TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE Juzuu 4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 15964
Pakua: 2528


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 15964 / Pakua: 2528
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NNE Juzuu 4

Mwandishi:
Swahili

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA NNE

﴿ وَلَا تُؤْتُوا السُّفَهَاءَ أَمْوَالَكُمُ الَّتِي جَعَلَ اللَّـهُ لَكُمْ قِيَامًا وَارْزُقُوهُمْ فِيهَا وَاكْسُوهُمْ وَقُولُوا لَهُمْ قَوْلًا مَّعْرُوفًا﴾

5.Wala msiwape wapumbavu mali zenu ambazo Mwenyezi Mungu amewajaalia kuwaendeshea maisha. Na muwakimu katika mali hiyo na muwavishe, na muwaambie maneno mazuri.

﴿ وَابْتَلُوا الْيَتَامَىٰ حَتَّىٰ إِذَا بَلَغُوا النِّكَاحَ فَإِنْ آنَسْتُم مِّنْهُمْ رُشْدًا فَادْفَعُوا إِلَيْهِمْ أَمْوَالَهُمْ وَلَا تَأْكُلُوهَا إِسْرَافًا وَبِدَارًا أَن يَكْبَرُوا وَمَن كَانَ غَنِيًّا فَلْيَسْتَعْفِفْ وَمَن كَانَ فَقِيرًا فَلْيَأْكُلْ بِالْمَعْرُوفِ فَإِذَا دَفَعْتُمْ إِلَيْهِمْ أَمْوَالَهُمْ فَأَشْهِدُوا عَلَيْهِمْ وَكَفَىٰ بِاللَّـهِ حَسِيبًا ﴾

6.Na wajaribuni mayatima mpaka wafikilie umri wa kuoa. Mkiwaona wana uwekevu, basi wapeni mali zao. Wala msizile kwa kuzifuja na kwa haraka kwa kuwa watakuwa wakubwa. Na aliye tajiri, basi na ajizuie; na atakayekuwa fukara, basi na ale kwa kiasi cha kawaida. Na mtakapowapa mali zao, basi washuhudizieni; na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa mhasibu.

MSIWAPE WAPUMBAVU MALI ZENU

Aya 5-6

LUGHA

Makusudio ya wapumbavu hapa ni wale wabadhirifu wanaotumia ovyo mali.

MAANA

Wala msiwape wapumbavu mali zenu.

Imesemekana kwamba msemo unaelekezwa kwa kila mwenye mali na kwamba anaamrishwa kutompa ambaye ataitumia pasipo mahali pake; ni sawa mbadhirifu awe ni mtoto au mke wa mwenye mali. Vilevile wasii wake au mtu wa kando. Pia imesemekana kuwa msemo unaelekezwa kwa mababa tu, kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewakataza kuwakabidhi watoto wao waasi mali waliyofadhiliwa na Mwenyezi Mungu na wanapozeeka wanaijutia. Ilivyo hasa ni kwamba msemo unaelekezwa kwa wasimamizi, kwa maana ya kuwa enyi wasimamizi msiwape wabadhirifu mnaowasimamia mali zao. Hilo linafahamika kutokana na Mwenyezi Mungu anavyoendelea kusema, 'Na muwakimu na muwavishe katika mali hiyo.' Kwa sababu huu ni msemo unaelekezwa kwa wasimamizi. Zaidi ya hayo Aya zilizotangulia zinawahusu wasimamizi kwa hiyo inakuwa vizuri kufungamana na hizo.

Mbadhirifu, ni yule anayetumia ovyo mali yake; huyu hawezi kutumia mali yake isipokuwa kwa idhini ya msimamizi (walii) wake. Lakini anaweza kutumia vitu visivyoambatana na mali. Tumezungumzia kwa urefu kuhusu hukumu za mbadhirifu katika kitab Fiqhul-Imam Jafer As-sadiq, mlango wa Hajr.

Unaweza kuuliza : Kama msemo ungekuwa unawahusu wasimamizi wa mali za wabadhirifu, ingelazimika kusema, 'mali zao' na wala sio 'mali zenu', Sasa imekuaje?

Jibu : Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametegemeza mali za wabadhirifu kwa wasimamizi wao kwa kuangalia kuwa ziko chini ya usimamizi wao. Na inajulikana kwamba kutegemezea kitu kunafaa hata kwa sababu ndogo tu.

KUMWAMINI MWENYEZI MUNGU NA TATIZO LA MAISHA

Mali zenu ambazo amewajaalia kuwaendeshea maisha

Razi anasema: "Maana yake ni kuwa maisha hayapatikani ila kwa mali. Ilipokuwa mali ndiyo sababu ya kuendesha maisha, ndipo Mwenyezi Mungu akaiita kuwa ni ya kuendeshea maisha kwa kutumia jina la chenye kusababishwa kwa sababu. Sababu anayomaanisha ni mali, na chenye kusababishiwa ni maisha" Mwenye kufuatilia Aya za Qur'an na Hadith za Mtume, ataona kuwa uislam umeipa kipaumbele mali katika maisha, mpaka kufikia hatua ya kulinganisha sawa na nafsi katika Aya kadhaa; kama vile Aya hii:

﴿ إِنَّ اللَّـهَ اشْتَرَىٰ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ أَنفُسَهُمْ وَأَمْوَالَهُم بِأَنَّ لَهُمُ الْجَنَّةَ﴾

"Hakika Mwenyezi Mungu amenunua kutoka kwa waumin nafsi zao na mali zao ili wapate pepo (9:111)

Hapo Mwenyezi Mungu ameuza pepo yake kwa mali itolewayo kwa ajili yake; sawa na mfanyi biashara anavyouza bidhaa yake kwa ajili ya mali inayotolewa kwa ajili ya maslahi yake. Aya nyingine ni ile isemayo;

