• Anza
  • Iliyopita
  • 5 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 6660 / Pakua: 2389
Kiwango Kiwango Kiwango
MEZA YA UCHUNGUZI

MEZA YA UCHUNGUZI

Mwandishi:
Swahili

MEZA YA UCHUNGUZI

KIMEANDIKWA NA: OMAR JUMAA MAYUNGA

KIMETOLEWA WAVUNI NA: TIMU YA AHLUL BAYT DIGITAL ISLAMIC LIBRARY PROJECT

PONGEZI

"Enyi waumini, mkimcha Mwenyezi Mungu atakuongozeni njia ya haki na atawafutieni makosa yenu na atakusameheni ". 8:29.

Uchamungu ni moja ya pambo Ienye thamani kwa binadamu na nikipimo cha haki na batili na kila ambacho kinamfanya mwanadamu kuwa karibu na Mwenyezi Mungu, kwani uchamungu ni vazi zuri Ienye thamani kila ataelivaa, hupata ukunjufu wa moyo na hima ya kutafuta haki hadi kufikia kikomo na kuwa karibu na Mwenyezi Mungu, kando ya neema zake, zikitiririka bila ya hesabu. Katika ulimwengu huo ambao umejaa ibilisi wenye rangi tofauti, wakiwa na mitego tofauti ili kuwanasa wanadamu kwa vishawishi vipotovu na kuwatowa katika misingi ya haki na ya ukweli na yenye mwelekeo wa tawhid. Wale ambao waliofahamu hila za ibilisi na wakakana kudhalilishwa kwa kufuata vishawishi vyake, kwa hakika hawa ni katika waongofu.

Jambo lakusikitisha, kwamba kwa upande mwingine makafiri wanahila zao, nara zao zaweza kuwa ni uchamungu na wakafanya vitendo viovu wakiona ni vyakumridhisha Mwenyezi Mungu, hali ya kughafilika kwamba huo ni upotovu na ni chanzo cha kuangamia, lakini Mwenyezi Mungu amewaahidi wale wamchae kuwaonyesha njia ya haki. Kitengo cha Utamaduni Ubalozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, unayo furaha ya kuchapisha kitabu, kwa jina: (MEZA YA UCHUNGUZI) kimeandikwa na mtafiti wa haki, si mwingine nae ni Sheikh Omar Juma Mayunga, mwandishi wa kitabu hiki amepata misuko suko mingi mpaka kufikia upeo wa haki, yeye ni mfano wa kuigwa kwani wengi bado wanayumba yumba katika kutafuta ukweli. Kwani haki ni lulu yenye thamani hupatikana kwa juhudi, ongeza uchamungu. Kwani uchamungu ni taa yenye kung'arisha njia ya haki, na wale ambao si wachamungu wakiitafuta haki hawaiyoni.

Sheikh Omar Jumaa Mayunga katika kitabu chake ametowa dalili za Qur'an na Sunna za Mtume(s.a.w.w) , ongeza tajruba zake katika kuitafuta haki na Uislam wa kweli ulioletwa na Mtume Muhammad(s . a . w .w ) akisaidiwa na nuru ya uchamungu ameweza kufikia chemchem ya chimbuko la haki. Tukiacha kupendelea katika itikadi na matamanio ya nafsi na wasi wasi wa ibilisi, tukiangalia kwa jicho la haki kitabu hiki kinaweza kuwa muamuzi na sababu ya kupata kheri za dunia na akhera. Kitengo cha Utamaduni kinasisitiza kuwa yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki ni yake Muandishi, Kitengo cha Utamaduni kimesaidia kuchapa copy 10,000 tunawaombea Mungu wote wanaotafuta haki na Uislamu wa kweli. Mustaffa Najarian Zadeh Mkurugenzi wa Kitengo cha Utamaduni, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dar es Salaam – Tanzania.

