TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
Kundi:

Matembeleo: 35748
Pakua: 3050


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Juzuu 9 Juzuu 10 Juzuu 11
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 20 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 35748 / Pakua: 3050
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

Mwandishi:
Swahili

18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NG’OMBE)

﴿وَإِذْ جَعَلْنَا الْبَيْتَ مَثَابَةً لِّلنَّاسِ وَأَمْنًا وَاتَّخِذُوا مِن مَّقَامِ إِبْرَاهِيمَ مُصَلًّى وَعَهِدْنَا إِلَىٰ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ أَن طَهِّرَا بَيْتِيَ لِلطَّائِفِينَ وَالْعَاكِفِينَ وَالرُّكَّعِ السُّجُودِ ﴾

125.Na tulipoifanya ile nyumba (Al-Kaaba) iwe mahali pa kuendewa na watu na mahali pa amani. Na pafanyeni alipokuwa akisimama (Maqamu) Ibrahim ni mahali pa kuswalia. Na tuliagana na Ibrahim na Ismail kuwa: Itakaseni nyumba yangu kwa ajili ya wale wenye kutufu na wenye kujitenga huko kwa ibada na wanaorukuu na kusujudu.

﴿وَإِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ رَبِّ اجْعَلْ هَـٰذَا بَلَدًا آمِنًا وَارْزُقْ أَهْلَهُ مِنَ الثَّمَرَاتِ مَنْ آمَنَ مِنْهُم بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ قَالَ وَمَن كَفَرَ فَأُمَتِّعُهُ قَلِيلًا ثُمَّ أَضْطَرُّهُ إِلَىٰ عَذَابِ النَّارِ وَبِئْسَ الْمَصِيرُ﴾

126.Na aliposema Ibrahim: Ewe mola wangu! Ufanye mji huu uwe wa amani na uwaruzuku wakazi wake matunda, wale wanaomwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho katika wao. Akasema Mwenyezi Mungu: Na mwenye kukufuru nitamstarehesha kidogo; kisha nitamsukumiza katika adhabu ya moto napo ni mahali pabaya kabisa pa kurejea.

NA TULIPOIFANYA ILE NYUMBA IWE MAHALI PA KUENDEWA

Aya 125-126

LUGHA

Nyumba: ni nyumba yoyote, lakini ikisemwa nyumba tu, basi itakuwa ni Al- Kaaba, kutokana na kutumika sana hivyo.

MAANA

Na tulipoifanya ile nyumba (Al-Kaaba) iwe mahali pa kuendewa na watu na mahali pa amani. Aya hii inaungana na Aya iliyotangulia (alipomfanyia mtihani Ibrahim). Maana yake ni kwamba Mwenyezi Mungu ameijaalia nyumba yake ni mahali pa kuendewa na watu makundi kwa makundi kwa ajili ya kutekeleza ibada na baadaye warudi makwao; kisha yaje makundi mengine, n.k. Vile vile ameifanya ni mahali pa kupata amani katika akhera. Kwa sababu mtu anapoifikia nyumba hiyo na akatekeleza ibada anajirudi na kutubia. Kwa hiyo nyumba ya Al-Kaaba inakuwa ni nyenzo ya kujitakasa na adhabu na mateso. Kama vile ambavyo ameifanya ni mahali pa amani katika dunia. Kwa sababu mtu mwenye kwenda mahali hapo anakuwa salama wala haingiliwi na yeyote kwa ubaya. Mtu anaweza kumwona mtu aliyemuua baba yake katika Haram (eneo la Al-kaaba) lakini akajitia hamnazo! Desturi hii imerithiwa tangu wakati wa Ismail(a.s) mpaka leo.

MKOSAJI KUKIMBILIA HARAM

Katika kitabu cha Al-Jawahir ambacho ni tegemeo kubwa la Fiqh ya Shia Jafariyyah kuna maelezo haya, ninamnukuu: Yeyote aliyekimbilia haram hapigwi haddi kwa kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.).

﴿وَمَن دَخَلَهُ كَانَ آمِنًا﴾

Na mwenye kuingia humo huwa katika amani (3:97)

Bali atapunguziwa chakula na atapewa kidogo tu kiasi cha kuzuwia tumbo ili atoke akapigwe haddi nje. Imepokewa riwaya sahihi kutoka kwa Imam Jafar Sadiq(a.s) kuhusu mtu ambaye amefanya jinai mahali pengine pasipokuwa Haram kisha akakimbilia kwenye Haram. Akasema Imam:

Hatapigwa haddi, lakini hatalishwa, hatapewa maji wala hatasamehewa, kwani akifanyiwa hivyo, kuna uwezekano wa kutoka nje ya Haram na apigwe haddi. Kama akifanya jinai ndani ya Haram atapigwa haddi ndani ya Haram, kwa sababu hakuihishimu Haram . Abu Hanifa amesema: Haifai kumwua aliyekimbilia kwenye Haram ametoa dalili kwa kauli ya Mwenyezi Mungu: Na tulipoifanya ile nyumba (Al- Kaaba) iwe mahali pa kuendewa na watu na mahali pa amani. Na pafanyeni alipokuwa akisimama Ibrahim ni mahali pa kuswali. Hiyo ni amri ya kuswali (Maqamu Ibrahim) mahali aliposimama Ibrahim.Mafaqihi wamekubaliana kuwa inatakikana kuswali hapo rakaa mbili za Tawaf ikiwezekana. Maana ya (Maqam Ibrahim) mahali aliposimama Ibrahim ni pale mahali maarufu ndani ya msikiti. Ama mwenye kusema kwamba makusudio yake ni msikiti wote, basi na atoe dalili ya kuthibitisha kauli yake hiyo.

Na tuliagana na Ibrahim na Ismaili kuwa itakaseni nyumba yangu kwa ajili ya wale wenye kutufu na wenye kujitenga kwa ibada na wanaorukuu na kusujudu. Maana yake, tulimwagiza Ibrahim na Ismaili kuiheshimu Al-Kaaba na kuiepusha na kila lisiloelekeana nayo; kama vile masanamu, najisi, upuuzi, uovu, majadiliano n.k. Na wawaamrishe watu hilo Wanye kutufu ni wale wanaoizunguka, wanaojitenga kwa ibada ni wanaokaa humo msikitini au wanaokaa karibu kwa ibada, na wanaorukuu na kusujudu, yaani wanaoswali. Na aliposema Ibrahim Ewe Mola wangu! Ufanye mji huu uwe wa amani. Hii ni dua na matamanio kutoka kwa Ibrahim kwa Mwenyezi Mungu kuijaalia Makka tukufu kuwa ni mji wa amani, yaani watu wake wasiwe na vita, mitetemeko, vimbunga n.k. Kuna kikundi cha wafasiri wamesema kwamba Mwenyezi Mungu ameiitikia dua ya Ibrahim, ambapo hakuna yeyote anayeikusudia Makka kwa uovu ila Mwenyezi Mungu humwangamiza, na mwenye kuikusudia kwa uadui basi uadui wake hauchukui muda mrefu. Na uwape wakazi wake matunda wale wanaomwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho. Ibrahim alipomaliza kujenga nyumba hiyo katika ardhi kame isiyokuwa na maji wala mmea wowote, alimwomba Mwenyezi Mungu s.w.t. aipe amani ardhi hii na iwe na rizki, wala hakuainisha aina ya riziki wala kule itakapotoka isipokuwa umuhimu ni kufikiwa na riziki vyoyote itakavyokuwa na popote itakapotoka. Mwenyezi Mungu Mtukufu aliitikia maombi ya Ibrahim. Ikawa riziki ya namna namna inakuja Makka kutoka sehemu mbali mbali; ikawa Makka ni kituo cha wasafiri na cha biashara. Katika hali hii ndipo Mwenyezi Mungu akasema katika Aya hii:

