TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA13%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Juzuu 9 Juzuu 10 Juzuu 11
  • Anza
  • Iliyopita
  • 20 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 39046 / Pakua: 4793
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu. Kitabu hiki kilicho mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London. Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo. Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana `kwenda na wakati. Sifa kubwa ya pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kungangania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo suala la madhehebu ni nyeti nchini humo,hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea, hiyo ilmsaidia sana hata

kuweza kutoa kitabu kiitwacho Al-Fiqh alaa madhaahibil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka hivi karibuni Inshaallah). Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri,na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa. Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Ruhusa imetolewa kwa yeyote anaetaka kukichapisha upya kitabu hiki kwa sharti tu kwamba asibadilishe chochote bila ya kutujulisha, na atutumie nakala moja baada ya kukichapisha. Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji. Mwisho, shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.Mchapishaji.

CHAPA YA PILI

Kutokana na maombi mengi ya wasomaji wetu wa Kiswahili, ambao ni wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu, walioko Afrika Mashariki na Kati, Uarabuni na hata nchi za Ulaya, tumeonelea kukichapisha tena Kitabu hiki ili kupunguza kiu yao kama si kuiondoa kabisa. Tafauti iliyojitokeza katika chapa hii ya pili ni utaratibu mpya uliotumika, ambapo baada ya Aya kufasiriwa, maelezo yake yanapatikana moja kwa moja chini yake bila ya kwenda kwenye ukurasa mwingine, na utaratibu huu ndio utakaotumika katika chapa zote zitakazofuata.

Vilevile tumejaribu sana kusahihisha baadhi ya makosa ambayo kibinadamu yalikuwa yamefanywa katika toleo la kwanza. Hatuna budi kuwashukuru wote waliotumia wakati na akili zao katika kufanikisha lengo hili adhimu, bila ya kuwasahau wafadhili na wasimamizi wetu.Mwenyezi Mungu awalipe kheri nyingi. Vilevile tunawashukuru sana wasomaji wetu amabao waliotukosoa, hivyo kuchangia, kwa kiasi kikubwa, kuisahisha chapa hii.Na tunawaomba waendelee kufanya hivyo. Mchapishaji

 DIBAJI

Sifa njema zote zinamstahiki Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe. Baada ya hayo: Mimi nimetunga mfululizo wa vitabu vidogo vidogo katika itikadi na misingi yake. Nimevitunga kulingana na mfumo na mantiki ya kizazi cha kisasa, ambacho hakiamini kitu ila kile kinachokitaka na chenye kuafikiana na malezi yake na maendeleo yake.

Alhamdulillah Mwenyezi Mungu amejaalia tawfiki na kufaulu kwa mfululizo huo na umerudiwa kuchapishwa mara nyingi. Kimsingi ni kuwa kila kazi inayoafikiana na hekima na lengo inayolikusudia, Mwen-yezi Mungu huipa ufanisi na tawfiki. Hakika tawfiki inatokana na Mwenyezi Mungu, hakuna shaka, lakini Mwenyezi Mungu amekataa kupitisha mambo isipokuwa kwa njia yake na desturi yake.

Kuandika juu ya karatasi tu, sio sharti la kufaulu katika kitu chochote; isipokuwa kufaulu ni kumridhisha na kumpendeza msomaji kile atakachokisoma. Msomaji naye hawezi kuridhia kitabu chochote, isipokuwa kiwe kwa ajili yake na sio kwa ajili ya mwandishi.Na huko kuridhia kunampa nguvu mwandishi kuendelea. Hapo ndipo msomaji na mwandishi wanapoathiriana. Kwa vyovyote ilivyo, kuenea kwa mfululizo huo wa vitabu vidogo vidogo kumenipa nguvu ya kutunga vitabu vikubwa na vipana; kama vile: Maalimu Falsafatil Islamiya, Alfiqhu Ala Madhahibil Khamsa, Fadhail Imam Ali n.k.

Mwenyezi Mungu naye akavifanyia vitabu hivi kama alivyofanyia vile vingine. Nikapata msukumo wa kutunga Fiqhul Imam Jaffar Assadiq katika juzuu sita kubwa; nacho kikawa kama vingine vilivyotangulia. Kwa hiyo vikanipa msukumo wa kutunga kitabu kikubwa na kitukufu, Tafsir ya Qur`an ambayo nimeiita Tafsir Al -Kashif.

Kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu na nguvu Zake, vile vile kwa tawfiki Yake na fadhila Zake, imetimia juzuu hii ninayow-aletea. Ndani yake mna Sura mbili kamili za Al-Fatiha na Al-Baqara. Sijui kama uhai utaniruhusu nione natija ya lile nililojitolea mhanga, au kwamba kudra itafanya kinyume? Na kama ikitimia Tafsir Al-Kashif je, itakuwa na mafanikio, kama ilivyokuwa kwa tungo nilizozitunga, ya kutoa matunda? Je, itazaa kitabu kingine baada yake kama ilivyokuwa kwa Fiqh?

Hayo ni maswali ambayo hapana ajuaye jawabu lake isipokuwa Mwenye tamko la kwanza na Mwenye uwezo wa juu.

﴿وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ مَّاذَا تَكْسِبُ غَدًا وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ بِأَيِّ أَرْضٍ تَمُوتُ﴾

Na nafsi yoyote haijui itachuma nini kesho, wala nafsi yoyote haijui itafia ardhi gani" (31:34)

Hata hivyo kuamini kwangu ukweli huu hakunizuii kuendelea na juhudi zangu. Kwa sababu, vile vile ninaamini kwamba azma yangu ya kujitahidi ina athari kubwa katika kuhakikisha yale ninayoyataka. Imani hii inanipa msukumo wa kutoa juhudi zangu zaidi, kwa kuogopa kupoteza fursa.

Kwa hivyo basi, nitaendelea kuandika na kuwa na ndoto ya kutimia na kufaulu mpaka kufa.Yeye peke yake ndiye ambaye atasimamisha nishati yangu.Nami nitaendelea kutoa juhudi zangu muda wote ule ambao mauti yatakuwa yako mbali nami.

Natamani sana yanijie mauti huku nikiwa ninaandika kulingania kwenye haki na uadilifu. Bali mapendeleo yangu ni kuingia peponi ili niweze kusoma na kuandika, nikiwa sina mawazo mengine yoyote ya kunishughulishi, nitakuwa sina mawazo ya kushughulikia familia na kadhalika.

Mara nyingi sana hunijia swali hili: Kama nikiingia peponi nitakuwa mvivu? Je, itawezekana nisome na niandike? Halafu hujijibu: Ndio, huko kuna yanayofuvi rahiwa na macho na yanayopendwa na nyoyo; hata kama moyo unapenda kusoma na kuandika. Kisha linanijia swali jingine: Nimwandikie nani na watu wote wa peponi ni wakamilifu?

Samahani kwa kuiachia kalamu iandike hayo; au kwa usahihi zaidi, kuiacha dhati yangu kujieleza. Kwa kweli mimi ni mtu wa kawaida tu, ambaye ni vigumu kumtenganisha na dhati yake na ambaye inakuwa vigumu kujizuia kuyaelezea yaliyo katika pango la moyo wake, wakati inapopatikana fursa ya kujieleza.

Kizazi cha kisasa Kila kitu kina sababu ya kutokea kwake, ni sawa kiwe ni cha kimaumbile, kama vile tufani na tetemeko; au cha kijamii, kama vile ujinga na ufukara; au kiwe ni katika mambo ya moyoni, kama vile imani na kufuru. Hakuna kitu chochote kinachotokea kwa sadfa bila ya sababu yoyote, au bila ya mipangilio yoyote. Nitayafafanua maelezo haya kwa swali na jibu lifuatalo:

Kwa nini kizazi cha sasa hakijishughulishi na misimamo ya kidini kama kilivyokuwa kizazi kilichopita? Vijana wengi wa kileo wameachana na ibada na mazingira ya kidini; bali imekuwa uzito sana kwao kusikiliza mawaidha na nasaha za kidini; hata msimamo mzuri wa kiutu - kama udugu, usawa, amani, kusaidiana, ukweli na uadilifu - haumo katika nyoyo zao kabisa.

Inapotokea kuuzungumzia basi wanauzungumzia katika ndimi zao tu, sio katika nyoyo zao; ila ikiwa kuna manufaa ya kibinafsi.

Jibu ni kuwa, mataifa ya Kiislamu ya Kiarabu na yasiyokuwa ya Kiarabu yalikuwa hayategemei misingi yoyote wala misimamo yoyote ila ile iliyotokana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu (s.w.t.) na Sunna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , sio iliyotokana na ujamaa au ubepari, wala demokrasia au ubaguzi. Hakuna kitu chochote walichotegemea isipokuwa wahyi wa Mwenyezi Mungu.

Humo ndimo mlimochukuliwa misingi ya itikadi, adabu, tabia na njia za taaluma. Vile vile kanuni na hukumu zinazotumiwa katika mahakama na mambo mengine ya kibinafsi na ya kijamii, yalitoka humo. Kwa hiyo, ndio maana yakawa mafundi-sho ya dini yako wazi katika bongo za watu wengi; wakawa wanayajua yanayotakiwa na sharia na yanayokatazwa. Yule aliyekuwa akiishi maisha ya dini alikuwa ndio tegemeo la wote na ndio mahali pa amana zao. Na,yule mbaye hana dini hakuaminiwa au kutegemewa katika jambo lolote.Yaani misimamo ya kijamii ilikuwa ni misimamo ya kidini.

Yeyote anayetoka katika msimamo huo,anakuwa ametoka katika usalama.Kisha siku zikapita, yakatokea mapinduzi kutoka nchi za Kimagharibi, wakavamia miji ya Kiislamu.Kwanza kabisa walielekea kwenye sharia ya Qur`an, wakaiondoa katika mahakama. Badala yake wakaleta kanuni za Kifaransa na za Kiingereza.Wakaondoa mafunzo ya kidini katika taaluma. Wakaanzisha majumba ya ufuska; kama vile mabaa, vilabu vya usiku pamoja na kila kitu ambacho waliona kingeweza kuondoa itikadi na maadili.

Kwa hiyo athari za Qur`an na Sunna za Mtume zikafichika katika maisha ya kijamii. Hata lugha ya Kiarabu pia ilipatwa na kile kilichopatwa na dini. Ndio kikawa kizazi hiki hakijishughulishi na dini wala maadili mema. Hiyo ni natija ya ufisadi waliokulia na kulelewa nao. Na kama kawaida, hali hiyo ilienea. Kwa hiyo ni makosa kukitenga kizazi na jamii yake na malezi yake. Hawakukosea wale waliosema: Panapofuka moshi hapakosi moto

Dawa Unaweza kuniuliza: Umeelezea ugonjwa, sasa dawa yake ni nini? Kwa kweli jibu la swali hili si la kujibiwa na msomi mmoja tu; hapana budi zikutane akili kubwa zenye ikhlas. Kwa sababu, tabia na ada zikiingia katika kizazi na zikabaki kwa muda mrefu, huwa zimemea. kazi rahisi kuzing`oa. Kwa vile zinafanya kazi katika nafsi, kama zinavyofanya kazi athari za kisayansi.

Kuzibadilisha kunahitaji juhudi na jihadi ndefu, zenye mashaka; kama juhudi aliyoifanya Mtume(s.a.w.w) katika kubadilisha ada za kijahiliya na itikadi zao. Kuna Hadith zinazoonyesha hayo; kama ile inayosema: "Uislamu ulianza katika hali ya ugeni na utarudi katika hali ya ugeni, kama ulivyoanza." Kwa hivyo, hauwezi kuepukana na ugeni wake na kutulia katika kurudi kwake, isipokuwa kwa kiongozi kama Mtume Muhammad(s.a.w.w) na Masahaba kama Wahajiri na Ansari Mwenyezi Mungu hashindwi kufanya Qur`an, sharia yake na maadili yake kuwa ndiyo inayotawala leo. Lakini ni juu yetu kufanya juhudi kadiri ya uwezo wetu, wala tusingoje muujiza wa mbinguni.