UTANGULIZI

Sheikh Umar Juma Mayunga alikwenda Kenya ambako baada ya mazungumzo ya kidini, alishauriwa na Sheikh Abdallah Nasser (wa Nairobi) na Haji Ali Muhammad Jaffer (wa Mombasa) kuwa atakaporudi Dar es Salaam aonane nami kwa maelezo zaidi. Alikuja kuonana nami, na swali lake la kwanza lilikuwa juu ya Taqiyah. Nilimpa jibu lililomtosheleza kutoka kwenye Qur'ani Tukufu na Ahadithi. Baada ya hapo alikuwa akinitembelea mara kwa mara na mambo yote aliyokuwa akiyaelewa vibaya (kutokana na propaganda za kiovu za Wahabiyyah) aliyaelewa vipasikavyo. Baada ya hapo aliyachambua matukio ya mwenye wakati wa mwisho wa maisha ya Mtukufu Mtume(s.a.w.w) na mara tu baada vitabu muhimu vya historia ya Kiislam kama vile Taarikh at-Tabari, Taarikh al-Kamil na Sirah Ibn Hisham; Sura zihusikanazo na historia za vitabu vya Ahadith kama vile Sahih Bukhari, Sahih Muslim, Kanzul Ummal, n.k. Baada ya kujifunza matukio hayo, alijifunza vitabu vya Kishia; na akavutiwa na ukweli wauzungumzao Shia.

Tangu hapo, amekuwa akizitembelea sehemu nyingi za Tanzania na Kenya. Huko Mombasa alitoa hotuba juu ya Ndoa ya Mut'a na baada ya hapo aliandika juu ya mada hiyo na kikachapishwa. Hivi hapa, ili kuusherekea mwaka wa 1400 wa Tukio la GhadiirKhum, amekiandika kitabu ulichokishika. Nimekicheki kitabu hiki na ninathibitisha kwamba rejea zilizotajwa kitabuni humu na tafsiri zao ni sahihi. Ninamwomba Allah Subhanahu wa Taala Akijaalie kitabu hiki kuwa njia ya hidaya kwa ajili ya watu na Amjaalie mwandishi wake Tawfiiq zaidi kuihudumia dini ya Mwenyezi Mungu kama inavyofundishwa mwenye Qur'an na Ahlul Bayt(a.s) .

Iwapo msomaji ye yote yule atataka kujua zaidi juu ya jambo lo lote lile lililotajwa kitabuni humu, anakaribishwa kumwandikia mwandishi huyu ambaye anwani yake imo kitabuni humu. Sayyid Saeed Akhtar Rizvi Mhubiri Mkuu Dar es Salaam Bilal Muslim Mission of Tanzania.

MWANDISHI WA KITABU HIKI

Jina langu ni OMAR JUMAA MAYUNGA. Nimezaliwa mwaka 1947 Mkoa wa Tabora katika Wilaya ya Igunga Tarafa ya Simbo. Mwaka 1957 baba yangu alianza kunisomesha Quran Tukufu, ilipofika mwaka 1959 nilianza masomo ya Kizungu katika Shule ya Msingi ya Simbo hadi mwaka 1962 nilipokaa nyumbani kuendelea na masomo ya Qur'an. Mwaka 1968 baba yangu alinipeleka mjini Tabora kusoma kwa Sheikh Mzee Fereji Farahani (Mwenyezi Mungu amrehemu) mpaka mwaka 1972 nilipokwenda Mombasa kujiunga na Madrasa ya Tahdhib Muslim School ambayo iliongozwa na Almarhum Al'ustadh Alwy Qasim. Kwa kipindi nilichosoma katika Madrasa hii, siwezi kusahau ukarimu niliopata nikiwa ugenini.

Kwanza kabisa Sheikh Muhamad Amran Bushir, ambaye yeye ndiye aliyenipokea kwa mara ya kwanza nyumbani kwake. Akanikirimu kwa ukarimu mkubwa, akanifanyia mambo yote na watoto wake.

Pili; Ustadh AIwy Qasimu aliyenipenda sana, akanisomesha kwa juhudi kubwa. Ustadh Alwy alinipatia vitabu vingi mbali mbali na akanisomesha kwa undani zaidi vitabu vya ibn Taymiyya, Ibn Qayyim Aljawziyya, na vya Muhammad Abdulwahabi.

Tatu; Maulamaa Sheikh Abdallah Saleh Alfarsy na Sheikh Muhammad Kasim Mazrui, ambao walikuwa machifu Kadhi wa Kenya. Kila mmoja alinisaidia sana kunipa maarifa na mwongozo mwema. Nilibaki katika Madrasa hii mpaka alipofariki Ustadh kwa ajali ya gari. Mwaka 1975 nilikwenda kusoma Ujiji - Kigoma, kwa Sheikh Khalfani Muhammad Kiumbe hadi 1976. Nikiwa Ujiji, Almarhum Mzee Husein Taufik Msanga alinihudumia kwakunipa kila masaada kwa muda wote nilioutumia katika masomo.

