TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
Kundi:

Matembeleo: 35402
Pakua: 2975


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Juzuu 9 Juzuu 10 Juzuu 11
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 20 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 35402 / Pakua: 2975
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

Mwandishi:
Swahili

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NGOMBE)

DINI NA ELIMU

Jambo la kushangaza ni kwamba hata wale wanaoamini kuwa ulimwengu umepatikana kibahati (sadfa), pia wanaamini ghaibu. Kwa sababu hakuna anayekataa kwamba kuamini sadfa ni ghaibu. Kwa vile hawakuiona hiyo sadfa kwa macho.Kwani wao wamepatikana baada ya kuja ulimwengu. Vile vile hawawezi kuijua kiakili; kwa vile akili bado haijaifanyia majaribio ya kukanusha au kuthibitisha.

La kushangaza zaidi ni kwamba wao wenyewe wanakadiria kuwa ulimwengu umepatikana kutokana na mada ndogo inayoitwa ether. Na hilo wanaliamini kwa imani isiyokuwa na shaka yoyote; kisha wanawakataza wengine wasiamini kupatikana nguvu yenye hekima yenye kupangilia vizuri mambo kwenye ulimwengu huu; ingawaje huku ndiko kuliko karibu zaidi na akili na moyo kuliko kufikiria kitu kipofu na kiziwi.

Kwa vyovyote iwavyo, ghaibu inajieleza kwa jina lake; inafahamika kwa wahyi tu, na sio kwa majaribio wala kwa nguvu ya kiakili. Sharti lake pekee ni kutopingana na akili, sio kutambuliwa na akili.Kwa hali hiyo basi, elimu ya sayansi haina nafasi ya kuwa juu ya wahyi. Umuhimu wa elimu ya sayansi unakuwa katika kumsaidia binadamu kujua hali ya maumbile na kuyatumia, na ni jawabu la kujua ni nguvu gani zinazofanya asili ya vitu, mimea na wanyama na vipi tutaunda ndege zinazokimbia kuliko sauti.

Sayansi haitambui ni nani aliyesababisha kupatikana maumbile (Nature) na utaratibu wake. Ama dini inatuambia sababu za kupatikana, na inatupa funguo kuu za kumjua aliyeumba ulimwengu na kutuongoza kwenye lile tunalohitajika kulifanya katika maisha haya, ili tuhakikishe kufikia lengo letu la kiroho na la kimaada (kimwili.) Viwanda au kilimo peke yake, au vyote kwa pamoja haviwezi kutekeleza matakwa yote ya binadamu na malengo yake. Kwa sababu mtu sio mwili tu; bali ni mwili, roho, mawazo na fikra. Katika mwili wa binadamu kuna rehema yenye kuenea iitwayo utu, na nuru yenye kuenea iitwayo akili ambayo inaufanya ulimwengu mkubwa uwe mdogo mbele yake.

Mahitaji yetu ya hisia, kama vile kula kunywa na kulala yamekuwa ni lazima kwetu, wala hatuna hiyari ya kuyaacha. Kwa hivyo tutake tusitake ni lazima tuyahangaikie; wala hakuna tofauti katika hilo kwa mjuzi au kwa asiyekuwa na ujuzi, kwa Mtume au asiyekuwa Mtume. Lakini mahitaji ya kiroho yanatofautiana kulingana na watu. Mara nyingi sana mtu huvunja matakwa yake, mapenzi yake na ghadhabu - jambo ambalo ni bora kabisa - lakini mtu hawezi kuacha mahitaji ya mwili wake.

Zaidi ya hayo, lau ingekuwa mtu ni mwili tu, ungeliweza kuhukumiwa na wataalamu wa sayansi, kama wanavyohukumu maada. Na wangeliweza kujua siri za nafsi na undani wake. Vile vile wangeliweza kubadilisha ukafiri kuwa imani na imani kuwa ukafiri; mapenzi kuwa chuki na chuki kuwa mapenzi; uzee kuwa ujana na ujana kuwa uzee, na mengineyo ambayo yanaweza kujaza kurasa.Natarajia kulifafanua zaidi suala hili katika sehemu zake zinazohusika nazo.

Makusudio ya maelezo haya ni kuonyesha kuwa maudhui ya elimu ya sayansi ni mbali na maudhui ya dini na wahyi. Sayansi ni maudhui ya kimaada yenye kuganda au kukua; na lengo lake ni kugundua nguvu za kimaada. Ama dini ni maudhui ya maisha ya binadamu kwa pande zake mbili za kimaada na za kiroho. Ukipenda unaweza kusema: maisha ya kiroho na ya kimatendo. Na lengo lake ni kutaka watu wote waishi maisha ya kuridhisha yenye ufanisi.

Ndio! Uislamu unaheshimu akili na elimu yenye manufaa, na unahimiza kuitafuta; bali unaizingatia kuwa ni wajibu kwa mwanamume na mwanamke. Elimu inawainua watu kupanda daraja.Kwa ajili hiyo basi ni wajibu juu ya Mwislamu kuitakidi kwamba hakuna kitu sahihi katika elimu au akili kinachopingana na Uislamu, wala hakuna kitu katika hukumu za Kiislamu kinachopingana na elimu au akili.Lakini sio kuwa akili inaweza kujua hukumu zote za dini. Unaweza kuuliza: Imethibiti Hadith kutoka kwa Mtume mtukufu(s.a.w..w) aliposema:Msingi wa dini yangu ni akili. Je, hiyo si inaonyesha kwamba akili inajua hukumu zote za dini ya Kiislamu?

