UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI0%

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Vitabu mbali mbali

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

Mwandishi: SHEIKH JA'AFAR SUBHANY
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi:

Matembeleo: 48391
Pakua: 4205

Maelezo zaidi:

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 24 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 48391 / Pakua: 4205
Kiwango Kiwango Kiwango
UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

Mwandishi:
Swahili

17

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

KUMUAPA MWENYEZI MUNGU KWA HAKI YA MAWALII

Miongoni mwa nukta wanazotofautiana Waislamu na Mawahabi ni kwamba, Mawahabi wanadai kuwa, ni haramu kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii, na pia kuapia kisichokuwa Mwenyezi Mungu. Wakati mwingine Mawahabi wanaona kuwa viapo hivi viwili ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu katika Ibada. Katika maelezo yafuatayo tutaisherehesha kwa urefu maudhui hii ili kupata hukmu sahihi ya kisheria.

KUMUAPA MWENYEZI MUNGU KWA HAKI YA MAWALII

Bila shaka Qur'an inawasifu baadhi ya waja wa Mwenyezi Munga inaposema:

الصَّابِرِينَ وَالصَّادِقِينَ وَالْقَانِتِينَ وَالْمُنفِقِينَ وَالْمُسْتَغْفِرِينَ بِالْأَسْحَارِ ﴿١٧﴾

"Wafanyao subira na wasemao kweli na watifu na watoao sadaka na wale wanaoomba msamaha saa zilizo kabla ya alfajiri". Qur'an, 3:17.

Basi lau mtu atasimama katikati ya usiku akasali kwa ajili ya Mola wake rakaa nyingi, kisha akanyenyekea kwa Mwenyezi Mungu huko akisema: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba kwa haki ya wanaokutaka msamaha wakati wa karibu ya al-fajiri, unisamehe dhambi zangu". Itakuwaje basi kauli yake hii tuione kuwa ni shirki katika Ibada? Bila shaka shirki katika Ibada maana yake ni "Kumuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, au ni kumzingatia asiyekuwa Mwenyezi Mungu kuwa ni Mungu na ndiyo chanzo cha matendo ya Kiungu". Ama mahala hapa (tunapopazungumzia) yule mtu anayeswali anamuelekea Mwenyezi Mungu na haombi chochote (kwa mwingine) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu. Basi iwapo tendo hili ni haramu, hapana budi kuwe kuna sababu nyingine isiyokuwa shirki.

Sisi hapa (nia yetu) tunataka kuwaelekeza Mawahabi wafahamu kwamba, Qur'an Tukufu imetaja kipimo na kanuni ili kufafanua na kupambanua baina ya mshirkina katika Ibada na yule mwenye Tauhidi, na kwa kipimo hiki imeweka kizuwizi mbele ya kila tafsiri itayofasiriwa kwa maoni (binafsi) juu ya maana ya "mshirikina." Kipimo hiki ni kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:

وَإِذَا ذُكِرَ اللَّـهُ وَحْدَهُ اشْمَأَزَّتْ قُلُوبُ الَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ بِالْآخِرَةِ وَإِذَا ذُكِرَ الَّذِينَ مِن دُونِهِ إِذَا هُمْ يَسْتَبْشِرُونَ ﴿٤٥﴾

"Na anapotajwa Mwenyezi Mungu peke yake, nyoyo za wale wasioamini Akhera huchukia, na wanapotajwa wale wasiokuwa Mwenyezi Mungu basi wao hufurahi". Qur'an, 39:45.

Na katika aya nyingine Qur'an inawataja waovu ambao ni wale wafanyao shirki inasema:

إِنَّهُمْ كَانُوا إِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا اللَّـهُ يَسْتَكْبِرُونَ ﴿٣٥﴾ وَيَقُولُونَ أَئِنَّا لَتَارِكُو آلِهَتِنَا لِشَاعِرٍ مَّجْنُونٍ ﴿٣٦﴾ بَلْ جَاءَ بِالْحَقِّ وَصَدَّقَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٣٧﴾

"Bila shaka wao walipokuwa wakiambiwa "Hakuna aabudiwaye kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, walikuwa wakipinga na husema je, sisi tuiache Miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu." Qur'an, 37:35-36.

Kwa hiyo basi kwa mujibu wa aya mbili hizi mushrik (mwenye kumshirikisha Mwenyezi Mungu) ni yule ambaye huchukia moyo wake atajwapo Mwenyezi Mungu peke yake, na hufurahi watajwapo Miungu batili, au hupinga upweke wa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Baada ya kipimo hiki cha Qur'an tunajiuliza, "Hivi yule mtu asimamaye katikati ya usiku na akamaliza saa nyingi akifanya Ibada na kuomba na akaswali mbele ya Mwenyezi Mungu kwa ikhlasi na unyenyekevu na akamuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii wake wema na akamuomba Mwenyezi Mungu kupitia kwa waja wake wema..... hivi kweli mtu huyu atakuwa mushrik kwa amali yake hii?! Basi ni kwa namna gani amepinga utajo wa Mwenyezi Mungu na ni vipi amekataa kukiri upweke wa Mwenyezi Mungu Mtukufu (hata aitwe ni mushrik)?!!! Ni kwa nini basi waandishi wa Kiwahabi wanategemea misingi ya kabuni na dalili dhaifu kuliko hata nyumba ya buibui, kisha wanawatuhumu Waislamu kuwa wanafanya shirki halafu wao wakajiona kuwa peke yao ndiyo taifa teule la Mwenyezi Mungu?! Vipi itafaa wawazingatie asilima 99% ya Waislamu kawa ni washirikina na wao wawaone Mawahabi toka Najdi kuwa ndiyo peke yao ni watu wa Tauhidi pamoja na kuyazingatia (maelezo) ya kipimo cha Qur'an? Na je, Mwenyezi Mungu amewapa uwakala Mawahabi wa kuifasiri maana ya shirki kama wapendavyo na waamue kwamba kundi hili ni washirikina wa kundi hili ni la watu wa Tauhidi? Ukweli ulivyo ni kwamba, "Mwenyezi Mungu ameweka kifuniko kwenye nyoyo zao basi wao hawafahamu (kitu)".

