• Anza
  • Iliyopita
  • 12 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9996 / Pakua: 2650
Kiwango Kiwango Kiwango
UKWELI WA USHIA

UKWELI WA USHIA

Mwandishi:
Swahili

UKWELI WA USHIA

TAMKO LA MUASSASATUR-RASULIL-AKRAM (S.A.W)

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHMA MWENYE KUREHEMU

Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote na sala na salam (rehma na amani) ziwe juu ya muongozaji kwenye njia ya haki na mtoa bishara na taa yenye kuangaza Muhammad na Ahli zake walio watwaharifu. Ama baada, wapinzani na maadui wa madhehebu ya Shia bado wanaendelea kati ya kipindi na kipindi kingine na kazi yao ya kuamsha na kueneza shubha zao na kusambaza maneno yao ya uzushi na yasiyo na ukweli wowote dhidi ya madhehebu ya Ahlul-bayti(a.s) na kwa kufanya hivyo hutarajia ya kuwa huenda wakafanikiwa kuziyumbisha na kuzitia shaka itikadi za watu wenye mustawa mdogo wa kielimu na kuwatoa kwenye itikadi zao za asili.

Lakini ukweli ni kwamba usaidizi wa pekee wa Mwenyezi Mungu mtukufu autoao kwa madhehebu ya haki wakati wote na bila kukoma huwa ni kizingiti na kizuizi kikubwa cha kuyafikia malengo yao hayo.

Pamoja na shubha zote na uzushi wote utolewao na uenezwao dhidi ya Ushia, tunakuta kwamba ukweli na haki daima ni yenye kudhihiri na haifichiki kamwe, na imekuwa ni yenye kudhihiri kupitia mikononi mwa wateule kati ya wafuasi wema ambao wamejitolea nafsi zao kwa ajili ya kuyanusuru madhehebu ya haki ambayo aliyaanzisha Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w .w) tangia kudhihiri na kuchomoza kwa Uislaam.

Na katika uwanja huu kuna vitabu vingi sana vilivyo andikwa na vilivyo madhubuti na vizuri, na kati ya vitabu hivyo ni kitabu kiitwacho (Haqaaiqu ani Shia) kilicho andikwa na mheshimiwa Ayatullahil-udhmaa Sayyid Swadiq Shirazy Mwenyezi (Mungu amrefushie umri) alicho kiandika katika masiku ya ujana wake, na kuthibitisha kwa dalili madhubuti haki na ukweli wa madhehebu ya Ahlul-bayti(a.s) .

Na kitabu hiki kimetofautiana na vitabu vingine na kuvipituka kutokana na umadhubuti pia umakini wa dalili zake na mfumo wake ulio mzuri na madhubuti na mwepesi ambao humfikisha msomaji kwenye kina cha shubha zitolewazo na kubainisha ubatilifu wake kwa njia nyepesi na rahisi na kwa umakini wa hali ya juu kabisa.

Na kauli ya mwisho ni kuwa: Hakika kitabu hiki pamoja na kuwa hajmu yake ni ndogo na ibara zake kuwa nyepesi, ukweli ni kwamba wakati huo huo ni kijitabu chenye faida na chenye undani katika maana, kwa hivyo basi hapana budi na inawapasa waumini wakisome na kukipitia au kuzitwalii bahthi zake na kufaidika na maudhui yake yenye kina na madhubuti, tukimtaraji Mwenyezi Mungu awape tawfiq (awawafikishe) kwa yale ayapendayo na kuyaridhia yeye Muumba subhanah.

1 UKWELI WA USHIA

KUENEZA ITIKADI YA USHIA NI FURSA YA THAMANI SANA KATIKA UMRI WA MTU

YAPANGENI VEMA MAMBO YENU NA WALA MSIYAACHE HORERA [1]

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHMA MWENYE KUREHEMU.

Sifa zote njema zinamstahiki Mola wa viumbe wote na sala na salam ziwe juu ya bwana wetu Muhammad na Aali zake walio watwaharifu, na laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu ya maadui zao wote hadi kitakapo simama kiama.(Mlivyonavyo vitakwisha na vilivyoko kwa Mwenyeezi Mungu ndivyo vitakavyo bakia) [2]

Aya hii ni miongoni mwa aya nyingi za kitabu kitukufu cha Allah na maana yake ni kuwa kila mlicho nacho ni chenye kutoweka na kumalizika bila shaka yoyote, na yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ni yenye kubakia milele. Kwa hakika katika usiku huu mmetekeleza na kusali sala mbili Maghribi na Isha, na Shekh Tusy (Radhi za Allah ziwe juu yake) alifariki na kuiaga dunia kabla ya zaidi y miaka elfu moja iliyo pita, lakini sehemu fulani ya thawabu za sala ya Magharibi na Isha mlizo zisali na kuzitekeleza ataandikiwa yeye, kwa sababu yeye alikuwa ni sababu ya kusaliwa sala hizi, kwani mas'ala mengi, pia Hadithi nyingi zilizo tufikia sisi zimetufikia kupitia kwake na kutokana na juhudi zake,Na mwenye kuwaongoza watu kwenye kheri ni kama mfanyaji wa kheri hiyo (katika thawabu)

Ni watu wangapi walio fanikiwa kusali katika usiku huu wa leo?! Bila shaka yoyote ni mamilioni kadhaa, sasa angalieni kiasi cha thawabu ambazo atazipata Shekh Swaduq kutokana na sala hizi pekee. Si vibaya kueleza kuwa Marhum Shekh Tusy alikuwa na ndugu ambae alifahamika kwa wema wake na kwamba alikuwa ni mtu alie shikamana na dini vema, lakini ndugu yake huyo hakutuachia athari yoyote,(kumbukumbu yoyote) na wote wawili walikuwa ni watoto wa baba mmoja na wakiishi wakati mmoja, lakini mamilioni haya ya thawabu yanamfikia Shekh Tusy kila siku wakati ambapo ndugu yake hapati thawabu hizo, kwa sababu hakuacha athari wala chembe yeyote katika dunia kama alizo ziacha ndugu yake wa tumbo moja.

Na jaribuni kuangalia(fanyeni Taswawwur) ya kuwa baada ya miaka elfu moja tokea sasa ni nani utajo wake utabakia na nani atasahaulika na kuto kumbukwa kabisa, kwa hivyo basi nyinyi mnaweza hivi sasa kufanya mambo au matendo ambayo yatakuwa ndio sababu ya kubakia utajo wenu na mkawa ni wenye kukumbukwa kwa muda wa maelfu kadhaa ya miaka na mkajipatia thawabu zisizo koma na kumalizika na zenye kuendelea milele na bila kukatika.

