TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA 22%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 16 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14652 / Pakua: 3572
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

KIMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

KIMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

KIMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

KUPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Sura Ya Tano: Al - Maidah

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri yenyewe ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea, hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho 'Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah' (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasyansi kama kina Enstein, Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo,vile vile kutaja nchi mbalimbali zikiwemo za Afrika; kama vile Afrika ya kusini, Zimbabwe nk, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho : Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa "Fawqahum ila yawmil qiyama" badala ya "Fawqahum yawamal qiyama" Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu jabal amail 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: " Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa, kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu."

Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubaliayale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿لَتَجِدَنَّ أَشَدَّ النَّاسِ عَدَاوَةً لِّلَّذِينَ آمَنُوا الْيَهُودَ وَالَّذِينَ أَشْرَكُوا وَلَتَجِدَنَّ أَقْرَبَهُم مَّوَدَّةً لِّلَّذِينَ آمَنُوا الَّذِينَ قَالُوا إِنَّا نَصَارَىٰ ذَٰلِكَ بِأَنَّ مِنْهُمْ قِسِّيسِينَ وَرُهْبَانًا وَأَنَّهُمْ لَا يَسْتَكْبِرُونَ﴾

82.Hakika utawakuta walio shadidi kuliko watu wote katika uadui kwa walio amini ni Mayahudi na washirikina. Na utawakuta walio karibu mno kwa mapenzi ni wale wanao sema: Sisi ni Manasara. Hayo ni kwa sababu wapo miongoni mwao makasisi na wamonaki, na kwa sababu wao hawafanyi kiburi.

﴿وَإِذَا سَمِعُوا مَا أُنزِلَ إِلَى الرَّسُولِ تَرَىٰ أَعْيُنَهُمْ تَفِيضُ مِنَ الدَّمْعِ مِمَّا عَرَفُوا مِنَ الْحَقِّ يَقُولُونَ رَبَّنَا آمَنَّا فَاكْتُبْنَا مَعَ الشَّاهِدِينَ﴾

83.Na wanaposikia yaliyoteremshwa kwa Mtume, utaona macho yao yanamiminika machozi kwa sababu ya haki waliyoitambua, wanasema: Mola wetu tumeamini tuandike pamoja na wanaoshuhudia

﴿وَمَا لَنَا لَا نُؤْمِنُ بِاللَّـهِ وَمَا جَاءَنَا مِنَ الْحَقِّ وَنَطْمَعُ أَن يُدْخِلَنَا رَبُّنَا مَعَ الْقَوْمِ الصَّالِحِينَ﴾

84.Na kwa nini tusimwamini Mwenyezi Mungu na haki iliyotujia, na hali tunatumai Mola atuingize peponi pamoja na watu wema?

﴿فَأَثَابَهُمُ اللَّـهُ بِمَا قَالُوا جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ الْمُحْسِنِينَ﴾

85.Basi Mwenyezi Mungu atawalipa, kwa yale waliyosema, Bustani zipitazo chini yake mito, Humo watakaa milele, Na hayo ndiyo malipo ya wafanyao mema.

﴿وَالَّذِينَ كَفَرُوا وَكَذَّبُوا بِآيَاتِنَا أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْجَحِيمِ﴾

86.Na wale waliokufuru na kuzikanusha Aya zetu, hao ndio watu wa motoni

UADUI WA MAYAHUDI NA URAFIKI WAWAKRISTO

Aya 82 - 86

MAANA

Hakika utawakuta walio maadui zaidi kuliko watu wengine kwa walioamini ni mayahudi na washirikina.

Yaani mayahudi na washirikina ndio waliokuwa maadui zaidi kwa Waislamu. Mara nyingi watu wameitolea ushahidi Aya hii, kuwa dini ya kikristo iko karibu zaidi na Uislam kuliko dini ya kiyahudi. Hilo ni kosa ikiwa inakusudiwa dini ya kiyahudi na ya kikristo kabla ya kugeuzwa. Kwa sababu dini kwa Mwenyezi Mungu na Mitume wake ni moja tu kwa upande wa itikadi na msingi yake. Na kama ikikusudia baada ya kubadilishwa, basi zote mbili ni sawa (Ukristo na Uyahudi) hakuna yenye afadhali.

Usahihi ni kuwa uhasama wa mayahudi na washirikina katika Uislam unatokana na mgongano baina ya mwito wa kiislam na tabia iliyokuwa imeshika kasi katika Bara arabu mwanzo wa utume. Tabia hiyo ilikua ni mashindano ya kupora mali na watumwa. Vilevile riba, ghushi na mengineyo ya kutumia nguvu na utapeli. Tabia hii iliambukiza wafanyibiashara wa kigeni, kama walivyoambukizwa viongozi wa kiyahudi waliokuwa wakimiliki viwanda na biashara ya ndani.

Ukaja mwito wa Muhammad(s.a.w.w) unaohimiza uadilifu na kukataa dhuluma na unyonyaji wa aina zote, na kuzuia unyonyaji wa mayahudi na washirikina. Kutokana na hali hiyo ndipo pande zote mbili zikakutana na kukubaliana kwa pamoja kujiepusha na dini na itikadi na kuungana mkono kupigana na Muhammad(s.a.w.w) , adui wa wote wawili.

Kwa ufafanuzi zaidi ni kuwa uadui wa mayahudi na washirikina kwa waislam, ulikuwa ni kwa msukumo wa kidunia na wala sio wa kidini, lakini mayahudi walijificha nyuma ya pazia la dini kwa kujionyesha na unafiki; sawa na wafanyavyo leo watu wanaotafuta chumo la haramu. Zaidi ya hayo ni kuwa mayahudi na washirikina wanashirikiana katika ubaguzi. Lakini washirikina pamoja na ujahili wao walikuwa na moyo usiokuwa mgumu, wakarimu na wenye fikra huru zaidi ya mayahudi. Ndio maana wengi wao wakamwamini Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na ni mayahudi wachache tu ndio waliomwamini Muhammad.

NI NANI WALIO KARIBU NAWAISLAMU KIMAPENZI

Na utawakuta walio karibu zaidi kwa mapenzi na waumini ni wale waliosema sisi ni wanaswara.

Baadhi wanaichukulia Aya hii na iliyo baada yake ni chombo cha kukoroga mambo, kwamba Uislamu unaelemea mojawapo ya majeshi mawili hivi sasa. Jambo hili ndilo lililotufanya tufafanue Aya hizi nne kwa namna ambayo haitaacha nafasi kwa wale wanaobadilisha mambo.

Hakika mwenye kuziangalia vizuri Aya hizi, hawezi kuwa na hata chembe ya shaka kuwa zinakamilishana na kwamba haifai kabisa kuifasiri moja pekee yake bila ya kuichanganya na wenzake.

Nazo ziko wazi kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakuwafanya bora manaswara, kwa ujumla, kuliko makundi mengine katika kuwa karibu kiurafiki, si kwa umbali wala karibu.

Isipokuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alikusudia kikundi maalum kutoka manaswara (wakristo) kwa dalili ya kuwa yeye hakuishia hapo tu bali aliendelea kusema: "Hayo ni kwa sababu wako miongoni mwao makasisi na watawa, na kwamba wao hawafanyi kiburi." Tena akaendelea kusema: Na wanaposikia yaliyoteremshwa kwa mtume, utaona macho yao yanamiminika machozi kwa sababu ya haki waliyoitambua; wanasema: "Mola wetu! Tumeamini basi tuandikie pamoja na wanaoshuhudia"

Maana yake ni kuwa miongoni mwa manaswara (wakristo) wako walioujua Uislamu,wakaukubali kwa kutii, kukinai na kwa imani.

Historia inathibitisha hivyo; kama ambavyo inathibitisha chuki ya manaswara kwa Uislam na Waislam. Kwa mfano: Fedheha ya Wataliano huko Tripoli ya Magharibi, na Wafaransa katika Algeria, Tunisia, Morocco na Syria, Vile vile fedheha ya Waingereza katika Misr, Iraq, Sudan n.k.