Na kazi ambayo tunaiweza kuifanya, nionavyo mimi,ni:

Kwanza : tuitilie mkazo dini katika mashule, hasa Qur`an, kuisoma, kuihifadhi na kuifasiri.Kwani hiyo ndiyo msingi. Kama wasimamizi wakikataa kufundisha dini katika mashule na watakataa tu,basi ni juu yetu kuanzisha Shule za kibinafsi kwa ajili ya lengo hilo tu. Tuanzishe Shule hizi kutokana na mamillioni yanayotolewa sabili kwa wanavyuoni wakubwa na wengine Wala sijui kama kuna kazi nyingine bora zaidi ya kutumia pesa hizo kuliko kufufua na kuyaeneza mafundisho ya dini.

Pili : kila mmoja katika watu wa dini atekeleza wajibu wake kwa ikhlasi, baada ya kujiandaa kuwa kiongozi mwenye mwamko, anayejua namna ya kuwakinaisha vijana, kuwa dini ndio chimbuko la msimamo ulio sawa, ambalo litawapa maisha mema zaidi.

Tatu : kuufafanua uhakika wa dini, kuufanya mwepesi kufahamika na kuutangaza kwa vitabu, hotuba, makala na matoleo kadhaa. Tumthibitishie mjinga na mwenye shaka kuwa Uislamu kwa sharia na maadili yake, unatosheleza kabisa mahitaji ya mwanadamu ya kiroho na ya kimaada; na unaweza kutatua matatizo yake; na kwamba una lengo la kumfanya afaulu katika dunia yake na akhera yake.

Msomaji atapata dalili ya hayo katika tafsiri hii ambayo inaunganisha dini na maisha, na ambayo imeshughulikia zaidi upande wa ubinadamu kuliko kushughulikia ufasaha wa maneno.

Mfasiri Tafsiri, kilugha, ina maana ya kubainisha. Na, katika istilahi ina maana ya elimu inayotafiti maana ya maneno ya Qur`an na yanavyohusika. Ili mfasiri awe na ubainifu katika ambayo yanamstahiki Mwenyezi Mungu, hana budi kuwa na maandalizi yafuatayo:-

Elimu za kiarabu kwa nyanja zake zote, elimu ya Fiqh na Misingi (usul) yake, Hadith na elimu ya Tawhid. Na miongoni mwa maandalizi hayo, kama wanavyoona wengine, ni elimu ya Tajwid na elimu ya kisomo cha Qur`an.

Kuna kitu kingine anachokihitajia mfasiri ambacho ni muhimu na kikubwa kuliko chochote katika walivyovitaja wafasiri katika utangulizi wa tafsiri zao. Kwa sababu, ndio msingi wa kwanza wa kufahamu maneno yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.); Wala sijamwona yeyote aliiyekielezea.

Kitu chenyewe ni kuwa, maana ya Qur`an hawezi kuyafahamu na hatayafahamu kwa uhakika wake na kujua ukubwa wake, isipokuwa yule mwenye kuyahisi ndani ya moyo na akili yake. Pia imani yake ichanganyike na maana ya Quan pamoja na damu yake na nyama yake. Hiyo ndiyo siri iliyo katika kauli ya Amirul Muminin, Ali(a.s.) :"Hiyo ni Qur`an iliyonyamaza na mimi ni Qur`an inayotamka."

Vile vile imenijia yakini wakati nikiendelea na tafsiri kwamba mfasiri yeyote asiyeleta fikra mpya, ijapokuwa moja tu, katika tafsiri yake yote, basi atakuwa hana akili ya mwamko, isipokuwa ana akili ya kusoma tu. Anamchorea mwingine yale anayoyasoma, kama inavyoonekana picha ya kitu katika kioo vile ilivyo kwa rangi na umbo.

Hiyo ni kwa sababu maana ya Quran yako ndani sana kiasi ambacho yeyote hawezi kuyafikia kwa vyovyote vile atakavyokuwa na elimu na fahamu; isipokuwa atagundua yale ambayo maarifa yake yanayamudu. Atakaposimama mfasiri aliyetangulia pale alipofikia, kisha akaja mwingine akafuata nyayo zake bila ya kuzidisha chochote ijapokuwa hatua moja tu, basi atakuwa ni kama kipofu kamili anayetegemea fimbo tu; anapoikosa anabakia pale alipo.

Nimepata rai nyingi na itikadi za hapa na pale wakati nilipokuwa nafasiri.Kwa kweli tafsiri imesahihisha fikra zangu nyingi za zamani. Nimekuwa na yakini kwamba hapana imani bila ya takua pepo haipati isipokuwa mwenye kujitahidi na akajitoa mhanga katika njia ya haki na kwamba hakuna msingi wowote katika misingi ya Kiislamu au tawi lolote katika matawi ya Kiislamu - katika kumwamini Mwenyezi Mungu au hukumu ndogo katika sharia - isipokuwa inafungamana na maisha.

Vile vile nimeyakinisha kuwa wengi wa wale ambao hawaujui Uislamu na makusudio yake ni wale wanaojinaki na Uislamu; na mengi ambayo atayakuta msomaji wakati wa kupekuwa kurasa za Tafsir hii, nimeyahusisha hayo katika vifungu mbali kwa vielelezo vyake.

Kwa kweli sijui kama kuna kazi ngumu na nzito kama kufasiri maneno ya Mwenyezi Mungu.Sio kazi rahisi kueleza matakwa yake Mwenyezi Mungu. Lakini jambo la kutia moyo, nikuwa mfasiri hufasiri maana ya Qur`an na makusudio yake kulingana na alivyofahamu yeye, sio kulingana na ilivyo hasa; sawa na mujtahid wa Fiqh ambaye hulipwa thawabu akifutu sawa na husamehewa akikosea, bali hupata thawabu, hata akikosea, kwa sababu ya juhudi yake na kutokuwa mvivu.

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

MWITO WA QURRAN

Mwenye kufuatilia Aya za Quran tukufu, akazingatia maana yake, atazikuta zina mfungamano mmoja tu katika kanuni zake zote na misingi yake. Vile vile katika sura zake na Aya zake. Mfungamano huu ni ule mwito wa kuwapa watu maisha mema yenye uadilifu, ustawi na amani. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اسْتَجِيبُوا لِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُمْ لِمَا يُحْيِيكُمْ﴾

"Enyi mlioamini mwitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapowaita katika yale yatakayowapa uhai." (8:24)

MWITO WA MWENYEZI MUNGU NA MTUME

Mwito wa Mwenyezi Mungu na Mtume kwenye maisha, una mfumo wake na nguzo zake maalum zinazousimamia Mwenyezi Mungu ameupanga mfumo wa kulingania kwa kumwambia Mtume wake mtukufu(s.a.w.w) :

﴿ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ﴾

"Waite kwenye njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora." (16:125)

MAKUSUDIO YA HEKIMA NA MAWAIDHA MAZURI

Makusudio ya hekima na mawaidha mazuri ni kuuambia moyo na akili, na kuuonyesha viumbe vya aina yake na vya ajabu. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿سَنُرِيهِمْ آيَاتِنَا فِي الْآفَاقِ وَفِي أَنفُسِهِمْ حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُ الْحَقُّ أَوَلَمْ يَكْفِ بِرَبِّكَ أَنَّهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ﴾

"Tutawaonyesha ishara zetu zilizo katika upeo wa mbali na katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli" (41:53)

Vile vile kuwahadharisha wapinzani na mwisho mbaya, na huwaonyesha mfano wa umma uliotangulia; kama alivyofanya Nabii Shuaib aliposema:

﴿وَيَا قَوْمِ لَا يَجْرِمَنَّكُمْ شِقَاقِي أَن يُصِيبَكُم مِّثْلُ مَا أَصَابَ قَوْمَ نُوحٍ أَوْ قَوْمَ هُودٍ أَوْ قَوْمَ صَالِحٍ وَمَا قَوْمُ لُوطٍ مِّنكُم بِبَعِيدٍ﴾

"Na enyi watu wangu! Kukhalifiana nami kusiwapelekee kuwasibu kama yaliyowasibu watu wa Nuh au watu wa Hud au watu wa Swaleh. Na watu wa Lut si mbali nanyi." (11:89)

Wakiendelea na inadi yao, na ikiwa hakuna dalili zaidi za kutoa, basi achana nao. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿فَإِنْ حَاجُّوكَ فَقُلْ أَسْلَمْتُ وَجْهِيَ لِلَّـهِ وَمَنِ اتَّبَعَنِ﴾

"Na kama wakikuhoji, basi sema nimeusalimisha uso wangu kumwelekea Mwenyezi Mungu na walionifuata (3:20)

﴿فَإِنَّمَا عَلَيْكَ الْبَلَاغُ وَعَلَيْنَا الْحِسَابُ﴾

"... Hakika ni juu yako kufikisha na ni juu yetu hisabu."(13:40)

Ama nguzo za mwito wa maisha mema, ni hizi zifuatazo:-

1. Hakika mtu hakupatikana kibahati tu, bila ya makusudio yoyote.

﴿وَاللَّـهُ خَلَقَكُمْ ثُمَّ يَتَوَفَّاكُمْ﴾

"Na Mwenyezi Mungu amewaumba kisha atawafisha" (16:70)

2. Mwenyezi Mungu hakumwacha mtu bure bure tu, ajihukumilie kimapenzi yake, bali amemuwekea njia ya sawasawa, ambayo haijuzu kuikengeuka: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أَيَحْسَبُ الْإِنسَانُ أَن يُتْرَكَ سُدًى﴾

"Hivi anadhani kuwa mtu ataachwa bure bure tu !" (75:36)

﴿فَوَرَبِّكَ لَنَسْأَلَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٩٢﴾ عَمَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴾

"Naapa kwa Mola wako tutawauliza wote yale waliyokuwa wakiyatenda." (15: 92-93)

3. Amani na kuchunga nidhamu. Mwenye kuiharibu na akafanya uharibifu katika nchi ataadhibiwa adhabu kali duniani, na katika akhera atakua na adhabu. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿إِنَّمَا جَزَاءُ الَّذِينَ يُحَارِبُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَيَسْعَوْنَ فِي الْأَرْضِ فَسَادًا أَن يُقَتَّلُوا أَوْ يُصَلَّبُوا أَوْ تُقَطَّعَ أَيْدِيهِمْ وَأَرْجُلُهُم مِّنْ خِلَافٍ أَوْ يُنفَوْا مِنَ الْأَرْضِ ذَٰلِكَ لَهُمْ خِزْيٌ فِي الدُّنْيَا وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابٌ عَظِيمٌ﴾

"Hakika malipo ya wale wanaopigana na Mwenyezi Mungu na Mtume wake na kufanya uovu katika nchi, ni kuua-wa au kusulubiwa au kukatwa mikono yao kwa mabadilisho au kuhamishwa katika nchi; hii ndio fedheha yao katika dunia na akhera watapata adhabu kubwa." (5:33)

4. Amani na nidhamu haiwezi kuwako na wala haitakuwako ikiwa kila mtu hatachunga heshima yake na uaminifu wake. Kwa sababu jamii njema, kwa mujibu wa Quran, ni ile isiyokuwa na mbegu ya ufisadi hata moja. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿مَن قَتَلَ نَفْسًا بِغَيْرِ نَفْسٍ أَوْ فَسَادٍ فِي الْأَرْضِ فَكَأَنَّمَا قَتَلَ النَّاسَ جَمِيعًا وَمَنْ أَحْيَاهَا فَكَأَنَّمَا أَحْيَا النَّاسَ جَمِيعًا﴾

"Mwenye kumuua mtu bila ya yeye kuua mtu au kufanya ufisadi katika nchi, basi ni kama amewaua watu wote; na mwenye kumwacha hai basi ni kama amewaacha hai watu wote." (5:32)

Hiyo ni kwamba hakika ya utu inakuwa kwa kila mmoja. Mwenye kumfanyia ubaya mmoja, atakuwa amewafanyia ubaya wote na mwenye kumfanyia wema mmoja, atakuwa amewafanyia wema wote.

Kusema kwake Mwenyezi Mungu: Mwenye kuua mtu bila ya yeye kumuua mwingine au kufanya ufisadi katika nchi", ni kuonesha kuwa kila mtu ana heshima yake ya kiutu, mpaka aivunje mwenyewe kwa kufanya kosa litakalovunja heshima yake hiyo.