Kwa hakika Mwenyezi Mungu alikadiria kuwa nchi ya India ibadilike na yote kugeuka na kuwa nchi ya Kiislaam, (yaani watu wake wote wabadilike na kuwa Waislaam), katika siku za usoni, na vizazi vyote vijavyo visilimu, vizazi vitokanavyo na waabudu masanamu, kama vile wenye kuabudu Ng'ombe, panya na wenye kuabudu jua. Kwa mfano kabla ya miaka mia moja iliyopita nchi ya Iran yote ilikuwa ni nchi ya kikafiri na baada ya miaka mia moja ili badilika yote na wakazi wake wote wakawa ni Waislaam wa madhehebu ya sunni, kisha wananchi wake wakaongoka na wengi wao au asilimia kubwa kati yao hivi leo wakawa ni wafuasi wa Madhehebu ya Ahlul-bayti(a.s) , na haya ndio yatakayo tokea katika nchi ya India vilevile, kwa utashi wake Allah.

Na hapa linajitokeza swali moja nalo ni kuwa: Baada ya miaka kadhaa, ni ipi nafasi yenu na dauru lenu katika mabadiliko hayo yatakayo tokea?! Inasemekana kuwa katika nchi ya India kuna zaidi ya watu milioni 600 wenye kuabudu masanamu, sasa ikiwa mmoja wenu atachukua jukumu la kusoma vizuri kitabu kitukufu cha watu wenye kuabudu masanamu kisha baada ya kufanya hivyo akachukua jukumu la kukusanya vijana na mabarobaro ambao ni watoto wa wenye kuabudu masanamu katika nchi ya India na akawafafanulia yaliyomo kwenye kitabu chao kitukufu na akawatolea mihadhara, pia akawakusanya wanafunzi wa vyuo vikuu na walimu, pia wasomi, wabunge, mawaziri na watawala kwa kutumia mantiki ya akili na akasema: Je nyinyi mmekinaika na mafundisho haya yaliyomo kwenye kitabu chenu kitakasifu?!

Na je mnafahamu ya kuwa mambo haya ya kutunga ni sehemu moja wapo ya itikadi yenu ya dini?! Niswadikisheni ya kuwa mmoja wenu anaweza kwa kufanya hivi kuziyumbisha Imani za maelfu miongoni mwao. Nitakutajieni baadhi ya mifano hai kati ya mambo yaliyomo kwenye kitabu chao kitakatifu, na kati ya hayo ni kuwa:Ikiwa mwanamume ataoa mwanamke na baada ya muda mrefu mwanamke yule asifanikiwe kuzaa au asimzalie mtoto na baada ya kuonana na madaktari na kumsisitizia au kumthibitishia ya kuwa mwanamume hana kizazi yaani ni tasa, inajuzu kwa mwanamke yule kulala na ndugu wa kiume wa mumewe ili aweze kupata mtoto mmoja tu na si zaidi, na mtoto yule hunasibishwa na kuambatanishwa na mumewe! Na jambo hili ni lenye kupingwa na nafsi ya kila kiumbe na ghera (wivu) inapinga kitu kama hicho, pia elimu inapinga kitu kama hicho.

Na katika mahala pengine kitabu hicho kitakatifu kina sema: Wakati mwingine hutokea mwanadamu kubadilika na kuwa Mungu kiasi kwamba yeye mwenyewe hahisii hivyo au bila ya yeye kuhisia! Na jambo hili ni jambo la batili na lisilo na maana yoyote kwa kiwango kikubwa.

Hakika kitabu chao hiki kimejawa na mambo ya kutunga na ya batili na ngano zisizo na maana, na anaweza mmoja wenu kuyafuatilia kwa karibu zaidi na kujua idadi yake na kuyaeleza wazi wazi bila kutumia matusi na kejeli. Kwa hivyo basi mas'ala muhimu kabisa katika dunia ni kuwaongoza viumbe, na Mtume(s.a.w.w) alimwambia Imam Amiril-muuminiin(a.s) :Ewe Ali ikiwa Mwenyezi Mungu alie takasika atamuongoza mtu mmoja kupitia kwako ni bora kwako (ni kheri kwako) kuliko vitu vyote vichomozewavyo na jua (vipatavyo mwanga wa jua) .[3]

Na ninakunukulieni kisa kingine, Imepokelewa katika moja wapo kati ya kitabu cha historia nacho ni (Atharul-bilaad wa Akhbaarul-ibaad) ya kuwa mtawala mmoja wa kisunni aliekuwa akitawala Iran alitengeneza muhuri wa chuma na akachonga kwenye muhuri huo Ibara hii (Abubakar wa Omar) na alikuwa akiwaonea na kuwadhulumu Mashia na akiwatawala kwa mabavu pia alikuwa akiwapiga muhuri huo kwenye mapaji ya nyuso zao baada ya kuuchemsha kwa moto, na kitabu hicho kinasimulia ya kuwa baadhi ya Mashia ambao walipigwa mhuri huo kwenye mapaji ya nyuso zao walikuwa hawatoki majumbani mwao kwa muda wote wa maisha yao na hawakutoka wala kuyahama majumba yao kutokana na aibu ya ibara hiyo kwa ndugu zao waumini ambao ni Mashia, na wakihofia masunni wasijekoge kupitia kwao.

Hebu jaribuni kuangalia na kuifikiria hali na mazingira magumu kama hayo wakati huo, lakini pamoja na yote hayo na mazingira hayo magumu na maonevu kama hayo, ugumu wa mazingira kama huu wa hali ya juu, Mashia walikuwa wakisindikiza majeneza ya masunni, hadi hivi leo Iran ikawa ni yenye itikadi ya Ushia, kwani mateso na maonevu yale hayakuwazuia kutekeleza majukumu yao bali waliendelea na juhudi za kuwaongoza waja na likathibiti na kuwa lile walilo litaka.