﴿أَوَلَمْ نُمَكِّن لَّهُمْ حَرَمًا آمِنًا يُجْبَىٰ إِلَيْهِ ثَمَرَاتُ كُلِّ شَيْءٍ﴾

Je hatukuwakalisha mahali patakatifu na pa amani yanakoletwa matunda ya kila aina. (28:57)

Ibrahimu aliwahusisha waumini tu katika kutaka riziki, kwa sababu Mwenyezi Mungu alikwisha mfahamisha kwamba katika kizazi chake kutakuwa watu madhalimu na Mwenyezi Mungu hakuuhaidi Uimamu kwa madhalimu. Akasema (Mwenyezi Mungu s.w.t.):Na mwenye kukufuru nitamstarehesha kidogo . Yaani Mwenyezi Mungu alimwambia Ibrahim: Mimi vile vile ninawaruzuku makafiri na hata mafasiki. Kwa sababu riziki ni kitu kingine na Uimamu ni kitu kingine, kwani Uimamu ni uongozi wa kidini na wa wakati, nao unahitajia imani, uadilifu na Isma. Ama riziki inakuwa kwa mwema na mwovu; kama vile maji na hewa. Madhambi na maasi hayana dhara yoyote katika umri na riziki katika maisha haya, isipokuwa athari yake itadhirhirika kesho siku ya kiyama ambapo watu watapata malipo yao.

﴿وَإِذْ يَرْفَعُ إِبْرَاهِيمُ الْقَوَاعِدَ مِنَ الْبَيْتِ وَإِسْمَاعِيلُ رَبَّنَا تَقَبَّلْ مِنَّا إِنَّكَ أَنتَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴾

127.Na Ibrahim alipoinua misingi ya ile Nyumba (Al-Kaaba) na Ismail (wakaomba): Ewe mola wetu! Tutakabalie;hakika wewe ndiye Msikizi Mjuzi.

﴿رَبَّنَا وَاجْعَلْنَا مُسْلِمَيْنِ لَكَ وَمِن ذُرِّيَّتِنَا أُمَّةً مُّسْلِمَةً لَّكَ وَأَرِنَا مَنَاسِكَنَا وَتُبْ عَلَيْنَا إِنَّكَ أَنتَ التَّوَّابُ الرَّحِيمُ ﴾

128.Ewe mola wetu! Utufanye tuwe ni wenye kusilimu kwako.Na miongoni mwa kizazi chetu pia ufanye umma uliosilimu kwako. Na utuonyeshe ibada zetu na utukubalie toba.Hakika wewe ndiye mwenye kukubali toba mwenye kurehemu.

﴿رَبَّنَا وَابْعَثْ فِيهِمْ رَسُولًا مِّنْهُمْ يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِكَ وَيُعَلِّمُهُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَيُزَكِّيهِمْ إِنَّكَ أَنتَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ﴾

129.Ewe mola wetu! Wapelekee mtume anayetokana na wao, awasomee Aya zako, na kuwafundisha Kitabu na hikima na awatakase.Hakika wewe ndiye mwenye nguvu mwenye hekima.

NAALIPOINUA IBRAHIM MISINGI YA ILE NYUMBA

Aya ya 127 - 129

HISTORIA YAAL-KAABA

Wafasiri na wanahistoria wametofautiana katika historia ya Al-Kaaba, kwamba je, ilikuako kabla ya Ibrahim, kisha ikaharibika ndipo akaijenga upya yeye na mwanawe Ismail kwa amri ya Mwenyezi Mungu mtukufu; au yeye (Ibrahim) ndiye aliyeanza kuijenga? Wafasiri wengi na wanahistoria wa Kiislamu wamesema kuwa ilikuwako kabla ya Ibrahim kwa miaka mingi. Baadhi wamesema ilianzishwa na Ibrahim(a.s) ; wengine wamenyamaza na kusema: Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi. Nasi tuko pamoja na hawa. Kwani akili haina nafasi hapa, na njia ya kujua itategemea athari au Aya za Quran au Hadith mkato. Na mimi sikupata kauli yoyote ya watafiti wa athari na uvumbuzi, na Quran haikuelezea waziwazi historia ya Al-Kaaba, bali inaelezea tu kwamba Ibrahim na mwanawe Ismail waliijenga na kusaidiana.Na hii haifahamishi kuwa ilikuwako au haikuako kabla ya Ibrahim.Na Hadithi mkato hakuna isipokuwa Hadithi Ahad (pwekesho). 34 Na Hadithi pwekesho ni hoja katika hukumu ya sheria tu. 35 Kwa vyovyote iwavyo sisi hatutaulizwa na Mwenyezi Mungu mtukufu wala hatuna wajibu wa kuijua historia ya kujengwa Al-Kaaba au kujua wakati ilipoanzishwa.

* 33 Hadithi iliyokubaliwa na wote katika maana na matamshi.

* 34 Hadith ambayo silsila (mfuatano) ya upokezi wake imekatika au Hadith ambayo haikubaliwi na wengi.

* 35 La Kushangaza zaidi ya niliyoyasoma kuhusu maudhui haya ni kauli ya Sayyid Tabatabai katika Tafsir Al-Mizan J1 Uk 196 Kukosekana kusihi mapokezi ya hadith hakuwajibishi kuitupa Hadith hiyo maadamu haihalifu akili au Hadith sahihi Inajulikana wazi kwamba kutohalifu akili na Hadithi thabiti ni sharti la yasiyothibiti, kwa sababu kutothibitika kusihi mapokezi kunatosha kuitupa Hadithi bila ya kuongeza sharti jengine; kama si hivyo basi itabidi kuitumia kila Hadithi isiyokuwa sahihi mpaka itakapohalifu akili au hadithi thabiti. Vile vile hatuna taklifa ya kujua kwamba hiyo ni sehemu ya pepo au ni ya ardhi na kwamba je, Adam na Mitume baada yake walihiji au la! Au kwamba hiyo Al-Kaaba ilipandishwa mbinguni wakati wa Tufani kisha ikateremshwa ardhini.? Pia hatuna taklifa ya kujua kwamba Hajarul-Aswad (jiwe jeusi) lililetwa na Jibril kutoka mbinguni au lilikuja pamoja na Adam kutoka peponi au lilibanduka kutoka Jabal Abu Qubays na kwamba je lilikua jeusi kwa sababu ya kuguswa na wenye dhambi. Na mengineyo ambayo hayana mapokezi yoyote isipokua Hadithi Ahad au visa visivyokuwa na ukweli.

