UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI0%

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Vitabu mbali mbali

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

Mwandishi: SHEIKH JA'AFAR SUBHANY
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi:

Matembeleo: 48431
Pakua: 4221

Maelezo zaidi:

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 24 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 48431 / Pakua: 4221
Kiwango Kiwango Kiwango
UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

Mwandishi:
Swahili

8

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

KUSWALI NA KUOMBA DUA KWENYE MAKABURI YA MAWALII

Miongoni mwa mambo ambayo Mawahabi wanayapigia kelele katika vitabu vyao na sehemu nyingine ni kuswali na kuomba dua kwenye makaburi ya Mawalii wa Mwenyezi Mungu, pia kuwasha taa katika sehemu hizo. Muanzilishi wa Uwahabi anasema katika moja ya risala zake iitwayo "Ziyaratul-Qubur" kama ifuatavyo: "Hakuna Imamu yeyote miongoni mwa Maimamu waliyotangulia aliyetaja kwamba, kuswali makaburini na kwenye maziyara ni jambo la Sunna, na wala kuswali na kuomba katika sehemu hizo kuwa ni bora, bali Maimamu wote wameafikiana kuwa, kuswali misikitini na majumbani ndiyo bora kuliko kuswali kwenye makaburi ya Mawalii na Wachamungu".[98] Na vile vile yamekuja maelezo yanayonasibishwa kuwa ni jawabu lililotolewa na wanachuoni wa Madina kama ifuatavyo: "Ama kukielekea chumba alichozikwa Mtume wakati wa kuomba dua, kilicho bora ni kulizuwia tendo hili, kama inavyoeleweka katika vitabu vya Madhehebu vinavyotegemewa, kwani upande uliyo bora kuelekewa ni upande wa Qibla". Jambo hili limevuka mpaka, kutoka kwenye kiwango cha wao Mawahabi kulizuwiya, mpaka kwenye kiwango cha kuwa ni shirki, kiasi kwamba leo hii wanalizingatia kuwa ni shirki na kila alitendaye kuwa ni mushriki. Bila shaka ni kwamba, kuswali kwa ajili ya huyo mwenye kaburi na kumuabudia au kumfanya yeye ndiyo Qibla katika swala itakuwa ni shiriki moja kwa moja.

Lakini ifahamike kwamba, hapa duniani hakuna Muislamu anayefanya namna hii kwenye makaburi ya Mitume na Mawalii, na hakuna anayemuabudia aliyezikwa hapo au kumuelekea katika sala. Kwa hiyo basi fikra hii ya kuwepo shirki ni uzushi na ni tuhuma zinazopandikizwa na Mawahabi. Hakika lengo la Waislamu kuswali na kuomba dua kwenye makaburi ya Mawalii ni kutaka kupata baraka za sehemu hizo ambazo zimehifadhi vipenzi miongoni mwa vipenzi ya Mwenyezi Mungu. Waislamu wanaitakidi kuwa mahali hapo pana daraja kubwa kwa sababu pameuhifadhi mwili wa mtu mtakatifu miongoni mwa watu watakatifu wa Mwenyezi Mungu. Hivyo basi, kuswali na kuomba dua sehemu hiyo kunampa thawabu nyingi mwenye kutenda hayo. Kuna swali ambalo niwajibu lijibiwe nalo ni hili: Je, kuwazika Mawalii wa Mwenyezi Mungu katika sehemu fulani huwa kunaifanya sehemu hiyo ipate aina fulani ya heshima au hapana? Iwapo itathibiti kuwa "ndiyo" kwa mujibu wa dalili za Qur'an na hadithi, basi kuswali na kuomba dua kwenye makaburi ya viongozi wa Uislamu ni jambo mustahabu na linazo thawabu nyingi.

Hata kama pengine lisithibiti jambo hili (kama tulivyotangulia kusema) haiwezekani kuharamisha kuswali na kuomba dua mahali hapo bali patajaaliwa kuwa ni kama sehemu nyingine tu ambazo inafaa kuswali na kuomba dua japokuwa hapana aina yoyote ya ubora. Hebu tuyaelekeze mazungumzo yetu kwenye maudhui yenyewe ambayo ni Je, maziyara na kaburi ya Mawalii yanaoutukufu na heshima maalum? Na Je kuna ushahidi ndani ya Qur'an na hadithi kuhusu jambo hili. Jawabu liko kama ifaatavyo:

1. Kisa cha As-Habul-Kahfi ambacho tumetangulia kueleza kwamba, waumini na watu wa tauhidi walisema kuhusu namna ya kuyafanya mazishi ya hao As-Habul-Kahfi. "Tuwajangee msikiti juu yao"[99] Hapa utaona kuwa, lengo lililowafanya waumini hao kujenga msikiti mahali walipozikwa As-Habul-Kahfi si jingine bali ni kwa ajili wapate kutekeleza faradhi zao ndani ya msikiti huo.[100] Waumini hao walikuwa wakifikiri kuwa: Mahali hapa pamekuwa patukufu na panaheshimika kwa sababu panahifadhi miili ya watu miongoni mwa waja wa Mwenyezi Mungu waliowachamungu, kwa hiyo hapana budi kutabaruku napo kwa kupafanya kuwa ni msikiti kwa ajili ya swala na ibada za Mwenyezi Mungu ili kupata thawabu nyingi zaidi.

