HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU23%

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU Mwandishi:
: AZIZI NJOZI
Kundi: Wanawake

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU
  • Anza
  • Iliyopita
  • 33 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 47724 / Pakua: 5540
Kiwango Kiwango Kiwango
HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

Mwandishi:
Swahili

5

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

MWANAMKE KATIKA QUR'ANI

Sasa tunataka kujibu swali iwapo Uislamu unamtazama mwanamke kuwa ni sawa na mwanaume kama binadamu au unamuona ni wa hadhi ya chini kuliko mwanaume. Falsafa maalum ya Uislamu juu ya haki za kifamilia. Kuhusiana na haki za mwanaume na mwanamke, Uislamu, una falsafa yake maalum ambayo ni tofauti, yale yaliyotokea miaka 1400 iliyopita na yanayotokea hivi sasa. Uislamu hauamini kuwa katika mambo yote mwanaume na mwanamke wana haki na majukumu yanayofanana.

Katika mambo fulani haki na majukumu yao ni tofauti na matokeo yake ni kuwa katika baadhi ya mambo nafasi yao inafanana na ya wanaume na katika baadhi ya mambo haifanani na ya wanaume. Hii sio kwa sababu Uislamu, kama falsafa nyingine, unamtazama mwanamke kwa dharau au jinsia yake sio bora kama ya mwanaume.

Uislamu unazitofautisha jinsia hizi mbili kwa sababu nyinginezo za msingi. Unaweza kuwasikia wafuasi wa mifumo ya Kimagharibi wakitaja kanuni za Kiislamu kama vile mahari, matunzo, talaka, ndoa za mitala na mengineyo, kuwa haya yote ni kama matusi kwa mwanamke na yanashusha hadhi yake. Wanawapotosha watu kuwa sheria na kanuni hizi hazina maana na ulazima na zinamfanya mwanaume aonekane ni bwana mkubwa. Wanasema kwamba katika kipindi chote cha historia, kabla ya karne ya 20, sheria na kanuni zote duniani ziliwekwa kwa kuzingatia kuwa mwanaume ni mwenye jinsia bora zaidi na kwamba mwanamke aliumbwa kwa maslahi na starehe ya mwanaume. Sheria zilizopitishwa na Uislamu pia ziko hivyo hivyo, zinampendelea mwanaume.

Wanadai kuwa Uislamu ni dini ya jinsia ya kiume. Hawamtambui mwanamke kuwa ni binadamu kamili. Hii ndio sababu haujampa haki sawa na mwanaume. Ungekuwa unamtambua kuwa ni binadamu kamili usingeruhusu ndoa za mitala (mke zaidi ya mmoja), usingehesabu ushahidi wa wanawake wawili kuwa ni sawa na wa mwanaume mmoja, usingeamuru gawio la mwanamke liwe nusu ya gawio la mwanaume, usingeamrisha papangwe bei ya mwanamke chini ya kivuli cha mahari na usingemfanya mwanamke awe tegemezi kwa mwanaume kwa upande wa matunzo, badala ya kufanya ajitegemee kiuchumi na kijamii.

Kwa kuzingatia yote haya ni dhahiri kuwa mafundisho ya Uislamu yanamtazama mwanamke kwa jicho la dharau. Uislamu unadai kuwa dini ya usawa lakini, katika mahusiano ya kifamilia hakuna usawa wowote uliozingatiwa. Wanashikilia kuwa katika suala la haki, Uislamu wazi wazi unampendelea mwanaume na ndio maana umempa miliki zote hizi. Tukipenda tunaweza kuweka hoja yao katika muundo wa kimantiki kuwa: Kama Uislamu unamhesabu mwanamke kuwa ni binadamu kamili ungekuwa umempa haki sawa na zinazofanana na zile za mwanaume, maadamu haujafanya hivyo basi haumhesabu kuwa ni binadamu kamili.

Usawa au kufanana? Hoja hii imejengwa juu ya msingi kwamba kwa vile heshima ya binaadamu ni sawa kwa mwanaume na mwanamke, hivyo lazima wote wapate haki zinazofanana bila kujali majukumu yao katika maisha. Hapana shaka, utu na heshima yao ni sawa kwao wao wote; wote wanapaswa kuwa na haki sawa. Lakini vipi kuhusu kufanana kwa haki zao?

Ikiwa badala ya kufuata kibubusa mawazo ya Kimagharibi tutaamua kufikiri sisi wenyewe, swali la kwanza linalokuja akilini ni iwapo kweli haki sawa zinamaanisha haki zinazofanana. Kwa kweli hayo ni mambo mawili tofauti. Usawa ni haki ya kuwa na daraja sawa kithamani na hadhi ambapo kufanana maana yake ni kulandana. Inawezekana baba akagawa mali zake kwa watoto wake watatu kwa usawa lakini sio kwa kulingana. Jaalia mali yake inajumuisha vitu mbali mbali kama vile maduka, mashamba na badhi ya mali zilizokodishwa. Baba kwa kuzingatia vipaji vyao na mambo ambayo kila mmoja anapenda, anaamua kumpa mmoja duka, mwingine shamba na wa tatu mali zilizokodishwa.

Anazingatia kuwa thamani ya mali aliyopewa kila mmoja wao ni sawa na wengine na kila mmoja amepewa kutokana na kipaji chake. Hivyo aligawa mali yake kwa usawa lakini sio kwa kulingana. Uwingi ni tofauti na ubora, na usawa ni tofauti na kufanana. Uislamu hauamini juu ya kulingana (uniformity) kwa mwanaume na mwanamke. Lakini wakati huo huo hauwapendelei wanaume katika maswala ya haki. Umezingatia kanuni ya usawa kati ya mwanamke na mwanaume lakini haukubaliani na kufanana kwa haki zao. Usawa ni neno linalifurahisha, kwa sababu linaashiria hali ya kutobagua. Lina utukufu maalum. Linaamsha na kuleta heshima, hasa linapohusiana na haki. Ni neno zuri lilioje 'Usawa na Haki.' Mtu yeyote mwema atafurahishwa na uzuri wake. Lakini hatuwezi tukaelewa ni kwa jinsi gani mambo yalifika hatua hii kiasi cha kuwa wengine ambao walikuwa vinara wa sayansi na falsafa nao wanataka kuingiza mawazo yao juu ya kufanana kwa haki kati ya wanawake na wanaume huku kwetu.

Hii ni sawa na mtu kuuza viazi vitamu kwa jina la mapeasi. Hapana shaka kuwa Uislamu haujatoa haki zinazofanana kati ya mwanaume na mwanamke katika mambo yote. Lakini pia haujaamuru majukumu na adhabu zinazofanana kwa jinsia hizi mbili. Yote kwa yote ni kuwa thamani ya jumla ya haki za mwanamke sio ndogo kuliko ile ya mwanaume. Tunataka kuthibitisha nukta hii. Hapa linazuka swali, kwa nini haki za mwanaume na mwanamke hazijafanana katika mambo yote. Je isingekuwa vizuri zaidi kama haki zao zingekuwa zinafanana katika mambo yote? Ili kulijadili hili swali kikamilifu, tutajadili chini ya vichwa vya habari vitatu. Mtazamo wa Uislamu juu ya nafasi ya mwanamke kutokana na maumbile yake. Athari za tofauti za kimwili kati ya mwanaume na mwanamke. Je, hili linasababisha tofauti ya haki zao pia? Ni nini falsafa ya sheria za Kiislamu, ambazo wakati fulani zinatofautisha kati ya mwanaume na mwanamke? Je falsafa hii bado ni thabiti?

Nafasi ya mwanamke katika utaratibu wa Kiislamu.

Qur'ani sio mkusanyiko tu wa sheria. Sio chombo cha sheria na kanuni kavu bila maelezo ya madhumuni yake. Ina sheria na pia ina historia, mawaidha ya kidini, maelezo ya malengo ya maisha, na maelfu ya mambo mengine katika sehemu mbalimbali, Qur'ani huelezea mambo yenye sura ya kisheria na katika sehemu nyingine hueleza lengo la maisha. Hufunua siri za dunia, mbingu, mimea, wanyama na wanaadamu. Huelezea siri za maisha na kifo, heshima na aibu, kupanda na kushuka, mali na umaskini.

Qur'ani sio kitabu cha falsafa, lakini kimeelezea kwa ufasaha sana maoni yake (Qur'ani) juu ya falsafa ya masomo matatu ya msingi; Ulimwengu, mwanadamu na jamii. Haiwafundishi wafuasi wake sheria peke yake, na haijishughulishi na mawaidha na nasaha (maonyo) peke yake, bali kwa kupitia tafsiri yake ya maisha (maumbile), huwapa wafuasi wake mtazamo maalum na namna pekee ya kufikiri. Msingi wa kanuni za Kiislamu juu ya masuala ya kijamii kama vile umiliki, serikali, haki za kifamilia n.k ni tafsiri ya maisha na mambo mengine tofauti tofauti.

Moja ya mambo yaliyoelezwa katika Qur'ani ni kuumbwa kwa mwanaume na mwanamke. Qur'ani haijakaa kimya juu ya jambo hili. Haijaacha mwanya kwa wadukuzi wa kifalsafa kuibua falsafa yao juu ya kanuni za mwanaume na mwanamke. Uislamu umetoa maoni yake juu ya mwanamke. Ili kujua maoni ya Uislamu juu ya mwanamke, tutazame Qur'ani inachosema juu ya tabia yake ya ndani. Dini nyingine pia zimelizungumzia suala hili, lakini ni Qur'ani peke yake ambayo katika Aya kadhaa inaelezea wazi wazi kuwa mwanamke ameumbwa kutokana na spishi za mwanaume, na wote mwanamke na mwanaume wana tabia za ndani zinazofanana.

Akimzungumzia Adam, Mwenyezi Mungu anasema;"Yeye (Allah) aliwaumba nyinyi wote kutokana na nafsi moja, na kutokana nayo (hiyo nafsi moja) akamuumbia mwenza wake (Suratun-Nisaa 4:1). Na juu ya mwanadamu kwa ujumla, Qur'ani inasema; "Amewaumbieni wake zenu kutokana na nyinyi. ' (Suratul Nisaa, Suratul Aali Imran na Suratul Ruum). Tofauti na vitabu vingine vya kidini hakuna sehemu yoyote katika Qur'ani ambapo imetajwa kuwa mwanamke ameumbwa kwa kutumia vitu duni au kuwa ana asili ya ukupe au ni wa asili ya upande wa kushoto. Uislamu hauungi mkono dhana ya kibiblia kuwa mwanamke ameumbwa kutokana na ubavu wa kushoto wa Adam. Uislamu hauna mtazamo wa dharau juu ya asili ya mwanamke na tabia zake za ndani.

Kuna nadharia nyingine ya dharau kwa wanawake iliyokuwa imeenea sana siku za nyuma, na imeacha alama mbaya katika siku za nyuma, na imeacha alama mbaya katika fasihi ya dunia. Kwa mujibu wa nadharia hiyo mwanamke ndio chanzo cha madhambi yote. Kuwepo kwake tu kunahamasisha uovu. Mwanamke ni shetani mdogo. Inasemekana kuwa katika kila dhambi na uhalifu uliotendwa na mwanaume kuna mkono wa mwanamke. Wanaume wenyewe hawatendi madhambi, ni wanawake wanaowasukumia kwenye madhambi. Pia inasemekana kuwa shetani hawezi kumwendea mwanaume moja kwa moja. Ni kupitia mwanamke ndio huwapotosha wanaume.

Shetani humchochea mwanamke na mwanamke humchochea mwanaume. Adam aliondolewa peponi kwa sababu ya mwanamke. Shetani alimshawishi Hawa, na ni Hawa aliyemshawishi Adam. Qur'ani imesimulia kisa hiki cha peponi lakini hakuna iliposema kuwa shetani au nyoka alipompotosha Hawa na Hawa akampotosha Adam. Haimlaumu Hawa wala haimuondoi katika hatia. Qur'ani inasema;"Tulimwambia Adam, 'Kaa Peponi; wewe na mke wako, na kuleni humo matunda popote mpendapo lakini msiusogelee mti ule msije kuwa miongoni mwa madhalimu ." (Suratul Baqara, 2:35). Inaweka kiwakilishi cha watu wawili. Pia Qur'ani inasema; "Kisha Shetani aliwatia wasiwasi." "Naye akawaapia (kuwaambia) kwa hakika mimi ni mmoja wa watoao shauri njema kwenu . (Suratul Aaraf 7:20-21).

Hivyo Qur'ani inapinga vikali dhana ya uongo iliyokuwa imeenea sana wakati wa kuteremshwa Qur'ani na miwangwi ambayo bado inasikika katika sehemu mbali mbali za dunia hii leo. Ilimuondoa mwanamke katika mashitaka kwamba yeye ni mchochezi wa dhambi na kwamba yeye ni shetani mdogo. Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ambayo imekuwepo ni juu ya nafasi ya kiroho ya mwanamke.

Ilidaiwa kuwa mwanamke hawezi kuingia peponi. Hana uwezo wa kiroho na msaada wa Mungu kumuwezesha kufanya hivyo. Hana uwezo wa kufikia ukaribu wa Mwenyezi Mungu kama mwanaume anavyoweza kufanya. Lakini Qur'ani katika Aya mbali mbali imesema wazi wazi kuwa malipo ya pepo na ukaribu na Mwenyezi Mungu havitegemei jinsia ya mtu.

Inategemea na imani na amali (vitendo), na hakuna tofauti kati ya mwanamke na mwanaume juu ya hili katika Qur'ani, wametajwa watakatifu wa kiume na watakatifu wa kike. Qur'ani imewatukuza wake wa Adam na Ibrahim na mama yake Nabii Isa na Musa. Imewataja wake wa Nuhu na Lut kuwa hawakuwa stahili ya waume zao na haijamshahau mke wa Firauni ambaye ametajwa kuwa ni mwanamke mtukufu aliyekuwa mikononi mwa mwanaume muovu. Katika visa vyake Qur'ani imeweka mizania. Mashujaa wake ni wa kiume na wa kike. Wakati, ikimzungumzia mama yake Nabii Musa, Qur'ani inasema, "Tulimjulisha mama yake Musa kwa kumwambia;'Muweke katika sanduku na mtupe katika mto. Mawimbi yatamfikisha ufukweni . (Suratul Taha; 20:39). Juu ya mama yake Issa, Qur'ani inasema kuwa alifikia daraja tukufu ya kiroho kiasi kwamba malaika walikuwa wakiongea naye wakati anasali. Alikuwa akipokea chakula kutoka peponoi. Daraja la kiroho lilimshangaza hata Zakaria, Mtume wa wakati huo.

Kumekuwa na mifano mingi ya wanawake mashuhuri na watakatifu katika historia ya Uislamu. Ni wanaume wachache tu wanaweza kufikia daraja la Khadija, mke kipenzi wa Mtume(s.a.w.w) na hakuna mwanaume anayefikia daraja la bibi Fatima Zahra, binti kipenzi wa Mtume isipokuwa Mtume mwenyewe na Imam Ali(a.s) . Ana daraja kubwa kuliko hata la watoto wake ambao ni Maimamu, na hata la Mitume wote isipokuwa Mtume wa mwisho.

Uislamu hauwabagui wanawake dhidi ya wanaume katika 'safari ya kumuendea Allah' isipokuwa humuona mwanaume kuwa mwenye kufaa zaidi kuchukua jukumu la utume, ambalo yaweza kuelezewa kama safari ya kurudi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwenda kwa watu. Nadharia nyingine ya dharau kwa wanawake inahusiana na kujihini na kutooa/kutoolewa. Baadhi ya dini zinaona kuwa tendo la ndoa ni kitu kichafu, kwa mujibu wa imani ya wafuasi wake, wanaoweza kufikia kilele cha juu cha daraja la kiroho ni wale tu ambao watamaliza maisha yao yote bila kuoa/kuolewa. Kiongozi mmoja wa dunia wa kidini anasema, "Kateni mti wa ndoa kwa shoka ya ubikira.' Viongozi hawa wa kidini wanavumilia ndoa tu kama uovu wenye nafuu.

Kwa maneno mengine wanashikilia kuwa kwa kuwa watu wengi hawawezi maisha ya bila kuoa/kuolewa na inaeleweka kwamba hawataweza kujidhibiti na hivyo kujiingiza katika zinaa za wanawake/wanaume wengi, basi ni bora waoe ili wasije kukutana na mwanamke zaidi ya mmoja. Watu hawa wanatetea kukaa bila kuoa au kuolewa na kujihini kwa sababu wanaona tendo la ndoa si kitu kizuri. Wanaona upendo kwa mwanamke kuwa ni uovu mkubwa wa kimaadili.

Uislamu unapinga vikali upuuzi huu. Unaiona ndoa kuwa ni taasisi tukufu na kukaa bila kuoa/kuolewa kuwa ni uchafu. Kumpenda mwanamke ni sehemu ya tabia ya Mtume. Mtukutu Mtume amesema; "Napenda vitu vitatu, manukato, mwanamke na swala." Bertrand Russel anasema, "Dini zote, isipokuwa Uislamu, zinalitazama tendo la ndoa kwa jicho baya. Uislamu unalitazama kwa maslahi ya kijamii, umeliwekea utaratibu maalum na kulidhibiti, lakini haulitazami kama uchafu." Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa mwanamke ameumbwa kwa maslahi ya mwanaume. Uislamu hausemi hivyo. Umeeleza malengo ya maisha kwa uwazi kabisa. Imeeleza kuwa dunia, mbingu, hewa, mawingu, mimea na wanyama vyote vimeumbwa kwa ajili ya mwanadamu. Haijasema mwanamke ameumbwa kwa ajili ya mwanaume. Kwa mujibu wa Qur'ani mwanaume ameumbwa kwa ajili ya mwanamke na mwanamke ameumbwa kwa ajili ya mwanaume.

