TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA 0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 13163
Pakua: 2194


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 16 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 13163 / Pakua: 2194
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَعْرِفُونَهُ كَمَا يَعْرِفُونَ أَبْنَاءَهُمُ الَّذِينَ خَسِرُوا أَنفُسَهُمْ فَهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ﴾

20.Wale tuliowapa Kitab wanamjua kama wanavyowajua wana wao, Wale ambao wamezitia hasarani nafsi zao hawaamini.

﴿وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَىٰ عَلَى اللَّـهِ كَذِبًا أَوْ كَذَّبَ بِآيَاتِهِ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الظَّالِمُونَ﴾

21.Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule amzuliaye Mwenyezi Mungu uwongo, Au azikadhibishaye ishara zake? Hakika madhalimu hawatafaulu.

﴿وَيَوْمَ نَحْشُرُهُمْ جَمِيعًا ثُمَّ نَقُولُ لِلَّذِينَ أَشْرَكُوا أَيْنَ شُرَكَاؤُكُمُ الَّذِينَ كُنتُمْ تَزْعُمُونَ﴾

22.Na siku tutakapowakusanya wote, kisha tutawaaambia wale walioshirikisha: Wako wapi washirikishwa wenu mliokuwa mnadai?

﴿ثُمَّ لَمْ تَكُن فِتْنَتُهُمْ إِلَّا أَن قَالُوا وَاللَّـهِ رَبِّنَا مَا كُنَّا مُشْرِكِينَ﴾

23.Kisha hautakuwa udhuru wao ila kusema Wallahi, Mola wetu! Hatukuwa washirikina.

﴿انظُرْ كَيْفَ كَذَبُوا عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ وَضَلَّ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَفْتَرُونَ﴾

24.Angalia jinsi wanavyojisemea uwongo wenyewe, Na yamepotea waliyokuwa wakiyazua.

WANAMFAHAMU KAMAWANAVYO WAFAHAMU WANAWAO

Aya ya 20 - 24

MAANA

Wale tuliowapa Kitab wanamjua kama wanavyowajua wana wao. Waliopewa Kitab ni Mayahudi na Wakristo, Dhamiri ya wanamjua inamrudia Muhammad(s.a.w.w) . Aya hii inawakabili maulama wa watu wa Kitab kwamba wao wanamjua vizuri Mtume wa mwisho, kama wanavyowajua wana wao, lakini wao wanaficha yale wanayoyajua. Maana haya yamekaririka katika Aya kadhaa, zikiwemo hizi zifuatazo:

﴿الَّذِينَ يَتَّبِعُونَ الرَّسُولَ النَّبِيَّ الْأُمِّيَّ الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ﴾

"Ambao wanamfuata Nabii asiyesoma wala kuandika ambaye wanamwona ameandikwa kwao katika Tawrat na Injil" (7:157)

﴿أَوَلَمْ يَكُن لَّهُمْ آيَةً أَن يَعْلَمَهُ عُلَمَاءُ بَنِي إِسْرَائِيلَ﴾

Je, haikuwa ishara kwao kwamba wanayajua haya maulama wa wana wa Israil? (26:197)

Yamekwishapita maelezo kwa ufafanuzi katika Juz. 2 (2:146) na Juz. 4 (4:164). Si lazima kwa watu wa Kitab, katika kuujua ukweli wa Muhammad(s.a.w.w) , wakute jina lake limeandikwa kwao katika Tawrat na Injil. Kila mwenye kuusoma Uislamu kwa somo sawa sawa na upekuzi, ataamini kwa imani isiyokuwa na tashwishi yoyote kwamba Uislamu ni haki na ukweli.

Na mawili hayo (haki na ukweli) ndiyo johari za Uislamu, nguzo yake na lengo lake kutokana na neno Lailaha illa Ilah (Hakuna Mungu isipokuwa Allah) ambalo linamaanisha usawa baina ya watu, kumpa mtu msimamo wa misingi ya kufanya amali na ikhlasi na wala sio kwa misingi ya mali, jaha na nasabu. Na vilevile mshikamano na majukumu ya kila kiongozi kwa wachini wake katika mwito wa amani na usalama, maendeleo na utulivu usiokuwa na mwisho.

Wale ambao wamezitia hasarani nafsi zao hawaamini.

Imepita, punde tu Tafsir yake katika Aya 12 ya Sura hii.

Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule amzuliaye Mwenyezi Mungu uwongo.

Makusudio ya dhulma hapa ni Ukafiri. Kwa sababu kila anayemzulia Mwenyezi Mungu uwongo, basi yeye ni kafiri. Hakuna tofauti yoyote baina ya anayemshirikisha na yule mwenye kugeuza hukumu yoyote katika hukumu zake kwa makusudi na kujua; na yule mwenye kudai unaibu wa maasum au kuwaombea viumbe haki, na hali anajua kuwa yeye ni mzushi na mwongo. Wote hawa ni makafiri waovu kwa Ijmai (kongamano), Kitab na Hadith.

Au azikadhibishaye ishara zake? Hakika madhalimu hawatafaulu.

Jumla iliyotangulia imeashiria yule anayeleta yasiyokuwepo; kama mwenye kumfanyia Mwenyezi Mungu washirika au mtoto. Na jumla hii inaashiria yule mwenye kukanusha vilivyopo, kama vile anayemkana

Mwenyezi Mungu kabisa. Hukumu ya wote wawili ni moja, kila mmoja wao ni dhalimu:

﴿مَا لِلظَّالِمِينَ مِنْ حَمِيمٍ وَلَا شَفِيعٍ يُطَاعُ﴾

"Madhalimu hawana rafiki mpenzi wala muombezi anayetiiwa" (40:18) "Na siku tutakapowakusanya wote, kisha tutawaambia wale walioshirikisha: Wako wapi washirikishwa wenu mliokuwa mnadai" Wanaomwamini Mwenyezi Mungu wako aina mbili: Kuna wale wanaoamini uungu wake na kuwa ni mmoja tu. Hawa wanaitwa wanaompwekesha Mungu (watu wa Tawhid). Na kuna wale wanaoamini uungu wake na uungu mwingine. Hawa ndio wale walioharibu imani yao kwa mchanganyiko huu; na wakawa sawa na wale wanaomkana Mwenyezi Mungu. Kwa sababu kumjaalia Mwenyezi Mungu mfano maana yake hasa ni kumkana Mwenyezi Mungu kabisa. Kwani ilivyo nikuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) hana mshabaha wala mfano:

"Hakuna kama mfano wake kitu chochote." (42:11)

Mwenyezi Mungu atawakabili washirikina na swali hili (wako wapi washirikishwa mliokuwa mnadai na mkiwataka msaada, kama mnavyomtaka msaada Mwenyezi Mungu) kwa njia ya kutahayariza na kukaripia, na wala sio kwa njia ya kuhakikisha.