Qur'an inalitaja jambo hili lililofanywa na Waumini hao bila ya kuwakemea wala kuwakosoa bali imenyamaza kabisa. Na lau tendo lao hili lingekuwa liko kinyume cha sheria au ni miongoni mwa mambo ya upuuzi yasiyofaa, Qur'an isingewanyamazia, bali ingewakemea kama ilivyo kawaida ya Qur'an kutokunyamazia itikadi batili.

2. Qur'an tukufu inawaamuru mahujaji wa nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu waswali kwenye "Maqam Ibrahim[a.s] nalo ni jiwe ambalo Nabii Ibrahim[a.s] alisimama juu yake alipokuwa akijenga Al-Kaaba. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema "Pafanye mahali alipokuwa akisimama Ibrahim pawe pa kusalia ". Qur 'an, 2:125.

Yeyote anayeisoma aya hii atafahamu wazi kabisa kwamba swala iliwajibika mahala hapo siyo kwa jingine bali ni kwa sababu ya Maqam Ibrahimu (jiwe aliposimama Nabii Ibrahim) na kwamba lilejiwe ndilo lilisababisha mahala hapo papate utukufu na heshima hiyo. Na utawaona Waislamu kwa mamilioni wanapafanya kuwa ni mahali pa kusalia na kuomba dua. Kama mambo yako namna hii kuhusu mahali tu aliposimama Nabii Ibrahimu, je haitapasa hali iwe ni kama hiyo kuhusu sehemu walizolala watu wa Mwenyezi Mungu na viongozi wa Uislamu? Je, haitakuwa swala inayoswaliwa katika makaburi yao ni bora kuliko swala inayoswaliwa sehemu nyinginezo? Ni kweli kwamba aya hii imeshuka kuhusu kusimama kwa Nabii Ibrahimu mahala pale, lakini je hivi haiwezekani tukatoa kutokana na aya hii hukmu inayoenea?

Khalifa Mansoor Al-Abbasi (Ad-Dawaaniqi) alimuuliza Imam Malik Bin Anas (Imam wa Madhehebu ya Malik) walipokuwa ndani ya Msikiti wa Mtume[s.a.w.w] akasema: "Ewe baba Abdillahi nielekee Qibla ndiyo niombe au nimuelekee Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Malik akasema: "Kwa nini wampa kisogo Mtume hali ya kuwa yeye ni wasila wako na ndiye wasila wa baba yako Adam[a.s] siku ya Kiyama? Iliyopo muelekee na umuombe, Mwenyezi Mungu atakukubalia maombi yako."[101] Mazungumzo haya yanatufahamisha kwamba dua kwenye kaburi la Mtume[s.a.w.w] ilikuwa haina mushkeli wowote, pia kwamba suali la Mansur kumuuliza Malik ilikuwa ni kutaka kupata nguvu ya kufanya maombi kwa kuelekea Qibla au kwenye kaburi la Mtume[s.a.w.w] , naye Imam Malik anatoa fatwa kwamba kuelekea kaburi Ia Mtume[s.a.w.w] katika dua ni kama kuelekea Qibla.

3. Lau tutayarejea maelezo ya safari ya Miiraji, ukweli ungelijitokeza wazi wazi kwa namna nyingi zaidi. Kuna maelezo yasemayo kwamba Mtume[s.a.w.w] katika safari hiyo alishuka "Madina" na kwenye "Mlima wa Sinai" na Baiti Allaham" na aliswali katika sehemu hizo.

Jibril alimwambia Mtume[s.a.w.w] : "Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu unazifahamu sehemu ulizoswali? Hakika umeswali katika "Taiibah". Na hapo ndipo utapohamia, na umeswali kwenye "Mlima Sinai" mahali ambapo Mwenyezi Mungu alimsemesha Mussa na pia umeswali katika Bait Allaham (Bait-lehem)" mahali alipozaliwa Issa[a.s] ."[102] Hadithi hii inafahamisha kwamba, inapendekezwa kuswali katika sehemu ambazo zimeguswa na Manabii, na kwamba sehemu hizo zimepata heshima na utukufu kwa sababu ya Nabii huyo.