Na leo hii[1] Marekani wanaaungana na mayahudi katika kulingamiza taifa la Palestina. Wanawapa silaha za kisasa maharamia hawa, kisha wanafanya uchokozi na kudai kuwa wao ndio waliochokozwa na kuungwa mkono na Marekani katika Baraza la Usalama na Umoja wa mataifa. Hapo Marekani husema: Huu ndio ukweli uadilifu na demokrasia.

Je, baada ya hayo na mengi yasiyokuwa haya, itasemwa kuwa wakristo wote wako karibu kwa urafiki na waislam? Haya hayasemwi ila na mjinga au mwenye kutaka kuwapoteza watu. Kisha mpotezaji huyu atasema nini kuhusu kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

"Na kwa nini tusimwamini Mwenyezi Mungu na haki iliyotujia, na hali tunatumai Mola atuingize pamoja na watu wema?."

Haki iliyowajia na kuiamini, ni ile waliyobashiriwa na Isa:

﴿وَمُبَشِّرًا بِرَسُولٍ يَأْتِي مِن بَعْدِي اسْمُهُ أَحْمَدُ﴾

"Na kutoa Bishara ya Mjumbe atakayekuja baada yangu aitwaye Ahmad" (61:6)

Hayo, bila shaka, yanatiliwa mkazo na kukanushwa na kauli yake Mwenyezi Mungu aliyoifuatilia bila ya upambanuzi wowote isemayo:

Basi Mwenyezi Mungu atawalipa, kwa yale waliyosema, Bustani zipitazo chini yake mito, humo watakaa milele na hayo ndiyo malipo ya wafanyao mema.

Ushahidi wa wema na kulipwa pepo kwa kundi hili la wakristo ni dalili ya mkato ya kusilimu, na kwamba ndilo pekee lililokusudiwa baada ya kusifiwa wema na thawabu.

Ama wakristo ambao wameikana haki baada ya kuijua au wakaipinga bila ya kuangalia dalili zake na ubadhirifu wake, hawa wamekemewa na Mwenyezi Mungu na kuwapa kiaga kwa kusema:

Na wale waliokufuru na kuzikadhibisha Aya zetu hao ndio watu wa Motoni.

Unaweza kuuliza : kuwa kauli ya waliokufuru na kuzikadhibisha Aya zetu, inamhusu kila mwenye kukufuru na kukadhibisha. Sasa je, kuna wajihi gani wa kuhusisha wakristo?

Jibu : Mfumo wa maneno unafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) baada ya kuahidi pepo wenye kuamini katika wakristo, amewaahidi moto wenye kung'ang'ania ukafiri miongoni mwao. Ameleta neno la jumla, ili kujumuisha kemeo kwa kila mwenye kuihalifu haki na kuipinga, jambo ambao halipingani na yale tuliyoyasema.

Kwa ufupi ni kuwa Aya hii iko wazi kuwa makusduio ni kundi mahsusi katika wakristo - wale waliojua haki na kuiamini. Na kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawaingiza peponi kwa sababu ya imani yao na amali yao njema.

Tukikadiria kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na utawakuta walio karibu kwa mapenzi na waumin ni wale waliosema sisi ni manaswara," inawakusanya wakristo wote, basi itawajibika tuiache dhahiri ya Aya na tuihusishe na wale walioamini katika wao kwa sababu mbili:

Kwanza : kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja katika Aya kadhaa kuwa manswara wamemfanyia Mungu washirika, wakaficha jina la Muhammad(s.a.w.w) na wakawafanya wanavyuoni wao na watawa wao kuwa waungu badala ya Mwenyezi Mungu. Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akakataza kuwafanya mayahudi na manswara kuwa marafiki. Na akasema:

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَتَّخِذُوا الْيَهُودَ وَالنَّصَارَىٰ أَوْلِيَاءَ﴾

"Enyi Mlioamini msiwafanye marafiki mayahudi na manswara" (5:51)

Tukiunganisha Aya hii, na zilizo mfano wa Aya hii, juu ya kauli yake Mwenyezi Mungu na utawakuta walio karibu zaidi kwa mapenzi na waumin ni wale waliosema sisi ni manswara," maana yanakuwa:

﴿مِّنْهُمْ أُمَّةٌ مُّقْتَصِدَةٌ وَكَثِيرٌ مِّنْهُمْ سَاءَ مَا يَعْمَلُونَ﴾

"Miongoni mwao wako watu washikao njia ya wastani, na wengi wao wanayoyafanya ni mambo mbaya" (5: 66)

Pili : ni kuwa wafasiri wanasema, Aya hii tunayoizungumzia ilishuka kwa sababu ya Najashi, mfalme wa Uhabeshi[2] aliyekuwa mnaswara (Mkiristo). Kwani Mtume(s.a.w.w) alipoona adhabu inayowapata sahaba zake kutoka kwa washirikina, mwanzo mwanzo wa mwito wa Uislam, aliwaamuru kuhamia Uhabeshi na kuwaambia: "Huko kuna mfalme ambaye hadhulumiwi mbele yake yeyote." Wakaenda huko, miongoni mwao akiwemo Jafar bin Abu Talib. Wakapata amani kwa Najashi na ujirani mwema. Hilo lilikuwa mnamo mwaka wa tano wa kutangazwa Utume.

Zimekuja Hadith Mutawatir kuwa Najashi na Baraza lake, la Mambo ya dini na mambo ya kidunia, walisilimu mikononi mwa Jafar bin Abu Talib baada ya kuwasomea Aya za Qur'an Tukufu na kutaja mazuri ya Uislam. Na kwamba walibubujikwa na machozi waliposikia Aya za Mwenyezi Mungu.

Baada ya hayo tunasema kwamba yule anayetolea ushahidi kauli ya Mwenyezi Mungu (Na utawakuta walio karibu zaidi kwa mapenzi na waumin ni wale waliosema sisi ni manswara) kwamba ukristo na wakristo kwa ujumla wote wako karibu zaidi na Uislamu na waislamu kuliko wengine, na kunyamazia Aya zinazokamilisha Aya hii, anayefanya hivyo huyo hakijui Kitabu cha Mwenyezi Mungu au ni mwenye kujionyesha tu kwa kutaka kuongeza chumvi kwa kuutumia Uislamu na Qur'an au anaweza kuwa ni mhaini anayezitia sumu fikra dhaifu katika Uislamu ili zikubali madai ya maadui wa dini, wanaowasaidia Israil na kuwapongeza kwa uchokozi wao kwa Waarabu na Waislam.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تُحَرِّمُوا طَيِّبَاتِ مَا أَحَلَّ اللَّـهُ لَكُمْ وَلَا تَعْتَدُوا إِنَّ اللَّـهَ لَا يُحِبُّ الْمُعْتَدِينَ﴾

87.Enyi mlioamini! Msiharamishe vizuri alivyowahalalishia Mwenyezi Mungu. Wala msipetuke mipaka. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wanaopetuka mipaka.

﴿وَكُلُوا مِمَّا رَزَقَكُمُ اللَّـهُ حَلَالًا طَيِّبًا وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي أَنتُم بِهِ مُؤْمِنُونَ﴾

88.Na kuleni katika vile alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu vilivyo halali na vizuri, na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye nyinyi mnamwamini.

MSIHARAMISHE VIZURI

Aya 87 - 88

MAANA

Enyi mlioamini! Msiharamishe vizuri alivyowahalalishia Mwenyezi Mungu.

Wamesema kuwa Aya hii imeshuka kwa Masahaba waliokuwa na hofu sana na Mwenyezi Mungu wakajiharamishia wanawake, vyakula vizuri na mavazi. Wakawa wanaswali usiku na kufunga mchana. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akawaita na kuwasomea Aya hii, akasema: Ama mimi ninaswali usiku na ninalala, ninafunga na ninafungua na ninawaendea wanawake. Basi atakayejiepusha na mwenendo wangu si katika mimi."

Na kauli yake Mwenyezi Mungu;Wala msipetuke mipaka. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wapetukao mipaka, inafahamisha kuwa kuharamisha halali ni sawa na kuhalalisha haramu, yote mawili ni dhulma na ukiukaji mipaka.

