TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Juzuu 5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 17308
Pakua: 2362


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 17308 / Pakua: 2362
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Juzuu 5

Mwandishi:
Swahili

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TANO

﴿ أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ أُوتُوا نَصِيبًا مِّنَ الْكِتَابِ يُؤْمِنُونَ بِالْجِبْتِ وَالطَّاغُوتِ وَيَقُولُونَ لِلَّذِينَ كَفَرُوا هَـٰؤُلَاءِ أَهْدَىٰ مِنَ الَّذِينَ آمَنُوا سَبِيلًا﴾

51.Je, huwajui ambao wamepewa fungu katika Kitabu wanaamini sanamu na taghuti na wakisema kwa ajili ya wale waliokufuru kuwa hao wameongoka zaidi katika njia ya haki kuliko walioamini.

﴿ أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ لَعَنَهُمُ اللَّـهُ وَمَن يَلْعَنِ اللَّـهُ فَلَن تَجِدَ لَهُ نَصِيرًا ﴾

52.Hao ndio waliolaaniwa na Mwenyezi Mungu, na ambaye Mwenyezi Mungu amemlaani, hatampatia wa kumsaidia.

WANAAMINI SANAMU NA TAGHUT

Aya 51 -52

LUGHA

Neno Jibt linatumika kwa maana nyingi. Makusudio yake hapa ni anayeabudiwa ambaye si Mungu (sanamu) Na Taghut ni aliyepetuka mipaka.

MAANA

Je, hawajui ambao wamepewa fungu katika Kitabu wanamini sanamu na taghuti.

Katika Aya zilizotangulia, Mwenyezi Mungu amewataja mayahudi kwa upotevu, upotezaji, kuyaweka maneno pasipo mahali pake na kupindua maneno. Kisha katika Aya hii amewataja kuwa wao wanaamini sanamu na taghuti; yaani masanamu wanayoyaabudu Maquraish.

Unaweza kuuliza : Imekuwaje Mwenyezi Mungu (s.w.t) kusema kuhusu mayahudi kwamba wao wanaamini sanamu na inajulikana wazi kuwa wao hawaamini masanamu ya Maquraish.

Jibu : mayahudi hawaamini masanamu ya Kiquraish katika nafsi zao, bali waliyakubali kiunafiki kwa kudanganya na kwa ajili ya kubagua na kumfanyia inadi Muhammad(s.a.w.w) na aliyemwamini. Wakawaambia waabudu masanamu: "Nyinyi mna njia ya uongofu zaidi kuliko waislamu."

Iliyo sawa ilikuwa ni kwa mayahudi wawasaidie waislamu dhidi ya waabudu masanamu kwa sababu waislam ni watu wa Kitabu na wanaikubali Taurat kinyume na waabudu masanamu.

Kwa hiyo mayahudi walikhalifu haki na wakasimama pamoja na washirikina, ndipo Mwenyezi Mungu akawataja kama waabudu masanamu. Kwa hali hiyo ndipo tunapoipata tafsiri ya:Hao wameongoka zaidi katika njia kuliko walioamini .

Yaani mayahudi walisema: Washirikina ni waongofu zaidi wa njia kuliko waumini, Kwa hiyo jibu la swali liko ndani ya Aya yenyewe. Kwa hali hii inatubainikia kuwa ishara ya hao ni ya waabudu masanamu na kwamba herufi lam katika neon: Lilladhina ni ya kwa ajili; yaani waliyoyasema ni kwa ajili ya kuwaridhisha wale waliokufuru, ambao ni washirikina wa kiquraish na hawakusema kwa kuamini wayasemayo.

Hao ndio waliolaaniwa na Mwenyezi Mungu

Nao ni mayahudi waliofanya unafiki wakasadiki masanamu kwa ukaidi na inadi kwa waislam wanaowasadi ki Mitume yao; kama vile Musa, Daud, Suleiman, Yahya na Zakariya.

Na ambaye Mwenyezi Mungu amemlaani, hatampatia wa kumsaidia.

Isipokuwa Amerika ambayo ilisheheneza Israil kwa silaha na kuisaidia tarehe 5 June; na Umoja wa Mataifa ukawatetea kwa namna ambayo mwarabu yeyote mwenye ikhlasi au mwislamu yeyote aliye muumin hatasahau hata ukipita muda gani.

Na sisi pamoja na majeraha tuliyo nayo, tunaamini kwa imani isiyo na shaka kwamba Mwenyezi Mungu peke yake ndiye msaidizi mwenye nguvu; na kwamba mwisho wa mambo utakuwa ni wa haki na uadilifu. Kwa hiyo ni juu ya wanaoitafuta haki kuvumilia, kutokuwa na pupa ya kuifikia, na kutotishwa na silaha ya adui kwa vyovyote atakavyokuwa na hatimaye kufaidika na majaribio.

﴿ أَمْ لَهُمْ نَصِيبٌ مِّنَ الْمُلْكِ فَإِذًا لَّا يُؤْتُونَ النَّاسَ نَقِيرًا ﴾

53.Au wao wana fungu katika ufalme? Basi hapo wasingewapa watu hata kitobwe cha kokwa ya tende

﴿ أَمْ يَحْسُدُونَ النَّاسَ عَلَىٰ مَا آتَاهُمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ فَقَدْ آتَيْنَا آلَ إِبْرَاهِيمَ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَآتَيْنَاهُم مُّلْكًا عَظِيمًا﴾

54.Au wanawahusudu watu kwa alichowapa Mwenyezi Mungu katika fadhila yake? Basi tuliwapa watoto wa Ibrahim Kitab na h ekima na tukawapa ufalme mkubwa.