'Wao (wanawake) ni nguo zenu na nyinyi (wanaume) ni nguo zao (2:187). Ingekuwa Qur'ani imeeleza kuwa mwanamke ni nyongeza (kiambatanisho) ya mwanaume na aliumbwa kwa ajili ya starehe yake (mwanaume) mtazamo huu ungekuwa umetazamwa katika sheria za Kiislamu, lakini Qur'ani haijasema hivyo. Hauyaelezei malengo ya maisha hivi. Haumuoni mwanamke kuwa ni kiambatanisho tu cha mwanaume. Ndio maana mtazamo huu haujazingatiwa katika sheria za Kiislamu. Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa mwanamke ni uovu usioepukika. Katika siku za nyuma, watu walimtazama mwanamke kwa dharau sana na walimuona kuwa ni chanzo cha mikosi na aina zote za matatizo.

Kinyume chake Qur'ani imesisitiza kuwa mwanamke ni baraka kwa mwanaume na ni chanzo cha raha na faraja kwake. Kwa mujibu wa nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa hawakuthamini mchango wa mwanamke katika uzazi. Waarabu wa kabla ya Uislamu na baadhi ya jamii nyingine waliomuona mwanamke kama mfuko tu wa kukuzia mbegu ya mwanaume.

Sehemu mbali mbali ya Qur'ani imesema:'Tumewaumba kutokanana na mwanaume na mwanamke. ' Wazo hili limeelezwa katika Aya nyingine za Qur'ani. Hivyo Uislamu ulikomesha fikra hiyo kuwa mwanamke ni mfuko tu wa kukuzia mbegu ya mwanaume. Ni dhahiri sasa kuwa Uislamu hauna kabisa mitazamo yoyote ya kumdharau mwanamke. Sasa muda umefika wa kueleza kwa nini haki za mwanaume na mwanamke hazifanani. Ni kufanana, hapana, Ni kulingana, sawa.

Tayari tumeshasema kuwa katika suala la mahusiano ya kifamilia na haki za mwanamke na mwanaume, Uislamu una falsafa yake ambayo ni tofauti kabisa na ile iliyokuwa ada (kawaida), miaka 1400 iliyopita na ilivyo sasa. Pia tumesema kuwa hakuna ubishi wowote kuwa mwanaume na mwanamke ni sawa kama binadamu na haki zao za kifamilia zinapaswa kuwa sawa kithamani. Kwa mtazamo wa Uislamu wao wote ni binadamu na hivyo wana haki sawa. Nukta inayopaswa kuangaliwa hapa ni kuwa mwanaume na mwanamke, kwa sababu ya tofauti zao za kijinsia, wanatofautiana katika mambo mengi. Asili yao haitaki wafanane.

Nafasi hii inataka wasifanane katika haki nyingi, majukumu, wajibu na adhabu. Katika nchi za Magharibi jitihada inafanyika sasa kuzifanya haki na majukumu yao kufanana, na kupuuza tofauti zao za asili na za ndani. Hapa ndio kuna tofauti kati ya mtazamo wa Kiislamu na mfumo wa Kimagharibi katika nchi yetu, nukta inayobishaniwa ni suala la kufanana kwa haki sio usawa wa haki kati ya mwanamke na mwanaume. Usawa wa haki ni nembo tu ambayo imewekwa kwa makosa katika zawadi hii ya Kimagharibi.

Mwandishi wa kitabu hiki katika vitabu na hotuba zake mara zote amejiepusha kutumia nembo hii ya uongo na kamwe hajakubali kulipa jina la usawa jambo ambalo kiuhalisia ni kufanana kwa haki. Ulaya ya kabla ya karne ya 20 ni mfano dhahiri wa dhulma kwa mwanamke. Mpaka mwanzoni mwa karne ya 20 mwanamke wa Ulaya alinyimwa haki za kibinadamu katika maisha ya kila siku na kisheria. Hakuwa na haki sawa wala zinazofanana na mwanaume.

Ni katika muongo uliopita ambapo kutokana na harakati za pupa, wameanza kumpa haki zake za msingi, lakini bado hajaweza kupata haki zinazochukuana na maumbile yake na mahitaji yake kimwili na kiroho. Kama mwanamke anataka haki na usawa na furaha katika familia lazima alitupilie mbali wazo la kufanana kwa haki. Hiyo ndio njia pekee ya kuimarisha uchangamfu kati ya mwanaume na mwanamke.

Katika hali hiyo, sio tu kwamba mwanaume atazikubali haki za mwanamke, lakini pia atakuwa tayari kumpatia, na katika baadhi ya mambo atatoa haki nyingi zaidi tena bila kumdanganya. Halikadhalika hatudai kuwa katika jamii ya Kiislamu mwanamke anapata haki sawa na mwanaume. Mara nyingi tumesema kuwa ni muhimu kwamba nafasi ya mwanamke iangaliwe upya na apewe haki lukuki ambazo Uislamu umempatia, na ambazo amekuwa akinyimwa katika kipindi chote cha historia. Hata hivyo, haifai kuiga staili na mifumo ya Kimagharibi kibubusa, mifumo ambayo imesababisha madhara makubwa huko Magharibi kwenyewe.

Tunachodai ni kuwa kutofanana kwa haki kati ya mwanaume na mwanamke, kwa mujibu wa mipaka ya maumbile na tofauti zao ndio kutenda haki zaidi. Hukidhi mahitaji ya haki za asili vizuri zaidi, hutoa hakikisho kwa furaha ya familia na huisukuma jamii mbele katika njia ya maendeleo bora zaidi. Inaweza kukumbukwa kuwa tunadai kuwa haki ya asili inataka kwamba, katika baadhi ya mambo, kuwe na kutokufanana kwa haki ya mwanaume na mwanamke.

Kwa vile linahusiana na falfsafa ya haki, suala hili lina sura ya kifalsafa asilimia mia moja. Linahusiana pia na kanuni ya haki na usawa, kanuni kuu za sheria ya Kiislamu na falsafa ya uanazuoni wa Kiislamu. Ni kanuni ya usawa iliyoleta mafundisho ya kukubaliana kati ya akili na sheria ya Mwenyezi Mungu. Kwa mujibu wa elimu ya sheria ya Kiislamu au tuseme ya Kishia, kama ikithibitika kuwa usawa unataka kuwa katika hali fulani, basi sura hiyo ndiyo itachukua sura ya kisheria bila kujali hoja zozote nyingine dhidi yake, kwani kwa mujibu wa mafundisho ya msingi ya Uislamu, sheria lazima katika hali yoyote isivunje au kuhalifu uadilifu wa asili na haki na za msingi.

Wanazuoni wa Kiislamu kwa kufafanua kanuni za usawa waliweka msingi wa falsafa ya haki, ingawa kufuatia matukio fulani ya kihistoria yasiyofurahisha, hawakuweza kuiendeleza kazi nzuri waliyoianza. Walikuwa ni Waislamu ambao, kwa mara ya kwanza walilitupia macho suala la haki za kibinadamu na kanuni za usawa, na walizitoa katika haki yake ya asili na kama kanuni zinazojitegemea bila kuathiriwa na sheria za kimikataba. Waislamu walikuwa vinara katika fani ya haki za asili za binadamu. Lakini hawakujaaliwa kuiendeleza kazi yao na hatimaye, baada ya karne nane, iliendelezwa na wasomi na wanafalsafa wa kizungu na wakajichukulia sifa hiyo.

Wazungu walileta falsafa za kijamii, kisiasa na kiuchumi na walijulisha watu, jamii na mataifa juu ya thamani ya maisha na haki za binadamu. Kwa maoni yetu mbali na sababu za kihistoria kulikuwa na sababu za kisaikolojia na kimkoa pia, ambazo ziliwazuia Waislamu wa Mashariki (Asia) kuendeleza suala la haki za msingi za binadamu.

Ni moja ya tofauti kati ya hulka ya nchi za Mashariki (Asia) na zile za Magharibi. Nchi za Mashariki zinazingatia maadili na za Magharibi zinazingatia haki. Mtu wa Mashariki ana upendo zaidi na anaamini kuwa lazima asamehe awe na moyo wa ubinadamu. Lakini mtu wa Magharibi anaamini kuwa kama binadamu lazima azijue na kuzilinda haki zake na lazima asiruhusu wengine wazipore. Utu unahitaji maadili na haki pia. Utu unahusiana na haki na maadili. Moja tu katika hizi haitoshi kuwa kigezo cha sifa bora za binadamu. Uislamu ulikuwa na hadi sasa unazingatia yote mawili haki na maadili.

Katika Uislamu, dhati, kusamehe, na matendo mema ni sifa takatifu na za kibinadamu. Lakini wakati huo huo mtu kujua haki zake na kuwa tayari kuzitetea, ni jambo takatifu na la kibinadamu. Hata hivyo, nchi za Mashariki kwa kiasi kikubwa zimekaliwa na Waislamu, na kwa hiyo, japokuwa awali yote yalikuwa yakizingatiwa maadili na haki lakini pole pole walijikuta wanabaki kushikilia maadili peke yake. Hivi sasa tunashughulikia suala la haki ambalo pia linaweza kuwa suala la kifalsafa na linafaa kujadiliwa kwa kirefu.

Inahusiana sana na maana halisi ya haki na ukweli halisi wa haki uadilifu na sheria uliokuwepo hata kabla ya kuwepo kwa sheria duniani, na ambao maana zake haziwezi kubadilishwa na sheria yoyote.

Montesquieu anasema, "Kabla ya sheria kutungwa na watu, kulikuwepo mahusiano yenye uadilifu baina ya watu kwa msingi wa sheria ambazo zilitawala mahusiano baina ya vitu vyote vilivyokuwepo. Ni kuwepo kwa mahusiano haya kulikosababisha kuundwa kwa sheria hizi. Kusema kwamba kabla ya watu kutunga sheria hapakuwa na uadilifu au dhuluma katika kuyaongoza na kuyadhibiti mahusiano ya watu ni sawa na kusema kuwa kabla ya mduara kuchorwa, nusu vipenyo vyake havilingani." Herbert Spencer anasema; "uadilifu unachaganganyika na kitu fulani mbali na hisia; yaani haki za msingi za binadamu. Lazima tuheshimu haki za binadamu ili uadilifu uwepo kiuhalisia." Wengi wa wasomi wa Ulaya wana mtazamo kuwa maazimio yote ya haki za binadamu yamechukuliwa kutoka katika haki za msingi za binadamu. Kwa maneno mengine, haki za msingi za binadamu zimechukuwa sura ya maazimio ya haki.

Kama tunavyojua, Montesquieu, Spencer n.k. wamesema kitu kimoja, juu ya uadilifu kama walichosema wanafalsafa wasomi wa Kiislamu juu ya msingi wa razini wa wema na uovu na kanuni ya usawa. Miongoni mwa Waislamu wamekuwepo wasomi ambao wamekana kuwepo kwa haki za asili na wanashikilia kuwa uadilifu ni jambo la kimkataba.

Halikadhalika, imani hii imekuwepo miongoni mwa wazungu. Mwanafalsafa wa Kiingereza, Thomas Hobbes alikana kabisa na akadai kuwa uadilifu sio kitu halisi. Azimio la haki za binadamu ni falsafa sio sheria. Ni kejeli kusema kuwa Azimio la Dunia la haki za binadamu ambalo linatoa hakikisho la usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke, imeidhinishwa na Bunge la nchi fulani, wanaume na wanawake wa nchi hiyo wanapaswa kuwa na haki sawa.

Hata hivyo, si jambo lililo katika mamlaka ya kisheria kwa Bunge la nchi yoyote kuidhinisha au kukataa Azimio kwa vile yaliyomo humo kwenye Azimio, hayana sura ya kimkataba, hivyo hayaangukii kwenye mamlaka yake ya kisheria. Azimio la Dunia hushughulikia haki za asili, zisizoondosheka na zisizobatilishika za binadamu na kama inavyodaiwa na Azimio lenyewe, haki hizi ni sehemu muhimu na ya lazima ya heshima ya mwanadamu na zimebuniwa na mamlaka yenye nguvu ya maumbile yenyewe.

Kwa maneno mengine, haki hizi zimetolewa na kupewa wanaadamu na chanzo kile kile kilichowapa akili, utashi na heshima. Kama ni hivyo, hali ya mambo yaliyomo katika Azimio hili inalazimisha kuwa hakuna mamlaka yoyote ya binadamu inayoweza kuyabuni au kuyafuta. Sasa hapa linakujaje suala la kuidhinisha Azimio hilo katika chombo cha kutunga sheria? Kwa kusema kweli, Azimio la Haki za Binadamu ni falsafa sio sheria. Na kama ni hivyo inafaa kuidhinishwa na wanafalsafa na sio na watunga sheria (wabunge).

Hakuna Bunge ambalo linaweza kutunga falsafa kwa kulumbana na kupiga kura. Vinginevyo kwa nini, muswada unaoelezea nadharia ya Einstein juu ya 'relativity' (kwamba vipimo vya mwendo nafasi na wakati vinawiana) au nadharia nyingine inayosema kuwa kuna maisha katika karne nyingine haijapelekwa Bungeni ili ikaidhinishwe na chombo kitukufu? Kiuhalisia, sheria ya asili haiwezi kupitishwa au kukataliwa kama sheria ya kimkataba.

Kupitisha sheria ya asili (maumbile) ni sawa na kupitisha sheria kuwa kupandikiza chipukizi la mpeasi kwenye muepo (tufaa) kutafanikiwa lakini kupandikiza mpeasi kwenye mforosadi (mulberry) hakutafanikiwa. Kila azimio lolote linapotolewa na kikundi cha wanafalsafa, kila taifa hupeleka kwa wanafalsafa wake, na kama watalipitisha basi ndio wananchi wote wa nchi hiyo wanapaswa kuzingatia maelekezo yake kama ukweli wa ziada wa kisheria. Mamlaka ya kisheria itapaswa kutopitisha sheria inayopingana na maelekezo hayo.

Lakini mataifa mengine hayatalazimika kuyazingatia maazimio haya maadamu hayajathibitishwa, kwa mujibu wa maoni yao, kuwa haki hizo zipo duniani. Na zaidi ya haya, kwa vile suala hili haliwezi kupimwa au kujaribiwa, halihitaji vifaa au maabara n.k Ni suala la kifalsafa ambalo vifaa vyake ni ubongo, akili na nguvu ya hoja. Hata kama mataifa mengine yatalazimika kuwafuata walio wengi katika suala la mantiki na falsafa na wanahisi kuwa hawana uwezo wa kutosha wa kufikiri kifalsafa wao wenyewe, sisi Waislamu hatuwezi kufuata mfano wao.

Tumeonyesha huko nyuma kuwa tuna uwezo mkubwa wa kushughulikia masuala ya mantiki na kifalsafa. Kwanini tuwafuate wengine leo? Inashangaza kwamba wakati wasomi wa Kiislamu walitilia uzito sana kanuni ya uadilifu na haki za msingi za binadamu na wanazikubali kama sheria ya dini, bila kusita wala ubishi wowote, yote haya yakakubaliwa na akili (kuwa ni haki), leo mambo yameharibika kiasi cha kuwa tunataka wabunge waidhinishe kutambuliwa kwa haki za binadamu. Falsafa haiwezi kuthibitishwa kwa kujaza kuponi.

Ni kejeli na dhihaka kubwa kuliko hata hiyo iliyotangulia, kujaribu kuamua suala la haki za binadamu kwa kuandaa kura za maoni kwa wavulana wadogo na wasichana wadogo. Je ni akili kweli kuchapisha kuponi na kuwaambia wavulana na wasichana wadogo waijaze ili kujua asili ya haki za binadamu na kama ni za aina moja au mbili. Hata hivyo, hapa tunataka kulijadili suala la haki za mwanamke kwa utaratibu mzuri na kifalsafa, na kwa kuzingatia haki za msingi za binadamu.

Tungependa kujua kama kanuni zinazotaka wanadamu wote wapate na kufaidi haki zao za msingi walizopewa na Mwenyezi Mungu, zinalazimisha au hazilazimishi kuwa mwanaume na mwanamke wawe na nafasi moja sawa katika haki zao. Tunawaomba wasomi, wanafalsafa na wanasheria wa nchi yetu, ambao wanaweza kuwa ni watu pekee wenye mamlaka ya kutoa maoni juu ya suala hilo na kuziangalia hoja zetu kwa jicho la umakinifu.

Tutawashukuru sana kama watatoa maoni yao ya kimamlaka kukubaliana na hoja zetu au kuzipinga. Katika kulijadili suala hili, ni muhimu kwanza kujadili msingi wa haki za binadamu. Haki za mwanaume na mwanamke zitajadiliwa baadaye. Katika muktadha huu, haitakuwa makosa kuzungumzia kidogo harakati za kutaka mabadiliko katika karne chache zilizopita, ambazo zimeleta wazo la usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke.

