TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS 0%

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS Mwandishi:
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

Mwandishi: Radio ya Kiswahili Tehran Iran
Kundi:

Matembeleo: 11872
Pakua: 1924

Maelezo zaidi:

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 10 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 11872 / Pakua: 1924
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

Mwandishi:
Swahili

4

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

SURAT YUNUS 50-56

Bismillahir Rahmanir Rahim. Assalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

Karibuni katika mfululizo huu wa 316 wa darsa la quran, tukiwa tunaendelea kuizungumzia sura ya 10 ya Yunus.

AYA ZA 50 NA 51

Tunaianza darsa yetu kwa aya za 50 na 51 ambazo zinasema:

قُلْ أَرَأَيْتُمْ إِنْ أَتَاكُمْ عَذَابُهُ بَيَاتًا أَوْ نَهَارًا مَّاذَا يَسْتَعْجِلُ مِنْهُ الْمُجْرِمُونَ ﴿٥٠﴾

50. Sema: Mwaonaje ikikufikieni hiyo adhabu yake usiku au mchana, basi kwa nini wenye makosa wanaitake ije haraka?

أَثُمَّ إِذَا مَا وَقَعَ آمَنتُم بِهِ آلْآنَ وَقَدْ كُنتُم بِهِ تَسْتَعْجِلُونَ ﴿٥١﴾

51. Tena Je! Ikishatokea mtaiamini? Ndio sasa tena? Na nyinyi mlikuwa mkiihimiza.

Aya hizi zinatoa jibu kwa wale wanaokanusha kufufuliwa kwa viumbe ambao walikuwa wakisema, hiyo adhabu ya Mwenyezi Mungu itatokea lini? Ndipo Bwana Mtume akatakiwa awajibu kuwa hivi nyinyi mnaoharakisha mteremshiwe adhabu, kama adhabu hiyo itakushukieni ghafla iwe ni mchana au pengine usiku mkiwa mmelala, mtafanya nini wakati huo? Je mtaweza kupata pa kukimbilia au kuwa na nguvu za kuizuia isikupateni? Kama mnadhani pia kwamba ikiwa mtaiamini haki pale mtakapoanza kuona ishara za kuteremka adhabu na kuwa imani yenu hiyo itaweza kukufaeni, basi dhana yenu hiyo ni batili, kwani pale itakaposhuka adhabu milango ya toba itafungwa na hivyo imani katika lahadha hiyo haitokuwa na taathira yoyote.

Miongoni mwa mafunzo tunayopata kutokana na aya hizi ni kuwa kuamini mtu wakati hatari iko mbele ya macho yake hakuna thamani yoyote, kwani imani ya aina hiyo si ya hiyari wala ya kuitakidiwa moyoni, bali ni imani inayotokana na khofu ya lisilo budi.

AYA YA 52

Ifuatayo sasa ni aya ya 52 ambayo inasema:

ثُمَّ قِيلَ لِلَّذِينَ ظَلَمُوا ذُوقُوا عَذَابَ الْخُلْدِ هَلْ تُجْزَوْنَ إِلَّا بِمَا كُنتُمْ تَكْسِبُونَ ﴿٥٢﴾

52. Kisha waliodhulumu wataambiwa: Onjeni adhabu ya kudumu. Kwani mtalipwa isipokuwa yale mliyokuwa mkiyachuma?

Katika aya zilizotangulia lilizungumziwa suala la adhabu ya Mwenyezi Mungu ya hapa duniani inayowashukia kwa ghafla waovu na waliomkufuru Mola Aliyetukuka.

Aya hii ya 52 inaashiria adhabu ya milele itakayowapata waovu hao siku ya Kiyama kwa sababu ya dhulma waliojitendea wao wenyewe na kuwatendea wanadamu wenzao.

Baadhi ya mafunzo tunayoyapata kutokana na aya hii ni kuwa katika mafundisho ya Uislamu mpaka wa dhulma hauishii katika kutenda dhulma kwa wengine tu, lakini hata madhambi anayoyafanya yeye mwenyewe mtu yanahesabika pia kuwa ni dhulma, kwani ufanyaji dhambi huo ni sawa na mtu kujidhulumu nafsi yake na pia kuwafanyia dhulma Mitume wa Allah ambao walitaabika na kupata mashaka mengi kwa ajili ya kuhakikisha uongofu utokao kwa Allah unawafikia waja wake.

Aidha aya inatuelimisha kuwa adhabu ya Mwenyezi Mungu itakuwa ya kiadilifu kulingana na amali zake mwenyewe mja, bila kuzidishiwa kitu.

AYA ZA 53 NA 54

Tunaiendeleza darsa yetu kwa aya za 53 na 54 ambazo zinasema:

وَيَسْتَنبِئُونَكَ أَحَقٌّ هُوَ قُلْ إِي وَرَبِّي إِنَّهُ لَحَقٌّ وَمَا أَنتُم بِمُعْجِزِينَ ﴿٥٣﴾

53. Na wanakuuliza: Je! ni kweli hayo? Sema: Ehe! Naapa kwa Mola wangu! Hakika hayo ni kweli nanyi hamuwezi kumshinda (Mwenyezi Mungu).

وَلَوْ أَنَّ لِكُلِّ نَفْسٍ ظَلَمَتْ مَا فِي الْأَرْضِ لَافْتَدَتْ بِهِ وَأَسَرُّوا النَّدَامَةَ لَمَّا رَأَوُا الْعَذَابَ وَقُضِيَ بَيْنَهُم بِالْقِسْطِ وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿٥٤﴾

54. Na lau kuwa kila nafsi iliyodhulumu inamiliki kila kilichomo duniani, bila shaka ingelitoa vyote kujikombolea. Na watakapoiona adhabu watajitahidi kuficha majuto yao. Na patahukumiwa baina yao kwa uadilifu nao hawatodhulumiwa.

