TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Juzuu 8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE22%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 17 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 13121 / Pakua: 3694
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Juzuu 8

Mwandishi:
Swahili

1

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA NANE

هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن تَأْتِيَهُمُ الْمَلَائِكَةُ أَوْ يَأْتِيَ رَبُّكَ أَوْ يَأْتِيَ بَعْضُ آيَاتِ رَبِّكَ ۗ يَوْمَ يَأْتِي بَعْضُ آيَاتِ رَبِّكَ لَا يَنفَعُ نَفْسًا إِيمَانُهَا لَمْ تَكُنْ آمَنَتْ مِن قَبْلُ أَوْ كَسَبَتْ فِي إِيمَانِهَا خَيْرًا ۗ قُلِ انتَظِرُوا إِنَّا مُنتَظِرُونَ ﴿١٥٨﴾

158.Je, wananogoja jingine ila wawafikie Malaika au afike Mola wako au ziwafikie baadhi ya ishara za Mola wako? Siku zitakapofika baadhi ya ishara za Mola wako, basi mtu haitamfaa imani yake ambaye hakuamini zamani, au hakuchuma kheri kwa imani yake.Sema: Ngojeni , sisi pia tunangoja.

إِنَّ الَّذِينَ فَرَّقُوا دِينَهُمْ وَكَانُوا شِيَعًا لَّسْتَ مِنْهُمْ فِي شَيْءٍ ۚ إِنَّمَا أَمْرُهُمْ إِلَى اللَّـهِ ثُمَّ يُنَبِّئُهُم بِمَا كَانُوا يَفْعَلُونَ ﴿١٥٩﴾

159.Hakika wale walioigawa dini yao na wakawa makundi makundi, huna uhusiano nao wowote. Hakika shauri lao liko kwa Mwenyezi Mungu tu. Kisha atawaambia yale waliyokuwa wakiyafanya.

مَن جَاءَ بِالْحَسَنَةِ فَلَهُ عَشْرُ أَمْثَالِهَا ۖ وَمَن جَاءَ بِالسَّيِّئَةِ فَلَا يُجْزَىٰ إِلَّا مِثْلَهَا وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿١٦٠﴾

160.Mwenye kufanya vizuri atalipwa mfano wake mara kumi. Na mwenye kufanya vibaya hatalipwa ila sawa na hivyo tu, Nao hawatadhulumiwa.

HAITAMFAA MTU ILA IMANI YAKE

Aya 158 – 160

MAANA

Je, wananogoja jingine ila wawafikie Malaika au afike Mola wako au ziwafikie baadhi ya ishara za Mola wako?

Swali hapo si la kuuliza bali ni la kukanusha. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja kwamba washirikina wamekana dalili za Qur’an, wakakataa kuzingatia maana yake, sasa anasema katika Aya hii kuwa wao hawataamini isipokuwa mambo matatu: Kuja Malaika, kuja Mola na kuja baadhi ya ishara. Hata hivyo Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakubainisha Malaika ambaye anapasa kuwajia ili waamini.

Je, ni Malaika wa mauti au mwingine? Wala pia hakubainisha makusudio ya kuja Mola, Je, ni kuja kwake kwa madai yao au ni kuja amri yake, kama ilivyotokea? Vilevile hakubainisha baadhi ya ishara, Je, ni ishara walizozitaka au ni alama za Kiyama?

Wafasiri wengi wamesema kuwa makusudio ya Malaika ni Malaika wa mauti. Na makusudio ya kuja Mola ni kuja adhabu na mateso yake. Na baadhi ya ishara, ni ishara za Kiyama.

Tafsir hii ndiyo iliyo karibu zaidi na maana. Kwa sababu, maneno yanayofuatia yanataja mambo haya matatu yakitambulisha kauli ya wafasiri na kuitilia nguvu; nayo ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

Siku zitakapofika baadhi ya ishara za Mola wako, basi mtu haitamfaa imani yake ambaye hakuamini zamani, au hakuchuma kheri kwa imani yake.

Anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu kwamba toba na imani wakati wa kuja mojawapo ya mambo haya matatu, haifai kitu; isipokuwa inayofaa ni imani na amali njema anayoichuma mumin kabla ya kutokea hayo. Kwani wakati wa kutolewa roho, au ishara za Kiyama au wakati wa kushuka adhabu huwa hakuna taklifa yoyote. Ikiwa hivyo, basi kuweko imani na kutokuweko ni sawa tu.

Kauli yake Mwenyezi Mungu: Au kuchuma kheri kwa imani yake, inaishiria kuwa kumwamini Mungu kunamwokoa mtu na kukaa milele tu motoni, lakini hakumwokoi na adhabu ya moto. Ama anayemwamini Mwenyezi Mungu na akafanya amali njema, basi hataguswa na moto.

Sema: Ngojeni haya mambo matatu,sisi pia tunangoja.

﴿ فَسَوْفَ تَعْلَمُونَ مَن يَأْتِيهِ عَذَابٌ يُخْزِيهِ﴾

“Punde tu mtajua ni nani itakayemjia adhabu ya kufedhehesha” (11:39).

Hakika wale walioigawa dini yao na wakawa makundi makundi, huna uhusiano nao wowote.

Hapa anaambiwa Mtume(s.a.w.w)

Kama ambavyo walihitalifiana wale walioigawa dini yao na wakawa makundi makundi, vilevile wafasiri nao wamekuwa makundi makundi katika kufasiri makusudio ya ‘walioigawa dini yao.’ Baadhi wamesema kuwa hao ni washirikina kwa kuwa baadhi yao wanaabudu masanamu, wengine nyota na baadhi yao mwanga na giza. Wafasiri wengine wamesema kuwa ni watu wa Kitab.

Kwani Mayahudi waligawanyika makundi ya Masadukayo, Mafarisayo na Mahaasid[1] Ama Wakristo wao waligawanya kanisa la Mashariki na la Magharibi.

Pia imesemekana kuwa ni makundi ya Kiislamu. Na ikasemekana kuwa ni wote wenye mila na vikundi.

Maelezo bora niliyosoma kuhusu tafsir ya Aya hii ni yale aliyosema mwenye tafsir Al-Manar: “Makusudio ya wale walioigawa dini yao wakawa vikundi ni watu wa Kitab. Na makusudio ya kujitenga nao Mtume ni kuhadharishwa Waislamu wasigawanye dini yao wakawa na vikundi kama watu wa Kitab, ili wajue kwamba wao wakifanya vitendo vya watu wa Kitab, basi Muhammad(s.a.w.w) atakuwa mbali nao.”

Hakika shauri lao liko kwa Mwenyezi Mungu tu.

Yeye peke yake ndiye anayemiliki hisabu na adhabu ya mwenye kufarikisha waja wake na kuleta uadui na chuki katika dini na penginepo.

