MAISHA YA BIBI KHADIJA

MAISHA YA BIBI KHADIJA0%

MAISHA YA BIBI KHADIJA Mwandishi:
Kundi: Waheshimiwa wa Kidini

MAISHA YA BIBI KHADIJA

Mwandishi: Syed A .A .Razwy
Kundi:

Matembeleo: 23480
Pakua: 3009

Maelezo zaidi:

MAISHA YA BIBI KHADIJA
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 16 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 23480 / Pakua: 3009
Kiwango Kiwango Kiwango
MAISHA YA BIBI KHADIJA

MAISHA YA BIBI KHADIJA

Mwandishi:
Swahili

MAISHA YA BIBI KHADIJA

Historia fupi ya maisha yake

KIMEANDIKWA NA: SAYYED A. A. RAZWY

KIMETARJUMIWA NA: AL-AKHY SALMAN Y. SHOU

KIMEHARIRIWA NA: DR. M. S. KANJU

Kimetolewa na kuchapishwa na: Al-Itrah Foundation

P. O. Box 1017

Dar-es-Salaam, Tanzania

Simu: +255 22 2110640

Fax: +255 22 2113107

Email: info@alitrah.org

Website: www.alitrah.org

MAISHA YA BIBI KHADIJA

UTANGULIZI

Khadija, mke wa kwanza wa Muhammad Mustafa, Mjumbe wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na Muumini wa kwanza, ambaye alikuwa na hisia za mtu asiye wa kawaida kabisa. Aliwajibika sana katika historia ya uchanga wa Uislamu. Alikuwa yeye pamoja na Abu Talib, mmoja miongoni mwa watu wawili wafadhili wakubwa kabisa wa Uislamu na Waislamu. Wakati ambapo Uislamu ulikuwa kwenye shinikizo la utekwaji wa kudumu; na ulikuwa umezingirwa kwa kipin-di cha mfululizo wa miaka mitatu, aliudhamini kwa kujitolea kwake mhanga wa kushangaza sana. Uthabiti wake usiobadilika, ushupavu wake, kuwa na uwezo wa kupeleka fikra mbali ya siku za usoni, na uthabiti wa imani yake kwa Mwenyezi Mungu, na kwa ujumbe wa Muhammad Mustafa - Mjumbe wake wa mwisho na mkubwa kuliko wote - haya mambo yalikuwa lazima yawepo kwani humo ndimo Uislamu uliegemea kwa kipindi cha miaka kumi ya mwanzo wake.

Kwa sababu zisizoeleweka, nafasi ya Khadija - ambayo ndiyo ilikuwa kiini cha kujenga hatima ya Uislamu- haijatambuliwa ipasavyo, kutoka kwa waandishi wengi wa wasifu na wanahistoria wa Kiislamu. Utambulisho kama huo ambao wameutoa, ni wa majaribio tu na bila uangalifu. Kwa kadiri ya ninavyo elewa na imani yangu mimi, wasifu halisi na sahihi wa Khadija, bado haujachapishwa. Huu ni upungufu mkubwa wa kusikitisha kwenye mvuto wa maandiko ya Uislamu, hususani wakati ambapo katika nchi za Magharibi kuna mwamko mkubwa wa imani ya Uislamu, na katika simulizi zinazohusiana na viongozi wake katika siku zake za mwanzo.

Maandishi yaliyopo hadi leo juu ya maisha ya Khadija katika vyanzo mbalimbali ni machache na vipandepande. Hata haya maandishi machache na vipande pande sio salama kutokana na maelezo yasiyobadilika au tafsiri potofu ya historia. Mwandishi wa wasifu au mwana historia, lazima alete hali ya msisimko ya kuelewa Uislamu sahihi, na lazima afanye makadirio ya haki ya majukumu ya watu wale ambao wameitengeneza historia yake. Khadija ni mmoja wa watu waliokuwa na uwezo mkubwa na muhimu katika historia yote ya Uislamu. Haiwezekani kuzungumzia historia ya Uislamu bila kuyataja mambo aliyoyafanya kama mchango wake uliofanikisha Uislamu kuendelea kuwepo, kuimarika, na hatimaye kupata ushindi.

Uislamu una deni lisilolipika kwa Khadija. Kwa hiyo, ninaamini kwamba kuchapishwa kwa wasifu wa Khadija - unaoakisi moyo wa kisayansi na kanuni za kisayansi - ambazo wakati fulani niliziona kuwa za muhimu, sasa zinawakabili waandishi wa wasifu na wana historia wa Kiislamu kama sharti la ziada. Sababu nyingine kwa nini inawalazimu Waislamu wote kupata fursa ya kuijua historia ya maisha ya Khadija, ni kwamba, kama alivyo mumewe, Muhammad Mustafa(s.a.w.w) yeye pia ni alama ya umoja wa umma wake. Yeye (Khadija) ni alama ambayo hulea umoja wa umma wa Waislamu.