Baada ya aya zilizotangulia kuelezea juu ya ushukaji wa adhabu ya Allah kwa waovu hapa duniani na ile itakayowapata huko akhera, aya hizi zinasema musiwe na shaka yoyote juu ya kushuka kwa adhabu ya Mwenyezi Mungu, kwani ahadi ya Mola itathibiti tu. Pamoja na kwamba yote aliyokuwa akiyatamka Bwana Mtume Muhammad(s.a.w.w) yalikuwa ni hakika na kweli tupu, lakini kutokana na uzito wa suala la kufufuliwa viumbe, hapa anaapa kwa jina la Mola Mwenyezi kuthibitisha kwamba kujiri kwa siku hiyo ya Kiyama hakuna chembe ya shaka, na wala hakuna atakayeweza kuikwepa siku hiyo au kuweza kukabiliana na adhabu yake.

Kwa hakika adhabu ya Mwenyezi Mungu siku ya Kiyama itakuwa kali na nzito kiasi kwamba, kila muovu atakuwa tayari kutoa mali na utajiri wote uliopo duniani ili aweze kuokoka na adhabu hiyo.

Lakini hiyo itabaki kuwa ni ya laiti ambayo haileti, kwa sababu kujuta wakati huo kwa yale aliyoyatanguliza mtu hakutosaidia kitu kwani mahakama ya Mwenyezi Mungu itatoa na kutekeleza hukumu kwa waja wote kwa msingi wa uadilifu.

Funzo mojawapo tunalolipata kutokana na aya hizi ni kuwa katika mahakama ya Mwenyezi Mungu si utajiri wala nguvu na uwezo wa kidunia vitakavyoweza kumsaidia mtu. Ni imani safi na sahihi, na amali njema zilizofanywa kwa ikhlasi, ndivyo vitakamvyomfaa mja siku hiyo.

AYA ZA 55 NA 56

Darsa hii ya 316 nahitimishwa na aya za 55 na 56 ambazo zinasema:

أَلَا إِنَّ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَلَا إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٥﴾

55. Jueni kuwa hakika vyote vilivyomo katika mbingu na katika ardhi ni vya Mwenyezi Mungu. Jueni kuwa hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki. Lakini wengi wao hawajui.

هُوَ يُحْيِي وَيُمِيتُ وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿٥٦﴾

56. Yeye ndiye anayefufua na anayefisha. Na kwake mtarejeshwa.

Sababu kuu inayowafanya wanaokufuru na kukanusha juu ya kuwepo kwa siku ya Kiyama ni shaka yao juu ya uwezo wa Allah s.w.t Hivyo aya tulizosoma zinasema kuwa ni nini ikakupitikieni kwamba Mwenyezi Mungu hana uwezo wa kuwafufua waliokufa na kuwalipa kwa waliyotenda? Kwani hamujui nyinyi kuwa kila kitu ni milki yake yeye, na yeye ndiye Muumba na Mmiliki wa ulimwengu, na kwamba uhai wenu na mauti yenu viko mikononi mwake yeye? Kama mnayakubali hayo, yawaje basi mnakuwa na shaka juu ya kiyama?

Aya hizi wapenzi wasomaji zinatuelimisha kuwa mmiliki halisi wa kila kitu ni Mwenyezi Mungu s.w.t, na umiliki wa wanaadamu kwa kitu chochote kile ni wa kupanga tu. Na ndiyo maana siku ya kiyama wale waliokufuru hawatokuwa na chochote cha kuweza kutoa kama fidia ili waweze kuokoka.

Aidha aya zinatuonyesha kuwa uwezo wa Allah wa kutawala kila kitu ni ithbati tosha ya uwezo wake wa kutekeleza kila anachoahidi. Kwa haya machache tunaifunga darsa yetu hii huku tunamwomba Mola atujaalie kuwa miongoni mwa wale watakaopata radhi zake na pepo ya milele, na atulinde na ghadhabu zake na adhabu ya moto, amin

Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

SURAT YUNUS 57-61

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kutuwafikisha kukutana tena katika darsa yetu hii.

AYA ZA 57 NA 58

Sura ya 10 ya Yunus ndiyo tunayoizungumzia kwa sasa, na hii ni darsa ya 317 tunayoianza kwa aya za 57 na 58 ambazo zinasema:

يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءَتْكُم مَّوْعِظَةٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَشِفَاءٌ لِّمَا فِي الصُّدُورِ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّلْمُؤْمِنِينَ ﴿٥٧﴾

57. Enyi watu Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uwongofu, na rehema kwa waumini.

قُلْ بِفَضْلِ اللَّـهِ وَبِرَحْمَتِهِ فَبِذَٰلِكَ فَلْيَفْرَحُوا هُوَ خَيْرٌ مِّمَّا يَجْمَعُونَ ﴿٥٨﴾

Sema: Kwa fadhila ya Mwenyezi Mungu na rehma yake! Basi nawafurahi kwa hayo. Haya ni bora kuliko hayo wanayoyakusanya.

Roho ya mwanadamu wapenzi wasomaji kama ulivyo mwili wake huzongwa na mashaka na magonjwa mbali mbali ya kinafsi na hivyo nayo pia huhitajia dawa. Maradhi ya kiroho kama vile kiburi, ghururi, ubakhili, uhasidi na riya, kama hayatopatiwa dawa huweza kumfanya mtu aishie kwenye ukafiri na unafiki na kumtoa kwenye njia ya uongofu.

