TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
Kundi:

Matembeleo: 35914
Pakua: 3093


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Juzuu 9 Juzuu 10 Juzuu 11
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 20 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 35914 / Pakua: 3093
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

Mwandishi:
Swahili

15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NG’OMBE)

﴿ قُلْ مَن كَانَ عَدُوًّا لِّجِبْرِيلَ فَإِنَّهُ نَزَّلَهُ عَلَىٰ قَلْبِكَ بِإِذْنِ اللَّـهِ مُصَدِّقًا لِّمَا بَيْنَ يَدَيْهِ وَهُدًى وَبُشْرَىٰ لِلْمُؤْمِنِينَ﴾

97.Sema: Anayemfanyia uadui Jibril Hakika yeye ameiteremsha Quran moyoni mwako, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, inayosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na ni uongozi na bishara kwa waumini.

﴿ مَن كَانَ عَدُوًّا لِّلَّـهِ وَمَلَائِكَتِهِ وَرُسُلِهِ وَجِبْرِيلَ وَمِيكَالَ فَإِنَّ اللَّـهَ عَدُوٌّ لِّلْكَافِرِينَ﴾

98.Anayemfanyia uadui Mwenyezi Mungu na Malaika wake na Mitume wake na Jibril na Mikail, basi Mwenyezi Mungu ni adui kwa makafiri.

﴿ وَلَقَدْ أَنزَلْنَا إِلَيْكَ آيَاتٍ بَيِّنَاتٍ وَمَا يَكْفُرُ بِهَا إِلَّا الْفَاسِقُونَ ﴾

99.Na hakika tumekuteremshia hoja zilizo wazi; na hawazikatai ila mafasiki.

﴿ أَوَكُلَّمَا عَاهَدُوا عَهْدًا نَّبَذَهُ فَرِيقٌ مِّنْهُم بَلْ أَكْثَرُهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ ﴾

100.Je, kila mara wanapofunga ahadi, kikundi katika wao huitupa? Bali wengi katika wao hawaamini.

ANAYEMFANYIA UADUI JIBRIL

Aya 97 - 100

LUGHA

Imesemekana kuwa maana ya neno Jibril ni mja wa Mungu (Abdullah) na Mikail ni mja mdogo wa Mwenyezi Mungu (Ubaidullah)

MAANA

Sema: Anayemfanyia uadui Jibril basi yeye ni kafiri, laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake.

Wamekubaliana wafasiri kwamba sababu ya kushuka Aya hii ni Mayahudi walimuuliza Mtume(s.a.w.w) kuhusu Malaika anayemteremshia wahyi. Akawajibu: Ni Jibril. Wakasema Ah! Huyo ni adui yetu, kwa sababu yeye huleta shida na vita na Mikail huleta amani na raha: lau angelikuwa Mikail ndiye anayekuletea wahyi tungelimwamini.

Wameufanya ushindani kwa dhahiri, kwanza kwenye ukabila wa Muhammad(s.a.w.w) kwamba wahyi ushuke kwa mmoja wa Waisrail. Mwenyezi Mungu na Mtume wake alipowashinda kwa hoja, wakabadilisha ushindani kwa Jibril sio Muhammad tena. Hakika ilivyo hasa - kama tulivyoelezea mwanzo - sio sababu ya Uarabu na Uyahudi au Jibril na Muhammad bali ni maslahi yao tu; ni uasherati, ulevi, riba na utapeli. Na wao wanafanya unafiki na kuficha uwongo wao. Kwa hivyo kwa upande wa malumbano na kuwapa hoja, Mwenyezi Mungu alisema:Hakika yeye ameiteremsha Quran moyoni mwako kwa idhini ya Mwenyezi Mungu inayosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake :

Yaani uadui wenu kwa Jibril hauna msingi, kwa sababu yeye ni mpelekaji wahyi tu, kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwenda kwa Muhammad. Na wahyi huo unasadikisha yaliyo katika Tawrat yenu, miongoni mwa sifa za Muhammad na bishara kwa wanaoamini. Kwa hivyo uadui wenu kwa Jibril ni uadui kwa Mwenyezi Mungu, wahyi, Tawrat, uongozi wa Mwenyezi Mungu kwa viumbe vyake na bishara kwa waumini.

Hakika tumekuteremshia hoja zilizo wazi na hawazikatai ila mafasiki: Yaani yaliyomjia Muhammad(s.a.w.w) hayana shaka baada ya kuwa na hoja na dalili, na wala hayakanushi isipokuwa mwenye kukufuru Mwenyezi Mungu; mwenye kuipinga haki. Makusudio ya ufasiki hapa ni ufasiki wa itikadi yaani ukafiri sio ufasiki wa vitendo ambao unatendwa na mtu anapokuwa na imani.

Je, Kila mara wanapofunga ahadi, kikundi katika wao huitupa? Ahadi walizozitupa Mayahudi na kuzivunja ni nyingi; Kama ya kumwamini Muhammad, ya kuacha kuwasaidia makafiri, ya kuwaamini Mitume na kutowaua na kutomwabudu yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu, n.k. kwa hiyo wakamkadhibisha Muhammad na wakawasaidia washirikina, walio maadui wao na wa Muhammad. Vile vile huko nyuma waliwakadhibisha Mitume wakawa tayari kumsulubu Masih, na waliabudu ndama na mengine mengi.

