MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE 0%

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE Mwandishi:
: SALMANI SHOU
Kundi: Misingi mikuu ya Dini

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

Mwandishi: KIMEANDIKWA NA SAYYID MUJTABAA MUUSAWIY LARI
: SALMANI SHOU
Kundi:

Matembeleo: 27506
Pakua: 2660

Maelezo zaidi:

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 28 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 27506 / Pakua: 2660
Kiwango Kiwango Kiwango
MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

Mwandishi:
Swahili

16

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA KUMI NA SITA

MATATIZO, SABABU YA KUAMKA

Watu waliolewa kiburi cha madaraka na mafanikio na ambao wamesahau kabisa maadili ya kibinadamu kwa sababu ya upotofu wa roho na hisia zao, wakati fulani wataona kwenye pembe mbali mbali za dunia, kwamba matokeo ya matukio yasiyopendeza huwafanya wakubali mabadiliko ya msingi na maendeleo ambayo huwafungulia mapazia ya usahaulifu. Wanaweza hata kuongozwa kwenye njia inayoelekea kwenye kiwango fulani cha ukamilifu wa maadili na maisha yao ya siku za usoni ambayo ni mazuri zaidi kuliko ya wakati huo. Hawa ni watu ambao matatizo yamedukiza mabadiliko makubwa kwao.

Tukizingatia athari zenye madhara za uzembe na ulevi wa kiburi kwa upande mmoja, na masomo mengi ya maadili yanayofundishwa tokana na matatizo kwa upande mwingine, inaweza kusemekana kwamba kutofaulu na matatizo ni hali zinazowiana kwa kadiri ambavyo zinakuwa na baraka kubwa; zinatoa mchango mzuri katika ujenzi wa utambuzi na utashi wa mwanadamu.

Matatizo basi, ni kitangulizi cha hali za juu zaidi na zilizoendelea za maisha; humtayarisha mwanadamu kwa ajili ya malipo yanayomngojea yeye, na kutoka kwenye witikio wake kuhusu jambo hili, inakuwa wazi kama amefikia kiwango cha juu cha uaminifu na kujitolea au amezama kwenye uoza. Qur'ani inasema:

لَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ فِي كَبَدٍ ﴿٤﴾

"Hakika tumemuumba mtu katika kupambana na taabu." (90:4)

Au inasema tena:

وَلَنَبْلُوَنَّكُم بِشَيْءٍ مِّنَ الْخَوْفِ وَالْجُوعِ وَنَقْصٍ مِّنَ الْأَمْوَالِ وَالْأَنفُسِ وَالثَّمَرَاتِ وَبَشِّرِ الصَّابِرِينَ ﴿١٥٥﴾ الَّذِينَ إِذَا أَصَابَتْهُم مُّصِيبَةٌ قَالُوا إِنَّا لِلَّـهِ وَإِنَّا إِلَيْهِ رَاجِعُونَ ﴿١٥٦﴾ أُولَـٰئِكَ عَلَيْهِمْ صَلَوَاتٌ مِّن رَّبِّهِمْ وَرَحْمَةٌ وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُهْتَدُونَ ﴿١٥٧﴾

"Hapana shaka tutakujaribui kwa chembe ya hofu, na njaa, na upungufu wamali na nafsi na matunda. Na wabashirie wenye subira. Wale ambao ukiwafika msiba wao husema: Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na kwake Yeye hakika tutarejea. Hao juu yao zitakuwa baraka zitokazo kwa Mola Wao na rehama. Nao ndio wenye kuongoka." (2:155-157).

Bila shaka Mwenyezi Mungu angeweza kuumba dunia isiyo na matatizo, magumu na maafa, lakini hiyo ingemaanisha kumnyang'anya binadamu uhuru na fursa ya kuchagua; binadamu angekuwa ameachwa katika dunia vivi hivi tu kama kiumbe kisicho na utashi au uwezo wa kuamua, kama vile kiumbe kingine chochote kisichokuwa na fikra na utambuzi.

Baada ya kupata hasara kubwa kabisa ya kupoteza uwezo wake wote wa asili na uhuru, ambao ndio rasilimali yake ya thamani sana, je, binadamu angeweza kuendelea kuelekea kwenye ukamilifu, au angeoza na kuanguka? Dunia je, pia isingepoteza ubora na uzuri wake wote, haya yakiwa yanaeleweka tu katika tofauti zao? Ni wazi kwamba uwezo wa kutofautisha na kuainisha huwezesha kuwepo kwa wema na uovu, uzuri na ubaya. Kwa kumpa binadamu neema isiyokadirika ya hiari na uwezo wa kuchagua, Mwenyezi Mungu ambaye hekima yake inadhihiri kwenye maumbile yote, alitaka kuonyesha kikamilifu uwezo wake wa kuumba viumbe vyenye kushuhudia hekima na nguvu zake.

