TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA PILI Juzuu 2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA PILI16%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA PILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 16 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 21649 / Pakua: 4884
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA PILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA PILI Juzuu 2

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London. Kama lilivyo jina la Tafsiri yenyewe ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo. Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati. Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kungangania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea, hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh alaa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine. Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasyansi kama kina Enstein, Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa. Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure, lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

MWISHO

Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji. Mchapishaji

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa. Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa. Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya Msahafu Mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswatu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146). Imeandikwa La Yaalamuun,(hawajui) badala ya Yaalamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile. Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu jabal amail Makosa ya chapa. Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idaha balagha arbai na sanah badala ya: Hattaidaha balagha ashuddahu arbai na sanah Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana. Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa, kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin)

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿سَيَقُولُ السُّفَهَاءُ مِنَ النَّاسِ مَا وَلَّاهُمْ عَن قِبْلَتِهِمُ الَّتِي كَانُوا عَلَيْهَا قُل لِّلَّـهِ الْمَشْرِقُ وَالْمَغْرِبُ يَهْدِي مَن يَشَاءُ إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ ﴾

142.Watasema wapumbavu miongoni mwa watu: Nini kilichowageuza kutoka Qibla chao walichokuwa wakikielelekea? Sema: Mashariki na Magharibi ni ya Mwenyezi Mungu, Humwongoza amtakaye kwenye njia iliyonyooka.

﴿وَكَذَٰلِكَ جَعَلْنَاكُمْ أُمَّةً وَسَطًا لِّتَكُونُوا شُهَدَاءَ عَلَى النَّاسِ وَيَكُونَ الرَّسُولُ عَلَيْكُمْ شَهِيدًا وَمَا جَعَلْنَا الْقِبْلَةَ الَّتِي كُنتَ عَلَيْهَا إِلَّا لِنَعْلَمَ مَن يَتَّبِعُ الرَّسُولَ مِمَّن يَنقَلِبُ عَلَىٰ عَقِبَيْهِ وَإِن كَانَتْ لَكَبِيرَةً إِلَّا عَلَى الَّذِينَ هَدَى اللَّـهُ وَمَا كَانَ اللَّـهُ لِيُضِيعَ إِيمَانَكُمْ إِنَّ اللَّـهَ بِالنَّاسِ لَرَءُوفٌ رَّحِيمٌ﴾

143. Na kama hivyo hivyo tumewafanya kuwa umma wa wastani, ili muwe mashahidi juu ya watu wote, na Mtume awe shahidi juu yenu. Na hatukukifanya Qibla ulichokuwa nacho ila tupate kumjua yule anayemfuata Mtume na yule atakayegeuka akarudi nyuma. Na kwa hakika lilikuwa ni jambo gumu isipokuwa kwa wale aliowaongoza Mwenyezi Mungu. Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwapotezea imani yenu. Hakika Mwenyezi Mungu kwa watu ni Mpole Mwenye kurehemu.

NINI KILICHOWAGEUZA KUTOKA QIBLA CHAO?

Aya 142

LUGHA

Amesema Ibnul Arabi katika tafsiri yake: Kila asiyejua hakika ya Dini ya Kiislamu huyo ni mpumbavu, kwa sababu yeye ana akili hafifu.

Neno: Qibla limechukuliwa kutoka katika neno Istqbal (kuelekea); yaani kila upande anaoulekea mtu.

MAANA

Watasema wapumbavu miongoni mwa watu: Nini kilichowageuza kutoka Qibla chao walichokuwa wakikielekea?

Mitume waliotangulia walikuwa wakiswali kuelekea Baitul Maqdis.Na Mtume Muhammad(s.a.w.w) alikuwa akitamani lau Qibla kinageuzwa kuwa Al-Kaaba. Mwenyezi Mungu aliyathibitisha matamanio yake, kama itakavyoelezwa.

MAKUSUDIO YA WAPUMBAVU

Makusudio ya wapumbavu hapa ni Mayahudi, ndio waliowalaumu Waislamu kwa kuacha kwao kuelekea BaitulMaqdis.

MAANA YA TAMKO SAYAQULU (WATASEMA)

Tamko Sayaqulu (Watasema) kwa dhahiri linafahamisha kuwa: Mwenyezi Mungu alimfahamisha Mtume wake Mtukufu kauli ya wajinga kabla ya kutokea. Ama yule anayesema kuwa neno Sayaqulu ingawaje kwa dhahiri linafahamisha muda wa mbele, lakini makusudio ni muda uliopita; na kwamba Mwenyezi Mungu alimwambia Mtume wake baada ya kusema wajinga, sio kabla ya kusema; na kwamba limekuja kwa muda ujao, kwa vile yaliyosemwa yalikuwa yamekwisha kadiriwa, ama kwa hakika kauli hii ni kujaribu kutoa tafsir nyingine (Taawil) bila ya dharura yoyote na bila ya dalili yoyote inayofahamisha hilo.

Kwa vyovyote ilivyo ni kwamba: Mwenyezi Mungu (s.w.t.) alimwamrisha Mtume wake Mtukufu Muhammad(s.a.w.w) kuwajibu wajinga hawa kwamba:Mashariki na Magharibi ni ya Mwenyezi Mungu; humwongoza amtakaye katika njia iliyonyooka . Yaani pande zote ni za Mwenyezi Mungu: Al-Kaaba na Baitul Maqdis ni sawa tu, lakini kwa hekima na masilahi mara nyingine humwongoza anayemtaka kwenye Baitul-Maqdis na mara nyingine kwenye Al-Kaaba.

KWA NINI KUSWALI UPANDE MAALUM?

Hili ni swali wanaloliuliza watu wengi kwa nini swala ni wajibu kwenye upande malum na haiswihi isipokuwa upande huo? Na hali yeye amekwisha sema waziwazi:

﴿ فَأَيْنَمَا تُوَلُّوا فَثَمَّ وَجْهُ اللَّـهِ﴾

Na popote mnakoelekea (mtazikuta) radhi za Mwenyezi Mungu (2:115)

Jibu :Kwanza : Mwenyezi Mungu s.w.t. amesema:

﴿ فَوَلِّ وَجْهَكَ شَطْرَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَحَيْثُ مَا كُنتُمْ فَوَلُّوا وُجُوهَكُمْ شَطْرَهُ﴾

...Na elekeza uso wako upande wa msikiti Mtakatifu (Al-Kaaba); na popote mlipo zielekezeni nyuso zenu upande huo... (2:144).

Aya hii ni ubainifu na Tafsir ya Aya 115 na makusudio yake ni kuelekea kwenye upande wowote katika swala ya Sunna na katika swala ya asiyejua Qibla kiko wapi. Makusudio ya Aya 144 ni kuelekea (Al-Kaaba) katika swala ya wajibu. Umekwishatangulia ufafanuzi wa hilo katika Aya 115.

Pili : kuswali swala kunategemea amri ya Mwenyezi Mungu. Kutokana na asili hii hapana budi tuangalie: Je inawezekana tuswali upande wowote tunaoutaka sisi au kwenye upande maalum. Ikiwa kauli ya kwanza ni sawa, basi itakuwa haiswihi swala isipokuwa kwenye upande ulioamrishwa tu; ni sawa iwe ni Al-Kaaba au Baitul-Maqdis au mahali pengine. Pia ifahamike kwamba kufuata amri ni jambo jengine na kuweko radhi za Mwenyezi Mungu kila upande ni jambo jengine. Hakika ibada ni katika mambo yanayongoja ubainifu wa Mwenyezi Mungu kupitia kwa Mtume wake, wala hakuna nafasi ya dhana na uwezekano; isipokuwa kwa kauli sahihi iliyo wazi. Na Mwenyezi Mungu aliaamrisha Waislamu kuswali kuelekea Baitul-Maqdis kwanza; lau wangeliswali kuelekea Al-Kaaba isingekubaliwa swala yao. Kisha Mwenyezi Mungu akawaamrisha kugeuka Al-Kaaba lau wangeling’ang’ania Baitul-Maqdis basi isingekubaliwa swala yao; pamoja na kuwa pande zote mbili ni za Mwenyezi Mungu. Hilo ni kwa sababu kipimo cha kusihi swala ni kuafikiana na sharti zote; kama vile ambavyo kuharibika swala ni kuhalifu amri.

UMMA WA WASTANI

Aya ya 143

LUGHA

Neno: Wast lina maana ya kati kati, na neno Wasat lina maana ya ubora, Mtume anasema:Bora ya mambo ni wastani. Linakuja neno wasata, Kwa maana ya kulingana sawa (wastani). Neno wastani na ubora yanakurubiana. Makusudio ya Wasat hapa ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ameijaalia dini ya Waislamu ni ya wastani; yaani ni ya kati na kati katika itikadi na maadili. Kwa upande wa itikadi hakuna ushirikina wala ulahidi, bali ni Tawhid tu, na kwa upande wa maadili sio ya kimaada wala kiroho, bali ni pande zote mbili kwa sharti ya kulingana sawa na kukamilika. Neno kurudi nyuma ni istiara yaani kueleza mtu anayemkufuru Mwenyezi Mungu na Mtume wake; Kwa sababu mwenye kuacha imani yake yuko katika daraja ya asiyeendelea mbele.

