HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2

HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 20%

HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2 Mwandishi:
Kundi: VITABU VYA HADITHI

HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2

Mwandishi: AMIRALY M.H.DATOO
Kundi:

Matembeleo: 19982
Pakua: 3231

Maelezo zaidi:

HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 11 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 19982 / Pakua: 3231
Kiwango Kiwango Kiwango
HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2

HADITH ZA MTUME s.a.w.w.NA MA-IMAMU a.s.V0L 2

Mwandishi:
Swahili

8

HADITH ZA MTUME (s.a.w.w).NA MA-IMAMU(a.s)

SEHEMU YA PILI

1560. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kutawaliwa na dhana mbaya hakubakii amani baina yake na rafiki yake ."[253]

1561. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Dhana mbaya hufisidi mambo na huchochea maovu ."[254]

1562. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadhari na ghera (inayotokana na kushuku) mahali si pake, kwani humtia mzima maradhi na humshuku asiyekuwa na hatia ."[255]

1563. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Humwoni mwenye kushuku kuwa mzima ."[256]

1564. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Yule ambaye dhana yake si nzuri humwogopa kila mtu. "[257]

1565. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Nyoyo zina kumbukumbu mbaya ambazo huchukiwa na akili ."[258]

1566. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwovu hamdhanii vizuri mtu mwingine kwa kuwa haoni kwake ila tabia yake mwenyewe ."[259]

1567. Qur'an Tukufu, Surah An-Nahl, 16, Ayah 105, inasema wazi kwamba mwongo yuko nje ya jamii ya Waislamu: Wanaozua uwongo ni wale wasioziamini ayah za Allah swt, na hao ndio waongo (hasa)!"

1568. Mtume Muhammad(s.a.w.w) . amesema: "Halahala na ukweli, kwani ukweli huongoza kwenye wema, na wema huongoza kwenye Jannat. Mtu haachi kusema ukweli na kutafuta ukweli mpaka aandikwe ni mkweli mbele ya Allah swt. Na jihadharini na uwongo, kwani uwongo huelekeza kwenye ufisadi, na ufisadi huelekeza kwenye Moto. Mtu haachi kusema uwongo na kufuata uwongo mpaka aandikwe ni mwongo mbele ya Allah swt ." [260]

1569. Mtume Muhammad(s.a.w.w) . amesema: "Watu wenye kuwasadiki upesi wengine ni watu wenye kusema kweli kuliko wengine; na watu wenye kuwakadhibisha zaidi wengine ni watu wenye kusema uwongo kuliko wote ." [261]

1570. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Lau vitu vingeainishwa (kwa ulingano wao), ukweli ungekuwa pamoja na ushujaa, na uwongo ungekuwa pamoja na uwoga. "[262]

1571. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amejata matunda ya kusema kweli katika usemi mfupi huu: "Msema kweli hujichumia vitu vitatu: kuaminiwa, kupendwa na kuheshimiwa. "[263]

1572. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: Usulu 'l-Kafi, jz. 1, uk. 460. "Msidanganywe na sala na saumu zao, kwani huenda mtu akawa amezoea kusali na kufunga na endapo ataziacha ataona taabu. Hivyo, wajaribuni katika kusema ukweli na kuweka amana ."

1573. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Tabia mbaya kabisa ni kusema uwongo. "[264]

1574. Al Imam Hasan Askari(a.s) . amesema: "Maovu yote yamewekwa katika nyumba moja, na ufunguo wake ni uwongo ."[265]

1575. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadharini na wanafiki, kwani wao ni wapotevu na wanapoteza (watu). Nyoyo zao zina maradhi lakini nyuso zao ni safi ."[266]

1576. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Maneno ya mnafiki ni matamu lakini moyo wake ni maradhi ."[267]

1577. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . ametoa taswira nzuri ya mnafiki kwa kusema: "Mfano wa mnafiki ni kama kondoo anayebabaika kati ya makundi mawili ya kondoo ." [268]

1578. Mtume Muhammad(s.a.w.w) . ametoa alama tatu za kauleni: "Na mnafiki ana alama tatu: anaposema husema uwongo, anapotoa ahadi huvunja, na anapoaminiwa hufanya hiana ." [269]

1579. Al Imam Muhammad Baqir(a.s) . amesema: "Ni uovu mno kwa mja kuwa na nyuso mbili na ndimi mbili. Humsifu nduguye mbele yake lakini humsengenya nyuma yake. Akifanikiwa humwonea wivu, na akipata mashaka humtupa ."[270]

1580. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mnafiki hujisifu mwenyewe na huwakejeli watu wengine ."[271]

