TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA 0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 13136
Pakua: 2176


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 16 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 13136 / Pakua: 2176
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA SABA Juzuu 7

Mwandishi:
Swahili

13

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَىٰ عَلَى اللَّـهِ كَذِبًا أَوْ قَالَ أُوحِيَ إِلَيَّ وَلَمْ يُوحَ إِلَيْهِ شَيْءٌ وَمَن قَالَ سَأُنزِلُ مِثْلَ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَلَوْ تَرَىٰ إِذِ الظَّالِمُونَ فِي غَمَرَاتِ الْمَوْتِ وَالْمَلَائِكَةُ بَاسِطُو أَيْدِيهِمْ أَخْرِجُوا أَنفُسَكُمُ الْيَوْمَ تُجْزَوْنَ عَذَابَ الْهُونِ بِمَا كُنتُمْ تَقُولُونَ عَلَى اللَّـهِ غَيْرَ الْحَقِّ وَكُنتُمْ عَنْ آيَاتِهِ تَسْتَكْبِرُونَ﴾

93.Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amzuliaye uwongo Mwenyezi Mungu. Au mwenye kusema: Nimeletewa Wahyi; na hali hakuletewa wahyi wowote Na yule asemaye: Nitateremsha kama alivyoteremsha Mwenyezi Mungu. Na lau ungewaona madhalimu watakapokuwa katika mahangaiko ya mauti na Malaika wamewanyooshea mikono. Zitoeni roho zenu; leo mtalipwa adhabu ifedheheshayo kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyasema juu ya Mwenyezi Mungu yasiyokuwa haki, na mlikuwa mkizifanyia kiburi ishara Zake.

﴿وَلَقَدْ جِئْتُمُونَا فُرَادَىٰ كَمَا خَلَقْنَاكُمْ أَوَّلَ مَرَّةٍ وَتَرَكْتُم مَّا خَوَّلْنَاكُمْ وَرَاءَ ظُهُورِكُمْ وَمَا نَرَىٰ مَعَكُمْ شُفَعَاءَكُمُ الَّذِينَ زَعَمْتُمْ أَنَّهُمْ فِيكُمْ شُرَكَاءُ لَقَد تَّقَطَّعَ بَيْنَكُمْ وَضَلَّ عَنكُم مَّا كُنتُمْ تَزْعُمُونَ﴾

94.Na hakika mtatujia wapweke kama tulivyowaumba kwanza. Na mmeacha nyuma yenu yale tuliyowapa. Na hatuwaoni waombezi wenu pamoja nanyi ambao mlidai ni washirika.

KUMZULIA UWONGO MWENYEZI MUNGU

Aya 93-94

MAANA

Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amzuliaye uwongo Mwenyezi Mungu.

Kumzulia Mwenyezi Mungu uwongo ni kumtengenezea mambo ambayo hayana chimbuko katika Qur’an wala Hadith au katika misingi ya akili. Na hayo yanakuwa kwa mambo yafuatayo:

• Kuhalalisha aliyoyaharamisha Mwenyezi Mungu au kuharamisha aliyoyahalalisha.

• Kumsingizia Mwenyezi Mungu, kwa makusudi, yale asiyokuwa nayo au kumfanyia washirika au kuwa ana watoto na mabinti.

• Kudai Utume kwa asiyekuwa Mtume. Hilo ameliashiria Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa kauli yake: Au mwenye kusema: Nimeletewa Wahyi; na hali hakuletewa Wahyi wowote. Jumla hii inaungana na ile ya ‘Amzuliaye Mwenyezi Mungu uwongo.’ Ni katika mlango wa kuunganisha mahsusi kwenye ujumla.

• Na yule asemaye: Nitateremsha kama alivyoteremsha Mwenyezi Mungu.Yaani mlaanifu huyu anadai kuwa ana uwezo wa kutunga Kitab kitakachofanana na Qur’an katika utukufu wake. Imesekana kuwa mtu huyo ni Abdullah bin Sa’d bin Abu Sarh. Wengine wamesema ni Nadhr bin Harith.

Kwa ufupi ni kwamba kila mwenye kumnasibishia Mwenyezi Mungu kitu chochote bila ya kutegemea kauli ya Mwenyezi Mungu na ya Mtume au misingi ya akili basi huyo ni mzushi, mwongo mkubwa na anayestahiki shutuma na adhabu.

Na lau ungewaona madhalimu wanavyokuwa katika mahangaiko ya mauti na Malaika wamewanyooshea mikono.

Mahangaiko ya mauti ni maumivu ya kukata roho, Wafasiri wametofautiana katika makusudio ya kunyoosha mikono ya Malaika. Je, makusudio ni kunyoosha kiuhakika wakati mtu anapokata roho, au ni fumbo tu la kufananisha vituko vya mauti?

Sisi hatuoni haja yoyote ya mzozo huu, Kwa sababu akili haikatai kuweko Malaika wala kuwa na mikono wanaoinyoosha au ndimi za kuzungumzia. Kwani Wahyi umelieleza hilo, kwa hiyo ni wajibu kuamini. Msingi huu wanautegemea Maulama wote Waislamu katika kuthibitisha itikadi na sharia.

Zitoeni roho zenu; leo mtalipwa adhabu ifedheheshayo kwa sababu ya yale mliyokuwa mkisema juu ya Mwenyezi Mungu yasiyokuwa ya haki, na mlikuwa mkizifanyia kiburi ishara zake.

Haya yote ni maneno ya Malaika wakiwaambia wazushi wakati wa kufa. Nayo ni lawama na shutuma kwa uzushi wao na kukana kwao haki. Kuna Hadith isemayo: "Anayekufa kiyama chake kimesimama." Kwa sababu hii wamesema baadhi ya wajuzi kwamba mtu ana viyama viwili, kidogo ambacho ni mauti na kikubwa, ufufuo.

