi, Iliyo katika yadi

1003. Ghubari likisabiki, Basara na Dimishiki, Yemeni na Yarimuki, Sanaa na Sandidi

1004. Na watu walio Rumu, Wakiliona fahamu, Ghubari kubwa adhimu, Wasilijue mradi

1005. Pasiwe asikiaye, Wala mtu aonaye, Wala mwenye akiliye, Zote zikawasharidi

1006. Pasiwe mwenye turusi, Wala mwendesha farasi, Kwa siaha na siasi, Awauavyo Sayyidi

1007. Pasiwe mshika fumo, Wala atokaye humo, Hali ya kiungurumo, Apita wote asadi

1008. Pasiwe mwenye fahamu, Wala akili timamu, Wote wali maghumumu, Wao na wao jawadi

1009. Pasiwe muweza toka, Wala muweza kwondoka, Kwa hali ya kutoweka, Wangi wasio idadi

1010. Kula mtu akadhani, Viumbe hata majini, Mbingu zinakuja chini, Haziko kule baidi

1011. Wakadhani kwa hakika, Samai zimekatika, Na mawingu yameshuka, Hapana shaka na budi

1012. Malaika wa samai, Wote wakatafazai, Hawashuki hawapai, Kwa fazaa na fuadi

1013. Majini na Malaika, Wakamuomba Rabuka, Huseni kunusurika, Allahumma Ya Wadudi

1014. Viwayo na dharubaye, Sawasawa na babaye, Watu wakasema ndiye, Apiganaye jihadi

1015. Wote wakasitatii, Apiganaye Alii, Kumbe hakufa yu hai, Daima zote abadi

1016. Akawatawanya damu, Huseni bun Imamu, Ikenenda milizamu, Kula bara ikabidi