MAANA

Tumewafanya kuwa umma wa wastani . Jumla hii ni ubainifu wa kauli ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

Humwongoza amtakaye kwenye njia iliyonyooka . (2:213).

Njia ya kubainisha hayo ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amewaneemesha wafuasi wa Muhammad(s.a.w.w) kwa uongofu. Linalodhihirisha zaidi uongofu huu ni kuwa Yeye amewajaalia wao kuwa katikati; yaani hawakuzidisha, kama vile kuwazidisha waungu, wala hawakupunguza; kama vile ulahidi (kumkana Mungu). Hayo ni upande wa kiitikadi. Ama upande wa kimadili wastani wake ni, kwa kuwa amewachanganyia mambo ya kiroho na ya kimwili katika mafunzo yake na maelekezo yake - sio ubahili wa kiroho wala ubadhirifu wa kimaada, bali kuna uwiano kati yao.

Baadhi wameifanya kauli hii ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: Tumewajaalia ni umma wa wastani, kuwa ni dalili ya hoja ya Ijmai. Lakini hiyo ni kutoa dalili mahali pasipokuwa pake. Kwa sababu haikuja kubainisha Ijmai, kwamba ni hoja au sio hoja. Wengine wamesema kwamba kauli hii ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.) inafahamisha kuwa kila Mwislamu ni mwadilifu kwa tabia. Hii pia nayo ni batil kabisa. Kwa sababu uadilifu hauthibiti isipokuwa kwa kujua au kwa ushahidi.

UKAMILIFU NA UWIANO KATIKA UISLAMU

Binadamu ni mwili uliotokana na mchanga unaokwisha na ni roho inayodumu inayotokana na siri ya Mwenyezi Mungu, kama alivyosema:

﴿ وَيَسْأَلُونَكَ عَنِ الرُّوحِ قُلِ الرُّوحُ مِنْ أَمْرِ رَبِّي ﴾

Na wanakuuliza kuhusu roho, Sema: Roho ni katika mambo ya mola wangu. (17:85).

Kwa vile vitu viwili hivyo (mwili na roho) vina mahitaji na matakwa ndipo ikaletwa sharia ya Kiislamu kwa ajili ya kutoa maelekezo ya msingi na nidhamu ili visizidiane. Kwa maneno mengine binadamu ni sehemu mbili, kupuuza moja wapo ni kumpuuza binadamu mwenyewe. Uislamu umekataza utawa na kuiepusha nafsi na maumbile ya kawaida, kama ambavyo umehalalisha starehe za maisha, kama kula, kuvaa vizuri nk. Atakayeziangalia Aya za Quran atakuta kwamba dunia yote imeumbwa kwa ajili ya uhai wa mtu kwa namna inayokubalika kwa wote, lakini wakati huo huo kuipupia kuifanyia hiyana na kuwazuia watu wengine na hiyo dunia ni ufisadi na hatari kwa usalama wa jamii. Riziki bora kabisa katika Uislamu ni ile iliyotolewa jasho.

Anas anasema: Siku moja tulikuwa na Mtume(s.a.w.w) safarini wengine wakawa wamefunga na wengine hawakufunga. Tukashuka sehemu fulani ilikuwa ni wakati wa joto. Basi waliofunga wakaanguka wote,ikawa wasiofunga wanawahudumia waliofunga. Mtume(s.a.w.w) akasema:Wasiofunga leo wamechukua malipo yote . Huu ndio msingi wa uwiano katika Uislamu. Sio ibada itayozuia kuhangaika wala sio ulafi utakayozuia kumwabudu Mwenyezi Mungu.

Ili muwe mashahidi juu ya watu na Mtume awe shahidi juu yenu.

Maana ya matamko haya yako wazi na maana ya kiujumla pia iko wazi. Lakini tatizo liko kwenye kuelezea sisi Waislamu ni mashahidi juu ya akina nani? Mtume(s.a.w.w) atakuwa shahidi kesho dhidi ya yule aliyehalifu miongoni mwetu, je sisi tutakuwa mashahidi dhidi ya wasiokuwa Waislamu ambao wamehalifu Kitabu na Sunna? Kauli zimekuwa nyingi na kugongana juu ya hilo; nami sikupata ya kunituliza. Nionavyo mimi ni kwamba Ulama wa Kislamu wanawajibu wa kuufikisha ujumbe wa Muhammad(s.a.w.w) kwa watu wawe ni Waislamu au si Waislamu wasiojua au wawe wanajua. Mwenye kutekeleza wajib huu Mtukufu, basi atakuwa shahidi dhidi ya yule aliyemfikishia kuwa hakuyatumia mafunzo. Na, atakayepuuza wajib huu na asiufikishe, basi

Muhammad(s.a.w.w) atakuwa shahidi dhidi yake kesho mbele ya Mwenyezi Mungu kwamba yeye amefanya hiyana. Kwa ufafanuzi zaidi tupige mfano huu: Mtu ana mali na mtoto mdogo, alipohisi kifo chake kiko karibu akamuusia mtu anaye mtegemea kwa dini yake amlee mtoto wake kutokana na mali atakayoiacha. Akitekeleza yule aliyeusiwa na mtoto akafaulu, basi nisawa, lakini mtoto akifanya uasi na akakataa mfunzo, basi aliyeusiwa atakuwa shahidi dhidi ya mtoto na kama aliyeusiwa ndiye aliyezembea, basi mzazi atakuwa shahidi dhidi ya aliyeusiwa. Vilevile sisi Ulama tuna majukumu makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu ya kufikisha mwito wa Kiislamu kwa watu wenye dini mbali mbali kwa hekima na mawaidha mazuri. Na atakayezembea wajib huu kesho atashuhudiwa na bwana wa viumbe na atahukumiwa. Hii ni ikiwa amepuuza, sikwambii ikiwa yeye ndiye sababu ya kupatikana shaka katika watu wake?

Na hatukukifanya Qibla ulichokuwa nacho ila tupate kumjua yule anayemfuata Mtume na yule atakayegeuka akarudi nyuma.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumwamrisha Mtume wake kugeuza Qibla baadhi ya watu walianza kutia shaka na kusema: mara huku na kesho kule. Na Mayahudi nao wakachukua fursa ya kuwatia shaka wajinga kuhusu Mtume. Hao Mayahudi walikuwa wamekuwa na wataendelea kuwa ni watu wa fitina na uvunjaji; wenye vitimbi na hadaha. Wanatengeneza matatizo na kumwekea vikwazo kila mwenye Ikhlas na wanajaribu kuzigeuza jamii kuzipeleka kwenye matatizo. Ndio tabia na maumbile yao. Ndivyo ilivyo, mara nyingi maadui wa haki wanawatumia wadhaifu wa akili na kuwafanya ni chombo cha kufanya vitimbi, uharibifu na vurugu. Imam Ali amewaelezea kwa ufasaha zaidi aliposema: Ni wanyama wasiokuwa na mchungaji wanamfuata kila atakayewapigia kelele ni (bendera) wanafuata upepo, hawakupata mwanga wa elimu wala hawana cha kutegemea. Mwenyezi Mungu alimpa habari Mtume wake Mtukufu kwamba wale wanaotia shaka si waumini halisi na tumewapatia mtihani huu ili ufichuke ukweli kwako na kwa wengine.

Na kwa hakika lilikuwa ni jambo gumu, ispokuwa kwa wale aliowaongoza Mwenyezi Mungu.

Ambao ni wenye imani halisi sio imani ya kuazima. Unaweza kuuliza: Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anajua kila kitu kabla ya kutokea, sasa kuna wajihi gani kusema: ili tumjue anayemfuata Mtume?

Jibu : Lengo hapa ni kumdhihirisha mtiifu na asiyekua mtiifu na libainike hilo mbele za watu. Wafasiri wengi wamesema kwamba Mwenyezi Mungu ana elimu mbili ya kujua kitu kabla ya kuwa ambayo ni elimu ya ghaib na elimu baada ya kuwa, ambayo ni elimu ya ushahidi na ndiyo iliyokusudiwa katika Aya hii, yaani Mwenyezi Mungu ametaka kujua baada ya kuwa, kama alivyo jua kabla ya kuwa.

Huku ni kucheza na maneno tu. Elimu ya Mwenyezi Mungu ni moja, elimu ya ghaib ndiyo hiyo hiyo elimu ya ushahidi

Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kupoteza imani yenu. Hakika Mwenyezi Mungu kwa watu ni mpole mwenye kurehemu

Hii ni bishara kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa wale wenye uthabiti katika imani yao kwa Mtume(s.a.w.w) kwa shida na raha. Wanafuata amri yake na wanaacha makatazo yake. Wafasiri wengi wamesema kuwa sababu ya kushuka Aya hii ni kwamba baadhi ya masahaba waliswali na Mtume kibla cha kwanza na wakafa kabla ya kugeuzwa kibla cha pili, akaulizwa Mtume kuhusu swala yao, ndipo Mwenyezi Mungu akateremsha Aya hiyo. Sisi hatutegemei mapokezi ya sababu za kushuka Aya isipokuwa machache tuliyo na yakini nayo. Kwa sababu maulamaa hawakujishughulisha sana na usahihi wake, kama walivyofanya kwa mapokezi ya hukumu.