Unaweza kuuliza : kwa nini Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema wako wapi washirikishwa wenu na wala hakusema wako wapi washirikishwa wangu, pamoja na kuwa makafiri ndiyo waliosema kuwa Mungu ana washirika na sio wao?

Jibu : Ni kwa kuwa wao ndiyo wako karibu zaidi na mnasaba huo; kwani wao ndio waliozusha ushirikina ambao hauna athari kabisa.

Kisha hautakuwa udhuru wao ila kusema Wallahi, Mola wetu! Hatukuwa washirikina.

Makusudio ya udhuru wao ni udhuru wao wa kushirikisha na kuabudu mizimu. Maana ni kuwa mwisho wa ushirikina waliozusha ni kiapo chao cha uovu kwamba wao hawakuwa washirikina.

Unaweza kuuliza : Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwasimulia watu hao: 'Wallahi Mola wetu! Hatukuwa washirikina' inapingana na kauli yake yake."Wala hawatamficha Mwenyezi Mungu na mazungumzo (yao)" (4:42)

Zaidi ya hayo ni kuwa inajulikana kuwa mtu hawezi kusema uongo Siku ya Kiyama.

Jibu : Katika Kiyama kutakuwa na vituo kadhaa, baadhi yake mtu ataweza kukana na ambapo katika kituo hicho miguu yake na mikono yake haitamtolea ushahidi wa yale aliyokuwa akiyafanya. Kwenye kituo hicho ndipo huchukuliwa kauli yake Mwenyezi Mungu: 'Wallahi Mola wetu! Hatukuwa washirikina' Na katika kituo kingine, atakiri ambapo hapatakuwa na nafasi ya kukana. Hapo ndipo huchukuliwa kauli yake Mwenyezi Mungu: "Wala hawataweza kumficha Mwenyei Mungu neno lolote" Ama kauli ya kuwa mtu atashindwa kabisa kusema uwongo siku ya Kiyama, inakanushwa na Aya isemayo:

﴿يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيَحْلِفُونَ لَهُ كَمَا يَحْلِفُونَ لَكُمْ وَيَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ عَلَىٰ شَيْءٍ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْكَاذِبُونَ﴾

"Siku atakayowafufua Mwenyezi Mungu wote; wamuapie kama wanavyoapa kwenu, na watadhani kwamba wamepata kitu. Kwa hakika hao ndio waongo hasa" (58: 18)

Swali la pili linatokana na jibu la swali la kwanza nalo ni kuwa: ikiwa mtu ataweza kusema uwongo kesho, bali hata kuapa, kama ilivyo katika maisha haya ya duniani. Basi kuna wajihi gani kuita akhera nyumba ya ukweli na kuiita nyumba yetu hii (dunia) nyumba ya uwongo?

Jibu : Makusudio ya kutofautisha huku ni kwamba uwongo hapa duniani unaweza ukamletea mtu manufaa au kumkinga na madhara, Ama huko akhera hautafaa chochote. Kwa maneno mengine, kushindwa kusema uwongo, ni kitu kingine na kuweza kusema bila ya manufaa ni kitu kingine.

Angalia jinsi wanavyojisemea uwongo wenyewe.

Msemo unaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) na makusudio yake ni kwa wote, nako ni kusataajabu kutokana na kukana kwao ushirikina na hali wamekufa juu ya ushirikina. Kila mwenye kukana jambo alilonalo au kudai asiyokuwa nayo kwa makusudi, basi amejidaganya mwenyewe, Mwenyezi Mungu na watu:

Na yamepotea waliyokuwa wakiyazua.

Hiyo inaungana na 'wanavyojisemea uwongo.' Maana yake ni angalia Ewe Muhammad vipi yamewapotea washirikina yale waliyokuwa wakiyatarajia kuwa yatawasaidia na kuwaombea.

﴿وَمِنْهُم مَّن يَسْتَمِعُ إِلَيْكَ وَجَعَلْنَا عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ أَكِنَّةً أَن يَفْقَهُوهُ وَفِي آذَانِهِمْ وَقْرًا وَإِن يَرَوْا كُلَّ آيَةٍ لَّا يُؤْمِنُوا بِهَا حَتَّىٰ إِذَا جَاءُوكَ يُجَادِلُونَكَ يَقُولُ الَّذِينَ كَفَرُوا إِنْ هَـٰذَا إِلَّا أَسَاطِيرُ الْأَوَّلِينَ﴾

25.Na miongoni mwao wako wanaokusikiliza, na tumezitia pazia nyoyo zao wasije kuyafahamu na mna uziwi masikioni mwao, Na wakiona kila Ishara hawaiamini. Hata wakikujia kujadaliana nawe wanasema waliokufuru: Hizi si chochote isipokuwa ni ngano za watu wa kale.

﴿وَهُمْ يَنْهَوْنَ عَنْهُ وَيَنْأَوْنَ عَنْهُ وَإِن يُهْلِكُونَ إِلَّا أَنفُسَهُمْ وَمَا يَشْعُرُونَ﴾

26.Nao wanamkatazia na wenyewe wanajitenga naye. Na hawaangamizi ila nafsi zao na hawatambui.

NYOYO ZAO ZINA PAZIA

Aya 25 - 26

MAANA

Na miongoni mwao wako wanaokusikiliza, na tumezitia pazia nyoyo zao wasije kuyafahamu na mna uziwi masikioni mwao.

Mwenyezi Mungu anamwambia Mtume wake katika Aya hii, baada ya kumwamrisha kuwambia hoja zinazowasimamia, Maana ni kuwa kundi katika hawa wapinzani wanamsikiliza Mtume, nao wanasoma Qur'an, lakini wao hawanufaiki nayo wala hawanufaiki na dalili na hoja nyingine- zo.

Kwa sababu wao tangu mwanzo waling'anga'ania inadi na kiburi, mpaka kung'angania huko kukapofua akili zao zisione haki na kukatia uziwi kwenye masikio yao.

Unaweza kuuliza : Dhahiri ya Aya inaonyesha kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyezipofua nyoyo zao akatia uziwi masikio yao. Kwa nini basi wastahiki shutuma na adhabu na hali ya kuwa wamelazimishwa hawana hiyari?

ibu: Kwa vile nyoyo za wapinzani hazikuitambua Qur'an na kunufaika nayo, na masikio yao hayakuisikiliza kwa usikizi wa kufahamu na kuzingatia, imesihi kusema, kimajazi, kwamba nyoyo zao zimefumba na katika masikio yao mna uziwi.