Bali wengi katika wao hawaamini. Yaani kuna kundi lililoabudu ndama na lililowaua Mitume, n.k; na wengi wao ingawaje hawakufanya hivyo, lakini bado ni makafiri, waovu. Kwa ufupi ni kwamba: asiyekuwa na haki anaweza kudai haki, na mwenye makosa anaweza kudai kuwa hana makosa. Wanayaweza hayo kwa mbinu za kusema. Lakini mara moja wanafedheheka zinapowashinda hoja na dalili ambazo hawawezi kuzikimbia; kama walivyofedheheka Mayahudi katika uwongo wao na madai yao kuwa wanafanya kama vile alivyoteremsha wahyi Mwenyezi Mungu.

Kuishi kwa amani na kumwamini mwenyezi mungu Wenye kulingania amani wanakusudia kuwa watamaliza tofauti za wanaozozana kwa mikutano. Lakini tumejifunza kuwa mazungumzo ya amani na haja ya kuwa na amani, hayawezi kufaa kitu kwa watu wenye kuangalia manufaa yao. Wenye tamaa hawawezi kuacha tamaa zao isipo-kuwa kwa njia ya vikwazo na vitisho. Maisha ya amani yanahitaji akili iliyofunguka na tabia njema. Ni tabia gani tukufu itakayokuwa mbele za mtu asiyeamini isipokuwa maada, ulanguzi na kutaka utajiri wa haraka haraka? Na ni hoja gani zitakazomkinaisha mwenye tamaa?

Inasemekana kwamba mataifa mawili makubwa ya Mashariki na Magharibi yanadai amani kati yao, lakini wakati huo huo kila mmoja anajitengeneza silaha za hali ya juu na kujikinga kwa kumhofia mwenzake. Kwa hivyo amani wanayodai ni ya maneno na wala si ya vitendo. Maumbile ya kiakili yanathibitisha kwamba kila taifa lina haki kamili katika kujiamulia mambo yake haliwezi kuingiliwa. Sasa je ni nani anayefuata misingi hii? Amani na haki haiwezi kupatikana kwa ukamilifu mpaka pande zote zinazohusika ziamini haki kwa njia ya haki. Ni muhali kuongoka kwenye heri na kutarajia heri yule asiyamini chochote isip-okuwa dhati yake na yule asiyejishug- hulisha na lolote zaidi ya manufaa.

﴿ وَلَمَّا جَاءَهُمْ رَسُولٌ مِّنْ عِندِ اللَّـهِ مُصَدِّقٌ لِّمَا مَعَهُمْ نَبَذَ فَرِيقٌ مِّنَ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ كِتَابَ اللَّـهِ وَرَاءَ ظُهُورِهِمْ كَأَنَّهُمْ لَا يَعْلَمُونَ﴾

101.Na walipojiwa na Mtume kutoka kwa Mwenyezi Mungu mwenye kusadikisha yale yaliyo pamoja nao, kikundi kimoja miongoni mwa wale waliopewa Kitabu cha Mwenyezi Mungu kilikitupa kitabu cha Mwenyezi Mungu nyuma ya migongo yao kama kwamba hawajui.

WALIPOJIWA NA MTUME

Aya 101

MAELEZO

Na walipojiwa na Mtume kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Ambaye ni Muhammad(s.a.w.w) ; aliyepelekwa na Mwenyezi Mungu kwa watu wote wakiwemo Mayahudi waliokuwa zama zake.Mwenye kusadikisha yaliyo pamoja nao . Yaani kusadikisha yaliyo katika Tawrat miongoni mwa misingi ya Tawhid na bishara ya Muhammad.Kikundi kimoja miongoni mwa wale waliopewa Kitabu. Nao ni wanavyuoni wa Kiyahudi.Kilitupa kitabu cha Mwenyezi Mungu nyuma ya migongo yao. Makusudio ya Kitabu, cha Mwenyezi Mungu, ni Quran. Imesemekana pia kuwa ni Tawrat, kwa sababu kumkana kwao Muhammad ni kuikana Tawrat ambayo imetoa bishara ya kuja Muhammad(s.a.w.w) . Hapa wanaingia wote Mayahudi na Manaswara. Kwani wote wamekipotosha Kitabu, hasa sehemu zile zinazofungamana na bishara ya kuja Muhammad(s.a.w.w) ; Bali hakuna tofauti kati ya Mayahudi na wale wanaoondoa maneno ya Mwenyezi Mungu kwa kufuata mapenzi yao.

