TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TATU Juzuu 3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TATU 20%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 12 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 17916 / Pakua: 3852
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TATU Juzuu 3

Mwandishi:
Swahili

1

2

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAAS|HIF JUZUU YA TATU

﴿أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِي حَاجَّ إِبْرَاهِيمَ فِي رَبِّهِ أَنْ آتَاهُ اللَّـهُ الْمُلْكَ إِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ رَبِّيَ الَّذِي يُحْيِي وَيُمِيتُ قَالَ أَنَا أُحْيِي وَأُمِيتُ قَالَ إِبْرَاهِيمُ فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ فَبُهِتَ الَّذِي كَفَرَ وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴾

258.Je, hukumjua aliyehojiana na Ibrahim juu ya Mola wake kwa sababu Mwenyezi Mungu alimpa ufalme? Ibrahim aliposema: Mola wangu ni yule ambaye huhuisha na kufisha. Yeye akasema: Mimi pia na huhuisha na kufisha. Ibrahim akasema: Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi. Akafedheheka yule aliyekufuru, na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

ALIYEHOJIANA NA IBRAHIM

Aya 258

MAANA

Mwenyezi Mungu, katika Aya iliyotangulia, amebainisha kuwa mtawala wa waumini ni Mwenyezi Mungu, na kwamba wao wanatoka katika giza la shaka kuingia kwenye mwangaza wa uongofu na imani. Na makafiri watawala wao ni mataghuti wanaowatoa kwenye mwangaza wa kimaumbile na kuwaingiza katika giza la ukafiri na upotevu. Baada ya hapo anatoa kisa, kwa Mtume wake mtukufu juu, ya Mumin aliyetoka kwenye giza la shaka na kuingia katika nuru ya imani, katika Aya ijayo. Na kisa cha kafiri aliyehojiana na Ibrahim juu ya Mola wake baada ya kutoka kwenye nuru ya kimaumbile kwenda kwenye giza la ukafiri, katika Aya hii.

Je, hukumjua yule aliyehojiana na Ibrahim juu ya Mola wake, kwa sababu Mwenyezi Mungu alimpa ufalme? Ibrahim aliposema: Mola wangu ni yule ambaye huhuyisha na kufisha. Yeye akasema: 'Mimi pia na huhuyisha na kufisha.'

Hii ni hoja anayoitaja Mwenyezi Mungu kwa Mtume na kwa watu wote katika mfumo wa kustaajabu pamoja na kukanusha. Ibrahim(a.s) alitoa mwito wa kutupiliwa mbali masanamu na mataghuti na kuwa kwenye dini ya uadilifu na usawa, lakini akapingwa na watawala., sio kwa kuona mwito wake sio sawa, bali ni kwa kuhofia manufaa na chumo lao na kupupia wasishuke vyeo vyao. Kama kawaida walianza kujadiliana na Ibrahim kwa maneno; waliposhindwa wakawa hawana la kusema, ispokuwa walitangaza vita na wakajaribu kummaliza kwa kumchoma katika moto; sawa na wanavyofanya wakoloni hivi sasa - wanaeneza propaganda za upotevu kwa njia ya magazeti, radio na mashirika ya habari yaliyonunuliwa; wakishindwa wanaanza kampeni za mapinduzi, wakishindwa hutupa mabomu ya Napalm kwa watu wanyonge wasiokuwa na hatia yoyote.

Basi yule ambaye amepetuka mpaka kwa mali na jaha alimuuliza Ibrahim: "Ni nani Mola wako?" Ibrahim akajibu: "Mola wangu ni yule anayempa uhai anayemtaka kisha huuondoa na wala hana anayeshirikiana naye katika hilo." Yule Taghuti akasema: "Mimi pia ninaweza hivyo." Akawaleta watu wawili; akamwua mmoja wao na kumwacha mwingine. Ibrahim alipoona kujigamba kwa Taghuti kwa kutegemea, maneno na kujitia kutofahamu hoja na maana halisi yaliyokusudiwa, alileta mfano mwingine ambao hauwezi kuingizwa makosa wala madai yoyote, akasema:

Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua Mashariki, basi wewe lichomoze Magharibi, Akafedheheka yule aliyekufuru

Kwa sababu alishindwa kubabaisha na kupotosha. Hivi ndivyo anavyojaribu kufanya kila mbatilifu - kujisifu na kufanya hila; hila zinaposhindwa hudangana akawa hana la kufanya. Kundi la wafasiri wamesema kuwa ni jawabu la pili la Ibrahim; la kwanza ni 'Ambaye huhuisha na kufisha' na la pili ni 'Basi wewe lichomoze magharibi' ili akate mjadala upesi bila ya kurefusha.

Razi na Sheikh Muhmmad Abduh, wanasema kuwa hilo ni kuleta mfano mwingine ili kufafanua zaidi dalili; kwa maana yakuwa yule ambaye anatoa uhai ndiye ambaye analichomoza jua kutoka mashariki; na kama ukiweza kuwafunika watu wako kwa mfano wa kwanza basi utashindwa kuwafunika katika mfano huu. Vyovyote itakavyokuwa, iwe ni majibu mawili au mifano miwili, lakini ni kwamba kafiri alishindwa na kuzibwa mdomo; na alishindwa kwa vile hana haki, naye hana haki, kwa vile ni kafiri.

Na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu

Ambao wamejidhulumu kwa kuinusuru batili na kuipinga haki. Aya haikutaja jina la Taghuti kwa sababu, muhimu ni kupata mazingatio ya kisa sio jina la mhusika. Imetangaa kwamba alikuwa ni Namrud bin Kan'an bin Sam bin Nuh. Inasemekana kwamba yeye ndiye wa mwanzo kuvaa taji kichwani; akatakabari na kudai uungu. Tutarudia kuelezea kisa cha Ibrahim na watu wake katika Sura ya Anbiya (Mitume) na sehemu nyinginezo.

﴿أَوْ كَالَّذِي مَرَّ عَلَىٰ قَرْيَةٍ وَهِيَ خَاوِيَةٌ عَلَىٰ عُرُوشِهَا قَالَ أَنَّىٰ يُحْيِي هَـٰذِهِ اللَّـهُ بَعْدَ مَوْتِهَا فَأَمَاتَهُ اللَّـهُ مِائَةَ عَامٍ ثُمَّ بَعَثَهُ قَالَ كَمْ لَبِثْتَ قَالَ لَبِثْتُ يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ قَالَ بَل لَّبِثْتَ مِائَةَ عَامٍ فَانظُرْ إِلَىٰ طَعَامِكَ وَشَرَابِكَ لَمْ يَتَسَنَّهْ وَانظُرْ إِلَىٰ حِمَارِكَ وَلِنَجْعَلَكَ آيَةً لِّلنَّاسِ وَانظُرْ إِلَى الْعِظَامِ كَيْفَ نُنشِزُهَا ثُمَّ نَكْسُوهَا لَحْمًا فَلَمَّا تَبَيَّنَ لَهُ قَالَ أَعْلَمُ أَنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴾

259.Au kama yule aliyepita karibu na mji nao umeangukiana sakafu zake, akasema: Mwenyezi Mungu atauhuisha vipi (mji) huu baada ya kufa kwake? Mwenyezi Mungu akamfisha kwa miaka mia, kisha akamfufua, akamuuliza: Umekaa muda gani? Akasema: Nimekaa muda wa siku moja au sehemu ya siku. Akasema: Bali umekaa miaka mia, tazama chakula chako na kinywaji chako hakikuharibika. Na mtazame punda wako na ili tukufanye uwe ni ishara kwa watu. Na itazame mifupa jinsi tunavyoinyanyua,kisha tunaivisha nyama. Basi yalipombainikia alisema: Najua kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu.

ALIYEPITA KARIBU NA MJI

Aya ya 259

MAANA

Aya iliyotangulia ilikuwa ni mfano kwa kafiri ambaye amemfanya Taghuti kuwa ni mlinzi na mtawala wake, na kutoka katika mwangaza na kuingia katika giza; na Aya hii ni mfano wa Mumin aliyemfanya Mwenyezi Mungu kuwa mtawala wake; akatoka gizani na kuingia katika mwangaza.

Au kama yule aliyepita karibu na mji nao umeangukiana sakafu zake akasema: Mwenyezi Mungu ataufufua vipi (mji) huu baada ya kufa kwake?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakufafanua jina la mji wala jina la aliyepitia, Hapo ndipo wakahitalifiana wafasiri - kwamba je, mtu huyo alikuwa kafiri, je alikuwa Uzairi (Ezra), Armila (Nehemia) au Khidhr? Vile vile wametofautiana kuhusu mji,je ulikuwa Baitil Maqdis au mji mwingine? Hakuna dalili yoyote juu ya hayo isipokuwa Hadith za Kiisrail tu. Maana ya mji ulioangukiana sakafu zake ni kuwa hauna watu na majumba yamevunjika umebaki magofu; na swali lilikuwa la kuuliza kufufuliwa watu wa mji sio mji wenyewe.

Yule anayedai kuwa aliyepita katika mji alikuwa kafiri kwa vile alitia shaka katika kudura ya Mwenyezi Mungu, tunamwambia kuwa, sio kila anayepitiwa na shaka akilini mwake na akataka ufafanuzi, ni kafiri; bali ni kinyume cha hivyo. Ibrahim alimtaka Mola wake amuonyeshe anavyohuisha waliokufa na hali yeye alikuwa akilingania imani na yakini. Zaidi ya hayo ni kwamba kutaka kujua zaidi kudura ya Mwenyezi Mungu ndio imani yenyewe. Kwa hivyo basi linabainika kosa la anayedai kuwa aliyepita mjini alikuwa kafiri sio kwa jengine ispokuwa tu, ati amesema: Mwenyezi Mungu ataufufua vipi (mji) huu baada ya kufa kwake? Hapana! Huko sio kukanusha, isipokuwa kubomoka huko alikokuona kulimfanya apigwe na butwaa na kushindwa kujua njia ambayo itawarudishia uhai watu wa mji huo.

Mwenyezi Mungu akamfisha kwa miaka mia.

Hayo yalikuwa ni mauti ya hakika sio majazi, Hapo hapahitaji taawil.

Kisha akamfufua

Alimfufua kama alivyokuwa. Wala si zito hilo kwa ambaye anauambia ulimwengu na kilicho katika ulimwengu 'kuwa', kikawa. Hakuna kitu cha ajabu kabisa kama kumlinganisha Muumbaji na viumbe katika uwezo Wake.

HISABU YA KABURINI

Akamuuliza: Umekaa muda gani?

Hili ni swali la kuthibitisha, sio la kutaka kufahamu.

Akasema: Nimekaa muda wa siku moja au sehemu ya siku.

Lau si Ijmai (kongamano la wanavyuoni) na hadithi ingeliwezekana kusema kuwa hakuna hisabu kaburini wala kuulizwa, isipokuwa siku ya ufufuo kwa kutegemea Aya hii na Aya nyingine inayosema:

﴿وَيَوْمَ تَقُومُ السَّاعَةُ يُقْسِمُ الْمُجْرِمُونَ مَا لَبِثُوا غَيْرَ سَاعَةٍ﴾

"Na siku kitakaposimama kiyama wataapa wenye makosa kuwa hawakudumu isipokuwa saa moja tu ..." (30:55)

Wala hakuna sababu ya wakosaji kuapa na kughafilika na muda uliopita toka kufa kwao isipokuwa kwa kukosa uhai, kwa sababu kuhisi muda hakuwi isipokuwa mtu huyo awe na uhai. Sheikh Mufid katika kitabu Awailul Maqalat anasema kwamba, watu baada ya kufa wako tabaka nne: Tabaka ya kwanza ni yule aliyeijua haki na akaitumia, Huyu atapewa uhai mzuri baada ya mauti kabla ya kufufuliwa. Tabaka ya pili ni yule aliyeijua haki na asiitumie kwa inadi. Huyu vile vile atakuwa hai lakini ataadhibiwa, Tabaka ya tatu ni yule aliyefanya madhambi na maasi kwa kupuuza, sio kwa inadi. Huyu uhai wake ni wenye kutiliwa shaka baada ya kufa na kabla ya kufufuliwa. Tabaka ya nne ni wenye kuzembea kufanya twaa bila ya inadi na walio wanyonge. Hawa hawatafufuliwa, bali watabaki katika ulimwengu wa mauti mpaka siku ya kufufuliwa.