Kisha atawaambia yale waliyokuwa wakiyafanya. Kuanzia wale watakaokubali mpaka wale wanaochochea:

﴿وَقَالَتْ أُولَاهُمْ لِأُخْرَاهُمْ فَمَا كَانَ لَكُمْ عَلَيْنَا مِنْ فَضْلٍ فَذُوقُوا الْعَذَابَ بِمَا كُنْتُمْ تَكْسِبُونَ﴾

“Na wa mwanzo wao watawaambia wa mwisho wao; basi nyinyi pia hamkuwa na ubora kuliko sisi. Basi onjeni adhabu kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyachuma.” (7:39)

Mwenye kufanya vizuri atalipwa mfano wake mara kumi. Na mwenye kufanya vibaya hatalipwa ila sawa na hivyo tu, Nao hawatadhulumiwa.

Kila lililo na radhi ya Mwenyezi Mungu na manufaa kwa watu basi ni zuri; na kila lenye machukivu ya Mwenyezi Mungu na ufisadi kwa watu basi ni baya.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni mwadilifu, mkarimu. Miongoni mwa uadilifu wake ni kumlipa mwenye kufanya uovu, adhabu inayolingana nao. Na miongoni mwa ukarimu wake ni kusamehe, na kumwongozea mtenda mema ziada inayofikia kumi, au mia saba, au isiyo na idadi kulingana na lengo la mtenda mema, sifa zake na hali yake. Angalia Juz 2. (2:261).

Kuna Hadith ya Mtume(s.a.w.w) isemayo: “Hakika Mwenyezi Mungu amesema: “Wema malipo yake ni kumi au zaidi, na uovu ni moja au kusamehewa. Basi ole wake yule ambaye kumi yake imeshindwa na moja yake”.

Anaendelea kusema Mtume: “Mwenyezi Mungu anasema: ‘Mja wangu akikusudia wema mwandikieni jema moja hata kama hatafanya; na akifanya basi mwandikieni kumi mfano wake, Kama atakusudia uovu, msimwandikie kitu; kama ataufanya basi mwandikieni moja.”

قُلْ إِنَّنِي هَدَانِي رَبِّي إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ دِينًا قِيَمًا مِّلَّةَ إِبْرَاهِيمَ حَنِيفًا ۚ وَمَا كَانَ مِنَ الْمُشْرِكِينَ ﴿١٦١﴾

161.Sema: Kwa hakika mimi Mola wangu ameniongoza katika njia iliyonyooka, dini yenye msimamo ndiyo mila ya Ibrahim mnyoofu, Wala hakuwa miongoni mwa washirikina.

قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٢﴾

162.Sema: Hakika Swala yangu na ibada zangu na uhai wangu na mauti yangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu.

لَا شَرِيكَ لَهُ ۖ وَبِذَٰلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ ﴿١٦٣﴾

163.Hana mshirika. Na hayo ndiyo niliyoamrishwa, na mimi ni wa kwanza wa Waislamu.

قُلْ أَغَيْرَ اللَّـهِ أَبْغِي رَبًّا وَهُوَ رَبُّ كُلِّ شَيْءٍ ۚ وَلَا تَكْسِبُ كُلُّ نَفْسٍ إِلَّا عَلَيْهَا ۚ وَلَا تَزِرُ وَازِرَةٌ وِزْرَ أُخْرَىٰ ۚ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّكُم مَّرْجِعُكُمْ فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ فِيهِ تَخْتَلِفُونَ ﴿١٦٤﴾

164.Sema: Je, nimtafute Mola mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu? Na hali yeye ni Mola wa kila kitu? Na kila nafsi haichumii ila (inajichumia) yenyewe. Wala mbebaji hatabeba mzigo wa mwingine. Kisha marejeo yenu ni kwa Mola wenu, naye atawaambia yale mliyokuwa mkihitalifiana.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَكُمْ خَلَائِفَ الْأَرْضِ وَرَفَعَ بَعْضَكُمْ فَوْقَ بَعْضٍ دَرَجَاتٍ لِّيَبْلُوَكُمْ فِي مَا آتَاكُمْ ۗ إِنَّ رَبَّكَ سَرِيعُ الْعِقَابِ وَإِنَّهُ لَغَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١٦٥﴾

165.Naye ndiye aliyewafanya makhalifa wa ardhi na akawainua baadhi yenu juu ya wengine ili awajaribu katika aliyowapa. Hakika Mola wako ni mwepesi wa kuadhibu. Na hakika yeye ni mwingi wa maghufira, mwenye huruma.

SEMA MOLA WANGU AMENIONGOZA

Aya 161 – 165

MAANA

Sema: Kwa hakika mimi Mola wangu ameniongoza katika njia iliyonyooka.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwataja wale walioigawanya dini yao wakawa vikundi, alimwamrisha Mtume wake kuwatangazia washirikina, watu wa Kitab na wengineo kuwa Mwenyezi Mungu amemwongoza Mtume kwa umbile safi, akili kamili na kwa wahyi utokao kwake, kwenye njia inayomweka mbali na batili na kumfikisha kwenyedini yenye msimamo ndiyo mila ya Ibrahim mnyoofu.

Yaani njia ambayo Mwenyezi Mungu amemuongoza nayo Mtume wake Muhammad ndiyo dini ya Nabii Ibrahim(a.s) kipenzi cha Mwenyezi Mungu ambayo wanaitukuza watu wa dini zote.

Wala hakuwa miongoni mwa washirikina.

Bali ni katika maadui wakubwa wa ushirikina na watu wake. Hili ni jibu la Washirikina wa Kiquraish ambao wanadai kwamba wao wako kwenye dini ya Nabii Ibrahim(a.s) .

Sema: Hakika Swala yangu na ibada zangu na uhai wangu na mauti yangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu.

Maudhui ya Aya iliyotangulia ni misingi ya dini na itikadi kwa kulinganisha na neno: ‘Wala hakuwa miongoni mwa washirikina’ na maudhui ya Aya hii ni matawi ya dini na sharia, kwa kulinganisha Swala na ibada.

Kuunganisha ibada kwenye Swala ni katika hali ya kuunganisha ujumla kwenye mahsusi; kama vile kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿وَمَا أُوتِيَ مُوسَىٰ وَعِيسَىٰ وَالنَّبِيُّونَ مِنْ رَبِّهِمْ﴾

Na waliyopewa Musa na Isa na Mitume kutoka kwa Mola wao” (3:84)

Uhai na mauti hapa ni fumbo la uthabiti na kuendelea. Maana ni kuwa ibada za Muhammad(s.a.w.w) na maisha yake yote ya kiitikadi, nia na amali, yanaekelea kwa Mwenyezi Mungu peke yake wala hakengeuki nayo mpaka kufa.