﴿ قَدْ نَرَىٰ تَقَلُّبَ وَجْهِكَ فِي السَّمَاءِ فَلَنُوَلِّيَنَّكَ قِبْلَةً تَرْضَاهَا فَوَلِّ وَجْهَكَ شَطْرَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَحَيْثُ مَا كُنتُمْ فَوَلُّوا وُجُوهَكُمْ شَطْرَهُ وَإِنَّ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ لَيَعْلَمُونَ أَنَّهُ الْحَقُّ مِن رَّبِّهِمْ وَمَا اللَّـهُ بِغَافِلٍ عَمَّا يَعْمَلُونَ ﴾

144.Kwa hakika tunakuona unavyogeuza geuza uso wako mbinguni; basi tutakuelekeza Qibla ukipendacho. Basi elekeza uso wako upande wa Msikiti Mtakatifu (Al-Kaaba). Na popote mlipo geuzeni nyuso zenu upande huo. Na hakika wale waliopewa Kitabu wanajua kwamba huo ni haki itokayo kwa Mola wao; na Mwenyezi Mungu si Mwenye kughafilika na yale wanayoyatenda.

﴿ وَلَئِنْ أَتَيْتَ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ بِكُلِّ آيَةٍ مَّا تَبِعُوا قِبْلَتَكَ وَمَا أَنتَ بِتَابِعٍ قِبْلَتَهُمْ وَمَا بَعْضُهُم بِتَابِعٍ قِبْلَةَ بَعْضٍ وَلَئِنِ اتَّبَعْتَ أَهْوَاءَهُم مِّن بَعْدِ مَا جَاءَكَ مِنَ الْعِلْمِ إِنَّكَ إِذًا لَّمِنَ الظَّالِمِينَ ﴾

145.Na hao waliopewa Kitabu hata ukawaletea hoja za kila namna, hawatafuata Qibla chako; na wala wewe si mwenye kufuata Qibla chao, wala baadhi yao si wenye kufuata Qibla cha wengine. Na kama ukifuata matamanio yao baada ya kukufikia elimu, utakuwa miongoni mwa madhalimu.

HAKIKA TUNAKUONA UNAVYOGEUZA USO WAKO

Aya 144-145

MAANA

Mwenye Majmaul-Bayan anasema: Imepokewa kutoka kwa Imam Jaffar Sadiq(a.s) kwamba:Kiligeuka Qibla baada ya kuswali Mtume (s.a.w.w), Makka kwa muda wa miaka 13 akielekea Baitul Maqdis. Na baada ya kuhamia Madina, aliswali miezi saba, kisha Mwenyezi Mungu akamwelekeza Al Kaaba .

SABABU YA KUTEREMSHWA AYA

Sababu hiyo ni kwamba Mayahudi walikuwa wakimkejeli Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa kumwambia: Wewe unatufuata sisi, unaswali kwenye Qibla chetu. Mtume akaingiwa na majonzi makubwa, akatoka usiku akawaana angalia pambizoni mwa mbingu, akingojea amri ya Mwenyezi Mungu kuhusu jambo hilo. Kulipokucha akaswali swala ya Adhuhuri katika msikiti wa Bani Salim, alipomaliza rakaa mbili alishukiwa na Jibril akamshika na kumgeuza upande wa Al-Kaaba, akamteremshia Aya hii:Kwa hakika tunakuona unavyogeuza geuza uso wako mbinguni, Mtume akaswali rakaa mbili kuelekea Baitul Maqdis na rakaa mbili kuelekea Al- Kaaba.

Basi elekeza uso wako upande wa Msikiti mtakatifu (Al Kaaba).

Ameusifu Msikiti kwa utakatifu, ambapo ni wajibu kuutakasa na ni haramu kuuvunjia heshima. Al-Kaaba ni sehemu ya Masjidul Haram (Msikiti Mtakatifu) nao ni sehemu ya Haram ambayo inakusanya Makka na mipaka yake, kama ilivyoelezwa katika vitabu vya Fiqh, katika mlango wa Hijja, katika masuala ya Ihram na kuwinda katika Haram. Yanayojulikana katika Quran ni kwamba amri ya wajib yoyote ya kisharia inayoelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu inawahusu watu wote, mfano:

﴿ وَأَقِمِ الصَّلَاةَ طَرَفَيِ النَّهَارِ وَزُلَفًا مِّنَ اللَّيْلِ﴾

Na simamisha Swala katika ncha mbili za mchana na mwanzo wa usiku. (11:114).

Haiwezekani kuwa amri ya wajib inahusika na yeye Mtume tu, ila kama kuna kitu kinachofahamisha hilo; kama Aya hii:

﴿ وَمِنَ اللَّيْلِ فَتَهَجَّدْ بِهِ نَافِلَةً لَّكَ﴾

Na katika usiku swali Tahajjud ([1] ), Hiyo niSunna kwa ajili yako... (17:79).

Neno: kwa ajili yako linafahamisha kwamba taklifa hii haimuhusu mtu mwingine isipokuwa yeye. Vile vile njia ya Quran ni kwamba taklifa zenye kuelekezwa kwa watu na Muhammad(s.a.w.w) pia huwamo, bila ya kuwako na tofauti hata ndogo ya mwelekezo huo kati yake na mwingine. Kwa hivyo umma unaingia katika kauli yake Mwenyezi Mungu: Basi elekeza uso wako upande wa Msikiti Mtukufu (Al-Kaaba).

Na popote mlipo geuzeni nyuso zenu upande huo .

Yaani popote mnapokuwa baharini au bara, kwenye tambarare au majabalini, Mashariki au Magharibi, ni juu yenu kuelekea Msikiti Mtukufu kwa sehemu ya mbele ya mwili, wala haijuzu kuupa mgongo katika swala au kuuelekea kwa upande wa kuume au kushoto, nk. Kutokana na hali hiyo Qibla kinahitalifiana kwa kuhitalifiana miji. Kwa ajili hii Waislamu wamejishughulisha sana na suala la Qibla na wakaweka elimu mahsus kwa jina la elimu ya Qibla, Kinyume na Wakristo ambao wanalazimiana na upande wa Mashariki daima na Mayahudi nao ni upande wa Magharibi popote walipo, hata kama hilo litalazimisha kuipa mgongo Baitul Maqdis.

Unaweza kuuliza: Ikiwa Umma unaingia katika msemo unaoelekezwa kwa Mtume na msemo unaolekezwa kwa Umma unamhusu Mtume; sasa kwa nini kukusanyika misemo inayoelekea sehemu mbili katika Aya moja na maudhui moja tena bila ya kuwako kitenganisho. Yaani Mwenyezi Mungu anasema elekeza uso wako- ewe Muhammad - upande wa Msikiti Mtakatifu, na popote mtakapokuwa - enyi Waislamu - elekezeni nyuso zenu upande uliko Msikiti Mtakatifu.

Jibu : Kugeuka Qibla ni tukio kubwa katika Uislamu na kulikuja kutokana na raghba ya Mtume(s.a.w.w) . Kwa hivyo Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akataka kumbainishia hilo, na kulitilia mkazo kwa kulikariri. Zaidi ya hayo ni kuwa kwa asili taklifa hiyo ni ya Muhammad(s.a.w.w) , kwa sababu imekuja kwa raghba yake na kufuatilia umma wake.

NI WAJIB WAKATI GANI KUELEKEA QIBLA?

Al Kaaba ni Qibla kwa aliye ndani ya Msikiti Mtakatifu ambao Al Kaaba imo ndani yake, Msikiti ni Qibla kwa watu wa Haram; yaani watu wa Makka na pembeni mwake na Haram au upande wake ni Qibla kwa watu wa Mashariki na Magharibi. Ni wajibu kuelekea Qibla katika swala za kila siku, swala ya ihitiyat, mafungu yaliyosahauliwa katika swala na sijda mbili za kusahau. Vile vile ni wajibu kuelekea Qibla kwa ajili ya swala yoyote ya wajibu, ikiwemo Swala ya tawaf, na Swala ya kumswalia maiti. Pia ni wajibu kumwelekeza Qibla mtu aliye katika hali ya kukata roho na wakati wa kumzika, na wakati wa kumchinja mnyama. Ama katika swala za sunna ni wajibu kuelekea Qibla katika hali ya utulivu tu, na wala sio wajibu katika hali ya kutembea na kupanda chombo cha kusafiria.