﴿ وَاتَّبَعُوا مَا تَتْلُو الشَّيَاطِينُ عَلَىٰ مُلْكِ سُلَيْمَانَ وَمَا كَفَرَ سُلَيْمَانُ وَلَـٰكِنَّ الشَّيَاطِينَ كَفَرُوا يُعَلِّمُونَ النَّاسَ السِّحْرَ وَمَا أُنزِلَ عَلَى الْمَلَكَيْنِ بِبَابِلَ هَارُوتَ وَمَارُوتَ وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ أَحَدٍ حَتَّىٰ يَقُولَا إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ فَلَا تَكْفُرْ فَيَتَعَلَّمُونَ مِنْهُمَا مَا يُفَرِّقُونَ بِهِ بَيْنَ الْمَرْءِ وَزَوْجِهِ وَمَا هُم بِضَارِّينَ بِهِ مِنْ أَحَدٍ إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ وَيَتَعَلَّمُونَ مَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنفَعُهُمْ وَلَقَدْ عَلِمُوا لَمَنِ اشْتَرَاهُ مَا لَهُ فِي الْآخِرَةِ مِنْ خَلَاقٍ وَلَبِئْسَ مَا شَرَوْا بِهِ أَنفُسَهُمْ لَوْ كَانُوا يَعْلَمُونَ ﴾

102.Wakafuata yale yaliyofuatwa na mashetani, katika ufalme wa Suleiman; na Suleiman hakukufuru, bali mashetani ndio waliokufuru, wakiwafundisha watu uchawi na yaliyoteremshwa kwa Malaika wawili, Haruta na Maruta, katika (mji wa) Babilon Wala hawakumfundisha yeyote mpaka wamwambie: Hakika sisi ni fitna (mtihani), basi usikufuru. Wakajifunza kwao mambo ambayo kwayo waliweza kumfarikisha mtu na mkewe. Wala hawakuwa wenye kumdhuru yoyote kwa hayo ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.Na wanajifunza yatakayowadhuru wala hayawanufaishi. Na kwa hakika wanajua kwamba aliyeyanunua haya hatakuwa na sehemu yoyote katika akhera. Na hakika ni kibaya kabisa walichouzia nafsi zao laiti wangelijua.

WAKAFUATA YALE YALIYOFUATWA NA MASHETANI

Aya 102

MAELEZO

Wafasiri hapa wamerefusha maneno.Wengi wao hawana tegemeo lolote isipokuwa ngano ambazo hazikubaliki kiakili: Razi amechafua karibu kurasa ishirini katika kufasiri Aya hii, akazidisha mikanganyo.Mwenye Majmaul-Bayan naye akafanya hivyo hivyo. Ama Sayyid Qutb yeye ameingilia kuelezea mambo ya kuzugwa watu, ndoto, athari, n.k. Na huku hasa ndiko kukimbia. Kwa hivyo nikabaki muda mrefu nikitafuta na kupekuwa vitabu na tafsir. Hakikutulia kiu changu hata kwenye tafsir ya Sheikh Muhammad Abduh na wanafunzi wake wawili - Al-Maraghi na mwenye Tafsir ya Al Manar, Bora zaidi ya niliyoyasoma katika mlango huu ni yale yaliyotajwa katika kitabu cha Annuwatu fi Haqli I-hayat cha Sayyid Ubaydiy, Mufti wa Musul (Iraq). Na haya ndiyo aliyoyasema ninamnukuu: Niliendelea kutofahamu maana ya Aya tukufu kiasi ambacho hakikunitosheleza kwa mfasiri yoyote, mpaka nilipotua kwenye historia ya Free Mason, ndipo nikajua maana yake.

Kutokana na kugongana wafasiri kiasi ambacho walionyesha kuwa Aya ina vitu viwili vyenye kutofautiana na kuingiza katika Aya hii ngano za watu wa kale ambazo sharia iliyowazi inazikataa, nimeona ni wajibu nikitumikie kitabu cha Mwenyezi Mungu kuthibitisha haya. Ulipotukuka Ufalme wa Suleiman, mfalme wa Babiloni alikuwa na chuki na tamaa katika Palestine na Syria, na akaingiwa na hofu badala ya tamaa yake. Wakafanya msafara watu wawili walio wajanja na werevu wakitafuta mafunzo yatakayowawezesha kuuharibu ufalme wa Suleliman. Wakaingia dini ya Kiyahudi na kuonyesha utawa, kama kawaida wakapata wafuasi, wakawa wanaharibu fikra za watu na kuacha chuki kwa Suleiman mpaka wakamzulia ukafiri. Watu hawa walikuwa kama Malaika kwa wanavy- oonyesha utawa. Lakini walikuwa ni mashetani na mafunzo yao yalikuwa kama uchawi kutokana na ufasaha, na mara kwa mara walikuwa wakitumia neno mfalme kwa mtu mwema, na neno shetani kwa mtu mwovu na neno uchawi kwa ibara ya fitina. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu kumzungumzia Yusuf, alivyozungumziwa:

﴿ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا مَلَكٌ كَرِيمٌ ﴾

...Hakuwa huyu ila ni Malaika mtukufu. (12:31)

Na kauli yake:

﴿ شَيَاطِينَ الْإِنسِ وَالْجِنِّ يُوحِي بَعْضُهُمْ إِلَىٰ بَعْضٍ زُخْرُفَ الْقَوْلِ غُرُورًا﴾

Mashetani katika watu na majini wakifundishana wao kwa wao maneno ya kupamba kwa udanganyifu. (6:112)

Vile vile kauli yake Mwenyezi Mungu akimzungumzia Walid:

﴿ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا سِحْرٌ يُؤْثَرُ ﴿٢٤﴾ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا قَوْلُ الْبَشَرِ ﴾

Hayakuwa haya ila ni uchawi ulionukuliwa, hayakuwa haya ila ni kauli ya binadamu. (74:24-25)

Na kuna Hadith inayosema:Katika ufasaha kuna uchawi.