1581. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amemdondoa Luqman akimwusia mwanawe haya: "Mnafiki ana alama tatu: ulimi wake hukinzana na moyo wake, moyo wake hukinzana na vitendo vyake, na dhahiri yake hukinzana na batini yake ."[272]

1582. Mtu mmoja alimwuliza Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) : "Mtu mmoja alikuja kwangu na kuniambia kwamba ananipenda sana. Vipi nitajua kama kweli ananipenda sana?" Imam (a.s) . akamjibu; "Tahini moyo wako. Ukimpenda, basi anakupenda. Tazama moyo wako. Ukimkataa mwenzako, basi mmoja wenu ana ila ."[273]

1583. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Dhamiri safi ni ushahidi bora zaidi wa ukweli kuliko lugha fasihi ."[274]

1584. Qur'an Tukufu, Surah Al Hujaraat, 49, Ayah 12, inatoa picha ya maana halisi ya usengenyaji katika jumla ndogo na fasihi: Je, mmoja wenu anapenda kula nyama ya nduguye aliyekufa?"

1585. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mimi nimetumwa kukukuzieni na kukukumilishieni maadili mema ."

1586. Mtume Muhammad(s.a.w.w) . amesema: "Ukiwepo katika baraza ambapo mtu mmoja husengenywa, basi msaidie mtu huyo, au wakataze wasengenyaji, au ondoka hapo ." [275]

1587. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mwenye kumtetea nduguye anayesemwa kwa ubaya wakati hayupo, hustahiki kwa Allah swt kuepushwa na Moto ." [276]

1588. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema pia: "Mwenye kumsengenya Mwislamu, Allah swt hatazikubali funga na sala zake za mchana na usiku arobaini mpaka asemehewe na msengenywa Na mwenye kumsema Mwislamu katika Mwezi wa Ramadhani, hatapewa thawabu ya kufunga. "[277]

1589. Mtume Muhammad(s.a.w.w) . wa Waislamu amewasifu Waislamu kwa sifa hii: "Mwislamu ni mwenye kuwasalimisha Waislamu kutokana na mikono na ulimi wake ."

1590. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kumsengenya ni juhudi za mtu dhaifu. "[278]

1591. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: "Yatakikana muumin awe ni kiburudisho cha (roho ya) muumin (mwenzake) kama vile maji baridi yanavyokata na kutuliza kiu ."[279]

1592. Al Imam Muhammad Baqir(a.s) . amesema: "Inatosha kuthibitisha aibu ya mtu anayeona aibu za watu wengine bila ya kuona yake mwenyewe, au anayewagombeza watu jambo ambalo yeye mwenyewe anashindwa kuliacha, au anayemwudhi rafiki yake kwa jambo lisilomhusu ."[280]

1593. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ameonyesha nukta muhimu juu ya maudhui hii pale aliposema: "Mtu bora kuliko wote mbele yako ni yule mwenye kukuonyesha aibu zako na kuisaidia nafsi yako ."[281]

1594. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye (kutaka) kutafuta aibu za watu, aanze na zake ."[282]

1595. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Inatosha mtu kujifanya mpumbavu mwenyewe kwa kutazama aibu za watu wengine huku akizificha zake ."[283]

1596. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema maneno matamu na yenye kuvutia kuhusu utambuaji na utibabu wa maradhi ya kinafsi kwa njia ya mtu mwenyewe kujichungua: "Ni lazima kwa mwenye akili kuichungua nafsi yake na kuziona dosari zake katika dini, maoni, maadili na adabu; kisha azikusanye (azihifadhi) katika kitabu na achukue hatua ya kuziangamiza ."[284]

1597. Qur'an Tukufu, Surah An-Nisaa, 4, Ayah 32, inasema:Wala msitamani vile ambavyo Allah swt amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine ."

1598. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: "Asili ya kijicho ni upofu wa moyo na ukanyaji wa fadhila na neema za Allah swt. Sifa hizo ni mabawa mawili ya ukafiri. Kijicho humtia mwanadamu katika uchungu wa daima na humwangamiza kabisa kabisa asiokoke kamwe ."[285]

1599. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema":Watendeeni sawasawa watoto wenu mnapowapa zawadi ." [286]

1600. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ametaja madhara ya kimwili ya kijicho: "Naustaajabia mghafala wa mahasidi juu ya uzima wa miili yao ."[287]

1601. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib (a.s). amesema: "Kijicho huuangamiza mwili. "[288]

1602. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadharini na uhasidi, kwani huitia ila nafsi. "[289]

