WAULIZE WANAOFAHAMU

WAULIZE WANAOFAHAMU0%

WAULIZE WANAOFAHAMU Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Misingi mikuu ya Dini

WAULIZE WANAOFAHAMU

Mwandishi: Muhammad Tijani As-samawi At-Tunisi
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi:

Matembeleo: 51036
Pakua: 5055

Maelezo zaidi:

WAULIZE WANAOFAHAMU
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 26 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 51036 / Pakua: 5055
Kiwango Kiwango Kiwango
WAULIZE WANAOFAHAMU

WAULIZE WANAOFAHAMU

Mwandishi:
Swahili

18

WAULIZE WANAOFAHAMU

TISHIO LA KUCHOMA MOTO NYUMBA YA BIBI FATIMA

Swali la 19

Ni kwa nini walitishia kuichoma moto nyumba ya bibi Fatimah?

Jawabu : Idadi kubwa ya Masahaba ambao hawakumpa baia Abubakr walibakia ndani ya nyumba ya Ali ibn Abi Talib, na lau Umar asingefanya haraka kuizunguka nyumba hiyo na kutishia kuichoma moto, basi jambo hilo lingepata nguvu na umma ungegawika makundi mawili moja la Ali na lingine la Abubakar. Lakini Umar kwa ajili ya kupasisha jambo lililokwisha tokea alitazama mtazamo wa mbali pale aliposema, "Lazima mtatoka kwenda kutoa baia la sivyo nitaichoma moto nyumba hii na waliomo, akikusudia Ali na Fatmah binti ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ." Na kwa kauli hii basi hakuweza kubakia katika watu yeyote ambaye nafsi yake inamtuma kuuvunja utiifu na akose kuingia katika baia. Basi je, ni utukufu gani mkubwa (uliokuwepo zama hizo) kuliko utukufu wa mwanamke bora ulimwenguni (Fatmah) na mumewe ambaye ni Bwana wa mawasii?

Swali la 20

Ni kwa nini Abu Sufiyan alinyamaza (asiseme kitu) pale Umar alipowatishia na kuwaonya?

Jawabu : Wakati Abu Sufiyan aliporejea Madina baada ya Mtume(s.a.w.w) kufariki, kwani Mtume alikuwa amempeleka Abu Sufiyan kwenda kukusanya zaka alishitukizwa na Ukhalifa wa Abubakr, na haraka alikwenda nyumbani kwa Ali ibn Abi Talib akamchochea afanye mapinduzi na awapige vita jamaa hao hali ya kuwa akimuahidi (kumsaidia) mali na watu. Lakini Ali(a.s) alimfukuza kwa kutambua nia yake, naye Abubakr na Umar walipofahamu jambo hilo walimwendea Abu Sufiyan wakamlainisha na kumuahidi kumpa kila kitu alichokikusanya katika sadaka hizo na kumshirikisha katika Ukhalifa kwa kumchagua mwanawe kuwa Gavana wa Sham. Basi Abu Sufiyan aliridhika na hayo na akawanyamazia, ndipo wakamchagua Yazid ibn Abi Sufiyan kuwa Gavana wa Sham, na alipokufa wakamteua nduguye Muawiyah ibn Abi Sufiyan achukue mahali pake na wakamuwezesha huyu Muawiyah kuufikia Ukhalifa.

Swali la 21

Je, Imam Ali aliridhia jambo hilo na akawapa baia jamaa hao?

Jawabu : Hapana kamwe Imam Ali hakuridhia jambo hilo na hakunyamaza bali alitoa hoja dhidi yao kwa kila kitu na hakukubali kuwapa baia licha ya vitisho vyao na maonyo. Ibn Qutaibah ameeleza ndani ya kitabu chake cha historia kwamba Imam Ali aliwaambia: "Wallahi sikupeni baia, ninyi ndio wenye haki kunipa baia mimi." Bali alimchukua mkewe bibi Fatmah akapita naye kwenye vikao vya Maansari, nao wakawa wanatoa sababu (kwa kusema) kwamba Abubakar amewawahi. Bukhari ameeleza kuwa Imam Ali hakutoa baia muda wote wa uhai wa bibi Fatimah, alipofariki bibi Fatmah na watu wakampuuza Imam Ali alilazimika kufanya sulhu na Abubakr, na Bibi Fatimah aliishi kwa muda wa miezi sita baada ya kifo cha Baba yake, Sasa je, bibi Fatmah alifariki akiwa hana baia wakati ambapo baba yake ambaye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: "Yeyote atakayekufa na hali ya kuwa hana baia basi atakufa mauti ya kijahiliya."

Na Je, Ali alikuwa anafahamu kwamba yeye ataishi mpaka baada ya Abubakr, basi akachelewa kumbai kwa muda huo wa miezi sita? Ifahamike kwamba, Ali hakunyamaza muda wote wa uhai wake, kwani kila alipopata fursa hukumbusha dhulma aliyofanyiwa na kuporwa haki yake, na hiyo inatosha kuwa ni dalili ya yale aliyoyasema kwenye hotuba yake inayojulikana kama hotuba ya Shaqshaqiyyah.

Swali la 22

Ni kwa nini walimchukiza na kumkasirisha bibi Fatmah wakati haja yao ilikuwa ni kuleta sulhu?

Jawabu : Bila shaka walikusudia kumchukiza bibi Fatmah kwa kumnyang'anya ardhi yake na milki zake na wakamnyima mirathi ya baba yake na wakayakanusha madai yake yote kiasi cha kumuondolea heshima yake na utukufu wake miongoni mwa watu kiasi wasimuamini endapo atachokoza kwa kuleta madai kuthibitisha matamko yanayohusu Ukhalifa. Na ndio maana Maansari walimtolea udhuru kwamba baia yao ameiwahi Abubakr, na lau mumewe (Ali) angewahi wasingempinga. Kwa ajili hiyo bibi Fatmah alimkasirikia mno Abubakr na Umar mpaka akawa huwaapiza katika kila sala anayoisali, na alimuusia mumewe kwamba asihudhurie jeneza lake yeyote miongoni mwao na amuepushe kabisa na watawala hao ambao yeye bibi Fatmah anawachukia. Na kwa hakika walikusudia kumuudhi ili wamuonyeshe Ali kuwa yeye ni dhaifu juu yao kuliko binti ya Mtume ambaye ndiye mwanamke bora ulimwenguni na ambaye Mwenyezi Mungu hukasirika kutokana na kukasirika kwake na huridhia kutokana na kuridhia kwake (Fatmah), kwa hiyo (Ali) hakuwa na la kufanya isipokuwa kunyamaza.

Swali la 23

Ni kwa nini wakuu wa Kiquraish waligomea jeshi la Usamah?

Jawabu : Pindi mambo yalipokuwa yamemkalia vizuri Abubakr na akawa ndiye Khalifa wa Waislamu kutokana na juhudi za Umar licha ya kutoridhika kwa wapinzani, Abubakr alimtaka Usamah asimchukue Umar ibn Khatab ili abakie akimsaidia kwenye mambo ya utawala, kwani yeye peke yake hawezi kuyakamilisha na hapana budi awe na watendaji ambao ni wenye nguvu na ususuavu ambao walimpinga Mtume(s.a.w.w) na wala hawakujali ghadhabu za Mwenyezi Mungu wala laana ya Mtume(s.a.w.w) kwa yule atakayegomea jeshi la Usamah miongoni mwa wale aliowateua yeye mwenyewe Mtume. Hapana shaka kwamba waliopanga kufanikisha suala hili (la Ukhalifa) ndiyo waliogomea jeshi la Usamah ili wapate kufanikisha jambo lao na kusaidiana kuimarisha misingi yao.