5. Utangamano kati ya watu unakuwa juu ya misingi ya kuchunga heshima kwa kila mtu bila ya kubagua kati ya mwanamume au mwanamke, mweusi au mweupe na tajiri au maskini, katika mila yoyote aliyo nayo. Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ameuthibitisha ubainifu huu kwa ibara fupi:

﴿وَلَقَدْ كَرَّمْنَا بَنِي آدَمَ ﴾

"Hakika tumemtukuza mwanaadamu..." (17:70)

Mwenye kuidharau heshima aliyopewa na Mwenyezi Mungu, atakuwa amemdharau Mwenyezi Mungu na sharia yake.

6. Kuamini Mwenyezi Mungu, Utume wa Muhammad(s.a.w.w) , siku ya mwisho na mengineyo, ni katika misingi ya dini na matawi yake, wala sio kuwa ni bendera ya dini inayopeperushwa na Quran. Kila msingi katika misingi ya Uislamu na kila hukumu katika hukumu zake, zina matunda na amali yenye manufaa. Mwenyezi Mungu amekukutanisha kumwamini yeye na amali njema katika Aya kadhaa. Ama kuamini Utume wa Muhammad(s.a.w.w) ni kuamini utu na wema wake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا رَحْمَةً لِّلْعَالَمِينَ ﴾

"Na hatukukutuma isipokuwa uwe rehema kwa walimwengu" (21: 107)

Ama kuingia peponi, kunafungamana zaidi na jihadi na amali njema katika maisha haya. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أَمْ حَسِبْتُمْ أَن تَدْخُلُوا الْجَنَّةَ وَلَمَّا يَعْلَمِ اللَّـهُ الَّذِينَ جَاهَدُوا مِنكُمْ وَيَعْلَمَ الصَّابِرِينَ ﴾

"Je mnadhani mtaingia peponi na hali Mwenyezi Mungu hajawajua wale waliopigania jihadi dini ya Mwenyezi Mungu miongoni mwenu na kuwajua waliofanya subira?" (3:142)

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اسْتَجِيبُوا لِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُمْ لِمَا يُحْيِيكُمْ﴾

"Enyi ambao mmeamini mwitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapowaita katika yale yatakayowapa uhai..." (8:24)

Hii ni dalili wazi kwamba mwito wowote ambao hauna muungano wowote wa maisha, basi sio wa dini. Na mwenye kuunasibisha kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, atakuwa ameizulia uwongo dini. Kwa misingi hii, ndipo nikajaribu kufasiri Aya za Quran tukufu na kuifafanua kwa ufafanuzi ufuatao:-

Njia Makusudio ya njia hapa ni udhibiti anaokwenda nao mtungaji, bila ya kukengeuka. Kwani kazi yoyote ambayo haina njia ni shaghalabaghala tu, itakayoongozwa na migongano.

Njia niliyofuata katika tafsiri hii, inafungamana na kudhibiti mambo yafuatayo:-

1. Nimeitazama Quran kwa mtazamo kuwa hakika yake na sera yake ni kitabu cha dini na uongozi, kutengeneza na kuweka sharia inayolenga kuwapa watu wote maisha yaliyo katika misingi iliyosalimika, inayoongozwa na amani na uadilifu na iliyojaa furaha na wema.Hayo nimetangulia kuyaeleza.

2. Baadhi ya wafasiri wa kwanza walijishughulisha zaidi na lugha, wakarefusha maneno katika kubainisha siri ya matamko na wakaweka maswali; mfano: Kwa nini imetajwa wau na wala isitajwe fa au kwa nini amesema mafasiki na wala asiseme madhalimu, n.k. Kisha wakajibu majibu yasiyo na umuhimu.Mimi sikuingilia jambo hili.

Ikiwa kila tafsiri imepondokea upande fulani, basi mimi nimepondokea kwenye namna ya kumkinaisha msomaji kwamba dini kwa misingi yake yote na matawi yake pamoja na mafunzo yake mengine, ina lengo la kumpatia mtu heri na heshima na kwamba mwenye kukengeuka lengo hili, atakuwa ameikengeuka hakika ya dini na njia ya maisha yaliyonyooka.

Ili kuweza kulifikia lengo langu hili, nimejaribu kwa juhudi zangu zote kuleta ufafanuzi mwepesi na ulio wazi, atakaoweza kuufahamu msomaji kwa kiwango chochote atakachokuwa. Kwa vile zama walizoishi wafasiri wa zamani hazikuwa zama za kudharauliwa dini, sharia yake na misimamo yake kama ilivyo sasa, ndio maana wafasiri hao walijishughulisha zaidi na fasihi kuliko kumkinaisha msomaji kuwa dini ni msimamo ulio sawa sawa. Kwa hiyo lugha ya tafsiri ya zama hizo sio ya zama hizi.

Hakika tafsiri ni fani kamili inayokwenda na wakati. Ndio maana mimi nimeielekeza tafsiri yangu katika kukinaisha kizazi cha kisasa kuwa dini inakwenda sambamba na maisha. Lakini hiyo haimaanishi kuwa mimi nimeghafilika na upande wenye kunufaisha, ambao umeonyeshwa na wafasiri wakubwa, la! Isipokuwa nimeufupisha upande huo na kuuonesha kwa uwazi zaidi, hata nimeonyesha rai yangu ndani yake hasa katika masuala nyeti ya kifalsafa; mfano: Kulazimishwa watu au kuwa na hiyari, uongofu na upotevu, Uimamu na Isma ya Mitume.

Pia shafaa, mwenye madhambi makubwa, hisabu ya kaburi na mengineyo. Vilevile mara nyingi nimehusisha kifungu maalum cha lugha, kwa ajili ya kutafsiri misamiati ambayo si maarufu. Mara nyingine nimeweka kifungu kingine cha irabu kwa ajili ya kubainisha hukumu za Kinahw (sarufi) kwa tamko lenye utatanishi, ijapokuwa wafasiri wa kisasa hawakujishughulisha nalo, lakini mimi nimeangalia matakwa ya baadhi ya wasomaji wa nahw, ingawaje ni wachache.

Ama usanii wa methali za maneno, elimu ya usemaji, ulinganishaji na uunganishaji, nimemwachia Zamakhshari katika Kash-Shaf, Al-Andalusi katika Bahrul-Muhit, na wengineo. Ili kuthibitisha kuwa lugha ya tafsiri inatofautiana kulingana na wakati, ninataja maneno ya Muhyiddin Ibn El-Arabi katika kitabu Futuhatil Makkiyya, Juzuu ya nne, mlango wa Hadhratul-hikma, kuhusu kuisoma Quran, ambayo yana maana ya undani kabisa na yanayoafikiana na nadharia za kisasa; hasa ile nadharia ya Uwiano (Relativity) ya Einstein, ambaye anazingatia kuwa wakati na mahali ndivyo vinavyosimamisha kitu. Anasema huyo Ibnul Arabi:

Msomaji anasoma alichokihifadhi katika Qur'an, anakuta katika kila kisomo maana ambayo hakuyakuta katika kisomo cha kwanza pamoja na kuwa herufi zinazosomwa ni zile zile, isipokuwa matukio na hali ndivyo vipya.Kwa hivyo hapana budi maana hayo yawe mapya. Kwa sababu, wakati wa kusoma kwa kwanza sio kwa pili.

Hapa aliposema,hapana budi kuwa maana hayo yawe mapya, maana yake ni kuwa, kitu kinakuwa kipya kwa kuwa kipya wakati ule. Amesema kweli mwanafalsafa Rasil, aliposema: Hakika watu wa zamani waligundua nadharia zilizothibitishwa na elimu kulingana na fikra na jitahadi zao; na zilikuwa ni rai za sawa; ambapo katika zama zao hizo hakukuwa na kitu zaidi ya jitihadi ya maoni."

3. Nimeangalia hadith zinazohusu Israil ambazo zimekuja katika baadhi ya tafsiri, nikazikuta ni vigano tu. Kitu kinachofahamisha zaidi uwongo wake, ni kuzinasibisha kwa Waisrail. Vilevile nimejipurukusha na riwaya zilizoelezea sababu za kushuka, isipokuwa chache tu. Kwa sababu, wanachuoni hawakudhibiti mategemezo yake na kupambanua kati ya dhaifu na sahihi; kama walivyofanya kwa riwaya za hukumu. Hata hizo nazo hawakuangalia sana zile za Sunna na kuchunguza kwa makini, isipokuwa katika wajib na haramu.Bali wameweka utafiti mbali katika vitabu vya Usuul.

Vilevile sikujishughulisha na pia kumshughulisha msomaji, kutaja kufungamana au kunasibiana kati ya Aya na Aya nyingine; kama walivyofanya wafasiri

Wengine, Kwa sababu, Quran haikufunuliwa kwa Mtume(s.a.w.w) kwa mpigo, bali iliteremshwa kwa nyakati maalum, mara nyingine kwa kufuatana na mara nyingine kwa kuchelewa; wala sura au Aya hazikupangwa kama tunavyozisoma hivi sasa.Quran, tuliyo nayo hivi sasa, ilipangwa tangu siku za Mtume(s.a.w.w) . Mpango huu haukufuata utaratibu wa kushuka sura, wala kuwa sura ni ya Makka au Madina; vile vile hakuna tarehe ya kushuka Aya. Hivyo tunakuta Sura ya Baqarah,Al-Imran na Maida ziko mwanzo wa msahafu baada ya Sura ya Fatiha, pamoja na kuwa zimeshuka Madina. Mara nyingine tunakuta sura iliyoshuka Madina ina Aya zilizoshuka Makka.

Mwenye tafsir ya Al-Manar, akimnukuu mwalimu wake, Sheikh Muhammad Abduh, katika Juzu ya pili, ukurasa 451, chapa ya

Pili: anasema: Quran sio kitabu cha fani cha kuwa na mlango mahsusi na makusudio fulani; isipokuwa ni kitabu cha uongozi na waadhi, inamgurisha mtu kutoka hili mpaka lile. Na mara kwa mara inarudia kwenye utafiti wa kusudio moja, kwa ibara nyingine na namna nyingine ya ubainifu, ili asichoke mwenye kupewa mawaidha na kuongozwa.

4. Kabla ya kitu chochote nimetegemea, katika kutafsiri Aya na kubainisha makusudio, Hadith zilizothibiti kwa Mtume(s.a.w.w) . Kwa sababu, ndizo zinazofasiri Quran na ni njia ya kujua maarifa yake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا ﴾

"Alichowapa Mtume kipokeeni na alichowakataza jiepusheni nacho" (59:7)

Ikiwa hakuna hadith, basi ninategemea dhahiri ya Aya na mpangilio wake. Kwa vile, msemaji mwenye hekima, ubainifu wake hutegemea yale anayoyafahamu yule anayemwambia kutokana na dalili zilizo wazi; kama ambavyo mwenye kuambiwa anachukua dhahiri hiyo tu, mpaka pale itakapothibitika kinyume. Kama ikija Aya nyingine katika maana ya Aya ya kwanza na ikawa ina ubainifu na kuwa wazi zaidi, basi ninazitaja pamoja ili zifafanuke zaidi. Kwa vile chimbuko la Quran ni moja, inajitamkia yenyewe na kujiletea ushahidi. Kama ikipingana dhahiri ya tamko pamoja na hukumu ya kiakili, basi ninaitafsiri kwa namna ambayo inaafikiana na akili, kwa kuizingatia hiyo akili kuwa ni dalili na hoja juu ya amali iliyo wajibu.

Ikiwa dhahiri ya tamko inapingana na Ijmai ya Waislamu katika nyakati zote kwenye masuala ya Kifiqh, basi huchukua Ijmai: kama kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿إِذَا تَدَايَنتُم بِدَيْنٍ إِلَىٰ أَجَلٍ مُّسَمًّى فَاكْتُبُوهُ ﴾

"Mnapowekeana deni kwa muda uliowekwa, basi iandikeni" (2:282)

Ambapo neno iandikeni limefahamisha wajibu, lakini Ijmai imesimamia juu ya kuwa kuandika deni ni sunna. Kwa hiyo hapo nimechukua kuwa ni suna na sio wajibu.

Ama kauli za wafasiri, sikuzifanya ni hoja mkataa na dalili peke yake; isipokuwa kutilia nguvu njia mojawapo, ikiwa tamko linachukua maana nyingi. Hata hivyo wafasiri wamefanya juhudi kubwa sana za kufafanua maana ya Quran na siri zake, na kuonyesha lugha inayofahamika na ngeni. Wamekitafsiri kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa juhudi ambayo haijapatikana mfano wake katika umma wa zamani au wa sasa.