Na kwa vile Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye aliyeumba nyoyo na masikio, imesihi kunasibisha upofu na uziwi kwake yeye kimajazi vilevile.

Ama kulingana na hali halisi ilivyo ni kuwa washirikina ndio wenye jukumu. Kwa sababu wao waliipinga haki kwa kutaka wenyewe. Yamekwishatangulia maelezo ya hayo katika Juz. 1(2:7)

Ni vizuri kuashiria kuwa Aya hii inafahamisha kwa uwazi kwamba Uislam hauna mfano na chochote kwa ulivyo; bali kwa natija zake na athari zake. Kwa hiyo usikizi na uoni ni utekelezaji wa akili, na akili ndiyo inayopanga matendo. Ikiwa kitendo hakikufanyika, basi usikizi na uoni utakuwa hauna maana yoyote; kwa dhahiri au si kwa dhahiri.

Kwa maneno mengine katika Uislamu, mambo yote ya ndani na ya nje, na ya ardhini na ya angani ni nyenzo za manufaa ya watu katika kupangilia maisha yao na kutatua matatizo yao.

Imam Ali(a.s) anasema:"Anadai kwamba yeye anamtaraji Mwenyezi Mungu. Amesema uwongo kwa nini matarajio yake hayaonekani katika vitendo vyake, na kila mwenye kutarajia (Mwenyezi Mungu) hujulikana matarajio yake katika vitendo vyake."

Na wakiona kila Ishara hawaiamini.

Muhammad(s.a.w.w) alifichua hakika ya waongo katika watu wapendao mali na jaha. Wakataharuki na kuhisi hatari ya masilahi yao wakakimbilia kukadhibisha na wakasema kuhusu Aya za Mwenyezi Mungu kuwa ni ngano za watu wa kale, na hali wao wana yakini kwamba Qur'an hii ni mwongozo, lakini wakawa wanaitia njia za shaka shaka na makosa ili wawatumie watu kutokana na upotevu wao na ubatilifu; sawa na wanavyofanya leo watu wa serikali ovu na kanuni za dhuluma.

Na wanamkatazia na wenyewe wanajitenga naye.

Dhamiri ya neno nao inawarudia wale waliopinga haki kwa kupupia masilahi yao. Dhamiri ya wanamkatazia na kujiweka mbali naye, inamrudia Muhammad(s.a.w.w) .

Waongo walikataza watu wasimfuate Muhammad(s.a.w.w) na wakampinga, vilevile walijaribu kumtesa na wakakusanya majeshi kwa ajili ya kumpiga vita. Si kwa lolote ila ni kwamba yeye amefichua mabaya yao.

Na hawaangamizi ila nafsi zao na hawatambui.

Walitaka kuufanyia vitimbi Uislamu na Mtume wake, balaa ikawafikia wao, walipoangamia baadhi yao siku ya Badr wengine wakajisalimisha wakiwa madhalili na wanyonge siku ya kutekwa Makka. Huu ndio mwisho wa kila mwenye kuzama na kung'ang'ania dhuluma na inadi.

﴿وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ وُقِفُوا عَلَى النَّارِ فَقَالُوا يَا لَيْتَنَا نُرَدُّ وَلَا نُكَذِّبَ بِآيَاتِ رَبِّنَا وَنَكُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ﴾

27.Na ungeliona watakapoonyeshwa moto wakawa wanasema. Laiti tungerudishwa (duniani) wala hatutakadhibisha ishara za Mola wetu na tutakuwa katika wanaoamini.

﴿بَلْ بَدَا لَهُم مَّا كَانُوا يُخْفُونَ مِن قَبْلُ وَلَوْ رُدُّوا لَعَادُوا لِمَا نُهُوا عَنْهُ وَإِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ﴾

28.Bali yamewadhihirikia waliyokuwa wakiyaficha zamani. Na kama wangalirudishwa, bila shaka wangeyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo.

﴿وَقَالُوا إِنْ هِيَ إِلَّا حَيَاتُنَا الدُّنْيَا وَمَا نَحْنُ بِمَبْعُوثِينَ﴾

29.Na kusema: Hakuna kingine ila maisha yetu ya dunia, wala sisi hatutafufuliwa.

﴿وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ وُقِفُوا عَلَىٰ رَبِّهِمْ قَالَ أَلَيْسَ هَـٰذَا بِالْحَقِّ قَالُوا بَلَىٰ وَرَبِّنَا قَالَ فَذُوقُوا الْعَذَابَ بِمَا كُنتُمْ تَكْفُرُونَ﴾

30.Na ungeliona watakaposimamishwa mbele ya Mola wao, Akasema: Je, si kweli haya? Watasema: Kwa nini? Tunaapa kwa Mola wetu. Atasema: Basi onjeni adhabu kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyakataa.

﴿قَدْ خَسِرَ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِلِقَاءِ اللَّـهِ حَتَّىٰ إِذَا جَاءَتْهُمُ السَّاعَةُ بَغْتَةً قَالُوا يَا حَسْرَتَنَا عَلَىٰ مَا فَرَّطْنَا فِيهَا وَهُمْ يَحْمِلُونَ أَوْزَارَهُمْ عَلَىٰ ظُهُورِهِمْ أَلَا سَاءَ مَا يَزِرُونَ﴾

31.Hakika wameshahasirika wale waliokadhibisha kukutana na Mwenyezi Mungu, na wamefuzu wale waliomwamini, mpaka itakapowajia ghafla saa (Kiyama) watasema: Oo! Majuto yetu juu ya yale tuliyoyapuuza! Nao watabeba mizigo yao migongoni mwao. Angalieni! Ni mabaya mno wanayoyabeba.

﴿وَمَا الْحَيَاةُ الدُّنْيَا إِلَّا لَعِبٌ وَلَهْوٌ وَلَلدَّارُ الْآخِرَةُ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ يَتَّقُونَ أَفَلَا تَعْقِلُونَ﴾

32.Na maisha ya dunia si kitu ila mchezo na upuzi. Na hakika nyumba ya akhera ni bora zaidi kwa wenye takua. Basi je hamtii akili?

WATAKAPOSIMAMISHWA MOTONI

Ay 27 - 32

MAANA

Na ungeliona watakapoonyeshwa moto.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amerudia kuelezea hali ya wakadhibishaji Siku ya Kiyama, na kwamba wao watakapoona adhabu waliyoandaliwa na thawabu walizoandaliwa waumini, watasema:

Laiti tungerudishwa duniani wala hatutakadhibisha ishara za Mola wetu na tutakuwa katika wanaoamini.