Mwaka 1976 nilikwenda kusoma Iringa kwa Sheikh Harith Khelef Khamis. Sheikh Harith kwa mapenzi yake makubwa juu yangu alinisomesha masomo mengi yenye maana sana. Nikiwa Iringa. Al'marhum Mzee Hasan Souf Imam wa Msikiti Mkuu wa Iringa, alinipokea akanipa chumba. Nilipata miada mingi mbalimbali kwa; Mzee Ali Fundi, Mzee Muhammad Bunnu, Mzee Muhammad Mbarak. Mpenzi wa roho yangu niliyeshikamana naye wakati mwingi, Al-haji Saburi Goha Momba ambave hatimaye alinioza binti yake.

Mwaka 1978 niliajiriwa katika Chuo cha Kiislamu- Chang'ombe, Dar es Salaam.

Mwaka 1980 Sheikh Abdallah Idd Chaurembo (Mwenyezi Mungu amrehemu) alinitaka niasisi "Madrasatu Ahli Sunnatu Waljamah" katika Msikiti wa Mtoro. Nilisomesha miezi mitatu nikaandika barua ya kujiuzulu ya tarehe 2J.5.1980 kwa nia ya kuasisi Madrasa yangu binafsi. Mwaka 1982 niliandika kitabu: "Jawabu la wazi kwa wateteao bid'a" kilichochapishwa Dar es Salaam tarehe 27.1J.1982.

Kitabu hiki kilitetea msimamo wa Kiwahabi, na kabla ya hapo niliandika Makala mbali mbali kwa mujibu wa matukio yaliyotokea kati yangu na baadhi ya Masheikh. Aidha mwaka 1982 nilikwenda mara nyingi Bujumbura, huko nilitoa mihadhara mingi mikubwa katika Msikiti wa Bwiza. Mihadhara hiyo niliielekeza Bujumbura tokea mwaka 1982 hadi 1985. Kisha nilielekeza mihadhara hiyo mjini Lusaka - Zambia. Mwaka 1985 vile vile nilikwenda Saudi Arabia katika Ofisi ya Muslim World League mara tatu, kwa lengo la kupanua mawasiliano baina ya Madrasa yangu na taasisi mbali mbali za Kimataifa.

Mwaka 1986 nilikwenda Mombasa - Kenya huko nilikutana na Sheikh Abdillah Nasir: Nilipata nafasi ya kuzungumza naye mambo mengi kuhusu msimamo wa dini. Jambo lililojitokeza zaidi katika mazungumzo yetu ni Usunni na Ushia, na ilipohitajika kupata vitabu vya Kishia ndipo aliponikutanisha na Sheikh Ali Muhammad Jaafar, Kiongozi wa Bilal Muslim Mission ya Kenya. Naye alinipatia vitabu "Aslus Shia wausuluha, Al-murajaatu, Fadhailu Lkhamsa." Niliporudi Dar es Salaam nilivisoma kwa makini na kufuatilia vitabu vya Kisunni vilivyoonyeshwa humo. Na nilikuwa karibu sana na Mwanachuo wa Kishia hapa Dar es Salaam Maulana Sayyid Saeed Akthar Rizvi. Nilikuwa na nukta kadhaa zilizonikera dhidi ya Shia, kwa hivyo nilimuomba Maulana Rizvi anipatie wakati wa kutosha ili tuzijadili hizo nukta. Mbali na shughuli zake nyingi alizokuwa nazo, Maulana alinipatia siku mbili kwa wiki. Baadhi ya nukta tulizozichambua ni:- Tahriful Qur'an, Imamah, Taqiyya, na Mut'a. Sayyid Saeed Akthar Rizvi mbali na kunijibu nukta hizi, lakini pia amenifundisha na kunionyesha mengi sana yaliyomo katika vitabu vya Kisunni. Kisha alinipa kitabu "AIghadir" akaninyesha yaliyomo humo, na Kisha tulifuatilia baadhi ya nukta zilizotajwa katika "Alghadir" kwa vitabu vya Kisunni. Kwa utafiti huu wa pamoja katika vitabu vya kutegemeka vya Kisunni, ambavyo ndivyo vimenifanya kuwa Shia lthnaasheri. Baadhi ya vitabu hivyo ni:- Sahihi Bukhari, Sahihi Muslim, Tarikhut Tabari, Tarikh Ibn Athir, Mizanul Itidal na Tafsir nyingi za Quran, nimeamua kuwa: "Mimi ni Shia Ithna-asheria, nitafuata sheria na kanuni zake katika uhai wangu na baadaye Insha-Allah". Tarehe J.9.1986 nilialikwa na Bilal Muslim Mission ya Kenya, katika Majlis ya kukumbuka mauaji ya Imam Husein(a.s.) .

