1
PAMOJA NA MITUME KATIKA NJIA YA MASHAKA
2. MZEE WA MITUME BAADA YA NABII IDRIS AS KUREJEA KWA MOLA WAKE
Watu wakaanza kuzusha mambo mapya (bid'a) katika dini, wakahitalifiana kwa tofauti kubwa na wakayarudia mambo yao ya zamani. Kikundi kidogo tu cha watu ndicho kilichoshikamana na mafunzo ya Nabii Idris
, na kufuata kama alivyoagizia. Wakabaki juu ya njia hiyo ambayo ilikataliwa na watu wengi. Katika kizazi cha Nabii Idris
alikuwepo mtu mmoja akiitwa Nuh. Alikuwa mrefu na mwenye fikra nyingi. Alijiweka mbali na watu kwenye majabali, alikuwa akila mimea ya ardhi tu na akimwabudu Mwenyezi Mungu Peke Yake. Alipofikia umri wa miaka arobaini ambapo maandalizi ya uongozi unapokamilika na msimamo anaoutaka Mwenyezi Mungu unapothibitika, alijiwa na Jibril
na kumwuliza: "Kwa nini umejitenga na watu?" Akamjibu: "Kwa sababu watu wangu hawamjui Mwenyezi Mungu, na kama wakinijua mimi wataniua." Jibril akamwambia: "Kama ukipewa nguvu utaweza kuwakabili?" Akajibu: "Hivyo ndivyo ninavyotaka."
Kwa hivyo, Jibril
akampa ujumbe wa Mola Wake na akamwamrisha aeneze mwito wa Mwenyezi Mungu. Akaondoka Nabii Nuh
kwa furaha kuelekea kwa jamii ya watu wake. Akawakuta wamejikusanya kwenye masanamu ambayo hayadhuru wala hayanufaishi chochote, na hayasikii wala hayaoni. Watu walikuwa wametawaliwa na upotevu wakawa viziwi na vipofu, hawasikii haki yoyote wala hawana uongofu wowote. Nabii Nuh
akawaendea haraka akiwa na fimbo yake nyeupe ya miujiza ikiwa ndiyo msaidizi wake. Akasimama mbele yao kuwalingania. Akawa kama kimondo kilichoshuka juu ya upotevu wao au kama mwangaza ulioangaza kwenye giza. Akawaambia: "Laa ilaaha illallaah! - Hapana Mungu apasaye kuabudiwa ila Allah!" Hilo likawa ni tamko lililotoka katika moyo wa kishujaa uliojaa imani, mategemeo na utulivu. Watu wakaathirika na tamko hilo na masanamu yao yakatikisika.
Wakasema madhalimu: ''Ni nani huyo?" Akasema Nabii Nuh
: "Ni mimi mja wa Mwenyezi Mungu; amenituma kwenu kuwa Mtume wenu." Madhalimu hao wakaanza kumwadhibu baada ya kumkanusha Mola wake na kuukadhibisha Utume wake. Lakini Nabii Nuh
akaendelea kuwalingania, nao pia wakaendelea kumkanusha na kumkadhibisha. Ilikuwa ni kawaida kwake kwenda katika hafla na mikutano yao akiwalingania dini, lakini watu walikuwa wakigeuka huku na huko na wengine wakiziba masikio yao ili wasisikie mwito wa haki. Watu walikuwa wakishikwa na mori kipumbavu. Walikuwa wakimwadhibu sana Mtume wao mpaka akizimia. Baada ya kuzimia, ami yake alikuwa akija kumchukua nyumbani kwake kumwuguza. Mara nyingine alikuwa akizimia kwa muda wa siku tatu mfululizo bila ya kuzinduka na anapozinduka alikuwa akiwaombea kwa kusema: "Ewe Mola waagu! Waongoze watu wangu kwani hakika wao hawajui." Umri wa Nabii Nuh
ukazidi na upotevu wa watu wake ukazidi pia. Akasubiri Nuh kwa subira kubwa lakini utaghuti wao na kiburi chao cha kukataa haki kikazidi pia.
Miaka mingi ikapita na watu hao wakabaki katika hali hiyo hiyo. Kizazi kimoja kikaondoka na kingine kikaja, lakini kila kimoja kiliendelea kumkadhibisha na kuukadhibisha Utume wake. Karne moja baada ya pili zikapita lakini kaumu ya Nuh ikaendelea na ukafiri na inadi yao. Ilikuwa kwamba mtu akijiona amezeeka na anakaribia kufa, basi humchukua mtoto wake kwa Nabii Nuh
na kumwambia: "Ewe mwanangu! Nitakapokufa usisikilize maneno ya mwendawazimu huyu." Katika misukosuko hii, Nabii Nuh
aliishi muda mrefu uliofikia miaka 950 akiwalingania watu wake, na katika muda huo ni watu wachache wapatao 80 tu ndio waliomwamini!