4. Bibi Hajir "Mama wa Ismail bin Ibrahim" alifikia daraja ya juu mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa sababu ya subira na kuvumilia taabu katika njia ya Mwenezi Mungu mambo ambayo yalisababisha Mwenyezi Mungu apafanye mahali alipokanyaga Mama huyu, kuwa ni mahali pa ibada na akawajibisha Mahujaji wa nyumba yake tukufu waende kama alivyokwenda Bibi Hajir baina va Milima miwili ya "Safaa na Marwaa", jambo ambalo Ibn Al-Qayyim ambaye ni mwanafunzi wa Ibn Taimiyya analikubali.[103] Sisi tunajiuliza, ikiwa uvumilivu wa Bibi Hajir kuyavumilia matatizo na taabu katika njia ya Mwenyezi Mungu kumesababisha kupapatia utukufu mahala zilipo kanyaga nyayo zake, na Mwenyezi Mungu akawajibisha kwa Waisiamu kuwa wamuabudu yeye Mwenyezi Mungu katika sehemu hiyo kwa kuenda baina ya Safaa na Marwaa, basi ni kwa nini kaburi la Mtume[s.a.w.w] lisiwe ni lenye baraka na utukufu wakati Mtume[s.a.w.w] alivumilia aina nyingi za matatizo na misiba na kero kwa ajili ya kuitengeneza jamii na kuiongoza?

5. Iwapo kuswali makaburini ni haramu katika sheria ya Kiislamu, basi ni kwa nini Bibi Aisha aliishi umri wake wote huku akiswali katika nyumba yake ambayo ndani yake mna kaburi la Mtume[s.a.w.w] ? Kama tutakubali kwamba hadithi ifuatayo ni sahihi yaani Mtume amesema: "Mwenyezi Mungu awalaani Mayahudi na Wakristo, wameyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa ni Misikiti".[104] Basi maana yake ni kwamba wao walikuwa wakiwaabudu Mitume wao na wakisujudu juu ya makaburi ya Manabii hao au kuyafanya makaburi hayo kuwa ndiyo kibla yao.

Na mambo haya mawili ni kinyume cha sheria tukufu ya Kiislamu. Lakini Mawahabi huitumia hadithi hii kuharamisha kuswali kwenye makaburi ya Mawalii wa Mwenyezi Mungu. Basi lau dalili ya hadithi hii ingekuwa sahihi, ni kwa nini basi Bibi Aisha ambaye ni mpokezi wa hadithi hii alimaliza karibu muda wa miaka hamsini ya umri wake akiswali na kufanya ibada ndani ya chumba ambacho amezikwa Mtume[s.a.w.w] .

6. Lau kaburi la Mtume[s.a.w.w] lisingekuwa na heshima na utukufu, ni kwa nini basi Abubakar na Omar walikazania wazikwe karibu na kaburi la Mtume[s.a.w.w] ? Hivyo basi hadithi hii inauhusiano gani na mwenendo wa Waislamu unaoruhusu kuswali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa kuelekea Qibla lakini karibu ya kaburi la Mtume[s.a.w.w] ili kupata ubora na thawabu nyingi?

7. Bibi Fatm az-Zah-Raa[a.s] alikuwa akizuru kaburi Ia Ammi yake Hamza kila siku ya ljumaa au kila wiki mara mbili, na alikuwa akilia na kuswali kwenye kaburi lake.

Al-Baihaqi anasema: Fatma [r.a] alikuwa akilizuru kaburi la Ammi yake Hamza kila ljumaa na kisha huswali hapo na kulia."[105] Bibi Fatma huyu ndiye yule ambaye zimepokelewa kwa Mtume hadithi sahihi zisemazo kwamba: "Radhi ya Fatma ndiyo radhi ya Mwenyezi Mungu na mjumbe wake, na ghadhabu ya Fatma ndiyo ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na mjumbe wake."[106] Ewe msomaji mpendwa, dalili zote hizi ukiongeza na mwenendo wa Waislamu wa kuswali na kuomba dua katika sehemu walizozikwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu, na wapenzi wake vinatia nguvu kuwa, kuswali na kuomba dua kwenye makaburi haya kuna thawabu nyingi na ubora mkubwa, na kwamba lengo ni kupata baraka zilizopo katika sehemu hizo na ni kutekeleza faradhi mahala hapo kwa kutaraji kukubaliwa mbele ya Mwenyezi Mungu. Lau tutakadiria kwamba hakuna dalili katika Qur'an na hadithi inayoonyesha ubora na heshima ya sehemu hizo na pia kwamba hakuna ubora wowote kuswali na kuomba dua mahala hapo, hata hivyo ni kwa nini iwe haramu kuswalia katika sehemu hizo? Na ni kwa nini basi sehemu hizi haziingii ndani ya kanuni ya Kiislamu yenye kuenea, ambayo inaizingatia ardhi yote kuwa ni mahali pa kufanyia ibada ya Mwenyezi Mungu kama alivyosema Mtume[s.a.w.w] : "Ardhi yote imefanywa kuwa ni msikiti na ni safi kwa ajili yangu."[107]