Tarehe 8.9.1986 mimi nilisoma Majlis katika ukumbi wa Huseiniyya Mombasa. Hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kupanda katika Mimbari na kusoma habari za watukufu wa nyumba ya Mtume(s.a.w.w) . Tarehe 20.1J.1987 nilialikwa kuhudhuria Mkutano mjini Tehran-Iran, mkutano ambao ulizungumzia mauaji ya kinyama walio fanyiwa ndugu zetu Mahujaji na askari wa Kisaudia katika Haram ya Makka. Katika Mkutano huo mimi nilipata nafasi ya kuhutubia kwa kulaani kitendo cha kinyama cha mauaji ambayo askari wa Kisaudi waliwauwa Mahujaji wasio na hatia. Mwaka 1987 nilifasiri Dua Kumayl kilichochapishwa Mombasa - Kenya Mwaka 1989, Tarehe 24.10.1989 niliandika kitabu:- "Mut'a ndoa sahihi" kilichochapishwa Dar es Salaam tarehe 8.3.1990. Tarehe 8.7.1990 nilialikwa kuhudhuria sherehe ya Imam Ali(a.s) mjini London. Sherehe ambayo mwaka 1410 Hijiria ilikuwa inatimia karne kumi na nne tokea Imam Ali(a.s) atangazwe na mtume(s.a.w.w) hadharani katika bonde la Khum. Nilibahatika kuchaguliwa na kamati ya maandalizi ya Mkutano huu kuwa mmoja wa watakaohutubia katika hafla hii. Tarehe 13.7.1990 katika majira ya jioni, nilihutubia katika ukumbi wa Hotel ya Ramada mjini London. Katika hafla hii kuna zawadi maalum ilitengwa kwa ajili ya wale watakaofanya vizuri. Mimi nilibahatika kutunikiwa saa yaa mkono yenye nembo ya ujumbe maalum wa lile agizo la Mtume(s.a.w.w) juu ya Imam Ali (a.s) siku ya Ghadir Khum, kuwa yeye Imam Ali(a.s) ni Kiongozi wa Waumini baada yake aliposema: "Ambaye mimi ni kiongozi wake, basi huyu Ali ni kiongozi wake".

UTANGULIZI

Ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwafikisha mara nyingine kukamilisha kuandika kitabu hiki, baada ya kitabu chetu:- "Mut'a ndoa sahihi." Mambo yanayoweza kuamsha misimamo ya watu na kuleta msukumo mpya katika kumwandaa binadamu ili apige hatua mbele, ni kujua habari za watukufu wao waliotangulia. Kwa sababu kujua habari za watangulizi wetu ni mizani ya kutupimia sisi tunaokuja baada yao. Katika kitabu hiki, nimetaja mambo ambayo ingawa yanajulikna na wengi, lakini ni mageni katika kusema. Wanaoyajua kuwa ni kweli si kidogo, lakini wengi wanaogopa kuyasema au wametiliwa itikadi potovu kuwa hayafai kusema. Bila shaka yakionekana katika kitabu hiki itakuwa dhambi kubwa kwao. Sisi nasi tunaamini kuwa Haki ni lazima isemwe, sawa sawa itawaridhi watu au haitawaridhi.

"Na lau haki ingefuata mapenzi yao basi mbingu na nchi zingeharibika ." 23:71.

Ninawashukuru wote waliokipitia Kitabu hiki kukisahihisha, na wakanipa maoni yao yenye thamani kubwa. Mwenyezi Mungu awalipe malipo mema duniani na akhera.