Yaani tutatubia na tufanye amali njema. Lakini masikitiko na mazingatio hayafai chochote ila ikiwa kumwogopa Mwenyezi Mungu na adhabu yake ni kabla ya kutokea adhabu. Ama baada ya kutokea, basi ni kulilia maiti na kusikitika yaliyofutu.

Bali yamewadhihirikia waliyokuwa wakiyaficha zamani.

Hataokoka kesho na adhabu ya Mwenyezi Mungu ila ambaye yuko wazi katika maisha haya, vitendo vyake vinaambatana na kauli yake; yote mawili yawe ni picha ya dhati yake na hali yake, mpaka viwe vyote ni kama kitu kimoja tu mbele ya Mwenyezi Mungu na watu.

Ama yule mwenye kuzibaziba, ambaye Muumba anayajua yale ayafanyayo na watu hawayajui, miongoni mwa ria na unafiki, huyu yatamdhihirikia malipo ya ria yake na unafiki wake; na nafsi yake itajutia uovu wake na kutamani kujisafisha kwa kurudishwa duniani, lakini wapi!

Na kama wangalirudishwa, bila shaka wangeyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo.

katika kusema kwao: Laiti tungerudishwa wala hatutakadhibisha ishara za Mola wetu na tutakuwa katika wanaoamini.

Tumesoma habari za wakosaji kadhaa ambao wanatubia wakiwa gerezani, lakini wanapotoka hurudia makosa yao. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَإِذَا مَسَّكُمُ الضُّرُّ فِي الْبَحْرِ ضَلَّ مَن تَدْعُونَ إِلَّا إِيَّاهُ فَلَمَّا نَجَّاكُمْ إِلَى الْبَرِّ أَعْرَضْتُمْ وَكَانَ الْإِنسَانُ كَفُورًا﴾

"Na inapowafikia dhara katika bahari hupotea wale mnawaomba isipokuwa Yeye tu, lakini anapowaokoa mkafika salama nchi kavu mnageuka; na mwanadamu ni mkanushaji mno" (17:67)

Na kusema: Hakuna kingine ila maisha yetu ya dunia, wala sisi hatutafufuliwa.

Yaani lau wangelirudishwa kwenye maisha yao ya mwanzo wangalisema waliyoyasema mwanzo: Hakuna ufufuo wala hisabu wala malipo.

Unaweza kuuliza : Vipi watakanusha na hali wao watakuwa wameshuhudia vituko vikubwa na wakaonyeshwa, mpaka wakataka kujitakasa nayo na kuahidi kuwa hawatarudia?

Jibu : Wao wanajua fika kwamba hisabu na adhabu itakuwa tu, hapana budi. Wakati huo huo wanajua kuwa lau wataitangaza haki na kuinyenyekea, chumo na faida zao watazikosa. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

﴿وَجَحَدُوا بِهَا وَاسْتَيْقَنَتْهَا أَنفُسُهُمْ ظُلْمًا وَعُلُوًّا﴾

"Na wakazikanusha (ishara zetu) na hali yakuwa nafsi zao zina yakini nazo kwa dhulma na kujivuna" (27:14)

Na ungeliona watakaposimamishwa mbele ya Mola wao , baada ya kukadhibisha kukutana naye. Atasema: Je, si kweli haya? Katika kufasiri Aya ya nne katika Sura hii tulisema kuwa Mwenyezi Mungu analingania kuamini haki pamoja na kusimamisha dalili yake. Mpingaji akiipinga, hoja inakuwa juu yake. Na Aya hii inatilia mkazo hilo na kutaja dalili na hoja walizozikanusha na kuzikadhibisha. Watasema: Kwanini? Tunaapa kwa Mola wetu. Hivi sasa yamepita yaliyopita na hakuna kilichobaki isipokuwa malipo yenye kulingana na adhabu kwa mwenye kukufuru na kukanusha.

Akasema: "Basi onjeni adhabu kwa sababu ya mliyokuwa mkikataa. Haya ni malipo ya kila mwenye kuiweka mbele dunia na kuiacha Akhera na akaificha haki kwa hawa ya nafsi yake.

Utauliza : Kauli yake Mwenyezi Mungu kwa Makafiri: 'Je, si kweli haya?' Na kauli yake: "Onjeni adhabu" mbona haziafikiani na kauli yake:"Wala hatawasemeza Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama" ? (2:174)

Jibu : Makusudio ni kwamba Mwenyezi Mungu hatawasemesha yale yanayowafurahisha, bali atawasemeza yanayowaudhi, kama ilivyo katika Aya hii, na ilivyo katika Aya isemayo:

"Atasema: Tokomeeni humo wala msinisemeze." (23:108)

Hakika wamekwishahasirika wale waliokadhibisha kukutana na Mwenyezi Mungu na wamefuzu wale waliomwamini, mpaka itakapowajia ghafla saa (Kiyama) watasema: Oo! Majuto yetu juu ya yale tuliyoyapuza!

Imam Ali anasema:"Matunda ya kupuuza ni majuto, na matunda ya uthabiti ni amani."

Nao watabeba mizigo yao migongoni mwao. Angalieni! Ni mabaya mno wanayoyabeba.

Mizigo ni dhambi na kuibeba mgongoni ni fumbo, yaani kuwa nayo; kama vile isemwavyo: "Amepandwa na shetani." Yaani yuko naye hamwachi. Maana ni kuwa wanaoikadhibisha haki ndio watu wenye hali mbaya zadi huko akhera.

Mmoja wa wafasiri wapya anasema: "Bali mnyama ana hali nzuri zaidi kwa sababu hubeba mizigo mizito,; na mnyama huutua mzigo wake akaenda kupumzika, lakini hawa watakwenda na mizigo yao kwenye Jahannam wakisindikizwa na dhambi."

Na maisha ya dunia si kitu ila mchezo na upuzi." Umetangulia mfano wake katika Juz 4 (3:185)

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿قَدْ نَعْلَمُ إِنَّهُ لَيَحْزُنُكَ الَّذِي يَقُولُونَ فَإِنَّهُمْ لَا يُكَذِّبُونَكَ وَلَـٰكِنَّ الظَّالِمِينَ بِآيَاتِ اللَّـهِ يَجْحَدُونَ﴾

33.Hakika tunajua kwamba yanakuhuzunisha yale wanayoyasema, Basi hakika hao hawakukadhibishi wewe, lakini madhalimu wanakataa ishara za Mwenyezi Mungu.

