TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Juzuu 5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 17260
Pakua: 2342


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 17260 / Pakua: 2342
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA TANO Juzuu 5

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TANO

﴿فَمَا لَكُمْ فِي الْمُنَافِقِينَ فِئَتَيْنِ وَاللَّـهُ أَرْكَسَهُم بِمَا كَسَبُوا أَتُرِيدُونَ أَن تَهْدُوا مَنْ أَضَلَّ اللَّـهُ وَمَن يُضْلِلِ اللَّـهُ فَلَن تَجِدَ لَهُ سَبِيلًا﴾

88.Mna nini nyinyi mmekuwa makundi mawili katika (habari ya) wanafiki, na hali Mwenyezi Mungu amewageuza kwa yale waliyoyachuma? Je,mnataka kumwongoza ambaye Mwenyezi Mungu amemuacha kupotea? Na ambaye Mwenyezi Mungu amemuacha kupotea, hatampatia njia

﴿وَدُّوا لَوْ تَكْفُرُونَ كَمَا كَفَرُوا فَتَكُونُونَ سَوَاءً فَلَا تَتَّخِذُوا مِنْهُمْ أَوْلِيَاءَ حَتَّىٰ يُهَاجِرُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَإِن تَوَلَّوْا فَخُذُوهُمْ وَاقْتُلُوهُمْ حَيْثُ وَجَدتُّمُوهُمْ وَلَا تَتَّخِذُوا مِنْهُمْ وَلِيًّا وَلَا نَصِيرًا﴾

89.Wanapenda lau mngekufuru kama walivyokufuru wao mkawa sawasawa, Basi msifanye katika wao marafiki mpaka wahame katika njia ya Mwenyezi Mungu. Wakikataa wakamateni na muwaue popote muwakutapo, wala msifanye katika wao rafiki wala msaidizi.

﴿إِلَّا الَّذِينَ يَصِلُونَ إِلَىٰ قَوْمٍ بَيْنَكُمْ وَبَيْنَهُم مِّيثَاقٌ أَوْ جَاءُوكُمْ حَصِرَتْ صُدُورُهُمْ أَن يُقَاتِلُوكُمْ أَوْ يُقَاتِلُوا قَوْمَهُمْ وَلَوْ شَاءَ اللَّـهُ لَسَلَّطَهُمْ عَلَيْكُمْ فَلَقَاتَلُوكُمْ فَإِنِ اعْتَزَلُوكُمْ فَلَمْ يُقَاتِلُوكُمْ وَأَلْقَوْا إِلَيْكُمُ السَّلَمَ فَمَا جَعَلَ اللَّـهُ لَكُمْ عَلَيْهِمْ سَبِيلًا﴾

90.Ila wale waliofungamana na watu ambao baina yenu na wao mna ahadi, au wakawajia hali ya vifua vyao vina dhiki kupigana nanyi au kupigana na watu wao, Lau Mwenyezi Mungu angelitaka angewasaliti nao wakapigana nanyi. Watakapojitenga nanyi, wasipigane nanyi na wakawapa amani, basi Mwenyezi Mungu hakuwafanyia njia ya kupigana nao.

IMEKUWAJE KUWA MAKUNDI MAWILI KATIKA HABARI YA MAKAFIRI

Aya 88-90

MAANA

Mna nini nyinyi mmekuwa makundi mawili katika habari ya wanafiki

Aya hii ilishuka kuwahusu wanafiki waliobaki katika mji wa Makafiri na wala wasihame kwenda Madina, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu: "Mpaka wahame." Kwa sababu Hijra (kuhama) inakuwa ni kutoka mji wa ukafiri kwenda kwenye mji wa uislam tu. Na kabla ya kutekwa Makka, mji wa Madina pekee ndio uliokuwa mji wa uislam.

Dhahiri ya Aya hii ni wazi kuwa hukumu ya aliyekuwa mnafiki, akabaki katika mji wa ukafiri sio hukumu ya mnafiki anayekaa katika mji wa kiislamu. Kwani Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameamrisha kuuawa hao na kuwateka, kinyume cha hawa.

Kabla ya kushuka amri hii Masahaba walitofautiana, wakagawanyika makundi mawili kuhusu hukumu ya wanafiki ambao wamebaki kwenye mji wa ukafiri. Kundi moja likaonelea kuwa ni lazima kuvunja uhusiano nao na kuacha kuwasaidia na chochote, tena kuwatangazia vita; sawa na aliyedhihirisha ushirikina na uadui kwa waislamu. Kundi jingine likaonelea kuweko kuvumiliana kuwasamehe na kuwafanyia muamala wa waislamu. Inaonyesha kuwa Mtume(s.a.w.w) alinyamaza kuhusu tofauti hizi mpaka Mwenyezi Mungu alipompa ufumbuzi kwa kusema kwake:

Mna nini nyinyi mmegawanyika makundi mawili katika habari ya wanafiki.

Yaani haitakikani mtofautiane kuhusu mambo yao, bali ni juu yenu kuwa na kauli moja ya kutovumiliana nao kwa hali yoyote ile; na Mwenyezi Mungu akabainisha sababu ya hilo kwa kusema kwake:

Na hali Mwenyezi Mungu amewageuza kwa yale waliyoyachuma.

Yaani amewarudisha kwenye hukumu, ya makafiri wanaopiga vita, ya kujuzu kuwaua na kuwateka. Kwa sababu hao ni kama kafiri anayepiga vita tu, au wana madhara zaidi kwa kubakia kwao kwenye mji wa ushirikina ambao hana faida nao isipokuwa adui wa uislamu.

UPOTEVU

Je, mnataka kumwongoza ambaye Mwenyezi Mungu amemuacha kupotea.

Hii inafahamisha kwamba lile kundi lililotaka kuwavumila lilikuwa na matumaini ya kuwa hao wanafiki watarudi kwenye uongofu, Mwenyezi Mungu akaikata tamaa yao kwa kusema:

Na ambaye Mwenyezi Mungu amemwacha kupotea hatampatia njia.

Unaweza kuuliza : Kwanza Mwenyezi Mungu -uliotukuka usemi wake - ameeleza kwamba Yeye amewageuza hao wanafiki kwa sababu ya kuchuma kwao na kuchagua kwao kubaki katika mji wa makafiri, kisha tena anasema kwamba Yeye ndiye aliyewapoteza, Kwa hiyo upotevu ameutegemeza kwake baada ya kuutegemeza kwao, Sasa kuna wajihi gani katika kukusanya yote mawili?