OMARI JUMAA MAYUNGA UIMAM

Msimamo wa Aya zilizokuja juu ya uongozi

ukisoma yalioandikwa katika vitabu mbali mbali na Hadithi zilizothibiti, na tarikh inayoonyesha katika jambo hili, utapata mambo makuu matatu ambayo yanaonyesha kuwa: Uimam (Ukhalifa) lazima uteuliwe na Mwenyezi Mungu. Na kwa upande wa pili utaona kuwa Nyimati zilizopita zilifuata uongozi uliochaguliwa na Mwenyezi Mungu, wala jambo hilo halikuachiwa watu wenyewe kwa njia ya kuchaguwana. Jambo la kwanza lililoongoza baina ya Mtume waliopita ilikuwa ni kusalimu amri na kufuata uongozi wa Mwenyezi Mungu, na kila alipoondoka Mtume aliweka atakaeshika nafasi yake. Wengi wao waliorithi kazi zoa walikuwa Manabii, hata hivyo baadhi yao hawakuwa Manabii bali walikuwa Mawasii tu. Jambo la pili: Uongozi katika nyimati zilizopita ulipatikana kwa njia ya kurithi baina ya vizazi katika koo za Mitume kama tunavyosoma katika Aya zifuatazo:

A. "Hakika Mwenyezi Mungu alimchagua Adam na Nuh na Kizazi cha Ibrahim na Kizazi cha Imrani juu ya walimwengu wote. Ni kizazi cha wao kwa wao, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia Mwenye kujua " (Qur’an: 3:33-34)

B. "Na tulimpa Isihaqa na Yaaquubu na tukaweka katika Kizazi chake Unabii na Kitabu , na tukampa ujira wake katika dunia. Nae katika akhera kwa hakika atakuwa miongoni mwa watu wema ." 29:27

C. "Na hakika tulimpeleka Nuhu na Ibrahim na tukauweka katika kizazi chao Unabii na kitabu ." 57:26

D.Mwenyezi Mungu alimweka Ibrahim kuwa Imam (Kiongozi wa watu). Ibrahim alimuomba Mola wake awape nafasi hiyo vile vile katika kizazi chake. Mwenyezi Mungu hakumkemea wala kumgombeza, ila alimwambia ya kuwa: "Haiwafakii ahadi yangu (Unabii and Uimam) watu madhalimu ." 2:124.

Nabii Musa(a.s) alipoomba kwa Mwenyezi Mungu ndugu yake Haruna awe msaidizi wake katika uongozi, Mwenyezi Mungu hakumkasirikia wala kumkatalia ombi hilo.

وَاجْعَل لِّي وَزِيرًا مِّنْ أَهْلِي ﴿٢٩﴾ هَارُونَ أَخِي ﴿٣٠﴾ اشْدُدْ بِهِ أَزْرِي ﴿٣١﴾ وَأَشْرِكْهُ فِي أَمْرِي ﴿٣٢﴾ كَيْ نُسَبِّحَكَ كَثِيرًا ﴿٣٣﴾ وَنَذْكُرَكَ كَثِيرًا ﴿٣٤﴾ إِنَّكَ كُنتَ بِنَا بَصِيرًا ﴿٣٥﴾ قَالَ قَدْ أُوتِيتَ سُؤْلَكَ يَا مُوسَىٰ ﴿٣٦

"Na unijaalie waziri katika jamaa zangu, Haruna ndugu yangu. Uniimarishe kwake nguvu zangu, na umshirikishe katika kazi yangu. Ili tukutukuze sana, na tukutaje kwa wingi. Hakika wewe unatuona, akasema hakika umepewa maombi yako ewe Musa" 20:29-36.

Musa alimweka Haruna kuwa Khalifa wake alipoondoka, kama Quran inavyosema:

وَوَاعَدْنَا مُوسَىٰ ثَلَاثِينَ لَيْلَةً وَأَتْمَمْنَاهَا بِعَشْرٍ فَتَمَّ مِيقَاتُ رَبِّهِ أَرْبَعِينَ لَيْلَةً وَقَالَ مُوسَىٰ لِأَخِيهِ هَارُونَ اخْلُفْنِي فِي قَوْمِي وَأَصْلِحْ وَلَا تَتَّبِعْ سَبِيلَ الْمُفْسِدِينَ ﴿١٤٢﴾

"Na tulimwahidi Musa siku thelathini na tukatimiza kwa kumi ikatimia miadi ya Mola wake siku arobaini. Na Musa akamwambia ndugu yake Haruna: Shika mahala pangu katika watu wangu na usuluhishe wala usifuate njia ya waharibifu." 7:142.

Katika Aya hizi tumeona nafasi ya Uongozi unavyoendelea kati ya Kizazi na Kizazi baina ya koo za Manabii.