Na kwa hivyo quran kutokana na mawaidha na maonyo yake ya mara kwa mara huweza kumkinga mtu na kumwezesha kuepuka madhambi mbali mbali. Kwa upande mwingine kwa kubainisha adhabu iliyoandaliwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya waovu, kitabu hicho cha mbinguni humzindua na kumtanabahisha mwanadamu na matendo yake maovu ili achukue hatua ya kuisafisha na kuitakasa roho yake. Ni wazi kwamba nafsi zilizo safi ndizo zinazoweza kupata taufiki ya kuufikia uongofu wa Allah (s.w.t).

Hivyo Mola Mwenyezi anamtaka Mtume wake awaeleze waumini kwamba rasilimali bora kabisa kwao ni hiyo imani yao kwa kitabu cha Allah na kushikamana kwao na kitabu hicho, na kwa kweli wana kila sababu ya kufurahia kupata neema hiyo kubwa na si kupaparikia vyeo na utajiri wa kidunia.

Baadhi ya mafunzo tunayopata kutokana na aya hizi ni kuwa quran ndiyo ponya na dawa bora kabisa kwa nyoyo zenye maradhi na nafsi zilizo chafu kimaadili.

Aidha kutokana na aya hizi tunabaini kuwa quran ndiyo hazina na kito chenye thamani kubwa zaidi kuliko utajiri wa aina yoyote ile wa kidunia. Kwa hakika fukara hasa ni yule mtu aliyekosa mafundisho matukufu ya kitabu hicho, hata kama atakuwa amejikusanyia mali na kila aina ya utajiri.

Na kinyume chake tajiri na aliye mkwasi hasa ni yule anayeishi maisha ya kiquran hata kama kwa mtazamo wa kimaada na kidhahiri hatokuwa na mali wala utajiri wowote.

AYA ZA 59 NA 60

Tunaiendeleza darsa yetu kwa aya za 59 na 60 ambazo zinasema:

قُلْ أَرَأَيْتُم مَّا أَنزَلَ اللَّـهُ لَكُم مِّن رِّزْقٍ فَجَعَلْتُم مِّنْهُ حَرَامًا وَحَلَالًا قُلْ آللَّـهُ أَذِنَ لَكُمْ أَمْ عَلَى اللَّـهِ تَفْتَرُونَ ﴿٥٩﴾

59. Sema: Je! Mwaonaje zile riziki alizo kuteremshieni Mwenyezi Mungu, nanyi mkafanya katika hizo nyengine haramu na nyengine halali. Sema:Je! Mwenyezi Mungu amekuruhusuni, au mnamzulia Mwenyezi Mungu tu?.

وَمَا ظَنُّ الَّذِينَ يَفْتَرُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّ اللَّـهَ لَذُو فَضْلٍ عَلَى النَّاسِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَشْكُرُونَ ﴿٦٠﴾

60. Na nini dhana ya wanaomzulia Mwenyezi Mungu kwa Siku ya Kiyama? Hakika Mwenyezi Mungu ana fadhila juu ya watu, lakini wengi wao hawashukuru.

Aya zilizotangulia zimezungumzia rehma na uongofu wa quran. Zikiendeleza yale yaliyokuja katika aya hizo aya hizi zinasema yule ambaye amejiweka mbali na quran hutumbukia kwenye mkumbo wa kufuata mambo ya uzushi na kubuni na kanuni zisizo na mashiko, ambayo yenyewe ni chanzo cha masaibu na matatizo mbali mbali yanayowatinga watu katika maisha yao. Kama ilivyo katika aya nyingine, quran tukufu inaashiria hapa tabia waliyokuwa nayo washirikina ya kujiharamishia kula wanyama wa miguu mine na baadhi ya mazao ya kilimo na badala yake wakivichukua vitu hivyo na kuviweka nadhiri kwa ajili ya masanamu yao.

Katika aya tulizosoma quran tukufu inawaambia washirikina hao kuwa riziki yenu nyinyi inatoka kwa Mwenyezi Mungu, na hivyo ni yeye ndiye mwenye haki ya kuamua kipi kiwe halali na kipi kiwe haramu kula, na wala sio nyinyi; vinginevyo muonyeshe kama mumepata idhini kutoka kwake yeye Allah s.w.t ya kufanya hayo, hali ya kuwa nyinyi hamjapewa haki hiyo.

Hivyo basi mjiandae kwenda kujieleza siku ya Kiyama kuhusu uzushi na uwongo huo mliojitungia.

Aya zinaendelea kubainisha kuwa neema za Mwenyezi Mungu kwa waja ni kielelezo cha fadhila na ukarimu wake Mola lakini wanaadamu si washukurivu wa neema hizo ambazo huwaondokea kutokana na kuzusha kwao aina kwa aina za mambo ya upotofu na yasiyo na msingi.

Baadhi ya mambo tunayojifunza kutokana na aya hizi ni kuwa neema zote zinatoka kwa Mwenyezi Mungu na hivyo ni yeye ndiye mwenye haki ya kuhalalisha na kuharamisha vitu, na si wanadamu kutokana na utashi na matamanio yao ya kinafsi wajiamulie watakavyo kuhalalisha hiki na kuharamisha kile.

Aidha aya zinatutaka tuelewe kuwa aliye na mamlaka ya kuweka sheria kwa ajili ya wanadamu ni Allah pekee, na hivyo sheria yeyote inayotungwa na wanadamu ikakinzana na sheria yake ni bidaa na haina itibari.