Na kuleni katika vile alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu vilivyo halali na vizuri. Imetangulia tafsir yake katika Juz.2 (2:168)

﴿لَا يُؤَاخِذُكُمُ اللَّـهُ بِاللَّغْوِ فِي أَيْمَانِكُمْ وَلَـٰكِن يُؤَاخِذُكُم بِمَا عَقَّدتُّمُ الْأَيْمَانَ فَكَفَّارَتُهُ إِطْعَامُ عَشَرَةِ مَسَاكِينَ مِنْ أَوْسَطِ مَا تُطْعِمُونَ أَهْلِيكُمْ أَوْ كِسْوَتُهُمْ أَوْ تَحْرِيرُ رَقَبَةٍ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ ثَلَاثَةِ أَيَّامٍ ذَٰلِكَ كَفَّارَةُ أَيْمَانِكُمْ إِذَا حَلَفْتُمْ وَاحْفَظُوا أَيْمَانَكُمْ كَذَٰلِكَ يُبَيِّنُ اللَّـهُ لَكُمْ آيَاتِهِ لَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ﴾

89.Mwenyezi Mungu hawachukuli kwa viapo vyenu vya upuuzi; lakini anawachukulia kwa mlivyoapa kwa nia. Basi kafara yake ni kuwalisha masikini kumi kwa wastani wa mnavyowalisha watu wenu, au kuwavisha au kumwacha huru mtumwa. Na asiyeweza kupata (hayo), basi afunge siku tatu. Hayo ndiyo kafara ya viapo vyenu. Na vichungeni viapo vyenu. Namna hii Mwenyezi Mungu anawabainisha Aya zake ili mpate kushukuru.

VIAPO VYA UPUUZI

Aya 89

MAANA

Mwenyezi Mungu Hawachukuli kwa viapo vyenu vya upuzi.

Viapo vya upuzi ni kuachia ulimi bila ya kukusudia; kama vile kusema: Hapana wallahi, kumjibu aliyeuliza Je umemwona fulani, au kusema: Sivyo wallah, kumjibu aliyesema: Hutaki hii na Viapo hivi havitiliwi manani wala havina kafara kama mtu akihalifu lile alilo liapia.

Na aliyesema hawezi kuhisabiwa kuwa mwongo, na mtu yeyote hawezi kumwambia umemwapia Mwenyezi Mungu uwongo.

Kwa maneno mengine ni kwamba viapo hivyo havina athari yoyote ya kiapo. Hata hivyo iliyo bora ni kuacha ikiwa mtu hajaghafilika.

Lakini anawachukulia kwa mlivyoapa kwa nia.

Yaani kiapo cha sharia ambacho ni wajibu kukitekeleza na kutiliwa manani, ni kile anachoapa mtu aliyebaleghe mwenye akili timamu, kwa kukusudia, kutaka na kuwa na hiyari.

Wameafikiana kuwa kiapo kinakamilika ikiwa ni kwa kuapa kwa jina la Allah au kwa mojawapo ya majina yake mema, kama vile Khaliq, Razak (Muumbaji na Mruzuku)

Shia na Hanafi wanasema: "Kiapo hakiwi kwa jina la Msahafu na Mtume au Al-Ka'aba, kutokana na Hadith isemayo:Ambaye ataapa, basi na ape kwa jina la Allah au aache."

Shafi, Malik au Hambal wanasema: "Kinakuwa kwa jina la Msahafu. Hambali amekua peke yake katika kusema kuwa kinakuwa kwa Mtume vilevile.

Basi kafara yake ni kuwalisha masikini kumi kwa wastani wa mnavyowalisha watu wenu, au kuwavisha au kumwacha huru mtumwa.

Akiapa na akavunja kiapo, yaani akifanya lile aliloliapia kuliacha au kuacha lile aliloapia kulifanya, ni wajibu kwake atoe kafara akihiyarishwa baina ya mambo matatu.

Kwanza : kuwalisha masikini kumi mlo moja kila mmoja, kwa pamoja au mbali mbali kwa sharti ya kuwa ni mlo wa chakula ambacho aghalabu yeye hula na famlia yake. Inajuzu kumpa masikini kibaba cha chakula badala ya mlo. Makusudio ya masikini, ni yule ambaye ni halali kumpa Zaka, Kibaba ni zaidi kidogo ya 800 gm.

Pili : ni kuwavisha masikini kumi. Inatosha ile inayoitwa nguo ya kawaida. Kwa sababu sharia haikuhusisha. Kwa hiyo yakachukulia maana yaliyozoeleka bila ya kutofautisha mpya na ya zamani; mradi tu isiwe imechakaa au iliyochanika.

Tatu : ni kumwacha huru mtumwa; wala hakuna utumwa leo.

Na asiyeweza kupata (hayo), basi afunge siku tatu.

Yaani akishindwa kuyapata hayo matatu yaliyotangulia, atafunga siku tatu. Na akishindwa kufunga, basi ataomba maghufira kwa Mwenyezi Mungu na kutaraji msamaha wake.

Hayo ndiyo kafara ya viapo vyenu.

Hayo ni ishara ya kulisha, kuvisha, kuacha huru mtumwa na kufunga baada ya kushindwa na mambo matatu.

Na vichungeni viapo vyenu. Kuvifanya ni vya kawaida. Kwani kiapo cha Mwenyezi Mungu kina heshima yake na utukufu wake. Mwenyezi Mungu anasema: "Wala msimfanye Mwenyezi Mungu ni pondokeo la viapo vyenu" Juz.2 (2:224)

Kuna Hadith isemayo:"Hakika Nabii wa Mwenyezi Mungu, Musa aliwaamuru waongo wasiape kwa Mwenyezi Mungu. Na mimi ninawaamuru waongo na wa kweli wasimwapie Mwenyezi Mungu."

Namna hii Mwenyezi Mungu anawabainishia Aya zake ili mpate kushukuru.

Amesema Razi: "Maana yako wazi." Hata hivyo Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaka kutukumbusha neema za kujua hukumu zake, ili tusizitoe mahali pengine.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِنَّمَا الْخَمْرُ وَالْمَيْسِرُ وَالْأَنصَابُ وَالْأَزْلَامُ رِجْسٌ مِّنْ عَمَلِ الشَّيْطَانِ فَاجْتَنِبُوهُ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ﴾

90.Enyi mlioamini! Hakika pombe na kamari na mizimu na mburuga ni uchafu katika kazi ya Shetani. Basi jiepusheni nayo, ili mpate kufaulu.

﴿إِنَّمَا يُرِيدُ الشَّيْطَانُ أَن يُوقِعَ بَيْنَكُمُ الْعَدَاوَةَ وَالْبَغْضَاءَ فِي الْخَمْرِ وَالْمَيْسِرِ وَيَصُدَّكُمْ عَن ذِكْرِ اللَّـهِ وَعَنِ الصَّلَاةِ فَهَلْ أَنتُم مُّنتَهُونَ﴾

91.Hakika Shetani anataka kuwaingizia uadui na bughudha baina yenu kwa pombe na kamari na kuwazuia kumkumbuka Mwenyezi Mungu na kuswali, basi je, mtakoma.

﴿وَأَطِيعُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُوا الرَّسُولَ وَاحْذَرُوا فَإِن تَوَلَّيْتُمْ فَاعْلَمُوا أَنَّمَا عَلَىٰ رَسُولِنَا الْبَلَاغُ الْمُبِينُ﴾

92.Na mtiini Mwenyezi Mungu na mtiini Mtume na tahadharini na mkikengeuka basi jueni kuwa ni juu ya mtume wetu kufikisha (ujumbe) tu waziwazi.

POMBE NA KAMARI

Aya 90 - 92

MAANA

Enyi mlioamini! Hakika pombe na kamari na mizimu na mburuga ni uchafu katika kazi ya shetani.

Tumezungumzia kwa ufafanuzi kuhusu pombe na kamari katika kufasiri Aya Juz.2 (2:219). Na kuhusu mizimu na Mburuga katika Aya ya 3 ya Sura hii tuliyonayo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amenasibisha kwa shetani kunywa pombe, kucheza kamari, kuabudu masanamu na kuagulia kwa mburuga. Kwa sababu Shetani ndiye anayapendekeza na kuwaghuri watu kwayo.

Basi jiepusheni nayo ili mpate kufaulu.