﴿ فَضَّلَ اللَّـهُ الْمُجَاهِدِينَ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ ﴾

"Amewafadhilisha Mwenyezi Mungu wanaopigana jihadi kwa mali zao na nafsi zao" (4:95)

Kwa sababu hiyo ndipo mafakih wakasema: "Asili katika kila kitu ni halali mpaka uthibitike uharamu isipokuwa damu tupu na mali, hizo asili yake ni haramu (mpaka uthibitike uhalali)." Qur'an imetumia neno 'kheri' kwa maana ya mali katika Aya nyingi mfano:

"Na hakika yeye kwa sababu ya kupenda mali ni bakhili." (100:8) Hapo mali imetafsiriTafsir

wa kutoka neon kheri. Hata baadhi ya wafasiri wamesema kuwa neno kheri limetumika kwa maana ya mali tu katika Qur'an, lakini sisi hatuafikiani na rai hii, ingawaje twajua kuwa Aya nyingi zimeamrisha amali njema, kusaidiana kwa kheri na kujiandaa kwa kujikinga na maadui wa dini na wa nchi , na kwamba haiwezekani kutekelezeka yote isipokuwa kwa mali. Mwenyezi Mungu amekataza kurundika mali na amewakemea wanaozirundika kwa adhabu kali; kama ambavyo amekataza kufanya israfu na ubadhirifu, na kuwachukulia wabadhirifu kuwa ni ndugu za mashetani, kwa sababu ubakhili na ubadhirifu unakwamisha maendeleo na uzaliishaji unaowafaa watu. Mtume(s.a.w.w) amesema:"Mwenyezi Mungu akiitakia nyumba kheri, basi huwaruzuku watu wake wepesi katika maisha na tabia nzuri." Na Imam Ali(a.s) amesema:"Mtu hawezi kuonja hakika ya imani, mpaka awe na mambo matatu; Fiqh katika dini, subira katika masaibu na ukadiriaji mzuri katika maisha." Imam ameunganisha imani na utatuzi wa maisha katika dunia hii, kwa sababu ukadiriaji mzuri wa maisha, maana yake ni kufanya kazi vizuri na kutumia mazao ya kazi katika njia yake inayonufaisha.

Hii ni dalili wazi kuwa dini haitengani na maisha; na kwamba imewekwa kwa ajili ya maisha bila ya shaka. Yeyote atakayetenganisha dini na maisha na kuona kuwa ni kiasi cha kuwa ni nembo, ibada na kujinyima starehe tu, basi ama atakuwa ni mjinga aliyechukua dini kutoka kwa wanaoifanyia istihzai, au atakuwa ni mpinzani wa haki. Tulipofasiri Aya ya 182 ya sura iliyotangulia (Al-Imran) katika kifungu cha 'matajiri ni mawakala' tulitaja kuwa mali yote ni ya Mwenyezi Mungu na kwamba mtu anaruhusiwa kuitumia mali kwa mipaka maalum, ambayo kama ataikiuka, basi atakuwa amenyang'anya. Hebu rudia kidogo sehemu hiyo, kwani inaambatana na maudhui haya. Tunaweza kuyarudia kama ikija Aya itakayofungamana nayo na tutafafanua tuliyoyataja huko na hapa. Kwa sababu fikra haiwezi kukienea kitu kwa pande zake zote isipokuwa inaelekea yote kwenye upande ule unaogusiwa na Aya, mapokezi au tukio lolote.

Na muwakimu katika mali hiyo na muwavishe.

Msemo unaelekezwa kwa wasimamizi wa wabadhirifu. Makusudio ni kuwa wasimamizi wawatimizie mahitaji yao ya chakula, nguo, makazi masomo, kuoa n.k.

Unaweza kuuliza : Kwa nini amesema 'katika mali hiyo' na wala hakusema kutoka katika mali hiyo?

Jibu : Lau angesema kutoka katika mali hiyo, basi ingelikuwa maana yake ni kuwa atumie asili ya hiyo mali (mtaji). Kwa hiyo ingelipungua au ingelikwisha yote. Ama kusema: 'Katika mali hiyo' ni kuwa mali iwe ni mtaji wa kutafutia riziki, kwamba msimamzi aizalishe mali hiyo na matumizi ya mbadhirifu yatokane na faida sio mtaji wenyewe. Swali la pili: Kwa nini amehusisha kivazi; na inajulikana kuwa kivazi ni katika jumla ya kukimu? Jibu: Amehusisha kivazi kwa kukipa umuhimu. Kwani huenda msimamizi akakipa umuhimu chakula na kughafilika na mavazi. Ndipo Mwenyezi Mungu akaikinga dhana hii kwa kutaja kivazi waziwazi. Msimamizi wa mbadhirifu ambaye ubadhirifu wake umeanzia utotoni mpaka akakua nao, ni baba, na babu. Ama ikiwa ubadhirifu aliuanzia ukubwani (baada ya kubaleghe), basi msimamizi atakuwa ni kadhi.

Na muwaambie maneno mazuri

Baadhi ya wasimamizi huenda wakaona kuwa ni lazima wale wanaowasimamia wawasikilize na kuwatii, kama mzazi na mtoto wake. Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akazindusha kwa kauli yake hii, ili kila msimamizi amchukulie upole anayemsimamia na kumfanyia mambo yamridhishayo na yanayomtuliza roho yake.

Na wajaribuni mayatima mpaka wafikilie umri wa kuoa. Mkiwaona wana uwekevu, basi wapeni mali zao.