Jibu : Uislamu unaanzia kwenye Uungu na Utume. Na kutokana na mawili hayo ndio yanachimbuka mafundisho yake na hukumu zake. Na njia ya kuyajua hayo ni akili. Kwa hivyo, maana ya Hadith tukufu ni kwamba Uislamu ambao misingi yake ni Uungu na Utume, unategemea akili kuuthibitisha huo Uungu na Utume, sio kuigiza na kufuata kama kipofu tu, au kufuata hekaya na vigano.2 Na wanasimamisha swala Mara nyingine serikali inaweza kumhukumu mtu kubaki katika mji fulani bila ya kutoka, na humlazimisha kupiga ripoti kituoni kwa ajili ya kuthibitisha kuweko kwake.

Kama akihalifu basi atatakiwa kujibu.Uislamu umemwekea mumin sharti maalum, atakaloweza kwalo kuthibitisha imani yake kwa Mwenyezi Mungu Aliyeumba mbingu na ardhi kila siku mara tano, na kumfanyia ikhlas katika amali zake zote. Quran inasema:

﴿ إِنِّي وَجَّهْتُ وَجْهِيَ لِلَّذِي فَطَرَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ حَنِيفًا وَمَا أَنَا مِنَ الْمُشْرِكِينَ﴾

Hakika mimi nimeulekeza uso wangu kwa yule Aliyeziumba mbingu na ardhi. Hali ya kuwa nimeacha dini zote za upotevu na mimi si miongoni mwa washirikina. (6:79)

*2 Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hujulikana kwa akili kutokana na njia ya ulimwengu. Na utume hujulikana kwa akili kutokana na miujiza.

﴿ قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٢﴾ لَا شَرِيكَ لَهُ وَبِذَٰلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ ﴾

Sema: hakika swala yangu na ibada zangu (zote) na uzima wangu, na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe vyote. Hana mshirika, na hayo ndio niliyoamrishwa na mimi ni wa kwanza wa waislamu (6:162-163)

Mwenye kuiacha swala kwa kuikana, basi ameritadi; na mwenye kuiacha kwa kupuuza atakuwa fasiki mwenye kustahili adhabu. Ndipo tunaikuta tafsiri ya Imam Ali(a.s) katika Nahjul-Balagha kuwa: Hakika Mtume ameifananisha swala na chemchemi ya maji moto iliyoko mlangoni kwa mtu; akiwa anaoga katika chemchemi hiyo mara tano kila siku hawezi kubakiwa na uchafu wowote. Yaani kudumisha swala kunautakasa moyo kutokana na kuritadi na ufasiki; kama unavyotakasika mwili kutokana na uchafu. Je, kuna uchafu unaoshinda ukafiri na ufasiki?

MAKUSUDIO YA KUTOA KATIKA YALE TULIYOWAPA

Kutoa hapa, kunakusanya yote anayoyatoa mtu katika njia ya kheri, iwe ni zaka au kitu kingine. Hakuna mwenye shaka kwamba kutoa kwa njia ya heri ni jambo zuri. Lakini je, kunapasa katika mali kutoa kitu kingine zaidi ya zaka na khums? Zimepokewa Hadith kwa upande wa sunni; kama vile kutoka kwa Tirmidhi, na kwa upande wa Shia; kama ilivyopokewa katika Al-Kafi; kwamba:katika mali, iko haki nyingine . Imam Sadiq(a.s.) ameifasiri haki hiyo kuwa:ni kitu anachotoa mtu katika mali yake akitaka atoe zaidi au kichache kwa kiasi cha vile anavyomiliki. Ametoa dalili Imam, kwa Aya isemayo:

﴿ وَالَّذِينَ فِي أَمْوَالِهِمْ حَقٌّ مَّعْلُومٌ ﴿٢٤﴾ لِّلسَّائِلِ وَالْمَحْرُومِ ﴾

Na ambao katika mali zao mna haki maalum (ya kupewa) masikini aombaye na anayejizuiya kuomba (70:24-25).

Wanavyuoni wengi wamelichukulia hilo kuwa ni sunna na wala sio wajib; isipokuwa Sheikh Saduq katika Shia. Imenukuliwa kutoka kwake kwamba zaidi ya zaka na khumsi, kuna haki nyingine iliyo ya lazima katika mali, inalazimika kuitoa kwa kiwango anachomiliki mtu; kingi au kichache. Vyovyote iwavyo, jambo ambalo halina shaka ni kuwa kutoa mali kwa njia ya kheri ni kujitwaharisha na uchafu na kujiokoa na adhabu ya moto. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا ﴾

Chukua sadaka katika mali zao uwasafishe na kuwatakasa kwazo.(9:103)

MAKUSUDIO YA YALIYOTEREMSHWA KWAKO

Na ambao wanaamini yaliyoteremshwa kwako. Manenoyanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) . Makusudio ya yaliyoteremshwa kwako, ni Quran na Hadith; Kwa sababu, yeye Mtume(s.a.w.w) :

﴿ وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾ إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ﴾

Wala hasemi kwa matamanio (ya nafsi yake). Hayakuwa haya (anayosema) ila ni wahyi uliofunuliwa (kwake). (53:3-4)

﴿ وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا﴾

Na anachowapa Mtume kichukueni, na anachowakataza jiepusheni nacho (59:7).