Jibu : Makusudio ya aliyeachwa kupotea na Mwenyezi Mungu sio kuwa ni kuumba upotevu kwao, la isipokuwa ni kwamba mwenye kukengeuka na njia ya haki na uongofu kwa matakwa yake akifuata njia ya batili na upotevu kwa hiyari yake, basi Mwenyezi Mungu ataachana naye na atamwacha na mambo yake. Hapana mwenye shaka kwamba mtu anayeachiwa na Mwenyezi Mungu, hatapata njia ila ya upotevu. Maana haya ndiyo yanayooana na kauli yake Mwenyezi Mungu:"Na hali Mwenyezi Mungu amewageuza kwa yale waliyoyachuma."

Kwa ufasaha zaidi ni kwamba kila mwenye kufuata njia ya haki, hakika Mwenyezi Mungu anamwingiza katika usaidizi wake na kumchunga kwa tawfiki yake:

﴿إِنَّ اللَّـهَ مَعَ الَّذِينَ اتَّقَوا وَّالَّذِينَ هُم مُّحْسِنُونَ﴾

"Hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wale wanaomcha na wale wafanyao mema" (16:128)

Usaidizi huu, kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa wanaomcha unaitwa uongofu, tawfiki, mapenzi na utegemezi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na kila mwenye kufuata njia ya upotevu, Mwenyezi Mungu huachana naye wala hamrudishi kwenye uongofu kwa kumlazimisha. Kuachana naye huku kunaitwa upotevu, utwezaji na kugeuzwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Kwa ibara moja ni kwamba upotevu kutoka kwa Mwenyezi Mungu maana yake ni ukombo sio usawa: na maana ya uongofu kutoka kwake Mwenyezi Mungu ni upole na upangaji wa mambo. Hapana budi kuwa hekima ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) inapelekea upole kwa mja wake na kutoepukana naye; sawa na mama asivyoepukana na mwanawe.

Ila itakapokuwa mja ndio sababu inayowajibisha kuepukana na Mwenyezi Mungu kwa njia ya kumwasi; kama mama anavyoepukana na mtoto wake aliyezidi sana kumwudhi.

Wanapenda lau mngekufuru kama walivyokufuru wao mkawa sawasawa.

Kila mtu anapendelea watu wote wawe upande wake, Imetangulia tafsiri yake katika 2:109

Basi msifanye katika wao marafiki mpaka wahame katika njia ya Mwenyezi Mungu, Baada ya kuhama Mtume(s.a.w.w) kwenda Madina, Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwajibisha kuhama (Hijra) kwenda Madina kwa kila mwislamu ila akishindwa au kupewa idhini na Mtume kubaki kwa masilahi yanayowarudia waislam.

Miongoni mwa Aya zilizohimiza kuhama ni:

﴿وَالَّذِينَ آمَنُوا وَلَمْ يُهَاجِرُوا مَا لَكُم مِّن وَلَايَتِهِم مِّن شَيْءٍ حَتَّىٰ يُهَاجِرُوا﴾

"Na wale walioamini lakini hawakuhama hamna haki ya kuwalinda hata kidogo mpake wahame" (8:72)

Siri ya hilo - kama uonavyo - ni kw amba Waislamu walikuwa wachache kabla ya kutekwa Makka. Kama wakitengana huku na huko watakuwa wanyonge na maadui watavamia. Lakini kama wakikusanyika mahali pamoja karibu na Mtume(s.a.w.w) watakuwa na nguvu na kuogopewa. Zaidi ya hayo kuna faida nyingi zinazotokana na kuwa pamoja na mshikamano.

Kukaendela kuhama kwenda Madina ni wajibu mpaka ilipotekwa Makka na Mtume, Mwenyezi Mungu akamnusuru mja wake na maadui zake na kuingia watu kwenye dini ya Mwenyezi Mungu makundi makundi, na kukawa hakuna sababu ya kuhama.

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema"Hapana kuhama baada ya kutekwa (Makka)."

Wakikataa wakamateni na muwaue popote muwakutapo.

Yaani hao wanafiki kama hawatawacha mji wa ukafiri na kuhama kwenda Madina na kuungana na Mtume na waislamu, basi wakamateni na muwaue popote mtakapowapata.

Wala msifanye katika wao rafiki wala msaidizi.

Yaani achaneni nao kabisa, msiwasaidie wala kuwalinda katika chochote.

Unaweza kuuliza : Uislamu ni dini ya uhuru na kuvumiliana na vikundi vyote na watu wa dini zote na sharia yake, ikilinda maisha ya watu, tena watu wote, na haki zao za kimaana na kimaada, bila ya kuangalia rai, maoni yao na itikadi zao. Sasa imekuwaje hapa unaamrisha kuwateka wanafiki na kuwaua popote watapopatikana?

Jibu : Kuna tofauti baina ya makundi na watu wa dini, bali hata na walahidi wanaotangaza maoni yao na itikadi zao kwa watu na wasidhamirie uadui kwa watu wala wasipange njama au kuwasaidia wanaovunja haki; kuna tofauti kubwa sana baina ya hawa na wanafiki ambao wamedhihirisha uislamu na kufichika na neno la uislamu na wakabaki katika mji wa makafiri kwa makusudio ya kuwafanyia vitimbi waislamu, kuwafanyia njama na kuwasaidia maadui. Kwa hiyo amri ya kuwateka na kuwaua ni malipo ya uadui wao na njama zao kwao. Ama kuvumiliana kwa uislamu na vikundi vingine na watu wa dini nyingine, kunafungamana na msingi wake katika kuuhami uhuru wa kila mtu na kuacha kulazimisha katika maoni na itikadi, iwe ya haki au ya batili, maadamu kila mtu ana mzigo wake, na watu wako katika amani.

Swali la pili lililotokana na jibu la swali la kwanza: Uislam unavumiliana na wanafiki; sawa na unavyovumilia na makundi mengine na watu wa dini nyingine kwa dalili ya kuwa Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake kujipurukusha nao; kama ilivyotangulia katika Aya 63 ya Sura hii: "Basi achana nao na uwape mawaidha"

Jibu : Aya hiyo ilishuka kwa wanafiki waliokuwa pamoja na Mtume(s.a.w.w) Madina. Hawakuwa na wasaa wa kushirikiana na washirikina kwa kuwa mbali nao na kuwa karibu na Mtume na vile vile nguvu za waislamu. Na Aya tuliyonayo (89) ilishuka kwa wanafiki waliong'anga'nia kubakia katika mji wa makafiri kwa ajili ya kuwachimba waislamu.