1603. Al Imam Zaynul Abidin(a.s) . alimwomba Allah swt hivi: "Ewe Allah swt! Teremsha rehema na baraka kwa Muhammad na Aali za Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) ; na nipe kifua kilichohifadhika na uhasidi, ili kwamba nisimwonee wivu yoyote kati ya viumbe Vyako juu ya fadhila Zako; wala nisione kijicho juu ya neema Zako ulizompa yeyote kati ya viumbe Vyako - ziwe ni neema za dini au dunia, afya au takwa, nyingi au nyepesi, ila kwamba nitamani bora zaidi kwa ajili yangu lakini kutoka Kwako peke Yako, (Ewe) usiye na mshirika."[290]

1604. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Shindaneni katika maadili yanayovutia, matumaini makubwa na mawazo matukufu ili mpate jazaa kubwa ."[291]

1605. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Lau Allah swt angeruhusu kiburi kwa waja wake, basi angewaruhusu Manabii na Mawalii Wake. Lakini Allah swt amewakataza kuwa na kiburi na amewaridhia kuwa na unyenyekevu. Hivyo, huweka videvu vyao juu ya ardhi (kumnyenyekea Allah swt), huzisugua nyuso zao kwenye ardhi, na huwanyenyekea waumini. "

1606. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Jiepusheni na kiburi, kwani mja anapotakabari, Allah swt husema: 'Mwandikeni mja huyu miongoni mwa waasi. " [292]

1607. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . ametaja kwa ufupi asili ya kinafsi ya ndweo na majivuno: "Hakuna mtu anayeugua kiburi ila kwamba amehisi uduni (dhila) nafsini mwake ."[293]

1608. Al Imam Musa bin Jaafar(a.s) . amesema: "Maringo na majivuno yana vidato; kimojawapo ni kumpambia mja amali yake mbaya akaiona nzuri na akaipenda na kufikiria kwamba amefanya vizuri ."[294]

1609. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadhari na kujipenda (kujiona) mwenyewe, kwani utazidiwa na wenye kukuchukia. "[295]

1610. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kiburi huharibu akili ."[296]

1611. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kudhoofisha fikra zake huimarisha ghururi yake. "[297]

1612. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Unyenyekevu ni kiini cha akili, na majivuno ni kiini cha ujinga ."[298]

1613. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kibur ni maradhi ya ndani ." [299]

1614. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kuona bora mwendo wake, hushindwa kurekebisha nafsi yake ."[300]

1615. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kujipenda nafsi yake haoni aibu zake, na lau angejua mema ya wengine angetengeneza dosari na hasara zake. "[301]

1616. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jikingeni kwa Allah swt kutokana na ulevi wa utajiri, kwani una nishai (ulevi) inayochelewa kutoka ."[302]

1617. Siku moja tajiri mmoja alikwenda katika baraza la Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . Baadaye akaja maskini mmoja na akakaa karibu na tajiri huyo. Tajiri akakusanya nguo zake alipomwona maskini amakaa ubavuni mwake. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . akamwambia tajiri: "Unaogopa umaskini wake ukuguse?" Tajiri akajibu: "Hapana!" Akamwuliza: "Unaogopa sehemu ya mali yako aipate yeye?" Akajibu: "Hapana!" Akamwuliza: "Unaogopa nguo zako ziingie uchafu?" Akajibu: "Hapana!" Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . akamwuliza: "Basi kwa nini umezikusanya nguo zako na umekikunja kipaji chako?" Tajiri akasema: "Ewe mtume wa Allah swt! Utajiri wangu na mali zangu zimenifumba macho yangu nisitambue uhakika, na zimenifanya niyaone mazuri yale mabaya yangu. Kwa kufuta kosa hilo lisilofaa, natoa nusu ya mali zangu kumpa maskini huyu." Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . akamwuliza maskini: "Je, unaikubali tuzo hiyo?" Maskini akakataa, na alipoulizwa sababu yake, akasema: "Naogopa nami pia nisiwe na sifa mbaya kama yake baada ya kuwa na utajiri mwingi."