AYA YA 61

Aya ya 61 ndiyo inayotuhitimishia darsa yetu hii. Aya hiyo inasema:

وَمَا تَكُونُ فِي شَأْنٍ وَمَا تَتْلُو مِنْهُ مِن قُرْآنٍ وَلَا تَعْمَلُونَ مِنْ عَمَلٍ إِلَّا كُنَّا عَلَيْكُمْ شُهُودًا إِذْ تُفِيضُونَ فِيهِ وَمَا يَعْزُبُ عَن رَّبِّكَ مِن مِّثْقَالِ ذَرَّةٍ فِي الْأَرْضِ وَلَا فِي السَّمَاءِ وَلَا أَصْغَرَ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْبَرَ إِلَّا فِي كِتَابٍ مُّبِينٍ ﴿٦١﴾

61. Na huwi katika jambo lolote, wala husomi sehemu yoyote katika Quran, wala hamtendi kitendo chochote ila Sisi huwa ni mashahidi juu yenu mnapo shughulika nayo. Na hakifichikani kwa Mola wako Mlezi chenye uzito hata wa chembe katika ardhi na katika mbingu, wala kidogo kuliko hicho wala kikubwa ila kimo katika Kitabu kilicho wazi.

Aya hii inaashiria elimu isiyo na mpaka ya Allah s.w.t iliyo na utambuzi wa hali na harakati zote za mwanadamu, na kuelewa kila tendo litendwalo, liwe kubwa au dogo, la siri na la dhahiri, linalojiri kila mahala na katika kila sekunde, iwe ni katika ulimwengu wa mbinguni au wa ardhini na kuyahifadhi yote hayo katika lauhim mahfuudh.

Kwa hakika matendo yote ya waja, mbali na kushuhudiwa moja kwa moja na yeye Mola Karima yanaandikwa na kuhifadhiwa pia na malaika wake ambao huwa pamoja na waja ili kushuhudia na kuyanakili mazuri yote na mabaya yote wanayotenda.

Baadhi ya nukta za kuzingatiwa katika aya hii ni kuwa matendo yetu yote bali hata yale yanayotupitikia akilini na katika nafsi zetu yanashuhudiwa na kujulikana na Mwenyezi Mungu sw pamoja na malaika wake. Na kwa kweli hakuna chochote kinachofichika kwao.

Wapenzi wasomaji darsa yetu ya juma hili inaishia hapa. Tunamwomba Mola atulinde na hatari ya kuhalalisha vile alivyoviharamisha yeye na kuharamisha vile vilivyohalalishwa na yeye Mola Karima. Amin.

Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

5

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

YUNUS 62-67

Bismillahir Rahmanir Rahim. Assalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kutuwafikisha kukutana tena katika darsa yetu hii.

ZA 62, 63 NA 64

Sura ya 10 ya Yunus ndiyo tunayoizungumzia kwa sasa, na hii ni darsa ya 318 tunayoianza kwa aya za 62, 63 na 64 ambazo zinasema:

أَلَا إِنَّ أَوْلِيَاءَ اللَّـهِ لَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ ﴿٦٢﴾

62. Jueni kuwa vipenzi vya Mwenyezi Mungu hawatakuwa na khofu (siku ya Kiyama) wala hawatahuzunika.

الَّذِينَ آمَنُوا وَكَانُوا يَتَّقُونَ ﴿٦٣﴾

63. Nao ni wale ambao waliamini na wakawa wanamcha Mungu.

لَهُمُ الْبُشْرَىٰ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ لَا تَبْدِيلَ لِكَلِمَاتِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿٦٤﴾

64. Wao bishara njema katika maisha ya dunia na katika Akhera. Hapana mabadiliko katika maneno ya Mwenyezi Mungu. Huko ndiko kufuzu kukubwa.

Katika darsa kadhaa zilizopita tulisoma aya zilizozungumzia hali ngumu ya adhabu watakayokabiliana nayo wale waliokufuru na kumshirikisha Allah s.w.t Aya tulizosoma hivi punde zinabainisha hali watakayokuwa nayo waumini wa kweli waliomcha Mwenyezi Mungu, ili kwa kulinganisha hali za makundi mawili hayo iweze kufahamika ni ipi njia ya saada na ipi yenye mwisho mbaya.

Utulivu wa roho na kutopatwa na ghamu wala hali yoyote ya huzuni ni miongoni mwa neema kubwa ambazo Allah atawatunuku waja wake wema. Waja ambao kutokana na kujiweka mbali na madhambi na maovu waliweza kujikurubisha kwenye chemchemu ya usafi, mema na mazuri yote yaani Allah sw na kwa taabiri ya quran tukufu kuingia kwenye kundi la mawalii yaani vipenzi vya Mwenyezi Mungu.

Ni wazi kuwa nafsi za watu kama hao siku zote humiminikiwa na rehma za bishara njema za Mola Karima na hivyo katu huwa hawapatwi na shaka, ugoigoi au hali ya ulegevu katika kutekeleza majukumu yao ya kidini.

Bwana Mtume Muhammad(s.a.w.w) amesema:"Kimya cha mawalii wa Mwenyezi Mungu ni dhikri, kutazama kwao ni ibra, maneno yao ni hikima na harakati zao katika jamii, ni sababu ya kupatikana baraka.

Naye Imam Ali(a.s) amesema:"Usije ukamdunisha mtu yoyote yule, kwani Mwenyezi Mungu ameficha mawalii wake miongoni mwa watu, hivyo si hasha yule umdunishaye akawa ni mmoja wao na wewe usijue" .

Baadhi ya mafunzo tunayopata kutokana na aya hizi ni kuwa yule ambaye moyo wake unamkhofu Mwenyezi Mungu tu hawezi kumkhofu yeyote mwengine. Aidha aya zinatuonyesha kuwa imani bila taqwa huwa haina athari; muumini wa kweli ni yule ambaye kila wakati anajichunga na kujiweka mbali na maovu na mambo machafu.