AMIRUL-MU'MINIINA (ALl[a.s] NA KUMUAPA MWENYEZI MUNGU KWA HAKI YA MAWALII

Tunaangalia kumuapa Mwenyezi Mungu kama ilivyo katika dua za Mawalii wake watukufu. Kwa mfano: Amirul-Mu'miniina Imam Ali[a.s] anasema katika maombi yake baada ya Sala ya usiku: "Ewe Mwenyezi Mungu mimi ninakuomba kwa heshima ya yule aliyejilinda kwako kutokana na adhabu yako na akazitumainia nguvu zako na akajikinga kwa kivuli chako na akashikamana na kamba yako na hakutegemea ila kwako".[202] Na anasema tena Imam Ali[a.s] katika dua aliyomfundisha Sahaba wake mmoja. "Na kwa haki ya wanaokuomba na wale wanaonyenyekea kwako na wanajilinda kwako na wanaodhalilika mbele yako na kwa haki ya kila mja mwenye kukuabudia katika kila sehemu ya nchi kavu au baharini au mbugani au mlimani, nakuomba maombi ya mtu mwenye shida mno...[203] Hivi kuna kitu gani kingine kisichokuwa kumpwekesha Mwenyezi Mungu ndani ya maombi haya yanayoihimiza roho na kuipeleka kwenye Ibada na kudhalilika mbele ya Mwenyezi Mungu.... Je, kuna matokeo mengine yasiyokuwa ya kuimarisha kumpwekesha Mwenyezi Mungu na (kuonyesha kuwa) hakuna mlinzi ila yeye, na kudhihirisha upendo kwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu na wapenzi wake, jambo ambalo linaonyesha kuwa ni kumuelekea Mwenyezi Mungu katika wakati ule ule?" Na kwa mantiki hii basi, tuhuma ya ukafiri na shirki inayotangazwa na Mawahabi (juu ya jambo hili) kuliko kitu kingine chochote ni lazima ikome.

Na inafaa kuyasoma maudhui haya kwa njia ya mantiki na dalili. Kwa ajili hii ndiyo maana utawaona baadhi ya Mawahabi waadilifu japo kidogo wametatua suala la "kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii", na wanasema kwamba jambo hili ni haramu au makruhu, kinyume cha huyu 'As-san-ani" Wahabi aliyekosa uadilifu ambaye ameyasoza mas-ala haya kwenye shirki. Na sasa basi baada ya kubainika msingi wa mazungumzo ni lazima kusoma maudhui ndani ya eneo la uharamu na karaha na kisha kubainisha dalili iliyo wazi juu ya kusihi kwa jambo hili na kufaa kwake. Kwa hiyo tunasema:

KUTHIBITI KWA KIAPO HIKI NDANI YA UISLAMU

Qadhiya ya kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii imekuja katika hadithi nyingi mutawatiri baadhi yake zimepokewa kwa Mtume[s.a.w.w] na nyingine zimepokewa toka kwa Maimamu wa nyumba ya Mtume[s.a.w.w] . Na kwa mujibu wa hadithi hizi haiwezekani kabisa kusema kwamba ni haramu au karaha kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii. Hebu tazama mifano ya hadithi hizo:

1. Hapo kabla imetangulia ishara kwamba, Mtume[s.a.w.w] alimfundisha kipofu aliyekuja kwa Mtume akimuomba Mtume[s.a.w.w] amuombee Mwenyezi Mungu ili macho yake yarudi. Mtume alimfundisha kipofu yule aseme! "Ewe Mwenyezi Mungu nakuomba na ninaelekea kwako kwa haki ya Mtume wako Muhammad Mtume wa Rehma". [204]

2. Abu Said Al-khudri amepokea toka kwa Mtume[s.a.w.w] dua hii ifuatayo: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi ninakuomba kwa haki yawanaokuomba na ninakuomba kwa haki ya mwendo wangu huu ". [205]

3. Naye Nabii Adam[a.s] alitubia kwa Mwenyezi Mungu akasema:

"Nakuomba kuta haki ya Muhammad unisamehe".[206]

4. Baada ya Mtume[s.a.w.w] kwisha kumzika Bibi Fatma binti Asad ambaye ni mama wa Imam Ali[a.s] , Mtume alimuombea dua mama huyu akasema: "Msamehe mama yangu Fatma binti Asad na uyakunjue makazi yake kwa haki ya Mtume wako na Manabii waliopita kabla yangu.[207] Dua hizi japokuwa hazina lile tamko lenyewe la kiapo, lakini madhumuni yake ni kiapo kwa kuwepo herufi ya "BAA" ambayo ni ya kiapo katika hadithi zote, kwani muombaji asemapoALLAHUMMA INNII AS-ALUKA BIHAQQIS-SAILIINA ALAIKA " maana yake ni, ninakuapa kwa haki yao.