Shutuma za Malaika kwa anayemzulia Mwenyezi Mungu uwongo, katika Kiyama kidogo, ni onyo la vituko vya Kiyama kikubwa atakavyokumbana navyo. Imam Ali anasema: "Kifo kwa Mumin ni kama kuvua nguo chafu na kufungua minyororo na kuvaa kanzu ya kifahari na kushukia kwenye maliwazo. Ama kwa kafiri, ni kama kuvua kanzu ya kifahari na kuvaa gwanda chafu, na kutoka kwenye maliwazo kwenda kwenye vitisho na adhabu kubwa."

Na hakika mtatujia wapweke kama tulivyowaumba kwanza.

Yaani mwanadamu atakutana na Mola wake kesho, kama alivyotoka tumboni mwa mamake hana chochote.

Afadhali angeliingia ardhini kama alivyotoka - haulizi wala haulizwi, lakini atarudi akiwa ni mwenye kuulizwa. Alhamdulilah, mwenye kuuliza ni mwadilifu hamdhulumu yeyote na atamfanyia mtu vile alivyowafanyia watu alipokuwa katika uhai wake wa kwanza. Ikiwa ni kheri basi itakuwa kheri na ikiwa ni shari basi ni shari.

Wametofautiana wanavyuoni kuhusu kufufuliwa kuwa je, ni kwa roho tu, au ni kwa roho na kiwiliwili pamoja. Dhahiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu: kama tulivyowaumba kwanza, inafahamisha kufufuliwa kwa roho na kiwiliwili kwa sababu vyote viwili vimeumbwa pamoja.

﴿كَمَا بَدَأْنَا أَوَّلَ خَلْقٍ نُّعِيدُهُ وَعْدًا عَلَيْنَا إِنَّا كُنَّا فَاعِلِينَ﴾

"Kama tulivyoanza umbo la awali tutalirudisha tena, Ni ahadi iliyo juu yetu, hakika sisi ni watendaji" (21:104)

Na mmeacha nyuma yenu yale tuliyowapa.

Mtu atarudi ardhini akiwa ameacha watu wake, marafiki mali na ufalme.

Na hatuwaoni waombezi wenu pamoja nanyi ambao mlidai ni washirika (wa Mwenyezi Mungu) kwenu.

Kama vile masanamu, nyota na mengineyo mliyokuwa mkiyaabudu na kuwatawalisha wafisadi na wapotevu.

Kwa hakika yamekatika (mahusiano) baina yenu.

Yaani hamna mawasiliano yoyote ya duniani.

Na yamewapotea mliyokuwa mkidai katika madai ya uwongo kwa wale mliowafikiria kuwa ni washirika au waombezi mbele yake, na yamepotea matumaini yenu baada ya kufichuka uhakika; na mwema ni yule atakayefuzu kupata radhi za Mwenyezi Mungu na maghufira yake.

﴿إِنَّ اللَّـهَ فَالِقُ الْحَبِّ وَالنَّوَىٰ يُخْرِجُ الْحَيَّ مِنَ الْمَيِّتِ وَمُخْرِجُ الْمَيِّتِ مِنَ الْحَيِّ ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ فَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ﴾

95.Hakika Mwenyezi Mungu ndiye mpasuaji mbegu na kokwa. Humtoa aliye hai katika maiti na ni mtoaji wa maiti katika aliye hai. huyo ndiye Mwenyezi Mungu basi mnageuzwa wapi?

﴿فَالِقُ الْإِصْبَاحِ وَجَعَلَ اللَّيْلَ سَكَنًا وَالشَّمْسَ وَالْقَمَرَ حُسْبَانًا ذَٰلِكَ تَقْدِيرُ الْعَزِيزِ الْعَلِيمِ﴾

96.Ndiye mpambazuaji wa asubuhi; ameufanya usiku kuwa mapumziko na utulivu, na jua na mwezi (kwenda) kwa hesabu, Hayo ndiyo makadirio ya Mweye nguvu, Mjuzi.

﴿وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ النُّجُومَ لِتَهْتَدُوا بِهَا فِي ظُلُمَاتِ الْبَرِّ وَالْبَحْرِ قَدْ فَصَّلْنَا الْآيَاتِ لِقَوْمٍ يَعْلَمُونَ﴾

97.Na yeye ndiye aliyewafanyia nyota ili muongoke kwazo katika viza vya bara na baharini. Hakika tumezifafanua ishara kwa watu wanaojua.

﴿وَهُوَ الَّذِي أَنشَأَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ فَمُسْتَقَرٌّ وَمُسْتَوْدَعٌ قَدْ فَصَّلْنَا الْآيَاتِ لِقَوْمٍ يَفْقَهُونَ﴾

98.Na Yeye ndiye aliyewaanzisha nyinyi kutokana na nafsi moja. Pako mahali pa kutulia na pa kupita njia. Hakika tumezifafanua ishara kwa watu wanaofahamu.

﴿وَهُوَ الَّذِي أَنزَلَ مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَخْرَجْنَا بِهِ نَبَاتَ كُلِّ شَيْءٍ فَأَخْرَجْنَا مِنْهُ خَضِرًا نُّخْرِجُ مِنْهُ حَبًّا مُّتَرَاكِبًا وَمِنَ النَّخْلِ مِن طَلْعِهَا قِنْوَانٌ دَانِيَةٌ وَجَنَّاتٍ مِّنْ أَعْنَابٍ وَالزَّيْتُونَ وَالرُّمَّانَ مُشْتَبِهًا وَغَيْرَ مُتَشَابِهٍ انظُرُوا إِلَىٰ ثَمَرِهِ إِذَا أَثْمَرَ وَيَنْعِهِ إِنَّ فِي ذَٰلِكُمْ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ﴾

99.Naye ndiye aliyeteremsha maji kutoka mbinguni na kwayo tunatoa mimimea ya kila kitu, Kisha tukatoa kutokana nayo kijani, Tukatoa ndani yake punje zilizopandana, Na katika mitende yakatoka kwenye makole yake mashada yaliyo karibu. Na bustani za miza bibu na mizaituni na mikomamanga. Yanayofanana na yasiyofanana. Angalieni matunda yake yanapozaa na kuiva kwake. Hakika katika hayo kuna ishara kwa watu wanaoamini.