Swali la 24

Je, ni kwa nini Imam Ali(a.s) alitengwa katika kila jambo na wala hawakumshirikisha kwa lolote lile?

Jawabu : Halihalisini kwamba jamaa hao waliwakumbatia watu wengi miongoni mwa wale walioachwa huru (siku ya Fat-hi Makkah) na wakawapa vyeo ndani ya serikali yao kwa kuwashirikisha kwenye Ukhalifa na wakawateua miongoni mwao wawe maamiri na watawala katika bara Arabu yote na katika kila miji ya Kiislamu. Miongoni mwa hao walioteuliwa ni Al-walid ibn Uqbah, Marwan ibn Al-hakam, Muawiyah na Yazid watoto wa Abu Sufiyan, Amri ibn Al-a's, Mughirah ibn Shu'ubah, Abu-hurairah na wengi wengineo ambao walikuwa wakimkera Mtume wa Mwenyezi Mungu. Lakini Ali walimtenga na kumpuuza wakamuacha kajifungia nyumbani kwake, wala hawakumshirikisha kwa lolote katika utawala wao kwa muda wote wa robo karne ili wamdhoofishe na kumdharaulisha na wawafanye watu wasimthamini, kwani watu ni watumwa wa dunia wanamfuata aliye na (nguvu za) utawala na cheo na mali. Na maadam Ali alikuwa hapati chakula chake cha siku moja isipokuwa kwa pato litokanalo na mkono wake na jasho lake, basi kwa vyovyote vile watu watamkimbia na wala hawatamfuata. Na ndivyo ilivyokuwa, hakika Ali alibakia katika hali hiyo kwa muda wote wa Ukhalifa wa Abubakr, Umar na Uthman akiwa ndani, na wote hawa wakifanya kila namna kumdhalilisha na kuizima nuru yake na kuzificha fadhila zake na cheo chake. hali ya kuwa Imam Ali hana chochote cha kidunia kitakacho wafanya watu wampende.

Swali la 25

Ni kwa nini waliwapiga vita waliozuwia zaka pamoja na kuwa Mtume alikataza jambo hilo?

Jawabu : Hiyo ni kwa sababu baadhi ya Masahaba walihudhuria baia ya (kula kiapo cha utii kwa) Imam Ali huko Ghadir Khum wakati walipokuwa wakirudi kutoka kwenye Hija ya kuaga hali ya kuwa wamefuatana na Mtume(s.a.w.w) Kwa ajili hiyo walijizuwia kutoa zaka hiyo kwa Abubakr kwa sababu wao hawakuwepo katika kifo cha Mtume wala hawakuwepo kwenye matukio yaliyofuatia kifo cha Mtume hasa juu ya kubadilika Ukhalifa kutoka kwa Ali kwenda kwa Abubakr. Hali hii ilisababishwa na wengi wao kutokuwa wakazi wa Madina, na hapana shaka kuwa baadhi ya habari ziliwafikia ya kwamba bibi Fatmah(a.s) amekosana nao na amewakasirikia, na pia kwamba Ali(a.s) amekataa kuwapa baia, na kwa yote hayo basi walikataa kutoa zaka kwa Abubakr mpaka mambo yawabainikie.

Hapo ndipo Abubakr na Umar na watumishi wa utawala wao walipoafikiana wawapelekee jeshi chini ya uongozi wa Khalid ibn Walid ambaye alikuwa ndiyo upanga wao, akaenda akazima upinzani wao na kunyamazisha fikra zao. Si hivyo tu bali aliwaua wanaume zao na kuwateka wanawake zao na watoto wao ili iwe ni onyo kwa yeyote ambaye nafsi yake itamshawishi kutotii au kuitia dosari heshima ya dola.

Swali la 26

Ni kwa nini walizuwia hadithi za Mtume zisiandikwe?

Jawabu : Tangu siku za mwanzo walifanya kila njia kuzuwia hadithi za Mtume, siyo tu kwa sababu hadithi hizo zinahusiana na suala la Ukhalifa na ubora wa Imam Ali, bali ni kwa kuwa nyingi katika hadithi hizo zinapingana na maneno yao na vitendo vyao ambavyo walikuwa wakivitumia kuendeshea mambo ya maisha na kuimarisha utambulisho wa dola mpya waliyoizusha juu ya misingi yake kwa mujibu wa ij-tihadi zao.

Swali la 27

Je, Abubakr alikuwa anaweza kumudu jukumu la Ukhalifa?

Jawabu : Abubakr hakuwa na uwezo wa kumudu uzito wa Ukhalifa, na lau Umar ibn Khatab na baadhi ya wenye hila miongoni mwa wakuu wa Kibanu Umayyah mambo yangemshinda. Historia imeandika kwamba, Abubakar siku zote alikuwa akitii maamuzi na maoni ya Umar ibn Khatab aliyekuwa mtawala mtendaji. Dalili ya hilo ni kile kisa cha wale wanaoimarishwa nyoyo zao katika dini ambao walimjia Abubakr mwanzoni mwa Ukhalifa wake, akawaandikia barua na akawatuma waende kwa Umar ambaye mambo yanayohusu mali yalikuwa mkononi mwake. Basi Umar aliichana barua ile na akawafukuza, wakarudi kwa Abubakr wakamuuliza; "Hivi wewe ndiye Khalifa au yeye?" Akawajibu: "Ni yeye kwa mapenzi ya Mungu."

Kadhalika wakati Abubakr alipoigawa sehemu ya ardhi kumgawia Uyaynah ibn Hisn na Aqra'a ibn Habis, basi Umar akakataa alipoisoma barua ya Abubakr na akaitemea mate akaifuta. Watu wale wakarudi kwa Abubakr hali ya kuwa wanalalamika kutokana na aliyoyafanya Umar na wakamwambia: "Wallahi hatufahamu hivi wewe ndiye Khalifa au Umar." Akasema; "Bila shaka yeye ndiyo Khalifa." Umar alipofika hapo hali ya kuwa amekasirika na kumuhoji Abubakr kwa maneno makali juu ya kutoa kwake ardhi hiyo, Abubakr alimwambia Umar, "Hivi sikukuambia kwamba wewe una nguvu kuliko mimi juu ya jambo hili la Ukhalifa.? Hakika wewe umenizidi nguvu."

Bukhari ameandika ndani ya sahihi yake kwamba, Umar alikuwa akiwahimiza watu wambai Abubakr na husema: "Bila shaka Abubakr ndiye Mwenzi wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na wa pili katika wawili (pangoni) na kwamba yeye ni mbora wa Waislamu kwa mambo yenu, basi simameni mumbai." Anas bin Malik anasema: "Nilimsikia Umar anamwambia Abubakr siku hizo, panda juu ya mimbari, hakuacha kumtaka apande mpaka akapanda juu ya mimbari na watu wote wakambai."

Swali la 28

Kwa nini Abubakr aliusia Ukhalifa kwa Umar kabla ya kufa kwake?

