TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
Kundi:

Matembeleo: 35673
Pakua: 3033


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Juzuu 9 Juzuu 10 Juzuu 11
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 20 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 35673 / Pakua: 3033
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA Juzuu 1

Mwandishi:
Swahili

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA KWANZA

AL - BAQARAH (NG’OMBE)

﴿ كَيْفَ تَكْفُرُونَ بِاللَّـهِ وَكُنتُمْ أَمْوَاتًا فَأَحْيَاكُمْ ثُمَّ يُمِيتُكُمْ ثُمَّ يُحْيِيكُمْ ثُمَّ إِلَيْهِ تُرْجَعُونَ﴾

28.Vipi mnamkanusha Mwenyezi Mungu na hali mlikuwa wafu akawafufua! Kisha atawafisha tena atawafufua,kisha kwake mtarejeshwa.

﴿ هُوَ الَّذِي خَلَقَ لَكُم مَّا فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا ثُمَّ اسْتَوَىٰ إِلَى السَّمَاءِ فَسَوَّاهُنَّ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ وَهُوَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴾

29.Yeye ndiye aliwaumbia vyote vilivyomo katika ardhi tena akakusudia kuumba mbingu na akazifanya saba. Naye ni mjuzi wa kila kitu.

MWANADAMU KWA DHATI YAKE NI HOJA

Aya 28 - 29

Vipi mnamkanusha Mwenyezi Mungu!

Kwa dhahiri ya mfumo wa maneno inaonyesha kwamba msemo katika Aya mbili hizi unaelekezwa kwa yule ambaye hanufaiki na chochote katika kupigiwa mfano, lakini ilivyo hasa msemo unamhusu kila anayemkufuru Mwenyezi Mungu pamoja na kuweko dalili hizi zisizokuwa na idadi ambazo ni pamoja na huyo kafiri mkanushaji. Kwani yeye kwa dhati yake ni dalili iliyo wazi ya kupatikana aliyemuumba.

Kama si hivyo ni nani basi aliyemfanya katika nidhamu hii kali kabisa, akakiweka kila kitu mahala pake panapohusika, kuanzia chembe hai za ubongo na moyo mpaka kwenye utumbo na maini, kwenye usikizi na uoni na mpaka kwenye miishilio isiyokuwa na mwisho. Kila kimoja kinatekeleza umuhimu wake kwa uangalifu bila ya usimamizi wowote kutoka kwa kiumbe.

Vile vile ni kutoka wapi umekuja ufahamu huu na akili ambayo mtu analikurubisha lililo mbali, kulisahilisha zito na kukusanya yaliyo katika ardhi katika nyumba moja, kisha akaendelea zaidi na kuweka athari zake mwezini.

Je haya na mengineyo yamekuja kibahati na (kisadfa) tu?Je kuna vitu hasa vinavyoendesha mpangilio huo? Je Sayansi inaweza kujibu hayo? Na je majibu yatatokana na kuhusika na majaribio ya Kisayansi?(14:34)

Walijaribu wenye kujaribu kujibu,lakini yakajitokeza maelfu ya maswali. Sisi hatukanushi kabisa kwamba wataalamu wa kisayansi wamefikilia kwenye ukweli wa kushangaza katika tiba, ukulima na viwanda, lakini wataalamu wa uhai wameambulia patupu wakitafuta siri ya uhai na asili yake; na hawana chochote isipokuwa dhana tu, ambayo haitoshei haki. Kimsingi, kila Sayansi inaposhindwa kutafsiri jambo hulihukumia kwa kinyume chake.

Ikawa kupatikana mtu ni nguvu ya hoja kuhusu kuwapo Mwenyezi Mungu (s.w.t.), inakuaje hoja hii ipinge hoja inayolazimiana nayo? Vipi mtu aliye na fasihi aweze kupinga fikra ya fasihi na balagha? Basi hapo ndio inakuwa siri ya kustaajabisha katika kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

Vipi mnakanusha Mwenyezi Mungu na hali mlikuwa wafu akawafufua.