WATU WA QIBLA

Watu wa Qibla, watu wa Quran, watu wa shahada mbili na Waislamu, yote hiyo ni misamiati iliyo katika maana moja. Ama lile jina la Wafuasi wa Muhammad (Mohammedan), ni jina tulilobandikwa na maadui wa Uislamu, wakiwa na maana kwamba sisi ni wafuasi wa mtu na wala sio wa dini ya Mwenyezi Mungu; kama Mabudha ambao ni wafuasi wa Budha na Wazaradashti ambao ni wafuasi wa Zaradasht. Kwa vyovyote vile lengo la kifungu hiki ni kuzindua kwamba umma wa Kiislamu, pamoja na kutofautiana miji yake, rangi na lugha, lakini unakusanywa na kuwa pamoja na misingi ya aina moja, ambayo ni ghali na yenye thamani zaidi kuliko uhai. Kwa sababu Waislamu wanadharau maisha kwa ajili ya misingi hiyo na wala hawawezi kuidharau misingi hiyo kwa ajili ya maisha. Misingi hiyo ni pamoja kumwamini Mwenyezi Mungu na kitabu chake, kumwamini Muhammad(s.a.w.w) na sera yake na kuswali kwa kuelekea Qibla. Basi mwenye kumkufurisha mwenye kuswali kwa kuelekea Qibla na akamtoa katika idadi ya Waislamu, atakuwa ameidhoofisha nguvu ya Uislamu na atakuwa amelichana jina la Waislamu, na kusaidia maadui wa dini, atake asitake.

Na hakika wale waliopewa kitabu wanajua kwamba huo ni haki itokayo kwa Mola wao.

Makusudio ya waliopewa kitabu ni Mayahudi na Wakristo, na wala sio Mayahudi peke yao, kama ilivyosemwa. Kwa sababu neno linaenea, na wala hakuna dalili ya kuhusisha. Wafasiri wametofautiana katika dhamiri ya neno Annahul-haqq kwamba je ni huo Msikiti au ni huyo Mtume? Sababu ya kutofautiana ni kwamba Mwenyezi Mungu nyuma amemtaja Mtume kwa kusema: Kwa hakika tunakuona unavyogeuza geuza uso wako na vile vile ametaja Msikiti Mtakatifu. Sisi tuko katika upande wa wanaosema kuwa dhamiri inarudia Msikiti kwa sababu ndilo tamko la karibu zaidi, na dhamiri inarudia tamko la karibu zaidi.

Kwa hiyo maana yanakuwa, watu waliopewa kitabu wanajua kabisa kwamba Ibrahim(a.s) ni baba wa Mitume na ni mkubwa wao ambaye alijenga Nyumba Tukufu (Al Kaaba), lakini wao wameikataa kwa vile tu, iko mikononi mwa Waarabu ambao wanaitumikia na kuihami. Lau isingelikuwa mikononi mwa Waarabu, Mayahudi wangelikuwa wa kwanza kuitukuza na wangeliiheshimu sana.

Na hao waliopewa kitabu hata ukiwaletea hoja za kila namna hawatafuata Qibla chako .

Yaani hawafuati mila yako, sembuse kufuata Qibla chao.Nao hawana hoja yoyote isipokuwa ujinga na ukaidi .Na wala wewe si mwenye kufuata Qibla chao .

Huenda baadhi ya watu wa Kitab walitaraji kuwa Mtume(s.a.w.w) atarudia Qibla alichokielekea kwanza, ndipo Mwenyezi Mungu akawakatisha tamaa kabisa kwa kauli yake hiyo; kama alivyomkatisha tamaa Muhammad(s.a.w.w) kuwa wao hawatafuata Qibla chake.

Wala baadhi yao si wenye kufuata Qibla cha wengine.

Mayahudi wanaswali kuelekea Magharibi na Wakristo wanaelekea Mashariki, wala kundi moja haliwezi kulifuata kundi jingine, vipi wataweza kufuata Qibla chako ewe Muhammad? Bali hata hao Mayahudi wanatofautiana; kama walivyo Wakristo. Mauaji yaliyotokea kati ya Wakatoliki na Waprotestant, hayana mfano wa fedheha yake katika zama zote.

Na kama ukifuata matamanio yao baada ya kukufikia elimu, utakuwa miongoni mwa madhalimu.

Ni muhali kuwa Mtume afuate matamanio yao, kwa sababu yeye ni masum (mwenye kuhifadhiwa na madhambi), lakini lengo la makatazo haya ni kumpa nguvu Mtume katika kuamiliana kwake na Mayahudi na kusimama nao imara, na kwamba hakuna heri yoyote ya kupatana nao wala hakuna,tumaini lolote kwao. Haliwezi kufaa jaribio lolote la kuwazuia na vitimbi na ufisadi wao. Kwa sababu wao wana maumbile ya shari. Kupinga haki na kumfanyia uovu anayewafanyia wema. Yamekwishaelezwa maelezo zaidi katika kufasiri Aya ya 120.

UISLAMU NAWATU WENYE UPENDELEO NA DINI ZAO

Ni jambo lenye kuingia akilini kwamba wataalamu wanaweza kuhitilafiana katika aina yoyote ya masuala yasiyokuwa ya kidini. Baada ya kukumbushana na kudurusi, huafikiana katika lile walilohitilafiana. Hilo limekwishatokea. Ama wakihitalifiana katika masuala ya dini mbali mbali, basi kuafikiana kwao ni muhali, hata kama zitakuwepo dalili elfu. Imethibiti kwa wataalamu wa elimu ya saikolojia, kwamba watu kubadili tabia yao ni rahisi zaidi tena sana kuliko kubadili dini yao.

Hilo ni kwamba watu wengi hutegemea dini za mababa na mababu. Hakuna dini iliyojulikana kukataza kufuata mababu isipokuwa Uislamu ambao umetegemea akili peke yake katika kuthibitisha misingi yake. Mwenye kuangalia Aya za Quran na Hadith za Mtume ataziona zimetilia umuhimu kufuatilia akili kwa kiasi kile kile zinavyoitilia umuhimu kumwamini Mwenyezi Mungu. Kwa sababu Imani hiyo haiepukani kabisa na nuru ya akili timamu katika kuongoka kwake.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿ الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَعْرِفُونَهُ كَمَا يَعْرِفُونَ أَبْنَاءَهُمْ وَإِنَّ فَرِيقًا مِّنْهُمْ لَيَكْتُمُونَ الْحَقَّ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴾

146.Wale tuliowapa Kitabu wanamjua yeye kama wanavyowajua watoto wao. Na hakika kundi katika wao wanaificha haki na hali wanaijua.

﴿ الْحَقُّ مِن رَّبِّكَ فَلَا تَكُونَنَّ مِنَ الْمُمْتَرِينَ ﴾

147.Haki ni iliyotoka kwa Mola wako. Basi usiwe miongoni mwa wanaofanya shaka.

WANAMJUA KAMAWANAVYOWAJUAWATOTO WAO

Aya 146-147

MAANA

Wale tuliowapa kitabu wanamjua kama wanavyowajua watoto wao. Yaani: wanavyuoni wengi wa Kiyahudi na wa Kikristo wanajua kwa usahihi na uwazi Utume wa Muhammad(s.a.w.w) ; kama wanavyowajua watoto wao, kwa namna isiyokuwa na shaka yoyote. Kwa sababu Tawrat na Injil zimetoa bishara ya kuja kwake na zikamtaja kwa sifa zake na alama zake ambazo hazikupatikana kwa mwingine yeyote. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ﴾

...Wanamkuta ameandikwa kwao katika Taurat na Injil... (7:157)

﴿ وَإِذْ قَالَ عِيسَى ابْنُ مَرْيَمَ يَا بَنِي إِسْرَائِيلَ إِنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُم مُّصَدِّقًا لِّمَا بَيْنَ يَدَيَّ مِنَ التَّوْرَاةِ وَمُبَشِّرًا بِرَسُولٍ يَأْتِي مِن بَعْدِي اسْمُهُ أَحْمَدُ فَلَمَّا جَاءَهُم بِالْبَيِّنَاتِ قَالُوا هَـٰذَا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴾

Na aliposema Issa bin Maryam: Enyi wana wa Israil! Mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu, nisadikishaye yaliyokuwa kabla yangu katika Tawrat na kutoa bishara ya Mtume atakayekuja baada yangu ambaye jina lake ni Ahmad. Lakini alipowajia kwa hoja zilizo wazi, walisema: Huu ni uchawi ulio wazi (61:6).

Abdallah bin Salam alikuwa ni mmoja wa maulamaa wa kiyahudi; kisha akasilimu. Miongoni mwa maneno aliyosema ni: Mimi ninaujua zaidi Utume wa Muhammad kuliko ninavyomjua mwanangu. Alipoulizwa kwa nini, alisema: Mimi sitii shaka kwamba Muhammad ni Mtume, lakini mtoto wangu, pengine mama yake amefanya hiyana.

Na hakika kundi katika wao wanaificha haki na hali wanaijua .

Ndio! wanaficha, hata kama wangeliona jina la Muhammad katika Lauhul Mahfudh, kwa sababu ya kupupia uongozi wa duniani na maslahi ya kibinafsi. Inadi hii ya kuficha haki haihusiki na Mayahudi na Wakristo tu, Kwani sababu ya kuficha haki ni ya kijumla. Tumekwisha waona baadhi ya Masheikh wanakana sifa za wenzao kwa sababu ya chuki na hasadi tu.

Haki ni iliyotoka kwa Mola wako, basi usiwe miongoni mwa wanaofanya shaka .