Juhudi imefanywa kwenye kitabu hiki kuweka pamoja maandishi yote yale juu ya maisha ya Khadija, ambayo yalipatikana katika vyanzo vingi vilivyotawanyika huku na huko. Lakini, hili ni juhudi ambayo lazima likubaliwe kwamba haina matumaini ya kutoshelezea. Huelekeza kwenye mukhtasari tu - ambao utakuwa ni wa kusomwa tu. kwa ajili ya rejea, mpaka hapo wakati utakapokuwa ambako maandiko sahihi zaidi juu ya somo hili yatakapo patikana. Hata hivyo, ni muhimu kwa Waislamu wote, hususan wanawake wa Kiislamu, wajue historia ya maisha ya Khadija na jinsi alivyotumikia Uislamu. Aliunganisha nafsi yake na Uislamu kwa ustadi wa hali ya juu sana hivyo kwamba Khadija alikuwa moyo na kiini cha Uislamu. Kwa maana halisi, Khadija aliishi na kufa kwa ajili ya Uislamu.

Kama wanawake wa Kiislamu wanatafuta furaha hapa duniani na wokovu baada ya kufa, lazima waishi kwa kuiga maisha ya utakatifu wa Khadija. Yeye ni kiongozi wa siri ya kufuzu kupata radhi ya Mwenyezi Mungu; na yeye ndiye mwenye ufunguo utakao wafungulia wao milan-go ya kufuzu katika sehemu mbili, duniani na Akhera. Angefurahi kugawana nao 'siri' hii, kama watataka kujua siri hiyo ni nini, na atafu-rahi kuwapa 'ufunguo' huo, kama watautafuta kutoka kwake. Mwenyezi Mungu na amrehemu Khadija na familia yake.

NENO LA MCHAPISHAJI

Kitabu kilichoko mikononi mwako, ni tarjuma ya kitabu cha Kiingereza, kwa jina la: "Khadijatul-Kubra" kilichandikwa na Mwanachuoni mwanahistoria na mtafiti, Sayyed A. A. Razwy Bibi Khadija alikuwa ndiye mke wa kwanza wa Mtukufu Mtume. Bibi huyu alikuwa tajiri miongomi mwa matajiri wakubwa wa Makka. Mtume alikuwa na miaka 25 alipomuoa bibi huyu, aliopofikisha miaka 40, alitoa tangazo la kwanza la utume wake, mtu wa kwamza kuamini utume wake alikuwa ni bibi Khadija, na hivyo kuamini Upweke (tawhid) wa Allah swt. Na kuwa Mwislamu wa kwanza ulimwenguni. Waabudu masanamu wa Makka hawakufaurahishwa na tangazo hili, ukazuka uadui mkubwa sana kati ya Mtukufu Mtume na waabudu masanamu hawa. Kutokana na hali hii ilibidi Khadija atumie utajiri wake wote kuuhami Uislamu chini ya hifadhi kubwa ya ami yake Mtume, Abu Talib. Mchango wa bibi huyu ni mkubwa sana katika Uislamu, lakini bahati mbaya yeye na Bwana Abu Talib wamekuwa ni madhulumu wa historia ya Uislamu. Si wanahistoria Mustashirik tu, bali hata wanahistoria wa Kiislamu wamekwepa kuandika wasifu wake kwa ukamilifu kama ambavyo wamekwepa kuandika kwa ukamilifu wasifu wa Bwana Abu Talib na kumsingizia ukafiri.

Katika kitabu hiki mwandishi ameandika angalau kwa kiasi cha kurid-hisha wasifu wa Bibi Khadija. Wasifu huu umeanzia kabla ya kuolewa na Mtukufu Mtume na baada ya kuolewa naye. Na mwandishi ameji-tahidi kuandika matukio muhumi yanayohusiana na bibi huyu, kwa kutumia vyanzo sahihi vya Kiislamu. Kutokana na umuhimu wa maudhui ya kitabu hiki, tumeona tukutoe kwa lugha ya Kiswahili ili kizidishe mwanga wa elimu kwa Waislamu wazungumzaji wa Kiswahili. Na hili ndilo lengo kubwa la Taasisi yetu ya 'Al-Itrah Foundation' katika kuwahudumia Waislamu, hususan wazungumzaji wa Kiswahili. Tunamshukuru Ndugu yetu al-Akhy Salman Y. Shou kwa kukubali jukumu hili la kukifanyia tarjuma kitabu hiki. Vile vile tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwa kitabu hiki. Mchapishaji: Al-Itrah Foundation S. L. P. 1017 Dar-es-salaam.