Sheikh Mufid amechukua ugavi huu kutokana na riwaya za Ahlul bait(a.s) ; miongoni mwa hizo ni: "Hataadhibiwa kila maiti, isipokuwa ataadhibiwa kwa ukafiri hasa na atapata neema kwa imani hasa; na wasiokuwa hawa wawili watapuuzwa na wala hawataulizwa mpaka siku ya ufufuo. "Haya tumeyazungumza kwa ufafanuzi katika kitabu Falsafatul Mabdai Wal Ma'ad mlango wa "Baina ya dunia na akhera" na mlango "Hisabu ya kaburi"

Akasema: Bali umekaa miaka mia, tazama chakula chako na kinywaji chako hakikuharibika.

Amesema hakikuharibika na hakusema havikuharibika, kwa maana ya kuwa chakula na kinywaji ni aina moja tu katika kuharibika haraka. Maana ya hakikuharibika ni kwamba havikubadilika, pamoja na kupita miaka, bali vimebakia katika hali yake. Huu ni muujiza wa Mungu, kwa sababu chakula na kinywaji huharibika haraka. Hapa nahofia yule anayejaribu kuiambatanisha Qur'an na sayansi asije akasema kuwa vilikuwa katika jokofu (friji).

Na mtazame punda wako

Jinsi alivyogeuka na kuoza, lakini chakula na kinywaji vimebakia katika hali yake.

Huu ndio muujiza zaidi na kudhihirisha kudura inavyogeuza kawaida. Kwa sababu anga ndiyo inayoathiri, kinywaji kingeharibika kabla ya punda, kwa sababu ndiye mwenye nguvu kuliko chakula na kinywaji. Kwa hivyo kufa punda na kudumu chakula, ni dalili ya kuwa Mwenyezi Mungu hashindwi na kitu chochote.

Inasemekana kuwa punda alibakia hai miaka mia bila ya kinywaji wala chakula, Kwa hali zote mbili, ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliyafanya hayo ili aondoe kustaajabu kwa Uzayr na kuona kwake ajabu ya kufufuliwa kwa mji huo; na pia ili amfanye kuwa ni hoja ya kupatikana ufufuo kwa yule atakayejua hali yake katika watu wa wakati huo. Hayo ndiyo makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Na ili tukufanye uwe ni ishara kwa watu"

Na itazame mifupa jinsi tunavyoinyanyua, kisha tunaivisha nyama

Wamehitalifiana kuhusu mifupa hii: Je ilikuwa ya Uzair au mifupa ya punda wake? Msemaji mmoja alisema kwamba hiyo ni mifupa ya mwenye punda, na kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifufua jicho lake kwanza ili aone sehemu iliyobakia ya mwili jinsi inavyokusanyika na kupata uhai. lakini huku ni kujisemea tu juu ya Mwenyezi Mungu bila ya elimu. Lenye nguvu zaidi ni kwamba hiyo ni mifupa ya punda kwa sababu mwenye punda alisema: "Nimekaa muda wa siku moja au sehemu ya siku." Kwani lau angeliiona mifupa yake ilivyoharibika, angelitambua urefu wa muda aliokaa Mwenyezi Mungu aliivika nyama; sawa na alivyoanza kumuumba. Imam Ali(a.s) anasema:"Kuisha dunia baada ya kuweko sio ajabu kuliko kuianzisha."

Basi yalipombainikia alisema: Najua kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza juu ya kila kitu.

Aliyasema haya baada ya kupitiwa na majaribio binafsi yasiyo na shaka. Vipi atie shaka na yeye ameshuhudia kwa macho miujiza mitatu: Kurudishwa hai baada ya kufa, kufufuliwa punda wake na kudumu chakula chake miaka mia bila kuharibika. Funzo tunalolipata kutokana na kisa hiki ni kwamba mwenye akili hatakikani kukanusha lile lisilotambuliwa na akili yake, au lisiloafikiana na aliyoyasoma katika kitabu au kusikia kutoka kwa mwalimu wake, bali inatakikana ajizuie hata lile analoona linatofautiana na kanuni za kimaumbile.Elimu imethibitisha kuwa hakuna kanuni ya maumbile kabisa.

﴿وَإِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ رَبِّ أَرِنِي كَيْفَ تُحْيِي الْمَوْتَىٰ قَالَ أَوَلَمْ تُؤْمِن قَالَ بَلَىٰ وَلَـٰكِن لِّيَطْمَئِنَّ قَلْبِي قَالَ فَخُذْ أَرْبَعَةً مِّنَ الطَّيْرِ فَصُرْهُنَّ إِلَيْكَ ثُمَّ اجْعَلْ عَلَىٰ كُلِّ جَبَلٍ مِّنْهُنَّ جُزْءًا ثُمَّ ادْعُهُنَّ يَأْتِينَكَ سَعْيًا وَاعْلَمْ أَنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴾

260.Na Ibrahim aliposema: Mola wangu! Nionyeshe jinsi unavyofufua wafu, (Mwenyezi Mungu) akasema: Huamini? Akasema: Kwa nini! (naamini) Lakini upate kutulia moyo wangu. Akasema: Basi chukua ndege wanne na uwakusanye kisha (uwachinje) uweke juu ya kila jabali sehemu katika wao. Kisha waite, watakujia mbio. Na jua kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

ILI MOYO WANGU UTULIE

Aya 260

MAANA

Maana ya Aya iko wazi, lakini wafasiri wanataka kupata sababu ya kusema kwa hali yoyote itakayokuwa. Kwa hiyo wakaulizana sababu iliyomfanya Ibrahim kuuliza hivi, pamoja na kujua kwamba yeye anaamini ufufuo kwa imani isiyo na shaka yoyote. Kisha wakahitalifiana katika jawabu lake kwa kauli kumi na mbili alizozitaja Razi Utafiti wao hauna msingi wowote, kwa sababu kuamini ghaibu hakupingani na kutaka kushuhudia kwa macho. Kwani kila mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu na Malaika Wake na yaliyokuja katika vitabu vyake katika habari za ghaibu, anatamani kushuhudia kwa macho yale aliyoyaamini kwa njia ya ghaibu na wahyi, isipokuwa Ali bin Abu Twalib aliyesema:"Lau nitaondolewa pazia siwezi kuzidisha yakini (yangu)" Vyovyote iwavyo Khalilurrahman (rafiki wa Mwenyezi Mungu)(a.s) aliamini ufufuo kwa imani ya ghaibu kwa njia ya wahyi, kama Mitume wengine; kisha akapenda kushuhudia tukio kwa macho yake baada ya kushuhudia kwa moyo wake na akili yake. Kwa hilo zitatimia kwake njia zote za maarifa - kwa moyo, akili na majaribio. Mwenyezi Mungu alilikubali ombi lake, akamwamrisha kuchukua ndege wane, awakusanye pamoja kisha awakatekate aweke fungu juu ya kila jabali; kisha awaite, watamjia haraka kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Tunalomalizia katika Aya hii ni kwamba: kutaka kufunuliwa siri ya uumbaji au ufufuo mara nyingine kunatokana na kutia shaka kwenye jambo hilo. Huko ndiko kunakopingana na kuamini kudura ya Mwenyezi Mungu na kuwa na imani na wahyi Wake na Mitume Yake. Mara nyingine kunatokana na kupenda kujua mambo na kupata maarifa pamoja na kuamini kudura ya Muumbaji na kuwa na imani na Mitume; hata kama hakuona jinsi Mwenyezi Mungu anavyofufua watu; kama ilivyokuwa kwa Ibrahim. Ombi hili halidhuru imani, lakini ni vigumu kulipata, bali haiwezekani, isipokuwa kwa Mtume, kama Ibrahim ambaye imani yake haitingishiki kwa kitu chochote, hata kama Mwenyezi Mungu hangemwitikia maombi yake. Kwa hivyo basi atakayeshartisha majaribio na kuona kuwa ndio sharti la kuamini kwake ufufuo, basi yeye ni kafiri kabisa. Lau angelikuwa ni mwenye kuamini kudura ya Mwenyezi Mungu kweli, asingelikuwa na haja ya sharti hili, kwa sababu kudura yake Mwenyezi Mungu haishindwi na kitu chochote mbinguni wala ardhini.

﴿مَّثَلُ الَّذِينَ يُنفِقُونَ أَمْوَالَهُمْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ كَمَثَلِ حَبَّةٍ أَنبَتَتْ سَبْعَ سَنَابِلَ فِي كُلِّ سُنبُلَةٍ مِّائَةُ حَبَّةٍ وَاللَّـهُ يُضَاعِفُ لِمَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ﴾

261.Mfano wa wale wanaotoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa punje moja iliyochipuza mashuke saba; katika kila shuke pana punje mia. Na Mwenyezi Mungu humzidishia amtakaye, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa, Mjuzi.

﴿الَّذِينَ يُنفِقُونَ أَمْوَالَهُمْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ ثُمَّ لَا يُتْبِعُونَ مَا أَنفَقُوا مَنًّا وَلَا أَذًى لَّهُمْ أَجْرُهُمْ عِندَ رَبِّهِمْ وَلَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ﴾

262.Wale wanaotoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu kisha wasifuatishie kile walichotoa na masimbulizi wala udhia, wao wana ujira wao kwa Mola wao, wala hawatakuwa na hofu, wala hawatahuzunika.

﴿قَوْلٌ مَّعْرُوفٌ وَمَغْفِرَةٌ خَيْرٌ مِّن صَدَقَةٍ يَتْبَعُهَا أَذًى وَاللَّـهُ غَنِيٌّ حَلِيمٌ ﴾

263.Kauli njema na kusamehe ni bora kuliko sadaka inayofuatishiwa na udhia na Mwenyezi Mungu ni Mkwasi, Mpole.

PUNJE MOJA INAYOTOA MASHUKE SABA

Aya 261 263

MAANA

Mwenye kufuatilia Aya za Qur'an na kuzingatia maana zake atazikuta kuwa zinatilia umuhimu misingi mitatu:

Kueneza mwito wa Kiislamu, Jihadi na kutoa mali katika njia ya Mwenyezi Mungu. hiyo ni kwamba misingi hii mitatu ina athari kubwa katika kuupa nguvu uislamu na kuenea kwake. Kwa hivyo Qur'an imehimiza misingi hiyo kwa mifano mbalimbali ya kupendekeza na kutisha. Zimeshatangulia Aya kadhaa za kuhimiza Jihadi na kutoa mali, na zitakuja nyingine. Hivi sasa mbele yetu kuna zaidi ya Aya kumi zinazozungumzia kutoa mali; katika hizo kuna zinazomwahidi mtoaji badali ya mia saba au zaidi; nyingine zinakataza kufuatishia sadaka kwa masimbulizi na udhia; pia kuna nyingine zinazoamrisha kutoa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa nia safi, na zinazoelezea kuwa kutoa kuwe kumetokana na chumo halali na zuri, sio chumo la haramu na baya n.k.( [4] )

Mfano wa wale wanaotoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu, ni kama mfano wa punje moja iliyochipuza mashuke saba; katika kila shuke pana punje mia, Na Mwenyezi Mungu humzidishia amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni mwenye wasaa Mjuzi.