Zaidi ya hayo Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume kuwafanyia amani wanafiki wakati waislamu walipokuwa dhaifu wenye wasaidizi wachache, Kisha akamwamrisha kuwaua baada ya kuwa uislamu una nguvu na wasaidizi (Ansari) wengi; sawa na alivyowaamuru kuvumilia kule Makka na kupigana jihadi walipokuwa Madina.

Baada ya kuamrisha Mwenyezi Mungu kuadhibiwa hao wanafiki maadui, aliwavua kutokana nao sehemu mbili: Sehemu ya Kwanza ni wale aliowaashiria kwa kauli yake:

Ila wale waliofungamana na watu ambao baina yenu na wao mna ahadi.

Hapa Mwenyezi Mungu Mtukufu anakusudia kwamba katika hao wanafiki mwenye kukimbilia kwa watu ambao wana mkataba wa amani na waislamu, basi mkimbizi huyu hatatekwa wala kuuawa kwa sababu yeye - katika hali hii - anakuwa ana salama na waislamu, sawa na aliyekimbilia kwao; Kwa hiyo hawatamwingilia.

Ni vizuri hapa tumnukuu Razi, anasema: "Jua kwamba hii inadhamini bishara kubwa kwa watu wenye imani. Kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu, aliondoa upanga kwa aliyewakimbilia waislamu, basi kumwondolea adhabu huko akhera aliyekimbilia kwenye mahaba ya Mwenyezi Mungu na mahaba ya Mtume wake ni zaidi." Hapana mwenye shaka kwamba kuwapenda Ahlul bait wa Mtume ni kumpenda Mwenyezi Mungu na Mtume, kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿قُل لَّا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ أَجْرًا إِلَّا الْمَوَدَّةَ فِي الْقُرْبَىٰ﴾

Sema: "Siwaombi malipo yoyote isipokuwa kuwapenda ndugu(kizazi changu) ." (42: 23)

Sehemu ya pili Mwenyezi Mungu amewaashiria kwa kusema:

Au wakawajia hali ya kuwa vifua vyao vina dhiki kupigana na nyinyi au kupigana na watu wao.

Yaani wale ambao wanaona uzito kupigana na waislamu pamoja na watu wao washirikina au kupigana na watu wao pamoja na waislamu, na wakaja kwa Mtume(s.a.w.w) kutaka awaridhie wawe katika msimamo usiofungamana na upande wowote, hawa vile vile wataachwa, hawatauawa wala hatatekwa yeyote katika wao; Kwa sababu hao si wapiga vita.

Mfano bora unaofasiri Aya hii ni ule uliokuja katika Majmaul-bayan kuwa jamaa katika Ashjai walikuja kwa Mtume(s.a.w.w) wakamwambia: "Nyumba yetu iko karibu na yako na tunachukia kukupiga vita na kuwapiga vita watu wetu; na tumekuja il tupatane. Akawakubalia na akapatana nao wakarudi.

Hakuna nguvu na ukweli wa dalili ya kuwa uislamu ni amani kwa mwenye amani na inampiga vita mwenye kupiga vita, kuliko dalili hii.

Lau Mwenyezi Mungu angelitaka angewasaliti nao wakapigana nanyi

Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) hajiingizi kwa matakwa yake ya Takwin[12] Katika mambo ya watu isipokuwa anakusudia kwa kauli yake hii kuwakumbusha waislamu fadhila zake kwao na kwamba inawezekana kuwakusanya wote kwa maadui wa waislamu, lakini Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaondolea hilo kwa wao kuwa na msimamo wa kutofungamana na sehemu yoyote. Kwa hiyo kusema kwake Lau Mwenyezi Mungu angelitaka angewasaliti nao wakapigana nanyi, maana yake ni angeliwafanya wawashambulie na wala asingewajalia na moyo wa kupatana. Na hii si katika matakwa ya Takwin, bali ni matakwa yaTawfiki kama sikosei.

Watakapojitenga nanyi, wasipigane nanyi na wakawapa amani, basi Mwenyezi Mungu hakuwafanyia njia ya kupigana nao.

﴿إِنَّمَا السَّبِيلُ عَلَى الَّذِينَ يَظْلِمُونَ النَّاسَ وَيَبْغُونَ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ﴾

"Hakika njia iko kwa wale wanaodhulumu watu na wakawafanyia jeuri katika ardhi pasipo haki" (42: 42)

﴿لَّا يَنْهَاكُمُ اللَّـهُ عَنِ الَّذِينَ لَمْ يُقَاتِلُوكُمْ فِي الدِّينِ وَلَمْ يُخْرِجُوكُم مِّن دِيَارِكُمْ أَن تَبَرُّوهُمْ وَتُقْسِطُوا إِلَيْهِمْ ﴾

"Mwenyezi Mungu hawakatazi kuwafanyia hisani na uadilifu wale ambao hawakupigana nanyi kwa ajili ya dini wala hawakuwafukuza katika nchi zenu" (60: 8)

"Na wakielekea katika amani, nawe pia ielekee" (8: 61)

Na Aya nyinginezo zinatoa mwito wa mapenzi, udugu na usawa, vilevile kusaidiana katika kila jambo lenye masilahi ya watu kwa njia yoyote. Kuchunga zaidi kwa haki kuliko katika uislamu ni kwamba unazingatia kuutumikia ubinadamu kuwa ndio uti wa mgongo wa dini, bali ndio njia pekee ya kumwelekea Mwenyezi Mungu.

﴿ سَتَجِدُونَ آخَرِينَ يُرِيدُونَ أَن يَأْمَنُوكُمْ وَيَأْمَنُوا قَوْمَهُمْ كُلَّ مَا رُدُّوا إِلَى الْفِتْنَةِ أُرْكِسُوا فِيهَا فَإِن لَّمْ يَعْتَزِلُوكُمْ وَيُلْقُوا إِلَيْكُمُ السَّلَمَ وَيَكُفُّوا أَيْدِيَهُمْ فَخُذُوهُمْ وَاقْتُلُوهُمْ حَيْثُ ثَقِفْتُمُوهُمْ وَأُولَـٰئِكُمْ جَعَلْنَا لَكُمْ عَلَيْهِمْ سُلْطَانًا مُّبِينًا ﴾

91. Mtawakuta wengine wanataka wapate amani kwenu na wapate amani kwa watu wao; kila wakirejezwa kwenye fitna hudidimizwa humo.