Jawabu : Hiyo ni kwa kuwa Umar ndiye aliyefanikisha kumtupa mbali Ali kutoka kwenye Ukhalifa, na ni kutokana na (yeye Umar) kuwa mpinzani mbaya wa Mtume(s.a.w.w) hapo mwanzo pia kwa namna alivyowaburuta Maansari wambai Abubakr na kuwalazimisha watu kwa nguvu kutoa baia mpaka mambo yakafikia kutishia kuchoma moto nyumba ya bibi Fatmah. Pia ni kwa kuwa yeye alikuwa ndiye Khalifa mtendaji kama tulivyotangulia kusema, yeye ndiye aliyekuwa na kauli ya mwanzo na ya mwisho, na hapana shaka kwamba yeye alikuwa miongoni mwa Waarabu wenye mtazamo wa mbali, kwa hiyo alifahamu kwamba Waislamu na hasa Maansari hawatakubali kumpa baia kutokana na tabia yake ya ukali na ususuavu na hasira zake za haraka haraka. Kwa sababu hizo basi akamtangulizi Abubakr kwa kuwa tabia yake ilikuwa ya upole na huruma naye amewatangulia kusilimu. Isitoshe Aisha bint yake Abubakr alikuwa ni mwanamke shupavu anayeweza kuyakabili mambo mazito na kubadilisha mambo, katika hali hiyo Umar alikuwa akitambua vyema kwamba Abubakr ni mfuasi wake na atatii maelekezo yake kwa kila atakalolipendekeza kwake.

Jambo hili halikuwa siri kwa Masahaba wengi juu ya yeye Abubakr kuusia Ukhalifa kwa Umar kutokana na maandiko yake, bila shaka Imam Ali alikwisha mwambia Umar tangu ile siku ya kwanza kuwa: "Leo hii mwandalie sehemu yake na umuimarishie, naye kesho atakurudishia." Kama alivyosema Sahaba mwingine kumwambia Umar wakati alipotoka na yale maandiko yaliyokuwa na usia wa Abubakr,(kisha Umar akajifanya kuwa hajui kilichomo, sahaba yule) akamwambia Umar, "Mimi nafahamu kilichomo, bila shaka wewe ulimtawalisha kipindi hicho cha kwanza naye amekutawalisha mwaka huu." Hivyo basi usia wa Abubakar kwa Umar ni jambo linaloeleweka kwa watu wote, na ikiwa Abubakr katika zama za uhai wake anakiri mbele ya watu wote kwamba Umar ana nguvu kuliko yeye, basi siyo ajabu kumpa utawala wakati wa kufa kwake.

Na kwa ajili hii inatubainikia kwa mara nyingine kwamba, yale wayasemayo Masunni kuwa Ukhalifa hauwezi kukubalika isipokuwa kwa njia ya mashauriano ni jambo ambalo halipo na wala halimo kabisa ndani ya mawazo ya Abubakr na Umar. Na ikiwa Mtume(s.a.w.w) alifariki na akaliacha jambo hili liwe katika mashauriano kati ya watu kama wanavyodai Masunni, basi bila shaka Abubakr alikuwa ni mtu wa mwanzo kubomoa msingi huu aliipinga Sunna ya Mtume(s.a.w.w) kwa kumuusia Umar baada yake.

Siku zote utawaona Masunni wanajinadi kwa fahari kubwa kwamba wao wanaamini mashauriano, na eti Ukhalifa haukubaliki isipokuwa kwa njia hiyo, na hukejeli kauli ya Mashia ambao wanaamini kuwa Ukhalifa haukubaliki isipokuwa utokane na maagizo yanayotoka kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake(s.a.w.w) .

Masunni wengi utawasikia wanaikosoa itikadi hii na kwamba ni kitu kilichoingizwa ndani ya Uislamu kutoka kwa Waajemi/Wairani ambao wanasema kuwa uongozi wa mambo ya Mwenyezi Mungu ni suala la urithi (wa kizazi maalum). Ni mara nyingi Masunni wanatolea ushahidi aya isemayo: "Na mambo yao ni kwa mashauriano kati yao." Na wanadai kwamba aya hiyo ilishuka kuhusu Ukhalifa na kwa dalili hii sisi tunayo haki ya kusema kwamba Abubakr na Umar walikwenda kinyume na kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume na hawakuvithamini vitu hivyo viwili kuhusu suala la Ukhalifa.

Swali la 29

Ni kwa nini Abdur-rahman ibn Auf alimuwekea sharti Imam Ali ibn Abi Talib kuwa ni lazima aongoze kwa mujibu wa Sunna ya Makhalifa hao wawili?

Jawabu : Miongoni mwa udhalili wa dunia mbele ya Mwenyezi Mungu, ni Abdur-Rahman ibn Auf kuwa mtu atakayeamua mustakabali wa umma wa Kiislam baada ya Umar, auchagulie umma mtu amtakaye yeye na amuondoshe asiyemtaka. Kamwe hilo haliwezekani, lakini yote hayo ilikuwa ni mipango ya Umar ambaye aliupatia kura ya turufu mkono wa Abdur-Rahman juu ya Masahaba wengine, na huyu Abdurrahman ibn A'uf yeye ni miongoni mwa Waarabu wenye vitimbi. Hapana shaka kwamba yeye ni miongoni mwa wajumbe wa kundi lililopanga mipango inayohusu Ukhalifa na namna ya kuuondosha kwa muhusika wake wa kisheria. Kwa kuwa Bukhari anakiri kwamba Abdur-rahman ibn Auf alikuwa akichelea jambo fulani kwa Ali, basi moja kwa moja naye alifanya kila njia kumtenga Imam Ali mbali na Ukhalifa kwa namna yoyote atakayoiweza. Huyu Abdur-rahman ibn Auf anafahamu kama walivyokuwa wakifahamu Masahaba wengine kwamba Ali(a.s) alikuwa hakubaliani na ij-tihadi za Abubakr na Umar na yale waliyoyabadilisha miongoni mwa hukumu za kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtume(s.a.w.w) , na alikuwa akijaribu kwa uwezo wake kuwapinga na kuwakemea.

Kwa sababu hiyo basi, Abdur-rahman akamuwekea sharti Imam Ali kwamba aongoze kwa mujibu wa Sunna ya Abubakr na Umar hali ya kuwa anajua tangu mwanzo kuliko mtu mwingine kwamba Ali hajipendekezi wala hasemi uongo na wala sharti hilo kamwe hatalikubali, ni kama ambavyo pia Abdur-rahman alikuwa anajua ya kwamba Uthrnan ibn Affan ambaye mkwewe, Maquraishi na wajumbe wote wa mipango hiyo watamfurahikia akichukua Ukhalifa.

Swali la 30

Je, hadithi ya Maimamu kumi na wawili inapatikana kwa Msunni?

Jawabu : Bukhari na Muslim wameithibitisha hadithi hiyo pia wanachuoni wote wa hadithi wa Kisunni wameithibitisha hadithi ya Mtume(s.a.w.w) isemayo "Dini haitaacha kusimama hadi siku ya Qiyama mpaka wawepo Makhalifa kumi na wawili na wote ni Maquraishi. Na hadithi hii imebakia kuwa ni mushkeli mkubwa ambao hauna jibu kwa Masunni, hapana yeyote miongoni mwa wanazuoni wao aliyethubutu kuwahesabu (Makhalifa hao) baada ya wale Khulafau-rashidina wanne, na watano ni Umar ibn Abdil-aziz, sasa wanabakia katika idadi hiyo (Makhalifa) saba ambao hawapo.