Na hapana shaka ya kuwa nyinyi nyote mmesikia jina la Allamah Al-majlisiy, kwa hakika alikuwa ni mwanazuoni mkubwa, na baba yake alikuwa ni miongoni mwa maulamaa wakubwa pia, na katika kizazi chake Allamah Al-majlisiy ambae tangu kufariki kwake hadi sasa kumepita miaka 300 walijitokeza wanazuoni na maulamaa wengi na marajiut- taqlidi na waandishi wa vitabu wakubwa na watoa mawaidha kwa watu, illa tunakuta kuwa babu wa juu kabisa wa Allamah alikuwa ni mfuasi wa madhehebu ya sunni, na vijana wa kishia wa Isfahani waliweza kumkinaisha na yeye kuamua kujiunga na madhehebu ya Shia, pamoja na kuwa zama zile zilikuwa na taasubi kubwa kabisa ya kimadhehebu, lakini ukweli ni kuwa vijana wale walikuwa na hima ya hali ya juu na wakaweza kuwafanya mashia vijana wengine wa kisunni. Nanyi ni juu yenu kufanya kama walivyo fanya waumini na wapigana jihadi hao, na ni wajibu juu yenu kwa ajili ya kulifikia na kulithibitisha lengo hilo au malengo hayo, kwanza kabisa mjifunze vema na muwe ni miongoni mwa maulamaa wakubwa ili muweze kufanya mahojiano na majadiliano na kuwakinaisha.

Na sikilizeni kisa hiki ambacho kilitokea kabla ya miaka arobaini iliyo pita. Wakati huo tulikuwa Karbalaa, jarida moja la wakati huo liliandika ya kuwa mwanazuini mmoja wa kisunni amekuwa Shia, na walipo muuliza kwa nini umebadilisha madhehebu yako? Akasema: Nimebadilisha kwa sababu ya herufi moja kati ya herufi za jarri iliyotajwa katika Qur'an tukufu! Wakamuuliza ni herufi ipi hiyo?

Akawajibu: Hakika mimi nimesoma Qur'ani mara nyingi sana na mara ya mwisho suratul-fatiha ikanifanya nisite na kusimama katika aya ya mwisho ya sura hiyo, na nilipo anza kusoma suratu (Inna fatahnaa laka fathan mubiinaa) hadi nikafika mwisho wa surat (Muhammad rasulullah walladhina maahu.) na ambayo inamaanisha maswahaba wa Mtume rehma na amani ziwe juu yake, na kuona ya kuwa sura inawazungumzia maswahaba wa Mtume na imewataja mara kumi kwa swigha ya jam'u (mfumo wa wingi) au kwa dhamiri za wingi ambazo d hamiri hizo zinawakusudia wao, lakini sura hiyo inapozungumzia ya kuwa malipo na jazaa zao walizo ahidiwa kuwa ni pepo na msamaha na malipo makubwa inasema:(Mwenyezi Mungu amewaahidi wale ambao wameamini na wa kafanya amali njema miongoni mwao)

Kwa hivyo basi herufi ya (Mim) inamaana ya (Baadhi), na herufi hii ilinifanya nifikirie na kujiuliza: Kwa nini Maswahaba wote hawaingii peponi kama tulivyo fundishwa?

Nikajisemea moyoni mwangu: Niwajibu niende na kufanya utafiti na udadisi kuhusu suala hili, na jambo hilo likanipa picha ya kuwa inawezekana suala hili likawa ni miongoni mwa mifumo ya Qur'an, lakini mimi nimeiona aya hii na kuikuta ikiwa wazi kabisa kwani herufi hiyo inamaana ya (Baadhi) ya (Maswahaba) na (sio wote) laa sivyo hakika Qur'an imewataja wote katika aya nyingi tofauti na katika aya hii, kwa hivyo nadharia ya uadilifu wa Maswahaba ikiwa imetenguka kwangu, na utafiti wangu ukanifikisha katika natija hii ya kuwa hawa (Baadhi) ya walio tajwa ni wafuasi wa Ali bin Abi Twalib (a.s) na wale walio shikamana na wilaya (utawala) yake na kutokana na utafiti huo nikawa Shia.

Kwa hivyo basi ni juu yenu kuyaandaa vema mambo yenu, na fanyeni juhudi kubwa na wala msipoteze fursa hii ya umri wenu, na someni vizuri na mtwalii sana (someni sana vitabu mbali mbali) mpaka muwe ni miongoni mwa watu wenye elimu, kwani watu wa batili hawana elimu na kila walicho nacho ni njozi za mashetani.

Imam Swaadiq (a.s) amesema: Ni juu yako kuwa na vijana (wenye umri mdogo) hakika wao ni wepesi sana kuelekea kwenye kila la kheri[4]

Na Al-ahdaath walo tajwa kwenye hadithi ni kizazi kipya, kwani vijana bado akili zao hazija oshwa, na wao ni wepesi zaidi katika kufanya kheri kuliko wengine. Kwa hivyo fanyeni harakati na nashati ili India na ulimwengu wote wawe ni Mashia watupu..insha allah.

2 UKWELI WA USHIA

WAOKOENI WATU KUTOKANA NA UJINGA UPOTOVU NA DHULMA KAMA IMAM HUSEIN (A.S) ALIVYO WAOKOA [5]

MANENO YA MHESHIMIWA AYA TULLAHIL-UDHMAA IMAM SAYYID SWADIQ SHIRAZIY (Mungu amzidishie umri) ALIYO YATOA KWA MNASABA WA KUMBUKUMBU ZA ASHURA SIKU ALIYO UWAWA SHAHIDI SAYYID SHUHADAA IMAM HUSEIN (A.S)

Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma mwenye kurehemu. Sifa zote njema na himidi ni za Mola wa viumbe wote na sala na salam ziwe juu ya Mtume wake alie muaminifu Muhammad(s.a.w.w) na Aali zake watwaharifu na laana iwe juu ya maadui zao wote. Ama baada, hakika Mwenyezi Mungu alie takasika alitaka kwa kufa shahidi Imam Hussein (a.s) kuweka mazingatio, kilio, ibra na kigezo kizuri, si kwa kizazi kilicho fuatia baada yake pekee, bali hata kwa Mitume na Manabii(a.s) ambao Imam Hussein alikuja baada yao(a.s).

Ama kuhusu mazingatio na kilio, kwa hakika alianza kutekeleza mambo hayo Muumba wa viumbe pale alipo muumba Adam(a.s) kwani Jibrilu alimtajia(a.s) watwaharifu watano ambao ni Muhammad, Ali, Fatima, Hassan, Hussein(a.s) na Adam akamwambia: Nina nini mimi kila ninapo mkumbuka Hussein macho yangu hutokwa na machozi, kisha kuamsha huzuni na majonzi yangu, na Mwenyezi Mungu mtukufu akamuambatanisha pamoja na manabii katika visa vyao kupita kwao katika ardhi tukufu ya Karbalaa na matatizo waliyo kumbana nayo katika ardhi hiyo, na hali hiyo ikaendelea katika muda wote mpaka Imam Hussein aliposema(a.s)

(Mimi ni muuliwa mwenye Ibra (mazingatio) hanikumbuki muumini yeyote isipokuwa hulia). Ama kuwa kwake ni mazingatio na kigezo, kwa hakika Imam Swadiq(a.s) aliashiria katika ziyara yake aliyo msomea babu yake Hussein(a.s) siku ya kumbukumbu ya Arobaini ya Imam Hussein huku akimzungumzia Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kumuashiria Hussein(a.s) : Na akajitolea damu yake katika njia yako ili awaokoe waja wako kutoka katika ujinga na utata wa upotovu (njia ya upotovu).