Wasipojitenga nanyi na kuwapa amani wala kuzuia mikono yao, basi wakamateni muwaue popote muwakutapo; na hao ndio ambao tumewafanyia hoja zilizo wazi juu yao.

MTAWAKUTA WENGINE

Aya 91

HAKUNA KUUANA WALA VITA KATIKA UISLAM

Aya zilizotangulia zimeonyesha namna mbali mbali za wale ambao Mtume(s.a.w.w) alipata kutoka kwao aina za vitimbi na uasi kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Aya hii inaonyesha sura nyingine ya kundi la watu ambao ni wengi kila wakati na kila mahali. Yaani wale wenye dhambi ambao hawana msimamo isipokuwa kugeukageuka tu; wanaamini msimamo fulani kwa muda tu; kisha wanaukanusha.

Sisi hatukatai kuwa binadamu anageuka kutokana na hali zake, hilo hutokea mara nyingi kama tulivyoeleza katika kufasiri 2: 143, kifungu cha 'Kubadilika hulka na fikra.' Lakini pamoja na yote haya tunaitakidi - kulingana na hali ilivyo - kwamba baadhi ya watu wana tabia ya kigeugeu wanabadilika kutoka hali hii hadi nyingine, hata kama wakiwa katika hali moja tu.

Mtawakuta wengine wanataka wapate amani kwenu na wapate amani kwa watu wao; kila wakirejezwa kwenye fitna hudidimizwa humo.

Makusudio ya kurejezwa ni kuitwa, fitna ni ukafiri na kudidizwa ni kuingia. Maana yake ni kuwa kundi hili kila linapoitwa kwenye ukafiri na kurtadi wanakubali na kuwa wabaya zaidi ya kafiri uliyethibiti ukafiri wake. Maelezo mazuri hasa kuelezea hali yao, ni yale waliyoyasimulia baadhi ya wafasiri kuwa, wao walikuwa wanaporudi kwa watu wao, mmoja wao huambiwa sema kombamwiko (mende) ni Mungu wangu na nyani ni Mungu wangu, naye hukubali na kusema hivyo hivyo.

Kadiri wanavyofikia watu hawa katika hali ya kuporomoka, kukosa utu, na kigeugeu baina ya ukafiri na imani, lakini Uislam unawaacha tu na mambo yao, maadam hawajafanya uadui wala vita. Ikiwa watafanya uchokozi na wakapigana, basi uislam unaamrisha kupigana nao popote walipo, ikiwa watakuwa wanaendelea na vita. Haya ndiyo aliyoyakusudia Mwenyezi Mungu kwa kusema kwake.

Wasipojitenga nanyi na kuwapa amani wala kuzuia mikono yao, basi wakamateni muwaue popote muwakutapo.

Hii ni dalili miongoni mwa dalili kadhaa zinazoelezewa na Qur'an na Hadith za Mtume kwamba msingi wa dini ya Kiislamu ni kutoua wala kupigana vita ila kwa kumzuia mwenye kupigana na kueneza ufisadi duniani.

Kwa hivyo basi uislamu umeruhusu vita kwa namna ile ile iliyoruhusu sheria za zamani na za sasa na kukubaliwa na akili zote. Pamoja na dalili zote hizi, maadui wa uislamu bado wanang'ania kusema kuwa uislam ni dini ya upanga; sawa na yule aliyesema: "Ni mbuzi tu hata kama akiruka."

Angalia Aya iliyotangulia kisha uikutanishe na hii, utaona kila moja inatilia mkazo kuwa vita havikukubaliwa katika sharia ila kwa kujikinga na kuondoa ufisadi.

﴿ وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ أَن يَقْتُلَ مُؤْمِنًا إِلَّا خَطَأً وَمَن قَتَلَ مُؤْمِنًا خَطَأً فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ وَدِيَةٌ مُّسَلَّمَةٌ إِلَىٰ أَهْلِهِ إِلَّا أَن يَصَّدَّقُوا فَإِن كَانَ مِن قَوْمٍ عَدُوٍّ لَّكُمْ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ وَإِن كَانَ مِن قَوْمٍ بَيْنَكُمْ وَبَيْنَهُم مِّيثَاقٌ فَدِيَةٌ مُّسَلَّمَةٌ إِلَىٰ أَهْلِهِ وَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مُّؤْمِنَةٍ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ شَهْرَيْنِ مُتَتَابِعَيْنِ تَوْبَةً مِّنَ اللَّـهِ وَكَانَ اللَّـهُ عَلِيمًا حَكِيمًا ﴾

92.Wala haiwi kwa muumini kumwua muumini (mwenzake) ila kwa kukosea. Na mwenye kumwua muumini kwa kukosea, basi amwache huru mtumwa mwislamu na atoe diya kwa watu wake ila watakapoifanya sadaka. Na ikiwa ni mmoja wa watu walio maadui zenu, naye ni muumin, basi ni kuacha huru mtumwa muumini. Na ikiwa ni katika watu ambao baina yenu nyinyi na wao pana ahadi, basi ni diya kwa watu wake na kumwacha huru mtumwa muumini. Na ambaye hakupata basi ni kufunga miezi miwi li yenye kufuatana. Ni kitubio kitokacho kwa Mwenyezi Mungu; na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima.

﴿ وَمَن يَقْتُلْ مُؤْمِنًا مُّتَعَمِّدًا فَجَزَاؤُهُ جَهَنَّمُ خَالِدًا فِيهَا وَغَضِبَ اللَّـهُ عَلَيْهِ وَلَعَنَهُ وَأَعَدَّ لَهُ عَذَابًا عَظِيمًا﴾

93.Na mwenye kumuua muumini kwa kukusudia, basi malipo yake ni Jahannam, ni mwenye kudumu humo; na Mwenyezi Mungu amemughadhibikia na amemlaani na amemwandalia adhabu kubwa.