Aliweka kwenye uhai wa mwanadamu uwezekano wa kutenda yote mema na mabaya, na ingawa hamlazimishi kutenda lolote kati ya hayo, wakati wote Mwenyezi Mungu anamtegemea mwanadamu kutenda wema. Mwenyezi Mungu haafiki uovu; ni tabia njema ndio inayopata ridhaa Yake, na kwa badala yake Yeye hutoa thawabu nyingi sana zisizo na kifani. Mwenyezi Mungu humwonya binadamu dhidi kufuata njia ya uovu na humhofisha na adhabu na mateso kama akifanya hivyo.

Hivyo, kwa kutumia uwezo wa hiari yake, ambayo Mwenyezi Mungu amempa, mwanadamu anaweza kufanya kama awezavyo, kwa kufuata mwongozo wa ki-Mungu na dhamira yake mwenyewe. Lakini, endapo wakati fulani atateleza na kufanya dhambi, njia inabaki wazi kwake kurudi kwenye utakaso na nuru, kwenye neema na huruma ya Mwenyezi Mungu. Hili peke yake ni udhibitisho zaidi wa ukarimu wa Mwenyezi Mungu na uadilifu unaovienea vyote, neema mojawapo nyingine ambayo amewapa waja wake.

Kama Mwenyezi Mungu angekuwa atoe thawabu haraka kwa waja wake wema kwa ajili ya tabia zao adilifu na matendo yao mema, wasingekuwa bora zaidi kwa namna yoyote kulinganishwa na watu waovu na wenye dhambi. Na kama watu waovu kiakili na kimatendo wakati wote wangepewa adhabu na mapatilizo ya papo hapo, maadili mema na utakatifu visingeweza kupata ubora wowote hapa duniani dhidi ya uovu na ukware.

Kanuni ya hitilafu, kwa kweli, ndio msingi wa dunia iliyoumbwa; ndio inayowezesha vitu kubadilika na kugeuka ili kwamba neema ya Mwenyezi Mungu ienee duniani. Kama maada ingekuwa isichukue maumbo tofauti kama matokeo ya migongano na viumbe vingine na maisha yasingekuwa na uwezo wa kuchukua miundo mengine, utofautishaji na maendeleo ya maisha hayangewezekana. Dunia isiyoyumba na kubadilika itafanana na mtaji usiotumika ambao hauzalishi faida yoyote. Kwa maumbile, mabadiliko ni mtaji unaozalisha faida. Kama mambo yalivyo ni kwamba inawezekana kwamba uwekezaji wa kiasi fulani cha mtaji uishie kwenye hasara, lakini usongevu wa wakati wote wa maada kwa ujumla haswa husababisha matokeo yenye faida. Hitilafu inayotokea katika miundo ya maada huishia kwenye maendeleo ya utaratibu wa maisha kuelekea kwenye ukamilifu.

Kuna swali fulani kuhusu kama uovu upo hapa duniani kwa maana halisi ya neno lenyewe. Endapo tutatazama kwa uangalifu, tutaona kwamba uovu wa vitu si sifa halisi; ni sifa ya uhusiano. Silaha zilizoko mikononi mwa adui yangu ni mbaya kwangu, na silaha iliyoko mikononi mwangu ni mbaya kwa adui yangu. Mimi na adui yangu tukiwekwa pembeni, silaha zenyewe zote ima sio mbaya au nzuri. Uelekeo wa maumbile unaweza kusemekana kuwa ni wa kimahesabu, yaani ni kwamba, mfumo wake umewekwa kwa namna ambayo hauwezi kutosheleza mahitaji yetu yote. Hata hivyo, tunataka kutimiza matakwa yetu yasiyo na idadi bila kukabiliana na kipingamizi chochote, na nguvu za asili hazitimizi matakwa yetu mengi tunayoyathamini, matakwa ambayo kwa hali yoyote ile hayana faida kwa mtazamo wa asili yetu muhimu ya kimaumbile. Maumbile hayazingatii matakwa yetu na hukataa kukubali mahitajio yetu. Kwa hiyo, tunapokutana na mambo yasiyo pendeza katika maisha yetu, tunakasirika bila uhalali wowote na tunaziita sababu hizo za kusumbuka kwetu kuwa ni "uovu."

Endapo mtu anataka kuwasha taa yake ambapo haina mafuta, hataanza kushusha pumzi na kulalamika au kulaani dunia yote! Wakati wote maumbile huelekea kwenye lenyo lililodhahiri, kupita juhudi na mapambano. Sababu maalum huamua kila hatua inayochukuliwa, na mabadiliko na maendeleo yanayofanyika hayakubuniwa kukidhi uthibitisho wa mwanadamu au kutosheleza matakwa yao. Lazima ikubalike kwamba baadhi ya matukio ya ulimwengu huu hayawezi kuendana na matakwa yetu, na si lazima tuvifikirie vitu visivyotupendeza kuwa ni udhalimu.