MAISHA YA BIBI KHADIJA

SURA YA KWANZA

MAKKAH MNAMO KARNE YA SITA

Mnamo Karne ya Sita A.D. Makka ilikuwa soko muhimu Arabuni. Mji huu ulikuwa kituo cha kimataifa cha biashara na uchuuzi. Mizigo kuto-ka India yenye bidhaa kama viungo, matunda, nafaka, vyombo vya ufinyanzi na nguo vilikuwa vikiteremshwa kwenye bandari za Yemen na kutoka hapo bidhaa hizo zilibebwa pamoja na zile za Arabu ya Kusini, kama vile kahawa, dawa, manukato na mafuta mazuri kwa kutumia ngamia kwenda Makka, na kutoka hapo kuendelea Syria hadi nchi zili-zozunguka bahari ya kati.

Makkah yenyewe ilikuwa kituo cha misafara mingi ya "udi na ubani" ya Arabuni na "viungo" vya India. Misafara mingine ilipitia Makka na Yathrib wakati inaelekea kaskazini ambako iliungana na misafara ya njia kubwa ya biashara ya hariri toka China. Misafara kutoka kaskazini, pia ilisimama Makka. Ngamia na farasi walibadilishwa hapo na mahitaji kujazwa tena hapo na halafu misafara huendelea hadi kwenye bandari za kusini ya rasi ya Bahari ya Arabuni.

Aidha, Makka ilikuwa kituo cha kubadilishana mali na bidhaa kwa ajili ya makabila ya Kiarabu yasiyo hamahama na yale yanayo hamahama; na ilikuwa sehemu ya kugawa bidhaa za kilimo na zilizotengenezwa na kupelekwa katikati ya Hijaz. Makabila hayo yalikuja kutoka mbali katikati ya Arabuni na hata Arabia ya mashariki kwa madhumuni ya kununua bidhaa hizo ambazo zilikuwa hazipatikani nchini kwao. Sehemu kubwa ya biashara hii ya maingiliano ya makabila ilifanyika Makka kwa mfumo wa kubadilishana mali kwa mali.

Makuraishi wa Makka walikuwa kabila muhimu sana kutoka Magharibi ya Arabuni. Wote walikuwa wafanyabiashara wakubwa. Kwa kufanik-isha usafirishaji wa hariri kutoka China, bidhaa kutoka Afrika Mashariki na vitu vya thamani kutoka India - Makuraish walitawala biashara kati ya ustaarabu wa Mashariki na ule wa nchi za Bahari ya Mediterania. Ni dhahiri kwamba sehemu kubwa ya biashara hii ilikuwa ya bidhaa za anasa, lakini bidhaa za kawaida pia zilikuwepo kwenye biashara, kama vile nguo za rangi za zambarau, majora ya nguo, nguo zisizowekwa urembo wa kufuma na zile ambazo ziliwekewa nakshi ya dhahabu, zafarani, melimeli, majoho, mablanketi, mishipi, manukato ya mgando, mvinyo na ngano.

Kwa jinsi hii, uzalishaji, uuzaji, ubadilishaji na usambazaji wa bidhaa, kuliwafanya Makuraishi kuwa matajiri. Lakini palikuwepo na kitu kingine kilichowafanya kuwa matajiri. Al-Kaaba na Jiwe lake Jeusi lilikuwa mashuhuri, vilijengwa mjini Makka. Waarabu walikwenda Makka kuhiji na kuitembelea Al- Kaaba. Kwao Makka ilikuwa takatifu kama vile Jerusalem ilivyokuwa kwa Wayahudi na Wakristo. Al-Kaaba ilikuwa hekalu kubwa la miungu wa masanamu waliomiliki-wa na koo za makabila mbalimbali ya Kiarabu. Mahujaji walileta sadaka nyingi na zisizo za kawaida kwa ajili ya kuwafurahisha wale Miungu Sanamu waliowaabudu. Mahujaji waliporudi makwao, makuhani wa hekalu walichukuwa sadaka zote kuwa mali yao. Misafara ya hija ilikuwa njia moja yenye kuwaingizia mali nyingi sana raia wa Makka.

Hata kama Makuraishi wa Makka wasingejishughulisha na biashara, bado wangenufaika na kutajirika kwa kazi za kutoa huduma mbalimbali ambazo walizifanya kwa kipindi cha mwaka mzima kuhudumia misafara ya biashara na mahujaji kutoka Kusini kwenda Kaskazini na kutoka Kaskazini kwenda Kusini. Lakini kama ambavyo imekwisha fahamika mwanzoni Makuraishi wengi walikuwa wafanya biashara hodari, kwa hiyo walileta utajiri mwingi Makka kutoka nchi jirani.