Wameulizana wafasiri, vipi Mwenyezi Mungu amepigia mfano punje inayotoa mazao haya na inajulikana kuwa haiko? Baadhi yao wakajibu kwamba hilo ni fumbo la wingi, sio kitu hasa. Wengine wamesema kuwa hayo ni makadirio; kwamba mwenye akili akijua kuwa punje yake itamletea mia saba, basi atatoa bila ya kusita. Hapana shaka kuwa wafasiri wameuweka mbali sana mfano huu, kwa vile wao wamelinganisha kilimo kilivyokuwa wakati wao; ambapo hakukuwa na zana zozote zaidi ya ng'ombe, punda na jembe la mkono. Lau wengelikuwa wakati huu wasingeona ajabu yoyote katika mifano ya Mwenyezi Mungu, baada ya elimu kuingia katika kila kitu na zana na pembejeo za kilimo zinazotumiwa.

Zaidi ya hayo kutoa kwa Mola hakupungui wala hakudhibitiki. Kwa hiyo ongezeko la mia saba sio kiwango cha mwisho cha fadhila zake na kutoa Kwake. Kwa ajili hiyo ndipo akasema:"Na Mwenyezi Mungu humzidishia amtakaye" Kama ambavyo ongezeko la mia saba linaweza kuzidi, basi vile vile linaweza kupungua, kulingana na hali ya kutoa kwenyewe. Huenda shillingi moja anayoitoa mtu na huku anaihitaji ikawa bora mbele za Mwenyezi Mungu kuliko shilingi elfu zinazotolewa na aliyetosheka nazo. Vile vile shilingi moja inayotolewa kwa ajili ya kuinua haki, dini na maadili, au inayotolewa katika manufaa ya watu na kuwatoa katika dhulma na ufukara, shilingi hiyo ambayo athari yake itabaki na manufaa yake kudumu muda mrefu, ni bora mara millioni kuliko maelfu yanayotumiwa katika anasa na maarusi ya watoto.

Wale wanaotoa mali zao katika njia ya Mwenyezi Mungu, kisha wasifuatishie kile walichotoa na masimbulizi wala udhia, wana ujira wao kwa Mola wao.

Mwenye Majmaul Bayan amesema: "Kusimbulia ni kumwambia uliyempa: Je, sikukufanyia wema? Au je, sikukupa? Na adha ni kusema: "Mwenyezi Mungu anipumzishe kwa kuniepusha nawe na aniondolee balaa kwa ajili yako." Maana ni kuwa, kutoa kunakobadilishiwa ziada na Mwenyezi Mungu, ni kule ambako mwelekeo wake ni kwa Mwenyezi Mungu peke Yake, sio kwa kutaka umashuhuri na kujionyesha na kuaibisha, kwa sababu hilo linabatilisha thawabu.

Kauli njema na kusamehe ni bora kuliko sadaka inayofuatishiwa na udhia.

Kauli njema ni maneno yanayokubaliwa na nyoyo. Makusudio ya kusamehe hapa ni kumsamehe mwenye kuomba ikiwa anaomba kwa lazima, au kutoa ufedhuli ikiwa mtu hakupata alichoomba; kama ilivyo kwa baadhi ya waombaji. Yaani kumkabili muombaji kwa maneno mazuri na kuwa na subira naye, ni bora mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko kutoa kwenye kukabiliana na maudhi. Mtume(s.a.w.w) anasema:"Muombaji akiomba msimkate maneno mpaka amalize, kisha mjibuni kwa upole; ama iwe ni kumpa (japo) kichache au kumwambia vizuri"

Na Mwenyezi Mungu ni Mkwasi.

Wa sadaka zote na twaa, na sisi ni mafukara tunaohitaji msaada wake, upole wake na thawabu zake.

Mpole

Hafanyi haraka kutoa adhabu katika maisha haya, isipokuwa anamwacha muasi mpaka siku isiyokuwa na shaka.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تُبْطِلُوا صَدَقَاتِكُم بِالْمَنِّ وَالْأَذَىٰ كَالَّذِي يُنفِقُ مَالَهُ رِئَاءَ النَّاسِ وَلَا يُؤْمِنُ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ فَمَثَلُهُ كَمَثَلِ صَفْوَانٍ عَلَيْهِ تُرَابٌ فَأَصَابَهُ وَابِلٌ فَتَرَكَهُ صَلْدًا لَّا يَقْدِرُونَ عَلَىٰ شَيْءٍ مِّمَّا كَسَبُوا وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الْكَافِرِينَ ﴾

264.Enyi mlioamini! Msiharibu sadaka zenu kwa masimbulizi na udhia; kama yule anayetoa mali yake kwa kuwaonyesha watu; wala hamwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho. Basi mfano wake ni kama mfano wa jabali ambalo juu yake pana udongo, kisha likafikiwa na mvua kubwa na ikaliacha tupu. Hawana uwezo wa chochote katika walivyovichuma; na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu makafiri.

﴿وَمَثَلُ الَّذِينَ يُنفِقُونَ أَمْوَالَهُمُ ابْتِغَاءَ مَرْضَاتِ اللَّـهِ وَتَثْبِيتًا مِّنْ أَنفُسِهِمْ كَمَثَلِ جَنَّةٍ بِرَبْوَةٍ أَصَابَهَا وَابِلٌ فَآتَتْ أُكُلَهَا ضِعْفَيْنِ فَإِن لَّمْ يُصِبْهَا وَابِلٌ فَطَلٌّ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ ﴾

265.Na mfano wa wale wanaotoa mali zao kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na uimara wa nafsi zao ni kama mfano wa bustani iliyo mahali pa juu, ikafikiwa na mvua kubwa ikatoa mazao yake maradufu; na isipofikiwa na mvua kubwa, basi manyunyu (huitoshea), Na Mwenyezi Mungu anayaona mnayotenda.

MUSIHARIBU SADAKA ZENU

Aya 264 -265

MAANA

Enyi mlioamini! Msiharibu sadaka zenu kwa masimbulizi na udhia; kama yule anayetoa mali yake kwa kuwaonyesha watu.

Katika Aya zilizotangulia Mwenyezi Mungu (s.w.t) amebainisha kwamba kuacha kusimbulia na kuudhi ni sharti la kupatikana malipo na thawabu katika kutoa; na kukosa kutoa sadaka na kauli njema ni bora kuliko kusimbulia na kuudhi, vilevile kwamba mwenye kutoa bila ya masimbulizi na udhia, atapewa malipo na thawabu bila ya hisabu; Akapigia mfano hilo kwa punje moja inayomrudishia mkulima punje mia saba. Baada ya kubainisha haya yote anampigia mfano, katika Aya hii mwenye masimbulizi na adha kuwa sawa na mnafiki anayejionyesha, ambaye anatoa mali yake kwa kutaka sifa kwa watu, sio kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na thawabu zake.

Wala hamwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho.

Yaani kitendo cha ria (kujionyesha) ni sawa na cha kafiri, kwa sababu wote hao hawataki radhi ya Mweneyzi Mungu. Kwa ajili hiyo ndipo zikaja Hadith Mutawatir kwamba: ria ni shirk iliyojificha.

Basi mfano wake ni kama mfano wa jabali ambalo juu yake pana udongo, kisha likafikiwa na mvua kubwa na ikaliacha tupu. Hawana uwezo wa chochote katika walivyovichuma.

Mwenyezi Mungu kwanza amemfananisha mwenye kusimbulia anayeudhi na mnafiki anayejionyesha; kisha akamfananisha na jabali ambalo juu yake pana udongo. Kwa dhahiri ni kwamba shabihi wa shabihi ni shabihi, kama vile rafiiki wa rafiki. Kwa hiyo inakuwa, mwenye kusimbulia anayeudhi, mnafiki na mwenye kuudhi na mwenye kujionyesha ni sawa na udongo juu ya jabali, na adha na ria ni kama mvua ambayo inaondosha udongo huo.

Na kauli ya Mwenyezi Mungu:"Hawana uwezo wa chochote." Maana yake ni kuwa: kama ambavyo hakuna yeyote katika viumbe anayeweza kurudisha udongo huo, vile vile hawawezi wenye kujionyesha na wenye kuudhi kurudisha sadaka zao. Makusudio ni kwamba: wao hawatanufaika nayo katika dunia, kwa sababu imekwishawatoka mikononi mwao; wala hawatanufaika nayo katika akhera kwa kuharibiwa na adha na ria.

Na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu makafiri

Makusudio ya kuongoza hapa, ni thawabu ya akhera, kwa sababu maneno yanahusu thawabu ya Mwenyezi Mungu, Na makusudio ya makafiri ni kila anayefanya amali kwa ajili ya mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Kuna Hadith tukufu inayosema;"Kitakapokuwa Kiyama, atanadi mnadi: 'wako wapi wale waliokuwa wakiwaabudu watu? Simameni mchukue malipo yenu kwa wale mliokuwa mkiwatumikia, kwa sababu mimi sikubali amali iliyochanganyika na kitu chochote katika dunia na watu wake.'"

Na mfano wa wale wanatoa mali zao kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na uimara wa nafsi zao, ni kama mfano wa bustani iliyo mahali pa juu, ikafikiwa na mvua kubwa ikatoa mazao yake maradufu, na kama isiponyeshewa na mvua kubwa, basi manyunyu (huitoshea).

Baada ya Mwenyezi Mungu kupiga mfano wa sadaka ya wenye kujionyesha na wenye kuudhi, amepiga mfano, katika Aya hii, sadaka ya mwenye kujitakasa; kama iliyo kawaida ya Mwenyezi Mungu kuleta mkabali wa vitu viwili vilivyo kinyume.

Ikiwa sadaka ya hao ni kama jabali lililofunikwa na mchanga, basi sadaka ya hawa ni kama bustani iliyo katika sehemu za miinuko, iliyojaa udongo ambao hauhofiwi kumomonyoka na kuondoka; sio kama ilivyo hali ya mchanga kidogo kwenye jabali; bustani hii huzaa matunda katika mwaka mara mbili zaidi ya inavyozaa bustani ya kawaida, wala haikauki kamwe kutokana na udongo wake ulivyo mzuri; inatosheka na mvua ndogo tu, kwa sababu ya rutuba yake na mazingira yake mazuri. Ama kauli yake Mwenyezi Mungu:"Kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na uimara wa nafsi zao," ni kuonyesha mambo mawili:

Kwanza : waumini wanataka radhi ya Mwenyezi Mungu kutokana na kutoa.

Pili : kutoa huku kunatokana na msukumo wa nafsi zao wenyewe na wala sio msukumo unaotoka nje.

Inasemekana kwamba uimara wa nafsi zao ni kwa maana ya kwamba wao wanajitahidi kutii kwa kutoa. Maana haya yanaweza kuwa sawa ikiwa herufi Min hapa iko katika maana ya Lam; kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿مِّمَّا خَطِيئَاتِهِمْ أُغْرِقُوا ﴾

"Kwa ajili ya makosa yao waligharikishwa ..." (71:25)

Baada ya hayo yote, Aya mbili hizi ni katika muujiza wa fasihi ambao huwezi kuupata mahali pengine isipokuwa katika maneno yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.) Kwanza, sadaka ya adha na sadaka ya ria ameifananisha na udongo ulioko kwenye jabali ambao unaondolewa na upepo na mvua. Kisha katika mkabala wa sadaka ya hasara, amefananisha na sadaka ya faida - sadaka ya imani, nayo ni kama bustani yenye rutuba inayotoa mazao kila mwaka, iwe na mvua nyingi au kidogo.