5. Bwana wa mashahidi Imam Hussein bin Ali[a.s] anasema alipokuwa akiomba: "Ewe Mwenyezi Mungu nakuomba kwa haki ya maneno yako, na kwa mafungamano ya enzi yako, na kwa haki ya wakaazi wa mbingu zako na ardhi yako na Manabii wako na Mitume wako, unikubalie (maombi yangu) kwani nimefikwa na jambo zito, basi nakuomba umpe rehma Muhammad na kizazi cha Muhammad na uyawepesishe mambo yangu". Na utakapoiangalia Sahifatu as-Sajadiyah iliyopokelewa toka kwa Imam wa nne katika Maimamu wa nyumba ya Mtume aitwaye Imam Zainul-abidina[a.s] humo utaona viapo vingi sana, na hii ndiyo dalili iliyo bora mno inayoonyesha kusihi kwa aina hii ya kutawassal..... Hebu angalia mifano ifuatayo:

6. Imam Zainul-abidina[a.s] anasema ndani ya dua yake siku ya Arafa "(Ewe Mola) kwa haki ya yule uliyemchagua miongoni mwa viumbe wako, na kwa haki ya yule uliyemteua kwa ajili yako, na kwa haki yake uliyemchagua kutoka miongoni mwa viumbe wako, na uliyemteua kwa ajili ya shani yako, na kwa haki ya yule ambaye umeunganisha kumtii yeye ndiyo kukutii wewe na ni yule ambaye umeunganisha kufanyiwa yeye uadui ni kufanyiwa wewe uadui.[208] .

7. Na wakati Imam Jaafar as-Saadiq alipozuru kaburi Ia Imam Ali[a.s] ambaye ni babu yake, mwishoni mwa ziyara yake aliomba akasema: "Ewe Mwenyezi Mungu nikubalie maombi yangu na upokee sifa ninazokutukuza, na unikutanishe na Mawalii wangu, kwa haki ya Muhammad na Ali na Fatma na Hasan na Husein."[209] Ewe msomaji Mtukufu, aina ya dua kama hizi zilizoshikamana na kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii wake zimekuja kwa wingi mno kutoka kwa Maimamu wa nyumba ya Mtume[s.a.w.w] , wenye ismah, na wala nafasi haitoshi kutaja zaidi ya tulizotangulia kuzitaja. Na dua zote hizi zinajulisha juu ya ruhusa ya kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii wake wema

DALILI ZA MAWAHABI JUU YA KUHARAMISHA

Mawahabi wametaja baadhi ya dalili za kuharamisha kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya Mawalii wake. Dalili hizo ni dhaifu hazifai kutolea hoja wala kutiliwa maanani. Na sasa tunazitaja sambamba na kuzijibu katika maelezo yafuatayo: Dalili ya Kwanza: Mawahabi wanasema: "Wanachuoni wa Kiislamu wameafikiana kwamba, kumuapa Mwenyezi Mungu kwa haki za viumbe wake ni haramu."[210] Jawabu Lake: Maana ya Ijmau ni kuafikiana wanachuoni wa Kiislamu katika zama moja au zama zote juu ya hukumu fulani miongoni mwa hukmu za kisheria. Hii ndiyo Ij-mai, nayo ni hoja ya kisheria kwa Masunni kwa sababu kuafikiana kwa wanachuoni juu ya hukumu fulani ni hoja kwao na ni hoja ya kisheria kwa Mashia kwa kuwa inadhihirisha kuwafikiana na maoni ya Imam aliye Maasum ambaye huwa anaishi miongoni mwa watu, ima akawa haonekani machoni pao au akawa yu waonekana. Sasa hivi hebu tuone je, Ij-mai ya wanachuoni ilithibiti kuharamisha mas-ala haya au hapana? Sisi kwa sasa tunayaacha kwanza maoni ya wanachuoni wa Kishia na yale ya wanachuoni wa Kisunni kuhusu mas-ala haya, na tunatosheka na kutaja fat-wa za Maimamu wa madhehebu manne kisha tunajiuliza; je maimamu wa madh-hebu manne wanayofat-wa inayoharamisha jambo hili?.

Iwapo walitoa fat-wa kuharamisha, basi tunachokitaraji ni watutajie Nassi ya fat-wa hiyo pamoja na kitabu ambacho fat-wa hiyo imo pia nambari ya ukurasa ilipo. Bila shaka vitabu vya Fiqhi na hadithi vya wanachuoni wa Kisunni havikulizungumzia kabisa jambo hili ili tuweze kuufahamu mtazamo wao katika qadhiya hii. Kwa hiyo basi iko wapi hiyo Ij-mai na maafikiano anayoyadai mtunzi wa kitabu kiitwacho "Al-hadiyatus-saniyyah"?!! Hapana shaka kwamba mtu pekee ambaye mtunzi huyu alinakili kutoka kwake uharamu wa jambo hili ni mtu "Maj-hul" asiyefahamika hali yake, asiye na utajo wowote anayeitwa "Al-izzu bin Abdis-salaam", basi je vitabu vyote vya wanachuoni wa Kiislamu vimo ndani ya maandiko yaliyomo katika kitabu kiitwacho Al-hadiyatus-saniyyah? Na je, wanachuoni wote wa Kiislamu wamo ndani ya huyu Al-izzu bin Abdus-salaam? Ukweli ulivyo ni kwamba yeye mwenyewe mtunzi wa kitabu hiki "Al-hadiyyatus-saniyyah" amesema ndani ya kitabu hiki kwamba, Abu Hanifa na mwanafunzi wake aliyekuwa akiitwa Abu Yusuf wametoa fat-wa kwamba ni karaha kuapa kwa haki ya viumbe lakini hawakuharamisha.

Baada ya hapo, je ina nafasi gani fat-wa ya mtu fulani mbele ya hadithi sahihi zilizopokelewa toka kwa Mtume[s.a.w.w] na Maimamu watukufu toka katika kizazi cha Mtume[s.a.w.w] ambao wanachuoni wa Kisunni wamekubaliana kuwa (Maimamu hao ndiyo kile kizito kidogo baada ya Qur'an na maneno yao ni hoja ya kisheria). Hadithi ya vizito viwili ni Mutawatiri toka kwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] na wameitaja wana sihahi na sunan na wanahadithi na wanahistoria, na hawezi kuipinga isipokuwa mjinga na hadithi yenyewe ni hii: Amesema Mjumbe wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] : "Hakika ninakuachieni vizito viwili, Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Kizazi changu watu wa nyumba yangu, ambavyo nikishikamana navyo hamtapotea baada yangu milele; na kwamba viwili hivyo havitaachana mpaka vinifikie kwenye haudh, basi angalieni ni vipi mtanifuata katika viwili hivyo." Zaidi ya hapo maelezo aliyoyataja mtunzi huyo toka kwa Abu Hanifa hayakuthibiti. Kwa kifupi tunasema, "Hakuna dalili yoyote ile ya Ij-mai juu ya mas-ala haya moja kwa moja."