Dhamiri ya jiepusheni nayo inarudia uchafu. Hiyo ni amri ya kujiepusha; na amri inafahamisha wajibu, hasa wakati wa kubainisha sababu. Na ameibainisha hapo kuwa sababu ya kujiepusha ni kufaulu. Hata kama kusingekuwa na dalili ya kuharamishwa pombe zaidi ya kuwekwa sawa na kuabudu sanamu, ingelitosha. Sikwambii tena kama tukiunganisha na (2:219, 7:32), Hadith Mutawatir na Ijmai ya Waislamu tangu wakati wa Mtume(s.a.w.w) mpaka siku ya mwisho.

Hakika Shetani anataka kuwaingizia uadui na bughudha baina yenu kwa pombe na kamari na kuwazuia kumkumbuka Mwenyezi Mungu na kuswali.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutilia mkazo uharamu wa pombe na kamari, na akakulinganisha na kuabudu masanamu na akakujaalia ni uchaTafsir fu unaotokana na adui wa mtu, na tena akabainisha kuwa njia ya kujiepusha ni kufaulu, baada ya yote haya. Anaonyesha Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwamba kwenye mambo mawili hayo kuna uharibifu mara mbili:Kwanza : wa kijamii - kutoelewana pamoja na kuleta chuki na undani baina ya watu.

Pili : ni wa kidini - kuzuia kumkumbuka Mwenyezi Mungu na ibada zake. Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akataka watu wakome kunywa pombe na kucheza kamari kwa ibara fasaha kabisaBasi je mtakoma ?

Uislamu unahimiza kwa mahimizo yote kuwa mtu aungane na Muumba wake na jamii yake, na kwamba mtu mbele ya Mungu na mbele ya watu, awe mwenye kuridhiwa na kuheshimiwa.

Na mtiini Mwenyezi Mungu na mtiini Mtume kwa kuacha pombe na kamari na mengineyo yaliyoharamishwa.

Na tahadharini isije ikawapata adhabu ya Mwenyezi Mungu, kama mkihalifu amri yake na amri ya Mtume wake. Imam Aliy(a.s) anasema:

"Mwenye kuinasihi nafsi yake zaidi ya watu (wote) ni yule anayemtii Mola wake zaidi yao. Na mwenye kuihadaa nafsi yake zaidi ya watu (wote) ni yule mwenye kuasi zaidi yao."

Na mkikengeuka basi jueni kuwa ni juu ya Mtume wetu kufikisha tu (ujumbe) waziwazi.

Naye ametekeleza kikamilifu, akasimamisha hoja na kutoka katika jukumu la kufikisha. Atakayehalifu ni yeye peke yake na jukumu lake.

﴿لَيْسَ عَلَى الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ جُنَاحٌ فِيمَا طَعِمُوا إِذَا مَا اتَّقَوا وَّآمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ ثُمَّ اتَّقَوا وَّآمَنُوا ثُمَّ اتَّقَوا وَّأَحْسَنُوا وَاللَّـهُ يُحِبُّ الْمُحْسِنِينَ﴾

93.Si dhambi juu ya wale walioamini na wakatenda mema wa vile walivyovila maadamu wakiwa na takua na wakiamini na wakitenda mema, tena wakawa na takua na wakaamini, tena wakawa na takua na wakafanya mazuri, Na Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao mazuri.

WENYE TAKUA NA KUAMINI

Aya 93

MAANA

Wafasiri wameafikiana kwamba iliposhuka Aya ya kuharamisha pombe, baadhi ya Masahaba walimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : Itakuwaje kwa ndugu zetu waliokufa wakiwa wanywaji?

Ndipo ikashuka Aya hii ambayo kwa ujumla inafahamisha kuwa mwenye kunywa pombe kabla ya kubainishwa hukumu yake, hapana vibaya juu yake ikiwa ni katika waumini wanaomcha Mungu. Kuanzia hapa ndipo mafakihi wakaafikiana kwamba kila kitu ni halali mpaka kikatazwe.

Baada ya kuafikiana wafasiri kuwa maana haya ndiyo makusudio katika Aya walihitalifiana katika sababu zinazowajibisha kukaririka takua mara tatu; ambapo mara ya kwanza kumetajwa, pamoja na Imani na amali njema, mara ya pili pamoja na Imani tu na mara ya tatu pamoja na uzuri.

Razi amenukuu, katika hilo, kauli tano. Mwenye Majmaul-bayan akasema: Makusudio ya takua ya kwanza ni kuacha kunywa pombe baada ya kuharamishwa; ya pili ni kudumu juu ya hilo na ya tatu ni kuacha maasi yote pamoja na kufanya mema.

Mmoja wa wafasiri wapya anasema: "Nafsi yangu bado haijatulia na chochote katika tafsir hii; wala Mwenyezi Mungu hajanifungulia chochote. Tunavyofikiria sisi - Mwenyezi Mungu ndiye mjuzi zaidi - ni kwamba lengo la kukaririka huku ni kubainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwamba mwenye takua ya kweli ni yule anayemcha Mwenyezi Mungu katika hali zake zote, ujana, uzee na ukongwe, na katika dhiki na faraja. Na kwamba mwenye kufa juu ya hilo basi yuko katika amani na usalama.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَيَبْلُوَنَّكُمُ اللَّـهُ بِشَيْءٍ مِّنَ الصَّيْدِ تَنَالُهُ أَيْدِيكُمْ وَرِمَاحُكُمْ لِيَعْلَمَ اللَّـهُ مَن يَخَافُهُ بِالْغَيْبِ فَمَنِ اعْتَدَىٰ بَعْدَ ذَٰلِكَ فَلَهُ عَذَابٌ أَلِيمٌ﴾

94.Enyi mlioamini! Hakika Mwenyezi Mungu atawajaribu kwa baadhi ya mawindo yatakayofikiwa na mikono yenu na mikuki yenu, ili Mwenyezi Mungu amjue ni nani anayemwogopa kwa ghaibu, Basi atakayeruka mipaka baada ya hayo, atapata adhabu iumizayo.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَقْتُلُوا الصَّيْدَ وَأَنتُمْ حُرُمٌ وَمَن قَتَلَهُ مِنكُم مُّتَعَمِّدًا فَجَزَاءٌ مِّثْلُ مَا قَتَلَ مِنَ النَّعَمِ يَحْكُمُ بِهِ ذَوَا عَدْلٍ مِّنكُمْ هَدْيًا بَالِغَ الْكَعْبَةِ أَوْ كَفَّارَةٌ طَعَامُ مَسَاكِينَ أَوْ عَدْلُ ذَٰلِكَ صِيَامًا لِّيَذُوقَ وَبَالَ أَمْرِهِ عَفَا اللَّـهُ عَمَّا سَلَفَ وَمَنْ عَادَ فَيَنتَقِمُ اللَّـهُ مِنْهُ وَاللَّـهُ عَزِيزٌ ذُو انتِقَامٍ﴾

95.Enyi Mlioamini! Msiue windo na hali mko katika Ihram. Na miongoni mwenu atakayemuua kwa kusudi, basi malipo (yake) yatakuwa ni mfano wa aliyemuua katika wanyama wa kufugwa, kama watavyohukumu waadilifu wawili miongoni mwenu, mnyama apelekwe Al-kaaba (kama sadaka); au kutoa kafara kwa kuwalisha masikini; au badala ya hayo ni kufunga; ili aonje ubaya wa jambo lake. Mwenyezi Mungu amekwisha yasamehe yaliyopita; na atakayerudia, Mwenyezi Mungu atampa adhabu; na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye nguvu mwenye kuadhibu.

﴿أُحِلَّ لَكُمْ صَيْدُ الْبَحْرِ وَطَعَامُهُ مَتَاعًا لَّكُمْ وَلِلسَّيَّارَةِ وَحُرِّمَ عَلَيْكُمْ صَيْدُ الْبَرِّ مَا دُمْتُمْ حُرُمًا وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ﴾

96.Mmehalalishiwa kuvua baharini na chakula chake, kwa manufaa yenu na kwa wasafiri. Na mmeharamishiwa kuwinda bara maadamu mko katika Ihram, Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

HAKUNA KUWINDA KATIKA HARAM WALA PAMOJA NA IHRAM

Aya 94 - 96

MAANA

Enyi Mlioamini! Hakika Mwenyezi Mungu atawajaribu kwa baadhi ya mawindo yanayofikiwa na mikono yenu na mikuki yenu.