﴿أَيَوَدُّ أَحَدُكُمْ أَن تَكُونَ لَهُ جَنَّةٌ مِّن نَّخِيلٍ وَأَعْنَابٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ لَهُ فِيهَا مِن كُلِّ الثَّمَرَاتِ وَأَصَابَهُ الْكِبَرُ وَلَهُ ذُرِّيَّةٌ ضُعَفَاءُ فَأَصَابَهَا إِعْصَارٌ فِيهِ نَارٌ فَاحْتَرَقَتْ كَذَٰلِكَ يُبَيِّنُ اللَّـهُ لَكُمُ الْآيَاتِ لَعَلَّكُمْ تَتَفَكَّرُونَ ﴾

266.Je, mmoja wenu anapenda kuwa na kitalu cha mitende na mizabibu ipitayo mito kati yake, naye humo hupata mazao ya kila namna, na uzee ukamfikia, kisha ana watoto walio dhaifu; mara kifikiwe na kimbunga chenye moto kiungue? Hivi ndivyo anavyowabainishia Mwenyezi Mungu ishara ili mpate kufikiri.

JE, MMOJA WENU ANAPENDA…?

Aya ya 266

MAANA

Aya hii inamwambia kila mwenye kufanya amali na akaifuatishia na jambo litakaloondoa malipo yake na thawabu zake; kama vile masimbulizi, udhia, kujionyesha, ukafiri na shirk. Hali ya kila mmoja katika hawa ni sawa na mwenye shamba analopatia manTafsir ufaa yeye na watoto wake, likapatwa na janga kubwa, likaangamia wakati ambapo analihitajia sana kutokana na uzee wake na udhaifu wa watoto wake ambao hawajaweza kujitegemea; na wala hana kitu kingine zaidi ya shamba hilo. Mfano huo ni kwamba mwenye kufanya heri, akaiharibu, siku ya Kiyama atakuwa na haja sana ya thawabu za amali alizozifanya, lakini atakuta amali zake zimekwenda bure, kwa vile alipokuwa akizifanya, hakukusudia radhi ya Mwenyezi Mungu; na wakati huo hataweza kufanya lolote; sawa na mzee aliyeunguliwa shamba lake baada ya kuwa mzee, naye ana watoto wanyonge wanaolihitajia. Kwa mfano huu ndio tunapata tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t):

Na uzee ukamfikia, kisha ana watoto walio dhaifu; mara kimbunga chenye moto kikifikie kiungue?

Wafasiri wanasema imehusisha kutajwa mitende na mizabibu, kwa sababu ndio matunda mazuri kwa manufaa ya kiafya, ladha na mandhari pia. Lakini jibu hilo lilikuja katika wakati walioishi ambapo hapakuwa na matofaha, Matunda damu wala Machungwa au miwa. Lau wangelikuwa wakati huu wangelisema kuwa zimetajwa kwa sababu ni matunda bora ya wakati huo. Kwa hali hiyo inatubainikia kwamba hukumu juu ya vitu vya mazingira inapasa iwe kwa kulingana na kufungamana na wakati na mahali. Unaweza kuuliza: Je, maneno hayapingani kuhusu kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t): "kitalu cha mitende na mizabibu." na kauli yake: "Naye humo hupata mazao ya kila namna?" (sasa je ni mitende na mizabibu iliyomo au mazao mengine?)

Jibu : Inawezekana kuwa mitende na mizabibu ndiyo mingi zaidi katika kitalu; au inawezekana vilevile kuwa makusudio ya mazao ni manufaa, kwa maana ya kuwa mwenye shamba anapata manufaa yake yote na faida.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَنفِقُوا مِن طَيِّبَاتِ مَا كَسَبْتُمْ وَمِمَّا أَخْرَجْنَا لَكُم مِّنَ الْأَرْضِ وَلَا تَيَمَّمُوا الْخَبِيثَ مِنْهُ تُنفِقُونَ وَلَسْتُم بِآخِذِيهِ إِلَّا أَن تُغْمِضُوا فِيهِ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ غَنِيٌّ حَمِيدٌ ﴾

267.Enyi mlioamini! Toeni katika vizuri mlivyovichuma na katika vile tulivyowatolea ardhini; wala msikusudie kutoa vilivyo vibaya, hali nyinyi wenyewe msingevipokea isipokuwa kwa kuvifumbia macho. Basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mkwasi, Mwenye kusifiwa.

﴿الشَّيْطَانُ يَعِدُكُمُ الْفَقْرَ وَيَأْمُرُكُم بِالْفَحْشَاءِ وَاللَّـهُ يَعِدُكُم مَّغْفِرَةً مِّنْهُ وَفَضْلًا وَاللَّـهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ ﴾

268.Shetani anawatisha na ufukara na anawaamrisha ubakhili; na Mwenyezi Mungu anawaahidi msamaha utokao kwake na fadhila na Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu, Mjuzi.

KUTOA KATIKA VIZURI

Aya ya 267 - 268

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuhimiza sadaka katika Aya iliyotangulia na kubainisha ambayo anapaswa kusifika nayo mwenye kutoa sadaka, ikiwa ni pamoja na kumtakasia Mwenyezi Mungu katika sadaka yake na kujiepusha na ria, masimbulizi na kuudhi, sasa anataja sifa za sadaka yenyewe - kwamba inatakiwa iwe inatokana na mali nzuri na sio chafu. Hapo ndipo itakuwa sadaka imekamilika kwa njia zake. Mwenyezi Mungu anasema:

Enyi mlioamini! Toeni katika vizuri mlivyovichuma na katika vile tulivyowatolea kutoka ardhini

Lau tukiangalia Aya hii kwa dhahiri bila ya kuangalia Hadith za Mtume zilizobainisha wajibu wa kimali na kuweka kiwango cha kiasi chake na matumizi yake na pia aina yake, tungelifahamu kwamba katika mali yote anayochuma mtu kuna haki ya Mwenyezi Mungu ambayo anapaswa kuitoa kwa ajili ya radhi yake Mwenyezi Mungu (s.w.t), kwa sharti ya kutoa kizuri katika anavyovimiliki sio vibaya. Aya iliyo wazi zaidi ya hii ni ile inayosema:

﴿لَن تَنَالُوا الْبِرَّ حَتَّىٰ تُنفِقُوا مِمَّا تُحِبُّونَ﴾

"Hamtapata wema mpaka mtoe katika vile mnavyovipenda ..." (3: 92)

Kutoa huku ni wajibu katika mali yote; ni sawa iwe imetokana na ufundi, biashara au kilimo. Vilevile urithi, madini au kitu kingine chochote, Haya ndiyo yanayofahamishwa na matamko ya Aya. Kwa sababu kutoa kumekuja kwa tamko la amri ambayo inafahamisha wajibu. Kauli yake Mwenyezi Mungu: "Katika vizuri mlivyovichuma" inakusanya uchumi wote; na kauli yake; Na katika vile tulivyowatolea kutoka ardhini" inakusanya mimea, madini na siku hizi petroli.

Lakini Hadith za Mtume - ambazo ni tafsiri na ubainifu wa Qur'an hasa Aya za hukumu za sheria - zimeweka kiwango cha mali ya Zaka au Khums, vile vile nadhiri au kafara. Zikabainisha kiasi cha kutoa na wanaopewa. Wanavyuoni wa kifiqh wamelieleza hilo kwa ufafanuzi katika mlango wa Zaka, Khums, kafara na nadhiri. Kwa hiyo Aya itakuwa ni ya kuleta sharia hiyo ya kutoa na kutilia mkazo; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿وَأَقِيمُوا الصَّلَاةَ وَآتُوا الزَّكَاةَ﴾

"Na simamisheni Swala na toeni Zaka ..." (2:110)

Wala msikusudie kutoa vilivyo vibaya

SABABU YA KUSHUKA AYA

Inasemekana kuwa sababu ya kushuka Aya ni kwamba baadhi ya Waislamu walikuwa wakitoa sadaka zile tende mbovu. Na jumla hii ni kutilia mkazo jumla ya kwanza ambayo ni "toeni katika vizuri." Kwa ujumla ni kuwa toeni vizuri na wala msitoe vibaya. Mafaqihi wametoa fatwa kwamba mwenye kumiliki aina ya mali ambayo baadhi yake ni nzuri na baadhi ni mbaya, haijuzu kwake kutoa mbaya, bali atatoa ile yenye uzuri wa wastani. Kama akichagua ile ya hali ya juu, basi ni bora zaidi. Lakini kama mali yote ni mbaya inajuzu kutoa mali mbaya kwa sababu haki inafungamana na dhati ya kitu kinachotolewa.

Hali nyinyi wenyewe msingevipokea isipokuwa kwa kuvifumbia macho.

Hii ni hoja fasaha kwa yule anayetoa sadaka mbaya, Imam Ali(a.s) anasema:"Kama unavyofanya nawe utafanyiwa." Shetani anawatisha na ufukara na anawaamrisha ubakhili. Maana ya kuwatisha na ufukara ni kuwatia wasiwasi wa kuwa na pupa na kuhofia kutoa, kuwa kunaleta ufukura na hali mbaya. Maana ya kuamrisha ovu ni kuhadaa kwa kutia kwake wasiwasi kufanya maasi na kuacha utii; kama vile ubakhili.

Na Mwenyezi Mungu anawaahidi msamaha utokao kwake na fadhila.

Mwenye kutoa vizuri katika mali yake kwa kutafuta radhi ya Mwenyezi Mungu (s.w.t), Mwenyezi Mungu amemuahidi mambo mawili:

Kwanza : kusamehe makosa yake mengi kama alivyosema:

﴿خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا ﴾

"Chukua sadaka katika mali zao, uwatakase na uwasafishe kwazo..." (9:103)

Pili : kumlipa kheri zaidi mwenye kutoa kuliko alichokitoa - Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَمَا أَنفَقْتُم مِّن شَيْءٍ فَهُوَ يُخْلِفُهُ وَهُوَ خَيْرُ الرَّازِقِينَ ﴾

"... Na chochote mtakachokitoa, basi Yeye atakilipa naye ni mbora wa wanaoruzuku" (34:39)

Miongoni mwa maneno ya hekima ya Imam Ali(a.s) ni:"Sadaka ni dawa yenye kuokoa," "Takeni riziki kwa sadaka" na"Fanyeni biashara na Mwenyezi Mungu kwa sadaka." Ilipokuwa roho ya dini inatawala kwenye nafsi na kwenye mwelekeo wa malezi na tabia za watu, ilikuwa baba anampa mtoto wake pesa na kumwamrisha kutoa sadaka kwa fukara kwa kuitakidi kwamba sadaka itamwandalia njia ya tawfik na kufaulu.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

وَوَاعَدْنَا مُوسَىٰ ثَلَاثِينَ لَيْلَةً وَأَتْمَمْنَاهَا بِعَشْرٍ فَتَمَّ مِيقَاتُ رَبِّهِ أَرْبَعِينَ لَيْلَةً وَقَالَ مُوسَىٰ لِأَخِيهِ هَارُونَ اخْلُفْنِي فِي قَوْمِي وَأَصْلِحْ وَلَا تَتَّبِعْ سَبِيلَ الْمُفْسِدِينَ ﴿١٤٢﴾

142. Na tulimwahidi Musa masiku thalathini na tukayazitimiza kwa kumi; ndipo ikatimia miadi ya Mola wake siku arubaini. Na Nabii Musa akamwambia ndugu yake Harun: Shika mahali pangu katika watu wangu na utengeneze wala usifu- ate njia ya waharibifu.

