WAULIZE WANAOFAHAMU

WAULIZE WANAOFAHAMU0%

WAULIZE WANAOFAHAMU Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Misingi mikuu ya Dini

WAULIZE WANAOFAHAMU

Mwandishi: Muhammad Tijani As-samawi At-Tunisi
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi:

Matembeleo: 49059
Pakua: 3932

Maelezo zaidi:

WAULIZE WANAOFAHAMU
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 26 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 49059 / Pakua: 3932
Kiwango Kiwango Kiwango
WAULIZE WANAOFAHAMU

WAULIZE WANAOFAHAMU

Mwandishi:
Swahili

9

WAULIZE WANAOFAHAMU

BUKHARI AMEANDIKA KATIKA SAHIHI YAKE

Bukhari ameandika katika sahihi yake juzuu ya nne mlango wa vitu alivyokuwa akiwapa Mtume wale wanaoimarishwa nyoyo zao, ndani ya Kitabul Jihadi Was-sair.

Imepokewa kutoka kwa Anas ibn Malik kwamba, "Wakati Mwenyezi Mungu alipomjaalia Mtume wake ghanima katika mali za Hawazin, aliwapa baadhi ya watu miongoni mwa Maquraishi, Ansari wakasema, Mwenyezi Mungu amsamehe Mtume wa Mwenyezi Mungu, anawapa Maquraishi na anatuacha sisi na hali panga zetu zinadondoka damu yao? Basi Mtume(s.a.w.w) akawakusanya hapo Qubbah na hakumuacha yeyote kisha akawaambia, Zikoje khabari zilizonifikia kutoka kwenu? Waliporudia usemi wao kwa Mtume, Mtume(s.a.w.w) akasema: Hakika mimi nawapa watu ambao hivi karibuni walikuwa katika ukafiri je, hamridhii watu wende na mali nanyi murudi majumbani kwenu mkiwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu? Basi Wallahi mtakachorudi nacho ni bora kuliko watakachorudinacho.Wakasema, Kwa nini tusiridhike ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika tumeridhia. Basi Mtume akawaambia, Hakika ninyi mtakuja ona upendeleo baada yangu, basi vumilieni mpaka mkutane na Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwenye Hauz, Anas alisema, Hatukuvumilia [2] .

Tunajiuliza : Je, hivi miongoni mwa Ansari wote kulikuwa na mtu japo mmoja aliyeongoka ambaye aliridhia alichokifanya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na akaamini kwamba Mtume hafuati matamanio ya nafsi yake wala hawezi kuacha haki? Na je, aliifahamu kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu kusudio hili aliposema:

فَلَا وَرَبِّكَ لَا يُؤْمِنُونَ حَتَّىٰ يُحَكِّمُوكَ فِيمَا شَجَرَ بَيْنَهُمْ ثُمَّ لَا يَجِدُوا فِي أَنفُسِهِمْ حَرَجًا مِّمَّا قَضَيْتَ وَيُسَلِّمُوا تَسْلِيمًا ﴿٦٥﴾

"Naapa kwa haki ya Mola wako hawawezi kuwa waumini (wa kweli) mpaka wakufanye wewe kuwa ni hakimu katika yale wanayokhitilafiana, kisha wasione uzito nyoyoni mwao juu ya hukumu uliyoitoa na wanyenyekee kabisa." (Qur'ani, 4:65).

Je, alikuwemo miongoni mwao aliyemtetea Mtume(s.a.w.w) wakati waliposema: "Mwenyezi Mungu amsamehe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Hakuna, hapakuwa na yeyote miongoni mwao aliyekuwa na kiwango cha imani iliyowajibishwa na aya tukufu, na kule kusema kwao baada ya usemi wa Mtume kuwa, "Kwa nini tusiridhike ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika tumeridhika." Ukweli haikuwa kwa kutosheka (na maelezo ya Mtumes.a.w.w ) na ndiyo maana ulikuja ushahidi wa Anas naye akiwa yu miongoni mwao pale aliposema, "Mtume alituusia kuvumilia lakini hatukuvumilia."

Bukhari ameandika ndani ya Sahihi yake katika juzuu ya tano, Babu ghaz-watil-hudai-biyyah katika Kitabul-maghazii. imesimuliwa kutoka kwa Ahmad ibn Ishkab, ametusimulia Muhammad ibn Fazail kutoka kwa Al-ala ibn Al-musayyab kutoka kwa baba yake amesema, "Nilikutana na Al-Bar-raa ibn A'zib (r.a) nikasema: Hongera, umefuzu, ulikuwa sahaba wa Mtume(s.a.w.w) na ukampa baia chini ya mti. Akasema:Ewe Mwana wa ndugu yangu, hakika wewe hujuwi tuliyoyazua baada yake " [3] .

Bila shaka Al-Barraa ibn A'zib amesema kweli, kwani wengi wa watu hawayafahamu waliyoyazua Masahaba baada ya Mtume wao kufariki, na miongoni mwake ikiwa ni kumdhulumu wasii wake na Ibn Ammi yake Mtume na kumtenga kwenye ukhalifa, pia walimdhulumu binti ya Mtume Fatimatuz-Zahraa na kumtishia kumchoma moto, na kupora haki yake miongoni mwa zawadi na urithi na khumsi, na pia waliukhalifu Usia wa Mtume na kubadilisha hukumu za sheria. Si hivyo tu bali walichoma moto vitabu vya Sunna ya Mtume na kuidhibiti isisimuliwe, kadhalika walimuudhi yeye Mtume(s.a.w.w) kwa kuwalaani na kuwauwa watu wa nyumba ya Mtume, kuwatenga na kuwatawanya kisha kuwapa uongozi wanafiki na waovu miongoni mwa maadui wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Basi yote hayo na mengineyo miongoni mwa waliyoyazusha Masahaba baada ya Mtume na yakabakia hayafahamiki kwa watu wengi ambao hawakufahamu ukweli isipokuwa yale yaliyopendekezwa na chuo cha Makhalifa (yaani Usunni), na yanayo kila namna ya mabadiliko katika hukumu za Mwenyezi Mungu na Mtume wake (kwa kuingizwa) ijtihadi mbali mbali za watu zilizoitwa kuwa ni Bid 'a nzuri.

Kwa Munasaba huu tunawaambia Masunni, "Enyi ndugu zetu msidanganyike kwa usahaba na kusuhubiana (na Mtume) basi huyu hapa Al-Bar-raa ibn Azib ambaye ni miongoni mwa watu wa mwanzo ambao walimpa baia Mtume(s.a.w.w) chini ya mti, anamwambia mtoto wa nduguye hali halisi ilivyo kwamba, usikudanganye usahaba wangu wala baia yangu chini ya mti, hakika wewe hujuwi niliyoyazua baada ya Mtume, na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema:

إِنَّ الَّذِينَ يُبَايِعُونَكَ إِنَّمَا يُبَايِعُونَ اللَّـهَ يَدُ اللَّـهِ فَوْقَ أَيْدِيهِمْ فَمَن نَّكَثَ فَإِنَّمَا يَنكُثُ عَلَىٰ نَفْسِهِ وَمَنْ أَوْفَىٰ بِمَا عَاهَدَ عَلَيْهُ اللَّـهَ فَسَيُؤْتِيهِ أَجْرًا عَظِيمًا ﴿١٠﴾

"Bila shaka wale wanaokupa baia kwa hakika wanambai Mwenyezi Mungu, msaada wa Mwenyezi Mungu uko juu yao, basi yeyote avunjaye ahadi hii anaivunja kwa kuidhuru nafsi yake..." (Qur'an, 48:10).