Aya hii inafahamisha kuwa mtoto hapewi mali mpaka awe na sifa mbili: Kubaleghe na kuwa mwekevu. Yamekongamana madhehebu yote ya Kiislam kuwa kutoa manii kunafahamisha kubaleghe; kwa mwanamume na mwanamke, katika umri wowote na hali yoyote; iwe ni usingizini au akiwa macho. Wametoa dalili kwa Aya hii na Aya nyingine isemayo:

"Na watoto miongoni mwenu watakapobaleghe, basi na wapige hodi" (24:59),ambapo limetumika neno 'hulum' lenye maana ya kukomaa mwili kijinsia. Na imethibiti Hadith kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kuwa yeye amesema; "Imeondolewa kalamu (ya kuandika amali) kwa watu watatu: Mtoto mdogo mpaka atoke manii, mwenda wazimu mpaka apone na aliyelala mpaka aamke" Ama uwekevu unathibiti kwa kupewa yatima mali yake kidogo aitumie. Ikiwa ataitumia vizuri, basi atakuwa ni mwekevu na atapewa mali yake, vyenginevyo atazuiliwa, hata kama atafikisha miaka mia. Abu Hanifa anasema: "Mbadhirifu atapewa mali yake akiwa na miaka 25 (hata kama si mwekevu), "Hashia ibni Abidin J. 5 mlango wa Hajr.

Wala msizile kwa kuzifuja.

Yaani enyi wasimamizi! Msipetuke mipaka mnayoruhusiwa katika kula mali mnazozisimamia. Kwa sababu msimamizi anaweza kula mali ya anayemsimamia kwa sharti ya kuwa awe fukara; kama itakavyoelezwa.

Na kwa haraka kwa kuwa watakuwa wakubwa.

Msimamizi anaweza kufanya haraka kuitumia mali ya yatima kwa kuhofia asiwe mkubwa akachukua mali yake. Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akakataza matumizi hayo ambayo faida yake inamwendea msimamizi, na akazindua kuhusu hatari ya uharamu wake.

Na aliyetajiri, basi na ajizuie; na atakayekuwa fukara, basi ale kwa kiasi cha kawaida.

Msimamizi ama atakuwa mwenye kujitosheleza au fukara, Kwa hiyo mwenye kujitosheleza ni lazima ajiepushe kula mali ya yatima na kukinai na riziki ya kutosha aliyopewa na Mwenyezi Mungu. Lakini kama ni fukara, basi inafaa kwake kutumia kiasi cha haja yake ya dharura bila ya kuzidisha. Kuna Hadith isemayo kuwa Mtume(s.a.w.w) aliulizwa na bwana mmoja kuhusu yatima akiwa hawezi kutumia mali yake kuwa atakula mali yake? Akamwambia: "Kula kwa njia ya kawaida," Na imesemekana atakula kwa njia ya mkopo, Lakini dhahiri ya Hadith inaibatilisha kauli hii.

Na mtakapowapa mali zao basi washuhudizeni: na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa mhasibu.

Shia na Hanafi wanasema kuwa si wajibu kwa msimamizi kushuhudiza utoaji wa mali ya anayemsimamia akiwa mwekevu au baleghe. Na amri ya kushuhudiza katika Aya hii, wameichukulia kuwa ni sunna kwa ajili ya kuondosha tuhuma na kujiepusha na uhasama. Shafii na Malik wamesema kuwa ni wajibu na wala sio sunna kwa kuchukulia dhahiri ya Aya hii.

﴿ لِّلرِّجَالِ نَصِيبٌ مِّمَّا تَرَكَ الْوَالِدَانِ وَالْأَقْرَبُونَ وَلِلنِّسَاءِ نَصِيبٌ مِّمَّا تَرَكَ الْوَالِدَانِ وَالْأَقْرَبُونَ مِمَّا قَلَّ مِنْهُ أَوْ كَثُرَ نَصِيبًا مَّفْرُوضًا﴾

7.Wanaume wana fungu katika walichoacha wazazi wawili na akraba, na wanawake (pia) wana fungu katika walichoacha wazazi wawili na akraba, kikiwa kidogo au kingi - fungu lililofaradhiwa.

﴿ وَإِذَا حَضَرَ الْقِسْمَةَ أُولُو الْقُرْبَىٰ وَالْيَتَامَىٰ وَالْمَسَاكِينُ فَارْزُقُوهُم مِّنْهُ وَقُولُوا لَهُمْ قَوْلًا مَّعْرُوفًا﴾

8.Na wakati wa kugawanya watakapohudhuria wenye ukuruba na mayatima na maskini, basi wapeni nao kitu katika hiyo na waambieni maneno mazuri.

﴿ وَلْيَخْشَ الَّذِينَ لَوْ تَرَكُوا مِنْ خَلْفِهِمْ ذُرِّيَّةً ضِعَافًا خَافُوا عَلَيْهِمْ فَلْيَتَّقُوا اللَّـهَ وَلْيَقُولُوا قَوْلًا سَدِيدًا ﴾

9.Na wachelee wale ambao lau nao kama wangeacha nyuma yao watoto wanyonge, wangehofia. Basi na wamche Mwenyezi Mungu na waseme kauli iliyo sawa.

﴿ إِنَّ الَّذِينَ يَأْكُلُونَ أَمْوَالَ الْيَتَامَىٰ ظُلْمًا إِنَّمَا يَأْكُلُونَ فِي بُطُونِهِمْ نَارًا وَسَيَصْلَوْنَ سَعِيرًا﴾

10.Hakika wale ambao wanakula mali ya yatima kwa dhulma, hakika wanakula moto matumboni mwao; na wataungua katika moto uwakao.

WANAUME WANA FUNGU

Aya 7 - 10

MAANA

Aya nne hizi, kila moja ina mtazamo wake kama ifuatavyo:

1.Wanaume wana fungu katika walichoacha wazazi wawili na akraba, na wanawake (pia) wana fungu katika walichoacha wazazi wawili na akraba, kikiwa kidogo au kingi - fungu lililofaradhiwa.