Tumeelezewa historia ya Nebukadnezzar, mfalme wa Babelon katika vita vya Palestin baada ya Suleiman na alivyoiharibu Baitul Maqdis. Na tunaiona Quran inatilia nguvu matukio ya historia katika Aya isemayo:

﴿ وَقَضَيْنَا إِلَىٰ بَنِي إِسْرَائِيلَ فِي الْكِتَابِ لَتُفْسِدُنَّ فِي الْأَرْضِ مَرَّتَيْنِ وَلَتَعْلُنَّ عُلُوًّا كَبِيرًا ﴿٤﴾ فَإِذَا جَاءَ وَعْدُ أُولَاهُمَا بَعَثْنَا عَلَيْكُمْ عِبَادًا لَّنَا أُولِي بَأْسٍ شَدِيدٍ فَجَاسُوا خِلَالَ الدِّيَارِ وَكَانَ وَعْدًا مَّفْعُولًا ﴾

Na tukawafahamisha wana wa Israil katika kitabu: Hakika nyinyi mtafanya uharibifu katika nchi mara mbili na kwa yakini mtatakabari kutakabari kukubwa. Basi ilipofika ahadi ya kwanza yake tukawapelekea watumishi wetu wenye mapigano makali, mno wakaingia majumbani kwa nguvu, na hii ilikuwa ahadi iliyotimizwa. (17:4-5)

Ukiyajua haya, basi tunasema: Dhamiri katika kauli ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.), na wakafuata, inawarudia Mayahudi wa Madina, ambao zimetangulia zaidi ya Aya sitini na mbili katika kuwaeleza wao tu. Utakapoyajua haya, kisha ukazingatia vizuri Aya zinazoambatana na Aya ya Suleiman, na ukafikiria kwa ndani kauli yake Mwenyezi Mungu juu ya ufalme wa Suleiman na madhumuni yake, utajua kwamba maana ya Aya tukufu ni kwamba Mayahudi wa Hijazi walikuwa wak-imfanyia Mtume wa Kiarabu vitimbi na propaganda kwa kufuata nyayo za mab-abu zao ambao waliwasaidia wajumbe wa Babilon katika kuvunja ufalme wa Suleiman.

UFAFANUZI

Tutafasiri Aya kwa misingi ya alivyofahamu Ubaydiy.Wakafuata. Yaani walifuata Mayahudi wa Madina waliokuwa zama za Mtume Muhammad(s.a.w.w) .Yale yaliyofuatwa na mashetani: Makusudio ya mashetani ni wadanganyifu; miongoni mwao ni wale watu wawili wa Babilon ambao walijionyesha kuwa ni watakatifu kumbe ni maibilisi.

Katika ufalme wa Suleiman. Yaani Mayahudi wa Madina walitumia dhidi ya Muhammad, sawa na vile walivyokuwa mababu zao Mayahudi dhidi ya ufalme wa Suleiman.Suleiman hakukufuru, bali mashetani ndio waliokufuru. Yaani kila walilomnasibishia Suleiman alikuwa yuko mbali nalo ulikuwa ni udanganyifu na uzushi wao.Wakiwafundisha watu uchawi: Yaani wanawafundisha watu mambo ya ubatilifu.Na yaliyoteremshwa kwa Malaika wawili . Yaani watu wawili wa Babilon waliodhihirisha utakatifu na ucha Mungu. Mak-usudio sio kuteremshiwa Wahyi wa Mitume, bali ni kiasi cha kupewa ilham na kufundishwa.Wala hawakumfundisha, yoyote mpaka wamwambie: Sisi ni fitna (mtihani) basi usikufuru Walikuwa wakisema hayo kwa unafiki ili wawapumbaze watu kwamba elimu zao ni za kutoka kwa Mungu na kwamba wao ni watakatifu, wasafi wa nia; sawa na anavyosema mlaghai kumwambia yule anayemfundisha kuandika chuki na mapenzi: Tahadhari kuandika hivi usije ukawafarikisha waliooana kisheria, au kumfanya mke wa mtu kumpenda asiyekuwa mumewe.Wakajifunza kwao mambo ambayo kwayo waliweza kumfarikisha mtu na mkewe.