MAKUSUDIO YA YALIYOTEREMSHWA KABLA YAKO

Makusudio ya yaliyoteremshwa kabla yako, ni yale yaliyoteremshiwa Mitume waliotangulia; kama vile Zabur ya Daud, Tawrat ya Musa na Injil ya Isa. Lakini hakuna athari yoyote hivi leo ya vitabu hivi kwa upande wa kiamali. Kwa sababu katika itikadi ya Waislamu ni kwamba, ama vitakuwa havipo au yale yaliyopo yamepotoshwa kabisa. Tuwaachie wenyewe wakristo mambo yanayofungamana na Injil.

Nimesoma katika kitabu kinachoitwa Voltar kilichotungwa na Johstone Lanson, na kufasiriwa na Muhammad Ghanimi Hilal, ukurasa wa 193, chapa ya 1962. Ninamnukuu: Inajulikana kuwa idadi ya Injili hizi ni hamsini na nne, na Injili nne ziliandikwa baadaye na ya nne ya Luka, ndiyo ya mwisho.

Amesema Elias Najma katika kitabu: Yaasu Almasih (Yesu Masih) ukurasa 11 chapa ya 1962: Mitume (anakusudia wanafunzi wa Masih) walipoona kuwa ni dharura kukusanya mafundisho ya Mola na mafundisho mengine, ndipo wakaona waandike baadhi ya mafundisho, matendo na miujiza. Hiyo hasa ndiyo tunayoiita Injili iliyoandikwa.Kwa hivyo imekuja Injili moja katika sura nne.

Huku ni kukiri wazi kwamba Injili nne sio kiini hasa cha wahyi wenyewe na herufi zake; kama ilivyo Quran; isipokuwa ni kunakili kwa mapokezi kutoka kwa Masih(a.s) ; kama vilivyo vitabu vya Hadith kwa Waislamu, ambao wamekusanya kauli za Muhammad(s.a.w.w) , matendo yake na miujiza yake. Tofauti ni kuwa wapokezi wa Injil ni wanne: Mathayo, Yohana, Marko na Luka. Wao ni wenye kuhifadhiwa na kufanya madhambi na makosa, kama wanavyodai wakristo na kwamba haifai kutia ila mapokezi yao.

Lakini Waislamu hakuna (Isma) kuhifadhiwa na dhambi kwa wapokezi wa Hadith; bali haifai kuchukua na kutumia mapokezi yao ila baada ya kuchunguza na kuhakikisha. Hakuna tofauti katika mantiki ya kiakili kati ya Injili nne na vitabu vya Hadith. Inawezekana kuvitoa makosa, madaamu tu ni kunakili kutoka kwa mtu. Ama tofauti ya Quran na Injil iko wazi. Kwa sababu vizazi mbali mbali vimeshindwa kuleta angalau sura moja tu iliyofanana na Quran. Elias amejaribu kuzuia mushkeli huu kwa kauli yake katika ukurasa wa 12: Kanisa linatolea ushahid Injili, na Injili inalishuhudia kanisa.Vyote viwili vinathibitishiana.

Ni wazi kwamba hivyo ni kuthibitisha madai kwa madai yenyewe. Ni sawa na anayesema: Mimi ni mkweli katika madai yangu kwa sababu mtu fulani ananishuhudia kuwa mimi ni mkweli, kama akiulizwa, Ni nani anayeshuhudia kuwa huyo mtu fulani ni mkweli? Atasema: Mimi ninashuhudia kuwa yeye ni mkweli.Kwa maana hii anakuwa shahidi ndiye huyo huyo anayedai. Aina hii ya maneno wanafalsafa huiita mzunguko wa kubabaisha akili. Kama vile Mshairi mmoja alivyosema: Kigeugeu kutuka, Kati yangu na muhibu Lau si mvi kuzuka, Habiba singenighibu Na asingeniepuka, Mvi singeniswibu.

Ubeti wa mwisho, kama unavyouona, unafanana na kupagawa na akili. Kwa sababu, maana yake ni kuwa kuondoka mpenzi wa mshairi kumetokana na huyo mshairi kuota mvi; na kwamba huko kuota mvi kwake kumesababishwa na kuondoka mpenzi wake.

* 3 Katika gazeti An-Nahaar la Beirut la tarehe 12.7.1964 kuna makala ndefu yenye maelezo kwamba wataalamu na wakikristo wamethibitisha kwa majaribio na kwa kompyuta kwamba barua nyingi zinazonasibishiwa Paulo, mwasisi mkubwa wa ukiristo, ni uongo. Kwa hivyo kuondoka na kuota mvi ni visababishi kwa wakati mmoja; kama kusema: Nimeshona nguo ili niivae na nimeivaa ili niishone.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NGOMBE)

﴿إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا سَوَاءٌ عَلَيْهِمْ أَأَنذَرْتَهُمْ أَمْ لَمْ تُنذِرْهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ ﴾

6.Hakika wale ambao wamekufuru ni sawa wao ukiwaonya au usiwaonye, hawataamini.