HUTOA ALIYE HAI KATIKA MAITI

Aya 95-99

MAANA

Katika Aya hizi kuna mifano ya ajabu katika viumbe ambavyo anayemiliki utengenezaji wake ni Mwenyezi Mungu peke yake. Vilevile kufahamisha kuwepo Mwenyezi Mungu na utukufu wake. Mifano imetajwa kwa mpango ufuatao:

Hakika Mwenyezi Mungu ndiye mpasuaji mbegu na kokwa.

Ukiweka mbegu ya ngano au kokwa ya tende katika ardhi itapasuka chini na juu. Upande wa chini itatoka mizizi na kushuka ardhini, na upande wa juu utatoka mti utakaorefuka hewani. Kisha ile mbegu au kokwa itapotea na mchanganyiko wote kuwa kitu kimoja, sehemu moja itakuwa ardhini na nyingine itakuwa kwenye hewa.

Hakuna mwenye shaka kwamba kazi yote hii inategemea sababu zake za kimaumbile; kama vile mchanga, maji, jua na hewa, lakini vyote hivyo vinaishia kwa Mwenyezi Mungu peke yake, kwa sababu yeye ndiye aliyeumba maumbile, msababishaji wa sababu na mpatishaji wa mada ya kwanza kwa neno 'Kuwa' na ikawa.

UHAI UMETOKA WAPI?

Humtoa aliye hai katika maiti na ni mtoaji wa maiti katika aliye hai.

Si ajabu kuzalika kitu hai kutoka kwa kilicho hai mfano wake; na kisicho na uhai kutoa kisicho na uhai. Vilevile chenye uhai kuzaa kisicho na uhai, au kinyume chake. Msemaji mmoja alisema: "Uhai unazalikana kutokana na nguvu ya asili ya maumbile." Tumwulize msemaji huyu:

Ni nani aliyeifanya ipatikane asili hiyo, nguvu zake na utendaji kazi wake? Ikiwa msukumano tu unatosha kuleta uhai bila ya kuweko msaada wa Mwenyezi Mungu, basi kwa nini wanasayansi wameshindwa kutengeneza uhai kama vile watengenezavyo vyombo vya jikoni na mengineyo; pamoja na kuwa wamejaribu wakaleta msukumano; lakni baada ya kukata tamaa walisema kwamba kutengeneza uhai ni kuzito kuliko kumrudisha mzee utotoni.

Hebu tuchukulie kuwa wao wanajiona watafaulu katika kutengeza chembehai, je, wamefaulu kutengeza mdudu mdogo tu?.

Tuache binadamu na ubongo wake na wanyama na maumbile yao ya ajabu na tupige mfano wa hawa wadudu tunaowaogopa na kupiga madawa kuwauwa. Baadhi ya wataalamu wa wadudu wanasema hivi: "Baadhi ya wadudu wanaishi katika nyuzi joto 50 chini ya sifuri; wengine wanaishi nyuzi joto hizi hizi juu ya sifuri, wengine katika hewa ya sumu na wengine katika visima vya mafuta, na wana utaratibu mzuri sana katika maisha yao na kazi zao."

Ikiwa mwanaadamu anaweza kugundua satalaiti, maroketi na akili za Elktroni, lakini hawezi kabisa kutengeza bawa la mbu au chembe moja ya mbawa zake. Akili ya binadamu ni kubwa lakini ukubwa wake ni wenye kuhemewa mbele ya uweza wa ajabu ulioumba mbu na chungu na nyuki!

Yote hayo yako wazi, Lakini msiba mkubwa ni kuwa tumejisahau, hatujiangalii sisi wenyewe na uwazi wa uweza wa Mwenyezi Mungu mwenye hekima. Kama tukiangalia tutazidi imani kwa kiwango kikubwa kwa muumba aliye mkubwa. Tunachohitajia ni imani na imani yetu inahitajia akili kwa sababu imani bila ya akili ni kama uso bila macho.

Ndiyo, tunahitaji kuamini uweza wa Mwenyezi Mungu ili tufasiri yale yaliyoshinda akili za mabingwa, ambazo zimeshindwa kufasiri maumbile ya uhai. Na wengi wenye akili hizo wanakimbilia kwenye kitu kilicho nyuma ya maumbile, Uwezo wenye hekima na ujuzi, wanaufasiri kwa kusema kuwa ni asili ya uhai,huyo ndiye Mwenyezi Mungu basi mmegeuzwa wapi?

Anaema Enstein: "Hakika uoni wetu wa kidini ndio unaloelekeza uoni wetu wa kielimu". Ustadh Tawfiq Al-Ahkim aliongeza katika kitabu chake Fannul-adab: 'Huku bila shaka ni kukiri dini. Hakuna mtaalamu yeyote katika waliopiata aliyesema kuhusu dini kama alivyosema huyu."

Nasi twaongeza juu ya kauli ya Al-Hakim, kwamba siri pekee ya kukubali wataalamu wa karne ya ishirini ni kuwa uoni wa dini ndio chimbuko la uoni wa kielimu, ni kuendelea kwa elimu katika karne hii na kuwa ilikuwa nyuma katika zama zilizopita. Kila inapopiga hatua elimu ndipo dini inapozidi kupata watetezi; kama Einstein anayekubali ukuu wa dini na kuamini kuwa ni haki ambayo haiingiliwi na batili mbele yake wala nyuma yake.