Sisi hatutaulizwa vitu vyote hivyo wala hatuna taklifu yoyote ya kujua si kwa njia ya wajibu, wala sunna; si kiakili wala kisheria.Wala hakuna faida yoyote ya kidini au dunia katika kuifanyia utafiti. Utafiti huu ulikuako kisha ukaenda na upepo; na yeyote anayetaka kuufufua, ni sawa na yule anaejaribu kurudisha nyuma mishale ya saa. Kitu ambacho tutaulizwa na kutakiwa kukifanya kuhusu Al-Kaaba ni kuikusudia kwa ajili ya Hijja na Umra kwa anayeweza kuiendea. Na vile vile kuiheshimu na kuitukuza na kuihami kwa kufuata nyayo za Mtume(s.a.w.w) Ahlul Bait wake(s.a.w.w), masahaba, wafuasi, wanachuoni na Waislamu wote. kwani hao wanaamini bila ya tashwishi yoyote kwamba kuiadhimisha nyumba ya Mwenyeezi Mungu ni kumwadhimisha Mwenyezi Mungu, na kuihami ni kuihami dini ya Mwenyezi Mungu. Amirul Muminin amesema: Amewawajibisha Mwenyezi Mungu kuhiji nyumba yake tukufu ambayo ameifanya ni kibla cha viumbe,wanaingia kama wanavyoingia wanyama na wanaingia makundi makundi kama njiwa. Ameijaalia Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni alama ya kumnyenyekea yeye (Mungu) na kuukubali Utukufu Wake. Ameijaalia ni alama ya Waislamu, na nikinga ya wenye kutaka hifadhi.

Ewe mola wetu! Tutakabalie. Hii ni dua kutoka kwa Ibrahim na Ismail ya kutaka thawabu kutokana na amali hii, kwa sababu maana ya kutakabaliwa mbele ya Mwenyezi Mungu ni kupata thawabu kutokana na amali atakayoikubali, kama vile ambavyo kukosa thawabu kunamaanisha kukataliwa amali. Hakuna mwenye shaka kwamba Mwenyezi Mungu ameitakabali dua yao na amewalipa thawabu kutokana na twaa hii. Kwa sababu yeye ndiye aliyefungua mlango wa dua, na hawezi kumfungulia mja mlango wa dua, hasa mwenye kumcha Mwenyezi Mungu, kisha amfungie mlango wa kutakabaliwa, kama alivyosema Amirul Muminini. Ewe Mola wetu! Utufanye tuwe ni wenye kusilimu kwako. Makusudio ya kusilimu hapa ni kufanya ikhlas katika itikadi na amali (matendo). Hapana mwenye shaka kwamba mwema mwenye kusifiwa, ni yule anayemnyen-yekea Mwenyezi Mungu Mtukufu katika mambo yake yote.Na miongoni mwa kizazi chetu (pia ufanye) umma uliosilimu kwako. Ameikubali dua yao na akajaalia katika kizazi chao mamilioni na mamilioni ya waislamu.

SHIA NA MABABU WA MTUME

Shia wamehusika na kauli ya kuwa baba wa Muhammad, na mababu zake, mama yake na nyanya zake wote hawa-kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu chochote na kwamba Muhammad tangu alipoumbwa alikuwa akigura (akihama) katika migongo mitakatifu mpaka kwenye tumbo la mfuko wa uzazi mtakatifu na hadi ilipotimu saa ya kuzaliwa kwake. Sheikh wa Shia mwenye kujulikana kwa jina la Sheikh Al-Mufid amesema katika sherhe ya Aqaid Aswaduq chapa ya mwaka 1371 A.H. uk 67: Hakika mababa wa Mtume(s.a.w.w) kuanzia baba yake Adam, walikuwa ni watu walio na imani, na Mwenyezi Mungu amemwambia Mtume wake Muhammad: Na mageuko yako kati ya wale wanaosujudu. (26:219) Mtume(s.a.w.w) amesema: Niliendelea kugurishwa katika migongo mitakatifu kwenda kwenye matumbo matakatifu mpaka Mwenyezi Mungu akanidhihirisha (kwa kuzaliwa) katika ulimwengu wenu huu. Kwa hiyo kauli ya Mtume inafahamisha kwamba mababu zake wote walikuwa wenye imani. Kwani lau baadhi yao wangekuwa makafiri isingelistahiki kusifiwa na utwahara kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu:Hakika washirikina ni najisi. (9:28)

Mtume alipowasifu mababu zake kwa utakatifu imefahamisha kwamba wao walikuwa waumini Utukubalie toba Sio lazima kwa mwenye kutaka msamaha awe na dhambi hasa ikiwa mwenye kutaka ni Mtume au wasii.Kwa sababu watu watukufu hawa wanajiona hawajafikia kuitekeleza haki ya Mwenyezi Mungu sawa sawa kadiri watakavyojitahidi katika ibada ya Mwenyezi Mungu. Kwani wao ndio wanaojua zaidi utukufu wa Mwenyezi Mungu. Na kwamba ibada ya mtu, vyovyote itakavyokuwa haiwezi kutekeleza haki ya utukufu huo usiokuwa na mwanzo wala mwisho. Ewe, Mola wetu! Wapelekee Mtume anayetokana na wao Ombi hili alilikubali Mwenyezi Mungu kwa kuleta Mtume wa mwisho na bwana wa Mitume wote.

Zimekuja Hadith kwa upande wa Shia na Sunni kwamba Mtume amesema: Mimi ni ombi la Ibrahim na ni bishara ya Isa. katika Quran Mwenyezi Mungu amesema: Yeye ndiye aliyemuinua Mtume katika wasiojua kusoma atokaye miongoni mwao anawasomea Aya zake na kuwatakasa na kuwafunza kitabu na hekima.Na kabla ya hayo walikuwa katika upotofu ulio dhahiri. (62:2) Amirul Muminin Ali(a.s) amesema:Alimpeleka Mwenyezi Mungu Muhammad kuwa ni Mtume na hakuna yeyote katika waarabu aliyekuwa akisoma kitabu au kudai Utume wala wahyi.