Masunni hawana njia vinginevyo nao waukubali Uimamu wa Ali na wanawe, Uimamu ambao Mashia wanaukubali na kwa kufanya hivyo wawe ni wafuasi wa watu wa nyumba ya Mtume, na au waipinge hadithi hii, jambo ambalo litavifanya vitabu vyao viwe tupu havina ukweli wowote isipokuwa uzushi mtupu. Zaidi ya hapo ni kwamba hadithi hii ambayo inahusisha Ukhalifa kwa Maquraish peke yao inapingana na ule msingi wa mashauriano ambao Masunni wanautetea, kwani uchaguzi na demokrasi inamkusanya kila mtu katika umma, na wala hailihusishi kabila maalum na kuyaacha makabila mengine bali inavuka kwenye makabila ya Kiarabu mpaka inafika kwenye makabila mengine miongoni mwa makabila ya Kiislamu yasiyokuwa ya Kiarabu.

Haya ndiyo majibu ya haraka kwa ufupi ili tumbainishie msomaji baadhi ya mas-ala ambayo huenda yakaichanganya akili yake, na hii ni kwa kuwa huenda akapata majibu kwa ufafanuzi ndani ya vitabu vya historia na vile vile ndani ya vitabu vyangu Thummah-tadaitu na Liakuuna Ma 'as-sadiqin. Basi ni juu ya mwenye kutafiti kuangalia rejea zinazo tegemewa, na ajitahidi kupata ukweli, azichambue riwaya na matukio ya kihistoria na kwa kupitia uchambuzi huo imbainikie haki ambayo imevishwa vazi la batili, alivue na aiangalie haki katika vazi lake la asili.

19

WAULIZE WANAOFAHAMU

MLANGO WA SABA

YANAYOHUSU HADITHI TUKUFU ZA MTUME (s.a.w.w)

Nitambainishia msomaji kwamba, tatizo la hadithi ni miongoni mwa matatizo ambayo leo hii Waislamu wanakabiliana nayo na hasa katika zama zetu hizi, kwani kuna wasomi waliohitimu kutoka vyuo vikuu vya Kiwahabi ambao wamesomea fani ya hadithi. Wasomi hao utawaona wamehifadhi hadithi ambazo zinakubaliana na madhehebu yao na itikadi zao za Kiwahabi, na sehemu kubwa ya hadithi ni zile zilizowekwa na watawala wa Kibanu Umayyah ambao lengo lao pia lilikuwa ni kuizima nuru ya Utume, na kwa kupitia hadithi hizo wamfanye Mtume(s.a.w.w) kuwa ni mtu aliyechanganyikiwa hafahamu anachokisema wala haelewi kuwa hadithi zake na matendo yake yanapingana na huwachekesha hata wenda wazimu.

Pamoja na kuwa wahakiki na wanachuoni wa Kisunni wamesimamia kuzichambua hadithi hizo, lakini kwa bahati mbaya sana bado kuna hadithi nyingi (zilizowekwa) ndani ya vitabu vya Kisunni vinavyotegemewa, pia vitabu vya Kishia navyo havikusalimika na uharibifu na uzushi huu. Lakini Mashia wanakiri kwamba wao hawana kitabu sahihi isipokuwa Kitabu cha Mwenyezi Mungu na kisichokuwa hicho basi ndani yake kuna uharibifu. Ama Masunni wao wanakubaliana kwamba sahihi mbili ya Bukhari na ile ya Muslim ni vitabu sahihi mno baada ya Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Si hivyo tu, bali wanasema kuwa kila kilichomo humo ni sahihi, na kwa ajili hiyo nitajaribu kumuwekea msomaji baadhi ya mifano katika hadithi ambazo Bukhari na Muslim wameziandika na ni hadithi ambazo yamo mambo yanayoporomosha utukufu wa Mtume Mtukufu(s.a.w.w) au utukufu wa watu wa nyumba ya Mtume(s.a.w.w) .

Nitajaribu pia katika mlango huu kuonesha baadhi ya hadithi ambazo ziliwekwa ili kuyatakasa matendo ya watawala wa Kibanu Umayyah na wale wa Kibanu Abbas, na kwa kweli kupitia hadithi hizo walikuwa wamekusudia kuitia dosari Ismah ya Mtume(s.a.w.w) ili tu wayahalalishe makosa yao na mauaji waliyoyafanya dhidi ya watu wasiokuwa na hatia. Hebu fuatilia maelezo yafuatayo: Eti, Mtume(s.a.w.w) ananyemelea Bukhari ameandika ndani ya sahihi yake, Kitabul-Istiidhan na katika Kitabud Diyat, mlango wa yeyote atakayechungulia ndani ya nyumba ya watu na wakamtoboa jicho lake hana fidia.

Muslim naye ndani ya sahihi yake, Kitabul-aadaab, mlango unaokataza kuangalia ndani ya nyumba ya wengine.

Imepokewa kutoka kwa Anas ibn Malik, "Kwamba mtu fulani alichungulia katika baadhi ya vyumba vya Mtume(s.a.w.w) , basi Mtume(s.a.w.w) akasimama akiwa na mshale au mishale, kama kwamba namuona Mtume anamnyemelea ili amchome." Bila shaka kwa mujibu wa mafunzo matukufu, hayakubaliani kuwa Mtume wa rehma ambaye ni mpole na mwenye huruma kwa waumini eti anaweza kufanya hivyo, kinachotakiwa kwa Mtume(s.a.w.w) ni kusimama na kumfunza adabu ya Kiislamu mtu yule aliyechungulia chumba cha Mtume na kumfahamisha kuwa kitendo alichokitenda ni haramu. Haiwi sawa kwa Mtume achukue mshale na kumvizia kumchoma na kumpofua jicho lake, sababu mtu yule anaweza kuwa alitenda hilo kwa nia njema, kwani chumba hicho hakikuwa miongoni mwa vyumba vya wakeze Mtume(s.a.w.w) , na dalili ya hilo ni kuwa Anas ibn Malik alikuwemo humo. Basi ni tuhuma gani hii aliyoielekeza kwa Mtume(s.a.w.w) na akaiona kuwa ni ya ususuavu ambayo (eti Mtume) anamnyemelea mtu kumpofua jicho? Tosheka kwamba mshereheshaji wa sahih Bukhari aliikosoa hadithi hii kama ifuatavyo: Kumvizia kwa maana ya kumjia hali ya kuwa hamuoni, hivi ndivyo walivyoifasiri hadithi hii. Na tendo hili halipatikani kwa Mtume(s.a.w.w) hawezi kufanya hivyo. Mtume anaadhibu adhabu kali na kuwatesa Waislamu.