Tazamo fupi la historia ya haki za wanawake Ulaya. Mazungumzo ya haki za binadamu yalianza karne ya 17. Waandishi na wanafalsafa wa karne ya 17 na 18, kwa uvumilivu mkubwa, waliyatangaza na kuyaeneza mawazo yao juu ya suala la haki za msingi na zisizobatilishika za binadamu. Jeans-Jacques Rouseau,Voltaire na Montesquieu ni miongoni mwa waandishi na wanafalsafa hawa. Matokeo ya kwanza ya kivitendo ya kuenea kwa mawazo yao yalikuwa ni mapambano ya muda mrefu kati ya watawala na raia wa Uingereza. Mwaka 1688 Waingereza walifanikiwa kumshawishi mfalme akubali kuwapa baadhi ya haki za kisiasa na jamii walizokuwa wameziandika katika hati iliyojulikana kama 'The Bill of Rights.' Matokeo mengine muhimu ya kuenea kwa mawazo haya yalikuwa ni Vita vya Uhuru vya Wamarekani dhidi ya Uingereza.

Makoloni kumi na tatu ya Uingereza huko Amerika ya kaskazini yaliasi, kufuatia kuwekewa kodi kubwa sana, na hatimaye walipata uhuru wao. Mwaka 1776 mkutano ulifanyika Philadelphia, mkutano ambao ulitoa Azimio la Uhuru. Dibaji yake inasema; "Tunauchukulia ukweli huu kuwa dhahiri kwamba watu wote wameumbwa wakiwa sawa na kwamba wamepewa na muumba wao haki fulani zisizoondosheka, na kwamba miongoni mwa hizo ni haki ya kuishi, uhuru na kupata furaha au kufurahia.

Ili kuhakikisha kupatikana kwa haki hizi, serikali zinawekwa na watu, zinapata madaraka yao kutokana na idhini ya watawaliwa; na kwamba wakati wowote serikali ya muundo wowote inapokiuka malengo haya, ni haki ya watu kuibadilisha au kuiondoa, na kuweka serikali mpya, ikijengwa chini ya msingi wa kanuni hizi na kupata madaraka yake kwa utaratibu huu, itawahakikishia wananchi usalama na furaha yao.

Na lile linaloitwa Azimio la Haki za Binadamu lilitolewa baada ya Mapinduzi ya Ufaransa, lina kanuni fulani za jumla zinazoonekana kuwa sehemu muhimu na ya lazima ya katiba ya Ufaransa. Azimio lina dibaji na ibara 17. Ibara ya kwanza inasema kuwa watu wote huzaliwa wakiwa huru na hubaki huru katika maisha yao yote. Haki zao zinafanana. Katika karne ya 19 mawazo mapya yalitokeza katika uwanja wa haki za binadamu kiuchumi, kijamii na kisiasa. Haya yalisababisha kuibuka kwa ujamaa, ushiriki wa wafanyakazi katika faida na kuiondoa serikali kutoka mikononi mwa mabepari kwenda mikoni mwa wavuja jasho (wafanyakazi).

Hadi mwanzoni mwa karne ya 20, majadiliano yote yalikuwa yamejikita juu ya haki ya watu dhidi ya serikali au haki za tabaka la wavuja jasho dhidi ya waajiri na makabaila. Katika karne ya 20, suala la haki za mwanamke dhidi ya haki za manaume liliibuka. Ni juzi tu katika karne ya 20 ambapo Uingereza iliyokuwa ikijulikana kama demokrasia kongwe, ilipotambua usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke. Ingawa Marekani kiujumla ilikuwa imezitambua haki za binadamu katika karne ya 18 katika Hati ya Azimio la uhuru, lakini bado haki ya kupiga kura kwa wote ilitolewa mwaka 1920.

Ufaransa pia ilitoa haki ya wanawake kupiga kura katika karne ya 20. Kwa kiasi fulani, katika karne ya 20 sehemu kubwa ya watu duniani walijitokeza kuunga mkono mabadiliko makubwa katika mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke, katika nyanja za haki na majukumu. Kwa mujibu wao lengo la uadilifu wa kijamii halingeweza kufikiwa kwa kufanya mabadiliko baina ya mataifa na kati ya wafanyakazi na waajiri na mabepari bila pia kuleta mabadiliko katika mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke.

Hii ndio maana dibaji ya Azimio la Haki za Binadamu kwa wote, lililotolewa mwaka 1948 linasema kwamba "Ambapo heshima ya utu wa mtu mmoja mmoja na usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke" Machafuko yaliyosababishwa na maendeleo ya kuboreka kwa mashine (mitambo) katika karne ya 19 na 20, na hali mbaya ya wafanyakazi iliyofuatia, hasa kwa wafanyakazi wa kike, yalisababisha macho yaelekezwe kwenye masaibu ya mwanamke na ndio maana suala la haki zao lilizingatiwa sana.

Mwanahistoria anasema, "Kwa vile serikali ilikuwa haijali, masaibu ya wafanyakazi na tabia ya waajiri wao, mabepari walifanya walivyopenda". Wamiliki wa viwanda walikuwa wakiwaajiri wanawake na watoto kwa ujira mdogo sana, na kwa vile masaa ya kufanya kazi yalikuwa mengi mno, wengi wao waliugua magonjwa mbali mbali na wengine walikufa katika umri mdogo." Hii ilikuwa ni historia fupi ya harakati za Haki za Binadamu Ulaya.

Kama tunavyojua, ibara zote za Azimio la Haki za Binadamu ambazo ni mpya kwa wazungu, zilishawekwa na Uislamu katika karne 14 zilizopita, na baadhi ya wasomi wa Kiarabu na Kiirani katika vitabu vyao wamefanya ulinganisho kati ya mafundisho ya Uislamu na maelekezo (masharti) ya ibara hizi. Bado kuna tofauti katika baadhi ya vipengele vya maazimio haya na mafundisho ya Uislamu. Hili ni somo la kuvutia. Kwa mfano Uislamu unakubali usawa kati ya haki ya mwanaume na mwanamke, lakini haukiubali kufanana kwa haki hizi. Heshima ya mwanadamu na haki za binadamu. Ambapo kuitambua heshima na utu wa mwanadamu na haki zisizoondosheka za wanaadamu wote ni msingi wa uhuru, haki na amani duniani."

"Ambapo kutozingatia na kudharau haki za kibinadamu kumesababisha vitendo vya kishenzi na kuikasirisha dhamira njema ya mwanadamu na kuja kwa ulimwengu ambao ndani yake watu watafurahia uhuru wa kujieleza na imani, na uhuru wa kuondokana na hofu na shida imetamkwa kuwa ni hamu kubwa ya watu wa kawaida." "Ambapo italazimu, ikiwa mwanadamu hana kimbilio, kama njia ya mwisho, ana haki ya kuasi utawala wa kidhalimu, na kwamba haki za binadamu zitapaswa kulindwa na utawala wa kisheria." "Itakapobidi, kukuza maendeleo ya uhusiano wa kirafiki kati ya mataifa." "Ambapo watu wa Umoja wa Mataifa, katika heshima ya utu wa mwanadamu na katika usawa wa haki za mwanaume na wanawake, na wamedhamiria kukuza maendeleo ya kijamii na kiwango cha ubora wa maisha, katika hali ya uhuru zaidi." "Ambapo Baraza kuu la umoja wa Mataifa linatamka Azimio hili la Haki za Binadamu kwa wote kama kigezo cha wote cha kupimia mafanikio ya watu wote na mataifa yote ili hadi kufika mwisho kila mtu na chombo cha jamii, kwa kulizingatia Azimio akilini mwao walijitahidi kwa kufundisha na kutoa elimu, kukuza tabia ya kuheshimu haki hizi na uhuru na kwa hatua za kimaendeleo za kitaifa na kimataifa, ili kulinda utambulisho na zingatio miongoni mwa nchi wanachama wenyewe na miongoni mwa watu wa nchi zilizo chini ya mamlaka yao ya kisheria" Kama tulivyoona mwanzo, kila neno na kila sentensi katika azimio hili limepigiwa hesabu kali, limechukuliwa kwa uangalifu mkubwa. Hili ni dhihirisho la maw azo ya wanafalsafa na wanasheria wataka mabadiliko wa karne nyingi. Nukta muhimu za dibaji ya Azimio la haki za binadamu.

Azimio hili lina ibara 30, japo baadhi ya ibara zimezidi kiasi na baadhi ya nukta zimerudiwa katika ibara nyingi. Nuktra muhimu za ibara ni kama ifuatavyo: Binadamu wote wana haki za msingi zisizobatilishika na haki ya kutambuliwa utu wao. Utu wa binadamu na haki za binadmau ni kwa ajili ya wote na hivi havigawiki. Vinawahusu watu wote bila kujali rangi, utaifa au jinsia. Binadamu wote ni wanafamilia, hivyo hakuna aliyebora kuliko mwingine. Kuzitambua kikamilifu haki za binadamu na utu wa binadamu ni msingi wa uhuru, haki na amani. Yaliyomo katika Azimio yanaashiria kuwa chanzo cha matatizo yote, vita, vitendo vya kishenzi vinavyofanywa na mtu mmoja mmoja na watu dhidi ya wengine ni kutozitambua haki za binadamu na utu wa binadamu.

Kutozitambua huku huwalazimisha baadhi kuasi dhidi ya wengine na hivyo kuhatarisha amani na usalama. Hitajio na kinachotamaniwa kikubwa zaidi katika kufanikisha azma hii ni kuzaliwa kwa dunia ambayo ndani yake kutakuwa hakikisho la uhuru wa imani, usalama na hali nzuri kimaisha pamoja na hakikisho la kuondokana na ukandamizaji, hofu na umasikini. Azimio lenye ibara 30 limeundwa ili kufikia lengo hili. Imani juu ya heshima kwa utu wa mwanadamu na haki za msingi za kibinadamu lazima ikaziwe na kuingizwa pole pole akilini mwa watu wote, kupitia ufundishaji na elimu.

Heshima kwa utu wa mwanadamu. Kwa vile Azimio la Haki za Binadamu limeundwa kwa msingi wa heshima kwa utu, uhuru na usawa kwa nia ya kufufua haki za binadamu, lazima liheshimiwe na kila mtu makini. Sisi watu wa Mashariki (Asia) tumekuwa tukiamini juu ya kuuheshimu utu wa binadamu kwa muda mrefu. Uislamu umetilia sana mkazo katika kuuheshimu utu pamoja na haki za binadamu, uhuru na usawa. Hao waliyoyahamasisha haya, wanastahiki shukrani zetu.

Hata hivyo, haya ni maandishi ya kifalsafa yaliyoandikwa na mikono ya kibinadamu, sio malaika. Hivyo kila mwanafalsafa anayo haki ya kuyachambua na kuonyesha nukta zake dhaifu. Hapana shaka kwamba Azimio la haki za Binadamu lina udhaifu wake, lakini hivi sasa hatuna nia ya kuonyesha udhaifu huo. Badala yake; tunaonyesha nukta zake nzuri.

Msingi wa Azimio hili ni heshima ya utu wa mwanadamu kwa sababu, kwa kuwa nazo hizo, mwanadamu anapata haki fulani ambazo viumbe wengine hawapati, kwa vile hawana utu huo. Hii ndio nukta nzuri ya Azimio hili. Falsafa ya Kimagharibi inamshusha hadhi mwanadamu. Hapa tena tulikutana na swali kongwe la kifalsafa; Ni nini asili ya utu wa mwanadamu ambao humtofautisha yeye na farasi, ng'ombe na njiwa? Hapa ndipo inapodhirika migongano kati ya msingi wa Azimio la Haki za Binadamu na tathhmini ya Kimagharibi juu ya mwanadamu. Falsafa ya Kimagharibi toka zamani imekuwa ikimshushia hadhi mwanadamu.

Chanzo cha yote ambayo yalikuwa yakisemwa zamani kuhusu mwanadamu na cheo chake kitukufu ilikuwa ni katika Mashariki (Asia). Sasa mifumo mingi ya falsafa ya Ulaya inayakejeli yote hayo. Mwanadamu kwa mtazamo wa Kimagharibi, amekuja (duniani) akiwa na cheo cha mashine. Kuwepo kwa roho na asili ya ukarimu kumekataliwa.

Wazo kwamba ulimwengu una lengo la msingi linaonekana kuwa ni wazo la kupinga maendeleo. Sasa hakuna mtu katika nchi za Magharibi anayeweza kusema kuwa mwanadamu ni mfalme wa viumbe. Kwa mujibu wa nadharia ya sasa ya kizungu, imani hiyo ilikuwa ni chipukizi (tawi) la unajimu wa Ptolem, ambayo ilikuwa inaaminika kuwa dunia ndio kitovu cha ulimwengu na nyota ziliaminika kuwa zinaizunguka dunia. Sasa kwa kuwa nadharia hii imeshakufa na kwa kutoweka kwake, hakuna nafasi tena ya mwanadamu kudai kuwa ni mfalme wa ulimwengu.

Kwa mujibu wa Wazungu, hata zamani ilikuwa ni kwa sababu ya ubinafsi wake ndio maana akajifanya kuwa bora kuliko viumbe wengine. Maisha yake ni ya kiumbo tu. Mtu akishakufa, mwili wake huoza na hapo ndio mwisho wa habari! Mzungu haamini kuwa roho inaweza kuishi peke yake. Kwa mtazamo huu, hajioni kuwa na tofauti yoyote kati yake na mimea na wanyama. Kwa hiyo anaona kuwa hakuna tofauti yoyote ile ya msingi kati ya asili ya vipawa vya kiakili na kiroho vya mwanadamu na sifa nyingine za maada kama vile joto, linalotoka kwenye makaa ya mawe.

Maisha kwa viumbe vyote, ikiwa ni pamoja na mwanadamu, yanamaanisha mapambano yasiyokwisha ya kuweza kuishi. Hii ndio kanuni ya msingi ya maisha. Mwanadamu mara zote amekuwa akipambana ili awe mshindi katika mapambano haya, na ili kuilinda nafasi (hadhi) yake amebuni kanuni za kimaadili kama vile uadilifu, wema, ushirikiano, uaminifu n.k. Kwa mujibu wa baadhi ya matapo yenye nguvu ya kifalsafa ya Kimagharibi mwanadamu ni mashine tu inayosukumwa na maslahi ya kiuchumi. Dini, maadili, falsafa, sayansi, fasihi na sanaa nyingine, vyote ni vikorombwezo tu. Miundo mbinu yake ni mfumo wa uzalishaji mali na ugawaji wa mali, na mambo haya ndiyo yanayotawala nyanja zote za maisha ya mwanadamu.

Sio hivyo tu, baadhi ya wanafalsafa wa Kimagharibi wana mtazamo kwamba vipengele vya kijinsia ndivyo vyenye ushawashi halisi wenye nguvu katika shughuli zote za mwanadamu. Maadili, falsafa, sayansi, dini na sanaa vyote hivyo ni miundo ilyobadilishwa na kurekebishwa ya jinsia. Hatuelewi ni jinsi gani tunaweza kuzungumzia utu wa mwanadamu na haki za msingi na ni jinsi gani tunaweza kuzifanya kuwa msingi wa matendo yetu yote, ikiwa tunakana kwamba maisha hayana lengo lolote la msingi, ikiwa tunafikiri kuwa mapambano ya kuweza kuishi na mapambano yatakayombakisha mwenye nguvu zaidi ndio sheria pekee zinazotawala maisha, ikiwa tunaamini kuwa mwanadamu ni mashine tu kama mashine nyingine (lakini) iliyopewa mikono ya binadamu, ikiwa tunashikilia kuwa hakuna roho na kwamba yote yanayozungumzwa juu ya roho ni kuzidisha chumvi kwa kiroho, ikiwa tunashikilia kuwa maslahi ya kiuchumi na ngono ndiyo yanayosukuma shughuli zote za mwanadamu, ikiwa tunajali kuwa wema na uovu ni dhana linganifu tu, ikiwa tuna maoni kuwa muongozo wa kimungu wa asili na wa kimaono ni upuuzi na ikiwa tutasema kuwa mwanadamu ni mtumwa wa matamanio yake na anaweza kunyenyekea kwa nguvu tu.

Maoni ya Kimagharibi juu ya mwanadamu yanapingana na utu wake na yameiporomosha hadhi yake katika kila pembe katika pembe ya sababu ya kuumbwa kwake, umbile lake, nia yake na dhamira yake. Baada ya kufanya yote haya, nchi za Magharibi zimetangaza Azimio la hali ya juu lenye busara kuhusu utu wa mwanadamu na cheo na haki za msingi zisizoondosheka na takatifu, na wametoa wito kwa kila mtu kulitekeleza hilo. Kabla ya kutoa Azimio hili la hali ya juu zuri na lenye busara, nchi za Magharibi kuhusu utakatifu na haki za asili za mwanadamu, wangeipitia upya tafsiri yao juu ya mwanadamu.

Tunakiri kuwa sio wanafalsafa wote wa Kimagharibi wana mtazamo huu. Wengi wao wanamtazama mwanadamu kama tunavyofanya sisi watu wa Mashariki (Asia). Tuna mtazamo ambao watu wengi wa Magharibi wanaung'ang'ania na ambao unawashawishi watu duniani kote. Azimio la Haki za Binadamu lilipaswa litolewe na wale ambao wanamuona mwanadamu kuwa ni zaidi ya roboti ambao wanafikiri kuwa malengo yake hayaishii kwenye silika za kibinadamu na kinyama na ambao wanaamini juu ya dhamira ya kibinadamu. Azimio la Haki za Binadamu lilipaswa litolewe na watu wa Mashariki ambao wanaamini kuwa mwanadamu ni khalifa wa Mwenyezi Mungu katika dunia. Qur'ani Tukufu inasema:

"Kwa hakika nitamuweka khalifa katika ardhi." (2:30) Ni wale tu wanaoamini kuwa mwanadamu ana lengo na makusudio ndio wanaoweza kuzungumzia juu ya haki za binadamu.

