MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE 0%

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE Mwandishi:
: SALMANI SHOU
Kundi: Misingi mikuu ya Dini

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

Mwandishi: KIMEANDIKWA NA SAYYID MUJTABAA MUUSAWIY LARI
: SALMANI SHOU
Kundi:

Matembeleo: 27627
Pakua: 2678

Maelezo zaidi:

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 28 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 27627 / Pakua: 2678
Kiwango Kiwango Kiwango
MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

Mwandishi:
Swahili

19

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA KUMI NA TISA

HIARI

Watetezi wa kundi hili la kifikra wanasema kwamba mwanadamu anajitambua mwenyewe kwamba anao uhuru katika matendo yake; anaweza kuamua kama atakavyo na akaanzisha mtindo wa bahati yake kwa mujibu wa hiari yake mwenyewe na mwelekeo wake. Uhai ambao huamuru wajibu wa mwanadamu, majuto anayohisi mwanadamu kwa matendo yake fulani anayoyafanya, adhabu ambayo sheria hutoa kwa wahalifu, matendo wanayotekeleza binadamu ili kubadili mwelekeo wa historia, msingi wa sayansi na teknolojia - yote haya ni mambo yanayothibitisha kwamba mwanadamu anao uhuru katika matendo yake.

Vivyo hivyo, suala la wajibu wa kidini wa mwanadamu, kutumwa kwa mitume, ulinganiaji wa ujumbe mtukufu wa ki-Mungu, na kanuni ya ufufuo na hukumu - yote haya yapo mokononi mwa utashi huru na uchaguzi wa mwanadamu katika matendo ayafanyayo. Ingekuwa haina maana kabisa kama Mwenyezi Mungu kwa upande moja, awashurutishe watu kufanya mambo fulani na kwa upande mwingine awalipe thawabu au awaadhibu. Kwa hakika ingekuwa si uadilifu, kama Muumba wa dunia angetuamuru sisi kufuata njia yoyote aliyochagua Yeye, kwa njia ya uwezo Wake na utashi Wake, na halafu atuadhibu sisi kwa matendo ambayo tumeyafanya bila ya hiari zetu.

Endapo matendo ya watu, kwa kweli yangekuwa matendo ya Mwenyezi Mungu basi uovu wote, ufisadi na ukatili lazima ungechukuliwa kuwa ni matendo ya Yake, ambapo dhati Yake tukufu hasa imeepukana na uovu na udhalimu wote huo. Kama usingekuwapo na uchaguzi huru kwa mwanadamu, dhana yote ya uwajibikaji wa mtu kidini ingekuwa sio ya haki. Dikteta mkandamizaji asingestahili kulaumiwa na mwadilifu asingestahili kusifiwa, kwa sababu wajibu una maana pale tu ndani ya nyanja ya nini kinachowezekana na kinachowezekana mtu kukipata.

Binadamu anastahili shutuma au sifa hapo tu ambapo ana uwezo wa kuamua na kutenda kwa uhuru, vinginevyo, pasingekuwepo na suala la shutuma au sifa. Wale wanaoshikamana na msimamo huo hapo juu wamefikia kiwango katika kutetea kanuni ya hiari ya mtu kiasi kwamba wanamuona mtu kama kiumbe chenye hiari kamili isiyopingika katika matendo yake yote ya hiari. Wanadhani kwamba Mwenyezi Mungu hawezi kuendeleza mamlaka yake juu ya hiari na matakwa ya viumbe Vyake na kwamba matendo ya hiari ya wanadamu hayapo kwenye eneo la mamlaka Yake. Huu, kwa ufupi, ndio msimamo wa watetezi wa hiari kamili.

Wale wasemao kwamba ni kanuni za kawaida na hiari ya wanadamu ndivyo vinavyoumba dunia hii ya ajabu, na kwamba si mzunguuko wa dunia wala matendo ya wanaadamu ambavyo vina uhusiano wowote na Mwenyezi Mungu, wanapachika athari zote kwenye mhimili unaopingana na Mwenyezi Mungu. Angalau kidogo sana, wanavifanya viumbe vilivyoumbwa kama washirika wa Mwenyezi Mungu katika maumbile Yake, au wanamweka mwumbaji kumpambanisha na Mwenyezi Mungu Muumba. Bila kujua wanachukulia kwamba asili za vitu vilivyoumbwa hazitegemei asili ya ki-Mungu.

Kujitegemea kwa kiumbe - kiwe binadamu au kinginecho mbali na mwanadamu - kunaingiza imani kwenye kiumbe hicho na kuwa mshirika wa Mwenyezi Mungu katika matendo Yake na kujitegemea Kwake, kunakomalizikia kwa wazi kabisa katika muundo wa uwili. Hivyo, binadamu anaondolewa kwenye kanuni ya juu sana ya umoja wa ki-Mungu na anatupwa kwenye mtego hatari wa ushirikina. Kukubali fikra za uhuru kamili wa binadamu ingekuwa kumwondolea Mwenyezi Mungu mamlaka Yake kwenye eneo fulani, ambapo kwa kweli, Yeye anaviene a viumbe vyote, kwani tungekuwa tunampa binadamu mamlaka yasiyo na vipingamizi na ya dhahiri kwenye nyanja ya matendo yake huru na ya hiari. Hakuna muumini wa kweli wa upweke wa Mwenyezi Mungu anayeweza kukubali kuwepo kwa uumbaji tofauti na ule wa Mwenyezi Mungu hata katika uwanja wenye mipaka wa matendo ya binadamu.

Wakati tunatambua uhalali wa sababu za asili na vipengele, lazima tuzingatie kuwa Mwenyezi Mungu ni chanzo cha kweli cha utaratibu na matukio yote na tutambue kwamba kama Mwenyezi Mungu angetaka, Angeweza kuutangua hata hapo penye eneo finyu linapotumika na kuufanya usiwe na kazi.

Kama ambavyo viumbe vyote hapa duniani vinavyokosa uhuru katika asili zao, viumbe vyote humtegemea Mwenyezi Mungu, pia vinakosa uhuru katika usababisho na utoaji wa athari. Kwa hiyo, tunayo kanuni ya umoja wa matendo, kwa kwa maana ya kutambua ukweli kwamba mpangilio wote wa maumbile, pamoja na vyanzo na athari zake, sheria na kanuni zake, ni kazi ya Mwenyezi Mungu na ni matokeo ya ridhaa Yake, kila jambo na chanzo linatokana Naye si tu asili ya uhai; lakini pia uwezo wa kutenda na kutoa athari.

Umoja wa matendo hautufanyi sisi tukanushe kanuni ya chanzo na athari na wajibu wake inaouchukua hapa duniani, au kuchukulia kila kitu kuwa kama ni matokeo ya moja kwa moja na yasiyopangwa ya utashi wa Mwenyezi Mungu, kwa namna ambayo kwamba kuwepo au kutokuwepo kwa mambo yasababishayo hakutaleta tofauti. Lakini tusihusishe usababisho huru kwenye mambo hayo, au kudhani kwamba uhusiano wa Mwenyezi Mungu na dunia ni kama ule wa msanii na kazi yake - mathalani, ule wa fundi rangi na kazi yake ya kupaka rangi. Kazi ya usanii inategemea msanii juu ya uanzilishwaji wake, lakini baada ya msanii kumaliza kazi yake, uzuri na mvuto wa kazi hiyo unakuwa huru na msanii huyo, kama msanii akitoweka hapa duniani, kazi yake nzuri sana bado itaendelea kuwepo.

Kudhania uhusiano wa Mwenyezi Mungu na dunia kuwa sawa na aina hiyo ni aina ya ushirikina. Yeyote anaye kanusha nafasi ya Mwenyezi Mungu ndani ya matukio na matendo ya wanadamu, hapo anafikiria kwamba uwezo wa Mwenyezi Mungu unasimama ghafla kwenye mipaka ya maumbile na utashi huru wa mwanadamu. Maoni kama hayo kimantiki hayakubaliki, kwa sababu inakuwa na maana ya kukanusha yote haya; uwezo wote wa Mwenyezi Mungu, na uwekeaji mipaka ile dhati isiyo na mipaka na ukomo.

Mtu mwenye kuzingatia maoni kama hayo atajiona yeye kama asiye na haja yoyote na Mwenyezi Mungu, jambo ambalo litasababisha awe muasi dhidi Yake na kujiingiza kwenye kila namna ya uovu. Kinyume chake, hisia za kumhitaji Mwenyezi Mungu, za kumtegemea Yeye na kunyenyekea Kwake, zina athari za uhakika juu haiba, tabia na mwenendo wa mwanadamu. Kutotambua chanzo kingine cha amri mbali na Mwenyezi Mungu, kiwe cha ndani au cha nje, uchu wa matamanio na matakwa vitakakuwa haviwezi kumburuza huku na kule, na hakuna mtu mwingine atakayeweza kumtawala kabisa.

Qur'ani Tukufu inamkatalia mwanadamu ushiriki wowote na Mwenyezi Mungu katika kuendesha mambo ya dunia hii:

وَقُلِ الْحَمْدُ لِلَّـهِ الَّذِي لَمْ يَتَّخِذْ وَلَدًا وَلَمْ يَكُن لَّهُ شَرِيكٌ فِي الْمُلْكِ وَلَمْ يَكُن لَّهُ وَلِيٌّ مِّنَ الذُّلِّ وَكَبِّرْهُ تَكْبِيرًا ﴿١١١﴾

"Na sema sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu ambaye hana mwana, wala hana rafiki wa kumsaidia kwa sababu ya udhaifu wake. Na mtukuze kwa utukufu mkubwa." (17:111).

Aya nyingi sana kwa wazi zinatangaza uwezo kamili na nguvu za Mwenyezi Mungu. Mathalani:

لِلَّـهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا فِيهِنَّ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿١٢٠﴾

"Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo. Naye ni Muweza wa kila kitu." (5:120),

وَمَا كَانَ اللَّـهُ لِيُعْجِزَهُ مِن شَيْءٍ فِي السَّمَاوَاتِ وَلَا فِي الْأَرْضِ إِنَّهُ كَانَ عَلِيمًا قَدِيرًا ﴿٤٤﴾

"Hapana kitu kinachoweza kumshinda Mwenyezi Mungu mbinguni wala katika ardhi. Hakika Yeye ni Mwenye kujua, Mwenye uwezo." (35:44).

Viumbe vya dunia hii vinamuhitaji Mwenyezi Mungu kwa ajili ya uhai wao na kuendelea daima, sana kama vinavyohitaji uanzilizwaji wao. Ujumla wa maumbile yote lazima upokee haki ya kuweza kuendelea kuwepo upya kila dakika au kinyume chake ulimwengu wote ungeporomoka. Ubunifu wa nguvu zote hapa duniani unafanana na ubunifu wa Mwenyezi Mungu na ni mwendelezo wa shughuli Zake. Kiumbe ambacho katika dhati yake kinategemea utashi wa ki-Mungu hakina uamuzi huru juu yake chenyewe.

Kama vile ambavyo taa ya umeme zinavyopata mwanga wao kutoka kwenye kituo cha umeme ambacho huwashwa kwanza, hivyo, pia lazima ziendelee kupokea nishati kutoka chanzo kile kile ili ziweze kuendelea kuwaka.

Qur'ani Tukufu inatangaza kwa kuisisitiza wazi wazi:

يَا أَيُّهَا النَّاسُ أَنتُمُ الْفُقَرَاءُ إِلَى اللَّـهِ وَاللَّـهُ هُوَ الْغَنِيُّ الْحَمِيدُ ﴿١٥﴾

"Enyi watu! Ninyi ndio wenye haja kwa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kujitosha, Msifiwa." (35:15).

Asili zote zinatokana na ridhaa Yake na zinamtegemea Yeye; matukio yote wakati wote yanaendelezwa Naye. Utaratibu wenye nguvu na mzuri kabisa wa ulimwengu umeelekezwa kwenye nguzo moja peke yake na huzunguka kwenye mhimili moja pekee. Imam Jafar as-Sadiq(a.s) alisema:"Uwezo na nguvu za Mwenyezi Mungu ni vitu vya juu sana kwa jambo lolote kutokea hapa duniani ambalo ni kinyume na ridhaa Yake." [43]

Kama Mwenyezi Mungu asingetupatia kanuni ya utashi huru na kama kila sekunde Asingetupatia uhai, rasilimali na nishati, kamwe tusingeweza kufanya lolote. Kwani ni kwa sababu ya ridhaa Yake isiyobadilika ambayo imeamua kwamba tufanye matendo ya hiari kwa mujibu wa huru, na hapo kutimiza wajibu ambao Ametupangia. Yeye Ameridhia kwamba mwanadamu lazima ajenge maisha yake ya baadae mwenyewe, mazuri au mabaya, yang'aayo au ya giza, kwa mujibu wa utambuzi na matakwa yake mwenyewe.

Matendo yetu ya hiari halafu yanahusishwa na sisi wenyewe na Mwenyezi Mungu. Tunaweza kutumia rasilimali ambazo Mwenyezi Mungu ametumilikisha kwa utambuzi kamili ama kwa kujiinua na kujiendeleza wenyewe kwa mujibu wa uchaguzi sahihi, au kujitumbukiza kwenye uovu, dhambi na mambo yaliyokithiri. Kama mambo yalivyo, ukweli unabaki pale pale kwamba upeo wa matendo yetu ya hiari umo nsdani ya mfumo uliokadiriwa; uwezo unatoka kwa Mwenyezi Mungu, na matumizi yake,

Chukulia kwamba mtu fulani ana moyo wa bandia, unaoendeshwa kwa nguvu ya betri ambayo tunaweza kuwasha na kuzima kutoka kwenye chumba cha udhibiti; wakati wowote tunapotaka, tunaweza kuzima swichi na kuusimamisha moyo kufanya kazi. Kile kilichopo ndani ya uwezo wetu ni mkondo wa umeme unaotoka kwenye betri kwenda kwenye moyo; tunaweza kuusimamisha wakati wowote. Lakini maadamu tunairuhusu betri kufanya kazi, huyo mtu ambaye moyo umepandikizwa ndani yake, ataendelea kuwa huru kufanya anavyotaka. Endapo atafanya tendo jema au ovu, bila shaka, itakuwa kwa mujibu wa hiari yake. Namna anavyotumia uwezo ambao tumempa hasa inategemea juu yake na sisi hatuhusiki kabisa.

Hali kadhalika, uwezo wetu unatoka kwa Mwenyezi Mungu na anaweza akatunyang'anya wakati wowote, lakini Ameweka namna amamo ambamo tunautumia uwezo huo hasa, kwa uchaguzi wetu wa moja kwa moja. Madhehebu ya Median. Viumbe vyote duniani vinakuwa na aina ya mwongozo maalum kwa hatua ya maendeleo ambayo vimefikia; aina zao mahsusi za mwongozo huendana na viwango tofauti vya maisha.

Inawezekana sisi kufafanua na kutambua nafasi yetu miongoni mwa viumbe tofauti katika ulimwengu huu. Tunajua kwamba mimea ni mateka mikononi mwa majaaliwa ya nguvu maumbile, wakati huo huo, ikionyesha matokeo fulani madogo ya kimaendeleo kuhusiana na mabadiliko katika mazingira yao.

Tunapo chambua tabia za wanyama, tunahisi kwamba wanazo sifa tofauti kabisa na zile za mimea. Ili waweze kupata lishe zao, wanyama wanapaswa kujiingiza kwenye eneo pana la mishughuliko, kwa kuwa maumbile hayawaaliki kwenye chakula ambapo mahitaji yao ya kilishe yamewekwa mbele yao. Wanyama wanahitaji nyenzo na vifaa fulani katika jitihada zao za kupata chakula, na vitu hivi maumbile yamekwishawapatia Ingawa wanyama wako chini ya mvuto wa nguvu wa silika, na kwa maana hii ni viumbe vinavyotiishwa, wanapata kiwango fulani cha uhuru kwa namna ambazo wanaweza kujinasua, kwa kiasi fulani, kutoka kwenye kifungo kikali cha maumbile.

Wanasayansi wanayo maoni kwamba wanyama ambao ni wanyonge zaidi, wana uhusiano na maumbile yao na viungo vyao vya asili, jinsi wanavyokuwa na nguvu zaidi kufuatana na silika zao na jinsi wanapata msaada wa moja kwa moja ulinzi zaidi wa maumbile. Kinyume chake, jinsi walivyoandaliwa kwa unafuu zaidi kuhusiana na uwezo wa kihisia na utambuzi na jinsi kiwango chao cha kujitegemea kinavyozidi kuwa kikubwa, ndivyo ambavyo wanaongozwa na silika kwa kiasi kidogo. Wakati wa kipindi cha mwanzo cha maisha yake, mtoto anafunikwa moja kwa moja na ulinzi mkubwa wa baba na mama yake; jinsi anavyoendelea kukua, hujitoa taratibu kwenye uangalizi wao wa pamoja.

Mwanadamu ambaye amepata kiwango cha juu zaidi cha maendeleo kama kiumbe pekee mwenye uwezo wa utashi huru ya kujitegemea na upambanuzi anacho kiwango cha chini kiasi cha uwezo wa kisilika. Jinsi anavyopata uhuru wake polepole, ndivyo anavyoendelea kushambuliwa na udhaifu kiasi katika uwezo wake wa fahamu.

Maumbile hutosheleza kwa namna mbali mbali mahitaji yote tofauti ya mimea. Kwenye ufalme wa wanyama, ingawa mama analazimika kufanya jitihada fulani kumbeba, kumlea na kumlinda mtoto wake, silika hutokeza mapema kwa mtoto na mama hahitaji kujihusisha na kumzoesha na kumfundisha silika hizo. Lakini kwa upande wa binadamu, tunaona kwamba hana silika za asili zenye nguvu, na uwezo wake wa kukataa mambo yasiyofaa na ya kuchukiza ya kimazingira ni dhaifu sana kuliko ule wa wanya- ma. Hivyo utegemezi wake kwa wazazi wake unaendelea kwa miaka mingi hadi hatimaye anapopata kujitegemea na kujitosheleza na akaweza kusimama kwa miguu yake mwenyewe.

Qur'ani Tukufu inasema wazi wazi kuhusu unyonge na udhaifu wa mwanadamu:

يُرِيدُ اللَّـهُ أَن يُخَفِّفَ عَنكُمْ وَخُلِقَ الْإِنسَانُ ضَعِيفًا ﴿٢٨﴾

"Mwenyezi Mungu anataka kukupunguzieni taabu, na mwanadamu ameumbwa dhaifu." (4:28).

Maumbile yamemwachia mwanadamu kwenye mbinu zake zaidi sana kuliko wanyama. Kwa mwanadamu tunaona, kwa upande moja, kujifunua kwa uhuru na kujitokeza kwa uwezo wa kukua na kupata utambuzi, na kwa upande mwingine, ongezeko utegemezi na uhitaji. Wakati mwanadamu anapokuwa na uhuru kiasi fulani, huendelea kuvutwa kwa nguvu sana kuingizwa ndani na ndani zaidi kwenye utumwa wa kuhitaji.

Hali hizi zinazotofautiana ya mipango tofauti ya maumbile, kwa mtazamo wa mabingwa fulani huunda vipengele ambavyo vinavyochochea ukuaji na maendeleo. Jinsi kiumbe anavyosonga mbele kwenye ngazi ya maendeleo, ndivyo kinavyokaribia kwenye uhuru. Kwa usahihi, ni kuhitaji na kukosa uwiano wa kihulka ndiko ambako huwezesha kukua na maendeleo kufanyika.

Kuhusu hiari na fursa ya kujieleza wao wenyewe, kipengele kinachopinga silika ya asili lazima kiwepo. Halafu, mwanadamu atanasa kati ya mivuto miwili inayopingana, kila mmojawapo ukitafuta kupata utii wake, hivyo kwamba analazimika kuchagua njia aitakayo, kwa hiari yake, akiwa anatambua, na kutegemea jitihada na maarifa yake. Akiwa huru kutokana na mambo yenye maamuzi na mawazo ya kabla ya kiakili, huanza kazi ya kujitengeneza na kujiendeleza mwenyewe katika misingi ya kanuni maalum na mifano.

Pindi anapokabiliwa na dalili hii ya hitilafu, mwanadamu hawezi kupata msimamo au kujichagulia njia yake sahihi kwa kujifanya kama mtambo unaojiendesha wenyewe au kuacha jitihada zote. Akibeba kama anavyofanya kwa mzigo wa dhamana ya ki-Mungu; ile zawadi kubwa ya ki- Mungu ambayo mbingu na ardhi havikustahili kupokea, mwanadamu pekee akithibitisha kustahili kuipokea, basi mwanadamu anakabiliwa na fursa mbili tu katika mgongano wake na harakati zake. Ama anakuwa mfungwa wa udikteta wa silika na matamanio yasiyodhibitika, hivyo kujijishusha hadhi na kujivunjia heshima, au kutoka kwenye uwezo wake mkubwa wa hiari, fikra na uamuzi, anaingia kwenye njia ya ukuaji na maendeleo na kuanza kupanda.

Wakati wowote kiumbe anapoachwa huru kutokana na utii wa kushurutishwa kwenye silika, hutupa minyororo ya utumwa, na kiumbe kutumia uwezo wa hulka na ule wa kutafuta; uelekevu wake wa fahamu unadhoofishwa na uwezo wake wa kiasili hupungua. Sababu ya hili ni kwamba kiungo chochote au uwezo ukiachwa umetulia na bila kutumika ndani ya kiumbe hai huwa kinadhoofika polepole. Kinyume chake jinsi kiungo au uwezo kitakavyotumika sana ndivyo kitakavyoendelea kukua na kujazwa nguvu.

Hivyo, pale mwanga wa utambuzi wa mwanadamu na hiari ya ubunifu, vinapotiwa msukumo na uwezo wa upambanuzi na akili, huangaza njia yake na kuamua matendo yake, uwezo wake wa utambuzi na fikra humwezesha kugundua ukweli na uhalisia mpya. Zaidi ya hayo, hali ya kutatizwa kwa binadamu na kusita kati kati ya nguzo mbili zinazopingana humwelekeza kutafakari na kuchambua, hivyo kwamba kwa kutumia busara anaweza kutofautisha kati ya njia iliyonyooka na njia potofu. Hii itamaamsha uwezo wake wa kiakili, itaimarisha uwezo wake wa tafakari, na kumpatia kiwango kikubwa zaidi cha nyendo na nguvu tele.

Umilikaji - tamaa ya uhuru, sayansi na ustaarabu - yote haya ni matokeo ya moja kwa moja ya mazoezi ya binadamu ya hiari yake. Pindi mtu anapopata uhuru na akaendeleza jitihada zake muhimu na za uhakika, anaweza kuendelea haraka katika hatua ya ukuaji na udhihirikaji wa vipengele vyote vya hulka yake, na tabia muhimu. Vipaji vyake na uwezo wake vitakapokomaa, atabadilishwa na kuwa chanzo cha manufaa na maadili katika jamii.

Tunaona matokeo ya hiari kila mahali, na mapambano yanayoendeshwa dhidi ya watetezi wake kutoka kwa wale ambao wanapinga jambo hili kwenyewe ni dalili ya wazi kwamba hawa wa mwisho, bila kutajwa bayana, wanalikubali hili.

Sasa, hebu tuone ni mipaka gani imewekwa kwenye uwezo wa kuchagua wa binadamu na ni uwezo gani anakuwa nao katika kutumia uelekevu huu. Fikra thabiti ya Shia, ambayo imechukuliwa kutoka kwenye Qur'ani na maneno ya Maimamu, inawakilisha madhehebu ya tatu, yaliyopo katikati ya wanaoitakidi majaaliwa na watetezi wa hiari kamilifu. Madhehebu haya hayasumbuliwi na upungufu na udhaifu wa madhehebu ya kuamini majaaliwa, ambayo inapingana na akili, dhamira na mifano yote ya kimaadili na kijamii na hukanusha uadilifu wa Mwenyezi Mungu kwa kumhusisha Yeye na uovu na udhalimu wote unaotokea, wala kwa kushikilia msimamo wa hiari dhahiri sio kwamba kunakanusha upekee wa uwezo wa Mwenyezi Mungu na kukataa upweke wa matendo ya Mwenyezi Mungu.

Ni dhahiri kwamba matendo yetu ya hiari hutofautiana na mienendo ya jua, mwezi na dunia, au nyendo wa mimea na wanyama. Uwezo wa hiari hutokea ndani mwetu na hutuwezesha kufanya au kutokufanya matendo fulani, hivyo kutupatia sisi uhuru wa kuchagua. Uwezo wetu wa kuchagua kwa hiari ama kufanya matendo mema au maovu hutokea kwenye uwezo wa kupambanua unaotumika kwa uhuru kamili. Lazima tutumie kipaji chetu cha uhuru wa kuchagua kwa makini sana; kwanza lazima tutafakari kiutu uzima na kwa uangalifu, tupime vitu kwa usahihi na halafu tufanye uchaguzi uliokusudiwa. Ni ridhaa ya Mwenyezi Mungu kwamba tutumie hiari yetu kwa njia hii katika dunia hii ambayo Ameiumba, kwa utambuzi na tahadhari.

Chochote tunachofanya ni wazi kwamba kimo kwenye upeo wa kitangulizi cha ujuzi na utashi wa Mwenyezi Mungu. Vipengele vyote vya maisha, vyote vinavyogusa hatima ya binadamu, kimewekewa mipaka na, pia na kwa masharti juu ya elimu Yake; kinafafanualiwa na mipaka ambayo tayari ipo kwenye ujuzi wa Mwenyezi Mungu. Zaidi ya hayo, sisi hatuko huru hata kwa sekunde moja kutokana na kuihitaji Dhati hiyo ambayo tumeunganishwa nayo, na matumizi ya uwezo wa asili katika maisha yetu hauwezekani bila ya msaada wa Mwenyezi Mungu wenye kuendelea. Kwa uwezo Wake mkuu kabisa, wenye kupita kiasi, Yeye anatuangalia kwa karibu sana, na kwa namna ambayo ipo nje ya udhaniaji wetu, Anao utambuzi kamili na mamlaka juu ya nia zetu zote na matendo yetu. Hatimaye, hiari zetu haziwezi kuvuka mipaka ya utaratibu ulioanzishwa na Mwenyezi Mungu katika maumbile haya, na kwa hiyo, hausababishi tatizo lolote kuhusu upweke wa matendo ya Mwenyezi Mungu.

Wakati akiwa anao uwezo wa kusababisha athari katika dunia hii kwa njia ya hiari yake, binadamu, yeye mwenyewe anatawaliwa na mlolongo wa sheria za asili. Anaingia duniani bila ya uchaguzi wowote kwa upande wake, na anafumba macho yake hapa duniani bila yeye mwenyewe kutaka kufanya hivyo. Maumbile yamemfunga kwa pingu za silika na mahitaji. Hata hivyo, binadamu anakuwa na nafasi na uwezo fulani; uhuru huzaa ubunifu ndani mwake ambao unamwezesha kutiisha maumbile na kuasisi utawala juu ya mazingira yake.

Imam Jafar as-Sadiq(a.s) alisema:"Ukweli wa jambo haukai kati ya mambo haya mawili haya; wala si katika majaaliwa au hiari." [44]

Kwa hiyo hiari inakuwepo, lakini haijumuishi kila kitu, kwa sababu kuweka fani tofauti kwa ajili ya binadamu itakuwa sawa na kumpa Mwenyezi Mungu mshirika katika matendo Yake. Hiari ambayo mwanadamu anakuwanayo imeridhiwa na Muumba wa asili, na amri ya Mwenyezi Mungu hudhihirika yenyewe katika muundo wa desturi na kanuni ambazo zinamtawala binadamu na maumbile yote, uhusiano wa asili, vyanzo na vipengele.

Kwa mtazamo wa Uislamu, binadamu wala si kiumbe cha kutengenezwa tayari, kinachokusudiwa kwenye kuamuliwa na majaaliwa, wala hakutupwa kwenye mazingira ya giza na yasiyo na malengo. Binadamu ni kiumbe kinachojawa na matumaini, vipaji, ustadi, ujuzi wa kubuni na mielekeo mbali mbali, ikiambatana na aina ya mwongozo uliojengeka mwilini. Kosa ambalo limefanywa na wenye kuamini katika majaaliwa na watetezi wa hiari isio na mipaka ni kwamba wamemdhani mwanadamu kuwa na njia mbili tu mbele yake: ama matendo yake yote lazima yahusishwe moja kwa moja kwa Mwenyezi Mungu, ili kwamba halafu apoteze uhuru wote na awe amekadiriwa katika matendo yake, au tunawajibika kukubali kwamba matendo yake ya hiari yanatokana na dhati inayojitegemea na isio na mipaka, maoni ambayo yanaingiza mipaka kwenye uwezo wa

Hata hivyo, ule ukweli kwamba tunayo hiari hauathiri upeo wa uwezo wa Mwenyezi Mungu, kwa sababu Ameridhia kwamba tufanya maamuzi yetu wenyewe kwa uhuru kabisa, kwa mujibu wa kanuni na desturi ambazo ameziweka. Kutoka kwenye mtazamo moja, matendo na kazi za binadamu yanaweza kuhusishwa naye mwenyewe, na kutoka kwenye mtazamo mwingine, yanahusishwa kwa Mwenyezi Mungu. Binadamu anao uhusiano wa moja kwa moja na wa haraka na matendo yake ambapo uhusiano wa Mwenyezi Mungu na matendo hayo sio wa moja kwa moja, lakini aina zote za uhusiano ni halisi na kweli. Imma hiari ya binadamu haiwezi kujiweka kwenye kupingana na utashi wa ki-Mungu, wala utashi wa binadamu hauko kinyume na kile anachokitaka Mwenyezi Mungu.

Watu wakaidi waioazimia kutokuamini, ambao wanapinga aina zote za mawaidha na maonyo, mwanzoni kabisa, wanachukua msimamo wao wa kimakosa kupitia matumizi ya hiari, halafu wanayaelewa matokeo ya ukaidi na upotofu wao wa moyo, kama adhabu, waliyoadhibiwa na Mwenyezi Mungu.

Kwa kutii matamanio ya nafsi zao duni, watu hawa madhalimu wanazuia nyoyo zao, macho yao na masikio yao kutokufanya kazi, na kama matokeo, huvuna hali ya kuteseka milele. Qur'ani inasema:

إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا سَوَاءٌ عَلَيْهِمْ أَأَنذَرْتَهُمْ أَمْ لَمْ تُنذِرْهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ ﴿٦﴾ خَتَمَ اللَّـهُ عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ وَعَلَىٰ سَمْعِهِمْ وَعَلَىٰ أَبْصَارِهِمْ غِشَاوَةٌ وَلَهُمْ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿٧﴾

"Hakika wale waliokufuru ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye, hawataamini. Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao, na juu ya macho yao pana kifuniko. Basi watapata adhabu kubwa." (2:6-7).

Wakati mwingine uovu na dhambi sio vya ukubwa kiasi kwamba vinafunga njia ya kurejea kwa Mwenyezi Mungu na ukweli. Lakini katika nyakati zingine yanaweza kufika kiwango kwamba kurudi kwenye utambulisho wa kweli wa kibinadamu inakuwa haiwezekani; halafu muhuri wa ukaidi unapigwa kwenye nafsi za wasioamini zilizochafuliwa. Haya ni matokeo ya kawaida kabisa ya tabia yao, yaliyoamuliwa na utashi na matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Kuwajibika kwa watu kama hao huazia matumizi ya hiari zao, na ukweli kwamba hawakupata baraka za mwongozo, haupunguzi kuwajibika kwao. Ipo kanuni imara na inayojidhihirisha yenyewe inayosema kuwa "chochote kinachoanzia kwenye hiari na kuishia kwenye lazima hakipingani na hiari." Imamu anasimuliwa kuwa amesema:"Mwenyezi Mungu alitaka kwamba mambo yatokee kupitia vyanzo na njia za msaada, na hakuamuru chochote isipokuwa kwa msaada wa chanzo; kwa hiyo, akaumba chanzo cha vitu vyote." [45]

Mojawapo ya vyanzo kilichotumiwa na Mwenyezi Mungu katika uumbaji Wake ni binadamu na utashi wake, kwa kuendana na kanuni kwamba vyanzo na njia maalum vimeanzishwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kutokea kila tukio hapa ulimwenguni: kutokea kwa tukio hulazimisha kuwepo kabla kwa vyanzo na njia husika, na kama isingekuwa kwa ajili ya hivyo, matukio hayo yasingetokea.

Hii ni kanuni ya jumla ambayo bila kipingamizi inatawala matendo yetu ya hiari vilevile. Fursa ya uchaguzi wetu na hiari vinakuja kufanya kiungo cha mwisho katika mnyororo wa vyanzo na njia ambavyo huishia utendaji wa kitendo kwa upande wetu.

Aya za Qur'ani ambazo zinahusisha vitu vyote kwa Mwenyezi Mungu na kuonyesha kama vinatokana Naye vinahusika na kutangaza utashi wa tangu kabla wa Mwumbaji kuwa ndio msanifu wa ulimwengu na kuelezea jinsi uwezo Wake unavyojumuisha na kupenya ndani ya mtiririko mzima wa uhai. Uwezo wake unaenea katika kila sehemu ya ulimwengu, bila kubakisha kitu, lakini nguvu za Mwenyezi Mungu zisizopingwa hazipunguzi utashi wa mwanadamu. Kwani ni Yeye ambaye anaifanya hiari hiyo kuwa sehemu ya mwanadamu, na ni Yeye anayeiweka juu ya mwanadamu huyo. Amemfanya binadamu kuwa huru kufuata njia anayochagua mwenyewe na hamuwajibishi mtu au watu kwa sababu ya dosari za mwingine.

Kama kuna lazima yoyote katika mambo ya binadamu, ni katika maana tu kwamba analazimika kuwa na hiari, kama matokeo ya utashi wa Mwenyezi Mungu, si kwa maana kwamba anahukumiwa kutenda kwa namna iliyoelekezwa. Kwa hiyo tunapofanya matendo mema bora zaidi, uwezo wa kuyatenda hayo unatoka kwa Mwenyezi Mungu, na fursa ya kutumia uwezo huo inatoka kwetu.

Aya nyingine za Qur'ani zinasisitiza kwa wazi kuhusu nafasi ya utashi wa binadamu na matendo, kwa dhahiri zikikataa kabisa maoni ya wenye kuamini majaaliwa. Inapotaka kuelekeza uzingativu wa binadamu kwa majanga na mateso anayoyavumilia katika dunia hii, huyaelezea kama ni matokeo ya matendo yake maovu. Kwenye Aya zote zinazohusu utashi wa Mwenyezi Mungu, hakuna hata moja inayoweza kupatikana kuhusisha matendo ya hiari ya binadamu kwenye utashi wa Mwenyezi Mungu. Hivyo Qur'ani inatangaza:

فَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَهُ ﴿٧﴾ وَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ شَرًّا يَرَهُ ﴿٨﴾

"Basi anayetenda lau chembe ndogo ya wema, ataiona! Na anayetenda chembe ya uovu atauona." (99 :7-8)

وَلَتُسْأَلُنَّ عَمَّا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٩٣﴾

" Na hakika mtaulizwa kwa yale mliyokuwa mkiyafanya." (16: 93).

سَيَقُولُ الَّذِينَ أَشْرَكُوا لَوْ شَاءَ اللَّـهُ مَا أَشْرَكْنَا وَلَا آبَاؤُنَا وَلَا حَرَّمْنَا مِن شَيْءٍ كَذَٰلِكَ كَذَّبَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ حَتَّىٰ ذَاقُوا بَأْسَنَا قُلْ هَلْ عِندَكُم مِّنْ عِلْمٍ فَتُخْرِجُوهُ لَنَا إِن تَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ وَإِنْ أَنتُمْ إِلَّا تَخْرُصُونَ ﴿١٤٨﴾

"Watasema wale walioshirikisha: Lau kuwa Mwenyezi Mungu angetaka tusingelishiriki sisi, wala baba zetu; wala tusingaliharamisha kitu chochote. Vivi hivi walikanusha waliokuwa kabla yao mpaka walipoonja adhabu yetu. Sema: Je, nyinyi mnayo ilimu mtutolee? Nyinyi hamfuati ila dhana. Wala hamsemi ila uwongo tu. (6:148).

Kama wokovu na upotofu wa binadamu ungekuwa utegemee ya utashi wa Mwenyezi Mungu, kusingekuwepo na dalili ya upotofu na udhalimu hapa duniani, wote wangefuata njia ya wokovu na haki, iwe wametaka au la. Wahalifu fulani wanaojitafutia visingizio vyao wamedai kwamba matendo yoyote ya dhambi watakayoyafanya yanaridhiwa na kupendelewa na Mwenyezi Mungu. Hivyo Qur'ani inasema:

وَإِذَا فَعَلُوا فَاحِشَةً قَالُوا وَجَدْنَا عَلَيْهَا آبَاءَنَا وَاللَّـهُ أَمَرَنَا بِهَا قُلْ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَأْمُرُ بِالْفَحْشَاءِ أَتَقُولُونَ عَلَى اللَّـهِ مَا لَا تَعْلَمُونَ ﴿٢٨﴾

"Na wanapofanya mambo machafu husema: Tumewakuta nayo baba zetu, na Mwenyezi Mungu ametuamrisha hayo, Sema: Hakika Mwenyezi haamrishi mambo machafu. Mnamzulia Mwenyezi Mungu msiyoyajua?" (7:28).

Kwa namna ile ambayo Mwenyezi Mungu ameridhia thawabu kwa matendo mema, ndivyo, pia ambavyo Ameridhia adhabu dhidi ya dhambi na uovu, lakini katika mifano yote miwili, kuridhia matokeo ni tofauti na kuridhia kitendo kinachosababisha matokeo. Uhai wa binadamu na athari za kawaida za matendo yake ni kweli yanategemea ridhaa ya Mwenyezi Mungu, lakini matendo yake ya hiari hutegemea utashi wake mwenyewe.

Mtazamo wa Uislamu, kama unavyotambuliwa na Shia, ni kwamba mwanadamu hana hiari kamili kiasi hicho, hivyo kwamba anaweza kufanya matendo nje ya mfumo wa ridhaa ya Mwenyezi Mungu na utashi Wake, ambao unachukua ulimwengu wote katika miundo ya sheria na kanuni za kudumu, hivyo kumshusha Mwenyezi Mungu kuwa kitu dhaifu na kinyonge anapokabiliwa na utashi wa viumbe Vyake mwenyewe. Wakati huo huo, binadamu pia sio mfungwa wa utaratibu ambao unamzuia kuchagua njia yake mwenyewe katika maisha na kumlazimisha, kama wanyama, kuwa mtumwa wa silika zake.

Qur'ani Tukufu inasema wazi kwenye Aya zake kwamba Mwenyezi Mungu amemuonyesha binadamu njia ya wongovu, bali analazimika imma kukubali mwongozo na ukombozi ama kuangukia kwenye upotofu na uovu:

إِنَّا هَدَيْنَاهُ السَّبِيلَ إِمَّا شَاكِرًا وَإِمَّا كَفُورًا ﴿٣﴾

"Hakika sisi tumembainishia njia. Ama ni mwenye kushukuru, au ni mwenye kukufuru."(76:3).

Kwa hiyo, kuvihusisha vitendo vya hiari vya binadamu kwa Mwenyezi Mungu, kunakataliwa na Qur'ani Tukufu.