KUWASHA TAA MAKABURINI

Kuwasha taa kwenye makaburi ya Mawalii wa Mwenyezi Mungu, jambo ambalo mawahabi wanadai kuwa ni haramu, halina umuhimu mkubwa kwa kuwa dalili pekee waitumiayo ni ile hadithi aliyoitaja An-Nasai kutoka kwa Ibn Abbas kwamba, "Mtume[s.a.w.w] amewalaani wanawake wanaozuru makaburi na wanaoyafanya kuwa ni misikiti na wale wanaayawasha taa". [108] [108] Hadithi hii na nyinginezo mfano wa hii zinahusika tu kama kuwasha taa huko kutakuwa ni kupoteza na kufuja mali au kutasababisha kujifananisha kwa baadhi ya nyumati na mataifa na dini batili, kama alivyolionyesha jambo hilo Al-Allamah as-Sindi katika sherehe ya hadithi hii aliposema: "Na katazo hilo ni kwa kuwa (kuwasha taa) husababisha kupoteza mali bila manufaa". [109] Ama kama lengo litakuwa ni kuwasha taa kwa ajili ya kusoma Qur'an, kuomba, kunyenyekea kwa Mwenyezi Mungu, kuswali na mengineyo katika mambo mustahabbu na wajibu pamoja na manufaa yanayo kubalika kisheria, basi haya yote hayana matatizo kabisa, "Saidianeni katika mema na uchamungu". (Qur'an, 5:2). Basi vipi itakuwa haramu? Ilivyo ndivyo ni kwamba, kuwasha taa makaburini ni jambo mustahabbu kisheria na linapendeza kiakili.

KUTAWAS-SAL KWA MAWALII WA MWENYEZI MUNGU

Mas-ala ya kutawasal Kwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu na wapenzi wake ni mas-ala yanayofahamika miongoni mwa Waislamu ulimwenguni kote, na zimekuja hadithi nyingi kuruhusu jambo hili na kulipendekeza. Kwa hiyo kutawas-sal siyo jambo geni bali ni jambo Ia kidini lililofahamika miongoni mwa Waislamu tangu mwanzoni mwa kuja Uislamu mpaka leo hii, na wala humkuti Muislamu anayelipinga. Kwa muda wote wa karne kumi na nne tangu kuja Uislamu, hapana yeyote aliyelipinga jambo hili isipokuwa Ibn Taymiyyah na wanafunzi wake katika karne ya nane Hijiriya. Na baada ya karne mbili akaja Muhammad bin Abdil-Wahab, ambaye yeye wakati mwingine akaona kuwa kutawas-sal kwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu ni Bid'a na wakati mwingine akaona kuwa eti ni kuwaabudu Mawalii hao. Hapana shaka yoyote kwamba kumuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni shiriki na ni haramu. Sisi sasa hivi hapa hatufanyi uchunguzi juu ya neon Ibada na uhakika wake ingawa jambo hili ni muhimu sana, lakini tutalizungumzia kwa ufafanuzi katika mahali pake maalum, kwa kuwa sasa hivi tunashughulika na kutawas-sal kwa Mawalii. Hivyo basi tunasema: Fahamu (ewe msomaji) kwamba, kutawas-sal kwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu kuna namna mbili:

1. Kutawas-sal kwa Mawalii wao wenyewe nafsi zao kama vile tukisema:

"Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nintawas-sal kwako kwa Mtume wako Muhammad[s.a.w.w] nikubalie haja yangu".

2. Kutawas-sal kwa cheo cha Mawalii na utukufu waliyonao mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kama vile tukisema: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi ninatawas-sal kwako kwa utukufu wa Muhammad na heshima yake na haki yake unikubalie haja yamgu." Kwa upande wa Mawahabi, wao wanaziharamisha namna zote mbili, wakati ambapo hadithi tukufu za Mtume[s.a.w.w] na sera ya Waislamu vinashuhudia kinyume cha madai ya Kiwahabi na pia vinatilia mkazo kuwa namna zote mbili zinafaa. Hivi sasa tunataja baadhi ya hadithi hizo moja baada ya nyingine, kisha tutaleta maelezo juu ya sera ya Waislamu, na hapo ndipo itakapoyeyuka na kupotea kauli ya mwenye kuharamisha tawas-sul na kuwa eti ni Bid'a.