Hana mshirika, Na hayo ndiyo niliyoamrishwa, na mimi ni wa kwanza wa Waislamu.

Aya hii ni ufafanuzi na usisitizo wa yaliyo katika Aya iliyotangulia – Tawhid na ikhlasi. Na Muhaammad ni Mwislamu wa kwanza katika umma wake kwa sababu yeye ndiye mwenye wito huo.

Sema: Je, nimtafute Mola mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu?

﴿فَأَيْنَمَا تُوَلُّوا فَثَمَّ وَجْهُ اللَّهِ﴾

Atakayemtafuta Mola huyo atampata wapi, na hali: “Mahala popote mnakoelekea ndiko kwenye uelekeo wa Mwenyezi Mungu? ”Juz. 1 (2:115)

Na hali yeye ni Mola wa kila kitu?

Na Mola wa kila kitu ni mmoja tu, hana wa kinyume chake.

KILA MTU NA MZIGO WAKE

Na kila nafsi haichumii ila (inajichumia) yenyewe.

Kila alifanyalo mtu liwe kheri au shari basi ni mazao ya silika yake na hali yake kwa ujumla. Anayenasibisha matendo ya mtu kwa mwingine, ni sawa na anayemnasibisha mtoto kwa asiyekuwa mama yake, na matunda kwa usiokuwa mti wake.

Wala mbebaji hatabeba mzigo wa mwingine.

Makusudio ya mzigo hapa ni dhambi. Jumla hii inatilia mkazo jumla iliyo kabla yake, na maana yake ni kwamba:

﴿ لَهَا مَا كَسَبَتْ وَعَلَيْهَا مَا اكْتَسَبَتْ ﴾

“Faida ya yale iliyoyachuma ni yake na hasara iliyochuma ni yake.” Juz. 2 (2:286).

Sio yaliyochumwa na nafsi nyingine.

Hii ndiyo asili ya kidini na kiakili; haiwezekani kuifuta au kuigeuza. Maulama wa lugha na fasaha wametoa masuala mengi na hukumu kwenye asili hii.

Utauliza : Aya hii inaonyesha kuwa kila mtu na lake tu, sasa uko wapi wajibu wa Jihadi, kutoa nasaha na kusaidiana katika wema na takua.

Jibu : Maadhui ya Aya hii yanahusiana na adhabu tu, na kwamba mtu hataadhibiwa kwa kosa la mwingine; wala haina uhusiano wowote na jihadi na nasaha na mengineyo, kwa umbali au karibu. Kwa sababu kuadhibiwa kwa kosa la mwingine ni jambo mbali na wajibu wa jihadi na kurekebisha ufisadi ni jambo jengine.

Swali la pili : watu wamezoea kutoa sadaka ya mali na chakula kwa ajili ya roho za maiti wao; wakasoma Qur’an na kuwapelekea thawabu; je, hii inajuzu kisharia? Na je, maiti wananufaika nayo, Kama ni hivyo, itakuwaje na ilivyo ni kuwa wafu hawaadhibiwi kwa maovu ya walio hai, basi iwe pia wasineemeke na mema yao?

Jibu : Tumesema kuwa akili na sharia inakataa kuadhibiwa mtu kwa kosa la mtu mwingine na kushirikishwa kwenye kosa hilo. Kuhusu thawabu, katika mtazamo wa akili, hakuna kizuizi kwa aliyefanya wema kumshirikisha asiyefanya wema ule katika thawabu anazostahiki kwa amali yake.

Na sharia imelieleza hilo, hivyo imepasa kulisadiki. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema: “Mwanadamu akifa, hukatika amali yake isipokuwa mambo matatu: Sadaka inayoendelea, au elimu inayopatiwa manufaa, au mtoto mwema atakayemwombea, dua?” Akaendelea kusema: “Atakayekufa na ana saumu anayodaiwa basi na amfungie walii wake”.

Akasema tena: “Mwenye kuingia makaburini akasoma Sura ya Yasin huwahafifishia waliozikwa hapo siku hiyo. Na anapata wema kwa idadi ya waliomo makaburi.” Imam Jafar As-sadiq(a.s) naye anasema: “Ni jambo gani linalomzuia mtu kuwafanyia wema wazazi wake mara kwa mara?”

Kwa hiyo Hadith hizi na nyinginezo zinafahamisha kwamba maiti ananufaika kwa kupelekewa thawabu kwa amali ya kheri. Na akili hailikatai hilo kabisa. Kwa sababu hilo linaafikiana na fadhila za Mwenyezi Mungu na ukarimu wake.

Lakini watu wamezidisha mno na kupetuka mipaka ya ilivyoelezwa. Na mafakihi wameafikiana kuwa kila mwenye kufanya ambalo halikuelezewa kwa makusudio ya kuwa linatiliwa mkazo na sharia basi amefanya uzushi (bid’a) katika dini na amemzulia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Kwa hiyo ni bora ampelekee thawabu maiti kwa kutarajia anufaike nazo, bila ya kukusudia kuwa hilo llimependekezwa na dini na sharia.

Kisha marejeo yenu ni kwa Mola wenu, naye atawaambia yale mliyokuwa mkihitalifiana.

Bila ya kutegemea akili au Wahyi; mkakubali yale mliyoyazoea na sio haki, na mkayakana yale yanayochukiwa na mapenzi yenu na matamanio yenu.

ARDHI NA NYUMBA

Naye ndiye aliyewafanya makhalifa wa ardhi na akawainua baadhi yenu juu ya wengine ili awajaribu katika aliyowapa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameiumba ardhi hii akaifanya ni mahali pema panapofaa kwa maisha ya binadamu kutokana na mazingira yake, mpangilio wake, umbo lake na kuwa mbali kwake na jua na mwezi. Akaiandalia yote anayoyahitaji mtu mpaka nyenzo za kujipumbaza na kujistarehesha; sawa na nyumba iliyokamilika kila kitu. Kisha akamweka mtu, ndani ya hiyo ardhi baada ya kumwandalia nyenzo zote za kunufaika na kheri zake na baraka zake.

Na hekima yake ikataka watu watofautiane katika nyenzo hizo na kwamba baadhi yao wawe zaidi ya wengine katika akili, elimu na nguvu za mwili. Na akawawekea njia iliyo sawasawa ili awajaribu wenye nguvu kuwa je wataishukuru neema hii na kuzielekeza nguvu zao kwenye masilahi yao na maslahi ya ndugu zao wanaadamu; au watazifanya ni nyezo za kudhulumu, kunyang’anya, kujiadhimisha na kujifaharisha?