Ali(a.s) Amirul-Mu'minin anaielezea dunia kama makazi ya mashaka, lakini hata hivyo, ni mahali pazuri kwa mtu anayeijua dunia sawa sawa. Ingawa yeye mwenyewe alikukabiliana na aina zote za matatizo na maudhi, kila wakati alikuwa anawatahadharisha wanadamu kuhusu uadilifu kamili ya Mwenyezi Mungu.38 Jambo lingine la muhimu ambalo ni lazima tusilisahau ni kwamba wema na ubaya haviwakilishi namna mbili pamoja za kipekee au sanjari katika mpango wa maumbile. Wema ni sawa na uhai, na uovu ni sawa na kutokuwepo uhai; popote kiumbe chenye uhai kinapotokea, kutokuwepo na uhai pia kunajiashiria.

Tunapozungumzia umaskini, ufukara na ujinga au maradhi tusidhani kwamba kila moja kina uhalisi wake peke yake; umasikini kwa kifupi ni 38 Nahju al-Balaghah, kilichohaririwa na Subhi Salh, uk. 493. kutokuwa na mali, ujinga ni kukosekana kwa elimu na maradhi ni kutokuwa na afya. Mali na elimu ni mambo halisi, lakini umaskini si kingine zaidi ya kuwa na mkononi na mifuko mitupu, na ujinga ni ukosefu wa elimu. Hivyo, umaskini na ujinga havina uhalisi wa kugusika; vinaelezeka kwa kupitia kutokuwepo kwa vitu vingine.

Ni vivyo hivyo kuhusu majanga na mabalaa ambayo huwa tunayafikiria kuwa ni uovu na chanzo cha mateso. Mambo haya ni aina ya hasara au kutokuwepo kitu, na yanakuwa mabaya kwa maana ya kwamba husababisha kuharibika au kutokuwepo kwa kitu kingine mbali na yenyewe. Mbali na haya, hakuna kitu kingine kwa kadiri kinavyoweza kuwepo kinachoweza kwa hali yoyote kuitwa kiovu au kibaya. Kama majanga yasingefuatana na magonjwa na kifo, kupotea na kuharibika kwa viumbe fulani, hivyo kuzuia uwezo wao wa kusambaa, yasingekuwa mabaya. Ni kupotea na kuharibika kunakotokana na maafa yenye asili ya ubaya. Chochote kilichopo duniani ni chema; uovu unafungamana na kutokuwepo kwa kitu, na kwa kuwa kutokuwapo kitu hakufanyi jamii juu ya maisha, hakikuumbwa kwa hiyo hakipo.

Kiumbe na kisicho kiumbe ni sawa na jua na kivuli chake. Wakati umbile likielekezwa kwenye jua linatupa kivuli. Kivuli ni nini? Kivuli hakijaumbwa na kitu chochote; kinategemea pale jua linapokuwa halifikishi miale yake mahali fulani kwa sababu ya kuwepo kizuizi; hakina chanzo au asili yake chenyewe binafsi.

Vitu vina uhai halisi kwa sababu ya kuwa vimeumbwa bila ya kuhusisha vitu vingine mbali na vyenyewe; kwa maana hii, vitu hivi sio viovu. Kwa falsafa ya maisha itokanayo na imani ya kuwepo Mwenyezi Mungu, ulimwenguni sawasawa na wema. Kila kiumbe kwa asili ni chema; kama ni kiovu, kinakuwa hivyo tu katika maana ya ulinganisho tu katika kukiunganisha na vitu vingine visivyokuwa hicho chenyewe. Uhai wa kila kiumbe sio wa kweli kwa kitu kingine mbali na chenyewe, na kisi- choguswa na viumbe.

Mbu wa malaria mwenyewe tu sio mwovu. Kama akielezewa kwa namna hiyo, ni kwa sababu ana madhara kwa mwanadamu na anasababisha ugonjwa. Ambacho kimeumbwa ni uhai wa kitu ndani yake na kwa chenyewe, ambacho ni uhai wa kweli; kuwepo kwa kitu kwa kubahatisha au wa kimasharti hakuna nafasi katika mpangilio wa maisha na sio kweli. Kwa hiyo, hatuwezi kuuliza kwa nini Mwenyezi Mungu ameumba vitu vyenye kuhusiana au vya kutegemea hali - masharti. Vitu vya kutegemea hali au vitu vya kufikirika havitenganishiki na vitu halisi vinavyotokana navyo; ni viambatani visivyoepukika na havichukui sehemu ya uhai wao. Mtu hawezi kuzungumzia vitu vya kutegemea hali (au shuruti ya kuwepo vitu vingine) kuwa vimeumbwa.