Mtiririko huu ikiwa umejengeka kwa Wahyi katika nyimati zilizopita katika suala la Khilafa, basi kubadili utaratibu huo katika Islam lazima ipatikane dalili na ufafanuzi. Jambo la tatu: Kumbukumbu za tarikh ya Mitume inaonyesha waziwazi kuwa: Kila alipoondoka Mtume aliweka mtu wa kushika mahala pake, na hapa tutaonyesha kwa ufupi: Wakati iliposhuka Aya 214 katika Sura ya Ash'Shuaraa, Mtukufu Mtume(s.a.w.w) alisema:

"Enyi Bani Abdil Muttalib! Hakika mimi wallahi simjui kijana yeyote katika Waarabu, aliyewaletea watu jambo bora kabisa kuliko nililokuleteeni mimi. Hakika mimi nimekuleteeni kheri ya dunia na ya akhera, Mwenyezi Mungu ameniamrisha nikuiteni kwake, basi nani kati yenu atakaenisaidia jambo hili ili awe ndugu yangu na wasii wangu na Khalifa wangu kwenu? Watu wote wakanyamaza, nikasema (Ali) na mimi ni mdogo wao kwa umri mng'avu wao wa macho, mkubwa wao wa tumbo, mnene wa miundi, mimi ewe Nabii wa Mwenyezi Mungu nitakuwa waziri wako. Pale pale akanishika shingo yangu, kisha akasema: Hakika huyu ni ndugu yangu, na wasii wangu, na Khalifa wangu kwenu, basi msikilizeni na mtiini ".

Akili, na maandiko, pamoja na matukio ya tarikh, vyote vinaonyesha kwa pamoja kuwa: Msingi wa asili katika hukumu ni maamuzi ya Mwenyezi Mungu tu peke yake, na yeye ndiye anayemtawalisha amtakae katika waja wake. Tukio la Ghadir Khum ni tangazo muhimu Ia uongozi mkuu, lililokamilisha dini na neema na radhi ya Mola. Tarehe kumi na nane mfungo tatu Mtukufu Mtume(s.a.w.w) alipokuwa akirejea Madina kutoka Makka katika mwaka wa kumi baada ya kumaliza ibada ya Hija alifika mahali katika bonde la Khum akiwa na Waislam zaidi ya laki moja. Mwenyezi Mungu akateremsha Aya: "Ewe Mjumbe fikisha uliyoteremshiwa kutoka kwa Mola wako, na kama hutafanya, basi hukufikisha ujumbe wake. Na Mwenyezi Mungu atakulinda na watu, hakika Mwenyezi Mungu hawaongozi watu wanaokufuru " 5:67.

Baada ya kushuka Aya hii, Mtume(s.a.w.w) alimshika mkono Imam Ali(a.s) akasema: "Ambaye mimi natawalia mambo yake, basi huyu Ali ni mtawala wake. Ee Mola! Muunge atakae muunga, na mfanyie uadui atakae mfanyia uadui ". Ilipokamilika hutuba ya Mtume(s.a.w.w) Masahaba walianza kutoa kiapo cha utiifu kwa Imam Ali (a.s) kama tunavyomnukuu hapa Umar bin Khattab:

"Hongera ewe mwana wa Abu Twalib sasa umekuwa kiongozi wangu na kiongozi wa Waislamu wote ".

Taz; Tarikhu Dhahbi J.2 Uk. 197 Tariku Baghdad J.8 Uk. 290 Tarikhu Ibn Asakir J.2 Uk. 45 Al Isaba J.1 Uk. 305 Tafsirul Kabir J.12 Uk. 49 Addurrul Manthur J.5 Uk. 182 Ansabul Ashraf J.2 Uk. 315 Albidayatu Wannihaya J.7 Uk. 359.