Na ni idadi kubwa ya Masahaba walivunja ahadi mpaka hata Mtume alimuusia Ibn Ammi yake Ali kuwapiga (waliovunja ahadi) kama yalivyokuja hayo katika vitabu vya historia.

Bukhari katika Sahih yake ndani ya juzuu ya kwanza na ya tatu katika mlango, Idhaa Nafaran-nasu Anil-Imam fi Salatil-jumuah ndani ya Kitabul-jumuah ameandika kama ifuatavyo. Ameeleza Jabir ibn Abdillah (r.a) amesema: "Ulifika msafara kutoka Sham umebeba vyakula na sisi tunasali pamoja na Mtume(s.a.w.w) sala ya Ijumaa, watu wakakimbia isipokuwa watu kumi na wawili, hapo ndipo iliposhuka aya hii isemayo: "Na waionapo biashara au (vitu) vya upuuzi huvikimbilia na wakakuacha umesimama..."[4] .

Huu ni mfano mwingine wa Masahaba wanafiki ambao hawamuogopi Mwenyezi Mungu wala kumnyenyekea. bali wanakimbia kutoka kwenye Sala ya Ijumaa ili wakaone msafara na biashara na wanamuacha Mtume wa Mwenyezi Mungu amesimama mbele ya Mwenyezi Mungu akitekeleza Faradhi yake kwa unyenyekevu mkubwa. Basi je, hawa ni Waislamu waliokamilika imani yao? Au wao ndio wanafiki wanaodharau Sala, na wasimamapo husiama kwa uvivu? Na hawaepukani miongoni mwao isipokuwa wale waliodumu pamoja na Mtume(s.a.w.w) kuikamilisha Sala ya Ijumaa na idadi yao ilikuwa kumi na wawili tu. Yeyote atakayefuatilia hali za Masahaba na kuchunguza habari zao, huenda akashangaa kwa matendo yao, na hapana shaka kwamba kukimbia kwao kutoka kwenye sala ya Ijumaa kulirudia mara nyingi, na kwa hiyo basi kitabu cha Mwenyezi Mungu kimelisajili tendo hilo kwa kusema: "Waambie kilichopo kwa Mwenyezi Mungu ni bora kuliko mambo ya upuuzi na biashara." Ili ufahamu vyema ewe msomaji Mtukufu kiwango cha heshima yao kwenye sala hii ambayo Waislamu wa leo wanaiheshimu zaidi kuliko wao, hebu basi iangalie riwaya hii ifuatayo.

Bukhari ameandika ndani ya Sahihi yake katika juzuu ya tatu mlango uitwao: Majaa Fil-gharsi" ndani ya Kitabul-Wakalah. Imepokewa kutoka kwa Sahl ibin Said (r.a) kwamba: "Hakika sisi tulikuwa tunafurahi katika siku ya Ijumaa, kwani tulikuwa na bibi Kizee fulani akichukua mizizi ya mmea uitwao 'Salaq' ambayo tulikuwa tukiipanda katika maeneo yetu, basi (kizee huyo) huiweka ndani ya chungu chake na kutia humo mbegu za Shairi. Sifahamu zaidi bali yeye alisema hakuna ndani yake mafuta, basi tukisha sali Ijumaa tunamtembelea na hutusogezea chakula hicho, tulikuwa tukifurahi siku ya Ijumaa kwa ajili hiyo, na tulikuwa hatuli wala hatupumziki isipokuwa baada ya sala ya Ijumaa " -[5] .

Ni maajabu yaliyoje kwa Masahaba hawa ambao hawaifurahii siku ya Ijumaa kwa kukutana na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na kusikiliza hotuba yake na mawaidha yake na kusali nyuma ya Mtume wao, wala hawafurahi kukutana wao kwa wao na mengine yaliyomo ndani ya siku hiyo ikiwa ni miongoni mwa baraka na rehma. Lakini Masahaba wanafurahia siku ya Ijumaa kwa ajili ya chakula maalum kilichoandaliwa na bibi kizee, na lau leo hii Muislamu fulani angesema kuwa siku ya Ijumaa anafurahi kwa ajili ya chakula, basi bila shaka angeonekana ni miongini mwa wasogeza wakati wasiojali dini!! Na tutakapotaka nyongeza ya uchunguzi na kufuatilia, tutawakuta wenye kushukuru (miongoni mwa Masahaba) ambao Qur'an Tukufu imewasifu ni wachache mno na idadi yao haizidi kumi na wawili, na hawa ndiyo (Masahaba) wema ambao hawakukimbia kufuata mambo ya upuuzi na biashara na kuiacha sala, na ndiyo hao hao ambao waliimarika katika Jihadi pamoja na Mtume(s.a.w.w) mahala pengi miongoni mwa nyanja nyingi ambazo masahaba wengine walikimbia na waligeuka nyuma wakatokomea. Bukhari ameandika ndani ya Sahihi yake juzuu ya nne katika mlango wa Yanayochukiza miongoni mwa mizozo na tofauti katika vita, Kitabul-Jihad Was-Sair, Imepokewa toka kwa Al-Bar-raa ibn Azib amesema: "Mtume(s.a.w.w) alimuweka Abdallah ibn Jubair (kuwa kiongozi) wa askari wa miguu siku ya Uhdi, na walikuwa watu hamsini, Mtume akasema, Mkituona tumeshambuliwa msiondoke mahala penu mpaka niwatumieni habari, akasema, Wallahi niliwaona wanawake wanakimbia na miundi yao inaonekana na bangiri zao wakipania nguo zao, basi watu wa Abdallah ibn Jubayr wakasema: 'Ghanimah' yaani Mali hizo, jamaa zenu wameshinda sasa mnangoja nini? Abdallah ibn Jubayr akawaambia: Je, mmesahau alivyokuambieni Mtume wa Mwenyezi Mungu, wakasema, Wallahi tutawafuata watu hao ili tupate ngawira. Walipowafuata mwenendo wao uligeuzwa na wakashambuliwa, hapo ndipo walipokimbia na Mtume akawa anawaita lakini hapakubaki pamoja na Mtume isipokuwa watu kumi na wawili, makafiri wakawauwa miongoni mwetu watu sabini..." [6] .

Na tukishayafahamu yale waliyoyaeleza wanahistoria kuhusu vita hivi (vya Uhdi) kwamba Mtume(s.a.w.w) alitoka akiwa na Masahaba elfu moja na wote wakiwa wamehamasika kwa Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu, lakini wakiwa wamehadaika kwa ushindi walioupata katika vita vya Badri, lakini ghafla waliasi amri ya Mtume(s.a.w.w) na wakasababisha mashambulizi haya mabaya ambayo waliuawa watu sabini akiwemo Hamza ammi yake Mtume(s.a.w.w) , na (Masahaba) wengine wakakimbia na hapakubaki pamoja na Mtume(s.a.w.w) katika uwanja wa vita isipokuwa watu kumi na wawili kama anavyosema Bukhari. Ama wanahistoria wengine wanashuka chini ya idadi hii mpaka watu wanne, tu. nao ni Ali ibn Abi Talib ambaye aliwazuwia washirikina akimlinda Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kwa mbele na Abud-dajjanah akimlinda Mtume kwa nyuma na Talha na Zubair na inasemekana Sahal ibn Hunaif. Kutokana na mazingira haya tunaifahamu vema kauli ya Mtume wa Mwenyezi Mungu aliposema, "Sioni atakayesalimika miongoni mwao isipokuwa mfano wa idadi ya ngamia wasiomchunga" Baadaye yatakuja maelezo kuhusu hadithi hii.