Wazazi wawili wanafahamika; na akraba ni ndugu wa karibu wa kwa baba au mama; wakiwemo watoto, wajukuu na kuendelea chini, mababa, mababu na kuendelea juu, kaka, dada na watoto wao, ami na shangazi na wajomba, mama wadogo na watoto wao. Wake kwa waume, wakubwa kwa wadogo; iwe ni shilingi moja au mamilioni. Kurithi wote hao ni lazima katika sharia ya kiislam, haijuzu kuikhalifu kwa namna yoyote ile kwa dalili ya kauli ya Mwenyezi Mungu: "Fungu lililofaradhiwa." Hiyo inabatilisha yale yaliyokuwako wakati wa ujahilia, ya kuwazuwiya wanawake na wavulana wadogo wasirithi si kwa chochote isipokuwa tu, hawapandi farasi wala hawamzuwii adui. Ndipo uislam ukathibitisha haki ya mtu kurithi kwa kuangalia umbile lake la kiutu na wala sio kwa misingi ya kuwa aweza kupigana kwa upanga na kufuma mshale.

Shia wametolea dalili Aya hii katika kubatilisha Asaba waliyoithibitisha Sunni - tutafafanua punde - ambayo ni kuwarithisha wanaume na kuacha wanawake kwa sababu fulani; kama vile ikiwa marehemu ameacha binti na mtoto wa kiume wa kaka na binti wa kaka. Hapo Sunni wanampa nusu bint, na nusu nyingine wanampa mtoto wa kiume wa kaka, lakini yule dadake hana chake ingawaje daraja ni sawa na huyu wa kiume. Au ikiwa maiti amemwacha dada, ami na shangazi Qur'an inawarithisha wake kwa waume, na wao wanawarithisha wanaume tu. Ama Mashia wao wanampa binti mali yote katika sura ya kwanza na ya pili. Kwa sababu yeye ndiye aliye karibu zaidi na marehemu kuliko kaka wa marehemu au mtoto wa kaka wa marehemu na zaidi kuliko ami yake.

2.Na wakati wa kugawanya watakapohudhuria wenye ukuruba na mayatima na maskini, basi wapeni nao kitu katika hiyo na waambieni maneno mazuri.

Makusudio ya wenye ukuruba ni jamaa wa karibu wa marehemu ambao wamezuilika kupata mirathi kutokana na kuweko walio karibu zaidi kama ndugu na mtoto au ami na ndugu n.k. Msemo katika 'wapeni' unaelekezwa kwa waritihi au manaibu wao, Ni wazi kwamba waritihi huwapa sadaka hao wakiwa mafukara. Ama mayatima na masikini waliokusudiwa hapa, ni wale ambao hawana undugu na aliyekufa. Na amri ya kutoa hapa ni ya sunna na wala sio ya wajibu. Kama vile kusema: "Toeni sadaka japokuwa ubale wa tende." Hapa kutoa sadaka sio wajibu, lakini ni sunna inayotiliwa mkazo.

3.Na wachelee (waogope) wale ambao lau nao kama wangeacha nyuma yao watoto wanyonge wangewahofia. Basi na wamche Mwenyenzi Mungu na waseme kauli iliyo sawa.

Neno 'Na wachelee', ni amri inayoelekezwa kwa wasimamizi wa mayatima maana yake ni kwamba, ni juu ya msimamizi kuifanyia mali ya yatima, kama vile ambavyo angependa yeye wafanyiwe watoto wake lau kama angekuwa amekufa, "Mtenda hutendewa"

Imepokewa kutoka kwa Imam Musa bin Jafer(a.s) Kwamba"Mwenyezi Mungu amemwandalia anayetumia vibaya mali ya yatima, mateso mara mbili. Kwanza hapa duniani, kuwa mali ya watoto wake nayo itatumiwa vibaya, Pili ni akhera, ambayo ni moto" Imam Ali(a.s) anasema:"Yafanyieni vizuri yaliyo baada ya wenzenu, watu watayafanyia vizuri yatakayokuwa baada yenu"

4.Hakika wale ambao wanakula mali ya mayatima kwa dhuluma hakika wanakula moto matumboni mwao; na wataungua katika moto uwakao.

Makusudio ya kula moto ni kula yale yawajibishayo adhabu ya moto. Hiyo ni katika kutumia kinachosababishwa ambacho ni moto kwa maana ya sababu ambayo ni kula haramu. Imeelezwa katika Hadith kwamba mwenye adhabu kubwa zaidi kati ya watu ni kiongozi dhalimu; mwenye kula mali ya yatima na mwenye kushuhudia uongo.

﴿يُوصِيكُمُ اللَّـهُ فِي أَوْلَادِكُمْ لِلذَّكَرِ مِثْلُ حَظِّ الْأُنثَيَيْنِ فَإِن كُنَّ نِسَاءً فَوْقَ اثْنَتَيْنِ فَلَهُنَّ ثُلُثَا مَا تَرَكَ وَإِن كَانَتْ وَاحِدَةً فَلَهَا النِّصْفُ وَلِأَبَوَيْهِ لِكُلِّ وَاحِدٍ مِّنْهُمَا السُّدُسُ مِمَّا تَرَكَ إِن كَانَ لَهُ وَلَدٌ فَإِن لَّمْ يَكُن لَّهُ وَلَدٌ وَوَرِثَهُ أَبَوَاهُ فَلِأُمِّهِ الثُّلُثُ فَإِن كَانَ لَهُ إِخْوَةٌ فَلِأُمِّهِ السُّدُسُ مِن بَعْدِ وَصِيَّةٍ يُوصِي بِهَا أَوْ دَيْنٍ آبَاؤُكُمْ وَأَبْنَاؤُكُمْ لَا تَدْرُونَ أَيُّهُمْ أَقْرَبُ لَكُمْ نَفْعًا فَرِيضَةً مِّنَ اللَّـهِ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيمًا حَكِيمًا﴾