Kwa hakika kuna wafasiri wakubwa na waliobobea katika fani mbali mbali za elimu ya Quran ambao walikuwa ni watu muhimu sana katika historia ya Kiislam. Kwa hiyo ingawaje kauli za mabingwa hao si hoja, kama kauli ya Masum, lakini zinaweza kuwa ni mwangaza juu ya maana yanayokusudiwa na kuuandaa njia ya kufahamu.

Makosa ya Chapa Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa. Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo.Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa Swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146) Imeandikwa La Yaalamuun, (hawajui) badala ya Yaalamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya pili, Sura (2:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawmal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile. Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil Makosa ya chapa.

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbaina sanah badala ya: Hatta idha balagha ashuddahu arbai- na sanah. Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana. Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa, kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu" . Na Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyoyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani.(Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

NAJILINDA KWA MWENYEZI MUNGU NA SHETANI ALIYEFUKUZWA

Kujilinda na Shetani Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

﴿فَإِذَا قَرَأْتَ الْقُرْآنَ فَاسْتَعِذْ بِاللَّـهِ مِنَ الشَّيْطَانِ الرَّجِيمِ ﴾

"Unaposoma Quran jilinde kwa Mwenyezi Mungu na shetani aliyefukuzwa" (16:98)

Amesema tena:

﴿وَإِمَّا يَنزَغَنَّكَ مِنَ الشَّيْطَانِ نَزْغٌ فَاسْتَعِذْ بِاللَّـهِ إِنَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ﴾

"Na kama wasiwasi wa shetani ukikusumbua basi jilinde kwa Mwenyezi Mungu. Yeye ni Mwenye kusikia mjuzi" (7:200)

Maana ya kujilinda Kujilinda huku kwa Mungu hakutoshi kwa kusema: Audhubillahi minashshaytwanir rajim tu, isipokuwa linalotakikana ni kumwamini Mwenyezi Mungu, kumtegemea na kumwogopa; hata kama mtu hakutamka hivyo. Mwenye kutenda umuhimu wowote kwa kuitakidi kuwa nyuma yake kuna nguvu inayomsaidia kutenda amali njema; mwenye kupondokea kufanya haramu, lakini twaa ya Mwenyezi Mungu ikamzuia na mwenye kuchanganyikiwa akaifanya sharia ndio kipimo, wote hao ni katika wale wanaojilinda kweli kwa Mwenyezi Mungu na shetani aliyefukuzwa.

Hakuna kitu kinachofafanua zaidi kujilinda kuliko mtu kumtegemea Muumba wake, kuwa na yakini kwamba mja mwingine hawezi kumdhuru wala kumnufaisha na kwamba kabisa hakuna kitu kitakachozidi hifadhi ya Mwenyezi Mungu.

Majaribio yametufundisha kwamba mwenye kumtukuza asiyekuwa Mwenyezi Mungu, amedhalilika; na mwenye kutaka uokovu kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu ameruka utupu; na matarajio hayawezi kupatikana kwa kuwakimbilia viongozi, chama, wala kwenye hazina za matajiri, bali Mwenyezi Mungu tu peke yake ambaye hana mshirika.

Shetani ni nani? Sisi hatujamwona Shetani ana kwa ana lakini ametolewa habari zake na wahyi. Kwa hivyo ni wajibu kusadiki kuwa yupo, na si wajibu kujua alivyo. Mwenyezi Mungu amemtaja katika Quran kwa sifa ya kupoteza watu na kuwaepusha na twaa ya Mwenyezi Mungu na amali ya heri. Kwa hiyo kila wazo linalokupitia moyoni au mtu anayejaribu kukuhadaa kukuweka mbali na twaa na kheri ya Mwenyezi Mungu, kukuhadaa kuasi sharia na kuuvika uovu na ubatilifu nguo ya uongofu, basi huyo ni Shetani wa hisia au wa kimaana.

Jambo la kushangaza ni kuwa mashetani watu nao wanaomba walindwe na shetani, hali wao wenyewe ni mashetani lakini hawajijui. Ni sawa na mtu anayesoma Quran na huku inamlaani mwenyewe; kama ilivyoelezwa katika hadith.Quran inamlaani mwongo aliye haini.Kwa hivyo huyo mwongo anapoisoma huwa amejitamkia laana yeye mwenyewe.

Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أُولَـٰئِكَ جَزَاؤُهُمْ أَنَّ عَلَيْهِمْ لَعْنَةَ اللَّـهِ وَالْمَلَائِكَةِ وَالنَّاسِ أَجْمَعِينَ ﴾

"Hao malipo yao ni kushukiwa na laana ya Mwenyezi Mungu na ya Malaika na ya watu wote". (3:87)

Hukumu ya Kusoma Audhubillah... kabla ya kusoma Quran ni sunna, wala si wajib; ni kama vile kuosha mikono na kusoma Bismillah kabla ya kula. Lau hiyo Audhubillahi ingelikuwa ni wajibu ingeliwajibishwa katika swala, mahali pa fatiha na Sura.Wanavyuoni wote wamesema kuwa si wajib. Mwenye Miftaahul-Karaama amesema: Hawakuhitalifiana katika hilo isipokuwa Ibn al-Junaid ambaye mafakihi wamemwita: aliyejitenga.

Mantiki ya Iblis Kwa mnasaba wa Audhu (kujilinda na Shetani) tutadokeza vigano alivyonasibishwa navyo Ibilisi. Kwa sababu ingawaje ni vigano, lakini vina picha wazi kwa watu wengi wa zama hizi; hasa wale wanaotaka kujinufaisha bila ya kuangalia maslahi ya wengine, kwa kufanya mbinu za kujaribu kila njia ya kucheza na maneno na kuficha haki. Tutayaonyesha hayo kwa matamko tu; bila ya kudhihirisha madhumuni.

Inasemekana kuwa Ibilisi alimwambia Mwenyezi Mungu (s.w.t):

Haijuzu kuniadhibu kwa kuacha kumsujudia Adam. Mwenyezi Mungu akamuuliza,Kwa nini? Akajibu: Kama ungelitaka hasa nimsujudie ungenifanyisha kwa nguvu. Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akamuuliza: Wakati gani ulijua kwamba sikukutaka umsujudie Adam? Je ulilijua hilo baada ya kukuamrisha na kuasi amri yangu?Au kabla ya kukuamrisha kusujudu? Akasema: Ni baada ya kuniamrisha.

Mwenyezi Mungu (s.w.t.).akasema: Basi umejishinda. Kwa sababu ulihalifu kabla ya kujua kuwa Mimi niliyataka yale uliyoacha kuyafanya. Zaidi ya hayo kama ningekufanyisha kwa nguvu, basi isingelikuwa amri. Utaona katika mantiki ya Ibilisi sura iliyo wazi kwamba Mwenyezi Mungu hawafanyishi wenye kuwajibikiwa na sharia kama vile anavyofanya katika kuumba kwa njia ya kun fayakun (kuwa, ikawa). Isipokuwa anawafanyisha kwa njia ya kuongoza matakwa ya mtu kwa sharia inayoelezwa ya kuamrisha mema na kukataza mabaya.

Inasemekana kuwa siku moja Ibilisi alikutana na Mtume Muhammad(s.a.w.w) akamwambia: Hakika Mwenyezi Mungu amekusifu kwa jina la kiongozi, na mimi amenisifu kwa jina la mpotezaji. Lakini uongozi na upotezaji vyote vinatokana na Yeye, kwa hiyo wewe na mimi hatuna chochote.

Mtume akasema:Hapana! Mimi hubainisha batili na kuikataza na kuitolea kiaga kibaya;hali wewe una unafiki na hadaa ya ubatilifu; na mtu ana uwezo, upambanuzi na hiyari. Kwa hivyo mwenye kufanya hiyari nzuri (akaongoka) anajifanyia mwenyewe, na mwenye kuifanya mbaya (akapotea) pia anajifanyia mwenyewe.

Imesemekana kuwa Ibilisi alimwendea Nabii Isa(a.s.) akamuuliza: Si unadai kuwa wewe una daraja kubwa kwa Mungu? Basi hebu jitupe kutoka juu tuone,je atakuokoa? Masihi akasema: Hakika Mwenyezi Mungu ndiye anayemjaribu mja wake na sio mja kumjaribu Mola wake.

Imesemekana kuwa baada ya gharika na kukauka maji, Ibilisi alimwendea Nuh(a.s.) akamwambia: Hakika wewe umenisaidia, kwa hiyo ninataka kukulipa. Nuh(a.s) : Akasema: Mungu apishe mbali! kumsaidia na kiumbe kama wewe. Akasema Ibilisi: Ndio hivyo. Nuh(a.s) : Akasema kwa nimekusaidia nini? Akasema Ibilisi: Umewaapiza watu wako ili waangamie wakaangamia, na nilikuwa nikijishughulisha usiku na mchana kuwapoteza kwa muda huo. Baada ya kuaangamizwa watu wako, sina kazi ya kufanya; sipati wa kumpoteza. Nuh(a.s) akasema: Utanilipa nini?

Akasema: Ninakunasihi usikasirike, kwa sababu hasira ya mtu inarahisisha kunifuata.Wala usihukumu kati ya watu wawili. Kama ukifanya hivyo, basi mimi nitakuwa wa tatu wenu. Wala usikae faragha na mwanamke kwani mimi hukuvutia kwake na yeye humvutia kwako. Kutokana na mantiki hii ya kishetani, inaonyesha kuwa Shetani ndiye mchochezi, na kwamba yeye huzipongeza silaha zenye kuangamiza.

HEKAYA

Inasemekana kwamba Mtume(s.a.w.w) na sahaba zake walimpitia mtu mmoja akirukuu na kusujudu kwa unyeyekevu. Wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni uzuri ulioje wa swala ya mja huyu! Mtume akasema:Huyu ndiye aliyemtoa baba yenu peponi .

LENGO LA HEKAYA

Lengo la hekaya hii ni kuwa haifai mtu kughurika na kuhadaika kwa zuhudi na ibada ya dhahiri.

Inasemekana kuwa Nabii Musa(a.s.) alikuwa akienda kuzungumza na Mola wake, ikatokea kukutana na Ibilisi, akamwambia Unakwenda wapi ewe uliyezungumza na Mwenyezi Mungu? Nabii Musa(a.s) akasema: Ninakwenda kwa Mola wangu kupokea maneno kutoka kwake na niko tayari kukuombea akusamehe kama utaniahidi kuungoa upotevu wako. Ibilisi akasema: Mimi sina haja ya kuombewa na wewe wala mwingine, bali ni juu Yake Yeye Mungu kutaka radhi yangu.(Mungu apishe mbali). Musa(a.s) akamwambia: Kafiri mkubwa we Mwenye laana! Ibilisi Akasema: Kwani nina dhambi gani mimi? Mungu alinitaka nimsujudie Adam, na mimi kwa iIkhlas yangu, siwezi kumsujudia asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Sasa tangu lini Ikhlas ikawa ni dhambi? Musa(a.s) akamjibu: Hii ni kuchezea maneno tu nako hakuwezi kukufaa wewe hata chembe, utaona yatakayokupata Kesho (Kiyama). Ibilisi akasema: Na wewe utaona nitakavyofanya kesho. Akasema: Utafanya nini?

Ibilisi akajibu: Nitamtaka Mwenyezi Mungu atimize ahadi Yake na nitamtolea hoja kwa kauli Yake:

﴿وَرَحْمَتِي وَسِعَتْ كُلَّ شَيْءٍ ﴾

"Na rehema yangu hukienea kila kitu" (7:156)

"Nami ni kitu, kwa hiyo ni wajibu rehema Yake inipate (inienee).Kama mimi si chochote, basi sitahisabiwa wala kuadhibiwa.

Akasema Musa(a.s) : Hakika rehema ya Mwenyezi Mungu inamwenea yule mwenye mwelekeo nayo, na wewe uko mbali sana nayo. Ibilisi akasema: Basi nitafanya njia nyingine. Nitawaita wafuasi wangu waliopotea na nitamtaka Mwenyezi Mungu (s.w.t.) naye awaite wafuasi Wake waumini, halafu ipigwe kura.Hapo atajulikana nani mshindi mwenye sauti ya wengi. Kama Mwenyezi Mungu akikataa kura, nitafanya maandamano makubwa mpaka nipate ninayotaka.