Sasa basi kama Mwenyezi Mungu Mtukufu amewakamia kwa moto watakapokimbia vita, akasema,

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا لَقِيتُمُ الَّذِينَ كَفَرُوا زَحْفًا فَلَا تُوَلُّوهُمُ الْأَدْبَارَ ﴿١٥﴾ وَمَن يُوَلِّهِمْ يَوْمَئِذٍ دُبُرَهُ إِلَّا مُتَحَرِّفًا لِّقِتَالٍ أَوْ مُتَحَيِّزًا إِلَىٰ فِئَةٍ فَقَدْ بَاءَ بِغَضَبٍ مِّنَ اللَّـهِ وَمَأْوَاهُ جَهَنَّمُ وَبِئْسَ الْمَصِيرُ ﴿١٦﴾

"Enyi mlioamini mkutanapo vitani na wale waliokufuru basi msiwageuzie migongo mkakimbia, na atakayegeuka siku hiyo akakimbia isipokuwa ageukaye kwa kushambulia au ili akaungane na sehemu nyingine za jeshi la Waislamu, vinginevyo atastahiki ghadhabu za Mwenyezi Mungu na mahala pake ni moto wa jahanam napo ni mahala pabaya pa kurejea." (Qur'ani, 8:16).

Basi ikoje daraja ya Masahaba hawa ambao wanaikimbia sala kwa ajili ya mambo ya mchezo na biashara na wanaikimbia Jihadi kwa hofu ya mauti na kumuacha Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) peke yake akiwa katikati ya maadui? Na katika hali zote mbili, walikimbia na kugeuka wote na Mtume hakubakia isipokuwa na watu kumi na wawili kwa makadirio ya juu, basi wana hali gani Masahaba enyi wenye kufikiri? Huenda baadhi ya wachunguzi wanaposoma hadithi mfano wa riwaya kama hizi wanayaona mambo haya kama ni madogo na wanadhani kuwa ni matukio ya kipuuzi ambayo Mwenyezi Mungu ameyasamehe na kwamba Masahaba hawakurudia tena kufanya hivyo.

Sivyo kabisa, bila shaka Qur'ani tukufu itatupatia ukweli unaotisha, hakika Mwenyezi Mungu amesajili kukimbia kwao siku ya Uhd kwa kusema: "Na kwa hakika Mwenyezi Mungu alikukamilisheni miadi yake mkawaua kwa idhini yake, mpaka mliporejea na mkagombana katika shauri lile na mkaasi baada ya yeye kukuonesheni mliyoyapenda. Wako miongoni mwenu wanaopenda dunia na wako miongoni mwenu wanaopenda akhera, kisha (Mwenyezi Mungu) akakuwekeni mbali nao ili akujaribuni, naye sasa amekusameheni, na Mwenyrzi Mungu ni Mwenye ihsani nyingi juu ya wanaoamini. Kumbukeni mlipokuwa mkikimbia mbio wala ninyi hamumngoji yeyote hali Mtume alikuwa anakuiteni nyuma yenu, (Mwenyezi Mungu) akakupeni huzuni juu ya huzuni, na ili msihuzunike (sana) kwa yale yaliyokupoteeni, wala kwa misiba iliyokupateni na Mwenyezi Mungu anayajua yote mnayoyatenda." (Qur'ani, 153).

Aya hizi zilishuka baada ya vita vya Uhdi ambavyo Waislamu walishambuliwa vibaya kwa sababu ya kupenda kwao starehe za dunia hasa wakati walipowaona wanawake wanapania nguo zao, miundi yao na bangiri zinaonekana kama alivyoeleza Bukhari. Wakamuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake(s.a.w.w) kama ilivyoeleza Qur'ani, basi je, Masahaba walilizingatia tukio hilo na wakatubia kwa Mwenyezi Mungu na kumuomba msamaha na hawakurudia tena kosa kama hilo? Sivyo kabisa, hakika wao hawakutubu na walirudia kosa kubwa zaidi kuliko hilo katika vita ya Hunain ambayo ilitokea mwishoni mwa uhai wa Mtume(s.a.w.w) , na idadi yao katika vita hiyo ilikuwa ni watu elfu kumi na mbili kama wanahistoria walivyoeleza. Pamoja na wingi wao walijitetea kwa kukimbia na hawakugeuka nyuma kama kawaida yao, wakamuacha Mtume wa Mwenyezi Mungu katikati ya maadui wa Mwenyezi Mungu miongoni mwa washirikina akiwa na watu tisa au kumi miongoni mwa Bani Hashim wakiongozwa na Ali ibn Abi Talib kama alivyoeleza Al-yaa'qubi katika tarikh yake na wengineo.

Sasa basi ikiwa kukimbia kwao siku ya Uhd lilikuwa ni jambo baya, hapana shaka kwamba, siku ya Hunain lilikuwa ni jambo baya zaidi na lenye kuchukiza mno, kwani wenye kusubiri ambao waliimarika pamoja na Mtume siku ya Uhdi walikuwa watu wanne katika elfu moja nayo ni sawa na mtu mmoja katika kila watu mia mbili na hamsini. Ama siku ya Hunain waliosubiri na wakaimarika walikuwa kumi katika idadi ya Masahaba elfu kumi na mbili nayo ni sawa na mtu mmoja katika kila watu elfu moja na mia mbili. Na iwapo vita vya Uhdi vilikuwa mwanzoni mwa Hijra na kwamba watu wengi walikuwa bado wachache na ndiyo hivi karibuni walikuwa katika zama za ujinga, basi ni ipi sababu yao katika vita ya Hunain ambayo ilitokea mwishoni mwa mwaka wa nane wa Hijra ya Mtume? Ilikuwa imebaki miaka miwili tu katika uhai wa Mtume, lakini pamoja na ukubwa wa idadi yao na maandalizi yao walikimbia bila kumgeukia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) . Qur'an Tukufu inabainisha wazi msimamo wao mbaya na kukiambia kwao katika vita hivyo kwa kusema:

وَيَوْمَ حُنَيْنٍ إِذْ أَعْجَبَتْكُمْ كَثْرَتُكُمْ فَلَمْ تُغْنِ عَنكُمْ شَيْئًا وَضَاقَتْ عَلَيْكُمُ الْأَرْضُ بِمَا رَحُبَتْ ثُمَّ وَلَّيْتُم مُّدْبِرِينَ ﴿٢٥﴾ ثُمَّ أَنزَلَ اللَّـهُ سَكِينَتَهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ وَعَلَى الْمُؤْمِنِينَ وَأَنزَلَ جُنُودًا لَّمْ تَرَوْهَا وَعَذَّبَ الَّذِينَ كَفَرُوا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ الْكَافِرِينَ ﴿٢٦﴾

"Na siku ya Hunain ambapo wingi wenu ulikupandisheni kichwa lakini haukukufaeni chochote na ardhi ikawa finyu juu yenu ingawa ilikuwa na nafasi kisha mkakimbia, hatimaye Mwenyezi Mungu akateremsha utulivu kwa Mtume wake na juu ya waumini, na akateremsha majeshi ambayo hamkuyaona na akawaadhibu wale waliokufuru na hayo ndiyo malipo ya makafiri." (Qitr'ani, 9:25-26).