Yaani ni maajabu yaliyoje ya kumkanusha kwenu Mwenyezi Mungu na hali nyinyi kwa dhati kabisa ni dalili wazi ya kuwepo Mwenyezi Mungu. Vyovyote mtakavyokanusha, je, mnaweza kukanusha kwamba nyinyi hamkuwa kitu chochote kisha ndipo mkawa kitu kinachosikia, kuona, kuhisi na kutambua, pamoja na kusema na kutenda? Je,hiyo si dalili inayoeleza kupatikana nguvu iliyoumba?

Kweli kabisa.Hakika binaadamu ni dhalimu mkubwa mwenye kukanusha mno! Hakukuwa kumkanusha Mwenyezi Mungu isipokuwa ni kukanusha na kutojijua huyo mkanushaji.11 Na asiyejijua, basi ndio hamjui mwingine. Kwa hali hiyo ndiyo tunapata tafsiri ya hadith tukufu: Anayejijua zaidi ni yule anayemjua zaidi Mola wake. Unaweza kuuliza: Ni akili gani inayoweza kujikanusha yenyewe?Je hayo yanaingia akilini? Tunajibu: Hakika hoja inalazimiana na chenye kutolewa hoja; na kukanusha ulazima kunapelekea kukanusha chenye kulazimiwa. Kwa hivyo mwenye kukanu-sha dalili ya matamko, kwa mfano, kutokana na maana iliyowekwa, atakuwa ameyakanusha matamko yenyewe atake asitake, wala hakumfalii yeye kuyakubali wakati anakanusha dalili zake.

Hivi ndivyo ilivyo kwa mwenye kumka-nusha Mwenyezi Mungu. Kwani kuwapo kwake ni dalili ya kuwapo muumbaji, na kupatikana muumbaji kunatolewa dalili na kupatikana kwake yeye mkanushaji. Basi akikanusha chenye kutolewa dalili ndio amekanusha dalili yenyewe, ambayo ndiyo huyo mkanushaji kwa dhati yake bila ya kujijua wala kujitambua. Hivyo ndivyo anavyofanya mjinga anayejiepusha na maumbile anayoishi nayo na kumpa uhai, kupinga dalili zilizo wazi na kuamini vigano na mambo ya kijinga.

MAUTI NA UHAI MARA MBILI

Makusudio ya kufa kwa kwanza kunak-oonyesha na neno Mlikuwa wafu ni kutokuwapo kwa mara ya kwanza, Na makusudio ya uhai wa kwanza, Akawafufua ni kuumbwa baada ya kutokuwapo.

* 11 Anasema Charlie Champlin, mchezaji sinema mashuhuri wa kimataifa, ambaye umashuhuri wake umezidi ule wa Gandi: Katika mamlaka isiyojulikana kuna nguvu isiyokuwa na mpaka. Na anasema Kierkegaard Hakika Mwenyezi Mungu anajitokeza kwenye nafsi yenye kukata tamaa katika wakati mgumu wa kukata tamaa na katika lindi la makosa. Mauti ya pili, Kisha atawaua, ni mauti haya yaliyozoeleka; na kufufuliwa mara ya pili ni kufufuliwa kwa ajili ya hisabu na malipo.

TENA ATAWAFUFUA

Unaweza kuuliza, je roho inafarikiana na mwili baada ya kwisha nguvu zake za uhai, kwa namna ambayo lau nguvu zingebakia, basi roho ingelibaki na bina -damu milele? Au ni kwamba inawezekana roho kufarikiana na mwili hata ukiwa na nguvu za kuishi kwa ukamilifu bila ya kutokea uharibifu wowote mwilini? Jibu: Watu wa kimaada wamechukulia kauli ya kwanza na wengine wamechukulia kauli ya pili. Ama kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

﴿ فَإِذَا جَاءَ أَجَلُهُمْ لَا يَسْتَأْخِرُونَ سَاعَةً﴾

...Utakapofika muda wao hawatakawia (hata) saa moja wala hawatatangulia (7:34)

Inaweza kuchukuwa njia zote mbili. Kwani haikubainisha sababu ya kufika muda wao.Je ni kuharibika mwili au ni kitu kingine. Kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿ الَّذِينَ خَرَجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَهُمْ أُلُوفٌ حَذَرَ الْمَوْتِ فَقَالَ لَهُمُ اللَّـهُ مُوتُوا﴾

...ambao walitoka katika majumba yao nao walikuwa maelfu wakiogopa mauti? Mwenyezi Mungu akawaambia Kufeni (2:243)

Na kauli yake:

﴿قَالَ أَنَّىٰ يُحْيِي هَـٰذِهِ اللَّـهُ بَعْدَ مَوْتِهَا فَأَمَاتَهُ اللَّـهُ مِائَةَ عَامٍ﴾

Akasema: Mwenyezi Mungu atuuhuisha vipi (mji) huu baada ya kufa kwake? Basi Mwenyezi Mungu alimfisha kwa miaka mia... (2:259)

Aya mbili hizo zinahusu matukio fulani tu.Haziingii katika matukio mingine.