HADITHI TUKUFU ZA MTUME [s.a.w.w]

Hadithi zinazojulisha kuwa kutawa-sal kwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu kunafaa ni nyingi mno, na zinapatikana katika vitabu vya Historia na hadithi. Katika maelezo yafuatayo tunataja sehemu yake tu:

HADITHI YA KWANZA

Imepokewa toka kwa Uthman bin Hunaif kwamba amesema: "Mtu mmoja kipofu alikuja kwa Mtume[s.a.w.w] akasema: "Niombee kwa Mwenyezi Mungu aniponye (upofu)". Mtume akamwambia, "Ukipenda nitaomba na ukipenda uvumilie na ndiyo bora". Yule mtu akamwambia Mtume: "Muombe Mwenyezi Mungu (aniponye"). Basi Mtume[s.a.w.w] akamuamuru kipofu yule atawadhe vizuri na aswali rakaa mbili na aombe kwa kutumia Dua hii. " Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba na ninaelekea kwako kupitia kwa Mtume wako Mtume wa Rehma, Ewe Muhammad hakika mimi naelekea kwa Mola wangu kupitia kwako katika haja yangu ili ikubaliwe, ewe Mwenyezi Mungu mfanye Muhammad kuwa muombezi wangu ." Ibn Hunaif anasema:"Basi Wallahi, tulikuwa hatujatawanyika tukiendelea kuzungumza mpaka aliingia kwetu kama kwamba hakuwa na ugonjwa (upofu)".

MAELEZO JUU YA SANAD YA HADITHI HII

Hakuna ubishi katika kusihi kwa Sanad ya hadithi hii, kwani hata huyo Imam wa Mawahabi "Ibn Taimiyyah" ameihesabu kuwa ni hadithi sahihi na akasema kuwa, makusudio ya "Abu Jaafar" jina linalopatikana katika Sanad ya Hadithi hi ni 'Abu Jaafar Al-Khatmi" na huyu Bwana ni mpokezi anayetegemewa. Imekuja katika Musnad ya Imam Ahmad (Abu Jaafar Al-Khatmi). Amma ndani ya Sunan Ibn Majah imekuja (Abu Jaafar) tu. Mwandishi wa Kiwahabi katika zama hizi aitwaye Ar-Rifai ambaye wakati wote anajaribu kuzifanya dhaifu hadithi zinazohusu Tawas-sul anasema kuhusu hadithi hii tuliyoitaja hapo kabla: "Hapana shaka kwamba hadithi hii ni sahihi na ni mashuhuri na imethibiti bila wasiwasi wala mashaka (kwamba) macho ya kipofu yule yalirudi (akawa anaona) kwa sababu ya Dua ya Mtume[s.a.w.w] ."[110] Na anasema tena:

"Hadithi hii wameileta An-Nasai na Al-Baihaqi, At-Tabran na At-Tirmidhi na AI-Hakim wao wametaja "Allhumma Shaf-Fihu Fihi" badala ya "Allahumma Shaf-Fihu Fiy-ya."[111] Mufti wa Makka Zaini Dahlan anasema: "Bukhari na Ibn Majah na Al-Hakim (ndani ya Mustadrak yake) pamoja na Jalalud-Dinis-Suyuti (katika Jaami' yake) wameitaja hadithi hii na Sanad zake ni sahihi. Na sisi tunaitaja hadithi hii kutoka katika rejea zifuatazo:

1. Sunan Ibn Majah, Juzuu ya kwanza, uk. 441 ikiwa ni hadithi na 1385, kimehakikiwa na Muhammad Fuad Abdul-Baqii, toleo la Dar-Ihyail-Kutubil-Arabiyya. Naye Ibn Majah anaeleza kutoka kwa Abu Is-Haqa kwamba yeye amesema: "Hadithi hii ni sahihi." Kisha akasema:

"Na ameipokea Tirmidhi katika kitabu "Abuwa-bul-ad-iyya" akasema, Hadithi hii ni ya kweli na ni sahihi gharib.

2. Musnad Ahmad bin Hanbal, Juzuu ya nne uk. 138, "kutoka kwa Athuman bin Hunaif" chapa ya "Maktabul-islami, Muasasah dari-Saadir/Beirut, na ameipokea hadithi hii kwa njia tutu.

3. Mustad-ra kus-sahihain ya Al-Hakim An-Nishapuri, Juzuu ya kwanza, uk. 313, chapa ya Haidar-abad/India. Amesema baada ya kuitaja hadithi hi:

"Hadithi hii ni sahihi kwa sharti ya Bukhari na Muslim lakini hawakuiandika"

. 4. Al-Jamius-Saghiru cha As-Suyuti, uk. 59, kutoka kwa Tirmidhi na Al-Hakim.