11.Mwenyezi Mungu anawausia kwa watoto wenu; fungu la mwanamume ni kama fungu la wanawake wawili. Wakiwa ni wanawake zaidi ya wawili, basi watapata theluthi mbili za alichokiacha (marehemu) na akiwa ni mmoja, basi atapata nusu, Na wazazi wake wawili kila mmoja atapata sudusi ya alichokiacha akiwa ana mtoto. Akiwa hana mtoto, na akarithiwa na wazazi wake wawili, basi mama yake atapata theluthi, Akiwa anao ndugu, basi mama yake atapata sudusi, Baada ya kutoa alivyousia au kulipa deni. Baba zenu na watoto wenu hamjui ni yupi katika wao aliye karibu zaidi kwa manufaa. Ni faradhi itokayo kwa Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi, mwenye hekima.

﴿ وَلَكُمْ نِصْفُ مَا تَرَكَ أَزْوَاجُكُمْ إِن لَّمْ يَكُن لَّهُنَّ وَلَدٌ فَإِن كَانَ لَهُنَّ وَلَدٌ فَلَكُمُ الرُّبُعُ مِمَّا تَرَكْنَ مِن بَعْدِ وَصِيَّةٍ يُوصِينَ بِهَا أَوْ دَيْنٍ وَلَهُنَّ الرُّبُعُ مِمَّا تَرَكْتُمْ إِن لَّمْ يَكُن لَّكُمْ وَلَدٌ فَإِن كَانَ لَكُمْ وَلَدٌ فَلَهُنَّ الثُّمُنُ مِمَّا تَرَكْتُم مِّن بَعْدِ وَصِيَّةٍ تُوصُونَ بِهَا أَوْ دَيْنٍ وَإِن كَانَ رَجُلٌ يُورَثُ كَلَالَةً أَوِ امْرَأَةٌ وَلَهُ أَخٌ أَوْ أُخْتٌ فَلِكُلِّ وَاحِدٍ مِّنْهُمَا السُّدُسُ فَإِن كَانُوا أَكْثَرَ مِن ذَٰلِكَ فَهُمْ شُرَكَاءُ فِي الثُّلُثِ مِن بَعْدِ وَصِيَّةٍ يُوصَىٰ بِهَا أَوْ دَيْنٍ غَيْرَ مُضَارٍّ وَصِيَّةً مِّنَ اللَّـهِ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَلِيمٌ ﴾

12.Nanyi mtapata nusu ya walichokiacha wake zenu ikiwa hawana watoto, Ikiwa wana watoto; basi mtapata robo ya walichokiacha baada ya kutoa walivyousia au kulipa deni, Na wao watapata robo ya mlichokiacha ikiwa hamna mtoto, Ikiwa mna mtoto, basi watapata thumni ya mlichokiacha, baada ya kutoa mlivyousia au kulipa deni. Ikiwa mwanamume au mwanamke anayerithiwa ni mkiwa naye ana ndugu wa kike au wa kiume, basi kila mmoja katika wao atapata sudusi. Wakiwa wengi zaidi ya hivyo, basi watashirikiana katika theluthi, baada ya kutoa yaliyousiwa au kulipa deni, pasi na kuleta dhara. Ni wasia utokao kwa Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mpole.

FUNGU LA MWANAMUME NI SAWA NA MARA MBILI YA MWANAMKE

Aya 11 - 12

MAANA

Wakati wa ujahiliya, sababu za kurithi zilikuwa ni tatu;

Kwanza : Nasaba, lakini kwa wanaume tu, wanaoweza kushika silaha na kupigana. Ama wanawake na wanaume dhaifu hawakuwa na urithi. Lakini uislam ukaeneza urithi kwa wote.

Pili : Mtoto wa kupanga; yaani mtu kumfanya mtoto wa mwengine kuwa mwanawe hasa katika urithi na mengineyo. Uislam umelikataa hilo kwa kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿ وَمَا جَعَلَ أَدْعِيَاءَكُمْ أَبْنَاءَكُمْ﴾

"Wala hakuwafanya watoto wenu wa kupanga kuwa wana wenu hasa" (33:4)

Tatu : Kuliana yaamini; yaani mtu kumwambia mwenzake: "Damu yangu ni yako, utanirithi na nitakurithi." Huu ulikubaliwa na uislam kwa ufafanuzi huu ufuatao: Mwanzo ilikuwa aliyehama (Muhajiri) pamoja na Mtume(s.a.w.w) kutoka Makka kwenda Madina akimrithi mwenzake aliyehama (Muhajir) ikiwa wana urafiki wa pamoja; na ilikuwa Muhajir anarithiwa na Muhajir tu, na si mwengine hata kama yuko karibu. Vile vile baada ya Mtume kuwafungisha undugu Sahaba zake walikuwa kama ndugu wawili wanaorithiana. Lakini baadaye uislam uliyafuta haya mawili (kuhama na kufungishwa undugu) Kwa Aya isemayo;

﴿ وَأُولُو الْأَرْحَامِ بَعْضُهُمْ أَوْلَىٰ بِبَعْضٍ فِي كِتَابِ اللَّـهِ ﴾

"Na ndugu wa tumbo wana haki zaidi wao kwa wao katika kitabu cha Mwenyezi Mungu" (8:75) Vile vile katika (33:6)

Kwa hiyo wajibu wa kurithi katika uislam, umethibiti juu ya mambo mawili: Nasaba na sababu. Na sababu ni mambo mawili Ndoa na usimamizi Utakuja ubainifu kulingana na mpango wa Aya. Ufuatao ni ufafanuzi wa matamko ya Aya mbili tulizonazo ambazo hizo pamoja na zinazofuatia zinazofungamana na urithi ni ufafanuzi wa aliyoyajumlisha Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kauli yake iliiyotangulia: "Wanaume wana fungu"

1.Mwenyezi Mungu anawausia kwa watoto wenu; fungu la mwanamume ni kama fungu la wanawake wawili.