"Enyi watu, bila shaka lazima mjitahidi sana kwa ajili ya Mola wenu, kujitahidi kukubwa kabisa hadi mtakapokutana Naye." (84:6). Azimio la haki za binadamu linaifaa mifumo ile ambayo inaamini kuwa mwanadamu ana muelekeo wa asili wa kutenda mema;"Naapa kwa roho na kwa yule aliyeifanya kuwa timilifu na aliyeipa ujuzi (elimu) juu ya uovu na uchamungu." (91:7-8). Azimio la haki za Binadamu haliafikiani na njia za fikra za Kimagharibi.

Kufikiri kwao kunazifaa tu tabia za watu wa kimagharibi ambao huua hisia za kibinadamu, hucheza na tabia za wanaadamu, hujali fedha zaidi kuliko mtu, huabudu mashine (mitambo), huona mali kama Mungu na huwanyonya wanaadamu wengine. Ubepari umepata nguvu na mamlaka yasiyo na kikomo kiasi cha kuwa ikitokea kuwa milionea mmoja atamrithisha mbwa wake kipenzi mali zake, mbwa huyo ataheshimika kuliko watu, watu wengi tu watamtumikia mbwa huyo kama makatibu muhtasi na makarani na wataonyesha heshima ya hali ya juu kwa mbwa huyo.

Leo hii swali kubwa la kijamii kwa mujibu wa Qur'ani, ni je, mwanadamu amejisahau mwenyewe? Sio tu kwamba amejisahau yeye tu bali amemsahau hata Mungu wake pia. Akili zake zote amezielekeza kwenye maisha ya kidunia na mali na amepuuza kabisa kujifikiria na kujipima. Anafikiri kuwa amepoteza roho yake. Mawazo kama haya ni ya hatari sana na yanaweza kuondoa kabisa thamani ya utu na ubinadamu.

Ustaarabu wa sasa unaweza kuzalisha kila kitu chenye ubora wa juu kabisa, lakini hauwezi kumtengeneza mtu halisi. Gandhi anasema kuwa mzungu anastahili kuitwa bwana wa dunia. Anamiliki raslimali zote za kidunia na anafanya vitu ambavyo mataifa mengine wanaamini kuwa ni Mungu tu anayeweza kuyafanya.

Lakini ni kitu kimoja tu ambacho mzungu hawezi kukifanya nacho ni kujifikiria na kujipima. Hilo peke yake linatosha kuthibitisha kutokuwa na maana kwa kumeremeta kwa ustaarabu wa kisasa. Kama ustaarabu wa Kimagharibi umemtaabisha mzungu kwa ulevi na ngono basi ni kwa sababu ya kujisahau na kujipoteza badala ya kujitafuta. Uwezo wake wa kivitendo wa kuvumbua, kugundua na kuzalisha zana za kivita unatokana na kujikwepa nafsi yake na sio kwa sababu ya uwezo wake wa kipekee wa kujidhibiti. Kuogopa kwake upweke, ukimya wake na tamaa yake ya fedha kumemfanya asiweze kusikia sauti yake ya ndani.

Kushindwa kwake kujitawala ndio kichocheo chake cha kuuteka ulimwengu. Hii ndio sababu kila anakokwenda mzungu hueneza mitafaruku na ghasia. Kama mtu akipoteza nafsi yake mwenyewe, hakuna faida yoyote kuushinda ulimwengu. Wale ambao wamefundishwa na Injili kuwa wamisionari wa ukweli, upendo na amani, wanazunguka kutafuta dhahabu na watumwa. Badala ya kutafuta msamaha wa Mwenyezi Mungu na uadilifu katika ufalme wa Mungu, kama Injili inavyofundisha wanatumia dini yao kama kifutio cha madhambi zao (kwa kumfanya Yesu, Mtume mtukufu wa Mungu kuwa kafara ya dhambi kwa kila amuaminiye). Badala ya kufundisha na kuhubiri ujumbe wa Mungu, wanawadondoshea mabomu watu wasio na hatia. Hii ndio sababu, Azimio la Haki za Binadamu linakiukwa na nchi za Magharibi. Falsafa inayofuatwa na watu wa Magharibi katika maisha yao kivitendo inafanya kushindwa kwa Azimio hili kusiepukike.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُهُمْ وَلَا يَضُرُّهُمْ وَكَانَ الْكَافِرُ عَلَىٰ رَبِّهِ ظَهِيرًا ﴿٥٥﴾

55. Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu. Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا مُبَشِّرًا وَنَذِيرًا ﴿٥٦﴾

56. Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

قُلْ مَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِلَّا مَن شَاءَ أَن يَتَّخِذَ إِلَىٰ رَبِّهِ سَبِيلًا ﴿٥٧﴾

57. Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

وَتَوَكَّلْ عَلَى الْحَيِّ الَّذِي لَا يَمُوتُ وَسَبِّحْ بِحَمْدِهِ وَكَفَىٰ بِهِ بِذُنُوبِ عِبَادِهِ خَبِيرًا ﴿٥٨﴾

58. Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ الرَّحْمَـٰنُ فَاسْأَلْ بِهِ خَبِيرًا ﴿٥٩﴾

59. Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi. Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اسْجُدُوا لِلرَّحْمَـٰنِ قَالُوا وَمَا الرَّحْمَـٰنُ أَنَسْجُدُ لِمَا تَأْمُرُنَا وَزَادَهُمْ نُفُورًا ﴿٦٠﴾

60. Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe? Na huwazidishia chuki.

تَبَارَكَ الَّذِي جَعَلَ فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَجَعَلَ فِيهَا سِرَاجًا وَقَمَرًا مُّنِيرًا ﴿٦١﴾

61. Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ خِلْفَةً لِّمَنْ أَرَادَ أَن يَذَّكَّرَ أَوْ أَرَادَ شُكُورًا ﴿٦٢﴾

62. Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

KAFIRI NI MSADIZI WA MPINZANI WA MOLA WAKE

Aya 55 – 62

MAANA

Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 11 (10 18).

Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

Yaani anawasaidia watu wa batili dhidi ya haki. Kila mwenye kusaidia batili atakuwa amesaidia dhidi ya Mwenyezi Mungu na kuwa adui yake; hata kama atamsabihi na kumtukuza kwa ulimi wake. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) :“Mwenye kumsaidia dhalimu na huku anajua kuwa ni dhalimu basi amejitenga na Uislamu.”

Kadiri nitakavyotia shaka, lakini siwezi kutia shaka kuwa mwenye kumtegemea dhalimu ni kafiri; bali kafiri aliye mwadilifu ni bora kuliko yeye. Aya za Qur’an kuhusu hilo ni nyingi na ziko wazi. Ama Hadith za Mtume zimepituka kiwango cha mutawatir.

Ndio! Ni wajibu wetu kuamiliana naye muamala wa kiislamu kwa vile tu ametamka: Lailaha illallah Muhammadurrasulullah (Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.)

Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 15 (17:105).

Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

Mimi sina tamaa ya mali yenu wala siwauzii pepo. Ninalotaka ni kutengeneza tu. Anayetaka kufanya njia ya kumwendea Mola miongoni mwenu, basi malipo yake yako kwa Mungu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz.12 (11:88).

Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

Ewe Muhammad! Toa bishara na onyo ukimtegemea Mwenyezi Mungu kwa kuwa na ikhlasi naye katika kauli yako na vitendo vyako na ujitakashe na kumfanyia mfano na kila lile ambalo halifanani na utukufu na ukuu wake. Yeye anamjua zaidi aliyepotea njia, na atamhisabu na kumlipa.

Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi.

Makusudio ya kustawi ni kutawala. Lililo na nguvu ni kuwa makusudio ya siku ni mikupuo, kwa sababu hakuna siku kabla ya kupatikana ulimwengu na jua. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:54), Juz. 11 (103), na Juz. 12 (11:7).

Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

Habari yake, ni habari ya huko kuumbwa mbingu na ardhi, ambako kunafahamika kutokana na mfumo wa Aya. Hapa kuna maneno yaliyotan- gulizwa na ya kukadiriwa. Maana ni: Yeye ni Mwingi wa rehema, ulizia habari za kuumbwa mbingu na ardhi kwa yule ajuaye ambaye ni Mwenyezi Mungu.

Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: ‘Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe?’ Na huwazidishia chuki.

Nabii(s.a.w.w) akiwaambia washirikina: ‘Mwabuduni Mwingi wa rehema, wala msiabudu masanamu,’ wao husema kwa kujitia hamnazo, kwa madharau, ni nani huyo unayetuambia tumwabudu unayemuita Mwingi wa rehema? Unataka tukutii wewe na tuwaasi baba zetu katika yale waliyokuwa wakiyaabudu?’

Ujinga na upumbavu huu unatukumbusha ujinga wa vijana wetu wanapoambiwa swalini na mfunge, husema: “Bado kuna Swala katika karne hii ya ishirini? Jambo la kushangaza ni kuwa vijana hawa wanaimba uhuru wa bianadamu; kama kwamba uhuru ni uzandiki na utu ni kujitoa kwenye misimamo.

Hawajui kuwa aliye huru ni yule anayemwabudu Mwenyezi Mungu wala hamnyenyekei asiyekuwa yeye na kwamba utu ni dini ya Mwenyezi Mungu ambayo inakataza maovu na munkar.

Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

Makusudio ya buruji ni mashukio ya jua na mwezi. Tazama Juz.14 (15: 16). Makusudio ya taa hapa ni jua, kutokana na kuunganisha na mwezi. Mahali pengine Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ الشَّمْسَ ضِيَاءً وَالْقَمَرَ نُورًا ﴿٥﴾

“Yeye ndiye aliyefanya jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru.” Juz.11 (10:5).

Wengine wametofautisha baina ya nuru na mwanga. Kwamba mwanga unategemea sayari moja kwa moja; kama vile mwanga wa jua, unatoka kwenye jua moja kwa moja.

Nuru inategemea sayari kupitia sayari nyingine; kama vile nuru ya mwezi inavyotegmea jua. Wametoa dalili wanaotofautisha, kwa Aya hiyo ya Juz. 11 (10:5) tuliyoitaja punde.

Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

Usiku unaondoka kisha unakuja mchana, nao unaondoka kisha unarudi usiku na kuendelea; wala hakuna unaobakia muda mrefu kuzidi kiasi cha haja ya viumbe.

Kufuatana kwa namna hii kunafahamisha kuweko mpangiliaji mwenye hekima. Kufuatana huku kunategemea harakati za ardhi, nazo zinategemea msababishaji wake wa kwanza.

Ama hekima ya mfuatano huu, ni kwamba lau lingelibakia giza tu, au mwangaza tu, maisha yangelikuwa magumu hapa ardhini.

Kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) ‘Kwa anayetaka kukumbuka,’ maana yake ni kuwa mwenye kutaka dalili ya kuweko Mwenyezi Mungu ataipata katika vitu vyote, vikiwemo kufuatana usiku na mchana.

Na kauli yake ‘Au anayetaka kushukuru,’ ni kuwa anayetaka kumshukuru Mweneyzi Mungu kwa neema yake naashukuru vile vile kwa kufuatana usiku na mchana, kwa sababu hilo ni katika neema kubwa.

وَعِبَادُ الرَّحْمَـٰنِ الَّذِينَ يَمْشُونَ عَلَى الْأَرْضِ هَوْنًا وَإِذَا خَاطَبَهُمُ الْجَاهِلُونَ قَالُوا سَلَامًا ﴿٦٣﴾

63. Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu. Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

وَالَّذِينَ يَبِيتُونَ لِرَبِّهِمْ سُجَّدًا وَقِيَامًا ﴿٦٤﴾

64. Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا اصْرِفْ عَنَّا عَذَابَ جَهَنَّمَ إِنَّ عَذَابَهَا كَانَ غَرَامًا ﴿٦٥﴾

65. Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam,’ hakika adhabu yake ni yenye kuendelea.

إِنَّهَا سَاءَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٦٦﴾

66. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa.

وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴿٦٧﴾

67. Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo.

وَالَّذِينَ لَا يَدْعُونَ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ وَلَا يَقْتُلُونَ النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّـهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَا يَزْنُونَ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ يَلْقَ أَثَامًا ﴿٦٨﴾

68. Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki, wala hawazini. Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

يُضَاعَفْ لَهُ الْعَذَابُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَيَخْلُدْ فِيهِ مُهَانًا ﴿٦٩﴾

69. Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

إِلَّا مَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ عَمَلًا صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ يُبَدِّلُ اللَّـهُ سَيِّئَاتِهِمْ حَسَنَاتٍ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٧٠﴾

70. Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.

وَمَن تَابَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَإِنَّهُ يَتُوبُ إِلَى اللَّـهِ مَتَابًا ﴿٧١﴾

71. Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

وَالَّذِينَ لَا يَشْهَدُونَ الزُّورَ وَإِذَا مَرُّوا بِاللَّغْوِ مَرُّوا كِرَامًا ﴿٧٢﴾

72. Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

وَالَّذِينَ إِذَا ذُكِّرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ لَمْ يَخِرُّوا عَلَيْهَا صُمًّا وَعُمْيَانًا ﴿٧٣﴾

73. Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawajifanyi ni viziwi nazo na vipofu.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا هَبْ لَنَا مِنْ أَزْوَاجِنَا وَذُرِّيَّاتِنَا قُرَّةَ أَعْيُنٍ وَاجْعَلْنَا لِلْمُتَّقِينَ إِمَامًا ﴿٧٤﴾

74. Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wanetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

أُولَـٰئِكَ يُجْزَوْنَ الْغُرْفَةَ بِمَا صَبَرُوا وَيُلَقَّوْنَ فِيهَا تَحِيَّةً وَسَلَامًا ﴿٧٥﴾

75. Hao ndio watakolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam.

خَالِدِينَ فِيهَا حَسُنَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٧٦﴾

76. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

قُلْ مَا يَعْبَأُ بِكُمْ رَبِّي لَوْلَا دُعَاؤُكُمْ فَقَدْ كَذَّبْتُمْ فَسَوْفَ يَكُونُ لِزَامًا ﴿٧٧﴾

77. Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

WAJA WA MWINGI WA REHEMA

Aya 63 – 77

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja sifa za makafiri na kiaga chao, kama kawaida yake, anataja sifa za waumini na malipo aliyowaandalia. Zifuatazo ndizo sifa zao:

1.Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu.

Imam Jafar Sadiq(a.s) anasema katika tafsiri ya hilo:“Ni yule mtu anayetembea kwenye asili yake aliyoumbiwa, hajikalifishi wala hajifanyi.” Ndio, anayetembea kwenye umbile lake aliloumbiwa, tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wapambe na wafuasi wanaomfuta nyuma na wengine mbele wakiwa wamepanda farasi au pikipiki na kupiga ving’ora vinavyohanikiza watu kwa sauti zake vikitangaza kuja kwake ili aachiwe njia, kwa ajili ya kumheshimu na kumtukuza.

2.Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

Makusudio ya kusemeshwa na wajinga ni kama vile kejeli zao, shutuma zao au mijadala ya hawa na masilahi. Amani ni kinaya cha kuachana nao, kwa kuwadharau na kuchunga mtu heshima yake. Maana ni kuwa, muumini akisikia neno ovu, aachane nalo; kama kwamba hakulisikia au kama anayekusudiwa ni mwingine sio yeye. Huu ndio mwepuko mwema aliousema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَاهْجُرْهُمْ هَجْرًا جَمِيلًا ﴿١٠﴾

“Na uwaepuke mwepuko mwema.” (73:10).

Hakuna mwenye shaka kwamba kuachana na jambo ni pale ikiwa hakuna uwezo au nguvu za kulikabili. Vinginevyo itakuwa ni wajibu kulikabili. Hapana budi kuihusisha Aya na hilo.

3.Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

Waumini wanasimama usiku kwenye giza wakifanya ibada ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu hilo liko mbali na ria, wala hawaupitishi usiku mikahawani na kwenye mambo ya mchezo mchezo tu, huku wakifuja mali na kupanga njama dhidi ya waumini na wenye ikhlasi. Mfano wa Aya hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:

كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ ﴿١٧﴾

“Walikuwa wakilala kidogo usiku.” (51:17).

4.Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam, hakika adhabu yake ni yenye kuendelea. haikwepeki na ni yakudumu. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa,

Waliamini Pepo na Moto, kutokana na waliyoyashuhudia na kuyaona; ndio wakauhofia moto wakaitumai pepo. Imam Ali(a.s ) anasema: “Wao na Pepo ni kama walioiona wakiwa ndani yake wananeemeshwa. Na wao na moto ni kama waliouona wakiwa ndani yake wanaadhibiwa.”

5.Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo, hakuna kupitisha kiasi, Si ubakhili wala ubadhirifu.

Huu ndio mwenendo wa Uislamu, wastani katika kila kitu; hakuna ulahidi wala waungu wengi, udikteta wala ukiritimba na hakuna kutaifisha mali ya mtu wala ubepari. Tazama Juz. 15 (17:29) kifungu cha ‘Uislamu na nadharia ya maadili.’

6.Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Mwenye kufanya riya au akamtii kiumbe katika kumuasi Muumba, basi huyo ni kama aliyemwomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki.