5. Tal-khisul-Mustad-rak cha Adh-dhahabi-alivefariki mwaka 748 A.H., kilichochapishwa katika Hashiya ya AI-Mustad-rak.

6. At-Tajul-Jamii, Juzuu ya kwanza, uk. 286, nacho ni kitabu kilichokusanya hadithi zilizomo katika sihahi tano isipokuwa sahih ya Ibn Majah. Baada ya haya hakuna haja ya majadiliano kuhusu Sanad ya Hadithi hii au kuitia dosari.

Ama maelekezo yake na mafunzo yaliyomo, lau utamuonyesha hadithi hii mtu anayefahamu vyema lugha ya Kiarabu tena mwenye akili safi na akajiepusha na chuki za Kiwahabi na kuchanganya kwao mambo kuhusu tawa-suli kisha umuulize: "Ni kitu gani Mtume[s.a.w.w] alimuamuru kipofu yule akifanye wakati akiomba dua ile"?

Kwa haraka tu jibu lake litakuwa: "Mtume[s.a.w.w] alimfundisha namna atakayo tawas-sal kwa Mwenyezi Mungu kupitia kwa Mtume wake Mtume wa Rehma na namna Mwenyezi Mungu atakavyokubali maombi yake". Maana hii ndiyo inayofahamika moja kwa moja kutokana na maneno yaliyomo katika hadithi iliyotajwa. Ndani ya maelezo yafuatayo tunaigawa hadithi hii katika mafungu ili kuongeza ufafanuzi.

FUNGU LA KWANZA

"Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi ninakuomba na ninaelekea kwako kupitia kwa Mtume wako." Neno "Mtume wako"linauhusiano na maneno mawili yaliyokuja kabla ya neno hili. Maneno hayo ni: "Ninakuomba na ninaelekea kwako". Kwa maneno yaliyo wazi tutasema kama ifuatavyo: Kipofu yule anamuomba Mwenyezi Mungu kupitia kwa Mtume[s.a.w.w] kama ambavyo anaelekea kwa Mwenyezi Mungu kwa kupitia heshima na utukufa wa Mtume[s.a.w.w] na wasila wake.

Kinachokusudiwa kwa neno "Mtume" siyo dua yake bali ni ile dhati yake tukufu. Ama anayesema kwamba neno dua limekadiriwa kabla ya neno Mtume na maana ya (As-aluka Binabiyyika) ni ninakuomba kwa dua ya Mtume wako, basi kusema hivyo ni madai bila ya dalili na ni kinyume cha maana iliyo dhahiri. Na sababu ya madai hayo yaliyo kinyume na dalili ni kuwa, yeye haitakidi kutawasal kwa dhati ya Mtume[s.a.w.w] ndiyo maana akalazimika na akakadiria kusema kwamba neno dua hapa limekadiriwa ili tu kwa njia hii apate kuitakasa itikadi yake ya kupinga kutawasal kwa Mtume mwenyewe.

FUNGU LA PILl

"Muhammad Nabii wa Rehma". Ili iweze kufahamika vyema kwamba makusudio katika Dua hiyo, ni kumuomba Mwenyezi Mungu kupitia kwa Mtume na dhati yake na heshima yake, basi imekuja jumla baada ya neno "Mtume wako" isemayo "Muhammad Nabii wa Rehma", ili ifafanue lengo wazi wazi.

FUNGU LA TATU

Sentensi isemayo "Ewe Muhammad, hakika mimi naelekea kwa Mwenyezi Mungu kupitia kwako", inajulisha kwamba kipofu yule alimfanya Mtume mwenyewe kuwa ndiyo wasila wa maombi yake, siyo dua ya Mtume[s.a.w.w] yaani yeye alitawassal kwa dhati ya Mtume siyo kwa dua ya Mtume.

FUNGU LA NNE

Na aliposema: "Mfanye Muhammad awe muombezi wangu", alikuwa na maana ya kusema kuwa: "Ewe Mola mfanye Muhammad[s.a.w.w] awe ndiye muombezi wangu na ukubali uombezi wake kwangu, katika haki yangu." Ewe msomaji mpenzi bila shaka imekudhihirikia kwamba nukta muhimu katika dua yote ni dhati ya Mtume[s.a.w.w] na shakhsiyya yake tukufu, na katika dua hii hakuna utajo wa dua ya Mtume asilan. Na kila atayedai kuwa kipofu yule alitawassal kwa dua ya Mtume na wala hakutawassal kwa dhati ya Mtume wala shakhsiyya yake, huyu atakuwa amejifanya kutoyaelewa maneno ya hadithi hii yaliyo wazi na amejifanya kutoifahamu hadithi hii. Nawe msomaji lau utaifanyia mazingatio kauli ya muombaji aliposema: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba na ninaelekea kwako kupitia kwa Mtume wako, Mtume wa Rehma" na aliposema tena muombaji huyo: "Ewe Muhammad hakika mimi naelekea kwa Mola wangu kupitia kwako", itakudhihirikia wazi wazi kwamba, lengo linalokusudiwa ni nafsi ya Mtume awe ndiyo wasila kupitishia maombi ya muombaji.