KUUA KWA KUTOKUSUDIA NA KUKUSUDIA

Aya 92-93

MAANA

Wala haiwi kwa muumin kumwua muumin (mwenzake) ila kwa kukosea. Na mwenye kumwua muumin kwa kukosea, basi amwache huru mtumwa mwislamu na atoe diya kwa watu wake ila watakapoifanya sadaka.

Kuua kuko aina tatu:

1. Kukusudia: Ni kudhamiria mtu mwenye akili aliyebaleghe kumwua mwingine moja kwa moja; kama vile kuchinja na kunyonga. Au kwa kusababisha; kama vile kutia sumu kwenye chakula au kumzuilia mtu asile mpaka afe na njaa.

Ukithibiti usawa wa muuaji na muuliwa kidini na kiungwana, na wala muuaji asiwe ni baba wa muuliwa, hapo msimamizi wa aliyeuliwa atakuwa na hiyari ya kumuua kwa kulipiza kisasi au kuchukua fidia ikiwa muuaji atakubali kuitoa.

Hiyari ya kulipiza kisasi na kuchukua fidia ni ya msimamizi (walii) katika kuua kwa makusudi, Akichagua fidia, basi muuaji anayo hiyari ya kutoa fidia au ajitolee kuuawa, Kwa hiyo msimamizi hawezi kumlazimisha muuaji kutoa fidia wala muuaji hawezi kumlazimisha msimamizi kuchuka fidia.

Fidia ya kisheria ni Dinar elfu moja ambazo ni sawa na 3.529 Kg za dhahabu.

2. Bila ya kukusudia: Ni kuwa muuaji amekusudia kitendo, lakini akakosea makusudio; kama kumpiga mototo kwa kumtia adabu akafa. Kuua kwa aina hii kunawajibisha fidia sio kisasi. Fidia yake ni Dinar elfu moja; kama fidia ya kukusudia. Tumezungumza kuhusu kuua kwa makusudi na shabihi - kusudio, katika kufasiri (2: 178 - 179)

3. Kukosea: Ni kuwa muuaji alikosea kitendo na makusudio; kama mwenye kupiga mshale mnyama ukampata mtu ukamuua, Hapo mtu siye aliyekusudiwa kufumwa wala kuuliwa. Haya ndiyo makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Na mwenye kumwua mwislamu kwa kukosea, basi amwache huru mtumwa mwislamu na diya kwa watu wake ila watakapoifanya sadaka.

Qur'an na Hadith kwa pamoja zimefahamisha kuwa mwenye kumuua mwislam kwa maksudi, basi ni wajibu kwake atoe kafara ya kumwacha huru mtumwa, kufunga miezi miwili yenye kufuatana na kuwalisha masikini sitini; atakusanya yote matatu, Hili ndilo linaloitwa kafara la kuchanganya.

Ikiwa kuua ni bila ya kukusudia au kukosea, basi atatoa kafara la kumwacha huru mtumwa; akishindwa afunge miezi miwili inayofuatana, akishindwa awalishe masikini sitini.

Fidia ya kuua kwa makosa mzigo wake utabebwa na walio baleghe wenye akili na walio na uwezo katika ndugu wa karibu wa upande wa baba; kama vile kaka, ami na watoto wao wanaume. Kiasi cha fidia ni 1000 Dinar. Fidia ni haki ya walii (wasimamizi) wa aliyeuliwa; wakipenda wataidai na wakitaka wataisamehe Ndipo Mwenyezi Mungu akasema,

ila wakiifanya sadaka .

Mafakihi wanasema limewajibishwa kafara kwa mwenye kuua bila kukusidia ili kuwa ni onyo la uzembe na h imizo la kuchukua tahadhari katika mambo yote. Imewajibishwa fidia kwa ndugu zake kwa kumuhurumia aliyekosea. Na kumewajibishwa kuchukuliwa kisasi kwa aliyeua makusdi, ili kumtia adabu kwa kukusudia haramu.

Na ikiwa ni mmoja wa watu walio maadui zenu, naye ni muumin, basi ni kuacha huru mtumwa muumin.

Makusudio ya watu walio maadui ni makafiri wenye vita na waislamu. Dhamiri ya 'naye' inarudia kwa aliyeuawa. Maana yake ni kuwa mwislamu akiua mtu kwa kuitakidi kwamba yeye ni kafiri, kisha ikabainika kuwa yeye ni mwislamu anayekaa kwa watu wake waliomakafiri, hapo hapatakuwa na chochote kwa muuaji zaidi ya kumwacha huru mtumwa; hakutakuwa na fidia. Kwa sababu watu wa aliyeuliwa ni makafiri, wakipewa fidia itawongezea nguvu kuwapiga vita waislamu.

Na ikiwa ni katika watu ambao baina yenu nyinyi na wao pana ahadi, basi ni diya kwa watu wake na kumwacha huru mtumwa muumin. Na ambaye hakupata basi ni kufunga miezi miwili yenye kufuatana.

Yaani ikiwa mwislamu aliyeuawa kimakosa anatokana na watu makafiri, lakini hawana vita na waislam kwa vile wana mkataba wa amani na waislamu, hapa itatolewa fidia kwa watu wake, hata kama ni makafiri, kwa sababu hukumu yao katika hali hii ni sawa na hukumu ya waislamu katika wajibu wa fidia.

Na ni juu ya muuaji kutoa kafara la kumwacha huru mtumwa, akishindwa afunge miezi miwli inayofuatana. Imewekwa sharia hii ya kafara kwa muuaji ili iwe ni toba kwa aliyoyafanya.

Na mwenye kumuua muumin kwa kukusudia, basi malipo yake ni Jahannam, ni mwenye kudumu humo; na Mwenyezi Mungu amemughadhibikia na amemlaani na amemwandalia adhabu kubwa.

Tumeeleza mwanzo wa maelezo namba (1) kuhusu hukmu ya aliyeua makusudi na kwamba yeye atauwawa ila akisamehe walii. Katika Aya hii Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anataja kwamba malipo yake huko akhera ni kukaa milele motoni, ghadhabu na laana ya Mwenyezi Mungu na adhabu kubwa.

Adhabu zote hizi nne ni kutilia mkazo. Makusudio ya ukubwa wa adhabu kutokana na kosa hili ni kuwa ni kosa kubwa la kutisha na kwamba ni katika madhambi makubwa ambayo hayana mfano wake zaidi ya ukafiri, Baadhi ya mafakihi wamesema: Ni udhihirisho zaidi wa ukafiri na maana yake.