Nafsi inayouliwa kwa haki na kwa uadilifu ni ile iliyoua nafsi nyingine bila ya haki, aliyezini akiwa kwenye ndoa, kurtadi dini au kuleta ufisadi katika ardhi.

Ufafanuzi wa hayo uko katika vitabu vya Fiqh.

Wala hawazini

Kwa sababu zinaa ni katika madhambi makubwa. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t). Akaiweka sawa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuua nafsi na akajaalia hukumu ya haya matatu ni kuuliwa kwa masharti yaliyotajwa kwenye vitabu vya fiqh.

Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

Hayo ni hayo ya shirk, kuua na kuzini. Na madhambi ni adhabu.

Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

Kuna adhabu gani kubwa na kufedheheka zaidi kuliko adhabu ya Jahannam? Si kwambii tena ikiwa itazidishwa pamoja na kudumu kusiko na mwisho.

Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

Mwenye kutubia dhambi ni kama asiyekuwa na dhambi, zaidi ya hayo, Mwenyezi Mungu atampa thawabu kwa kule kutubia kwake na atampa mema kulingana na maovu ya dhambi zake; kiasi ambacho toba itafuta maovu ya dhambi.

إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ ﴿١١٤﴾

“Hakika mema huondoa maovu.” Juz. 12 (11:114).

Haya ndiyo maana ya ‘Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema’ kwa sababu uovu, kwa ulivyo, haustahiki kuwa wema, wala wema, kwa ulivyo, haustahiki kuwa uovu’

Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

Baada ya kubainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya iliyotangulia kwamba mwenye kutubia atampa thawabu za mwenye kufanya mema, hapa anamsifu kuwa amerejea kwa Muumba wake kurejea kuzuri.

7.Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

Neno ‘hawawi’ limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu ‘laa yash-hadu- una’ kama ilivyotumika tafsiri hiyo katika Juz. 2 (2:185). Makusudio ya uzushi ni mambo ya batili na upuzi ni kila lisilo na kheri. Maana ni kuwa waumini hawahudhurii vikao vya ubatilifu wala hawavisaidii, sikwambii kuvifanya. Pia hawashiriki mazungumzo yasiyokuwa na kheri na wanapoyapitia hayo masiko yao huyaepuka; kama wanavyoziepusha ndimi zao kuayatamka; sawa na nyuki anavyopita haraka kwenye mzoga na harufu mbaya.

8.Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawaji- fanyi ni viziwi nazo na vipofu.

Mshairi huwa anasikiliza mashairi kwa umakini kabisa. Vile vile kila mwenye kuhusika na jambo akizungumziwa huwa anakuwa makini nalo sana anapolisikilza. Mtu unapomzungumzia jambo lililo mbali naye atakuepuka na hayo mazungumzo yako, hata kama ni ya uongofu na mwangaza.

Hapa ndipo inabainika siri ya muumini kuikubali Qur’an, na kafiri kuachana nayo. Mumin anakikubali Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa vile anakiamini na kutambua maana yake na makusudio yake. Anakikuta kwenye nafsi yake, itikadi yake, matendo yake mema na malipo aliyomuandalia Mola wake.

Kafiri anakipa mgongo Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa sababu anakipinga na hajui malengo yake na siri yake; wala hapati humo isipokuwa kushutumiwa na kukosolewa itikadi yake na sifa zake na pia makaripio ya ukafiri wake.

9.Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

Muovu huwa anatamaani watu wamfuate katika uovu wake, sio kwa kuwa amekinai kuwa yuko kwenye uongofu kutoka kwa Mola wake, hapana! Isipokuwa anataka kupunguza lawama na shutuma na kufunika kosa lake kwa kuwa wengi wakosefu. Lakini hataki mkewe na watoto wake wawe hivyo; kama vile mgonjwa asivyopenda watu wake wapatwe na ugonjwa alio nao.

Ama yule aliye mwema na mwenye takua ana yakini na dini yake na ana busara katika mambo yake. Kwa hivyo huwa anatamaani kwa dhati ya moyo kimsingi na kiitikadi kuwa watu wote wafuate njia yake na kwamba watoto wake wakimuiga yeye huwa anafurahi.

Kwa hiyo wenye ikhlasi humuomba Muumba wao wapate wa kuwaiga, sio kwa kuziba vitendo vyao kwa watu wala kutaka jaha duniani na kuchukua mali kwa kutumia haki za Mwenyezi Mungu; bali ni kwa kujipendekeza mbele ya Mwenyezi Mungu aliye peke yake.

Hao ndio watakaolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

Ghorofa ni kinaya cha makao ya juu. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha wasifu wa wenye takua na watiifu, sasa anataja malipo yao watakayoyapata kwake, ambayo ni kudumu katika raha, amani na neema pamoja na heshima.

Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja subira hapa kuashiria kuwa kila mwenye haki hana budi kupata taabu na udhia kutoka kwa wasio na haki na kwamba thawabu za Mwenyezi Mungu hatazipata ispokuwa mwenye kuwa na uvumilivu na subira na akaendelea kuwa na msimamo kadiri hali itakavyokuwa ngumu.

Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

Makusudio ya neno ‘duakum’ hapa ni kupewa mwito kutokana na maneno yanayovutia, lakini mlikadhibisha. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ ﴿٥٢﴾

“Basi watawaita nao hawatawaitikia.” Juz. 15 (18:52)

Kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapa mwito kwenye imani na utiifu kupitia kwa Mtume wake.

Maana ni kuwa nyinyi washirikina hamstahiki hata kutajwa pia lau si kuwa mliitwa kwenye imani na utiifu, ili kuweko na hoja siku ya hisabu na malipo, ikiwa hamtasikia na kuitikia mwito. Nanyi mmeupinga mwito na mkadhibishaji aliyetoa mwito huo, basi adhabu inawastahiki na ni lazima.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Sura Ya Ishirini Na Sita: Surat Shua’rau.

Twabrasiy amesema imeshuka Makka isipokuwa Aya 224 hadi mwisho, zimeshuka Madina. Ina Aya 227

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehma Mwenye kurehemu.

طسم ﴿١﴾

1. Twaa Siin Miim.

تِلْكَ آيَاتُ الْكِتَابِ الْمُبِينِ ﴿٢﴾

2. Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

لَعَلَّكَ بَاخِعٌ نَّفْسَكَ أَلَّا يَكُونُوا مُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

إِن نَّشَأْ نُنَزِّلْ عَلَيْهِم مِّنَ السَّمَاءِ آيَةً فَظَلَّتْ أَعْنَاقُهُمْ لَهَا خَاضِعِينَ ﴿٤﴾

4. Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

وَمَا يَأْتِيهِم مِّن ذِكْرٍ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ مُحْدَثٍ إِلَّا كَانُوا عَنْهُ مُعْرِضِينَ ﴿٥﴾

5. Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao.

فَقَدْ كَذَّبُوا فَسَيَأْتِيهِمْ أَنبَاءُ مَا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٦﴾

6. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

أَوَلَمْ يَرَوْا إِلَى الْأَرْضِ كَمْ أَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ زَوْجٍ كَرِيمٍ ﴿٧﴾

7. Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٨﴾

8. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٩﴾

9. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

HUENDA UKAANGAMIZA NAFSI YAKO

Aya 1-9

MAANA

Twaa Siin Miim.

Umetangulia mfano wake mwanzo wa Sura Baqara, Juz. 1

Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

Hizo ni ishara ya Aya za Sura hii, kitabu ni Qur’an na chenye kubainisha ni kubainisha haki na kudhihirisha.

Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) kwamba asiikere na kuiumiza nafsi yake kwa sababu ya watu wake kuukataa uongofu na haki. Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:35) na Juz. 15 (18:6).

Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu: Poa moyo wako! Lau tungelitaka waamini kwa nguvu tungeliteremsha adhabu kutoka mbinguni waione kwa macho na kuwaambia chagueni imani au adhabu; bila shaka wao wangelisalimu amri kwa unyenyekevu.

Lakini je, hii itahisabiwa kuwa ni imani? Hapana! Imani ya kweli inakuwa kwa utashi na hiyari, sio kwa kulazimishwa kwa nguvu. Ndio maana tukawakadiria kheri na shari, tukawaamrisha hili na kuwakataza lile; kisha tukawaachia hiyari, waweze kustahiki thawabu kwa utiifu na adhabu kwa uasi.

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifanya hivyo katika zama za Musa(a.s) kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na tulipoinua mlima juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawaangukia. Tukawaambia: shikeni kwa nguvu tuliyowapa.” Juz. 9 (7: 171).

Jibu : kwa hakika Qur’an Tukufu inafahamisha waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ana muamala maalum na Mayahudi usiofanana na waja wengine. Kwa sababu wao wana tabia za pekee zisizokuwa na mfano. Tumelizungumzia hilo kwa ufafanuzi zaidi kwa anuani ya ‘Mayahudi hawana mfano’ katika Juz. 1: (2:63-66).

Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

Tumewaongoza washirikina, kupitia kwako ewe Muhammad, kwenye yale yaliyo na kheri yao na masilahi yao, wakaachana nayo, wakayadharau na kuyafanyia masikhara. Basi nawe achana nao na watakumbana na adhabu waliyoahidiwa tu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:68).

Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

Alikufuru Mungu aliyekufuru huku akiona dalili na ubainifu wa kupatikana kwake na ukuu wake. Miongoni mwa dalili hizi ni kutoa mimea ya aina na rangi mbali mbali. Kwa maelezo zaidi angalia Juz.7 (6:99) na Juz. 13 (13:3).

Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Kwa nguvu zake anawashinda mataghuti na rehema zake anawapa muda bila ya kuwaharakishia adhabu mpaka awajie mbashiri na muonyaji na kuwapa fursa ya kufikiria vizuri na kutubia.

Imam Ali(a.s) anasema:“Hasira zake hazimfanyi kuacha huruma yake, wala huruma haimfanyi kupuuza adhabu yake.”

وَإِذْ نَادَىٰ رَبُّكَ مُوسَىٰ أَنِ ائْتِ الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠﴾

10. Na Mola wako alipomwita Musa kwamba nenda kwa watu madhalimu.

قَوْمَ فِرْعَوْنَ أَلَا يَتَّقُونَ ﴿١١﴾

11. Watu wa Firauni. Hawaogopi?

قَالَ رَبِّ إِنِّي أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ ﴿١٢﴾

12. Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

وَيَضِيقُ صَدْرِي وَلَا يَنطَلِقُ لِسَانِي فَأَرْسِلْ إِلَىٰ هَارُونَ ﴿١٣﴾

13. Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

وَلَهُمْ عَلَيَّ ذَنبٌ فَأَخَافُ أَن يَقْتُلُونِ ﴿١٤﴾

14. Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

قَالَ كَلَّا فَاذْهَبَا بِآيَاتِنَا إِنَّا مَعَكُم مُّسْتَمِعُونَ ﴿١٥﴾

15. Akasema, sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu. Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza.

فَأْتِيَا فِرْعَوْنَ فَقُولَا إِنَّا رَسُولُ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote.

أَنْ أَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿١٧﴾

17. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

قَالَ أَلَمْ نُرَبِّكَ فِينَا وَلِيدًا وَلَبِثْتَ فِينَا مِنْ عُمُرِكَ سِنِينَ ﴿١٨﴾

18. Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi?

وَفَعَلْتَ فَعْلَتَكَ الَّتِي فَعَلْتَ وَأَنتَ مِنَ الْكَافِرِينَ ﴿١٩﴾

19. Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

قَالَ فَعَلْتُهَا إِذًا وَأَنَا مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Akasema: Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.

فَفَرَرْتُ مِنكُمْ لَمَّا خِفْتُكُمْ فَوَهَبَ لِي رَبِّي حُكْمًا وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٢١﴾

21. Basi niliwakimbia nilipowahofia. Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

وَتِلْكَ نِعْمَةٌ تَمُنُّهَا عَلَيَّ أَنْ عَبَّدتَّ بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٢٢﴾

22. Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

MUSA

Aya 10 – 22

MAANA

Aya hizi hadi kufikia Aya ya 28 ni za kisa cha Musa ambacho kimetangulia mara kadhaa. Katika Juz. 16 (20: 9) tumeleza sababu za kukaririka kisa hicho.

Na Mola wako alipomwita, Musa kwamba nenda kwa watu madhal- imu watu wa Firauni.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:24).

Hawaogopi?

Hii ni jumla nyingine, maana yake ni kuwa, umefika wakati sasa Firauni na watu wake waogope mwisho wa uovu na utaghuti.

Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

Katika Juz. 16 (20 45) ni: “Ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.”

Yaani asije akatuwahi kutuadhibu kabla kufikishia ujumbe.

Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Musa kupeleka ujumbe wake kwa Firauni. Na hili, kwa upande mmoja, ni jambo zito na lenye mashaka sana, kutokana na utaghuti wa Firauni na nguvu za utawala wake. Na kwa upande mwingine, ujumbe wenyewe ni mzito.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwambia Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) :

إِنَّا سَنُلْقِي عَلَيْكَ قَوْلًا ثَقِيلًا ﴿٥﴾

“Hakika sisi tutakuteremshia kauli nzito.” (73:5).

Musa alikuwa ni mwepesi wa kughadhibika kwa ajili ya haki, na ulimi wake ulikuwa na kigugumizi kinachomzuia kutamka. Kwa hiyo akahofia kutotekeleza vizuri ujumbe mkuu. Hakuna yeyote anayehofia kutekeleza haki ya Mwenyezi Mungu kuliko mitume; hasa wale Ulul-a’zm. Hii inatokana na isma. Ndipo Musa akamtaka Mwenyezi Mungu kumtuma Jibril kwa nduguye, Harun, ili awe msaidizi wake katika jambo hili muhimu.

Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

Anaishiria lile tukio la kumuua mtu wa upande wa Firauni pale alipom- saidia mtu wa upande wake; kama ilivyoelezwa katika Aya hii:

فَوَجَدَ فِيهَا رَجُلَيْنِ يَقْتَتِلَانِ هَـٰذَا مِن شِيعَتِهِ وَهَـٰذَا مِنْ عَدُوِّهِ فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ ﴿١٥﴾

“Na akakuta humo watu wawili wanapigana – mmoja ni katika wenzake na mwingine ni katika maadui zake. Yule aliye katika wenzake akamtaka msaada juu ya adui yake. Musa akampiga ngumi akammaliza.” (28:15).

Musa alihofia kuchukua risala ya Mwenyezi Mungu kwa Firauni asije akamuua kabla kukamilisha lengo, lakini akiwa na nduguye na ikatokewa kuuawa, basi atachukua nafasi yake kuendeleza malengo.

Akasema – Mwenyezi Mungu –sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu, Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

Musa alihofia dhiki ya kifua, kufungika ulimi na kuuliwa, lakini Mwenyezi Mungu akamhakikishia usalama na akamwambia kuwa hakuna kitu kitaka- chokuwa katika hayo, kwa sababu mimi nitawasaidia na kuwanusuru. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20: 46 – 47).

Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi? Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

Musa na Harun walielekea kwa Firauni, wakaingia kwake wakiwa wamevaa deraya ya sufu, mikononi mwao wakiwa na fimbo. Wakampa mwito wa kumwamini Mungu na kumpa sharti la kusilimu na kutii ili utawala wake ubakie na kudumu enzi yake.

Firauni aliwabeza wawili hawa, waliompa masharti ya kudumu utawala na enzi yake, wakiwa hawana cheo chochote wala mali. Hakutaka kuwaua kwa kuhofia asiambiwe kuwa ameshindwa na hoja akakimbilia upanga.

Lakini Firauni anaweza kuwa na hoja gani? Ni kwa mantiki gani atakayoweza kujadili? Hana kitu isipokuwa kuvungavunga na kumtajia Musa yaliyopita.

Je, hatukukulea na ukakaa nyumbani kwetu miaka, kisha ukatuulia mtu wetu na ukakimbia? Hii ndio shukrani yako? Zaidi ya hayo unadai kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwetu? Unataka tukusikize na kukutii na sisi ndio mabwana zako na wafadhili wa neema zako?

Kisha Firauni akawegeukia watu wa baraza lake na akasema: “Basi mbona hakuvikwa vikukuku vya dhahabu?” (43:53). Kwenye dhahabu tu ndio kuna kuwa na siri ya mantiki ya mataghuti. Hakuna utume wala ubwana au ubora isipokuwa kwa ajili ya dhahabu na dhahabu yenyewe.

Musa (a.s) akamjibu kuhusu kuua akasema: “Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.”

Yaani sikuelewa kuwa ngumi yangu itamuua. Nami nilikusudia kukinga na kutia adabu, nikakosea makusudio. Basi mimi nina dhambi gani katika hilo? Kukusudia ni nguzo ya msingi ya kosa la jinai kwa watu wa sharia.

Basi niliwakimbia nilipowahofia.

Sikukimbia hukumu ya uadilifu, bali nilikimbia dhulma kwa kuhofia kunichukulia kuwa ni muuaji wa makusudi. Kuna mmoja alimwambia Musa:

إِنَّ الْمَلَأَ يَأْتَمِرُونَ بِكَ لِيَقْتُلُوكَ فَاخْرُجْ إِنِّي لَكَ مِنَ النَّاصِحِينَ ﴿٢٠﴾

“Hakika wakubwa wanashauriana kukuua. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanaokupa nasaha.” (28:20).

Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

Firauni alimtajia Musa ufukara na utoro; Musa naye akamwambia kuwa utukufu haupimwi kwa mali wala kwa ufalme; isipokuwa uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu, humpatia amtakaye katika waja wake. Na mimi Mwenyezi Mungu amenitunukia elimu ya dini yake na sharia yake kwa njia ya kheri na usawa na akanitukuza kwa kunituma kwako na kwa watu wako.