Na lau lengo ingekuwa ni dua ya Mtume ndiyo wasila ingelazimika kusema: "Ewe Mwenyezi Mungu nakuomba kwa (kupitia) dua ya Mtume". Baada ya haya tuliyoyaeleza hivi punde hakuna mush-keli unaobakia miongoni mwa mish-keli aliyoitaja yule mwandishi wa Kiwahabi katika Kitabu kiitwacho "At-Tawas-Sul Ilaaz HaqiqatitTawas-sul". Mish-keli hiyo tumeitaja pamoja na majibu yake ndani ya kitabu chetu kiitwacho "At-Tawas-sul" kuanzia ukurasa wa 147 mpaka 153 na unaweza kurejea ukaona.

HADITHI YA PILl KUTAWAS-SAL KWA HAKI YA WAOMBAJI

Amepokea Atiya Al-aufi kutoka kwa Abu Said Al-Khudri kwamba Mtume[s.a.w.w] amesema: "Yeyote atakayetoka nyumbani mwake kwenda kuswali akasema: Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba kwa haki ya wanaokuomba, na ninakuomba kwa haki ya mwendo wangu huu kwani mimi sikutoka kwa maringo na majivuno, wala kujionyesha wala kutaka sifa, nimetoka kwa kuogopa ghadhabu zako na kutafata radhi zako, basi ninakuomba unilinde kutokana na moto na unisamehe madhambi yangu, kwani hapana anayesamehe madhambi isipokuwa wewe.[112] (Atakayesema hivi) Mwenyezi Mungu atamuelekea mtu huyo kwa dhati yake na watamtakia msamaha malaika sabini elfu." Hadithi hii iko wazi mno katika maana yake na inajulisha kwamba mtu anayo ruhusa ya kutawas-sal kwa heshima ya Mawalii na daraja walizonazo na cheo chao mbele ya Mwenyezi Mungu. Basi na awafanye Mawalii hawa kuwa ndiyo wenye kukaa kati na kuwa waombezi, ili haja zake zikubaliwe na dua zake zipokelewe.

HADITHI YA TATU KUTAWAS-SAL KWA HAKI YA MTUME MTUKUFU [s.a.w.w]

Nabii Adam[a.a.w.w] yalipomtokea mambo ambayo ilivyokuwa ni bora yasimtokee, naye akarejea kwa Mwenyezi Mungu kutokana na hayo yaliyomtokea, alipokea maneno kutoka kwa Mola wake kama Qur'an Tukufu inavyoonyesha:

فَتَلَقَّىٰ آدَمُ مِن رَّبِّهِ كَلِمَاتٍ فَتَابَ عَلَيْهِ إِنَّهُ هُوَ التَّوَّابُ الرَّحِيمُ ﴿٣٧﴾

"Kisha Adam akapokea maneno kutoka kwa Mola wake, na Mola wake akakubali toba yake hakika yeye ni mwingi wa kupokea (toba) na ni mwingi wa huruma."[113] Qur'an, 2:37.

Wafasiri wa Qur'an na wataalam wa hadithi wamefafanua na kutoa rai zao na mtazamo wao kuhusu aya hii na maana yake, na wamefanya hivyo kutokana na kutegemea kwao baadhi ya hadithi ili kupata maana ya aya hii. Yafuatayo ni maelezo ambayo ndani yake tutataja hadithi hizo ili tuone matokeo ambayo tunaweza kuyapata baada ya kuzitaja hizo hadithi.

At-Tabrani katika Al-muujamus-Saghir na Al-Hakim katika Mustadrak yake, na Abunuaim Al-Isfahani katika Hil-yatulAuliyai, Baidhawi naye katika Dalailun-nubuwat, na Ibn Asakir Ad-Dimishqi katika Tarikh yake, As-Suyuti naye ndani ya Tafsirud-duril Manthur, Al-A'lusiy yeye katika Tafsiri Ruhul-maan wote hawa wametoa mapokezi kutoka kwa Umar bin Al-Khatab naye kutoka kwa Mtume[s.a.w.w] kwamba Mtume amesema: "Wakati Adam alipokosea lile alilolikosea, alinyanyua kichwa chake juu akasema, Nakuomba (Ewe Mwenyezi Mungu) kwa haki ya Muhammad unisamehe, Mwenyezi Mungu akampelekea wahi Adam (akamwambia) huyu Muhammad ni nani? Adam akasema:

Limetukuka Jina Lako (Ewe Mwenyezi Mungu), wakati nilipokuwa nimeumbwa nilinyanyua kichwa changu, kuiangalia arshi yako, basi niliona maandishi (yasemayo) hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah na Muhammad ni mjumbe wa Allah nikasema, bila shaka hapana kiumbe Mtukufu mbele yako kuliko yule ambaye umeliweka jina lake pamoja na jina lako, Mwenyezi Mungu akampelekea Adam wahi (akamwambia) huyo ndiyo Nabii wa mwisho katika kizazi chako, na lau si yeye nisingekuumba wewe."[114] Akinakili toka kwa At-Tabrani na Abunuaim na AI-Bayhaqi na matni ya hadithi imenakiliwa kutoka kwa Ad-durul-Manthoor.