Mwenyezi Mungu anabainisha kwamba alimuimarisha Mtume wake na wale waliosubiri pamoja naye kwenye vita kwa kuwateremshia utulivu, kisha akawatia nguvu kwa jeshi la Malaika wakapigana pamoja nao na akawapa ushindi dhidi ya Makafiri, wala hakukuwa na haja ya msaada wa wale walioritadi ambao waliwakimbia maadui kwa hofu ya kufa, na kwa kufanya hivyo wakamuasi Mola wao na Mtume wao, na kila Mwenyezi Mungu alipowapa mtihani aliwakuta ni wenye kushindwa!! Bukhari ameandika ndani ya Sahih yake katika juzuu ya tano mlango wa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu isemayo; "Na siku ya Hunain ulikupandisheni kichwa wingi wenu na haukuwasaidieni chochote," Kitabul-Maghazi kwamba: Abu Qatadah amesema:"Ilipokuwa siku ya Hunain, nilimuangalia mtu fulani miongoni mwa Waislamu anapigana na mtu fulani miongoni mwa washirikina na mwingine miongoni mwa washirikina anamvizia Muislamu kwa nyuma ili amuue, basi nikafanya haraka kumuendea yule anayemvizia, basi akanyanyua mkono wake ili anipige upanga (nikamuwahi) nikampiga mkono wake nikaukata kisha akanishika na kunikumbatia kwa nguvu sana mpaka nikaogopa kisha akaniachia na akatoka nikamsukuma na kumuua. Waislamu walielemewa (wakakimbia) nami nikawa pamoja nao, basi mara ghafla (nikamuona) Umar ibn Khatab akiwa ndani ya kundi la watu nikamwambia, Mbona hivi," watu wamepatwa na nini? akasema, Hiyo ni amri ya Mungu. (Sahih Bukhari Juzuu ya 5 uk.101).

Wallahi mambo aliyoyafanya Umar siku hiyo ni ajabu, lakini huyu ndiye Umar ambaye mbele ya Masunni anaonekana kuwa ni shujaa mno miongoni mwa Masahaba kama siyo shujaa kupita wote kabisa. Kwa mujibu wa Masunni, wao wanamuona kwamba eti ni mtu ambaye kupitia kwake Mwenyezi Mungu aliutia nguvu Uislamu na kwamba Waislamu hawakuutangaza wazi wazi Uislamu ila baada ya kusilimu kwa Umar. Hapana shaka historia imetupatia msimamo sahihi na wa kweli na ni jinsi gani Umar alivyokimbia siku ya Khaibar, pale Mtume alipomtuma aende katika mji wa Khaibar akauteke (uwe chini ya himaya ya Kiislamu) na akamtuma pamoja na jeshi akashindwa yeye pamoja na wanajeshi wake na wanajeshi aliofuatana nao wakarudi hali wakimtuhumu kwa woga na yeye akiwatuhumu wao kwa woga. Kama ambavyo aligeuka na akakimbia siku ya Hunain yeye na waliokimbia au huenda alikuwa ni wa kwanza kukimbia na watu wakamfuata kwa kuwa yeye alikuwa ndiye shujaa wao, na ndiyo maana tunamuona Abu Qatada anamgeukia Umar kati ya maelfu ya watu waliokimbia anamuuliza kana kwamba anashangazwa akamwambia, "Watu wamepatwa na nini?"

Umar ibn Khatab siyo tu alikimbia jihadi na kumuacha Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) katikati ya maadui miongoni mwa washirikina, bali alimdanganya Abu Qatada kwa kumwambia; "Hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu...!" Je, hivi Mwenyezi Mungu ndiye aliyemuamuru Umar ibn Khatab akimbie vita? Au amemuamrisha kusimama imara na kusubiri ndani ya vita na asikimbie? Kwani Mwenyezi Mungu amesema kumwambia Umar na wenzake, "Enyi mlioamini mtakapokutana vitani na wale waliokufuru msiwakimbie. " (Qur'ani, 8:15).

Kama ambavyo Mwenyezi Mungu alichukua ahadi kwa Umar na kwa wenzake kwa jambo hilo ambalo limekuja ndani ya Qur'ani kwamba: "Na kwa yakini walikwisha fanya ahadi na Mwenyezi Mungu zamani ya kwamba, hawatageuza migongo (yao watakapokuja makafiri kuwashambulia) na ahadi ya Mwenyezi Mungu itaulizwa." Basi vipi baba Hafsa akimbie vita na kudai kuwa hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu? Hakika yuko mbali na aya hizi zenye kubainisha ukweli, au (tuseme), "Katika nyoyo zao kuna makufuli?" Hapa sisi hatukusudii kuichunguza hali ya Umar ibn Khatab kwani tutamtengea mlango maalum wa kwake, lakini hadithi ya Bukhari inaathiri na haikutupa nafasi ya kuacha kuleta dokezo juu ya Umar kwa haraka kabla ya kufika wakati wake, na kilicho cha muhimu sasa hivi ni ushahidi wa Bukhari kwamba, pamoja na wingi wa idadi ya masahaba lakini walikimbia siku ya vita vya Hunain, na yeyote anayesoma vitabu vya historia kuhusu vita hivyo yatamdhihirikia mambo ya ajabu mno.

Iwapo amri ya Mwenyezi Mungu Masahaba wengi hawakuitii kama tulivyokwishaona hapo kabla, basi siyo ajabu kwao kupinga amri za Mtume(s.a.w.w) hali ya kuwa yu hai. Ama amri zake baada ya kufa kwake (naapa kwa baba yangu na mama yangu) na nimeyakuta mambo mengi yanayotokana nao ikiwa ni pamoja na kupuuza (maamrisho) na kuzibadilisha (hukumu zake). Hakika hapana ubaya kuyasimulia hayo. Masahaba na maamrisho ya Mtumes.a.w.w ) zama za uhai wake. Hebu na tuanze na maamrisho ambayo Mtume aliyaamrisha zama za uhai wake, maamrisho ambayo yalipambana na kutotiiwa na uasi kutoka kwa hawa Masahaba. Sisi hatutazungumzia ila yale tu aliyoyaandika Bukhari ndani ya Sahihi yake ili tufupishe maelezo, hatutajishughulisha na Sihah zingine za Kisunni kwasababu hapana shaka kabisa katika sahihi zingine kuna ibara nyingi mno zilizowazi na zilizofafanuliwa vyema. Bukhari ameandika ndani ya Sahih yake, juzuu ya tatu mlango wa sharti za jihadi na mapatano na wapiganaji, Kitabus-Shurut. Baada ya Bukhari kukileta kisa cha Hudaibiyyah na upinzani wa Umar ibn Al-khat-tab kwa kitu ambacho Mtume wa Mwenyezi Mungu amekiwafiki, na pia kukitilia mashaka mpaka akamwambia Mtume waziwazi, "Hivi wewe siye Nabii wa Mwenyezi Mungu wa kweli?"... Mpaka mwisho wa tukio Bukhari anasema: "Alipomaliza suala la kuandika Sul-hu ya Hudaibiyyah Mtume wa Mwenyezi Mungu alisema kuwaambia Masahaba wake, Simameni mchinje kisha mnyoe. Akasema; Wallahi hakuna mtu aliyesimama miongoni mwao mpaka akarudia mara tatu, hakuna aliyesimama. Mtume akaingia ndani kwa Ummu Salamah akamuelezea yaliyomkuta kutoka kwa watu." (Sahih Bukhari Juz.3 uk.182).