Kiumbe ambacho ni halisi kina umuhimu wa lazima wa kupata uhai wake kutoka kwa Muumbaji. Ni vitu vile tu na sifa zile ambazo ni halisi ambavyo vinapatikana nje ya akili. Sifa za kuhusiana hutengenezwa na akili na hazipatikani kuwepo nje yake, hivyo mtu hawezi kumtafuta muumbaji. Zaidi ya hayo, kitu chenye uwezekano wa kuwepo ni ulimwengu wote kwa ujumla, pamoja na vitu vyote vilivyomo humo na sifa ambazo hazitenganishiki nao; ulimwengu uwakilisha kitu kisichogawanyika. Kutokana na sehemu ya inayofaa kutazamia hekima ya Mwenyezi Mungu, ama ulimwengu lazima uwepo katika mfumo ambao ni wa pekee juu yake, au usiwepo kabisa.

Ulimwengu usio na utaratibu au kanuni ya kisababishi, dunia ambayo wema na uovu havikuachanishwa, ingekuwa ni kitu kisichowezekana na ni njozi. Si rahisi kudhania kwamba sehemu moja ya dunia inaweza kuwepo na nyingine isiwepo. Maumbile ni kitu kizima kamili, kama muundo na umbo la mtu, na viungo vyake havitenganishiki.

Mwenyezi Mungu si muhitaji wa chochote na moja ya matokeo ya hili ni kwamba huweka viumbe kwa uhuru kabisa, kama mtu karimu ambaye ukarimu wake mkubwa hautazamii shukrani, au kama fundi stadi ambaye wakati wote hushughulika na kutengeneza vitu vipya. Ukarimu mkubwa kama huo na ubunifu unafafanua dhati ya Mola Mtukufu ambaye ishara zake zinaonekana na ziko wazi kwenye kila kiumbe.

17

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA KUMI NA SABA

BAADHI YA VIPENGELE VYA TOFAUTI

Tuchukulie kwamba mwenye kiwanda ameajiri wafayakazi wenye ujuzi na wasio na ujuzi kukiendesha na kukisimamia kiwanda chake. Wakati wa kuwalipa mishahara yao unapofika, anawalipa wale wajuzi na wenye sifa ambao kazi yao ni ya kiwango cha juu, malipo makubwa zaidi ya yale ya wafanyakazi wasio na ujuzi. Sasa je, tofauti hii katika mishahara ni haki au sio haki? Mmiliki wa kiwanda anatenda kwa usawa au kwa upendeleo? Bila shaka kuna tofauti iliyoingia hapa, lakini hatuwezi kuiita ubaguzi. Uadilifu haumtaki mmiliki wa kiwanda kuwalipa wafanyakazi wasio na ufundi mshahara sawa na wale wenye ujuzi. Ina maana badala yake kwamba anapaswa kulilipa kila kundi kile linachostahili kupata. Kanuni ya aina hii itafafanua kwa uwazi kabisa kadirio linalolingano kwa kila kazi na kuchangia kwenye ustawi wa mahali hapo pa kazi.

Kutofautisha katika masuala kama haya ni aina ya uadilifu yenye kujieleza vizuri na ya kivitendo, bila kufanya hivyo ingekuwa sawa na ukandamizaji, ubaguzi na dhuluma; ingekuwa ni matokeo ya tathmini pungufu ya thamani wakilishi ya vitu katika kuvitofautisha kwake.

Tunapoitazama dunia kwa ujumla na kuchambua sehemu zake mbali mbali, tunaona kwamba kila sehemu ina nafasi na kazi yake maalum na imefunikwa na sifa ambazo zinafaa juu yake. Katika kutambua huku, tunaweza kuelewa umuhimu wa mabadiliko katika maisha ya binadamu, ya mwanga na giza, ya kufuzu na kushindwa, kwa ajili ya kudumisha ulinganifu wa dunia kwa ujumla.

Kama dunia ingekuwa inafanana, bila ya mabadiliko au tofauti, aina zenye tofauti na nyingi za viumbe zisingekuwepo. Ni katika aina mbali mbali hizi na wingi wake uliopo hasa ambamo tunaiona fahari na utukufu wa dunia. Uamuzi wetu juu ya vitu utakuwa na mantiki, sahihi na wa kukubalika wakati tutakapo zingatia ulingano uliopo ulimwenguni na uhusiano ambao kwa manufaa kabisa unaunganisha sehemu zake mbalimbali na kila moja yao, si pale tunapochunguza sehemu moja katika mtindo wa kuitenga yote kabisa.

Mpango wa maumbile umeegemezwa kwenye ulinganifu, juu ya upatikanaji na uwezo; kile kinachothibitika kabisa katika maumbile ni utofautishaji, si ubaguzi. Uzingatiaji huu unatuwezesha kuchunguza jambo hili kwa busara zaidi na kwa uhakika. Ubaguzi unamaanisha kutofautisha miongoni mwa vitu vyenye upatikanaji mmoja uleule na vilivyomo katika mazingira mamoja yaleyale. Utofautishaji unamaanisha kuonyesha tofauti miongoni mwa uwezo usio sawa na usiotawaliwa na mazingira mamoja.