Yaani yale wanayofikiria kuwa yanaweza kutenganisha mtu na mkewe kama wanav-yochukua watu kutoka kwa walaghai, maandishi ya mapenzi na chuki. Kwa ujumla ni kwamba Aya haifahamishi kuthibiti athari ya uchawi wala kukanusha. Kwa sababu kauli yake Mwenyezi Mungu:Wakijifunza kwao ambayo waliweza, sio hukumu ya uhakika ya kutenganisha mtu na mkewe: Sawa na kusema kunywa kiponyesho, yaani kilichowekwa kwa ajili ya uponyeshaji. Kwa ufupi ni kwamba: Aya haithibitishi wala haikanushi. Mara nyingi hekima ya kiungu hupitisha kubainisha kwa upande fulani na kwa ujumla kwa upande mwingine; hasa katika masuala yasiyo ya kiitikadi. Wala hawakuwa wenye kumdhuru yoyote kwa hayo ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Yaani hawawezi kumdhuru yoyote vyovyote iwavyo kwa sababu ya kusoma na kuandika; kama akidhurika basi ni kutokana na sadfa tu, kwamba mtu amedhurika na sababu nyingine ya nje ikaonekana ni sababu hii. Makusudio ya idhini ya Mwenyezi Mungu ni sababu ya nje iliyodhuru.Na wanajifunza yatakayo wadhuru wala hayawanufaishi. Ni kiini macho tu, na kiini macho hudhuru wala hakinufaishi. Na kwa hakika wanajua kwamba aliyenunua haya hatakuwa na sehemu yoyote katika akhera.

Wanajua wao kwamba mwenye kupendelea ulaghai hana fungu mbele za Mwenyezi Mungu.Na bila shaka ni kibaya kabisa walichouzia nafsi zao. Yaani wamebadilisha kitu cha thamani kwa kitu duni.Imepita tafsiri yake katika Aya ya 61 ya sura hii.

﴿ وَلَوْ أَنَّهُمْ آمَنُوا وَاتَّقَوْا لَمَثُوبَةٌ مِّنْ عِندِ اللَّـهِ خَيْرٌ لَّوْ كَانُوا يَعْلَمُونَ ﴾

103.Na lau wangeamini na kuogopa, basi thawabu zitokazo kwa Mwenyezi Mungu zingekuwa bora kwao, laiti wangelijua.

LAU WANGEAMINI

Aya 103

MAELEZO

Baada ya Mwenyezi Mungu kuyaorodhesha maasi ya Mayahudi na kampeni zao mbaya dhidi ya Muhammad(s.a.w.w) , amesema kuwa ukafiri wao huu na upinzani wao hautawafaa kitu. Lau wangelimwamini Muhammad, kama ilivyowaamrisha Tawrat yao, wangelistarehe na kupata daraja ya juu kwa Mwenyezi Mungu.

Amirul Mumini anasema:Hakika kumcha Mungu ni ngome yenye nguvu na uovu ni ngome dhalili, haiwakingi watu wake wala haimhifadhi mwenye kuikimbilia. Fahamuni kuwa kumcha Mungu (takuwa) kunavunja uti wa mgongo wa makosa na hupatikana malengo kwa yakini.

UCHAWI NA HUKUMU YAKE

Mafaqihi wa Kishia wamezungumzia sana kuhusu uchawi, na wamerefusha maneno katika kuelezea maana yake, mafungu yake, yanayowezekana na yasiyowezekana. Pia wamezungumzia kuhusu kufundisha, kujifundisha na kuutumia. Uchawi uliozungumziwa na Quran ni namna fulani ya udanganyifu na hadaa, kwa kuufanya uwongo uwe haki. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ فَإِذَا حِبَالُهُمْ وَعِصِيُّهُمْ يُخَيَّلُ إِلَيْهِ مِن سِحْرِهِمْ أَنَّهَا تَسْعَىٰ ﴾

...Tahamaki kamba zao na fimbo zao zikaonekana mbele yake (Musa) zinakwenda mbio kwa uchawi wao. (20:66)

﴿ وَمَا هُم بِضَارِّينَ بِهِ مِنْ أَحَدٍ إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ ﴾

...Hawakuwa wenye kumdhuru yeyote kwa hayo ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu (2:102)

Imam Sadiq(a.s) amesema kwamba:uchawi uko namna nyingi; kama vile wepesi na haraka na kufanya hila, kwa sababu wenye hila wamegeuza uzima kuwa ugonjwa na maana kuwa hila.

Ama mambo ya kuandika, kuzungua na kutumia azima au kutabana na mengineyo ambayo yamesemekana kuwa yana athari, kama kufungwa mume wakati wa ndoa kiasi cha kushindwa kumwingilia mke. Vile vile mambo ya kuzidisha mapenzi, kutia chuki kati ya watu wawili na kuwatumia malaika na mashetani katika kupiga ramli na kutopoa, yote hayo, Shahidi wa pili ameyazungumzia katika Masalik mlango wa biashara akisema kuwa: Wanavyuoni wengi wa Kishia wanaitakidi kwamba ni mambo ya kuwazia na dhana zisizokuwa na msingi wowote; na baadhi yao wanaona kuwa ni matukio ya kweli. Na yeye ni miongoni mwa wasemao kuwa ni hakika. Bukhari amepokea katika Sahih yake J-4, mlango wa kisa cha Iblis na Askari wake, kwamba Mtume alirogwa mpaka akawa anaonekana kama anafanya kitu na wala hakifanyi. Lakini hayo ameyakanusha mmoja wa Maimamu wa Kihanafi katika kitabu Ahkamul-Quran J-1; Uk.55 chapa ya mwaka 1347 A.H.