وَلَمَّا جَاءَ مُوسَىٰ لِمِيقَاتِنَا وَكَلَّمَهُ رَبُّهُ قَالَ رَبِّ أَرِنِي أَنظُرْ إِلَيْكَ قَالَ لَن تَرَانِي وَلَـٰكِنِ انظُرْ إِلَى الْجَبَلِ فَإِنِ اسْتَقَرَّ مَكَانَهُ فَسَوْفَ تَرَانِي فَلَمَّا تَجَلَّىٰ رَبُّهُ لِلْجَبَلِ جَعَلَهُ دَكًّا وَخَرَّ مُوسَىٰ صَعِقًا فَلَمَّا أَفَاقَ قَالَ سُبْحَانَكَ تُبْتُ إِلَيْكَ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٤٣﴾

143. Na alipofika Musa kwenye miadi yetu Na Mola wake akamsemeza, alisema: Mola wangu nionyeshe nikutazame. Akasema: Hutaniona, lakini tazama jabali, kama litakaa pahali pake ndipo utaniona. Basi Mola wake alipojionyesha kwa jabali alilifanya lenye kuvunjika vunjika, na Musa akaanguka hali amezimia. Alipozinduka alisema: kutakasika ni kwako! Natubu kwako na mimi ni wa kwanza wa wanaoamini.

قَالَ يَا مُوسَىٰ إِنِّي اصْطَفَيْتُكَ عَلَى النَّاسِ بِرِسَالَاتِي وَبِكَلَامِي فَخُذْ مَا آتَيْتُكَ وَكُن مِّنَ الشَّاكِرِينَ ﴿١٤٤﴾

144. Akasema: Ewe Musa! Mimi nimekuteua kwa watu kwa ujumbe wangu na kwa kusema nawe kwangu; basi yashike ninayokupa, na uwe miongoni mwa wanaoshukuru.

وَكَتَبْنَا لَهُ فِي الْأَلْوَاحِ مِن كُلِّ شَيْءٍ مَّوْعِظَةً وَتَفْصِيلًا لِّكُلِّ شَيْءٍ فَخُذْهَا بِقُوَّةٍ وَأْمُرْ قَوْمَكَ يَأْخُذُوا بِأَحْسَنِهَا سَأُرِيكُمْ دَارَ الْفَاسِقِينَ ﴿١٤٥﴾

145. Na tukamwandikia katika mbao kila kitu mawaidha na ufafanuzi wa kila jambo. Basi yashike kwa imara na uwaamrishe watu wako washike mazuri yake zaidi, Nitawaonyesha makao ya wafasiki.

Aya 142 – 145

MAANA

Na tulimwahidi Musa masiku thalathini na tukayazitimiza kwa kumi; ndipo ikatimia miadi ya Mola wake siku arubaini.

Nabii Musa(a.s) alimtaka Mola wake amteremshie Kitab atakachowaongozea watu kwenye yale wanayoyahitajia katika mambo ya dini yao. Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akamwahidi kuteremshia Kitab baada ya siku thalathini, na utaendelea ushukaji wake kwa siku kumi. Kwa ujumla itakuwa muda wa miadi na wa kushuka ni siku arubaini.

Hapa tumefafanua baada ya kueleza kwa ujumla kwenye Juz. 1 (2:51).

Na Musa akamwambia ndugu yake Harun: Shika mahali pangu katika watu wangu na utengeneze wala usifuate njia ya waharibifu.

Nabii Musa alipoondoka alimwachia mahali pake ndugu yake Harun kwa Wana wa Israel; akampa nasaha kusimamia mambo yao na kuyatengeneza. Akamhadharisha na tabia zao zinazopondokea zaidi kwenye ufisadi. Ni jana tu walipokodolea macho ibada ya masanamu mpaka Nabii Musa akawaambia kuwa ni watu wajinga.

Harun akakubali nasaha kwa moyo mkunjufu, kama anavyokubali nasaha kaimu kiongozi mwenye ikhlasi kutoka kwa kiongozi wake mwaminifu.

Na alipofika Nabii Musa kwenye miadi yetu ambayo aliiweka Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumpa Tawrat,

Na Mola wake akamsemeza bila ya kumwona kwa sababu:

وَمَا كَانَ لِبَشَرٍ أَن يُكَلِّمَهُ اللَّـهُ إِلَّا وَحْيًا أَوْ مِن وَرَاءِ حِجَابٍ أَوْ يُرْسِلَ رَسُولًا ﴿٥١﴾

“Haikuwa kwa mtu aseme na Mwenyezi Mungu ila kwa wahyi au kwa nyuma ya pazia au kumtuma mjumbe” (42:51)

Nabii Musa alisema:Mola wangu nionyeshe nikutazame.

Baadhi ya maulamaa wanasema kuwa Nabii Musa hakumwomba Mola wake kumwona kwa ajili yake isipokuwa ni kwa ajili ya watu wake. Lakini hii inapingwa na kauli yake Nabii Musa pale aliposema:

Kutakasika ni kwako, na natubu kwako.

Vyovyote iwavyo ni kwamba Nabii Musa alitaka kuona, ni sawa iwe ni kwa ajili yake au kwa ajili ya wengine, sisi hatuoni ubaya wowote katika ombi hili, kwa sababu nafsi ya mtu ina hamu ya kutaka kujua yanayokuwa na yasiyokuwa hasa kuona kile ambacho kitazidisha utulivu wa nafsi.

Ibrahim(a.s) alitaka mfano wa hayo. Angalia Juz.3 (2:260).

Akasema: Hutaniona.

Kwa sababu kumwona Mwenyezi Mungu ni muhali. Tumeyazungumza hayo kwa ufafanuzi katika kufasiri Juz. 1(2:51).

Lakini tazama jabali, kama litakaa mahali pake utaniona.

Nabii Musa aligeuka kwenye jabali ili amwone Mwenyezi Mungu, mara akaanguka chini na hakuona chochote. Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifanya hivi ili kumfahamisha Nabii Musa(a.s) kwamba kumwona Mwenyezi Mungu hakuwezekani kwake wala kwa mwingine.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliuwekea sharti uwezekano wa kuonekana kwake kwa kutulia mahali jabali na jabali halikutulia, Kwa hiyo kumwona Mwenyezi Mungu hakuwezekani.

Mfumo huu alioutumia Mwenyezi Mungu hapa ni kama ule wa kusema: Nitafanya hivi kunguru akiota mvi, Au akipita ngamia kwenye tundu ya sindano.

Basi Mola wake alipojionyesha kwenye jabali alilifanya lenye kuvunjika vunjika.

Yaani ilipodhihiri amri ya Mola wake; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَجَاءَ رَبُّكَ وَالْمَلَكُ صَفًّا صَفًّا ﴿٢٢﴾

“Akaja Mola wako na Malaika (wamejipanga) safu kwa safu.” (89:22).

Yaani ikaja amri ya Mola wako.

Na Musa akaanguka chini amezimia.

Akawa hana fahamu kwa kishindo cha ghafla, Mwenyezi Mungu akamhurumia akazinduka.

Alipozinduka alisema: Kutakasika ni kwako! Natubu kwako. Kwa kukuomba kukuonana mimi ni wa kwanza wa wanaoamini.

Kwa sababu wewe ni mtukufu zaidi ya kuonekana kwa jicho.

Makusudio ya wa mwanzo sio kulingana na hisabu ya wakati; isipokuwa makusudio yake ni uthabiti na kutilia mkazo.

Akasema: Ewe Musa! Mimi nimekuteua kwa watu kwa ujumbe wangu na kwa kusema nawe kwangu; basi yashike ninayokupa, na uwe miongoni mwa wanaoshukuru.”

Baada ya Nabii Musa kunyenyekea kwa muumba wake, Mwenyezi Mungu alimkumbusha neema yake, kubwa zaidi ni Utume na kuzungumza na Mwenyezi Mungu. Makusudio ya watu ni watu wa zama zake, kwa dalili ya kauli yake: Kwa ujumbe wangu. Kwani Mwenyezi Mungu aliwachagua Mitume wengi kabla ya Nabii Musa na baada yake.

Ama kuhusika kwake na kuzungumza naye hakuna dalili ya ubora zaidi. Ikiwa kunafahamisha ubora wowote basi kupelekewa roho mwaminifu kwa mwisho wa Mitume na bwana wa Mitume ndio daraja ya juu na bora zaidi.

Na tukamwandikia katika mbao kila kitu mawaidaha na ufafanuzi wa kila jambo.

Makusudio ya mbao ni Tawrat kwa sababu ndiyo aliyoteremshiwa Nabii Musa, ndani yake mna mawaidha na upambanuzi wa hukumu.

“Kila jambo ni neno la kiujumla, lakini limekusudia mahsusi; yaani kila linalofungamana na maudhui ya risala miongoni mwa mawaidha, hukumu, misingi ya itikadi, kama vile kumwamini Mwenyezi Mungu, Mitume yake na siku ya mwisho, na hukumu za sharia, kama halali na haramu. Kwa hiyo kauli yake: Mawaidha na maelezo ni ubainifu wa tafsiri ya kauli yake kila jambo. Kwa sababu makusudio ya maelezo ni kubainisha hukumu za kisharia.

Basi yashike kwa imara.

Yaani ichunge Tawrat na uitumie kwa ukweli wa nia.

Na uwaamrishe watu wako washike mazuri yake zaidi.

Kila aliloliteremsha Mwenyezi Mungu ni zuri, lakini kuna yaliyo mazuri zaidi. Mwenyezi Mungu mtukufu anasema: “Na fanyeni wema, Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema.”

Nitawaonyesha makao ya wafasiki.

Yaani fasiki na dhalimu atafikwa na majanga. Haya ndiyo niliyoyafahamu kutokana na jumla hii kabla ya kupitia tafsir, Baada ya kuzipita nikakuta kauli kadhaa. Miongoni mwazo ni kwamba Mwenyezi Mungu atawaonyesha makao ya Firauni na watu wake baada ya kuangamizwa kwao. Nyingine inasema kuwa atawaonyesha ardhi ya Sham iliyokuwa mikononi mwa waabudu mizimu wakati huo.

سَأَصْرِفُ عَنْ آيَاتِيَ الَّذِينَ يَتَكَبَّرُونَ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَإِن يَرَوْا كُلَّ آيَةٍ لَّا يُؤْمِنُوا بِهَا وَإِن يَرَوْا سَبِيلَ الرُّشْدِ لَا يَتَّخِذُوهُ سَبِيلًا وَإِن يَرَوْا سَبِيلَ الْغَيِّ يَتَّخِذُوهُ سَبِيلًا ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا وَكَانُوا عَنْهَا غَافِلِينَ ﴿١٤٦﴾

146. Nitawatenga na ishara zangu wale wanaofanya kiburi katika ardhi pasipo haki. Na wakiona kila ishara hawaiamini; na wakiona njia ya uongofu hawaishiki kuwa ndiyo njia; lakini wakiona njia ya upotofu wanaishika kuwa ndiyo njia. Hayo ni kwa sababu wao wamezikadhibisha ishara zetu na wameghafilika nazo.

وَالَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا وَلِقَاءِ الْآخِرَةِ حَبِطَتْ أَعْمَالُهُمْ هَلْ يُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٤٧﴾

147. Na wale waliozikadhibisha ishara zetu na mkutano wa akhera, amali zao zime- poromoka. Kwani watalipwa isipokuwa yale waliyokuwa wakiyatenda?

وَاتَّخَذَ قَوْمُ مُوسَىٰ مِن بَعْدِهِ مِنْ حُلِيِّهِمْ عِجْلًا جَسَدًا لَّهُ خُوَارٌ أَلَمْ يَرَوْا أَنَّهُ لَا يُكَلِّمُهُمْ وَلَا يَهْدِيهِمْ سَبِيلًا اتَّخَذُوهُ وَكَانُوا ظَالِمِينَ ﴿١٤٨﴾

148. Na baada yake watu wa Musa walimfanya ndama kutokana na mapambo yao, kiwiliwili kilichokuwa na sauti, Je, hawakuona kwamba huyo hasemi nao wala hawaongozi njia? Walimfanya na wakawa wenye kudhulumu.