Makusudio ya baadhi ni mawindo ya bara tu. Kauli yake Mwenyezi Mungu yanayoafikiwa na mikono yenu na mikuki" ni fumbo la kuwinda, bila ya shaka. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameharamisha kuwinda bara katika Haram[3] na katika hali ya Ihram[4] jambo ambalo ni jepesi; sawa na alivyowaharimishia Wana wa Israil kuvua samaki siku ya Jumamosi (sabato).

Ili Mwenyezi Mungu amjue ni nani anayemwogopa kwa ghaibu.

Yaani Mwenyezi Mungu amewajaribu kwa kuharamisha kuwinda katika hali hii ili ampambanue yule anayemwogopa katika siri kama yule anayemtii katika dhahiri na yule anayejionyesha kwa kumtii na kumwogopa mbele ya watu na kumwasi katika uficho.

Basi atakayeruka mipaka baada ya hayo, atapata adhabu iumizayo.

Yaani mwenye kuhalifu amri ya Mwenyezi Mungu kwa kuwinda baada ya ubainifu huu na hoja, basi atastahiki adhabu ya Mwenyezi Mungu na mateso.

MAANA YA KUJARIBU KWA MWENYEZI MUNGU

Unaweza kuuliza : kuwa kwa Mwenyezi Mungu halifichiki lolote lilo katika ardhi wala katika mbingu; sasa kuna wajihi gani wa kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hakika Mwenyezi Mungu atawajaribu, na kauli yake:"Ili Mwenyezi Mungu amjue anayemwogopa"

Jibu : Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) hamjaribu mja wake ili ajue ambayo hakuwa akijua, hapana! Kwani yeye anamjua zaidi kuliko yeye mwenyewe. Isipokuwa anamtia mtihani kwa mambo mengi; kama haya yafuatayo:-

Kuyafasiri yale yalioko katika nafsi ya mja yajitokeze. Ambapo hekima imepitishwa kutowahisabu watu kwa yale anayoyajua kwao wala yale yanayokuwa katika nafsi zao katika silika. Isipokuwa atawahisabu na matukio ya matendo. Silika ya kinafsi peke yake haina haja ya kuhisabiwa wala kupewa adhabu, maadam iko ndani tu ya binadamu na athari yake haionekani kwa macho au kusikiwa kwa masikio.

Imam Ali(a.s) anasema: "Mwenyezi Mungu anasema:Jueni kuwa mali zenu na watoto wenu ni fitna. Maana yake ni kuwa anawajaribu kwa mali na watoto ili abainike mwenye kuichukia riziki yake na mwenye kuridhia ugawanyo wake, ingawaje Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni mjuzi zaidi kuliko nafsi zao, lakini ni kudhihirisha vitendo ambavyo vinastahiki thawabu na adhabu.

Kumpambanua mwovu na mwema na kuidhihirisha hakika yake mbele ya watu na kumchukulia vile anavyostahiki. Na hayo, mara nyingi sana, hutokea katika maisha ya watu.

Kwa mfano wewe unajua Zedi ni katika watu wa elimu na maarifa. Ikawa yeye yuko baina ya watu wasiojua ujuzi wake, nawe ukataka wajue mwamko wake na elimu yake. Kwa hiyo ukamuuliza mbele ya watu, ili aseme na ajulikane.

Au pengine unajua kwamba yeye ni duni mjinga, na watu wanamdhania kuwa ni mjuzi mwenye hekima. Kwa hiyo ukafanya hivyo hivyo udhihirishe ujinga wake na uduni wake.

Watu wengi wao wenyewe hawajijui na wanasema : lau tungelikuwa na hali fulani, basi tungefanya kadha wa kadha. Kwa hiyo Mwenyezi Mungu huwapa uwezo na fursa ili awe na hoja juu yao na ijulikane hakika yao na hali yao. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَمِنْهُم مَّنْ عَاهَدَ اللَّـهَ لَئِنْ آتَانَا مِن فَضْلِهِ لَنَصَّدَّقَنَّ وَلَنَكُونَنَّ مِنَ الصَّالِحِينَ ﴿٧٥﴾ فَلَمَّا آتَاهُم مِّن فَضْلِهِ بَخِلُوا بِهِ وَتَوَلَّوا وَّهُم مُّعْرِضُونَ﴾

"Na miongoni mwao wako waliomwahidi Mwenyezi Mungu kuwa: Akitupa katika fadhila zake, kwa hakika tutatoa sadaka na kwa hakika tutakuwa katika wanaotenda mema. Alipowapa katika fadhila yake wakaifanyia ubakhili na wakageuka na huku wao wanapuuza" (9:75-76)

Wana wa Israil walimtaka Musa awafanyie siku ya kupumzika na kufanya ibada, Mwenyezi Mungu akawajaalia siku ya Jumamosi (sabato).

Wakaahidi kutofanya chochote siku hiyo; kama walivyotaka, lakini ikawa samaki wanawajia sana siku hii na inapokwisha Jumamosi na samaki nao hupotea. Wana wa Israil wakafanya hila ya kuwavua na wakavunja ahadi.

Kwa hiyo kwenye wajihi wa kwanza tulioueleza - kudhihiri vitendo vinavyostahiki thawabu na adhabu, ndiyo yamechukuliwa maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu "Hakika atawajaribu Mwenyezi Mungu, ili amjue Mwenyezi Mungu anayemwogopa. Na ili awajue Mwenyezi Mungu wale walioamini" na mfano wa Aya hii.

Enyi mlioamini! Msiue windo na hali mko katika Ihram.

Wameafikiana Mafakihi kwamba kuwinda ndani ya Haram haijuzu kwa aliye katika Ihram na asiye katika Ihram. Ama nje ya Haram inajuzu kuwinda kwa asiyekuwa katika Ihram. Lau atachinja aliye katika Ihram windo basi litakuwa ni mfu ulio haramu kuliwa na watu wote.

Imeelezwa katika Kitab Fiqhu Sunna cha Sayyid Sabiq kwamba mpaka wa Haram ya Makka kwa upande wa Kaskazini ni sehemu inayaoitwa Tani'm, kilomita 6 kutoka Makka. Upande wa kusini ni mahali panapoitwa Ardhah, kilomita 12. Upande wa Mashariki ni Ja'rana kilomita 15.

Na miongoni mwenu atakayemua kwa kusudi, basi malipo (yake) yatakuwa ni mfano wa aliyemuua katika wanyama wa kufugwa, kama watakavyo hukumu waadilifu wawili miongoni mwenu. Mnyama apelekwe Al-K'aaba (kama sadaka); au kutoa kafara kwa kuwalisha masikini au badala ya hayo ni kufunga.

Mwenye kuwa katika Ihram akiuwa, au akiwa hayuko katika Ihram, lakini ameuwa ndani ya haramu, basi ikiwa mnyama aliyemuuwa ana mfano katika aina tatu za wanyama wa kufugwa - Ngamia, Ngombe, Kondo au Mbuzi, basi atakuwa na hiyari ya kuchinja mfano wa mnyama aliyeuliwa na mtoe sadaka; au kutoa thamani ya mnyama anyefanana na aliyemuua. Anunue chakula na kukitoa sadaka kwa masikini kila masikini vibaba viwili, kilogram 1.6 takriba. Wengine wamesema kuwa atatoa kibaba kimoja, au afunge kwa kila vibaba viwili siku moja, au kwa kila kibaba kimoja kulingana na kauli nyingine.

Maana ya "Kama watakavyohukumu waadiifu wawili" ni kushuhudia watu wawili waadilifu, kuwa mnyama huyu wa kufuga ni sawa na mnyama aliyeuawa.

Maana ya "Mnyama apelekwe Al-Kaaba" ni kuchinjwa huyo mnyama jirani ya Al-Kaaba na kutolewa nyama yake kwa masikini.

Ikiwa hakupata mfano katika aina zile tatu za wanyama wa kufugwa, basi atatoa kima cha mnyama mwingine wa kufugwa na anunue chakula na kukitoa sadaka; au kufunga, kwa ufafanuzi uliotangulia.