1618. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Wafanyieni uadilifu watoto wenu katika kutoa zawadi kama vile mtakavyopenda wakufanyieni uadilifu kwa mema na mapenzi ." [303]

1619. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mcheni Allah swt na adiliana na watoto wenu kama vile mpendavyo wakutendeeni wema. " [304]

1620. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Wafanyie (Wamisri) uadilifu, endeana nao kwa upole, changamka nao, na fanya insafu katika kuwatazama pia ili kwamba watukufu wasitazamie dhuluma kutoka kwako wala wanyonge wasikate tamaa ya kuona uadilifu kutoka kwako ."[305]

1621. Mabalozi wa Allah swt ni waasisi wa uadilifu na waratibu wa sera ya ukamilifu wa mwanadamu. Katika zama za ukhalifa wa Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) ., siku moja Aqil alikwenda kwa ndugu yake mtawala (yaani Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . Baada ya kumwelezea matatizo yake na umaskini wake, akamshika nduguye (Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ampe karibu mani moja (ratili mbili) ya ngano zaidi kuliko sehemu yake kutoka Baitul Maal (Hazina). Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . badala ya kumkubalia akamsogezea kipande cha chuma kilichopashwa moto ili kumwonya. Aqil akapiga kelele. Hapo Imam(a.s) . akamwambia: "Ewe Aqil! Mamako akulilie! Unapiga kelele hivyo kwa kuogopa kipande cha chuma tu kilichopashwa moto na mtu, lakini mimi nitavumilia vipi moto utakaowashwa kwa ghadhabu za Allah swt? Je, inafaa wewe upige kelele kwa sababu ya kuungua mwili, nami nivumilie adhabu ya roho?" Baada ya ya kusema hayo, akaongeza: "Wallahi! Hata kama nitapewa dunia nzima pamoja na utajiri wake wote ili kwamba nimnyang'anye siafu ganda la shayiri alilonalo mdomoni mwake, sitafanya hivyo kamwe! Mimi ni duni na haina thamani kuliko ganda hilo hata kutaka kumuudhi siafu."

1622. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kutosamehe ni aibu mbaya kuliko zote, na kulipiza kisasi ni dhambi kubwa kuliko zote ."[306]

1623. Vile vile Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amewasifu waungwana wanasamehe makosa ya wengine, kwa kusema: "Ni murua wa watukufu kusamehe makosa kwa haraka. "[307]

1624. Mambo mazuri na mabaya hayawi kamwe sawasawa katika dunia hii. Hivyo, ni afadhali kulipa ubaya kwa amali njema kabisa ili kwamba yule aliyekufanyia ubaya na uadui awe ni rafiki yako wa karibu. Msamaha huwa na thamani kubwa sana wakati mtu anapokuwa na uwezo na nguvu za kulipiza. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . ameihesabu sifa hii tukufu kuwa ni miongoni mwa sifa njema za Mitume na wachaji: "Msamaha wakati wa (kuwepo) uwezo (wa kulipiza ubaya) ni miongoni mwa mienendo ya Mitume na wacha-Mungu. "[308]

1625. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ameutaja msamaha kama ni silaha bora kabisa ya kuwapigia wapinzani: "Mlaumu nduguyo kwa (kumfanyia) mema, na jiepushe na shari yake kwa kumfadhili ."[309]

1626. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amefichua uhakika wa ndani wa maana ya kinyongo na chuki kwa kutoa usemi mfupi: "Moyo wa mwenye kinyongo ni mgumu kuliko nyoyo zote. "[310]

1627. Wakati wa adhabu ya roho daima humtesa mwenye chuki. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kinyongo huadhibu nafsi na huzidisha adhabu yake. "[311]

1628. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: Ghuraru 'l-Hikam, uk. 490. "Dhamiri zinapotibiwa ndipo siri zinapojitokeza na kuonekana."

1629. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Chuki ni moto wa ndani ndani usiozimika ila kwa ushindi. "[312]

1630. Chuki hukoka moto wa hamaki. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Chuki huwasha hasira ."[313]

1631. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kuondoa chuki hutuliza moyo na akili yake. "[314]

1632. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mja mwenye furaha ni yule ambaye moyo wake hauna chuki wala wivu. "[315]

1633. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: "Hamaki huziba (nuru ya) moyo wa mwenye hekima. Asiyeweza kuidhibiti hamaki yake hawezi kuitawala akili yake. "[316]

1634. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye kuiacha hamaki yake ipande, huharakisha mauti yake. "[317]

1635. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadhari na hamaki, kwani mwanzo wake ni wendawazimu na mwisho wake ni majuto ."

1636. Vile vile Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Hamaki ni moto uliokokwa, mwenye kuipoza hamaki huuzima (moto wake), na mwenye kuiachilia huwa ni wa kwanza kuungua humo. "[318]

1637. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ametuusia tuwe na subira na uvumilivu ili tuweze kukabiliana na hasira na hamaki, kwa sababu tunavihitajia hivyo kuepukana na maumivu yake. "Jilindeni kutokana na ukali wa hamaki na jiandaeni kupambana nao kwa kuvunja hamaki na kwa kuvumilia. "[319]

1638. Vile vile Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kujidhibiti wakati wa kushikwa na hasira humsalimisha mtu wakati wa maangamizo. "[320]