﴿وَلَقَدْ كُذِّبَتْ رُسُلٌ مِّن قَبْلِكَ فَصَبَرُوا عَلَىٰ مَا كُذِّبُوا وَأُوذُوا حَتَّىٰ أَتَاهُمْ نَصْرُنَا وَلَا مُبَدِّلَ لِكَلِمَاتِ اللَّـهِ وَلَقَدْ جَاءَكَ مِن نَّبَإِ الْمُرْسَلِينَ﴾

34.Na hakika walikadhibishwa Mitume kabla yako, wakavumilia juu ya kukadhibishwa na kuudhiwa, mpaka ikawafikia nusura yetu. Na hakuna wa kubadilisha maneno ya Mwenyezi Mungu, Na bila shaka zimekujia baadhi ya habari za Mitume hao.

﴿وَإِن كَانَ كَبُرَ عَلَيْكَ إِعْرَاضُهُمْ فَإِنِ اسْتَطَعْتَ أَن تَبْتَغِيَ نَفَقًا فِي الْأَرْضِ أَوْ سُلَّمًا فِي السَّمَاءِ فَتَأْتِيَهُم بِآيَةٍ وَلَوْ شَاءَ اللَّـهُ لَجَمَعَهُمْ عَلَى الْهُدَىٰ فَلَا تَكُونَنَّ مِنَ الْجَاهِلِينَ﴾

35.Na ikiwa ni makubwa kwako huku kukataa kwao, basi kama unaweza kutafuta njia ya chini kwa chini katika ardhi au ngazi kwendea mbinguni na kuwaletea ishara. Na kama Mwenyezi Mungu angelitaka, bila shaka angeliwakusanya kwenye uongofu. Basi usiwe miongoni mwa wajinga

﴿إِنَّمَا يَسْتَجِيبُ الَّذِينَ يَسْمَعُونَ وَالْمَوْتَىٰ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ ثُمَّ إِلَيْهِ يُرْجَعُونَ﴾

36.Hakika wanaokubali ni wale tu wanaosikia, Na wafu Mwenyezi Mungu atawafufua kisha watarejeshwa kwake.

﴿وَقَالُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ آيَةٌ مِّن رَّبِّهِ قُلْ إِنَّ اللَّـهَ قَادِرٌ عَلَىٰ أَن يُنَزِّلَ آيَةً وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ﴾

37.Na husema: Kwa nini hakuteremshiwa ishara kutoka kwa Mola wake? Sema: Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza wa kuteremsha ishara yoyote, lakini wengi wao hawajui.

TUNAJUA KUWA YANAKUHUZUNISHA

Aya 33 - 37

MAANA

Hakika tunajua kwamba yanakuhuzunisha yale wanayoyasema.

Msemo unaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) , Dhamir ya 'wanayoyasema' inawarudia wale waliomkadhibisha Mtume(s.a.w.w) . Ama yale wanayoyasema bali waliyasema hasa, ni yale yaliyoashiriwa na Mwenyezi Mungu (s.w.t):

﴿ثُمَّ تَوَلَّوْا عَنْهُ وَقَالُوا مُعَلَّمٌ مَّجْنُونٌ﴾

Kisha wakampa mgongo na wakasema: Amefunzwa (na) ni mwendawazimu." (44:14)

"Wakasema Makafiri: Hakika huyu ni mchawi dhahiri." (10:2) Na mengineyo.

Basi hakika hao hawakukadhibishi wewe, lakini madhalimu wanakataa ishara za Mwenyezi Mungu.

Kila mwenye kumpiga vita mwenye haki, basi ameipiga vita haki yenyewe, na kila mwenye kumdharau Mtume kwa kuwa yeye anachukua risala ya aliyemtuma, basi atakuwa amemdharau yule aliyemtuma na sio Mtume mwenyewe.

Washirikina wa Makka walikuwa wakimwita Muhammad(s.a.w.w) mkweli mwaminifu, kabla ya Utume. Alipowaletea risala ya Mwenyezi Mungu na kuwasimamishia hoja, walimpiga vita na wakamwita mwendawazimu, mchawi nk.

Kwa hiyo kumkadhibisha kwao huku na hali hii, ni kukadhibisha risala ya Mwenyezi Mungu na hoja zake. Hakuna linalofahamisha hilo kwa dalili zaidi ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿إِنَّ الَّذِينَ يُبَايِعُونَكَ إِنَّمَا يُبَايِعُونَ اللَّـهَ يَدُ اللَّـهِ فَوْقَ أَيْدِيهِمْ﴾

"Hakika wale wanaokubai, kwa hakika wanambai Mwenyezi Mungu; mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao" (48:10)

Na hakika walikadhibishwa Mitume kabla yako, wakavumilia juu ya kukadhibishwa na kuudhiwa, mpaka ikawafikia nusura yetu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake ikiwa watakukadhibisha, basi wamekadhibishwa Mitume kabla yako na wakaudhiwa katika kufikisha risala yake, wakavumilia juu ya maudhi mpaka ikawajia nusura. Kwa hiyo nawe vumilia kama walivyovumilia; na Mwenyezi Mungu atakunusuru kama alivyowanusuru.

Huu ndio mzunguko wa maisha - mvutano baina ya kheri na shari na haki na batili. Ni muhali kwa mpigania haki asipate maudhi kutoka katika maadui wa haki. Vilevile haki haiwezi kushinda ila wapatikane watakaoinusuru wavumilivu katika jihadi ya haki na wainunue kwa nafsi zao, watu wao na mali zao.

Ni desturi ya Mwenyezi Mungu, wala huwezi kupata mabadiliko katika desturi ya Mwenyezi Mungu, Hii ndio maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Na hakuna wa kubadilisha maneno ya Mwenyezi Mungu.

Wala sijui wakati ambao wabatilifu wamekuwa na nguvu kuliko wakati huu tunaoishi. Wameweka vituo vya kijeshi kila mahali, vituo vya kuharibu, silaha kali za kumaliza watu na kubomoa. Wanatawala nyenzo za wananchi wadhaifu, mabenki, magazeti, uchapishaji na usambazaji, Mpaka yule mtu aliye mwaminifu mwenye ikhlasi anajikuta ametupwa hawezi kutoa makala huru au kutangaza haki kupitia kwenye Idhaa. Lakini mhaini, popote atakapoelekea atapata mapokezi na kutukuzwa [7] .

Na bila shaka zimekujia baadhi ya habari za Mitume hao.

Yaani tumekusimulia kabla yale yaliyowapata Mitume kutokana na watu wao na jinsi walivyovumilia katika kukadhibishwa na maudhi, na kwamba mwisho ushindi ulikuwa wao.