Hata hivyo, wako baadhi ya Masahaba waliopinga kitendo hiki cha kutoa kiapo cha utiifu kwa Imam Ali(a.s) Baada ya Masahaba kutoa kiapo cha utiifu kwa Imam Ali(a.s) Harithi bin Nuuman Al'fahri, alimkabili Mtume(s.a.w.w) akamwambia: Ewe Muhammad! umetuamrisha kushuhudia kuwa hapana apasae kuabudiwa ila Mwenyezi Mungu na wewe ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu, tumekubali. Umetuamrisha kusali mara tano kila siku, tumekubali. Umetuamrisha kutoazaka katika mali yetu, tumekubali. Umetuamrisha kufunga mwezi wa Ramadhani kila mwaka, tumekubali. Umetuamrisha Kuhiji AI'kaaba, tumekubali. Kisha hukutosheka yote haya mpaka umempandisha mtoto wa ammi yako juu ya shingo zetu! Hili ni wazo lako au ni amri kutoka kwa Mwenyezi Mungu?" Mtume(s.a.w.w) akajibu: "Wallahi, hapana apasae kuabudiwa ila Mwenyezi Mungu, hili si langu isipokuwa ni Wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu ". Harithi akaondoka zake na huku akisema: "Ee Mola! ikiwa haya anayosema Muhammad ni kweli, basi tuteremshie mvua ya mawe au tuletee adhabu nyingine kali". Naam, pale pale alipokuwa, Mwenyezi Mungu akamdondoshea kijiwe kikagonga utosini kikatokezea kwenye tundu ya nyuma akafa papo hapo. Mwenyezi Mungu akateremsha Aya ya kwanza na ya pili katika Suratul Ma'ariji: "Muombaji aliomba juu ya adhabu itakayotokea, kwa makafiri hapana awezae kuzuia"

Taz: Tafsirul Qurtubi J.18 Uk. 278.

Tukio la Ghadir Khum ni ujumbe muhimu sana kwa Waislamu, na kila anayeshuhudia: "LAA ILAHA ILLA LLAHU MUHAMMADUN RASULULLAH" Lazima vile vile atoe kiapo cha utiifu kwa uongozi wa Ahlul Bait(a.s) . Kwa sababu tarikh inaonyesha kuwa Masahaba waliokataa kutoa kiapo chao kwa Imam Ali, Mwenyezi Mungu aliwaadhibu. Katika hao walioadhibiwa ni huyu Harithi bin Nuumani Al'fahri, kama ulivyoona kisa chake hapo juu. Pia tarikh inaonyesha kuwa Sahaba Zaid bin Ar'qam alipotengua kiapo chake cha utiifu kwa Ahlul Bait, alipofuka macho yake mara moja. Taz: Manaqibul Imam Ali Uk. 23.

MUBAHALA

Kabla hatujaingia ndani kuzungumzia suala la Mubahala, kwanza ni vizuri tufahamishe maana ya Mubahala. Muhabala ni: Kuapizana. Ujumbe wa Kikristo kutoka Najran ulifika kwa Mtume kujadili suala la Nabii Isa(a.s) . Mtume aliwajulisha kuwa:

إِنَّ مَثَلَ عِيسَىٰ عِندَ اللَّـهِ كَمَثَلِ آدَمَ خَلَقَهُ مِن تُرَابٍ ثُمَّ قَالَ لَهُ كُن فَيَكُونُ ﴿٥٩﴾

Hakika mfano wa Isa mbele ya Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa Adam, aliumbwa kwa udongo kisha akamwambia: Kuwa naye akawa. (Qur’an 3:59).

Kwakuwa Nabii Isa alizaliwa bila baba, Wakristo wamedhani kuwa baba yake ni Mwenyezi Mungu. Aya hii inaondoa dhana hiyo ambayo inapingana na utukufu wa Mwenyezi Mungu, na inawapigia mfano wa ajabu zaidi katika kuumbwa Adam bila ya baba wala mama. Aliumbwa kwa udongo kisha akaambiwa: kuwa naye akawa, na kwa neno hilo hilo Nabii Isa(a.s) ndivyo alivyoumbwa. Ujumbe huo ulipokuwa haukukubaliana na hoja hii, Mwenyezi Mungu akateremsha Aya:

فَمَنْ حَاجَّكَ فِيهِ مِن بَعْدِ مَا جَاءَكَ مِنَ الْعِلْمِ فَقُلْ تَعَالَوْا نَدْعُ أَبْنَاءَنَا وَأَبْنَاءَكُمْ وَنِسَاءَنَا وَنِسَاءَكُمْ وَأَنفُسَنَا وَأَنفُسَكُمْ ثُمَّ نَبْتَهِلْ فَنَجْعَل لَّعْنَتَ اللَّـهِ عَلَى الْكَاذِبِينَ ﴿٦١﴾

"Na atakayehojiana nawe (Muhammad) katika hili baada ya ujuzi uliokufikia, waambie: Njooni tuwaite watoto wetu na watoto wenu, na wanawake wetu na wanawake wenu, na nafsi zetu na nafis zenu, kisha tuombe kwa kunyenyekea tuijaalie laana ya Mwenyezi Mungu iwashukie wenye kusema uongo." (Qur’an 3:61).