Ingawaje wafanya biashara wa Makka walipeleka msafara mmoja tu Syria na mmoja Yemen kwa kipindi cha mwaka mzima, palikuwepo na misafara mingine mingi sana midogo midogo ambayo ilifanya biashara katika sehemu nyingi za ghuba ya Uajemi mwaka mzima. Mingi ya misafara hiyo ama ilianzia humo humo Makka au ilipitia Makka kwen-da sehemu nyingine. Kwa hiyo, kulikuwepo na msongomano mkubwa wa misafara ya biashara Makka. Misafara ilitofautiana kwa ukubwa. Kuanzia Misafara ya "wenyeji" iliyo na kiasi cha chini kabisa ngamia kumi, mpaka ya misafara ya "kimataifa" yenye wingi wa ngamia kiasi cha kufikia maelfu. Kupanga misafara ya biashara ilikuwa shughuli kubwa katika Bara Arabu.

SURA YA PILI

Maisha ya Mwanzo ya Khadija alizaliwa Makka. Alikuwa mtoto wa kike wa Khuwaylid bin Asad bin Abdul Uzza bin Qusayy. Qusayy alikuwa babu aliyejulikana sana kwenye ukoo wa Khadija vile vile kwenye ukoo wa Muhammad Mustafa, wa uzao wa Bani Hashim, aliyekuja kuwa Mtume wa Uislamu(s.a.w.w) . Kwa hiyo Khadija alitokana na nasaba yenye asili moja na Bani Hashim. Baada ya Bani Hashim, familia yake ilikuwa tukufu na yenye kuheshimika sana Arabuni pote. Familia ya Khadija haikuwa mashuhuri kwa utajiri tu bali pia kwa ubora wa tabia yake. Khuwaylid, baba wa Khadija pia alikuwa mfanyabiashara kama wenzake wengine wengi wa kabila la Quraysh wa Makka. Kama walivyokuwa wafanyabiashara wa kabila la Qurayshi wengi, baba yake Khadija naye alipata mafanikio ya utajiri kutokana na biashara ya nje. Wafanyabiashara wa Makka walituma misafara miwili kila mwaka mmoja wakati wa kiangazi ambao ulikwenda Syria na mwengine wakati wa kipupwe ambao ulipelekwa Yemen.

Misafara hii ya kibiashara ilibeba mazao ya jangwani na bidhaa zilizo tengenezwa Makka na sehemu za jirani yake na ziliuzwa kwenye masoko ya Syria na Yemen. Aidha waliuza farasichotara Syria. Aina hii ya farasi ilithaminiwa sana Syria na nchi jirani. Baada ya kuuza bidhaa zao na farasi-chotara wao, wafanyabiashara hao walileta nafaka, mafuta ya zeituni, matunda, kahawa, nguo, bidhaa za anasa na vitu vingine vilivyotengenezwa kwa ajili ya kuviuza Makka. Hivyo walipata faida Syria, Yemen na Makka. (Biashara hii ya Makka imetajwa kwenye Qur'ani Majid, Sura ya 106) Biashara ya nje ilikuwa ndio msingi mkubwa wa uchumi wa Makka. Makka ilikuwa haina ardhi ya kilimo wala maji ya kilimo cha umwagiliaji. Watu wa Makka, katika hali hiyo, hawakuweza kulima mazao ya chakula. Walitegemea biashara baina yao na Syria na Yemen ili wajilishe. Kutokana na faida waliyopata walinunua nafaka na vitu vingine muhimu katika maisha.

Kila msafara ulikuwa na kiongozi. Kiongozi huyu alitakiwa kuwa mtu mwenye sifa zisizo za kawaida. Usalama na kufaulu kwa msafara katika biashara ya mauzo na manunuzi, ilitegemea sana maamuzi ya kiongozi. Kiongozi alikuwa na kazi ya kulinda msafara usishambuliwe na wanyang'anyi na mabedui wa jangwani. Kiongozi aliweza kufanya kazi hii kwa kuandikisha wapiganaji kutoka makabila mbalimbali na kuunda vikosi kufuatana na ukubwa wa msafara. Vikosi vilisindikiza misafara mpaka mwisho wa safari. Misafara yote iliyokwenda masafa marefu, ilikuwa chini ya ulinzi wa kijeshi.