Utakuja ufafanuzi wa kuua nafsi kwa dhulma 'Inshaallah' katika kufasiri (5:32), Na yemetangulia maelezo ya kudumu motoni katika kufasiri (2, 257) kifungu cha 'kudumu motoni.'

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا ضَرَبْتُمْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَتَبَيَّنُوا وَلَا تَقُولُوا لِمَنْ أَلْقَىٰ إِلَيْكُمُ السَّلَامَ لَسْتَ مُؤْمِنًا تَبْتَغُونَ عَرَضَ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا فَعِندَ اللَّـهِ مَغَانِمُ كَثِيرَةٌ كَذَٰلِكَ كُنتُم مِّن قَبْلُ فَمَنَّ اللَّـهُ عَلَيْكُمْ فَتَبَيَّنُوا إِنَّ اللَّـهَ كَانَ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرًا ﴾

94.Enyi mlioamini! Mtakaposafiri katika njia ya Mwenyezi Mungu, basi hakikisheni wala msimwambie mwenye kuwapa Salaam: Wewe si mwislam. Mnataka mafao ya duniani na kwa Mwenyezi Mungu kuna ngawira nyingi! Hivi ndivyo mlivyokuwa nyinyi hapo mbeleni, na Mwenyezi Mungu akawafanyia hisani. Basi hakikisheni; hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa mnayoyatenda.

KUUDHIHIRISHA UISLAM KUNATOSHA KUWA NI KUUTHIBITISHA

Aya 94

MAANA

Enyi mlioamini! Mtakaposafiri katika njia ya Mwenyezi Mungu, basi hakikisheni, wala msimwambie mwenye kuwapa salamu: Wewe si mwislamu.

Wameafikiana wafasiri na wapokezi wa Hadith sababu iliyowajibisha kushuka Aya hii ni kuwa Mtume alituma kikosi katika Masahaba wakakutana na mtu mmoja mwenye mali; kama kondoo n.k. Wakamdhania ni kafiri; akatamka neno la kufahamisha uislamu wake, katika maamkuzi au tamko la shahada n.k. Baadhi wakaona hiyo ni kutaka kujiokoa na kifo, waka mwua.

Mtume alipolijua hili alihisi taabu na kumlaumu muuaji akasema: Hakika amehifadhika na kuuliwa kwa tamko hilo. Akamwambia - kama inavyoelezwa katika baadhi ya riwaya - "Huoni kuwa umeupiga mapande moyo wake!"

Matamshi ya Aya hayakatai maana haya, Kwani kauli yake, mtakaposafiri katika njia ya Mwenyezi Mungu, basi thibitisheni, Maana yake mtakapokwenda kwen ye Jihadi pelelezeni; msikimbilie kumua ambaye mnamtilia shaka katika dini yake na uadui wake; wala msimwambie mwenye kuwapa salamu wewe si mwislamu. Kwa sababu kila mwenye kudhihirisha uislamu anayo haki waliyonayo waislam; hasa katika mambo ya kuhifadhi damu na mali ama batini yake inajulikana kwa Mungu peke yake.

Mnataka mafao ya duniani na kwa Mwenyezi Mungu kuna ngawira nyingi!

Inafahamisha kuwa lililowapelekea kuua ni tamaa ya mali aliyokuwa nayo. Hilo ndilo lililowafanya wawaze kuwa kudhihirisha kwake tamko la uislamu kulikuwa na makusudio ya kuokoka. Ni mara nyingi sana mtu kufikiria yale yasiyo ya uhakika. Inakuwa hali ilivyo ni vingine, hata kama anajua ndivyo hivyo, Haya ndiyo maajabu ya mtu.

kwa hali yoyote Mwenyezi Mungu amewatanabahisha makosa yao haya na kwamba wao wameharakia ngawira na ngawira za Mwenyezi Mungu na neema zake hazina idadi, ambazo atawabadilishia na mali ya aliyeuwa wa zaidi na zaidi,

Hivyo ndivyo mlivyokuwa nyinyi zamani

Hili ni jibu lao na kukivunja kitendo chao kwa mantiki ya kiakili na ya hali halisi.

Taarifa yake ni kuwa nyinyi hapo mwanzo mlikuwa washirikina, kisha mkaingia katika Uislam kwa tamko lile lile alilolitamka yule aliyeuliwa; na Mtume alilikubali kutoka kwenu. Kwa tamko hili zimehifadhiwa damu zenu na mali zenu. Kwa hiyo ilikuwa ni juu yenu kumkubalia yule mliyemuua kama vile Mtume alivyowakubalia nyinyi, Hivi ndivyo walivyo watu wengi, wanataka wengine waridhie uchache, lakini wao wenyewe hawaridhii.

Na Mwenyezi Mungu akawafanyia hisani

Kwa kuwakubalia uislam na kuwafanya ni katika Masahaba kwa kutamka tu tamko la shahada, wala Mtume hakuyachunguza yaliyo nyoyoni mwenu. Kwa nini hamkufanyia mwingine vile alivyowafanyia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w)

Basi hakikisheni; hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa mnayoyatenda.

Yaani kuanzia sasa msifanye kitu mpaka muwe na uhakika nacho wala msimwadhibu yeyote kwa tuhuma au dhana. Hakika Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa matukio yenu na ana hisabu kwa mnavyostahiki. Mafakihi wameiingiza Aya hii katika Aya za hukumu[13] na wakatoa hukumu mbili za sharia.

Kwanza : Wajibu wa kuhakikisha katika kila kitu, hasa katika hukumu za kisharia na zaidi hasa katika damu na mali; ambapo wamewajibisha mafakihi katika mawili hayo kujichunga na kufanya ihtiyat na wakaongezea pia kuhusiana na tupu.

Pili : Kila mwenye kutamka tamko la uislamu na akasema mimi ni mwislamu, basi hukumu yake ni hukumu ya waislam katika ndoa urithi na mengineyo ambayo yanafungamana na mtu akidhihirisha uislamu tu. Sio kwa undani.