Kikundi kimoja cha waumini kilikuwa kikiadhibiwa pamoja naye lakini kilikuwa na subira ndogo, hivyo wakamwomba Nabii Nuh
awaombee makafiri iwateremkee balaa. Wakati huo miaka 300 ilikuwa imekwishapita tangu alipoanza kuwalingania watu. Akakusudia kuwaombea balaa makafiri, mara akajiwa na malaika 12,000 ambao ni miongoni mwa malaika watukufu. Wakamwambia Nabii Nuh
: "Tunakuomba usiwaombee balaa watu wako." Akasema Nabii Nuh
: "Ninawapa muda mwingine wa miaka 300." Ilipofika miaka 600, hakukuwepo hata mmoja aliyemwamini. Akakusudia kuwaombea balaa. Malaika wakamjia tena na wakamtaka asiwaombee balaa. Nabii Nuh
akaongeza muda mwingine wa miaka 300.
Ilipotimia miaka 900, akakusudia kuwaombea balaa. Mwenyezi Mungu akamteremshia wahyi akisema: "Hataamini yeyote katika watu wako isipokuwa yule aliyekwisha amini.
" (11:36) Akasema Nabii Nuh
: "Ewe Mola wangu! Usimwache juu ya ardhi mkazi yeyote katika makafiri
." (71:26) Mwenyezi Mungu akaitikia dua yake. Ikaja tufani kubwa, yakamiminika maji kutoka mbinguni na zikabubujika chemchemi kutoka ardhini mpaka majabali yakafunikwa kwa maji. Watu wote wakaangamia isipokuwa wale walioingia katika safina ambayo ilikuwa ikikata mawimbi makubwa kama jabali. Safina ilisheheni jozi moja ya kila aina ya viumbe.
Kisha Mwenyezi Mungu akaamrisha ardhi imeze maji yake na mbingu iache kunyesha, na ikapitishwa amri ya kuangamizwa makafiri. Safina ikatua kwenye mlima mmoja ikiwa na watu 80 tu waliomwamini Nabii Nuh AS. Kisa hiki cha Nabii Nuh mtukufu ni mwujiza mmoja miongoni mwa miujiza michache katika historia. Ingawa Nabii Nuh
alijitahidi kuwalingania watu wake kwa muda wa miaka 950 aliokaa nao, lakini waliendelea na upinzani wao na hawakuzidi chochote isipokuwa ukafiri na ulahidi. Hivyo, adhabu iliwashukia ambayo iliwataabisha na kuwaangamiza wote bila ya kumhurumia au kumwacha mtu yeyote.
3. NABII IBRAHIM
UTHABITI NA JIHADI YA NABII IBRAHIM
Aliposhuka Nabii Nuh
kutoka katika safina yake kwa salama pamoja na waumini aliokuwa nao, hapo tena watoto wake na wafuasi wakaimarisha nchi, naye akamshukuru Mwenyezi Mungu na kuridhika. Miaka 50 baada ya gharika, Nabil Nuh
akafariki dunia. Umma wake ukaanza kuzidi kwa kuzaliana kizazi baada ya kizazi. Lakini baadaye watu wakaanza kuhitalifiana. Kuna wale ambao walishikilia imara imani kwa kushikamana na mafunzo ya Nabii Nuh
, na wengine wakapotea kwa kufuata matamanio yao, na kwa kuacha kumwabudu Mwenyezi Mungu na kufanya mambo maovu. Kizazi cha Nabii Nuh
kikagawanyika kati ya waumini ambao walikuwa katika kizazi cha Sam na ndicho kizazi kilichotoa mitume na mawasii, na wengine makafiri ambao walikuwa kizazi cha Hami na Kanaan na wengineo. Mambo yakaendelea vivyo hivyo huku Mwenyezi Mungu akipeleka manabii katika baadhi ya vijiji. Wengine wakaongoka na wengine wakapotea, wakaangamizwa na kuadhibiwa.
Hatimaye, Mwenyezi Mungu akampeleka Mtume Mtukufu Ibrahim
kwa watu wote. Nabii Ibrahim
akawatingania watu wamwabudu Mwenyezi Mungu Peke Yake, akayavunja masanamu na akaamrisha mema na kukataza maovu. Katika zama zake alikuwepo mfalme dhalimu akijulikana kwa jina la Namrud bin Kanaan ambaye alimiliki nchi akaueneza ufalme wake kwa vitimbi na hadaa. Namrud alikuwa na waziri aitwaye Azar ambaye alikuwa mnajimu na kuhani na mwenye hadhi kubwa sana mbele ya mfalme. Katika unajimu wake akaona kuwa atatokeza mtu mkubwa ambaye atauangusha ufalme na kuleta dini mpya. Akampasha mfalme habari hiyo, naye mfalme akafazaika. Kisha Azar akamwambia kuwa bado hajazaliwa mtu huyo. Mfalme akaogopa kidogo na akasema: "Tutawatenga wanawake na waume zao ili asizaliwe huyu mtoto, na wale wenye mimba tutawaangalia atakayezaa mtoto wa kiume tutamwua." Kisha mfalme akauliza: "Atazaliwa wapi mtotohuyo?" Azar akamjibu: "Katika mji huuhuu."