﴿خَتَمَ اللَّـهُ عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ وَعَلَىٰ سَمْعِهِمْ وَعَلَىٰ أَبْصَارِهِمْ غِشَاوَةٌ وَلَهُمْ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴾

7.Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao; na juu ya macho yao pana kifuniko, basi watakuwa na adhabu kubwa.

NJIA YA UISLAMU

Aya 6-7

Ukiwaonya au usiwaonye, Yameshatangulia maelezo kuwa: mafundisho na misingi ya Kiislamu yapo aina mbili: Itikadi na amali; yaani mizizi na matawi; au itikadi na sharia: Vyovyote utakavyoita ni sawa.

Maudhui ya kiitakadi yanaambatana na nafsi ya mtu na hisia zake, na maudhui ya sharia ni amali za mtu na vitendo vyake. Uislamu umetoa mwito wa kuuamini kiitikadi na kisharia. Njia ambayo Uislamu umefuata kueneza mwito wake katika mambo Kwa hivyo kuondoka na kuota mvi ni visababishi kwa wakati mmoja; kama kusema: Nimeshona nguo ili niivae na nimeivaa ili niishone. Yanayoambatana na itikadi, imebainishwa katika Aya hii.

﴿دْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ إِنَّ رَبَّكَ هُوَ أَعْلَمُ بِمَن ضَلَّ عَن سَبِيلِهِ وَهُوَ أَعْلَمُ بِالْمُهْتَدِينَ﴾

Waite kwenye njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora.Hakika Mola wako ndiye anayemjua aliyepotea katika njia yake, naye ndiye anayewajua walioongoka. (16:125)

MAKUSUDIO YA HEKIMA NA MAWAIDHA MAZURI

Makusudio ya hekima na mawaidha mazuri, ni kutegemea akili ambayo inaweza kuyafahamu, kama vile Uungu ambao binadamu anaweza kufikia kujua kwa kuangalia vitu na kupeleleza katika maumbile na maumbile ya mbingu na ardhi. Vile vile Utume wa Muhammad(s.a.w.w) ambao watafiti wanaweza kuujua kutokana na sera yake na mfumo wa risala yake.

Ama njia ya Uislamu katika kujua yale ambayo akili pekee haitoshi kama vile ghaibu, basi inabidi kutegemea wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kupitia kwa Mtume ambaye Utume wake unathibitishwa na dalili za kiakili na ukweli wa yale anayoyaeleza kutoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) Ama njia ya kuthibitisha sharia ni kitabu (Quran), Sunna (Hadith) na akili. Misingi mitatu hii inakusanyika juu ya masilahi na ufisadi, wema na uovu au uadilifu na dhuluma, vyovyote utakavyopenda unaweza kuita.

Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَيُحِلُّ لَهُمُ الطَّيِّبَاتِ وَيُحَرِّمُ عَلَيْهِمُ الْخَبَائِثَ وَيَضَعُ عَنْهُمْ إِصْرَهُمْ وَالْأَغْلَالَ الَّتِي كَانَتْ عَلَيْهِمْ﴾

Na kuwahalalishia vizuri na kuwaharimishia vibaya na kuwaondolea mizigo yao na minyororo iliyokuwa juu yao... (7:157)

﴿يَسْأَلُونَكَ مَاذَا أُحِلَّ لَهُمْ قُلْ أُحِلَّ لَكُمُ الطَّيِّبَاتُ﴾

Wanakuuliza wamehalalishiwa nini, sema; mmehalalishiwa kila vilivyo vizuri... (5:4)

﴿وَأَوْحَيْنَا إِلَيْهِمْ فِعْلَ الْخَيْرَاتِ﴾

...na tukawapelekea wahyi kufanya heri... (21:73)

Kwa hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha uadilifu, na kufanya hisani, na kuwapa jamaa na anakataza uchafu na uovu na dhulma (16:90)

Kwa ufupi ni kuwa katika itikadi kuna yanayotegemea akili na yanayotegemea wahyi. Hukumu za sheria ziko katika masilahi na mambo ya uharibifu. Wameuitikia Uislamu na mwito wake walioamini yasioonekana, na wakatoa zaka; na wameyakataa hayo makafiri na wanafiki.Mwenyezi Mungu amewataja waaumini kwanza katika Aya zilizotangulia,Pili ametaja makafiri, na tatu anawataja wanafiki na sifa zao; kama zitakavyoeleza katika Aya zinayofuatia.

MWENYE KULAZIMIANA (KUSHIKAMANA) NA HAKI

Watu katika kulazimiana na haki na kuacha kulazimiana nayo wako aina mbili: Wa kwanza ni yule anayelazilimiana nayo kwa njia ya haki, ni sawa iwe imeafikiana na lengo lake au imetofautiana nalo, bali yeye hana matakwa yanayotofautiana na haki; na kwa ajili ya haki anajitolea mhanga na kuvumilia mashaka, sawa na mgonjwa anayevumilia uchungu wa dawa na maumivu ya mkasi kwa kutaka afya.