AYA ZA 65 NA 66

Zifuatazo sasa ni aya za 65 na 66 za sura yetu ya Yunus ambazo zinasema:

وَلَا يَحْزُنكَ قَوْلُهُمْ إِنَّ الْعِزَّةَ لِلَّـهِ جَمِيعًا هُوَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴿٦٥﴾

65. Wala yasikuhuzunishe maneno yao. Hakika utukufu wote ni wa Mwenyezi Mungu.Yeye ndiye asikiaye na ajuaye.

أَلَا إِنَّ لِلَّـهِ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ وَمَا يَتَّبِعُ الَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ شُرَكَاءَ إِن يَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ وَإِنْ هُمْ إِلَّا يَخْرُصُونَ ﴿٦٦﴾

66. Jueni kuwa ni vya Mwenyezi Mungu vyote vilivyomo mbinguni na ardhini. Na wala hawawafuati hao wanaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu kuwa ni washirika wake. Wao hawafuati ila dhana tu na hawasemi ila uwongo.

Mushirikina wa Makka walikuwa wakimsingizia Bwana Mtume kila sifa mbovu kama vile kusema kwamba yeye ni mshairi, kuhani na mchawi bali hata mwendawazimu na wakisema: maneno haya ayasemayo Muhammad anafundishwa na watu wengine.

Na wakati mwingine wakisema kuwa yeye ni mtu kama wao tu wala lolote la ubora zaidi yao.

Katika kuyajibu maneno hayo yasiyo na msingi ya Mushirikina Allah sw anamliwaza Mtume wake kwa kumwambia, irada ya Mola wako imeshakata na kuhukumu kuwa wewe na wafuasi wako muwe na izza na utukufu; nao hao mushirikina hawawezi kufanya lolote kukabiliana na irada hiyo.

Na sababu ni kuwa ulimwengu na kila kilichomo ndani yake viko chini ya mamlaka yake Mola wako aliyetukuka, na kwa hivyo wale wanaowaendea waola ghairi ya Mwenyezi Mungu mtukufu si wao wenyewe wala hao waungu wao bandia walio na uwezo wa kufanya lolote.

Aya hii pamoja na mambo mengine inatuelimisha kuwa mojawapo ya mbinu zinazotumiwa na maadui wa Uislamu ni kuharibu haiba na shakhsiya ya viongozi wa dini hiyo tukufu.

Na hilo halikuishia katika zama za mwanzoni mwa kudhihiri kwa Uislamu bali linaendelea kushuhudiwa hata katika zama zetu hizi. Hata hivyo Allah sw ameshaahidi kuwa maadui hao katu hawatofanikiwa kwa kupitia njia hiyo kulifikia lengo lao hilo.

AYA YA 67

Tunaihitimisha darsa yetu ya 318 kwa aya ya 67 ambayo inasema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ اللَّيْلَ لِتَسْكُنُوا فِيهِ وَالنَّهَارَ مُبْصِرًا إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يَسْمَعُونَ ﴿٦٧﴾

67. Yeye (Mwenyezi Mungu) ndiye aliyekujaalieni usiku mpate kutulia humo, na mchana wa kuonea. Hakika katika hayo zimo ishara kwa watu wanaosikia.

Aya iliyopita imeashiria utawala mutlaki wa Allah s.w.t katika ulimwengu na kila kilichomo ndani yake.

Aya tuliyosoma ya 67 inagusia tadbiri yenye hikima kubwa ya Mola na kueleza kuwa mfumo wa mabadiliko ya usiku na mchana ni mojawapo ya madhihirisho ya uwezo wa Mola Mwenyezi katika uendeshaji wa ulimwengu.

Katika aya mbali mbali za quran usiku umetajwa kuwa kitoa utulivu cha mwanadamu. Ni wazi kwamba wakati ambapo utulivu wa kiwiliwili unayumkinika kwa kulala na kupumzika, utulivu wa roho hupatikana kwa dua, minong'ono na kushtakia mja hali yake kwa Mola na Muumba wake.

Aya hii pamoja na mambo mengine inatuelimisha kuwa mfumo tuushuhudiao wa ulimwengu haukutokea kwa bahati tu bali ni kitu kilichoumbwa na kuendeshwa kwa lengo na irada maalumu.

Kwa haya machache wapenzi wasomaji tunaifunga darsa yetu ya juma hili.

Inshallah Mwenyezi Mungu atujaalie kuwa miongoni mwa waja wake washukurivu wa neema zake na wanaozingatia na kuyatafakari maumbile ya ulimwengu ili kuweza kuitambua ipasavyo adhama ya Mola wao... Amin. Wassalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

YUNUS 68-73

Assalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

Karibuni katika mfululizo huu wa 319 wa darsa ya quran, tukiwa tunaendelea kuizungumzia sura ya 10 ya Yunus.

AYA ZA 68, 69 NA 70

Tunaianza darsa yetu kwa aya za 68, 69 na 70 ambazo zinasema:

قَالُوا اتَّخَذَ اللَّـهُ وَلَدًا سُبْحَانَهُ هُوَ الْغَنِيُّ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ إِنْ عِندَكُم مِّن سُلْطَانٍ بِهَـٰذَا أَتَقُولُونَ عَلَى اللَّـهِ مَا لَا تَعْلَمُونَ ﴿٦٨﴾

68. Wamesema: Mwenyezi Mungu amejifanyia mtoto. Ameepukana na hayo. Yeye ni Mkwasi Mwenye kujitosheleza. Ni vyake vilivyomo mbinguni na vilivyomo ardhini. Nyinyi hamna uthibitisho wowote wa haya. Mnamzulia Mwenyezi Mungu msiyoyajua?