Na desturi hii itakupitia wewe, kama iliyowapita wao, wala hakuna mwenye kubadilisha maneno ya Mwenyezi Mungu.

Na ikiwa ni makubwa kwako huku kukataa kwao, basi kama unaweza kutafuta njia ya chini kwa chini katika ardhi au ngazi kwendea mbinguni na kuwaletea ishara.

Aya hii ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu kumwambia Mtume wake Mtukufu:

﴿فَلَا تَذْهَبْ نَفْسُكَ عَلَيْهِمْ حَسَرَاتٍ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ بِمَا يَصْنَعُونَ﴾

"Basi roho yako isitoke kwa majonzi juu yao; hakika Mwenyezi Mungu anayajua yote wanayoyafanya." (35:8)

Aya zote hizi mbili zinatoa picha jinsi Mtume(s.a.w.w) alivyokuwa akipata jakamoyo na uchungu kutokanana upinzani wa washirikina kwa mwito wake.

Yaliyompata Mtume kutoka kwa watu wake ni yale yanayoondoa upole wa mpole. Lakini yeye akavumilia na kuwa na matumaini; wala hakuwaapiza bali aliwaombea, akisema:"Ewe Mola wangu! Wasamehe watu wangu, hakika wao hawajui"

Pamoja na hayo yote alikuwa akihisi uchungu kwa kufuru zao. Ndipo Mwenyezi Mungu akamwambia kwa Aya hii, ili kumpoza na kumwondolea matumaini na aachane nao; kisha angoje kidogo, aone vile utakavyokuwa mwisho wa wakadhibishaji.

Na kama Mwenyezi Mungu angelitaka, bila shaka angeliwakusanya kwenye uongofu.

Razi anasema kuwa: "Hii inafahamisha kuwa yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu hataki makafiri waamini, bali anataka kuwabakisha kwenye ukafiri.

Lakini hii itakuwa ni dhuluma hasa, na Mwenyezi Mungu hawadhulumu waja. Usahihi wa maana ya jumla hii, ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) hataki kumlazimisha yeyote katika kumwamini, bali anamwachia hiyari yake baada ya kumsimamishia hoja kwa dalili na ubainifu. Lau angelitaka waja wake waamini kwa kusema 'kuwa ikawa', basi asingelikufuru yeyote katika wao. Lakini hekima yake Mwenyezi Mungu Mtukufu ilitaka ajiingize katika mambo ya watu kama mwamrishaji na mwenye kutoa nasaha, si kama Muumba mwenye nguvu, Umetangulia ufafanuzi katika Juz. 1 (2:26)

Basi usiwe miongoni mwa wajinga.

Atakuwaje Mtume Mtukufu miongoni mwa wajinga na hulka zake ni hulka za Qur'an? Msemo huu umefaa kuelekezwa kwa mtukufu wa viumbe, kwa vile unatoka kwa Muumba wa viumbe na sio kwa kwa aliye kama yeye.

Wanaokubali ni wale tu wanaosikia, Na wafu Mwenyezi Mungu atawafufua kisha watarejeshwa kwake.

Aya hii ni mfano wa Aya isemayo:

﴿إِنَّكَ لَا تُسْمِعُ الْمَوْتَىٰ وَلَا تُسْمِعُ الصُّمَّ الدُّعَاءَ إِذَا وَلَّوْا مُدْبِرِينَ﴾

"Hakika huwezi kuwasikilizisha wafu wala huwezi kuwasikilizisha viziwi mwito wanapogeuka kurudi nyuma" (27:80)

Maana ni kuwa: Ewe Muhammad! Wale unaopupia waonyeke hawakusikii kwa kufahamu na kuzingatia. Kwa sababu kupenda dunia kumewafanya kama wafu, na wafu haitakikani kuwaambia chochote; bali wanaachwa na mambo yao mpaka siku ya kiyama, watakapoiona adhabu ambayo hawataweza kuikimbia.

Na husema: Kwa nini hakuteremshiwa ishara kutoka kwa Mola wake?

Utauliza : vipi wanasema hivi na hali Mwenyezi Mungu amemteremshia Muhammad(s.a.w.w) ishara na hoja kadhaa na ubainifu.

Jibu : Makusudio ya ishara hapa ni muujiza ule walioutaka wao kuwa ni sharti la wao kumwamini Muhammad(s.a.w.w) ; hawakusudii muujiza unaomkinaisha mwenye kuitafuta haki, Lau wangeliutaka huo wasingelisema hivyo.

Sema: Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza wa kuteremsha ishara yoyote , ile wanayotaka, lakini yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu haiteremshi kwa kuitikia matakwa na hawaa zao; isipokuwa anateremsha miujiza kulingana na inavyopitisha hekima yake.

Lakini wengi wao hawajui , kuwa anateremsha miujiza kulingana na hekima Yake na sio hawa za watu.

﴿وَمَا مِن دَابَّةٍ فِي الْأَرْضِ وَلَا طَائِرٍ يَطِيرُ بِجَنَاحَيْهِ إِلَّا أُمَمٌ أَمْثَالُكُم مَّا فَرَّطْنَا فِي الْكِتَابِ مِن شَيْءٍ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّهِمْ يُحْشَرُونَ﴾

38.Na hakuna mnyama katika ardhi wala ndege arukaye kwa mbawa zake, ila ni umma kama nyinyi, Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote. Kisha watakusanywa kwa Mola wao.

﴿وَالَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا صُمٌّ وَبُكْمٌ فِي الظُّلُمَاتِ مَن يَشَإِ اللَّـهُ يُضْلِلْـهُ وَمَن يَشَأْ يَجْعَلْهُ عَلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ﴾

39.Na wale waliokadhibisha ishara zetu ni viziwi na mabubu wako gizani. Amtakaye Mwenyezi Mungu humpoteza na amtakaye humweka katika njia iliyonyooka.

WANYAMA NA NDEGE NI UMMA

Aya 38-39

LUGHA

Mnyama, ni kila anayetembea katika ardhi wakiwa ni: Watu, wanyama na wadudu.

MAANA

Na hakuna mnyama katika ardhi wala ndege arukaye kwa mbawa zake, ila ni umma kama nyinyi.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha katika Aya hii kwamba baina yetu na wanyama kuna aina ya kufanana, lakini hakufafanua aina yenyewe. Je, tunafanana katika kuwa wao ni viumbe wa Mwenyezi Mungu; au katika kumwamini Mwenyezi Mungu na kumsifu kwa sifa zake njema? Au tunafanana katika kuwa wao ni aina zinazojulikana kwa majina; kama zinavyojulikana koo na kabila? Au ni katika kupanga maisha yao na kufanya mambo kulingana na masilahi?