Dalili Ya Pili: Baada ya kuibatilisha dalili ya kwanza ya Mawahabi na kubainisha kutokusihi kwa dalili hiyo, sasa tunataja dalili yao ya pili nayo ni kauli ya mmoja wao anasema: "Kwa hakika kuomba kwa haki ya viumbe haifai, kwani viumbe hawana haki juu ya Muumba."[211] Jawabu Lake: Bila shaka kutoa ushahidi kama huu ni ijtihadi dhidi "Nassi" iliyo wazi, basi lau viumbe wasingekuwa na haki yoyote katika dhimma ya Muumba mtukufu, ni kwa nini basi Nabii Adam[a.s] na Mtume Muhammad[s.a.w.w] walimuapa Mwenyezi Mungu kwa haki hizi (za viumbe) na walimuomba Mwenyezi Mungu kwa sababu ya haki hizi kama ilivyokuja katika hadithi zilizotangulia?!! Zaidi ya hapo, wanasemaje watu hawa (Mawahabi) juu ya aya za Qur'an ambazo zinathibitisha haki za waja wema wa Mwenyezi Mungu juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu."[212] Pia watasemaje jun ya hadithi tukufu zinazothibitisha haki hizo? Soma aya zifuatazo:

1. "Na ni haki juu yetu kuwanusuru wenye kuamini" Qur'an, 30:47.

2. "Hii ndiyo ahadi na haki juu ya Mwenyezi Mungu ndani ya Taurati na Injili". Qur'an, 9:111.

3. "Namna hii, ni haki juu yetu kuwaokoa walioamini". Qur'an, 10:103.

4. "Kukubali toba ni juu ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya wale wanaofanya uovu kwa ujinga". Qur'an, 4:17. Kwa kuongezea juu ya aya zilizotangulia kuna hadithi nyingi zinazohusu jambo hili, na hebu ona mifano ifuatayo:

1) "Ni haki juu ya Mwenyezi Mungu kumsaidia aliyeowa kwa kutaka kujizuwiya na mambo aliyoyaharamisha Mwenyezi Mungu".[213]

2) Mtume[s.a.w.w] amesema: "Watu wa aina tatu ni haki juu ya Mwenyezi Mungu kuwasaidia, mpiganaji katika njia ya Mwenyezi Mungu, na Mtumwa mwenye kutaka kujikomboa, na mwenye kuoawa kwa kutaka kujizuwiya kutenda maovu ". [214]

3) "Je, unafahamu ni ipi haki ya waja waliyonayo juu ya Mwenyezi Mungu"?[215] Naam,.... inaeleweka wazi kwamba hakuna yeyote ambaye kwa dhati yake anayo haki juu ya Mwenyezi Mungu, hata kama atamuabudu Mwenyezi Mungu kwa muda wa karne nyingi hali ya kumkhofu na kumnyenyekea Mwenyezi Mungu, kwani kila alichonacho mja, kimetoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, hakuna alichokitoa mja yeye mwenyewe kwa nafsi yake katika njia ya Mwenyezi Mungu eti ili astahiki kwa dhati yake kupewa thawabu. Basi tunauliza, nini maana ya "haki". Jawabu: Hakika makusudio ya haki katika Ibara hizi, ni malipo, na daraja ambavyo Mwenyezi Mungu huwapa waja wake wanapomtii na kumfuata yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu, na haya yote ni ziyada na ubora na umuhimu autoao Mwenyezi Mungu (kwa waja wake), na hii inaonyesha upole (huruma) na utukufu wake. Basi haki hii ambayo kwayo tunamuapa Mwenyezi Mungu ni haki aliyoiweka yeye Mwenyezi Mungu juu yake siyo kwamba mja anayo haki juu ya Mwenyezi Mungu, na maana hii imeelekezwa katika baadhi ya hadithi tukufu za Mtume[s.a.w.w] . Na hii ni kama karadha anayowakopa Mwenyezi Mungu waja wake aliposema, "Nani atakayemkopesha Mwenyezi Mungu kopesho zuri. " Qur'an, 2:245.

Kwa hakika utendaji huu wa Mola na kutoa haki kwa waja wake unatokana na huruma yake Mwenyezi Mungu na uangalizi wake mkubwa kwa waja wake wema kiasi cha kujiona dhati yake tukufu kuwa ni yenye kudaiwa na waja wake na anawaona waja wake kuwa ndiyo wenye haki juu yake. Na ndani ya hali hii (iliyopo baina ya Mwenyezi Mungu na waja wake) inahamasisha na kutia nguvu ya kumtii Mwenyezi Mungu jambo ambalo liko wazi.