Itakuwa si sahihi kama tutsema kwamba ingekuwa nzuri zaidi kwa kila kitu hapa duniani kuwa namna moja na isitofautiana, kwani mwendo wote, shughuli na ubadilikaji motomoto tunaouona duniani unawezeshwa na utofautishaji. Binadamu anazo njia nyingi za kutambua na kuzoea uzuri, pindi panapokuwepo ulinganisho baina ya uzuri na ubaya. Mvuto unaowekwa na uzuri, kwa maana fulani, ni kuakisi kwa ubaya na uwezo wake wa kurudisha nyuma.

Kwa njia hiyo hiyo, kama binadamu asingejaribiwa na kutahiniwa katika maisha, uchamungu na maadili mema vingekuwa havina thamani, na kungekuwa hakuna sababu ya kutakasa roho ya mtu na hakuna kitu cha kumfanya mtu ajizuie matamanio yake. Kama turubai zima limekuwa katika hali moja ya kufanana, hatuwezi kusema hiyo ni picha, ni tofauti za rangi mbali mbali na mpangilio wake ndio ambao huonyesha ustadi wa msanii. Ili utambulisho wa kitu ujulikane, ni muhimu kitofautishwe na vitu vingine, kwani kipimo ambacho hutumika kutambua vitu au watu ni tofauti za ndani au nje zilizopo baina yao.

Moja ya ajabu za maumbile ni tofauti katika uwezo na vipaji ambavyo viumbe vimepewa. Ili kuhakikisha maisha ya jamii yanaendelea, maumbile yamempa kila mtu seti maalum ya muonjo na uwezo, ambavyo muingiliano wao unahakikisha nidhamu ya jamii, kila mtu hutimiza baadhi ya mahitaji ya jamii na anachangia katika kutatua baadhi ya matatizo yake.

Tofauti ya kawaida baina ya watu kuhusu uwezo wao huwa inasababisha wao kuhitajiana. Kila mmoja wao huchukua baadhi ya kazi za jamii kwa mujibu wa muonjo na uwezo wake, na maisha ya kijamii yanayohifadhiwa kwa njia hiyo humwezesha mtu kusonga mbele na kuendelea.

Hebu tuchukue jengo au ndege Ulaya kama mfano. Kila kimojawapo cha vitu hivi kina sehemu nyingi tofauti, visehemu vigumu na vilivyopangwa vinavyo tofautiana sana kwa ukubwa na maumbo, tofauti hii inatokana kwenye wajibu ambao kila sehemu inao kwenye kitu kizima hicho.

Kama tofauti hii isingekuwa iwepo kwenye umbile la ndege Ulaya, basi isingekuwa ndege Ulaya tena isipokuwa mchanganyiko wa vyuma mbali mbali. Kama utofautishaji ni dalili ya uadilifu wa kweli katika ndege Ulaya, lazima pia iwe ni ishara ya uadilifu wa ki-Mungu miongoni mwa viumbe vyote vya dunia pamoja na binadamu. Zaidi ya hayo, lazima tutambue kwamba upambanuzi miongoni mwa viumbe ni asili kwenye chimbuko lao. Mwenyezi Mungu haumbi kitu kwa matumizi ya pekee na tofauti ya utashi Wake; utashi Wake haitumiki kwa kitu kipekee. Ulimwengu wote tangu mwanzo hadi mwisho ulitokea kuwepo kwa zoezi moja la utashi Wake; ilikuwa ni hili ambalo limeviwezesha viumbe katika kuongezeka kwao kusiko na ukomo, kuja kuwepo.

Halafu, ipo sheria na utaratibu maalum ambao hudhibiti vipimo yote vya muumbo. Ndani ya mfumo wa visababishi, hutoa daraja na nafasi ya pekee kwa kila kitu. Matakwa ya Mwenyezi Mungu kuumba na kuutengemaza ulimwengu ni sawa na utaratibu Wake ulioko tayari ndani yake. Zipo thibitisho za kifalsafa za uhakika zinazounga mkono pendekezo hili, na pia imefafanuliwa kwenye Qur'ani:

إِنَّا كُلَّ شَيْءٍ خَلَقْنَاهُ بِقَدَرٍ ﴿٤٩﴾ وَمَا أَمْرُنَا إِلَّا وَاحِدَةٌ كَلَمْحٍ بِالْبَصَرِ ﴿٥٠﴾

"Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo, na amri Yetu haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho." (54:49-50).