Akiwa marehemu ameacha watoto wa kiume na wa kike, wa kiume watapata sawa na sehemu ya wanawake wawili. Ikiwa wako wengine katika mirathi; kama vile mume au mke, baba au mama, au baba na mama. Kila mmoja atachukua fungu lake - kama tutakavyofafanua - na sehemu itakayobaki watapewa watoto wa kike na wa kiume; ambapo wa kike watachukua nusu ya watakayopata wa kiume. Hiyo ni kwa kuafikiana madhehebu zote za kiislam. Vilevile yameafikiana madhehebu yote kwamba, marehemu akiacha mtoto wa kiume na wajukuu, basi mtoto wa kiume atawazuia wajukuu kurithi; ni sawa wajukuu wawe wa kike au wa kiume. Yametofautia madhehebu ikiwa ataacha mtoto wa kike mmoja, wawili au zaidi bila ya kuacha mtoto wa kiume. Madhehebu mane yamesema kuwa mtoto wa kike mmoja atachukua nusu tu; wawili au zaidi watachukua theluthi mbili tu; kitakachobaki watapewa wengine.

Shia Imamia wamesema kuwa mali yote ni ya mtoto wa kike akiwa mmoja au zaidi, wengineo hawana chao, Kwa Ufafanuzi zaidi rejea kitabu chetu Ahwalushshakhsiya Alal-madhahibil Khamsa.

2.Na wakiwa ni wanawake zaidi ya wawili, basi watapata theluthi mbili za alichokiacha (marehemu). Na akiwa ni mmoja, basi atapata nusu.

Mwenye Majmaul-bayan amesema: "Dhahiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni kwamba watoto wa kike wawili hawastahiki theluthi mbili, isipokuwa zaidi ya wawili lakini Umma umesema kwa pamoja kuwa hukumu ya wawili ni sawa na ya zaidi ya wawili." Na hivi ndivyo sahihi hasa, na kila sababu au taawili zozote zinazoelezwa kuhusu zaidi ya wawili ni za kukisia tu. Hata hivyo hilo si muhimu, la muhimu zaidi ni kubainisha tofauti za madhehebu ya kiislam kuhusu mirathi ya watoto wa kike ikiwa marehemu hakuacha wa kiume. Kwa kauli moja mafakihi wameafikiana kuwa marehemu akiwa ameacha mtoto wa kike mmoja, atapata nusu kuwa ni fungu lake. Wakiwa ni wawili na zaidi watachukua theluthi mbili. Lakini wamehitalifiana kuhusu nusu itakayobaki baada ya kupewa binti mmoja na theluthi itakayobaki baada ya kupewa mabinti wawili, ipewe nani?

Sunni wamesema, itapewa kaka wa marehemu kwa kutegemea riwaya ya Taus kutoka kwa Ibn Abbas naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kwamba yeye amesema:"Yaambatanisheni mafungu na watu wake na kinachobakia ni cha asaba waume" Shia wameikanusha Hadith ya Taus; kwa sababu yeye ni mwongo mno([11] ) .

Na wamesema kuwa nusu ya pili itarudishwa kwa binti kwa hiyo atachukua mali yote. Kwa maana ya kuwa atachukua nusu kama fungu lake na nusu ya pili kwa kurudishiwa. Vile vile wakiwa wawili na zaidi watachukua theluthi iliyobaki. Dalili yao Shia ni kuwa Qur'an imefaradhisha theluthi mbili kwa wawili, na zaidi ya nusu kwa bint mmoja. Kwa hiyo hapana budi kuweko na mtu atakayechukua sehemu iliyobaki; na Qur'an haikumweleza mtu huyo, Ndio maana kukazuka kutofautiana. Kwa hivyo basi ikawa hakuna kilichosalia isipokuwa Aya hii:

Na ndugu wa tumbo wanahaki zaidi wao kwa wao. (8:75) na (33:6) Ambapo inafahamisha kuwa aliye karibu zaidi ndiye anayestahiki kuliko mwengine, Hakuna mwenye shaka kwamba binti yuko karibu zaidi ya kaka.

Zaidi ya hayo sio Shia peke yao waliosema kuwa mali yote ni ya binti mmoja au zaidi, bali Hanafi na Hambal pia wamesema kuwa marehemu akiacha binti mmoja au zaidi na asipatikane yeyote mwenye fungu au asaba basi mali yote ni ya binti, inagawaje Aya inasema: " basi watapata theluthi mbili za (mali) aliyoiacha, lakini akiwa ni mmoja basi atapata nusu" Ikiwa Aya hii haimzuwii mtoto wa kike kuchukua mali yote katika namna waliyoielezea Hanafi na Hambal, basi vile vile haiwezi kumzuia kwa namna nyingine. Kwa sababu dalili ya Aya ni moja haiwezi kugawanyika kwa namna yoyote ile. Vile vile Hanafi na Hambal wamesema: Ikiwa marehemu ataacha mama bila ya mwengine yeyote mwenye fungu na asaba, basi mama atachukua mali yote. Thelutuhi ikiwa ni fungu lake na theluthi mbili kurudishiwa yeye, ingawaje Aya inasema: "basi mama yake atachukua theluthi" Ikiwa inawezekana kwa mama kuchukua mali yote ingawaje fungu lake ni theluthi, basi hata mtoto wa kike pia atachukua yote inagawaje fungu lake ni nusu au theluthi mbili. Haya tumeyaeleza kwa ufafanuzi zaidi katika kitabu Ahwalush-shakhsiyya Ala madhahibil-khamsa, Na pia katika Juzuu ya sita ya Fiqh Imam Jafar As-Sadiq(a.s) .

Na Baraza kuu la waislam la Misr limetoa kitabu kikubwa kiitwacho Daw'atu-taqrib, ambacho ndani yake mna utafiti kamili wa suala hili. Yale tuliyoyanakili ya Hanafi na Hambali yametoka katika kitabu Mughni cha Ibn Quddam na Mizani Shi'rani katika mlango wa Faraidh.

3.Na wazazi wake wawili kila mmoja wao atapata sudusi ya alichokiacha akiwa anaye mtoto.

Neno Walad (mtoto) linatumika kwa mtoto wa kike na kiume. Kwa sababu neno hilo linaotakana na Wilada (kuzaa), ambako kunaweza kuwa kwa wa kike na wa kiume. Na Qur'an imelitumia neno hilo kwa maana hayo pale iliposema: "Mwenyezi Mungu anausia kwa watoto wenu; mwanamume ni kama fungu la wanawake wawili." Au pale iliposema:"Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwa na mtoto" (19:35) Makusudio ya wazazi wawili hapa ni baba na mama tu, haingii babu na bibi (nyanya). Ikiwa marehemu ameacha wazazi wawili na watoto, itaangaliwa: Ikiwa katika watoto yuko wa kiume wazazi watachukua sudusi([12] ) kila mmoja, kinachobaki ni cha watoto hata ikiwa mtoto wa kiume ni mmoja tu. Ikiwa hakuna wa kiume, na wa kike wakawa zaidi ya mmoja, basi wazazi watachukua theluthi, na theluthi mbili zitakuwa ni za watoto wa kike, Hilo wameafikiana waislam wote.

Ikiwa mtoto wa kike ni mmoja tu pamoja na wazazi wawili, basi wazazi wawili kila mmoja atachukua sudusi na mtoto fungu lake ni nusu. Hapo itabaki sudusi ambayo Sunni wanasema itarudishwa kwa baba tu. Ama Shia wanasema itarudishwa kwa baba, mama na mtoto ikiwa mama hana kizuizi (kwa kuwepo ndugu wa marehemu); waitagawa mali mafungu matano moja la baba, moja la mama na matatu ya binti. Ikiwa mama atazuilika kwa kuwepo ndugu, basi ziada itarudishwa kwa baba na binti kwa mafungu manne, yaani ziada itagawanywa mafungu manne moja la baba na matatu ya binti.

4.Akiwa hana mtoto na akarithiwa na wazazi wake wawili; basi mama yake atapata theluthi, Akiwa anao ndugu, basi mama yake atapata sudusi.

Ikiwa marehemu hana mtoto wala mjukuu ikawa mirathi yake inakwenda kwa babake na mamake tu, basi mama atachukua theluthi ikiwa marehemu hana ndugu watakaomzuia mama kilichozidi sudusi. Ikiwa wapo hao ndugu, basi mama atachukua sudusi tu, kinachobaki katika hali zote mbili ni cha baba, Madhehebu yametofautiana kuhusu idadi ya ndugu ambao watamzuia mama. Maliki wamesema, uchache wake ni kaka wawili na si kina dada. Hanafi Shafii na Hambali wamesema ni kaka wawili au dada wawili. Shia wanasema ni kaka wawili au mmoja na dada wawili; au dada wanne kwa sharti ya kuwa wawe ni ndugu wa marehemu baba mmoja mama mmoja au baba mmoja, na wawe wamekwisha zaliwa wakati wa kufa mrithiwa, sio kwenye mimba na pia baba awe hai, Hawa ndio ndugu wanaomzuwiya mama kurithi theluthi, lakini wao wenyewe hawarithi kitu wakati huo.

5.Baada ya kutoa alivyousia au kulipa deni.

Marehemu akiacha mali, kwanza itatumiwa katika mazishi yake (sanda na mahali pa kuzikwa). Kisha yatalipwa madeni yake ikiwemo Hijja, Zaka, Khums na nadhiri, kisha utatekelezwa wasia wake usiozidi theluthi ya mali. Baada ya hapo ndipo utaangaliwa urathi ambao ni kama kutoa kilichozidi haja.

Unaweza kuuliza : Ikiwa deni limetangulia wasia, mbona halikutangulia kutajwa katika Aya hii?

Jibu : Kutangalia huko kutajwa hakumaanishi kutangulia katika hukumu na utekelezaji. Kwa sababu kuunganisha kwa 'au' hakumaanishi kufuata mpango - kama ilivyo kinahau - isipokuwa kunamaanisha usawa katika hukmu. Ni kama vile kusema lianze lipi baada ya mazishi? Jibu litatokana na kupatikana dalili nyingine. Imethibiti kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) na Ijmai kwamba hakuna wasia wala mirathi isipokuwa baada ya kulipwa deni; na pia kuna Hadith nyingi zinazofahamisha kuwa marehemu ni rehani wa madeni yake.

6.Baba zenu na wa watoto wenu, hamjui ni yupi katika wao aliye karibu zaidi kwa manufaa. Ni faradhi itokayo kwa Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi mwenye hekima.

Hii ni jumla iliyoingia kati inayoonyesha kuwa siri ya makadirio ya mirathi haiwezi kufahamika kiakili isipokuwa anayeijua ni yule aliyemuumba mwanadamu; Yeye peke yake ndiye ajuaye linalomdhuru mtu na kumnufaisha. Aya hii inafaa kuwa ni dalili kwamba hukumu za Mwenyezi Mungu zimewekwa kwa masilahi ya mtu na utengeneo wake. Kwa hivyo basi tunapata dalili ya imani ya mtu kwa matendo yake mema na tunapata dalili ya uovu wake kwa matendo yake maovu. Ni faradhi itokayo kwa Mwenyezi Mungu sio kutoka kwa mtu ambaye anatawaliwa na matamanio. Tumeona tume nyingi za kutunga sheria na mabunge yakiweka sheria na kanuni kwa ajili ya masilahi ya wenye nguvu na kuwaonea wanyonge.