KUMUAPIA ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU MTUKUFU

Kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni miongoni mwa mambo ambayo Mawahabi wana uchungu nayo sana na ni katika mas-ala ambayo wao wanayakemea na kuyapigia kelele kwa kutumia kalamu zao potofu. Mwandishi wa Kiwahabi aitwaye As-San-Ani, yeye kwa mawazo yake anaona kuwa kumuapia asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni shirki!![216] Vile vile mtunzi wa Kitabu kiitwacho 'Al-Hadiyyatus-Saniyya, yeye kwa mawazo yake anaona kuwa (kumuapia asiyekuwa Mwenyezi Mungu) ni shirki ndogo.[217]

DALILI ZINAZORUHUSU KUMUAPIA ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU

Dalili Ya Kwanza: Bila shaka Qur'an ndicho kile kizito kikubwa na ndicho kiongozi cha juu na ndiyo kiigizo hai kwa kila Muislamu. Ndani yake utaona viapo vingi katika mahali pengi vya kumuapia asiyekuwa Mwenyezi Mungu kiasi kwamba kuvitaja kwa uchambuzi kutapelekea kurefusha uchambuzi wa maudhui hii. Kwa mfano: Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Surat As-Shamsi peke yake ameapa kwa vitu vinane vikiwa ni miongoni mwa viumbe vyake. Vitu hivyo ni: Jua, Mwanga wa Jua, Mwezi, Mchana, Usiku, Mbingu, Ardhi na nafsi ya mtu. Qur'an, 91:1-7. Kama ambavyo Mwenyezi Mungu katika Surat "An-Naziat" ameapia vitu vitatu, na akaapa kwa vitu viwili katika Surat "Al-Mursalat" na pia vimekuja viapo kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu katika Surat "At-Tariq", "Al-Qalam" "Al-Asr", na "Al-Balad". Qur'an, 79:1-3 na 77:1-3. Hebu angalia mifano ya aya za kiapo cha kumuapia asiyekuwa Mwenyezi Mungu ndani ya Sura zingine (zaidi ya tulizozitaja hapo juu). "Naapa kwa (Miti Ya) Tini na Zaituni, na kwa Mlima Sinai, na kwa Mji huu wenye Amani". Qur'an, 95.1-3.

"Naapa kwa usiku ufunikapo, na kwa mchana uangazapo ". Qur'an, 96:1-2. "Naapa kwa Al-Fajri, na kwa masiku kumi, na kwa Shafaa na Witri na kwa usiku unapopita ". Qur'an, 89:1-4.

وَالطُّورِ ﴿١﴾ وَكِتَابٍ مَّسْطُورٍ ﴿٢﴾ فِي رَقٍّ مَّنشُورٍ ﴿٣﴾ وَالْبَيْتِ الْمَعْمُورِ ﴿٤﴾ وَالسَّقْفِ الْمَرْفُوعِ ﴿٥﴾ وَالْبَحْرِ الْمَسْجُورِ ﴿٦﴾

"Naapa kwa Mlima, na kwa Kitabu kilichoandikwa katika karatasi ya ngozi kikakunjuliwa, na kwa nyumba inayozuriwa, na kwa sakafu (mbingu) iliyonyanyuliwa, na kwa bahari zilizojazwa (maji). Qur'an, 52:1-6.

لَعَمْرُكَ إِنَّهُمْ لَفِي سَكْرَتِهِمْ يَعْمَهُونَ ﴿٧٢﴾

"Naapa kwa uhai wako, bila shaka wao wako katika upofu wanahangaika". Qur'an, 15:72.

Basi ni vipi itafaa kuhukumu kwamba kuapia kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni shirki na ni haramu, hali ya kuwa kuna aya nyingi za Qur'an zimelitaja jambo hilo?

Ikiwa mtu atasema, "Kiapo hiki kinamuhusu Mwenyezi Mungu peke yake".

Jawabu: Sivyo kabisa, bila shaka Qur'an ni Kitabu cha muongozo kwa watu, na watu wanakichukulia kuwa ni kiigizo cha kufuata, basi lau ingekuwa aina hii ya kiapo ni haramu kwa waja wa Mwenyezi Mungu, Qur'an ingelazimika kuhadharisha kwamba kiapo hiki ni miongoni mwa mambo yanayomuhusu Mwenyezi Mungu. Na ilipokuwa tahadhari hii haikutajwa, basi imekuwa ni dalili ya kutokuhusika kwa kiapo hiki kwa Mwenyezi Mungu peke yake. Wako baadhi ya watu miongoni mwa wale wasiojua malengo ya Qur'an wanasema kwamba "Inawezekana kuwa jambo litokalo kwa Mwenyezi Mungu likawa zuri, na jambo hilo hilo likafanywa na mwingine likawa baya". Jawabu la madai haya liko wazi, kwani kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu lau ingekuwa ni shirki na ni kumshabihisha kwa Mwenyezi Mungu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, basi ni kwa nini shirki hii hii (ndogo au kubwa) imetoka kwake Mwenyezi Mungu? Je, Hivi inasihi kwa Mwenyezi Mungu yeye mwenyewe kujiwekea mshirika na akamkataza mwingine kufanya shirki kama hii? Dalili Ya Pili: Mtume[s.a.w.w] aliapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu katika mahala pengi. Miongoni mwake ni:

1. Muslim katika Sahihi yake amepokea (hadithi ifuatayo). Kuna mtu fulani alikuja kwa Mtume[s.a.w.w] akasema, "Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu ni sadaka gani yenye malipo makubwa"? Mtume akasema, "Amma naapa kwa baba yako, wewe ni lazima utapewa khabari yake nayo ni kwamba wewe unatoa sadaka wakati wewe ni mzima na unaipenda mali, unaogopa ufakiri na unatarajia kuendelea kuishi."[218]

2. Muslim amepokea tena (hadithi ifuatayo): "Kuna mtu fulani kutoka Najdi, alikuja kwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] akitaka kuufahamu Uislamu, Mtume[s.a.w.w] akasema: "Ni Kusali Sala tano kila siku." Yule mtu akasema; Je, kuna wajibu juu yangu zaidi ya Sala tano? Mtume akasema: Hapana, isipokuwa ukitaka kufanya Sunna na ufunge mwezi wa Ramadhani". Yule mtu akasema: Ninawajibu mwingine juu yangu zaidi ya huu? Mtume akasema: "Hapana, isipokuwa ukifunga Sunna na Mtume akamtajia mtu huyo Zaka". Yule mtu akasema: "Kuna wajibu juu yangu zaidi ya huu"? Mtume akasema: "Hapana, isipokuwa ukitaka kufanya Sunna". Yule mtu aliondoka huku akisema, "Namuapa Mwenyezi Mungu sintazidisha zaidi ya hivi (nilivyofundishwa) wala sintapunguza." Mjumbe wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] akasema, "Naapa kwa Baba yake, kama anasema kweli, basi amefaulu". Au alisema, "Naapa kwa Baba yake, kama anasema kweli ataingia Peponi." [219]