﴿لَّا يَسْتَوِي الْقَاعِدُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ غَيْرُ أُولِي الضَّرَرِ وَالْمُجَاهِدُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ فَضَّلَ اللَّـهُ الْمُجَاهِدِينَ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ عَلَى الْقَاعِدِينَ دَرَجَةً وَكُلًّا وَعَدَ اللَّـهُ الْحُسْنَىٰ وَفَضَّلَ اللَّـهُ الْمُجَاهِدِينَ عَلَى الْقَاعِدِينَ أَجْرًا عَظِيمًا ﴾

95.Hawawi sawa waumini waliokaa - wasiokuwa wenye madhara - na wenye kupigana jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zao na nafsi zao. Amewatukuza Mwenyezi Mungu katika cheo wale wapiganao katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zao na nafsi zao kuliko waliokaa, Na wote Mwenyezi Mungu amewaahidi wema. Na amewatukuza Mwenyezi Mungu wenye kupigana Jihadi kwa malipo makubwa kuliko waliokaa.

﴿دَرَجَاتٍ مِّنْهُ وَمَغْفِرَةً وَرَحْمَةً وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا﴾

96.Ni vyeo kutoka kwake na maghufira na rehema. Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira mwenye kurehemu.

WENYE KUPIGANA JIHAD NA WENYE KUKAA

Aya 95 - 96

MAANA

Hawawi sawa waumini waliokaa - wasiokuwa wenye madhara - na wenye kupigana jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zao na nafsi zao.

Mwenye kubaki nyuma asiende katika jihadi kwa udhuru wa kisheria; kama vile upofu, ulemavu na mengineyo, basi amesamehewa, bali atapata malipo mema akiwa ni muumin mwenye ihlasi anayependa ushindi wa dini, na heri ya watu wake; na anayependelea lau angalikuwa mzima akashiriki na wanaopigana jihadi.

Kuna Hadith isemayo:"Mtu yuko pamoja na anayempenda." Yaani, mwenye kumpenda mwenye kupigana jihadi si kwa chochote ila kwa kuwa yeye ni mwanajihadi, basi naye ana malipo ya wapigania jihadi; mwenye kumpenda mkweli kwa sababu ya ukweli wake basi yeye yuko katika cheo chake; mwenye kumpenda dhalimu katika dhulma yake; basi yeye ni mshirika wake na mwenye kumpenda kafiri kwa ukafiri, basi ni kama yeye. Hii ndiyo hukumu ya wenye kukaa wasiokuwa na siha nzuri.

Ama wale wasiokuwa na udhuru katika wao wataangaliwa. Wakikaa bila ya kwenda kwenye jihadi ambayo wamewajibishiwa wao na wengineo; yaani kuwa vita ni vya wote. Hapo hawatasamehewa, bali watalaumiwa na ni wenye kustahili adhabu.

Kwa sababu wao wameasi, kwa hiyo haifai kuwalinganisha na wapiganaji kwa hali yoyote kwa sababu kulinganisha ni kushirikisha; na hawa hawakushirikiana na wapigana jihadi katika kitu chochote; hata kama ikiwa jihadi ni faradhi kifaya (ya kutosheana), isiyokuwa na haja ya kushiriki wote, lakini bado wapigana jihadi ni bora kuliko waliokaa. Kwa sababu wao wamechagua uvivu - kujiuzulu na vita. Hawa ndio waliokusudiwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hawawi sawa waumini waliokaa"

Kwa hiyo maana yanakuwa ni hawawi sawa mbele ya Mwenyezi Mungu waliokaa, walio wazima na wale wapigania Jihadi ambao haikuwa jihadi ni wajibu kwao tu, bali ilikuwa wajibu kwa wote kwa njia ya kifaya, lakini wao ndio walioziba wajibu huu na wakautekeleza kwa ukamilifu na kuuondoa kwa waliobaki. Ni maana haya ambayo ameyakusudia Mwenyezi Mungu na kuyafafanua kwa kauli yake:

Amewatukuza Mwenyezi Mungu katika cheo, wale wapiganao katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zao na nafsi zao kuliko waliokaa.

Baada ya Mwenyezi Mungu kukanusha usawa baina yao na baina ya wale waliokaa anabainisha yale yaliyowapambanua wapigania Jihadi; ambayo ni ubora wao katika cheo kuliko waliokaa.

Kwa hiyo inakuwa kauli yake hii ni ufafanuzi baada ya kueleza kwa ujumla. Na siri ya kutukuzwa ni kama tulivyoeleza, kuchukua majukumu ya ulinzi peke yao; sawa na lau adui anashambulia mji, kukatokea kikundi kuwazuiwa kinyume cha kikundi kingine, hapo kimsingi kikundi cha kwanza kitatofautika na kikundi cha pili.

Ingawaje kikundi cha pili hakitaadhibiwa baada ya cha kwanza kusimamia wajibu na kupatikana lengo lililotakikana. Kwa hiyo ndio Mwenyezi Mungu akasema:

Na wote Mwenyezi Mungu amewaahidi wema

Lakini tena akarudia kutilia mkazo na kuhimiza Jihadi kwa kusema:

Na amewatukuza Mwenyezi Mungu wenye kupigana Jihadi kwa malipo makubwa kuliko waliokaa.

Na akabainisha malipo haya makubwa kuwa:Ni vyeo kutoka kwake na maghufira na rehema .

Cheo kimoja tu kutoka kwa Mwenyezi Mungu ni bora kuliko ulimwengu na vilivyomo ndani yake, je itakuwaje vyeo vingi! Ama rehema yake, hakuna kitu bora zaidi kuliko hiyo ila ambaye imetokana naye. Na inatosha kwa maghufira yake kuwa ni kusalimika na adhabu yake na machukivu yake.

Haya ndiyo maghufira, rehema na cheo kwa Mwenyezi Mungu. Mwenye kupata moja tu, atakuwa katika walio juu, sikwambii atakayeyapata yote! "Ewe Mola wangu! Hakika mimi nakuomba wepesi katika rehema yako na maghufira yako; na wewe wajua kuwa mimi naihitajia.