Wa pili ni yule ambaye hajilazimishi na kitu chochote wala hakina thamani chochote mbele yake isipokuwa kile chenye kuafikiana na matakwa na mapenzi yake. Wala hajali ufafanuzi wowote hata kama uko sawa. Huyu mwenye kujipurukusha na haki atakuwa na moja ya mambo mawili: Ama atakuwa anajipurukusha na haki kwa ndani na nje (katika moyo na katika ulimi wake) au atakuwa anajipurukusha kwa ndani tu sio nje, basi huyu wa kwanza ni kafiri na wa pili ni mnafiki kama inavyojulikana katika Quran. Mwenye kulazimiana na haki anatofautiana na asiyelazimika nayo kwa njia nyingi. Miongoni mwa njia hizo ni kama hizi zifuatazo:

Mwenye kulazimiana na haki anatambua majukumu yake, lakini asiyejilazimisha, hayatambui.

Mwenye kushikamana na haki haamini kitu isipokuwa pamoja na dalili yenye kukinaisha, lakini asiyeshikamana nayo haamini kitu kinachoitwa dalili, hoja au mantiki yoyote. Jema kwake sio jema ila lile analolikusudia yeye. Hata kama akikosea hajirekebishi bali anaendelea kuliboresha lile alilolikosea.

Mwenye kulazimiana na haki anatoa nafasi kwa mpinzani, anamsikiliza na anakuwa tayari kujirekebisha akiona amekosea. Hiyo ndiyo maana ya neno lake Mwenyezi Mungu:

﴿الَّذِينَ يَسْتَمِعُونَ الْقَوْلَ فَيَتَّبِعُونَ أَحْسَنَهُ﴾

Ambao husikiliza kauli wakafuata zile zilizo nzuri zaidi... (39:18).

Lakini kwa mtu asiyelazimiana na haki kwake ni kama kisa cha Paa huruka.

* 4 Inasemekana kuwa watu wawili waliona kitu kwa mbali, mmoja akasema: Yule ni paa. Mwengine akasema: Hapana ni kunguru Baada ya muda kidogo yule kunguru akaruka. Yule aliyepata,akamwambia mwenzake, Waona? Yule aliyekosa akasema: Ah! ni paa tu ijapokuwa ameruka! ndio ikawa ni mithali.

Mwenyezi Mungu amewafananisha wale wanaokakamia kwenye upotevu wao kwa ibara ya undani na akaielezea katika Aya nyingi tukufu kama hii:

﴿وَقَالُوا قُلُوبُنَا فِي أَكِنَّةٍ مِّمَّا تَدْعُونَا إِلَيْهِ وَفِي آذَانِنَا وَقْرٌ وَمِن بَيْنِنَا وَبَيْنِكَ حِجَابٌ فَاعْمَلْ إِنَّنَا عَامِلُونَ﴾

Na wakasema; nyoyo zetu zi katika vifuniko kwa yale unayotuitia, na katika masikio yetu mna uziwi na baina yetu na wewe kuna pazia, basi fanya (yako) na sisi tunafanya (yetu) (41:5)

Mwenye kushikamana na haki anasamehewa makosa yake kama akikosea baada ya kufanya utafiti na upekuzi, lakini mwengine hakubaliwi udhuru; na malipo yake ni laana na adhabu. Watu wengi zaidi hawaamini wala hawaridhii isipokuwa maslahi yao yanayowahusu tu kwa njia wanayoijua au wasiyoijua.

Utamkinaisha vipi mjinga kuwa, mtukufu zaidi wa watu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule anayemcha Mungu zaidi, na hali yeye mwenyewe anajitukuza kwa nasabu yake? Au utamkinaishaje mtawala kwa uadilifu wakati ambapo utawala wake umesimamia dhuluma? Au utawezaje kumkinaisha mlanguzi kwa uharamu wa ulanguzi wakati ukiwa huo ulanguzi ndio msingi wa utajiri wake?

Wote hao wanaoivunja haki ndio aliowakusudia Mwenyezi Mungu kwa kusema: Ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye hawatoamini. Unaweza kuuliza, itakuwaje kuhusu wale ambao hawako katika kundi la wale wanaoshikamana na haki na wale wasioshikamana nayo, kama vile wajinga wanaodhania mambo tu, ambao wanafanya haraka kusadiki bila ya hoja wala dalili yoyote isipokuwa wanafanya hivyo kujilinda na kutaka usalama tu? Jibu: Hakika hao ni kama wendawazimu na wanyonge.

﴿فَأُولَـٰئِكَ عَسَى اللَّـهُ أَن يَعْفُوَ عَنْهُمْ وَكَانَ اللَّـهُ عَفُوًّا غَفُورًا﴾

Basi hao huenda Mwenyezi Mungu akawasamehe, Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kusamehe Mwingi wa maghfira. (4.99)

Swala la pili, kwa dhahiri kauli yake Mwenyezi Mungu: Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao, ni kwamba amewazuia kuamini na kufuata haki. Kwa hivyo inakuwa kafiri amelazimishwa na hana hiyari basi hastahiki shutuma wala adhabu?

Jibu: Kila kitu ambacho hakina manufaa yoyote na wala hakitekelezi matakwa kinakuwa ni sawa tu, kiwepo au kisiwepo. Lengo linalokusudiwa kwa moyo ni kunufaika na kuongoka kwa dalili zilizo sahihi, kama vile ambavyo lengo la kusikia ni kunufaika na sauti zinazosikika, na lengo la macho ni kuona vinavyoshuhudiwa.