Musa aliendelea kumjibu Firauni, kuhusu malezi na akasema:

Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

Yaani unanisimbulia kwa malezi yako kwangu na unajitia kutojua kuwa sababu ni uadui wako wa kuwachinja watoto wa kiume wa watu wangu na kuwatia utumwani watoto wao wa kike? Mama yangu alipohofia wewe kunichinja akanitupa baharini na matokeo yake yakawa ni kuishi mimi mbali ugenini bila ya huruma ya mama na mapenzi ya baba? Hii ndiyo fadhila yako kwangu? Firauni alizibwa mdomo, akaanza kuwatafuta wabatilifu wake; kama utakavyoona katika kifungu kifuatacho.

قَالَ فِرْعَوْنُ وَمَا رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٢٣﴾

23. Akasema Firauni: Na ni nani huyo Mola wa walimwengu wote?

قَالَ رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ ﴿٢٤﴾

24. Akasema: Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.

قَالَ لِمَنْ حَوْلَهُ أَلَا تَسْتَمِعُونَ ﴿٢٥﴾

25. Akawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

قَالَ رَبُّكُمْ وَرَبُّ آبَائِكُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٢٦﴾

26. Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

قَالَ إِنَّ رَسُولَكُمُ الَّذِي أُرْسِلَ إِلَيْكُمْ لَمَجْنُونٌ ﴿٢٧﴾

27. Akasema: Hakika mtume wenu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

قَالَ رَبُّ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُمْ تَعْقِلُونَ ﴿٢٨﴾

28. Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

قَالَ لَئِنِ اتَّخَذْتَ إِلَـٰهًا غَيْرِي لَأَجْعَلَنَّكَ مِنَ الْمَسْجُونِينَ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

قَالَ أَوَلَوْ جِئْتُكَ بِشَيْءٍ مُّبِينٍ ﴿٣٠﴾

30. Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?

قَالَ فَأْتِ بِهِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٣١﴾

31. Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

فَأَلْقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعْبَانٌ مُّبِينٌ ﴿٣٢﴾

32. Akaitupa fimbo, mara ikawa nyoka dhahiri.

وَنَزَعَ يَدَهُ فَإِذَا هِيَ بَيْضَاءُ لِلنَّاظِرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao.

قَالَ لِلْمَلَإِ حَوْلَهُ إِنَّ هَـٰذَا لَسَاحِرٌ عَلِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi, mjuzi.

يُرِيدُ أَن يُخْرِجَكُم مِّنْ أَرْضِكُم بِسِحْرِهِ فَمَاذَا تَأْمُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani?

قَالُوا أَرْجِهْ وَأَخَاهُ وَابْعَثْ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٣٦﴾

35. Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini.

يَأْتُوكَ بِكُلِّ سَحَّارٍ عَلِيمٍ ﴿٣٧﴾

37. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

MAJIBIZANO BAINA YA MUSA NA FIRAUNI

Aya 23 – 37

MAANA

Akasema Firauni: Na ninani huyo Mola wa walimwengu wote?

Ewe Musa! Wewe unadai kuwa ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote; hebu tubainishie jinsi yake na hakika yake huyo Mola?

Akasema: “Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.”

Musa alisema: Mwenyezi Mungu hajulikani isipokuwa kwa sifa zake na athari zake; zikiwa ni pamoja na huku kuumbwa ulimwengu huu wa ajabu katika mpangilio wake na nidhamu yake. Basi fikirini na mzingatie ikiwa mna akili zinazoweza kutambua kuwa nidhamu hii haiwezekani ila kwa uweza wa ujuzi na hekima.

Firauniakawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

Yaani mnasikia maajabu hayo. Hatujawahi kusikia haya kwa mababa zetu wa kwanza.

Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

Musa alisema kwa kusisitiza kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa ulimwengu, muumba wenu na muumba wa baba zenu wa mwanzo na pia ndiye muumba wa huyu Firauni mnayemfanya mungu na kumwabudu.

Akasema: Hakika mtume wenu huyu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

Musa ni mwendawazimu katika mantiki ya Firauni, kwa nini? Kwa sababu amesema Firauni si mungu bali ni kiumbe. Mantiki haya ya kifirauni anayo kila anayedai asichokuwa nacho. Yeyote anayedai kuwa na elimu naye ni mjinga, ikhlasi naye ni mhaini au ukweli naye ni mrongo, basi yeye yuko katika mila ya Firauni na desturi yake. Lau atapata wanaomwamini atasema: Mimi ndiye mola wenu au simjui mungu mwingine kwenu zaidi ya mimi; kama alivyosema Firauni.

Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

Musa aliendelea kushikilia msimamo wake kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu. Akaashiria kuchomoza jua na kuchwa kwake, ambapo Firauni hawezi kujasiri kusema kuwa yeye ndiye anayelichomoza jua mashariki na kulipeleka magharibi.

Kwa hiyo alipigwa na butwaa aliposikia maneno haya kutoka kwa Musa; sawa na alivyopigwa na butwaa Namrud kabla yake, pale Ibrahim(a.s) alipomnyamazisha kwa kusema:

فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ ﴿٢٥٨﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi.”

Juz. 3 (2:258).

Firauni alipoishiwa, alikereka, akawa anatoa vitisho naakasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

Jela na kutesa ndio silaha pekee ya utawala muovu wa mabavu dhidi ya haki uadilifu na uhuru, tangu zamani. Lakini jihadi ya wakombozi na ukakamavu wao, unaifanya silaha ya mataghuti ishindwe kwenye shingo zao na vifua vyao; kama ilivyoshindwa silaha ya Firauni.

Walisema wa kale: Mwenye kuchomoa upanga wa dhulma atauliwa nao.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

فَكُلًّا أَخَذْنَا بِذَنبِهِ فَمِنْهُم مَّنْ أَرْسَلْنَا عَلَيْهِ حَاصِبًا وَمِنْهُم مَّنْ أَخَذَتْهُ الصَّيْحَةُ وَمِنْهُم مَّنْ خَسَفْنَا بِهِ الْأَرْضَ ﴿٤٠﴾

“Kila mmoja tulimtesa kwa makosa yake. Kati yao wapo tuliowapelekea kimbunga cha changarawe, na kati yao wapo walionyakuliwa na ukelele na kati yao wapo ambao tuliwadidimiza katika ardhi.” (29:40).

Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?” Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

Musa hakuogopa vitisho vya Firauni na akamwambia kwa kujiamini kuwa utanifanya mfungwa hata kama ni mwenye haki, kwa kukuletea dalili isiyo na shaka kwako na kwa mwingine?

Atajibu nini Firauni? Je, amwambie ndio nitakufunga hata kama ni mwenye haki? Hawezi kumwambia hivi, kwa sababu itakuwa ni kukubali ukweli kuwa Musa ni Mtume wa Mola wa viumbe wote na kwamba yeye ni mzushi katika madai yake ya uungu. Kwa hiyo ndio akalazimika kusema lete hiyo dalili kama wewe ni mkweli.

Akaitupa fimbo mara ikawa nyoka dhahiri. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani? Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

Aya hizi sita zimetangulia katika Juz. 9 (7:107 - 112) zikifanana kiutaratibu, kimpangilio na hata herufi; isipokuwa katika mambo mawili:

Hapa imesemwa: ‘mchawi mkubwa’ na kule ikasemwa ‘mchawi’ hakuna tofauti katika maneno haya isipokuwa kutilia mkazo.

Hapa imesemwa: ‘Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi,’ na kule imesemwa: ‘Wakasema wakuu wa watu wa Firauni: Hakika huyu ni mchawi mjuzi.’ Tofauti hapa ni kubwa kama inavyojionyesha.

Kwa sababu hapa aliyesema ni Firauni kuwaambia wakuu na kule wakuu ndio waliosema kumwambia Firauni. Sasa je, kuna wajihi gani wa kuunganisha baina ya Aya mbili hizi?

Jibu : Sikupata ishara yoyote ya hilo katika tafsiri nilizonazo, wala sijui sababu yake. Kwa vyovyote iwavyo, jibu ninaloliona ni kuwa Firauni ndiye aliyeanza kuwaambia jamaa zake kuwa huyu ni mchawi; kisha jamaa zake nao wakaanza kuambiana kuwa ni kweli Musa ni mchawi; kama ilivyo kwa wanaoongozwa, wanaigiza kiongozi wao na kutolea ushahidi kauli zake.

Hapo basi hakuna kupingana baina ya Aya mbili. Firauni aliwaambia jamaa zake nao wakamwambia yeye kwa kumwigiza.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُهُمْ وَلَا يَضُرُّهُمْ وَكَانَ الْكَافِرُ عَلَىٰ رَبِّهِ ظَهِيرًا ﴿٥٥﴾

55. Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu. Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا مُبَشِّرًا وَنَذِيرًا ﴿٥٦﴾

56. Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

قُلْ مَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِلَّا مَن شَاءَ أَن يَتَّخِذَ إِلَىٰ رَبِّهِ سَبِيلًا ﴿٥٧﴾

57. Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

وَتَوَكَّلْ عَلَى الْحَيِّ الَّذِي لَا يَمُوتُ وَسَبِّحْ بِحَمْدِهِ وَكَفَىٰ بِهِ بِذُنُوبِ عِبَادِهِ خَبِيرًا ﴿٥٨﴾

58. Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ الرَّحْمَـٰنُ فَاسْأَلْ بِهِ خَبِيرًا ﴿٥٩﴾

59. Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi. Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اسْجُدُوا لِلرَّحْمَـٰنِ قَالُوا وَمَا الرَّحْمَـٰنُ أَنَسْجُدُ لِمَا تَأْمُرُنَا وَزَادَهُمْ نُفُورًا ﴿٦٠﴾

60. Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe? Na huwazidishia chuki.

تَبَارَكَ الَّذِي جَعَلَ فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَجَعَلَ فِيهَا سِرَاجًا وَقَمَرًا مُّنِيرًا ﴿٦١﴾

61. Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ خِلْفَةً لِّمَنْ أَرَادَ أَن يَذَّكَّرَ أَوْ أَرَادَ شُكُورًا ﴿٦٢﴾

62. Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

KAFIRI NI MSADIZI WA MPINZANI WA MOLA WAKE

Aya 55 – 62

MAANA

Na wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha badala ya Mwenyezi Mungu.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 11 (10 18).

Na kafiri daima ni msaidizi wa mpinzani wa Mola wake.

Yaani anawasaidia watu wa batili dhidi ya haki. Kila mwenye kusaidia batili atakuwa amesaidia dhidi ya Mwenyezi Mungu na kuwa adui yake; hata kama atamsabihi na kumtukuza kwa ulimi wake. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) :“Mwenye kumsaidia dhalimu na huku anajua kuwa ni dhalimu basi amejitenga na Uislamu.”

Kadiri nitakavyotia shaka, lakini siwezi kutia shaka kuwa mwenye kumtegemea dhalimu ni kafiri; bali kafiri aliye mwadilifu ni bora kuliko yeye. Aya za Qur’an kuhusu hilo ni nyingi na ziko wazi. Ama Hadith za Mtume zimepituka kiwango cha mutawatir.

Ndio! Ni wajibu wetu kuamiliana naye muamala wa kiislamu kwa vile tu ametamka: Lailaha illallah Muhammadurrasulullah (Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.)

Na hatukukutuma ila uwe mbashiri na muonyaji.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 15 (17:105).

Sema: Siwaombi ujira juu yake, isipokuwa mwenye kutaka ashike njia iendayo kwa Mola wake.

Mimi sina tamaa ya mali yenu wala siwauzii pepo. Ninalotaka ni kutengeneza tu. Anayetaka kufanya njia ya kumwendea Mola miongoni mwenu, basi malipo yake yako kwa Mungu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz.12 (11:88).

Na mtegemee aliye hai ambaye hafi na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kuwa yeye ni mwenye habari za dhambi za waja wake.

Ewe Muhammad! Toa bishara na onyo ukimtegemea Mwenyezi Mungu kwa kuwa na ikhlasi naye katika kauli yako na vitendo vyako na ujitakashe na kumfanyia mfano na kila lile ambalo halifanani na utukufu na ukuu wake. Yeye anamjua zaidi aliyepotea njia, na atamhisabu na kumlipa.

Ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita, kisha akastawi juu ya Arshi.

Makusudio ya kustawi ni kutawala. Lililo na nguvu ni kuwa makusudio ya siku ni mikupuo, kwa sababu hakuna siku kabla ya kupatikana ulimwengu na jua. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:54), Juz. 11 (103), na Juz. 12 (11:7).

Mwingi wa rehema! Uliza habari zake kwa ajuaye.

Habari yake, ni habari ya huko kuumbwa mbingu na ardhi, ambako kunafahamika kutokana na mfumo wa Aya. Hapa kuna maneno yaliyotan- gulizwa na ya kukadiriwa. Maana ni: Yeye ni Mwingi wa rehema, ulizia habari za kuumbwa mbingu na ardhi kwa yule ajuaye ambaye ni Mwenyezi Mungu.

Na wanapoambiwa msujudieni Mwingi wa rehema, wanasema: ‘Ni nani huyo mwingi wa rehema? Je, tumsujudie unayetuamrisha wewe?’ Na huwazidishia chuki.

Nabii(s.a.w.w) akiwaambia washirikina: ‘Mwabuduni Mwingi wa rehema, wala msiabudu masanamu,’ wao husema kwa kujitia hamnazo, kwa madharau, ni nani huyo unayetuambia tumwabudu unayemuita Mwingi wa rehema? Unataka tukutii wewe na tuwaasi baba zetu katika yale waliyokuwa wakiyaabudu?’

Ujinga na upumbavu huu unatukumbusha ujinga wa vijana wetu wanapoambiwa swalini na mfunge, husema: “Bado kuna Swala katika karne hii ya ishirini? Jambo la kushangaza ni kuwa vijana hawa wanaimba uhuru wa bianadamu; kama kwamba uhuru ni uzandiki na utu ni kujitoa kwenye misimamo.

Hawajui kuwa aliye huru ni yule anayemwabudu Mwenyezi Mungu wala hamnyenyekei asiyekuwa yeye na kwamba utu ni dini ya Mwenyezi Mungu ambayo inakataza maovu na munkar.

Amekuwa na baraka yule aliyejaalia katika mbingu buruji na akajaalia humo taa na mwezi wenye nuru.

Makusudio ya buruji ni mashukio ya jua na mwezi. Tazama Juz.14 (15: 16). Makusudio ya taa hapa ni jua, kutokana na kuunganisha na mwezi. Mahali pengine Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ الشَّمْسَ ضِيَاءً وَالْقَمَرَ نُورًا ﴿٥﴾

“Yeye ndiye aliyefanya jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru.” Juz.11 (10:5).

Wengine wametofautisha baina ya nuru na mwanga. Kwamba mwanga unategemea sayari moja kwa moja; kama vile mwanga wa jua, unatoka kwenye jua moja kwa moja.

Nuru inategemea sayari kupitia sayari nyingine; kama vile nuru ya mwezi inavyotegmea jua. Wametoa dalili wanaotofautisha, kwa Aya hiyo ya Juz. 11 (10:5) tuliyoitaja punde.

Naye ndiye ambaye ameujaalia usiku na mchana kufuatana, kwa yule anayetaka kukumbuka au anayetaka kushukuru.

Usiku unaondoka kisha unakuja mchana, nao unaondoka kisha unarudi usiku na kuendelea; wala hakuna unaobakia muda mrefu kuzidi kiasi cha haja ya viumbe.

Kufuatana kwa namna hii kunafahamisha kuweko mpangiliaji mwenye hekima. Kufuatana huku kunategemea harakati za ardhi, nazo zinategemea msababishaji wake wa kwanza.

Ama hekima ya mfuatano huu, ni kwamba lau lingelibakia giza tu, au mwangaza tu, maisha yangelikuwa magumu hapa ardhini.

Kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) ‘Kwa anayetaka kukumbuka,’ maana yake ni kuwa mwenye kutaka dalili ya kuweko Mwenyezi Mungu ataipata katika vitu vyote, vikiwemo kufuatana usiku na mchana.

Na kauli yake ‘Au anayetaka kushukuru,’ ni kuwa anayetaka kumshukuru Mweneyzi Mungu kwa neema yake naashukuru vile vile kwa kufuatana usiku na mchana, kwa sababu hilo ni katika neema kubwa.

وَعِبَادُ الرَّحْمَـٰنِ الَّذِينَ يَمْشُونَ عَلَى الْأَرْضِ هَوْنًا وَإِذَا خَاطَبَهُمُ الْجَاهِلُونَ قَالُوا سَلَامًا ﴿٦٣﴾

63. Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu. Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

وَالَّذِينَ يَبِيتُونَ لِرَبِّهِمْ سُجَّدًا وَقِيَامًا ﴿٦٤﴾

64. Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا اصْرِفْ عَنَّا عَذَابَ جَهَنَّمَ إِنَّ عَذَابَهَا كَانَ غَرَامًا ﴿٦٥﴾

65. Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam,’ hakika adhabu yake ni yenye kuendelea.

إِنَّهَا سَاءَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٦٦﴾

66. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa.

وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴿٦٧﴾

67. Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo.