Kigano hiki kina lengo la kwamba watu wa batili ni wengi zaidi kuliko watu wa haki, kwa sababu haki ni nzito na batili ni nyepesi; kama alivyosema Amirul Muminin, Ali(a.s.) :Yapasa mwenye akili kutoangalia wingi kuwa ni kipimo cha haki, wala uchache kuwa ni kipimo cha batili.

Katika Nahjul-Balagha, amesema:Hakika kundi kubwa ni watu wa batili hata wakiwa wengi; na kikundi kidogo ni watu wa haki hata wakiwa wachache.

Quran tukufu nayo inasema:

﴿وَأَكْثَرُهُمْ لِلْحَقِّ كَارِهُونَ ﴾

Na wengi wao ni wenye kuchukia haki. (23:70)

﴿وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴾

Lakini watu wengi hawajui.(12:21)

﴿وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَشْكُرُونَ ﴾

Lakini watu wengi hawashukuru.(12:38)

﴿وَأَكْثَرُهُمْ لَا يَعْقِلُونَ ﴾

Na wengi wao hawatumii akili (5:103)

﴿بَلْ أَكْثَرُهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ ﴾

Bali wengi wao hawaamini (2:100)

Kuna Hadith inayosema:Wakikutana wasaidizi wa Ibilisi wanaweza kujaza Mashariki na Magharibi . Na kwa madondoo haya, na mengineyo mengi, ndipo Shia wakasema: Khalifa wa Mtume ni kama Mtume; huchaguliwa na Mwenyezi Mungu; siye yule anayechaguliwa na watu. Huyo anayechaguliwa na watu ni Mfalme wa watu; si Khalifa wa dini. Ama mkuu wa dini, kwa Shia, ni yule mwenye sifa zilizoelezwa. Sio yule anayechaguliwa na watu wala si yule anayewekwa na kiongozi wa kidunia.

Na kwa nini isiwe hivyo? Je,watu wenye matamanio ya dunia wanaweza kuaminika kuongoza dini ya Mwenyezi Mungu? Basi kama ni hivyo na wawachague na kuwapigia kura Mitume, na walifaradhishe hilo kwa Mwenyezi Mungu. Ametakata kabisa Mwenyezi Mungu na yale wayasemayo madhalimu. Natija ya kimantiki ni kwamba Khalifa wa Mtume hawi, na hatakuwa, isipokuwa kwa usimulizi unaotokana na Mtume mwenyewe, na kwamba mkuu wa dini ni yule mwenye sifa zilizosimuliwa.

Mwenye kujipachika ukuu wa dini bila ya kuwa na sifa zilizotajwa, basi atakuwa amemzulia Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, na ameruka patupu mwenye kuzua. Kwa hivyo basi, yote hayo yanafahamisha kuwa suala lolote haliwezi kuwa la kweli mpaka liwe limefuata haki; na kwamba mbinu za kucheza na maneno, haziwezi kuifanya batili iwe haki, au haki iwe batili, wala kisichoingia akilini kiingie akilini; hata kama hizo mbinu zitakuwa za hali ya juu kiasi gani.

Tutakalolifahamu ni kuwa mwenye mbinu hizo ni mwanafunzi hodari wa Ibilisi katika kuificha haki, na kuifunika na moshi wa hadaa.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHMA MWENYE KUREHEMU

BISMILLAH

Tamko hili tukufu ni nembo maalum ya Waislamu. Kwalo Wanaanzia maneno na vitendo vyao vyote; na iko kwenye daraja ya pili baada ya shahada mbili. Ama wasiokuwa Waislamu, huanza: Kwa jina Lako ewe Mwenyezi Mungu Kwa jina Lake Mtukufu, kwa jina la Mwenye kuanza, na Mwenye kuishiliza au Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu n.k.

Huondolewa hamza katika neno ism katika Bismillahi, linapotamkwa na kuandikwa kwa sababu ya kutumiwa sana. Na, huondolewa hamza kwa kutamkwa, na sio kwa kuandika mahali pengine; kama vile sabbihisma rabbikal -aala na Uqsimu billah.

MAANA YA TAMKO: ALLAH

Tamko: Allah (Mwenyezi Mungu) lina maana ya Mwenye kuabudiwa kwa haki, ambaye husifika na sifa zote za utukufu na ukamilifu, wala hakisifiwi kwa sifa hiyo kitu kingine chochote.

Inasemekana kuwa Mwenyezi Mungu ana jina moja Tukufu, na kwamba atakayelijua, basi atamiminikiwa na heri na atakuwa na miujiza. Lakini sisi tunaamini na kuitakidi kwamba kila jina la Mwenyezi Mungu ni tukufu; yaani huyo Mwenyezi Mungu ni Mtukufu. Kwa sababu haiwezekani kabisa kuufanya upande mmoja ni bora kuliko upande mwingine, kuboresha kutaleta ushirika na kuzidi; na ambaye hana mfano wa kitu chochote, hawezi kushirikiana na yeyote katika kitu.

MAANA YA NENO: RAHMAN

Neno: Rahman (Mwingi wa Rehema) ni sifa.Limechukuliwa kutoka katika Rahma (Rehema). Maana yake kwa upande wa Mwenyezi Mungu ni kufanya hisani na kwa upande wa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, lina maana ya upole.

BISMILLAH

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehma Mwenye kurehemu wa moyo. Limezoeleka kutumiwa kwa maana ya dhati yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.), likawa ni katika majina mema ya Mwenyezi Mungu.

Mwenyezi Mungu anasema:

﴿قُلِ ادْعُوا اللَّـهَ أَوِ ادْعُوا الرَّحْمَـٰنَ أَيًّا مَّا تَدْعُوا فَلَهُ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَىٰ﴾

Sema! Muombeni (kwa jina la) Mwenyezi Mungu, au muombeni (kwa jina la) Mwingi wa rehema; kwa jina lolote mnalomwita (itafaa), kwani ana majina mema. (17:110)

MAANA YA NENO: RAHIM

Neno: Rahim (Mwenye kurehemu) vile vile, ni sifa. Limechukuliwa kutoka katika neno Rahma. Wafasiri wengi wametofautisha kati ya matamko haya (Rahman na Rahim) kwamba Rahman ni rehema yenye kuenea kwa muumini na kafir; na Rahim ni rehema yenye kuwahusu waumini peke yao. Wakasema: Ewe Mwingi wa Rehema katika dunia na Akhera na ewe Mwenye Kurehemu akhera tu. Ama mimi nasema: Ewe Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu katika dunia na akhera.

Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أَهُمْ يَقْسِمُونَ رَحْمَتَ رَبِّكَ﴾

Je,wao wanaigawa rehema ya Mola wako? (43:32).

MAANA YA BISMILLAAHI RAHMANI RAHIM

Kwa ujumla maana ya Bismillaahi rahmani rahim ni kwamba: wewe unaanza kitendo chako kwa kumtaka msaada ambaye rehema Yake imekienea kila kitu, na kusajili katika nafsi yako kwamba unayoyafanya ni kwa jina lake, sio kwa jina lako wala kwa jina la mwingine yeyote asiyekuwa Yeye. Si kama vile anavyosema mtumishi wa serikali kuwaambia raia: Kwa jina la taifa ninawaambia kadhaa. Bismillah inafahamisha kwamba kitendo unachofanya ni halali hakina shaka ya haramu. Kama kitendo ni haramu na ukakifanya kwa Bismillaah, basi utakuwa umeasi mara mbili kwa mpigo:

Kwanza : ni kuwa kitendo chenyewe ni haramu.

Pili : ni kuwa umesema uongo kwa kukinasibisha na Mwenyezi Mungu. Ametakasikia Mwenyezi Mungu na hayo kabisa.

HUKUMU YA BISMILLAH

Hukumu ya Bismillah Kwa upande wa Shia Imamiya, ni sehemu ya sura, na wamewajibisha kuisoma kwa sauti katika swala ambayo ni wajibu kusoma Alhamdu na sura kwa sauti; kama vile swala ya Asubuhi (Al-fajr) na rakaa mbili za mwanzo za swala ya Maghrib na Isha. Ni sunna kusoma kwa sauti katika swala ambayo haisomwi kwa sauti kama vile swala ya Adhuhuri na Alasiri.

Hanafi na Maliki wamesema kuwa inajuzu kuiacha Bismillaah katika swala, kwa sababu si sehemu ya sura. Shafi na Hambali wamesema ni sehemu ya sura; ispokuwa Hambal wamesema kuwa isisomwe kwa sauti wakati wowote wa swala. Shafi nao kwa upande wao, wakasema isomwe kwa sauti katika swala ya Asubuhi (Al-fajr) na rakaa mbili za Maghribi na Isha.

Hapa kauli ya Shafi na Hambal haziko mbali na kauli ya Imamiya.

Kwa ujumla ni kwamba herufi hizi za Bismillah zinatengeneza jina la Mwenyezi Mungu Mtukufu na sifa Zake. Hutamkwa na kuandikwa kama maneno mengine, lakini lina heshima na hukmu mahsusi. Haijuzu kuliandika juu ya karatasi, au kwa wino, kalamu au kitu chochote kilicho najisi.Vile vile haijuzu kuligusa bila ya twahara.

Wataalamu wa Fiqhi wa Kiimamiya wamefutu kwamba mwenye kuutupa msahafu makusudi katika uchafu, kuupiga teke, kuupasua kwa dharau, au kuufanyia kitu chochote kinachoonyesha dharau, basi amekuwa kafiri aliyeritadi. Msemaji mmoja amesema kuwa Sura ya Fatiha imekusanya maana yote ya Qurran, na kwamba Bismillah imekusanya maana yote ya Fatiha, na herufi Ba katika Bismillah imekusanya maana yote ya Bismillah. Hatimaye herufi Ba inakuwa imekusanya maana yote ya Quran.Msemaji huyu ni kama yule anayejaribu kuuingiza ulimwengu pamoja na ardhi yake na mbingu yake katika yai bila ya kulikuza yai hilo au kuufanya mdogo ulimwengu!

NEMBO YA UISLAMU

Nilisoma makala katika gazeti la Al-Jumhuriyya la Misri la tarehe 21 Aprili 1967 yaliyoandikwa na Dhiyau Rayis, kwamba yeye alisoma makala katika jarida la fasihi la mwandishi mashuhuri wa Kiarabu akisema (Huyo mwandishi) alipokuwa Uingereza, aliwahi kubishana vikali na msomi mmoja Mwingereza kuhusu Uislamu na Ukristo. Akasema yule Mwingereza kupingana na Waislamu wote: Mimi ninaifupisha misingi yote ya Kikristo kwa neno moja tu,Upendo, Je unaweza wewe Mwislamu kuleta tamko linalokusanya misingi ya Kiislamu? Yule mwandishi akajibu: Ndio neno hilo ni Tawhid.

Baada ya Rayis kunakili mazungumzo haya akasema: Jawabu halikuwa sawa. Akataja sababu kadhaa za kutomwafiki kwake, kisha akasema: Lau swali hili ningeulizwa mimi, ningelijibu kuwa ni Rehema. Akatoa dalili kwa Aya nyingi na Hadith nyingi, akianzia na Bismillahir rahmanir rahim mpaka Aya inayosema:

﴿ وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا رَحْمَةً لِّلْعَالَمِينَ﴾

Nasi hatukukutuma ila uwe rehema kwa walimwengu. (21:107)

Amesema kweli Rayis kwamba jawabu la yule mwandishi halikuwa sawa.Lakini hata yeye Rayis pia jawabu lake halikuafiki,kwa kuchagua neno rehema.Kwa sababu hakuzidisha kitu katika aliyoyasema Mwingereza. Amechukua neno upendo na kulifasiri rehema. Kwa hiyo Uislamu unakuwa hautofautiani na Ukristo.

Lau mimi ningelikuwa pamoja na yule mwandishi, ningelijibu kwa neno unyoofu.(msimamo) Kwa sababu ni neno lenye kukusanya unyoofu katika itikadi tawhidi, vitendo, maadili, hukumu, na mafundisho yote yaliyo na rehema mapenzi na kusaidiana. Rehema ni moja katika misingi ya Kiislamu na sio Uislamu kamili; kama vile ambavyo tawhidi ni msingi katika misingi ya Uislamu na sio misingi yake yote.