Je, hushangai ewe msomaji kutokana na Masahaba kutotii na kuasi kwao amri ya Mtume(s.a.w.w) , hata baada ya kurudia mara tatu ikawa hakuna mtu yeyote miongoni mwao aliyemuitikia Mtume? Mahala hapa, sina budi kuueleza mjadala uliofanyika baina yangu na baadhi ya wanachuoni huko Tunis baada ya kutoka kitabu changu kiitwacho Thummah-Tadaytu, na kwa kuwa wao walisoma ndani yake ufafanuzi wangu juu ya Sul-hu ya Hudaibiyyah, basi wao kwa upande wao walitoa uchambuzi kuhusu sehemu hii kwa kusema: "Ikiwa Masahaba waliasi amri ya Mtume(s.a.w.w) ya kuchinja na kunyoa, hawakuitekeleza amri yake yeyote mbona Ali ibn Abi Talib alikuwa pamoja nao naye hakuitekeleza amri ya Mtume(s.a.w.w) . Mimi niliwajibu kama ifuatavyo:

Kwanza : Ali ibn Abi Talib alikuwa hahesabiwi kuwa ni miongoni mwa Masahaba, bali yeye ni ndugu wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na Ibn Ammi yake Mtume na ni mume wa Binti yake na baba wa watoto wa Mtume. Kwa hakika Ali alikuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu upande mmoja na watu wengine walikuwa upande mwingine, basi mpokezi wa hadithi ndani ya Sahih Bukhari anaposema kwamba Mtume(s.a.w.w) aliwaamuru Masahaba wake kuchinja na kunyoa, basi Abul-Hasan(a.s) hakuhesabiwa kuwa miongoni mwao, kwani yeye yu katika daraja ya Harun kwa Musa. Je, hamuoni kwamba sala ya Mtume haiwi kamili mpaka iongezwe juu yake sala ya kizazi cha Mtume, na Ali ndiyo Bwana (kiongozi) wa kizazi cha Muhammad bila mpinzani yeyote? Hivyo basi Abubakr, Umar, Uthman na Masahaba wote sala zao hazisihi mpaka ndani yake uwemo utajo wa Ali ibn Abi Talib pamoja na Muhammad ibn Abdillah.

Pili : Bila shaka Mtume(s.a.w.w) siku zote alikuwa akimshirikisha nduguye Ali kuhusu mnyama wa kuchinja, kama hali hiyo ilivyotokea katika Hija ya mwisho wakati Ali alipofika kutoka Yemen na Mtume akamuuliza; "Je, umechinja kichinjo gani ewe Ali?" Akasema, "Kile alichochinja Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ." Basi Mtume akamshirikisha katika kichinjo chake. Tukio hili wamelieleza wanahadithi wote na wana historia, basi hapana budi kuwa alikuwa pia mshirika wake siku ya Hudaibiyyah. Tatu: Hapana shaka Ali ndiye alikuwa muandishi wa mapatano siku ya Hudaibiyyah kwa imla ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na hakumpinga Mtume kwa lolote muda wote wa uhai wake, siyo katika munasaba wa Hudaibiyyah wala sehemu nyingine, na Historia haikusajili kwamba yeye Ali (a.s) alipinga amri ya Mtume au kuasi japo mara moja, hapana kabisa hakufanya hivyo na wala hakukimbia hata mara moja kwenye vita na kumuacha nduguye na Ibn Ammi yake katikati ya maadui, bali alikuwa siku zote akijitolea nafsi yake.

Kwa kifupi ni kwamba, Ali ibn Abi Talib yeye ni kama nafsi ya Mtume na ndiyo maana Mtume alikuwa akisema: "Haifai kwa mwingine yeyote kuwa na janaba msikitini isipokuwa mimi na Ali." Wengi wa hao niliokuwa nikijadiliana nao walitosheka kwa maelezo niliyoyaleta na wakakiri kwamba Ali ibn Abi Talib hakwenda kinyume na amri ya Mtume wa Mwenyezi Mungu katika uhai wake. Bukhari ameandika katika Sahihi yake juzuu ya nane, mlango wa Karahiyatul-khilaf Kitabul-i'tisam bil-kitabi Was-Sunnah. Imepokewa kutoka kwa Abdallah ibn Abbas amesema: "Pindi mauti yalipomkabili Mtume(s.a.w.w) alisema, na hali yakuwa nyumbani humo wamo watu, akiwemo Umar ibn Khat-tab, Mtume akasema: Nipeni karatasi na kidawati nikuandikieni maandiko ambayo kamwe hamtapotea baada yake. Umar akasema, Bila shaka Mtume amezidiwa na maradhi, nanyi mnayo Qur'ani, basi kinatutosha Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Wakahitilafiana watu waliokuwemo ndani ya nyumba, na wakazozana, wengine wanasema mpeni Mtume wa Mwenyezi Mungu akuandikieni maandiko ambayo hamtapotea baada yake, na wengine wanasema alivyosema Umar. Walipozidisha hitilafu yao na makelele mbele ya Mtume(s.a.w.w) , Mtume akasema Niondokeeni. Basi Ibn Abbas siku zote akawa husema, Hakika msiba mkubwa kuliko yote ni ule uliopita baina ya Mtume na baina ya kuwaandikia maandiko yale kutokana na hitilafu zao na fujo zao" [7] .

Na hii ni amri nyingine ya Mtume wa Mwenyezi Mungu ambayo Masahaba waliikabili kwa kuipinga na kuiasi na kumtia dosari Mtume(s.a.w.w) . Kwa kuongezea ni kwamba, Umar ibn Khatab alisema mbele ya Mtume(s.a.w.w ) alipowataka wamletee karatasi na kidawati ili awaandikie maandiko ambayo yatawazuwia wasipotee Umar akasema: "Bila shaka Mtume anaweweseka" Mwenyezi Mungu atulinde (kutokana na matamko ya aina hiyo).

Lakini Bukhari aliistahi ibara hiyo na kuibadilisha kuwa "Maradhi yamemzidi" kwa kuwa tu aliyesema ni Umar ibn Khatab. Na utamuona pindi anapolipuuzia jina la Umar ndani ya riwaya hii husema, "Wakasema Mtume wa Mwenyezi Mungu anaweweseka, na huku (kupinda mapokezi ya hadithi) ndiyo uaminifu wa Bukhari katika kunakili hadithi. (Baadaye tutamtengea mlango wake maalum). Kwa hali yoyote ile, wengi wa wanachuoni wa hadithi na wanahistoria wameeleza kuwa, Umar ibn Khatab ndiye aliyesema "Bila shaka Mtume wa Mwenyezi Mungu anaweweseka." Na ndipo Masahaba wengi wakamfuatia wakasema kama alivyosema yeye mbele ya Mtume(s.a.w.w) . Sisi tunajaribu kuiangalia hali halisi ya msimamo huo unaotisha na sauti kali, wingi wa makelele na kuhitilafiana kwao mbele ya Mtume(s.a.w.w) , na iwe kwa namna yoyote ile iliyoelezwa katika riwaya hii, lakini riwaya haielezi ukweli halisi wa jinsi ya tukio namna lilivyokuwa isipokuwa kidogo tu, kama ambavyo tutakaposoma kitabu cha historia kinachoeleza maisha ya Musa (a.s) , kitabu hicho kieleze kwa namna yoyote ile, lakini hakiwezi kufikia ufafanuzi wa filamu ya sinema tunayoishuhudia kwa macho. Bukhari ameandika ndani ya Sahih yake, juzuu ya saba, mlango wa Yanayoruhusiwa miongoni mwa ghadhabu na kuwa mkali kwa ajili ya amri ya Mwenyezi Mungu Kitabul-adab, amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alijenga kijichumba kilichotengenezwa kwa makuti au jamvi, basi Mtume(s.a.w.w) alitoka akaswali mahala hapo watu wakamfuata kisha wakaja usiku mwingine, walipofika Mtume akakawiya hakutoka, wakapaza sauti zao na wakaugonga mlango, (Mtume) akawatokea hali ya kuwa mwenye ghadhabu akawaambia hamukuacha kutenda kitendo chenu mpaka nikadhani kwamba hii itafaradhishwa kwenu, basi nendeni mukaswali majumbani mwenu kwani sala iliyo bora ni ile aswaliyo mtu nyumbani mwake isipokuwa sala ya faradhi" [8] .