Na waja hapa: Haimaanishi kikundi fulani, au umma fulani, au kizazi fulani. Na Kuokoa: Ni kuashiria kwenye mambo waliyo tihaniwa nayo watu wale. Na bado mtihani huo upo. Kama kutumbukia katika mabalaa ya aina tofauti na mambo ya kila aina ambayo msingi wake ni ujinga na upotovu. Na Kubabaika: Ambako kumewakumba watu wengi katika mwendo mzima wa maisha yao na mwisho wao (yaani akhera yao). Hizi ndio nukta ambazo zinaunda sehemu fulani kati ya malengo ya Imam Hussein(a.s) katika kauli zake na matendo yake katika historia ya Ashura.

Ni uzuri ulioje kwa waumini kila mahala walipo na kila mmoja wao kusimama na kutekekeza jambo hilo la kheri katika nyanja mbali mbali. Na kufanya awezalo kulifanya kama kufanya maandalizi ya kuwafikishia walimwengu wote habari zihusianazo na upande wa kufanya mazingatio na kulia kwa ajili ya Imam, kwa kufanya majlisi ya kumbukumbu za kufa shahidi kwa Imam Husein na kudhihirisha alama na shiari za Imam Hussein ambazo ndio kitu cha kuendeleza na kudhihirisha alama na shiari za Mwenyezi Mungu alie takasika, na kwa hakika Qur'an tukufu amelisifia jambo hili kuwa ni katika uchaji wa Mwenyezi Mungu

Na haya ndio ambayo yaliifanya hali ya kulia kwa mfazaiko kusiko kwa kisheria na kuliko kemewa kisheria katika misiba yote, liwe ni jambo lenye kusifika na kuamrishwa kulifanya na kupewa malipo juu ya jambo hilo ikiwa litafanyika kwa ajili ya Ashura, na katika njia ya bwana wa mashahidi Imam Husein(a.s).

Na haya ndio mazingatio na kilio vitu viwili ambavyo vimekuwa mutawaatir na mashuhuri na kupokelewa kwa wingi kutoka kwa Watu wa nyumba ya utume na ujumbe wa Allah (a.s) hadi macho yao yakapatwa na vidonda, na kuhusiana na hilo Imam Ridhaa(a.s) amesema katika hadithi iliyo pokelewa kutoka kwake na Rayyaan bin Shabiib ya kuwa:

(Hakika siku ya Husein Imeyatia vidonda macho yetu)([6] ) . Na haya ndio yaliyo sababisha kutokwa machozi macho yale matwaharifu ya walii mtukufu wa Mwenyezi Mungu Imam Mahdi mwenye kusubiriwa (rehma za Mwenyezi Mungu zowe juu yake na Mwenyezi Mungu aharakishe kudhihiri kwake na faraja yake tukufu) kama ilivyo pokelewa katika ziara ya (An-nahiyatul-muqaddasa):

(Na kwa hakika nitakulili damu badala ya machozi). Na kuhusu mazingatio na kigezo, mambo ambayo Imam Husein(a.s) aliyatangaza na kuyadhihirisha mara kadhaa wa kadhaa tangu alipotoka katika mjiwa wa babu yake Mtume wa Mwenyezi Mungu na kuyarudia katika mji mtukufu wa Makka, na katika muda wote alipokuwa njiani akielekea Karbalaa tukufu, na katika Karbalaa, na katika Usiku wa Ashura, na siku ya Ashura, katika hotuba yake barua zake na maneno yake mbali mbali, na kupitia muamala wake katika mwendo huu wa ushindi, na mazingatio yale ni kusimama kidete kwa kufanya juhudi kubwa kwa ajili ya kuwatenga pia kuwaepusha watu wote na ujinga na upotovu.

Na haliwezi kuthibitika hilo isipokuwa kwa kufanya juhudi kubwa na kuwa na ikhlaas kwa ajili ya Mwenyezi Mungu alie takasika. Na kujitolea muhanga kwa kiwango kikubwa na cha hali ya juu katika njia ya kuwaelimisha watu na waja wa Mwenyezi Mungu mtukufu, na kuieneza nuru ya Ahlul bayti(a.s) kila upande na kila mahala na katika kila mji na kijiji, na katika kila nyumba na vibanda vya makuti, na kuifikisha kwa kila mtu wanamume kwa wanamke, mabinti kwa vijana.

Na kutekeleza mfumo na mwenendo wa Imam Husein(a.s) katika kuitumia Ashura kwa ajili ya kuwaokoa waja wa Mwenyezi Mungu mtukufu kutokana na dhuluma na mauaji yaliyopo katika zama hizi, umwagaji wa damu, na kuonekana kuwa ni kikundi kidogo chenye kufuata batili na kuadhibiwa, na kudharauliwa kwa mambo matukufu ambayo watu wengi katika siku hizi wamekuwa wakiyavunjia heshima yake, na hasa hasa waislaam katika sehemu tofauti za Ardhi hii.

Na kwa ajili ya kueneza misingi ya Uislaam na matawi yake. Kupitia vyombo vyote vya habari na tabligh. Katika nyanja mbali mbali za maisha. Na Mwenyezi Mungu ndie mwenye kuombwa msaada awawafikishe wote kupata mazingatio haya na kigezo hiki, na awawafikishe kupata mazingatio pia kutokwa na machozi, nae ndie mwenye kutegemewa.

3 UKWELI WA USHIA

SISI SI KATIKA MASHIA WA ALI (A.S) IKIWA HATUKUZIHESABIA NAFSI ZETU KILA SIKU [7]

MIONGONI MWA MANENO YA MHESHIMIWA AYATULLAHIL-UDHMAA SAYYID SWADIQ SHIRAZIY(Mwenyezi Mungu amzidishie umri)

Hakika Amirul-muuminiin Imam Ali bin Abi Twalib(rehma za Allah ziwe juu yake) alikuwa na orodha ya majina ya watu fulani wanaume kwa wanawake na orodha hiyo ikiwa imeandikwa juu yake (Si katika sisi), na kwa hakika Amirul-muuminiin aliwasifia na kuwaelezea watu hao ya kuwa watu hao ni miongoni mwa watu ambao hawakuzihesabia nafsi zao na wala hawakuya angalia matendo yao).

