MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU 0%

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU Mwandishi:
Kundi: Vitabu mbali mbali

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU

Mwandishi: NDUGU ZETU WA KISUNNI
Kundi:

Matembeleo: 44434
Pakua: 3442

Maelezo zaidi:

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 22 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 44434 / Pakua: 3442
Kiwango Kiwango Kiwango
MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU

Mwandishi:
Swahili

2

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU

SURA YA PILI

MAANA YA DINI KWA MTAZAMO WA MAKAFIRI

Makafiri wanatafsiri dini kuwa ni:

(i) "Imani inayohusiana na mambo ya kiroho baina ya binaadamu na Mwenyezi Mungu au njia ya kuhusiana na Mwenyezi Mungu" (Kamusi ya Kiswahili sanifu)

(ii) "Imani juu ya kuwepo Mungu Muumba aliye muweza na mwenye nguvu juu ya kila kitu, Mmiliki wa ulimwengu, ambaye amempa binaadamu roho ambayo huendelea kuishi baada ya kifo cha mwili" (Oxford Advanced Learner's Dictionary of Current English). Kutokana na tafsiri hii ya dini iliyonukuliwa kutoka kwenye kamusi ya Kiswahili na ya Kiingereza, tunajifunza mambo makubwa mawili:

Kwanza : kwa mtazamo wa makafiri dini inahusiana na imani ya kuwepo Allah (s.w). Hivyo wenye dini ni wale tu wanaoamini kuwepo kwa Allah (s.w), na wale wasioamini kuwepo kwake hawana dini. Ni katika mtazamo huu V. I. Lenin katika kitabu chake "Socialism and Religion (Ujamaa na Dini) amedai: "Everybody must be absolutely free to profess any religion he pleases or no religion whatever; i.e. to be an atheist which every socialist is as a rule..." Tafsiri:

"Kila mtu hanabudi kuwa huru kabisa kufuata dini yoyote anayotaka au asiwe na dini kabisa, yaani awe kafiri, jambo ambalo inambidi kila mjamaa awe kama sheria..."

Pili : kwa mtazamo wa makafiri, dini inahusiana na mambo ya kiroho au ulimwengu wa kiroho tu, na haihusiani kabisa na ulimwengu wa kimaada (wa vitu). Ni kwa mtazamo huu kwa makafiri, matendo ya wafuasi wa dini yamegawanywa katika sehemu mbili, matendo ya dini na matendo ya dunia. Katika mtazamo huu pia Waislamu hulaumiwa na makafiri kuwa wanachanganya dini na siasa, dini na uchumi; dini na utamaduni, na kadhalika.

MAANA YA DINI KWA MTAZAMO WA UISLAMU

Kwa mtazamo wa Uislamu"Dini" ni utaratibu wa maisha wanaoufuata binaadamu katika kuendesha maisha yao ya kila siku ya kibinafsi na kijamii.

Ni katika maana hii ya dini Allah (s.w) huuliza katika aya ifuatayo:

﴿أَفَغَيْرَ دِينِ اللَّـهِ يَبْغُونَ وَلَهُ أَسْلَمَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ طَوْعًا وَكَرْهًا وَإِلَيْهِ يُرْجَعُونَ﴾

"Je, (watu) wanataka dini isiyokuwa ya Mwenyezi Mungu na hali kila kilichomo mbinguni na ardhini kimejisalimisha kwake kipende kisipende. Na kwake watarejeshwa wote" (3:83)

Kutokana na aya hii tunajifunza kuwa:

Kwanza : kuna dini nyingi zinazofuatwa na watu hapa ulimwenguni, lakini dini iliyostahiki watu wenye "akili timamu" waichague, ni ile dini inayofuatwa na maumbile yote.

Pili : dini ya maumbile yote ya mbinguni na ardhini si nyingine, ila ni ile ya kujisalimisha katika kufuata sheria za maumbile alizoziweka Muumba. Tukirejea kwenye sayansi ya maumbile (natural science) tunajifunza kuwa kila kitu kilicho hai na kisicho hai (living and nonliving thing) ili kiwepo ni lazima kifungamane na sheria za maumbile za kibailojia, kifizikia na za kikemia (Biological, Physical and Chemical laws). Kwa mtazamo huu hata miili yetu pia imejisalisha kwa muumba kwa kufuata sheria za maumbile pasina hiari kama inavyosisitizwa katika aya ifuatayo:

﴿فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ حَنِيفًا فِطْرَتَ اللَّـهِ الَّتِي فَطَرَ النَّاسَ عَلَيْهَا لَا تَبْدِيلَ لِخَلْقِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴾

"Basi uelekeze uso wako katika dini iliyo sawa sawa ndilo umbile Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu (yaani dini hii ya Kiislamu inawafikiana bara bara na umbile la binaadamu).Hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe vya Mwenyezi Mungu.Hiyo ndio dini iliyo ya haki lakini watu wengi hawajui." (30:30)

Kwa ufupi, aya hii inatukumbusha kuwa miili yetu imejisalimisha kwa Allah (s.w) bila ya hiari kwa kufuata bara bara sheria za maumbile zinazofungamana na ufanyaji kazi wa kila kiungo cha mwili.Chakula kinayeyushwa tumboni, moyo unasukuma damu, mapafu, ini, figo, na viungo vingine mwilini hufanyakazi kwa kufuata sheria za Muumba na wala sio kwa kufuata sheria walizozitunga wanaadamu katika mabunge yao.

Tatu : Uislamu ni mfumo wa maisha uliofungamana na kanuni na sheria alizoziweka Muumba ili watu waendeshe maisha yao ya kibinafsi na kijamii sambamba na hali halisi ya maumbile yaliyowazunguka. Wale watakaoamua kwa hiari yao kufuata kanuni na sheria alizoziweka Allah (s.w) katika kukiendea kila kipengele cha maisha yao ya kila siku watakuwa ni Waislamu, waliojisalimisha kwa Muumba wao kama ilivyojisalimisha miili yao na maumbile yote ya mbinguni na ardhini. Hawa wataishi kwa furaha na amani hapa ulimwenguni, kwani wataepukana na maisha yale ya kupingana na maumbile yaliyowazunguka. Ama wale watakaokataa kufuata kanuni na sheria alizoziweka Muumba na badala yake wakaweka mfumo wa maisha unaopingana na kanuni na sheria hizo watakuwa ni makafiri, walioamua kupingana na maumbile yote yaliyowazunguka. Kwa vyovyote vile watakuwa wameamua kuishi maisha ya upinzani na vurugu.

Nne : kimantiki, ni lazima iwepo siku ya Hisabu ambapo watu wote watahudhurishwa mbele ya mahakama ya Muumba na Mmiliki wa maumbile yote, ili walipwe kutokana na uamuzi wao katika kuchagua na kufuata "dini". Wale waliojisalimisha kwa Allah (s.w) na kufuata "dini" yake, pamoja na kuishi maisha ya nuru (ya Amani na Heshima) hapa duniani, watakuwa na maisha ya furaha na amani ya kudumu huko Peponi. Ama wale waliompinga Allah (s.w) kwa kuweka na kufuata mifumo ya maisha kinyume na "dini" yake, pamoja na kuishi maisha ya giza (ya khofu na huzuni) hapa duniani, watakuwa na maisha ya dhiki na adhabu kubwa huko Motoni kama tunavyojifunza katika aya ifuatayo:

﴿اللَّـهُ وَلِيُّ الَّذِينَ آمَنُوا يُخْرِجُهُم مِّنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ وَالَّذِينَ كَفَرُوا أَوْلِيَاؤُهُمُ الطَّاغُوتُ يُخْرِجُونَهُم مِّنَ النُّورِ إِلَى الظُّلُمَاتِ أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ النَّارِ هُمْ فِيهَا خَالِدُونَ﴾

"Mwenyezi Mungu ni Mlinzi (kiongozi) wa wale walioamini. Huwatoa katika giza na kuwaingiza katika nuru.Lakini waliokufuru, walinzi (viongozi) wao ni Matwaghuut.Huwatoa katika nuru na kuwaingiza katika giza.Hao ndio watu wa Motoni, humo wakakaa milele". (2:257)

Mwanaadamu hawezi kuishi bila Dini Mwanaadamu hawezi kuishi bila dini kwa sababu zifuatazo:

(a) Maana halisi ya dini Tunaona kuwa maana halisi ya dini kwa mtazamo wa Qur'an ni utaratibu au mfumo wa maisha anaoufuata mwanaadamu katika kuendesha maisha yake ya kila siku. Hivyo kwa vyovyote vile mwanaadamu katika kuendesha maisha yake ya kila siku atakuwa anafuata dini moja au nyingine.Hana namna yoyote ya kuishi bila dini.

(b) Umbile la Mwanaadamu ni la kidini Ukizingatia maana halisi ya dini, kuwa dini ni utaratibu wa maisha, utadhihirikiwa kuwa umbile la mwanaadamu ni la kidini. Umbile la mwanaadamu kama maumbile mengine yaliyomzunguka hufuata mfumo maalum bila ya matashi au hiari ya mwanaadamu. Kwa maana nyingine umbile la mwanaadamu limedhibitiwa na sheria za maumbile (natural Laws - biological, chemical, and physical laws). Kwa mfano, ukichunguza hatua anazozipitia mwanaadamu katika tumbo la uzazi mpaka kuwa kiumbe kamili, ni utaratibu madhubuti ambao uko nje kabisa ya uwezo au matashi yake. Kuhusu kuumbwa kwa mwanaadamu Allah (s.w) anatukumbusha katika Qur-an:

﴿وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ مِن سُلَالَةٍ مِّن طِينٍ ﴿١٢﴾ ثُمَّ جَعَلْنَاهُ نُطْفَةً فِي قَرَارٍ مَّكِينٍ ﴿١٣﴾ ثُمَّ خَلَقْنَا النُّطْفَةَ عَلَقَةً فَخَلَقْنَا الْعَلَقَةَ مُضْغَةً فَخَلَقْنَا الْمُضْغَةَ عِظَامًا فَكَسَوْنَا الْعِظَامَ لَحْمًا ثُمَّ أَنشَأْنَاهُ خَلْقًا آخَرَ فَتَبَارَكَ اللَّـهُ أَحْسَنُ الْخَالِقِينَ﴾

Na kwa yakini tulimuumba mwanaadamu kwa udongo ulio safi, kisha tukamuumba kwa tone la manii lililowekwa katika makao yaliyohifadhika. Kisha tukalifanya tone hilo kuwa kitu chenye kuning'inia na tukakifanya hicho chenye kuning'inia kuwa pande la nyama, kisha tukalifanya pande hilo la nyama kuwa mifupa, na mifupa tukaivisha nyama,kisha tukamfanya kiumbe kingine. Basi Ametukuka Allah, Mbora wa waumbaji (23:12-14)

Si tu kuwa mwanaadamu hana mamlaka na kuzaliwa kwake, bali pia hana mamlaka na kukua kwake, na kufa kwake kama tunavyokumbushwa tena katika Qur-an:

﴿يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِن كُنتُمْ فِي رَيْبٍ مِّنَ الْبَعْثِ فَإِنَّا خَلَقْنَاكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ مِنْ عَلَقَةٍ ثُمَّ مِن مُّضْغَةٍ مُّخَلَّقَةٍ وَغَيْرِ مُخَلَّقَةٍ لِّنُبَيِّنَ لَكُمْ وَنُقِرُّ فِي الْأَرْحَامِ مَا نَشَاءُ إِلَىٰ أَجَلٍ مُّسَمًّى ثُمَّ نُخْرِجُكُمْ طِفْلًا ثُمَّ لِتَبْلُغُوا أَشُدَّكُمْ وَمِنكُم مَّن يُتَوَفَّىٰ وَمِنكُم مَّن يُرَدُّ إِلَىٰ أَرْذَلِ الْعُمُرِ لِكَيْلَا يَعْلَمَ مِن بَعْدِ عِلْمٍ شَيْئًا وَتَرَى الْأَرْضَ هَامِدَةً فَإِذَا أَنزَلْنَا عَلَيْهَا الْمَاءَ اهْتَزَّتْ وَرَبَتْ وَأَنبَتَتْ مِن كُلِّ زَوْجٍ بَهِيجٍ﴾

Enyi watu! Kama mumo katika shaka juu ya ufufuo, basi (tazameni namna tulivyokuumbeni)! Kwa hakika tulikuumbeni kwa udongo, kisha kwa manii, kisha kuwa kitu chenye kuning'inia, kisha kuwa kipande cha nyama kinachoumbika na kisichoumbika, ili tukubainishieni. Nasi tunakikalisha tumboni tunachokitaka mpaka muda uliowekwa, kisha tunakutoeni kwa hali ya utoto, kisha tunakuleeni mpaka mfikie baleghe yenu.Na kuna wanaokufa (kabla ya kufikia umri huu). Na katika nyinyi kuna wanaorudishwa katika umri dhalili, asijue chochote baada ya kule kujua kwake (22:5)

Aya hizi zinatukumbusha na kututhibitishia kuwa kuumbwa kwa mwanaadam, kukua kwake na kufa kwake hufuata utaratibu madhubuti uliowekwa na Muumba wake bila ya hiari yake.

Vile vile ukizingatia ufanyaji kazi wa mwili wa mwanaadamu utagundua kuwa mwili wa mwanadamu ni mashine ya ajabu inayofanya kazi kwa kufuata utaratibu uliofungamana na sheria madhubuti. Kwa mfano ukichunguza mwili wa mwanaadamu utakuta kuwa kuna mifumo mbali mbali kama vile mfumo wa usagaji chakula (digestion system), mfumo wa hewa (respiratory system), mfumo wa fahamu (nervous system), mfumo wa uzazi (reproduction system) na kadhalika. Mifumo hii hufanya kazi yake kwa kufuata utaratibu na sheria madhubuti nje kabisa ya mkono wa mwanaadamu. Utaona kuwa mwili wa mwanaadamu hufanya kazi yake na kumwezesha mwanaadamu kuwa katika hali ya uzima alionao, kwa kufuata sheria madhubuti za maumbile zilizowekwa na Muumba wake kama tunavyofahamishwa katika Qur-an:

﴿ فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ حَنِيفًا فِطْرَتَ اللَّـهِ الَّتِي فَطَرَ النَّاسَ عَلَيْهَا لَا تَبْدِيلَ لِخَلْقِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴾

Basi uelekeze uso wako katika dini iliyo sawa sawa - ndilo umbile Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu (yaani dini hii ya Kiislamu inaafikiana bara bara na umbile la binaadamu).Hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe vya Mwenyezi Mungu.Hiyo ndiyo dini ya Haki, lakini watu wengi hawajui. (30:30)

Katika aya hii tunajifunza kuwa mwili wa mwanaadamu hufuata dini ya Allah (s.w), yaani hufuata bara bara utaratibu au sharia madhubuti alizoweka Allah (s.w). Lakini mwanaadamu mwenyewe katika kuendesha maisha yake ya kila siku ana uhuru kamili wa kufuata dini ya Allah (s.w) kwa kufuata kwa ukamilifu na kwa unyenyekevu sharia madhubuti alizoziweka Allah (s.w) katika kukiendea kila kipengele cha maisha (rejea juzuu ya 2 EKP uk. 33 au kufuata dini za watu kwa kufuata utaratibu wa maisha walioufuma watu katika kukiendea kila kipengele) kinyume na utaratibu wa Allah (s.w). Na katika kuutumia uhuru huu,Allah (s.w) anamtanabahisha mwanaadamu.

﴿أَفَغَيْرَ دِينِ اللَّـهِ يَبْغُونَ وَلَهُ أَسْلَمَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ طَوْعًا وَكَرْهًا وَإِلَيْهِ يُرْجَعُونَ﴾

Je, wanataka dini isiyokuwa ya Mwenyezi Mungu na hali kila kilichomo mbinguni na ardhini kinamtii yeye, kipende kisipende?Na kwake watarejeshwa wote. (3:83).

Aya hii inamtanabahisha mwanaadamu ili achukue uamuzi wa busara wa kufuata dini ya Allah (s.w), ambayo dini hiyo ndiyo inayofuatwa na mwili wake na maumbile mengine yote yaliyomzunguka. Ni dhahiri kwamba atakapoamua kufuata dini nyingine yoyote isiyokuwa dini ya mwili wake, atakuwa ameamua kufuata utaratibu wa maisha unaopingana na umbile lake, na matokeo yake ni kukosa furaha na amani, katika maisha au kuishi maisha ya migongano, vurugu na huzuni.

(c) Vipawa vya Mwanaadamu Vipawa vya mwanaadamu ni sababu nyingine inayomfanya mwanaadamu asiweze kuishi bila ya kufuata dini moja au nyingine. Mwanaadamu anatofautiana sana na viumbe wengine, hasa katika suala la kufuata utaratibu wa maisha, kutokana na vipawa alivyotunukiwa na Muumba wake ambavyo hatuvioni kwa viumbe wengine. Vipawa hivi ni: -Akili na fahamu ya hali ya juu ambayo humwezesha kuwaza, kufikiri na kutafakari juu ya yeye mwenyewe na mazingira yake.

-Utambuzi wa binafsi (self consciousness) ambao humuwezesha mwanaadamu kufahamu mambo mbali mbali, kutambua mambo na kuyahusisha, kuyachambua, kuyalinganisha, n.k.

-Elimu (uwezo wa kujielimisha na kuelimika) ambayo humuwezesha mwanaadamu kufahamu mambo mbali mbali na kumuwezesha kutenda kwa ufanisi na kuwa na hadhi ya juu kuliko viumbe vyote.

-Huria (uhuru wa kuamua na kutenda atakavyo) - humuwezesha mwanaadamu kufuata utaratibu wa maisha anaoutaka. Vipawa hivi vyote kwa pamoja humtofautisha sana mwanaadamu na viumbe vingine. Humpa uwezo mkubwa na kumfanya auangalie ulimwengu na umbile lake pamoja na vyote vilivyomo kwa mtazamo wenye kutofautiana mno na ule wa viumbe wengine. Kwa mfano, kutokana na utambuzi binafsi (self consciousness) mwanaadam anatambua uhusiano wake na watu wa familia yake. Kuna baba, mama, dada, kaka, mke, watoto na ndugu wengine ambao anapaswa kushirikiana nao mpaka kufa. Hapa lazima mwanaadam aamue mwendo atakaoufuata ili kuwa na uhusiano unaostahiki baina yake na watu hawa.

Pia mwanaadamu ana uhusiano na watu wasio hesabika ulimwenguni, wengine ni majirani zake, wengine marafiki wengine ni maadui zake. Kuna wenye haki juu yake na wako wenye haki zake. Pia mwanaadamu ana uhusiano na viumbe vingine vyenye uhai na visivyo na uhai. Kwa ujumla vyote hivi vipo kwa kumsaidia yeye lakini mwanaadamu anapaswa aamue namna ya kuvitumia kwa manufaa yake yeye mwenyewe na wale wanaomzunguka.

Hivyo, ni dhahiri kuwa ni lazima mwanaadamu awe na njia iliyojenga mwenendo wake juu ya namna atakavyoshirikiana na wanaadamu wenziwe na viumbe vyote vinavyomzunguka kwa sababu katika hali halisi ya maumbile jambo hili la uhusiano haliendeshwi na silka (instinct) kama ilivyo kwa viumbe wengine.

Njia hii inayojenga mwenendo baina yake na mazingira yake ndio dini yake - njia yake ya maisha.

Pia mwanadamu ameumbwa katika namna ambayo hawezi kujitosheleza mwenye.Kwa namna moja au nyingine ni mwenye kuwategemea wanaadam wenziwe na viumbe vingine. Hivyo utaona kwamba mwanaadam hawezi kuishi bila ya kuwa na maingiliano na wanaadamu wenzake, viumbe vingine na mazingira yake yote kwa ujumla. Kutokana na sababu hiyo basi utaona kuwa kila mwanaadamu anafuata utaratibu wa maisha (dini) ambao hujenga uhusiano wa maisha baina yake na mazingira yake.

Suala lingine ni mwanaadamu kuwa na akili ya hali ya juu kuliko viumbe vingine vyote katika ardhi hii. Hatusemi kuwa wanyama hawana akili kabisa lakini sio katika daraja ya juu kama ilivyo akili ya wanaadamu. Kwao wao hitajio muhimu ni silka inayowawezesha kuishi na kuzaana na akili kama wanayo si hitajio kubwa kama lile la silka. Kazi yake ni kuwawezesha kutambua mahitajio yao ambayo ni lazima wayafuate ili waweze kuishi na kuzaana.

Swali ni kwamba; kwa nini mwanaadamu ana akili zaidi kuliko viumbe vingine (wanyama)? Kwa kweli hakuna sababu nyingine isipokuwa ni kumuwezesha mwaanadam kutambua njia ya maisha inayomfahamisha na kumuelekeza kwenye lengo la maisha yake hapa duniani. Mwanaadamu atakapoacha kutumia akili yake kwa kazi hii atakuwa hana tofauti na mnyama katika kuendesha maisha yake ya kila siku na wakati mwingine atakuwa na mwenendo mchafu zaidi kuliko ule wa mnyama kama Qur-an inavyotutanabahisha:

﴿وَلَقَدْ ذَرَأْنَا لِجَهَنَّمَ كَثِيرًا مِّنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ لَهُمْ قُلُوبٌ لَّا يَفْقَهُونَ بِهَا وَلَهُمْ أَعْيُنٌ لَّا يُبْصِرُونَ بِهَا وَلَهُمْ آذَانٌ لَّا يَسْمَعُونَ بِهَا أُولَـٰئِكَ كَالْأَنْعَامِ بَلْ هُمْ أَضَلُّ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْغَافِلُونَ﴾

Na bila shaka tumewaumbia moto wa Jahannam - wengi katika majini na watu (kwa sababu hii). Nyoyo (akili) wanazo lakini hawafahamu kwazo, macho wanayo lakini hawaoni kwayo, na masikio wanayo lakini hawasikii kwayo. Hao ni kama wanyama bali wao ni wapotofu zaidi. (7:179).

Kwa hiyo, mwanaadamu ana akili ya juu kuliko jamii ya viumbe vingine ili aweze kuamua ni njia gani ya maisha inayostahiki kufuatwa.

Hivyo, kutokana na vipawa alivyonavyo, mwanaadamu hujisaili maswali kama: Nini chanzo cha ulimwengu na nini lengo la kuwepo dunia na uhai wa mwanaadamu na ni vipi mwanadamu aishi ili afikie lengo hili? Maswali haya ni lazima yapatiwe majibu ili maisha yaweze kuwa na maana na muelekeo. Majibu yatakayotolewa ndio yatakayokuwa msingi wa dini ya mwenye kutoa majibu hayo. Kwa mfano kama mtu atatoa jawabu kuwa chanzo cha ulimwengu ni bahati nasibu (chance creation) yaani hauna muumbaji na uhai ikiwa ni pamoja na maisha ya mwanaadamu hauna lengo, basi mtu huyo atayajenga maisha yake juu ya msingi kwamba hakuna Mungu.Hivyo njia yake ya maisha au dini yake itakuwa ya kikafiri.

Kwa ujumla vipawa hivi vya hali ya juu alivyotunukiwa mwanaadamu, kuliko viumbe wengine humlazimisha mwanaadamu kufungika katika mfumo wa maisha ya kijamii katika kuendea kila kipengele cha maisha yake ya kila siku katika uchumi, siasa, utamaduni, na kadhalika. Mfumo huo wa maisha utakuwa ndio dini yake. Kwa mtazamo wa Uislamu tumeona kuwa dini ni utaratibu au mfumo wa maisha anaofuata binaadamu, katika kukiendea kila kipengele cha maisha yake ya kibinafsi na kijamii. Hivyo kwa vyovyote vile binaadamu katika kuendesha maisha yake ya kila siku atakuwa anafuata dini moja au nyingine. Akifuata mfumo wa maisha aliouweka Mwenyezi Mungu, ambao ni sawa na mfumo wa maisha unaofuatwa na maumbile yote (Qur-an 3:83) atakuwa anafuata Dini ya Kiislamu - dini ya kujisalimisha kwa Allah (s.w) kwa kufuata kanuni na sheria alizoziweka Allah (s.w) katika kukiendea kila kipengele cha maisha. Binaadamu akiamua kufuata mifumo ya maisha iliyojengwa kwa kanuni na sheria zilizowekwa na watu, zinazopingana na kanuni na sheria za Allah (s.w) atakuwa anafuata dini za Kikafiri - Mifumo ya maisha inayopingana na mfumo wa maisha aliouweka Allah (s.w).

Hivyo katika kuishi hapa duniani watu wanagawanyika katika makundi makuu mawili - kundi la Waislamu wanaoufuata mfumo wa maisha aliouweka Allah (s.w) na kundi la Makafiri wanaofuata mifumo ya maisha waliyoibuni watu kama inavyobainika katika Qur-an:

﴿هُوَ الَّذِي خَلَقَكُمْ فَمِنكُمْ كَافِرٌ وَمِنكُم مُّؤْمِنٌ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ﴾

"Yeye ndiye aliyekuumbeni (nyote).Wengine wenu ni Makafiri na wengine wenu ni Waislamu. Na Mwenyezi Mungu anayaona (yote) mnayoyafanya" (64:2)

Kwanini Uislamu Ndio Dini Pekee Inayostahiki Kufuatwa na Watu?

﴿الدِّينَ عِندَ اللَّـهِ الْإِسْلَامُ﴾

Hakika dini mbele ya Allah ni Uislamu..." (3:19)

﴿ فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ حَنِيفًا فِطْرَتَ اللَّـهِ الَّتِي فَطَرَ النَّاسَ عَلَيْهَا لَا تَبْدِيلَ لِخَلْقِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴾

"Basi uelekeze uso wako katika Dini iliyo ya haki kabla ya kufika hiyo siku isiyozuilika, inayotoka kwa Mwenyezi Mungu; siku hiyo watatengana (Waumini wende Peponi na Makafiri wende Motoni)." (30:43)

Kutokana na aya hizi tunajifunza kuwa pamoja na kuwepo dini nyingi (mifumo mingi ya maisha) hapa ulimwenguni dini ya Haki anayoiridhia Allah (s.w) ni Uislamu. Hivyo Uislamu ndio dini pekee inayostahiki kufuatwa na watu kwa sababu zifuatazo:

Kwanza : ndio dini ya kweli na ya uhakika kwa sababu imefumwa na Allah (s.w) aliye mjuzi wa kila kitu. Allah (s.w) ndiye aliyemuumba binaadamu kwa lengo maalumu, na hivyo ndiye pekee anayestahiki kumuwekea utaratibu wa maisha utakaomuwezesha kufikia lengo la kuumbwa kwake kwa wepesi. Tunakumbushwa katika Qur-an:

﴿سَبِّحِ اسْمَ رَبِّكَ الْأَعْلَى ﴿١﴾ الَّذِي خَلَقَ فَسَوَّىٰ ﴿٢﴾ وَالَّذِي قَدَّرَ فَهَدَىٰ﴾

"Litukuze jina la Mola wako aliye Mtukufu.Aliyeumba (kila kitu na) kukitengeneza na akakikadiria (kila kimoja lengo lake) na akakiongoza (kufikia lengo hilo)." (87:1-3)

Dini nyingine zote wanazofuata watu ni dini za upotofu kwa sababu zinabuniwa na wanaadamu wasio na ujuzi wala uwezo wa kazi hiyo. Mifumo yao ya maisha imefumwa kwa dhana wakiongozwa na matashi ya nafsi zao. Tujihadhari na wazushi hawa wa dini kama Allah (s.w) anavyotuasa:

﴿وَإِن تُطِعْ أَكْثَرَ مَن فِي الْأَرْضِ يُضِلُّوكَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ إِن يَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ وَإِنْ هُمْ إِلَّا يَخْرُصُونَ﴾

"Na kama ukiwatii wengi katika (hawa) waliomo ulimwenguni watakupoteza na njia ya Mwenyezi Mungu. Hawafuati ila dhana tu, na hawakuwa ila ni wenye kuzua (tu basi)." (6:116)

Pili : Uislamu ndio mfumo wa maisha pekee unaolandana na umbile la binaadamu na maumbile yote yaliyomzunguka. Yaani kanuni na sheria zilizowekwa na Uislamu zinakwenda sambamba na kanuni na sheria zinazofuatwa na maumbile yote, kwani mtunzi wake ni yule yule mmoja, Allah (s.w). Ni kwa msingi huu, Allah (s.w) anatanabahisha watu:

﴿أَفَغَيْرَ دِينِ اللَّـهِ يَبْغُونَ وَلَهُ أَسْلَمَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ طَوْعًا وَكَرْهًا وَإِلَيْهِ يُرْجَعُونَ﴾

"Je, (watu) wanataka dini isiyokuwa ya Mwenyezi Mungu na hali kila kilichomo mbinguni na ardhini kimejisalimisha kwake kipende kisipende?..." (3:83)

﴿فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ حَنِيفًا فِطْرَتَ اللَّـهِ الَّتِي فَطَرَ النَّاسَ عَلَيْهَا لَا تَبْدِيلَ لِخَلْقِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴾

"Basi uelekeze uso wako katika dini iliyo sawa sawa ndilo umbile Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu.Hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe vya Mwenyezi Mungu.Hiyo ndio dini iliyo ya Haki lakini watu wengi hawajui." (30:30).

Hivyo kwa kuwa Uislamu ni dini ya maumbile, ndio pekee inayoweza kuiongoza jamii kwa uadilifu na kuleta furaha na amani ya kweli.

Tatu : ndio dini pekee inayofuatwa na walimwengu wote wa sehemu zote na wa nyakati zote. Mitume wote wa Mwenyezi Mungu kuanzia Adam(a.s) mpaka kuishia kwa Muhammad(s.a.w.w) , wamefundisha na kufuata dini moja- Uislamu-kama tunavyokumbushwa katika aya zifuatazo:

﴿شَرَعَ لَكُم مِّنَ الدِّينِ مَا وَصَّىٰ بِهِ نُوحًا وَالَّذِي أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ وَمَا وَصَّيْنَا بِهِ إِبْرَاهِيمَ وَمُوسَىٰ وَعِيسَىٰ أَنْ أَقِيمُوا الدِّينَ وَلَا تَتَفَرَّقُوا فِيهِ﴾

"Amekupeni sheria ya dini ile ile aliyomuusia Nuhu, na Tuliyokufunulia wewe na Tuliyowausia Ibrahim na Mussa na Issa, kwamba simamisheni dini (Uislamu) wala msifarikiane kwayo..." (42:13)

﴿وَجَاهِدُوا فِي اللَّـهِ حَقَّ جِهَادِهِ هُوَ اجْتَبَاكُمْ وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ مِّلَّةَ أَبِيكُمْ إِبْرَاهِيمَ هُوَ سَمَّاكُمُ الْمُسْلِمِينَ مِن قَبْلُ وَفِي هَـٰذَا لِيَكُونَ الرَّسُولُ شَهِيدًا عَلَيْكُمْ وَتَكُونُوا شُهَدَاءَ عَلَى النَّاسِ﴾

"Na ipiganieni dini ya Mwenyezi Mungu kama inavyostahiki (kupiganiwa).Yeye amekuchagueni (muwe umma ulio bora). Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika dini.(Nayo dini hii) ni mila ya baba yenu Ibrahimu; yeye (Mwenyezi Mungu) alikuiteni Waislamu tangu (katika vitabu vya zamani) huko; na katika (Qur-an) hii pia (mumeitwa jina hilo) ili awe Mtume shahidi juu yenu na nyinyi muwe mashahidi juu ya watu (waliotangulia)..." (22:78).

Pia Uislamu ni dini isiyoruhusu ubaguzi wa aina yoyote kama tunavyokumbushwa katika aya ifuatayo:

﴿يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنَّا خَلَقْنَاكُم مِّن ذَكَرٍ وَأُنثَىٰ وَجَعَلْنَاكُمْ شُعُوبًا وَقَبَائِلَ لِتَعَارَفُوا إِنَّ أَكْرَمَكُمْ عِندَ اللَّـهِ أَتْقَاكُمْ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ﴾

"Enyi watu! Kwa hakika tumekuumbeni (nyote) kwa (yule) mwanamume (mmoja, Adam) na (yule yule) mwanamke (mmoja, Hawwa). Na tumekufanyieni mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane (tu basi). Hakika aheshimiwaye sana miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule amchaye Mungu zaidi katika nyinyi. Kwa yakini Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye habari (za mambo yote)." (49:13)

Nne : Uislamu ni utaratibu wa maisha uliokamilika.Uislamu unamuelekeza binaadamu namna ya kuendesha kila kipengele cha maisha yake ya kibinafsi na ya kijamii. Uislamu umeweka utaratibu unaozingatia watu kama walivyo. Kwa kutambua kuwa mtu anakamilika kwa kuwa na mwili na roho, Uislamu umeweka utaratibu wa kuustawisha mwili na roho. Uislamu umetuwekea kanuni na sheria zinazotuwezesha kujenga afya zetu na kukuza utu (ucha Mungu) wetu.

Pia, kwa kutambua kuwa watu ni viumbe wanaotakiwa waishi kijamii (social beings) na kutegemeana, Uislamu umetoa mwongozo na kuweka kanuni na sheria ambazo humuwezesha kila mtu binafsi na jamii kwa ujumla kuishi maisha ya furaha na amani. Uislamu umeweka mifumo ya kijamii kama vile siasa, uchumi, utamaduni, na kadhalika juu ya misingi ya haki na Uadilifu.

Tano : ni dini pekee inayomuongoza binaadamu namna ya kumiliki hisia zake.Uislamu unatuelekeza, tufanyeje tunapokuwa katika furaha kubwa. Kwa mfano Uislamu unatuelekeza kuwa tunapokuwa na sherehe, tule na kunywa vilivyo vizuri na halali lakini tusifanye israfu na tumtaje na kumsifu Allah (s.w) kwa wingi.

Pia Uislamu unatuelekeza la kufanya pindi tunapofikwa na jambo la kutuhuzunisha sana. Kwa mfano, Uislamu unatuelekeza kuwa tunapofikwa na msiba wa aina yoyote, tusubiri na tuone kuwa,hilo lililotokea ni katika Qadar ya Allah (s.w), kama tunavyokumbushwa katika aya zifuatazo:

﴿وَلَنَبْلُوَنَّكُم بِشَيْءٍ مِّنَ الْخَوْفِ وَالْجُوعِ وَنَقْصٍ مِّنَ الْأَمْوَالِ وَالْأَنفُسِ وَالثَّمَرَاتِ وَبَشِّرِ الصَّابِرِينَ ﴿١٥٥﴾ الَّذِينَ إِذَا أَصَابَتْهُم مُّصِيبَةٌ قَالُوا إِنَّا لِلَّـهِ وَإِنَّا إِلَيْهِ رَاجِعُونَ﴾

"Na Tutakutieni katika msuko suko wa hofu na njaa na upungufu wa mali na wa watu na wa matunda. Na wapashe habari njema wanaosubiri.Ambao uwapatapo msiba husema: Hakika Sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na kwake Yeye tutarejea".( 2:155- 156)

﴿مَا أَصَابَ مِن مُّصِيبَةٍ فِي الْأَرْضِ وَلَا فِي أَنفُسِكُمْ إِلَّا فِي كِتَابٍ مِّن قَبْلِ أَن نَّبْرَأَهَا إِنَّ ذَٰلِكَ عَلَى اللَّـهِ يَسِيرٌ ﴿٢٢﴾ لِّكَيْلَا تَأْسَوْا عَلَىٰ مَا فَاتَكُمْ وَلَا تَفْرَحُوا بِمَا آتَاكُمْ وَاللَّـهُ لَا يُحِبُّ كُلَّ مُخْتَالٍ فَخُورٍ﴾

"Hautokei msiba katika ardhi wala katika nafsi zenu ila umekwisha andikwa katika Kitabu kabla hatujaumba.Kwa yakini hilo ni sahali kwa Mwenyezi Mungu.Ili msihuzunike sana juu ya kitu kilichokupoteeni, wala msifurahi sana kwa alichokupeni. Na Mwenyezi Mungu hampendi kila ajivunaye, ajifaharishaye" (57:22-23)

Sita : Uislamu ni dini ya haki kama inavyobainika katika Qur-an:

﴿هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُونَ﴾

"Yeye (Allah (s.w) ndiye aliyemleta Mtume wake kwa uongofu na dini ya haki ili aijaalie (dini hii) kushinda dini zote ijapokuwa watachukia washirikina" (9:33)

Dini ya haki hapa ina maana kuu mbili;

Maana ya kwanza : ni kuwa Uislamu ni dini ya Allah (s.w), mjuzi na mwenye Hikima. Allah (s.w) ndiye anayestahiki kuwaundia binaadamu dini kwa kuwa ndiye aliyewaumba kwa lengo maalumu na kwa hiyo ndiye mwenye haki pekee ya kuwawekea wanaadamu utaratibu wa maisha na kuuambatanisha na mwongozo utakaowawezesha kufikia kwa ufanisi lengo hilo.

Maana ya pili : ni kuwa Uislamu ni dini ya kusimamia haki za binaadamu katika jamii kwa uadilifu kuliko dini yoyote ile. Mitume na Vitabu vya Allah (s.w) vimeshushwa ili kuwafundisha watu uadilifu na kuwaamuru wasimamishe uadilifu kama tunavyojifunza katika aya ifuatayo:

﴿لَقَدْ أَرْسَلْنَا رُسُلَنَا بِالْبَيِّنَاتِ وَأَنزَلْنَا مَعَهُمُ الْكِتَابَ وَالْمِيزَانَ لِيَقُومَ النَّاسُ بِالْقِسْطِ وَأَنزَلْنَا الْحَدِيدَ فِيهِ بَأْسٌ شَدِيدٌ وَمَنَافِعُ لِلنَّاسِ وَلِيَعْلَمَ اللَّـهُ مَن يَنصُرُهُ وَرُسُلَهُ بِالْغَيْبِ إِنَّ اللَّـهَ قَوِيٌّ عَزِيزٌ﴾

"Kwa hakika tuliwapeleka Mitume wetu kwa dalili wazi wazi na Tukaviteremsha vitabu na uadilifu pamoja nao, ili watu wasimamie uadilifu. Na tumekiteremsha (tumekiumba) chuma chenye nguvu nyingi na manufaa kwa watu, na ili Mwenyezi Mungu ajulishe anayemnusuru na Mitume yake na hali ya kuwa hawamuoni Mwenyezi Mungu.Kwa yakini Mwenyezi Mungu ni mwenye nguvu mwenye kushinda" (57:25).

Katika aya hii tunajifunza kuwa silaha zinatokana na chuma na aina nyingine za madini, nani zana zinazotakaiwa zitumiwe na waumini ili kusimamisha haki na uadilifu katika jamii. Katika aya nyingi za Qur-an waumini wa Kiislamu wameamrishwa kupigana na madhalimu ili kuhakikisha haki inapatikana katika jamii kwa kila raia kama tunavyojifunza katika aya zifuatazo:

﴿فَلْيُقَاتِلْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ الَّذِينَ يَشْرُونَ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا بِالْآخِرَةِ وَمَن يُقَاتِلْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَيُقْتَلْ أَوْ يَغْلِبْ فَسَوْفَ نُؤْتِيهِ أَجْرًا عَظِيمًا ﴿٧٤﴾وَمَا لَكُمْ لَا تُقَاتِلُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَالْمُسْتَضْعَفِينَ مِنَ الرِّجَالِ وَالنِّسَاءِ وَالْوِلْدَانِ الَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا أَخْرِجْنَا مِنْ هَـٰذِهِ الْقَرْيَةِ الظَّالِمِ أَهْلُهَا وَاجْعَل لَّنَا مِن لَّدُنكَ وَلِيًّا وَاجْعَل لَّنَا مِن لَّدُنكَ نَصِيرًا﴾

Basi nawapigane katika njia ya Mwenyezi Mungu wale wanaouza maisha (yao) ya dunia kwa (kununua) ya Akhera.Na anayepigana katika njia ya Mwenyezi Mungu kisha akauawa au akashinda, tutampa ujira mkuu). Na mna nini hampigani katika njia ya Mwenyezi Mungu na (katika kuwaokoa) wale walio dhaifu - katika wanaume na wanawake na watoto - ambao husema: "Mola wetu! Tutoe katika mji huu ambao watu wake ni madhalimu, na tujaalie tuwe tuna mlinzi anaetoka kwako." (4:74-75).

Wale walioamini wanapigana katika njia ya Mwenyezi Mungu, lakini waliokufuru wanapigana katika njia ya (Twaghuut).

﴿فَقَاتِلُوا أَوْلِيَاءَ الشَّيْطَانِ إِنَّ كَيْدَ الشَّيْطَانِ كَانَ ضَعِيفًا﴾

Basi piganeni na marafiki wa Shetani. Hakika hila za Shetani ni dhaifu. (4:76).

Saba : Uislamu ni mfumo wa maisha pekee ulioweka utaratibu wa kumbakisha binaadamu katika maadili ya utu. Uislamu umemuwekea binaadamu ibada maalumu zenye lengo la kumtakasa na kumuwezesha kuwa na maadili mema yatakayopelekea kujenga mazingira ya furaha na amani katika jamii. Ibada hizi maalumu ni Swala, Zakat, Saum, Hija, n.k. Namna ibada hizi zinavyofanya kazi katika kumbakisha binaadamu katika maadili ya utu imefafanuliwa vyema katika kitabu cha pili (Nguzo za Uislamu).

Sababu hizi tano za msingi, zatosha kuwa vigezo vya kumfanya mtu achague Uislamu kuwa utaratibu pekee wa maisha wa kufuata katika kuendea kila kipengele cha maisha yake. Dini zote zilizoundwa na watu, zimekosa kabisa sifa hizi na ni zenye kumhasirisha binaadamu katika maisha ya dunia na akhera.Na hata mazingira yetu yanathibisha hili.

﴿وَمَن يَبْتَغِ غَيْرَ الْإِسْلَامِ دِينًا فَلَن يُقْبَلَ مِنْهُ وَهُوَ فِي الْآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ﴾

"Na anayetaka dini isiyokuwa ya Kiislamu basi haitakubaliwa kwake.Naye akhera atakuwa katika wenye khasara (kubwa kabisa) (3:85)

ZOEZI

2 1. (a) Maana ya dini kwa mtazamo wa Makafiri ni.............................

(b) Maana ya dini kwa mtazamo wa Uislamu ni............................

2. Katika kuishi hapa duniani watu wamegawanyika makundi makubwa mawili:

(i).............................

(ii).................................................

3. Kwa mtazamo wa Uislamu hakuna mtu anayeishi bila ya kufuata dini moja au nyingine kwa sababu: .....................................

4. Uislamu ndio dini pekee inayostahiki kufuatwa na watu kwa sababu tano zifuatazo: (i)...................................

(ii)....................................

(iii)....................................

(iv)...................................

(v)...................................

(vi)...................................

(vii)..................................

5. Kwanini Mwanadamu hawezi kuunda mfumo wa maisha utakao watendea haki na uadilifu walimwengu wote?