Itakuwa ni makosa kudhania kwamba utofautishaji na uhusiano uliowekwa na Mwenyezi Mungu katika uumbaji Wake ni sawa na uhusiano wa kidesturi uliopo katika jamii ya binadamu. Uhusiano wa Mwenyezi Mungu na viumbe vyake si jambo la kawaida au kutambulikana tu; ni uhusiano utokanao kwenye lile tendo hasa la uumbaji wenyewe. Utaratibu ambao ameuweka kwenye vitu vyote ni matokeo ya Yeye kukiumba kitu hicho. Kila kiumbe hupokea kutoka kwa Mwenyezi Mungu kiasi cha ukamilifu na uzuri ambao kina uwezo wa kuupokea.

Kama usingekuwepo utaratibu maalum wa kuudhibiti ulimwengu, kiumbe chochote kingeweza, katika uelekeo wa mwendo wake, kusababisha kutokeza kwa kiumbe kingine chochote, na sababu ya athari vingeweza kubadilishana nafasi zao. Lakini ni lazima ieleweke kwamba mahusiano muhimu miongoni mwa vitu yamekadiriwa na ni ya lazima; kituo na sifa iliyowekwa kwenye kitu huambatana bila kutengana nacho, kwa daraja lolote na kiwango chochote kitakachokuwa nacho. Hakuna kitu kinachoweza kwenda kinyume na kiwango ambacho kimekadiriwa kwa yake na kuchukua daraja ya kiumbe kingine. Utofautishaji ni kiambata cha viwango vya viumbe, kinachoviwekea vipimo vinavyotofautiana vya udhaifu na nguvu, upungufu na ukamilifu.

Ikatuwa ubaguzi kama vitu viwili vilikuwa na uwezo sawa wa kupokea ukamilifu lakini ukatolewa kwa kimojawapo tu na kingine kikanyimwa. Kiwango cha kiumbe ambacho kipo katika mpango wa maumbile hakiwezi kulinganishwa na madaraja ya kawaida ya jamii ya binadamu. Viwango hivyo ni halisi, si vya kawaida, na havihamishiki. Kwa mfano wanadamu na wanyama hawawezi kubadilishana nafasi kwa namna ile ile watu binafsi wanavyoweza kubadilishana kazi na vyeo wanavyokalia katika jamii.

Uhusiano unaounganishwa kila kisababisho na athari zake na kila athari na chanzo chake hutokana na asili ya chanzo na athari kwa mpango huo. Kama kitu ni chanzo, ni hivyo kwa sababu ya sifa fulani ambayo haiwezi kuachanishwa nacho, na kama kitu ni athari, ni hivyo kwa sababu ya sifa ya kimsingi juu yake, ambayo si nyingine mbali na namna ya kuwepo kwake. Halafu, upo utaratibu muhimu na mzito sana unaounganisha viumbe vyote, na kiwango cha kila kiumbe ndani ya mpango huo unafanana na asili yake. Kwa kadiri utofautishaji unavyohusika kwenye upungufu uliopo kwenye asili, si ubaguzi, kwa sababu mmiminiko wa neema za Mwenyezi Mungu hautoshelezi kwa ukweli kujitokeza na kuwepo; upokeaji wa chombo kinachotakiwa kupokea neema hiyo pia ni muhimu. Ni kwa sababu hii kwamba viumbe fulani hupatwa na kutojiweza na havipati viwango vya juu; haiwezekani kwamba kitu kipate uwezo wa kuwa kiumbe au ukamilifu mwingine na kwamba Mwenyezi Mungu asikipatie sifa hiyo.

Suala la namba (numerali) unafanana hasa; kila tarakimu ina nafasi yake iliyokadiriwa. Mbili huja baada ya moja na haiziwezi kubadilishana nafasi hiyo. Kama tutabadilisha nafasi ya tarakimu, tutakuwa wakati huo tumebadilisha asili yake. Ni wazi kwa hiyo, kwamba viumbe vyote vinamiliki madaraja yaliyokadiriwa na visaidizi na huwa chini ya mlolongo wa sheria imara na zisizobadilika. sheria ya Ki-Mungu kwa kawaida haifanyi kuwa kitu tofauti kilichoumbwa, bali fikra ya kinadharia iliyochukuliwa kutoka kwenye hali ile ambayo vitu huonekana kuwepo. Kile ambacho kina uhai wa nje kinakuwa na viwango na daraja ya kiumbe, kwa upande mmoja, na mfumo wa chanzo na athari, kwa upande mwingine. Hakuna kinachotokea nje ya mpango huu, ambacho si kingine mbali na ile desturi ambayo imetajwa na Qur'ani:"Na hutakuta mabadiliko katika kawaida ya Mwenyezi Mungu." (35:43).