Kwa hali yoyote iwayo ni kuwa wataalamu wengi wamechunguza tabia na kazi za wanyama, wadudu na ndege na wakafikia kwenye siri za ajabu zinazoshuhudia kuweko mpangaji mwenye hekima, Tutataja baadhi ya mifano.

Ndovu huweka mahakama kwa mhalifu na ndovu aliyekosea huhukumiwa kwa kutengwa na kundi la wengine ili aishi peke yake katika upweke.

Kunguru anapohisi hatari itakayowapata wenzake huwaonya kwa sauti maalum. Ama katika hali ya furaha hutoa sauti iliyo karibu na kicheko.

Utauliza : Kuna faida gani katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu kusema arukaye kwa mbawa zake ambapo kumtaja Ndege kunafahamisha moja kwa mja kuruka kwa mbawa?

Jibu : Hakuna faida, tuijuayo, isipokuwa ufasaha wa maneno.

Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote.

Imesemekana kuwa makusudio ya Kitab hapa ni lawhim-mahfudh (ubao maalum wenye kuhifadhiwa) wenye kukusanya yaliyokuwa na yatakayokuwa.

Kauli ya pili, inasema ni fumbo la ujuzi wa Mwenyezi Mungu kujua makusudio ya mtu, na kauli zake na vitendo vyake.

Kauli ya tatu, inasema ni Qur'an na kwamba Mwenyezi Mungu amebainisha ndani yake kila yapasayo kubainishiwa watu, miongoni mwa misingi ya dini na matawi yake na yanayofungamana nayo, Nasi tumeichagua kauli hii katika kufasiri Aya ya (2:2) Juz. 1, kifungu Qur'an na sayansi.

Kisha watakusanywa kwa Mola wao.

Dhahiri ya maneno inafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu atawakusanya wanyama na ndege siku ya Kiyama, kama atakavyowakusanya watu. Vilevile Aya isemayo:"Na wanyama mwitu watakapokusanywa." (82:5)

Maulama wengi wamesema hivyo kwa kutegemea Aya hizo mbili na Hadith isemayo: "Hakika Mwenyezi Mungu atawachukulia kisasi watu kutokana na wenye pembe."

Sisi tuko pamoja na Ibn Abbas aliyesema kuwa makusudio ya kukusanywa wanyama ni mauti yao; kama ilivyopokewa katika Hadith: "Anayepatwa na kifo ndiyo kiama chake." Kwa sababu hisabu na adhabu ni baada ya kukalifiwa na sharia na kuzihalifu. Wala hakuna kukalifiwa na sharia ila pamoja na akili; na wanyama na ndege hawana akili, kwa hiyo hawakalifiwi na sharia.

Kwa sababu hizo basi, hawatakusanya kwa ajili ya hisabu. Lau wanyama wangelichukuliwa hisabu basi ingefaa zaidi watoto wadogo wachukuliwe hisabu. Ama Hadith ya 'kuchukua kisasi', ni fumbo la uadilifu wa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Na kwamba yeye hataacha kidogo wala kikubwa ila atakidhibiti.

Ikiwa Mwenyezi Mungu atawaadhibu wenye pembe wakimpiga mtu, basi vizuri zaidi ni kutuharimishia sisi kuwachinja wanyama. Ama kauli ya anayesema kuwa Mwenyezi Mungu atayabadilisha maumivu ya mtu kwa mnyama, hiyo ni kumsemea Mwenyezi Mungu bila ya ujuzi wowote.

Na wale waliokadhibisha ishara zetu ni viziwi na mabubu wako gizani. Yaani wao ni kama viziwi, kwa sababu wao hawasikii mwito wa haki, na ni kama mabubu kwa sababu wao hawaitamki haki waliyoijua na wako katika giza la kufuata na giza la ushirikina, ukafiri, ufasiki na dhambi.

Amtakaye Mwenyezi Mungu humpoteza na amtakaye humweka katika njia iliyonyooka.

Yametangulia maelezo kuhusu uongofu na upotevu katika Juz.1 (2:26) na Juz.2 (4:88).

﴿قُلْ أَرَأَيْتَكُمْ إِنْ أَتَاكُمْ عَذَابُ اللَّـهِ أَوْ أَتَتْكُمُ السَّاعَةُ أَغَيْرَ اللَّـهِ تَدْعُونَ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ﴾

40.Sema: niambieni, kama ikiwafikia adhabu ya Mwenyezi Mungu au ikiwafikia ile saa, je, mtamuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni wakweli?

﴿بَلْ إِيَّاهُ تَدْعُونَ فَيَكْشِفُ مَا تَدْعُونَ إِلَيْهِ إِن شَاءَ وَتَنسَوْنَ مَا تُشْرِكُونَ﴾

41.Bali yeye tu ndiye mtakayemuomba, Atawaondolea mnayomuomba akitaka, Na mtawasahau mnaowashirikisha .

﴿وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا إِلَىٰ أُمَمٍ مِّن قَبْلِكَ فَأَخَذْنَاهُم بِالْبَأْسَاءِ وَالضَّرَّاءِ لَعَلَّهُمْ يَتَضَرَّعُونَ﴾

42.Kwa hakika tulipeleka (Mitume) kwa umma zilizokuwa kabla yako; kisha tukawatia katika shida na madhara ili wapate kunyenyekea.

﴿فَلَوْلَا إِذْ جَاءَهُم بَأْسُنَا تَضَرَّعُوا وَلَـٰكِن قَسَتْ قُلُوبُهُمْ وَزَيَّنَ لَهُمُ الشَّيْطَانُ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴾

43.Basi mbona wasinyenyekee ilipowafikia adhabu yetu? Lakini nyoyo zao zilikuwa ngumu na shetani akawapambia waliyokuwa wakiyafanya.

﴿فَلَمَّا نَسُوا مَا ذُكِّرُوا بِهِ فَتَحْنَا عَلَيْهِمْ أَبْوَابَ كُلِّ شَيْءٍ حَتَّىٰ إِذَا فَرِحُوا بِمَا أُوتُوا أَخَذْنَاهُم بَغْتَةً فَإِذَا هُم مُّبْلِسُونَ﴾

44.Basi waliposahau yale waliyokumbushwa tuliwafungulia milango ya kila kitu, mpaka walipofurahia yale waliyopewa tuliwakamata kwa ghafla; na mara wakawa wenye kukata tamaa.