BISHARA YA MAHDI MWENYE KUONGOJEWA

Kama walivyotoa Mitume bishara ya Muhammad,yeye naye alitoa bishara ya Mahdi kutoka katika kizazi chake. Mimi nimetunga kitabu juu ya suala hilo nilichokiita Al Mahdil Muntadhar Wal-aql (Mahdi mwenye kungojewa na akili) katika kitabu hicho nimenakili Hadith nyingi kutoka upande wa Shia na Sunni; na zimetoka nakala nyingi na kurudiwa na wachapishaji Daarul-malayin pamoja na kitabu Allahu wal-aql, Al-akhira wal-aql na Annubuwwat wal-aql. Vitabu hivyo vinne vimekusanywa kuwa kitabu kimoja kwa jina Al Islamu wal-aql (Uislamu na akili). Kitabu kilichokusanya zaidi kuhusu suala hili katika nilivyovisoma ni kitabu kinachoitwa Muntakhabul-athari fil - Imam thani ashar cha Sayyid Lutfillah Assafi kilichokuwa na kurasa zaidi ya 500, ambacho ni rejea bora zaidi. Baada ya kuchapishwa kitabu Al-Mahdil muntadhar wal-aql nilisoma maneno marefu ya Muhyiddin aliye mashhuri kwa jina la Ibnul Arabi, nanukuu sehemu ya maneno hayo. Mwenyezi Mungu anaye Khalifa atakayetoka ikiwa nchi imejaa dhulma na jeuri ili aijaze uadilifu... na khalifa huyo ni kutoka katika kizazi cha Mtume(s.a.w.w) kutoka katika kizazi cha Fatima(a.s) , jina lake linafanana na jina la babu yake, Mtume wa Mwenyezi Mungu ...Atafanyiwa baia kati ya rukni na maqam, anafanana na Mtume kwa umbo naye atakuwa na uso mwangavu mwenye pua ndefu... Atawaongoza watu kwa desturi ya Mtume(s.a.w.w) . Na babu yake alisema kumhusu yeye: Atafuata athari yangu bila kukosea na hiyo ndiyo Isma. Hayo yamo katika kitabu Futuhatil-Makkiyya kilichochapishwa na Darulkutubil- Arabiya uk 327 na kuendelea.

﴿وَمَن يَرْغَبُ عَن مِّلَّةِ إِبْرَاهِيمَ إِلَّا مَن سَفِهَ نَفْسَهُ وَلَقَدِ اصْطَفَيْنَاهُ فِي الدُّنْيَا وَإِنَّهُ فِي الْآخِرَةِ لَمِنَ الصَّالِحِينَ ﴾

130.Na ni nani atajitenga na mila ya Ibrahim isipokuwa anayeitia nafsi yake katika upumbavu? Na hakika sisi tulimtakasa (Ibrahim) katika dunia; na hakika yeye katika akhera atakuwa miongoni mwa watu wema.

﴿إِذْ قَالَ لَهُ رَبُّهُ أَسْلِمْ قَالَ أَسْلَمْتُ لِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴾

131.Mola wake alipomwambia silimu; akasema Nimesilimu kwa Mola wa walimwengu wote.

﴿وَوَصَّىٰ بِهَا إِبْرَاهِيمُ بَنِيهِ وَيَعْقُوبُ يَا بَنِيَّ إِنَّ اللَّـهَ اصْطَفَىٰ لَكُمُ الدِّينَ فَلَا تَمُوتُنَّ إِلَّا وَأَنتُم مُّسْلِمُونَ ﴾

132.Na Ibrahimu akawausia haya wanawe, na pia Yaqub: Enyi wanangu! Hakika Mwenyezi Mungu amewachagulia dini hii; basi msife ila nanyi mmekuwa Waislamu.

﴿أَمْ كُنتُمْ شُهَدَاءَ إِذْ حَضَرَ يَعْقُوبَ الْمَوْتُ إِذْ قَالَ لِبَنِيهِ مَا تَعْبُدُونَ مِن بَعْدِي قَالُوا نَعْبُدُ إِلَـٰهَكَ وَإِلَـٰهَ آبَائِكَ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا وَنَحْنُ لَهُ مُسْلِمُونَ ﴾

133.Je, mlikuwapo yalipomfikia Yakub mauti, alipowaambia wanawe: Je, mtaabudu nini baada yangu? Wakasema: Tutamwabudu Mola wako na Mola wa baba zako, Ibrahim na Ismail na Is-haka; Mungu mmoja tu, na sisi tunasilimu kwake.

﴿تِلْكَ أُمَّةٌ قَدْ خَلَتْ لَهَا مَا كَسَبَتْ وَلَكُم مَّا كَسَبْتُمْ وَلَا تُسْأَلُونَ عَمَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴾

134.Huo ni umma uliokwisha pita.Utapata Uliyoyachuma nanyi mtapata mtakayoyachuma; wala hamtaulizwa waliyokuwa wakiyafanya.

NA NI NANI ATAJITENGA NA MILA YA IBRAHIM

Aya ya 130 - 134

MAANA

Na ni nani atajitenga na mila ya Ibrahim isipokuwa anayeitia nafsi yake katika upumbavu? Haya ni matahayarizo kwa Mayahudi na Manasara na washirikina wa Kiarabu ambao hawakumwamini Muhammad. Siri ya matahayarizo haya ni kwamba Mayahudi wanajifaharisha kwa kunasibika kwao na Israil: Na Israil ndiye Yaqub bin Is-hak bin Ibrahim; Manaswara nao wanajifaharisha kwa Isa na nasabu ya Isa kwa upande wa mama inaambatana na Israil vile vile. Ama washirikina wa Kiarabu wengi wao wanatokana na Adnani nasabu yao inarudia kwa Ismail bin Ibrahim kuongezea kwamba wao walipata heri wakati wa kijahili kwa baraka za nyumba iliyojengwa na Ibrahim. Kwa hiyo wote wanajifaharisha kwa Ibrahim na mila ya Ibrahim na inajulikana wazi kwamba Muhammad(s.a.w.w) anatokana na kizazi cha Ibrahim na yuko katika mila ya Ibrahim. Kwa hivyo mwenye kumk-anusha Muhammad na mila yake ndio amemkanusha Ibrahim na mila yake. Hapana shaka kwamba mwenye kukanusha matokeo ya utukufu na fahari yake, basi yeye ni safihi (mpumbavu) sawa na mwenye kufanya mambo ya kumwangamiza yeye mwenyewe.

Hakika sisi tulimtakasa (Ibrahim) katika dunia; Yaani tulimfanya safi mwenye kutakata na uchafu; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّـهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ وَيُطَهِّرَكُمْ تَطْهِيرًا ﴾

Mwenyezi Mungu anataka kuwaondolea uchafu enyi watu wa nyumba (ya Mtume) na kuwatakasa kabisa kabisa. (33.33)

Na hakika yeye katika Akhera atakuwa miongoni mwa watu wema.Kwa uwazi kabisa ni kwamba yeye katika dunia yuko hivyo; kwa sababu Uislamu unaiunganisha akhera na amali za duniani; ambaye katika dunia atakuwa mwema na mwenye busara, basi huko akhera pia atakuwa hivyo na ambaye katika dunia atakuwa mwovu na kipofu basi huko akhera pia atakuwa hivyo.