1639. Al Imam Muhammad al-Baquir(a.s) . amesema: "Kitu gani kilicho kiovu zaidi kuliko hamaki wakati mtu aliyepandwa na hamaki hutoa roho iliyoharamishwa na Mungu.? "[321]

1640. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . ametoa mwongozo mzuri wa kufanya wakati mtu anapopandwa na hamaki: "Ikiwa mmoja wenu atapandwa na hamaki, kama amesimama akae chini, na kama amekaa alale. Na kama hamaki haikupoa baada ya kufanya hivyo, basi atawadhe kwa maji baridi au aoge-kwani moto hauzimiki ila kwa maji ." [322]

1641. Al Imam Muhammad al-Baquir(a.s) . amesema: "Allah swt hakumruhusu mtu yeyote kwenda kinyume katika mambo matatu: " Kuweka amana ya mwema au mwovu; kutimiza ahadi ya mwema au mwovu; na kuwatendea mema wazazi wema au waovu. "

1642. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . ametaja kuvunja ahadi kama ni alama mojawapo ya unafiki: "Mwenye kuwa na sifa nne (zifuatazo) ni mnafiki; na hata akiwa nayo mojawapo kati ya hizo pia atasifika kwa unafiki isipokuwa aiache: " Mwenye kusema uwongo anapozungumza; mwenye kuvunja ahadi anapoahidi; mwenye kufanya hiana anapoaminiwa; na mwenye kufisidi anapogombana. " [323]

1643. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ameandika: "Jihadhari usiwasimange raia zako kwa hisani ulizowafanyia, wala usijione bora kwa ajili ya kazi unazowafanyia, na unapowaahidi usiende kinyume na ahadi zako. Hakika masimango huharibu hisani, na kujiona huondoa nuru ya haki, na kuvunja ahadi husababisha kuchukiwa na Allah swt na watu. Allah swt anasema: katika Qur'an Tukufu, Surah Ass'af, 61, Ayah 3 'Ni chukizo kubwa mbele ya Allah swt kusema msiyoyatenda." Mustadriku 'l-Wasa'il, jz. 2, uk. 85.

1644. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Kutimiza ahadi hufuatana na uaminifu, nami sikijui kinga kinachokinga vizuri zaidi kuliko kutimiza ahadi. "[324]

1645. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mtu asimwahidi mwanae asipoweza kutimiza. " [325]

1646. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ameonyesha namna ya mtu kusuhubiana na mwenzake: "Ukimchagua mtu kuwa rafiki yako, basi kuwa mtumishi wake na mwonyeshe uaminifu wako wa kweli na moyo safi. "[326]

1647. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mwenye furaha kayaya kuliko watu wote ni yule mwenye kuingiliana na watu watukufu na ambaye huendeana na watu bila ya kuwadhulumu, huzungumza nao bila ya kuwadanganya, na huahidiana nao bila ya kuvunja. Hakika mtu kama huyu amekamilisha murua wake, amedhihirisha uadilifu wake, na anastahiki udugu na urafiki wake. "

1648. Allah swt amezitaja sheria alizowatungia waja wake kama ni amana, na amekataza kabisa kufanya khiana ya aina yoyote: katika Qur'an Tukufu, Surah Al-Anfaal, 8, Ayah 27, Enyi mlioamini! Msimfanyie khiana Allah swt na Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . na mkakhini amana zenu na hali mnajua.

1649. Vile vile Allah swt amesema: katika Qur'an Tukufu, Surah An-Nisaa, 4., Ayah 58, Hakika Allah swt anakuamrisheni kuzirudisha amana kwa wenyewe.

1650. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Ukomo cha khiana ni kumfanyia khiana rafiki mpendwa na kuvunja ahadi. "[327]

1651. Vile vile Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mtu mwovu kuliko wote ni yule asiyeamini kuweka amana wala hajizuii kufanya khiana. "[328]

1652. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Jihadharini na khiana kwani ni dhambi mbaya kabisa; na kwamba mwenye kukhini ataadhibiwa katika Moto kwa khiana yake. "[329]

1653. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . "Halahala na kusema ukweli na kurejesha amana kwa mwema au mwovu, kwani sifa mbili hizi ni ufunguo wa riziki. "[330]

1654. Al Imam Zaynul 'Abediin ibn Hussein ibn 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Halahala na kuweka amana. Naapa kwa yule aliyembaathi Muhammad kwa haki kuwa Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w), kwamba lau mwuaji wa babangu Husayn bin Ali angenipa upanga ule aliomwulia bababngu, kumwekea amana, nisingemfanyia khiana. "[331]