Unyoofu ndio kipimo sahihi cha ukamilifu ambao mtu aweza kuufikilia wema wa dunia na Akhera. Ndio maana tunakariri katika swala zetu usiku na mchana: Tuongoze njia iliyonyooka. Mwenyezi Mungu amesema kumwambia Mtume wake mtukufu(s.a.w.w) :

﴿فَاسْتَقِمْ كَمَا أُمِرْتَ وَمَن تَابَ مَعَكَ وَلَا تَطْغَوْا إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ﴾

Endelea na unyoofu kama ulivyoamrishwa, (wewe) na wale wanaoelekea (kwa Mwenyezi Mungu) pamoja nawe; wala msiruke mipaka.Hakika Yeye anayaona mnayoyatenda. (11:112)

Amesema tena:

﴿إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ﴾

Hakika wale waliosema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu kisha wakafuata unyoofu, hao Malaika huwateremkia (wakiwaambia): Msiogope wala msihuzunike, na furahini kwa Pepo mliyokuwa mkiahidiwa. (41:30)

Hakuna kitu kinachofahamisha zaidi kwamba unyoofu ni muhimu, kuliko neno la Ibilisi aliyelaaniwa:

﴿قَالَ فَبِمَا أَغْوَيْتَنِي لَأَقْعُدَنَّ لَهُمْ صِرَاطَكَ الْمُسْتَقِيمَ ﴾

Basi nitawakalia (waja wako) katika njia yako iliyonyooka... (7:16)

Kuna Hadith tukufu inayosema kuwa Sufyan Thaqafi alimwambia Mtume: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Niambie neno ambalo sitamuuliza mtu mwingine baada yako milele.Mtume wa Mwenyezi Mungu akamwambia:Sema nimemwamini Mwenyezi Mungu, kisha ufuate unyoofu (msimamo).

Kwa ufupi maana ya unyoofu ni kuwa ndani ya mipaka ya Mwenyezi Mungu bila ya kukengeuka na haki kwa kuifuata batili na kuacha uongofu na kuwa katika upotevu. Vile vile kuwa kwenye njia iliyonyooka, njia ya (wale) ambao Mwenyezi Mungu amewaneemesha, sio ya wale walioghadhibikiwa wala waliopotea.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - FATIHA

BISMILLAH (UFUNGUZI)

SURA YA KWANZA KUSHUKA

Wametofautiana kuhusu mahali iliposhuka, imesemwa kuwa ni Makkah wengine wakasema ni Madina bali kuna kundi jengine linasema kuwa imeshuka mara mbili Makkah na Madina.Hata hivyo wafasiri wengi wamesema imeshuka Makkah.

Tofauti hii, kwa hakika, haina faida kwani surah hii tukufu haina Aya zozote zinazotofautiana kimaana kwa kutofautiana kushuka. Majina yake Wametaja majina mengi; yaliyo maarufu ni haya yafuatayo:-

Faatiha (ufunguzi) : Kwa sababu ndiyo sura ya kwanza katika msahafu, na ni wajibu kuisoma mwanzo wa swala. Pia mafundisho, kwa ujumla, yalikuwa yakianzwa kwa sura hiyo.

Al-Hamdu : kwa sababu ndilo tamko la mwanzo katika sura hiyo.

Ummul-Kitab na Ummul-Quran (mama wa Quran) : kwa sababu imetangulia sura nyingine, ijapokuwa ni kwa kimandishi tu.Kwani mama huwatangulia wanawe. Na kwa vile imekusanya misingi miwili; kutaja utawala wa Mungu na utumwa wa mja, na mambo mawili hayo ndiyo nguzo ya mafundisho ya Quran.

Sabu’ul-Mathani (Saba mbili) : kwa sababu ina aya saba, au ina Aya saba zinazorudiwa mara mbili katika swala, au ni kwa sababu inataja maambo mawili: Mola na mja wake.

Vyovyote iwavyo majina haya yana mwelekeo kidogo.

Ayah 1-7

﴿بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ ﴾

1.Kwa jina la Mwenyezi Mungu,Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

﴿الْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴾

2.Sifa njema (zote) ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe (vyote).

﴿لرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ ﴾

3.Mwingi wa Rehema Mwenye Kurehemu.

﴿ مَالِكِ يَوْمِ الدِّينِ﴾

4.Mwenye kumiliki Siku ya Malipo.

﴿يَّاكَ نَعْبُدُ وَإِيَّاكَ نَسْتَعِينُ ﴾

5.Wewe tu tunakuabudu, na Wewe tu tunakuomba msaada.

﴿اهْدِنَا الصِّرَاطَ الْمُسْتَقِيمَ﴾

6.Tuongoze njia iliyonyooka.

﴿صِرَاطَ الَّذِينَ أَنْعَمْتَ عَلَيْهِمْ غَيْرِ الْمَغْضُوبِ عَلَيْهِمْ وَلَا الضَّالِّينَ ﴾

7.Njia ya (wale) uliowaneemesha; Sio ya (wale) waliokasirikiwa wala ya (wale) waliopotea.

SIFA NJEMA (ZOTE) NI ZA MWENYEZI MUNGU

Sifa njema (zote) ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe (vyote).

Jumla hii ni habari, kwa maana ya insha; Kwa sababu msomaji anakusudia kuleta sifa njema za Mwenyezi Mungu, wala sio kutoa habari za kuthibitisha sifa Zake njema.

Jumla hiyo ina maana ya mafunzo kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa waja wake, jinsi watakavyomsifu Mwenyezi Mungu. Yaani:Semeni enyi Waja wangu! Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu.

Maana ya sifa njema (zote) ni za Mwenyezi Mungu, ni kumsifu kwa kukusudia kumwadhimisha katika hali zote, hata katika madhara. Amirul Muminin(a.s) anasema katika moja ya khutba zake za Nahjul-Balagha:

Tunamsifu Mwenyezi Mungu kwa neema zake, kama tunavyomsifu kwa balaa.

Muhammad, Ahmad, Mahmuud na Hamdaan, ni majina yaliyochukuliwa kutoka katika neno Al-Hamdu. Neno Hamd linakuja kwa kukisifu kitu unachokiridhia. Mwenyezi Mungu (s.w.t) hapa anataja Mahmuud (chenye kusifika) akisema:

﴿عَسَىٰ أَن يَبْعَثَكَ رَبُّكَ مَقَامًا مَّحْمُودًا﴾

Huenda Mola wako akakuinua cheo chenye kusifika (17:79)

Neno: Rabb linaweza kutumiwa kwa maana ya Bwana na Mwenye kumiliki.Maana zote mbili zinasihi hapa, lakini maana ya Mola Muumbaji ndiyo inayoelekea zaidi katika aya hii tukufu.

MAKUSUDIO YA ALALAMIN (VIUMBE)

Makusudio ya Alalamin (viumbe) hapa ni; kila kisichokuwa Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo linaenea kwa viumbe vyote.

MAANA YA RABBIL-AALAMIN (MOLA WA VIUMBE VYOTE)

Maana ya Rabbil-Aalamin (Mola wa viumbe vyote) ni Muumbaji wa kila kitu, na mwenye kupangilia vizuri.

NENO MOLA

Neon: Mola linafahamisha utukufu; yaani:Hakika mimi ninamsifu Mwenyezi Mungu kwa sababu Yeye ni Mola wa viumbe vyote.

MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

Mwingi wa rehema mwenye kurehemu: Maelezo yake yameshapita katika maelezo ya Bismillah Miongoni mwa maneno ya Amirul Muminin katika kumsifu Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anasema:Ghadhabu haimshughulishi (asiwe) na rehema wala rehema haimshughulishi (asiwe) na mateso.

Nilivyofahamu jumla mbili hizi ni kwamba ghadhabu ya Mwenyezi Mungu kwa waasi, na adhabu yao kesho, haimzuii Yeye kuwarehemu katika maisha haya wanayostarehe kwa neema yake na kwamba rehema Yake kesho haiwaondolei waumini balaa na maovu katika maisha haya. Mwenye kumiliki siku ya malipo Neno Din lina maana nyingi; miongoni mwayo ni malipo. Na maana haya ndiyo yanayonasibiana na hapa, ambapo siku hiyo italipwa kila nafsi yale iliyoyachuma.

NENO MAALIKI

Neno: Maaliki husomwa kwa alifu, kwa maana ya kuhusisha (umilikaji); kama inavyosemwa: Fulani ndiye mwenye kumiliki bustani hii (mwenye kuhusika nayo). Pia husomwa Maliki bila ya Alifu (kwa kutovuta) kwa maana ya mfalme, kama inavyosemwa: Mfalme wa Ugiriki, kwa maana ya Mtawala.

Visomo vyote viwili vinatumika, ingawaje cha kwanza ndicho kinachotumika zaidi.Maana inayokuja haraka akilini, kwa kusoma namna zote mbili ni moja: Kuwa kila kitu kiko mikononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake, leo na kesho. Yeye ni Mola wa viumbe vyote, na Mola wa Siku ya malipo. Lengo ni kukemea watu na maasia na kuwavutia katika twaa. Katika Nahjul Balagha Imam Ali(a.s) amesema:

Hakika sisi hatumiliki chochote kwa Mwenyezi Mungu, wala hatumiliki isipokuwa kile alichotumilikisha. Alipotumilikisha kile ambacho Yeye amekimiliki huwa ametukalifisha nacho, na anapotuondolea huwa ametuondolea taklifa yake.

Wewe tu tunakuabudu, na Wewe tu tunakuomba msaada. Mja kumzungumzia Mola wake kwa dhamiri ya Mmoja (Wewe tu) ni kwa ajili ya kumtakasa katika Umoja wake, na pia kumtakasa na shirk. Kwa ajili hii, halinganiwi Mwenyezi Mungu kwa tamko la wingi. Ama dhamiri ya wingi (sisi) katika neno tunakuabudu na tunakuomba msaada ni ya mwenye kusema (mja) pamoja na mwingine, wala sio ya kutukuza.

Ibada inathibitika kwa Saumu, Swala, Hijja na Zaka kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu. Vile vile inathibitika kwa huduma yoyote ya kibinadamu ya kutekeleza haja za watu. Kuna Hadith inayosema:Watu wa mema duniani ni wa mema Akhera. Bora wa watu ni yule mwenye kuwafaa zaidi watu.

MAANA YA WEWE TU TUNAKUABUDU NA WEWE TU TUNAKUOMBA MSAADA

Sio kwamba Mungu ni wa kuabudiwa tu basi iwe imetosha. Bali vile vile Aya inafahamisha kuwa mtu ni kiumbe kitakatifu aliyekombolewa (aliyehuru) kutokana na utumwa na unyonge isipokuwa kwa haki tu, ambayo iko juu ya kila kitu na wala haikaliwi juu. Kimsingi ni kwamba uhuru usiowekewa mpaka na haki, hubadilika na kuwa machafuko. Katika maneno yenye faida niliyoyasoma, yanayohusiana na mlango huu, ni maneno ya Jean Paul Sartre, aliposema, Hakika uhuru hasa ni akujilaz- imisha mtu kujitolea nafsi yake na uhuru wake katika kuwatumikia wengine.

KISA

Kulikuwa na watu wawili wakitembea katika bustani. Mmoja alikuwa na fimbo akicheza nayo.Mara ikagusa ncha ya pua ya mwenzake. Alipomlaumu kwa kitendo hicho, yule mwenye fimbo akajigamba: Nina uhuru bwana! Mwenzake akamwambia, Uhuru wako una mpaka; mwisho wake ni pua yangu!

Mimi siupingi uhuru ikiwa mpaka wake ni kumwamini Mwenyezi Mungu na kumwabudu Yeye peke yake. Kwa sababu mwenye kuabudu haki tu atakuwa amejikomboa na batili; na mwenye kujikomboa na kuabudu haki, bila ya shaka atakuwa mtumwa wa batili. Haiwezekani kutofautisha katika mawili hayo isipokuwa kwa yule ambaye hana mpangilio; asiyeamini halali wala haramu, wala kuamini kitu chochote kingine isipokuwa nafsi yake peke yake.

*1 Sartre mwanzo alikuwa na nadharia ya Existentialism (kuwako) akidai kwamba kila mtu na lake, na hanasibiani na chochote isipokuwa kuwako kwake peke yake. Huko kuwako kwake hakuwezi kuthibiti isipokuwa kwa kuwa huru bila ya kuwa na kikwazo chochote au sharti lolote. Ama dini, misingi, na kuweka mambo katika vipimo, ni upuuzi. Hakuna heri isipokuwa heri ya mtu mwenyewe wala hakuna shari isipokuwa shari yake mwenyewe.