Ili aonaje ubaya wa jambo lake.

Kuwinda katika Haram au katika hali ya Ihram ni kuvunja mwiko wa Mwenyezi Mungu, kwa hiyo ndio akaadhibiwa mwindaji kwa kafara hiyo iliyotajwa. Maana ya ubaya wa jambo lake, ni mwisho wa kitendo chake kibaya.

Mwenyezi Mungu amekwishayasamehe yaliyopita ; ya kuwinda kabla ya kuharamishwa.Na atakayerudia kuwinda,Mwenyezi Mungu atampa adhabu kwa kung'ang'ania kwake dhambi.

Mmehalalishiwa kuvua baharini na chakula chake, kwa manufaa yenu na kwa wasafiri.

Dhamiri katika chakula chake inarudia bahari, kwa sababu mna vinavyoliwa visivyo vuliwa. Inawezekana kuwa dhamiri inarudia kinachovuliwa; na maana yawe Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehalalisha kuvua na kula vilevile. Makusudio ya wasafiri ni wale wasiokuwa katika Ihram.

Na mmeharamishiwa kuwinda bara maadamu mko katika Ihram.

Yaani kuvua baharini ni halali kwa hali yoyote. Imam Jafar Assadiq(a.s) anasema:Usihalalishe chochote katika mawindo - ya bara - ukiwa katika Ihram. Wala usipokuwa katika Ihram pia usimfahamishe aliye katika Ihram au asiye katika Ihram, akawinda na wala usimwonyeshe kwani katika hayo kuna fidia kwa mwenye kufanya makusudi.

Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

Yaani jitahidi ni katika kumtii na kutafuta radhi zake, ili awalipe wema siku ya ufufuo.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿جَعَلَ اللَّـهُ الْكَعْبَةَ الْبَيْتَ الْحَرَامَ قِيَامًا لِّلنَّاسِ وَالشَّهْرَ الْحَرَامَ وَالْهَدْيَ وَالْقَلَائِدَ ذَٰلِكَ لِتَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَأَنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ﴾

97.Mwenyezi Mungu amefanya Al-Kaaba nyumba tukufu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja na vigwe; hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliyomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

﴿اعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ وَأَنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ﴾

98. Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwingi wa kurehemu.

﴿مَّا عَلَى الرَّسُولِ إِلَّا الْبَلَاغُ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ مَا تُبْدُونَ وَمَا تَكْتُمُونَ﴾

99.Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu, na Mwenyezi Mungu anajua mnayo yadhihirisha na mnayoyaficha.

NYUMBA TAKATIFU

Aya 97-99

MAANA

Mwenyezi Mungu ameifanya Al-Kaaba, nyumba takatifu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitakatifu na wanyama wa kuchinja na vigwe.

Kisimamo cha watu; yaani mahali pa ibada na ibada za Hijja. Miezi mitakatifu ni ile minne Rajab, Dhul-qa'da, Dhul-Hijja na Muharram[5] Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameharamisha kupigana huko na katika miezi hiyo; ispokuwa kutetea nafsi au mali. Anasema:

﴿وَلَا تُقَاتِلُوهُمْ عِندَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ حَتَّىٰ يُقَاتِلُوكُمْ فِيهِ﴾

"Wala msipigane nao karibu na Msikiti Mtakatifu mpaka wakupigeni huko" (2:191) Na akasema tena:

﴿الشَّهْرُ الْحَرَامُ بِالشَّهْرِ الْحَرَامِ وَالْحُرُمَاتُ قِصَاصٌ فَمَنِ اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ ﴾

"Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu; na vitu vitakatifu vina kisasi. Basi wanaowachokoza, pia nanyi wachokozeni kwa kadiri walivyowachokoza" (2:194)

Mnyama wa kuchinja, ni wale wanaochinjwa Makka. Na kigwe ni ukambaa anaofungwa nao mnyama wa kuchinja kuwa ni alama ya kufahamisha kuwa ni wa Al-Kaaba ili asitaradhiwe na yeyote. Kwa hiyo kuunganisha vigwe kwa wanyama ni kuunganisha maalum katika ujumla.

Makusudio ya kutaja chinjo pamoja na Nyumba takatifu na miezi mitakatifu ni kwamba mnyama wa kuchinja inapasa awe salama yeye na anayemchunga, kwa sababu yeye anakusudia Haram tukufu.

Bali ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewapa amani ndege na wanyama walio katika haramu yake; isipokuwa mwewe, kipanga, kunguru, panya, nge, mbwa anayeuma watu na kila tunayemuona anaudhi.

Hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa kila kitu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha miko ya Al-Kaaba, miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja, anaashiria kwamba hekima ya sharia hii ni kuwa watu wajue kwamba Mwenyezi Mungu anajua ufafanuzi wa mambo katika ardhi na katika mbingu; na ambayo yana masilahi kwa watu katika dini yao na dunia yao.

Kuna masilahi gani makubwa zaidi ya usalama wa maisha ya mtu na mali yake ijapokuwa ni kwa kipindi fulani. Tumeyaona mataifa makubwa yanayotwangana, wakati huu, yakiafikiana kuwa baadhi ya miji iwe ni maeneo maalumu ya amani, haijuzu kwa taifa linalopigana kuishirikisha katika vita wala kuweka vituo vya kijeshi katika ardhi hiyo au kupita wanajeshi wake.

Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekutanisha adhabu na rehema na maghufira ili mja awe anahofia adhabu yake na kutaraji rehema yake. Kwa sababu mja, akiwa na hofu atajiepusha na maasi na akiwa na matarajio atajitahidi katika twaa.

Razi anasema: "Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja kuwa yeye ni mkali wa kuadhibu, kisha akafuatishia kwa wasifu wa rehema na maghufira. Na huu ni uzinduzi juu ya undani kuwa kupatikana kiumbe ni kwa ajili ya rehema. Na kwa dhahiri ni kuwa mwisho hauwi ila kwa rehema" Hiyo ni kweli kabisa.

Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu.

Hatakiwi jingine zaidi ya hilo, ambapo hapana udhuru baada ya kufikisha kwa anayepuuza na kupetuka mpaka. Ama hisabu na adhabu hiyo ni juu ya Mwenyezi Mungu pekee Yake. Mwenyezi Mungu anasema:

"Hakika ni juu yako kufikisha tu, na ni juu yetu hisabu." (13:40)

Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyadhihirisha katika kauli na vitendo na mnayoyaficha. Haya ni makemeo kwa anayeinyamazia haki, na hasa yule anayeifanyia biashara kwa kujipanua na jina la dini na la nchi.

﴿قُل لَّا يَسْتَوِي الْخَبِيثُ وَالطَّيِّبُ وَلَوْ أَعْجَبَكَ كَثْرَةُ الْخَبِيثِ فَاتَّقُوا اللَّـهَ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ﴾

100.Sema: Hawi sawa habithi na mwema, hata ukikupendeza wingi wa habith, Basi mcheni Mwenyezi Mungu enyi wenye akili ili mpate kufaulu.

WINGI WA MWOVU

Aya 100

MAANA

Aya hii inarudufu Aya ile isemayo:

﴿لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ﴾

"Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi, watu wa Peponi ndio wenye kufuzu" (59:20)

Wingi wa habithi ni anayoyamiliki miongoni mwa jaha na mali. Mwenye akili hawezi kumweka sawa habithi, na mwema hata kama ana mali nyingi na jaha kubwa. Kwa sababu jaha na mali hazimfanyi mwovu kuwa mwema; wala ufakiri na udhaifu haumfanyi mwema kuwa mwovu.

Mtu habith katika kipimo cha dini ni yule anayeasi hukumu za Mwenyezi Mungu katika kitabu chake na Sunna za Mtume wake. Na katika desturi ya watu ni yule wanayemhofia kwa shari yake na wasiyemwamini kwa jambo lolote na kutomsadiki katika kauli au vitendo vyake. Kimsingi ni kwamba mwenye sifa hizi, ni mbaya pia mbele ya Mwenyezi Mungu. Mtume wa Mwenyezi Mungu anasema:"Utukufu zaidi wa imani ni kuaminiwa na watu." Ama mtu mwema ni yule aliye kinyume cha mtu habithi katika sifa zake zote.