Ndiye mpambazuaji wa asubuhi; ameufanya usiku kuwa mapumziko na utulivu, na jua na mwezi (kwenda) kwa hesabu.

Mwenyezi Mngu (s.w.t) ametaja katika Aya zlizotangulia mifano ya utukufu wake kwa kupatikana uhai kwenye ardhi; na katika Aya hii ametaja mifano mitatu ya mbinguni:

Kwanza : kuwa ameitoa asubuhi kwenye usiku, hilo ni fumbo la kupatikana mchana ambao watu wanahangaikia riziki na kupanga mambo yao.

Pili : kwamba yeye Mwenyezi Mungu ameuleta usiku kwa ajli ya kutulia na kupumzika kutokana na machovu za kazi ya mchana kutwa.

Tatu : kwamba ameweka Jua na Mwezi kwa kiasi mahsusi cha haraka na polepole kwa namna ambayo ardhi inakuwa na harakati mbili: Harakati za masaa 24, hisabu ya siku moja, na harakati za mwaka, ambazo ndani yake mna misimu mine ambayo ni hisabu ya mwaka mmoja. Mwenyezi Mngu (s.w.t) amesema:

﴿هُوَ الَّذِي جَعَلَ الشَّمْسَ ضِيَاءً وَالْقَمَرَ نُورًا وَقَدَّرَهُ مَنَازِلَ لِتَعْلَمُوا عَدَدَ السِّنِينَ وَالْحِسَابَ﴾

"Yeye ndiye aliyelijaalia Jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru na akaupimia vituo ili mjue idadi ya miaka na hisabu' (10:5)

Utauliza : kwa hiyo basi kupatikana usiku na mchana ni natija ya mzunguko wa ardhi , basi kuna wajihi gani wa kutegemeza kwa Mwenyezi Mungu?

Jibu : kwa sababu yeye ndiye Muumba mbingu na ardhi na kwake yeye ndio mwisho wa sababu zote , kwa hali yoyote ni kuwa makusudio ya kwanza ya kila yaliyokuja katika Aya hizi ni kuwa hakuna kitu katika vitu vya ulimwengu vilivyopatikana kwa sadfa na kibahati, isipokuwa kumetokana na aliye Mjuzi, Mwenye hekima aliyekipa kila kitu umbile lake na kukikadiria.

Hayo ndiyo makadirio ya weye nguvu, Mjuzi, Na Yeye ndiye aliyewafanyia nyota ili muongoke kwazo katika viza vya bara na baharini. Hakika tumezifafanua ishara kwa watu wanaojua.

Nyota hapa ni kutoa Jua na Mwezi kama inavyofahamika kutokana na mpangilio wa maneno. Katika kitabu Qur-an walilmul-hadith anasema bingwa wa falaki James Jentis: "Tunapotaka kujua nyumba fulani katika mji iko wapi tunauliza jina la mtaa kisha namba yake, basi ni hivyohivyo katika nyota, kwani katika hizo kuna zilizo maarufu kwa majina yake mahsusi nazo ni alama muhimu wanazozifuata mabaharia katika majahazi yao na waendeshao vyombo na wapanda wanyama. Ni misafara mingapi inyokwenda kwa ramani ya mbinguni na nyota wakati dira inapoacha kufanya kazi?"

Na Yeye ndiye aliyewaanzisha nyinyi kutokana na nafsi moja. Pako mahali pa kutulia na pa kupita njia. Hakika tumezifafanua ishara kwa watu wanaofahamu.

Nafsi iliyoumbwa kila moja kutokana nayo ni mtu wa kwanza ambaye watu wote wametokana naye ambaye ni Adam.

Tumezungumzia kwa ufafanuzi tulipofasiri Juz.4 (4:1) Razi ametaja kauli sita katika kufasirimahali pa kutulia na pa kupita njia .

Wafasiri wengi wamesema 'kutulia' ni kutulia manii katika migongo ya wanaume na 'pa kupita njia' kuwa katika matumbo ya uzazi ya wanawake. Katika Aya hakuna linalofahamisha hilo, wala lolote katika maana sita alizozinukuu Razi.

Imepokewa kutoka kwa Imam Sadiq(a.s) kwamba: yeye amegawanya waumini katika mafungu mawili; mwenye kuamini imani ya kweli inayotulia mpaka kufa, ambaye maneno yake yanaafikiana na vitendo vyake, na mumini ambaye imani yake inalegalega iko kwa muda tu, inamwondoka kabla ya kufa; maneno yake yanatofautiana na vitendo vyake.

Hakika tumezifafanua ishara kwa watu wanaofahamu.

Na asiyefahamu dalili hizi za ulimwengu juu ya ukuu wa muumbaji, mwanzilishi, basi huyo ni katika wale waliokusudiwa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿صُمٌّ بُكْمٌ عُمْيٌ فَهُمْ لَا يَعْقِلُونَ﴾

"Ni viziwi ni mabubu ni vipofu kwa hivyo hawafahamu" (2:171)

Naye ndiye aliyeteremsha maji kutoka mbinguni na kwayo tunatoa mimea ya kila kitu.

Mvua ndio chimbuko la maji tamu, lau si hiyo ardhi ingelikuwa kame isiyo na uhai. Mwenyezi Mungu ametegemeza kushuka maji kwake yeye, kwa sababu yeye ndiye msababishaji wa sababu, kwake huanza kila kitu hata kama mzunguko utakuwa mrefu kiasi gani.

Kisha tukatoa kutokana nayo kijani.

Dhamiri ya 'nayo' inarudia kwenye mimea. Makusudio ya kijani ni ubichi, yaani kutokana na mmea huchipua matawi mabichi. Inasemekana kuwa maana ya kijani hapa ni ubichi zaidi.