Vyovyote iwavyo hatuna kitu kinachotuthibitishia, lakini tunayoshuhudia ni kwamba watu wengi wanafikiwa na mauti nao bado wabichi wakiwa na afya nzuri na kwamba wengi wanatembea na kufurahi nao wako katika umri mkubwa na magonjwa tele. Madaktari wengi mahodari wanamwambia mgonjwa utakufa baada ya saa chache tu, lakini akaishi muda mrefu!

UFUFUO

Ufufuo katika Uislamu ni msingi wa tatu baada ya Tawhid na Utume, misingi ambayo tumeshaielezea. Mwenyezi Mungu ameyatolea habari marejeo (ufufuo) aliposema:

﴿ ثُمَّ يُحْيِيكُمْ ثُمَّ إِلَيْهِ تُرْجَعُونَ﴾

Kisha atawafufua kisha kwake mtarejeshwa.

Ametoa dalili au kuukurubisha uwezekano wa ufufuo katika Aya nyingi. Miongoni mwazo ni:

﴿أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّ اللَّـهَ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَلَمْ يَعْيَ بِخَلْقِهِنَّ بِقَادِرٍ عَلَىٰ أَن يُحْيِيَ الْمَوْتَىٰ﴾

Je! hawaoni kwamba Mwenyezi Mungu aliyeziumba mbingu na ardhi na hakuchoka kwa kuziumba, ana uwezo wa kuwafufua wafu? (46:33)

﴿يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِن كُنتُمْ فِي رَيْبٍ مِّنَ الْبَعْثِ فَإِنَّا خَلَقْنَاكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ مِنْ عَلَقَةٍ ﴾

Enyi watu! Kama mmo katika shaka juu ya ufufuo, basi kwa hakika tuliwaumba kutokana na udongo, kisha kutokana na manii, kisha kutokana na kipande cha damu... (22:5)

Hakuna anayetia shaka kwamba Mwenye kuumba kitu huwa rahisi kwake kuvikusanya viungo vyake baada ya kuwa mbali mbali; bali kukusanya ni rahisi zaidi kuliko kuumba tena. Mwenye kujenga jumba kubwa ni rahisi kwake kujenga kibanda.12

Ninacho kitabu maalum nilichoandika cha maudhui haya kinachoitwa Alakhira wal aql kisha nikayalinganisha na kitabu Al-Islam wal aql ambavyo vimechapishwa mara nyingi sana.

YALIYO KATIKA ARDHI

Baada ya Mwenyezi Mungu kumkumbusha mtu neema ya kupatikana kwake, anamtajia wingi wa neema alizonazo, ikiwa ni pamoja na kula na kunywa, mavazi, vipando, mandhari na mengineyo katika starehe za ardhi na heri zake zisizohisabika. Wametoa dalili mafakihi kwa kauli ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

﴿ هُوَ الَّذِي خَلَقَ لَكُم مَّا فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا ث﴾

Yeye ndiye aliyewaumbia vyote vilivyo katika ardhi.

Kwamba vitu vyote kabla ya kuja sharia ni halali, na kwamba haimfailii kiumbe kuharamisha kitu isipokuwa kwa dalili. Mwenyezi Mungu anasema:

*12 Mnamo mwaka 1959 Mustafa Mahmud, Mmisri, alitunga kitabu Allahu Wal-insan (Mungu na mtu) katika kitabu hicho alikana Mungu na ufufuo, nami nikamjibu kwa kutunga kitabu Allahu wal-Aqli (Mungu na Akili) mpaka sasa kimechapishwa mara tano. Ilipofika tarehe 10.4.1967 nilimsomeya makala Mustafa Mahmud katika jarida la Ruz Al-Yusuf, inayosema: Imani yangu inashikilia kwamba mimi nilikuwako kabla ya maisha yangu haya kwa jina jingine, na kwamba mimi sitaisha baada ya kufa kwangu isipokuwa nitarudi kwenye uhai kwa namna nyingine, na maisha yanaendelea.