Mtume(s.a.w.w) hawezi kutia shaka yale yaliyotoka kwa Mola wake na ni muhali kuyatilia shaka; na Mwenyezi Mungu anajua kuwa Mtume wake Mtukufu hawezi kutia shaka. Lengo la Aya hii ni kubainisha kwamba aliyomteremshia Muhammad hayana shaka wala matatizo yoyote kabisa. Mtu akiyakanusha na kuyapinga basi atakuwa anafanya hivyo kwa inadi na ukaidi tu.

MIMI NA MHUBIRI

Tarehe 15-7-1963 alinitembelea mtaalamu wa mambo ya nchi za mashariki Mkristo kutoka Italia ambaye alikuwa akizungumza lugha ya Kiarabu vizuri. Basi tukawa na mjadala kwa mdomo na kwa maandishi. Miongoni mwa aliyosema ni kuwa: Quran inakiri wazi wazi kuhusu Injil, kwa nini Waislamu wanaikana? Nikamjibu kuwa: Quran inakiri Injil iliyobashiri Utume wa Muhammad(s.a.w.w) ; kama ilivyosema:

﴿ وَمُبَشِّرًا بِرَسُولٍ يَأْتِي مِن بَعْدِي اسْمُهُ أَحْمَدُ﴾

...Na mwenye kutoa bishara ya Mtume atakayekuja baada yangu ambaye jina lake ni Ahmad... (61:6).

﴿ يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ ﴾

...Wanamuona ameandikwa kwao katika Tawrat na Injil... (7:157). Kisha Quran inaendelea kusema:

﴿ إِنَّ مَثَلَ عِيسَىٰ عِندَ اللَّـهِ كَمَثَلِ آدَمَ خَلَقَهُ مِن تُرَابٍ ثُمَّ قَالَ لَهُ كُن فَيَكُونُ﴾

Hakika mfano wa Issa kwa Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa Adam; alimuumba kwa udongo kisha akamwambia kuwa basi akawa. (3:59)

Injil yenu inasema: Issa ni Mungu, sasa vipi mnatutaka tuiamini na wakati huo huo tuiamini Quran? Ikiwa Wakristo wanakataa kupingana na kukosana katika hukumu ya akili tu, na kukubali kuwa akili inaweza kupingana na kutoafikiana katika dini na itikadi, basi Waislamu wanaliona hilo ni muhali; haliwezekani kiakili na kidini na katika kila kitu. Kwa sababu misingi ya dini kwao inakuwa ndani ya akili tu.

﴿ وَلِكُلٍّ وِجْهَةٌ هُوَ مُوَلِّيهَا فَاسْتَبِقُوا الْخَيْرَاتِ أَيْنَ مَا تَكُونُوا يَأْتِ بِكُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴾

148.Na kila mmoja ana mwelekeo anaouelekea. Basi shindaneni kufanya mema. Popote mtakapokuwa, Mwenyezi Mungu atawaleta nyote pamoja. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.

﴿ وَمِنْ حَيْثُ خَرَجْتَ فَوَلِّ وَجْهَكَ شَطْرَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَإِنَّهُ لَلْحَقُّ مِن رَّبِّكَ وَمَا اللَّـهُ بِغَافِلٍ عَمَّا تَعْمَلُونَ ﴾

149Na popote uendapo utakako kuwa elekeza uso wako kwenye Msikiti Mtakatifu; na hiyo ndiyo haki itokayo kwa Mola wako. Na Mwenyezi Mungu si Mwenye kughafilika na yale mnayoyatenda.

﴿ وَمِنْ حَيْثُ خَرَجْتَ فَوَلِّ وَجْهَكَ شَطْرَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَحَيْثُ مَا كُنتُمْ فَوَلُّوا وُجُوهَكُمْ شَطْرَهُ لِئَلَّا يَكُونَ لِلنَّاسِ عَلَيْكُمْ حُجَّةٌ إِلَّا الَّذِينَ ظَلَمُوا مِنْهُمْ فَلَا تَخْشَوْهُمْ وَاخْشَوْنِي وَلِأُتِمَّ نِعْمَتِي عَلَيْكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَهْتَدُونَ ﴾

150.Na popote utakapotoka utakokuwa elekeza uso wako upande wa Msikiti Mtakatifu, na popote mlipo elekezeni nyuso zenu upande (uliko msikiti) huo ili watu wasiwe na hoja juu yenu, isipokuwa wale waliodhulumu miongoni mwao. Basi msiwaogope, niogopeni Mimi, ili niwatimizie neema Zangu na ili mpate kuongoka.

﴿ كَمَا أَرْسَلْنَا فِيكُمْ رَسُولًا مِّنكُمْ يَتْلُو عَلَيْكُمْ آيَاتِنَا وَيُزَكِّيكُمْ وَيُعَلِّمُكُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَيُعَلِّمُكُم مَّا لَمْ تَكُونُوا تَعْلَمُونَ ﴾

151. Kama tulivyomleta Mtume kwenu anayetokana na nyinyi, anayewasomea Aya zetu na kuwatakasa na kuwafundisha Kitabu na hekima na kuwafundisha mliyokuwa hamyajui.

﴿ فَاذْكُرُونِي أَذْكُرْكُمْ وَاشْكُرُوا لِي وَلَا تَكْفُرُونِ ﴾

152.Basi nikumbukeni nitawakumbuka, na nishukuruni wala msinikufuru.

KILA UMMA ULIKUWA NA QIBLA CHAKE

Aya ya 148-152

MAANA

Na kila mmoja ana mwelekeo anaoulekea . Alipotaja Mwenyezi Mungu Qibla ambacho amewaamrisha Waislamu kukielekea ambacho ni Al Kaaba, na akataja kuendelea kwa Mayahudi na Manaswara kuelekea mielekeo yao, alibainisha kuwa siri ya kungangania huku kwamba kila umma ulikuwa na Qibla chake uliojichagulia kuelekea na wala haukiachi, hata kama ubaya wa mwelekeo wenyewe uko wazi kama jua. Kwa hiyo kauli Yake hii inafanana na kauli Yake:

﴿كُلُّ حِزْبٍ بِمَا لَدَيْهِمْ فَرِحُونَ﴾

...Kila kikundi kinafurahia kilicho nacho (30:32). Hayo ndiyo niliyoyafahamu kutokana na dhahiri ya tamko. Wafasiri wameleta kauli nyingi katika Aya hii; mwenye Majmau ametaja nne.

Basi shindaneni kufanya mema .Popote mtakapokuwa Mwenyezi Mungu atawaleta nyote pamoja, hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu .

Yaani achaneni na watu wa Kitab na washirikina walio wakaidi, na mfanye amali njema. Kwani marejeo yenu kesho ni kwake Mwenyezi Mungu, ambapo atalipwa thawabu mwenye haki na mwenye kufanya wema na kuadhibiwa mwenye batili mtenda maovu. Kama wanavyosema wafasiri maana ya:Popote mtakapokuwa Mwenyezi Mungu atawaleta nyote pamoja, ni ahadi ya thawabu kwa watiifu na kiaga cha adhabu kwa waasi. Ama kusema kwake:Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu, ni dalili na sababu ya kuwezekana kufufuliwa viumbe baada ya mauti.

Na popote uendapo elekeza uso wako kwenye Msikiti Mtakatifu.

Unaweza kuuliza: Kwa nini Mwenyezi Mungu hapa amekariri kuelekea Msikiti Mtakatifu mara tatu na katika Aya ya 149 mara mbili; yaani amekariri mara tano mfululizo?

Jibu : Mwenye Majmaul-Bayan ametaja kauli tatu, na Razi ameleta tano. Miongoni mwa kauli hizo ni lile jibu lililozoeleka linalorithiwa ambalo ni, kutilia mkazo na umuhimu. Nafsi yangu haikutulia kabisa katika kauli hizo. Na mimi sina chochote cha kusema isipokuwa huenda kukariri huku hapa ni kutokana na jambo lililohusu wakati huo ambalo hatulijui. Kuna mambo mengi ambayo hayaingii katika udhibiti na hisabu. Inajulikana wazi kuwa mapokezi ya Aya na sababu zake yako ya kiujumla na mahsusi, na haifai kwa yeyote kutafsiri au kuleta taawili, kwa kutegemea dhana bila ya kupata asili yake yoyote.

Ili watu wasiwe na hoja juu yenu.

Wafasiri wengi wamesema kuwa Mtume(s.a.w.w ) alipokuwa akiswali kuelekea Baitil Maqdis; Washirikina na Waarabu wakasema: Vipi Muhammad anadai kwamba yeye yuko kwenye dini ya Ibrahim, na wala haswali kuelekea Al Kaaba aliyokuwa akiswali Ibrahim na Ismail? Na watu wa Kitab wakasema Yaliyo katika Vitabu vyetu ni kwamba Mtume atakayeletwa katika kizazi cha Ismail ataswali kuelekea Al Kaaba na wala sio Baitul Maqdis, sasa vipi tunaweza kuukubali Utume wa Muhammad. Kwa hiyo wakaifanya kuwa hoja, wanayoitumia kwa dhana yao. Mwenyezi Mungu akambadilishia Qibla kuelekea Al Kaaba na akaifanya ndio Qibla cha kudumu kwa Mtume na Waislamu wote mpaka siku ya malipo, ili hawa na wengine wasibakiwe na hoja yoyote.