Tukatoa ndani yake punje zilizopandana.

Dhamiri ya 'ndani yake' ni ndani ya hiyo kijani, yaani tunatoa mashuke katika matawi kama vile ya ngano nk, na kama mfano wa, tunda la komamanga ambalo tembe zake zinapandana.

Na katika mitende yakatoka kwenye makole yake mashada yaliyo karibu.

Yaani ni rahisi kuyachuma au kuwa kukurubiana kwa wingi wake.

Na bustani za miabibu na mizaituni na mikomamanga.

Yaani tunatoa katika mimea aina hizi tatu. Mwenyezi Mungu amezitaja kwa njia ya kupigia mfano ambayo kutokana nazo itajulikana mingine.

Yanayofanana na yasiyofanana.

Katika mimea kuna inayofanana katika umbile na ladha na mingine haifananai.

Angalieni matunda yake yanapozaa na kuiva kwake.

Yaani zingatieni vipi linatoka tunda mwanzo, linakuwa dogo lisilo na manufaa kisha linabadilika badilika mpaka kuiva na kuwa na ladha tamu.

Hakika katika hayo kuna ishara kwa watu wanaoamini.

Makusudio ya wanaoamini siyo wale wanaoamini tu, bali ni wale wanaotikia mwito wa imani na kunufaika na dalili na hoja. Ama wenye nyoyo zilizofungwa wanazipita kama wanyama.

Kwa ufupi makusudio ya kwanza ya mifano hii ya ardhini na mbinguni ni kuleta uzindushi kuwa vitu vya ulimwengu huu na vilivyomo ndani yake vinatokana na uanzilishi na upangiliaji.

Ni muhali kuwa vimekuja kisadfa katika mtazamo wa kiakili na kimaumbile.

Hizo mbili zinahukumu kwa mkato kwamba kila liliopo limepatikana kwa matakwa na makusudio na kwa hekima ya hali ya juu anayoijua mjuzi na mjinga, wala hakuna kitu kinachobatilisha sadfa kama vile kukaririka tukio moja kila zinapokaririka sababu zake.

14

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿وَجَعَلُوا لِلَّـهِ شُرَكَاءَ الْجِنَّ وَخَلَقَهُمْ وَخَرَقُوا لَهُ بَنِينَ وَبَنَاتٍ بِغَيْرِ عِلْمٍ سُبْحَانَهُ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يَصِفُونَ﴾

100.Na wamemfanyia Mwenyezi Mungu washirika majini, Hali yeye amewaumba. Na wamemsingizia kuwa na wana wa kike na wa kiume bila ujuzi. Ametakasika na ametukuka juu ya hayo wanayombandikiza nayo.

﴿بَدِيعُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَنَّىٰ يَكُونُ لَهُ وَلَدٌ وَلَمْ تَكُن لَّهُ صَاحِبَةٌ وَخَلَقَ كُلَّ شَيْءٍ وَهُوَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ﴾

101.Mbunifu wa mbingu na ardhi. Inawezekanaje awe na mwana hali hana mke, Na ameumba kila kitu. Naye ni Mjuzi wa kila kitu.

﴿ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ فَاعْبُدُوهُ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ وَكِيلٌ﴾

102.Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu hakuna Mola (mwingine) isipokuwa Yeye; Muumba wa kila kitu, Kwa hivyo mwabuduni yeye. Na yeye ni mtegemewa wa kila kitu.

﴿لَّا تُدْرِكُهُ الْأَبْصَارُ وَهُوَ يُدْرِكُ الْأَبْصَارَ وَهُوَ اللَّطِيفُ الْخَبِيرُ﴾

103.Hayamfikii macho, Bali yeye huyafikia macho. Naye ni Mpole Mwenye habari.

﴿قَدْ جَاءَكُم بَصَائِرُ مِن رَّبِّكُمْ فَمَنْ أَبْصَرَ فَلِنَفْسِهِ وَمَنْ عَمِيَ فَعَلَيْهَا وَمَا أَنَا عَلَيْكُم بِحَفِيظٍ﴾

104.Hakika zimewajia busara kutoka kwa Mola wenu. Basi atakayefungua macho ni faida yake mwenyewe; na atakayeyapofua ni hasara yake mwenyewe, Nami si mtunzaji wenu.

﴿وَكَذَٰلِكَ نُصَرِّفُ الْآيَاتِ وَلِيَقُولُوا دَرَسْتَ وَلِنُبَيِّنَهُ لِقَوْمٍ يَعْلَمُونَ﴾

105.Na namna hii tunazifafanua ishara na waseme umesoma. Na ili tuyabainishe kwa watu wanaojua.

﴿اتَّبِعْ مَا أُوحِيَ إِلَيْكَ مِن رَّبِّكَ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ وَأَعْرِضْ عَنِ الْمُشْرِكِينَ﴾

106.Fuata uliyopewa wahyi kutoka kwa Mola wako. Hakuna Mola (mwingine) isipokuwa Yeye; na jitenge na washirikina.

﴿وَلَوْ شَاءَ اللَّـهُ مَا أَشْرَكُوا وَمَا جَعَلْنَاكَ عَلَيْهِمْ حَفِيظًا وَمَا أَنتَ عَلَيْهِم بِوَكِيلٍ﴾

107.Na kama Mwenyezi Mungu angetaka wasingeshirikisha. Na hatukukufanya uwe mtunzaji wao wala wewe si mlinzi juu yao.

WAMEMFANYIA MWENYEZI MUNGU WASHIRIKA

Aya 100-107

MAANA

Na wamemfanyia Mwenyezi Mungu washirika majini.