Kwa nadharia hii Satre anatoa dalili kuwa mtu amekuja kutoka katika ulimwengu usiojulikana,na anaelekea ulimwengu usiojulikana na kwamba yeye alikuwako kabla ya kanuni za kiakili na za kidini. Kwa hiyo, yeyote atakayejitia katika dini au katika msingi wowote, atakuwa amejifunga na kuuacha uhuru wake na kwa hivyo amejikanushia kuwako kwake.

Kisha akabadilisha falsafa yake hii akaingia katika falsafa ya Uhuru mkubwa, nao ni uhuru kwa ajili ya mamilioni; kwamba mtu anaichumia, nafsi yake, ikiwa atajiweka katika kuwahudumia wengine; kwambamtu hasa ni yule anayelazimiana na misingi hii. Badala ya kuwa anazungumzia juu ya hali ya mtu mmoja peke yake, akawa Satre anazungumzia juu ya haki za watu wengi na kulitetea hilo!

MAKUSUDIO YA NJIA ILIYONYOOKA

Tuongoze njia iliyonyooka : Makusudio ya njia iliyonyooka si elimu tu, bali ni elimu pamoja na tawfiki katika vitendo (amali). Mwenye kukutakia uongofu amekutakia heri yote, na mwenye kukutakia elimu amekutakia baadhi ya heri.

Maajabu ni kuwa watu wengi wanakuwa wazito kuomba uongofu, hasa wanavyuoni na watu wakubwa, pamoja na kujua kuwa Mtukufu Mtume(s.a.w.w) alikuwa akikariri kuomba uongofu usiku na mchana katika swala zake na sehemu nyinginezo.

Sijui kama kuna uongofu na tawfiki bora na kubwa zaidi kuliko ile ya mtu kugundua aibu zake mwenyewe na kujilaumu, na kumchoma sana.Kwa kutambua hayo inawezekana mtu kuokoka. Mwenyezi Mungu atukinge na ghururi na maovu yake!

MAKUSUDIO YA WALIOKASIRIKIWA NA WALIOPOTEA

Njia ya (wale) uliowaneemesha; sio ya (wale) waliokasirikiwa wala ya (wale) waliopotea . Imepokewa Hadith kwamba:makusudio ya waliokasirikiwa ni Wayahudi, na waliopotea ni Wakristo . Lakini tamko la Aya ni la jumla, wala sio mahsusi au kuvua wengine (kubagua).

Kila mtiifu anaingia katika neema na rehema ya Mwenyezi Mungu, na kila mwenye kuasi ni mwenye kupotea na kughadhibikiwa.

LENGO LA SURA NZIMA YA FATIHA

Vyovyote iwavyo, lengo la Aya hii na sura nzima ya Fatiha, ni kuwa mja asimame mbele za Bwana wake akiwa ni Muumini mwenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu, mwenye kushukuru, mwenye kumsifu, mwenye ikhlasi, na mwenye kuomba tawfiki kwa elimu na kwa vitendo.

Na kila mtu ataikuta amali aliyoitanguliza kwa Muumba wake. Ama maneno tu, hayana athari isipokuwa kujikurubisha na twaa, au kujiweka mbali na maasia.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NGO’MBE)

SURA YA PILI

Amesema mwenye Majmaul-Bayan kwamba: sura hii yote imeshuka Madina, isipokuwa Aya ya 281.

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

﴿ الم ﴾

1.Alif Laam Miim

﴿ ذَٰلِكَ الْكِتَابُ لَا رَيْبَ فِيهِ هُدًى لِّلْمُتَّقِينَ ﴾

2.Hiki ni kitabu kisicho na shaka ndani yake; ni uwongozi kwa wamchao Mwenyezi Mungu.

﴿ الَّذِينَ يُؤْمِنُونَ بِالْغَيْبِ وَيُقِيمُونَ الصَّلَاةَ وَمِمَّا رَزَقْنَاهُمْ يُنفِقُونَ ﴾

3.Ambao wanaamini ghaibu na wanasimamisha Swala na wanatoa katika yale tuliyowapa.

﴿ وَالَّذِينَ يُؤْمِنُونَ بِمَا أُنزِلَ إِلَيْكَ وَمَا أُنزِلَ مِن قَبْلِكَ وَبِالْآخِرَةِ هُمْ يُوقِنُونَ ﴾

4.Na ambao wanaamini yaliyoteremshwa kwako, na yaliyoteremshwa kabla yako na akhera wana yakini nayo.

Amesema mwenye Majmaul-Bayan kwamba: sura hii yote imeshuka Madina, isipokuwa Aya ya 281.

﴿ أُولَـٰئِكَ عَلَىٰ هُدًى مِّن رَّبِّهِمْ وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴾

5.Hao wako juu ya uwongozi utokao kwa Mola wao, na hao ndio wenye kufaulu.

MIANZO YA BAADHI YA SURA

Aya 1- 5

﴿الم﴾

Alif Lam Mim :

Wamehitalifiana wanavyuoni kuhusu makusudio ya mwanzo huu na ya mianzo ya sura nyingine inayofanana na hii mfano:

Alif Laam Miim Raa, Kaaf Haa Yaa Ayn Swaad na Haa Miim. Imesemekana kuwa herufi hizo ni katika elimu ya ghaibu ambayo Mwenyezi Mungu hakuidhihirisha kwa yeyote.Lakini sidhani kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anaweza kuwaambia watu jambo asilotaka walijue. Zaidi ya hayo Mwenyezi Mungu amewakemea wale ambao hawaifikiri vizuri Quran, aliposema:

﴿أَفَلَا يَتَدَبَّرُونَ الْقُرْآنَ أَمْ عَلَىٰ قُلُوبٍ أَقْفَالُهَا ﴾

Je,hawaizingatii (hii) Quran au katika nyoyo zao kuna kufuli? ( 47:24).

Pia imesemekana mianzo hii ni majina ya sura; vilevile imesemwa ni majina ya Mwenyezi Mungu, aidha ikasemwa kuwa; ni ya Muhammad(s.a.w.w) nk.. Lakini linaloelekea zaidi ni kauli inayosema kwamba: Mwenyezi Mungu (s.w.t.) baada ya kuwaambia wapinzani walete mfano wa Quran, au sura kumi, au moja; na wakashindwa, ndipo akataja herufi hizi. Yaani, kitabu hiki ambacho ni muujiza, hutokana na herufi hizi ambazo hata watoto na wajinga pia wanazitumia, lakini nyinyi mmeshindwa.

Kwa hivyo kushindwa kwenu ni dalili wazi kwamba kuna siri, na siri yenyewe ni kuwa hii Quran ni wahyi wa kidini sio usanii wa kidunia.

QURAN NA SAYANSI

Kauli yake Mwenyezi Mungu:Ni uwongozi kwa wamchao Mwenyezi Mungu , ni dalili wazi kwamba Quran si kitabu cha elimu ya Historia, wala Falsafa, au elimu ya Fizikia au ya Hesabu; isipokuwa ni kitabu cha elimu ya uongofu wa mwana-adamu katika dunia na akhera, au sema: Quran ni kitabu cha dini, maadili, itikadi na sharia.

Kama utauliza : Ikiwa Quran ni kitabu cha dini, mbona basi kuna Aya zinazohusu mambo ya kilimwengu; kama vile:

﴿وَالشَّمْسُ تَجْرِي لِمُسْتَقَرٍّ لَّهَا ﴿٣٨﴾ وَالْقَمَرَ قَدَّرْنَاهُ مَنَازِلَ﴾

Na jua linakwenda mpaka kituoni pake; na mwezi tumeupimia vituo (36:38- 39).

Jibu : Lengo la Aya hizi sio kutubainishia hali ya maumbile kwa undani wa kielimu - kwani hilo limeachiwa akili na majaribio yake - isipokuwa lengo la kwanza la kutajwa Aya hizo ni kwamba, kujua ulimwengu na nidhamu yake kutatuongoza kujua kuwa kuna Mungu, na kwamba huu ulimwengu haukupatikana kibahati tu bila ya kukusudiwa; kama wanavyodai watu wa kimaada. Bali ulipatikana kwa matakwa ya kihekima. Mwenyezi Mungu amelibainisha hilo katika Aya isemayo:

﴿سَنُرِيهِمْ آيَاتِنَا فِي الْآفَاقِ وَفِي أَنفُسِهِمْ حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ﴾

Tutawaonyesha ishara zetu zilizo katika upeo wa mbali na zilizo katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli. (41:53).

Yaani, tutawafafanulia makafiri - kwa vile watakavyoufahamu ulimwengu kutokana na mipangilio mizuri ya Mwenyezi Mungu - kuwa wao wako katika upotevu. Quran inapotoa mwito wa kuangalia ulimwengu, inasema kwa lugha iliyo wazi kuwa dalili za ulimwengu ni hoja ya kweli na ni dalili yenye nguvu zaidi juu ya kuwapo Mungu, kuliko kitu chochote. Baadhi ya wenye hekima wamesema: Mwenyezi Mungu ana vitabu viwili: Kitabu kinachosomwa na kitabu cha akili, ambacho ni ulimwengu.

Ni kweli kuwa Quran inahimiza kusoma sayansi na kila elimu itakayompa binadamu ufanisi. Lakini kuhimiza ni kitu kingine na kuwa ni kitabu cha elimu hiyo ni kitu kingine. Katika ambayo yanatia nguvu na kuunga mkono kwamba Quran ni kitabu cha uongofu, sharia, na maadili mema, na kwamba Quran imeteremshwa kwa lengo hili, ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿هَـٰذَا بَصَائِرُ مِن رَّبِّكُمْ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ﴾

Hizi (Aya za Quran) ni dalili zitokazo kwa Mola wenu na ni uongofu na rehema kwa watu wanaoamini. (7:203).

Amesema tena:

﴿كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ لِتُخْرِجَ النَّاسَ مِنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ﴾

(Hiki) ni kitabu tulichokiteremsha kwako ili uwatoe watu katika giza uwapeleke kwenye nuru. (14:1).

Na Mtume mtukufu(s.a.w.w) anasema:Hakika hapana jingine, nimetumwa kutimiza tabia njema . Na amesema Amirul Muminin(a.s) katika hotuba ya 174, ya Nahjul-Balagha:

Hakika Quran ni dawa ya ugonjwa mkubwa sana wa kufuru, unafiki na upotevu.

Kwa maneno haya tunapata tafsiri ya Aya isemayo:

﴿وَنُنَزِّلُ مِنَ الْقُرْآنِ مَا هُوَ شِفَاءٌ وَرَحْمَةٌ لِّلْمُؤْمِنِينَ وَلَا يَزِيدُ الظَّالِمِينَ إِلَّا خَسَارًا ﴾

Na tunateremsha katika Quran yale ambayo ni ponyo na rehema kwa wanaoamini, wala hayawazidishi madhalimu ila hasara tu! (17:82).

Kama utauliza mara ya pili: Unasemaje kuhusu Aya hii.

﴿مَّا فَرَّطْنَا فِي الْكِتَابِ مِن شَيْءٍ﴾

Hatukupuuza kitabuni kitu chochote, (6:38)

si inafahamisha kuwa katika Quran kuna elimu zote?

Jawabu : Kutosha kila kitu huwa ni kulingana na mahitaji. Ukisema: Nyumba hii ina kila kitu; itafahamika kwamba ina mahitaji ya mwenye kukaa humo. Kama ukisema: Kitabu cha Fiqh kina kila kitu, itafahamika kuwa mna masuala yote ya kifiqh. Quran ni kitabu cha dini. Kwa hiyo pale Mungu aliposema. Hatukupuza kitabuni kitu chochote, maana yake ni kila kinachoambatana na heri ya mtu na uongofu wake. Swali la tatu: Unasemaje kuhusu vitabu hivi vyenye majina kama: Quran na Sayansi, Uislamu na tiba ya kisasa, na vingenevyo?