Mola wake alipomwambia silimu akasema: Nimesilimu kwa Mola wa walimwengu. Unaweza kuuliza,Je, Mwenyezi Mungu alimtaka Ibrahim asilimu (anyenyekee) kabla ya kumpa Utume au baada yake? Kwa sababu haiwezekani Mwenyezi Mungu kumpa wahyi asiyekuwa Mtume.Na pia hawezi kuteremsha wahyi kwa mtu ila baada ya kusilimu (kunyenyekea).

Jibu : Hakika kauli yake Mwenyezi Mungu: Silimu (Nyenyekea) akasema nimesilim ni fumbo la kuwa Ibrahim ni msafi mwenye Ikhlas na kwamba yeye ndiye mwenye kuchukua utume na ujumbe kwa ukamilifu. Kwa hivyo makusudio yake ni kumsifu Ibrahim kutokana na Ikhlasi yake, twaa yake na kufuata kwake amri. Wakati huo huo ni matahayarizo kwa Mayahudi, manaswara na washirikina wa Makka ambao wanajifaharisha kwa Ibrahim, kisha wanamuasi na kumpinga yule aliyekuja kuhuyisha mila ya Ibrahim na kueneza desturi na itikadi yake.

Na Ibrahim akawausia haya wanawe na Yaqub pia: Enyi wanangu! Hakika Mwenyezi Mungu amewachagulia dini hii; basi msife ila nanyi mmekuwa Waislamu. Yaani thibitini juu ya Uislamu mpaka kufa ili mfufuliwe juu ya Uislamu na mumkabili Mwenyezi Mungu kwa huo Uislamu.

HAKI YA MTOTO KUTOKAKWA MZAZI

Aya hiyo iliyotangulia inatambulisha kwamba mzazi ana jukumu kubwa na malezi ya mtoto wake na kumwongoza kwenye dini ya haki. Imam Zaynul- Abidin(a.s) Amesema: Ama haki ya mtoto wako ni kujua kuwa anatokana na wewe na kwamba wewe una jukumu la kuitengeneza vizuri adabu yake na kumfahamisha kuhusu Mola wake Mtukufu na kumsaidia kumtii. Basi mwamrishe amali ambayo anajua kuwa atapata thawabu kwa kufanya wema, na kupata dhambi kwa kufanya mabaya.

Je mlikuwapo yalipomfikia Yaqub mauti. Kumfikia mauti ni wakati wa kufa, alipopata alama za kufa. Mwenye Majmau anasema: Mayahudi wanadai kuwa Yaqub alipokufa aliwausia wanawe kushikamana na Uyahudi. Ndio Mwenyezi Mungu akabatilisha madai yao juu ya Yaqub; sasa vipi mnadai mambo ya uongo? Kwa hakika ni kwamba Yaqub aliwaambia wanawe: Je mtaabudu nini baada yangu? Unaweza kuuliza kwamba neno nini hutumiwa kwa kisicho na akili, sasa imekuaje hapa kutumiwa kwa mwenye kuabudiwa kwa haki? Jibu: Wakati huo watu walikuwa wakiabudu masanamu, ndipo likaletwa swali kutokana na vile wanavyoabudu sio kutokana na uhaki wa kuabudu. Kwa hiyo maana itakuwa ni kitu gani mtaabudu? Wakasema: Tutamwabudu Mola wako na Mola wa baba zako, Ibrahim na Ismail na Is-hak, Mungu mmoja tu, na sisi tunasilimu Kwake. Unaweza kuuliza Yaqub ni mtoto wa Is-hak, na Ismail ni ami yake (ndugu wa baba yake) sasa imekuwaje kumwingiza Ismail pamoja na mababa? Jibu: Ami yuko katika daraja ya baba kwa sababu ni nduguye na anaadhimishwa kama anavyoadhimishwa baba.Iko Hadith ya Mtume(s.a.w.w) inayosema; kuwa Mtume alisema:Nirudishieni baba yangu yaani ami yake Abbas.

Huo ni umma uliokwishapita. utapata ulioyachuma, nanyi mtapata mtakayoyachuma. Aya hii inaashiria kawaida ya mambo, kwamba natija za amali zote na athari zake zitamrudia mwenye kutenda peke yake, hawezi kunufaika nazo mwenye nasaba naye na wala hazitamdhuru mwingine. Uislamu umethibitisha kawaida hii kwa mifumo mbali mbali ya maneno, kama vile anavyosema Mwenyezi Mungu:...Wala hatabeba mbebaji mzigo wa mwingine (6:164)

Na kwamba mtu hatapata ila yale aliyoyafanya. (53:39) Pia Mtume(s.a.w.w) amesema kumwambia mwanawe Fatima:Ewe Fatima! Fanya amali wala usiseme mimi ni binti wa Muhammad, kwa sababu mimi sitakutoshea wewe na kitu chochote kwa Mwenyezi Mungu. Na mengineyo. Kufafanua zaidi maudhui haya kutafahamisha kwamba mpaka leo sisi hatujui mambo yaliyo wazi kabisa.

19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NG’OMBE)

﴿وَقَالُوا كُونُوا هُودًا أَوْ نَصَارَىٰ تَهْتَدُوا قُلْ بَلْ مِلَّةَ إِبْرَاهِيمَ حَنِيفًا وَمَا كَانَ مِنَ الْمُشْرِكِينَ﴾

135.Na wakasema: Kuweni Mayahudi au Manaswara ndio mtaongoka Sema: Bali (tunashika) mila ya Ibrahim Mwongofu, wala hakuwa katika washirikina.

﴿قُولُوا آمَنَّا بِاللَّـهِ وَمَا أُنزِلَ إِلَيْنَا وَمَا أُنزِلَ إِلَىٰ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ وَالْأَسْبَاطِ وَمَا أُوتِيَ مُوسَىٰ وَعِيسَىٰ وَمَا أُوتِيَ النَّبِيُّونَ مِن رَّبِّهِمْ لَا نُفَرِّقُ بَيْنَ أَحَدٍ مِّنْهُمْ وَنَحْنُ لَهُ مُسْلِمُونَ ﴾

136.Semeni: Tumemwamini Mwenyezi Mungu na yale tuliyoteremshiwa na yale yaliyoteremshwa kwa Ibrahim na Ismail na Is-hak na Yaqub na wajukuu na waliyopewa Musa na Isa na pia yale waliyopewa Manabii (wengine) kutoka kwa Mola wao; hatutafautishi baina ya yeyote katika hao na sisi tumesilimu (tumenyenyekea) kwake.