MAONI YETU JUU YA HADITHI HII

Kinyume cha mazowea tuliyonayo kuwatambulisha watu hao au nafsi hizo. Qur'an inazungumzia nafsi au watu kwa kutumia neno "AL-KALIMAH" kinyume cha matumizi yetu ya kawaida kuhusti neno hili. Kwa mfano Mwenyezi Mungu anasema:

(a) "Mwenyezi Mungu anakupa bishara njema ya Yahya mwenye kumsadikisha neno atokaye kwa Mwenyezi Mungu. Qur'an, 3:39

(b) Kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo: "Ewe Mariam, Mwenyezi Mungu anakupa bishara njema ya neno atokaye kwake jina lake ni Masih Isa mwana wa Mariam ". Qur'an, 3:45.

(c) "Hakika Masih Isa mwana wa Mariam ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu na ni neno lake ." Qur'an, 4:171

(d) Kauli ya Mwenyezi Mungu: "Waambie lau kama bahari ingekuwa ndiyo wino kwa (kuandikia) maneno ya Mola wangu, basi bahari ingekwisha." Qur'an, 18:109.

(e) Kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo: "Na bahari hii (ikafanywa wino) na bahari nyingine saba (zikaongezwa), maneno ya Mwenyezi Mungu yasingelikwisha. " Qur'an, 31:27. Tukiziangalia aya hizi inawezekana kabisa kusema kwamba: Makusudio ya "Kalimaat" yaani katika ile aya isemayo "Akapokea Adam kutoka kwa Mola wake maneno" makusudio yake ni dhati tukufu yenye heshima ambayo kwayo Nabii Adam alitawas-sal kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Na katika hadithi iliyotangulia utaliona jina la Muhammad[s.a.w.w] tu ndiyo lililotajwa. Ama katika hadithi zilizoko katika madheheb ya haki (Shia) utaona hadithi hii imepokewa kwa sura inayokubaliana na aya tukufu ya Qur'an, pia utaikuta imepokewa kwa namna mbili. Wakati mwingine neno "Kalimaat" limefasiriwa kwa maana ya majina ya watukufu watano[a.s] , na wakati mwingine limefasiriwa kwa sura zao zenye nuru. Hebu itazame hadithi ifuatayo: "Hakika Adam aliona kwenye arshi pameandikwa majina matukufu yenye heshima akauliza, majina hayo (ni ya kina nani)? Akaambiwa, haya ni majina ya viumbe watukufu mno kwa daraja mbele ya Mwenyezi Mungu, kuliko viumbe wote na majina hayo ni, Muhammad, Ali, Fatma, Hasan na Husein. Basi Adam[a.s] akatawas-sal kwa Mola wake kupitia kwao ili kukubaliwa toba yake na kunyanyuliwa daraja yake.[115] Na baadhi ya hadithi zinajulisha kwamba Adam[a.s] aliona Sura za nuru za watukufu watano, basi akatawas-sal kwazo baada ya kuziona. (Kwa ufafanuzi zaidi tazama Tafsir AI-Burhan, juz. 1, uk. 87, Hadith na 13, 15, na 16.)

2. Na tunaporejea vitabu vya historia na hadithi inatudhihirikia kwamba, Qadhiya ya Adam kutawas-sal kwa Mtume Muhammad[s.a.w.w] lilikuwa ni jambo mashuhuri miongoni mwa watu, ndiyo manna utamkuta Imam Malik bin Anas (Imam wa Madhehebu ya Malik) anasema kumwambia Mansur Ad-Dawaniq katika Msikiti wa Mtume[s.a.w.w] : "Mtume ni wasila wako na ni wasila wa Baba yako Adam". Nao washairi wa Kiislamu wameuonyesha ukweli huu katika mashairi yao. Mmoja wa washairi hao anasema: "Kwa Mtume[s.a.w.w] Mwenyezi Mungu alikubali maombi ya Adam na aliokolewa Nuhu ndani ya Safina." [116] Mwingine naye anasema: Ni watu ambao kwao lilisameheka kosa la Adam, nao ndiyo wasila na nyota zing'aazo.[117]