Dhahiri ya jumla inafahamisha kwamba: kuswali kuelekea Al Kaaba kunavunja hoja ya wapinzani. Ama kuwa ni kina nani hao wapinzani, Aya haikubainisha. Inawezekana kuwa njia ya kukata hoja ya wapinzani ni kuwa Al Kaaba imejengwa na Ibrahim(a.s) na akaswali hapo. Hilo ni lenye kuafikiwa na wote na Muhammad atafuata mwendo wa Ibrahim.

Isipokuwa wale waliodhulumu miongoni mwao.

Yaani hakuna hoja yoyote juu yako ukiswali, isipokuwa kwa mpinzani asiye na haki ambaye hategemei dalili za kiakili katika upinzani wake wala uongozi wa kidini isipokuwa kung’ang’ania, na ukaidi.

Basi msiwaogope,niogopeni Mimi.

Yaani msiogope lawama katika haki, Mimi pekee ndiye ninayewamilikia manufaa na madhara. Ibnul Arabi katika tafsiri yake anasema: Maana ya niogopeni ni; jueni Utukufu Wangu ili makafiri wasijifanye watukufu kwenu. Amirul Muminin(a.s) anasema:Amekuwa mkubwa Muumbaji katika nafsi zao akawa mdogo asiyekuwa yeye katika macho yao .

Na ili niwatimizie neema zangu na ili mpate kuongoka.

Yaani nimewaneemesha kwa Uislamu na nimewatimizia neema kwa kuwapa Qibla chenu kilichowafanyia umoja na kuwakusanya na kinachoelekewa na watu wa mataifa mbali mbali ya pembe zote za dunia, yenye makabila na lugha mbali mbali.

KATIBA YA UISLAMU

Mtaalamu mmoja anasema kuwa katiba ya Uislamu ina vipengele vitatu: Mwenyezi Mungu mmoja, Kitabu kimoja na Qibla nimoja. Waislamu hukusanyika kutoka pembe zote za dunia kila mwaka ili wamwabudu Mwenyezi Mungu mmoja kwa sharia hiyo moja kwenye nchi mmoja, nchi ya mji wa kiroho. Hivi ndivyo ulivyokuwa umoja wa itikadi, sharia na mji, ili wakumbuke Waislamu kwamba wao hata kama wakitofautiana miji, lugha, rangi na nasaba, lakini wanakuwa wamoja kwa dini, wanaabudu Mwenyezi Mungu mmoja na ni wananchi wa nchi mmoja.

Kama tulivyomleta Mtume kwenu anayetokana na nyinyi, anayewasomea Aya zetu na kuwatakasa na kuwafundisha Kitabu na hekima na kuwafundisha mliyokuwa hamyajui.

Wanavyuoni wana maneno mengi na marefu katika maana ya neno hekima. Tunavyofahamu sisi ni kuwa kila kinachowekwa mahali pake panapostahili, kiwe ni kitendo au kauli, basi ni hekima.

Hali yoyote iwayo, maana ya jumla ya Aya hii ni kwamba: Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amewaneemesha Waarabu kwa Qibla; kama alivyowaneemesha kwa Muhammad(s.a.w.w) ambaye ni katika wao na anatokana na wao. Amewapa umbo jipya; akawatwaharisha na uchafu wa shirk na tabia mbaya. Kwa hiyo, kwa fadhila zake, wakawa ni watu wa dini na sharia ya Mwenyezi Mungu ambayo misingi yake ni uadilifu na usawa; kama ambavyo wamekuwa na dola iliyopanuka, mpaka lugha yao ikawa kubwa na ikaenea kwa sababu ya Quran na fasihi yake.

Hapana mwenye kutia shaka kwamba lau si Muhammad na kizazi cha Muhammad, Waarabu wasingelikuwa na historia wala turathi zozote; wasingekuwa na chochote zaidi ya kuabudu masanamu, ujinga na kuwazika watoto wa kike wakiwa hai, ili kuepuka gharama za kuwalisha. Bali Muhammad(s.a.w.w) , Mwarabu, ni neema kubwa juu ya watu wote. Kwa sababu yake, watu wamepiga hatua za haraka katika nyanja za elimu na maendeleo. Uhakika huu wameukiri na kuusajili wataalamu wa Kimagharibi wale wasiokuwa na ubaguzi, na tumeyanakili baadhi katika kitabu Al-Islam Wal-aql (Uislamu na Akili). Kwa ajili ya neema hiyo aliyowaneemesha Waarabu, ndio Mwenyezi Mungu akawataka wamkumbuke na kumshukuru na akahadharisha wasije wakaikufuru neema na hisani, kwa kusema:

Basi nikumbukeni nitawakumbuka na nishukuruni wala msinikufuru.

Yaani nikumbukeni kwa utii nami nitawakumbuka kwa malipo na thawabu. Na mnishukuru juu ya neema ya Uislamu na Utume kwa Muhammad ambaye anatokana na nyinyi wala msinikufuru. Mahali pengine Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ لَئِن شَكَرْتُمْ لَأَزِيدَنَّكُمْ وَلَئِن كَفَرْتُمْ إِنَّ عَذَابِي لَشَدِيدٌ ﴾

...Kama mkishukuru nitawazidishia, na kama mkikufuru basi adhabu yangu ni kali sana. (14:7).

Amirul Mumini Ali(a.s) alisema:Mwenyezi Mungu hawezi kufungua mlango wa shukrani na akafunga wa malipo . Anaendelea kusema:Mkumbukeni sana Mwenyezi Mungu, kwani huo ndio ukumbusho mzuri, na kuweni na raghba katika aliyowaahidi wanaomcha Mwenyezi Mungu, kwani ahadi Yake ni ya kweli sana .

KUMSHUKURU MNEEMESHAJI

Moja kwa moja akili inafahamu kuwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ni wajibu kwa kila aliye baleghe mwenye akili, hata kama isingeshuka Aya yoyote au kuja Hadith yoyote ya kuwajibisha kushukuru. Kwani Yeye Mtukufu ndiye Muumbaji Mwenye kuruzuku. Maana ya kumshukuru Mwenyezi Mungu (s.w.t.) baada ya kuitakidi kwamba Yeye ndiye mwanzilishi na kwamba Yeye ni muweza wa kila kitu: ni kutii amri Zake na makatazo Yake na kutegemeza mambo kwake peke Yake. Hayo ni kwa upande wa Mwenyezi Mungu (s.w.t.), Ama mtu akimfanyia wema mtu kama yeye, je inapasa, yule aliyefanyiwa wema kumshukuru aliyemfanyia wema, kiasi ambacho kama hakumshukuru kwa namna fulani atakuwa ni mwasi mwenye kustahiki adhabu? Hapana mwenye kutia shaka kwamba kumshukuru aliyekutendea wema ni jambo zuri, bali hiyo ni alama ya watu wema. Ama kuwa ni wajibu au la, hakuna dalili juu yake. Kwa hiyo kila habari iliyokuja kuhusu kumshukuru mwenye kutoa neema asiyekuwa Mwenyezi Mungu, Mtume au Ahlul Bait wake, ni pendekezo tu ya kuwa ni vizuri; kama alivyosema Ali(a.s) :Ukiwa unammudu adui yako, basi ufanye msamaha ndio shukrani ya uwezo huo wa kummudu.

Kumsamehe aliyekufanyia ubaya sio wajib, lakini ni Sunna kwa Ijmai. Ama msemo unaosemwa sana: Asiyeshukuru kiumbe ndio hamshukuru Muumba, hiyo ni hukumu ya kimaadili tu, siyo ya lazima. Hata hivyo kukanusha neema na kumwambia aliyekufanyia wema: Hukufanya wema ni haramu, kwa sababu ni uwongo; na kumfanyia uovu ndio haramu kabisa, kwa sababu uovu ni haramu kwa dhati yake, hata kwa mtu asiyekufanyia wema. Lakini pamoja na hayo wajibu wa kushukuru ni jambo jingine na uharamu wa uwongo na uovu ni jambo jingine.

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اسْتَعِينُوا بِالصَّبْرِ وَالصَّلَاةِ إِنَّ اللَّـهَ مَعَ الصَّابِرِينَ﴾

153.Enyi mlioamini! Takeni msaada kwa subira na swala; hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wanaosubiri.

﴿ وَلَا تَقُولُوا لِمَن يُقْتَلُ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ أَمْوَاتٌ بَلْ أَحْيَاءٌ وَلَـٰكِن لَّا تَشْعُرُونَ ﴾

154.Wala msiseme kwamba wale waliouawa katika njia ya Mwenyezi Mungu ni wafu, bali wa hai lakini nyinyi hamtambui.