Aya hii imefahamisha kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemleta mtu katika ardhi hii kwa ajili ya elimu na matendo yenye kunufaisha.

Utauliza : Utaiunganishaje Aya hii na Aya isemayo:

﴿ وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ ﴾

“Na sikuumba majini na watu ila waniabudu?.” (51:56)

Jibu : Hazipingani Aya hizi mbili. Kwa sababu elimu na kazi yenye kunufaisha ni ibada ya Mwenyezi Mungu, bali ni katika ibada bora, na twaa iliyo kamili.

Hakika Mola wako ni mwepesi wa kuadhibu.

Anawajaribu waja wake ili ampambanue mwovu na mwema, amwadhibu huyu na kumpa thawabu yule.

Na hakika yeye ni mwingi wa maghufira, mwenye huruma.

Huruma yake haina mpaka, wala msamaha wake hauna kifungu chochote, Ndio! Toba inajaalia msamaha ndio malipo yake yenye kulingana na unabaki msamaha wa ukarimu na kutoa kwa aombaye, hana wa kumlazimisha, isipokuwa yeye mwenyewe mtukufu. Hii ndiyo dalili ya kauli yake:

﴿ وَمَا أَصَابَكُمْ مِنْ مُصِيبَةٍ فَبِمَا كَسَبَتْ أَيْدِيكُمْ وَيَعْفُو عَنْ كَثِيرٍ ﴾

“Na masaibu yanayowasibu ni kwa sababu ya yaliyochumwa na mikono yenu; na Mwenyezi Mungu husamehe mengi.” (42:30).

Yaani mengi yaliyochumwa na mikono yetu.

Mola! tuokoe na yanayotokana na sisi wenyewe na tunakuomba utusamehe mizigo yetu wenyewe!

MWISHO WA SURA YA SITA: AL-AN'AM

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA NANE

Sura Ya Saba: Sura Al-A’raf

Imeteremshwa Makka, isipokuwa Aya 163, Mwenye Majmau anasema imeshuka Madina. Ina Aya 205.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu

﴿١﴾ المص

1. Alif Lam Mim Swad

كِتَابٌ أُنزِلَ إِلَيْكَ فَلَا يَكُن فِي صَدْرِكَ حَرَجٌ مِّنْهُ لِتُنذِرَ بِهِ وَذِكْرَىٰ لِلْمُؤْمِنِينَ ﴿٢﴾

2. Kitab kimeteremshwa kwako, basi isiwe dhiki kifuani mwako kwacho ili upate kuonya kwacho na kiwe ni ukumbusho kwa wanaoamini.

اتَّبِعُوا مَا أُنزِلَ إِلَيْكُم مِّن رَّبِّكُمْ وَلَا تَتَّبِعُوا مِن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ قَلِيلًا مَّا تَذَكَّرُونَ ﴿٣﴾

3. Fuateni mliyoteremshiwa kutoka kwa Mola wenu, Wala msifuate wasimamizi badala yake, Ni machache mnayoyakumbuka.

KITABU KIMETEREMSHWA KWAKO

Aya 1 – 3

MAANA

Alif Lam Swad

Hizi huandikwa na kutamkwa kwa majina ya herufi zake kama zilivyo. Yamepita maelezo yake katika Juz.1 mwanzo wa Sura ya pili (Al- Baqara).

Kitab kimeteremshwa kwako, basi isiwe dhiki kifuani mwako kwacho, Ili upate kuonya kwacho na kiwe ni ukumbusho kwa wanaoamini.

Maneno anaambiwa Mtume Muhammad(s.a.w.w) , Makusudio ya Kitab ni Qur’an, na waumini ni kila anayenufaika na Qur’an, ni sawa iwe ni sababu ya kuamini kwake au kuimarisha imani yao waendelee nayo.

Maana ni kuwa: Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameteremsha Qur’an kwa Mtume(s.a.w.w) ili awaonye kwayo walahidi na washirikina na watu wa dini za ubatilifu; na ili wanufaike nayo watu wenye maumbile safi.

Kazi hii inampa uzito Mtume(s.a.w.w) kutoka kwa makafiri ambao anawakabili kwa Qur’an. Kwa sababu, inalenga katika kubatilisha itikadi zao na hali zao ambazo wamezirithi kutoka kwa mababu zao wa jadi. Hapo Mtume alipata dhiki kutokana na inadi na upinzani wao.

Mwenyezi Mungu anasema:

وَلَقَدْ نَعْلَمُ أَنَّكَ يَضِيقُ صَدْرُكَ بِمَا يَقُولُونَ ﴿٩٧﴾

“Na kwa hakika sisi tunajua kwamba kifua chako kinadhikika kwa yale wayasemayo” (15:97) .

Na akasema tena Mwenyezi Mungu:

إِنَّا سَنُلْقِي عَلَيْكَ قَوْلًا ثَقِيلًا ﴿٥﴾

“Hakika sisi tutakuteremshia kauli nzito” (73:5)

Fuateni mliyoteremshiwa kutoka kwa Mola wenu.

Katika Aya iliyotangulia Mwenyezi Mungu amemwamrisha Mtume wake kufikisha na kutojali upinzani. Katika Aya hii anawaamrisha watu wamfu- ate Mtume na waitumie Qur’an.

Ali Al-Murtadha(a.s) anasema: “Hatawaadhibu Mwenyezi Mungu watu wajinga kwa kutojifundisha, mpaka awaadhibu wenye elimu kwa kutofundisha” Na kinyume chake pia.

Wala msifuate wasimamizi badala yake.

Kwa sababu hakuna badala ya Qur’an ila upotevu na matamanio.

Ni machache mnayoyakumbuka na hali mnawaidhika na mawaidha ya Mwenyezi Mungu na nasaha zake. Kwa sababu nyinyi hamwogopi mwisho utakuwaje; na anayewaidhika ni yule anayeogopa.

Kauli yake ‘ni machache mnayokumbuka’ ni kuashiria uchache wa wale wanaowaidhika.