Kwa hivyo basi muumini yeyote akitaka asiwe katika hawa ni juu yake kila usiku unapo ingia aweke angalau dakika tano maalum, na katika dakika hizo ayarejee matendo yake yote aliyo yatenda katika siku ile, je yalikuwa ni matendo mazuri ? na akiyakuta matendo yake aliyo yatenda ni mazuri basi amshukuru Mwenyezi Mungu alie takasika juu ya hilo, na ikiwa matendo yake ni mabaya, basi amuombe Mwenyezi Mungu alie takasika msamaha na aazimie ya kuwa hatorudia tena kufanya matendo hayo.Kwani Imam Kaadhim(a.s) anasema:

(Si katika sisi mtu ambae haihesabii nafsi yake katika kila siku, akifanya mema humuomba Mwenyezi Mungu amuwafikishe kutenda mema zaidi, na akifanya maovu humuomba Mwenyezi Mungu msamaha kutokana na maovu hayo na kurejea kwake)[8] .

Hakika kila mtu anatabia maalum na ana matakwa maalum, kwa hivyo maisha yanapo mzonga na matatizo ya kimaisha kumtatiza, basi tabia yake hubadilika na kuwa mbaya, kwa hivyo Qur'ani tukufu na Ahlul-bayti(a.s) wamesisitiza na kusema ya kuwa mtu mwenye tabia njema ataingia peponi ama mtu mwenye tabia mbaya kwa hakika mtu huyo ataingia motoni.

Imepokelewa katika riwaya ya kwamba mwanamke mmoja katika zama za Mtume(s.a.w.w) tangu asubuhi hadi jioni alikuwa akijishughulisha na ibada bila kupumzika, na katika masiku mengi ya mwaka alikuwa akifunga, lakini mwanamke huyo alikuwa na kasoro moja, nayo ni kuwa tabia yake ilikuwa ni mbaya na alikuwa akimuudhi jirani yake kwa ulimi wake mbaya, Mtume(s.a.w.w) akasema kuhusina na mwanamke huyo: (Hakuna kheri yoyote kwa mwanamke huyo, yeye ni mtu wa motoni)([9] ) Kwa hivyo ni juu ya kila mtu kufanya juhudi kwa ajili ya kujipamba na tabia njema kati ya jamaa zake, watu wake wa karibu, majirani zake na watu walioko pembezoni mwake. Hakika Mwenyezi Mungu anampenda mtu mwenye kutoa huduma na ambae anawasaidia watu na kutatua matatizo yao.

Ninawausia wanaume kwa wanawake usia mbili: Usia wa kwanza, Mkumbukeni Imam Husein(a.s) wakati wote, kuomboleza kifo cha Imam Husein ni tawfiki ya Mwenyezi Mungu ambayo huipata Muumini, na maombolezo hayo huwa ni wasila na nyenzo ya kutatua matatizo yote ya kidunia, kwa hivyo basi ni wajibu kuwe na vikao vya kila wiki kwa ajli ya kukumbuka mauaji ya Imam Husein(a.s) katika majumba yenu.

Na ninakumbuka ya kuwa kulikuwa na mtu mmoja alikuwa akija kumtembelea marehemu kaka yangu, na kaka yangu kama ada yake anapokutana na waumini alikuwa daima akimhimiza na kumsisitizia kuweka vikao na kufanya majlisi za kumkumbuka za Imam Husein katika nyumba yake, na bwana yule alikuwa akitoa udhuru ya kuwa nyumba yake ni ndogo na haitoshi kuweza kufanya hivyo kwa sababu nyumba yake ina chumba kimoja chenye ukubwa wa mita kumi na mbili tu, Marehemu Imam akamwambia:

Fanya majlisi katika chumba hicho kila wiki kwa muda wa saa moja. Yule bwana akaitikia wito na kufanya vile na kutokana na baraka za vikao vya kila wiki alivyo kuwa akivifanya katika chumba kile kidogo, na akisomea kwenye chumba hicho maombolezo ya msiba wa Imam Husein(a.s) , baadae bwana yule akawa ni katika wafanya biashara wakubwa kabisa kiasi kwamba akawa ni mwenye kumiliki majumba na akawa ni mwenye kumiliki vitu vingi visivyo kuwa na hesabau ( yaani akawa tajiri mkubwa).

Ama usia wa pili ni kutekeleza usia wa Imam Swadiq(a.s) kwa Mashia (wafuasi) wake ambao alisema katika usia huo:

Ni juu yenu enyi ndugu zangu waumini kuzitilia umuhimu itikadi za vijana na kufanya juhudi kubwa katika kuzirekebisha na kuziweka sawa zisiyumbe, na ziimarisheni dhidi ya watu wa batili na itikadi za batili na mbaya.

Fanyeni juhudi ya kufuatana nao na kuwa nao wakati wote mnapokwenda katika vikao vya Imam Husein(a.s) , na wasikilizieni na muwafahamishe pia muangalie ni kitu gani wanacho fikiria na vipi wanafikiri, na wala msikabiliane nao kwa ukali na msiwafanyie ugumu, ikiwa mtaweza kujibu ishkali na maswali yao basi jambo hilo ni zuri sana, laa sivyo fuataneni nao kwa mtu anae weza kujibu mswali yao na kubatilisha ishkali zao, kwa mfano katika zama za Mtume mtukufu(s.a.w.w) na katika zama za maima watwaharifu(juu yao sala na sala zilizo bora kabisa) vijana wengi waliongoka katika itikadi zao na tabia zao, na Abu dharri alikuwa ni mmoja wa vijana hao, kwani Abu dharri alikuwa ni mshirikina lakini alisilimu na kuamini na akawa ni mtu mwenye kupigiwa mfano na akawa mfano mwema na wa aina ya pekee, na Bwana Othumani bin Affan alifanya kile kitendo cha kumfukuza na kumpekeleka kaskazini mwa nchi ya lebanoni ili asiufedhehi utawala wake na asieneze fadhila za Ahlul-bayti(a.s) , lakini Aba Dharri kwa maneno yake na ushupavu wake na tabia yake aliweza kuwaongoa vijana wengi sana wa miji ile ambao baadae wakawa ni miongoni mwa watu wenye kuwatawalisha Ahlul-bayti(a.s) na wao wakaweza kuueneza Ushia katika miji ya Jabal Aamil na kaskazini mwa Lebanoni hadi hivi leo.