Namrud akatoa amri. Watumishi wake wakaanza ufisadi wao katika mji kwa kuwadhalilisha watu, kumtenganisha mtu na mkewe, kuwaua watoto wa kiume na kuwasaliza wanawake. Hali hiyo ikaendelea na huku mji ukiwa umejaa misukosuko na vikwazo. Naam. Namrud alitaka hivyo na Mwenyezi Mungu akataka vingine. Namrud akajaribu kufanya dawa aliyoitaka kwa kutumia uwezo wake na nguvu yake, lakini uwezo wa ghaibu (usioonekana) ukapitisha lile lililolitaka. Kwa hivyo, uwezo wa Namrud ukashindwa, na akazaliwa Ibrahim kwa kificho katika pango la jabali. Ibrahim akakua haraka haraka mpaka akawa kijana. Baada ya kufariki baba yake muumini, Tarikh, akalelewa na ami yake kafiri, Azar, aliyekuwa waziri wa mfalme. Ibrahim akawa anaishi katika kitovu cha ukafiri, makao ya nguvu za kidhalimu, chimbuko la uovu wote na shimo Ia uchafu na maradhi yote, katika nyumba ya ami yake ambaye alikuwa na uwezo na sauti katika mji.
Azar alimpenda sana Ibrahim kuliko watoto wake aliowazaa, kwa vile alivyoona utukufu wake ushujaa, tabia nzuri, ukweli na vitendo safi. Azar alikuwa akitengeneza masanamu katika jumba la mfalme na yanapokuwa mengi huwapa watoto wake wakauze barabarani na wachukue faida inayopatikana katika biashara hiyo. Ibrahim alipokua, Azar akamtaka ashiriki katika kuuza masanamu ili apate fedha za kuongezea matumizi yake ya maisha. Ibrahim ambayo moyo wake haujawahi kuingia doa la ukafiri wala kuingia shaka, akapata fursa ya kutekeleza ujumbe wake mzito, wakati ambapo mji ulikuwa umejaa dhuluma, wafuasi madhalimu na makafiri wenye kuitakidi nguvu ya mfalme jabari.
Kwa sababu hii, Nabii Ibrahim
akaanza kuwazindua watu na kutoa wito kabla ya kumkabili mfalme. Akaanza kuyafunga kamba za shingoni yale masanamu na kuyaburura huku akiwalingania watu akisema: "Ni nani anayetaka kununua kitu kisichofaa wala kunufaisha?" Kisha anayatosa katika maji machafu kwa ajili ya kuyadharau na kuwafahamisha watu kuwa hayana uwezo wowote. Hiyo ndiyo hatua ya kwanza aliyoifanya kwa miungu ya uwongo na lilikuwa pigo la nguvu lililowapofusha wenye kughafilika. Kisha akawa anafikiria viumbe wale waliodanganywa na matamanio yao wakaabudu asiyekuwa Mungu. Baadhi yao wakiabudu masanamu ya kuchonga na wengine wakielekea kwenye sayari kama vile Zuhura, mwezi au jua wakiviabudu na kuviomba msaada.
Nabii Ibrahim
akawa anawahoji kwa hoja za kiakili kwa kuithibitisha haki, kuibatilisha batili na kuwaongoza watu kwenye njia iliyonyooka. Akawa nao mpaka ilipotokeza Zuhura. akapiga kelele akisema: "Huyu ndiye mola wangu!" Akangoja mpaka ilipotua, akasema: "Sipendi wanaopotea." Kisha alipoangalia mbinguni akaona mwezi umetokeza upande wa mashariki kama mashua ya fedha inayotembea katika bahari ya nuru. Akasema: "Huyu ndiye mola wangu. Huyu ni mkubwa." Alisema haya kulinganisha ukubwa na nguvu ili kudhihirisha ujinga wao. Mwezi ulipotua na kupotea, akasema: "Asiponiongoza Mola wangu, bila shake nitakuwa miongoni mwa watu wapotevu." Zikapita saa, mara akaona jua linachomoza. Akasema. "Huyu ndiye mola wangu. Huyu mkubwa zaidi." Akakaa pamoja na wale wajinga wanaoabudu jua, akasubiri mpaka lilipotua jua akasema: 'Enyi watu wangu! Mimi simo katika hayo mnayoyashirikisha. Kwa hakika, mimi nimeuelekeza uso wangu kwa Yule aliyeziumba mbingu na ardhi, kwa kujihalisisha. Mimi si miongoni mwa washirikina." (6:77-79) Kwa njia hii hoja zake zilishinda na ikatoweka batili ya watu wake na upotevu wao. Nabii Ibrahim
akashinda katika vita vya kifikra na akawashinda washirikina.