﴿ وَلَنَبْلُوَنَّكُم بِشَيْءٍ مِّنَ الْخَوْفِ وَالْجُوعِ وَنَقْصٍ مِّنَ الْأَمْوَالِ وَالْأَنفُسِ وَالثَّمَرَاتِ وَبَشِّرِ الصَّابِرِينَ ﴾

155.Na hakika tutawajaribu kwa chembe ya hofu na njaa na upungufu wa mali na wa nafsi na wa matunda, Na wape bishara wanaosubiri.

﴿ الَّذِينَ إِذَا أَصَابَتْهُم مُّصِيبَةٌ قَالُوا إِنَّا لِلَّـهِ وَإِنَّا إِلَيْهِ رَاجِعُونَ ﴾

156.Ambao ukiwapata msiba, husema: Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na Kwake Yeye tutarejea.

﴿ أُولَـٰئِكَ عَلَيْهِمْ صَلَوَاتٌ مِّن رَّبِّهِمْ وَرَحْمَةٌ وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُهْتَدُونَ ﴾

157.Hao juu yao zitakuwa baraka zitokazo kwa Mola wao na rehema, na hao ndio wenye kuongoka.

TAKENI MSAADAKWA SUBIRA

Aya 153-157

SUBIRA

Enyi mlioamini! Takeni msaada kwa subira na swala; hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wanaosubiri.

Mwenye Tafsiri ya Al-Manar anasema kuwa: Subira (uvumilivu) katika Quran imetajwa mara sabini. Hiyo inafahamisha umuhimu wake, na Mwenyezi Mungu ameijaalia ni kitu cha kuusiana katika Sura Al Asr kwa kuikutanisha na haki, kwani mwenye kuilingania haki hana budi kuwa nayo.

Mwenye Bahrul Muhit ameiweka mbali sana aliposema: Subira na swala ni nguzo mbili za Uislamu.Ameghafilika na Hadith inayosema: Umejengwa Uislamu juu ya mambo matano: Kushuhudia kuwa hakuna Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, kusimamisha swala, kutoa zaka, kufunga mwezi wa Ramadhan na kuhiji Makka kwa mwenye kuweza njia ya kuendea. Subira haimo katika nguzo hizo. Pia ameghafilika kuwa kuna taklifa za lazima ambazo Mukallaf anatakiwa kuzifanya na ataadhibiwa kwa kuziacha; kama, swala kulipa deni, n.k. Na kuna taklifa nyingine ambazo ni za kimwongozo, zimekuja kinasaha, zinafanana na amri, lakini mukallaf hawezi kuadhibiwa kwa kuziacha; kama usafi, kuosha mikono kabla ya kula, kukatazwa kushiba sana, n.k. Sasa yako wapi haya na nguzo za dini, ambazo mwenye kuziacha anakuwa ametoka katika dini? Kisha subira haisifiwi hiyo yenyewe hasa, isipokuwa inasifiwa ikiwa ni nyenzo ya kufikilia jambo kuu; kama subira katika jihad takatifu, subira juu ya ufukara na uhitaji, subira kwa ajili ya kuipata elimu na subira juu ya matatizo ya familia na kulea watoto. Vile vile subira juu ya kumwokoa mwenye kudhulumiwa, subira juu ya kauli ya mtu mpumbavu kwa kukinga shari, au kufanya subira kwa kumkosa mpenzi asiyesahaulika. Kwani kuendelea kufazaika ni kuzidisha msiba; kama alivyosema Amirul Muminin Ali(a.s) :

Mwenye kuyakuza masaibu madogo,Mwenyezi Mungu humwingiza kwenye makubwa.

Bazar Jamhar aliulizwa: Kwa nini ewe mfalme mwenye hekima husikitiki kwa yaliyokupita wala hufurahi kwa yaliyopo? Akasema: Yaliyopita hayawezi kufutika kwa majonzi wala yaliyopo hayawezi kudumu kwa furaha.

Mwingine alisema: Siwezi kusema kitu kilichokwisha kuwa na tamani kisingekuwa au ambacho hakikuwa natamani kingekuwa. Mara nyingine subira huwa mbaya; kama kusubiri juu ya njaa na uwezo wa kufanya kazi upo, na kusubiri juu ya ukandamizwaji. Katika hali hii subira nzuri ni kumkabili dhalimu.

Unaweza kuuliza, kuna uhusiano gani kati ya swala na subira mpaka zikakutanishwa pamoja katika Aya?

Jibu : Maana ya subira ni kutulizana moyo ingawaje una machungu. Hiyo inahitajia kumtegemea Mwenyezi Mungu na kuamini kuwa Yeye Yu pamoja na wenye kusubiri. Hakuna mwenye shaka kwamba swala inatilia mkazo mategemeo haya na ni hakikisho la imani hii, kuongezea kwamba kumwomba Mwenyezi Mungu kunapunguza machungu ya masaibu.

Wala msiseme kwamba wale waliouawa katika njia ya Mwenyezi Mungu ni wafu, bali wa hai, lakini nyinyi hamtambui.

Mfano wa Aya hii ni kama nyingine isemayo:

﴿ وَلَا تَحْسَبَنَّ الَّذِينَ قُتِلُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ أَمْوَاتًا بَلْ أَحْيَاءٌ عِندَ رَبِّهِمْ يُرْزَقُونَ﴾

Wala usiwadhanie wale waliouawa katika njia ya Mwenyezi Mungu kuwa ni wafu, bali wa hai wanaruzukiwa kwa Mola wao. (3:169).

Inajulikana kuwa kila anayefariki hurejea kwa Mola wake, awe mwema au mwovu, shahidi au asiyekuwa shahidi; isipokuwa kwamba mwema anaondoka kwenye maisha ya chini kwenda kwenye maisha ya juu na mwovu inakuwa kinyume chake.

Hapa imehusishwa kutajwa shahidi; ama ni kwa kueleza cheo chake mbele za Mwenyezi Mungu kwa kuhimiza ushahidi; au ni kwa kutokana na yaliyonakiliwa kutoka kwa Ibn Abbas, kwamba Aya ilishuka kwa sababu ya waliouliwa katika vita vya Badr ambao ni Muhajirin kumi na nne na Ansar wanane; ikasemwa ameuawa fulani na fulani; ndipo ikashuka Aya hii. Haya hayako mbali, kwani kauli ya Mwenyezi Mungu: Msiwaite wafu, inafahamiisha hilo. Vyovyote iwavyo, ambalo tunapaswa kuamini ni kwamba mwenye kufa shahidi kwa kuupigania Uislamu au kitu chochote kinachofungamana na haki, uadilifu na utu, atakuwa anahama kutoka ulimwengu unaoonekana kwenda kwenye ulimwengu usioonekana na huko atakuwa na maisha mema. Na kwamba yeye anatofautiana na aliyekufa kifo cha kawaida. Amirul Muminin anasema:Naapa kwa yule ambaye nafsi ya mtoto wa Abu Twalib iko mikononi mwake, kupigwa mapigo elfu ya panga ni bora kwangu kuliko kufa kitandani. Ama hakika ya maisha ya shahidi baada ya mauti na kuhusu riziki anayoneemeshwa ni jambo tusilolijua na wala hatuna haja ya kulifanyia utafiti. Kwa sababu ni jambo tusilokalifishwa kulijua.

THAMANI YA PEPO

Na hakika tutawajaribu kwa chembe ya hofu na njaa na upungufu wa mali na wa nafsi na wa matunda. Na wapashe habari njema wanaosubiri.

Yeyote anayefuata haki ni lazima aigharimie kwa nafsi yake, watu wake au mali yake; na kila haki inavyokuwa kubwa, ndivyo gharama inavyokuwa kubwa, lau kama si hivyo wanaopigania haki wasingelikuwa na fadhla yoyote; na watu wote wasingelifuata haki. Kwa hali hiyo ndiyo tunapata tafsiri ya Hadith hii tukufu:Misukosuko amepewa mumin . na kwamba:wenye misukosuko zaidi ni Mitume; kisha wanaowafuatia . Vile vile misukosuko ya Mitume inakuja kwa kadiri ya daraja zao. Mtume mtukufu(s.a.w.w) amesema:Hakuudhiwa Mtume kama nilivyoudhiwa mimi .

Amirul Muminini amesema:Hakika haki ni nzito lakini nzuri, na batili ni hafifu, lakini mbaya. Inatosha kuwa ni ushahidi kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿مْ حَسِبْتُمْ أَن تَدْخُلُوا الْجَنَّةَ وَلَمَّا يَأْتِكُم مَّثَلُ الَّذِينَ خَلَوْا مِن قَبْلِكُم مَّسَّتْهُمُ الْبَأْسَاءُ وَالضَّرَّاءُ ﴾

Mnadhani kuwa mtaingia peponi, na hali hamjajiwa na mfano wa wale waliopita kabla yenu? Yaliwapata mashaka na madhara... (2:214).

Aya hii inafahamisha kuwa pepo haipati isipokuwa mwenye kujitolea mhanga katika njia ya Mwenyezi Mungu, Na kujitolea mhanga hakuwi katika uwanja wa vita vya jihadi na watu wa shirk peke yake, bali machukivu yoyote anayoyavumilia mtu kwa ajili ya kuipigania haki na uadilifu ni kujitoa mhanga kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na ni thamani ya pepo; hata kama kupigania kwenyewe ni kwa neno la kumjibu dhalimu kumsaidia mwenye haki.