1655. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mwenye kutenda kitendo kiovu atalipwa (hapahapa) duniani. " [332]

1656. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Uaminifu katika (kuweka) amana ni alama ya usafi wa mwenye imani. "[333]

1657. Vile vile Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Khiana ni dalili ya upungufu wa uchaji na utovu wa dini. "[334]

1658. Al Imam Sajjad(a.s) . amesema: "Una wajibu wa kumlea (Mwanao) kwa adabu nzuri, kumwongoza kwa Mola wake Mtukufu, na kumsaidia katika kumtii. "[335]

1659. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Wenye akili huhitajia adabu kama vile shamba linavyohitajia mvua. "[336]

1660. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Hakuna jambo linalochukiwa mno katika Uislamu kama uchoyo. " [337]

1661. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Mwenye kuwa na raha kidogo kabisa kati ya watu wote ni bakhili. " [338]

1662. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Allah swt amrehemu mtu anayebana mengi (ziada) ya maneno yake, na anayetoa ziada ya mali yake. " [339]

1663. Vile vile Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Jihadhari na uchoyo, kwani uchoyo umewaangamiza waliokutangulia, umewafanya wamwage damu zao, na wahalalishe yaliyoharamishwa. " [340]

1664. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Nashangaa juu ya bakhili mwovu; huuharakisha umaskini anaokimbia na huupoteza utajiri anaotafuta. Huishi katika dunia maisha ya maskini na atahukumiwa katika Akhera kwa hesabu ya matajiri. "[341]

1665. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Ukarimu wa mtu huwafanya maadui zake wampende, na ubakhili wake humfanya achukiwe na watoto wake. "[342]

1666. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Uroho na uchoyo umesimama juu ya msingi wa shaka na kutoaminiwa. "[343]

1667. Al Imam Musa al-Kadhim(a.s) . ameelezea juu ya thamani ya ukarimu: "Karimu mwenye murua yuko katika ulinzi wa Allah swt; na Allah swt hamwachi mpaka amtie Peponi. Allah swt hamtumi Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w). wala Wasii yeyote ila kwamba huwa ni karimu; wala hakutokea mwema yeyote ila kwamba alikuwa karimu. Babangu hajafariki mpaka aliponiusia ukarimu ."[344]

1668. Al Imam Muhammad al-Baquir(a.s) . ameshabihisha maisha ya mroho na taswira hii:. "Mfano wa mwenye tamaa ya dunia ni kama kiwavi cha nondo, kila akizidi kujizungushia nyuzi (za hariri) ndivyo hujifungia mpaka kufa kwa kujisonga roho." Usulu 'l-Kafi, Babu ya Huba ya Dunia

1669. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Jihadharini na uchu wa mali, kwani uliwaangamiza waliokutangulieni. Uchu uliwashawishi mabakhili na wakafanya ubakhili; uliwaamrisha kukata ujamaa na wakakata; na uliwaamrisha ufisadi na wakafanya ufisadi. " [345]

1670. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Epukaneni na mwenye tamaa, kwani kuingiliana naye huleta udhalili na mashaka. "[346]

1671. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Mwenye tamaa ni mfungwa wa udhalili na kifungo chake hakifungiki. "[347]

1672. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . ameashiria jambo hili kwa usemi murua: "Mtukufu kuliko wote ni yula ambaye hukata tamaa (juu ya watu), hushika ukinaifu na uchaji, na huacha uroho na tamaa, kwani tamaa na uroho ni sawa na umaskini, na kukata tamaa (juu ya watu) na ukinaifu ni utajiri wa dhahiri. "[348]

1673. Anayejifanya mtumwa wa tama na uchu, huutia maradhi mwili na roho yake. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . anasema: "Kila mwenye tamaa ni mgonjwa. "[349]

1674. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema; "Tamaa huchafua nafsi, huharibu dini (imani) na huondoa uungwana. "[350]

1675. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . ametaja matatizo yanayotokana na tamaa: "Mwenye tamaa husumbuliwa na matatizo saba mabaya:

1. Fikra inayomdhuru mwili wake na isiyomnufaisha;

2. hamu (hima) isiyokwisha;

3. tamaa isiyompa raha ila baada ya kufa na wakati wa

kupumzika huona taabu zaidi;

4. hofu isiyoacha kumhangaisha;

5. huzuni inayofanya maisha yake machungu bila ya kuwa

na faida;

6. hesabu isiyomsalimisha na adhabu ya Allah swt ila

asemehewe na Allah swt; na

7. adhabu asiyoweza kuikimbia wala kuiepuka."[351]

1676. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . amesema: "Tamaa humsukuma mtu kwenye mabaya. "[352]