Hili ilikuwa tarehe ishirini na nne mfungo tatu mwaka wa kumi, Mtume akawaita ili waanze kuapizana. Wakajibu: "Ngojea tujadiliane". Walipokwenda faragha, wakamuuliza Askofu Abdul Masih; ana Maoni gani katika suala hili? Akajibu: Enyi Wakristo: Wallahi nyinyi mnajua kuwa Muhammad ni Nabii aliyeletwa na amekuja na ushahidi ulio wazi juu ya jambo la huyu (isaa.s. ). Wallahi hakuna watu walioapizana na Nabii wakasalimika, ikiwa mtaapizana naye mtaangamia". Usqufu yeye aliwaambia: "Enyi Wakristo: Mimi naziona nyuso hizi (kundi la Mtume) kama zitamuomba Mwenyezi Mungu auondoe mlima kutoka mahala pake, Wallahi atauondoa. Msiapizane naye mtaangamia, na hatabaki Mkristo ye yote hapa duniani mpaka siku ya Kiama ".

Alipoulizwa Ahtam, akawaambia: Niacheni nikamuulize Muhammad, alipomkabili Mtume akamuuliza, "Ewe Abulqasim'! Unatoka na kina nani kwa ajili ya maapizano haya?" Mtume(s.a.w.w) akamjibu: "Ninaapizana nanyi nikiwa na watu bora hapa duniani na watukufu mno mbele ya Mwenyezi Mungu, nao ni hawa (akawaonyesha) Ali, Fatima, Hasan na Husein." Wakaogopa kuapizana na Mtume, na badala yake wakaomba sulhu kwa Mtume(s.a.w.w) kwa kutoa dirham arobaini elfu.

Taz: Tarikh Ibn Athir J.2 Uk. 200. Tafsirul Qurtubi J.4 Uk. 104. Tafsirul Ibn Kathir J.1 Uk. 376-379. Tafsirul Khazin J.1 Uk. 359-360. Tafsirul Maragh J.3 Uk. 175. Tafsirul Kabir J.8 Uk. 81. Zadul Masir J.1 UK. 399.

Katika Ayatul Mubahala, iliposema: "Tuwaite watoto wetu " Mtume(s.a.w.w) alimwita:Hasan na Husein . Iliposema: " Na wanawake wetu " Mtume(s.a.w.w) alimwita: "Fatima bint Muhammad ". Iliposema: " Na nafsi zetu " mtume akamwita: "Ali ". Kwa hivyo Ali bin Abi Talib ni nafsi ya Mtume Muhamad(s.a.w.w) . Tukio hili Ia Mubahala tukilitazama kwa upande wa pili, linatukumbusha lile tukio la "Kisaa " Iliposhuka Ayatut Tat'hir:

إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّـهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ وَيُطَهِّرَكُمْ تَطْهِيرًا ﴿٣٣﴾

Hakika Mwenyezi Mungu anataka kukuondoleeni uchafu watu wa nyumba (ya Mtume) na (anataka) kukutakaseni sana sana" (Qur’an 33:33).

Iliposhuka Aya hii Mtume alimchukua Ali na Fatima na Hasan na Husein, akawafunika nguo kisha akasema: "Ee Mola! Hawa ni watu wa nyumba yangu, basi waondolee uchafu na uwatakase sana sana ". Mama Ummu Salma (mke wa Mtume) alipotaka kuingia humo, Mtume(s.a.w.w) akamzuia: Kama ambavyo kwenye tukio la Mubahala ulipofika wakati wa kuomba maombi maalum kwa ajili ya maapizano kati yake na Wakristo wa Najrani, Mtume alimchukua Ali na Fatima na Hasan na Husein tu. Ingawa wakati huo Mtume(s.a.w.w) alikuwa nao wakeze, na Masahaba ambao ni marafiki zake pia, lakini hapa hawakuingia. Wake za Mtume na Masahaba hawakuingia katika "KISAA" na hawakusimama katika uwanja wa Mubahala, kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwahusisha darja hii Ahlul Bait tu peke yao. Taz: Tafsirul Khazin J.3 Uk. 259 Tafsirul Ibn Kathir J.3 Uk. 494 Tafsirul Qurtubi J.14 Uk. 183 Zadul Masir J.6 Uk. 381.