Kwa hivyo, zikiweko dalili za kutosha juu ya hakika na mtu akawa anaendelea kungangania upotevu wake, hiyo inamaanisha kuwa hakunufaika na moyo wake, na moyo wake haukunufaika na yale yanayotakikana kunufaika nayo; mpaka inakuwa kama vile ameumbwa bila ya moyo au kwa moyo uliofungwa, haufunguki kwa haki.Kwa hivyo, inajuzu kusifiwa mtu mwenye moyo uliosusuwaa kuwa yeye hana moyo. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَذِكْرَىٰ لِمَن كَانَ لَهُ قَلْبٌ أَوْ أَلْقَى السَّمْعَ وَهُوَ شَهِيدٌ ﴾

Hakika katika hiyo mna ukumbusho kwa mwenye moyo au kwa ategaye sikio, naye mwenyewe yupo anashuhudia. (50:37)

Ingawa moyo upo, lakini sio kitu maadamu uko mbali na uongofu. Kwa hivyo inakuwa kunasibishiwa Mwenyezi Mungu kupiga muhuri nyoyo zao ni kwa njia ya majazi sio ya hakika. Hayo yanatiliwa nguvu na maelezo ya kifuniko, kwani tunaona hakuna kifuniko katika masikio na macho ya makafiri. Hivyo basi hakuna muhuri wa kikweli katika nyoyo. Ama yale masuala ya Jabr na Ikhtiyar (kulazimishwa na hiyari) kwamba je, mtu analazimishwa au ana hiyari, utakuja ufafanuzi wake Inshallah.

﴿وَمِنَ النَّاسِ مَن يَقُولُ آمَنَّا بِاللَّـهِ وَبِالْيَوْمِ الْآخِرِ وَمَا هُم بِمُؤْمِنِينَ ﴾

8.Na kuna katika watu wasemao: Tumemwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, na hali ya kuwa wao si wenye kuamini.

﴿يُخَادِعُونَ اللَّـهَ وَالَّذِينَ آمَنُوا وَمَا يَخْدَعُونَ إِلَّا أَنفُسَهُمْ وَمَا يَشْعُرُونَ﴾

9.Wanataka kumdanganya Mwenyezi Mungu na wale walioamini, lakini hawadanganyi ila nafsi zao; nao hawatambui.

﴿فِي قُلُوبِهِم مَّرَضٌ فَزَادَهُمُ اللَّـهُ مَرَضًا وَلَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ بِمَا كَانُوا يَكْذِبُونَ ﴾

10.Nyoyoni mwao mna maradhi na Mwenyezi Mungu amewazidishia maradhi, basi watakuwa na adhabu iumizayo kwa sababu ya kule kusema kwao uongo.

﴿وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا تُفْسِدُوا فِي الْأَرْضِ قَالُوا إِنَّمَا نَحْنُ مُصْلِحُونَ ﴾

11.Na wanapoambiwa msifanye ufisadi katika ardhi husema, bali sisi ni watengezaji tu.

﴿ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْمُفْسِدُونَ وَلَـٰكِن لَّا يَشْعُرُونَ ﴾

12.Hakika wao ndio wafisadi, lakini hawatambui.

﴿وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ آمِنُوا كَمَا آمَنَ النَّاسُ قَالُوا أَنُؤْمِنُ كَمَا آمَنَ السُّفَهَاءُ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ السُّفَهَاءُ وَلَـٰكِن لَّا يَعْلَمُونَ﴾

13.Wanapoambiwa: Aminini kama walivyoamini watu, husema: Je, tuamini kama walivyoamini wapumbavu.Hakika wao ndio wapumbavu, lakini wao hawajui.

﴿وَإِذَا لَقُوا الَّذِينَ آمَنُوا قَالُوا آمَنَّا وَإِذَا خَلَوْا إِلَىٰ شَيَاطِينِهِمْ قَالُوا إِنَّا مَعَكُمْ إِنَّمَا نَحْنُ مُسْتَهْزِئُونَ﴾

14.Na wanapokutana na walioamini husema, tumeamini na wanapokuwa peke yao kwa mashetani wao husema: Hakika sisi tu pamoja nanyi tunawacheza shere tu.

﴿اللَّـهُ يَسْتَهْزِئُ بِهِمْ وَيَمُدُّهُمْ فِي طُغْيَانِهِمْ يَعْمَهُونَ﴾

15.Mwenyezi Mungu atawalipa shere yao na kuwaacha katika upotofu wao wakitangatanga ovyo.

﴿أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ اشْتَرَوُا الضَّلَالَةَ بِالْهُدَىٰ فَمَا رَبِحَت تِّجَارَتُهُمْ وَمَا كَانُوا مُهْتَدِينَ ﴾

16.Hao ndio walionunua upotofu kwa uongofu, lakini biashara yao haikupata faida wala hawakuwa ni wenye kuongoka.