Na nyinyi mtokao katika mji wa Isfahani.. je mnafahamu ya kuwa Allamah Al-majlisiy alie zikwa katika mji wenu wa Isfahani babu yake wa juu kabisa hakuwa ni Shia?! Lakini kijana wa kawaida wa kishia aliweza kumkinaisha babu yake juu ya ukweli wa Ushia na itikadi ya Ahlul-bayti na Allamah Al-majlisiy akawa ni Shia mwenye Kuwatawalisha Ahlul-Bayti? Na sisi Mashia bado tunafaidika na Athari zake na elimu zake pia vitabu vyake mbali mbali, na huenda nyinyi nyote mmesikia kitabu chake cha riwaya kilicho kikubwa (Buharul-anwaar) ambacho alikusanya ndani yake maneno mazuri na maneno ya Maimam watwaharifu yenye nuru (rehma za mwenyezi Mungu ziwe juu yao wote).

Kwa hivyo ni juu yetu, enyi ndugu waumini, tuwe kama kijana yule ambae aliongoka kupitia kwake babu yake Allamah Al-majlisiy, hadi tuweze kuwapata watu mfano wa Allamah Al-majlisy. Ni juu yetu kuwangoza viumbe na hasa vijana miongoni mwao ili Ushia ubakie ukiwa ni wenye nguvu na ukiwa imara na wafuasi wake wawe ni wenye kuongezeka siku hadi siku. Na mwisho ninakuombeeni tawfiq na kila la kheri na namuomba Mwenyezi Mungu ayakubali matendo yenu na msitusahau katika dua zenu.

4 UKWELI WA USHIA

KUSUJUDU JUU YA UDONGO

SAMI : Ewe Ali kwa hakika nyinyi Mashia mnamshirikisha Mwenyezi Mungu, kwa kusujudu kwenu juu ya udongo, je udongo huo sio kiasi kidogo cha udongo ulio kauka mnao uabudu kinyume cha Mwenyezi Mungu?

ALI: Niruhusu nikuulize swali moja.

SAMI: Bila wasi wasi wowote uliza.

ALI : Je ni wajibu kusujudu juu ya kiwiliwili cha Mwenyezi Mungu mtukufu? SAMI: Hakika kauli yako hii ni kufru, kwa sababu Mwenyezi Mungu hana kiwiliwili, haonekani kwa macho, wala haguswi kwa kiwiliwili, na mwenye kuitakidi ya kuwa Mwenyezi Mungu ana kiwiliwili basi yeye ni kafiri. Hakika sijda ni wajibu ifanyike kwa ajili ya Mwenyezi Mungu pekee, yaani lengo la kusujudu na kunyenyekea inabidi liwe ni Mwenyezi Mungu alie takasika, ama kusujudu juu ya Mwenyezi Mungu hiyo ni kufru (huo ni ukafiri).

ALI : Kutokana na maneno yako haya imethibiti kuwa kusujudu kwetu juu ya udongo si shirki, kwa sababu sisi tunasujudu juu ya udongo, si kwamba tunausujudia udongo. Na tujaalie jambo lililo muhali ya kuwa, lau kama tunge kuwa tunaitakidi kwa mfano ya kuwa udongo ndio (Mwenyezi Mungu) basi ilikuwa ni lazima kuusujudia, si kusujudu juu yake, kwa sababu hakuna mtu yeyote anaesujudu juu ya Mola wake.

SAMI : Hakika ni mara ya kwanza kwangu kusikia uchambuzi kama huu, na kwa hakika ni uchambuzi ulio sahihi, kwani lau kama nyinyi mnge kuwa mnauzingatia (Udongo) kuwa ni Mungu msinge sujudu juu yake, na kusujudu kwenu juu yake ni dalili ya kuwa ninyi hamuuzingatii udongo huo kuwa ni Mungu. SAMI: Basi niruhusu nikuulize swali.

ALI : Uliza.

SAMI: Basi ni sababu ipi iwafanyayo muendelee kusujudu juu ya udongo kwa wakati wote, na kwa nini hamsujudu juu ya vitu vingine, kama mnavyo sujudu juu ya udongo?

ALI: Kuna hadithi tukufu iliyo pokelewa kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kwa makubaliano ya madhehebu zote za Waislaam ya kuwa Mtume(s.a.w.w) alisema:

(Kwa hakika ardhi imefanywa kwangu iwe ni mahala pa kusujudia na mahala pa kujitwahirishia)[10] Kwa hivyo basi udongo halisi ndio ambao inajuzu kusujudu juu yake kwa makubaliano ya makundi yote ya Waislaam, kwa sababu hiyo sisi wakati wote husujudu juu ya udongo ambao waislaam wote wamekubaliana juu ya kuwa inajuzu kusujudu juu yake.

SAMI : Wamekubaliana vipi Waislaam wote juu ya jambo hilo?

ALI: Mwanzo kabisa alipo kuja Mtume(s.a.w.w) katika mji wa madina, na kujenga msikiti katika mji huo, je msikiti huo ulikuwa umetandikwa kwa mazulia?

SAMI: Hapana.. haukuwa umetandikwa kwa mazulia.

ALI: Basi Mtume(s.a.w.w) na Waislaam walikuwa wakisujudi juu ya nini?

SAMI : Walikuwa wakisujudu juu ya ardhi yenye udongo au mchanga.ALI : Kwa hivyo sala zote za Mtume(s.a.w.w) zilikuwa zikifanyika juu ya ardhi, na alikuwa akisujudu juu ya udongo, vile vile Waislaam katika zama zake na baada yake walikuwa wakisujudu juu ya udongo. Kwa hivyo kusujudu juu ya udongo bila shaka yoyote ni jambo lililo sahihi, na kwa maana hiyo sisi tunasujudu juu ya udongo kwa kufuata sira na sunna ya Mtume na kwa kufuata nyendo za Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , na kwa maana hiyo sala zetu bila shaka ni sahihi

SAMI : Basi nyinyi Mashia kwa nini hamsujudu juu ya kitu kingine tofauti na udongo muuchukuao na kuubeba pamoja nanyi kutoka katika ardhi nyingine, au kwa nini hamsujudu kwenye udongo mwingine?