قُلْ إِنَّ الَّذِينَ يَفْتَرُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ لَا يُفْلِحُونَ ﴿٦٩﴾

69. Sema: Wale wanaomzulia Mwenyezi Mungu uwongo hawatafaulu.

مَتَاعٌ فِي الدُّنْيَا ثُمَّ إِلَيْنَا مَرْجِعُهُمْ ثُمَّ نُذِيقُهُمُ الْعَذَابَ الشَّدِيدَ بِمَا كَانُوا يَكْفُرُونَ ﴿٧٠﴾

70. Hiyo ni starehe ya katika dunia tu, kisha kwetu ndiyo marejeo yao ni kwetu. Hapo tutawaonjesha adhabu kali kwa sababu ya kukufuru kwao.

Moja kati ya itikadi porofu na ya uzushi ambayo walikuwa nayo watu wa kaumu na uma zilizopita na ambayo inashuhudiwa pia hata hii leo ni kumjaalia Mwenyezi Mungu kuwa na wana na kuwanasibisha na yeye Mola Mwenyezi. Katika historia ya Uyahudi, wafuasi wa dini hiyo walimfanya Uzair mwana wa Mungu, nao wakristo wakatenda hayo hayo kuhusiana na Nabii Issa mwana wa Maryam. Hali ya kuwa kwanza kabisa ni kwamba Mwenyezi Mungu hana mke hata awe na mtoto.

Pili : ni kuwa Allah hahitaji kuwa na mwana, na tatu ni kwamba mtu ambaye ni kiumbe aliyeumbwa kamwe hawezi kuwa mwana wa Mungu kwa sababu jinsia ya mtoto hutokana na ile ya wazazi wake wawili yaani baba na mama, hali ya kuwa kama tulivyotangulia kusema Mwenyezi Mungu aliyetukuka ametakasika na sifa ya kuwa na mke.

Kuhusiana na kauli zote hizo za batili na zisizo na mashiko quran tukufu inasema wale wanaotamka maneno hayo wajue kwamba lazima watawajibika kwayo, na siku ya kiyama watakuja kupata adhabu kali kwa sababu ya uzushi huo waliomnasbishia nao Mwenyezi Mungu (s.w.t)

Baadhi ya yale tunayojifunza kutokana na aya hizi ni kuwa Mola mtukufu hatishwi na upweke hata ahitajie mwana kwa ajili ya kuuondoa upweke huo.

Hahitajii msaada hata na awe na shida ya kuwa na msaidizi, na wala hachelei kuondoka hata iwepo haja ya mrithi wa baada yake. Subhanallah, ametakasika Mola aliyetukuka na kasoro zote hizo bali na nyinginezo.

Aidha aya zinatuonyesha kuwa lau mja angelinganisha mapungufu yaliyonayo maisha ya kupita ya dunia na hilaki ya adhabu isiyoweza kukadirika ya akhera basi angechunga na kujiweka mbali na kutamka mengi na kutenda mengi yanayomghadhibisha Mola wake.

AYA YA 71

Ifuatayo sasa ni aya ya 71 ambayo inasema:

وَاتْلُ عَلَيْهِمْ نَبَأَ نُوحٍ إِذْ قَالَ لِقَوْمِهِ يَا قَوْمِ إِن كَانَ كَبُرَ عَلَيْكُم مَّقَامِي وَتَذْكِيرِي بِآيَاتِ اللَّـهِ فَعَلَى اللَّـهِ تَوَكَّلْتُ فَأَجْمِعُوا أَمْرَكُمْ وَشُرَكَاءَكُمْ ثُمَّ لَا يَكُنْ أَمْرُكُمْ عَلَيْكُمْ غُمَّةً ثُمَّ اقْضُوا إِلَيَّ وَلَا تُنظِرُونِ ﴿٧١﴾

71. Wasomee khabari za Nuhu alipowaambia watu wake: Enyi watu wangu! Ikiwa kukaa kwangu nanyi na kukumbusha kwangu Aya za Mwenyezi Mungu kunakuchukizeni, basi mimi namtegemea Mwenyezi Mungu. Nanyi tengenezeni mambo yenu na hao washirika wenu. Tena shauri lenu hilo lisifichikane kwenu. Kisha nihukumuni.Wala msinipe muhula.

Nabii Nuh(a.s) ni mmoja wa Mitume wateule wa Allah ambaye kwa miaka mingi sana alifanya kazi ya kuwalingania watu wa kaumu yake, lakini ni wachache tu miongoni mwao waliomuamini na akthari yao waliendelea kubaki kwenye shirki na ukafiri.

Aya hizi ambazo zilishuka huko Makka zinawaliwaza waislamu ambao walikuwa katika unyonge na hali ngumu ya maisha na kuwataka wawe na imani ya kupata msaada wa Mwenyezi Mungu na kuelewa kwamba Allah s.w.t yuko pamoja na wao na hivyo wasimame imara kama alivyosimama Nabii Nuh(a.s) ambaye licha ya vitisho na kila aina ya njama za wapinzani wa haki alisimama peke yake na kubeza nguvu na vitisho vyao kwa kuwaambia jumuikeni pamoja nyote na amueni chochote mnachotaka kuamua juu yangu, lakini jueni kwamba mimi nimetawakal kwa Mwenyezi Mungu na kutegemea nguvu na uwezo wake yeye tu.

Aya hii inatuelimisha kuwa historia ya waliotutangulia inabainisha wazi kwamba haki ni yenye kubaki na mwisho wa batili ni kutoweka na kwa hakika kuelewa yaliyojiri huko nyuma kunatoa mwanga wa kuonyesha njia ya huko tunakoelekea.

AYA ZA 72 NA 73

Aya za 72 na 73 ndizo zinazotuhitimishia darsa yetu ya juma hili. Aya hizo zinasema:

فَإِن تَوَلَّيْتُمْ فَمَا سَأَلْتُكُم مِّنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ وَأُمِرْتُ أَنْ أَكُونَ مِنَ الْمُسْلِمِينَ ﴿٧٢﴾

72. Lakini mkikengeuka (khiyari yenu). Mimi sikuombeni ujira. Ujira wangu hauko ila kwa Mwenyezi Mungu. Na nimeamrishwa niwe miongoni mwa wanaojisalimisha kwake.