وَالَّذِينَ لَا يَدْعُونَ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ وَلَا يَقْتُلُونَ النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّـهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَا يَزْنُونَ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ يَلْقَ أَثَامًا ﴿٦٨﴾

68. Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki, wala hawazini. Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

يُضَاعَفْ لَهُ الْعَذَابُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَيَخْلُدْ فِيهِ مُهَانًا ﴿٦٩﴾

69. Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

إِلَّا مَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ عَمَلًا صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ يُبَدِّلُ اللَّـهُ سَيِّئَاتِهِمْ حَسَنَاتٍ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٧٠﴾

70. Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.

وَمَن تَابَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَإِنَّهُ يَتُوبُ إِلَى اللَّـهِ مَتَابًا ﴿٧١﴾

71. Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

وَالَّذِينَ لَا يَشْهَدُونَ الزُّورَ وَإِذَا مَرُّوا بِاللَّغْوِ مَرُّوا كِرَامًا ﴿٧٢﴾

72. Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

وَالَّذِينَ إِذَا ذُكِّرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ لَمْ يَخِرُّوا عَلَيْهَا صُمًّا وَعُمْيَانًا ﴿٧٣﴾

73. Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawajifanyi ni viziwi nazo na vipofu.

وَالَّذِينَ يَقُولُونَ رَبَّنَا هَبْ لَنَا مِنْ أَزْوَاجِنَا وَذُرِّيَّاتِنَا قُرَّةَ أَعْيُنٍ وَاجْعَلْنَا لِلْمُتَّقِينَ إِمَامًا ﴿٧٤﴾

74. Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wanetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

أُولَـٰئِكَ يُجْزَوْنَ الْغُرْفَةَ بِمَا صَبَرُوا وَيُلَقَّوْنَ فِيهَا تَحِيَّةً وَسَلَامًا ﴿٧٥﴾

75. Hao ndio watakolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam.

خَالِدِينَ فِيهَا حَسُنَتْ مُسْتَقَرًّا وَمُقَامًا ﴿٧٦﴾

76. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

قُلْ مَا يَعْبَأُ بِكُمْ رَبِّي لَوْلَا دُعَاؤُكُمْ فَقَدْ كَذَّبْتُمْ فَسَوْفَ يَكُونُ لِزَامًا ﴿٧٧﴾

77. Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

WAJA WA MWINGI WA REHEMA

Aya 63 – 77

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja sifa za makafiri na kiaga chao, kama kawaida yake, anataja sifa za waumini na malipo aliyowaandalia. Zifuatazo ndizo sifa zao:

1.Na waja wa Mwingi wa rehema ni wale wanaotembea ardhini kwa unyenyekevu.

Imam Jafar Sadiq(a.s) anasema katika tafsiri ya hilo:“Ni yule mtu anayetembea kwenye asili yake aliyoumbiwa, hajikalifishi wala hajifanyi.” Ndio, anayetembea kwenye umbile lake aliloumbiwa, tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wapambe na wafuasi wanaomfuta nyuma na wengine mbele wakiwa wamepanda farasi au pikipiki na kupiga ving’ora vinavyohanikiza watu kwa sauti zake vikitangaza kuja kwake ili aachiwe njia, kwa ajili ya kumheshimu na kumtukuza.

2.Na wajinga wakiwasemesha, husema: ‘Salama.’

Makusudio ya kusemeshwa na wajinga ni kama vile kejeli zao, shutuma zao au mijadala ya hawa na masilahi. Amani ni kinaya cha kuachana nao, kwa kuwadharau na kuchunga mtu heshima yake. Maana ni kuwa, muumini akisikia neno ovu, aachane nalo; kama kwamba hakulisikia au kama anayekusudiwa ni mwingine sio yeye. Huu ndio mwepuko mwema aliousema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَاهْجُرْهُمْ هَجْرًا جَمِيلًا ﴿١٠﴾

“Na uwaepuke mwepuko mwema.” (73:10).

Hakuna mwenye shaka kwamba kuachana na jambo ni pale ikiwa hakuna uwezo au nguvu za kulikabili. Vinginevyo itakuwa ni wajibu kulikabili. Hapana budi kuihusisha Aya na hilo.

3.Na wale wanaokesha kwa ajili ya Mola wao kusujudu na kusimama.

Waumini wanasimama usiku kwenye giza wakifanya ibada ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu hilo liko mbali na ria, wala hawaupitishi usiku mikahawani na kwenye mambo ya mchezo mchezo tu, huku wakifuja mali na kupanga njama dhidi ya waumini na wenye ikhlasi. Mfano wa Aya hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:

كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ ﴿١٧﴾

“Walikuwa wakilala kidogo usiku.” (51:17).

4.Na wale wanaosema: ‘Mola wetu! Tuondolee adhabu ya Jahannam, hakika adhabu yake ni yenye kuendelea. haikwepeki na ni yakudumu. Hakika hiyo ni mbaya kuwa kituo na mahali pa kukaa,

Waliamini Pepo na Moto, kutokana na waliyoyashuhudia na kuyaona; ndio wakauhofia moto wakaitumai pepo. Imam Ali(a.s ) anasema: “Wao na Pepo ni kama walioiona wakiwa ndani yake wananeemeshwa. Na wao na moto ni kama waliouona wakiwa ndani yake wanaadhibiwa.”

5.Na wale ambao wanapotumia hawafanyi israfu wala hawafanyi uchoyo wanakuwa katikati baina ya hayo, hakuna kupitisha kiasi, Si ubakhili wala ubadhirifu.

Huu ndio mwenendo wa Uislamu, wastani katika kila kitu; hakuna ulahidi wala waungu wengi, udikteta wala ukiritimba na hakuna kutaifisha mali ya mtu wala ubepari. Tazama Juz. 15 (17:29) kifungu cha ‘Uislamu na nadharia ya maadili.’

6.Na wale ambao hawamwombi mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Mwenye kufanya riya au akamtii kiumbe katika kumuasi Muumba, basi huyo ni kama aliyemwomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu.

Wala hawaiui nafsi aliyoiharamisha ila kwa haki.

Nafsi inayouliwa kwa haki na kwa uadilifu ni ile iliyoua nafsi nyingine bila ya haki, aliyezini akiwa kwenye ndoa, kurtadi dini au kuleta ufisadi katika ardhi.

Ufafanuzi wa hayo uko katika vitabu vya Fiqh.

Wala hawazini

Kwa sababu zinaa ni katika madhambi makubwa. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t). Akaiweka sawa na kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuua nafsi na akajaalia hukumu ya haya matatu ni kuuliwa kwa masharti yaliyotajwa kwenye vitabu vya fiqh.

Na mwenye kuyafanya hayo atapata madhambi.

Hayo ni hayo ya shirk, kuua na kuzini. Na madhambi ni adhabu.

Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama na atadumu humo kwa kufedheheka.

Kuna adhabu gani kubwa na kufedheheka zaidi kuliko adhabu ya Jahannam? Si kwambii tena ikiwa itazidishwa pamoja na kudumu kusiko na mwisho.

Isipokuwa atakayetubia na akatenda matendo mema, basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe mwenye kurehemu.

Mwenye kutubia dhambi ni kama asiyekuwa na dhambi, zaidi ya hayo, Mwenyezi Mungu atampa thawabu kwa kule kutubia kwake na atampa mema kulingana na maovu ya dhambi zake; kiasi ambacho toba itafuta maovu ya dhambi.

إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ ﴿١١٤﴾

“Hakika mema huondoa maovu.” Juz. 12 (11:114).

Haya ndiyo maana ya ‘Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema’ kwa sababu uovu, kwa ulivyo, haustahiki kuwa wema, wala wema, kwa ulivyo, haustahiki kuwa uovu’

Na aliyetubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kwa Mwenyezi Mungu toba ya kweli.

Baada ya kubainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya iliyotangulia kwamba mwenye kutubia atampa thawabu za mwenye kufanya mema, hapa anamsifu kuwa amerejea kwa Muumba wake kurejea kuzuri.

7.Na wale ambao hawawi kwenye uzushi, na wanapopita kwenye upuzi hupita kwa heshima zao.

Neno ‘hawawi’ limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu ‘laa yash-hadu- una’ kama ilivyotumika tafsiri hiyo katika Juz. 2 (2:185). Makusudio ya uzushi ni mambo ya batili na upuzi ni kila lisilo na kheri. Maana ni kuwa waumini hawahudhurii vikao vya ubatilifu wala hawavisaidii, sikwambii kuvifanya. Pia hawashiriki mazungumzo yasiyokuwa na kheri na wanapoyapitia hayo masiko yao huyaepuka; kama wanavyoziepusha ndimi zao kuayatamka; sawa na nyuki anavyopita haraka kwenye mzoga na harufu mbaya.

8.Na wale ambao wanapokumbushwa ishara za Mola wao hawaji- fanyi ni viziwi nazo na vipofu.

Mshairi huwa anasikiliza mashairi kwa umakini kabisa. Vile vile kila mwenye kuhusika na jambo akizungumziwa huwa anakuwa makini nalo sana anapolisikilza. Mtu unapomzungumzia jambo lililo mbali naye atakuepuka na hayo mazungumzo yako, hata kama ni ya uongofu na mwangaza.

Hapa ndipo inabainika siri ya muumini kuikubali Qur’an, na kafiri kuachana nayo. Mumin anakikubali Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa vile anakiamini na kutambua maana yake na makusudio yake. Anakikuta kwenye nafsi yake, itikadi yake, matendo yake mema na malipo aliyomuandalia Mola wake.

Kafiri anakipa mgongo Kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa sababu anakipinga na hajui malengo yake na siri yake; wala hapati humo isipokuwa kushutumiwa na kukosolewa itikadi yake na sifa zake na pia makaripio ya ukafiri wake.

9.Na wale ambao wanasema: Mola wetu! Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wenye takua.

Muovu huwa anatamaani watu wamfuate katika uovu wake, sio kwa kuwa amekinai kuwa yuko kwenye uongofu kutoka kwa Mola wake, hapana! Isipokuwa anataka kupunguza lawama na shutuma na kufunika kosa lake kwa kuwa wengi wakosefu. Lakini hataki mkewe na watoto wake wawe hivyo; kama vile mgonjwa asivyopenda watu wake wapatwe na ugonjwa alio nao.

Ama yule aliye mwema na mwenye takua ana yakini na dini yake na ana busara katika mambo yake. Kwa hivyo huwa anatamaani kwa dhati ya moyo kimsingi na kiitikadi kuwa watu wote wafuate njia yake na kwamba watoto wake wakimuiga yeye huwa anafurahi.

Kwa hiyo wenye ikhlasi humuomba Muumba wao wapate wa kuwaiga, sio kwa kuziba vitendo vyao kwa watu wala kutaka jaha duniani na kuchukua mali kwa kutumia haki za Mwenyezi Mungu; bali ni kwa kujipendekeza mbele ya Mwenyezi Mungu aliye peke yake.

Hao ndio watakaolipwa ghorofa kwa walivyosubiri na watakuta humo maamkuzi na salaam. Watadumu humo kituo na makao mazuri.

Ghorofa ni kinaya cha makao ya juu. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha wasifu wa wenye takua na watiifu, sasa anataja malipo yao watakayoyapata kwake, ambayo ni kudumu katika raha, amani na neema pamoja na heshima.

Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja subira hapa kuashiria kuwa kila mwenye haki hana budi kupata taabu na udhia kutoka kwa wasio na haki na kwamba thawabu za Mwenyezi Mungu hatazipata ispokuwa mwenye kuwa na uvumilivu na subira na akaendelea kuwa na msimamo kadiri hali itakavyokuwa ngumu.

Sema, Mola wangu asingewajali lau si kupewa kwenu mwito, lakini nyinyi mmewakadhibisha, basi (adhabu) ni lazima.

Makusudio ya neno ‘duakum’ hapa ni kupewa mwito kutokana na maneno yanayovutia, lakini mlikadhibisha. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ ﴿٥٢﴾

“Basi watawaita nao hawatawaitikia.” Juz. 15 (18:52)

Kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapa mwito kwenye imani na utiifu kupitia kwa Mtume wake.

Maana ni kuwa nyinyi washirikina hamstahiki hata kutajwa pia lau si kuwa mliitwa kwenye imani na utiifu, ili kuweko na hoja siku ya hisabu na malipo, ikiwa hamtasikia na kuitikia mwito. Nanyi mmeupinga mwito na mkadhibishaji aliyetoa mwito huo, basi adhabu inawastahiki na ni lazima.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Sura Ya Ishirini Na Sita: Surat Shua’rau.

Twabrasiy amesema imeshuka Makka isipokuwa Aya 224 hadi mwisho, zimeshuka Madina. Ina Aya 227

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehma Mwenye kurehemu.

طسم ﴿١﴾

1. Twaa Siin Miim.

تِلْكَ آيَاتُ الْكِتَابِ الْمُبِينِ ﴿٢﴾

2. Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

لَعَلَّكَ بَاخِعٌ نَّفْسَكَ أَلَّا يَكُونُوا مُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

إِن نَّشَأْ نُنَزِّلْ عَلَيْهِم مِّنَ السَّمَاءِ آيَةً فَظَلَّتْ أَعْنَاقُهُمْ لَهَا خَاضِعِينَ ﴿٤﴾

4. Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

وَمَا يَأْتِيهِم مِّن ذِكْرٍ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ مُحْدَثٍ إِلَّا كَانُوا عَنْهُ مُعْرِضِينَ ﴿٥﴾

5. Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao.

فَقَدْ كَذَّبُوا فَسَيَأْتِيهِمْ أَنبَاءُ مَا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٦﴾

6. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

أَوَلَمْ يَرَوْا إِلَى الْأَرْضِ كَمْ أَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ زَوْجٍ كَرِيمٍ ﴿٧﴾

7. Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٨﴾

8. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٩﴾

9. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

HUENDA UKAANGAMIZA NAFSI YAKO

Aya 1-9

MAANA

Twaa Siin Miim.

Umetangulia mfano wake mwanzo wa Sura Baqara, Juz. 1

Hizo ni Aya za Kitabu kinachobainisha.

Hizo ni ishara ya Aya za Sura hii, kitabu ni Qur’an na chenye kubainisha ni kubainisha haki na kudhihirisha.

Huenda ukaiangamiza nafsi yako kwa kuwa hawawi waumini.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) kwamba asiikere na kuiumiza nafsi yake kwa sababu ya watu wake kuukataa uongofu na haki. Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:35) na Juz. 15 (18:6).

Tungelipenda tungeliwateremshia kutoka mbinguni ishara zikainyenyekea shingo zao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu: Poa moyo wako! Lau tungelitaka waamini kwa nguvu tungeliteremsha adhabu kutoka mbinguni waione kwa macho na kuwaambia chagueni imani au adhabu; bila shaka wao wangelisalimu amri kwa unyenyekevu.

Lakini je, hii itahisabiwa kuwa ni imani? Hapana! Imani ya kweli inakuwa kwa utashi na hiyari, sio kwa kulazimishwa kwa nguvu. Ndio maana tukawakadiria kheri na shari, tukawaamrisha hili na kuwakataza lile; kisha tukawaachia hiyari, waweze kustahiki thawabu kwa utiifu na adhabu kwa uasi.

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu (s.w.t) alifanya hivyo katika zama za Musa(a.s) kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na tulipoinua mlima juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawaangukia. Tukawaambia: shikeni kwa nguvu tuliyowapa.” Juz. 9 (7: 171).

Jibu : kwa hakika Qur’an Tukufu inafahamisha waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ana muamala maalum na Mayahudi usiofanana na waja wengine. Kwa sababu wao wana tabia za pekee zisizokuwa na mfano. Tumelizungumzia hilo kwa ufafanuzi zaidi kwa anuani ya ‘Mayahudi hawana mfano’ katika Juz. 1: (2:63-66).

Na hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mwingi wa rehema ila hujitenga nao. Kwa hakika wamekadhibisha, kwa hivyo zitakujawafikia habari za yale waliyokuwa wakiyafanyia stihizai.

Tumewaongoza washirikina, kupitia kwako ewe Muhammad, kwenye yale yaliyo na kheri yao na masilahi yao, wakaachana nayo, wakayadharau na kuyafanyia masikhara. Basi nawe achana nao na watakumbana na adhabu waliyoahidiwa tu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:68).

Je hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri. Hakika katika hayo kuna ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

Alikufuru Mungu aliyekufuru huku akiona dalili na ubainifu wa kupatikana kwake na ukuu wake. Miongoni mwa dalili hizi ni kutoa mimea ya aina na rangi mbali mbali. Kwa maelezo zaidi angalia Juz.7 (6:99) na Juz. 13 (13:3).

Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Kwa nguvu zake anawashinda mataghuti na rehema zake anawapa muda bila ya kuwaharakishia adhabu mpaka awajie mbashiri na muonyaji na kuwapa fursa ya kufikiria vizuri na kutubia.

Imam Ali(a.s) anasema:“Hasira zake hazimfanyi kuacha huruma yake, wala huruma haimfanyi kupuuza adhabu yake.”

وَإِذْ نَادَىٰ رَبُّكَ مُوسَىٰ أَنِ ائْتِ الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠﴾

10. Na Mola wako alipomwita Musa kwamba nenda kwa watu madhalimu.

قَوْمَ فِرْعَوْنَ أَلَا يَتَّقُونَ ﴿١١﴾

11. Watu wa Firauni. Hawaogopi?

قَالَ رَبِّ إِنِّي أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ ﴿١٢﴾

12. Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

وَيَضِيقُ صَدْرِي وَلَا يَنطَلِقُ لِسَانِي فَأَرْسِلْ إِلَىٰ هَارُونَ ﴿١٣﴾

13. Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

وَلَهُمْ عَلَيَّ ذَنبٌ فَأَخَافُ أَن يَقْتُلُونِ ﴿١٤﴾

14. Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

قَالَ كَلَّا فَاذْهَبَا بِآيَاتِنَا إِنَّا مَعَكُم مُّسْتَمِعُونَ ﴿١٥﴾

15. Akasema, sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu. Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza.