﴿فَقُطِعَ دَابِرُ الْقَوْمِ الَّذِينَ ظَلَمُوا وَالْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ﴾

45.Ikakatwa mizizi ya watu waliodhulumu; na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe vyote.

SEMA NIAMBIENI

Aya 40 - 45

MAANA

Sema: niambieni, kama ikiwafikia adhabu ya Mwenyezi Mungu au ikiwafikia ile Saa, je, mtamuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni wakweli?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwamrisha Mtume wake awaambie washirikina: Niambieni kama ikiwafikia adhabu, kama ile iliyoteremshiwa wale waliokadhibisha Mitume yao; au yakiwafikia maumivu makubwa ya mauti na vitisho vya Kiyama, je katika hali hii, mtayaita masanamu na mizimu mliyokuwa mkiabudu na kudai kuwa itawaondolea fazaa na adhabu?

Makusudio ya Aya hii ni kuwa Makafiri kesho watajivua na yale waliyokuwa wakiyaabudu na kukimbilia kwa Mwenyezi Mungu baada ya kuwabainikia kuwa hakuna hila wala nguvu ila kwa msaada wake Yeye tu peke yake bila ya kuwa na mshirika.

MWENYEZI MUNGU NA MAUMBILE

Bali yeye tu ndiye mtakayemuomba.

Baada ya kuwauliza kuwa mtamwomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu siku ya vituko vikubwa, amelithibithisha jibu kwa kusema kwake:(Bali yeye tu ndiye mtakayemuomba) .

Hilo ndilo jibu linaloaminiwa na kujibiwa na umbile ambalo Mwenyezi Mungu amewaumbia watu, katika dunia na akhera, Na sio maana ya umbile la Mwenyezi Mungu kuwa mtu atamtambua Muumba hivi hivi tu bila ya dalili. Hapana! Kama ni hivo basi kusingelitokea mtu yeyote wa kumkanusha Mwenyezi Mungu.

Hakika maana ya umbile hili ni kuwa Mwenyezi Mungu amempa mtu maandalizi ya kufahamu dalili zinazofahamisha kuweko Mwenyezi Mungu, na dalili hizi haepukani nazo kwa hali yoyote. Anayekufuru anakufuru kwa kuzembea na kupuuza kwa kuepuka kuchunguza dalili na hoja. Kwa hiyo ndipo akastahiki adhabu kwa kupuuza huko.

Kwani hakuna tofauti kabisa katika mtazamo wa akili, baina ya mwenye kuacha kufanya amali, kwa makusudi, na huku anajua; na yule mwenye kuiacha haki akafuta batili kwa kutojua lakini ana uwezo wa kujua na kupambanua uongufu na upotevu, lakini akaacha kwa kupuuza na kudharau.

Inawezekana maandalizi hayo yakajificha nyuma ya pazia la kufuata maelezo na matamanio; sawa na linavyojificha jua nyuma ya mawingu, ikafikiriwa kwa yule asiyejua sitara hizo kuwa yeye amemkana Mwenyezi Mungu kwa kukosa dalili na dalili iko katika dhati yake na maumbile yale ambayo amemuumbia Mwenyezi Mungu. Na siku ya Kiyama sitara hii iliyozuka itaondoka na kudhihiri hakika iliyo wazi wala hakutasalia nafasi ya shaka na ukanusho.

Atawaondolea mnayomuomba akitaka.

Yaani nyinyi washirikina mtaacha siku ya Kiyama, kuomba masanamu mliyokuwa mkiyaabudu duniani na mtamwomba Mwenyezi Mungu peke yake, wakati hakika ya kila jambo itakapodhihiri.

Na mtawasahau mnaowashirikisha.

Yaani nyinyi washirikina siku ya Kiyama mtaacha kuyaomba masanamu mliyokuwa mkiyaabudu duniani na kumwomba Mwenyezi Mungu peke yake wakati itakapodhihiri hakika ya kila kitu.

Kwa hakika tulipeleka (Mitume) kwa umma zilizokuwa kabla yako; kisha tukawatia katika shida na madhara ili wapate kunyenyekea.

Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) hawaadhibu waja wake ila baada ya kuwapelekea mjumbe atakayewaongoza kwenye njia ya uongofu. Kama hawakuongoka anawapa fursa ili wajirudi wenyewe, na kuwatia katika mtihani kwa mabalaa ili wanyenyekee na watubie, lakini wao waling'ang'ania maasi; kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Aya inayofuatia hii.

Basi mbona wasinyenyekee ilipowafikia adhabu yetu? Lakini nyoyo zao zilikuwa ngumu na shetani akawapambia waliyokuwa wakiyafanya.

Mwenyezi Mungu, ambaye zimetukuka sifa zake, anasema kuwa wao hawakunyenyekea ilipowafikia shida duniani wala hawakumdhalilikia Mwenyezi Mungu kwa kuacha inadi yao, bali waling'ang'ania ukafiri, na shetani akawa nyuma yao akiwapambia upotevu na ufisadi.

Aya hii inafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamkubali kila anayekimbilia kwake, hata kama kukimbia kwake ni kwa vikwazo vya shida na balaa. Hivi ndivyo alivyo aliye mkarimu na adhimu. Hamnyimi mwenye kuomba wala hamkatishi tamaa, kwa namna yoyote lengo na msukumo wake utakavyokuwa.

Basi waliposahau yale waliyokumbushwa tuliwafungulia milango ya kila kitu mpaka walipofurahia yale waliyopewa tuliwakamata kwa ghafla; na mara wakawa wenye kukata tamaa.

Aliwaonya kwanza kwa kauli kupitia kwa Mitume. Pili, kwa vitendo alipowapa mtihani kwa shida na madhara.

Waliponga'ang'ania ukafiri na inadi aliwafungulia milango ya riziki na raha, ili kuwasimamishia hoja na kuwavuta kidogo kidogo kwa neema baada ya mtihani wa nakama.

Walipofurahia raha na kuzidi kiburi na wala wasielekee kwenye uongofu, basi Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa namna wasiyofikiria, wakajuta kwa kuzembea na wakakata tamaa ya kuokoka.

Kwa ufupi ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) mara nyingine aliwapa dhiki na mara nyingine furaha kwa kupenda waongoke; sawa na afanyavyo mzazi kumhurumia mwanawe akitaka atengenekewe.

Lakini wala hawakushukuru raha wala kuwaidhika na balaa. Wakang'olewa wote asibakie yeyote katika wao, ili wapate funzo watakaokuja baada yao.

Ikakatwa mizizi ya watu waliodhulumu; na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe vyote.

Kwa sababu ya kuwaneemesha kwake waumin na kuwanusuru na watu wa kufuru na ufisadi.