Kwa masikitiko makubwa ni kwamba, Umar ibn Khatab alikwenda kinyume na amri ya Mtume(s.a.w.w) na akawakusanya watu kwenye sala ya Sunna katika zama za Ukhalifa wake akasema kwa tendo hilo kuwa, "Hakika hii ni Bid'a na ni Bid'a nzuri. " Kwenye uzushi wake huu, walimfuata Masahaba wengi ambao walikuwa wanayakubali maoni yake na kumuunga mkono kwa kila alifanyalo na alisemalo. Ni Ali ibn Abi Talib na watu wa nyumba yake tu ndiyo waliomkhalifu Umar nao ndio ambao walikuwa hawafanyi isipokuwa kwa mujibu wa maamrisho ya kiongozi wao ambaye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na hawakumkubali mwingine badala yake. Kama ikiwa kila Bid'a ni upotevu na kila upotevu ni motoni, basi unafikiria nini juu ya mambo yaliyozushwa ili kupinga maamuzi ya Mtume(s.a.w.w) ?

Bukhari ameandika katika Sahih yake juzuu ya tano mlango wa Ghaz-watu Zaidi ibn Haritha Kitabul-maghazi. Imepokewa kutoka kwa Ibn Umar (r.a) amesema, "Mtume wa Mwenyezi Mungu alimpa uamirijeshi Usama juu ya watu, lakini wakapinga (Usama) kupewa uamirijeshi, Mtume akasema, Ikiwa mnapinga uamiri wake kwa hakika mlikwishaupinga uamirijeshi wa baba yake kabla yake, namuapa Mwenyezi Mungu hakika baba yake alistahiki mno uamiri na alikuwa ni mtu nimpendaye, na huyu ni miongoni mwa watu niwapendao baada ya baba yake."[9] . Kisa hiki wamekieleza wanahistoria kwa upana, na wameeleza jinsi Mtume wa Mwenyezi Mungu alivyowalaani waliobakia nyuma wasiende kwenye msafara wa Usamah ambaye ni kijana mdogo aliyekuwa hajafikia hata umri wa miaka kumi na saba, na Mtume alimpa uamiri wa jeshi ambalo ndani yake alikuwemo Abubakr, Umar, Talhah, Zubair na Abdur-rahman ibn A'ufi na wakuu wengine wa Kiquraish wote. Lakini katika jeshi hilo Mtume hakumtia humo Ali ibn Abi Talib wala Sahaba yeyote aliyekuwa akimpenda Ali(a.s) .

Kama ilivyo kawaida ya Bukhari, siku zote hufupisha matukio na huzikata hadithi ili kulinda heshima ya viongozi waliopita miongoni mwa Masahaba, pamoja na hali hiyo ndani ya hayo aliyoyaandika yanatosha kwa mwenye kutaka kuifikia haki. Bukhari pia ameandika ndani ya Sahih yake juzuu ya pili mlango wa Onyo kwa anayefululiza kufunga usiku na mchana Kitabus-Saum. Imepokewa kutoka kwa Abuhurairah amesema:"Mtume(s.a.w.w) alikataza kufululiza katika saumu, mtu mmoja miongoni mwa Waislamu akamwambia Mtume, Mbona wewe unafululiza ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Mtume akasema:Nani kati yenu aliye kama mimi? Mimi nikilala Mola wangu hunilisha na kuninywesha. Walipokataa kuacha kufululiza Mtume alifululiza pamoja nao siku moja kisha siku nyingine hatimaye wakauona mwezi, Mtume akasema; Lau (mwezi) ungechelewa ningekuongezeeni. " [10] Hili ni kama onyo kwao walipokataa kuacha kufululiza.

Wakoje Masahaba hawa ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anawakataza kitu hawakataziki na anakariri katazo lake lakini hawasikii. Je, hawakusoma kauli ya Mwenyezi Mungu aliposema:

وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٧﴾

" Anayokupeni Mtume yachukuweni, na anayokukatazeni yaacheni, mcheni Mwenyezi Mungu, hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu. " (Qur'ani, 59:7).

Pamoja na onyo la Mwenyezi Mungu kwa yeyote anayemkhalifu Mtume wake, kuwa (atamuadhibu) adhabu kali, baadhi ya Masahaba hawayapi uzito wowote makemeo na maonyo ya Mwenyezi Mungu.

Iwapo hali yao ndiyo hii, basi hapana shaka juu ya unafiki wao japokuwa walijionesha kuwa wanasali sana, na kufunga na kuwa wakali katika dini mpaka wakafikia daraja ya kuharamisha kukutana na wake zao ili tu wasije kwenda Mina na huku dhakari zao zikidondoka manii, na wakigomea yale ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu anayatenda kama ilivyotangulia katika uchambuzi uliopita. Bukhari ameandika ndani ya Sahih yake juzuu ya tano, mlango wa Mtume kumpeleka Khalid ibn Walid kwa Bani Judhaimah Kitabul-maghazi. lmepokewa kutoka kwa Az-zuhri naye toka kwa Salim nave kapokea kutoka kwa baba yake amesema: "Mtume(s.a.w.w) alimtuma Khalid ibn Walid kwenda kwa Bani Judhaimah, Khalid aliwaita kwenye Uislamu ikawa hawakuweza kutamka vizuri hicho, "Tumesilimu," bali wakawa wanasema, Swaba 'naa, basi Khalid akaanza kuwauwa na kuwateka, na akampa kila mmoja wetu mateka wake kiasi kwamba siku moja Khalidi alimuamuru kila mtu miongoni mwetu amuuwe mateka wake mimi nikasema; Wallahi mimi simuuwi mateka wangu wala mtu yeyote katika jamaa zangu hatamuuwa mateka wake. Tulipofika kwa Mtume na tukamuelezea hali hiyo, alinyanyua mikono yake juu kisha akasema: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika najitakasa kwako kutokana na yale aliyoyatenda Khalid akasema hivyo mara mbili."[11] Wanahistoria wamelielezea tukio hili kwa upana zaidi, na wametaja namna Khalid alivyotenda maasi haya mabaya yeye mwenyewe na wale waliomtii miongoni mwa baadhi ya Masahaba, na hawakufuata maamrisho ya Mtume yanayokataza kumuua mtu yeyote aliyesilimu. Kwa hakika ni maasi makubwa ambayo yalimwaga damu ya watu isiyo na makosa, na hasa kwa kuwa Mtume(s.a.w.w) alimuamuru Khalid awalinganie kwenye Uislamu na hakumuamuru kuwaua. Khalid ibn Walid, ulimzidi ufahari wa zania za kijahiliya (kabla kuja Uislamu) na chuki ya kishetani ikambeba, kwani hawa Bani Judhaimah walipata kumuua ammi yake Khalid aliyekuwa akiitwa Al-Fakih ibn Al-Mughirah katika zama za Kijahiliyyah, ndiyo maana Khalid akawahadaa watu hao akawaambia wekeni silaha zenu chini kwani watu wamekwisha silimu hakuna hatari yoyote ni amani tupu kisha akaamrisha (wakakamatwa) wakafungwa mikono na waliuawa watu wengi miongoni mwao.