وَكَم مِّن قَرْيَةٍ أَهْلَكْنَاهَا فَجَاءَهَا بَأْسُنَا بَيَاتًا أَوْ هُمْ قَائِلُونَ ﴿٤﴾

4. Na vijiji vingapi tuliiangamiza; ikafikia adhabu yetu usiku au katika wakati wa kailula.

فَمَا كَانَ دَعْوَاهُمْ إِذْ جَاءَهُم بَأْسُنَا إِلَّا أَن قَالُوا إِنَّا كُنَّا ظَالِمِينَ ﴿٥﴾

5. Basi hakikuwa kilio chao, ilipowafikia adhabu yetu, ila kusema: Hakika sisi tulikuwa madhalimu.

فَلَنَسْأَلَنَّ الَّذِينَ أُرْسِلَ إِلَيْهِمْ وَلَنَسْأَلَنَّ الْمُرْسَلِينَ ﴿٦﴾

6. Kwa hakika tutawauliza wale waliopelekewa (Mitume) na pia kwa hakika tutawauliza (Mitume) waliopelekwa.

فَلَنَقُصَّنَّ عَلَيْهِم بِعِلْمٍ وَمَا كُنَّا غَائِبِينَ ﴿٧﴾

7. Tena kwa hakika tutawasimulia kwa ujuzi, wala hatukuwa mbali.

وَالْوَزْنُ يَوْمَئِذٍ الْحَقُّ فَمَن ثَقُلَتْ مَوَازِينُهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٨﴾

8. Na kipimo siku hiyo kitakuwa haki, Basi ambao uzani wao utakuwa mzito, hao ndio wenye kufaulu.

وَمَنْ خَفَّتْ مَوَازِينُهُ فَأُولَـٰئِكَ الَّذِينَ خَسِرُوا أَنفُسَهُم بِمَا كَانُوا بِآيَاتِنَا يَظْلِمُونَ ﴿٩﴾

9. Na ambao uzani wao utakuwa hafifu, basi hao ndio waliozitia hasara nafsi zao kwa sababu ya kuzidhulumu Ishara zetu.

وَلَقَدْ مَكَّنَّاكُمْ فِي الْأَرْضِ وَجَعَلْنَا لَكُمْ فِيهَا مَعَايِشَ قَلِيلًا مَّا تَشْكُرُونَ ﴿١٠﴾

10. Na hakika tumewamakinisha katika ardhi na tukawawekea humo mahitaji ya maisha, Ni shukrani ndogo mnazotoa.

NA MIJI MINGAPI TULIIANGAMIZA

Aya 4-10

MAANA

Na miji mingapi tuliiangamiza; ikafikia adhabu yetu usiku au katika wakati wa kailula [2] .

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumwamrisha Mtume wake Mtukufu kuonya kwa Qur’an na kuamrisha watu kuifuata, katika Aya hii, anataja maangamizo ya waliopita ambao aliwaangamiza kwa sababu ya kupinga kwao Mwenyezi Mungu na kukadhibisha Mitume yake, na kwamba yeye Mwenyezi Mungu aliwateremshia adhabu usiku au wakati wa kailula, mchana, ambao ni wakati wa raha na amani, ili adhabu iwaumize zaidi.

Wafasiri wengi wanasema kuwa kaumu ya Nabii Lut walijiwa na adhabu usiku. Nami nashangaa sijui wameyatoa wapi haya, na Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

إِنَّ مَوْعِدَهُمُ الصُّبْحُ أَلَيْسَ الصُّبْحُ بِقَرِيبٍ ﴿٨١﴾ …

“Hakika miadi yao ni asubuhi, Je, asubuhi si karibu” (11:81).

Kuna kikundi cha wafasiri waliosema kuwa kuna mageuzi ya kutanguliza maneo katika Aya hii tunayoifasiri; Kwa sababu kuangamia kunakuja baada adhabu, Kwamba isomeke hivi: Ni miji mingapi ilifikiwa na dhabu yetu tuliiangamiza? Razi ametaja njia tatu za kuawili Aya hii na Tabrasi akazidisha ya nne.

Ilivyo hasa ni kuwa hakuna wajibu wowote wa kupangilia maneno kulingana na maana ya hali halisi, ikiwa utaratibu wa hali halisi uko wazi na unajulikana na wote; kama ilivyo katika Aya. Na herufi “Fa’, kama ambavyo inakuja kwa maana ya kufuatisha, vilevile inakuja ikiwa ni ya ziada na ya kufasiri, Hapa, herufi ‘Fa’ inafasiri aina ya maangamivu waliyoyapata washirikina.

Basi hakikuwa kilio chao, ilipowafikia adhabu yetu, ila kusema: Hakika sisi tulikuwa madhalimu.

Washirikina walikuwa wakitambika kwa majina ya masanamu wakiwa wameamini kabisa. Lakini walipoona adhabu walijitenga na waungu wao na wakaelekea kwa Mwenyezi Mungu wakikiri ukafiri na ushirikina wao, lakini ni baada ya kukatika taklifa zote na kufungwa mlango wa toba.

Kwa hakika tutawauliza wale waliopelekewa (Mitume) na pia kwa hakika tutawauliza (Mitume) waliopelekwa.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuelezea maangamivu yao duniani anaelezea kuwa wao wataulizwa huko akhera na wataulizwa Mitume pia, wawatolee ushahidi.

Tena kwa hakika tutawasimulia kwa ujuzi, wala hatukuwa mbali.

Mwenyezi Mungu hatatosheka na kuwauliza tu na kuwauliza Mitume, bali yeye pia atawasomea kila kitu walichokisema na kukifanya:

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا أَحْصَاهُ اللَّـهُ وَنَسُوهُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ﴿٦﴾

“Siku Mwenyezi Mungu atakapowafufua wote, awaambie yale waliyoya- tenda; Mwenyezi Mungu ameyadhibiti, na wao wameyasahau; na Mwenyezi Mungu ni shahidi wa kila kitu.” (58:6)

Mkusudio yake ni kuwatia msukosuko watambue nakama ya Mwenyezi Mungu na ghadhabu yake kwao, yakiwa ni malipo ya uasi na ukaidi wao.

MIZANI YA MATENDO

Na kipimo siku hiyo kitakuwa haki.

Maneno yamekuwa mengi kuhusu hakika ya mizani ambayo atapimia Mwenyezi Mungu matendo ya watu; mpaka baadhi ya watu wakasema kuwa mizani hiyo itakuwa na mikono miwili.

Tunavyofahamu sisi kuhusu mizani hii – na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi – ni kuwa ni kipimo ambacho kitampambanua mtiifu na mwasi na mwema na mwuovu. Kipimo chenyewe ni amri ya Mwenyezi Mungu na makatazo yake.

Ukifika wakati wa Hisabu, huangaliwa aliyoyafanya na aliyoyaacha mwanaadamu, na hulinganisha kati ya aliyoamrishwa na Mwenyezi Mungu kuyafanya na aliyoyaacha. Vitendo vyake vikifuatana na amri ya Mwenyezi Mungu na makatazo yake, basi atakuwa ni katika waliofaulu, na kama si hivyo atakuwa ni katika wale ambao uzani waao umekua hafifu na kuwa katika madhalimu waliojihasiri wenyewe na adhabu ya moto.

Kwa maneno mengine ni kwamba kila kitu katika maisha haya kina msingi na udhibiti wake, iwe ni sayansi, fasihi au fani yoyote nyingine. Na kwayo hutofautiana na kingine, bali uzuri wake na ubaya wake unajulikana kutokana na misingi hiyo.