ALI : Kwanza kabisa: Mashia wanasema kuwa inajuzu kusujudu juu ya kila ardhi sawa iwe ni ile iliyo shikamana na kuwa kama jiwe au mchanga. Pili: Nisharti sehemu ya kusujudia iwe twahara, yaani isiwe na najisi, kwa hivyo basi haijuzu kusujudu juu ya ardhi iliyo najisika, au mchanga usio twahara, kwa maana hiyo ndio maana tunabeba kipande cha udongo mkavu ulio twahara, na kwa kufanya hivyo tunaepukana na hali ya kusujudu juu ya udongo ambao hatujui ya kuwa ni twahara au laa. Na kwa kuongezea ni kuwa, sisi tunasema kuwa inajuzu kusujudu juu ya udongo wa ardhi au ardhi ambayo hatujui kuwa ni najsi au laa.

SAMI : Ikiwa kwa kufanya hivyo mnataka kusujudu juu ya udongo halisi ulio twahara.. kwa nini hambebi mchanga ili muweze kusujudu juu yake?ALI : Kwa sababu kubeba mchanga husababisha kuchafuka kwa nguo, kwani mahala popote utakapo wekwa katika nguo nilazima nguo hiyo itachafuka, kwa sababu hiyo sisi huuchanganya na kiasi fulani cha maji kisha tunauacha ukauke, ili tunapo ubeba usisababishe kuchafuka kwa nguo.

Kisha kusujudu juu ya kipande cha udongo ulio kauka kuna dalili zaidi juu ya unyenyekevu na khushui kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mtukufu. Hakika sijda ndio mwisho wa unyenyekevu, kwa sababu hiyo haijuzu kukisujudia kitu kingine tofauti na Mwenyezi Mungu alie takasika. Kwa hivyo basi ikiwa lengo la kusujudu ni kwa ajili ya kumnyenyekea Mwenyezi Mungu, kila sijda ambayo itakuwa ni yenye kuonyesha na kudhihirisha unyenyekevu zaidi, hakuna shaka yoyote kuwa itakuwa ni nzuri sana.

Kwa ajili hiyo imekuwa ni sunna sehemu ya kusujudia iwe chini zaidi kuliko sehemu ya mikono na miguu, kwani kufanya hivyo ni dalili zaidi juu ya unyenyekevu kwa Mwenyezi Mungu mtukufu. Na vilevile ni sunna kuipakaza pua kwa udongo wakati wa sijda. Kwa sababu kufanya hivyo kuna dalili zaidi juu ya unyenyekevu na khushuu'i kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Kwa maana hiyo kusujudu juu ya ardhi, au juu ya kipande cha udongo ulio mkavu ni vizuri zaidi kuliko kusujudu juu ya vitu vingine tofauti na vitu viwili hivyo kati ya vitu ambavyo inajuzu kusujudu juu yake, kwani kufanya hivyo ni kuweka sehemu ya mwili iliyo tukufu zaidi- ambayo ni paji la uso- juu ya ardhi- kwa ajili ya kumnyenyekea Mwenyezi Mungu mtukufu na kudhalilika mbele ya utukufu wake Mwenyezi Mungu.

Ama mwanadamu-katika hali ya sijda- kuweka paji lake la uso juu ya zulia lenye thamani ya juu na lililo tengenezwa na kupambwa kwa madini kama Fedha, Akiki, Dhahabu na mengineyo, au juu ya nguo yenye thamani kubwa. jambo hilo ni kati ya mambo yanayopunguza hali ya unyenyekevu na khushuu 'i, na huenda kufanya hivyo kukapelekea kuto dhalilika mbele ya Mwenyezi Mungu mtukufu.

Kutokana na hayo je inawezekana kusujudu juu ya kitu kinacho mzidishia mtu unyenyekevu mbele ya Mola wake kikazingatiwa kuwa ni shirki na kufru? Na kusujudu juu ya kitu kinacho ondoa unyenyekevu kwa ajili Mwenyezi Mungu mtukufu kikazingatiwa kuwa ni kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu? Hakika hiyo si jambo lingine bali ni kauli ya uzushi na uongo.

SAMI : Basi ni maneno gani haya yalipo juu ya udongo ambao mnasujudu juu yake?

ALI: Kwanza kabisa: si kweli kuwa sehemu zote za udongo huo zimeandikwa juu yake, kwa hakika kuna udongo mwingi ambao haukuandikwa hata herufi moja. Pili: Udongo ulio andikwa katika upande fulani ni udongo ulio chukuliwa katika ardhi tukufu ya Karbalaa.[11] [2] je katika hilo kuna shirki? Na je hilo linautoa udongo huo katika hukumu ya kujuzu kusujudu juu yake? Hapana kamwe.

SAMI : Je udongo wa ardhi ya(Karbalaa) unakhususiya gani kwani tunawaona Mashia wengi wanajifunga tu na kusujudu juu ya udongo huo vyovyote itakavyo kuwa?

ALI : Sababu ya kufanya hivyo ni kuwa imepokelewa katika Hadithi tukufu:

(Kusujudu juu ya udongo wa kaburi la Husein kunavuka vizuizi saba)[12] Yaani kusujudu juu ya udongo huo kunapelekea kukubaliwa kwa sala, na sala hiyo kupanda kwa Mwenyezi Mungu mtukufu juu ya mbingu saba. Na haikuwa hivyo isipokuwa ni kwa kufahamu ubora wa udongo huo, ubora ambao haupatikani katika udongo mwingine tofauti na udongo mtukufu wa Karbalaa.

SAMI : Je kusujudu juu ya udongo wa kaburi la Husein kunaifanya sala iwe ni yenye kukubaliwa mbele ya Mwenyezi Mungu mtukufu hata kama sala hiyo itakuwa batili?

ALI : Mashia wanasema kuwa sala ambayo haikutimiza masharti ya kusihi kwake ni batili, haikubaliwi. Lakini sala iliyo timiza masharti yote ya kusihi kwake ni yenye kukubalika mbele ya Mwenyezi Mungu, na huenda isikubaliwe, kwa maana kuwa hapewi thawabu mtu kwa sala hiyo, kwa hivyo sala iliyo saliwa juu ya udongo wa kaburi la Imam Husein ikiwa ni sahihi, hukubaliwa na kupewa thawabu juu ya sala hiyo, kwa hivyo basi kusihi ni kitu, na kukubaliwa kwa sala ni kitu kingine.

SAMI : Je ardhi (tukufu ya Karbalaa) ni tukufu zaidi kuliko ardhi yote hata ardhi ya Makka na Madina, hadi kusujudu juu yake kuwe bora?

ALI: Kuna kizuizi gani katika hilo?