فَكَذَّبُوهُ فَنَجَّيْنَاهُ وَمَن مَّعَهُ فِي الْفُلْكِ وَجَعَلْنَاهُمْ خَلَائِفَ وَأَغْرَقْنَا الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الْمُنذَرِينَ ﴿٧٣﴾

73. Lakini walimkadhibisha. Basi tukamuokoa pamoja na waliokuwa naye katika jahazi. Na tukawafanya wao ndio waliobakia. Na tukawazamisha wale waliozikadhibisha Aya zetu. Basi angalia vipi ulikuwa mwisho wa wale walioonywa (wasisikie).

Katika harakati yao ya kuwalingania watu njia ya Mwenyezi Mungu Mitume sio tu walikuwa tayari kukabiliana na hatari yoyote hata inayotishia maisha yao lakini pia hawakutarajia kupata chumo au mali yoyote ile ya dunia kwa sababu ya kazi hiyo nzito waliyokuwa wakifanya. Kwa maneno mengine ni kuwa hawakuwa wakitarajia chochote kwa watu mkabala wa kheri waliyokuwa wakiwafikishia.

Na ndiyo maana walikuwa wakiwaeleza bayana watu wao kwamba msidhani kuwa msipotuamini, kuna hasara tutakayopata kwani hatutarajii kupata ujira au malipo yoyote yale kutoka kwenu; sisi tunafanya yale tu tuliyoamrishwa na Mola wetu. Kisha aya zinaendelea kubainisha mwisho na hatima ya wapingaji haki na kueleza kuwa kwa kuteremka adhabu ya Mwenyezi Mungu na dhoruba kali, maji yalifunika kila kitu na ni wale waliokuwa wamepanda jahazi na Nabii Nuh ndio wao tu waliookoka na wakawa warithi wa ardhi, na kwamba hakuna mwisho mwingine unaowapata wale wanaoonywa wakapuuza zaidi ya huo uliowapata waliomkadhibisha Nauh as.

Kwa haya machache wapenzi wasomaji ndiyo tumefikia tamati ya darsa hii ya 319 ya quran. Tunamwomba Mwenyezi Mungu atulinde na kila aina ya shirki na kutuwafikisha kumwabudu kwa ikhlasi na kumtakasia dini yake. Amin.

Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

6

TAFSIRI YA SUURAT YUUNUS

YUNUS 74-78

Bismillahir Rahmanir Rahim. Assalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kutuwafikisha kukutana tena katika darsa yetu hii.

AYA 74 NA 75

Sura ya 10 ya Yunus ndiyo tunayoizungumzia kwa sasa, na hii ni darsa ya 320 tunayoianza kwa aya 74 na 75 ambazo zinasema:

ثُمَّ بَعَثْنَا مِن بَعْدِهِ رُسُلًا إِلَىٰ قَوْمِهِمْ فَجَاءُوهُم بِالْبَيِّنَاتِ فَمَا كَانُوا لِيُؤْمِنُوا بِمَا كَذَّبُوا بِهِ مِن قَبْلُ كَذَٰلِكَ نَطْبَعُ عَلَىٰ قُلُوبِ الْمُعْتَدِينَ ﴿٧٤﴾

74. Kisha tukawapeleka Mitume (wengi) baada yake kwa watu wao. Nao wakawajia na hoja waziwazi. Lakini hawakuwa wenye kuamini waliyoyakadhibisha kabla yake.

ثُمَّ بَعَثْنَا مِن بَعْدِهِم مُّوسَىٰ وَهَارُونَ إِلَىٰ فِرْعَوْنَ وَمَلَئِهِ بِآيَاتِنَا فَاسْتَكْبَرُوا وَكَانُوا قَوْمًا مُّجْرِمِينَ ﴿٧٥﴾

75. Namna hivi tunapiga muhuri juu ya nyoyo za watu warukao mipaka." Kisha baada ya hao tukamtuma Musa na Haruni kwa Firauni na watu wake wakubwa, kwa hoja zetu. Lakini walijivuna, wakawa watu maasi.

Aya tulizosoma zinaashiria utaratibu alioweka Mwenyezi Mungu mtukufu kuhusiana na utumaji wa Mitume mmoja baada ya mwingine kwa ajili ya kuwafikishia waja wake risala ya uongofu na kusema kuwa manabii walikuwa na miujiza mbali mbali kwa ajili ya kuthibitisha ukweli kwamba risala walizokuja nazo zinatoka kwa Mwenyezi Mungu mtukufu.

Na kwa hakika ukweli huo uliwathibitikia wale waliofikishiwa risala hizo. Pamoja na hayo akthari ya watu hawakuwa tayari kuikubali haki kutokana na kutopea kwenye ufuska na mambo machafu vitu ambavyo havikubaliani na sifa ya kushikamana na mafundisho ya dini.

Ijapokuwa wakati ilipotokea tufani ya gharika katika enzi za Nabii Nuh(a.s) makafiri wote waliangamizwa, na ni wale tu waliokuwa wamemwamini Mtume huyo na kuabiri pamoja naye jahazini ndio waliookoka, lakini baada ya Nabii huyo walizuka tena makafiri na mushirikina wengi na hivyo na kupelekea Mwenyezi Mungu kutuma manabii wengine kadhaa wakiwemo Ibrahim, Ismali, Hud, Saleh, Yaaqub, Yusuf n.k.

Pamoja na hayo watu waliendelea kuonyesha inadi, ukaidi na upinzani dhidi ya haki na kama walivyokuwa wakanushaji waliowatangulia hawakuwa tayari kuacha maovu ya kiitikadi na kimatendo na kuamini wito wa haki.