وَلَمَّا سُقِطَ فِي أَيْدِيهِمْ وَرَأَوْا أَنَّهُمْ قَدْ ضَلُّوا قَالُوا لَئِن لَّمْ يَرْحَمْنَا رَبُّنَا وَيَغْفِرْ لَنَا لَنَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ ﴿١٤٩﴾

149. Na walipojuta na wakaona kwamba wamekwishapotea walisema: Kama Mola wetu hataturehemu na kutusamehe bila shaka tutakuwa miongoni mwa waliopata hasara.

NITAWAEPUSHIA AYA ZANGU

Aya 146 – 149

MAANA

Nitawatenga na ishara zangu wale wanaofanya kiburi katika ardhi pasipo haki.

Wenye kufanya kiburi katika ardhi ni wale wanaopinga haki na wasiotaka kutawaliwa nayo. Kusema kwake bila ya haki ni kwa ufafanuzi, sio kwa kuvua; sawa na kusema: “Na wakiwaua mitume bila ya haki.”

Neno Aya katika Qur’an mara nyingine hutumia kuwa ni Aya zenye misingi ya itikadi na hukumu ya sharia na mfano wake. Mara nyingine hutumi- ka kuwa ishara yaani hoja na dalili zenye kuthibitisha uungu na utume.

Ikiwa makusudio ni maana ya kwanza katika Aya hii tunayoifasiri, basi maana yatakuwa kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) anazihifadhi Aya na kuzilinda zisipotolewe; sawa na kauli yake: “Hakika sisi ndio tuliouteremsha ukumbusho huu na hakika ndio tutakaoulinda”

Na ikiwa makusudio ni maana ya pili, yaani ishara kwa maana ya dalili na hoja, basi maana ni kwamba baada ya wapinzani kujiepusha nazo na kuacha kuzisikiliza, basi Mwenyezi Mungu ataachana nao, wala hatawategemeza kwenye imani. Tumekwisha elezea hilo mara kadhaa; kama vile katika kufasiri Juz.5 (4:88).

Na wakiona kila ishara hawaiamini; na wakiona njia ya uongofu hawaishiki kuwa ndiyo njia; lakini wakiona njia ya upotofu wanaishika kuwa ndiyo njia. Hayo ni kwa sababu wao wamezikadhibisha ishara zetu na wameghafilika nazo.

Huu ni ubainifu wa hakika ya wenye kiburi na sababu inayowajibisha kiburi chao vilevile. Ama hakika yao ni kuwa wao hawajizuilii na uovu wala hawapondokei kwenye uongofu.

Sababu inayowajibisha hilo ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaletea hoja na dalili; akawataka wazichunguze, wazizingatie na wazitumie vile inavyotakikana, wakakataa na wakaendelea kuzipinga tena bila ya kuzichunguza. Lau kwamba wao wangeliziitikia na kuzichunguza dalili hizo kungeliwapelekea kuamini na kuikubali haki; wala wasingelikua na kiburi na kufanya ufisadi katika nchi.

Na wale waliozikadhibisha ishara zetu na mkutano wa akhera, amali zao zimeporomoka. Kwani watalipwa isipokuwa yale waliyokuwa wakiyatenda?

Kila asiyemwamini Mwenyezi Mungu na kukutana na Mola wake, basi yeye ni katika wale watakaoangamia kesho na yote yale aliyokuwa akijifaharisha nayo yatakuwa si lolote. Hayo ni malipo ya ukafiri wake na inadi yake.

Yamenipendeza yale aliyoyasema mfasiri mmoja Mwenyezi Mungu amughufirie na amrehemu, namnukuu: “Kuporomoka amali kunachukuliwa kama wanavyosema: ‘Ameporomokaa ngamia.’ ikiwa amekula mmea wenye sumu na tumbo lake likafura kisha akafa.

Hiyo ndiyo sifa ilivyo kwa batili inayowatokea wenye kukadhibisha ishara za Mwenyezi Mungu na kukutana na akhera, Mwongo hufura mpaka watu wanamdhania kuwa ni mkubwa mwenye nguvu, kisha huporomoka, kama alivyoporomoka yule ngamia, aliyekula mmea wa sumu.”

Na baada yake watu wa Musa walimfanya ndama kutokana na mapambo yao, kiwiliwili kilichokuwa na sauti.

Imetangulia kuelezwa katika Aya 142 kuwa Nabii Musa(a.s) alikwenda kwa miadi ya Mola wake, na kwamba yeye alimpa ukaimu nduguye Harun kwa watu wake. Vilevile imeelezwa katika Aya 138 kwamba Wana wa Israel baada ya kupita bahari walimtaka Nabii Musa awafanyie sanamu watakayoiabudu; si kwa lolote isipokuwa tu wameona ni vizuri waabudu masanamu.

Kwa hivyo mara tu Nabii Musa alipokuwa mbali nao waliitumia nafasi hiyo; Msamaria (Samiri): akakusanya mapambo ya wanawake akaten- geneza ndama; akatengeneza katika umbo ambalo liliweza kutoa sauti ya ndama.

Akawaambia huyu ni Mola wenu na Mola wa Musa; wakaingilia kumwabudu. Harun aliwakataza, lakini hakuweza kuwazuia, na hawakum- sikiliza isipokuwa wachache, Yametangulia kudokezwa hayo katika kufasiri Juz, 1 (2: 51), Pia yatakuja tena maelezo.

Aya hii tuliyo nayo, inatilia nguvu yale tuliyoyakariri katika Juzuu ya kwanza na ya pili, kuwa Israeli haithibiti ila kwenye misingi ya matamanio na hawaa; ikiwa ni kweli kuwa matamanio ni misingi.

Je, hawakuona kwamba huyo hasemi nao wala hawaongozi njia? Walimfanya na wakawa wenye kudhulumu.

Haya ndiyo mantiki ya kimaumbile na akili ambayo inakataa mtu amwabudu Mungu aliyemtengeneza kwa mkono wake, lakini waisraili hawana akili wala maumbile au dini.

Na walipojuta na wakaona kwamba wamekwishapotoea walisema: Kama Mola wetu hataturehemu na kutusamehe bila shaka tutakuwa miongoni mwa waliopata hasara.

Hii ndiyo sifa nzuri pekee na ndiyo ya kwanza na ya mwisho, iliyosajiliwa na Qur’an kwa waisrael kwa ujumla, bila ya kuangalia uchache wa wachache waliomwamini Nabii Musa hadi mwisho.

Baadhi ya Wafasiri wamechukulia dhahiri toba ya Bani Israel kwamba wakati huo ilikuwa ni masalia ya maandalizi ya wema, kisha masalia hayo yakaenda; wala haikubaki athari yoyote kwao ya kuonyesha kujiandaa kwa kheri. Kuchukulia huku hakuko mbali na ukweli na kunaashiriwa na Aya isemayo:

ثُمَّ قَسَتْ قُلُوبُكُم مِّن بَعْدِ ذَٰلِكَ فَهِيَ كَالْحِجَارَةِ أَوْ أَشَدُّ قَسْوَةً ﴿٧٤﴾

“Kisha nyoyo zenu zikawa ngumu baada ya hayo, zikawa kama mawe au ngumu zaidi” Juz.1(2: 74)

Aya hii ni baada ya kisa cha ng’ombe ambacho kilitokea baada ya kuabudu ndama.

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

وَلَمَّا رَجَعَ مُوسَىٰ إِلَىٰ قَوْمِهِ غَضْبَانَ أَسِفًا قَالَ بِئْسَمَا خَلَفْتُمُونِي مِن بَعْدِي أَعَجِلْتُمْ أَمْرَ رَبِّكُمْ وَأَلْقَى الْأَلْوَاحَ وَأَخَذَ بِرَأْسِ أَخِيهِ يَجُرُّهُ إِلَيْهِ قَالَ ابْنَ أُمَّ إِنَّ الْقَوْمَ اسْتَضْعَفُونِي وَكَادُوا يَقْتُلُونَنِي فَلَا تُشْمِتْ بِيَ الْأَعْدَاءَ وَلَا تَجْعَلْنِي مَعَ الْقَوْمِ الظَّالِمِينَ ﴿١٥٠﴾

150. Aliporudi Musa kwa watu wake naye ameghadhibika na kuhuzunika. Akasema: Ni uovu ulioje mlionifanyia nyuma yangu! Je, mmeitangulia amri ya Mola wenu na akazitupa mbao na akamkata kichwa ndugu yake akimvuta kwake. Akasema: Ewe mtoto wa mama yangu! Hakika watu hawa wamenidharau na wakakaribia kuniua. Basi usiwafurahishe maadui juu yangu wala usinifanye pamoja na watu madhalimu.

قَالَ رَبِّ اغْفِرْ لِي وَلِأَخِي وَأَدْخِلْنَا فِي رَحْمَتِكَ وَأَنتَ أَرْحَمُ الرَّاحِمِينَ ﴿١٥١﴾

151. Akasema: Mola wangu! Nisamehe mimi na ndugu yangu na utuingize katika rehema yako na wewe ni mwenye kurehemu kushinda wote wenye kurehemu.

إِنَّ الَّذِينَ اتَّخَذُوا الْعِجْلَ سَيَنَالُهُمْ غَضَبٌ مِّن رَّبِّهِمْ وَذِلَّةٌ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَكَذَٰلِكَ نَجْزِي الْمُفْتَرِينَ ﴿١٥٢﴾

152. Hakika wale walioabudu ndama, itawapata ghadhabu kutoka kwa Mola wao na madhila katika maisha ya dunia, Na hivyo ndivyo tunavyowalipa wazushi.

وَالَّذِينَ عَمِلُوا السَّيِّئَاتِ ثُمَّ تَابُوا مِن بَعْدِهَا وَآمَنُوا إِنَّ رَبَّكَ مِن بَعْدِهَا لَغَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١٥٣﴾

153. Na wale waliotenda maovu, kisha wakatubia baada yake na wakaamini, hakika Mola wako baada ya hayo ni mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

وَلَمَّا سَكَتَ عَن مُّوسَى الْغَضَبُ أَخَذَ الْأَلْوَاحَ وَفِي نُسْخَتِهَا هُدًى وَرَحْمَةٌ لِّلَّذِينَ هُمْ لِرَبِّهِمْ يَرْهَبُونَ ﴿١٥٤﴾

154. Na ilipomtulia ghadhabu Musa, aliziokota zile mbao na katika maandiko yake mna uongozi na rehema kwa wanaomwogopa Mola wao.

ALIPORUDI MUSA KWA WATU WAKE

Aya 150-154

MAANA

Aliporudi Musa kwa watu wake naye ameghadhibika na kuhuzunika.

Nabii Musa(a.s) alipokuwa mlimani akizungumza na Mola wake mtuku- fu, alipewa habari na Mola wake kuwa watu wake wameabudu ndama baada yako; kama inavyofahamisha Aya isemayo:

قَالَ فَإِنَّا قَدْ فَتَنَّا قَوْمَكَ مِن بَعْدِكَ وَأَضَلَّهُمُ السَّامِرِيُّ ﴿٨٥﴾ فَرَجَعَ مُوسَىٰ إِلَىٰ قَوْمِهِ غَضْبَانَ أَسِفًا ﴿٨٦﴾

“Akasema: Sisi tumewatia mtihani watu wako bada yako na Msamaria amewapoteza. Nabii Musa akarudi kwa watu wake kwa ghadhabu na kusikitika.” (20:85-86).