﴿فَإِنْ آمَنُوا بِمِثْلِ مَا آمَنتُم بِهِ فَقَدِ اهْتَدَوا وَّإِن تَوَلَّوْا فَإِنَّمَا هُمْ فِي شِقَاقٍ فَسَيَكْفِيكَهُمُ اللَّـهُ وَهُوَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴾

137.Basi wakiamini kama mnavyoamini itakuwa wameongoka. Na wakikengeuka basi wao wamo katika upinzani tu. Basi Mwenyezi Mungu atakutoshea (na shari yao),Na yeye ndiye msikizi mjuzi.

﴿صِبْغَةَ اللَّـهِ وَمَنْ أَحْسَنُ مِنَ اللَّـهِ صِبْغَةً وَنَحْنُ لَهُ عَابِدُونَ ﴾

138.(Huu ni) upakaji rangi wa Mwenyezi Mungu. Na ni nani aliye mzuri kwa upakaji rangi kuliko Mwenyezi Mungu? Na sisi tunamwabudu Yeye.

NAWAKASEMA: KUWENI MAYAHUDI AU MANASWARA

Aya ya 135-138

MAANA

Na wakasema: Kuweni Mayahudi au Wakristo mtaongoka. Dhamiri katika wakasema inawarudia watu wa Kitabu; maana yake walisema Mayahudi kuweni Mayahudi mtaongoka kwa sababu uongofu, wanavyodai wao, unatokana na wao tu peke yao.Na Wakristo nao walisema hivyo hivyo. Mwenyezi Mungu anamwambia Mtume wake Mtukufu Muhammad(s.a.w.w) :Sema bali (tunashika) mila ya Ibrahim. Yaani hatuwafuati Mayahudi wala Wakristo, bali tunafuata mila ya Ibrahim. Tumeyataja yanayoelekeana na haya katika Aya ya 111-113 ya sura hii.

MJADALAWA KIMANTIKI

Huenda mtu akasema: Mayahudi wamedai kuwa na haki, Wakristo nao wakadai kuwa na haki, na Muhammad(s.a.w.w) naye aka-sema bali Ibrahim ndiye mwenye haki sio Mayahudi wala Wakristo; na kauli zote hizi ni madai. Sasa basi ikiwa itafaa kwa Mayahudi na Wakristo kutumia mantiki haya yasiyofaa, basi itakua haifai kuyafa-nanisha kwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake; Je, kuna njia gani?

Jibu : Makusudio ya: Bali (tunashika) mila ya Ibrahim ni kuyabatilisha madai ya Mayahudi na kuwanyamazisha, na wala sio kuthibitisha uhakika hasa. Inawezekana mtu kuipinga hoja ya mtesi wake kwa kitu ambacho sio hoja yake bali ni hoja iliyo mfano wake; kama vile kuyavunja madai ya Wakristo kwa Adamu ambaye hana baba; pale waliposema kwamba Masih ni Mungu, kwa sababu hana baba.Na Adam naye hana baba, lakini hawamwiti Mungu. Aina hii ndiyo inayoitwa mjadala wa kimantiki.

Kwa hiyo njia ya kuwanyamazisha Mayahudi na Wakristo ambayo tunayo ni:- Mayahudi na Wakristo wanahitalifiana kidini na kiitikadi. Kila kundi linalikufurisha kundi jingine, lakini wakati huo huo wanaafikiana juu ya usahihi wa dini ya Ibrahim. Kwa dhahiri kabisa ni kwamba Ibrahim hakuwa Yahudi wala Mkristo bali aliacha dini za upotefu akashikamana na dini ya haki na hakuwa katika washirikina. Hakuwa Yahudi kwa vile hakusema kuwa Uzayr ni mtoto wa Mungu, wala hakumfananisha Mwenyezi Mungu; kama walivyodai kwamba Mwenyezi Mungu ni mzee mmoja mwenye mvi za kichwani na kidevuni. Vile vile Ibrahim hakuwa Mkristo kwa sababu hakusema Masih ni mtoto wa Mungu kwa vile hilo ni shirk.

Maadam Mayahudi na Wakristo wanaikubali dini ya Ibrahim, basi inawalazimu wawe ni wenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu, bali pia wanalazimika wahiji Al-Kaaba tukufu; kama alivyokuwa Ibrahim akiitakidi na kufanya, na kama alivyoitakidi Muhammad na kufanya; na wao hawakumpwekesha Mwenyezi Mungu wala hawakuhiji. Kwa hiyo wao ni waongo; na Muhammad ni mkweli na mwaminifu juu ya dini ya Mwenyezi Mungu na mila ya Ibrahim. Kwa maneno mengine ni kwamba kushikamana na lile lililoafiki ambalo ni dini ya Tawhid aliyokuwa nayo Ibrahim na aliyonayo Muhammad hivi sasa, ni bora kuliko kuchukua lile lenye hitilafu ambalo ni Uyahudi na kumfananisha kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu, na Ukristo na utatu wake.Semeni: Tumemwamini Mwenyezi Mungu .Yaani semeni enyi Waislamu.Na yale tuliyoteremshiwa ambayo ni Quran . Na yale yaliyoteremshwa kwa Ibrahim nazo ni sahifa za Ibrahim; Inasemekana zilikuwa kumi. Na Ismail na Is-hak.

Hao ni watoto wa Ibrahim. Ismail ndiye mkubwa kuliko Is-hak; mama yake ni Hajar na mama wa Is-hak ni Sara. Yaqub ni mtoto wa Is-hak. Hao wote hawakuteremshiwa sahifa, isipokuwa ziliteremshwa kwa Ibrahim, lakini inafaa kusema kuwa zimeteremshiwa wote kwa kuangalia kwamba wao walikuwa wakiabudu na kulingania kutokana na sahifa hizi; sawa na vile inavyofaa, kwa sisi Waislamu kusema: tumeteremshiwa Quran, kwa vile tunaamini na kufanya amali kutokana nayo na tunailingania.Na Wajukuu. Hao ni wajukuu wa Yaqub kutokana na watoto wake kumi na wawili; Ni kama makabila ya Kiarabu katika uzao wa Ismail. Katika kizazi hicho kuna mitume wengi; kama vile Daud, Suleiman, Yahya, Zakariya. Vile vile waumini wengine ambao walifanya ibada kutokana na sahifa za Ibrahim(a.s) .

Na waliyopewa Musa na Isa Ni Taurat na Injil na pia wengine waliyopewa Manabii.Kama Zaburi aliyoteremshiwa Daud.Hatutofautishi baina ya yeyote katika hao. Yaani tunawaamini wote, wawe na kitabu au la. Sisi sio kama Mayahudi na Wakristo ambao wanaamini baadhi na kukanusha baadhi, bali wote kwetu ni sawa katika kuukubali utume wao. Kimsingi ni kwamba kuwaamini wote ni wajibu kwa njia ya ujumla, na wala hatukukalifishwa kuwajua kwa upambanuzi ila baada ya ubainifu kutoka katika Quran, au Hadith. Basi wakiamini kama mnavyoamini nyinyi itakuwa kweli wameongoka. Yaani wakiamini imani sahihi ambayo ni Tawhid yenye kutakata na aina yoyote ya shirk, na pia wakiwakubali Mitume wote akiwemo Muhammad; kama vile wanavyofanya Waislamu kwa Mitume wote bila ya kuwabagua wengine, wakifanya hivyo, basi watakuwa wameongoka. Wala makusudio sio kuwa waamini dini mfano wa dini ya Kiislam.Kwa sababu Uislamu hauna cha kufananisha.