Vile vile Sheikh Muhammad Abduh amekanusha katika kufasiri Sura ya Falaq.Sisi tuko pamoja na wale wanaouona uchawi kuwa hauna msingi wowote. Imam Sadiq anasema: Uchawi ni wenye kushindwa kabisa kugeuza aliyoumba Mwenyezi Mungu... Lau mchawi angelikuwa na uwezo angelijizuwia asizeeke na pia angelijikiinga na maafa na magonjwa pia angelizuwia uzee, na ufukara. Na kwamba uchawi ni fitina inayotenganisha watu wanaopendana na kuleta uadui kwa wanaosikilizana.Vyovyote iwavyo, wameafikiana mafaqihi wa Kishia kwamba adhabu ya mchawi ni kuuliwa akiwa ni Mwislamu. Akiwa si Mwislamu ni kutiwa adabu ya viboko na jela, kama atakavyoona hakimu.

*27 Mwenye kutaka ufafanuzi kuhusu uchawi na hukum yake asome kitabu Al-Jawahir mlango wa Biashara na mlango wa kisasi. Vile vile kwenye kitabu Makasib cha Sheikh Ansari. Mwenye Jawahir anasema : sio kila Jambo geni ni uchawi, kwani elimu nyingi zina athari za ajabu; kama vile wanavyofanya wazungu wakati huu. Hivi sasa ni mwaka 1967; miaka 121 imepita tangu alipokufa mwandishi huyu mkuu. Lau angelikuwako wakati huu asingeliona ajabu. Kwa sababu kila la ajabu hivi sasa litakuwa ni la kawaida wakati ujao.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَقُولُوا رَاعِنَا وَقُولُوا انظُرْنَا وَاسْمَعُوا وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ أَلِيمٌ﴾

104.Enyi mlioamini msiseme Raaina bali semeni Undhurnaa na sikilizeni; na makafiri wana adhabu iumizayo.

﴿مَّا يَوَدُّ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ وَلَا الْمُشْرِكِينَ أَن يُنَزَّلَ عَلَيْكُم مِّنْ خَيْرٍ مِّن رَّبِّكُمْ وَاللَّـهُ يَخْتَصُّ بِرَحْمَتِهِ مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ ذُو الْفَضْلِ الْعَظِيمِ﴾

105.Hawapendi waliokufuru miongoni mwa watu wa kitabu wala washirikina mteremshiwe heri kutoka kwa Mola wenu. Na Mwenyezi Mungu humhusisha kwa rehema zake amtakaye; na Mwenyezi Mungu ni mwenye fadhila kubwa.

ENYI MLIOAMINI

Aya 104 - 105

MAELEZO

Enyi mlioamini msiseme Raaina bali semeni Undhurna Mwenye Majmaul-Bayan anasema: Waislamu walikuwa wakisema Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Raina; Yaani tusikilize. Mayahudi nao wakalitumia neno hili kwa maana ya mpumbavu (katika lugha yao). Walipolaumiwa, wakasema tunasema kama wasemavyo Waislamu. Ndipo Mwenyezi Mungu akawaka-taza hilo kwa kauli yake: Msiseme Raina na semeni: Undhurna. Makusudio ya Undhurna katika Aya ni kuangalia Mtume hali yao wakati anapozungumza; angoje ili wafahamu na waelewe maneno yote.

Uzindushi Mwito wa kwanza katika Sura ya Baqara umekuja kwa watu wote na mwito wenyewe ni Uislamu na kumwabudu Mwenyezi Mungu; pale aliposema Mwenyezi Mungu (s.w.t.) katika Aya ya 21:Enyi watu mwabuduni Mola wenu ambaye amewaumba... Mwito wa pili ulikuwa kwa wana Israil, taifa kubwa ambalo lilileta taifa la Kikristo. Mwito huu wa pili ulikuja kukumbusha kuondolewa mateso kwa waana wa Israil na kupatiwa neema; ni pale aliposema Mwenyezi Mungu katika Aya 40:Enyi wana wa Israil kumbukeni neema yangu niliyowaneemesha.... Mwito wa tatu umekuja kwa umma wa Muhammad(s.a.w.w) katika Aya hii:Enyi mlioamini msiseme Raaina , ambayo ni kuwafundisha Waislamu adabu za sheria baada ya kusilimu na kumwamini Mwenyezi Mungu. Utaratibu huu wa miito hii mitatu ndio utaratibu wa kikawaida; yaani kuanza kuwalingania watu kwenye imani ya Mwenyezi Mungu, kisha kumtajia fadhila za Mwenyezi Mungu yule mwenye kumwamini Mungu kabla ya Utume tena kumfunza kuamini adabu za Mwenyezi Mungu yule mwenye kuamini Utume. Hii ni namna mojawapo ya ufasaha wa Quran.Hawapendi waliokufuru miongoni mwa watu wa kitabu wala washirikina mteremshiwe heri kutoka kwa Mola wenu.

Si ajabu kwa washirikina, Wayahudi na wakristo pamoja na makafiri, kuchukia yote aliyoteremshiwa Muhammad na vile alivyohusishwa na Mwenyezi Mungu kwa fadhila na hidaya na utengeneo; isipokuwa ajabu ni kutolichukia hilo.Na Mwenyezi Mungu humhusisha kwa rehema Zake amtakaye . Amirul Muminin anasema:Makusudio ya rehema hapa ni Utume .