Misingi hiyo na udhibiti huo inaitwa mizani, makisio, njia na mwamuzi. Basi hivyo hivyo hisabu katika akhera ina misingi na udhibiti ambao Qur’an imeipa jina la Mizan na Swirat.

Kwa hiyo misingi hii au Mizani hii ya matendo ya watu ni amri ya Mwenyezi Mungu na makatazo yake. Kazi yake katika kumhukumu mtu kesho, ni kama kazi ya fiqhi na kanuni katika kuhukumiwa mshitakiwa katika maisha ya hapa duniani.

Basi ambao uzani wao utakuwa mzito.

Nao ni wale ambao matendo yao yamelingana na misingi ya amri za Qur’an na makatazo yake yakawa makamilifu.

Hao ndio wenye kufaulu.

Kwa sababu hawakuanguka mtihani.

Na ambao uzani wao utakuwa hafifu.

Nao ni wale ambao umedhihirika umbali baina ya matendo yao na hukumu za Mwenyezi Mungu na mafunzo yake.

Basi hao ndio waliozitia hasara nafsi zao kwa sababu ya kuzidhulumu Aya zetu.

Wafasiri wengi wamesema kuwa makusudio ya kuzidhulimu hapa ni kuzikufuru, lakini sawa ni kukadhibisha Aya za Mwenyezi Mungu kwa hali yoyote, kama inavyoonyesha Aya yenyewe, ni sawa Aya hizo ziwe zinafahamisha umoja wa Mwenyezi Mungu, ujumbe wa Mitume yake, ufufuo au halali yake na haramu yake.

Na hakika tumewamakinisha katika ardhi na tukawawekea humo mahitaji ya maisha, Ni shukrani ndogo mnazotoa.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuwamrisha washirikina kufuata waliyoteremshiwa, na kuwahofisha na adhabu ya dunia na akhera, sasa anawakumbusha neema yake kwao; na kwamba yeye ndiye aliyewaweka katika ardhi hii akawapa uwezo wa kuitumia kwa maslahi yao.

Mmoja wa wafasiri wa kisasa anasema: “Lau si Mwenyezi Mungu kumakinisha mtu katika ardhi hii, asingeliweza kiumbe huyu dhaifu kuyamudu maumbile”.

وَلَقَدْ خَلَقْنَاكُمْ ثُمَّ صَوَّرْنَاكُمْ ثُمَّ قُلْنَا لِلْمَلَائِكَةِ اسْجُدُوا لِآدَمَ فَسَجَدُوا إِلَّا إِبْلِيسَ لَمْ يَكُن مِّنَ السَّاجِدِينَ ﴿١١﴾

11. Na hakika tuliwaumba, kisha tukawatia sura, Kisha tukawaambia Malaika: Msujudieni Adam; Basi waka- sujudu wote isipokuwa Iblisi hakuwa miongoni mwa walio- sujudu.

قَالَ مَا مَنَعَكَ أَلَّا تَسْجُدَ إِذْ أَمَرْتُكَ قَالَ أَنَا خَيْرٌ مِّنْهُ خَلَقْتَنِي مِن نَّارٍ وَخَلَقْتَهُ مِن طِينٍ ﴿١٢﴾

12. Akasema (Mwenyezi mungu): Nini kilichokuzuia kumsujudia nilipokuamrisha? Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye, umeniumba kwa moto naye umemuumba kwa udongo.

قَالَ فَاهْبِطْ مِنْهَا فَمَا يَكُونُ لَكَ أَن تَتَكَبَّرَ فِيهَا فَاخْرُجْ إِنَّكَ مِنَ الصَّاغِرِينَ ﴿١٣﴾

13. Akasema: Basi shuka kutoka huko, haikufalii kufanya kiburi humo. Basi toka, hakika wewe ni miongoni mwa walio duni.

قَالَ أَنظِرْنِي إِلَىٰ يَوْمِ يُبْعَثُونَ ﴿١٤﴾

14. Akasema: Nipe muda mpaka siku watakapofufuliwa.

قَالَ إِنَّكَ مِنَ الْمُنظَرِينَ ﴿١٥﴾

15. Akasema (Mwenyezi mungu): Utakuwa katika waliopewa muda.

قَالَ فَبِمَا أَغْوَيْتَنِي لَأَقْعُدَنَّ لَهُمْ صِرَاطَكَ الْمُسْتَقِيمَ ﴿١٦﴾

16. Akasema: Kwa kuwa umenipoteza, basi hakika nitawakalia katika njia yako.

ثُمَّ لَآتِيَنَّهُم مِّن بَيْنِ أَيْدِيهِمْ وَمِنْ خَلْفِهِمْ وَعَنْ أَيْمَانِهِمْ وَعَن شَمَائِلِهِمْ وَلَا تَجِدُ أَكْثَرَهُمْ شَاكِرِينَ ﴿١٧﴾

17. Kisha hakika nitawaendea kwa mbele yao na nyuma yao na kuumeni kwao na kushotoni kwao; wengi katika wao hutawakuta wenye kushukuru.

قَالَ اخْرُجْ مِنْهَا مَذْءُومًا مَّدْحُورًا لَّمَن تَبِعَكَ مِنْهُمْ لَأَمْلَأَنَّ جَهَنَّمَ مِنكُمْ أَجْمَعِينَ ﴿١٨﴾

18. Akasema: Toka humo, hali ya kuwa ni mwenye kufedheheka na mwenye kufukuzwa. Atakayekufuata miongoni mwao, basi hakika nitaijaza Jahannam kwa nyinyi nyote.

NA HAKIKA TULIWAUMBA

Aya 11-18

ASILI YA MTU

MAANA

Na hakika tuliwaumba, kisha tukawatia sura.

Maneno haya wanaambiwa wanaadamu, Maana ya ‘tuliwaumba’ ni kuwa yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu aliianzisha asili yetu ya kwanza kutokana na mchanga na sisi akatutoa kutokana na tone la manii ambalo linaishia kwenye mchanga. Makusudio ya tuliwatia sura ni kwamba yeye amejaalia mada ya kwanza aliyotuumba kwayo kuwa ni mtu kamili; kama alivyosema:

أَكَفَرْتَ بِالَّذِي خَلَقَكَ مِن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ سَوَّاكَ رَجُلًا ﴿٣٧﴾ …

“Je, unamkufuru yule aliyekuumba kwa udongo, tena kwa tone la manii, kisha akakufanya mtu kamili?. (18:37).

Kwa hiyo tofauti baina ya kuumba na kutia sura ni kwamba kuumba maana yake ni kukipatisha kitu na kukianzisha. Ama kukitia sura ni kukipa kitu sura hasa baada ya kukianzisha.