Baada ya kuingilia kuandika tafsiri, nimekuwa na yakini isiyo na shaka yoyote kwamba hataingia peponi isipokuwa yule aliyeudhiwa na akavumilia kwa subira, ijapokuwa ni ukandamizwaji na balaa katika njia ya haki na uadilifu. Kwa uchache ni kuifunga nafsi yake na yaliyoharamishwa au kufanya juhudi kwa ajili ya mwingine; hata kama ni mzazi au mtoto. Kipimo cha pepo ni kuvumilia mashaka kwa kumridhisha Mwenyezi Mungu. Ama kuingia peponi kutokana na raha mstarehe ni jambo lililo mbali sana.

Ambao ukiwapata msiba husema: Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na kwake Yeye tutarejea.

Maana ya:hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, ni kukiri ufalme na utumwa; na maana ya:kwake Yeye tutarejea, ni kukubali ufufuo baada ya mauti. Kisha kujaribiwa kwa misukosuko ni mtihani ambao unadhihirisha hakika ya mtu. Mumini mwenye akili hayumbishwi na misukosuko; wala hawezi kupayuka payuka na maneno ya ukafiri na ufasiki na ujinga, bali anakuwa na subira; wala misukosuko haiwezi kumwondolea akili yake na imani yake. Ama mwenye akili na imani dhaifu anatawaliwa na shetani, anafuata mwenendo wote wa kufuru na shutuma na hushuka chini kwenye udhalili. Kauli nzuri kuhusu haya ni ile ya bwana wa mashahidi, Hussein bin Ali, siku ya msiba wa Karbala:Watu ni watumwa wa ulimwengu na dini iko kwenye ndimi zao, wanaipeleka kule kwenye maisha yao wakijaribiwa na misukosuko, huwa wachache wenye dini.

Hao juu yao zitakuwa baraka zitokazo kwa Mola wao, na rehema.

Baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu ni takrima na ni cheo cha juu; na rehema Yake kwa waja wake ni huruma yake kwao na kuwaongoza kwenye heri na kuwaneemesha.

Katika Hadith imeelezwa:Hakuna Mwislamu yeyote aliyepatwa na masaibu, akakimbilia amri ya Mwenyezi Mungu kwa kusema: Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu na kwake Yeye tutarejea. Ewe Mola wangu Wewe ndiwe unayeyatoshea masaibu yangu, basi nilipe katika masaibu hayo na unipe badali bora, isipokuwa Mwenyezi Mungu humlipa na humpa badali bora.

AINA YA MALIPO YA WANAOSUBIRI

Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa: Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amewapa wenye kusubiri aina nane za malipo na utukufu:

1. Mapenzi: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَاللَّـهُ يُحِبُّ الصَّابِرِينَ ﴾

...Na Mwenyezi Mungu anawapenda wanao subiri . (3:146).

2. Ushindi: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿إِنَّ اللَّـهَ مَعَ الصَّابِرِينَ ﴾

...Hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wanao subiri. (2:153).

3. Ghorofa za peponi: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أُولَـٰئِكَ يُجْزَوْنَ الْغُرْفَةَ بِمَا صَبَرُوا ﴾

Hao ndio watakaolipwa ghorofa kwa kuwa walisubiri. (25:75).

4. Malipo mengi: Mwenyezi Mugnu anasema:

﴿إِنَّمَا يُوَفَّى الصَّابِرُونَ أَجْرَهُم بِغَيْرِ حِسَابٍ ﴾

Hakika wanaosubiri watapewa ujira wao pasipo hisabu... (39:10)

5. Bishara: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَبَشِّرِ الصَّابِرِينَ﴾

Na wape bishara wanaosubiri. (2:155).

6 & 7. Baraka na rehema: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿أُولَـٰئِكَ عَلَيْهِمْ صَلَوَاتٌ مِّن رَّبِّهِمْ وَرَحْمَةٌ﴾

Hao juu yao zitakuwa baraka zitokazo kwa Mola wao na rehema. (2:157).

8. Uongofu: Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُهْتَدُونَ ﴾

Na hao ndio wenye kuongoka (2:157)

﴿إِنَّ الصَّفَا وَالْمَرْوَةَ مِن شَعَائِرِ اللَّـهِ فَمَنْ حَجَّ الْبَيْتَ أَوِ اعْتَمَرَ فَلَا جُنَاحَ عَلَيْهِ أَن يَطَّوَّفَ بِهِمَا وَمَن تَطَوَّعَ خَيْرًا فَإِنَّ اللَّـهَ شَاكِرٌ عَلِيمٌ ﴾

158.Hakika Swafaa na Mar-wa ni katika alama za Mwenyezi Mungu. Basi anayehiji kwenye nyumba hiyo au akafanya Umra,si kosa kwake kuvizunguuka. Na anayefanya heri, basi Mwenyezi Mungu ni Mwenye shukrani (na) Mjuzi.

SWAFA NA MARWA

Aya 158

LUGHA

Swafa na Mar-wa ni vilima viwili vilivyoko Makka karibu na Al Kaaba. Mahujaji na wanaofanya Umra huenda Saay kati ya vilima hivyo.

MAANA

Hakika Swafa na Mar-wa ni katika alama za Mwenyezi Mungu.

Ibada ziko namna mbali mbali na wakati mbali mbali. Kwa kuangalia wakati, kuna zile za kila siku ambazo ni swala, na nyingine ni za kila mwaka ambazo ni kufunga Ramadhani na pia iko ya mara moja tu, katika umri nayo ni kuhiji kwa mwenye kuweza. Hijja ni moja ya nguzo tano zilizojengewa Uislamu, ambazo ni: Shahada mbili, kusimamisha swala, kutoa zaka, kufunga Ramadhan na kuhiji Al Kaaba. Umrah ni ada kama Hijja, lakini katika Umrah hakuna kwenda Arafa, wala kulala Muzdalifa au kutupa mawe Mina. Utakuja ufafanuzi wake Inshaallah katika Aya ya 196 na Sura nyingine zinazozungumzia hilo. Kwa ujumla ni kwamba aina zote za ibada ikiwemo Hijja hazina nafasi ya kufanyiwa Ijtihadi wala kuelezwa sababu yoyote; isipokuwa inatosha nasi (nukuu) ya Quran na Hadith tu na kila ambalo litazidi hayo, Mungu (s.w.t.) hajaliridhia.

Linaloonyeshwa na Aya hii, ni kwamba Swafa na Mar-wa ni sehemu za kufanyiwa ibada kunakoonyeshwa na kauli yake:

Basi anayehiji kwenye nyumba hiyo au kufanya Umra, si kosa kwake kuvizunguka .

Kuzunguka huku ndiko kunakojulikana kwa jina la Saay kati ya Safa na Mar-wa. Ama namna ya kufunya Saay na idadi ya mizunguko yake na kuanzia Safa, utakuja ubainifu wake mahali pake Inshaallah. Unaweza kuuliza: kufanya Saay kati ya Swafa na Mar-wa katika Hijja ni wajibu kwa Ijmai pamoja na kuwa ibara ya: Si kosa, inafahamisha kufaa jambo hilo na wala sio lazima na kwamba hakuna dhambi kuliacha?

Jibu : Kauli yake Mwenyezi Mungu: Si kosa, haikuja kubainisha hukumu ya Saay kuwa ni wajibu au la, isipokuwa imekuja kubainisha kuwa Saay ni sharia na Uislamu unaikubali na kuithibisha. Ama maarifa ya hukumu yake na je, ni faradhi au ni sunna, hayo yanafahamishwa na dalili nyingine.

Zimekuja Hadith mutawatir za Mtume na wamekongamana Waislamu juu ya wajibu wa kufanya saay katika Hijja ya Kiislamu. Katika Majmaul-Bayan anasema Imam Jaffar Sadiq amesema:Waislamu walikuwa wakiona kwamba Swafa na Marwa ni mambo yaliyozushwa wakati wa Jahiliya, ndipo akateremsha Mwenyezi Mungu (s.w.t.) Aya hizi. Yaani anaziondoa dhana hizi na kubainisha kwamba Swafa na Mar-wa vinatokana na Uislamu tangu asili; washirikina wakivizunguukia huwa wanajikurubisha kwa masanamu, lakini Waislamu huwa wanavizungukia kwa kumtii Mwenyezi Mungu na kufuata amri yake.

Na anayefanya heri basi Mwenyezi Mungu ni Mwenye shukrani (na) mjuzi.

Yaani anayefanya wema kwa kufanya Saay kati ya Safa na Mar-wa baada ya kutekeleza wajibu alionao, basi Mwenyezi Mungu atamlipa wema kwa wema wake. Shaakir (mwenye shukrani) ni katika sifa za Mwenyezi Mungu, na maana ya Mwenyezi Mungu kumshukuru mja wake mtiifu, ni kuwa radhi naye na kumpa thawabu kutokana na shukrani yake na utiifu wake.


3

4

5

6

7

8

9

10

11

12