Ghadhabu ilidhihiri kwa kusema:Ni uovu ulioje mlionifanyia nyuma yangu! Je, mmeitangulia amri ya Mola wenu.

Aliwaacha kwenye Tawhid, lakini aliporudi aliwakuta kwenye shirk.

Ama amri ya Mola wao ambayo hawakuingoja ni kumngoja Nabii Musa siku arubaini.

Hii inafahamishwa na Aya isemayo:

أَفَطَالَ عَلَيْكُمُ ﴿٨٦﴾

“Je, umekuwa muda mrefu kwenu?” (20:86).

Kama ambavyo ghadhabu yake ilidhihiri kwa kauli, Vilevile ilidhihiri kwa vitendo:

Na akazitupa mbao na akamkamata kichwa ndugu yake akimvuta kwake.

Wamesema baadhi ya maulama kuwa Nabii Musa alitupa Tawrat nayo ina jina la Mwenyezi Mungu na akamvuta nduguye Harun naye ni mja mwema. Imekuwaje na Nabii Musa ni ma’sum? Baada ya kujiuliza huku wakaanza kuleta taawili na kutafuta sababu.

Ama sisi hatu hatuleti taawili wala kutafuta sababu, bali tunayaacha maneno na dhahiri yake. Kwa sababu isma haibadilishi tabia ya maumbile ya binadamu na kumfanya ni kitu kingine wala haimuondolei sifa ya kuridhia na kukasirika hasa ikiwa ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu; tena ikiwa ni ghafla kama ilivyomjia Nabii Musa(a.s) .

Amekaa na watu siku nyingi akiwafundisha tawhid na dini ya Mwenyezi Mungu, kiasi cha kutulia imani yao; halafu ghafla tu waache yote na waingie kwenye shirki bila ya sababu yoyote ya maana.

Wengine wamesema kuwa Nabii Musa alikuwa mkali na Haruna alikuwa mpole. Sisi tunasemaNabii Musa alikuwa mwenye azma kubwa, mwenye nguvu ya alitakalo na mwenye kujiamini; na Haruna naye alikuwa chini kidogo ya Nabii Musa kulingana na masilahi.

Akasema: Ewe mtoto wa mama yangu! Hakika watu hawa wamenidharau na wakakaribia kuniua. Basi usiwafurahishe maadui juu yangu wala usinifanye pamoja na watu madhalimu.

Anakusudia madui ni wale walioabudu ndama; kama kwamba anamwambia nduguye: unachinganya mimi na maadui zangu na maadui zako, tena unanivuta mbele yao wanicheke. Vipi unanichanganya nao kwenye hasira zako na mimi niko mbali nao na vitendo vyao? Tena nimewapinga na wala sikuzembea kuwapa nasaha na tahadhari!

Hapo Nabii Musa akarudi chini na kumuonea huruma nduguye, akasema: Mola wangu! Nisamehe mimi na ndugu yangu na utuingize katika rehema yako na wewe ni mwenye kurehemu kushinda wote wenye kurehemu.

Alijiombea maghufira yeye mwenyewe kwa ukali wake kwa nduguye, kisha akamuombea maghufira nduguye kwa kuhofia kuwa hakufanya bidii ya kuwazuia na shirk. Bila shaka Mwenyezi Mungu, aliitikia maombi ya Nabii Musa kwa sababu yeye ni mwenye kurehemu kushinda wenye kurehemu; na pia kujua kwake ikhlasi ya Nabii Musa na nduguye Harun.

Hakiaka wale walioabudu ndama, itawapata ghadhabu kutoka kwa Mola wao na madhila katika maisha ya dunia. Na hivyo ndivyo tunavyowalipa wazushi

Unaweza kuuliza kuwa : dhahiri ya Aya hii nikuwa wale walioabudu ndama wamekasirikiwa na Mwenyezi Mungu na hali wao walitubia na kuomba maghufira; kama ilivyoeleza Aya ya 149 ya Sura hii na Aya nyingine inasema:

ثُمَّ إِنَّ رَبَّكَ لِلَّذِينَ عَمِلُوا السُّوءَ بِجَهَالَةٍ ثُمَّ تَابُوا مِن بَعْدِ ذَٰلِكَ وَأَصْلَحُوا إِنَّ رَبَّكَ مِن بَعْدِهَا لَغَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١١٩﴾

“Kisha hakika Mola wako kwa waliotenda uovu kwa ujinga; kisha wakatubia baada ya hayo na wakatenda mema; bila shaka Mola wako ni mwingi wa maghufira mwenye kurehemu” (16:119).

Kwa hiyo vipi walazimiane na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu ya milele na laana ya daima?

Baadhi wamejibu kuwa : waabudu ndama waligawanyika mafungu mawili baada ya kurudi Nabii Musa, Kundi moja lilitubia toba sahihi. Hao ndio waliosamhewa na Mwenyezi Mungu. Na wengine waling’ang’ania ushirikina; kama vile Msamaria na wafuasi wake. Hawa ndio waliokasirikiwa na Mwenyezi Mungu na akawadhalilisha katika maisha ya duniani.

Ilivyo ni kwamba kwenye Aya hakuna ufahamisho wowote wa makundi haya. Jibu linalonasibu zaidi ni kuwa Mwenyezi Mungu alijua kuwa Mayahudi milele hawatubii wala hawatatubia toba ya kiuhakika ambayo hawatarudia. Hakia hii inafahamishwa na tabia yao na sera yao. Kwani wao walikuwa na wanaendelea kuwa ni watu wasiokatazika wala kukanyika na ufisadi na upotevu ila kwa kutumia nguvu peke yake.

Swali la pili : Mayahudi leo wanayo dola inayoitwa Israil, kwa hiyo hawana udhalili; je hili si jambo linalopingana na dhahiri ya Aya?

Jibu : Hapana! Tena hapana! Hakuna dola wala haitakuwa dola ya Mayahudi milele; kama kilivyosajili kitabu cha Mwenyezi Mungu. Israil sio dola, kama dola nyingine; isipokuwa ni kambi ya jeshi; kama vile askari wa kukodiwa waliowekwa na wakoloni kulinda masilahi yao na kuvunja nguvu za wazalendo. Tumeyathibitisha hayo katika kufasiri Juz.4 (3:112) na Juzuu nyenginezo.

Vilevile katika kitabu Min huna wa hunaka (Huku na huko) mlango wa man baa’ dinahu li shaitan (Mwenye kumuuzia dini yake shetani)

Na wale waliotenda maovu, kisha wakatubia baada yake na wakaami- ni, hakika Mola wako baada ya hayo ni mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

Maana ya Aya yako wazi, na mfano wake umekwishapita mara nyingi. Lengo la kutajwa kwake baada ya Aya iliyotangulia ni kutilia mkazo kwamba mwenye kutubia na akarudi kwa Mola wake kwa ikhlasi na asirudie maasi, kama walivyofanya waisrail, basi Mwenyezi Mungu (s.w.t) atamrehemu, awe ni mwisraili au Mkuraysh n.k.

Na ilipomtulia ghadhabu Musa, aliziokota zile mbao na katika maandiko yake mna uongozi na rehema kwa wanaomwogopa Mola wao.

Nabii Musa ni Mtume aliye ma’sum, hilo halina shaka, lakini yeye ni binadamu, anahuzunika na kufurahi, anridhia na kukasirika. Hasira zilimpanda alipoona watu wake wamertadi dini ya Mwenyezi Mungu. Hasira aliiacha alipombwa na ndugu yake, Harun; na Mungu akamwahidi kuwaadhibu walortadi.

Baada ya Nabii Musa kurudia hali yake ya kawaida, alizirudia zile mbao alizokuwa amezitupa alipokuwa amekasirika na akatulizana kutokana na yaliyomo ndani yake katika uongofu kwa yule ambaye moyo wake utaifungukia kheri na rehema zilizomo kwa yule anayeogopa adhabu ya Mwenyezi Mungu. Hekima ya Mwenyezi Mungu imepitisha kumpa radhi na rehema kila mwenye kumtii kwa kuogopa adhabu yake, na kumletea adhabu na mateso kila mwenye kuasi kwa kubweteka na rehema yake.

وَاخْتَارَ مُوسَىٰ قَوْمَهُ سَبْعِينَ رَجُلًا لِّمِيقَاتِنَا فَلَمَّا أَخَذَتْهُمُ الرَّجْفَةُ قَالَ رَبِّ لَوْ شِئْتَ أَهْلَكْتَهُم مِّن قَبْلُ وَإِيَّايَ أَتُهْلِكُنَا بِمَا فَعَلَ السُّفَهَاءُ مِنَّا إِنْ هِيَ إِلَّا فِتْنَتُكَ تُضِلُّ بِهَا مَن تَشَاءُ وَتَهْدِي مَن تَشَاءُ أَنتَ وَلِيُّنَا فَاغْفِرْ لَنَا وَارْحَمْنَا وَأَنتَ خَيْرُ الْغَافِرِينَ ﴿١٥٥﴾

155. Na Musa akachagua watu sabini katika kaumu yake kwa miadi yetu. Lilipowashika tetemeko alisema: Mola wangu! Lau ungetaka ungeliwaangamiza wao na mimi zamani. Unatuangamiza kwa sababu ya yale waliyoyafanya wajinga katika sisi? Halikuwa hilo ila ni adhabu yako, humpoteza kwayo umtakaye na kumwongoza umtakaye, Wewe ndiye mlinzi wetu. Basi tughufurie na uturehemu nawe ndiye bora wa kughufiria.

وَاكْتُبْ لَنَا فِي هَـٰذِهِ الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الْآخِرَةِ إِنَّا هُدْنَا إِلَيْكَ قَالَ عَذَابِي أُصِيبُ بِهِ مَنْ أَشَاءُ وَرَحْمَتِي وَسِعَتْ كُلَّ شَيْءٍ فَسَأَكْتُبُهَا لِلَّذِينَ يَتَّقُونَ وَيُؤْتُونَ الزَّكَاةَ وَالَّذِينَ هُم بِآيَاتِنَا يُؤْمِنُونَ ﴿١٥٦﴾

156. Na utuandikie mema katika dunia hii na katika akhera, Sisi tunarejea kwako. Akasema: Adhabu yangu nitamsibu nayo nimtakaye; na rehema yangu imekienea kila kitu. Nitaiandika kwa ajili ya wale wanaoogopa, na wanaotoa Zaka na wanaoziamini ishara zetu.

الَّذِينَ يَتَّبِعُونَ الرَّسُولَ النَّبِيَّ الْأُمِّيَّ الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ يَأْمُرُهُم بِالْمَعْرُوفِ وَيَنْهَاهُمْ عَنِ الْمُنكَرِ وَيُحِلُّ لَهُمُ الطَّيِّبَاتِ وَيُحَرِّمُ عَلَيْهِمُ الْخَبَائِثَ وَيَضَعُ عَنْهُمْ إِصْرَهُمْ وَالْأَغْلَالَ الَّتِي كَانَتْ عَلَيْهِمْ فَالَّذِينَ آمَنُوا بِهِ وَعَزَّرُوهُ وَنَصَرُوهُ وَاتَّبَعُوا النُّورَ الَّذِي أُنزِلَ مَعَهُ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿١٥٧﴾

157. Ambao wanamfuata Nabii asiyesoma wala kuandika ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawrat na Injili ambaye anawaamrisha mema na anawakataza maovu, na anawaahalalishia vizuri na kuwaharamishia vibaya, na kuwaondolea mizigo yao na minyororo iliyokuwa juu yao. Basi wale walioamini na wakamheshimu na wakamsaidia na wakafuata nuru iliyoteremshwa pamoja naye, Hao ndio wenye kufaulu.