Na wakikengeuka basi wao wamo katika upinzani tu . Yaani kila anayeipinga haki anakuwa amejitoa kundini na kujitofautisha.Basi Mwenyezi Mungu atakutoshea Kwani vitimbi viovu vinawapata wenyewe. Kwa ufupi ni kwamba Uislamu unakataa ubaguzi, unatoa mwito wa kusaidiana kwa misingi ya kheri na uadilifu, unaikubali haki popote ilipo na unawataka wafuasi wake wafungue nyoyo kwa watu wote kwa mapenzi na Ikhlasi.

(Huu ni) upakaji rangi wa Mwenyezi Mungu. Ni dini ya haki ambayo inautwaharisha moyo na akili kutokana na uchafu; na wala sio kuzama katika maji, (ya kubatiza) kama wanavyofanya Wakristo. Muhyiddin Ibnul-Arabi katika tafsir yake anasema: Hakika kila mwenye madhehebu na itikadi anapambika na itikadi yake, dini na madhehebu yake. Wenye kuabudu kutokana na mila wanapambika na pambo la kiongozi wao. Na wenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu wanapambika na pambo la Mwenyezi Mungu ambalo hakuna pambo zuri zaidi ya hilo na wala hakuna jengine baada yake!

﴿قُلْ أَتُحَاجُّونَنَا فِي اللَّـهِ وَهُوَ رَبُّنَا وَرَبُّكُمْ وَلَنَا أَعْمَالُنَا وَلَكُمْ أَعْمَالُكُمْ وَنَحْنُ لَهُ مُخْلِصُونَ﴾

139.Sema: Je mnahojiana nasi juu ya Mwenyezi Mungu? Na hali yeye ni Mola wetu na Mola wenu? Na sisi tuna vitendo vyetu, nanyi mna vitendo vyenu; na sisi tunamfanyia Ikhlas yeye.

﴿أَمْ تَقُولُونَ إِنَّ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ وَالْأَسْبَاطَ كَانُوا هُودًا أَوْ نَصَارَىٰ قُلْ أَأَنتُمْ أَعْلَمُ أَمِ اللَّـهُ وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّن كَتَمَ شَهَادَةً عِندَهُ مِنَ اللَّـهِ وَمَا اللَّـهُ بِغَافِلٍ عَمَّا تَعْمَلُونَ﴾

140.Au Mnasema kuwa Ibrahim na Ismail na Is-haq na Yaqub na wajukuu (zake) walikuwa Mayahudi au Manaswara? Sema: Je, nyinyi mnajua zaidi au Mwenyezi Mungu? Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule afichaye ushahidi alio nao utokao kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika na hayo mnayoyafanya.

﴿تِلْكَ أُمَّةٌ قَدْ خَلَتْ لَهَا مَا كَسَبَتْ وَلَكُم مَّا كَسَبْتُمْ وَلَا تُسْأَلُونَ عَمَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴾

141.Huo ni umma uliokwishapita. utapata uliyoyachuma nanyi mtapata mliyoyachuma wala hamtaulizwa waliyokuwa wakifanya.

JE MNAHOJIANA NASI JUU YA MWENYEZI MUNGU?

Aya 139-141

MAANA

Yamekwishatangulia maelezo katika Aya ya 92-96 kwenye kifungu cha Maslahi ndio sababu, kwamba Mayahudi walimpinga Mtume kwa ajili ya masilahi yao na mali waliyokuwa wakiichuma kwa njia ya riba na utapeli.Vile vile pombe, kamari na mengineyo yaliyoharamishwa na Uislamu. Na walimwambia Mtume: Wewe siye Mtume kwa sababu Mwenyezi Mungu hapeleki Mtume asiyekuwa Myahudi. Yaani wanadai kwamba Mwenyezi Mungu ni wao peke yao na kwamba yeye ni Mungu wa kabila na sio Mungu wa Ulimwengu. Vile vile viongozi wa kikristo na mamwinyi wa kiquraishi walimpinga Mtume kwa kuhofia vyeo vyao na masilahi yao. Wakatoa sababu za uongo, kama walivyotoa Mayahudi. Wakristo walisema kama ilivyoelezwa katika tafsiri mbali mbali: Lau Mwenyezi Mungu angelituma Mtume, basi angelikuwa katika kabila letu sio mwarabu. Ama mamwinyi wa kikuraish, nao walisema: Lau Mwenyezi Mungu angelipeleka Mtume kutoka katika kabila la Waarabu basi angelimtuma kutoka katika tabaka la kitajiri lenye nguvu; kama ilivyoonyesha Aya hii:

﴿وَقَالُوا لَوْلَا نُزِّلَ هَـٰذَا الْقُرْآنُ عَلَىٰ رَجُلٍ مِّنَ الْقَرْيَتَيْنِ عَظِيمٍ ﴾

Na walisema: Kwa nini hii Quran haikuteremshwa kwa mtu mkubwa katika miji miwili hii? (43:31)

﴿أَوْ يُلْقَىٰ إِلَيْهِ كَنزٌ أَوْ تَكُونُ لَهُ جَنَّةٌ يَأْكُلُ مِنْهَا﴾

Au (mbona) hakuangushiwa hazina (ya mali); au (kwa nini) asiwe na bustani ale katika hiyo? (25:8)

Kila kitu kinaweza kuwa na mjadala na hoja; hata kuweko Mwenyezi Mungu pia; isipokuwa kitu kimoja tu, hakiwezi kuwa na ubishani milele kwa wale wanaomjua Mwenyezi Mungu, nacho ni kuihusisha rehema ya Mwenyezi Mungu na neema Yake kwa watu fulani tu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:Je wao wanaigawa rehema ya Mola wako?... (43:32).Kwa hivyo ndio Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) kuwaambia wale waliokanusha.