Mpango wa maumbile umekuwa kwenye mlolongo wa sheria zilizo sehemu ya asili yake. Nafasi ya kila kiumbe kilichomo humo imebainishwa wazi wazi, na kuwepo kwa viwango na daraja mbalimbali za uhai ni matokeo ya lazima ya hali ya utaratibu wa muumbile, ambao bila kuepuka husababisha kutokeza jamii mbali mbali na utofautishaji. Mabadiliko na utofautishaji ni vitu ambavyo vyenyewe havikuumbwa; ni sifa zisizotenganishika za viumbe vyote. Kila chembe ulimwenguni imepokea kila chochote ilichokuwa na uwezo wa kukipokea; hakuna dhulma au ubaguzi uliokiadhibu, na ukamilifu wa ulimwengu - unaofanana na jedwali la kuzidisha katika uamrishaji wake sahihi na usiobadilika - hapo umehakikishwa.

Wayakinifu ambao wanachukulia kuwepo kwa mabadiliko na utofautishaji kwenye utaratibu wa asili kama ushahidi wa ukandamizaji na udhalimu na hudhani kwamba ulimwengu hautawaliwi na uadilifu, bila shaka watahisi maisha kama ni magumu, yanayochukiza na kuchosha. Uamuzi huo wa haraka haraka wa wayakinifu unaokabiliwa na dhiki na matatizo ni sawa na uamuzi wa mtoto anayemtazama mwenye bustani anayepogowa matawi ya mti ya kijani yanayostawi vizuri wakati wa msimu wa kuchipua. Bila kutambua makusudi na umuhimu wa kupogowa huko, mtoto huyo atafikiri kwamba mwenye bustani ni mharibifu na mjinga. Kama neema zote za dunia zingewekwa chini ya mamlaka ya myakinifu, bado asingetosheka. Kwani, pindi dunia inapoonekana haina lengo na ikiwa juu ya msingi wa udhalimu, haina maana kwa binadamu kutafuta haki, na katika dunia ambayo inakosa lengo, ni upumbavu kwa mwanadamu kujiwekea lengo.

Ikiwa chimbuko na hatima ya binadamu ni kama wayakinifu wanavyoyaeleza, kana kwamba binadamu ni nyasi zinazojiotea zenyewe na halafu zikatoweka, basi mwanadamu lazima awe kiumbe dhalili kuliko viumbe vyote. Kwani angekuwa anaishi kwenye dunia ambayo imekosa mvuto wote, ulinganifu na utulivu. Mawazo, hisia na wasiwasi vingemsababishia huzuni, ikiwa si chochote zaidi ya mzaha mkali aliofanyiwa na maumbile ili kumwongezea mateso na unyonge na kumzidishia taabu.

Kama mtu mwenye uwezo na kipaji angekuwa ajitolee kuhudumia jamii ya binadamu, ingekuwa na faida juu yake? Ibada maadhimisho ya baada ya kifo chake na kutoa heshima inayofanyika kwenye kaburi lake, yasingemnufaisha hata kidogo; hayo yangekuwa kudumisha hadithi ama maelezo ya kinafiki, kwa sababu mtu anayehusika angekuwa si chochote zaidi ya umbile lililokusanywa na maumbile kwa ajili ya kiburudisho chake kama kitu cha kuchezea kwa muda wa siku chache kabla ya kugeuzwa kuwa ukufi wa vumbi.

Kama tukiangalia majaaliwa ya wengi wa watu ambao wakati wote wanapambana na aina mbalimbali za huzuni, wasiwasi, kuishiwa na kutofaulu, hali inaonekana kufifia zaidi. Kwa msimamo kama huo wa maisha ya mwanadamu, pepo pekee ambayo uyakinifu unaweza kumpa mwanadamu ni wingi wa hofu na mateso. Msimamo wa myakinifu kwamba mwanadamu anakosa uhuru na hiari unamfanya awe kiumbe dhalili zaidi. Falsafa ya maisha ya mtazamo wa mwelekeo mmoja tu ya kiyakinifu ingekuwa na maoni kwamba binadamu ni kama roboti lenye mtambo na nguvu ya chembechembe zake zinazoendeshwa na maumbile. Je, akili na silika ya binadamu - bila kutaja hali halisi za maisha - vinaweza kukubali tafsiri ya kawaida na finyu ya binadamu kama hiyo, maisha yake na hatima yake?

Kama tafsiri hii ingekuwa ya kweli, mwanadamu angekuwa hana uwezo wa kuona furaha kama mwanasesere wa mtoto. Akiwa katika hali kama hiyo, binadamu angelazimika kufanya hisia zake na mielekeo kuwa ndio msingi wa maadili na kipimo cha tathmini, kuamua kila jambo kufuatana na faida na hasara binafsi. Angefanya kila juhudi kuharibu kila kipingamizi kwenye njia yake na kulegeza vizuizi vyote juu ya matamanio yake ya kimwili. Kama binadamu angekuwa afanye vinginevyo, angeonekana kama mtu wa nyuma na mjinga.

Mtu yoyote mwenye kiwango kidogo sana cha utambuzi na anaamua jambo kwa njia ya uadilifu na bila kupendelea ataziona hizi dhana zenye uoni mfinyu na za ajabu kuwa halali, hata kama zingepambwa kwa kiasi gani cha ghilba ya kifalsafa na kisayansi.

Binadamu mwenye falsafa ya maisha ya kidini, anaiona dunia kama mfumo wa utaratibu wenye utambuzi, dhamira, ufahamu na lengo. Hekima kuu ya Mwenyezi Mungu inayotoa uadilifu inatawala juu ya ulimwengu na kila chembe ya uhai na inaziangalia shughuli na matendo yote. Mtu wa kidini, kwa hiyo, anahisi hali ya kuwajibika kwa kuhusiana na ufahamu ambao unatawala ulimwengu, na anajua kwamba dunia iliyoumbwa na kusimamiwa na Mwenyezi Mungu ni muhimu kuwa ni dunia ya umoja, utulivu na nzuri. Anaelewa kwamba hitilafu na uovu vinakuwa vinapatikana kwa ufahamu wa ziada baada ya tafakari ya mwanzoni na kufanya wajibu wa msingi katika upatikanaji wa wema na kutokeza kwa umoja na utulivu.

Zaidi ya hayo, kwa mujibu wa falsafa hii ya maisha ambayo inaweka kielelezo cha upeo mpana kwa ajili ya mwanadamu, maisha hayaishii kwenye dunia hii, na wala maisha ya dunia hii hayakufungwa kwenye hali nzuri ya kimali, utajiri au kuwa huru kutokana na kutofanya juhudi na kutopata matatizo. Muumini wa dini ataiona dunia kama njia ambayo lazima ipitwe, kama mahali pa mitihani, na kama uwanja wa juhudi. Ndani mwake uadilifu wa matendo ya wanadamu hupimwa. Mwanzoni mwa maisha yajayo, wema na uovu katika fikira, imani na matendo ya wanadamu yatapimwa katika mizani sahihi kabisa. Uadilifu wa Mwenyezi Mungu utadhihirika katika hali yake halisi, na kunyimwa kokote kunakoweza kuwa kumefika binadamu hapa duniani, iwe kuhusu mali au vinginevyo, kutafidiwa juu yake.

Kwa kuzingatia kuhusu hatima yake inayomngojea binadamu na kuelewa kubatilika kwa mambo mazuri ya dunia ya kiyakinifu, mtu anaelekeza ufahamu wake kwa kujitahidi kuelekea kwa Mwenyezi Mungu tu. Lengo lake linakuwa ni kuishi kwa ajili Yake na kufa kwa ajili Yake. Hayazingatii mabadiliko ya dunia hii tena. huviangalia vitu vya muda mfupi kwa thamani yake kama vilivyo tu, na haruhusu kitu chochote kushawishi moyo wake. Kwani anajua kwamba nguvu za ushawishi zitasababisha ubinadamu wake kufifia na kumwangusha kwenye kimbunga cha upotofu wa uyakinifu.

Kwa kuhitimisha, tungeongezea kwamba hata ukiachilia mbali suala la uwazi, kuwepo kwa hitilafu hapa duniani haimaanishi udhalimu. Ukandamizaji na udhalimu una maana kwamba mtu fulani anafanyiwa ubaguzi ingawa naye anayo haki sawa na ya mwingine. Lakini viumbe havina "madai" yoyote kwa Mwenyezi Mungu wala kamwe hawakuwa nayo, hivyo basi, endapo baadhi ya vitu vinapata ubora juu ya vingine hii haihesabiki kama dhulima.

Hatuna chochote cha kwetu wenyewe: kila pumzi na kila pigo la moyo, kila fikira na wazo linalopita kwenye akili zetu, yanachukuliwa kwenye hazina ambayo sisi hatuimiliki na hatujafanya kitu katika kujenga. Hazina hiyo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliyotuzawadia sisi wakati wa kuzaliwa.

Pindi tunapoelewa kwamba chochote tulicho nacho si chochote isipokuwa ni zawadi ya ki-Mungu, itadhihirika kwamba tofauti miongoni mwa zawadi anazowapatia wanadamu ziko kwenye msingi wa hekima Yake lakini hazihusiani na ama haki au udhalimu, kwa sababu hapakuwepo na suala la stahili yoyote au madai yoyote upande wetu.

Maisha haya yenye ukomo na ya muda mfupi ni zawadi kwetu, zawadi ya kutoka kwa Muumba; Anayo hiari kamili katika kuamua aina na kiasi cha zawadi Anayotoa, na hatuna dai lolote kwake. Kwa hiyo, hatuna haki ya kukataa hata kama zawadi tunayopewa bure kabisa, inaonekana ndogo na isiyo na maana sana.