Bukhari ameandika ndani ya sahih yake, katika Kitabut-tibb juzuu ya saba uk. 13, mlango wa kuyafanya dawa maziwa ya ngamia, na katika mlango wa kufanya dawa kwa mkojo wa ngamia amesema: Ametusimulia Thabit kutoka kwa Anas kwamba kuna watu walikuwa na ugonjwa fulani wakasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu tupokee na utupe chakula." Mtume akawaamuru waende kwa mchungaji wake wa ngamia, ili wakanywe maziwa ya ngamia na mkojo wake, wale jamaa wakaenda na wakanywa maziwa ya ngamia na mkojo wake. Basi miili yao ilipotengenea walimuua yule mchungaji na wakawaswaga wale ngamia, habari hizo zikamfikia Mtume(s.a.w.w) , akatuma watu wawatafute jamaa hao. Walipopatikana wakaletwa, Mtume akawakata mikono yao na miguu yao na akawapiga misumari ya moto machoni mwao, basi nilimuona mtu miongoni mwao anaiuma ardhi kwa ulimi wake mpaka anakufa."

Hivi kuna Mwislamu yeyote anayeweza kuamini kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ambaye anakataza kuadhibu kwa aina hiyo, kisha yeye mwenyewe anawaadhibu jamaa hawa kwa kuwakata mikono yao na miguu yao na kuwapigilia misumari ya moto machoni mwao kwa kuwa wao wamemuua mchungaji wake? Na lau mpokezi wa riwaya hii angesema kuwa jamaa hawa walimuadhibu vikali yule mchungaji (kabla ya kumuuwa), basi Mtume angekuwa na nafasi ya kuwaadhibu vivyo hivyo, lakini haikuja hivyo, Sasa itakuwaje Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) awaadhibu vikali namna ile bila hata ya kufanya uchunguzi wala kuwapa nafasi ya kujitetea ili abainike ni nani aliyeua miongoni mwao naye auawe? Labda baadhi ya watu watasema kuwa, wote walishiriki kumuua mchungaji yule, basi je, haikuwa sawa kwa Mtume kuwasamehe na kuwaachilia? Kwani wao walikuwa Waislamu kwa dalili ya wao waliposema "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu," hivi tuseme Mtume wa Mwenyezi Mungu hakuisikia kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

وَإِنْ عَاقَبْتُمْ فَعَاقِبُوا بِمِثْلِ مَا عُوقِبْتُم بِهِ وَلَئِن صَبَرْتُمْ لَهُوَ خَيْرٌ لِّلصَّابِرِينَ ﴿١٢٦﴾

"Na mkiteswa basi nanyi lipizeni kwa kiwango kilekile mlichoteswa, na mkivumilia hiyo ni kheri kwa wenye kuvumilia." (Quran, 16:126).

Na iwapo aya hii ilishuka kwa Mtume(s.a.w.w) wakati moyo wake ulipomuuma kutokana na kuuawa kwa ammi yake Hamzah ibn Abdil-muttalib bwana wa mashahidi ambaye makafiri walimpasua tumbo lake na wakala maini yake kisha wakamkata sehemu za siri. Mtume alikasirika sana alipomuona ammi yake akiwa katika hali hiyo na akasema, "Mwenyezi Mungu akiniwezesha nitalipiza kwa watu wapatao sabini." Hapo ndipo iliposhuka aya hii Mtume(s.a.w.w) akasema: "Ewe Mola wangu nimekwishavumilia." Mtume akamsamehe muuaji aliyemuua ammi yake kwa kuwa kusamehe ndiyo tabia ya Mtume(s.a.w.w) . Hindu (mke wa Abu Sufiyan) ndiye aliyekitesa kiwiliwili kitukufu cha ammi ya Mtume na kula maini yake.

Na miongoni mwa yatakayokujulisha ubovu wa riwaya hii ni kwamba, mpokeaji mwenyewe ameikosoa alipoimalizia kwa kusema: "Qatadah amesema, amenisimulia Muhammad ibn Sayarin kwamba, tukio hilo lilitokea kabla ya kushuka hukumu za adhabu." Kwa hakika haiwezekani kwa Mtume kujiamulia mwenyewe kabla Mola wake hajambainishia, na ikiwa Mtume katika mas-ala madogo haamui mpaka Wahyi umshukie basi hebu fikiria kwa mambo yanayohusu kumwagika damu na hukumu za adhabu? Bila shaka ni rahisi sana kwa yeyote mwenye kuzingatia na kufahamu kwamba riwaya hiyo ni miongoni mwa riwaya za uzushi zitokanazo na Banu Umayyah na wafuasi wao, ili tu kwa kupitia riwaya hizo wawaridhishe watawala wao ambao hawaoni vibaya kuwauwa watu wasio na makosa kwa kuwadhania na kuwatuhumu peke yake, kisha huwatesa mateso makali, na dalili ya hilo ni maelezo yaliyoko mwishoni mwa -riwaya hiyo aliyoiandika Bukhari anasema: Salaam amesema "ilinifikia khabari kwamba Hajjaaj alimwambia Anasi , Hebu niambie adhabu kali aliyopata kuadhibu Mtume(s.a.w.w) ." Anas akaisimulia hadithi hii, habari zikamfikia Hasan naye akasema, "'Natamani asingemsimulia habari hizi."

Ndani ya riwaya hii umo uzushi ili kumridhisha Hajjaj At-thaqafi ambaye alieneza uovu katika nchi na akaua maelfu ya Mashia (wafuasi) wa watu wa nyumba ya Mtume(s.a.w.w) wasiokuwa na hatia na aliwaadhibu vikali, kwani alikuwa akiwakata mikono na miguu na kuwatia machoni misumari ya moto na kuzitoa ndimi zao kutokea kwenye koromeo na akiwasulubu mpaka jua linawaunguza. Na riwaya kama hii inayatakasa matendo yake kwani yeye ataonekana kuwa anafuata mwendo wa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa kutumia kigezo cha kali ya Mwenyezi Mungu isemayo, "Mnacho kiigizo chema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu."- La haula wala quwwata illa billah. Na kwa ajili hiyo ndiyo maana Muawiyyah alikuwa na namna nyingi za kuwaadhibu na kuwatesa Waislamu waliokuwa wakimfuata Ali, kwani ni mara ngapi aliwachoma moto na akawazika wakiwa hai na kuwasulubu kwenye mashina ya mitende? Na miongoni mwa namna (za kuadhibu) alizozizusha waziri wa Muawiyah aitwaye Amru ibn Al-a's ni kuwa, yeye alimuadhibu vikali Muhammad ibn Abubakr kisha akamfunga ndani ya ngozi ya punda na kumtupa motoni. Na katika kuutetea wenda wazimu wao na kupenda kwao wanawake na wajakazi hebu soma yafuatayo:

(Eti) Mtume anapenda mno jimai. Bukhari ameandika ndani ya sahih yake katika Kitabul-ghusli, Babu idhaa Jaama 'a thumma A 'ada Waman Daara A 'la nisaaihi fighuslin-wahidin. Amesema:"Muadh ibn Hisham ametusimulia akasema: Amenisimulia baba yangu kutoka kwa Qataadah amesema: ametusimulia Anas ibn Malik amesema: Mtume alikuwa akiwazingukia wake zake kwa saa moja usiku na mchana na hali ya kuwa idadi yao ni kumi na mmoja, nikamwambia Anas: Hivi alikuwa anaweza kufanya hivyo? Akasema: Sisi tulikuwa tukizungumza kwamba yeye amepewa nguvu ya wanaume thelathini." Bila shaka hii ni riwaya ya uzushi iliyokusudiwa kumtia aibu Mtume(s.a.w.w) ili kulihalalishia baraza la Utawala na vitendo vya Muawiyah na Yazid asiye na haya. Yawezekanaje Anas ibn Malik akafahamu kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alikuwa akiwaingilia wakeze kumi na moja kwa muda wa saa moja? Je, Mtume ndiye aliyemwambia hivyo au alikuwepo? Najilinda kwa Mwenyezi Mungu dhidi ya maneno ya uzushi, na alizipata wapi habari za kuwa Mtume(s.a.w.w) alipewa nguvu za wanaume thelathini?