﴿مَثَلُهُمْ كَمَثَلِ الَّذِي اسْتَوْقَدَ نَارًا فَلَمَّا أَضَاءَتْ مَا حَوْلَهُ ذَهَبَ اللَّـهُ بِنُورِهِمْ وَتَرَكَهُمْ فِي ظُلُمَاتٍ لَّا يُبْصِرُونَ﴾

17.Mfano wao ni kama mfano wa aliyekoka moto, na ulipoyaangaza yaliyo pambizoni mwake, Mwenyezi Mungu akaondoa nuru yao hiyo na kuwaacha katika kiza hawaoni.

﴿صُمٌّ بُكْمٌ عُمْيٌ فَهُمْ لَا يَرْجِعُونَ ﴾

18.Ni viziwi, mabubu (na) vipofu kwa hivyo hawatarejea.

﴿أَوْ كَصَيِّبٍ مِّنَ السَّمَاءِ فِيهِ ظُلُمَاتٌ وَرَعْدٌ وَبَرْقٌ يَجْعَلُونَ أَصَابِعَهُمْ فِي آذَانِهِم مِّنَ الصَّوَاعِقِ حَذَرَ الْمَوْتِ وَاللَّـهُ مُحِيطٌ بِالْكَافِرِينَ﴾

19.Au ni kama mvua kubwa itokayo mawinguni, ndani yake mkawa na giza na radi na umeme, wakawa wanatia vidole vyao masikioni mwao kwa ajili ya mingurumo, na kuogopa kufa. Na Mwenyezi Mungu amewazunguka hao makafiri.

﴿يَكَادُ الْبَرْقُ يَخْطَفُ أَبْصَارَهُمْ كُلَّمَا أَضَاءَ لَهُم مَّشَوْا فِيهِ وَإِذَا أَظْلَمَ عَلَيْهِمْ قَامُوا وَلَوْ شَاءَ اللَّـهُ لَذَهَبَ بِسَمْعِهِمْ وَأَبْصَارِهِمْ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴾

20.Unakaribia umeme huo kunyakua macho yao, kila unapowaangazia hutembea ndani yake na unapowafanyia giza husimama. Na lau Mwenyezi Mungu angetaka, angeliondoa kusikia kwao na kuona kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ni muweza wa kila kitu.

WANAFIKI

Aya 8 - 20

Kwanza: Mwenyezi Mungu amewataja waumini, hao ni ambao wameifanyia ikhlas haki kwa ndani na nje. Kisha akawataja makafiri ambao wamefanya ukafiri ndani na nje.

Hivi sasa imekuja zamu ya wanafiki ambao wamedhihirisha Imani na kumbe sio waumini; kufuru ya hawa ni chafu zaidi ya ukafiri na ameichukia zaidi Mwenyezi Mungu; ndio maana Mwenyezi Mungu amewataja sana katika Aya kumi na tatu, wakati ambapo amefupiliza kuwataja makafiri katika Aya mbili tu.

Si hivyo tu, bali hata ameteremsha Sura maalum ya wanafiki. Aya hizi ziko wazi kabisa hazihitaji taawili wala ufafanuzi; ni kama Aya inayosema:

﴿فَإِنَّ اللَّـهَ كَانَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمًا ﴾

Hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa kila kitu (33:54).

Kwa hivyo tutatosheka na maelezo haya yanayofuatia:-

NI NANI MNAFIKI?

Kila mmoja wetu anataka awe anatajika katika watu; angalau watu wasimpinge katika mambo yake wala wasimtusi; hasa ikiwa maisha yake na kazi yake inategemea watu watakavyomwamini. Kwa hivyo basi mtu wa namna hii siku zote anakuwa na shaka hata kama halikutokea jambo la kumtilia shaka, ijapokuwa kuna kawaida ya kuchukulia usahihi juu ya kitendo cha Mwislamu.

* 5 Maulama wa kifqh wana kawaida waliyoiita kuchukulia usahihi kitendo cha Mwislamu. Kwa mfano umemwona mtu anakunywa maji na hujui ni ya halali au haramu; au ulijua kuwa ni haramu, ukatia shaka je, anakunywa kwa ajili ya dawa au hajui kama ni haramu au anakunywa tu bila ya udhuru wowote? Basi ni lazima uchukulie usawa tu, mpaka idhihiri kinyume. Kwa vyovyote iwavyo kila anayewaficha watu, na kujidhihirisha na mambo asiyokuwa nayo na akaogopa siri isifichuke, basi huyo ni mwongo, mnafiki, mwenye kujionyesha na mwenye hadaa; hata kama atapata kuaminiwa na watu wote, bali huko kuaminiwa kunazidisha kosa lake na ni balaa mbele za Mwenyezi Mungu na pia ni balaa mbele za watu siku siri ikifichuka.

Unaweza kuuliza, kama watu wakiitakidi kuwa kitu fulani ni haramu na mtu mwengine akaitakidi kati yake na Mwenyezi Mungu kuwa ni halali, akawa anakifanya kwa kujificha kwa kuogopa maneno ya watu je, atahisabiwa ni mnafiki? Je, ni wajibu awabainishie watu yale anayoitakidi? Je atakuwa ana lawama kama akinyamazia makosa yao?

Jibu: Hakuna ubaya wowote wa kufanya lile ambalo mtu anaitakidi kuwa ni halali; wala hawezi kuhesabiwa kuwa ni katika wanafiki maadamu roho yake imetulia.