JE RIZIKI NI BAHATI AU MAJAALIWA?

Unaweza kuuliza : Ikiwa habithi anachukiwa na Mwenyezi Mungu na mwema anaridhiwa na Mwenyezi Mungu, kwa nini basi habithi anafaulu katika maisha haya na kuneemeshwa kwa jaha na utajiri, na mwema anaanguka na wala hapati matakwa yake?

Jibu : Maisha yana desturi na kanuni zinazokwenda nayo, na hazigeuki kwa hali yoyote ile. Kwa sababu hisia na uoni unakataa mkorogano katika ulimwengu. Desturi na kanuni hizi ni katika matengenezo ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: Kwa sababu yeye ni muumbaji wa asili na vilivyomo katika asili.

Kimsingi ni kuwa desturi ya kawaida ya tabia inakataa kuwa mali, afya na ilimu, vishuke tu kutoka mbinguni. Isipokuwa vitu hivi na mfano wake vinakuja kwa njia zake na sababu zake za kimaumbile. Elimu inatokana na kujifundisha, afya inatokana na lishe na kinga, na mali inatokana na kazi. Kwa hiyo mwenye kujifunza hujua, mwenye kujiepusha na visababishi vya maradhi husalimika, mwenye kujinyonga atakufa tu; awe mwema au mwovu, mumin au kafiri.

Kwa hiyo wema au imani hauoteshi ngano wala hauponeshi ugonjwa wala haumfanyi asiyejua kuwa mjuzi, Yote haya na mfano wake yanakwenda kwa desturi ya tabia na desturi ya tabia inakwenda kwa matakwa ya Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka.

Kwa sababu yeye ndiye aliyejaalia kujifundisha ndio sababu ya elimu na kujikinga ndio sababu ya afya na kupanda kuwa ndio sababu ya kuvuna. Yeye ni Muumba wa kila kitu na kwake yeye ni mwishilio wa kila jambo.

Ndiyo! kuchuma mali kuna njia nyingi, na milango mingi, nyingine Mwenyezi Mungu amezihalalisha na nyingine akaziharamisha. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehalalisha biashara, kilimo na viwanda; na akaharamisha riba, utapeli, rushwa, kupora na ulanguzi.

Mwenye kuchuma mali kwa njia ya halali hunasibishwa chumo lake kwake, kwa sababu yeye amejitahidi na kufanya bidii kuitafuta, na vilevile hunasabishwa kwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu yeye ndiye aliyepitisha sababu hizi na kuzihalalisha kwa kila azitakaye, awe mwema au mwovu.

Ama mwenye kuchuma mali kwa njia za haramu; kama vile riba na unyang'anyi; chumo lake litanasibishwa kwake na kwa hali aliyoitumia, wala halinasibishwi kwa Mwenyezi Mungu, kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu ameharamisha njia hizi kwa mwema na mwovu.

Utasema : Haya yote ni kweli, lakini hayajibu swali wala hayatatui mushkeli. Tumewahi kumuona mwema na mwovu wote wakifuata njia za sharia za riziki, na kuzitafuta riziki kwa njia zile alizozihalalisha Mwenyezi Mungu na kuziharamisha, lakini pamoja na hayo, riziki inakuwa zaidi kwa mwovu aliye habith na kuwa dhiki kwa mwema, pengine huyu mwema ametoa juhudi maradufu ya yule mwovu, bali mara nyingine riziki humjia mwovu bila ya kutazamia wala maandalizi au juhudi, na inazuilika kumwendea mwema anapoitazamia na kuifanyia maandalizi na juhudi?

Jibu : Baadhi ya watu wanakimbilia kulifasiri hilo kwa kusema ni sadfa au bahati. Hakuna kinachofahamika kutokana na maelezo hayo zaidi ya kushindwa kwao kutoa tafsiri sahihi. Vinginevyo wasingelikimbilia kwenye maelezo ya kubahatisha tu.

Kwa hiyo sisi tunapinga Sadfa na bahati na tunaamini kwa imani ya mkato kwamba kuna chaguo la juu linajiingiza kwa sababu tusizozijua. kwa vile elimu katika masuala hayo na mfano wake, bado ni changa. Na kushindwa kwa elimu hakumaanishi kuwa kitu hakiko. Imani yetu hii inatiliwa mkazo na kauli zake Mwenyezi Mungu zifuatazo:

﴿وَاللَّـهُ فَضَّلَ بَعْضَكُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ فِي الرِّزْقِ﴾

"Na Mwenyezi Mungu amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine katika riziki" (16:71)

﴿اللَّـهُ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ﴾

"Mwenyezi Mungu hukunjua riziki kwa amtakaye na huidhikisha (13:26) Ay a hii imekuja kwa herufi zake katika 17:30, 28:82, 29:62, 30:37, 34: 36, 34: 39, 39:52, 42:12.

Kwa hiyo basi aliyesema au anayesema: Mwenyezi Mungu amemtajirisha fulani kwa kuwa yeye ni mwema basi atakuwa anazungumza mantiki ya Firaun na kupima kwa kipimo cha Shetani. Hekima yake Mwenyezi Mungu Mtukufu imetaka kumlipa mwema malipo mazuri na kumwadhibu mwovu katika akhera inayobakia sio katika hii dunia inayokwisha. Hii ni Nyumba ya matendo na ile ni Nyumba ya Hisabu. Zaidi ya haya ni kuwa wingi wa mali wa mwovu huenda ukawa ni balaa kwake na sababu ya kuadhibiwa kwake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ذَرْهُمْ يَأْكُلُوا وَيَتَمَتَّعُوا وَيُلْهِهِمُ الْأَمَلُ فَسَوْفَ يَعْلَمُونَ﴾

"Waache wale na wafurahi na iwazuge tamaa, watakuja jua." (15:3)

﴿يَتَمَتَّعُونَ وَيَأْكُلُونَ كَمَا تَأْكُلُ الْأَنْعَامُ وَالنَّارُ مَثْوًى لَّهُمْ﴾

"Hujistarehesha na hula kama walivyo wanyama, na moto ndio makazi yao." (47:12)

Kwa ufupi ni kwamba riziki inategemea mambo mawili. Kuhangaika na matakwa ya Mwenyezi Mungu. Asiyehangaika ataishi omba omba; na mwenye kuhangaika Mwenyezi Mungu humruzuku kutokana na bidii yake, akitaka humpa nyingi na akitaka humpa chache.

Uhakika huu umo katika maumbile ya binadamu na anaufanya bila ya kujitambua. Mfanya biashara humwomba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amruzuku kupata soko zuri la bidhaa zake na watu wazikubali. Mkulima anamwomba Mungu aiteremshie mimea yake mvua; wala hamuombi kumwoteshea mimea bila ya mvua.

Mimi hapa namwomba Mwenyezi Mungu ampe tawfiq mwanangu katika masomo yake na kufaulu mtihani; wala si mwombi akipe mawazo chuo kikuu kimpatie shahada bila ya kusoma na kufanya mtihani. Iko methali isemayo: Mgaagaa na upwa hali wali mkavu.

Pengine inawezekana mahangaiko yasiambulie kitu, lakini pamoja na hayo inatakikana kupanga mipango na kuongeza juhudi. Kwa sababu kuongeza juhudi, kutumia mipango, na kuvumilia tabu ni sababu ya matakwa ya kufaulu kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَسْأَلُوا عَنْ أَشْيَاءَ إِن تُبْدَ لَكُمْ تَسُؤْكُمْ وَإِن تَسْأَلُوا عَنْهَا حِينَ يُنَزَّلُ الْقُرْآنُ تُبْدَ لَكُمْ عَفَا اللَّـهُ عَنْهَا وَاللَّـهُ غَفُورٌ حَلِيمٌ﴾

101.Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza. Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa. Mwenyezi Mungu ameyasamehe hayo. Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira Mpole.

﴿قَدْ سَأَلَهَا قَوْمٌ مِّن قَبْلِكُمْ ثُمَّ أَصْبَحُوا بِهَا كَافِرِينَ﴾

102.Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

MSIULIZEULIZE MAMBO

Aya 101-102

MAANA

Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza.