Unaweza kuuliza kuwa : wafuasi wa Darwin wanasema kwamba mtu kwanza alipatikana katika sura isiyokuwa hii aliyo nayo sasa; kisha ikageukageuka mpaka kufikia ilivyo sasa.

Jibu : sisi tuko pamoja na dalili za kielimu zisizokubali shaka na dhana za kupinga; Kwa sababu pale tu inapozuka dhana, basi dalili hubatilika. Hii ni hakika ya ubainifu iliyo wazi hawaipingi hata wenye nadharia ya majaribio ambao wamesema chimbuko la maarifa ni lazima litokane na majaribio ya kuhisi.

Dalili kubwa waliyoitegemea wenye nadharia ya mageuzi ni ufukuaji wa vitu vya kale; kuwa wamegundua aina za wanyama, wengine ni bora zaidi. Na kwamba muda wa wale waliokuwa bora zaidi umechelewa kuliko wa wale walio duni na kwamba kuna kushabihiana na binadamu katika mambo mengi.

Sisi hatupingi ugunduzi huu lakini, hauthibitishi nadharia ya Darwin, Kwa sababu hauleti uhakika usio na shaka kuwa aliye bora amekuwa kutokana na aliye duni, bali hilo haliwezekani na inawezekana kuwa kila mmoja kati ya aliye bora na duni ni aina nyingine iliyopatikana kutokana na hali inayo afikiana nayo, kisha ikatoweka wakati ilipobadilika hali yake, kama zilivyotoweka aina nyinginezo za wanyama na mimea.

Ikiwa mambo mawili yanawezekana, basi kuchukua moja tu, na kuacha jingine ni kujichukulia madaraka.

Katika niliyoyasoma ni kwamba wataalamu wengi, wakiwemo walahidi, walikuwa wakiamini nadharia ya Darwin, lakini walipoingia katika nyanja za elimu wakabadilika kutokana na yale tuliyoyataja; na kwamba mtu ana aina pekee za kiakili na kiroho zinzohusiana naye, zinazomfanya awe tofauti na viumbe vingine.

Kisha tukawaambia Malaika: Msujudieni Adam, Basi wakasujudu wote isipokuwa Iblisi hakuwa miongoni mwa waliosujudu.

Umetangulia mfano wake katika Juz.1 (2:82)

Akasema: Nini kilichokuzuia kumsujudia nilipoamrisha?

Makusudio ya kusujudu hapa ni kusujudu kwa kimaamkuzi, sio kwa kiibada, nako ni kumtii Mwenyezi Mungu, kwa sababu ni amri yake.

Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye, umeniumba kwa moto naye umemuumba kwa udongo.

Chochote akifanyacho Iblisi, lazima atakitafutie visibabu; na sharti la msingi la kila kisababu katika mantiki yake ni kukhalifu matakwa ya Mwenyezi Mungu na radhi yake. Hiyo ndiyo asili ya kwanza anayoitege- mea Iblis katika kauli zake na vitendo vyake.

Fakihi anajitahidi kufanya utafiti ili aongoke kwenye hukumu alizoziwekea sharia Mwenyezi Mungu, lakini Iblisi kwake yeye sharia za hukumu ni zile zenye msingi wa “Mwenyezi Mungu anasema hivyo nami nasema hivi.”

Mwenyezi Mungu alimwamuru Iblisi amsujudie Adam, lakini akakataa wala asiombe msamaha, bali alijigamba kwa kusema: “Vipi nimsujudie ambaye mimi ni mbora wake.” Kama kwamba anamwambia Mwenyezi Mungu Mtukufu: Ilikuwa wafaa wewe umwamuru Adam anisujudie mimi, sio mimi nimsujudie yeye.

Kwa hivyo utukufu, kwa mantiki ya Iblis ni kwa kuangalia asili, sio kwa kumcha Mwenyezi Mungu; na kwa Mwenyezi Mungu ni vitendo na takua si kwa asili. Na elimu kwa Iblis ni kukisia (Qiyasi) na matamanio; na kwa Mwenyezi Mungu ni Wahyi na hukmu ya kiakili ambayo uwazi wake haufanyi kutofautiana watu wawili.

Kwa hiyo, mwenye kuangalia asili yake au akaifanyia kiasi dini kwa rai yake, basi atakuwa amemfuata Iblis atake asitake.

Mwenye Tafsir Al-Manar anasema: “Imepokewa Hadith kutoka kwa Jafar As-sadiq, kutoka kwa baba yake, naye kutoka kwa babu yake kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: “Wa kwanza aliyeifanyia makisio (qiyas) dini ni Iblis, Mwenyezi Mungu alimwambia amsujidie Adam, yeye akasema ni bora kuliko huyo”

Kisha akaendelea kusema Jafar: “Mwenye kulifanyia makisio (qiyas) jambo la dini, Mwenyezi Mungu atamkutanisha na Iblis siku ya kiyama.”

Utauliza : Aya hii inafahamisha kuwa uhai unapatikana kutokana na moto kama vile Aya nyingine isemayo:

وَخَلَقَ الْجَانَّ مِن مَّارِجٍ مِّن نَّارٍ ﴿١٥﴾

“Na akaumba majini kwa ulimi wa moto” (55:15)

Na Aya nyingine inasema:

وَجَعَلْنَا مِنَ الْمَاءِ كُلَّ شَيْءٍ حَيٍّ ﴿٣٠﴾

“Na tukafanya kwa maji kila kitu kilicho hai” (21:30)

Jibu : Vitu hai vilivyotajwa katika Qur’an tukufu viko aina nyingi: Kuna ulimwengu wa Malaika, wa majini na vile vilivyomo katika ardhi hii. Aina hii ya tatu ndiyo ambayo uhai wake uko katika maji, kama vile wanyama, mimea na watu. Hiyo ndiyo iliyokusudiwa kiujumla katika kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Na tukafanya kwa maji kila kitu kilicho hai.’

Na kuna viumbe vingine ambavyo uhai wake uko katika moto. Kwa maneno mengine ni kwamba maji ni lazima kwa maisha ya mwanaadamu kulingana na maumbile yake, pia wanyama na mimea. Lakini hii haikanushi kuwa kuna viumbe vingine ambavyo moto ni lazima katika maisha yao. Wataalamu wa elimu ya wadudu wanasema: Kuna aina ya wadudu ambao maisha yao yanategemea hewa ya sumu na visima vya mafuta (Petroli)!

Akasema: Basi shuka kutoka huko, haikufalii kufanya kiburi humo. Basi toka, hakika wewe ni miongoni mwa walio duni.