HAIKUWA ILA NI ADHABU YAKO

Aya 155 – 157

MAANA

Na Musa akawachagua watu sabini katika kaumu yake kwa miadi yetu.

Wafasiri wamerefusha maneno kuhusu Aya hii na zikagongana kauli zao katika kuifasiri. Wakatofautiana katika kubainisha miadi, kuwa je, ni miadi ya kuteremshwa Tawrat au mingine?

Vilevile wametofautiana kuwa ni kwa nini Nabii Musa aliwachagua watu sabini katika watu wake, Je, ni kwa kuwa wao walimtuhumu Nabii Musa na kumwambia hatutakuamini mpaka tusikie maneno ya Mwenyezi Mungu kama unavyosikia wewe; ndipo akasuhubiana nao ili asikie, kama alivyosikia; au ni kwa sababu nyingine?

Vilevile wametofautiana wafasiri katika sababu ambayo aliwaadhibu Mwenyezi Mungu, Hatimae wakahitalifiana kuwa je, mtetemeko uliwaua au ulikurubia tu kuvunja migongo yao, lakini hawakufa?

Katika Aya hakuna kidokezo chochote cha yale waliyoyachagua kikundi katika wafasiri. Linalofahamika ni kuwa tu, Nabii Musa aliwachagua watu sabini ili aende nao kwa miadi ya Mola wake. Kwa hali ilivyo ni kuwa uchaguzi huo ulikuwa ni kwa amri ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu Nabii Musa hafanyi ila aliloamrishwa; na kwamba Mwenyezi Mungu ali- wateremshia hao sabini aina ya adhabu kulingana na hekima ilivyoka.

Basi hatuna cha kuthibitisha miadi ilivyo kuwa wala sababu ya kuchagua au ya adhabu.

Ni kweli kwamba kauli ya Nabii Musa kumwambia Mwenyezi Mungu:Unatuangamiza kwa sababu ya yale waliyoyafanya wapumbavu katika sisi? inafahamisha kwamba wao walifanya yaliyowajibisha maangamizi, lakini halikubainishwa walilolifanya; nasi hatuna haki ya kusema tusiyoyajua.

Lilipowashika tetemeko alisema: Mola wangu! Lau ungetaka ungeli- waangamiza wao na mimi zamani!

Nabii Musa alichagua watu sabini walio bora katika watu wake akaenda nao kwenye miadi ya Mola wake, walipofika huko wakaangamia wote akabakia, peke yake. Hilo ni tatizo la kukatisha tamaa hakuna la kufanya tena. Je, arudi peke yake kwa wa Israel? Atawajibu nini wakimuuliza watu wao?

Hakuna kimbilio kabisa isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu. Basi akanyenyekea kwa Mwenyezi Mungu amwondolee tatizo hilo na akatamani lau Mwenyezi Mungu angelimwangamiza pamoja nao kabla ya kuja nao hapa.

Kisha akasema kumwambia mtukufu aliye zaidi:

Unatuangamiza kwa sababu ya yale waliyoyafanya wajinga katika sisi?

Yaani wewe ni mtukufu na mkuu kuliko kufanya hivyo. Kwa sababu wewe ni Mpole na Mkarimu.

Halikuwa hilo ila ni adhabu yako, humpoteza kwayo umtakaye na humwongoza umtakaye.”

Neno Fitna lililofasiriwa adhabu hapa, lina maana nyingi; ikiwemo upote- vu na ufisadi; kama ilivyo katika Aya ya 26 ya Sura hii. Maana nyingine ni kupigana na majaribu, mara nyingi hutumiwa kwa maana ya adhabu; kama anavyosema Mwenyezi Mungu:

وَاتَّقُوا فِتْنَةً لَّا تُصِيبَنَّ الَّذِينَ ظَلَمُوا مِنكُمْ خَاصَّةً ﴿٢٥﴾

“Na jikingeni na adhabu ambayo haitawasibu waliodhulumu peke yao” (8:25).

Haya ndiyo makusudio yake katika Aya hii tuliyonayo, Dhamir ya hilo inarudia tetemeko ambalo limekwishatajwa. Maana ya kumpoteza amtakaye, ni kuwa Mwenyezi Mungu humpelekea tetemeko, ambalo ndio adhabu, yule amtakaye katika waja wake, na maana ya kumwongoza ni kumwepushia tetemeko amtakaye.

Maana ya kijumla ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) huteremsha adhabu kwa amtakaye anayestahiki na kumwondolea asiyestahiki. Kwa hiyo inatubainikia kuwa kauli yake halikuwa hilo ila ni adhabu yako, maana yake yanafungamana na yaliyotangulia na yaliyo baada yake; na kwamba haijuzu kuitolea dalili kuwa upotevu unatokana na Mwenyezi Mungu.

Vipi Mwenyezi Mungu ampoteze mtu kisha amwaadhibu kwa upotevu huo? Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kutaka kuwadhulumu waja. Hakika Shetani ni adui mwenye kupoteza na inatosha kuwa Mola wako ni mwongozi na mwenye kunusuru.

Kwa maelezo zaidi rudia Juz.1 (2:26).

Wewe ndiye mlinzi wetu, Basi tughufurie na uturehemu nawe ndiwe bora wa kughufuria. Na utuandikie mema katika dunia hii na katika akhera. Sisi tunarejea kwako”

Hakuna tafsir bora ya Munajat huu, kama kauli ya bwana wa mashahidi, Imam Husein bin Ali(a.s) wakati alipozungukwa na maelfu kila upande akiwa peke yake. Akakimbilia kwa Mola wake na kumtaka hifadhi dhidi ya maadui zake akisema:

“Ewe Mola wangu wewe ndiye matarajio yangu katika kila shida, Kila jambo lililonishukia wewe ni tegemeo, Ni matatizo mangapi ya kukatisha tamaa, ya kuondokewa na marafiki na kufuatwa na maadui, uliyoniteremshia, kisha nikakushitakia wewe, kwa kuwa sina mwingine zaidi yako, nawe ukanitatulia na kunifariji! Basi wewe ndiye mtawalia kila neema,mwenye kila hisani na mwisho wa matakwa yote!”

Akasema: Adhabu yangu nitamsibu nayo nimtakaye katika wananostahiki adhabu.

Kwa sababu matakwa ya Mwenyezi Mungu yanapitia kwenye haki na uadilifu tu, hakuna mchezo wala dhulma mbele ya Mwenyezi Mungu.

Razi anasema: “Amesoma Hasan: Usibu bihi man Asaa kwa sin (nitam- sibu nayo mwenyewe kufanya uovu), na Shafii amechagua kisomo hiki.”

REHMA YA MWENYEZI MUNGU INAMFIKIA IBLISII

Qur’an hutumia neno Rehma ya Mwenyezi Mungu kwa maana ya msaada wake na kwa thawabu zake. Maana ya usaidizi kutoka kwake Mwenyezi Mungu ni kwamba vitu vyote vilivyoko, hata Iblisi, vinamhitajia Mwenyezi Mungu katika kubakia kwake na kuendelea kwake; kama ambavyo vinamhitajia yeye katika asili ya kupatikana kwake, na kwamba yeye ndiye anayevisaidia kubaki wakati wote, kiasi ambacho lau msaada wake huo utakiepuka kitu kitambo kidogo cha mpepeso wa jicho, basi kitu hicho hakitakuwako tena.

Ufafanuzi zaidi wa rehma hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:

وَلَوْ يُؤَاخِذُ اللَّـهُ النَّاسَ بِمَا كَسَبُوا مَا تَرَكَ عَلَىٰ ظَهْرِهَا مِن دَابَّةٍ وَلَـٰكِن يُؤَخِّرُهُمْ إِلَىٰ أَجَلٍ مُّسَمًّى ﴿٤٥﴾

“Lau Mwenyezi Mungu angeliwachukulia watu kwa waliyoyachuma, asin- geliacha juu ya ardhi hata mnyama mmoja” (35:45).

Rehma hiyo ndiyo iliyokusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu:Na rehma yangu imekienea kila kitu hata Iblisi aliyelaaniwa. Ama rehma kwa maana ya thawabu, Mwenyezi Mungu (s.w.t) humpa anayemwamini na kumcha. Ndiyo aliyoiashiria kwa kusema kwake. Nitaiandika kwa ajili ya wale wanaoogopa maasi na wakafuata amri ya Mwenyezi Mungu na kuacha makatazo yake.

Na wanaotoa Zaka.

Ametaja Zaka badala ya Swala. Kwa sababu mtu hupituka mpaka kwa kujiona amejitoshea.

Na wanaoziamini ishara zetu ambao wanamfuata Nabii asiyesoma wala kuandika.

Rehma ya Mwenyezi Mungu ambayo ni kwa maana ya thawabu haipati isipokuwa mwenye kumwogopa Mwenyezi Mungu, akatoa mali kwa kupenda kwake na akauamini utume wa Nabii Muhammad(s.a.w.w) kama utamfikia ujumbe wake.

Amehusisha kutaja mali kutokana na tulivyoyadokezea, na pia kuwa mazungumzo ni ya Mayahudi ambao mali ndio Mola wao hakuna mwingine isipokuwa yeye. Mwenyezi Mungu amemsifu Nabii Muhammad(s.a.w.w) , katika Aya hii kwa sifa hizi zifuatazo:-

1.Nabii Asiyesoma Wala Kuandika.

Hiyo ni sifa inayomhusu yeye tu, kinyume cha Mitume wengine, kutambulisha kuwa licha ya kuwa hivyo lakini amewatoa watu kutoka katika giza mpaka kwenye mwangaza, akaathiri maisha ya umma wote wakati wote na mahali kote.

2.Ambaye Wanamkuta Ameandikwa Kwao Katika Tawrat Na Injil.

Rudia Juz.1 (2:136) na Juz.6 (4:163).

3.Ambaye Anawaamrisha Mema Na Anawakataza Maovu.

Rudia Juz, 4 (3:104 - 110).

4.Na Anawahalalishia Vizuri Na Kuwaharamishia Vibaya.

5.Na Kuwaondolea Mizigo Na Minyororo Iliyokuwa Juu Yao.

Makusudio ya minyororo ni mashaka. Mwenyezi Mungu aliwaharamishia waisrail baadhi ya vitu vizuri, vilivyodokezwa kwenye Juz.8 (6:146); kama ambavyo sharia ya Nabii Musa ilikuwa ngumu na yenye mashaka; kiasi kwamba mwenye kutubia katika waisrael hakubaliwi toba yake ila kwa kujiua:

فَتُوبُوا إِلَىٰ بَارِئِكُمْ فَاقْتُلُوا أَنفُسَكُمْ ﴿٥٤﴾

“Basi tubuni kwa Muumba wenu na jiueni” Juz.1 (2:54).

Kwa hiyo Mwenyezi Mungu amewaambia waisrael ambao wamemkuta Nabii Muhammad(s.a.w.w) kwamba wao wakisilimu watahalalishiwa vizuri vilivyokuwa haramu, na atawaondolea mashaka katika taklifa. Kwa sababu Nabii Muhammad ametumwa na sharia nyepesi isiyo na mikazo.

Basi wale waliomwamini.

Makusudio ni waliomwamini Nabii Muhammad(s.a.w.w) miongoni mwa Mayahudi na wengine.

Na wakamheshimu.

Yaani kumsaidia katika mwito wake na kumheshimu kwa cheo chake.

Na wakamsaidia juu ya maadui zake.

Na wakafuata nuru iliyoteremshwa pamoja naye.

Yaani wakafanya matendo kwa mujibu wa Qur’an.Hao ndio wenye kufaulu duniani na akhera.


5

6

7

8

9

10