Kauli yake Mwenyezi Mungu 'Msiulize' inaishiria kuwa baadhi ya Masahaba walikuwa waking'ang'ania kuuliza mambo yasiyokuwa na dharura yoyote kuyajua na huenda jibu lake likawaudhi waulizaji. Kuna riwaya isemayo kuwa mtu mmoja alimuuliza Mtume(s.a.w.w) : "Ni nani baba yangu?" Mtume akamwambia, "baba yako ni Fulani" Mwingine akauliza "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Baba yangu yuko wapi? Mtume akajibu: "Yuko motoni," ndipo ikashuka Aya hiyo.

Riwaya nyingine inasema kuwa Mtume alisema: "Mwenyezi Mungu amewafaradhishia kuhiji, basi hijini." Wakauliza: "Kila mwaka ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Mtume akanyamaza. Wakarudia kuuliza, akasema La; lau ningelisema naam, ingelikuwa wajib." Ndipo ikashuku Aya hii. Riwaya hii ndiyo yenye nguvu kuliko ile ya kwanza.

Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa.

Yaani msijikalifishe kuuliza mambo ila baada ya kuteremshwa Qur'an. Mtakapoanza kuuliza Mtume(s.a.w.w) atawadhirishia mliyokuwa mkiyauliza.

Kwa hali hii, inatubainikia kuwa riwaya ya Hija ndiyo yenye nguvu katika sababu ya kushuka Aya, kuliko riwaya ya kuuliza mababa na wahenga wa Masahaba. Kwa sababu Qur'an inaanza kuleta itikadi na sharia na wala sio kuanzia kwa mababa na mababu wa Masahaba. Katika Hadith imeelezwa:"Hakika Mwenyezi Mungu ameweka mipaka msiikiuke; amewafaradhishia faradhi msizipoteze; ameharamishia vitu msivifanye; na ameacha vitu vingine si kwa kusahau, lakini ni kwa kuwahurumia, basi vikubalini wala msivifanyie utafiti".

Mwenyezi Mungu amesamehe hayo

Yaani maswali yenu yaliyotangulia, kwa hiyo msiyarudie. Imesemekana kuwa maana yake ni amezuia kutaja vitu mlivyoviulizia, basi nanyi jizuieni wala msijikalifu kuviulizia. Tafsir zote mbili zina uwezekano hazikataliwi na dhahiri ya tamko.

Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mpole.

Humsamehe mkosaji akikosea tena.

Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwakataza kuuliza mambo wasiyokuwa na haja nayo, anawapigia mfano wa watu waliokuwa kabla yao, waliuliza wakang'ang'ania kuuliza. Walipobainishiwa na Mwenyezi Mungu walichukia wakaasi na wakastahiki adhabu. Lau wangeliacha kuuliza ingelikuwa bora kwao.

Wafasiri wamerefusha maneno katika kubainisha makusudio ya watu waliouliza, kisha wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza, lakini Aya haikubainisha. Pamoja na hivyo, tunaweza kusema kuwa watu waliouliza wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza ni wana wa Israil, kwa sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu akiwasimulia:

﴿فَقَدْ سَأَلُوا مُوسَىٰ أَكْبَرَ مِن ذَٰلِكَ فَقَالُوا أَرِنَا اللَّـهَ جَهْرَةً ﴾

"Hakika walimtaka Musa makubwa kuliko hayo, Walisema: Tuonyeshe Mwenyezi Mungu waziwazi" (4:153)

﴿مَا جَعَلَ اللَّـهُ مِن بَحِيرَةٍ وَلَا سَائِبَةٍ وَلَا وَصِيلَةٍ وَلَا حَامٍ وَلَـٰكِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا يَفْتَرُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ وَأَكْثَرُهُمْ لَا يَعْقِلُونَ﴾

103.Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami; Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

﴿وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ تَعَالَوْا إِلَىٰ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَإِلَى الرَّسُولِ قَالُوا حَسْبُنَا مَا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا أَوَلَوْ كَانَ آبَاؤُهُمْ لَا يَعْلَمُونَ شَيْئًا وَلَا يَهْتَدُونَ﴾

104.Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama baba zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَيْكُمْ أَنفُسَكُمْ لَا يَضُرُّكُم مَّن ضَلَّ إِذَا اهْتَدَيْتُمْ إِلَى اللَّـهِ مَرْجِعُكُمْ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ﴾

105.Enyi mlioamini! Jiangalie nafsi zenu. Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka. Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu. Atawaambia yale mliyokuwa mkiyatenda.

HAKUNA BAHIRAWALA SAIBA

Aya 103-105

MAANA

Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami.

Bahira, ni ngamia aliyetobolewa masikio, watu wa wakati wa Jahilia walikuwa wakifanya hivyo, ikiwa ngamia atazaa mimba kumi ; na inasemekana ni mimba tano. Wanamwacha bila ya kutumiwa na mtu yoyote. Saiba ni ngamia waliyemwekea nadhiri kwa waungu, na wana mwacha akijilisha mwenyewe popote bila ya kufungwa wala kuwa na mchungaji sawa na Bahira.

Wasila ni mbuzi anayezaa mtoto wa kiume na wa kike pamoja. Desturi yao ilikuwa kama akizaa mume wanamfanya ni wa waungu na akizaa mke ni wao. Iwapo atazaa mume na mke pamoja, hawamchinji mume wakisema kuwa ameunganishwa na dada yake. Hami ni dume aliyezalisha mimba kumi, wanamwacha hazuiliwi na maji wala malisho, wakisema ameuhami mgongo wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha kwamba yote hayo hayamo katika dini, na kwamba dume, jike na mbuzi, vyovyote wanavyofanyiwa, wanabakia na uhalali wake kama walivyokuwa mwanzo na wala hawaharamishwi na porojo hizo.

Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

Watu wa kijahilia walikuwa wakikubali kuweko kwa muumba kwa dalili kwamba wao wamenasibishia uharamu wa Hami, Saiba, Bahira na Waswila, lakini pamoja na hayo Mwenyezi Mungu amewanasibishia ukafiri.

Kwa sababu wao wamemnasibishia uharamu kwa uwongo na uzushi. Kwa hiyo, basi kila anayemnasibishia Mwenyezi Mungu na yasiyokuwa na dalili ya Kitab wala Hadith ya Mtume wake basi huyo ni kafir kwa sharti ya kutegemea kumnasibishia Mungu, huku akijua kutokuwepo dalili.

Hii, kwa lugha ya watu wa sharia, huitwa Bid'a (uzushi). Kuna Hadithi isemayo: "Kila bid'a ni upotevu na kila upotevu ni motoni".

Ilivyo ni kuwa kufaradhia huko kuko mbali na hali halisi ilivyo, Ni nani anayemnasibishia hukumu Mwenyezi Mungu huku akijua kuwa hakuna dalili. Pengine anaweza akadhani ni dalili, lakini kumbe sio dalili.

Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: "Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama babu zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

Razi anasema: "Maana yanajulikana, nayo ni jibu la kuwapinga watu wa Taqlid (kufuata)". Tumezungumzia kuhusu Taqlid katika Juz.2 (2:170)

Enyi mlioamini! Jiangalieni nafsi zenu, Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka, Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu.

Razi ametaja njia nane za kufasiri Aya hii. Mmoja wa wafasiri wapya ameandika kurasa 33. Lililowafanya wawili hawa na wengineo kurefusha mambo hivi ni kuwa kuamrisha mema ni wajibu na dhahiri ya Aya inafahamisha kutokuwa wajib na kwamba ni juu ya mtu kujishughulikia mwenyewe. Ama wengine wana majukumu yao juu ya nafsi zao wala si wajibu kwa yoyote kuiongoza au kuikanya nafsi ya mwingine.

Ilivyo tafsir ya Aya hii ni kwamba, ni juu ya mtu kuamrisha mema. Kuamrisha kwake kukinufaisha basi hayo ndiyo yanayotakikana. Vinginevyo basi atakuwa ametekeleza lile aliloamrishwa wala hautamdhuru upotevu wa aliyepotea.

Mwenye jukumu baada ya kuamrisha ni yule aliyepotea na wala sio mwamrishaji. Tafsir hii imetilia mkazo wajibu wa kuamrisha mema na sio kupinga.


3

4

5

6

7

8

9