Kwa hakika hayo ni madhambi makubwa kwa (kumzulia) Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ambaye uhai wake wote alipigania dini, kufanya ibada, kufundisha na kuelekeza mema kwa umma wke. Ni kitu gani wnachokiamini wapumbavu hawa pale wanapojitokeza na upuuzi kama huu? Ni kama kwamba wao kwa mujibu wa akili zao zilizochafuliwa na matamanio ya kinyama, walikuwa wakijifaharisha mbele ya jamaa zao kutokana na kuingilia mno wanawake na kuwa na nguvu nyingi za kuingilia. Na kwa kweli riwaya hizo zilizushwa ili kumchafulia Mtume(s.a.w.w) heshima na utukufu wake, na pili kuuhalalisha tabia ya kutokuwa haya waliyokuwa nayo watawala na Makhalifa ambao waliyajaza majumba yao wajakazi na wanawake bila ya mpaka kwa kuwa tu imewamiliki mikono yao ya kuume. Naye Anas ibn Malik msimulizi wa hadithi hii atasema nini pale Ummul-muuminina Aisha mke wa Mtume ambaye alikuwa akisema kuwa Mtume(s.a.w.w) yuko kama wanaume wengine kuhusu suala la jimai?

Muslim ameandika ndani ya sahih yake, Kitabut-taharah Babu naskhil-mai, minal-mai Wawujiibul-ghusli bil-tiqail-khitanain. Imepokewa kutoka kwa Abuz-zubair, kutoka kwa Jabir ibn Abdillahi naye kutoka kwa Ummukul-thuum naye kutoka kwa Aisha mke wa Mtume(s.a.w.w) amesema: "Kuna mtu alimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuhusu mwanaume aliyemuingilia mkewe kisha hakukidhi haja yake je wakoge wote wawili? na Aisha alikuwa amekaa (hapo) basi Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema: hakika mimi hufanya hivyo na huyu ( yaani bibi Aisha) na kisha tunakoga." Kisha mwenye kuisherehesha hadithi hii katika hamish ya sahih Muslim anaongeza kauli yake anasema: "Thumma yuksilu maana yake kama ilivyo ndani ya Misbah ni Aksalal-mujamiu ni kuwa atakapotoka bila ya kutoa manii kwa ajili ya uchovu au kitu kingine."

Sasa basi ikoje hali hii kwa Mtume ambaye amepewa nguvu za wanaume thelathini (kama ilivyodai riwaya ya Anas)? Riwaya hii ni riwaya nyingine miongoni mwa riwaya ambazo ziliwekwa na wazushi, Mwenyezi Mungu awalaani na awazidishie adhabu kali mara dufu, vinginevyo ni nani mwenye akili atakayekubali riwaya kama hizi eti zimetokana na Mtume ambaye atakuwa hana haya kiasi gani mpaka amweleze mwanaume yule tena mbele ya mkewe mambo ambayo muumini wa kawaida anaona aibu kuyasema maneno kama hayo? Na kwa kutaka kuhalalisha muziki na kucheza ngoma, vitu ambavyo vilipata umashuhuri katika zama za utawala wa Banu Ummayyah hebu sikiliza maelezo yafuatayo: Mtume anachungulia ngoma na kusikiliza muziki. Bukhari ameandika ndani ya sahihi yake katika Kitabun-nikaah mlango wa kupiga dufu kwenye harusi na sherehe amesema: Ametusimulia Bishr ibn Al-mufadhal, ametusimulia Khalid ibn Dhak-waan amesema: "Rabii binti Mu'awadh ibn Afraa, Mtume(s.a.w.w) alikuja akaingia wakati nikichezwa harusi akakaa kitandani kwangu kama ulivyokaa wewe na mimi, basi wajakazi wetu wakawa wanapiga dufu na wanawaombolezea wale waliouawa siku ya Badri, miongoni mwa wazee wangu, basi mmoja wao alisema: Kati yetu yupo Nabii ambaye anayajua yatakayotokea kesho, Mtume akasema: Acha maneno haya sema yale uliyokuwa ukiyasema."

Kama ambavyo Bukhari amesimulia ndani ya sahihi yake, Kitabul-jihaad babiid-darq, na pia Muslim ndani ya sahihi yake Kitabul-i'idain Babiir-rnkhsati Fil-laibi ladhi la ma'asiyala fihi. Imepokewa kutoka kwa bibi Aisha amesema: "Mtume aliingia kwangu nami nikiwa na wajakazi wawili wakiimba nyimbo ya Buatha (jina la mahali), akalala juu ya godoro na akageuza uso wake, basi Abubakar akaingia akanikemea akasema (haifai) mazumari ya shetani mbele ya Mtume, Mtume akamuelekea Abubakr akasema. Waache (wacheze) alipopuuza nikawaashiria wakatoka." Na imepokewa kutoka kwa Aisha amesema: "Ilikuwa siku ya Idi, kuna Msudani mrnoja alikuwa akicheza kwa ngoma na mikuki, sasa imma nilimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu au yeye alisema, Je, unapenda kuangalia, nikasema ndiyo, basi akanisimamisha nyuma yake na shavu langu likiwa shavuni kwake na huku akisema, endeleeni enyi bani Ar-fadah mpaka nilipochoka. Akasema kuniambia; Umetosheka? Nikasema, Ndiyo, akasema, Basi nenda." Kama alivyosimulia Muslim ndani ya sahihi yake. Kitabus-salatul-i'idaini Babur-rukhsat Fillaib. Kutoka kwa Aisha amesema: "Walikuja Wahabeshi siku ya sikukuu wakiruka ruka ndani ya msikiti, basi Mtume(s.a.w.w) akaniita nikaweka kichwa changu begani kwake nikawa naangalia mchezo wao mpaka mimi nikawa ndiye niliyeondoka na kuacha kuwaangalia."

Vile vile Bukhari ameandika ndani ya sahihi yake, Kitabun-nikah, Babu dhihabin-nisai was-sib-yan Ilal-u'rsi. Imepokewa kutoka kwa Anas ibn Malik amesema: "Mtume(s.a.w.w) aliwaona wanawake na watoto wanakuja kutoka harusini, basi haraka alisimama akasema: Bila shaka ninyi ni watu mupendazao mno kwangu mimi." Mwenye kuisherehesha Bukhari, anasema: "Mum Tannan (tamko la Kiarabu) maana yake ni kuwa Mtume alisimama kwa haraka mno kwa kuwafurahia." Na ili wahalalishe uharamu dhidi ya pombe na ulevi, hebu angalia maelezo yafuatayo: (Eti) Mtume anakunywa pombe ya zabibu! Bukhari ameandika ndani ya sahih yake Kitabun-nikah katika mlango wa mwanamke kusimama mbele ya wanaume harusini na kuwahudumia maji ya zabibu, pia ndani ya mlango wa maji ya zabibu na kinywaji kisicholewesha harusini. Imepokewa kutoka kwa Abu Hazim, nave kutoka kwa Sahl amesema: "Pindi Abu Usaid As-said alipoowa, alimwita Mtume(s.a.w.w) na Masahaba wake, basi hakuwatengenezea chakula wala kuwasogezea isipokuwa (kazi hiyo ilifanywa na) mkewe ambaye ndiye Ummu Usaid." Kitakachokujulisha ni kwamba wao wanakusudia kwa riwaya hii kwamba Mtume(s.a.w.w) alikunywa Nabidh huenda makusudio siyo ile pombe ya zabibu au tende inayofahamika, bali hayo yalikuwa ni mazoweya kwa Waarabu kuziweka tende ndani ya maji ili kuondosha harufu ya maji, kwa hiyo siyo ile Nabidhi yenyewe, na baadhi yao wanaona kuwa inafaa kuitumia.