Kwa sababu taklifa ya jambo hasa inafungamana na yeye sio watu, bali hata anasamehewa katika makosa. Kwani hakuna dhambi katika kufanya jambo kwa makosa bila ya kukusudia. Ama kubainisha uhakika ni wajibu kwake kwa upande wa kuamrisha mema na kukataza mabaya; kwa sababu kosa liko katika hukumu sio katika maudhui. Aya tulizonazo zinazungumzia wanafiki ambao iliwathibitikia hoja na haki ya Utume wa Muhammad(s.a.w.w) lakini walingangania upinzani tu kwa inadi, kama ilivyokuwa kwa washirikina ambao walifanya inadi na wakapigana vita. Tofauti iliyopo kati ya washirikina na wanafiki, ni kwamba washirikina walitangaza upinzani wao na wakasema wazi: Hatuifuati haki kwa sababu mafukara wameifuata Quran inasema:

* 6 Ukimwona mtu anakula nyama ya nguruwe na yeye anajua kuwa ni nyama ya nguruwe, lakini hajui hukumu yake ya haramu, basi yakupasa umwongoze kwenye hukumu ya Mwenyezi Mungu. Hali hiyo ndiyo inayoitwa kutojua hukumu. Ama akiwa anajua hukumu, lakini anaitakidi kwamba nyama hii anayoila ni nyama ya kondoo lakini kumbe ni nguruwe, sio wajibu juu yako kumbainishia, kwa sababu yeye ana udhuru. Wa kwanza huitwa asiyejua hukumu, na wa pili huitwa asiyejuwa maudhui.

﴿قَالُوا أَنُؤْمِنُ لَكَ وَاتَّبَعَكَ الْأَرْذَلُونَ﴾

Wakasema: Je, tukuamini wewe, hali ya kuwa wanyonge ndio wanaokufuata. (26:111)

Ama wanafiki wao waliikataa haki kwa sababu moja au nyingine lakini wao walifanya upinzani wakadhihirisha Uislamu kwa woga na hadaa, wakawa ni wabaya zaidi kuliko makafiri. Kwani makafiri udhahiri wao na undani wao ulikuwa sawa tu, kama vile mlevi anavyokunywa pombe njiani. Lakini wanafiki walificha yale yaliyo katika dhamira zao kama mwovu anayevaa nguo za watakatifu.

Hadaa hiyo inafahamisha kuwa mnafiki hana kizuizi chochote cha dini au akili, wala cha haki au uadilifu; dhamiri yake haishtuki maadamu yuko mbali na macho ya watu. Basi mtu wa namna hii ni vigumu sana kurudia kwenye heri. Kwa hivyo ndio Mwenyezi Mungu amewataja wanafiki katika Aya hizi kwa sifa ya hadaa, kughafilika, maradhi ya moyo na upumbavu. Vile vile kughurika, kufuata matamanio, uchafu na kuendelea na upotevu. Watu wanawaita kwa jina la wapelelezi, vibaraka waharibifu na wenye kujionyesha.

Watu hao wapo hivi sasa; kama walivokuwa wakati wa Mtume na kabla yake, na wataendelea katika vizazi vijavyo. Lakini ni wenye kulaaniwa popote walipo, hata wakiwa makaburini mwao. Kama wakifaulu basi ni kwa muda. Ama kufaulu kwa wakweli kunaendelea. Ibara nzuri niliyoisoma kuhusu wanafiki ni kauli ya Muhyiddini maarufu kwa jina la Ibnul Arabi katika Juzuu ya nne ya kitabu Futuhatil-Makkiyyah. Ni uzuri uliyoje wa aliyoyasema Mwenyezi Mungu: Wanawastahi watu, ambao wana maumbile ya kusahau.Na wala hawamstahi Mwenyezi Mungu ambaye hapotei wala hasahau, afadhali wangelifanya kinyume. Maana ya ibara hiyo ni kwamba lau mnafiki angelikuwa anafikiria vizuri na akawa anafikiria kidogo na kuwa na akili, angelificha makosa yake kwa Mwenyezi Mungu - kama inawezekana - sio kwa watu.Kwa sababu watu hawawezi kumnufaisha wala kumdhuru. Ambaye ananufaisha na kudhuru ni Yeye (Mungu) peke yake. Kwani watu wanasahau uovu wanaouona; watamzungumzia mwenye uovu huo wakati fulani tu baadaye wanasahau na kunyamaza, kama vile hakukutokea kitu chochote. Tumeona wengi waliofanya madhambi makubwa makubwa yakawafedhehesha mpaka mtu akajificha kutokana na ubaya wa vitendo vyake, halafu baadaye mtu akajitokeza kwa watu, wakakaa naye, wakaamiliana naye kama mtu mwema.

Tena pengine wakamtegemea na kumpa cheo kikubwa hata kuweza kusimamia mambo matakatifu ya kidini ambayo hakuyasimamia yeyote isipokuwa Mtume au wasii wake. Mbali ya kuwa watu husahau pia wanasifu na kutusi kulingana na matakwa yao na matamanio. Kwa hiyo, mwenye akili atamwogopa Mwenyezi Mungu wala hataogopa watu, bali atajichunga yeye mwenyewe na kujiepusha na yale anayoyaonea haya. Na hakuna mtu mwoga kama yule anayefanya kwa siri yale anayoyaonea haya kuyafanya dhahiri.