Baada ya Masahaba wengi wema kutambua makusudio ya Khalid, walikimbia kutoka kwenye jeshi hilo wakaenda kwa Mtume(s.a.w.w) na wakampa habari zilivyo, Mtume wa Mwenyezi Mungu alijitakasa kutokana na tendo la Khalid, na akamtuma Ali ibn Abi Talib akaenda lipa fidia za damu iliyomwagwa huko na mali iliyoharibiwa. Na ili kulifahamu (vyema) tukio hili kwa ufafanuzi, si vibaya kuyasoma maandiko aliyoyaandika Abbas Mahmud Al-I'qad katika kitabu chake kiitwacho, Abqariyyatu Khalid ukurasa wa 57 na 58 lakini ameeleza kwa njia ya kupotosha maelezo kama ifuatavyo: Baada ya ushindi wa Maka, Mtume alielekeza umuhimu wa kueneza dini kwa kuzisafisha sehemu za majangwani zinazoizunguka Maka kutokana na ibada za masanamu, hivyo basi alituma vikosi kwenda kwenye makabila ya sehemu hizo ili kuyalingania Uislamu na kupata uhakika wa nia za makabila hayo. Miongoni mwa vikosi hivyo ni kile cha Khalid kwenda kwa Bani Judhaimah na kikosi hicho kilikuwa na watu karibu mia tatu na hamsini wakiwemo Muhajirina na Ansari na Bani Sulaim, na Mtume aliwatuma wakalinganie dini wala hakuwaamuru kupigana. Hawa Bani Judhaimah walikuwa ni kitongoji kikali mno zama za Jahiliyyah na wakiitwa kuwa ni "Walamba Damu" na miongoni mwa watu waliouawa na Bani Judhaimah zama hizo ni Alfakihu ibn Al-Mughirah na nduguye ambao wote ni ammi zake Khalid ibn Walid, na wengine waliouawa na Bani Judhaimah ni mzazi wa Abdur-Rahman ibn Auf, na Malik ibn Rashid na nduguze watatu miongoni mwa Bani Sulaim (wote hawa) waliuawa mahala pamoja, na wengine (waliuawa) kutoka makabila mengine mbali mbali.

Khalid ibn Walid alipofika kwa Bani Judhaimah wao walifahamu kuwa miongoni mwa watu waliokuja na Khalid wamo Bani Sulaim, basi wakabeba silaha zao na wakajiandaa kwa vita kisha wakakataa kuteremka kwenye vipando vyao. Khalid akawauliza, "Je, ninyi ni Waislamu?" Inasemekana baadhi yao walimjibu ndiyo, na wengine walimjibu wakasema, "Saba'naa Saba'naa" yaani tumekwisha aacha kuabudu sanamu. Kisha akawauliza, "Nini basi maana ya kubeba kwenu silaha?" Wakasema, "Bila shaka baina yetu na baadhi ya jamaa wa Kiarabu kuna uadui, tumechelea kuwa labda ninyi ndiyo hao hiyo ndiyo sababu ya sisi kuchukua silaha." Basi Khalid akawaambia, "Wekeni silaha chini kwani watu wamekwisha silimu." Mtu mmoja miongoni mwao aitwaye Jahdam akawapigia ukelele wenziwe akasema, "Ole wenu enyi kizazi cha Judhaimah huyo ni Khalid, Wallahi hakuna jambo litakalotokea baada ya kuweka silaha isipokuwa mtatekwa, na hakuna kitakachotokea baada ya kutekwa isipokuwa ni kuuawa, Wallahi mimi kamwe siweki silaha yangu chini." Basi wenziwe waliendelea kumrai mpaka akawa miongoni mwa walioweka silaha zao na wengine wakatawanyika. Hapo ndipo Khalid alipoamuru wakamatwe wakafungwa mikono wakauawa. Bani Sulaim na Waarabu wengine wakamtii Khalid katika mauaji hayo, lakini Muhajirina na Ansari wakamkemea Khalid na kumwambia asimuuwe yeyote isipokuwa iwe imeamuriwa na Mtume(s.a.w.w) kuwa auawe. Hatimaye habari zikamfikia Mtume, basi alinyanyua mikono juu mbinguni na akasema mara tatu; "Ewe Mwenyezi Mungu najitakasa kwako kutokana na matendo aliyoyafanya Khalid ibn Walid" na akamtuma Ali ibn Abi talib aende kwa Banu Judhaimah akalipe fidia ya damu iliyomwagwa na mali zao zilizoharibiwa. Kwa hakika Masahaba wengi wakubwa walichukizwa na tukio hilo, ikiwa ni pamoja na wale waliokuwepo kwenye kikosi hicho na wale ambao hawakuwepo. Abdur-rahman alikasirika sana mpaka akamtuhumu Khalid kwamba aliwauwa jamaa hao kwa makausudi ili alipe kisasi cha ammi zake." Mwisho wa kunukuu maneno ya Al-Iq-Qad.

Basi haya ndiyo aliyoyataja Al-Iqqa'd kwa njia ya kupotosha ndani ya kitabu chake kiitwacho Ab-Qariyatu Khalid. Huyu Al-iqa'ad ni kama walivyo wasomi wengi wa Kisunni, baada ya kukisimulia kisa hiki kwa ukamilifu anatafuta sababu za kupoza na kumpamba Khalid ibn Walid, lakini ni sababu ambazo hazisimami na kuwa dalili za kumtakasa Khalid kutokana na matendo yake, wala akili iliyosalimika haiwezi kuzikubali sababu hizo. Na huyu Al-iqad hana sababu yoyote isipokuwa ni kule kuandika, Abqariyatu Khalid kwa maana ya Ushujaa wa Khalid. Kwani kila alichokileta miongoni mwa sababu ni dhaifu mfano wa nyumba ya buibui na yeyote azisomaye ataona ubovu na unyonge wa utetezi uliomo. Basi vipi anamtetea Khalid hali yakuwa yeye mwenyewe ameshuhudia katika maneno yake kuwa Mtume(s.a.w.w) aliwatuma kwenda kulingania watu na hakuwaamrisha kufanya mauaji, na amekiri kwamba Banu Judhaimah waliweka sialaha zao chini baada ya kuwa walikuwa wamezibeba wakati Khalid alipowahadaa kwa kuwaambia, "Wekeni silaha chini, kwani watu wamekwisha silimu." Amekiri pia kwamba, Jahdam ambaye alikataa kuweka silaha na akawaonya jamaa zake kwamba Khalid atawageuka pale alipowaambia, "Ole wenu huyo ni Khalid, Wallahi hakuna jambo litakalotokea baada ya kuweka silaha zenu isipokuwa kutekwa na hakuna litakalotokea baada ya kutekwa isipokuwa ni kuuawa, Wallahi siweki silaha yangu kamwe." Al-iqad amesema kwamba, Bani Judhaimah hawakuacha kumrai mwenzao mpaka akaweka silaha yake, na kitendo chao hiki kinajulisha juu ya Uislamu wa watu hawa na nia yao njema.

Sasa iwapo Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliwatuma kulingania watu dini na wala hakuwaamuru kuua kama ulivyoshuhudia wewe Iqa'ad, basi Khalid anazo sababu zipi zilizomfanya aende kinyume na amri za Mtume(s.a.w.w) ? Hili ni tatizo sifikirii kama unaweza kulitatua ewe iqa'ad. Na kama watu hawa waliweka silaha zao na wakatangaza Uislamu wao .na wakamzidi jamaa yao aliyekuwa ameapa kutokuweka silaha yake na hatimaye wakamkinaisha kama ulivyo kiri wewe I'qaad, basi ni ipi hiyo sababu iliyomfanya Khalid awafanyie khiana na kuwaua hali kawafunga na hawana hata silaha? Hapana shaka wewe umesema kwamba, "Khalid aliamrisha wafungwe na kuwaelekeza kwenye panga na kuwaua." Hapa umezua tatizo jingine na sikufikiria kwamba unaweza kupata ufumbuzi wake ewe Iqa'ad. Na je, hivi Uislamu umewaamuru Waislamu kuwaua watu ambao hawajawashambulia? Tena kwa kukadiria tu kwamba jamaa hao hawakutangaza Uislamu wao, sivyo kabisa hii ndiyo hoja wanayoitumia Mustashirikina Orientalist Kisha umekiri mara nyingine kwamba Mtume(s.a.w.w) hakumuamuru Khalid kuwaua jamaa hao pale uliposema kwamba: "Muhajirina na Ansari walimkemea Khalid asimuue yeyote isipokuwa iwe ni amri ya Mtume(s.a.w.w) kuwaua." Basi sababu gani uliyonayo ewe Iqa'ad hata umtakase Khalid? Inatosha kuwa ni jibu dhidi ya Iqa'ad ya kwamba yeye amebatilisha sababu zake yeye mwenyewe na kuzipinga zote pale alipokiri kwa kusema: "Na kwa hakika Masahaba wengi wakubwa walichukizwa na tukio hilo, ikiwa ni pamoja na wale waliokuwepo kwenye kikosi hicho na wale ambao hawakuwepo ." Basi iwapo Masahaba wakubwa walishinikiza kumpinga Khalid mpaka wakakimbia kutoka kwenye jeshi lake na wakamshitakia kwa Mtume(s.a.w.w) , na kama Abdur-rahman ibn Auf alimshutumu Khalid kuwa aliwaua jamaa hao kwa makusudi ili alipe kisasi cha ammi zake kama alivyoshuhudia hayo I'qaad, na iwapo Mtume(s.a.w.w) alinyanyua mikono yake juu mbinguni na akasema mara tatu: "Ewe Mwenyezi Mungu, mimi najitakasa kwako kutokana na aliyoyafanya Khalid ibn Walid."