* 36 Makusudio ya miji miwili ni Makka na Taif na wanayemkusudia Makka ni Walid bin Al- Mughira na katika Taif ni Urwa bin Masud Athaqafi. Je mnahojiana nasi juu ya Mwenyezi Mungu? Na hali nyinyi mnajua kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu anajua zaidi anayestahiki Utume na asiyestahiki! Basi msimwingilie Mola wenu, ni juu yetu sisi na nyinyi kuikubali hukumu Yake sio kufanya mjadala katika matakwa Yake na hiyari Yake. Hayo ndio maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Na hali Yeye ni Mola wetu na Mola wenu. Na sisi tuna vitendo vyetu; na nyinyi mna vitendo vyenu. Kauli hii ni sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿لَكُمْ دِينُكُمْ وَلِيَ دِينِ﴾

Mna dini yenu nami nina dini yangu. (109:6) Yaani athari ya ugomvi wenu katika khiyari ya Mwenyezi Mungu ya kunineemesha mimi, itawarudia nyinyi peke yenu; kama vile ambavyo madhara ya ukafiri yanamrudia kafiri na manufaa ya imani yanamrudia mumin. Na sisi tunamfanyia Ikhlasi Yeye tu. Sio nyinyi kwa sababu mnamhukumu Mwenyezi Mungu na mnataka afanye vile mtakavyo nyinyi. Ama sisi mambo yote tunamwachia Yeye na tunakubali hukumu Yake. Je mnasema kuwa Ibrahim na Ismail na Ishaq na Yaqub na wajukuu (zake) walikuwa Mayahudi au Wakristo.

Hayo yanaungana na Mnahojiana nasi juu ya Mwenyezi Mungu? Maana yake ni jambo gani kati ya mawili mnalolingangania? Je ni kusema kwenu kwamba Mwenyezi Mungu hamtumi Mtume mwarabu au ni kuwa mko kwenye dini ya Ibrahim na watoto wake na wajukuu zake? Mkingangania jambo la kwanza basi Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi anapouweka ujumbe wake. Na kama mkingangania jambo la pili, basi Ibrahim aliachana na dini zote za upotofu akashikamana na dini ya haki. Hakuwa Myahudi wala Mkristo. Kwani dini hizo zilizotokea baada yake na baada ya watoto wake na wajukuu zake. Kwa hiyo kauli yenu ni batili haina hoja. Quran inatuongoza katika ubishani huu kwenye mfumo ambao unatakikana tuufuate kwa kutegemea mantiki ya kiakili yatakayowakinaisha wote wenye akili.

Sema: Je, nyinyi mnajua zaidi au Mwenyezi Mungu? Tumetangulia kueleza kuwa Mayahudi na Wakristo, kila kundi lilisema ndilo linalostahiki utume; ndipo Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume Wake Mtukufu kuwajibu kwa kauli Yake:Je nyinyi mnajua zaidi mahali alipouweka ujumbe Wake au ni Yeye? Ujumbe ni wa Mwenyezi Mungu na unatoka kwa Mwenyezi Mungu, vipi mnataka kumchagua nyinyi? Je, nyinyi ni mawasii wa Mungu? Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo kabisa. Je, kuna mjinga zaidi ya asiyejua kitu amwambie mgunduzi wa chombo cha anga za juu kuwa mimi ninajua zaidi kuliko wewe? Sijaona kauli iliyo fasaha zaidi ya kumfanya mtu kuwa mjinga kuliko kauli hii ya Mwenyezi Mungu(Je,nyinyi mnajua zaidi au Mwenyezi Mungu?) Tunamtaka maghufira Mwenyezi Mungu na kumtaka hifadhi kutokana na wanayoyasema na wanavyofanya wabatilifu:Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule afichae ushahidi alionao utokao kwa Mwenyezi Mungu? Yaani enyi Mayahudi na Wakristo, ushahidi kutoka kwa Mwenyezi Mungu mmeusoma katika Tawrat. Nao ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) atatuma Mtume mwarabu kutoka katika kizazi cha Ismail(a.s) , lakini pamoja na hayo mmeuficha ushahidi mkamkosea Mwenyezi Mungu kwa kukigeuza Kitabu chake kwa batili na kuipinga haki. Kwa hiyo mnapasa laana na adhabu.

Huo ni umma uliokwishapita, utapata uliyoyachuma nanyi mtapata mtakayoyachuma.

Aya hii imekwishatangulia katika Aya ya 134 herufi kwa herufi. Huko imebainisha kwamba Ikhlas ya Ibrahim(a.s) na utukufu wake hauwezi kuwafaa nyinyi na kitu chochote. Hapa imekuja kwa kubainisha kwamba amali ya Mayahudi na Wakristo haiafikiani na itikadi ya Ibrahim na amali yake. Kwa hiyo madai yao kwamba wao wako kwenye mila ya Ibrahim ni uwongo na uzushi.Hayo tumeyazungumza katika tafsir ya Aya ya 48.

USHAHIDI

Ni wajibu kwa kila mtu aliyebalehe mwenye akili kuitikia mwito wa kutoa ushahidi; wala haifai kwake kukataa bila ya udhuru. Mwenyezi Mungu anasema:Na mashahidi wasikatae wanapoitwa. (2:282)

Imam Jaafar Assadiq amesema: Anapokuita mtu ili ushuhudie juu ya deni au haki yoyote usichelewe. Jukumu la kuchukua ushahidi linawajibisha kuutoa na ni haramu kuuficha. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَلَا تَكْتُمُوا الشَّهَادَةَ وَمَن يَكْتُمْهَا فَإِنَّهُ آثِمٌ قَلْبُهُ﴾

Wala msifiche ushahidi na atakayeuficha basi hakika moyo wake ni wenye kuingia dhambini... (2:283)

Amesema Imam Assadiq(a.s) :Mwenye ushahidi asikatae kuutoa atakapotakiwa na atoe nasaha wala asilaumiwe. Ndio, inawezekana kuacha kutoa ushahidi kwa kuhofia madhara au kumhofia mwingine asiyekuwa na hatia. Kwa sababu hakuna kudhuriana katika Uislamu kutokana na Ijmai na Hadith mahsus.

WENYE KUFANYA IKHLAS

Uislamu unawahoji wabatilifu, unawalaumu kwa kiakili na dhamiri. Vile vile unawanasihi kwa uzuri na kuwaamrisha mema, lakini hauwachukulii hatua nyingine zaidi ya mawaidha mazuri isipokuwa kama wakipetuka mpaka, wakafanya uadui kuwapoteza watu wema na kuipoteza haki kwa uzushi na propaganda za uongo.Wakifanya kitu katika hivi itapasa kuwatia adabu. Ameyabainisha Mwenyezi Mungu hayo katika Aya nyingi, kwa mfano:Na kama wakiacha basi usiweko uadui ila kwa madhalimu. (2:193)

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَيْكُمْ أَنفُسَكُمْ لَا يَضُرُّكُم مَّن ضَلَّ إِذَا اهْتَدَيْتُمْ إِلَى اللَّـهِ مَرْجِعُكُمْ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ﴾

Enyi mlioamini lililo lazima juu yenu ni nafsi zenu.Hawawadhuru waliopotoka ikiwa mmeongoka. Marejeo yenu yote ni kwa Mwenyezi Mungu; basi atawaambia mliyokuwa mkiyatenda. (5:105)

Na Aya nyingine ni hii tuliyonayo: Na sisi tuna vitendo vyetu nanyi mna vitendo vyenu na sisi tunamfanyia Ikhlasi Yeye

MWISHO