HUSUDA NA HASIDI

Husuda ni tabia za watu wengi, isipokuwa wale waliohifadhiwa na Mwenyezi Mungu, na wala haiko kwa washirikina, Mayahudi au Manaswara peke yao, bali iko pia kwa Waislamu wengi; hata kwa wanavyuoni wakubwa na baadhi ya wale wenye vyeo vya kuwa Marja (Mufti mkubwa) wa kidini ingawaje cheo hicho ndicho pekee kinachokurubiana na cheo cha maasum. Mwenyezi Mungu, Mitume Maimamu na wenye hekima, wamezungumzia sana kuhusu hasadi. Miongoni mwa hayo ni kauli ya Imam Jafar Sadiq: Hasadi asili yake ni upofu wa moyo na kukana fadhila za Mwenyezi Mungu, na hayo yote mawili ni mbawa za kufuru. Lugha fasaha zaidi niliyoiona katika kuisifu hasadi ni kauli ya bwana wa mafasaha na kiongozi wa wenye hekima, Amirul Muminin(a.s) alipowaeleza kuwa ni mahasidi wa raha na wenye kutilia mkazo balaa. Akasema tena: Inatosha kuwa ni shari kwa mahasidi kuhuzunika wakati unapofurahi. Huenda itakuwa ni vizuri kunakili mfano huu kutoka kwa mwanahekima mmoja aliyesema: Mfano wa hasidi ni kama mtu anayetupa jiwe kwa adui yake, kisha jiwe limrudie mwenyewe upande wa kuume na apandwe na hasira. Mara ya pili tena analitupa kwa nguvu kuliko kwanza, na limrudie upande wa kushoto na hapo ataingiwa na chuki na kisha alitupe jiwe kwa nguvu zote na hamasa halafu limrudie kichwani na limjeruhi na huku adui yake yuko salama.

Ni muhali kwa hasidi kuweza kutubu husuda yake, kwa sababu hasidi ni sawa na mwoga na bakhili. Atawezaje bakhili na mwoga kutubu? Ndio maana Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume kuwaambia mahasidi

﴿قُلْ مُوتُوا بِغَيْظِكُمْ﴾

....Sema; kufeni na ghadhabu zenu. (3:119).

﴿مَا نَنسَخْ مِنْ آيَةٍ أَوْ نُنسِهَا نَأْتِ بِخَيْرٍ مِّنْهَا أَوْ مِثْلِهَا أَلَمْ تَعْلَمْ أَنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴾

106.Aya yoyote tunayoifuta au kuisahaulisha tunaleta iliyo bora kuliko hiyo au iliyo mfano wake. Hujui kwamba Mwenyezi Mungu ni muweza wa kila kitu?

﴿أَلَمْ تَعْلَمْ أَنَّ اللَّـهَ لَهُ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا لَكُم مِّن دُونِ اللَّـهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا نَصِيرٍ ﴾

107. Hujui kwamba Mwenyezi Mungu ni mfalme wa mbingu na ardhi? Nanyi hamna mlinzi wala msaidizi asiyekuwa Mwenyezi Mungu.

AYA YOYOTE TUNAYOIFUTA

Aya 106 - 107

KUFUTA

Kwanza tutaeleza maana ya kufuta kwa ujumla katika hukumu za sheria, kisha maana ya kufuta katika Quran.

Maana ya kufuta katika hukumu ya sheria ni kuja dalili inayofahamisha kuthibiti hukumu ya sheria kwa kudumu na kuendelea muda wote; baada ya kutumika hukumu hiyo kwa muda fulani, inakuja dalili nyingine ya kuthibitisha kwamba hukumu ile ilihusika na kipindi fulani tu; na kwamba masilahi yanahukumilia kutumika katika wakati fulani tu, sio kila wakati. Lakini hekima ya Mwenyezi Mungu ilidhihirisha kudumu na kuendelea. Sawa na Daktari ambaye anaona masilahi ya mgonjwa ni kutokula nyama kwa muda wa wiki moja tu, lakini akaona ni vizuri amfiche ule muda wa kumka-taza.Baada ya kupita wiki moja akamruhusu kula nyama. Kwa hivyo kufuta kunakuwa kwa maana ya kufuta yale yaliyoonekana kuwa ni ya kudumu na wala sio kuwa ni kwa sababu ya kutojua au kubadili mawazo.

Hakuna mwenye kutia shaka kwamba kufuta kwa maana haya kumethibiti katika sheria ya Kiislamu; kwani sheria imefuta baadhi ya hukumu zake zilizotangulia; kama vile sharia za Musa na Isa. Bali hukumu za Quran zenyewe zinafutana; kama vile kugeuza Qibla kuwa Al-Kaaba (huko Makka) baada ya kuwa Baytul-Maqdis (huko Jerusalem).

Ama kufuta katika Quran kunawezekana kukugawanywa katika njia tatu: 1. Kufuta Aya kisomo na hukumu, yaani kuondolewa tamko lake na hukumu yake.

2. Kufutwa kisomo tu; kufutwa tamko na kubaki hukumu.

3. Kufutwa hukumu tu, si kusomwa, yaani inasomwa lakini haichukuliwi dhahiri yake baada ya kutumiwa wakati fulani. Lakini fungu la kwanza na la pili hayapo, kwa sababu yataleta upungufu na mageuzi katika Quran ambayo haifikiwi na batili mbele yake wala nyuma yake.