Kiongozi wa msafara pia alitakiwa kuwa na kipaji cha pekee kwa kumuongoza kwenye jangwa lisilo na njia wakati wa mchana, na alitakiwa kuwa na uwezo wa kutambua njia ya msafara wakati wa usiku. Kiongozi alitakiwa kuwa na ujuzi wa kuzitumia nyota katika safari wakati wa usiku. Alikuwa anatakiwa kuhakikisha kuwepo kwa maji wakati wa safari ndefu ya kwenda Syria au kwenda Yemen. Alitakiwa kuchukuwa tahadhari dhidi ya majanga yasiyotegemewa kama vile kim-bunga cha mchanga na msongamano wa miale ya taa za misafara. Alikuwa anatakiwa kuwa na uwezo wa kutoa huduma ya kwanza ya tiba endapo msafiri aliugua au aliumia. Kwa ujumla, kiongozi alitakiwa kuwa na uwezo wa kushughulikia dharura yoyote ile. Wafanyabishara wa Makka, walimteua kiongozi wa misafara yao baada ya kuchunguza historia yake kwa uangalifu sana. Jopo la wasafiri wazoefu lilipitia majina ya watu waliopendekezwa kwa kazi hiyo.

Jopo la wachunguzi halikuridhishwa na sifa yoyote iliyo chini ya kiwango cha uwezo wa kiongozi wa msafara kuongoza kwa ustadi kwenye njia zisizo na michoro kwenye "bahari" ya mchanga, na kufaulu kwake kurudisha misafara ya "meli za jangwa" yaani ngamia pamoja na mizigo yao nyumbani salama. Ili akubalike kwa jopo, mtahiniwa alitakiwa kuonyesha kwamba alikuwa na uzoefu wa kutosha sana kuhusu utarati-bu wa usafirishaji wa misafara ya biashara na "vitambulisho" vyake vil-itakiwa awe hana kosa.

Mama yake Khadija alikufa mnamo mwaka wa 575 A.D.,na Khuwayled baba yake, alikufa mnamo mwaka wa 585 A.D. Baada ya kifo cha Khuwayled, watoto wake walirithi utajiri wake na waligawana mali hiyo. Utajiri una hatari zake. Utajiri unaweza kumfanya mtu akaishi maisha ya kubweteka na anasa. Khadija alitambua tabia ya utajiri kwa undani, na aliamua kutoruhusu utajiri kumfanya yeye asifanye kazi. Khadija alikuwa na akili ya kiwango kisicho cha kawaida na uwezo wa tabia ya kuishinda changamoto ya utajiri, na aliamua kujenga himaya ya urithi kutoka kwa baba yake. Alikuwa na ndugu wengi lakini miongoni mwa wote hao, ni yeye peke yake ndiye aliyerithi uwezo wa baba yao kuwa tajiri. Lakini alionyesha katika kipindi kifupi sana kwamba hata kama hangekuwa amerithi utajiri wa baba yake, bado angeweza kupata utajiri kwa bidii yake mwenyewe.

Baada ya kifo cha Khuwayled, Khadija alichukuwa kazi ya kusimamia biashara ya familia na aliipanua haraka sana. Faida aliyoipata aliwasaidia fukara, wajane, watoto yatima, wagonjwa na wasiojiweza. Endapo palikuwepo na wasichana fukara, Khadija aliwasaidia waolewe na aliwapa mahari. Mmoja wa wajomba zake alijitolea kumsaidia kama mshauri wake katika kuendesha biashara, na ndugu zake wengine katika familia pia walimsaidia katika biashara wakati wowote alipohitaji msaada wao. Lakini hakumtegemea mtu yeyote katika kufanya uamuzi. Khadija alitegemea zaidi uamuzi wake mwenyewe ingawaje alikubali kushauriwa na kufikiria namna ya kuutumia ushauri huo. Ndugu wakubwa katika familia walitambua kwamba alikuwa hapendi ubia.

Wafanya biashara wengi waliokuwa na mizigo ya kuuza Syria au Yemeni, walisafiri na misafara yao wenyewe na kushugulikia mauzo yao binafsi. Lakini wakati mwingine mfanyabiashara alishindwa kuon-doka Makka. Katika hali kama hiyo mfanyabiashara huyo alimkodi mtu kwenda na msafara badala yake. Mtu aliyeteuliwa kwa madhumuni haya, alitakiwa awe na tabia njema kwa uaminifu wake na uwezo wa kufanya biashara. Mtu wa namna hii aliitwa Wakala au Meneja.