Kwani itakuwaje kama utanineemesha na kunikwasisha? Kwani unahofia maghufira yako yatakwisha na hazina ya rehema yako (itakwisha)? Au ni nini ewe Mola wangu! Au ni kwa kuwa mimi nina dhambi? Ndio, lakini hujui kwamba mimi najua kuwa hakuna kimbilio ila kwako tu na kwamba kunanifurahisha mimi kunisamehe! Ewe Mola wangu! Ikiwa mimi ni muongo kwa niliyosema, basi nifanyie vile ninavyostahiki, na ikiwa ni mkweli kwa niliyoyasema, basi fanya vile unavyostahiki"

ALI NA ABU BAKR

Amesema Razi (ninamnukuu): "Wamesema Shia kuwa Aya hii: Amewatukuza Mwenyezi Mungu wenye kupigana Jihadi kwa malipo makubwa kuliko wenye kukaa. Inafahamisha kuwa Ali bin Abu Twalib ni bora kuliko Abu Bakr. Kwa vile Ali alipigana Jihadi zaidi ya Abu Bakr" Kipimo cha utofauti ni kuwa Ali alikuwa ni katika waliopigana Jihadi katika alivyomzidi Abu Bakr, na Abu Bakr alikuwa katika waliokaa. Ikiwa hivyo basi imewajibika kuwa Ali(a.s) ni bora kuliko Abu Bakr." Kisha Razi akawajibu Shia kwa kuse ma: "Tunawaambia: Kuua kwa Ali makafiri kulitokana na Mtume, kwa hiyo itawalazimu kwa hukumu yenu hii ya Aya, kuwa Ali ni bora kuliko Muhammad(s.a.w.w) . Na haya hayasemwi na mwenye akili. Kama mkisema: Kupigana Jihadi kwa Mtume pamoja na Makafiri ni kukubwa zaidi kuliko kwa Ali, kwa sababu Mtume alikuwa akipigana kutokana na dalili na ubainifu, kuondoa shubha na upotevu, na kwamba jihadi hii ni kamilifu zaidi kuliko hiyo. Basi tunasema: Na sisi tukubalieni kuhusu Abu Bakr kama mfano wake."

Huku ni ni kulala kabisa kwa mwanafalsafa wa wafasiri na wala siwezi kukuita kusinzia. Kwa sababu hizi zifuatazo:-

Kwanza : kila mwenye kumlinganisha Muhammad(s.a.w.w) na mmoja wa maswahaba zake, katika kuleta dalili na ubainifu, basi atakuwa ametoka katika uislamu, atake asitake. Kwa sababu Muhammad anatoa ubainifu kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu -kama tutakavyoeleza- na maswahaba wanatoa kutokana na mafunzo yake. Kwa hiyo basi cheo cha kwanza ni cha Mwenyezi Mungu peke yake hana mshirika, cha pili ni cha Muhammad peke yake hana mwenzake na kuwamini wote wawili kuko daraja moja.

Kwa vile kumwamina Mungu na mitume yake ni nguzo moja katika nguzo zinazousimamisha uislam, haitoshi moja peke yake. Ukhalifa na uswahaba ni matawi ya kumwamini Mungu na Mitume, na tawi haliwezi kufananishwa na shina.

Pili : Maana yaliyo wazi ya neno wenye kupigana Jihadi katika Aya, ni Jihadi kwa upanga, si kwa kingine kwa kukiri Razi katika tafsiri yake. Lakini yeye ameghafilika na aliyoyasema na akajipinga mwenyewe.

Hebu tuiache dhahiri ya Aya na tafsiri zote, tumrudie yule ambaye Qur'an imeteremshwa kwenye moyo wake na tumwulize, ni yupi mbora wa watu? Tumsikilize atajibu nini, Amepokea Muslim katika sahih yake, kwamba mtu mmoja alimwuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Ni nani mbora wa watu?" Akasema:"Ni mtu anayepigana Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa nafsi yake na mali yake."

Sote tunajua kuwa Ali alipigana zaidi Jihadi; kama alivyosema Razi, kwa hivyo anakuwa mbora wa watu, isipokuwa Mtume(s.a.w.w) ; ambapo hakuna chochote zaidi ya daraja ya utume ila Uungu - kama tulivyobainisha - Na kila mmoja anajua kwa uwazi kwamba Jihadi kwa nafsi ni bora na kubwa kuliko Jihadi kwa mali. Kwa sababu mali hutolewa katika njia ya Jihadi kwa nafsi, lakini nafsi haitolewi katika njia ya mali.

Tatu : Hakika Mtume Mtukufu(s.a.w.w) - kama tulivyotangulia kueleza - hakutoa dalili na hakubainisha,wala hakuondoa utatanishi yeye mwenyewe; bali yote yanatoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alikuwa akimwelezea Muhammad(s.a.w.w) naye akifikisha kwa kunukuu kwa herufi, Muhammad anaambiwa.

"Sema: Ataihuisha yule aliyeiumba mara ya kwanza" (36:79)

"Sema: Je, yuko katika washirika wenu aongozaye katika haki?" (10: 35)

﴿قُلْ فَأْتُوا بِسُورَةٍ مِّثْلِهِ وَادْعُوا مَنِ اسْتَطَعْتُم مِّن دُونِ اللَّـهِ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ﴾

"Sema: Hebu leteni Sura moja mfano wake na muwaite muwezao asiyekuwa Mwenyezi Mungu mkiwa mnasema kweli." (10: 38)

﴿قُلْ أَفَاتَّخَذْتُم مِّن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ لَا يَمْلِكُونَ لِأَنفُسِهِمْ نَفْعًا وَلَا ضَرًّا﴾

"Sema: Je, mnawafanya wengine badala yake kuwa ni walinzi na hawajifai wenyewe kwa nafuu wala dhara" (13: 16)

Na Aya nyingine kadha, Jambo la ajabu ni kuwa Razi ameghafilika nazo baada ya kurefusha ufafanuzi na tafsiri zake. Ajabu ya maajabu ni pale aliposema: "Basi na sisi tukubalieni kuhusu Abu Bakr kama mfano wake;" yaani kama mlivyomkubalia Muhammad.

Hapana! tena hapana mara elfu! Si sisi wala mwislam yeyote atakayekukubalia wewe au mwengine kuwa Abu Bakr awe na mfano wa aliyo nayo Muhammad(s.a.w.w) (katika kuleta dalili, hoja na kuondoa utatanishi na upotevu. Ila ikiwa Abu Bakr ni Mtume anayeteremshiwa Wahyi.

Zaidi ya haya cheo cha Ali katika elimu hakikurubiwi na yeyote katika Masahaba. Inatosha kuwa ni ushahidi wa hilo. Hadith mutawatir iliyopokewa kutoka kwa Mtume inayosema: "Mimi ni jiji la elimu na Ali ni mlango wake." Zimehifadhiwa turathi za kiislam kutokana na elimu ya Ali, kiasi ambacho hakikuhifadhiwa kutoka kwa Abu Bakr wala Sahaba mwengineo.