3. Hadithi hii (Tuliyoitaja) imekuja pia katika Musnad ya Ahmad bin Hanbal na mwishoni mwa hadithi hii katika Musnad ya Ahmad imekuja kwamba Mtume[s.a.w.w] . alimwambia yule mtu, "Naapa kwa maisha yangu, ikiwa utaamrisha mema na kukataza maovu ni bora kuliko kukaa kimya".[220] Na kuna hadithi nyingine ambazo nafasi ya kitabu haitoshelezi kuzitaja.[221] Naye Amirul-Mu'miniina Ali Ibn Abi Talib[a.s] ambaye anazingatiwa kuwa ni mfano ulio wazi wa malezi ya Kiislamu na uongozi mtukufu, aliapia nafsi yake tukufu zaidi ya mara moja katika khutba zake na barua zake na maneno yake.[222] Vile vile Bwana Abubakr bin Abi Qahafah aliapa kwa baba wa mtu aliyekuwa akizungumza naye.[223]

KUAPA KWA ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU KATIKA MADHEHEBU MANNE

Kabla hatujaleta dalili za Mawahabi zinazoharamisha kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, ni bora tukaleta fat-wa za Maimamu wa madhehebu manne kuhusu mas-ala haya. Kwa ufafanuzi zaidi unaweza kurejea kitabu kiitwacho "Al-Fiq-hu Alal-Madhahibil-Ar-Baa", mlango wa kiapo Juz. 1, uk. 75 Chapa ya Misri. Ama Madh-hebu ya Kihanafi, wao wanasema kwamba, "Kuapia baba na uhai kama vile mtu akasema, "Naapa kwa baba yako, au akasema, naapa kwa uhai wako" na mfano wa viapo hivi, jambo hili ni karaha (makruhu). Nao Mashafii wao wanasema kwamba; "Kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, ikiwa si kwa itikadi ya shirki, basi jambo hili ni makruhu." Ama madhehebu ya Kimaliki, wao wanasema, "Bila shaka kuapia vitu vitukufu na vyenye heshima, kama Nabii na Al-Kaaba, kuna kauli mbili, haramu na karaha." Lakini iliyo mashuhuri baina yao (wenye Madhehebu ya Malik) ni haramu.

Na kwa upande wa Madh-hebu ya Hanbal wao wanasema kwamba, kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu na sifa zake ni haramu hata kama kiapo hicho kitakuwa ni kuapia Manabii au mmoja wa Mawalii wa Mwenyezi Mungu. Hizi ndizo fat-wa za Maimamu wa madh-hebu manne. Nasi sasa hivi hatuko katika msimamo wa kujadiliana na wale wasemao kuwa ni Haramu (kuapa kwa asiye Mwenyezi Mungu). (Tunachoweza kusema) ni kwamba fat-wa zao ni jitihada yao dhidi ya nassi ya Qur'an na Sunna ya Mtume[s.a.w.w] na sera ya Mawalii wa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kadhalika wanachuoni wa madhehebu haya wameufunga mlango wa Ijtihadi kwao wao kwa hiyo wakajikuta wamelazimika kufuata maoni ya wale Maimamu wanne peke yao. Sisi hatuyaamini maneno waliyonasibishiwa Maimamu hao juu ya mas-ala haya, kwani AI-Qastalani amesema kuwa, "Imam Malik bin Anas alikuwa akisema kuwa ni karaha kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu".[224]

Pia kuwanasibishia Madh-hebu ya Hanbal kuwa wanasema ni haramu haikuthibiti vile vile kwa sababu, Ibn Qud-damah anaeleza katika kitabu kiitwacho "Al-Mughni" alichokiandika ili kuihuisha Fiqhi ya Kihanbal anasema, "Ahmad bin Hanbal ametoa fat-wa kuwa inafaa kuapia kwa Mtume[s.a.w.w] , na kwamba kiapo kinathibiti kwa kuwa Mtume ni moja ya nguzo mbili za shahada. Na amesema Ahmad bin Hanbal: "Lau (Mtu) ataapa kwa kumuapia Mtume, kiapo chake kitathibiti na kama hatatekeleza kiapo chake basi itamlazimu kutoa kafara". Pamoja na kauli zilizo tangulia, haiwezi kuthibitika moja kwa moja kuwa Maimamu wa madhehebu haya manne wametoa Fat-wa kuharamisha kuapia kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Ewe msomaji mpendwa, baada ya kuzichunguza fat-wa za Maimamu wa madh-hebu manne, sasa tunahamia kwenye kutaja hadithi mbili ambazo Mawahabi wamezishikilia katika kuharamisha kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na kwa kutumia hadithi hizo, Mawahabi wamemwaga damu ya watu wasiyokuwa na makosa na kuwashambulia mimilioni ya Waislamu kwa kuwakufurisha. Kwa hakika Mawahabi waliushambulia mara mbili mji mtakatifu wa Karbala, moja ya mashambulizi hayo lilikuwa mwaka 1216 A.H. na jingine mwaka 1259 A.H., na hawakumhurumia mdogo wala mkubwa kiasi kwamba waliwauwa Waislamu elfu sita katika muda wa siku tatu tu, na walipora kila kitu cha thamani kubwa kichokuwa katika Haram Tukufu ya Imam Husein, na tendo lao hili ni la kufuata nyayo za matendo yaliyofanywa na majeshi ya Yazid Ibn Muawiyah wakati yalipoushambulia mji wa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] . Lakini ni kwa nini? Ni kwa nini basi kufanya mashambulizi haya yenye chuki?