Washirikina wako aina nyingi, kuna waliofanya masanamu ni miungu, kuna walioabudu nyota, walioabudu Iblisi na waliofanya giza kuwa ni Mungu. Kundi jingine wamefanya majini kuwa ni washirika wa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu ameeleza kuwapo Malaika na kwamba amewaumba kutokana na moto.

Katika Aya tuliyo nayo Mwenyezi mungu ameeleza tu kikundi ambacho kimewafanya majini ni washirika wa Mwenyezi Mungu, lakini hakubainisha aina ya majini hawa walioabudiwa na washirikina, je ni majini wa kuwazia tu au ni wengineo?

Kwa ajili hii ndipo wafasiri wakatofautiana, Kuna waliosema ni Ibilisi wengine wakasema ni giza na mengineyo ambayo hayana msingi wowote wa kielimu kabisa.

Kwa maana yoyote itakavyokuwa ni kwamba Mwenyezi Mungu amewajibu washirikina hawa kwa kifupituHali yeye amewaumba , na dhamir ya Amewaumba inawarudia majini. kwani wao ndio walio karibu na hiyo dhamir.

Inawezekana kuwa inawarudia wshirikina au wote, kwa sababu Mwenyezi Mungu ameumba majini na watu; kwa maana yakuwa ni vipi Mwenyezi Mungu awe na washirika naye ni Muumba wa kila kitu?

Na wamemsingizia kuwa na wana wa kike na wa kiume bila ujuzi.

Washirikina wa kiarabu walisema kuwa malaika ni mabinti wa Mungu, Mayahudi wakasema Uzair ni mwana wa Mungu na wakristo wakasema Masih ni mwana wa Mungu Maneno yote hayo ni dhana na madai bila ya ujuzi.

Ametakasika na ametukuka juu ya wanayombandikiza nayo.

Ametakata Mwenyezi Mungu na upungufu na yuko juu kuliko wanavyomsifu nayo, Mbunifu wa mbingu na ardhi. Yaani ameziumba bila ya mfano uliotangulia.

Inawezekanaje awe na mwana hali hana mke wa jinsia yake wala wa jinsia nyingine, kwa sababu hana mfano na kitu kingine naye ni mwenye kujitosha na kila kitu. Umetangulia ufafanuzi katika kufasiri Juz.5 (4:50)

Na ameumba kila kitu.

Na muumbwa hawezi kuwa mshirika na Muumba.

Naye ni Mjuzi wa kila kitu.

Pamoja na hayo ati hajui kama ana mtoto; lau angekuwa naye angelimjua. Kwa hivyo kuacha kujua jambo hakumaanishi kutokuwepo kulingana na asiyekiuwa Mwenyezi Mungu. Ama kulingana na Mwenyezi Mungu ni kuwa ujuzi wake hauepukani na kupatikana yanayojulikana.

Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu hakuna Mola (mwingine) isipokuwa Yeye; Muumba wa kila kitu, Kwa hivyo mwabuduni yeye.

Msemo unaelekezwa kwa washirikina maana ni kuwa Mwenyezi Mungu amekusanya sifa zote za upweke, akaumba ulimwengu na vilivyomo na kupanga mambo yote basi yeye ndiye mwenye haki ya kumpwekesha kwa ibada wala msimshirikishe na yeyote pia msimnasibishie mke na mwana.

Hayamfikii macho.

Tumezungumzia kwa ufafanuzi kuhusu kumwona Mungu katika kufasiri Juz.1 (2:55)

Bali yeye huyafikia macho na mengineyo kwa sababu Yeye amekizunguka kila kitu.

Naye ni Mpole, Mwenye habari.

Mpole kwa waja wake, mwenye habari ya matendo yao na makusudio yao.

Hakika zimewajia busara kutoka kwa Mola wenu.

Makusudio ya busara hapa ni dalili na hoja za kuwepo Mwenyezi Mungu na kuwa Yeye ni mmoja, zikiwamo zile zilizotangulia kupasua mbegu na kokwa (konde), kuumba usiku na mchana, kuumba watu kutokana na nafsi moja na kuteremsha maji ambayo ni uhai wa kila kitu. Kutumia busara kuwa ni dalili ni katika hali ya kutumia kisababishi kuwa ni sababu. Kwani busara ni kujua kunakotokana na na moyo; na kujua huku kunatokana na dalili na hoja.

Basi atakayefungua macho ni faida yake mwenyewe; na atakayeyapofua ni hasara yake mwenyewe.

Baada ya kutoa dalili za mkato juu ya haki, hapa Mwenyezi Mungu anasema kuwa atakayefuata basi ameifanyia nafsi yake na atakayehalifu basi ameifanyia ubaya nafsi yake mwenyewe.

﴿إِنْ أَحْسَنتُمْ أَحْسَنتُمْ لِأَنفُسِكُمْ وَإِنْ أَسَأْتُمْ فَلَهَا﴾

"Mkifanya wema mnajifanyia wema nafsi zenu, mkifanya ubaya mnajifanyia nafsi zenu" (17:7)

Na namna hii tunazifafanua ishara na waseme umesoma. Na ili tuyabainishe kwa watu wanaojua.

Wakati wa Ujahiliyya Waarabu walikuwa hawajui kusoma, hawana elimu yoyote. Waliposikia Qur'an na wakaona fani za fasihi, aina kwa aina za hoja zinazowazima wao na yale wanayoyatukuza, Lakini bado waliendelea kukataa. Hali yao ilipokuwa hivyo walitafuta vijisababu wakasema: "Ewe Muhammad, Qur'an hii uliyokuja nayo umejifundisha tu wala sio Wahyi kutoka kwa Mungu".

Kwa maelekezo haya inatubainikia kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu: 'Na namna hii tunazifafanua ishara,' maana yake ni, tumetermsha katika Qur'an aina na dalili na ubainifu kwa makusudio ya kuongoka kwazo washirikina na waache kumwambia Mtume kuwa wewe umesoma.