﴿قُلْ أَرَأَيْتُم مَّا أَنزَلَ اللَّـهُ لَكُم مِّن رِّزْقٍ فَجَعَلْتُم مِّنْهُ حَرَامًا وَحَلَالًا قُلْ آللَّـهُ أَذِنَ لَكُمْ أَمْ عَلَى اللَّـهِ تَفْتَرُونَ﴾

Sema: Je, mnaonaje zile riziki alizowateremshia Mwenyezi Mungu kisha mkafanya katika hizo (kuwa) haram na (nyingine) halali. Sema, Je, Mwenyezi Mungu amewaruhusu au mnamzulia Mwenyezi Mungu tu? (10:59)

Pengine hutolewa dalili kwa Aya hii kwamba ardhi haimilikiwi. Kinachofaa kumilikiwa ni kile kinachozalishwa na ardhi. Kwa sababu Mwenyezi Mungu anasema: Amewaumbia vilivyomo ardhini na hakusema amewaumbia ardhi.

MBINGU SABA

Maana ya neno istawa hapa ni kukusudia. Kuzihusisha mbingu saba hakufahamishi kuwa ndio hizo hizo tu wala hakukanushi kabisa kuwapo nyinginezo. Wamethibitisha wanavyuoni wa elimu ya usul na lugha kwamba idadi sio ufahamisho, mwenye kusema mimi ninamiliki vitabu saba haimaanishi kwamba hamiliki vingine. Analitilia nguvu hilo Mwenyezi Mungu (s.w.t.) alipomwambia Mtume wake(s.a.w.w) :

﴿إِن تَسْتَغْفِرْ لَهُمْ سَبْعِينَ مَرَّةً فَلَن يَغْفِرَ اللَّـهُ لَهُمْ﴾

Hata ukiwaombea msamaha mara sabini, Mwenyezi Mungu hatawasamehe. (9:80)

Mtume(s.a.w.w) akasema:Lau ningelijua kuwa Mwenyezi Mungu atawasamehe nikizidisha sabini ningelifanya. Huenda ikawa sababu ya kutaja saba ni kwamba hizo saba zina mambo maalum yasiyopatikana katika mbingu nyingine.

﴿ وَإِذْ قَالَ رَبُّكَ لِلْمَلَائِكَةِ إِنِّي جَاعِلٌ فِي الْأَرْضِ خَلِيفَةً قَالُوا أَتَجْعَلُ فِيهَا مَن يُفْسِدُ فِيهَا وَيَسْفِكُ الدِّمَاءَ وَنَحْنُ نُسَبِّحُ بِحَمْدِكَ وَنُقَدِّسُ لَكَ قَالَ إِنِّي أَعْلَمُ مَا لَا تَعْلَمُونَ ﴾

30. Na Mola wako alipowaambia Malaika mimi nitaweka Khalifa katika ardhi. Wakasema (Malaika) utaweka humo watakaofanya uharibifu humo na kumwaga damu, hali sisi tunakutakasa kwa sifa zako na kukutaja kwa utakatifu wako? Akasema Mwenyezi Mungu: Hakika mimi nayajua msiyoyajua.

﴿ وَعَلَّمَ آدَمَ الْأَسْمَاءَ كُلَّهَا ثُمَّ عَرَضَهُمْ عَلَى الْمَلَائِكَةِ فَقَالَ أَنبِئُونِي بِأَسْمَاءِ هَـٰؤُلَاءِ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴾

31.Na akamfundisha Adam majina ya vitu vyote, kisha akaviweka mbele ya Malaika akasema: Niambieni majina ya vitu hivi ikiwa mnasema kweli.

﴿ قَالُوا سُبْحَانَكَ لَا عِلْمَ لَنَا إِلَّا مَا عَلَّمْتَنَا إِنَّكَ أَنتَ الْعَلِيمُ الْحَكِيمُ ﴾

32.Wakasema: Utakatifu ni wako hatuna elimu isipokuwa ile uliyotufundisha; hakika wewe ndiwe mjuzi, mwenye hekima.