Khadija alikuwa mtu wa nyumbani pia ndugu zake na binamu zake hawakupenda kusafiri na misafara. Kwa hiyo, alimuajiri wakala wakati wowote msafara ulipotoka kwenda nje ya Hijazi, na kumfanya wakala huyo kuwa na madaraka ya kupeleka bidhaa zake kwenye masoko ya nje kuziuza huko. Kwa uwezo mzuri wa kuteua mawakala, na kununua na kuuza wakati na mahali muafaka aliweza kupata faida kubwa sana, na baadaye, akawa mfanyabiashara tajiri sana wa Makka. Ibn Sa'ad anase-ma kwenye Tabqaat yake kwamba misafara ya wafanya biashara wa Makka ilipoanza safari, mzigo wa Khadija peke yake ulikuwa sawa na mizigo ya wafanyabishara wengine wote wa Qurayish katika msafara huo. Alikuwa dhahiri kwa kila mtu ni kama msemo "golden touch" "mguso wa dhahabu" yaani kila atakacho kigusa hata kama ni vumbi litageuka kuwa dhahabu. Watu wa Makka, katika hali hiyo, walimpa jina la Malkia wa Qurayish. Aidha walimwita Malikia wa Makka.

Wakati huo Bara Arabu ilikuwa jamii ya kipagani, na Waarabu wali-abudu masanamu mengi na miungu masanamu, ambao waliamini walikuwa na uwezo wa kuleta bahati njema kwao. Lakini ibada yao ya kuabudu masanamu haikuwa adilifu na ilikuwa ibada ya kishenzi, tabia, mila zao na adabu zilikuwa za kukatisha tamaa. Ulevi ulikuwa mojawapo wa uovu wao, na walikuwa wacheza kamari wasiokanyika. Walikuwa wanagaagaa kwenye shimo la dhambi na ujinga. Qur'an Majid inasadikisha hali yao kwenye Aya ifuatayo:

هُوَ الَّذِي بَعَثَ فِي الْأُمِّيِّينَ رَسُولًا مِّنْهُمْ يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِهِ وَيُزَكِّيهِمْ وَيُعَلِّمُهُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَإِن كَانُوا مِن قَبْلُ لَفِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٢﴾

"Yeye ndiye aliyempeleka Mtume kwenye watu wasiojua kusoma, awa-somee Aya zake na awatakase na awafunze Kitabu na Hekima, ijapokua kabla ya haya walikuwa katika upotofu ulio dhahiri" (Qur'an 62:2).

Lakini si kwamba nchi ilikuwa haina watu ambao waliona ibada ya masanamu kuwa ya kuchukiza. Watu hawa ambao walikuwa wachache sana kwa idadi waliitwa "Mahanifi" ("Hanifs") yaani wanaume na wanawake "ambao waliasi ibada ya kuabudu masanamu." Makka nayo ilikuwa na watu hao wachache kwa idadi "Mahanifi" na baadhi yao walikuwa kwenye ukoo wa Khadija. Mmoja wao alikuwa binamu yake wa kwanza, Waraqa bin Naufal. Waraqa alikuwa mkubwa katika ndugu zake wote, na nywele zake zote zilikwisha kuwa rangi ya jivu. Aliwashutumu Waarabu kwa kuabudu masanamu na kwa kuacha njia ya kweli ya mababu zao - Mitume Ibrahim na Ismaili. Ibrahim na Ismaili walifundisha somo la Tauhiid -Imani ya Kumpwekesha Muumba. Lakini Waarabu walisahau somo hilo, na wakaingia kwenye shiriki. Waraqa aliwadharau Waarabu kwa ibada yao ya kishirikina na maadili ya ufisadi. Yeye mwenyewe alifu-ata dini ya Mtume Ibrahim, mtumishi wa kweli na Mwaminifu wa Mwenyezi Mungu. Hakumshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu chochote. Hakuwa mlevi na hakucheza kamari. Na alikuwa mwema kwa fukara na walioishiwa.

Mojawapo ya tabia za kutisha za Waarabu wakati ule ilikuwa ni kuwazi-ka watoto wa kike wakiwa hai, punde wazaliwapo. Pale ambapo Waraqa alisikia kwamba mtu alitaka kumzika mtoto akiwa hai, alik-wenda kumshauri mtu huyo asifanye hivyo, na kama sababu ya kumuua mtoto huyo ilikuwa umaskini, alijitolea kumkomboa mtoto huyo na kumlea kama mtoto wake. Katika mifano mingi, baba wa mtoto alijutia kosa lake baadaye, na alikuja kumdai mtoto wake. Waraqa alikuwa aki-taka ahadi thabiti kutoka kwa baba mhusika kumpenda mwanae wa kike na kumtendea wema, na hapo tu ndipo alipomruhusu amchukue.

Waraqa aliishi kwenye zama za ulimwengu wa upagani. Ulimwengu karibu ulikuwa unakaribia kufurika Mwanga wa Uislamu - Dini ya Mwenyezi Mungu - iliyo bora sana - Imani ya zama za kale, iliyoanzishwa karne nyingi za nyuma na Ibrahim Rafiki na Mtumishi wa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Alikwisha mteuwa Mtumishi wake Muhammad Mustafa bin Abdullah, wa ukoo wa Bani Hashim, kuwa Mjumbe Wake mpya na wa mwisho hapa duniani. Mtume Muhammad(s.a.w.w) alikuwa anaishi Makka wakati huo lakini alikuwa bado hajatangaza ujumbe wake.