Ama fungu la tatu linawezekana na limethibiti; ndilo walilolikubali Waislamu wote na wafasiri wote, na limetungiwa vitabu mahsusi. Hivi sasa kimetolewa kitabu kikubwa kwa jina Annasikh wal-mansukh (Inavyofuta na inayofutwa) cha Dkt. Mustafa Zaydi wa Misri. Kwa ujumla inaonyesha kuwa hukumu ya sharia ikithibiti kwa njia sahihi haiwezekani kufutwa isipokuwa kwa Aya ya Quran au kwa Hadith mutawatir. Kwa sababu kufuta ni jambo kubwa na la muhimu. Kwa hivyo kufuta hakuwezi kuthibiti kwa habari moja. Kwa sababu kila umuhimu hauna budi kuenea na kutangaa midomoni. Mtu mmoja tu akinakili tukio kubwa au watu wengi, lakini bila ya kuenea, itakuwa ni uwongo. Kwani huoni kifo cha mtu mashuhuri kinanukuliwa na watu wengi! Vile vile mapinduzi! Lakini kifo cha mtu wa kawaida hunukuliwa na baadhi ya majirani na ndugu tu! Ufafanuzi zaidi uko katika Usulul-fiqh (elimu ya misingi ya Fiqh)

MAANA

Aya yoyote tunayoifuta au kuisahauliza, tunaleta iliyo bora kuliko hiyo au iliyo mfano wake.Wafasiri wengi wanasema kwamba Mayahudi walikuwa wakisema kuwa: Muhammad anawaamrisha masahaba zake jambo kisha anawakataza, leo anasema hili kesho anasema lile, lau anayoyasema kama yangelikuwa ni wahyi, kusingelitokea mgongano huu. Ndipo ikashuka Aya hii, kuwajibu.Makusudio ya Aya, ni Aya za Quran tukufu, kwani maana haya ndiyo yanayokuja haraka kwenye fahamu. Amenakili Sheikh Maraghi katika tafsir yake kutoka kwa mwalimu wake, Sheikh Muhammad Abduh, kwam- ba makusudio ya Aya ni muujiza unaofahamisha utume wa Mtume; kwamba Mwenyezi Mungu anampa Mtume muujiza wa Mtume mwingine, kisha anauacha na kuumpa Mtume mwingine muujiza mwingine. Maana haya yenyewe yako sawa, lakini mpangilio wa Aya unayakataa. Maana yanayoelezwa na wanavyuoni na kundi kubwa la wafasiri ni Aya za Quran.

Maana ya kufuta Aya ya Quran ni kubakia tamko na kisomo pamoja na kuacha hukumu iliyofahamishwa na Aya hiyo ambayo iliwahi kutumika wakati fulani. Ama maana ya neno Nunsiha likisomwa bila ya harufi Hamza litakuwa lina maana ya kusahau; yaaani kuacha sio kwa kughafilika nayo yani twaiacha kama ilivyo bila ya mabadiliko. Kwani yafaa kusema kitu hiki nimekisahau kwa maana ya kukiacha kama kilivyo. Na likisomwa kwa Hamza, litakuwa na maana ya kuchelewesha na kuahirisha yaani tunaacha kuiteremsha mpaka wakati mwingine.

Vyovyote iwavyo kupatikana herufi Ma ya sharti haifahamishi kutokea kufutwa hasa,bali inafahamisha kuwa lau inatokea, basi Mwenyezi Mungu angelileta bora kuliko ile iliyofutwa. Hujui kwamba Mwenyezi Mungu ni muweza wa kila kitu, hujui kwamba Mungu ni wake ufalme wa mbingu na ardhi? Inasemekana kwamba msemo hujui unaelekezwa kwa Mtume na makusudio yake ni Waislamu ambao walidhikika kutokana na upinzani wa Mayahudi na wengineo kuhusu kufutwa. Ilivyo hasa ni kwamba msemo unaelekezwa kwa kila anayeona ajabu kufutwa au yule anayeumizwa na upinzani. Maana yake ni kuwa kufutwa sio jambo geni.

Kimsingi ni kwamba Mwenyezi Mungu anamiliki kila kitu na anapanga na kupitisha anavyotaka, iwe ni kufuta au kubakisha bila ya kufutwa. Ama kuhusisha kutaja mbingu na ardhi kunafahamisha kukusanya vitu vyote. Kwa sababu mbingu na ardhi zinakusanya viumbe vyote vya juu na vya chini.Nanyi hamna mlinzi wala msaidizi asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Yaani msijali enyi waumini kwa anayepinga suala la kufutwa au kitu chochote katika dini yenu; kiumbe hawezi kuwadhuru maadamu Mwenyezi Mungu ndiye anayetia nguvu na ndiye msaidizi.

Kwa ufupi ni kwamba kufuta ni haki, hakuna kizuwizi cha kutoka akilini au kwenye sharia, kinyume na wanavyofikiri wakanushaji na wapinzani! Tafsir Al-Kashif: Juzuu ya Kwanza Sura Al-Baqara 187