Ama kauli yake: 'Ili tuyabainishe kwa watu wanaojua' maana yake ni tunazifanua Aya za Qur'an ili wanufaike nazo wale wanaojua maana yake uwaongoze kwenye imani na haki. Ama wajinga na wapotevu hakuna matarajio ya kuongoka kwao. mwisho wa mambo ni kuwa Aya hizi zinakata nyudhuru zao na kuwa ni hoja juu yao.

Fuata uliyopewa wahyi kutoka kwa Mola wako. Hakuna Mola (mwingine) isipokuwa Yeye; na jitenge na washirikina.

Hii ni amri ya Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake ya kuonya na kutoa bishara kwa Qur'an na kudumu juu ya hilo wala asijali ukanushaji wa washirikina na kukadhibisha na istihzai zao.

La kushangaza ni kauli ya asemaye kuwa Aya hii ni mansukh (imefutwa hukumu yake) na Aya ya kupigana. Mwenyezi Mungu hakumwamrisha Mtume kuacha kupigana na washirikina katika Aya hii mpaka isemwe kuwa ni mansukh ila amemwamrisha kufuatilila kuilingania haki na kutojali ukadhibishaji wa washirikina.

Kimsingi ni kuwa kulingania haki bila ya kujali ni jambo jingine na kupigana ni jambo jingine. Sharti ya kwanza ya naskh na mansukh (yenye kufuta na yenye kufutwa hukmu) ni kuwa maudhui yawe mamoja.

Na kama Mwenyezi Mungu angetaka wasingeshirikisha.

Yaani Yeye Mwenyezi Mungu mtukufu hakutaka kuwasukuma kwenye imani au kuwalazimisha kuacha ushirikina kwa neno 'kuwa ikawa' ambalo ameliumbia ulimwengu. Lau angelitaka waamini kwa matakwa haya basi wasingeshirikisha. Angalia tafsiri ya Juz.1 (2:26).

Na hatukukufanya uwe mtunzaji wao wala wewe si mlinzi juu yao.

Jumla ya kwanza na ya pili zina maana moja au maana yanayokurubiana wala hatufahamu lengo lolote la hilo isipokuwa kutilia mkazo; bali mkazo huu vilevile ni mkazo wa kauli yake: 'Na jitenge na washirikina.' Kwa sababu lau angelikuwa ni mtunzaji na mlinzi wao, basi isingelijuza kujitenga nao.

﴿إِنَّ إِلَيْنَا إِيَابَهُمْ ﴿٢٥﴾ ثُمَّ إِنَّ عَلَيْنَا حِسَابَهُم﴾

"Hakika ni kwetu sisi marejeo yao, kisha ni juu yetu sisi hesabu yao" (88:25-26)

﴿وَلَا تَسُبُّوا الَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ فَيَسُبُّوا اللَّـهَ عَدْوًا بِغَيْرِ عِلْمٍ كَذَٰلِكَ زَيَّنَّا لِكُلِّ أُمَّةٍ عَمَلَهُمْ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّهِم مَّرْجِعُهُمْ فَيُنَبِّئُهُم بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴾

108.Wala msiwatukane wale wanaoomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu wasije wakamtukana Mwenyezi Mungu kwa jeuri bila ya kujua, Kama hivyo tumewapambia kila umma vitendo vyao. Kisha marejeo yao yatakuwa kwa Mola wao, naye atawaambia yale waliyokuwa wakiyatenda.

﴿وَأَقْسَمُوا بِاللَّـهِ جَهْدَ أَيْمَانِهِمْ لَئِن جَاءَتْهُمْ آيَةٌ لَّيُؤْمِنُنَّ بِهَا قُلْ إِنَّمَا الْآيَاتُ عِندَ اللَّـهِ وَمَا يُشْعِرُكُمْ أَنَّهَا إِذَا جَاءَتْ لَا يُؤْمِنُونَ﴾

109.Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu kwa ukomo wa viapo vyao, kuwa ikiwafikia ishara bila shaka wataiamini. Hakika ishara ziko kwa Mwenyezi Mungu tu. Na ni kitu gani kitakachowatambulisha ya kuwa zitakapowafikia hawataamini?

﴿وَنُقَلِّبُ أَفْئِدَتَهُمْ وَأَبْصَارَهُمْ كَمَا لَمْ يُؤْمِنُوا بِهِ أَوَّلَ مَرَّةٍ وَنَذَرُهُمْ فِي طُغْيَانِهِمْ يَعْمَهُونَ﴾

110.Na tutazigeuza nyoyo zao na macho yao kama walivyokuwa hawakuamini mara ya kwanza, Na tutawaacha katika upotevu wao wakimangamanga.

MSIWATUKANE

Aya 108-109

MAANA

Wala msiwatukane wale wanaoomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu wasije wakamtukana Mwenyezi Mungu kwa jeuri bila ya kujua.

Wamesema kuwa Waislamu walikuwa wakiwatusi makafiri na wao huwajibu kwa kumtukana Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kauli hii haiko mbali sana na maana. Mara nyingi hutokea hivyo kwa wanaotofautiana kidini.

Tamko la Aya pia halilikatai hilo, bali imepokewa kutoka kwa Imam Jafar Aswadiq(a.s) kwamba aliulizwa kuhusu kauli ya Mtume:"Hakika shirki inajificha zaidi kuliko mtambao wa chungu kwenye jiwe jeusi katika usiku wa giza"

Akajibu:"Waumini walikuwa wakiwatukana wanaoabudiwa na washirikina na wakawa wanamtukana anayebudiwa na waumini. Waumini wakakatazwa kuwatukana waungu wao ili makafiri wasimtukane Mungu wa waumini.