Waraqa alikuwa mmojawapo wa watu wachache sana wa Makka walioelimika. Inasemekana alitafasiri Biblia kutoka kwenye lugha ya Kiebrania kuwa Kiarabu. Aidha alikwisha soma vitabu vingine vilivyoandikwa na wanatheolojia Wayahudi na Wakristo. Alikuwa mtafutaji makini wa ukweli ndani ya giza la dunia inayoendelea kuwa ndani ya giza nene zaidi, na alikuwa na nia ya kuupata ukweli huo kabla ya kifo chake, lakini hakujua angeupataje. Khadija aliathiriwa sana na fikira za Waraqa na alikubaliana na Waraqa kuichukia ibada ya masanamu na watu waabuduo masanamu. Hakumshirikisha Muumba na kitu chochote. Kama alivyokuwa Waraqa na ndugu wengine katika familia, naye pia alikuwa mfuasi wa Mitume Ibrahim na Ismaili. Khadija alikuwa Muwahhid (mwenye kumwamini Mungu Mmoja wa Pekee)! Khadija hakujua kwamba baada ya miaka michache hatima yake ingeingiliana na hatima ya Muhammad Mustafa, Mtume wa Imani ya Mungu Mmoja (Tauhiid); na hatima ya Uislamu, imani ya Mungu Mmoja.

Kabla ya Uislamu Bara Arabu ilikuwa haina mpango wowote wa kisi-asa, na haikuwa na miundo mbinu ya aina yoyote. Hapakuwepo na mahakama au polisi au mfumo wowote wa sheria. Kwa hiyo, hapakuwepo na chombo cha kuzuia utendaji wa makosa, au kuwazuia wahalifu. kama Mwarabu alifanya kosa, hakuonyesha kujuta kokote. Badala yake alijivuna na kutamba kwamba angeweza kufanya lolote bila kujali, na kuweza kuwa katili na mkorofi. Rasi yote ya Arabuni iliendeshwa kwa mfumodume. Mwanamke hakuwa na daraja kwa vyovyote vile. Waarabu wengi waliamini kwamba wanawake walileta mikosi. Kwa ujumla waliwaona wanawake kama mali inayohamishika na si watu. Mwanaume aliweza kuoa wanawake wengi kwa idadi aliyopenda. Na wakati akifa, mtoto wake wa kiume wa kwanza aliwarithi wanawake (wakeze marehemu baba yake) wote isipokuwa mama yake. Kwa maneno mengine aliwaoa mama zake wa kambo wote isipokuwa mama yake aliyemzaa. Jambo kama hili, sheria na kanuni za maadili hazikuwepo kumzuia kwa njia yoyote ile. Uislamu ulisitisha desturi hii kisheria.

Waarabu walioishi kabla ya Uislamu hawakuwa na maadili mema. Mwarabu alitumia maisha yake yote kwenye ghasia za kivita. Mauaji na uporaji ilikuwa ndio kazi yake kubwa. Aliwatesa wafungwa wake wa kivita hadi kufa, na kuwatesa wanyama ilikuwa moja ya mambo yake ya kupitisha wakati. Mwarabu alikuwa na ukaidi wa hisia ya utukufu, ambao ulifanya auwe mtoto wake mwenyewe wa kike. Kama mkewe alizaa mtoto wa kike, alikuwa hawezi kuzuia uchungu na hasira zake.

وَإِذَا بُشِّرَ أَحَدُهُم بِالْأُنثَىٰ ظَلَّ وَجْهُهُ مُسْوَدًّا وَهُوَ كَظِيمٌ ﴿٥٨﴾ يَتَوَارَىٰ مِنَ الْقَوْمِ مِن سُوءِ مَا بُشِّرَ بِهِ أَيُمْسِكُهُ عَلَىٰ هُونٍ أَمْ يَدُسُّهُ فِي التُّرَابِ أَلَا سَاءَ مَا يَحْكُمُونَ ﴿٥٩﴾

Na mmoja wao akibashiriwa kwa msichana, uso wake unasawijika, naye kajaa chuki. Anajificha asionekane na watu kwa ubaya wa aliyo bashiriwa! Je, akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni? Tazama uovu wa wanavyo hukumu!. (Qur'ani 16:58-59)

Mara nyingi Mwarabu alimuua mwanae wa kike kwa kuogopa kwamba angekuwa mateka wa kivita wakati wa vita vya kikabila, na kwa hiyo, kuwa mtumwa wa adui, na daraja lake kama mtumwa kungeleta aibu kwa familia yake na kabila lake. Angeweza pia kumuua kwa kuhofia kwake umasikini. Aliamini kwamba binti yake angekuwa tatizo la kiuchumi kwake. Uislamu ulifanya mauaji ya watoto kuwa ni dhambi kubwa kabisa.

وَلَا تَقْتُلُوا أَوْلَادَكُمْ خَشْيَةَ إِمْلَاقٍ نَّحْنُ نَرْزُقُهُمْ وَإِيَّاكُمْ إِنَّ قَتْلَهُمْ كَانَ خِطْئًا كَبِيرًا ﴿٣١﴾

"Wala msiwaue wana wenu kuogopa umasikini. Sisi tunawaruzuku wao na nyinyi. Hakika kuwaua hao ni hatia kubwa." (Qur'an 17:31).

Vilevile walikuwepo Waarabu ambao hawakuwaua watoto wao, lakini waliwanyang'anya haki zao zote. Walifikiri kwamba kwa vile binti zao watakapoolewa watakwenda kuingia nyumba nyingine za waume wao, hapakuwepo na haja ya kutumia gharama yoyote juu yao. Ilikuwa katika mazingira ya namna hii ambayo Khadija alizaliwa, akakua na kuishi mazingira ya "kumkataa mwanamke." Kutokea nyumbani kwake Makka, Khadija aliendesha biashara iliyokuwa inaendelea kukua na kuenea kwenye nchi za jirani. Kile ambacho alikwisha faulu kukipata kingekuwa cha kusifika katika nchi yoyote, katika kipindi chochote na kwa mtu yoyote mwanamume au mwanamke. Lakini mafanikio yake yamesifika mara mbili pale ambapo mtu atafikiria ule "mfumodume" wa kumpinga mwanamke, ulioen-dekezwa na Waarabu. Huu ni uthibitisho wa uwezo wake wa kumudu hatima yake kwa kutumia akili yake, nguvu ya dhamira na tabia. Wafanyabiashara wenzake walikubali mafanikio yake walipomwita Malikia wa Makuraishi na Malkia wa Makka kama ambavyo imetamk-wa huko nyuma.

Lakini zaidi ya sifa, Khadija pia alipata cheo cha tatu. Aliitwa "Twahira" maana yake ni "aliyetakasika." Nani aliyempa cheo cha "Twahira"? Ajabu ni kwamba, alipata cheo hiki, kutoka kwa Waarabu haohao waliokuwa na sifa mbaya kwa ujeuri, majivuno, kiburi na ujinsia. Lakini, tabia ya Khadija ilikuwa mfano mzuri wa kuigwa hivyo kwamba ilitambuliwa hata na wao, na wakamwita "aliyetakasika." Ilikuwa ni kwa mara ya kwanza katika historia ya Arabuni kwa mwanamke kuitwa Malikia wa Makka na aidha kuitwa "Twahira." Waarabu walimwita Khadija Malkia wa Makka kwa sababu ya utajiri wake na walimwita Tahira kwa sababu ya utakatifu wa sifa zake. Pia walikuwa wanaelewa kwamba alikuwa na tabia njema. Kwa hiyo alikuwa mtu wa kuheshimika hata kabla ya Uislamu - kipindi cha Ujahiliya.

Ilikuwa ni jambo lisilopingika kwamba Khadija angetamaniwa na Waarabu mashuhuri na wana wa Wafalme. Wengi wao walipeleka posa ili wamuoe. Lakini hakutaka kuolewa na yeyote kati yao. Wengi wa hao watu mashuhuri na wana wa Wafalme waling'ang'ania kutaka wamuoe. Bila kukatishwa tamaa na kukataa kwake, waliendelea kutumia washen-ga wanaume na wanawake wenye kuheshimika kuendelea kumbem-beleza. Lakini bado aliwakataa wote. Hii labda ni kwa sababu Khadija hakutilia maanani sana umuhimu wa uongozi wa mfumo-dume uliotawaliwa na wanaume katika jamii "inayowapiga vita wanawake." Kukataa kwa Khadija kuolewa na Waarabu mashuhuri na wenye hadhi za juu, kulizua dhana nyingi kwamba ni mwanamume wa aina gani atakaye muoa. Lilikuwa ni Swali ambalo hata Khadija mwenyewe hakuweza kulijibu. Lakini majaliwa yalifahamu jibu lake; alikuwa aolewe na mwanaume ambaye si tu alikuwa bora kabisa kuliko wote katika nchi yote ya Arabu lakini alikuwa pia bora sana kuzidi viumbe wote. Ilikuwa ni majaliwa yake iliyomchochea kukataa maombi ya kuolewa na binadamu wa kawaida.