Muslim amethibitisha riwaya hii ndani ya sahihi yake, Kitabul-ashrubah mlango unaoruhusu Nabidh ambayo haikukolezwa na haileweshi, na kutokana na hapa ndipo watawala (wa Kibanu Ummayyah) waliporuhusu pombe kwa madai kuwa ni halali madam haileweshi. Matendo waliyokuwa nayo watawala wa Kibanu Ummayyah na Banu Abbas hebu angalia maelezo yafuatayo: (Eti) Mtume hajiheshimu Bukhari amesimulia ndani ya sahih yake, Kitabul-hajji, Babu ziyarati yaumin-nahr, kutoka kwa bibi Aisha amesema: "Tulihiji pamoja na Mtume(s.a.w.w) tukafanya ifadha siku ya kuchinja, basi Safiya akaingia katika siku zake, Mtume(s.a.w.w) akamtaka Safiyyah kile ambacho mume hukitaka kwa mkewe, basi mimi nikasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu hakika yeye yumo ndani ya siku zake." Basi ni ajabu iliyoje kwa Mtume huyu ambaye anapenda kumuingilia mkewe mbele ya ushuhuda wa mkewe mwingine, kiasi mke huyo anamjulisha Mtume kuwa mke yule yumo ndani ya siku zake za hedhi hali yakuwa yule mke aliyekusudiwa na Mtume hajui kitu, kwa hiyo (Aisha) ndiye anamfahamisha Mtume wa Mungu kuwa ana hedhi!! (Eti) Mtume hana haya.

Kama alivyoandika Muslim ndani ya sahih, Kitabul-fadhail, Babu fadhail Uthman ibn Afan amesema Muslim: Kutoka kwa mama Aisha mkewe Mtume(s.a.w.w) na Uthman wamesimulia kwamba, "Abubakr alipiga hodi nyumbani kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) hali ya kuwa Mtume amelala kitandani kwake na amevaa shuka ya Aisha, basi Mtume akamkaribisha Abubakr naye akiwa katika hali hiyo hiyo, basi Mtume akamtimizia Abubakr shida yake (iliyomleta) kisha akaondoka, Uthman anasema, Kisha Umar alipiga hodi na akakaribishwa, hali ya kuwa Mtume yuko katika hali ile ile, Mtume akamtimizia shida yake kisha akaondoka, Uthman anasema, kisha nilibisha hodi mimi, basi Mtume akakaa na akamwambia Aisha ajifunike nguo zake. Basi nikamaliza shida yangu kisha nikatoka. Hapo Aisha akasema, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu mbona sikukuona unafadhaika kwa ajili ya Abubakr na Umar (r.a.) kama ulivyofadhaika kwa Uthman? Mtume akasema: Hakika Uthuman ni mtu mwenye haya nami nilichelea kumkaribisha nikiwa katika hali ile ili asije akashindwa kunieleza shida yake.? Ni Mtume gani huyu ambaye anawakaribisha Masahaba wake hali ya kuwa kalala amejifunika shuka ya mkewe kitandani kwake na pembeni yake yupo mkewe ambaye amevaa vazi la faragha, mpaka anapokuja Uthman akakaa ndipo Mtume anamuamuru mkewe kujifunika nguo (je, ni kweli haya)? (Eti) Mtume hajisitiri. Bukhari ameandika ndani ya sahih yake, Kitabus-salat. Babu Karahiyyat-tit-taari fis-salat, na vile vile Muslim ameandika ndani ya Kitabul-haidh, Babul-I'itinai bihifdhil-aurah.

Imepokewa kutoka kwa Jabir ibn Abdallah, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu alikuwa pamoja nao akibeba mawe kwa ajili ya Al-ka'abah akiwa amevaa shuka, basi ammi yake Mtume bwana Abbas akasema kumwambia Mtume; "Ewe mwana wa ndugu yangu lau ungeifungua shuka yake ukaifunga mabegani ili isiharibiwe na mawe, basi Mtume akaifungua na kuifunga mabegani, mara akadondoka na kuzimia, basi Mtume kuonekana tena uchi baada ya hapo." Angalia ewe msomaji tuhuma hizi alizozushiwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , Mtume ambaye haya ameifanya kuwa ni miongoni mwa nguzo za imani, Mtume ambaye ni mwenye haya mno kuliko hata mwali aliyeko ndani, na hawakutosheka na riwaya za Mtume kutokujiheshimu na kufunua mapaja yake mbele ya Sahaba zake, bali mpaka wamemtuhumu Mtume kuwa alikaa uchi kwa riwaya hii waliyoizusha. Hivi kweli Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa watu hawa alikuwa ni mjinga kiasi hiki cha kusikiliza maneno ya ammi yake na akafunua uchi wake mbele za watu? Namuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu aniepushe kutokana na maneno ya mashetani na maibilisi ambao wanamzulia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Mtume huyu ambaye wakeze na watu wa karibu yake hawakupata kuona utupu wake, jambo ambalo sheria inamruhusu kuwaonesha wakeze utupu wake. Pamoja na hayo Ummul Muuminina Aisha anasema: Sikupata kamwe kuangalia wala kuuona utupu wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) .[169] Basi kama haya ndiyo mahusiano baina ya Mtume na wakeze ambao walikuwa wakikoga pamoja naye ndani ya chombo kimoja na Mtume hujisitiri utupu wake nao hawakupata kuuona kamwe basi vipi (itawezekana) kwa Masahaba wake na watu wengine?

Bila shaka yote hayo ni miongoni mwa uzushi na maovu ya Kibanu Ummayyah ambao walikuwa hawakuacha kufanya maovu ya kila aina, na kwa namna maovu yao yalivyokithiri kuna mmoja miongoni mwa makhalifa wa kibanu Umayyah aliyekuwa akifurahia maneno ya mshairi miongoni mwa washairi ambaye humuambia Khalifa huyo nyimbo za mapenzi kisha Khalifa huyo akasimama na kuvua nguo halafu akabusu dhakari yake, kwa hiyo siyo ajabu kwa watu hao kumvua nguo Mtume(s.a.w.w) .