﴿ قَالَ يَا آدَمُ أَنبِئْهُم بِأَسْمَائِهِمْ فَلَمَّا أَنبَأَهُم بِأَسْمَائِهِمْ قَالَ أَلَمْ أَقُل لَّكُمْ إِنِّي أَعْلَمُ غَيْبَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَأَعْلَمُ مَا تُبْدُونَ وَمَا كُنتُمْ تَكْتُمُونَ ﴾

33.Akasema: Ewe Adam waambie majina yake. Alipowaambia majina yake. Alisema (Mwenyezi Mungu): Sikuwaambia kwamba mimi ninajua siri za mbinguni na za ardhini; tena najua mnayoyadhihirisha na mliyokuwa mkiyaficha.

MOLAWAKO ALIPOWAAMBIA MALAIKA

Aya 30 - 33

MAKUSUDIO YA MAJINA

Makusudio ya majina katika kauli yake Mwenyezi Mungu: Na Mwenyezi Mungu akamfundisha Adam majina ya (vitu) vyote, ni: maana ya majina, nayo ni ya vitu vya ulimwengu na sifa zake. Mwenye Majmaul-Bayan anasema: Hakika majina bila ya maana hayana faida wala kuonyesha ubora wake. Imam Sadiq(a.s) Aliulizwa kuhusu hayo majina akasema:Ni milima na mabonde. Kisha akaonyesha busati lililokuwa chini yake akasema: Hili ni miongoni mwayo, yaani kila kitu mpaka busati hili pia.

MALAIKA

Hakuna njia ya kuwajua Malaika na hakika yao kwa hisia na majaribio wala kwa akili na kukisia au kwa kitu chochote isipokuwa kwa njia ya wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kupitia midomoni mwa Mitume yake. Mwenye kukanusha wahyi kimsingi haifai kumzungumzia habari ya Malaika kwa hali yoyote. Kwa sababu wao ni tawi na wahyi ni asili (shina). Ikiwa hapana budi kulumbana naye basi ni lazima iwe ni kuhusu fikra ya wahyi na kuswihi kwake tu.

Hapa hatukusudii kulumbana na anayekanusha wahyi, kwa vile tumekwishafafanua; isipokuwa tunamwambia yule mwenye kukanusha: Si haki kulazimisha rai yako juu ya yule mwenye kuamini wahyi; kama si hivyo basi ingelijuzu kwake kulazimisha rai yake kwako. Kama ukimwambia mwenye kuamini wahyi kuwa imani yake ni batili kwa vile yeye hategemei majaribio, atakujibu kwamba kuamini kwako kuwa wahyi ni batili vilevile hakukutegemea kwenye majaribio, kwa sababu kukanusha kwako na uthibitisho wa mwenye kuamini, maudhui yake ni mamoja, nayo ni wahyi.Ikiwa majaribio, hayathibitishi wahyi pia hayaukanushi.

Kwa maneno mengine kuamini kutokuwepo ghaibu ni sawa na kuamini kuwepo, yote mawili ni ghaibu katika ghaibu. Kimsingi ni kwamba ghaibu haifai kuipinga kwa ghaibu. Sartre, mwandishi na mwanafalsafa mashuhuri wa Kifaransa akiwajibu wanaoamini maada alisema: Nyinyi mnapokanusha kuwepo Mwenyezi Mungu ndio mnafafanua ghaibu kwa ukamilifu, kama wanaoamini mifano ambao wanakubali kuwepo kwa Mwenyezi Mungu. Hakika yakini ya kimaada ya kukanusha ghaibu, inategemea dalili ile ile anayoitegemea mwenye kuamini kuswihi ghaibu.Kwa hivyo basi imebainika kwamba imani ya kimaada inajipinga yenyewe.