Kama kwamba waumni wamemshirikisha Mwenyezi Mungu bila ya kujua, Kauli yake Mwenyezi Mungu 'bila ya kujua', Ni ishara ya ujinga wa washirikina. Katika Aya kuna ufahamisho wazi kuwa; ambalo lina madhara zaidi ya manufaa ni haramu na kwamba Mwenyezi Mungu hatiiwi anapoasiwa.

Kama hivyo tumewapambia kila umma vitendo vyao.

Maana ya dhahiri ya jumla hii ni kuwa Mwenyezi Mungu kama alivyowapambia vitendo vyao, vilevile amewapambia wengine vitendo vyao hata washirikina. Lakini hakuna mwenye shaka kwamba maana haya sio makusudio, kwa sababu Shetani ndiye anayewapambia washirikina uasi kwa nukuu ya Aya 43 ya Sura hii.

Zaidi ya hayo ni kuwa Mwenyezi Mungu hamwamrishi mja wake ukafiri na ampambie kisha amwadhibu, bali ni kinyume na hayo. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ حَبَّبَ إِلَيْكُمُ الْإِيمَانَ وَزَيَّنَهُ فِي قُلُوبِكُمْ وَكَرَّهَ إِلَيْكُمُ الْكُفْرَ وَالْفُسُوقَ وَالْعِصْيَانَ﴾

"Lakini Mwenyezi Mungu ameipendezesha kwenu imani na akaipamba nyoyoni mwenu na amewaafanya muuchukie ukafiri na ufasiki na uasi" (49:7)

Kwa ajili hii tunatilia nguvu kuichukulia Aya kuwa Mwenyezi Mungu amewaumba watu katika hali inayoona vizuri vitendo anavyovifanya mtu na inayokwenda na desturi na akampa akili ya kupambanua baya na zuri. Lau angeliwaumba katika hali ambayo inaona ubaya wa vitendo vyake vyote, asingelifanya chochote. Haya ndiyo maana ya kauli yake hiyo Mwenyezi Mungu: 'Tumewapambia kila umma vitendo vyao' sawa na kauli yake:

﴿كُلُّ حِزْبٍ بِمَا لَدَيْهِمْ فَرِحُونَ﴾

"Kila kundi linafurahia kwa waliyo nayo" (23:53)

Nasi tunasema: "Kila mtu huridhia amali yake".

Kisha marejeo yao yatakuwa kwa Mola wao, naye atawaambia yale waliyokuwa wakiyatenda.

Kwa hiyo waumini waache kutukana waungu wa washirikina, maadamu Mwenyezi Mungu atawaadhibu.

Unaweza kuuliza : kuwa anayemtukana Mwenyezi Mungu au Mtume wake ni wajibu kumuua, lakini mbona Aya hii inafahamisha kuwa ataachiwa hisabu yake na adhabu yake siku ya Kiyama?

Jibu : Aya hii ilishuka Makka, siku waislamu walipokuwa dhaifu, wakiwa bado hawajapewa ruhusa ya kupigana. Kwa sababu kupigana wakati huo kulikuwa ni kama kujiua. Ama ulipokuwa na nguvu Uislamu, ikawa ni wajibu kutekeleza hukumu ya kuuawa kwa mwenye kutukana; wala haijuzu kuchelewesha.

Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu kwa ukomo wa viapo vyao, kuwa ikiwafikia ishara bila shaka wataiamini.

Mwenyezi Mungu (swt) alimpa nguvu Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) kwa dalili za kutosha juu ya Utume wake, lakini washirikina wa Kikuraishi wakamtaka Muhammad(s.a.w.w) muujiza maalum na kufanya ndio sharti la kuamini kwao. Wakaapa kwa kiapo cha nguvu kuwa kama Muhammad atawakubalia maoni yao watamwamini. Ndipo Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume wake kuwaambia:

Hakika ishara ziko kwa Mwenyezi Mungu huziteremsha kwa hoja inayowasimamia wote. Zaidi ya hapo huteremsha au huacha kuteremsha kwa hekima yake na kupitisha kwake.

Waumini wakatamani Mwenyezi Mungu aitikie maombi ya makafiri kwa kuwataka wasilimu na waamini. Mwenyezi Mungu akawaambia kwa kauli yake:

Na ni kitu gani kitakachowatambulisha ya kuwa zitakapowafikia hawataamini?

Yaani kutoka wapi mmejua kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) akiteremsha muujiza waliotaka makafiri wataacha kufuru yao na inadi yao? Yametangulia maelezo kwa ufafanuzi katika kufasiri Sura hii, Aya 34 - 37 na katika kufasiri Juz.1 (2:118)

Na tutazigeuza nyoyo zao na macho yao kama kama walivyokuwa hawakuamini mara ya kwanza.

Tutazigeuza nyoyo zao na macho yao ni fumbo la kujua Mwenyezi Mungu hakika yao, Dhamir ya kumwamini inamrudia Muhammad au Qur'an. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu anajua kuwa washirikina hawataamini baada ya kushuka muujiza waliotaka, bali wao wataendelea kung'ang'ania upotevu wao wa kwanza waliokuwa nao kabla ya kushuka muujiza wanaoutaka. Wao ni watafutaji wa batili na upotevu, na wala sio watafutaji wa haki na uongofu.

Na tutawaacha katika upotevu wao wakimangamanga.

Yaani baada ya kung'anga'ania upotevu, pamoja na kusimamishiwa hoja, tutawaacha na upotevu wao mpaka ifike siku watakayopata malipo ya amali yao, Yamekaririka maana haya katika Aya kadhaa.

MWISHO WA JUZUU YA SABA

15

SHARTI YA KUCHAPA

Sharti ya kuchapa au kusambaza ni kutaja rejeo hili. haki zote zimehifadhiwa na Taasisi ya Al-Hasanain Taasisi ya Imamu Husein(a.s)

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini(a.s) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini.