MUANDAMO WA MWEZI

MUANDAMO WA MWEZI 18%

MUANDAMO WA MWEZI Mwandishi:
Kundi: Midahalo na majadiliano kielimu

MUANDAMO WA MWEZI
  • Anza
  • Iliyopita
  • 23 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 62342 / Pakua: 6745
Kiwango Kiwango Kiwango
MUANDAMO WA MWEZI

MUANDAMO WA MWEZI

Mwandishi:
Swahili

1

3

MUANDAMO WA MWEZI

SEHEMU YA TATU

IKHTILAFU SIO UPINZANI

MNASEMA

"3. Ikhtilafu Sio Upinzani Tunapenda kumfahamisha ndugu Juma kwamba mara nyingi inaweza kutokezea katika jambo moja watu kutofautiana lakini hawapingani. Ni vyema kuelewa kwamba upinzani umo katika Siasa za kilimwengu na mambo mengine sio katika masuala ya Dini. Katika Dini hutokea Ikhtilafu. Masahaba (Radhiya Allaahu 'Anhum) pia walikuwa wakikhitilafiana katika baadhi ya mambo, lakini hawakuwa wakipingana. Kila mmoja aliweza kushika mwendo wake bila kugombana na mwenzake. Ama pale ulipotokea upinzani kwa bahati mbaya - jambo hilo liliwapelekea kugombana au kupigana vita, kwani jambo hilo ni katika amali za Kishetani. Lakini mara walipotanabahi juu ya udhaifu huo waliomba toba kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na kutakana misamaha baina yao Na huo bila shaka ndio mwendo wa watu wema.

Kwa bahati nzuri semina na makongano yote yaliyofanyika ndani na nje ya Zanzibar hapajatokea kuitwa 'pinzani' wala neno 'upinzani' halijatumika hata mara moja. Bali semina zote zilizowahi kufanyika zimekuwa zikisisitiza maneno ya 'umoja' na 'kuelimishana' wala sio 'kupingana.'

Neno 'upinzani' haliko katika midomo ya Wanavyuoni. Tanasikitika sana kuwa Ndugu yetu Juma Muhammad Rashid amelitumia neno ambalo si zuri la 'upinzani' na kulikariri katika kitabu chake zaidi ya mara 33. Kwa kweli hizo si kauli za wenye busara na hikma, bali ni kama alivyozoea kuzitumia. Kwa mfano pale alipokuwa akimlalamikia Shaykh Naaswir Bachuu, alisema: (Tazama pia katika uk. 109-110 uone upinzani alioutoa hapo halafu linganisha upinzani huo na upinzani alioutoa kabla ya hapo, utaona jinsi gani mwanamume alivyokuwa bingwa wa kubadilika! Na hili si jengine bali ni lile Waswahili wanalolisema: "Mfa maji hukamata maji.")

Tunamshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwamba kwa upande wa hapa kwetu Tanzania watu wanaruhusiwa kufunga na kufungua kwa mujibu wa misimamo yao (yote miwili) bila ya kugombana. Swala za 'Iyd kwa upande wa watu wanaofuata mwezi unapoonekana popote duniani wamekuwa wakiswali misikitini na viwanjani bila ya bughudha yoyote. Bali hata katika familia moja yenye misimamo hiyo tofauti, watu hawagombani. Huko ndiko kukhitilafiana sio kupingana".

JAWABU

Nakubaliana na nyinyi sana kwamba ikhtilafu si ugomvi. Lakini nyinyi wenyewe mutakumbuka kwamba munasisitiza kufata wanavyuoni. Wanavyuoni wa Kiislamu wanapozungumzia rai tafauti hutumia maneno haya: "Na ikapingwa kauli hii". Au:"Upinzani wa mwanzo ni kadha wa kadha..". Au: Na wakasema wale watupingao au waliotafauti na sisi. Au "Wakavutana". Au "Wamesukumana". Hizi ndio lugha za wanavyuoni na mimi nimechukua kutoka kwao. Nao kwa lugha hizo huwa hawakusudi kwamba kulikuwa na ugonvi, bali wanakusudia kwa kumekuwa ikhtilafu. Kwa hivyo, mimi sijakusudia upinzani kwa maana ya ugonvi, bali naku sudia kutokuafiki rai au kauli Fulani, na hilo ni jambo linalosemwa na wajuzi.

SEHEMU YA NNE

JUMA AMPINGA AL-IMAMU AL-SHAUKANI

MNASEMA 4.

Ndugu Juma Anampinga Al- Imam Shawkani Jambo jengine la kusikitisha ni kuwa ndugu Juma haonyeshi kuwaheshimu Wanavyuoni au kuwapa hadhi zao wanazostahiki. Wanavyuoni wana heshima zao hata pale wanapokosea. Ni vyema kuelewa kwamba Al Imam Shawkani alikuwa ni miongoni mwa Wanavyuoni wakubwa kama ilivyoelezwa kwenye historia yake fupi katika kitabu cha "Kuandama Kwa Mwezi" cha Shaykh Naaswir Bachuu Uk 35. Al Imam Shawkani aliandika vitabu vingi vya kukubalika pamoja na Tafsiri yake ya Qur-aan Tukufu inayojulikana kwa jina la "Fathul Qadir."

JAWABU

Al-Imamu Al-Shawkani - bali hata aliye chini ya yeye sana kwa elimu - ninamuheshimu sana. Na katika kitabu changu nimemnukuu kwa kumpa laqabu anayostahiki. Sehemu nyingi nimemwita Imamu. Huku ni kukikiri kuwa ni mtu wa maarifa mapana kwani Imamu hawi mtu yeyote bali ni yule aliyekusanya zana nyingi za elimu. Labda sehemu moja tu nilimwita Sheikh, nayo pia ni laqabu ya heshima. Sasa vipi munasema kwamba simpi heshima yake. Tukumbuke kwamba kumuheshimu mwanachuoni, si maana yake kwamba tusimpinge au kujadili maneno yake. Kufanya hivyo si kumuheshimu bali ni kumtakasa, nalo ni kosa. Pili: kwani nyinyi wale Maimamu wakubwa munaowapinga katika suala hili la muandamo wa mwezi huwa ndio mumewavunjia heshima yao?

MNASEMA

Ndugu Juma katika kujikweza kama kwamba yeye ana elimu kubwa zaidi na kwamba anakubalika zaidi kuliko Al Imam Shawkani, anathubutu kusema: ((Huo ndio upinzani wa pili wa Al-imamu Al-shaukaniy, lakini kama unavyoona jawabu yetu ya kwanza inajibu baadhi ya nukta zilizomo katika upinzani huu.)) [ uk : 111]". Kisha akamfananisha Al Imam Shawkani na watu wa kawaida (yaani labda ni mtu wa mitaani asiyekuwa na elimu) kwa kusema: ((Maneno haya ya Al-imamu Al-shaukaniy - kama yalivyo maneno ya watu wengi wa kawaida.))

JAWABU

Haya! Ubaya uko wapi hapa? Sasa nyinyi ndio munamuheshimu au munamtakasa. Kwani nani kasema kuwa mwenye elimu hajibiwi katika kutafuta haki? Ikiwa Ibn Abbaas kapingwa na watu ambao hawamuoni hata vumbi lake, itakujakuwa Al-Imamu Al-Shawkani. Kwani Sheikh Bachoo yeye katika hicho kitabu chake si anawapinga wanavyuoni wote waliotangulia Afrika Mashariki, au tuseme na yeye anajikweza na kujifanya ana elimu?! Kwa kweli haya ni maneno ya aliyefilisika: asiye na hoja.

Ama kauli yenu: "Kisha akamfananisha Al Imam Shawkani na watu wa kawaida (yaani labda ni mtu wa mitaani asiyekuwa na elimu)" hayana maana, kwani nimesema: ((Maneno haya ya Al-imamu Al-shaukaniy - kama yalivyo maneno ya watu wengi wa kawaida.)). Sasa sijui ni mtu gani wa mitaani aliye na daraja ya uimamu! Enyi walimwengu! Hebu fahamuni munayoyasoma. Mimi nafananisha kauli na kauli: si mtu na mtu. Al-Shawkani nimempa hadhi yake ya uimamu, lakini alichokisema hakikubaliki kwani hakina dalili za kisharia. Au munataka tuchukue tu kwa sababu msemaji ni fulani bila ya kutazama kilichosemwa?

MNASEMA

Ndugu Juma katika kumuandama Al Imam Shawkani anaendelea kusema: ((Penye andiko huwa hapana ijtihadi;)) kama kwamba Al Imam Shawkani alikuwa hajui Qur-aan wala Hadiyth. Au kama kwamba Al Imam Shawkani anampinga Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

Jawabu Inaonekana nyinyi muko mashariki na elimu iko magharibi! Tafadhali fungeni safari muifate. Kauli ya Imamu yeyote awaye inarejeshwa katika dalili za kisharia. Maimamu wanakosea pia na mifano iko mingi. Na kutajia mifano mitatu tu:

1) Al-Imamu Al-Nawawi kunukuu Hadithi ifatayo:

"Tulikuwa tunasafiri pamoja na Mtume(s.a.w.w) , miongoni mwetu wako waliofunga na wako waliokula, na wako waliotimiza (rakaa za Sala) na wako waliopunguza. Basi aliyefunga hakumtia kasoro asiyefunga; wala asiyefunga (hakumtia kasoro) aliyefunga; wala aliyepunguza (rakaa katika Sala) (hakumtia kasoro) aliyetimiza; wala aliyetimiza (hakumtia kasoro) aliyepunguza." Hadithi hii kainukuu Al-imamu Al-nawawi katika Sharhu Sahihi Muslim na akainasibisha na Sahaba Abi Said Al-khudriy katika masimulizi ya Muslim katika Sahih yake. Wakati Hadithi hii haimo katika Sahihu Muslim. Hadithi ya Abi Said Al-khudriy alioiashiria Al-imamu Al-nawawi - katika mlango huo huo - ni Hadithi na. 95/2612, nayo inasema: "Tulikuwa tunasafiri pamoja na Mtume(s.a.w.w) katika mwezi wa Ramadhani. Hakumtia aibu aliyefunga kutokana na aliyekula, wala aliyekula kwa sababu ya kula kwake."

Na mfano wa Hadithi hii ni Hadithi na. 93/2610 na 96 /26134 na Hadithi nyengine tatu zinazofata mpaka mwisho wa mlango huo, wala hakuna maneno yanayosema: "Wala (hakumtia aibu) aliyepunguza (rakaa katika Sala) juu ya aliyetimiza; wala aliyetimiza juu ya aliyepunguza:" maneno haya hayamo katika Hadithi hio ya Muslim, bali kilichomo ni mas-ala ya kufunga na kutokufunga tu kwa msafiri katika mwezi wa Ramadhani. Na kwa sababu hii ndio maana Al-Shaukaniy akampinga Al-imamu Al-nawawi kwa maelezo yake hayo. Je tuseme Al-Imamu Al-Shawkani naye kafanya kosa kumpinga Al-Imamu Al-Nawawi, au kafanya wajibu wake wa kudhihirisha haki. Na je Al-Imamu Al-Nawawi kawa ndio si mwanachuoni tena kwa sababu hapa kakosea?! Fahamu ziko wapi?!!!!!!!!

Ibn Hisham: Ibn Hisham Al-Ansari ni bingwa mkubwa wa lugha. Katika kitabu chake Qatru Al-Nada anasema kwamba miongoni mwa sharti za kufanya kazi masdar ni kuwa baina yake na mtendwa wake pasiwe na kitu kilichokaa katikati. Anasema (Sharti) ya saba ni kuwa (ili masdar ifanye kazi) basi isiwe yenye kupambanuliwa kutokana na mtendwa wake. Na kwa hivyo, (w atu wa Nahau) wakairejesha kauli ya aliyesema kwamba (neno yawma katika Aya: Yawma tubla Al-Sarair ni mtendwa wa neno "Raj'ihi", kwani baina yao pamekuwa na upambanuzi kwa kuwekwa khabar.

Hayo ni maneno ya Ibn Hisham pamoja na kundi la wanavyuoni. Sasa someni Aya hii:

Neno It'am ni masdar; na neno yatiman na miskinan ni watendwa wa Masdar hio. Hata Ibn Hisham mwenyewe alipoingia kueleza migawanyiko ya masdar 'aamil katoa mfano wa Aya hii hii. Haya je tumfate Ibn Hisham au tufate dalili za kielimu? Na je Ibn Hisha tayari kageuka kuwa mtu wa mitaani kwa sababu hapa kakosea? Kwa hivyo, wanavyuoni wanakosea, na wanapokosea na sisi pakitubainikia kwa dalili sahihi kuwa hili ni kosa huwa tunazinduana kuwa hili ni kosa, hata akiwa aliyelifanya ni nani, wala huko hukumpunguzii mwanachuoni kima chake, kwani hakuna asiyekosea. Na nadhani hivyo ndivyo Uislamu unavyotutaka.

Al-Hafidh Ibn Hajar: Kuna Hadithi inasema: "(Kasimulia Abu Said Al-Khudri) kwamba kikundi cha Masahaba wa Mtume (s.a.w.) walipita kwa kabila moja la Kiarabu, mtu mmoja kati yao akadonolewa (na ng'e), wakasema: 'Kuna mzinguaji kati yenu?' Mmoja wao akamzingua kwa Al-Hamdu. Basi akapewa kikundi cha ghanam (kondoo au mbuzi) akakataa kukichukua. Wakaja kwa Mtume(s.a.w.w) wakamtajia hayo, akasema: 'Aliyechukua kwa zinguo la batili (ndiye aliye chukua haramu), (ama wewe) kwa hakika umechukua kwa zinguo la haki. Chukueni na mie munipe sehemu yangu". Hadithi hii pia kaipokea Al-Bukhari kutoka kwa Abu Sa'id bin Al-Mu'allah na kutoka kwa Ibn Ibn Abbas kwa lafdhi tafauti kidogo.

Al-Hafidh Ibn Hajar kawakosoa waliosema kuwa Hadithi hii imesimuliwa kutoka kwa Abu Sa'id Al-Khudri. Anasema Ibn Hajar: "Al-Ghazali na Al-Fakhr Al-Razi wakifatiwa na Al-Baydhawi wamekinasibisha kisa hiki kwa Abu Sa'id Al-Khudri nalo ni kosa, bali yeye (mwenye kisa hiki) ni Abu Sa'id Al-Mu'alla". Tazama Fat-hu Al-Bari j. 9, uk. 5076, katika sherehe ya Hadithi na. 4474. Nami nasema: lakini maelezo hayo ya Ibn Hajar ya kuwakosoa Al-Ghazali, Al-Razi na Al-Baydhawi, bado ni maelezo ya kufirikiwa kwani kisa hiki kimesimuliwa pia na Muslim Hadithi na. 2201, na Abu Dawud Hadithi na. 3415 na wengine kutoka kwa Abu Sa'id Al-Khudri. Kwa hivyo, Al-Ghazali na wenziwe hawakukosea isipokuwa ikiwa Ibn Hajar anadai kuwa sanad hizo ni dhaifu na ya Al-Bukhari yenye kusema kuwa muhusika alikuwa ni Abu Sa'id Al-Mu'allah ndio sanad sahihi.

Utaona kwamba Ibn Hajar kawakosoa wanavyuoni wengine. Wakati pia na yeye kakosea katika kuwakosoa huko kwani walivyosema wao ndivyo ilivyo katika Sahihu Muslim. Sasa tusema wanavyuoni hawa wakubwa tayari wameshakuwa watu wa mitaani kwa kukosowana huku? Jamani! Sisi tumeambiwa tuwaheshimu Maulamaa: sio tuwatakase na kwamba hata mtu akikosea asiambiwe. Sasa kama kanuni inayokubalika kwa Umma mzima inasema: "Penye andiko huwa hapana ijtihadi", je Al-Imamu Al-Shawkani akenda kinyume na kanuni asirejeshwe kwa sababu yeye ni mwanachuoni mkubwa. Nakukumbusheni maneno yenu yaliomo kitabuni mwenu muliposema: "Kutegemea maneno, matupu ya mwanachuoni kama ni Khaas bila ya kuonyesha dalili zenye kukubalika kifani, huo utakuwa ni udhaifu". Haya mumeyasema nyinyi kuzipinga kauli za wanavyuo ni musiokubaliana nao. Sasa vipi munanilaumu kwa kitu mukitendacho?!

Ingelikwa dharau lau nilisema kuwa Al-Shawkani hana akijuacho. Na mimi ni nani hata niseme kuwa Al-Shawkani hajui?! Mimi nadai kuwa hapa kakosea. Sasa nyinyi, ili iwe mumenijibu basi mubainishe kuwa: "Aa si kweli hakukokesea, na kanuni hio si kweli haipo". Hapo itakuwa mumenijibu. Lakin munaleta maneno ya mtu aliyefilisika na hoja munasema: "Kama kwamba Al Imam Shawkani alikuwa hajui Qur-aan wala Hadiyth. Au kama kwamba Al Imam Shawkani anampinga Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)". Kwani nyinyi hao munaowapinga munaitakidi kuwa hawajui Qur-ani na Hadithi au wanampinga Allaah na Mtume Wake(s.a.w.w) , au kwa sababu munahisi kuwa wamejitahidi na kukosea? Kwanini nyinyi mujiweke katika dhana safi na wenzenu muwaweke kwenye dhana mbovu?

Munasema Angalia katika kitabu chake Ndugu Juma kwenye uk 108 - 109 ameeleza misimamo ya Wanazuoni wawili mashuhuri; yaani Al Imam Badru Din na Shaykh Al Khalil ambao wamejaribu kuukosoa msimamo wa Al Imam Shawkan lakini kwa njia nzuri. Wote wawili wameonyesha kwamba ile ni Ijtihadi ya Al- Imam Shawkani katika kumfahamu Ibni ''Abbas katika kisa cha Kuraib wala hawakumfanya Al Imam Shawkani kama ni mpinzani. Ni vyema kuelewa pia kwamba wanaweza kutokea Wanavyuoni wengine wanaoweza kusema pia kwamba na hizo ni Ijtihadi za Al Imam Badru Din na Shaykh Al Khalil katika kumfahamu Al Imam Shawkani. Wala huwezi kusema kuwa Al Imam Shawakani alikuwa halifahamu andiko, Shaykh Al Khalil ndio amelifahamu andiko. Hizo zote ni Ijtihadi katika kukifahamu kisa cha Kuraib.

Jawabu Hapa hakuna sula la nani analifahamu andiko, suala ni kuwa mujibu wa Usulul Hadithi (elimu ya Hadithi), maneno ya Ibn Abbbaas yasemayo: "Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume(s.a.w.w) ," je yanazingatiwa kuwa ni Hadithi au si Hadithi? Hakuna hapa suala la kumfata Al-Imamu Al-Shawkani wala Al-Imamu Al-Khalili wala Imamu atayekuja: wote wanarejeshwa katika kanuni (pr iciples) zile zile na hakuna mwenye uwezo wa kuwa juu ya kanuni: kanuni ziko juu ya wote. Kwa hivyo, sisi tulipompinga Al-Imamu Al-Shawkani na kumuunga mkono Al-Imamu Badru Al-Din, si kwa sababu yule ni Al-Shawkani na huyu ni Al-Khalili au kwa sababu yule ni mtu wa madhehebu iliotafauti na yetu, bali ni kuwa huyu kasema kitu kilicho sawa na kanuni za Hadithi; yule kenda kinyume na kanuni. Pamoja na hayo, hatupingi ijtihadi ya Al-Imamu Al-Shawkani.

SEHEMU YA TANO

NDUGU JUMA ANATOA RAI BINAFSI

Munasema 5. Ndugu Juma Anatoa Rai Binafsi Katika kitabu chake alichokiandika, Ndugu Juma ameonyesha udhaifu wake wa kulazimisha kujaribu kujibu hoja za kitabu cha Shaykh Naaswir Bachuu. Maneno yake mengi yametawaliwa na ubinafsi. Hakupenda kuwa muadilifu katika kueleza hoja zake ingawa yeye mwenyewe anapokwama kihoja hujifanya kumgomba Shaykh Naaswir Bachuu huku akimwambia: (Kwa ufupi ni kuwa hii ni hoja ambayo haina faida yoyote ya kielimu, lakini tunaijadili kwa ajili ya watu wa mitaani tu).

Jawabu Hizo ni tuhuma zenu baada ya kushindwa kujibu hoja zangu. Sijui nani anayejilazimisha kujibu hoja na ambaye anakwama? Na hayo maneno: (Kwa ufupi ni kuwa hii ni hoja ambayo haina faida yoyote ya kielimu, lakini tunaijadili kwa ajili ya watu wa mitaani tu), niliyatoa baada kuwa nimeshajibu hoja au nilisema hivyo tu ikawa basi? Sasa asiyemuadilifu ni mimi au nyinyi ambao munataka kuonesha kitu tafauti na kilivyo. Mimi niliyasema hayo baada ya kuwa nimeshajibu, kisha ndio nikabainisha kwamba kielimu - yaani kwa watu wa mustawa wa elimu - suala hilo alililolileta Sheikh Nassor Bachoo halina maana lakini kulijadili kwangu ni kwa kuzingatia akili za watu wa mitaani. Nyinyi mumeyachukua maneno haya na kufanya kuwa ni ushahidi kuwa sikujibu bali nimekwama. Munadhani mutawadanganya watu na watu vitabu vyote wanavyo?!

MNASEMA

Ni kweli kwamba mlango wa Ijtihadi uko wazi, lakini si vyema katika wakati wetu huu mtu kutoa rai binafsi za kujikweza bila kunukuu hoja za Wanazuoni waliotangulia tena wanaokubalika. Katika kitabu cha Shaykh Naaswir Bachuu kuna hoja nyingi mno zilizotajwa kutoka kwenye vitabu vya Wanazuoni wakubwa ambao wameonyesha misimamo mbali mbali juu ya maudhui haya ya muandamo wa mwezi, lakini Ndugu Juma hakuijibu hata moja zaidi ya kumponda Al Imam Shawkani. Angalia misimamo ya Wanazuoni waliotajwa katika kitabu cha 'Kuandama Kwa Mwezi' cha Shaykh Naaswir Bachuu uk 5 - 11, 51 - 56, 59 - 74, 129 - 133. Pia angalia: 'Makubaliano Katika Mikutano Ya Wanavyuoni' yalivyoelezwa ambayo ndugu Juma ameyafumbia macho uk 134 - 155.

JAWABU

Kwanza mimi si mujtahid, kwa hivyo huo mlango uko wazi kwa mujtahidin. Ikiwa nyinyi wenzangu mumefikia daraja hio, basi musiwache kuupita mlango huo ili nasi tufaidike kwa ijtihada zenu. Lakini maandishi yenu yanaonesha kuwa hata daraja talabatul 'Ilmi hamujafikia. Pili ni kuwa aliyefikia daraja ya ijtihad halazimiki kunukuu maneno ya wanavyuoni wengine. Hata akinukuu basi hanukuu kwamba ndio dalili yake bali ni kuonesha kuwa wako waliosema kauli kadha. Kwa hivyo, kauli yenu: "Lakini si vyema katika wakati wetu huu mtu kutoa rai binafsi za kujikweza bila kunukuu hoja za Wanazuoni waliotangulia tena wanaokubalika" si kauli sahihi. Tatu: Hata mujtahid si kwamba ana haki ya kusema kitu kinyume na kanuni za lugha na usuli. Nakusudia kanuni walizokubaliana Umma mzima au zisizopingana na Qur-ani na Suna.

Nne: Katika mjadala huwa hapategemewi fulani kanena, bali panategemea dalili za Kisharia na maneno ya fulani hurudishwa katika dalili za kisharia. Na hicho ndicho nilichokifanya. Nakukumbusheni kauli yenu muliposema: "Kutegemea maneno, matupu ya mwanachuoni kama ni Khaas bila ya kuonyesha dalili zenye kukubalika kifani, huo utakuwa ni udhaifu". Na wanavyuoni nimewanukuu wengi. Lakini narudia tena kauli za wanavyuoni ni hoja pale walipokubaliana: si walipotafautiana. Wakitafautiana, basi huwa kauli zao si hoja, bali kila mmoja anaambiwa lete hoja ya Kisharia.

Sasa mimi hata nikinukuu wanavyuoni wa dunia nzima, ikiwa sikutoa ushahidi unaokubalika kielimu ni kazi bure. Ama Al-Imamu Al-Shaukani yeye tumeyajadili maneno yake kiurefu kwa vile Sheikh Bachoo na wengine wameonekana kuyategemea zaidi maneno yake. Na pia Al-Shawkani ndiye aliyeijadili Hadithi husika kwa urefu kulikoni wengine. Ama madai yenu muliposema: "Kumponda Al Imam Shawkani". Mimi nakanusha kwa nguvu dai hilo, mimi sijamponda bali sikukubaliana naye kwa vile nimeona hoja alizotoa ni kinyume na kanuni za Hadithi na Usuliil Fiq-hi. Sasa ili nanyi muwe mumenisomesha basi onesheni kuwa hoja zake ni sawa kwa mujibu wa kanuni za Hadithi na Usulil-Fiq-hi.

MUNASEMA

Angalia Ndugu Juma alivyokuwa akijenga baadhi ya hoja zake binafsi (za umimi) pale aliposema: (Nasi tunasema kwamba Aya ndio, lakini hoja yake katika Aya hio ni hoja dhaifu sana .) [uk. 71] ((Isipokuwa upinzani ambao - mimi kwa upande wangu - nauona kuwa una muelekeo juu ya tafsiri hii tulioitoa hapa,)) [uk. 62] Ziko wapi hapa hoja za Wanavyuoni wanaokubalika zaidi ya kudai: (Mimi kwa upande wangu nauona) au: (Ninasema bila shaka)

JAWABU

Na nyinyi munasema: "Sisi tunamjibu hivi.." wala hakuna mwanachuoni aliyejibu hivyo mulivyojibu nyinyi, ni rai zenu binafsi tu. Kwa hivyo, na nyinyi muna ubinafsi. Aidhan Sheikh Bachoo anasema: "Ni kweli kwamba msimamo wa upande wetu". Mimi sioni tafauti ya maneno "Sisi" au "Nasi" na maneno "Upande wetu" zote ni dhamiri (pronouns) za ubinafsi. Kwa hivyo, kosa hili nimejifunza kutoka kwenu. Ama kauli yangu (Isipokuwa upinzani ambao - mimi kwa upande wangu - nauona kuwa una muelekeo juu ya tafsiri hii tulioitoa hapa)". Ninasema:

1) Kama hilo nimelisema kwa mtazamo wangu, mulitaka niwadanganye watu niwambie hivi ndivyo walivyosema wanavyuoni. Mimi sighushi kama munavyofanya mimi: langu nasema kuwa hili ni langu; na la wanavyuoni nasema kuwa hili kalinena fulani.

2) Pili ni kuwa mulitakiwa munukuu kile nilichokisema kisha mukijibu kama mulikusudia kutafuta ukweli. Lakini hamukufanya hivyo, na badala yake munatafuta kitu ambacho munadhania kuwa hiki kitamtia aibu Juma ndio munataja. Sasa nikisema ninavyoona mimi, kitu gani kilichokuwa haramu hapa ni hii kauli au ni yale nilioyasema. Kama ni hii kauli, basi uharamuu wanaufanya wanavyuoni wote wa Umma, kwani kwenye rai zao binafsi husema: Au yaani ninavyoona mimi. Kama uharamu uko katika yale nilioyasema, tafadhali yanukuuni kisha muyajadili na kubainisha kosa liko wapi.

3) Tatu ni kuwa narudia tena kwamba kitabu cha mjadala huwa hakitegemei kauli za wanavyuoni, bali huwa kinajadili mambo kwa mujibu wa misingi yake ya kilugha na kiusuli na hivi ndivyo nilivyofanya. Sasa kama nyinyi munadai kuwa nimekosea kwa mujibu wa fani hizi, tafadhali nukuuni maneno yangu na muonesha kosa liko wapi.

4

MUANDAMO WA MWEZI

SEHEMU YA SITA

MUANDAMO WA KIFALAKI NA MUANDAMO WA KISHARI'AH

UTANGULIZI MFUPI JUU YA SEHEMU HII

Kabla sijaendelea na kunukuu jawabu niliojibiwa na ndugu zangu kuhusu maudhui ya sehemu hii, ni vyema kwanza ninukuu nilioyasema katika kitabu ambayo wao ndio wanayajadili. Kufanya hivyo, ni kuwawezesha wasomaji kuona udhifu uko wapi. Katika kitabu, chini ya anwani

MUANDAMO WA KIFALAKI NI NINI?

nilisema yafatayo: Ni ukweli usiopingika kwamba ufahamu sahihi wa kitu chochote kile unafungamana mfungano wa nguvu na walazima na ufahamu wa dhana (concept) yake sahihi. Kwa hivyo, ni kawaida kwamba muhubiri anapohubiri juu ya maudhui fulani, kwa mfano jografia, kama hakufafanua tangu mwanzo na kuweka wazi, basi suala la kwanza ataloulizwa ni "Jografia ni nini?"

Maudhui yetu katika sehemu hii ni hii dhana sahihi ya muandamo wa mwezi: je kuandama kwa mwezi ni nini katika dhana yake ya uhakika? Qur-an Tukufu, imeashiria muandamo wa mwezi katika baadhi ya Aya zake. Na hii ni pale Allah Aliposema:"Na Mwezi tumeupimia vituo mpaka ukarejea (kuwa mwembamba) kama karara kongwe (la mtende) . Na anasema Allah :"Yeye (Allah) Ndiye aliyelifanya jua kua muanga na mwezi kua nuru na akaupimia (huo mwezi) vituo, ili mujue idadi ya miaka na hisabu."

MAELEZO JUU YA AYA HIZI

Aya mbili hizi zinathibitisha kwamba mwezi una Manazil (vituo) ambayo hupitia ndani yake. Watu wa elimu ya falaki wanasema kwamba Manazil haya ni ishirini na nane ambayo yamo katika Buruji (constellations) kumi na mbili. Majina ya buruji hizo ni:

1) Al-hamal (Aries, Kondoo dume).

2) Al-thaur (Taurus. Ngo'mbe dume).

3) Al-jawzaa (Gemini. Mapacha).

4) Al-sartan (Cancer. Kaa).

5) Al-asad (Leo. Simba).

6) Al-sunbula (Virgo. Mashuke).

7) Al-mizan (Libra. Mezani).

8) Al-a'qrab (Scorpio. Nge).

9) Al-qaws (Sagittarius. Upinde).

10) Al-jadyu (Capricon. Mtoto wa mbuzi).

11) Al-dalwu (Aquarius. Ndoo).

12) Al-hut (Pisces. Samaki).

Hayo ndio majina ya buruji kumi na mbili, kwa mujibu wa wanaojihusisha na elimu za falaki. Buruji hizo kumi na mbili zina vituo ishirini na nane (28). Kila Buruji moja ina vituo viwili na thuluth. Vituo hivyo ni:

1) Al-shartan. 2) Al-butain. 3) Al-thurayya. 4) Al-dabran. 5) Al-haq'a. 6) Al-han'a. 7) Al-dhiraa. 8) Al-nnathra. 9) Al-ttarf. 10) Al-jabha. 11) Al-kharatan. 12) Al-sarfa. 13) Al-awaa. 14) Al-simak. 15) Al-ghafr. 16) Al-zubanayan. 17) Al-iklil. 18) Al-qalb. 19) Al-shaula. 20) Al-na'aim. 21) Al-baladda. 22) Sa'adu Al-dhabih. 23) Sa'adu Bula'a. 24) Sa'du Su'ud. 25) Sa'ad Al-akhbiya. 26) Al-far'u Al-muqaddam. 27) Al-far'u Al-muakkhar. 28). Batnu Al-hut.

Haya ndio majina ya manazil ishirini na nane kwa mujibu wa wataalamu wa falaki. Kilichomashuhuri katika vitabu vingi vya kale ambavyo vimezungumzia mas-ala haya ni kuwa buruji ya kwanza ambayo ni Al-hamal (Aries), vituo vyake ni: Al-shartan, Al-butain na thuluthi moja ya Al-thuraya. Miongoni mwa hawa ni Al-qurtubiy kama ilivyo katika tafsiri yake. Na hivyo ndivyo walivyosema wengi wengineo ambao nimebahatika kuona maandishi yao juu ya maudhui hii. Lakini hata hivyo mmoja wa wataalamu wetu waliokuweko Zanzibar, naye ni Sheikh Yusuf alikuwa anasema kwamba buruji haziko thabiti (not constant), bali kila miaka sabiini (70), zinaondoka na kujongea mbele, jambo ambalo linazifanya kuingia katika manazil mengine baada ya miaka. Hatimae nikaikuta kauli hii imo katika kitabu "AHKAMU AL-HAKIM" cha mwanachuoni mashuhuri wa falaki wa Misri Al-ustadh Abdul-fattah Al-sayyid Al-tukhi Al-falaki. Anasema: "Jua kwamba manazil (vituo) ni zile nyota tunazoziona usiku. Na waliotangulia walikuwa wakiziita nyota thabiti (fixed stars), kwa sababu ya kudhani kwao kwamba zimesimama kwa ajili ya kwenda kwake kidogo kidogo. Lakini elimu ya sasa imegundua kwamba zinakwenda lakini kidogo kidogo sana ambapo zinakata daraja moja (one degree) katika (kipindi cha) miaka 66 taqriban." Mwisho wa kunukuu.

Kauli ya Sheikh Yusuf inaashiria kwamba labda yeye anaamini kwamba majina ya manazil ni zile sehemu zilizokaa nyota: si ule mkusanyiko wenyewe wa nyota (constellation). Kwa hali yoyote ile - kumbu kumbu yangu - ni kuwa kwa mujibu wake, Manazil (vituo) hayo tulioyataja kuwa ni ya Al-hamal - nayo ni Al-shartan, Al-butain na thuluth Al-thuraya - kwa sasa yamo katika buruji ya Al-thaur (Taurus. Ngo'mbe dume). Kauli yake hii inawafikiana na kauli ya Al-tukhi katika kitabu chake hicho.

Mwezi unakata kila kituo kimoja kwa muda wa siku moja, ikimaanisha kwamba siku ishirini na nane (28), huwa umekamilisha safari yake. Na hapo hufichika kidogo kwa siku moja au mbili kisha hudhihiri na kuonekana tena duniani. Suala ni kuwa je kukamilika huku kwa mzunguko wa mwezi ndio muandamo wa mwezi Kisharia? Umejua - kutokana na hayo yaliotangulia - kwamba mwezi unakamilisha mzunguko wake kwa muda wa siku ishirini na nane (28), na ili uonekane duniani unahitaji kupitiwa na siku moja au mbili. Kuanzia hapa utaanza kujua tafauti baina ya muandamo wa mwezi kisharia na muandamo wake kifalaki. Pia utaanza kuona namna gani Sh. Nassor Bachoo katika kitabu chake alivyochanganya baina ya hali mbili hizi wakati alipokuwa akizungumzia maudhui hii.

MAELEZO YA SH. NASSOR BACHOO

Sh. Nassor Bachoo ni mmoja wa Wazanzibari waliojitokeza kuzungumzia mas-ala haya. Katika kitabu chake, Sheikh kaizungumzia maudhui hii na akanukuu Aya ya 5 ya Sura ya 10 ambayo ni ya pili katika Aya tulizozinukuu kabla. Baada ya maelezo alisema: "Qur-an inalieleza suala la kuandama kwa mwezi kama ni tukio moja wapo kati ya matukio yaliyopangwa na Mwenyezi Mungu kutukia kila mwezi mara moja duniani kote." Mwisho wa kunukuu.

Ukianzia uk. 5. hadi uk. 8, wa kitabu chake, utaona kwamba Sh. Nassor Bachoo anathibitisha mwenendo wa mwezi kupitia katika Manazil (vituo) yake. Ufupisho wake - kama tulivyotangulia kusema - ni kuwa mwezi unasafiri kwa muda wa siku ishirini na nane (28) kupitia katika vituo hivyo, na siku moja au mbili hupotea kisha kudhihiri na kuweza kuonekana duniani. Sheikh aliishia maneno yake kwa kusema: "Baada ya maelezo haya tunatumai tumeweza kuelewa mtazamo wa Qur-an juu ya kuandama kwa mwezi." Mwisho wa kunukuu. Sasa ukitazama sentensi mbili hizi za Sh. Bachoo, utaona kuwa anakusudia kuthibitisha kitu kimoja kwa Aya ambayo haimpatii malengo yake. Anachokusudia kukithibitisha Sh. Bachoo - kwa inavyoonesha kutokana na maandishi yake - ni kuwa muandamo ni mmoja duniani kote na kwa hivyo - bila shaka anakusudia kusema - kwamba sote tufunge kwa muandamo mmoja huo. Ndio maana akasema: "Qur-an inaeleza suala la kuandama kwa mwezi kama ni tukio moja wapo kati ya matukio yaliopangwa na Mwenyezi Mungu kutukia kila mwezi mara moja duniani kote." Lakini dai kwamba Qur-an inasema kuwa muandamo wa mwezi unatokea mara moja tu dunia nzima - ikiwa anakusudia muandamo wa kisharia nao bila shaka ndio anaouzungumzia - si sahihi. Na sijui wapi Qur-an imesema hivi?!

Qur-an imezungumzia muandamo wa mwezi katika hali mbili: Hali ya kwanza: ni ya muandamo wa kifalaki. Na huu sio ule tunaouita muandamo. Hapa tutatumia tu neno "Muandamo" kwa ajili ya kufahamiana. Huu ndio ambao unazungumziwa na Aya hizo tulizotangulia kuzinukuu. Na ndio unaotokea mara moja duniani kote. Hali ya pili: ni ya muandamo wa Kisharia. Huu umetajwa katika Aya ya 189 ya Sura ya 2, ambapo Allah anasema:

"Wanakuuliza kuhusu miezi miandamo. Sema hivyo ni vipimo kwa ajili ya watu na Hija." Sasa katika Aya zote mbili hizi hakuna ufafanuzi wowote wenye kuonesha kwamba muandamo wa mwezi wa kisharia ni mmoja au vipi? Bali Aya hii ya pili, inaonesha tu kwamba katika Sharia kuna kitu miandamo ya mwezi. Lakini vipi miandamo hio: hakuna ufafanuzi wowote ule uliotolewa katika Aya hii. Kwa hivyo madai hayo ya Sh. Nassor Bachoo kwamba Qur-an inasema kwamba muandamo ni mmoja ni kitu kimoja na maelekezo ya Aya ni kitu chengine.

Kwa kufahamu zaidi ni kuwa Aya alioitolea ushahidi juu ya fikra yake, inasema:"Yeye (Allah) Ndiye aliyelifanya jua kua muanga na mwezi kua nuru na akaupimia (huo mwezi) vituo, ili mujue idadi ya miaka na hisabu."

Sasa utaona kwamba Aya hii imetaja vitu viwili: jua na mwezi. Na vyote hivi vinazunguka katika falaki (orbits) zake na vinapita katika manazil (vituo) yale yale na vinapita katika buruji (constellations) zile zile. Sasa cha kustaajabisha ni kuwa vipi Sh. Nassor Bachoo ajenge hoja kwa Aya hii kuthibitisha muandamo mmoja na asijenge hoja kwa Aya hii kuthibitisha wakati (time) mmoja wa kusali?! Ninachokusudia kukisema ni kuwa Aya imetaja kwamba Allah ndiye aliyeumba jua na mwezi. Kisha akataja Illa (sa babu) ya kuumba vitu viwili hivyo. Akasema"Ili mupate kujua idadi ya miaka na hisabu (nyengine)." Kwa lugha nyengine sababu ya kuumbwa jua na mwezi, ni kutuwezesha kudhibiti hisabu za miaka na hisabu za mambo mengine. Sasa kama sababu hii - kwa mujibu wa Sheikh Nassor Bachoo - ndio iliohalalisha au kuwajibisha kuuzingatia muandamo mmoja wa mwezi duniani kote kwa mujibu wa Aya hii, kipi kimeharamisha kuuzingatia mtenguko mmoja wa jua kuwa ni alama ya kuthibitisha wakati mmoja wa sala duniani kote, wakati Aya hii kama ilivyoutaja mwezi kuwa ni chombo cha kudhibitia wakati ndivyo ilivyolitaja jua kwa lengo hilo hilo?

Ubainifu wa haya ni kuwa kama Mtume(s.a.w.w) alivyosema kwamba:fungeni kwa kuuona mwezi, vivyo hivyo ndivyo alivyosema Allah"Salini kwa kutenguka jua." Na Aya hio aliotunakilia Sh. Nassor Bachoo inazungumzia mambo yote mawili jua na mwezi. Kwa hivyo, ilitakiwa fiq-hi ya Sh. Bachoo iliojengeka juu ya Aya hio, ilihusishe jua kama ilivyouhusisha mwezi, kwani Aya inazungumzia mwenendo wa jua na mwezi. Na kwa hivyo, jua likitenguka Makka watu wa Zanzibar wasali?!

Kuanzia hapa utaanza kuona kwamba Aya hio ni kitu kimoja na fikra ya Sh. Nassor Bachoo ni kitu chengine. Qur-an imeeleza tu kwamba mzunguko wa jua na mwezi ni kwa ajili ya kujua miaka na hisabu, na miandamo ya mwezi ni vipimo vya nyakati na Hija: haikufafanua kwamba mwezi wa kisharia unaandama mara moja au kumi na moja. Ufafanuzi huu unaweza kupatikana baada ya kuzikusanya dalili zote zinazohusu maudhui hii kutoka katika Hadithi. Ama Qur-an Aya zake katika maudhui hii ni Mujmala (hazikufafanuliwa).

Baada ya haya, utaona kwamba tatizo sugu kwa walio wengi ni kutokutafautisha baina ya muandamo wa mwezi kifalaki (astronomically) na muandamo wake Kisharia. Muandamo wa kifalaki ni kutimiza kwa mwezi msafara wake kutoka katika kituo ulichoanzia hadi kufikia kituo cha mwisho. Muandamo huu ndio ambao ni mmoja dunia nzima, nao sio muandamo wa Kisharia: muandamo wa kisharia wa mwezi ni kitu chengine kabisa. Dhana (concept) sahihi ya kuandama kwa mwezi kisharia ni kuuona kwa macho baada ya siku ishirini na tisa au thalathini au kukamilisha idadi ya siku thalathini, kama Hadithi ilivyoeleza kwa uwazi. Sasa muandamo huu wa Kisharia, si lazima kwamba ukithibiti mahala pamoja uwe umethibiti mahala pengine. Kwa hivyo, Sheikh katika maelezo yake kachanganya baina ya muandamo wa kisharia na muandamo wa kifalaki na akaufanya muandamo wa kifalaki unaothibiti mara moja duniani kuwa ni sawa na muandamo wa kisharia ambao unatafautika kwa kutafautiana jografia ya ulimwengu kama tutavyoeleza baadae Inshaa Allah". Mwisho wa kunukuu nilioyasema kitabuni mwangu.

JAWABU NILILIPATA

Wanasema ndugu zetu wakijibu maelezo hayo: "6. Muandamo Wa Kifalaki Na Muandamo Wa KiShari'ah Kama kawaida yake ndugu yetu Juma amezusha dhana mpya katika mas-ala ya mwezi ambayo inakwenda kinyume kabisa na mitazamo ya Wanavyuoni, katika kulihusisha suala hilo na utaratibu wa kufunga na kufungua Ramadhaan. Amejaribu kuugawa muuandamo wa mwezi katika sehemu mbili kama alivyodai mwenyewe katika kitabu chake uk 18 kwa kusema: ((Hali ya kwanza: ni ya muandamo wa kifalaki.)) na (Hali ya pili: ni ya muandamo wa Kisharia.)

Hatujui dhana hii potofu ameitoa wapi kwani hakuweza kuthibitisha hata kauli moja ya Mwanachuoni yeyote aliyegawa muandamo au aliyesema kuna miandamo miwili (ya Kifalaki na ya Kisheria). Hoja sio kusema unavyoona wewe binafsi, kama mara nyingi alivyojaribu kuonya yeye mwenyewe ndugu Juma kwamba pasitumike 'hoja za mitaani' lakini bahati mbaya yeye mwenyewe anakwenda kinyume na kauli zake hizo".

JAWABU

Kwanza : maneno yenu "Kama kawaida yake" hayaoneshi kuwa muna insafu. Tukichukulia kuwa maneno "Muandamo wa kifalaki" ni istilahi mpya, je kitendo hiki cha kutoa istilahi mpya kimejikariri mara ngapi katika kitabu changu hata iwe "Kama kawaida yake". Ni wazi kwamba lengo lenu si kujadili bali ni kuponda na kutia aibu baada ya kushindwa kukijibu kitabu changu kwa hoja za kielimu zinazokubalika.

pili : Maneno "Inakwenda kinyume kabisa na mitazamo ya Wanavyuoni" yanaonesha kuwa hamujui mukisemacho, mwaporoja tu! Kwenda kinyume ni kuwa moja anasema "Kaja" mwengine anasema "Hakuja", huku ndio kwenda kinyume. Ama kusema kitu kipya tu ambacho hakijasemwa huko hakuitwi kwenda kinyume. Ingekuwa ni kinyume lau kuna wanazuoni waliokataa kwamba hakuna muandamo wa kifalaki, mimi nikauthibitisha, hapo ndio kwenda kinyume.

Tatu : Ilikuwa ni wajibu wenu kunukuu maneno yangu yote niliosema kisha mukayajibu: sio kuwambia watu "Amejaribu kuugawa muuandamo wa mwezi katika sehemu mbili kama alivyodai mwenyewe katika kitabu chake uk 18 kwa kusema: (Hali ya kwanza: ni ya muandamo wa kifalaki.) na (Hali ya pili: ni ya muandamo wa Kisharia."

Nnne : Tazameni maneno yangu vizuri nilisema: "Hali ya kwanza: ni ya muandamo wa kifalaki. Na huu sio ule tunaouita muandamo. Hapa tutatumia tu neno "Muandamo" kwa ajili ya kufahamiana. Huu ndio ambao unazungumziwa na Aya hizo tulizotangulia kuzinukuu. Na ndio unaotokea mara moja duniani kote". Maneno haya yote mumeyaruka ili mupate kufikia lengo lenu; lakini watu hamuwadanganyi kwani wanasoma na kujionea. Kwa hivyo, ni wazi - kwa kila mwenye akili licha ya mwenye elimu - kwamba mimi sikuuita huo kuwa ni muandamo, bali nimetumia lugha hio ili kutaka kuikurubisha maudhii katika fahamu za watu kuwa mwezi unakuwa umekamilisha safari yake baada ya kuvikata vituo ishirini na nane, na hapo huwa umemaliza mzunguko wake. Na huu ndio tuoweza kuuthibitisha kwa Aya zenye kutaja kupita kwa mwezi kwenye manazili.

Tano : Eleweni kwamba kinachotazamwa katika uwanja wa elimu si istilahat (technical terms), bali ni uhakika (facts) Yaani hali hio ya mw ezi kukamilika safari yake ndio uhakika (facts) na hilo jila nililoupa ni istilah tu. Sasa kama mulikuwa ni watu wa kufahamu mungelijadili uhakika (facts) na kubainisha kwamba nilivyosema sivyo. Ama istilahat (technical terms) mtu anawez a kukikipa kitu jina lolote lile kwani muhimu ni kuwa afahamike anakusudia nini. Na hili ni jambo ambalo wanavyuoni wanalizungumzia sana katika vitabu vyao vya Usuli na Furu'i, na ndio makusudio yao pale wanaposema: Hakuna kuvutana ka tika maneno ya kitaalamu au ya kifani (technical terms). Lakini kwa vile wenzetu walivyokuwa masikini wa elimu, basi wameona kule kutaja muandamo wa falaki - pamoja na kuwa nimebainisha kuwa huo si muandamo, bali natumia neno hilo ili kufahamiana - kuwa hilo ni kosa la jinai kwani ni jina ambalo halikutumiwa na wanavyuoni! Maskini wenzetu!

Sita : Ni kudai kwenu kwamba sikunukuu kauli za Maulamaa. Sijui munataka Maulamaa gani tena. Rejeeni maandiko yangu nilipozungumzia mas-ala haya muone kauli za Al-Tukhi, Al-Baghawi, Al-Zamakhshari, Al-Qurtubi na wengine wengi. Au hawa si wanavyuoni?! Saba: Ni kuwa nyinyi katika kukipinga Qias cha Sala na funga mumeleta hoja zenu binafsi: hakuna mjuzi yeyote anayetoa hoja hizo. Nazo ni hoja zenye kuonesha uchache au utovu wa maarifa.

MUNASEMA

"Ukiangalia katika kitabu cha "Kuandama Kwa Mwezi" uk 6 - 7 cha Shaykh Naaswir Bachuu, utaona kwamba yeye hakuporoja, bali amenukuu hoja za Wanavyuoni katika vitabu zaidi ya kumi. Baadhi yao ni kama vifuatavyo:- Tafsiri ya Durul-Manthuur: Imam as-Suyuuty katika tafsiri yake iitwayo "Durul-Manthuur" ameandika hivi "Amepokea Al-Khalib katika vitabu vya nyota kutoka kwa Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'Anhu) kwamba kauli ya Mungu isemayo: "Na mwezi tumeupanga vituo husafiri (vituoni humo) hadi kurudi ukiwa kama karara la mtende." Amesema: "Ni vituo ishirini na nane ambavyo mwezi hutua humo kwa muda wa mwezi mzima, kumi na nne kati ya hivyo vipo magharibi na kumi na nne vyenginevyo viko mashariki."

Baada ya kuvitaja vituo hivyo akaendelea kusema: "Utakapomaliza (kusafiri katika) vituo ishirini na nane, hurudi ukiwa kama karara la mtende, kama ulivyokua mwanzo wa mwezi." (Durul-Manthuur: J. 5, uk. 495) Tafsiri ya Qurtubiy: Naye Imam Al-Qurtubiy amesema haya yafuatayo: "Na vituo vilivyotajwa katika aya hii ni ishirini na nane...." Akavitaja kwa majina kisha akasema: "Mwezi unapofika katika kituo cha mwiisho hurudi tena katika kituo cha mwanzo, kwa hivyo humaliza mzunguko mmoja katika siku ishirini na nane, kisha hufichika, kisha huchomoza tena katika sura ya uchanga (mwandamo) na kurejea katika safari yake kwenye vituo vilivyotajwa". (Tafsirul-Qurtubiy J. 8, uk. 21)".

Jawabu

Je katika kitabu changu hayamo hayo mulioyanukuu kutoka kwa Sheikh Nassor Bachoo hata langu liwe porojo lake lisiwe? Je mimi pia sikunukuu kauli za wanavyuoni juu ya Haya. Bali mimi nimenukuu kutoka kwa mtu ambaye alimu ya nyota ndio fani yake, naye ni Al-Tukhi, huyu ni bora katika fani hii kuliko hao wafasirina. Hebu rejeeni ukurasa wa 17-22 wa chapa ya pili ya kitabu Ushahidi Uliowekwa Wazi. Bali mimi nimewasiliana na mtaalamu wa falaki anayekubalika na akasema kuwa hakuna makosa katika nilioyaandika, na barua yangu kwake na majibu yake nimeyaweka katika uk. 11-13, wa kitabu changu. Tafadhali rejeeni huko. Pili ni kuwa Sheikhe wenu Bachoo ndiye aliyekosea alipotoa hoja kwa Hadithi ya kutunga. Kama alivyodai kwamba Kuraib hajulikani na wanavyuoni wa Hadithi, na akadai kuwa Al-Imamu Abu Muslim Al-Rawahi (Ibadhi) ni miongoni mwa waliosema kuwa muandamo mmoja unatosheleza duniani kote. Yote haya nyinyi munayafumbia macho na kusema "Sheikh Nassor hakuporoja". Ni wazi kwamba hamutafuti haki, bali ni ushabiki tu.

MNASEMA

Wala haina maana kwamba Shaykh Naaswir Bachuu, kwa kuzinukuu tafsiri hizo anaashiria kuwa watu wafunge kwa kutumia huo alioita ndugu Juma 'Mwezi wa falaki. Jawabu Mimi nilichokisema ni hiki: Sh. Nassor Bachoo ni mmoja wa Wazanzibari waliojitokeza kuzungumzia mas-ala haya. Katika kitabu chake, Sheikh kaizungumzia maudhui hii na akanukuu Aya ya 5 ya Sura ya 10 ambayo ni ya pili katika Aya tulizozinukuu kabla. Baada ya maelezo alisema: Qur-an inalieleza suala la kuandama kwa mwezi kama ni tukio moja wapo kati ya matukio yaliyopangwa na Mwenyezi Mungu kutukia kila mwezi mara moja duniani kote. Mwisho wa kunukuu.

Ukianzia uk. 5. hadi uk. 8, wa kitabu chake, utaona kwamba Sh. Nassor Bachoo anathibitisha mwenendo wa mwezi kupitia katika Manazil (vituo) yake. Ufupisho wake - kama tulivyotangulia kusema - ni kuwa mwezi unasafiri kwa muda wa siku ishirini na nane (28) kupitia katika vituo hivyo, na siku moja au mbili hupotea kisha kudhihiri na kuweza kuonekana duniani. Sheikh aliishia maneno yake kwa kusema: "Baada ya maelezo haya tunatumai tumeweza kuelewa mtazamo wa Qur-an juu ya kuandama kwa mwezi." Mwisho wa kunukuu.

KISHA NAMI NIKANENA

Sasa ukitazama sentensi mbili hizi za Sh. Bachoo, utaona kuwa anakusudia kuthibitisha kitu kimoja kwa Aya ambayo haimpatii malengo yake. Anachokusudia kukithibitisha Sh. Bachoo - kwa inavyoonesha kutokana na maandishi yake - ni kuwa muandamo ni mmoja duniani kote na kwa hivyo - bila shaka anakusudia kusema - kwamba sote tufunge kwa muandamo mmoja huo. Ndio maana akasema: "Qur-an inaeleza suala la kuandama kwa mwezi kama ni tukio moja wapo kati ya matukio yaliopangwa na Mwenyezi Mungu kutukia kila mwezi mara moja duniani kote." Lakini dai kwamba Qur-an inasema kuwa muandamo wa mwezi unatokea mara moja tu dunia nzima - ikiwa anakusudia muandamo wa kisharia nao bila shaka ndio anaouzungumzia - si sahihi. Na sijui wapi Qur-an imesema hivi?!

Kwa hivyo, ni wazi kwamba mimi napinga kutoa kwake (Sheikh Bachoo) ushahidi kwa Aya hio kama ni dalili ya muandamo wa mwezi. Nasema kuwa Aya haina maana ya muandamo wa mwezi bali ina maana ya kukakamilika mzunguko wa mwezi ambako ndiko nimekuita "Muandamo wa kifalaki" yaani the moon has been astronomically born: not judicially. Ama muandamo wa mwezi kisharia ni:

1) Kuuona kwa macho siku ya mwezi 29.

2) Kutimiza idadi ya siku 30.

Huu ndio muandamo wa mwezi kisharia. Ama kukamilika mzunguko, huo si muandamo kisharia kwani mwezi unaweza kukamilika mzunguko na usionekane duniani wala kusiwe na uwezekano wa kuonekana. Kwa hivyo, bado hamujajibu nilivyosema. Nasema kuwa Sheikhe wetu alivyoihusisha Aya hio, basi kakosea. Lakini hamutaki kukiri kwa sababu hamutafuti haki, mwatafuta kumlinda mtu fulani na kumshambulia fulani; na kuisapoti rai fulani na kuipinga nyengine hata kama ushahidi unakusuteni. Kiufupi ni kuwa Sheikh Bachoo aliposema hivyo, alikuwa anathibitisha muandamo mmoja kwa kutumia Aya hio, sasa vipi tena mutadai kuwa: "Wala haina maana kwamba Shaykh Naaswir Bachuu, kwa kuzinukuu tafsiri hizo anaashiria kuwa watu wafunge kwa kutumia huo alioita ndugu Juma 'Mwezi wa falaki."

MNASEMA

"Kwanza ni vyema kuelewa kwamba hakuna hiyo dhana ya muandamo wa kifalaki lakini kitaaluma kuna: "mwezi mpya" usioonekana (the invisible new moon) na "mwezi mchanga" unaonekana (the visible young crescent ). Ndio maana Shaykh Naaswir Bachuu akaandika katika kitabu chake uk 87 - 88 kwa kusema hivi: Tukirejea katika mada yetu ya kuandama kwa mwezi, itakuwa vizuri hapa kama tutamnukuu mtaalamu wa elimu hii ya annga (Astronomy), Dr. S. K. Abdali katika makala yake iliyochapishwa katika gazeti la Al-Ittihad la Mombasa Kenya, litolewalo mwaka mara nne; la kipindi cha Januari - Julai 1979. Amesema: "... Huu 'mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon) ambao majira yake hupatikana katika makalenda na magazeti, usichanganywe na mwezi mchanga unaoonekana (the visible young crescent) ambao (kutokana na mwezi huo mchanga) huanza mwezi mpya katika kalenda ya Kiislam...".

Hapa tunajifunza jambo moja muhimu kuwa 'mwezi mpya' (new moon) ni tofauti na 'mwezi mchanga' (young crescent). Na mwezi mchanga ndio tunaoutumia Waislam kujua kalenda (tarehe) yetu. Kwa hivyo hapa Shaykh Naaswir anasisitiza jambo la kutumika mwezi unaoonekana katika hukumu ya muandamo. Pili: Katika kitabu kizima cha Shaykh Naaswir kimeandikwa kwa msisitizo wa kutosha wa kwamba hukumu ya kufunga na kufungua ni lazima uonekane mwezi muandamo au kukamilisha siku 30 kama patapatikana udhuru wa kutoonekana mwezi siku ya tarehe 29. Ameyasema hayo Shaykh Naaswir akiwa anajua fika kwamba huo mwezi (aliouita ndugu Juma wa Falaki) hauna hukumu ya kufanya mtu afunge au afungue, kwani hauonekani kwa macho ya kawaida (the invisible new moon). Unajulikana kwa mahesabu ya Kitaalamu au kwa kuangaliwa kwa vyombo vya Kitaalamu.

JAWABU 1)

Kwanza nimeshakujibuni kuwa: wanavyuoni wote wanakubali na wamesema kuwa: Hakuna kujadiliana katika maneno ya kitaalamu au ya kifani. Kwa hivyo, je mwezi huo tuuite ni mwezi wa kifalaki kama alivyouita Juma Mazrui au tuuite 'Mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon) kama alivyouita mtaalamu wa falaki, hili si muhimu kielimu. Muhimu je huo aliouita Juma Mazrui kuwa ni muandamo wa kifali upo au haupo? Tena, je makusudio yake kwa kuuita muandamo wa kifalaki ni sawa na makusudio ya yule mtaalamu wa kifalaki alipouita 'Mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon). au Juma Mazrui anakusudia kitu chengine na mtaalamu wa falaki anakusudia kitu chengine? Haya ndio mambo ambayo wenye elimu huyajadili: sio kujadili majina, bali kinachojadiliwa ni uhakika (facts).

2) ni kuwa kama munatoa hoja kama hizo, basi hata hio dhana ya 'Mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon) pia katika Uislamu haipo. Hii Qur-ani na hizo Hadithi za Mtume (s.a.w.) haya nitoleeni palipoandikwa 'Mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon). Ni wazi kwamba jina hilo halipo katika Uislamu, lakini suala ni kuw a je uhakika (facts) wa 'Mwezi mpya' usioonekana (the invisible new moon) upo au haupo.

Wataalamu huwa wanatafiti uhakika (facts ) kisha wakishakugundua kitu wanakipa jina. Jina huwa ni jipya na uhakika hua upo zamani. Na jina la kitaala mu huwa linatafautika katika nchi hadi nchi; zama hadi zama; bali wakati mwengine baina ya mtaalamu au mpekuzi mmoja na mwengine. Lakini ndugu zetu, hamutaki kujiweka katika nafasi yenu aliokupeni Allah ya uchache wa maarifa, kisha munawambia watu wanajikweza, sijui nani anayejikweza. 3) Tatu: Eleweni tena, mimi nilikuwa najibu kitu gani? Mimi nilikuwa napinga kuhusishwa Aya"Yeye (Allah) Ndiye aliyelifanya jua kua muanga na mwezi kua nuru na akaupimia (huo mwezi) vituo, ili mujue idadi ya miaka na hisabu" na suala la muandamo wa mwezi Kisharia: nasema Aya hii haina uhusiano huo kamwe.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُهُمْ وَلَا يَضُرُّهُمْ وَكَانَ الْكَافِرُ عَلَىٰ رَبِّهِ ظَهِيرًا ﴿٥٥﴾

55. Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu. Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا مُبَشِّرًا وَنَذِيرًا ﴿٥٦﴾

56. Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

قُلْ مَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِلَّا مَن شَاءَ أَن يَتَّخِذَ إِلَىٰ رَبِّهِ سَبِيلًا ﴿٥٧﴾

57. Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

وَتَوَكَّلْ عَلَى الْحَيِّ الَّذِي لَا يَمُوتُ وَسَبِّحْ بِحَمْدِهِ وَكَفَىٰ بِهِ بِذُنُوبِ عِبَادِهِ خَبِيرًا ﴿٥٨﴾

58. Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ الرَّحْمَـٰنُ فَاسْأَلْ بِهِ خَبِيرًا ﴿٥٩﴾

59. Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi. Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اسْجُدُوا لِلرَّحْمَـٰنِ قَالُوا وَمَا الرَّحْمَـٰنُ أَنَسْجُدُ لِمَا تَأْمُرُنَا وَزَادَهُمْ نُفُورًا ﴿٦٠﴾

60. Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe? Na huwazidishia chuki.

تَبَارَكَ الَّذِي جَعَلَ فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَجَعَلَ فِيهَا سِرَاجًا وَقَمَرًا مُّنِيرًا ﴿٦١﴾

61. Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ خِلْفَةً لِّمَنْ أَرَادَ أَن يَذَّكَّرَ أَوْ أَرَادَ شُكُورًا ﴿٦٢﴾

62. Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

KAFIRI NI MSADIZI WA MPINZANI WA MOLA WAKE

Aya 55 – 62

MAANA

Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 11 (10 18).

Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

Yaani anawasaidia watu wa batili dhidi ya haki. Kila mwenye kusaidia batili atakuwa amesaidia dhidi ya Mwenyezi Mungu na kuwa adui yake; hata kama atamsabihi na kumtukuza kwa ulimi wake. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) :“Mwenye kumsaidia dhalimu na huku anajua kuwa ni dhalimu basi amejitenga na Uislamu.”

Kadiri nitakavyotia shaka, lakini siwezi kutia shaka kuwa mwenye kumtegemea dhalimu ni kafiri; bali kafiri aliye mwadilifu ni bora kuliko yeye. Aya za Qur’an kuhusu hilo ni nyingi na ziko wazi. Ama Hadith za Mtume zimepituka kiwango cha mutawatir.

Ndio! Ni wajibu wetu kuamiliana naye muamala wa kiislamu kwa vile tu ametamka: Lailaha illallah Muhammadurrasulullah (Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.)

Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 15 (17:105).

Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

Mimi sina tamaa ya mali yenu wala siwauzii pepo. Ninalotaka ni kutengeneza tu. Anayetaka kufanya njia ya kumwendea Mola miongoni mwenu, basi malipo yake yako kwa Mungu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz.12 (11:88).

Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

Ewe Muhammad! Toa bishara na onyo ukimtegemea Mwenyezi Mungu kwa kuwa na ikhlasi naye katika kauli yako na vitendo vyako na ujitakashe na kumfanyia mfano na kila lile ambalo halifanani na utukufu na ukuu wake. Yeye anamjua zaidi aliyepotea njia, na atamhisabu na kumlipa.

Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi.

Makusudio ya kustawi ni kutawala. Lililo na nguvu ni kuwa makusudio ya siku ni mikupuo, kwa sababu hakuna siku kabla ya kupatikana ulimwengu na jua. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:54), Juz. 11 (103), na Juz. 12 (11:7).

Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

Habari yake, ni habari ya huko kuumbwa mbingu na ardhi, ambako kunafahamika kutokana na mfumo wa Aya. Hapa kuna maneno yaliyotan- gulizwa na ya kukadiriwa. Maana ni: Yeye ni Mwingi wa rehema, ulizia habari za kuumbwa mbingu na ardhi kwa yule ajuaye ambaye ni Mwenyezi Mungu.

Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: ‘Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe?’ Na huwazidishia chuki.

Nabii(s.a.w.w) akiwaambia washirikina: ‘Mwabuduni Mwingi wa rehema, wala msiabudu masanamu,’ wao husema kwa kujitia hamnazo, kwa madharau, ni nani huyo unayetuambia tumwabudu unayemuita Mwingi wa rehema? Unataka tukutii wewe na tuwaasi baba zetu katika yale waliyokuwa wakiyaabudu?’

Ujinga na upumbavu huu unatukumbusha ujinga wa vijana wetu wanapoambiwa swalini na mfunge, husema: “Bado kuna Swala katika karne hii ya ishirini? Jambo la kushangaza ni kuwa vijana hawa wanaimba uhuru wa bianadamu; kama kwamba uhuru ni uzandiki na utu ni kujitoa kwenye misimamo.

Hawajui kuwa aliye huru ni yule anayemwabudu Mwenyezi Mungu wala hamnyenyekei asiyekuwa yeye na kwamba utu ni dini ya Mwenyezi Mungu ambayo inakataza maovu na munkar.

Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

Makusudio ya buruji ni mashukio ya jua na mwezi. Tazama Juz.14 (15: 16). Makusudio ya taa hapa ni jua, kutokana na kuunganisha na mwezi. Mahali pengine Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ الشَّمْسَ ضِيَاءً وَالْقَمَرَ نُورًا ﴿٥﴾

“Yeye ndiye aliyefanya jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru.” Juz.11 (10:5).

Wengine wametofautisha baina ya nuru na mwanga. Kwamba mwanga unategemea sayari moja kwa moja; kama vile mwanga wa jua, unatoka kwenye jua moja kwa moja.

Nuru inategemea sayari kupitia sayari nyingine; kama vile nuru ya mwezi inavyotegmea jua. Wametoa dalili wanaotofautisha, kwa Aya hiyo ya Juz. 11 (10:5) tuliyoitaja punde.

Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

Usiku unaondoka kisha unakuja mchana, nao unaondoka kisha unarudi usiku na kuendelea; wala hakuna unaobakia muda mrefu kuzidi kiasi cha haja ya viumbe.

Kufuatana kwa namna hii kunafahamisha kuweko mpangiliaji mwenye hekima. Kufuatana huku kunategemea harakati za ardhi, nazo zinategemea msababishaji wake wa kwanza.

Ama hekima ya mfuatano huu, ni kwamba lau lingelibakia giza tu, au mwangaza tu, maisha yangelikuwa magumu hapa ardhini.

Kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) ‘Kwa anayetaka kukumbuka,’ maana yake ni kuwa mwenye kutaka dalili ya kuweko Mwenyezi Mungu ataipata katika vitu vyote, vikiwemo kufuatana usiku na mchana.

Na kauli yake ‘Au anayetaka kushukuru,’ ni kuwa anayetaka kumshukuru Mweneyzi Mungu kwa neema yake naashukuru vile vile kwa kufuatana usiku na mchana, kwa sababu hilo ni katika neema kubwa.

وَعِبَادُ الرَّحْمَـٰنِ الَّذِينَ يَمْشُونَ عَلَى الْأَرْضِ هَوْنًا وَإِذَا خَاطَبَهُمُ الْجَاهِلُونَ قَالُوا سَلَامًا ﴿٦٣﴾

63. Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu. Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

وَالَّذِينَ يَبِيتُونَ لِرَبِّهِمْ سُجَّدًا وَقِيَامًا ﴿٦٤﴾

64. Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا اصْرِفْ عَنَّا عَذَابَ جَهَنَّمَ إِنَّ عَذَابَهَا كَانَ غَرَامًا ﴿٦٥﴾

65. Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam,’ hakika adhabu yake ni yenye kuendelea.

إِنَّهَا سَاءَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٦٦﴾

66. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa.

وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴿٦٧﴾

67. Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo.

وَالَّذِينَ لَا يَدْعُونَ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ وَلَا يَقْتُلُونَ النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّـهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَا يَزْنُونَ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ يَلْقَ أَثَامًا ﴿٦٨﴾

68. Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki, wala hawazini. Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

يُضَاعَفْ لَهُ الْعَذَابُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَيَخْلُدْ فِيهِ مُهَانًا ﴿٦٩﴾

69. Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

إِلَّا مَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ عَمَلًا صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ يُبَدِّلُ اللَّـهُ سَيِّئَاتِهِمْ حَسَنَاتٍ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٧٠﴾

70. Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.

وَمَن تَابَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَإِنَّهُ يَتُوبُ إِلَى اللَّـهِ مَتَابًا ﴿٧١﴾

71. Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

وَالَّذِينَ لَا يَشْهَدُونَ الزُّورَ وَإِذَا مَرُّوا بِاللَّغْوِ مَرُّوا كِرَامًا ﴿٧٢﴾

72. Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

وَالَّذِينَ إِذَا ذُكِّرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ لَمْ يَخِرُّوا عَلَيْهَا صُمًّا وَعُمْيَانًا ﴿٧٣﴾

73. Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawajifanyi ni viziwi nazo na vipofu.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا هَبْ لَنَا مِنْ أَزْوَاجِنَا وَذُرِّيَّاتِنَا قُرَّةَ أَعْيُنٍ وَاجْعَلْنَا لِلْمُتَّقِينَ إِمَامًا ﴿٧٤﴾

74. Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wanetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

أُولَـٰئِكَ يُجْزَوْنَ الْغُرْفَةَ بِمَا صَبَرُوا وَيُلَقَّوْنَ فِيهَا تَحِيَّةً وَسَلَامًا ﴿٧٥﴾

75. Hao ndio watakolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam.

خَالِدِينَ فِيهَا حَسُنَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٧٦﴾

76. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

قُلْ مَا يَعْبَأُ بِكُمْ رَبِّي لَوْلَا دُعَاؤُكُمْ فَقَدْ كَذَّبْتُمْ فَسَوْفَ يَكُونُ لِزَامًا ﴿٧٧﴾

77. Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

WAJA WA MWINGI WA REHEMA

Aya 63 – 77

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja sifa za makafiri na kiaga chao, kama kawaida yake, anataja sifa za waumini na malipo aliyowaandalia. Zifuatazo ndizo sifa zao:

1.Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu.

Imam Jafar Sadiq(a.s) anasema katika tafsiri ya hilo:“Ni yule mtu anayetembea kwenye asili yake aliyoumbiwa, hajikalifishi wala hajifanyi.” Ndio, anayetembea kwenye umbile lake aliloumbiwa, tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wapambe na wafuasi wanaomfuta nyuma na wengine mbele wakiwa wamepanda farasi au pikipiki na kupiga ving’ora vinavyohanikiza watu kwa sauti zake vikitangaza kuja kwake ili aachiwe njia, kwa ajili ya kumheshimu na kumtukuza.

2.Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

Makusudio ya kusemeshwa na wajinga ni kama vile kejeli zao, shutuma zao au mijadala ya hawa na masilahi. Amani ni kinaya cha kuachana nao, kwa kuwadharau na kuchunga mtu heshima yake. Maana ni kuwa, muumini akisikia neno ovu, aachane nalo; kama kwamba hakulisikia au kama anayekusudiwa ni mwingine sio yeye. Huu ndio mwepuko mwema aliousema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَاهْجُرْهُمْ هَجْرًا جَمِيلًا ﴿١٠﴾

“Na uwaepuke mwepuko mwema.” (73:10).

Hakuna mwenye shaka kwamba kuachana na jambo ni pale ikiwa hakuna uwezo au nguvu za kulikabili. Vinginevyo itakuwa ni wajibu kulikabili. Hapana budi kuihusisha Aya na hilo.

3.Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

Waumini wanasimama usiku kwenye giza wakifanya ibada ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu hilo liko mbali na ria, wala hawaupitishi usiku mikahawani na kwenye mambo ya mchezo mchezo tu, huku wakifuja mali na kupanga njama dhidi ya waumini na wenye ikhlasi. Mfano wa Aya hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:

كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ ﴿١٧﴾

“Walikuwa wakilala kidogo usiku.” (51:17).

4.Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam, hakika adhabu yake ni yenye kuendelea. haikwepeki na ni yakudumu. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa,

Waliamini Pepo na Moto, kutokana na waliyoyashuhudia na kuyaona; ndio wakauhofia moto wakaitumai pepo. Imam Ali(a.s ) anasema: “Wao na Pepo ni kama walioiona wakiwa ndani yake wananeemeshwa. Na wao na moto ni kama waliouona wakiwa ndani yake wanaadhibiwa.”

5.Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo, hakuna kupitisha kiasi, Si ubakhili wala ubadhirifu.

Huu ndio mwenendo wa Uislamu, wastani katika kila kitu; hakuna ulahidi wala waungu wengi, udikteta wala ukiritimba na hakuna kutaifisha mali ya mtu wala ubepari. Tazama Juz. 15 (17:29) kifungu cha ‘Uislamu na nadharia ya maadili.’

6.Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Mwenye kufanya riya au akamtii kiumbe katika kumuasi Muumba, basi huyo ni kama aliyemwomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki.

Nafsi inayouliwa kwa haki na kwa uadilifu ni ile iliyoua nafsi nyingine bila ya haki, aliyezini akiwa kwenye ndoa, kurtadi dini au kuleta ufisadi katika ardhi.

Ufafanuzi wa hayo uko katika vitabu vya Fiqh.

Wala hawazini

Kwa sababu zinaa ni katika madhambi makubwa. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t). Akaiweka sawa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuua nafsi na akajaalia hukumu ya haya matatu ni kuuliwa kwa masharti yaliyotajwa kwenye vitabu vya fiqh.

Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

Hayo ni hayo ya shirk, kuua na kuzini. Na madhambi ni adhabu.

Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

Kuna adhabu gani kubwa na kufedheheka zaidi kuliko adhabu ya Jahannam? Si kwambii tena ikiwa itazidishwa pamoja na kudumu kusiko na mwisho.

Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

Mwenye kutubia dhambi ni kama asiyekuwa na dhambi, zaidi ya hayo, Mwenyezi Mungu atampa thawabu kwa kule kutubia kwake na atampa mema kulingana na maovu ya dhambi zake; kiasi ambacho toba itafuta maovu ya dhambi.

إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ ﴿١١٤﴾

“Hakika mema huondoa maovu.” Juz. 12 (11:114).

Haya ndiyo maana ya ‘Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema’ kwa sababu uovu, kwa ulivyo, haustahiki kuwa wema, wala wema, kwa ulivyo, haustahiki kuwa uovu’

Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

Baada ya kubainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya iliyotangulia kwamba mwenye kutubia atampa thawabu za mwenye kufanya mema, hapa anamsifu kuwa amerejea kwa Muumba wake kurejea kuzuri.

7.Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

Neno ‘hawawi’ limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu ‘laa yash-hadu- una’ kama ilivyotumika tafsiri hiyo katika Juz. 2 (2:185). Makusudio ya uzushi ni mambo ya batili na upuzi ni kila lisilo na kheri. Maana ni kuwa waumini hawahudhurii vikao vya ubatilifu wala hawavisaidii, sikwambii kuvifanya. Pia hawashiriki mazungumzo yasiyokuwa na kheri na wanapoyapitia hayo masiko yao huyaepuka; kama wanavyoziepusha ndimi zao kuayatamka; sawa na nyuki anavyopita haraka kwenye mzoga na harufu mbaya.

8.Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawaji- fanyi ni viziwi nazo na vipofu.

Mshairi huwa anasikiliza mashairi kwa umakini kabisa. Vile vile kila mwenye kuhusika na jambo akizungumziwa huwa anakuwa makini nalo sana anapolisikilza. Mtu unapomzungumzia jambo lililo mbali naye atakuepuka na hayo mazungumzo yako, hata kama ni ya uongofu na mwangaza.

Hapa ndipo inabainika siri ya muumini kuikubali Qur’an, na kafiri kuachana nayo. Mumin anakikubali Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa vile anakiamini na kutambua maana yake na makusudio yake. Anakikuta kwenye nafsi yake, itikadi yake, matendo yake mema na malipo aliyomuandalia Mola wake.

Kafiri anakipa mgongo Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa sababu anakipinga na hajui malengo yake na siri yake; wala hapati humo isipokuwa kushutumiwa na kukosolewa itikadi yake na sifa zake na pia makaripio ya ukafiri wake.

9.Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

Muovu huwa anatamaani watu wamfuate katika uovu wake, sio kwa kuwa amekinai kuwa yuko kwenye uongofu kutoka kwa Mola wake, hapana! Isipokuwa anataka kupunguza lawama na shutuma na kufunika kosa lake kwa kuwa wengi wakosefu. Lakini hataki mkewe na watoto wake wawe hivyo; kama vile mgonjwa asivyopenda watu wake wapatwe na ugonjwa alio nao.

Ama yule aliye mwema na mwenye takua ana yakini na dini yake na ana busara katika mambo yake. Kwa hivyo huwa anatamaani kwa dhati ya moyo kimsingi na kiitikadi kuwa watu wote wafuate njia yake na kwamba watoto wake wakimuiga yeye huwa anafurahi.

Kwa hiyo wenye ikhlasi humuomba Muumba wao wapate wa kuwaiga, sio kwa kuziba vitendo vyao kwa watu wala kutaka jaha duniani na kuchukua mali kwa kutumia haki za Mwenyezi Mungu; bali ni kwa kujipendekeza mbele ya Mwenyezi Mungu aliye peke yake.

Hao ndio watakaolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

Ghorofa ni kinaya cha makao ya juu. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha wasifu wa wenye takua na watiifu, sasa anataja malipo yao watakayoyapata kwake, ambayo ni kudumu katika raha, amani na neema pamoja na heshima.

Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja subira hapa kuashiria kuwa kila mwenye haki hana budi kupata taabu na udhia kutoka kwa wasio na haki na kwamba thawabu za Mwenyezi Mungu hatazipata ispokuwa mwenye kuwa na uvumilivu na subira na akaendelea kuwa na msimamo kadiri hali itakavyokuwa ngumu.

Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

Makusudio ya neno ‘duakum’ hapa ni kupewa mwito kutokana na maneno yanayovutia, lakini mlikadhibisha. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ ﴿٥٢﴾

“Basi watawaita nao hawatawaitikia.” Juz. 15 (18:52)

Kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapa mwito kwenye imani na utiifu kupitia kwa Mtume wake.

Maana ni kuwa nyinyi washirikina hamstahiki hata kutajwa pia lau si kuwa mliitwa kwenye imani na utiifu, ili kuweko na hoja siku ya hisabu na malipo, ikiwa hamtasikia na kuitikia mwito. Nanyi mmeupinga mwito na mkadhibishaji aliyetoa mwito huo, basi adhabu inawastahiki na ni lazima.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Sura Ya Ishirini Na Sita: Surat Shua’rau.

Twabrasiy amesema imeshuka Makka isipokuwa Aya 224 hadi mwisho, zimeshuka Madina. Ina Aya 227

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehma Mwenye kurehemu.

طسم ﴿١﴾

1. Twaa Siin Miim.

تِلْكَ آيَاتُ الْكِتَابِ الْمُبِينِ ﴿٢﴾

2. Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

لَعَلَّكَ بَاخِعٌ نَّفْسَكَ أَلَّا يَكُونُوا مُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

إِن نَّشَأْ نُنَزِّلْ عَلَيْهِم مِّنَ السَّمَاءِ آيَةً فَظَلَّتْ أَعْنَاقُهُمْ لَهَا خَاضِعِينَ ﴿٤﴾

4. Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

وَمَا يَأْتِيهِم مِّن ذِكْرٍ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ مُحْدَثٍ إِلَّا كَانُوا عَنْهُ مُعْرِضِينَ ﴿٥﴾

5. Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao.

فَقَدْ كَذَّبُوا فَسَيَأْتِيهِمْ أَنبَاءُ مَا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٦﴾

6. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

أَوَلَمْ يَرَوْا إِلَى الْأَرْضِ كَمْ أَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ زَوْجٍ كَرِيمٍ ﴿٧﴾

7. Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٨﴾

8. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٩﴾

9. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

HUENDA UKAANGAMIZA NAFSI YAKO

Aya 1-9

MAANA

Twaa Siin Miim.

Umetangulia mfano wake mwanzo wa Sura Baqara, Juz. 1

Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

Hizo ni ishara ya Aya za Sura hii, kitabu ni Qur’an na chenye kubainisha ni kubainisha haki na kudhihirisha.

Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) kwamba asiikere na kuiumiza nafsi yake kwa sababu ya watu wake kuukataa uongofu na haki. Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:35) na Juz. 15 (18:6).

Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu: Poa moyo wako! Lau tungelitaka waamini kwa nguvu tungeliteremsha adhabu kutoka mbinguni waione kwa macho na kuwaambia chagueni imani au adhabu; bila shaka wao wangelisalimu amri kwa unyenyekevu.

Lakini je, hii itahisabiwa kuwa ni imani? Hapana! Imani ya kweli inakuwa kwa utashi na hiyari, sio kwa kulazimishwa kwa nguvu. Ndio maana tukawakadiria kheri na shari, tukawaamrisha hili na kuwakataza lile; kisha tukawaachia hiyari, waweze kustahiki thawabu kwa utiifu na adhabu kwa uasi.

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifanya hivyo katika zama za Musa(a.s) kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na tulipoinua mlima juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawaangukia. Tukawaambia: shikeni kwa nguvu tuliyowapa.” Juz. 9 (7: 171).

Jibu : kwa hakika Qur’an Tukufu inafahamisha waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ana muamala maalum na Mayahudi usiofanana na waja wengine. Kwa sababu wao wana tabia za pekee zisizokuwa na mfano. Tumelizungumzia hilo kwa ufafanuzi zaidi kwa anuani ya ‘Mayahudi hawana mfano’ katika Juz. 1: (2:63-66).

Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

Tumewaongoza washirikina, kupitia kwako ewe Muhammad, kwenye yale yaliyo na kheri yao na masilahi yao, wakaachana nayo, wakayadharau na kuyafanyia masikhara. Basi nawe achana nao na watakumbana na adhabu waliyoahidiwa tu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:68).

Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

Alikufuru Mungu aliyekufuru huku akiona dalili na ubainifu wa kupatikana kwake na ukuu wake. Miongoni mwa dalili hizi ni kutoa mimea ya aina na rangi mbali mbali. Kwa maelezo zaidi angalia Juz.7 (6:99) na Juz. 13 (13:3).

Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Kwa nguvu zake anawashinda mataghuti na rehema zake anawapa muda bila ya kuwaharakishia adhabu mpaka awajie mbashiri na muonyaji na kuwapa fursa ya kufikiria vizuri na kutubia.

Imam Ali(a.s) anasema:“Hasira zake hazimfanyi kuacha huruma yake, wala huruma haimfanyi kupuuza adhabu yake.”

وَإِذْ نَادَىٰ رَبُّكَ مُوسَىٰ أَنِ ائْتِ الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠﴾

10. Na Mola wako alipomwita Musa kwamba nenda kwa watu madhalimu.

قَوْمَ فِرْعَوْنَ أَلَا يَتَّقُونَ ﴿١١﴾

11. Watu wa Firauni. Hawaogopi?

قَالَ رَبِّ إِنِّي أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ ﴿١٢﴾

12. Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

وَيَضِيقُ صَدْرِي وَلَا يَنطَلِقُ لِسَانِي فَأَرْسِلْ إِلَىٰ هَارُونَ ﴿١٣﴾

13. Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

وَلَهُمْ عَلَيَّ ذَنبٌ فَأَخَافُ أَن يَقْتُلُونِ ﴿١٤﴾

14. Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

قَالَ كَلَّا فَاذْهَبَا بِآيَاتِنَا إِنَّا مَعَكُم مُّسْتَمِعُونَ ﴿١٥﴾

15. Akasema, sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu. Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza.

فَأْتِيَا فِرْعَوْنَ فَقُولَا إِنَّا رَسُولُ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote.

أَنْ أَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿١٧﴾

17. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

قَالَ أَلَمْ نُرَبِّكَ فِينَا وَلِيدًا وَلَبِثْتَ فِينَا مِنْ عُمُرِكَ سِنِينَ ﴿١٨﴾

18. Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi?

وَفَعَلْتَ فَعْلَتَكَ الَّتِي فَعَلْتَ وَأَنتَ مِنَ الْكَافِرِينَ ﴿١٩﴾

19. Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

قَالَ فَعَلْتُهَا إِذًا وَأَنَا مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Akasema: Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.

فَفَرَرْتُ مِنكُمْ لَمَّا خِفْتُكُمْ فَوَهَبَ لِي رَبِّي حُكْمًا وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٢١﴾

21. Basi niliwakimbia nilipowahofia. Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

وَتِلْكَ نِعْمَةٌ تَمُنُّهَا عَلَيَّ أَنْ عَبَّدتَّ بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٢٢﴾

22. Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

MUSA

Aya 10 – 22

MAANA

Aya hizi hadi kufikia Aya ya 28 ni za kisa cha Musa ambacho kimetangulia mara kadhaa. Katika Juz. 16 (20: 9) tumeleza sababu za kukaririka kisa hicho.

Na Mola wako alipomwita, Musa kwamba nenda kwa watu madhal- imu watu wa Firauni.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:24).

Hawaogopi?

Hii ni jumla nyingine, maana yake ni kuwa, umefika wakati sasa Firauni na watu wake waogope mwisho wa uovu na utaghuti.

Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

Katika Juz. 16 (20 45) ni: “Ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.”

Yaani asije akatuwahi kutuadhibu kabla kufikishia ujumbe.

Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Musa kupeleka ujumbe wake kwa Firauni. Na hili, kwa upande mmoja, ni jambo zito na lenye mashaka sana, kutokana na utaghuti wa Firauni na nguvu za utawala wake. Na kwa upande mwingine, ujumbe wenyewe ni mzito.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwambia Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) :

إِنَّا سَنُلْقِي عَلَيْكَ قَوْلًا ثَقِيلًا ﴿٥﴾

“Hakika sisi tutakuteremshia kauli nzito.” (73:5).

Musa alikuwa ni mwepesi wa kughadhibika kwa ajili ya haki, na ulimi wake ulikuwa na kigugumizi kinachomzuia kutamka. Kwa hiyo akahofia kutotekeleza vizuri ujumbe mkuu. Hakuna yeyote anayehofia kutekeleza haki ya Mwenyezi Mungu kuliko mitume; hasa wale Ulul-a’zm. Hii inatokana na isma. Ndipo Musa akamtaka Mwenyezi Mungu kumtuma Jibril kwa nduguye, Harun, ili awe msaidizi wake katika jambo hili muhimu.

Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

Anaishiria lile tukio la kumuua mtu wa upande wa Firauni pale alipom- saidia mtu wa upande wake; kama ilivyoelezwa katika Aya hii:

فَوَجَدَ فِيهَا رَجُلَيْنِ يَقْتَتِلَانِ هَـٰذَا مِن شِيعَتِهِ وَهَـٰذَا مِنْ عَدُوِّهِ فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ ﴿١٥﴾

“Na akakuta humo watu wawili wanapigana – mmoja ni katika wenzake na mwingine ni katika maadui zake. Yule aliye katika wenzake akamtaka msaada juu ya adui yake. Musa akampiga ngumi akammaliza.” (28:15).

Musa alihofia kuchukua risala ya Mwenyezi Mungu kwa Firauni asije akamuua kabla kukamilisha lengo, lakini akiwa na nduguye na ikatokewa kuuawa, basi atachukua nafasi yake kuendeleza malengo.

Akasema – Mwenyezi Mungu –sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu, Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

Musa alihofia dhiki ya kifua, kufungika ulimi na kuuliwa, lakini Mwenyezi Mungu akamhakikishia usalama na akamwambia kuwa hakuna kitu kitaka- chokuwa katika hayo, kwa sababu mimi nitawasaidia na kuwanusuru. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20: 46 – 47).

Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi? Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

Musa na Harun walielekea kwa Firauni, wakaingia kwake wakiwa wamevaa deraya ya sufu, mikononi mwao wakiwa na fimbo. Wakampa mwito wa kumwamini Mungu na kumpa sharti la kusilimu na kutii ili utawala wake ubakie na kudumu enzi yake.

Firauni aliwabeza wawili hawa, waliompa masharti ya kudumu utawala na enzi yake, wakiwa hawana cheo chochote wala mali. Hakutaka kuwaua kwa kuhofia asiambiwe kuwa ameshindwa na hoja akakimbilia upanga.

Lakini Firauni anaweza kuwa na hoja gani? Ni kwa mantiki gani atakayoweza kujadili? Hana kitu isipokuwa kuvungavunga na kumtajia Musa yaliyopita.

Je, hatukukulea na ukakaa nyumbani kwetu miaka, kisha ukatuulia mtu wetu na ukakimbia? Hii ndio shukrani yako? Zaidi ya hayo unadai kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwetu? Unataka tukusikize na kukutii na sisi ndio mabwana zako na wafadhili wa neema zako?

Kisha Firauni akawegeukia watu wa baraza lake na akasema: “Basi mbona hakuvikwa vikukuku vya dhahabu?” (43:53). Kwenye dhahabu tu ndio kuna kuwa na siri ya mantiki ya mataghuti. Hakuna utume wala ubwana au ubora isipokuwa kwa ajili ya dhahabu na dhahabu yenyewe.

Musa (a.s) akamjibu kuhusu kuua akasema: “Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.”

Yaani sikuelewa kuwa ngumi yangu itamuua. Nami nilikusudia kukinga na kutia adabu, nikakosea makusudio. Basi mimi nina dhambi gani katika hilo? Kukusudia ni nguzo ya msingi ya kosa la jinai kwa watu wa sharia.

Basi niliwakimbia nilipowahofia.

Sikukimbia hukumu ya uadilifu, bali nilikimbia dhulma kwa kuhofia kunichukulia kuwa ni muuaji wa makusudi. Kuna mmoja alimwambia Musa:

إِنَّ الْمَلَأَ يَأْتَمِرُونَ بِكَ لِيَقْتُلُوكَ فَاخْرُجْ إِنِّي لَكَ مِنَ النَّاصِحِينَ ﴿٢٠﴾

“Hakika wakubwa wanashauriana kukuua. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanaokupa nasaha.” (28:20).

Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

Firauni alimtajia Musa ufukara na utoro; Musa naye akamwambia kuwa utukufu haupimwi kwa mali wala kwa ufalme; isipokuwa uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu, humpatia amtakaye katika waja wake. Na mimi Mwenyezi Mungu amenitunukia elimu ya dini yake na sharia yake kwa njia ya kheri na usawa na akanitukuza kwa kunituma kwako na kwa watu wako.

Musa aliendelea kumjibu Firauni, kuhusu malezi na akasema:

Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

Yaani unanisimbulia kwa malezi yako kwangu na unajitia kutojua kuwa sababu ni uadui wako wa kuwachinja watoto wa kiume wa watu wangu na kuwatia utumwani watoto wao wa kike? Mama yangu alipohofia wewe kunichinja akanitupa baharini na matokeo yake yakawa ni kuishi mimi mbali ugenini bila ya huruma ya mama na mapenzi ya baba? Hii ndiyo fadhila yako kwangu? Firauni alizibwa mdomo, akaanza kuwatafuta wabatilifu wake; kama utakavyoona katika kifungu kifuatacho.

قَالَ فِرْعَوْنُ وَمَا رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٢٣﴾

23. Akasema Firauni: Na ni nani huyo Mola wa walimwengu wote?

قَالَ رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ ﴿٢٤﴾

24. Akasema: Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.

قَالَ لِمَنْ حَوْلَهُ أَلَا تَسْتَمِعُونَ ﴿٢٥﴾

25. Akawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

قَالَ رَبُّكُمْ وَرَبُّ آبَائِكُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٢٦﴾

26. Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

قَالَ إِنَّ رَسُولَكُمُ الَّذِي أُرْسِلَ إِلَيْكُمْ لَمَجْنُونٌ ﴿٢٧﴾

27. Akasema: Hakika mtume wenu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

قَالَ رَبُّ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُمْ تَعْقِلُونَ ﴿٢٨﴾

28. Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

قَالَ لَئِنِ اتَّخَذْتَ إِلَـٰهًا غَيْرِي لَأَجْعَلَنَّكَ مِنَ الْمَسْجُونِينَ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

قَالَ أَوَلَوْ جِئْتُكَ بِشَيْءٍ مُّبِينٍ ﴿٣٠﴾

30. Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?

قَالَ فَأْتِ بِهِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٣١﴾

31. Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

فَأَلْقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعْبَانٌ مُّبِينٌ ﴿٣٢﴾

32. Akaitupa fimbo, mara ikawa nyoka dhahiri.

وَنَزَعَ يَدَهُ فَإِذَا هِيَ بَيْضَاءُ لِلنَّاظِرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao.

قَالَ لِلْمَلَإِ حَوْلَهُ إِنَّ هَـٰذَا لَسَاحِرٌ عَلِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi, mjuzi.

يُرِيدُ أَن يُخْرِجَكُم مِّنْ أَرْضِكُم بِسِحْرِهِ فَمَاذَا تَأْمُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani?

قَالُوا أَرْجِهْ وَأَخَاهُ وَابْعَثْ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٣٦﴾

35. Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini.

يَأْتُوكَ بِكُلِّ سَحَّارٍ عَلِيمٍ ﴿٣٧﴾

37. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

MAJIBIZANO BAINA YA MUSA NA FIRAUNI

Aya 23 – 37

MAANA

Akasema Firauni: Na ninani huyo Mola wa walimwengu wote?

Ewe Musa! Wewe unadai kuwa ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote; hebu tubainishie jinsi yake na hakika yake huyo Mola?

Akasema: “Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.”

Musa alisema: Mwenyezi Mungu hajulikani isipokuwa kwa sifa zake na athari zake; zikiwa ni pamoja na huku kuumbwa ulimwengu huu wa ajabu katika mpangilio wake na nidhamu yake. Basi fikirini na mzingatie ikiwa mna akili zinazoweza kutambua kuwa nidhamu hii haiwezekani ila kwa uweza wa ujuzi na hekima.

Firauniakawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

Yaani mnasikia maajabu hayo. Hatujawahi kusikia haya kwa mababa zetu wa kwanza.

Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

Musa alisema kwa kusisitiza kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa ulimwengu, muumba wenu na muumba wa baba zenu wa mwanzo na pia ndiye muumba wa huyu Firauni mnayemfanya mungu na kumwabudu.

Akasema: Hakika mtume wenu huyu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

Musa ni mwendawazimu katika mantiki ya Firauni, kwa nini? Kwa sababu amesema Firauni si mungu bali ni kiumbe. Mantiki haya ya kifirauni anayo kila anayedai asichokuwa nacho. Yeyote anayedai kuwa na elimu naye ni mjinga, ikhlasi naye ni mhaini au ukweli naye ni mrongo, basi yeye yuko katika mila ya Firauni na desturi yake. Lau atapata wanaomwamini atasema: Mimi ndiye mola wenu au simjui mungu mwingine kwenu zaidi ya mimi; kama alivyosema Firauni.

Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

Musa aliendelea kushikilia msimamo wake kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu. Akaashiria kuchomoza jua na kuchwa kwake, ambapo Firauni hawezi kujasiri kusema kuwa yeye ndiye anayelichomoza jua mashariki na kulipeleka magharibi.

Kwa hiyo alipigwa na butwaa aliposikia maneno haya kutoka kwa Musa; sawa na alivyopigwa na butwaa Namrud kabla yake, pale Ibrahim(a.s) alipomnyamazisha kwa kusema:

فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ ﴿٢٥٨﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi.”

Juz. 3 (2:258).

Firauni alipoishiwa, alikereka, akawa anatoa vitisho naakasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

Jela na kutesa ndio silaha pekee ya utawala muovu wa mabavu dhidi ya haki uadilifu na uhuru, tangu zamani. Lakini jihadi ya wakombozi na ukakamavu wao, unaifanya silaha ya mataghuti ishindwe kwenye shingo zao na vifua vyao; kama ilivyoshindwa silaha ya Firauni.

Walisema wa kale: Mwenye kuchomoa upanga wa dhulma atauliwa nao.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

فَكُلًّا أَخَذْنَا بِذَنبِهِ فَمِنْهُم مَّنْ أَرْسَلْنَا عَلَيْهِ حَاصِبًا وَمِنْهُم مَّنْ أَخَذَتْهُ الصَّيْحَةُ وَمِنْهُم مَّنْ خَسَفْنَا بِهِ الْأَرْضَ ﴿٤٠﴾

“Kila mmoja tulimtesa kwa makosa yake. Kati yao wapo tuliowapelekea kimbunga cha changarawe, na kati yao wapo walionyakuliwa na ukelele na kati yao wapo ambao tuliwadidimiza katika ardhi.” (29:40).

Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?” Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

Musa hakuogopa vitisho vya Firauni na akamwambia kwa kujiamini kuwa utanifanya mfungwa hata kama ni mwenye haki, kwa kukuletea dalili isiyo na shaka kwako na kwa mwingine?

Atajibu nini Firauni? Je, amwambie ndio nitakufunga hata kama ni mwenye haki? Hawezi kumwambia hivi, kwa sababu itakuwa ni kukubali ukweli kuwa Musa ni Mtume wa Mola wa viumbe wote na kwamba yeye ni mzushi katika madai yake ya uungu. Kwa hiyo ndio akalazimika kusema lete hiyo dalili kama wewe ni mkweli.

Akaitupa fimbo mara ikawa nyoka dhahiri. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani? Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

Aya hizi sita zimetangulia katika Juz. 9 (7:107 - 112) zikifanana kiutaratibu, kimpangilio na hata herufi; isipokuwa katika mambo mawili:

Hapa imesemwa: ‘mchawi mkubwa’ na kule ikasemwa ‘mchawi’ hakuna tofauti katika maneno haya isipokuwa kutilia mkazo.

Hapa imesemwa: ‘Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi,’ na kule imesemwa: ‘Wakasema wakuu wa watu wa Firauni: Hakika huyu ni mchawi mjuzi.’ Tofauti hapa ni kubwa kama inavyojionyesha.

Kwa sababu hapa aliyesema ni Firauni kuwaambia wakuu na kule wakuu ndio waliosema kumwambia Firauni. Sasa je, kuna wajihi gani wa kuunganisha baina ya Aya mbili hizi?

Jibu : Sikupata ishara yoyote ya hilo katika tafsiri nilizonazo, wala sijui sababu yake. Kwa vyovyote iwavyo, jibu ninaloliona ni kuwa Firauni ndiye aliyeanza kuwaambia jamaa zake kuwa huyu ni mchawi; kisha jamaa zake nao wakaanza kuambiana kuwa ni kweli Musa ni mchawi; kama ilivyo kwa wanaoongozwa, wanaigiza kiongozi wao na kutolea ushahidi kauli zake.

Hapo basi hakuna kupingana baina ya Aya mbili. Firauni aliwaambia jamaa zake nao wakamwambia yeye kwa kumwigiza.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُهُمْ وَلَا يَضُرُّهُمْ وَكَانَ الْكَافِرُ عَلَىٰ رَبِّهِ ظَهِيرًا ﴿٥٥﴾

55. Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu. Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا مُبَشِّرًا وَنَذِيرًا ﴿٥٦﴾

56. Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

قُلْ مَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِلَّا مَن شَاءَ أَن يَتَّخِذَ إِلَىٰ رَبِّهِ سَبِيلًا ﴿٥٧﴾

57. Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

وَتَوَكَّلْ عَلَى الْحَيِّ الَّذِي لَا يَمُوتُ وَسَبِّحْ بِحَمْدِهِ وَكَفَىٰ بِهِ بِذُنُوبِ عِبَادِهِ خَبِيرًا ﴿٥٨﴾

58. Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ الرَّحْمَـٰنُ فَاسْأَلْ بِهِ خَبِيرًا ﴿٥٩﴾

59. Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi. Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اسْجُدُوا لِلرَّحْمَـٰنِ قَالُوا وَمَا الرَّحْمَـٰنُ أَنَسْجُدُ لِمَا تَأْمُرُنَا وَزَادَهُمْ نُفُورًا ﴿٦٠﴾

60. Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe? Na huwazidishia chuki.

تَبَارَكَ الَّذِي جَعَلَ فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَجَعَلَ فِيهَا سِرَاجًا وَقَمَرًا مُّنِيرًا ﴿٦١﴾

61. Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ خِلْفَةً لِّمَنْ أَرَادَ أَن يَذَّكَّرَ أَوْ أَرَادَ شُكُورًا ﴿٦٢﴾

62. Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

KAFIRI NI MSADIZI WA MPINZANI WA MOLA WAKE

Aya 55 – 62

MAANA

Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 11 (10 18).

Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

Yaani anawasaidia watu wa batili dhidi ya haki. Kila mwenye kusaidia batili atakuwa amesaidia dhidi ya Mwenyezi Mungu na kuwa adui yake; hata kama atamsabihi na kumtukuza kwa ulimi wake. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) :“Mwenye kumsaidia dhalimu na huku anajua kuwa ni dhalimu basi amejitenga na Uislamu.”

Kadiri nitakavyotia shaka, lakini siwezi kutia shaka kuwa mwenye kumtegemea dhalimu ni kafiri; bali kafiri aliye mwadilifu ni bora kuliko yeye. Aya za Qur’an kuhusu hilo ni nyingi na ziko wazi. Ama Hadith za Mtume zimepituka kiwango cha mutawatir.

Ndio! Ni wajibu wetu kuamiliana naye muamala wa kiislamu kwa vile tu ametamka: Lailaha illallah Muhammadurrasulullah (Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.)

Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 15 (17:105).

Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

Mimi sina tamaa ya mali yenu wala siwauzii pepo. Ninalotaka ni kutengeneza tu. Anayetaka kufanya njia ya kumwendea Mola miongoni mwenu, basi malipo yake yako kwa Mungu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz.12 (11:88).

Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

Ewe Muhammad! Toa bishara na onyo ukimtegemea Mwenyezi Mungu kwa kuwa na ikhlasi naye katika kauli yako na vitendo vyako na ujitakashe na kumfanyia mfano na kila lile ambalo halifanani na utukufu na ukuu wake. Yeye anamjua zaidi aliyepotea njia, na atamhisabu na kumlipa.

Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi.

Makusudio ya kustawi ni kutawala. Lililo na nguvu ni kuwa makusudio ya siku ni mikupuo, kwa sababu hakuna siku kabla ya kupatikana ulimwengu na jua. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:54), Juz. 11 (103), na Juz. 12 (11:7).

Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

Habari yake, ni habari ya huko kuumbwa mbingu na ardhi, ambako kunafahamika kutokana na mfumo wa Aya. Hapa kuna maneno yaliyotan- gulizwa na ya kukadiriwa. Maana ni: Yeye ni Mwingi wa rehema, ulizia habari za kuumbwa mbingu na ardhi kwa yule ajuaye ambaye ni Mwenyezi Mungu.

Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: ‘Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe?’ Na huwazidishia chuki.

Nabii(s.a.w.w) akiwaambia washirikina: ‘Mwabuduni Mwingi wa rehema, wala msiabudu masanamu,’ wao husema kwa kujitia hamnazo, kwa madharau, ni nani huyo unayetuambia tumwabudu unayemuita Mwingi wa rehema? Unataka tukutii wewe na tuwaasi baba zetu katika yale waliyokuwa wakiyaabudu?’

Ujinga na upumbavu huu unatukumbusha ujinga wa vijana wetu wanapoambiwa swalini na mfunge, husema: “Bado kuna Swala katika karne hii ya ishirini? Jambo la kushangaza ni kuwa vijana hawa wanaimba uhuru wa bianadamu; kama kwamba uhuru ni uzandiki na utu ni kujitoa kwenye misimamo.

Hawajui kuwa aliye huru ni yule anayemwabudu Mwenyezi Mungu wala hamnyenyekei asiyekuwa yeye na kwamba utu ni dini ya Mwenyezi Mungu ambayo inakataza maovu na munkar.

Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

Makusudio ya buruji ni mashukio ya jua na mwezi. Tazama Juz.14 (15: 16). Makusudio ya taa hapa ni jua, kutokana na kuunganisha na mwezi. Mahali pengine Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ الشَّمْسَ ضِيَاءً وَالْقَمَرَ نُورًا ﴿٥﴾

“Yeye ndiye aliyefanya jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru.” Juz.11 (10:5).

Wengine wametofautisha baina ya nuru na mwanga. Kwamba mwanga unategemea sayari moja kwa moja; kama vile mwanga wa jua, unatoka kwenye jua moja kwa moja.

Nuru inategemea sayari kupitia sayari nyingine; kama vile nuru ya mwezi inavyotegmea jua. Wametoa dalili wanaotofautisha, kwa Aya hiyo ya Juz. 11 (10:5) tuliyoitaja punde.

Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

Usiku unaondoka kisha unakuja mchana, nao unaondoka kisha unarudi usiku na kuendelea; wala hakuna unaobakia muda mrefu kuzidi kiasi cha haja ya viumbe.

Kufuatana kwa namna hii kunafahamisha kuweko mpangiliaji mwenye hekima. Kufuatana huku kunategemea harakati za ardhi, nazo zinategemea msababishaji wake wa kwanza.

Ama hekima ya mfuatano huu, ni kwamba lau lingelibakia giza tu, au mwangaza tu, maisha yangelikuwa magumu hapa ardhini.

Kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) ‘Kwa anayetaka kukumbuka,’ maana yake ni kuwa mwenye kutaka dalili ya kuweko Mwenyezi Mungu ataipata katika vitu vyote, vikiwemo kufuatana usiku na mchana.

Na kauli yake ‘Au anayetaka kushukuru,’ ni kuwa anayetaka kumshukuru Mweneyzi Mungu kwa neema yake naashukuru vile vile kwa kufuatana usiku na mchana, kwa sababu hilo ni katika neema kubwa.

وَعِبَادُ الرَّحْمَـٰنِ الَّذِينَ يَمْشُونَ عَلَى الْأَرْضِ هَوْنًا وَإِذَا خَاطَبَهُمُ الْجَاهِلُونَ قَالُوا سَلَامًا ﴿٦٣﴾

63. Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu. Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

وَالَّذِينَ يَبِيتُونَ لِرَبِّهِمْ سُجَّدًا وَقِيَامًا ﴿٦٤﴾

64. Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا اصْرِفْ عَنَّا عَذَابَ جَهَنَّمَ إِنَّ عَذَابَهَا كَانَ غَرَامًا ﴿٦٥﴾

65. Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam,’ hakika adhabu yake ni yenye kuendelea.

إِنَّهَا سَاءَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٦٦﴾

66. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa.

وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴿٦٧﴾

67. Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo.

وَالَّذِينَ لَا يَدْعُونَ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ وَلَا يَقْتُلُونَ النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّـهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَا يَزْنُونَ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ يَلْقَ أَثَامًا ﴿٦٨﴾

68. Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki, wala hawazini. Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

يُضَاعَفْ لَهُ الْعَذَابُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَيَخْلُدْ فِيهِ مُهَانًا ﴿٦٩﴾

69. Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

إِلَّا مَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ عَمَلًا صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ يُبَدِّلُ اللَّـهُ سَيِّئَاتِهِمْ حَسَنَاتٍ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٧٠﴾

70. Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.

وَمَن تَابَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَإِنَّهُ يَتُوبُ إِلَى اللَّـهِ مَتَابًا ﴿٧١﴾

71. Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

وَالَّذِينَ لَا يَشْهَدُونَ الزُّورَ وَإِذَا مَرُّوا بِاللَّغْوِ مَرُّوا كِرَامًا ﴿٧٢﴾

72. Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

وَالَّذِينَ إِذَا ذُكِّرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ لَمْ يَخِرُّوا عَلَيْهَا صُمًّا وَعُمْيَانًا ﴿٧٣﴾

73. Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawajifanyi ni viziwi nazo na vipofu.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا هَبْ لَنَا مِنْ أَزْوَاجِنَا وَذُرِّيَّاتِنَا قُرَّةَ أَعْيُنٍ وَاجْعَلْنَا لِلْمُتَّقِينَ إِمَامًا ﴿٧٤﴾

74. Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wanetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

أُولَـٰئِكَ يُجْزَوْنَ الْغُرْفَةَ بِمَا صَبَرُوا وَيُلَقَّوْنَ فِيهَا تَحِيَّةً وَسَلَامًا ﴿٧٥﴾

75. Hao ndio watakolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam.

خَالِدِينَ فِيهَا حَسُنَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٧٦﴾

76. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

قُلْ مَا يَعْبَأُ بِكُمْ رَبِّي لَوْلَا دُعَاؤُكُمْ فَقَدْ كَذَّبْتُمْ فَسَوْفَ يَكُونُ لِزَامًا ﴿٧٧﴾

77. Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

WAJA WA MWINGI WA REHEMA

Aya 63 – 77

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja sifa za makafiri na kiaga chao, kama kawaida yake, anataja sifa za waumini na malipo aliyowaandalia. Zifuatazo ndizo sifa zao:

1.Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu.

Imam Jafar Sadiq(a.s) anasema katika tafsiri ya hilo:“Ni yule mtu anayetembea kwenye asili yake aliyoumbiwa, hajikalifishi wala hajifanyi.” Ndio, anayetembea kwenye umbile lake aliloumbiwa, tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wapambe na wafuasi wanaomfuta nyuma na wengine mbele wakiwa wamepanda farasi au pikipiki na kupiga ving’ora vinavyohanikiza watu kwa sauti zake vikitangaza kuja kwake ili aachiwe njia, kwa ajili ya kumheshimu na kumtukuza.

2.Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

Makusudio ya kusemeshwa na wajinga ni kama vile kejeli zao, shutuma zao au mijadala ya hawa na masilahi. Amani ni kinaya cha kuachana nao, kwa kuwadharau na kuchunga mtu heshima yake. Maana ni kuwa, muumini akisikia neno ovu, aachane nalo; kama kwamba hakulisikia au kama anayekusudiwa ni mwingine sio yeye. Huu ndio mwepuko mwema aliousema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَاهْجُرْهُمْ هَجْرًا جَمِيلًا ﴿١٠﴾

“Na uwaepuke mwepuko mwema.” (73:10).

Hakuna mwenye shaka kwamba kuachana na jambo ni pale ikiwa hakuna uwezo au nguvu za kulikabili. Vinginevyo itakuwa ni wajibu kulikabili. Hapana budi kuihusisha Aya na hilo.

3.Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

Waumini wanasimama usiku kwenye giza wakifanya ibada ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu hilo liko mbali na ria, wala hawaupitishi usiku mikahawani na kwenye mambo ya mchezo mchezo tu, huku wakifuja mali na kupanga njama dhidi ya waumini na wenye ikhlasi. Mfano wa Aya hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:

كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ ﴿١٧﴾

“Walikuwa wakilala kidogo usiku.” (51:17).

4.Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam, hakika adhabu yake ni yenye kuendelea. haikwepeki na ni yakudumu. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa,

Waliamini Pepo na Moto, kutokana na waliyoyashuhudia na kuyaona; ndio wakauhofia moto wakaitumai pepo. Imam Ali(a.s ) anasema: “Wao na Pepo ni kama walioiona wakiwa ndani yake wananeemeshwa. Na wao na moto ni kama waliouona wakiwa ndani yake wanaadhibiwa.”

5.Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo, hakuna kupitisha kiasi, Si ubakhili wala ubadhirifu.

Huu ndio mwenendo wa Uislamu, wastani katika kila kitu; hakuna ulahidi wala waungu wengi, udikteta wala ukiritimba na hakuna kutaifisha mali ya mtu wala ubepari. Tazama Juz. 15 (17:29) kifungu cha ‘Uislamu na nadharia ya maadili.’

6.Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Mwenye kufanya riya au akamtii kiumbe katika kumuasi Muumba, basi huyo ni kama aliyemwomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki.

Nafsi inayouliwa kwa haki na kwa uadilifu ni ile iliyoua nafsi nyingine bila ya haki, aliyezini akiwa kwenye ndoa, kurtadi dini au kuleta ufisadi katika ardhi.

Ufafanuzi wa hayo uko katika vitabu vya Fiqh.

Wala hawazini

Kwa sababu zinaa ni katika madhambi makubwa. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t). Akaiweka sawa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuua nafsi na akajaalia hukumu ya haya matatu ni kuuliwa kwa masharti yaliyotajwa kwenye vitabu vya fiqh.

Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

Hayo ni hayo ya shirk, kuua na kuzini. Na madhambi ni adhabu.

Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

Kuna adhabu gani kubwa na kufedheheka zaidi kuliko adhabu ya Jahannam? Si kwambii tena ikiwa itazidishwa pamoja na kudumu kusiko na mwisho.

Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

Mwenye kutubia dhambi ni kama asiyekuwa na dhambi, zaidi ya hayo, Mwenyezi Mungu atampa thawabu kwa kule kutubia kwake na atampa mema kulingana na maovu ya dhambi zake; kiasi ambacho toba itafuta maovu ya dhambi.

إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ ﴿١١٤﴾

“Hakika mema huondoa maovu.” Juz. 12 (11:114).

Haya ndiyo maana ya ‘Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema’ kwa sababu uovu, kwa ulivyo, haustahiki kuwa wema, wala wema, kwa ulivyo, haustahiki kuwa uovu’

Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

Baada ya kubainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya iliyotangulia kwamba mwenye kutubia atampa thawabu za mwenye kufanya mema, hapa anamsifu kuwa amerejea kwa Muumba wake kurejea kuzuri.

7.Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

Neno ‘hawawi’ limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu ‘laa yash-hadu- una’ kama ilivyotumika tafsiri hiyo katika Juz. 2 (2:185). Makusudio ya uzushi ni mambo ya batili na upuzi ni kila lisilo na kheri. Maana ni kuwa waumini hawahudhurii vikao vya ubatilifu wala hawavisaidii, sikwambii kuvifanya. Pia hawashiriki mazungumzo yasiyokuwa na kheri na wanapoyapitia hayo masiko yao huyaepuka; kama wanavyoziepusha ndimi zao kuayatamka; sawa na nyuki anavyopita haraka kwenye mzoga na harufu mbaya.

8.Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawaji- fanyi ni viziwi nazo na vipofu.

Mshairi huwa anasikiliza mashairi kwa umakini kabisa. Vile vile kila mwenye kuhusika na jambo akizungumziwa huwa anakuwa makini nalo sana anapolisikilza. Mtu unapomzungumzia jambo lililo mbali naye atakuepuka na hayo mazungumzo yako, hata kama ni ya uongofu na mwangaza.

Hapa ndipo inabainika siri ya muumini kuikubali Qur’an, na kafiri kuachana nayo. Mumin anakikubali Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa vile anakiamini na kutambua maana yake na makusudio yake. Anakikuta kwenye nafsi yake, itikadi yake, matendo yake mema na malipo aliyomuandalia Mola wake.

Kafiri anakipa mgongo Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa sababu anakipinga na hajui malengo yake na siri yake; wala hapati humo isipokuwa kushutumiwa na kukosolewa itikadi yake na sifa zake na pia makaripio ya ukafiri wake.

9.Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

Muovu huwa anatamaani watu wamfuate katika uovu wake, sio kwa kuwa amekinai kuwa yuko kwenye uongofu kutoka kwa Mola wake, hapana! Isipokuwa anataka kupunguza lawama na shutuma na kufunika kosa lake kwa kuwa wengi wakosefu. Lakini hataki mkewe na watoto wake wawe hivyo; kama vile mgonjwa asivyopenda watu wake wapatwe na ugonjwa alio nao.

Ama yule aliye mwema na mwenye takua ana yakini na dini yake na ana busara katika mambo yake. Kwa hivyo huwa anatamaani kwa dhati ya moyo kimsingi na kiitikadi kuwa watu wote wafuate njia yake na kwamba watoto wake wakimuiga yeye huwa anafurahi.

Kwa hiyo wenye ikhlasi humuomba Muumba wao wapate wa kuwaiga, sio kwa kuziba vitendo vyao kwa watu wala kutaka jaha duniani na kuchukua mali kwa kutumia haki za Mwenyezi Mungu; bali ni kwa kujipendekeza mbele ya Mwenyezi Mungu aliye peke yake.

Hao ndio watakaolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

Ghorofa ni kinaya cha makao ya juu. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha wasifu wa wenye takua na watiifu, sasa anataja malipo yao watakayoyapata kwake, ambayo ni kudumu katika raha, amani na neema pamoja na heshima.

Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja subira hapa kuashiria kuwa kila mwenye haki hana budi kupata taabu na udhia kutoka kwa wasio na haki na kwamba thawabu za Mwenyezi Mungu hatazipata ispokuwa mwenye kuwa na uvumilivu na subira na akaendelea kuwa na msimamo kadiri hali itakavyokuwa ngumu.

Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

Makusudio ya neno ‘duakum’ hapa ni kupewa mwito kutokana na maneno yanayovutia, lakini mlikadhibisha. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ ﴿٥٢﴾

“Basi watawaita nao hawatawaitikia.” Juz. 15 (18:52)

Kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapa mwito kwenye imani na utiifu kupitia kwa Mtume wake.

Maana ni kuwa nyinyi washirikina hamstahiki hata kutajwa pia lau si kuwa mliitwa kwenye imani na utiifu, ili kuweko na hoja siku ya hisabu na malipo, ikiwa hamtasikia na kuitikia mwito. Nanyi mmeupinga mwito na mkadhibishaji aliyetoa mwito huo, basi adhabu inawastahiki na ni lazima.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Sura Ya Ishirini Na Sita: Surat Shua’rau.

Twabrasiy amesema imeshuka Makka isipokuwa Aya 224 hadi mwisho, zimeshuka Madina. Ina Aya 227

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehma Mwenye kurehemu.

طسم ﴿١﴾

1. Twaa Siin Miim.

تِلْكَ آيَاتُ الْكِتَابِ الْمُبِينِ ﴿٢﴾

2. Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

لَعَلَّكَ بَاخِعٌ نَّفْسَكَ أَلَّا يَكُونُوا مُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

إِن نَّشَأْ نُنَزِّلْ عَلَيْهِم مِّنَ السَّمَاءِ آيَةً فَظَلَّتْ أَعْنَاقُهُمْ لَهَا خَاضِعِينَ ﴿٤﴾

4. Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

وَمَا يَأْتِيهِم مِّن ذِكْرٍ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ مُحْدَثٍ إِلَّا كَانُوا عَنْهُ مُعْرِضِينَ ﴿٥﴾

5. Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao.

فَقَدْ كَذَّبُوا فَسَيَأْتِيهِمْ أَنبَاءُ مَا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٦﴾

6. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

أَوَلَمْ يَرَوْا إِلَى الْأَرْضِ كَمْ أَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ زَوْجٍ كَرِيمٍ ﴿٧﴾

7. Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٨﴾

8. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٩﴾

9. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

HUENDA UKAANGAMIZA NAFSI YAKO

Aya 1-9

MAANA

Twaa Siin Miim.

Umetangulia mfano wake mwanzo wa Sura Baqara, Juz. 1

Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

Hizo ni ishara ya Aya za Sura hii, kitabu ni Qur’an na chenye kubainisha ni kubainisha haki na kudhihirisha.

Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) kwamba asiikere na kuiumiza nafsi yake kwa sababu ya watu wake kuukataa uongofu na haki. Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:35) na Juz. 15 (18:6).

Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu: Poa moyo wako! Lau tungelitaka waamini kwa nguvu tungeliteremsha adhabu kutoka mbinguni waione kwa macho na kuwaambia chagueni imani au adhabu; bila shaka wao wangelisalimu amri kwa unyenyekevu.

Lakini je, hii itahisabiwa kuwa ni imani? Hapana! Imani ya kweli inakuwa kwa utashi na hiyari, sio kwa kulazimishwa kwa nguvu. Ndio maana tukawakadiria kheri na shari, tukawaamrisha hili na kuwakataza lile; kisha tukawaachia hiyari, waweze kustahiki thawabu kwa utiifu na adhabu kwa uasi.

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifanya hivyo katika zama za Musa(a.s) kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na tulipoinua mlima juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawaangukia. Tukawaambia: shikeni kwa nguvu tuliyowapa.” Juz. 9 (7: 171).

Jibu : kwa hakika Qur’an Tukufu inafahamisha waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ana muamala maalum na Mayahudi usiofanana na waja wengine. Kwa sababu wao wana tabia za pekee zisizokuwa na mfano. Tumelizungumzia hilo kwa ufafanuzi zaidi kwa anuani ya ‘Mayahudi hawana mfano’ katika Juz. 1: (2:63-66).

Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

Tumewaongoza washirikina, kupitia kwako ewe Muhammad, kwenye yale yaliyo na kheri yao na masilahi yao, wakaachana nayo, wakayadharau na kuyafanyia masikhara. Basi nawe achana nao na watakumbana na adhabu waliyoahidiwa tu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:68).

Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

Alikufuru Mungu aliyekufuru huku akiona dalili na ubainifu wa kupatikana kwake na ukuu wake. Miongoni mwa dalili hizi ni kutoa mimea ya aina na rangi mbali mbali. Kwa maelezo zaidi angalia Juz.7 (6:99) na Juz. 13 (13:3).

Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Kwa nguvu zake anawashinda mataghuti na rehema zake anawapa muda bila ya kuwaharakishia adhabu mpaka awajie mbashiri na muonyaji na kuwapa fursa ya kufikiria vizuri na kutubia.

Imam Ali(a.s) anasema:“Hasira zake hazimfanyi kuacha huruma yake, wala huruma haimfanyi kupuuza adhabu yake.”

وَإِذْ نَادَىٰ رَبُّكَ مُوسَىٰ أَنِ ائْتِ الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠﴾

10. Na Mola wako alipomwita Musa kwamba nenda kwa watu madhalimu.

قَوْمَ فِرْعَوْنَ أَلَا يَتَّقُونَ ﴿١١﴾

11. Watu wa Firauni. Hawaogopi?

قَالَ رَبِّ إِنِّي أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ ﴿١٢﴾

12. Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

وَيَضِيقُ صَدْرِي وَلَا يَنطَلِقُ لِسَانِي فَأَرْسِلْ إِلَىٰ هَارُونَ ﴿١٣﴾

13. Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

وَلَهُمْ عَلَيَّ ذَنبٌ فَأَخَافُ أَن يَقْتُلُونِ ﴿١٤﴾

14. Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

قَالَ كَلَّا فَاذْهَبَا بِآيَاتِنَا إِنَّا مَعَكُم مُّسْتَمِعُونَ ﴿١٥﴾

15. Akasema, sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu. Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza.

فَأْتِيَا فِرْعَوْنَ فَقُولَا إِنَّا رَسُولُ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote.

أَنْ أَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿١٧﴾

17. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

قَالَ أَلَمْ نُرَبِّكَ فِينَا وَلِيدًا وَلَبِثْتَ فِينَا مِنْ عُمُرِكَ سِنِينَ ﴿١٨﴾

18. Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi?

وَفَعَلْتَ فَعْلَتَكَ الَّتِي فَعَلْتَ وَأَنتَ مِنَ الْكَافِرِينَ ﴿١٩﴾

19. Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

قَالَ فَعَلْتُهَا إِذًا وَأَنَا مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Akasema: Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.

فَفَرَرْتُ مِنكُمْ لَمَّا خِفْتُكُمْ فَوَهَبَ لِي رَبِّي حُكْمًا وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٢١﴾

21. Basi niliwakimbia nilipowahofia. Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

وَتِلْكَ نِعْمَةٌ تَمُنُّهَا عَلَيَّ أَنْ عَبَّدتَّ بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٢٢﴾

22. Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

MUSA

Aya 10 – 22

MAANA

Aya hizi hadi kufikia Aya ya 28 ni za kisa cha Musa ambacho kimetangulia mara kadhaa. Katika Juz. 16 (20: 9) tumeleza sababu za kukaririka kisa hicho.

Na Mola wako alipomwita, Musa kwamba nenda kwa watu madhal- imu watu wa Firauni.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:24).

Hawaogopi?

Hii ni jumla nyingine, maana yake ni kuwa, umefika wakati sasa Firauni na watu wake waogope mwisho wa uovu na utaghuti.

Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

Katika Juz. 16 (20 45) ni: “Ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.”

Yaani asije akatuwahi kutuadhibu kabla kufikishia ujumbe.

Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Musa kupeleka ujumbe wake kwa Firauni. Na hili, kwa upande mmoja, ni jambo zito na lenye mashaka sana, kutokana na utaghuti wa Firauni na nguvu za utawala wake. Na kwa upande mwingine, ujumbe wenyewe ni mzito.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwambia Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) :

إِنَّا سَنُلْقِي عَلَيْكَ قَوْلًا ثَقِيلًا ﴿٥﴾

“Hakika sisi tutakuteremshia kauli nzito.” (73:5).

Musa alikuwa ni mwepesi wa kughadhibika kwa ajili ya haki, na ulimi wake ulikuwa na kigugumizi kinachomzuia kutamka. Kwa hiyo akahofia kutotekeleza vizuri ujumbe mkuu. Hakuna yeyote anayehofia kutekeleza haki ya Mwenyezi Mungu kuliko mitume; hasa wale Ulul-a’zm. Hii inatokana na isma. Ndipo Musa akamtaka Mwenyezi Mungu kumtuma Jibril kwa nduguye, Harun, ili awe msaidizi wake katika jambo hili muhimu.

Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

Anaishiria lile tukio la kumuua mtu wa upande wa Firauni pale alipom- saidia mtu wa upande wake; kama ilivyoelezwa katika Aya hii:

فَوَجَدَ فِيهَا رَجُلَيْنِ يَقْتَتِلَانِ هَـٰذَا مِن شِيعَتِهِ وَهَـٰذَا مِنْ عَدُوِّهِ فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ ﴿١٥﴾

“Na akakuta humo watu wawili wanapigana – mmoja ni katika wenzake na mwingine ni katika maadui zake. Yule aliye katika wenzake akamtaka msaada juu ya adui yake. Musa akampiga ngumi akammaliza.” (28:15).

Musa alihofia kuchukua risala ya Mwenyezi Mungu kwa Firauni asije akamuua kabla kukamilisha lengo, lakini akiwa na nduguye na ikatokewa kuuawa, basi atachukua nafasi yake kuendeleza malengo.

Akasema – Mwenyezi Mungu –sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu, Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

Musa alihofia dhiki ya kifua, kufungika ulimi na kuuliwa, lakini Mwenyezi Mungu akamhakikishia usalama na akamwambia kuwa hakuna kitu kitaka- chokuwa katika hayo, kwa sababu mimi nitawasaidia na kuwanusuru. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20: 46 – 47).

Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi? Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

Musa na Harun walielekea kwa Firauni, wakaingia kwake wakiwa wamevaa deraya ya sufu, mikononi mwao wakiwa na fimbo. Wakampa mwito wa kumwamini Mungu na kumpa sharti la kusilimu na kutii ili utawala wake ubakie na kudumu enzi yake.

Firauni aliwabeza wawili hawa, waliompa masharti ya kudumu utawala na enzi yake, wakiwa hawana cheo chochote wala mali. Hakutaka kuwaua kwa kuhofia asiambiwe kuwa ameshindwa na hoja akakimbilia upanga.

Lakini Firauni anaweza kuwa na hoja gani? Ni kwa mantiki gani atakayoweza kujadili? Hana kitu isipokuwa kuvungavunga na kumtajia Musa yaliyopita.

Je, hatukukulea na ukakaa nyumbani kwetu miaka, kisha ukatuulia mtu wetu na ukakimbia? Hii ndio shukrani yako? Zaidi ya hayo unadai kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwetu? Unataka tukusikize na kukutii na sisi ndio mabwana zako na wafadhili wa neema zako?

Kisha Firauni akawegeukia watu wa baraza lake na akasema: “Basi mbona hakuvikwa vikukuku vya dhahabu?” (43:53). Kwenye dhahabu tu ndio kuna kuwa na siri ya mantiki ya mataghuti. Hakuna utume wala ubwana au ubora isipokuwa kwa ajili ya dhahabu na dhahabu yenyewe.

Musa (a.s) akamjibu kuhusu kuua akasema: “Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.”

Yaani sikuelewa kuwa ngumi yangu itamuua. Nami nilikusudia kukinga na kutia adabu, nikakosea makusudio. Basi mimi nina dhambi gani katika hilo? Kukusudia ni nguzo ya msingi ya kosa la jinai kwa watu wa sharia.

Basi niliwakimbia nilipowahofia.

Sikukimbia hukumu ya uadilifu, bali nilikimbia dhulma kwa kuhofia kunichukulia kuwa ni muuaji wa makusudi. Kuna mmoja alimwambia Musa:

إِنَّ الْمَلَأَ يَأْتَمِرُونَ بِكَ لِيَقْتُلُوكَ فَاخْرُجْ إِنِّي لَكَ مِنَ النَّاصِحِينَ ﴿٢٠﴾

“Hakika wakubwa wanashauriana kukuua. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanaokupa nasaha.” (28:20).

Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

Firauni alimtajia Musa ufukara na utoro; Musa naye akamwambia kuwa utukufu haupimwi kwa mali wala kwa ufalme; isipokuwa uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu, humpatia amtakaye katika waja wake. Na mimi Mwenyezi Mungu amenitunukia elimu ya dini yake na sharia yake kwa njia ya kheri na usawa na akanitukuza kwa kunituma kwako na kwa watu wako.

Musa aliendelea kumjibu Firauni, kuhusu malezi na akasema:

Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

Yaani unanisimbulia kwa malezi yako kwangu na unajitia kutojua kuwa sababu ni uadui wako wa kuwachinja watoto wa kiume wa watu wangu na kuwatia utumwani watoto wao wa kike? Mama yangu alipohofia wewe kunichinja akanitupa baharini na matokeo yake yakawa ni kuishi mimi mbali ugenini bila ya huruma ya mama na mapenzi ya baba? Hii ndiyo fadhila yako kwangu? Firauni alizibwa mdomo, akaanza kuwatafuta wabatilifu wake; kama utakavyoona katika kifungu kifuatacho.

قَالَ فِرْعَوْنُ وَمَا رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٢٣﴾

23. Akasema Firauni: Na ni nani huyo Mola wa walimwengu wote?

قَالَ رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ ﴿٢٤﴾

24. Akasema: Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.

قَالَ لِمَنْ حَوْلَهُ أَلَا تَسْتَمِعُونَ ﴿٢٥﴾

25. Akawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

قَالَ رَبُّكُمْ وَرَبُّ آبَائِكُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٢٦﴾

26. Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

قَالَ إِنَّ رَسُولَكُمُ الَّذِي أُرْسِلَ إِلَيْكُمْ لَمَجْنُونٌ ﴿٢٧﴾

27. Akasema: Hakika mtume wenu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

قَالَ رَبُّ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُمْ تَعْقِلُونَ ﴿٢٨﴾

28. Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

قَالَ لَئِنِ اتَّخَذْتَ إِلَـٰهًا غَيْرِي لَأَجْعَلَنَّكَ مِنَ الْمَسْجُونِينَ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

قَالَ أَوَلَوْ جِئْتُكَ بِشَيْءٍ مُّبِينٍ ﴿٣٠﴾

30. Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?

قَالَ فَأْتِ بِهِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٣١﴾

31. Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

فَأَلْقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعْبَانٌ مُّبِينٌ ﴿٣٢﴾

32. Akaitupa fimbo, mara ikawa nyoka dhahiri.

وَنَزَعَ يَدَهُ فَإِذَا هِيَ بَيْضَاءُ لِلنَّاظِرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao.

قَالَ لِلْمَلَإِ حَوْلَهُ إِنَّ هَـٰذَا لَسَاحِرٌ عَلِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi, mjuzi.

يُرِيدُ أَن يُخْرِجَكُم مِّنْ أَرْضِكُم بِسِحْرِهِ فَمَاذَا تَأْمُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani?

قَالُوا أَرْجِهْ وَأَخَاهُ وَابْعَثْ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٣٦﴾

35. Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini.

يَأْتُوكَ بِكُلِّ سَحَّارٍ عَلِيمٍ ﴿٣٧﴾

37. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

MAJIBIZANO BAINA YA MUSA NA FIRAUNI

Aya 23 – 37

MAANA

Akasema Firauni: Na ninani huyo Mola wa walimwengu wote?

Ewe Musa! Wewe unadai kuwa ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote; hebu tubainishie jinsi yake na hakika yake huyo Mola?

Akasema: “Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.”

Musa alisema: Mwenyezi Mungu hajulikani isipokuwa kwa sifa zake na athari zake; zikiwa ni pamoja na huku kuumbwa ulimwengu huu wa ajabu katika mpangilio wake na nidhamu yake. Basi fikirini na mzingatie ikiwa mna akili zinazoweza kutambua kuwa nidhamu hii haiwezekani ila kwa uweza wa ujuzi na hekima.

Firauniakawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

Yaani mnasikia maajabu hayo. Hatujawahi kusikia haya kwa mababa zetu wa kwanza.

Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

Musa alisema kwa kusisitiza kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa ulimwengu, muumba wenu na muumba wa baba zenu wa mwanzo na pia ndiye muumba wa huyu Firauni mnayemfanya mungu na kumwabudu.

Akasema: Hakika mtume wenu huyu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

Musa ni mwendawazimu katika mantiki ya Firauni, kwa nini? Kwa sababu amesema Firauni si mungu bali ni kiumbe. Mantiki haya ya kifirauni anayo kila anayedai asichokuwa nacho. Yeyote anayedai kuwa na elimu naye ni mjinga, ikhlasi naye ni mhaini au ukweli naye ni mrongo, basi yeye yuko katika mila ya Firauni na desturi yake. Lau atapata wanaomwamini atasema: Mimi ndiye mola wenu au simjui mungu mwingine kwenu zaidi ya mimi; kama alivyosema Firauni.

Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

Musa aliendelea kushikilia msimamo wake kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu. Akaashiria kuchomoza jua na kuchwa kwake, ambapo Firauni hawezi kujasiri kusema kuwa yeye ndiye anayelichomoza jua mashariki na kulipeleka magharibi.

Kwa hiyo alipigwa na butwaa aliposikia maneno haya kutoka kwa Musa; sawa na alivyopigwa na butwaa Namrud kabla yake, pale Ibrahim(a.s) alipomnyamazisha kwa kusema:

فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ ﴿٢٥٨﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi.”

Juz. 3 (2:258).

Firauni alipoishiwa, alikereka, akawa anatoa vitisho naakasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

Jela na kutesa ndio silaha pekee ya utawala muovu wa mabavu dhidi ya haki uadilifu na uhuru, tangu zamani. Lakini jihadi ya wakombozi na ukakamavu wao, unaifanya silaha ya mataghuti ishindwe kwenye shingo zao na vifua vyao; kama ilivyoshindwa silaha ya Firauni.

Walisema wa kale: Mwenye kuchomoa upanga wa dhulma atauliwa nao.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

فَكُلًّا أَخَذْنَا بِذَنبِهِ فَمِنْهُم مَّنْ أَرْسَلْنَا عَلَيْهِ حَاصِبًا وَمِنْهُم مَّنْ أَخَذَتْهُ الصَّيْحَةُ وَمِنْهُم مَّنْ خَسَفْنَا بِهِ الْأَرْضَ ﴿٤٠﴾

“Kila mmoja tulimtesa kwa makosa yake. Kati yao wapo tuliowapelekea kimbunga cha changarawe, na kati yao wapo walionyakuliwa na ukelele na kati yao wapo ambao tuliwadidimiza katika ardhi.” (29:40).

Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?” Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

Musa hakuogopa vitisho vya Firauni na akamwambia kwa kujiamini kuwa utanifanya mfungwa hata kama ni mwenye haki, kwa kukuletea dalili isiyo na shaka kwako na kwa mwingine?

Atajibu nini Firauni? Je, amwambie ndio nitakufunga hata kama ni mwenye haki? Hawezi kumwambia hivi, kwa sababu itakuwa ni kukubali ukweli kuwa Musa ni Mtume wa Mola wa viumbe wote na kwamba yeye ni mzushi katika madai yake ya uungu. Kwa hiyo ndio akalazimika kusema lete hiyo dalili kama wewe ni mkweli.

Akaitupa fimbo mara ikawa nyoka dhahiri. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani? Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

Aya hizi sita zimetangulia katika Juz. 9 (7:107 - 112) zikifanana kiutaratibu, kimpangilio na hata herufi; isipokuwa katika mambo mawili:

Hapa imesemwa: ‘mchawi mkubwa’ na kule ikasemwa ‘mchawi’ hakuna tofauti katika maneno haya isipokuwa kutilia mkazo.

Hapa imesemwa: ‘Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi,’ na kule imesemwa: ‘Wakasema wakuu wa watu wa Firauni: Hakika huyu ni mchawi mjuzi.’ Tofauti hapa ni kubwa kama inavyojionyesha.

Kwa sababu hapa aliyesema ni Firauni kuwaambia wakuu na kule wakuu ndio waliosema kumwambia Firauni. Sasa je, kuna wajihi gani wa kuunganisha baina ya Aya mbili hizi?

Jibu : Sikupata ishara yoyote ya hilo katika tafsiri nilizonazo, wala sijui sababu yake. Kwa vyovyote iwavyo, jibu ninaloliona ni kuwa Firauni ndiye aliyeanza kuwaambia jamaa zake kuwa huyu ni mchawi; kisha jamaa zake nao wakaanza kuambiana kuwa ni kweli Musa ni mchawi; kama ilivyo kwa wanaoongozwa, wanaigiza kiongozi wao na kutolea ushahidi kauli zake.

Hapo basi hakuna kupingana baina ya Aya mbili. Firauni aliwaambia jamaa zake nao wakamwambia yeye kwa kumwigiza.


5

6

7

8

9

10

11

12

13

14

15

16