﴿ فَمِنْهُم مَّنْ آمَنَ بِهِ وَمِنْهُم مَّن صَدَّ عَنْهُ وَكَفَىٰ بِجَهَنَّمَ سَعِيرًا ﴾

55.Katika wao kuna walio mwamini na katika wao kuna waliojiepusha naye; na Jahanam yatosha kuwaunguza.

HAWAWAPI WATU HATA CHEMBE

Aya 53-55

MAANA

Bado maneno yako kwa mayahudi. Mwenyezi Mungu katika Aya ya 44 amewataja kwa upotevu na upotezaji; katika Aya 45 uadui wao kwa waislamu katika Aya ya 46 kwa kugeuza maneno; katika Aya 49 kwa kujitukuza; katika Aya 50 kwa uzushi na katika Aya ya 51 kwa inadi, ukaidi na kuboresha ibada ya sanamu kwa unafiki. Katika Aya hii Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawataja kwa ubakhili:

Au wao wana fungu katika Ufalme? Basi hapo wasingewapa watu hata kitobwe cha kokwa ya tende.

Maana ni kuwa mayahudi hawana dola wala ufalme. Lau wangelikuwa na sehemu ya ufalme, wangeliwazuilia watu wote heri na wasingelimwachia yeyote kitu; hata kiasi cha kitobwe cha kokwa ya tende kilicho kidogo sana kisichotumika.

Amesema kweli Mwenyezi Mungu Mtukufu, Walikuwa na wanaendelea kuwa hawawezi kuona neema ya Mwenyezi Mungu kwa mja yeyote miongoni mwa waja wake ila hujaribu kuiondoa kwa njama au kwa riba au kwa kudanganya kwa binti zao na wake zao. Na wakipata nguvu kidogo hunyang'anya na kumwaga damu.

Kuanzia siku walipovamia ardhi ya Palestina mwaka 1948, waliwatoa wazalendo nchini mwao baada ya kuwachinja wanawake na watoto kila mahali.

Na mnamo mwaka 1967 waisrail, kwa kusaidiwa na wakoloni, walivamia sehemu nyingine ya ardhi ya waarabu. Kikakaririka kitendo chao cha kwanza, cha kuua na kufukuza. Hili sio geni katika historia yao na tabia zao. Waarabu wametawala na ukaendelea utawala wao miaka kadhaa; ukaenea mashariki na magharibi; na mayahudi walikuwa ni miongoni mwa raia zao; wakafanya uadilifu kwa wote na kuwafanyia wema mayahudi na watu wa dini nyinginezo; mpaka wakasema watunzi wa kimagharibi; kama vile Gustav Lebon: "Haikujua historia utawala wenye huruma zaidi ya Waarabu." Wameshuhudia kama hivyo wengineo "chombo humimina kilicho nacho" anasema Ibin Swafiy.

Itakuwa ni vizuri kunakili aliyoyataja mwenye Al-amanar wakati wa kufasiri Aya hii, katika mwaka wa 60 wakati Palestina ilipokuwa katika utawala wa dola ya Uthmaniya, Ninamnukuu: "Maana yanayopatikana katika Aya hii, ni kwamba hawa mayahudi ni watu wachoyo na wabakhili sana, wanaona tabu kunufaika mwengine yeyote kutokana nao. Wakiwa na utawala wanawazuilia watu wasinufaike hata kidogo, japokuwa ni kitu kipuuzi tu. Basi kwa nini isiwe uzito kwao kutokea Mtume wa kiarabu (Muhammad) ambaye ana milki wakiwemo mayahudi?

Sifa hii bado wanayo hadi leo. Ikiwa juhudi zao za kuunda serikali katika Palestina zitafanikiwa, basi watawafukuza wa islamu na wakristo na hawatawapa hata kitobwe cha kokwa ya tende. Dalili ziko kwamba wanajaribu kumiliki ardhi takatifu na kuwazuia wengine na sababu zote za kupata riziki. Wameweka akiba ya mali nyingi sana kwa ajili ya hilo. Kwa hiyo ni wajibu kwa serikali ya Uthmaniya kutowapa nafasi mayahudi katika Palestina wala wasiwaache wakamiliki ardhi na kuhamia kwa wingi. Kwani hilo lina hatari kubwa.

Mwenye Tafsir Al-manar anasema Aya haithibitishi wala kukanusha kutawala mayahudi Palestina; isipokuwa inabainis ha tabia watakayokuwa nayo lau watatawala Palestina.

Haya ndiyo aliyoyasema ulama katika maulama wa Kiislam kuhusu tafsiri ya Aya hii, Ameisema miaka arobaini kabla ya kupatikana serikali ya Israel katika Palestina. Hii haifahamishi kitu zaidi ya kufahamisha ukweli wa Nabii Muhammad(s.a.w.w) katika Utume wake na ujumbe wake, pale alipotoa habari kwa Wahyi wa Mwenyezi Mungu kabla ya zaidi ya miaka 1300, kwamba mayahudi lau watamiliki na kutawala wangelikuwa na yale yaliyotokea mwaka 1948 na 1967.

﴿ أَفَمَن شَرَحَ اللَّـهُ صَدْرَهُ لِلْإِسْلَامِ فَهُوَ عَلَىٰ نُورٍ مِّن رَّبِّهِ فَوَيْلٌ لِّلْقَاسِيَةِ قُلُوبُهُم مِّن ذِكْرِ اللَّـهِ أُولَـٰئِكَ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ﴾

Je, ambaye Mwenyezi Mungu ameufungua moyo wake kwa uislam akawa yuko katika nuru itokayo kwa Mola wake (ni sawa na mwenye moyo mgumu)? Basi adhabu kali itawathubutukia wale wenye moyo mgumu wasimkumbuke Mwenyezi Mungu. Hao wamo katika upotevu ulio wazi (39:22)

Au wanawahusudu watu kwa alichowapa Mwenyezi Mungu katika fadhila yake?

Hii nayo ni sifa nyingine katika sifa za mayahudi, hasadi. Makusudio ya watu hapa ni Mtume Muhammad(s.a.w.w) na waumini walio pamoja naye. Na hasadi yao mayahudi ni kutokana na dini ya haki aliyopewa Muhammad na waumi- ni na kumakinishwa katika ardhi.

Mayahudi waliposhindwa kuizuwia neema hii kwa waislamu, waliungana na washirikina dhidi ya waislam, wakaenezea propaganda dhidi ya uislamu na Mtume wake. Hatimaye uovu ukawazungukia wao na wakafukuzwa Hijaz kwa yale waliyokuwa wakiyafanya.

Basi tuliwapa watoto wa Ibrahim Kitabu na hekima na tukawapa Ufalme mkubwa.

Makusudio ya Kitabu ni Zabur ya Daud, Taurat ya Musa na Injil ya Isa. Hekima ni Utume na elimu: maana yake kwa nini mnamhusudu Muhammad(s.a.w.w) na waarabu kwa sababu ya Utume na kumakinika katika nchi? Mwenyezi Mungu amekwishawapa nyinyi mfano wa hayo katika waliopita; kama vile Yusuf, Daud na Suleiman.

Katika wao kuna waliomwamini na katika wao kuna waliojiepusha naye. Wafasiri wametofautina katika dhamiri ya 'waliomwamini;' kuwa je ni kumwamini Muhammad(s.a.w.w) , au Ibrahim au Kitabu? Lenye nguvu zaidi ambalo linaafikiana na maana na kusaidiwa na kuzingatia ni kuwa dhamiri inamrudia kila Mtume aliyepewa Kitabu na hekima.

Neno 'kila Mtume' hata kama halikutajwa katika Aya waziwazi, lakini linafahamika kutokana na mfumo wa maneno.

Kwa vyovyote iwavyo, hakuna tofauti kuwa maana ya Aya ni kwamba si jambo geni kwa hao na mfano wao kutomwamini Muhammad(s.a.w.w) . Kwani Mitume waliotangulia waliaminiwa na kikundi na wakakanushwa na kundi jingine. Na kundi la ukanushaji lilikuwa kubwa; kama asemavyo (s.w.t):

﴿ فَمِنْهُم مُّهْتَدٍ وَكَثِيرٌ مِّنْهُمْ فَاسِقُونَ﴾

"Wengine katika wao walikuwa waongofu na wengi katika wao walikuwa mafasiki" (57:26)

Jahannam yatosha kuwaunguza wale wapingao haki

﴿ إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِنَا سَوْفَ نُصْلِيهِمْ نَارًا كُلَّمَا نَضِجَتْ جُلُودُهُم بَدَّلْنَاهُمْ جُلُودًا غَيْرَهَا لِيَذُوقُوا الْعَذَابَ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَزِيزًا حَكِيمًا ﴾

56.Hakika ambao wamezikufurisha Aya zetu tutawatia motoni; kila zitakapoiva ngozi zao, tutawabadilishia ngozi nyingine ili waonje adhabu ya Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye nguvu na Mwenye hekima.

﴿ وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ سَنُدْخِلُهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَدًا لَّهُمْ فِيهَا أَزْوَاجٌ مُّطَهَّرَةٌ وَنُدْخِلُهُمْ ظِلًّا ظَلِيلًا﴾

57.Na ambao wameamini na wakatenda amali njema, tutawaingiza katika pepo zenye kupita mito chini yake, ni wenye kudumu milele humo; wana humo wake waliotakaswa na tutawatia katika vivuli vya daima.

KUBADILISHA NGOZI NYINGINE

Aya 56 - 57

MAANA

Hakika ambao wamezikufuru Aya zetu tutawatia motoni; kila zitakapoiva ngozi zao, tutawabadilisha ngozi nyingine

Aya hii ni ubainifu wa mwisho wa Aya iliyotangulia, Na Jahannam yatosha kuwaunguza. Makusudio ya Aya hapa ni kila lililothibiti katika dini kwa dharura; mfano ujuzi wa Mwenyezi Mungu na uweza wake, Malaika, pepo moto na mengineyo yanayorudia kwenye misingi ya dini. Vilevile mfano wa wajibu wa kufunga, Swala, uharamu wa zina, pombe na mengineyo katika masuala ya kifiqhi na ya matawi ya dini. Hakuna mwenye shaka kwamba kukanusha ni kukufuru; na je kutia shaka ni kukufuru pia.? Hilo tumelifanyia utafiti kwa ufafanuzi, wakati wa kufasiri Aya 115 ya sura Al-imran kifungu 'mwenye kuacha uislam.'

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni mwadilifu, hilo halina shaka. Anapoiunguza ngozi ya mwasi inaondoka na kuisha; kisha huumba ngozi nyingine mpya na kuiadhibu, je, huko si kuadhibui ngozi ambayo haikumuasi? Jambo ambalo halijuzu kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu?Jibu : Imepokewa Hadith kutoka kwa Imam Jaffar as-Sadiq(a.s) inayojibu swali hili:"Hakika ngozi ni hiyo hiyo, si nyingine . Akapiga mfano wa tofali unapolivunjavunja mpaka likawa mchanga, kisha ukalichanganya tena na maji na kutengeza tofali jipya. Hapo litakuwa ndio hilo hilo katika mada yake, lakini ni jengine katika sura yake. Si mbali kuwa 'kubadilisha ngozi' ni fumbo la adhabu na uchungu wake. Katika hali zote ni kwamba linalopatikana kwetu ni kuamini uadilifu wa Mwenyezi Mungu na uweza wake, Ama ufafanuzi hatuna jukumu nao.

Ili waonje adhabu

Yaani lililosababisha kubadilishwa ngozi ni kuhisi kwao adhabu ya kudumu. Aina hii ya adhabu inahusika na mkanushaji, na msihrikina na ambaye watu humwogopa kwa shari yake. Nasi daima, kufa na kupona, tuna imani ya Lailaaha illa illah, Muhammad rasuulu llah, na tunamfanyia uadui kila mwovu. Wanavyuoni wanasema: Watakaoingizwa motoni na wasitoke ni watano: Mwenye kudai uungu, kama vile Namrud na Fir'aun, mwenye kukanusha uungu moja kwa moja, mwenye kumfanyia Mungu washirika, mnafiki na muuaji wa nafsi isiyo na hatia.

Kwa dhahiri ni kuwa mnafiki zaidi ni yule anayeleta vita kwa jina la mwenye kulinda amani; mwenye kuwafanya watumwa watu kwa jina la kuchunga uhuru; mwenye kunyang'anya chakula cha watu kwa jina la kunyanyua maisha yao na mwenye kueneza uovu kwa jina la maendeleo.

Na ambao wameamini na wakatenda amali njema…

Umetangulia mfano wa tafsir yake katika Sura Al-imran Aya 15. Kwa hiyo haihitaji tafsir.

﴿ إِنَّ اللَّـهَ يَأْمُرُكُمْ أَن تُؤَدُّوا الْأَمَانَاتِ إِلَىٰ أَهْلِهَا وَإِذَا حَكَمْتُم بَيْنَ النَّاسِ أَن تَحْكُمُوا بِالْعَدْلِ إِنَّ اللَّـهَ نِعِمَّا يَعِظُكُم بِهِ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ سَمِيعًا بَصِيرًا ﴾

58.Hakika Mwenyezi Mungu anawaamuru kurudisha amana kwa wenyewe. Na mtakapohukumu baina ya watu muhukumu kwa uadilifu. Hakika Mwenyezi Mungu anawapa mawaidha mazuri sana. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye kusikia ni mwenye kuona.

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَطِيعُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُوا الرَّسُولَ وَأُولِي الْأَمْرِ مِنكُمْ فَإِن تَنَازَعْتُمْ فِي شَيْءٍ فَرُدُّوهُ إِلَى اللَّـهِ وَالرَّسُولِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ذَٰلِكَ خَيْرٌ وَأَحْسَنُ تَأْوِيلًا﴾

59.Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu na mtiini Mtume na wenye mamlaka katika nyinyi. Na kama mkipingana katika jambo, basi lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake mkiwa mwamwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho. Hilo ni bora zaidi na mwisho mzuri.

UAMINIFU NA UADILIFU

Aya 58 - 59

MAANA

Hakika Mwenyezi Mungu anawaamuru kurudishia amana kwa wenyewe.

Aya mbili zimekusanya wajibu wa kutekeleza amana na uadilifu katika hukumu na kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume na mwenye madaraka katika nyinyi. Zimekuja Hadith kadha na Aya kadhaa katika kuhimiza kuchunga amana na kuitekeleza kwa mwenyewe awe mwema au mwovu. Kwa sababu ni haki yake kama binadamu, sio kwa kuwa ni mwema au mwovu. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَخُونُوا اللَّـهَ وَالرَّسُولَ وَتَخُونُوا أَمَانَاتِكُمْ وَأَنتُمْ تَعْلَمُونَ﴾

"Enyi mlioamini msimkhini Mwenyezi Mungu na Mtume wala msikhini amana zenu" (8:27)

Mtume anasema: "Hana imani asiyekuwa na uaminifu, wala hana dini asiyekuwa na ahadi" Lakini hakuna katika Qur'an wal a Hadith - kwa tunavyojua - maelezo kamili ya amana. Tunavyofahamu ni kuwa amana ni dhamana iliyoko kwako kwa ajili ya mtu mwingine. Ni juu yako kuichunga na kuilinda na kuirudisha kwa mwenyewe anapoitaka kama ilivyo. Ukiizuia au kuirudisha pungufu, basi wewe ni mhaini wa hukumu ya Qur'an na Hadith.

Si lazima amana iwe ni kitu kinachoonekana, kama vile mali na kitabu, la inaweza kuwa ni siri, nasaha au kazi. Vilevile si lazima mwenyewe hiyo amana awe mtu hasa; inaweza kuwa ni dini au elimu, bali hata nafsi yako yenyewe ikawa ndiyo yenye amana.

Amana ya dini na elimu ni yale unayoyajua katika halali ya Mwenyezi Mungu na haramu yake na katika heri na shari. Amana hii itathibiti kwa kufanya unayoyajua. Ama amana ya nafsi yako iliyoko kwako, ni lile lililo la masilahi zaidi kwa dunia ya hiyo nafsi na akhera yake.

Kwa maneno mengine, mwaminifu ni yule anayetekeleza kwa ukamilifu bila ya upungufu, ni sawa aliyewajibisha wajibu huu ni dini, elimu, nchi, jamii au kitu chochote kingine.

Kwa hiyo basi amana sio muonjo ulio katika chakula au kinywaji hiki sio kile, au kuwa ni mwanamke huyu si yule wala sio wasifu unaowapendeza watu; kama upole, bali amana ni mshikamano wa maisha na msimamo wake ambao bila huo maisha hayaendi sawa.

Kwenye maana hayo Imam Ali(a.s) ameishiria kwa kusema:"Amana ni nidhamu ya umma"; yaani umma hautengenei mambo yake ila ikiwa kila mtu atatekeleza yanayotakikana kwake. Na amesema tena:"Ambaye siri yake haitofautiani na dhahiri yake na vitendo vyake havitofautiani na maneno yake, basi atakuwa ametekeleza amana na amewafanyia ikhlasi waja. Na mwenye kuipuuza amana akawa anafanya hiyana na wala asiepushe nafsi yake na dini yake kwa uhaini basi atakuwa amejiingiza katika fedheha duniani, na akhera atapata udhalili na fedheha. Na hakika hiyana kubwa ni kuuhaini umma, na fedheha kubwa ya utapeli ni kuutapeli umma."

Miongoni mwa dalili za kuutukuza uaminifu ni kauli ya mafakihi: "Mwenye kuutangazia vita uislamu na waislamu na akahalalisha damu zao na mali zao si kwa chochote ila kwa kuchukia Tawhid, basi ni halali mali yake na damu yake wala haiwi halali amana yake."

Imam Zainul-abidin(a.s) anasema:"Lau aliyemuua baba yangu angaliniwekea amana upanga aliomuulia, nisingelimuhini."

Mtu mmoja alimuuliza Imam Arridha(a.s) : "Yahudi amenihini Dirham elfu; kisha faida yake ikaingia mikononi mwangu, Je, nimlipizie?" Imam akamjibu:"Ikiwa amekudhulumu usimdhulumu."

Katika riwaya nyingine amesema:"Ikiwa amekuhini usimuhini wala usijiingize katika aliyokufanyia." Siri katika hilo ni kwamba amana ni haki ya mwenyewe kwa sifa ya kuwa ni mtu sio kuwa ni mwislamu wala mshirikina au si mwema wala mwovu, Tutarudia kuelezea uaminifu tutakapofasiri Aya 72 ya Sura ya Ahzab.

Na mutapohukumu baina ya watu muhukumu kwa uadilifu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwajibisha kurudisha amana kwa wenyewe, amefuatisha wajibu wa uadilifu katika kuhukumu baina ya watu, Kwa sababu asiyechunga haki za watu, hana haki ya kuwa hakimu. Wajibu wa uadilifu siyo kwa hakimu tu, bali mtawala vile vile, na mtawala mwadilifu ni yule anayejishughulisha na nyanja zote za maisha; kama vile afya maendeleo, chakula na uhuru kwa wote.

Kabla ya kila kitu ni wajibu kutomwacha mtawala mwenye tamaa - mzalendo au asiyekuwa mzalendo - kutawala mambo ya watu. Matukio tuliyoyapitia yamethibitisha kwamba chimbuko la kwanza na la mwisho la matatizo yaliyotufika ni kutokana na kuwarudisha wezi na wasiokuwa na ujuzi kwenye madaraka na vyeo vya juu.

Ama uadilifu wa hakimu unakuwa katika kuwafanyia kwake usawa watesi wawili katika kila kitu na kila mwenye haki kumpa haki yake, bila ya kuangalia dini yake na itikadi yake; urafiki wake na uadui wake au utukufu wake na uduni wake.

Katika Historia ya sheria hakuna sharia iliyojihimu na kulitilia mkazo hilo kuliko sheria ya Kiislam. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema:"Mwenye kufanywa hakimu amechinjwa bila ya kisu." Anaonyesha kuwa wajibu wa hakimu ni mzito sana; Kwa sababu inabidi kupigana jihadi kwa nafsi yake na kufanya bidii ikiwa haki haiko. Na akasema tena:"Mahakimu ni watatu: wawili watakuwa motoni na mmoja peponi."

Ama yule atakayekuwa peponi, ni yule aliyejua haki akaihukmu, na wale wawili wataokuwa motoni ni aliyewahukumu watu bila ya ujuzi, na aliyekuwa anaijua haki, lakini akahukmu kinyume chake."

Hakika mwenyezi Mungu anawapa mawaidha mazuri sana.

Makusudio ya mawaidha hapa ni amri ya kurudisha amana. Neno mazuri linatambulisha kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) haamrishi ila ambalo ndani yake mna kheri na masilahi.

WENYE MAMLAKA NI NANI

Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu na mtiini Mtume na wenye mamlaka katika nyinyi.

Maneno na mabishano yamekuwa mengi kuhusu makusudio ya 'wenye mamlaka' na sifa zao; kama ambavyo watawala wamejibandika nayo kuwa ni wajibu kuwatii au angalau kuwanyamazia.

Vile vile kundi la mafakihi limetoa dalili kwa Aya hiyo kuwa chimbuko la sharia na misingi yake linathibiti kwa mambo manne:

1. Kitabu cha Mwenyezi Mungu; kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu:"Mtiini Mwenyezi Mungu."

2. Hadith za Mtume; kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu:"Na mtiini Mtume."

3. Ijmai; kutokana na kauli yake:"Na wenye mamlaka"

4. Kiyasi; kutokana na kauli yake:"kama mkizozana katika jambo basi lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume." Wakadai kwamba maana yake ni kuwa: likisieni lile lisilo na nukuu (nassi) kutoka katika Qur'an na Hadith. Utakuja ufafanuzi wa hilo.

Hakuna tofauti kuwa Qur'an na Hadith ni machimbuko ya msingi ya sharia. Ama Ijmai na Kiyasi wametofautiana katika hoja yake na katika ufahamisho wa Aya juu yake. Yafuatayo ni madhumuni ya Aya na rai zilizosemewa juu ya Aya hiyo:

1. Hakuna waliotafoutiana katika waislam kwamba kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume kunakuwa ni kufanya amali kwa Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadith za Mtume wake na kwamba hiyo ni misingi miwili katika ibara moja:Mwenye kumtii Mtume basi amemtii Mwenyezi Mungu. (4:80),

Alichowaletea Mtume kichukueni na alichowakataza kiacheni. (59:7),Wala hasemi kwa matamanio; hayakuwa haya ila ni Wahyi uliofunuliwa. (53: 3- 4)

Kuanzia hapo ndio wameafikiana waislam kwa kauli moja kukataa kila linalonasibishwa kwa Mtume(s.a.w.w) kama linapingana na msingi katika misingi ya Qur'an na hukumu zake.

Unaweza kuuliza : Kwa nini kukaririka neno utiifu katika kumtaja Mtume na wala halikukaririka wakati wa kutaja wenye mamlaka?

Jibu : Ni kwa ajili ya kutanabahisha kwamba kumtii Mtume ndio asili kwa dhati yake; sawa na kumtii Mwenyezi Mungu. Kwa sababu hiyo ndiyo ikawa kauli ya kila mmoja wao ni chimbuko katika machimbuko ya sharia, lakini si hivyo katika kuwatii wenye mamlaka. Bali ni tawi la kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume. Hakika wenye mamlaka ni wapokezi wa Mtume.

2. Neno miongoni mwenu, linafahamisha kwa uwazi wazi kwamba hakimu wa waislam anapasa awe ni miongoni mwao, wala haifai kabisa kuwa si miongoni mwao. Hilo linatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu:Na Mwenyezi Mungu hatawafanyia makafiri njia ya kuwashinda waumini. (4:141)

3. Wametofautiana katika makusudio ya wenye mamlaka baada ya kuafikiana kwao juu ya sharti la uislam; kuna waliosema: Ni makhalifa (Khulafau rrashidun). Na waliosema kuwa ni makamanda wa jeshi. Na wengine wakasema ni maulama wa kidini. Sheikh Muhammad Abduh amesema: Wao ni machifu watawala, maulama, viongozi wa jeshi na viongozi wengineo ambao watu wanawarudia katika haja na masilahi. Wakiafikiana hawa juu ya jambo, ni wajibu kuwatii kwa sharti ya kuwa wawe waaminifu na wasihalifu amri ya Mwenyezi Mungu wala Sunna ya Mtume wake. Na wawe na hiyari katika utafiti wao wa amri na kuafikiana kwao.

Shia wamesema kuwa Mwenyezi Mungu ameunganisha kwa herufi (Wau) baina ya kuwatii wenye mamlaka na kumtii Mt ume bila ya sharti lolote; na kuunganishwa kwa herufi (Wau) kunahukumia kuchanganya na kushirikiana katika hukumu. Maana ya haya ni kuwa kuwatii wenye mamlaka ni kumtii Mtume na kwamba amri yao ni amri yake.

Hakuna mwenye shaka kwamba daraja hii tukufu haiwi ila kwa anayesifika na kustahiki twaa hii na hakuna kitu kitakachomfanya astahiki hayo isipokuwa kuhifadhika na makosa na maasi (isma). Ndiko pekee kunakokufanya kumtii yeye na kumtii Mtume kuwe sawa.

Arrazi amekiri waziwazi fikra ya Isma kwa kusema kuwa wenye mamlaka ambao ni wajibu kuwatii hapana budi wawe ni maasumin (waliohifadhiwa na dhambi). Na Arrazi - kama anavyojulikana - ni miongoni mwa maulama wakubwa wa kisunni; mwanafalsafa na mfasiri wao, Haya ndiyo aliyoyasema ninamnukuu; "Jua kwamba kauli yake Mwenyezi Mungu, wenye mamlaka inafahamisha kwetu kwamba Ijmai ni hoja.

Dalili ya hilo ni kwamba: Mwenyezi Mungu ameamrisha kutiiwa wenye mamlaka moja kwa moja kat ika Aya hii. Na ambaye Mwenyezi Mungu anaamrisha atiiwe hapana budi awe amehifadhiwa na makosa; Kwa sababu lau asingelikuwa amehifadhiwa na makosa basi itakuwa anakadiriwa kufanya makosa, ambapo Mwenyezi Mungu ameamrisha afuatwe.

Kwa hiyo hilo litakuwa ni kuamrisha kufanywa makosa; na inajulikana kwamba kumfuata mwenye makosa kumekatazwa. Kwa hiyo imethibiti kwamba makusudio ya wenye mamlaka waliotajwa katika Aya hapana budi wawe wamehifadhiwa na makosa."

Hivi ndivyo walivyosema Shia katika kufasiri Aya hii, Tofauti iliyoko kati yao na Sunni ni katika kufuatilia na kumwainisha huyo mwenye kuhifadhiwa na makosa (maasum). Sunni wanasema kuhifadhiwa ni kwa umma. Wamefasiri umma kuwa ni watatuzi. Wengi wao wakasema ni baadhi ya watatuzi. Shia wamesema kuwa makusudio ya wenye mamlaka ni Ahlul-bayt ambao wametakaswa na makosa na kutwahirishwa na uchafu.

Kwa hiyo fikra ya Isma haihusiki na Shia tu, na wala sio waliosema peke yao, bali iko kwa Sunni; kama ambavyo iko kwa Shia. Hivyo kuchukulia kuwa shia tu ndio waliosema kauli hiyo ni kwa ajili ya ukaidi tu, na kueneza utengano.

Shia wametoa dalili juu ya Isma kwa Ahlul-baiti, kwamba: ni kipawa cha Mwenyezi Mungu, Anawahusu watu anaowaridhia miongoni mwa waja wake. Haiwezekani mtu kuitafuta mwenyewe Isma kwa namna yoyote atakavyojitahidi; kinyume na sifa nyingine. Kwa hiyo njia ya kujua Isma inajulikana kwa wahyi tu.

Na imethibiti kauli wazi katika Qur'an na Hadith juu ya Isma ya Ahlul- bait. Miongoni kwa hayo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّـهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ وَيُطَهِّرَكُمْ تَطْهِيرًا﴾

"Hakika Mwenyezi Mungu anataka kuwaondolea uchafu (Enyi) Ahlul-baiti na kuwatakasa kabisa kabisa" (33:33)

Pia kauli yake Mjumbe wa Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenye kunitii mimi ndio amemtii Mwenyezi Mungu; na mwenye kuniasi amemuasi Mwenyezi Mungu; na mwenye kumtii Mwenyezi Mungu, ndio amenitii mimi na mwenye kumwasi ameniasi mimi." Ameipokea Hakim katika Mustadrak na akasema: "Hii ni Hadith sahihi."

Vilevile ameisahihisha Dhahabiy katika Tal-khisu al-mustadrka, Katika kitabu hicho kuna hadith ya Mtume(s.a.w.w) amesema:"Ali yuko pamoja na Qur'an na Qur'an iko pamoja na Ali, viwili hivyo havitatengana mpaka vinijie katika Birika."

Vile vile amepokea Tirmidhi katika Musnad yake, Hakim katika Mustadrak yake na Ibn Hajar katika Sawaiq yake kutoka kwa Mtume Mtukufu(s.a.w.w) kwamba yeye amesema:"Ewe Mola wangu izungushe haki pamoja na Ali popote aendapo." Pia Imam Ibn Hambal, Tirmidhi, Hakima na Ibn Hajar, wamepokea kauli yake Mtume(s.a.w.w) :" Mimi nawaachia vitu ambavyo kama mkishikamana navyo hamtapotea baada yangu, navyo ni vizito viwili: Kitabu cha Mwenyezi Mungu na kizazi changu Ahlul-bait wangu."

Imekuwa mashuhuri Hadith kutoka kwa Mtume isemayo: "Hakika mfano wa Ahlul-bait wangu kwenu ni kama mfano wa safina ya Nuh, mwenye kuipanda ataokoka." Na Hadithi nyinginezo nyingi, zote hizo zimeandikwa katika vitabu vya Hadith vya Sunni na sahih zao, na zimepokewa na wategemewa wao.

Shia wamezikusanya na kuziwekea vitabu maalum vya zamani na vya kisasa. Vya zamani ni kama Kitab shafi cha Shariff Murtadha, Tal-khisu shafi cha Sheikh Tusi, Nahjul-haq cha Allama Hilli na katika Hadith za Mujallad wa tatu katika A'yanusha Shia cha Sayyid Muhsin Amin. Vile vile Dalailus-swidq cha Sheikh Mudhaffir na Muraja't cha Sharafuddin.

Kwa ujumla ni kwamba Shia na Sunni wanaamini Isma kwa pamoja kama msingi[7] Vile vile wameafikiana Shia na Sunni wengi kwamba wenye mamlaka waliotajwa katika Aya wamehifadhiwa na dhambi.

Pia wanaafikiana kwamba dalili ya kuhifadhiwa kwao ni kwamba Mwenyezi Mungu amewajibisha watiiwe kama alivyowajibisha kutiiwa yeye Mwenyezi Mungu na Mtume. Lakini Sunni wakatofautiana na Shia kuwa makusudio ya wenye mamlaka waliohifadhiwa na makosa, ni watatutuzi wa mambo au ni Ahlul-bait?

Sunni wakasema ni watatuzi wa mambo. Shia wakasema ni Ahlul-bait. Kwa sababu Isma ni kipawa cha Mwenyezi Mungu, hakijulikani ila kwa kauli wazi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na Mtume. Na imethibiti kauli kutokana nao juu ya Isma ya Ahlul-bait, Kwa hiyo makusudio ya wenye mamlaka ni Ahlul-bait si wengineyo.

Kwa maneno mengine ni kuwa wenye mamlaka katika Aya ni wenye kuhifadhiwa na makosa kwa sababu ya wajibu wa kuwatii wao. Kwa sababu ambaye ni wajibu kumtii ni maasum. Vile vile kunathibiti kuhifadhiwa kwa Ahlul-baiti kwa kauli wazi na hakukukuthibiti kwa wengineo. Na ambaye kumethibiti kuhifadhiwa kwake, basi ni wajibu kumtii. Kwa hiyo natija ni kuwa Ahlul-baiti ndio wenye mamlaka si wengineo. Kama kusema: Msikilize mwenye kunasihi aliye mwaminifu, wala hakuna mwaminifu ila Zaid. Kwa hiyo natija ni msikilize Zaid. Katika ambayo wameyatolea dalili Shia juu ya kutojuzu kuwafuata watatuzi katika mambo ya kidini ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:"Lakini watu wengi hawajui." Na kauli yake:"Na wengi wao hawaelewi." (5:103)

Maana ya haya ni kuwa haki haijulikani kwa kuangalia idadi ya watu, wawe wengi au wachache isipokuwa hujulikana kwa kuchukuliwa kutoka katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wake na hukumu ya kiakili ya msingi ambayo hakuna wanaotofautiana, - Kwa kuongeza - ninaandika maneno haya katika mwezi Machi 1968 na uchaguzi wa wabunge wa Lebanon umeuma mchanga; watu wanasongamana kwenye masanduku ya kura ili wamchague aliyenunua sauti za watu baada ya mnada, au yule aliyewaahidi watu wake kutekeleza matakwa yao.