KHALIFA

Makusudio ya Khalifa katika Aya ni Adam, baba wa watu na kila mtu aliyeko na atakayekuwako katika kizazi chake wakati wowote na mahali popote. Wajihi wa kumwita Khalifa ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) alimpa nafasi ya kuchukua hatamu za uongozi wa ardhi hii na kutafuta yaliyomo ndani yake miongoni mwa nguvu na manufaa na kufaidika nayo. Katika kauli ya Malaika:

* 13 Angalia kifungu cha Sartre na madhehebu ya kimaada katika kitabu chetu Falsafatul- Mabdai Wal-Maad, tulichokitunga kuwajibu wenye Falsafa ya kimaada. Utaweka humo watakaofanya uharibifu na kumwaga damu. Inaonyesha kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) aliwafahamisha Malaika kwa njia fulani kabla ya kumuumba Adam, kwamba lau binadamu atakuwa katika ardhi hii angeliasi kwa ufisadi na kumwaga damu. Kutokana na hali hiyo ndio wakaona ajabu vipi Mwenyezi Mungu amlete ambaye atamuasi na wao wanamtukuza kwa sifa zake na kumtaja kwa utakatifu wake? Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akawabainishia hekima ya kuumbwa mtu na kwamba huko ni kuandaa kujulisha lile wasilolijua na uharibifu wake katika ardhi hauwezi kuondoa faida ya kupatikana kwake. Hapo Malaika wakatosheka na wakatii.

Kwa hivyo Mwenyezi Mungu Mtukufu hakumuumba mwanaadamu ili afanye maasi na maovu, bali amemuumba kwa ajili ya elimu na amali yenye manufaa na akamkataza ufisadi na madhara. Akikhalifu na kuasi basi huadhibiwa kadri anavyostahiki. Aya hii inafahamisha kwamba elimu na yanayoambatana nayo, ina cheo kikubwa mbele za Mwenyezi Mungu na Malaika wake, kwa sababu Mwenyezi Mungu amefanya bora kumuumba mtu kwa ajili ya elimu na maarifa na alipowaonyesha hilo, Malaika walitoa udhuru kwa kusema: Utakatifu ni wako hatuna elimu isipokuwa ile uliyotufundisha. Ikiwa lengo la kuumbwa mtu ni elimu na amali, basi mwenye kuiacha atakuwa ameivunja hekima ya kuwepo.

Naogopa kusema kuwa lau Malaika wakati huo wangejua athari ya mabomu ya kitonoradi (Nuclear) na mabomu ya sumu (Napalm) waliyotumia Wamarekani huko Vietnam, basi wasingelikinai kabisa...

*14 Inasemekana kuwa katika ardhi walikuwepo watu kabla ya Adam wetu, na kwamba wao walifanya uharibifu kisha wakaangamia wote na Malaika walikuwa wakilijua hilo.Namuomba msamaha Mwenyezi Mungu ambaye anajua vile tusivyovijua sisi wenyewe.

SOMO WAZI

Somo ambalo ni lazima tufaidike nalo katika majibizano ya Mwenyezi Mungu na Malaika wake, ni kwamba mtu, vyovyote atakavyofikia katika elimu, nguvu na ukubwa, hawezi kuepuka kufanyiwa majibizano, malumbano na kushauriwa. Mwenyezi Mungu mwenyewe tu aliye mtukufu alitoa nafasi kwa Malaika ajadiliane nao na kujibizana ambako kunafanana na upinzani; na wao hawakujizuia na hilo, bali walijitia ushujaa wa elimu.

Mwenyezi Mungu akawachukulia upole katika kuwajibu na kuwabainishia dalili kwa upole wakakubali kwa kuridhia na kukinai, sio kwa kukemewa. Pia Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akafungua mlango wa majibizano pamoja na Iblis mwenye laana ambaye alijibizana naye kwa kusema: Umeniumba kwa moto na yeye umemuumba kwa udongo..., kama yatakavyokuja maelezo.

Basi ni juu ya wale wanaojiona kuwa hawawezi kupingwa wachukue faida ya somo hili la wazi. Wakijitoa na kujibiwa watakuwa wanajifanya juu zaidi ya Mwenyezi Mungu, bila ya kujua. Anasema Amirul Muminin Ali(a.s) :Msinich-anganye na watu wenye kujifanya wala msinidhanie kuwa nitaona uzito kwa haki niliyoambiwa wala kujifanya mkubwa. Kwani mwenye kuona uzito wa haki anayoambiwa au uadilifu atakaoonyeshwa, basi kuyafanya hayo mawili itakuwa uzito zaidi kwake. Msijizuwie na haki iliyosemwa au ushauri wa uadilifu. (Nahjul-Balagha, Khutba Na. 213).