Sababu yake ni kuwa, Waislamu hawa walikuwa wakimuapa Mwenyezi Mungu kwa haki ya watoto wa Mtume[s.a.w.w] na wakiwapenda.

Hadithi ya Kwanza: Hakika mjumbe wa Mwenyezi Mungu alimsikia Omar akisema, "Namuapa baba yangu". Mtume akamwambia, "Hakika Mwenyezi Mungu anakukatazeni kuapa kwa baba zenu, basi kama kuna yeyote mwenye kuapa na amuape Mwenyezi Mungu au anyamaze (asiape)".[225]

Jawabu : Kwanza, huenda katazo la kuwaapa wazazi (wao) lilikuja kwa sababu wazee hao wengi wao walikuwa ni washirikina waliokuwa wakiabudu masanamu, kwa hiyo hawana ubora wala utukufu kiasi cha kuweza yeyote yule kuwaapia. Na bila shaka kuna hadithi imekuja kutoka kwa Mtume[s.a.w.w] kwamba: "Musiapie kwa wazee wenu wala kwa masanamu".[226] Na imepokelewa vile vile kwamba: "Musiapie kwa Baba zenu wala mama zenu wala kwa miungu."[227]

Pili: Makusudio ya katazo la kuapa kwa baba, (Mtume alipokataza kuapa kwa baba makusudio yake) ilikuwa ni kile kiapo ambacho kinatumika katika hukumu ya kesi ili kuondoa kutokuelewana na uhasama kwani wanachuoni wa Uislamu wanaafikiana kwamba, kiapo ambacho kinatumika kwa ajili ya kuondosha kutoelewana na ugomvi ni kuapa kwa Mwenyezi Mungu na sifa zake, ama kiapo kingine hiki hakiingii mahala hapa. Pamoja na kuwepo kwa Qarina hizi zilizowazi..... Basi vipi itawezekana kusema kwamba Mtume[s.a.w.w] alikataza kuapia kwa vitu vitakatifu kama vile Al-Kaaba na Qur'an na Mawalii wa Mwenyezi Mungu hali ya kuwa tunafahamu kwamba katazo lilikuwa linahusu mahali maalum na Mtume mwenyewe alikuwa akiapia vitu visivyokuwa Mwenyezi Mungu? Hadithi ya Pili: Ibn Omar aliijiwa na mtu mmoja akamwambia, "Je, Niapie Al-Kaaba"? Ibnu Omar akamwambia yule mtu, "Hapana (usiapie Al-Kaaba) lakini apa kwa Mola wa al-Kaaba, kwani Omar alikuwa akiapa kwa baba yake na Mtume akamwambia, usiapie kwa baba yako kwani yeyote mwenye kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu bila shaka atakuwa amefanya shirki".[228]

Jibu La Kwanza: Bila shaka hadithi hii imefungamana na mambo matatu:

1. Mtu aliyekuja kwa Ibn Omar akasema niape kwa al-Kaaba? Akamjibu kwa kusema, hapana, lakini apa kwa Mola wa Al-Kaaba.

2. Omar bin Khatab alikuwa akiapa kwa baba yake, Mtume[s.a.w.w] akamkataza kufanya hivyo.

3. Mtume[s.a.w.w] . alibaimsha ubaya wa kufanya hivyo kuta kusema "Yeyote atayeapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu atakuwa kafanya shirki".

Kiapo chenye uhakika katika hadithi hiyo kama yalivyokuja maneno ya Mtume[s.a.w.w] ni kuwa, iwapo kinachoapiwa siyo katika vitu vitakatifu kama vile kafiri na sanamu.

Lakini Ibn Omar alifanya Ij-tihadi kwa kusema kuwa, kauli ya Mtume isemayo "Yeyote mwenye kuapa kwa asiye Mwenyezi Mungu atakuwa kafanya shirki" ambayo aliisema kutokana na kuapiwa kwa mshirkina ambaye ni Khattab mzazi wa Omar, Ibn Omar alijitahidi (kutoa maoni yake) kuwa eti kauli hiyo ya Mtume inakusanya pia kuapa kwa vitu vitakatifu, kama vile al-Kaaba, hali ya kuwa anafahamu kuwa maneno ya Mtume[s.a.w.w] yalikuja kutokana na kiapo cha kumuapia mshirkina kama tulivyofafanua wakati tukiichambua ile hadithi iliyotangulia. Kwa hiyo basi maneno ya Mtume[s.a.w.w] yalikuwa katika kanuni maalumu aliyoiweka kwamba, ikiwa kinachoapiwa ni kitu kisichokuwa kitakatifu. Lakini Ibn Omar alifanya Ij-tihadi akayafanya maneno ya Mtume kuwa yanakusanya zaidi ya maana hiyo. Na Ij-tihad yake hiyo ni hoja juu yake mwenyewe na siyo juu ya mwingine.

Bila shaka hapo kabla tumefafanua ya kwamba, Mtume[s.a.w.w] alikuwa akiapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu mara nyingi tu. Basi inapasa tuichukue kauli yake isemayo; "Yeyote mwenye kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu atakuwa kafanya shirki" iwe kwa maana ya kuapia kwa mshirikina na mfano wake, na siyo kwa maana ya kuapia vitu vitukufu kama vile Qur'an na al Kaaba na Mtume. Na hii itakuja kutokana na dalili kwamba Mtume aliweka kanuni hii wakati Omar alipoapa kwa baba yake ambaye ni mshirikina. Ibn Omar alipoieneza hadithi hii na kuingiza kuapa kwa asiyekuwa mshirikina hiyo in ij-tihadi yake mwenyewe bila ya dalili. (Pengine) utauliza: Ni kwa nini Mtume[s.a.w.w] aliona kuwa kuapia kwa mshirikina ni shirki? Jawabu Lake: Ni kwamba, kuapa kwa mshirikina ni miongoni mwa aina za kumpa nguvu mshirkina na kumtukuza na kuithibitisha dini yake na itikadi yake potofu.