Salaam zimfikie yule aliyesifu baadhi ya uchaguzi kwa kusema: "Mtu anaitikiwa pamoja na ukorofi wake. Mwengine anafuatwa kwa sababu ya udugu pamoja na maovu chungu nzima aliyonayo." Mwengine akasema: "Ni wachungwa mazuzu wanaufata kila sauti ya mchungaji, Ni bendera wanafuata upepo. Hawakupata mwanga wa elimu wala hawakuegemea nguzo thabiti.

Na kama mkipingana katika jambo, basi lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Tumetangulia kusema kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu mtiini Mwenyezi Mungu na mtiini Mtume - kwa maafikiano ya wote inafahamisha kushikamana na Qur'an na Hadithi; na kwamba kauli yake Mwenyezi Mungu. Na wenye mamlaka katika nyinyi, inafahamisha - kwa shia - wajibu wa kuwatii Ahlul-bait; na kwa sunni wengi inafahamisha kuwatii watatuzi wa mambo. Sasa tuzungumzie kauli hii, Na kama mkipingana. Je inafahamisha wajibu wa kutumia kiasi au iko mbali na hayo?

Kabla ya jawabu tutupe swali hili: Kwa nini Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawajibisha kurudishwa mapingano Kwake na kwa Mtume tu, bila ya wenye mamlaka, ambapo Yeye amewajibisha kuwatii wote watatu?

Jibu : Kwa sababu mzozo huenda ukatokea katika kuwajua hao wenye mamlaka; kama ambavyo limetokea hilo.

Sunni wakasema: Ni watatuzi wa mambo na Shia wakasema ni Ahlul-bait. Kwa hiyo katika mzozo huu inabidi kurudia Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Hadith za Mtume wake. Kwa ajili hiyo ndio Shia wakatoa dalili Aya ya tat-hir[8] na Hadith. Sasa turudie kwenye wajibu wa kutumia kiasi au kutotumia.

(Qiyas), ni kutoa hukumu ya tukio iliyoelezwa wazi na sharia kwa tukio jengine ambalo hukumu yake haikuelezwa wazi; kwa kushirikiana matukio mawili katika sababu zilizotolewa na fakihi.

Mfano sheria, imeeleza kuwa nyanya wa upande wa mama anarithi na wala isielezwe wa upande wa baba. Tukamrithisha nyanya wa upande wa baba kwa kuchukulia kiasi cha wa upande wa mama. Kwa sababu wote ni nyanya.

Sunni wamesema kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu; Mkipingana katika jambo lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume inafahamisha kusihi qiyasi; kuwa maana yake ni lirudisheni kwenye tukio alilolibainisha Mwenyezi Mungu hukumu yake; yaani linalofanana nalo.

Shia wamesema kuwa Aya iko mbali kabisa na qiasi wala haifahamishi zaidi ya kurudia Qur'an na Hadith katika masuala ya kidini inapotokea tofauti baina ya mafakihi, Na kauli za maimamu walio maasum zinaingia katika hadith. Kwa sababu ni riwaya kutoka kwa babu yao Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) .

Ama njia yao katika ambalo halikuelezwa wazi katika Kitab wala Hadith ni kurudia kwenye hukumu ya akili ya mkato iliyo dhahiri ambayo haiwezi kutofautiana. Mfano ubaya wa mateso bila ya ubainifu; na ambayo wajibu hautimii ila kwalo, basi ni wajib, Kwa hiyo qiasi sio katika kauli hii. Kwa sababu natija zake zote ni za kudhania; na dhana haitoshelezi kitu [9] .

Katika waliyoyatolea dalili Shia kuhusu kubatilika kwa qiyas ni kwamba mambo ya kawaida, inasihi kuyafanyia qiyas, Kwa vile sababu zake ziko kwenye ukawaida, Ama hukumu za kidini haisihi kufanya qiyas. Kwa sababu sharia imekusanya pamoja vitu vinavyotofautiana; kama katika mambo yanayovunja udhu ambapo imeweka sawa kulala na kukojoa.

Mkiwa mnamuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho.

Mwenye Majmau anasema: "Ni ubainifu wa uwazi ulioje wa kauli hii!" Nasi twasema: Ni uzuri ulioje wa tafsir wa hiyo!

Hilo ni bora zaidi na mwisho mzuri

Yaani kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume, na kuirudisha hukumu ya kutofautiana kwa Qur'an na Hadith ni mwisho mzuri. Hii ni ikiwa tutalifasiri neno Taawil katika Aya hii kwa maana ya mwishilio.

Imesemekana kuwa makusudio ya neno Taawil hapa ni tafsiri ambapo maana yatakuwa ni tafsir ya Mwenyezi Mungu na Mtume katika mnayopingana ni bora na nzuri kuliko tafsiri yenu.

Vyovyote iwavyo neno Taawil linachukua maana zote mbili