Jibu :Kwanza : kabisa, kila anayejaribu kulinganisha kati ya uvumbuzi wa kielimu wa kisasa au wa kizamani na Qurani, atakuwa anajaribu jambo lisilowezekana. Kwa sababu elimu ya binadamu ina mpaka kulingana na nguvu yake ya kiakili; na Quran ni elimu ya Mwenyezi Mungu ambayo haina mpaka. Itakuwaje kitu kilicho na mpaka kiafikiane na kisichokuwa na mpaka?

Pili : elimu ya binaadamu inaingiliwa na makosa. Kwa sababu inakuwa ni dhana na makisio; inakosea na kupata. Mara ngapi tumewaona wataalamu wakikongamana juu ya nadharia fulani na kudai kuwa ni kweli mia kwa mia; kisha wao wenyewe au wale watakaokuja baada yao wanagundua kuwa ni makosa mia kwa mia? Quran ni yenye kuhifadhiwa na makosa. Itakubalika vipi kuoanisha chenye makosa na kile kisicho na makosa? Kisha je tuendelee kugeuza Quran kila yanapogeuka makisio ya elimu na nadharia zake? Hapana. Ndio! hapana ubaya kujisaidia na ugunduzi wa kielimu katika kufahamu baadhi ya Aya, lakini kwa sharti ya kutoufanya huo ugunduzi kuwa ni kipimo cha ukweli na kusihi Quran, bali hata kutozifanya hizo elimu kuwa ndio nyezo za kufahamu siri ya Quran na kufahamu hekima ya baadhi ya hukumu zake.

Inawezekana kuwa hili ndilo lililowafanya watungaji kutunga vitabu kama: Quran na Sayansi n.k. Vyovyote iwavyo, sisi tuna yakini kwamba tuna hoja zenye nguvu katika dini yetu, na tuna dalili za kutosha juu ya ukweli wake; hatuna haja kabisa na vilivyo kwa wengine. Bali tunaamini kwamba wengine ndio walio na haja kwetu katika hilo. Kwa hakika historia ya binadamu haitapata dini yenye utengeneo zaidi ya dini ya Kiislamu, wala kitabu chenye kunufaisha zaidi ya kitabu chake, au Mtume mtukufu zaidi ya Mtume wake. Na yule ambaye hakuongoka kwa dalili za Quran na mwito wake wa maisha mema, basi hataweza kukinaishwa na ugunduzi wa kisayansi wa sasa au wa zamani.

Kuna kitu nilichokifikiria ambacho huenda kikapunguza machovu ya msomaji kuhusu majibu ya yule anayejaribu kuilinganisha Quran na ugunduzi wa sayansi; kama ifuatavyo:

Uzayr alipita katika mji uliokufa, akiwa na punda wake, chakula chake na kinywaji chake akastaajabu na kusema:

﴿ أَنَّىٰ يُحْيِي هَـٰذِهِ اللَّـهُ بَعْدَ مَوْتِهَا﴾

Mwenyezi Mungu atauhuisha vipi (mji) huu baada ya kufa kwake? (2:259).

Mwenyezi Mungu akataka kuuondoa mshangao wake. Akamfisha miaka mia. Chakula na kinywaji alichokuwa nacho, kilibakia katika hali yake bila ya kuharibika katika muda wote huo. Kisha Mwenyezi Mungu akamfufua na akataka kumwonyesha miujiza yake ya ajabu, akamwambia:

﴿ فَانظُرْ إِلَىٰ طَعَامِكَ وَشَرَابِكَ لَمْ يَتَسَنَّهْ﴾

Tazama chakula chako na kinywaji chako hakikuharibika (2:259).

Hebu angalia msomaji! Je,chakula cha Uzayr kilikuwa katika jokofu (friji)? Swali hili linamhusu mwenye kuilinganisha Quran na elimu ya kisasa.

Hakuna anayetia shaka kwamba jokofu hili ambalo lilihifadhi chakula na kinywaji kwa muda wa miaka mia, pengine linaweza kuwa ni sampuli ya mwaka 2000, na wala siyo ya mwaka 1967. Ndio! Inawezekana kulinganisha sayansi na kufahamu maana ya Quran tukufu; hasa kwa upande wa nadharia ya relativity (uwiano). Kwa vile kufahamu kunahusika na upande fulani katika maana yake, na kunatofautiana na hali ya anayesoma au anayesikiliza.

Kama mtu akisema kuwa tofauti hii haihusiki na Quran peke yake, kwa sababu nadharia ya uwiano ni ya jumla, isiyokubali kuhusishwa, tutajibu: Hiyo ni sawa, lakini maana ya Quran yamejiandaa na hilo. Na hili linatilia nguvu maelezo yetu kwamba mtu mwenye kuganda na kauli za wafasiri bila ya kuongeza kitu, atakuwa na akili ya kusoma tu, lakini sio akili ya mwamko. Basi twamuomba Mwenyezi Mungu azijaalie fahamu zetu katika Aya zake kuwa ni za mwamko na sio fahamu za kunakili.

Wamchao Mwenyezi Mungu Maana ya neno kucha (takua) kilugha ni kujichunga na kitu chochote. Na maana yake kisheria ni kujikinga na hasira za Mwenyezi Mungu na adhabu Yake, kujikinga na kuuacha wajibu na kutenda haram. Amesema Amirul Mumini Ali(a.s) :Kumcha Mwenyezi Mungu ndio msingi wa tabia njema. Wengine wamesema:kumcha Mwenyezi Mungu ni kuwa Mwenyezi Mungu asikuone na lile alilokataza na kutoacha alilokuamrisha.

Kumcha Mungu ndiko kunakomfanya mtu kuwa bora mbele ya Mwenyezi Mungu.Quran inasema:

﴿ نَّ أَكْرَمَكُمْ عِندَ اللَّـهِ أَتْقَاكُمْ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ ﴾

Hakika Mtukufu wenu zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule amchae Mungu zaidi. (49:13).

Unaweza kuuliza, ikiwa wenye kumcha Mungu ni wenye kuongoka, basi wana haja gani ya kuongozwa? Je mwanachuoni anahitaji wa kumfundisha? Jibu: Hakika mwalimu hufundisha wanafunzi wote wajinga na wenye akili, lakini wale wanaonufaika na mwalimu ni wale wenye akili wanaojitahidi

ambao mwisho wao utakuwa ni kufaulu. Kwa hivyo ni sawa tukisema kuwa mwalimu ni wa wenye kufaulu. Vile vile Quran tukufu imewaeleza watu wote, lakini wanaonufaika nayo ni wale waumini wenye kumcha Mungu. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ وَالَّذِينَ اهْتَدَوْا زَادَهُمْ هُدًى وَآتَاهُمْ تَقْوَاهُمْ ﴾

Na wale wanaokubali kuongoka Mwenyezi Mungu anawazidishia uongofu. (47:17)

WANAOAMINI GHAIBU

MAARIFA

Inasemekana kuwa mwanachuoni mmoja mkubwa aliyekuwa na heshima na cheo kikubwa huku watu wakimzunguka kwa kumuuliza maswali na kumnyenyekea, alionewa kijicho na mpinzani wake mmoja. Akamuuliza swali la kutatiza kwa sauti kubwa, ili wote wasikie. Mwanachuoni akasema: Sijui. Muulizaji akasema: Mahali ulipo ni pa anayejua sio pa asiyejua. Akasema mwanachuoni: Ole wako! Hapa ni mahali pa anayejua kitu sio kila kitu; anayejua kila kitu hana mahali.

Ndio! ni muhali kwa mtu kujua kila kitu. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ وَمَا أُوتِيتُم مِّنَ الْعِلْمِ إِلَّا قَلِيلًا﴾

Nanyi hamkupewa katika elimu ila kidogo tu. (17:85).

Hakuna mtu yeyote anayezaliwa na ujuzi, isipokuwa hupata maarifa muda baada ya muda, kutokana na sababu fulani; hata hilo jina lake pia halijui, isipokuwa baada ya kuitwa mara kwa mara. Wajuzi wa fani ya maarifa wametaja sababu nyingi za maarifa ambazo ni:

1. Kujua kutokana na hisia tano: Kujua rangi kwa kuona, sauti kwa kusikia,harufu kwa kunusa, ladha kwa kuonja na ugumu kwa kugusa. Vile vile kuna yale anayoyahisi mtu kwa hisia za kindani; kama njaa, shibe, mapenzi na chuki.

2. Kupata maarifa kutokana na uchunguzi na majaribio.

3. Kujua kwa misingi ya kikawaida; yaani kushirikiana na kukubaliana akili zote; mfano: Moja na moja ni mbili; na chenye kunufaisha ni bora kuliko chenye kudhuru. Au kujua kutokana na majaribio; kwa mfano kuamua kwamba kila kipande cha chuma ni kigumu, baada ya kujaribu kipande kimoja tu. Kwa hiyo hukumu inaenea kwa vyuma vyote lakini maarifa yametokana na majaribio ya kimoja.

4. Kujua bila ya kupata maalumati yoyote ya hisia, majaribio au nguvu ya akili; bali kupata moja kwa moja. Hilo ni baada ya jitihadi ya kuitakasa nafsi na uchafu; kama wasemavyo masufi. Kwa ufasaha zaidi ni kwamba moyo mbele za msufi ni kama akili kwa wengine. Kama ilivyo akili kutambua baadhi ya vitu vingine kwa kujitahidi na kuangalia vizuri, basi hivyo hivyo moyo nao hutambua baadhi ya vitu bila ya jitihadi ya nafsi; kama kuhisi mapenzi, na chuki. Na hutambua vitu vingine baada ya jitihadi ya nafsi; kama kujua kuweko Muumbaji.

Kwa hiyo jitihadi ya akili kwetu sisi inafanana na jitihadi ya nafsi kwa masufi. Wala hakuna yeyote anayeweza kubishana na sufi katika maoni yake na itikadi yake. Kwa sababu ukimuuliza dalili, atakujibu kwamba imani yangu na elimu yangu inatoka katika dhati yangu peke yake. Na kama ukimuuliza: Kwa nini imani na elimu hii haitokei katika dhati za watu wote? Atakujibu: Kwa sababu wao hawakupitia majaribio ya kiroho niliyoyapitia mimi.

Sisi tunajiweka kando na msimamo wa kisufi, bila ya kufungamana na upande wowote. Hatuwezi kuuthibitisha, kwa sababu tuko mbali na tunavyoelewa na tulivyozowea. Pia hatuwezi kuukanusha, kwa sababu mamia ya

wanavyuoni katika kila zama hata katika zama zetu wanaamini kuwako nguvu ya usufi; na kutofautiana kwao kihali, kidini , na hata kilugha.Hatuna hoja yoyote inayokanusha majaribio ya kiutu kabisa. Inawezekana kuwa majaribio ya kisufi yanafanana na vipindi ambavyo anapata ilham (anafunukiwa) mshairi na msanii, lakini jambo hili linamuhusu yeye peke yake; wala hana hoja kwa mwingine.

GHAIBU (YASIYOONEKANA)

Kuna vitu ambavyo hakuna njia ya kuvijua kwa hisia, majaribio au nguvu ya akili, kama vile Lawhin Mahfudh (ubao uliohifadhiwa), Malaika, Iblis, Hisabu ya kaburi, Pepo na Moto.Vile vile miujiza ya Mitume; kama fimbo kugeuka kuwa nyoka, kufufua watu, n.k. Akili haiwezi kugundua mambo hayo wala hatujayaona. Yote hayo ni makusudio ya ghaibu katika neno lake Mwenyezi Mungu: wanaamini ghaibu.

Kwa hiyo ghaibu ni ile ambayo haijulikani isipokuwa kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kupitia katika ulimi wa ambaye umethibitika Utume wake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ وَعِندَهُ مَفَاتِحُ الْغَيْبِ لَا يَعْلَمُهَا إِلَّا هُوَ﴾

Na kwa Mwenyezi Mungu ziko funguo za siri hapana azijuaye ila Yeye (6:59)

Kwa hali hii, inatubainikia kuwa kuamini ghaibu ni sehemu ya Uislamu, na kwamba asiyeiamini sio Mwislamu.

Vile vile inabainika kuwa jambo ambalo halijulikani kwa kuona, majaribio au akili; au lisilosimuliwa na Kitabu cha Mwenyezi Mungu wala mapokezi ya Mtume, basi litakuwa ni katika vigano. Na vigano vingi vinatokana na mapokezi ya Mayahudi na mfano wao.


3

4

5

6

7

8

9

10

11

12

13

14

15