7.Nanyi mtapata nusu ya walichokiacha wake zenu, ikiwa hawana watoto, Ikiwa wana watoto basi mtapata robo ya walichokiacha baada ya kutoa walivyousia au kulipa deni.

Waislam wote wameafikiana kuwa mke na mume wanashiriki katika mirathi na warithi wote. Mume atapata nusu ikiwa mke hana mtoto aliyezaa naye au aliyezaa na mume mwengine. Na mke atapata robo ikiwa ana mtoto aliyezaa naye au aliyezaa na mke mwengine.

8.Na wao watapata robo ya mlichokiacha ikiwa hamna motto, Ikiwa mna mtoto, basi watapata thumni ([13] ) ya mlichokiacha baada ya kutoa mliyousia au kulipa deni.

Mke atapata robo ya mali ya mumewe ikiwa hana mtoto aliyezaa naye au aliyezaa na mke mwengine, na atapata thumuni ikiwa ana mtoto aliyezaa naye au aliyezaa na mwengine. Madhehebu mane yameafikiana kuwa makusudio ya mtoto (Walad) hapa ni mtoto wa marehemu na mjukuu aliyezaliwa na mtoto wa kiume tu, awe mume au mke. Ama mjukuu aliyezaliwa na mtoto wa kike hawezi kumzuia mke au mume kupata fungu lake kubwa. Bali Shafi na Maliki wamesema kuwa mjukuu wa mtoto wa kike harithi wala hamzuwii mwengine, kwa sababu yeye ni upande wa kukeni (fungu la rihami).

Shia Imamia wamesema kuwa makusudio ya mtoto ni mtoto yeyote na mjukuu yeyote wa mtoto wa kike au wa mtoto wa kiume. Kwa hiyo mjukuu wa kike wa mtoto wa kike atawazuilia mke na mume kupata fungu kubwa na pia atarithi.

Wake wakiwa wengi watashirikiana katika robo au thumni kwa kugawana sawa sawa. Madhehebu mane yamesema: "Ikiwa marehemu hana mrithi zaidi ya mumewe au mkewe, basi kinachobaki hakirudishwi kwa mume huyo wala mke - Taz. Kitabu Mughni cha Ibn Quddama, Shia Imamia wametofautiana katika hilo kwa kauli tatu: Kwanza: Kurudishwa kinachobaki kwa mume tu, sio kwa mke. Kauli hii ndiyo maarufu kwa mafaqihi wa siku hizi na ndivyo wanavyofanya. Pili: Kurudishiwa mke au mume katika hali zote. Tatu: Kurudishiwa mke au mume wakati wa kughibu Imam mwadilifu. Na sisi tuko kwenye rai hii ambayo pia ni rai ya Sheikh Saduq, Najibuddin bin Said, Allama Hilly na Shahidi wa kwanza. Tumetaja dalili za kuchagua rai hii katika kitab Fiqhul-Imam Jafar As-Sadiq(a.s)

9.Ikiwa mwanamume au mwanamke anayerithiwa ni mkiwa naye ana ndugu wa kiume au wa kike, basi kila mmoja katika wao atapata sudusi, Wakiwa wengi zaidi ya hivyo, basi watashirikiana katika theluthi.

Neno Kalala (ukiwa, kutokuwa na baba wala mtoto) limekuja mara mbili katika Qur'an, moja ikiwa hapa na jengine mwisho wa Sura hii. Makusudio yake hapa ni ndugu wasiokuwa baba na mama au mtoto. Neno hilo anaitwa nalo marehemu anayerithiwa na ndugu wa kiume au wa kike walio hai kama ambavyo anaitwa nalo mrithi ndugu wa kiume au wa kike aliye hai. Maana zote mbili - kama uzionavyo - zinafuatana. Kwa hiyo yoyote utakayoichukua ni sawa.

Wafasiri wameafikiana kuwa makusudio ya ndugu wa kiume au wa kike katika Aya hii ni ndugu wa upande wa kwa mama tu; bali hata wengine wamesoma Qiraa cha minalummi (wa upande wa mama). Ama mirathi ya ndugu wa kiume au wa kike kwa baba na mama au kwa baba tu, hukumu yake itakuja katika Aya iliyoko mwisho wa sura hii. Madhehebu yameafikiana kwamba mmoja katika ndugu (mtoto wa mama) atapata sudusi awe mwanamume au mwanamke. Wakiwa ni zaidi,wawe wa kike au wa kiume au mchanganyiko watapata theluthi kwa kugawana sawa sawa, mwanamke sawa na mwanamume.

10.Baada ya (kutoa) yaliyousiwa au kulipa deni pasi na kuleta dhara.

Yametangulia maelezo kuwa hakuna mirathi ila baada ya kulipwa deni na kutekelezwa wasia. Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekataza kuleta dhara katika deni na wasia. Dhara katika deni ni kukiri au kuusia deni lisilokuwepo kwa kukusudia kuwadhuru warithi. Na dhara katika wasia ni kuzidisha kiwango cha theluthi ya mali yake, Kama akifanya hivyo utekelezaji wake utategemea ruhusa ya warithi. Hadith inasema: "Kuwaacha warithi wako wakiwa wanaojitosheleza ni bora kuliko kuwaacha hali ya kuwa ni mafukara omba omba.

"Ni wasia utokao kwa Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu ni mjuzi mpole.

Kila anachousia Mwenyezi Mungu ni wajibu kitekelezwe.