Kwa kifupi sisi tunaikubali asili ya hadithi lakini hatukubali Ij-tihad ya Ibn Omar kutokana na yeye kwenda kinyume na Sunna ya Mtume[s.a.w.w] na sera ya Masahaba. Kanuni iliyotajwa ndani ya hadithi ya Mtume Mtukufu[s.a.w.w] inahusu kile alichokiapia Omar, wala haikusanyi kamwe vitu vitukufu vya Kiislamu. Na ama kuapia Al-Kaaba na Qur'an na Manabii na Mawalii mahala pasipokuwa na kesi na hukumu zake jambo hilo liko nje ya kanuni hiyo ya ujumla, na siyo shirki wala haramu. Jawabu la Pili: Hapa kuna Jawabu jingine lililo wazi zaidi kuliko lile la kwanza, nalo ni lifuatalo): Bila shaka kauli ya Mtume[s.a.w.w] aliposema: "Yeyote atakayeapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu basi atakuwa kafanya shiriki". Inaashira kiapo maalum tu nacho ni kuapia masanamu kama vile lata na uzza (miungu iliyokuwa ikiabudiwa na Maquraishi) wala hakimuingizi mtu mshirikina licha ya vitu vitukufu. Jawabu hili, linaungwa mkono na hadithi aliyoipokea An-Nasai ndani ya Sunan yake kwamba, Mtume[s.a.w.w] amesema: "Yeyote atakayeapa akasema katika kiapo chake, Naapa kwa Lata na Uzza, basi mtu huyu na (Atoe Shahada) aseme; "La illaha Ila-llahu." [229] Pia hadithi aliyoipokea ndani ya kitabu hicho hicho kwamba Mtume[s.a.w.w] amesema: "Msiape kwa baba zenu wala mama zenu wala kwa miungu". Bila shaka hadithi ya kwanza inajulisha kuwa, itikadi za Kijahiliya zilikuwa zimeacha mabaki yake katika baadhi ya nafsi za watu, basi wakawa huapia Masanamu yao waliyokuwa wakiyaabudu kinyume cha Mwenyezi Mungu, ndipo Mtume[s.a.w.w] akawaamuru kusema "La illaha ila llahu" ili kuondosha mabaki hayo ya itikadi za Kijahiliyya.

Na yale mapokezi yaliyopokelewa na Imam wa Mahanbali yanafahamisha kuwa kauli yake Mtume[s.a.w.w] isemayo, "Yeyote atakayeapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu basi atakuwa kafanya shirki". Hadithi iko peke yake tu. Baadaye akaja huyu Ibn Omar akaingiza Ij-tihadi yake binafsi kwamba, kiapo (kilichotajwa katika hadithi) kinakusanya kiapo cha kumuapia baba na vitu vitakatifu. Lakini (kwa mujibu wa hadithi hiyo) kuapia kwa wazazi na vitu vitakatifu havikuwemo ndani ya hadithi hiyo, na aliyeviingiza humo ni Ibn Omar. Ile hadithi aliyoipokea Imam wa Madh-hebu ya Hanbal ni hii ifuatayo: Imepokewa kutoka kwa Ibn Omar amesema, Baba yangu alikuwa akiapa, Mtume akamkataza akasema; "Yeyote atakayeapa kwa asiye Mwenyezi Mungu basi atakuwa kafanya shirki". Bila shaka unaiona hadithi ya Mtume[s.a.w.w] imepwekeka kutokana na maneno ya Ibn Omar na haikuja na Waw ya Atfu au Fau ya Tafrigh, bali amesema; "Fanahahun-Nabiyyu" (Yaani Mtume akamkataza) akasema: Jambo ambalo linajulisha kwamba hadithi hii ilitoka katika wakati mwingine na haikuwa na nyongeza yoyote.

Ewe msomaji mpendwa mukhtasari wa maelezo yaliyomo ndani ya mlango huu tulioeleza uko kama ifuatavyo:

1. Kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu hapana kizuwizi chochote kishera, na kiapo hicho kimeanzia kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu ndani ya Qur'an Tukufu na Mtume wa Mwenyezi Mungu[s.a.w.w] na pia Khalifa wa Mtume Amirul-Mu'minina Ali[a.s] na Waislamu.

2. Kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu si sahihi (Lakini hutusemi haijuzu), si sahihi katika hukumu na kesi, bali ni lazima kumuapa Mwenyezi Mungu au kuapa kwa moja ya sifa zake ambazo ndizo dhati yake tukufu, na hili limethibiti kwa dalili maalum wala halina uhusiano katika uchunguzi huu. Bila shaka hadithi mbili ambazo Mawahabi wapotofu wamezitolea dalili juu ya kuharamisha kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, hazina uhusiano na kile ambacho sisi tunakizungumzia yaani kuapa kwa vitu vitukufu vya Kiislamu kama Qur'an, al-Kaaba, Manabii, Maimamu na Mawalii, bali hadithi hizo zinahusu kuapia mambo yasiyokuwa matukufu kama vile wazazi washirikina na masanamu yaliyokuwa yakiabudiwa zama za jahiliya. Namna hi kwa maelezo haya kile kifuniko cha Uislamu walichokivunja Mawahabi wapotovu kinaondoka, kifuniko ambacho hukivalisha ule mtazamo wao wa kipekee na fikra zao potofu. Sifa zote njema Anastahiki Mwenyezi Mungu.