Na (vile vile) kama Mtume(s.a.w.w) alimtuma Ali akiwa na mali ambayo aliitoa fidia kwa damu na mali za Bani Judhaimah zilizoharibiwa mpaka akawaridhisha kama alivyoshuhudia Iqa'ad, hii inajulisha kwamba jamaa hao walisilimu, lakini Khalid aliwadhulumu na kuwashambulia. Sasa je, kuna yeyote mwenye kuuliza amuulize Iqa'ad anayejaribu kumtaksa Khalid kwamba, "Je, yeye Iq a'ad' anajua zaidi kuliko Mtume wa Mwenyezi Mungu ambaye alijitakasa mbele ya Mwenyezi Mungu mara tatu kutokana na vitendo vya Khalid? Au anajua mno kuliko wale Masahaba wakubwa ambao walimkemea Khalid? Au anajua mno kuliko wale Masahaba waliokuwepo kwenye tukio na wakakimbia kutoka kwenye kikosi hicho kutokana na uzito wa yale waliyoyaona miongoni mwa matendo yake mabaya? Au anajua mno kuliko Abdurrahman ibn A'uf ambaye alikuwa pamoja na Khalid katika kikosi hicho, na hapana shaka anamtambua vyema Khalid kuliko Iqa'ad, lakini alimshutumu kwa mauaji ya jamaa hao kwa makusudi ili alipe kisasi cha Ammi zake? Mwenyezi Mungu autokomeze ung'ang'anizi wa kipofu na chuki za kijinga ambavyo vinageuza ukweli. Iwe iwavyo, pamoja na Bukhari kulifupisha tukio hili na kuliandika kwa mistari minne, lakini hicho kidogo alichokiandika kimetosheleza kuufahamu mwenendo wa Khalid na Masahaba wengine ambao walimtii katika mauaji ya Waislamu wasio na hatia, na Iqa'ad amewataja kwa kusema: "Banu Sulaim na wengine miongoni mwa Waarabu aliokuwa nao Khalid, walimtii katika mauaji ya Banu Judhaimah." Lakini Bukhari hawakuwaondoa katika Masahaba waliomtii Khalid ila watu wawili au watatu waliokimbia kutoka katika jeshi na kurudi kwa Mtume na kumshitaki Khalid. Ewe Iqa'ad huwezi kabisa kutukinaisha kwamba Muhajirina na Ansar ambao idadi yao ilikuwa mia tatu na hamsini kama ulivyobainisha hivyo wewe mwenyewe eti hawakumtii Khalid katika mauaji ya jamaa hao, na kuwa walikimbia wote kutoka kwenye jeshi, hili halikubaliki kwa mtafiti yeyote yule. Lakini hilo ni jaribio lako la kulinda heshima ya waliopita miongoni mwa Masahaba na kuufunika ukweli kwa gharama yoyote ile, lakini fahamu kwamba sasa wakati umefika wa kuondoa kifuniko hicho na kuitambua haki.

Huyu Khalid ibn Walid anayo mauaji mengi mabaya aliyoyafanya ambayo historia imetusimulia hasa yale ya siku alipofika Bat-tah wakati Abubakr alipomteua aongoze jeshi kubwa lenye Masahaba wakubwa wakubwa wa mwanzoni. Huko kwa mara nyingine alimfanyia khiyana Malik ibn Nuwairah na watu wake walipoweka silaha zao chini, yeye akafunga mikono kisha wakauawa hali ya kuwa wamefungwa, na kisha Khalid akamuingilia mke wa Malik aliyekuwa akiitwa Laila Ummu Tamim katika usiku ule ule aliouawa mumewe. Umar ibn Khat-tab aliposimama kumrudishia kisasi akamwambia:"Umemuua mtu Muislamu kisha umemuingilia mkewe, Wallahi nitakupiga kwa mawe ewe adui wa Mwenyezi Mungu." Lakini Abubakr alisimama upande wa Khalid kumtetea akamwambia Umar "Mwache Khalid bila shaka yeye amejitahidi akakosea." Na hili ni tukio jingine ambalo kulifafanua inachukua muda na kwa kweli ni halifai hata kulieleza. Basi ni mara ngapi mwenye kudhulumiwa hunyang'anywa haki yake kwa kuwa anayemdhulumu ana nguvu? Na ni mara ngapi dhalimu hutetewa uovu wake kwa kuwa ni tajiri na yu karibu na mtawala?

Basi huyu Bukhari wakati anaeleza kisa cha Banu Judhaimah anakikata na anasema: "Mtume alimpeleka Khalid kwa Banu Judhaimah akawaita kwenye Uislamu, wakashindwa kutamka vizuri kuwa "Tumesilimu, Aslamnaa bali wakawa wanasema; Saba 'anaa, Saba 'anaa " Ewe Bukhari, hawa Banu Judhaimah walikuwa ni Waajemi au walikuwa Waturuki, Wahindi au Wajerumani mpaka wasiweze kusema, "Aslamnaa, yaani Tumesilimu? Au wao ni miongoni mwa Makabila ya Kiarabu ambayo Qur'ani ilishuka kwa lugha yao? Lakini ung'ang'anizi wa kipofu na njama kubwa ambazo zimepita ili tu kuilinda heshima ya Masahaba ndizo zilizomfanya Bukhari aseme maneno kama haya kwa lengo la kumtakasa Khalid ibn Walid. Huu nao ni utata, kwani anasema: "Khalid akawauliza ninyi ni Waislamu?" Kisha I'qaad anasema, "Inasemekana baadhi yao walimjibu ndiyo, na baadhi yao walimjibu, Saba'anaa Saba'naa...

Neno hili Inasemekana linajulisha wazi kwamba watu hawa kina Iqa'ad, Bukhari n..k.. hung'ang'ania kitu ambacho huenda kikawachanganya mawazo watu ili wapate kumtakasa Khalid ibn Walid, kwa kuwa Khalid ibn Walid ndiyo upanga ulio tayari kutumiwa na mtawala, naye ndiye mtetezi wa Ukhalifa wa mabavu ambaye pamoja na wafuasi wake ndiyo watekelezaji wa nguvu zenye kupambana na kila yule ambaye nafsi yake inamuambia kuwa atoke na apinge yote yaliyopitishwa na mashujaa wa Saqifah siku aliyofariki Mtume(s.a.w.w) .