فَأْتِيَا فِرْعَوْنَ فَقُولَا إِنَّا رَسُولُ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote.

أَنْ أَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿١٧﴾

17. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

قَالَ أَلَمْ نُرَبِّكَ فِينَا وَلِيدًا وَلَبِثْتَ فِينَا مِنْ عُمُرِكَ سِنِينَ ﴿١٨﴾

18. Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi?

وَفَعَلْتَ فَعْلَتَكَ الَّتِي فَعَلْتَ وَأَنتَ مِنَ الْكَافِرِينَ ﴿١٩﴾

19. Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

قَالَ فَعَلْتُهَا إِذًا وَأَنَا مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Akasema: Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.

فَفَرَرْتُ مِنكُمْ لَمَّا خِفْتُكُمْ فَوَهَبَ لِي رَبِّي حُكْمًا وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٢١﴾

21. Basi niliwakimbia nilipowahofia. Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

وَتِلْكَ نِعْمَةٌ تَمُنُّهَا عَلَيَّ أَنْ عَبَّدتَّ بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٢٢﴾

22. Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

MUSA

Aya 10 – 22

MAANA

Aya hizi hadi kufikia Aya ya 28 ni za kisa cha Musa ambacho kimetangulia mara kadhaa. Katika Juz. 16 (20: 9) tumeleza sababu za kukaririka kisa hicho.

Na Mola wako alipomwita, Musa kwamba nenda kwa watu madhal- imu watu wa Firauni.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:24).

Hawaogopi?

Hii ni jumla nyingine, maana yake ni kuwa, umefika wakati sasa Firauni na watu wake waogope mwisho wa uovu na utaghuti.

Akasema: Mola wangu! Hakika mimi naogopa watanikadhibisha.

Katika Juz. 16 (20 45) ni: “Ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.”

Yaani asije akatuwahi kutuadhibu kabla kufikishia ujumbe.

Na kifua changu kinadhikika, na ulimi wangu haukunjuki vyema, basi mtumie ujumbe Harun.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Musa kupeleka ujumbe wake kwa Firauni. Na hili, kwa upande mmoja, ni jambo zito na lenye mashaka sana, kutokana na utaghuti wa Firauni na nguvu za utawala wake. Na kwa upande mwingine, ujumbe wenyewe ni mzito.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwambia Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) :

إِنَّا سَنُلْقِي عَلَيْكَ قَوْلًا ثَقِيلًا ﴿٥﴾

“Hakika sisi tutakuteremshia kauli nzito.” (73:5).

Musa alikuwa ni mwepesi wa kughadhibika kwa ajili ya haki, na ulimi wake ulikuwa na kigugumizi kinachomzuia kutamka. Kwa hiyo akahofia kutotekeleza vizuri ujumbe mkuu. Hakuna yeyote anayehofia kutekeleza haki ya Mwenyezi Mungu kuliko mitume; hasa wale Ulul-a’zm. Hii inatokana na isma. Ndipo Musa akamtaka Mwenyezi Mungu kumtuma Jibril kwa nduguye, Harun, ili awe msaidizi wake katika jambo hili muhimu.

Nao wanalo kosa juu yangu basi naogopa wasije wakaniua.

Anaishiria lile tukio la kumuua mtu wa upande wa Firauni pale alipom- saidia mtu wa upande wake; kama ilivyoelezwa katika Aya hii:

فَوَجَدَ فِيهَا رَجُلَيْنِ يَقْتَتِلَانِ هَـٰذَا مِن شِيعَتِهِ وَهَـٰذَا مِنْ عَدُوِّهِ فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ ﴿١٥﴾

“Na akakuta humo watu wawili wanapigana – mmoja ni katika wenzake na mwingine ni katika maadui zake. Yule aliye katika wenzake akamtaka msaada juu ya adui yake. Musa akampiga ngumi akammaliza.” (28:15).

Musa alihofia kuchukua risala ya Mwenyezi Mungu kwa Firauni asije akamuua kabla kukamilisha lengo, lakini akiwa na nduguye na ikatokewa kuuawa, basi atachukua nafasi yake kuendeleza malengo.

Akasema – Mwenyezi Mungu –sivyo kabisa! Nendeni na ishara yetu, Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni wajumbe wa Mola wa walimwengu wote. Ya kwamba uwaachilie wana wa Israil waende nasi.

Musa alihofia dhiki ya kifua, kufungika ulimi na kuuliwa, lakini Mwenyezi Mungu akamhakikishia usalama na akamwambia kuwa hakuna kitu kitaka- chokuwa katika hayo, kwa sababu mimi nitawasaidia na kuwanusuru. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20: 46 – 47).

Akasema: Je, hatukukulea utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi? Na ukatenda kitendo chako ulichokitenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

Musa na Harun walielekea kwa Firauni, wakaingia kwake wakiwa wamevaa deraya ya sufu, mikononi mwao wakiwa na fimbo. Wakampa mwito wa kumwamini Mungu na kumpa sharti la kusilimu na kutii ili utawala wake ubakie na kudumu enzi yake.

Firauni aliwabeza wawili hawa, waliompa masharti ya kudumu utawala na enzi yake, wakiwa hawana cheo chochote wala mali. Hakutaka kuwaua kwa kuhofia asiambiwe kuwa ameshindwa na hoja akakimbilia upanga.

Lakini Firauni anaweza kuwa na hoja gani? Ni kwa mantiki gani atakayoweza kujadili? Hana kitu isipokuwa kuvungavunga na kumtajia Musa yaliyopita.

Je, hatukukulea na ukakaa nyumbani kwetu miaka, kisha ukatuulia mtu wetu na ukakimbia? Hii ndio shukrani yako? Zaidi ya hayo unadai kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwetu? Unataka tukusikize na kukutii na sisi ndio mabwana zako na wafadhili wa neema zako?

Kisha Firauni akawegeukia watu wa baraza lake na akasema: “Basi mbona hakuvikwa vikukuku vya dhahabu?” (43:53). Kwenye dhahabu tu ndio kuna kuwa na siri ya mantiki ya mataghuti. Hakuna utume wala ubwana au ubora isipokuwa kwa ajili ya dhahabu na dhahabu yenyewe.

Musa (a.s) akamjibu kuhusu kuua akasema: “Nililifanya hilo nikiwa miongoni mwa wasioelewa.”

Yaani sikuelewa kuwa ngumi yangu itamuua. Nami nilikusudia kukinga na kutia adabu, nikakosea makusudio. Basi mimi nina dhambi gani katika hilo? Kukusudia ni nguzo ya msingi ya kosa la jinai kwa watu wa sharia.

Basi niliwakimbia nilipowahofia.

Sikukimbia hukumu ya uadilifu, bali nilikimbia dhulma kwa kuhofia kunichukulia kuwa ni muuaji wa makusudi. Kuna mmoja alimwambia Musa:

إِنَّ الْمَلَأَ يَأْتَمِرُونَ بِكَ لِيَقْتُلُوكَ فَاخْرُجْ إِنِّي لَكَ مِنَ النَّاصِحِينَ ﴿٢٠﴾

“Hakika wakubwa wanashauriana kukuua. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanaokupa nasaha.” (28:20).

Na Mola wangu akanitunukia hukumu na akanijaalia niwe miongoni mwa mitume.

Firauni alimtajia Musa ufukara na utoro; Musa naye akamwambia kuwa utukufu haupimwi kwa mali wala kwa ufalme; isipokuwa uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu, humpatia amtakaye katika waja wake. Na mimi Mwenyezi Mungu amenitunukia elimu ya dini yake na sharia yake kwa njia ya kheri na usawa na akanitukuza kwa kunituma kwako na kwa watu wako.

Musa aliendelea kumjibu Firauni, kuhusu malezi na akasema:

Na hiyo ndiyo neema ya kunisimbulia na wewe umewatia utumwani wana wa Israil?

Yaani unanisimbulia kwa malezi yako kwangu na unajitia kutojua kuwa sababu ni uadui wako wa kuwachinja watoto wa kiume wa watu wangu na kuwatia utumwani watoto wao wa kike? Mama yangu alipohofia wewe kunichinja akanitupa baharini na matokeo yake yakawa ni kuishi mimi mbali ugenini bila ya huruma ya mama na mapenzi ya baba? Hii ndiyo fadhila yako kwangu? Firauni alizibwa mdomo, akaanza kuwatafuta wabatilifu wake; kama utakavyoona katika kifungu kifuatacho.

قَالَ فِرْعَوْنُ وَمَا رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٢٣﴾

23. Akasema Firauni: Na ni nani huyo Mola wa walimwengu wote?

قَالَ رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ ﴿٢٤﴾

24. Akasema: Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.

قَالَ لِمَنْ حَوْلَهُ أَلَا تَسْتَمِعُونَ ﴿٢٥﴾

25. Akawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

قَالَ رَبُّكُمْ وَرَبُّ آبَائِكُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٢٦﴾

26. Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

قَالَ إِنَّ رَسُولَكُمُ الَّذِي أُرْسِلَ إِلَيْكُمْ لَمَجْنُونٌ ﴿٢٧﴾

27. Akasema: Hakika mtume wenu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

قَالَ رَبُّ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُمْ تَعْقِلُونَ ﴿٢٨﴾

28. Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

قَالَ لَئِنِ اتَّخَذْتَ إِلَـٰهًا غَيْرِي لَأَجْعَلَنَّكَ مِنَ الْمَسْجُونِينَ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

قَالَ أَوَلَوْ جِئْتُكَ بِشَيْءٍ مُّبِينٍ ﴿٣٠﴾

30. Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?

قَالَ فَأْتِ بِهِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٣١﴾

31. Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

فَأَلْقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعْبَانٌ مُّبِينٌ ﴿٣٢﴾

32. Akaitupa fimbo, mara ikawa nyoka dhahiri.

وَنَزَعَ يَدَهُ فَإِذَا هِيَ بَيْضَاءُ لِلنَّاظِرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao.

قَالَ لِلْمَلَإِ حَوْلَهُ إِنَّ هَـٰذَا لَسَاحِرٌ عَلِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi, mjuzi.

يُرِيدُ أَن يُخْرِجَكُم مِّنْ أَرْضِكُم بِسِحْرِهِ فَمَاذَا تَأْمُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani?

قَالُوا أَرْجِهْ وَأَخَاهُ وَابْعَثْ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٣٦﴾

35. Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini.

يَأْتُوكَ بِكُلِّ سَحَّارٍ عَلِيمٍ ﴿٣٧﴾

37. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

MAJIBIZANO BAINA YA MUSA NA FIRAUNI

Aya 23 – 37

MAANA

Akasema Firauni: Na ninani huyo Mola wa walimwengu wote?

Ewe Musa! Wewe unadai kuwa ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote; hebu tubainishie jinsi yake na hakika yake huyo Mola?

Akasema: “Ni Mola wa mbingu na ardhi ikiwa nyinyi mna yakini.”

Musa alisema: Mwenyezi Mungu hajulikani isipokuwa kwa sifa zake na athari zake; zikiwa ni pamoja na huku kuumbwa ulimwengu huu wa ajabu katika mpangilio wake na nidhamu yake. Basi fikirini na mzingatie ikiwa mna akili zinazoweza kutambua kuwa nidhamu hii haiwezekani ila kwa uweza wa ujuzi na hekima.

Firauniakawaambia waliomzunguuka: Je, hamsikii?

Yaani mnasikia maajabu hayo. Hatujawahi kusikia haya kwa mababa zetu wa kwanza.

Akasema: Ni Mola wenu na Mola wa baba zenu wa kwanza.

Musa alisema kwa kusisitiza kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa ulimwengu, muumba wenu na muumba wa baba zenu wa mwanzo na pia ndiye muumba wa huyu Firauni mnayemfanya mungu na kumwabudu.

Akasema: Hakika mtume wenu huyu mliyetumiwa ni mwenda wazimu.

Musa ni mwendawazimu katika mantiki ya Firauni, kwa nini? Kwa sababu amesema Firauni si mungu bali ni kiumbe. Mantiki haya ya kifirauni anayo kila anayedai asichokuwa nacho. Yeyote anayedai kuwa na elimu naye ni mjinga, ikhlasi naye ni mhaini au ukweli naye ni mrongo, basi yeye yuko katika mila ya Firauni na desturi yake. Lau atapata wanaomwamini atasema: Mimi ndiye mola wenu au simjui mungu mwingine kwenu zaidi ya mimi; kama alivyosema Firauni.

Akasema: Ni Mola wa mashariki na magharibi na viliomo baina yake, ikiwa nyinyi mna akili.

Musa aliendelea kushikilia msimamo wake kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu. Akaashiria kuchomoza jua na kuchwa kwake, ambapo Firauni hawezi kujasiri kusema kuwa yeye ndiye anayelichomoza jua mashariki na kulipeleka magharibi.

Kwa hiyo alipigwa na butwaa aliposikia maneno haya kutoka kwa Musa; sawa na alivyopigwa na butwaa Namrud kabla yake, pale Ibrahim(a.s) alipomnyamazisha kwa kusema:

فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ ﴿٢٥٨﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi.”

Juz. 3 (2:258).

Firauni alipoishiwa, alikereka, akawa anatoa vitisho naakasema: Kama ukimfanya mungu mwingine asiyekuwa mimi basi bila shaka nitakufanya miongoni mwa wafungwa.

Jela na kutesa ndio silaha pekee ya utawala muovu wa mabavu dhidi ya haki uadilifu na uhuru, tangu zamani. Lakini jihadi ya wakombozi na ukakamavu wao, unaifanya silaha ya mataghuti ishindwe kwenye shingo zao na vifua vyao; kama ilivyoshindwa silaha ya Firauni.

Walisema wa kale: Mwenye kuchomoa upanga wa dhulma atauliwa nao.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

فَكُلًّا أَخَذْنَا بِذَنبِهِ فَمِنْهُم مَّنْ أَرْسَلْنَا عَلَيْهِ حَاصِبًا وَمِنْهُم مَّنْ أَخَذَتْهُ الصَّيْحَةُ وَمِنْهُم مَّنْ خَسَفْنَا بِهِ الْأَرْضَ ﴿٤٠﴾

“Kila mmoja tulimtesa kwa makosa yake. Kati yao wapo tuliowapelekea kimbunga cha changarawe, na kati yao wapo walionyakuliwa na ukelele na kati yao wapo ambao tuliwadidimiza katika ardhi.” (29:40).

Akasema: Ijapokuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?” Akasema: Kilete basi kama wewe ni katika wakweli.

Musa hakuogopa vitisho vya Firauni na akamwambia kwa kujiamini kuwa utanifanya mfungwa hata kama ni mwenye haki, kwa kukuletea dalili isiyo na shaka kwako na kwa mwingine?

Atajibu nini Firauni? Je, amwambie ndio nitakufunga hata kama ni mwenye haki? Hawezi kumwambia hivi, kwa sababu itakuwa ni kukubali ukweli kuwa Musa ni Mtume wa Mola wa viumbe wote na kwamba yeye ni mzushi katika madai yake ya uungu. Kwa hiyo ndio akalazimika kusema lete hiyo dalili kama wewe ni mkweli.

Akaitupa fimbo mara ikawa nyoka dhahiri. Na akautoa mkono wake. Mara ukawa mweupe kwa watazamao. Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi. Anataka kuwatoa katika ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani? Wakasema: Mwache kidogo yeye na ndugu yake, na uwatume wakusanyao watu mijini. Wakuletee kila mchawi mkubwa, mjuzi.

Aya hizi sita zimetangulia katika Juz. 9 (7:107 - 112) zikifanana kiutaratibu, kimpangilio na hata herufi; isipokuwa katika mambo mawili:

Hapa imesemwa: ‘mchawi mkubwa’ na kule ikasemwa ‘mchawi’ hakuna tofauti katika maneno haya isipokuwa kutilia mkazo.

Hapa imesemwa: ‘Akasema kuwaambia wakuu waliomzunguka: Hakika huyu ni mchawi mjuzi,’ na kule imesemwa: ‘Wakasema wakuu wa watu wa Firauni: Hakika huyu ni mchawi mjuzi.’ Tofauti hapa ni kubwa kama inavyojionyesha.

Kwa sababu hapa aliyesema ni Firauni kuwaambia wakuu na kule wakuu ndio waliosema kumwambia Firauni. Sasa je, kuna wajihi gani wa kuunganisha baina ya Aya mbili hizi?

Jibu : Sikupata ishara yoyote ya hilo katika tafsiri nilizonazo, wala sijui sababu yake. Kwa vyovyote iwavyo, jibu ninaloliona ni kuwa Firauni ndiye aliyeanza kuwaambia jamaa zake kuwa huyu ni mchawi; kisha jamaa zake nao wakaanza kuambiana kuwa ni kweli Musa ni mchawi; kama ilivyo kwa wanaoongozwa, wanaigiza kiongozi wao na kutolea ushahidi kauli zake.

Hapo basi hakuna kupingana baina ya Aya mbili. Firauni aliwaambia jamaa zake nao wakamwambia yeye kwa kumwigiza.


4

5

6

7

8

9

10

11

12

13