Baada ya manabii hao, Nabii mwingine mteule yaani Musa as akiwa pamoja na ndugu yake Harun amani ya Allah iwe juu yake, walitumwa kwa Firauni ili kumfikishia wito wa Lailaha illa llah. Lakini naye pia pamoja na watu wake walitakabari na kuipa mgongo haki.

Baadhi ya mafunzo tunayoyapata kutokana na aya hizi ni kuwa Allah sw amehakikisha kwamba anawapelekea waja wake Mitume wa kuwalingania uongofu, lakini wakati huo huo amempa mwanadamu uhuru kamili wa kuchagua kati ya kuamini na kuikufuru haki, kwani hakutaka mwanadamu aiamini na kuifuata dini yake ya haki kwa kulazimishwa na kutezwa nguvu.

AYA ZA 76 NA 77

Zifuatazo sasa ni aya za 76 na 77 ambazo zinasema:

فَلَمَّا جَاءَهُمُ الْحَقُّ مِنْ عِندِنَا قَالُوا إِنَّ هَـٰذَا لَسِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿٧٦﴾

76. Basi ilipowajia haki kutoka kwetu walisema: Bila shaka huu ni uchawi dhahiri.

قَالَ مُوسَىٰ أَتَقُولُونَ لِلْحَقِّ لَمَّا جَاءَكُمْ أَسِحْرٌ هَـٰذَا وَلَا يُفْلِحُ السَّاحِرُونَ ﴿٧٧﴾

77. Akasema Musa: Mnasema (hivi) juu ya haki ilipokujieni? Huu ni uchawi? Na wachawi hawafaulu!.

Mojawapo ya mbinu zilizokuwa zikitumiwa na wapinzani wa Mitume na hasa wale vigogo wa ukafiri na shirki ilikuwa ni kuzusha tuhuma zisizo na msingi kwa waja hao wateule wa Allah.

Na ndiyo maana Quran tukufu inaeleza kuwa takriban Mitume wote hawakusalimika na tuhuma za kusingiziwa kuwa ni wachawi, ili miujiza waliyokuja nayo ionekane kuwa ni vitendo vya hila na hadaa na wao wenyewe wachukuliwe kuwa ni watu wajanja na matapeli. Kama aya zinavyoeleza, wakati Firauni alipoona ameshindwa kukabiliana na hoja za kimantiki za wito wa haki wa Nabii Musa aliamuru wachawi wake wote wakusanywe pamoja ili kumfanya Mtume huyo wa Allah aonekane naye pia kuwa ni mchawi tu kama walivyo wachawi wake.

Hali ya kuwa alichokuwa akikieleza Nabii Musa ni kwamba nyinyi kina Firauni na watu wenu hamjawahi kunishuhudia hapo kabla nikifanya uchawi au kiini macho, lakini sasa nimekuja na wito wa haki na kuthibitisha ukweli wa Utume wangu kwa kukuonyesheni muujiza mnanisingizia kuwa ni mchawi na maneno yangu nayo mnadai kuwa ni uchawi. Ukweli ni kuwa hicho ni kisingizio tu kwa ajili ya kuipa mgongo haki.

Baadhi ya mafunzo tunayopata kutokana na aya hizi ni kuwa viongozi wa dini wanatakiwa waelewe kuwa siku zote watakuwepo watu katika jamii watakaowapiga vita na kuipinga haki na hata kutaka haki hiyo ionekane kuwa ni batili.

AYA YA 78

Wapenzi wasomaji, darsa ya 320 inahitimishwa na aya ya 78 ambayo inasema:

قَالُوا أَجِئْتَنَا لِتَلْفِتَنَا عَمَّا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا وَتَكُونَ لَكُمَا الْكِبْرِيَاءُ فِي الْأَرْضِ وَمَا نَحْنُ لَكُمَا بِمُؤْمِنِينَ ﴿٧٨﴾

78. Wakasema: Je umetujia ili utuachishe tuliyowakuta nayo baba zetu na ili ukubwa uwe wenu nyinyi (wawili) katika nchi (hii)? Wala sisi hatukuaminini nyinyi.

Kwa sababu ya kuonyesha heshima ya wazee wao waliowatangulia watu wengi huwa hawako tayari kuacha mila na desturi walizozioea na kurithi kutoka kwao, na kujenga dhana kwamba kila kilichosemwa na hao mababa na mababu zao kilikuwa sahihi, na mtu yeyote yule hana haki ya kusema kinyume na dhidi ya hayo. Hali ya kuwa kuwaheshimu waliotangulia ni kitu kimoja na kung'ang'ania bila hoja bali kwa taasubi na ukereketwa tu kila lililosemwa na kutendwa na wao, na kuhisi sisi wa baada ya wao tufanye kile kile kilichofanywa na wao hata kama si sahihi, hicho nacho ni kitu kingine kabisa.

Na ni kwa mantiki hiyo isiyo sahihi, ndio maana wapinzani wa Mitume walikuwa wakishikilia kwamba maadamu wazee wetu walikuwa wakiabudu masanamu, sisi hatuko tayari kuamini bali hata kusikia kitu kingine ghairi ya hicho. Funzo mojawapo tunalopata kutokana na aya hii ni kuwa kushikilia kufuata kibubusa itikadi potofu za waliotangulia ni miongoni mwa sababu kuu zilizowafanya watu wengi wapinge risala za Mitume wao. Wapenzi wasomaji darsa ya 320 imefikia tamati. Tunamwomba Allah atuonyeshe haki na kutuwafikisha kuifuata, na atuonyeshe batili na kutuwezesha kuiepuka. Amin.

Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.