Nabii Ibrahim
hakutosheka na hatua hizi mbili katika kuwaongoza watu kwenye njia ya haki, bali alifikiria njia nyingine itakayovunja ibada ya masanamu na itakayowapeleka watu kwenye ibada ya Mwenyezi Mungu. Mfalme alizizuia fikra za watu zisipanuke na badala yake akizifanya finyu. Hivyo, huwa ni vigumu kuleta mapinduzi hasa ya kiitikadi na kiibada kwa jamii hiyo. Nabii Ibrahim
alingojea muda mrefu mpaka ilipofika siku ya sikukuu ya washirikina, wakatoka kwenda jangwani wakicheza na kusherehekea, na kuziacha tupu nyumba zao. Namrud pamoja na watu wake wakaelekea jangwani. Watu wakamjia Nabii Ibrahim
na wakamtaka aende nao kwenye sikukuu yao, lakini akakataa kwa kujitia ni mgonjwa.
Mji ulipobaki mtupu, akaanza mbinu yake. Akaenda katika nyumba yao ya ibada yenye miungu iliyoganda isiyoona chochote wala kujua lolote akiwa amechukua sururu. Alipofikia kwenye jiwe lililochongwa ambalo linahukumu mimea na roho, akasimama mbele yake. Akaliwekea kila sanamu chakula na kuliambia: "Kula na useme!" Akalipiga kila sanamu kwa sururu na kulivunja vipandevipande. Akafanya hivyo moja baada ya jingine mpaka likabaki sanamu kubwa ambalo akaliwekea sururu kwenye shingo yake. Kisha akarudi akisubiri mambo yatakavyokuwa. Mfalme aliporudi na watu wake, mara wakaona masanamu yamevunjikavunjika, siyo katika hali waliyoyaacha. Wakasema: "Ni nani aliveifanyia hivi miungu yetu?" Baadhi yao wakasema: "Tumemsikia kijana mmoja akiwataja waungu wetu kwa ubaya. Jina lake ni Ibrahim."
Wakamleta Nabii Ibrahim
katika hadhara ya watu. Namrud akamwuliza: "Ni nani aliyewafanyia hivi miungu yetu?'' Nabii Ibrahim
akajibu huku akiwachezea shere na moyo wake ukiwa imara. "Aliyefanya hivyo ni huyo mkubwa wao." Akaashiria lile sanamu kubwa alilolitundikia sururu shingoni mwake. Akasema "Mwulizeni ikiwa anaweza kutamka." Tamko hili likatoa cheche za moto zilizochoma batili na kumwangazia mtu mwangaza na kumwelekeza kwenye akili yake na umbile lake aliloumbwa. Qur'an inasema: "Basi wakajirudi nafsi zao na wakasema 'Hakika nyinyi mlikuwa madhalimu.' Kisha wakainamisha vichwa vyao, (wakasema:) "Hakika umekwishajua kwamba hawa hawasemi.' Akasema: Je, mnaabudu badala ya Mwenyezi Mungu (miungu) isiyokufaeni chochote wala kukudhuru? Kefule yenu na hivyo mnavyoviabudu kinyume cha Mwenyezi Mungu. Je, hamfikiri?' Wakasema: 'Mteketezeni kwa moto na muinusuru miungu yenu, ikiwa nyinyi ni watendao jambo.'" (21:64-68)
Washirikina wakakoka moto waliokusanyia kuni kwa muda mrefu. Wakafikiria kuwa hiyo ni adhabu yake na iwe ni fundisho kwa yule atakayefuata njia nyingine isiyokuwa ya mfalme. Mvuke wa moto ilikuwa mkali kwa kadiri kwamba ungeweza kumchoma ndege aliyepita juu umbali wa farsakh moja yaani kilometa nane. Namrud akakaa juu ya jumba lake kubwa. Nabii Ibrahim
akaletwa mbele ya watu. Wakafikiria namna ya kumtupa motoni kwa vile hawakuweza kuukaribia moto kutokana na ukali wake. Kwa kufuata maelekezo ya Iblisi, wakatengeneza panda kubwa na wakamweka juu yake. Nabii Ibrahim
akakaa imara, hakusikitika wala hakujuta kwa aliyoyafanya, baji lilimfurahusha hilo kwa kuyakinisha kuwa hiyo ndiyo njia ya pekee ya kutekeleza lengo lake.
Azar, ami yake, akaja na kumkuta Nabii Ibrahim
amewekwa kwenye panda bila ya kuwa na wasiwasi wowote. Akampiga makofi na kumwambia: "Wacha mambo yako hayo." Nabii Ibrahim
akakataa kuuacha msimamo wake wa haki. Panda ikavutwa na Nabii Mtukufu akarushwa katika moto. Malaika akamija na kumwuliza kama anataka haja yoyote kwake. Akasema: "Ninaye Mola Ambaye hivi sasa anajua hali yangu."
Alipoukaribia moto, Mwenyezi Mungu aliuambia: "Ewe moto kuwa baridi na salama juu ya Ibrahim.