Na maradhi haya ya kinafsi yamezagaa miongoni mwao mpaka leo hii limekuwa ni jambo la kawaida kwa baadhi ya watu wasiojali matendo yao tena hawaithamini kabisa tabia njema na kuwa na haya, hadi sasa kumekuweko na vilabu na mikusanyiko ya uchi kila mahali wanakusanyika wanaume na wanawake wakijionyesha kuwa, Ewe Mola wetu sisi ndiyo hawa kama ulivyotuumba, na kwa jinsi walivyohalalishia kuichezea dini na hukumu za sheria hebu angalia yafuatayo:- Mtume anasahau ndani ya sala yake. Bukhari ameandika ndani ya sahihi yake, Kitabul-adabi, Babu maa yajuzu Min dhikrin-nasi, na Muslim ndani ya sahih yake Kitabul-masajid wamawaadhi 'is-salat, Babus Sahwi fis-salat Was-sujudi laha. Imepokewa kutoka kwa Abu Hurairah amesema: "Mtume alitusalisha sala ya adhuhuri rakaa mbili kisha akatoa salamu, kisha akasimama kwenye gogo mbele ya msikiti na akaweka mikono yake juu yake, na miongoni mwa watu waliokuwepo ni Abubakr na Umar wao wakaogopa kumuuliza Mtume. Basi watu wenye haraka wakatoka wakasema, je, sala imepunguzwa? Katika hao alikuwemo mtu mmoja ambaye Mtume alikuwa akimwita Dhul-yadain, mtu huyo akasema. Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu umesahau au sala imepunguzwa? Mtume akasema, sikusahau na wala haijapunguzwa, watu wakasema, Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu umesahau, Mtume akasema: Amesema kweli Dhul-yadain."

Basi Mtume akasimama na kusali rakaa mbili kisha akatoa Takbira akasujudu kama anavyosujudu au akarefusha zaidi kisha akanyanyua kichwa chake akatoa takbira kisha akasujudu sijda yake au zaidi, kisha akanyanyua kichwa chake akatoa takbira.

Haiwezekani kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kusahau ndani ya sala yake akakosa kufahamu ni rakaa ngapi amesali, na inaposemwa kwamba aliambiwa kuwa amepunguza (rakaa za) sala na akasema, Sikusahau wala haikupunguzwa, bila shaka huo ni uongo uliolenga kuwatakasa Makhalifa wao ambao mara nyingi walikuwa wakija kwenye sala hali ya kuwa wamelewa hawajui ni rakaa ngapi wanasali, na kisa kinachomhusu amiri wao aliyewasalisha rakaa nne kwenye sala ya asubuhi kisha akawageukia akawaambia, Niwaongezeni au mmetosheka? Ni kisa mashuhuri ndani ya vitabu vya historia.

Kama alivyoandika Bukhari ndani ya sahih yake, Kitabul-adhan, Balm Idha Qaamar-rajulu a'nyasaaril-Imam amesema: Imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas (r.a) amesema: "Nililala nyumbani kwa Maimuna, na Mtume alikuwa huko usiku huo, basi Mtume akatawadha kisha akasimama anasali, nami nikasimama kushoto kwake, basi akanishika na kuniweka kulia kwake akasali rakaa kumi na tatu kisha akalala mpaka akawa anakoroma na alikuwa akilala hukoroma, kisha muadhini alimjibu na akatoka akaswali bila ya kutawadha." Amru amesema, "Nikamsimulia Bukaira akasema, Kuraibu amenisimulia habari hiyo." Riwaya kama hizi za uongo dhidi ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) zinawafanya maamiri na masultani wa Kibanu Umayyah na bani Abbas na wengineo waipuuze sala na wapuuze kutawadha na wapuuze kila kitu kiasi kwamba mfano huo umeenea kwetu sisi. Mtume kuapa kisha akavunja kiapo chake Bukhari amesimulia ndani ya sahihi yake Kitabul-maghazi, kisa cha Oman na Bahrain, babu Qudumil-Ash-ariyyin wa Ahlul-Yaman. Imesimuliwa kutoka kwa Abu Qulaibah naye kutoka kwa Zuhdam amesema , "Abu Musa alipofika aliukirimu mtaa huu wa kabila la Juhrum, na sisi tulikuwa tumekaa naye huku anakula kuku. Miongoni mwa watu waliokuwepo, kuna mtu fulani alikuwa kakaa, basi akamwita aje kula akasema, mimi nimemuona anakula kitu ambacho sikukipenda. Abu Musa akasema, Njoo hakika mimi nilimuona Mjumbe wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akila chakula hiki.

Yule mtu akasema, Mimi nilikwisha apa kuwa sintakula chakula hicho. Yeye akasema, njoo nikueleze jambo kuhusu kiapo chako. Kwa hakika sisi tulimuendea Mtume(s.a.w.w) tukiwa ni kikundi cha kabila la Ash-ari, tukamuomba atupatie kipando akakataa kutupatia, hatimaye Mtume akaletewa ngawira ya ngamia akaamuru tupewe ngamia watano.

Tulipokwisha kuwachukuwa tukasema, Tumemsahaulisha Mtume kiapo chake basi kamwe sisi si wenye kufaulu. Basi mimi nikamwendea nikasema, Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu hakika wewe uliapa kwamba hutatupatia kipando na sasa umetupatia. Mtume akasema. Ndiyo lakini siwezi kuapa kisha nione kinyume chake kuwa ni bora kuliko kiapo hicho ila nitafanya kile ambacho ni bora kuliko kiapo hicho."

Hebu mwangalie Mtume huyu ambaye Mwenyezi Mungu Mtukufu ametuma ili awafunze watu kuvitekeleza viapo na wala wasivivunje isipokuwa kwa kutoa kafara. Lakini yeye mwenyewe anaamrisha kitu kisha yeye hakitendi anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

لَا يُؤَاخِذُكُمُ اللَّـهُ بِاللَّغْوِ فِي أَيْمَانِكُمْ وَلَـٰكِن يُؤَاخِذُكُم بِمَا عَقَّدتُّمُ الْأَيْمَانَ فَكَفَّارَتُهُ إِطْعَامُ عَشَرَةِ مَسَاكِينَ مِنْ أَوْسَطِ مَا تُطْعِمُونَ أَهْلِيكُمْ أَوْ كِسْوَتُهُمْ أَوْ تَحْرِيرُ رَقَبَةٍ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ ثَلَاثَةِ أَيَّامٍ ذَٰلِكَ كَفَّارَةُ أَيْمَانِكُمْ إِذَا حَلَفْتُمْ وَاحْفَظُوا أَيْمَانَكُمْ كَذَٰلِكَ يُبَيِّنُ اللَّـهُ لَكُمْ آيَاتِهِ لَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿٨٩﴾

"Mwenyezi Mungu hatakuadhibuni kwa viapo vyenu vya upuuzi, lakini atakuadhibuni kwa viapo mlivyoviapa kwa nia mliyoifunga barabara, basi (kama hamukuvitekeleza viapo vyenu) kafara yake ni kuwalisha masikini kumi kwa chakula cha kawaida mnachowalisha watu wa nyumbani mwenu au kumpa uhuru Mtumwa, lakini asiyeweza kupata hayo. Basi afunge siku tatu, hii ndiyo kafara ya viapo vyenu mnapoapa, na vilindeni viapo vyenu (msiape kisha mkakosa kuvitimiza) namna hivi ndiyo Mwenyezi Mungu anavyokubainishieni Aya zake ili mupate kushukum" (Qur'an, 5:89).

Na amesema tena Mwenyezi Mungu: "Na wala msitengue viapo baada ya kuvithibitisha ". (Qur'an 16:91).

Lakini jamaa hawa hawakumuachia Mtume(s.a.w.w) namna yoyote ya ubora na heshima, (wakamzulia mambo chungu nzima).