SAMI: Hakika udongo wa(Makka tukufu) ambao tangu kutelemka kwa Adam(a.s) bado ni ardhi ya Kaaba, na ardhi ya (Madinatu- lmunawwarah) ardhi ambayo ndani yake kunakiwiliwili cha Mtume mtukufu(s.a.w.w) zinakuwa na daraja la chini zaidi kuliko daraja la ardhi ya Karbalaa? Hili ni jambo la ajabu! Na je Husein bin Ali ni bora kuliko babu yake Mtume wa Mwenyezi Mungu?

ALI: Hapana. hakika utukufu wa Husein ni chembe ndogo ya utukufu wa Mtume(s.a.w.w) , na utukufu wa Husein ni sehemu ndogo ya utukufu wa Mtume(s.a.w.w) , na nafasi ya Husein mbele ya Mwenyezi Mungu mtukufu si kwa ajili ya jambo lingine bali ni kwa sababu ya kuwa yeye ni Imam alie fuata dini ya babu yake Mtume wa Mwenyezi Mungu hadi kufa shahidi katika hilo. Hapana, daraja ya Husein si chochote isipokuwa ni sehemu ndogo tu ukilinganisha na daraja ya Mtume(s.a.w.w). Lakini.. kutokana na ukweli kuwa Husein aliuliwa yeye na Ahli-bayti wake, na answari wake katika njia ya kuusimamisha Uislaam, na kuimarisha kanuni zake, na kuulinda usichezewe na watu wenye kufuata matamanio ya nafsi zao, Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kufa kwake shahidi alimpa badala yake mambo matatu:

1-Kujibiwa kwa maombi chini ya kuba la kaburi lake.

2-Maimamu kutokana na kizazi chake.

3- Udongo wa kaburi lake kuwa ni dawa na tiba ya maradhi mbali mbali.

Kwa hivyo Mwenyezi Mungu akautukuza udongo wa kaburi lake kwa sababu yeye aliuwawa katika njia yake kwa mauaji yaliyo mabaya sana na ya kikatili, na wanawake wake wakachukuliwa mateka,, Maswahaba wake kuuwawa, na mabalaa mengi tofauti na hayo yaliyomfika kwa ajili ya dini..je katika hilo kuna kizuizi chochote? Na je kuufadhilisha udongo wa Kaarbalaa juu ya udongo wa sehemu nyingi ya ardhi hata juu ya ardhi ya Madina maana yake ni kuwa Husein(a.s) ni bora kuliko Mtume(s.a.w.w) ? bali suala ni kinyume chake. Kwani kuutukuza udongo wa kaburi la Husein ni kumtukuza Husein, na kumtukuza Husein(a.s) ni kumtukuza Mwenyezi Mungu na Mtume wake(s.a.w.w).

SAMI : Haya ni kweli, na mimi nilikuwa nikidhania ya kuwa mnamfadhilisha Husein(a.s) hata kuliko Mtume(s.a.w.w) , na hivi sasa nimefahamu ukweli kuhusu suala hili, na ninakushukuru kwa maneno yako haya mazuri ambayo umenifahamisha na kunizindua kwayo, na wakati wote nitachukua na kubeba kipande cha ardhi tukufu ya Karbalaa ili nikitumie kusujudu juu yake popote nitakapo kwenda kusali.. kama ambavyo nitaacha kusujudu juu ya kitu chochote mfano wa zulia na madini.

ALI : Kwa hakika mimi nilitaka kukubainishia ya kuwa tuhuma hizi zielekezwazo kwetu sisi Mashia, hazina ukweli wowote, bali ni uongo mtupu ulio pangwa na kuelekezwa kwetu na watu waovu kati ya maadui wa Waislaam, wanao jiita kuwa ni waislaam, huenda ukajipamba na ukweli wakati wote, na wala usijali na kujishughulisha na utakayo yasikia dhidi ya Mashia bila kufanya utafiti kuhusu ukweli wa madai hayo na ukweli wake.

ambao walimuamini Nuhu katika tufani na kupanda juu ya kuba hiyo.

Na Abu jaafar Imam Baaqir(a.s) amesema: Al-ghaadhiriyyah ni kipande cha ardhi ambacho Mwenyezi Mungu alizungumza na Musa(a.s) bin Imran katika sehemu hiyo na ni sehemu alipo muokolea Nabii Nuhu, na sehemu hiyo ni sehemu tukufu sana kati ya ardhi ya Mwenyezi Mungu, lau kama si hivyo basi Mwenyezi Mungu asinge ipa amana ya kuvihifadhi viwiliwili vya mawalii wake na watoto wa Mtume wake, (Hakika wamekufa katika ardhi ya Karbalaa manabii mia mbili na mawasii mia mbili) basi yazuruni makaburi yetu katika ardhi ya Ghaadhiriyyah. Na Mwenyezi Mungu ameifanya ardhi ya Karbalaa kuwa ni haram yenye amani na yenye baraka kabla Mwenyezi Mungu haja iumba ardhi ya kaaba na akaifanya kuwa ni haram (sehemu tukufu) kwa muda wa miaka ishirini na nne elfu, na ardhi ya Karbalaa na maji ya mto Furati ni ardhi ya kwanza na maji ya mwanzo kabisa yaliyo takaswa na Mwenyezi Mungu na yaliyo barikiwa)

Rejea ziara: Kaamiluz-ziyaarat cha Ibnu Qawlawaihi Jaafar bin Muhammad Al-qumiy (368 hijiria) ukurasa 444-445 mlango wa 88 kuhusu ubora wa Karbalaa. Na imepokelewa kutoka kwa Alaa bin Abi Aathah amesema: Nimehadithiwa na Ra'asi Jaaluut, kutoka kwa baba yake amesema: Sikupita Karbalaa isipokuwa nilikuwa nikimkimbiza mnyama wangu hadi ninapo ivuka sehemu hiyo, amesema: nikamuuliza kwa nini? Akasema: Tulikuwa tukizungumza ya kuwa mtoto wa nabii atauwawa katika sehemu hiyo. Akasema: Na nilikuwa nikiogopa nisije nikawa ni mimi, wakati alipo uliwa Husein tukasema: haya ndio tuliyo kuwa tukiyazungumza. Akasema: Na baada ya tukio hilo nilikuwa kila nipitapo sehemu hiyo nilikuwa nikipita kwa kutembea taratibu na sikuwa ni mwenye kukimbia)

Tariikhut-twabariy juzu ya 5 393. matukio ya mwaka 60 hijiria,

Al-kaamil fit-tarikh juzu ya 4 90. Matukio ya mwaka 61 hijiria.