" (21:69) Mara moto ukageuka kuwa bustani kijani na Nabii Ibrahim
akiwa amekaa kwenye kitandiko akizungumza na Jibril
. Namrud akawa anaangalia mandhari ile kwa mbali. Akapata mfadhaiko kwa kushindwa kwa vitendo vyake, akawa anasema. "Mwenye kutaka kujichukulia Mola na achukue mfano wa Ibrahim." Nabii Ibrahim
akatoka motoni na Namrud akawa hana Ia kusema. Lakini hata hivyo aliendelea na ukafiri wake na kumfukuza Nabii Ibrahim
. Nabii Ibrahim
akayakabili yote hayo kwa moyo imara na thabiti, na hakuacha kusema kuwa Namrud alikuwa kwenye upotofu na kwamba yeye na watu wake wamechukiwa na Mola Mtukufu. Huu ni muhtasari wa historia ya maisha ya Nabi Ibrahim
ambayo imejaa jihadi.
4. NABII MUSA
Karne baada karne zikapita, kizazi baada ya kizazi vikazaliwa, ulimwengu ukaharibika na kurekebika, na watu wengine wakaamini na wengine wakakufuru. Mwenyezi Mungu akawatuma Mitume mmoja baada ya mwingine, na umma ukaendelea na ukafiri na kumkataa Mungu isipokuwa wachache tu. Dola ya Qibtiya ndiyo ikawa yenye maendeleo katika historia ya binadamu. Katika Misri walikuwepo wafalme waliokuwa wakiitwa mafirauni ambao walitawala watu na kumiliki miji na kukawa na ufisadi mwingi. Alikuwepo Firauni mmoja, jina lake Walid bin Musawab ambaye aliwatawala watu na akadai kwamba ni mungu. Alikuwa akiwafanyia watu vile alivyotaka kwa madai kwamba yeye ndiye aliyewaumba, aliyewaruzuku na kuwamiliki. Katika dola hiyo ya Qibtiya, kulikuwepo kundi moja Ia Wana wa Israili (Bani Israil) waliobaki Misri ambao ni wana wa Nabii Ya'qub. Walikuwa ni watu wanyonge, jeshi lao halikuwa na nguvu na walikuwa wakipingana na mafirauni. Mafirauni walikuwa wakiwakandamiza kufanya kazi ngumu na kuwalipa malipo madogo au kuwapa kazi duni; na walikuwa wakiwachukulia kama ni wanyama walioumbwa kwa ajili yao.
Wana wa Israil walikuwa wakingojea kutimia ahadi ambayo ilikuwa ikipokewa kutoka kizazi baada ya kingine kwamba angedhihiri baina yao mtu mmoja ambaye atapambana na Firauni na kumshinda. Kila wakati ulivyozidi kupita ndivyo walivyoendelea kumngoja kwa hamu. Kwa muda mrefu wakamngoja, lakini ahadi yao haikutimia mpaka wakakaribia kukata tamaa. Utawala wa Qibtiya ukazidisha dhuluma ya kinyama kwa kuwachinja watoto wao wa kiume na kuwabakiza watoto wa kike, ili watakapokua wawafanye vijakazi na watumishi wao. Hatimaye, Mwenyezi Mungu akampeleka Nabii Musa
kuwa Mtume wao.Kuzaliwa kwake kulikuwa ni kwa kificho na matatizo kama kuzaliwa kwa Nabii Ibrahim
. Musa akakua katika malezi ya Firauni na akafanywa kama mtoto wake kwa vile hakuwa na mtoto atakayerithi kiti chake. Akawa anaitwa Musa bin Firauni na alikuwa akitembea katika jumba la mfalme vile alivyopenda. Siku moja Mwisraili moja aligombana na Mqibti mmoja. Musa akamsaidia Mwisraili na akampiga ngumi Mqibti ambaye akaanguka chini na kufa. Mkasa huo ukawashtua Waqibti, wakawa wanataka fidia kwa mtu wao. Waliwatilia shaka Wana wa Israili, lakini hawakumjua aliyeua, na wakawa wakimtafuta huku na huko.
Kesho yake, Musa alipokuwa akitembea njiani akamwona yule Mwisraili aliyemsaidia akigombana na Mqibti mwingine. Musa akataka kumsaidia yule Mwisraili, akamkaribia ili amshike Mqibti. Yule Mwisraili akadhania kuwa Musa anataka kumshika yeye. Akapiga kelele huku watu wakimsikia akisema: "Unataka kuniua, ewe Musa kama ulivyoua jana." Watu wakajua kwamba Musa ndiye aliyeua. Firauni akajua kuwa kijana aliyemlea amekuwa adui wake sasa, kwa sababu ameungana na jamaa zake Waisraili kwa kuwasaidia na kutumia nguvu zake kwa ajili ya wanyonge. Kwa hivyo, Firauni akakasirika na akawa anahofia ufalme wake. Akaamrisha auawe. Ili kuiokoa nafsi yake, Musa akakimbia kutoka Misri kuelekea Madain ambapo hapakuwa chini ya mamlaka ya Firauni. Akakaa huko na akaoa binti ya Nabii Shuayb
. Baada ya hapo, Musa akaamua kurudi Misri. Alipofika Mlima Sinai, Mwenyezi Mungu akamtuma na ujumbe wa dini mpya. Akampa azma, uthabiti na miujiza, na akampa ndugu yake Harun kuwa msaidizi wake.
Wakenda kwenye baraza la Firauni, mtawala taghuti, hali ya kuwa wao ni wanyonge wasiokuwa na kitu. Wakataka kumzungumzia mambo aliyoyachukia kwamba aikufurishe nafsi yake na amwamini Mungu, aondoe madai yake ya uwongo ya uungu na amwabudu Mungu Aliye Mmoja. Manabii Musa na Harun
walitaka kufanya jihadi hiyo bila ya kuwa na jeshi, mali au msaada wowote isipokuwa walimtegemea Mwenyezi Mungu tu. Nabii Musa
akaanza kusema: "Mimi ni Mjumbe wa Mola wa viumbe vyote." Firauni akasema: "Basi lete muujiza ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
" (7:104-106).
Akatupa fimbo yake iliyokuwa na ncha mbili, mara ikageuka nyoka. Firauni akaiangalia akaona inatoa ndimi za moto. Akaogopa na kuanza kupiga kelele: "Ewe Musa! Ichukue." Akaichukua na ikageuka fimbo. Firauni akarudi kwenye upotevu wake, akasema: "Hakika hawa wawili ni wachawi." Akataka shauri la watu wake na wasaidizi wake jinsi ya kufanya na hali wamekuja na hoja na dalili za ushindi. Wakamshauri wamfunge Nabii Musa
pamoja na nduguye, kisha wawakusanye wachawi watakaoshindana And from this chain of narrators kwa uchawi na watamshinda, na ndipo itakapokuwa rahisi kuwahukumu. Firauni akawafiki rai hiyo. Wahubiri wawili watukufu wakafungwa pamoja na wachawi wengine wa Kiisraili.
Akatuma katika miji na vitongoji aletwe kila mchawi na kila anayejifundisha uchawi katika vijana wa Kiisraili. Wachawi na watu wengi wakakusanyika katika siku ya sikukuu. Wakaja ili washangilie ushindi wa wachawi na wawafanyie vitimbi Nabii Musa
na Nabii Harun
pamoja na watu woa na wathibitishe ibada ya Firauni na watu wake. Wachawi wakatupa kamba na fimbo zao na zikageuka nyoka wakizunguka huku na huko. Ukawa ni uchawi mkubwa uliowapumbaza watu. Wakawafuata wachawi na hadhi kubwa. Nabii Musa
akatupa fimbo yake, mara ikegeuka nyoka anayokwenda mbiombio, akawameza nyoka wao wote na kuwaogopesha wachawi, Firauni na Hamana, na huku wafuasi wao wakiwa wanashuhudia.
Watu wakaanza kukimbia kiasi ambacho walikuwa wengi kutokana na msongamano wa kukimbizana. Firauni akaanguka na kuzirai. Kisha Nabii Musa
akamchukua nyoka na akarudia kuwa fimbo kama kwanza. Fimbo na kamba zilizokuwa nyoka mbele ya watu zote zikamezwa kama vile hakukuwako na kitu chochote. Wachawi wakashindwa na wakasujuduu na kusema: Tumemwamini Mola wa Harun na Musa." Wachawi na Wana wa Israili wote pamoja na kikundi cha Waqibta wakamwamini Nabii Musa
. Lakini Firauni ambaye hakutaka haki wala mwangaza alibaki katika batili na giza. Firauni akaona kwamba batili inategemea nguvu isiyokuwa na hoja yoyote wala dalili yoyote, hivyo akaamua kuwaadhibu wachawi. Akawaambia: "Kwa nini mmemwamini kabla sijawapa idhini? Hakika huyo ni mkubwa wenu ambaye amewafundisha." Kisha akawatesa vibaya kwa kuikata mikono na miguu yao na akawasulubu kwenye shina Ia mtende. Akawafanya kuwa ni mazingatio na ono kwa anayefikiria kuipinga itikadi ya Firauni au atakayedhihirisha kumfuata Manabii Musa na Harun
.
Firauni mkatili alikuwa akimwadhibu kila aliyemwamini Nabii Musa na nduguye. Mateso yote hayo hayakupunguza kitu katika azma ya Nabii Musa
wala hayakudhoofisha nguvu ya matakwa, ukakamavu na uthibiti wake, bali akaendelea kutangaza upinzani wake dhidi ya Firauni kwa uwazi kabisa, kuongoza kundi lililoniwamini kwenye kheri na kuwakinga kiasi alivyoweza na kumtaka Firauni kuwaachia wafungwa wao. Ingawa Firauni na waziri wake Hamana na askari wao waliendelea na ukafiri na upinzani wao dhidi ya Nabii Musa
, lakini pamoja na yote hayo Nabii Musa
alibaki katika matumaini yake ya kuwaongoza watu wake kwenye haki. Akaendelea kuwalingania katika imani kwa amri ya Mwenyezi Mungu na akawadhihirishia miujiza ya damu, chawa, nzige, tufani, vyura na mengineyo, lakini halikumzidishia hilo Firauni isipokuwa upinzani na ukafiri. Nabii Musa
akapigana jihadi dhidi ya Firauni na watu wake mpaka Mwenyezi Mungu akawaangamiza katika Mto Naili. Baada ya hapo akapigana na Wana wa Israili waasi ambao upinzani wao dhidi ya haki unaendelea hadi hivi leo.
5. NABII ISA BIN MARYAM
Ni utukufu usiokuwa na mpaka ambao lau tungetaka kuuelezea kwa matamko tusingefaulu. Ni mapinduzi yenye kudumu ambayo hayalinganishwi na mapinduzi ya nchi yoyote au maendeleo yoyote, bali ni mapinduzi yaliyo kusanya itikadi, amali (harakati) na haki. Huo ni utukufu tunaouona katika maisha ya Nabii Isa bin Maryam
(Yesu Kristo) aliyefanya mapinduzi ya vikwazo vyote na ufisadi, na akaendeleza jihadi katika uhai wake na akaendeleza vita vya damu mpaka akashinda na ukathibiti ushindi mpaka Siku ya Kiyama. Maryam binti Imran AS alikuwa bibi mwema na mwenye utukufu ambaye alikuwa mfano katika historia ya wanawake. Mama yake aliweka nadhiri kumweka wakfu aliyemo tumboni mwake ili kuitumikia dini. Alipomzaa Maryam
, akasema: "Mola wangu nimemzaa mwanamke!" Kisha akamweka katika nyumba takatifu (Baytul Muqaddas); na Maryam
akawa akisali, akifunga na kuabudu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, akiwa mbali na watu.
Maryam AS akabaki katika mihrabu kwa muda wa miaka kadhaa katika malezi ya Nabii Zakariya
. Kisha akachukuwa mimba kwa idhini ya Mwenyezi Mungu bila ya kuguswa na mwanamume yeyote, kama vile Mwenyezi Mungu alivyoweza kuumba kiumbe bila ya kutanguliwa na kitu chochote au mfano wowote. Ulipomija uchungu wa kuzaa, akajitenga na jamaa zake, akaenda mahali upande wa mashariki mwa msikiti penye shina Ia mtende ambapo akamzaa Masihi ambaye alikuwa mfano bora na msimamo wa kiutu. Kisha akarudi kwa jamaa zake akiwa amembeba. Jamaa zake wakamfokea Maryam: "Umemtoa wapi huyu? Baba yako hakuwa mtu mbaya wala mama yako hakuwa mzinifu!" Akawaashiria mtoto aliyezaliwa, wakasema: "Tutazungumza vipi na mtoto mchanga aliye kitandani?" Walikuwa wakimdhania dhana mbaya bibi huyu mtakatifu, naye akawa hasemi kwa kutekeleza saumu yake ya kutozungumza. Mara mtoto akaanza kuzungumza, akisema: "Hakika mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu, amenipa kitabu na amenifanya Mtume." Nabii Isa
akaziba midomo yao. Masihi Isa
akakua na akawalingania watu kwa sala na saumu na kuwa na tabia nzuri na kuiacha dunia na kuifuata Akhera ambayo ni maisha bora yenye kudumu. Watu wakawa wanampinga kama ilivyokuwa kwa Mitume wengine. Masihi Isa
alikuwa imara kuwaongoza wafuasi wake. Wakawa wanasafiri mashariki na magharibi wakiwahubiria watu na kuwalingania kusimama dhidi ya wafalme na ujeuri wao, ambao walikuwa wamezama katika matamanio ya kidunia. Hakika adhabu kali wanayoipata Mitume kutoka kwa makafiri inatokana na ukosefu wa imani ya watu wao na kuendelea kwao na upinzani juu ya kuwa Mitume wao walikuwa wakiwaonyesha dalili na ushahidi waziwazi.
Nabii isa
alidhihirisha miujiza yake kwa kuwaponesha vipofu na wenye ukoma na kuwafufua watu wakawa wakitoka makaburini mwao wakisema na kujua mambo. Habari hizo zikaenea kwa watu wengi na wakawa wanawapeleka wagonjwa kwake. Kipofu mmoja alikuwa haoni tangu kuzaliwa kwake, Nabii Isa
anampangusa kwa mkono wake mtukufu mara anaanza kuona. Wagonjwa ambao waganga walishindwa kuwatibu waliletwa kwake, naye akawaponesha bila ya dawa yoyote. Mtu mmoja alifiwa na mpenzi wake, akamwendea Nabii isa
, naye akamfufua kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Akamfanya ndege kutokana na udongo, na miujiza mingine kadhaa. Lakini pamoja na miujiza yote hiyo, makafiri waliendelea kumwudhi, kumtukana na kumtoa maanani. Mara nyingine walimtuhumu na kumpiga magumi pamoja na kuwaudhi wafuasi na wasaidizi wake. Wakaendelea na upinzani huo mpaka wakafikiria kumwua kwa kudhani kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya kuizima nuru ya haki. Njama yao ya kumwua ikashindwa, na Mwenyezi Mungu akampaza na wakamwua mtu aliyefananishwa na Nabii Isa
.
MUHTASARI WA VISA VYA JIHADI
1. Mwenyezi Mungu alimtuma Nabii Salih
akiwa na umri wa miaka 16. Alibaki miongoni mwa watu wake kwa muda wa miaka 120, lakini hawakuitika mwito wake. Hakika yeye aliwalingania watu wake kwa miaka 104.
2. Nabii Ibrahim
alikuwa peke yake kuulingania umma kumpwekesha Mwenyezi Mungu wakati giza lilipotanda katika historia ya ulimwengu, na alibaki miongoni mwa watu wake miaka kadhaa, lakini hakuna mtu yeyote aliyemwamini.
3. Nabii Lut
alitumwa Madain katika ardhi ya Sham. Akawahubiria watu, lakini hakukuwazidisha chochote isipokuwa ukafiri na ukanaji; hata mkewe ambaye alikuwa mshiriki katika maisha yake, alikuwa akishirikiana na makafiri.
4. Nabii Yusuf bin Ya'qub
alipigana jihadi na nafsi kama mwamba mbele ya bahari. Alizungukwa na matatizo katika maisha yake yote akiwa ndani ya kisima, pamoja na msafara, katika nyumba ya Aziz, katika jela na mbele ya mfalme. Alipokuwa kifungoni alimwomba Mwenyezi Mungu pekee bila kujali kuwa alikuwa mfungwa aliye mbali na kwao.
5. Nabii Ayyub
alipewa mtihani na Mola wake kwa kuisha mali yake, kufiwa na watoto wake na kupata maradhi katika viungo vyake vyote isipokuwa akili tu! Iblisi akawahadaa watu wake, wakamfukuza na kumweka mbali na mji. Akashukuru na kusubiri mpaka kapona.
6. Mwenyezi Mungu alimtuma Nabii Shuayb
. Wakamkanusha na wakaukanusha Utume wake: wakamfukuza katika mji na wakawaua wasaidizi wake. Akawalingania tu mpaka ikawakuta adhabu.
7. Nabii Khidhr
alikimbia kutoka nyumbani mwa baba yake ambaye alikuwa mfalme. Akaukimbia ufalme akaenda kumwabudu Mwenyezi Mungu na kuwalingania watu kumwabudu Yeye tu.
8. Nabii Daniel
alibaki katika shimo la kisima miaka kadhaa akinywa maji yake na kunywa maziwa ya simba ambaye alitiwa ndani pamoja naye. Chakula choa kilikuwa udongo wa kisima.
9. Nabii Yunus bin Mata
alitumwa kwa watu wake akiwa na umri wa miaka 30 akawa anawalingania kwenye imani kwa muda wa miaka 33. Hawakumwamini isipokuwa watu wawili tu!
10. Mwenyezi Mungu akamtuma Mtume wa Kihabeshi (Kiethiopia) ambaye aliwalingania watu wake kwa Mwenyezi Mungu, lakini wakamkadhibisha, wakampiga vita na wakamchimbia handaki na kumchoma humo pamoja na wafuasi wake. Mpaka hapa tunamaliza muhtasari huu wa historia ya Mitume na Manabii mashujaa, na masaibu waliyoyapata katika njia yao ya mashaka kuelekea kwenye uongofu. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa taufiki na tunamwomba atufanikishe kufuata njia ya Mitume na kuongoka kwa mwendo wao. Hakika Yeye Ndiye Mwenye kutoa taufiki.
Muhammad Taqi al-Mudarrisi
Karbala - Iraq
1385/6 Hijria
1965 Miladia
Kwa jina la Allah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu
1. Hakika waumini wote ni ndugu.
2. Jumuia ya Udugu wa Kiislamu ni taasisi ya
utamaduni yenye malengo yafuatayo:
a) Kueneza fikra na utamaduni wa Kiislamu kwa mapana zaidi.
b) Kustawisha mfungamano wa kindugu na mapenzi kati ya Waislamu.
c) Kusaidiana na taasisi na jumuia zote za Kiislamu na za kibinadamu.
d) Kutoa mchango katika kutatua matatizo ya Kiislamu ili kuusaidia Umma wa leo na kutoa maoni halisi ya Kiislamu.
Kwa hivyo, tunawaomba ndugu wote wa Kiislamu wana wa Umma huu, kusaidiana na kushirikiana nasi katika kutekeleza malengo hayo matukufu. Mnaweza kutuandikia kwa anwani hii
SHARTI YA KUCHAPA
Sharti ya kuchapa au kusambaza ni kutaja rejeo hili. haki zote zimehifadhiwa na Taasisi ya Al-Hasanain Taasisi ya Imamu Husein
Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini
ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini.
MWISHO WA KITABU