1677. Al Imam 'Ali ibn Abi Talib(a.s) . vile vile amesema: "Matokeo ya tamaa ni kumtia mtu katika aibu. "[353] .

1678. Mtume Muhammad Mustafa(s.a.w.w) . amesema: "Miongoni mwa (alama za) uungwana ni mtu kunyamaza kimya na kumsikiliza ndugu yake anaposema. " [354]

1679. Al Imam Muhammad al-Baquir(a.s) . amesema: "Na jifunze kusikiliza vizuri kama vile unavyojifunza kusema vizuri, wala usimkatize mtu yeyote anaposema. "

1680. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: "Mja hataipata imani halisi mpaka atakapoacha ubishi hata kama ni haki. "[355]

1681. Al Imam Had(a.s) . amesema: "Ubishi huharibu urafiki wa muda mrefu, huvunja uhusiano ulio madhubuti, na sehemu ndogo ya kitu kinachopatikana ni mashindano - na mashindano yenyewe ni chanzo hasa cha kutosikilizana. "

1682. Al Imam Ja'afer as-Sadiq(a.s) . amesema: "Epukaneni na mabishano, kwani huunguza moyo, huleta unafiki na husababisha chuki. "[356]

1683. Mtume Mtukufu(s.a.w.w) . akasema, "Hakika,miongoni mwa dalili za saa, ni kuwa 1. watu watapuuza sala

2. watafuata matamanio yao wenyewe

3. wataelekeza kujipendelea wao wenyewe, watawaheshimu matajiri,

4. na watauza Dini yao kwa manufaa ya kidunia

5. wakati huo roho na moyo wa Muumin itayayuka (kwa huzuni) kama chumvi inavyoyayuka katika maji, kwa sababu ataona mambo yaliyoharamishwa na

hataweza kuyabadili." Salman akasema: "Haya yatatokea, ewe Mtume wa Allah swt?" Mtume Mtukufu(s.a.w.w) . akasema: "Ndiyo, naapa kwa Aliyonayo roho yangu mkononi mwake."

"Ewe Salman, 6. wakati huo watawala watakuwa wadhalimu

7. Mawaziri watakuwa waasi,

8. na wadhamini (wale waliopewa amana kwa kuaminiwa) watafanya hiana,

9. hakika wakati huo maovu yatakuwa mema na mema yatakuwa maovu,

10. wale wafanyao hiana wataaminiwa na waaminifu watafikiriwa kuwa si waaminifu;na mwongo atasadikiwa,na msema kweli atahesabiwa mwongo.

11. Wakati huo kutakuwapo na utawala wa wanawake,

12. Masuria watashauriwa,

13. na watoto watakaa juu ya mimbar,

14. udanganyifu utahesabiwa kuwa ni uerevu

15. na Zaka itakuwa ni kama kutozwa faini;na mateka ya vita (yaani mali ya ummah) yatakuwa kama ni mali ya mtu binafsi;na mtu atakuwa mjeuri kwa wazazi wake na atakuwa mwema kwa marafiki zake,

16. na wakati huo kutatokea na nyota zenye mikia (comets)."

Salman akasema: "Haya yatatokea,ewe Mtume wa Allah swt?" Mtume Mtukufu(s.a.w.w) . akasema: "Ndiyo,naapa kwa Aliyonayo roho yangu mkononi mwake." "Ewe Salman!

17. wakati huo mwanamke atakuwa mshiriki wa mumewe katika biashara,

18. na mvua itakuwa moto sana

19. na watu wema watabaki katika huzuni;na masikini hawata heshimiwa;na wakati huo masoko yatakaribiana,

20. Tena huyu atasema,"Mimi sikuuza chochote,na yule atasema, "Mimi sikupata faida yoyote." Kwa hivyo hutamkuta mtu yeyote asiyemlalamikia Allah swt. "Ewe Salman!

21. tena itatokea iwapo watu watawazungumzia watawala wao, watawaua, na ikiwa watanyamaza kimya, watanyang'anywa mali yao, watanyimwa heshima zao,watamwaga damu yao na mioyo ya watu itajaa woga;kisha hutamwona mtu yeyote ila atakuwa mwoga,mwenye khofu,ametishika na ameshstushwa" "Ewe Salman!

22. Bila shaka wakati huo mambo fulani yataletwa kutoka Mashariki

23. na mambo fulani yataletwa kutoka Magharibi,

24. Basi ole kwa watu walio dhaifu (wa imani) katika Ummah wangu kutokana na hayo; Ole ya Allah swt iwe kwa hayo. Wao hawatakuwa na huruma juu ya

wadogo wao,wala hawatamsamehe yeyote aliyefanya kosa.Miili yao itakuwa ya wanadamu,lakini mioyo yao itakuwa ya mashetani." "Ewe Salman!

25. Wakati huo wanaume watawaashiki wanaume,

26. na wanawake watawaashiki wanawake;

27. na watoto wa kiume watapambwa kama wanawake;

28. na wanaume watajifanya kama wanawake

29. na wanawake wataonekana kama wanaume;

30. na wanawake watapanda mipando

31. Hapo tena patakuwepo laana ya Allah swt juu ya wanawake wa Ummah wangu."Ewe Salman!

32. Bila shaka wakati huo Misikiti itapambwa (kwa dhahabu n.k.) kama inavyofanywa katika masinagogi na makanIssa,

33. na Qur'an zitapambwa (kwa nakshi na rangi za kupendeza n.k.)

34. na minara (ya misikiti) itakuwa mirefu;na safu za watu wanaosimama katika sala zitazidi,lakini nyoyo zao zitachukiana na maneno yao

yatatofautiana." "Ewe Salman! 35. Wakati huo wanaume watatumia mapambo ya dhahabu;kisha watavaa hariri,na watatumia ngozi za chui." "Ewe Salman! 36. Wakati huo riba itakuwako,

37. na watu wata- fanyia biashara kwa kusemana na rushwa

38. na dini itawekwa chini,na dunia itanyanyuliwa juu."Ewe Salman!

39. Wakati huo talaqa zitazidi

40. na mipaka ya Allah swt hayatasimamishwa

41. Lakini hayo hayatamdhuru Allah swt."Ewe Salman!

42. Wakati huo watatokea wanawake waimbaji,

43. na ala za muziki

44. na wabaya kabisa watawatawala Ummah wangu."

"Ewe Salman!

45. Wakati huo matajiri katika Ummah wangu watakwenda Kuhiji kwa matembezi,na walio wastani kwa biashara,na masikini kwa kujionyesha.

46. Hivyo basi wakati huo watakuwapo watu ambao watajifundisha Qur'an si kwa ajili ya Allah swt na wataifanya Qur'an kama ala ya muziki.

47. Na watakuwapo watu ambao watasoma dini si kwa ajili ya Allah swt

48. na idadi ya wanaharamu itazidi

49. watu wataiimba Qur'an,

50. na watu watavamiana kwa uroho wa kidunia."

"Ewe Salman!

51. Haya yatatokea wakati heshima zitakapo- ondoka,na madhambi yatatendwa

52. na watu waovu watakuwa na uwezo juu ya watu wema,

53. na uongo utaenea na mabishano (matusi) yatatokea

54. na umasikini utaenea,

55. na watu watajiona kwa mavazi yao

56. na itakuwepo mvua wakati si wake

57. na watu watacheza dama, kamari na Ala za muziki,

58. na hawatapenda kuhimizana mema wala kukatazana maovu

59. na kwa ajili hali itakavyokuwa hata itafikia wakati huo kuwa Muumin atakuwa na heshima ndogo kuliko hata mjakazi

60. na wanaosoma na wanaotumia wakati wao katika kumwabudu Allah swt watalaumiana.

61. Hao ndio watu watakaoitwa wachafu na wanajisi katika Ufalme wa mbinguni."

"Ewe Salman!

62. Wakati huo matajiri hawataogopa chochote isipokuwa mtu masikini; hadi kwamba masikini wataendelea kuomba kati ya ijumaa mbili,na hawatamwona mtu yeyote wa kutia chochote mikononi mwao."

"Ewe Salman!

63. Wakati huo itazungumzwa Ruwaibidhah."

Salman akauliza:"Ni nini Ruwaibidhah ? Ewe Mtume wa Allah swt, baba na mama yangu wawe fidia kwako."

Mtukufu Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w). akajibu:

64. "Watu fulani watazungumza kuhusu mambo ya watu ambayo hayakuwahi kuzungumzwa namna hii zamani.

65. Tena baada ya muda mchache machafuko yatatokea duniani,na kila nchi itafikiri kuwa machafuko yapo katika nchi yao tu."

66. "Watabaki katika hali hiyo kwa muda ambao Allah swt atapenda wabaki;

67. kisha ardhi itatapika vipande vya moyo wake dhahabu, fedha na madini mengineyo; (Hapo Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w).) alinyosha kidole chake

penye nguzo, na akasema: "Kama hizi (kwa ukubwa), lakini siku hiyo dhahabu wala fedha hazitamsaidia mtu yeyote. Na hii ndiyo maana ya maneno ya Allah swt 'Hakika dalili Zake zimekuja.'