Imesemeka kuwa dhamir ya ‘huko’ inarudia Pepo, Wengine wakasema ni mbinguni. Sisi hatujishughulishi na ufafanuzi ikiwa haukutajwa katika Qur’an wala Hadith, tunatosheka na ujumla.

Mfumo wa maneno unaonyesha kwamba dhamir inarudia kwenye daraja ya juu mbele ya Mwenyezi Mungu; maana yakiwa kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimfukuza Iblis kutoka katika rehema yake hadi kwenye laana yake, ikiwa ni malipo ya kiburi chake na kujizuilia kwake kumtii Mwenyezi Mungu. Kwani kumsujudia Adam ni amri ya Mwenyezi Mungu na ni kumtii Mwenyezi Mungu na sio Adam. Kila anayejiona kuwa sawa ni kukataa hukumu ya Mwenyezi Mungu, basi anastahiki laana mpaka siku ya malipo.

Akasema: Nipe muda mpaka siku watakapofufuliwa.

Iblis alikuwa na haja nafsini mwake - atakayoifafanua - ya kutaka kupewa muda.

Akasema - Mwenyezi Mungu Mtukufu -:Utakuwa katika waliopewa muda . Inasemekana Iblis alitaka muda mpaka siku ambayo watafufuliwa wafu wote kwa ajili ya hisabu na malipo, Mwenyezi Mungu akakataa maombi haya, akampa muda mpaka siku ya kufa wote walio hai, ambao umeashiriwa na Aya isemayo:

قَالَ فَإِنَّكَ مِنَ الْمُنظَرِينَ ﴿٣٧﴾ إِلَىٰ يَوْمِ الْوَقْتِ الْمَعْلُومِ ﴿٣٨﴾

“Akasema: Hakika wewe ni katika waliopewa muda mpaka siku ya wakati maalum” (15: 37 – 38).

Na siku hiyo ni ile saa ya kupuziwa Parapanda ambayo imeelezwa na Aya isemayo:

وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَصَعِقَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ ﴿٦٨﴾

“Na itapulizwa parapanda watoke roho waliomo ardhini na waliomo mbinguni …” (39: 68)

Akasema: Kwa kuwa umenipoteza, basi hakika nitawakalia katika njia yako iliyonyooka.

Iblis alijiwekea mkakati kuwa atalipizia kisasi kwa kiumbe huyu aliyekuwa ni sababu ya kufukuzwa kwake kutoka katika rehema ya Mwenyezi Mungu kwenda kwenye laana. Akabainisha aina hii ya kujilipiza kwamba yeye ataikalia na kuziba njia, kwa Adam na kizazi chake, ile ielekeayo kwa Mwenyezi Mungu na kwenye twaa yake.

Kisha hakika nitawaendea kwa mbele yao na nyuma yao na kuumeni kwao na kushotoni kwao; wengi katika wao hutawakuta wenye kushukuru.

Kuwaendea kwake kwa pande hizi nne ni fumbo la ushawishi wake na jitihada yake katika kuwapoteza, kiasi ambacho hataacha maasi yoyote ila huwahada kwayo, wala twaa yoyote ila huwazuia.

Mwenyezi Mungu akiwaamrisha jihadi na kujitolea mhanga, basi Iblisi huwapendekezea uhai. Na kama Mwenyezi Mungu (s.w.t) akiwahimiza kujitolea mali katika njia yake Mwenyezi Mungu, basi mlaanifu huyu huwahofisha na ufukara.

Ikiwa Mwenyezi Mungu Mtukufu anawakataza pombe, zinaa na kamari, yeye huwavutia huko kwenye anasa na matamanio. Mungu akiwapa kiaga cha moto na kuwaahidi Pepo, basi adui huyu wa Mwenyezi Mungu huwaambia, hakuna Pepo wala moto.

Basi namna hii huhisabu kila haki kuwa ni batil na kila msimamo kuwa ni kombo. Hii inafanana kabisa na wale waliouza dini yao kwa shetani wak- iboresha vitendo vya wakoloni, wakiua wanawake na kuwafukuza wasio na hatia nchini mwao.

Akasema: Toka humo, hali ya kuwa ni mwenye kufedheheka na mwenye kufukuzwa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemhusisha Iblisi na kufedheheka na kufukuzwa kwa kuwa yeye Mwenyezi Mungu alimteremsha cheo alichokuwa nacho.

Atakayekufuata miongoni mwao, basi hakika nitaijaza Jahannam kwa nyinyi nyote.

Yaani Jahannam itakuwa yake na wanachama wake waliomfuata. Aya hii ni kama ile isemayo:

لَأَمْلَأَنَّ جَهَنَّمَ مِنكَ وَمِمَّن تَبِعَكَ مِنْهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٨٥﴾

“Kwa hakika nitaijaza Jahannam kwa wewe na wale wanaokufuata miongoni mwao wote” (38:85)

Hapa kuna maswali yanayotaka kujibiwa:

1.Kwanza , Je, maneno yalikuwa ni moja kwa moja au ni kwa kupitia hali fulani?

2.Pili , kauli ya Iblis: “Umenipoteza” inafahamisha kwamba kupotea kwake kulitokana na Mwenyezi Mungu, vipi atamwadhibu?

3.Tatu , kwa nini Mwenyezi Mungu amempa muda Iblis naye anajua ufisadi wake na kuwaharibu wengine?

Tutajibu maswali haya matatu kwa ufupi sana:

Jibu la kwanza, ni kuwa sisi tunaamini kuweko kwa majibizano hayo, kwa vile Wahyi umefahamisha hilo na akili hailipingi hilo, na si juu yetu kufanya utafiti wa aina ya majibizano hayo yalivyokuwa, maadamu Wahyi haukufafanua.

Kuhusu jibu la pili, upotevu unatokana na Iblis, na wala hautokani na Mwenyezi Mungu Mtukufu. Iblis mwenyewe amekiri kuwa yeye ni mpotezaji katika Aya isemayo:

وَلَأُغْوِيَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٣٩﴾ إِلَّا عِبَادَكَ مِنْهُمُ الْمُخْلَصِينَ ﴿٤٠﴾

“Na nitawapoteza wote isipokuwa waja wako waliosafishwa” (15:39 –40)

Na vipi Mwenyezi Mungu ampoteze mja kisha amwadhibu kwa upotevu? Mwenyezi Mungu ametakata kabisa na hayo.

Ama kauli ya Iblis “Umenipoteza” Maana yake ni kwa kuwa umenifanyia mtihani wa kuniamrisha kumsujudia Adam, mtihani ambao umeniingiza katika uovu na uasi, basi nami nitafanya hivi na vile. Kwa maneno mengine ni kuwa Iblis anasema kwa kuwa umeniamrisha na nikaasi amri yako, basi sitamwacha yeyote atii amri yako.

Jibu la swali la tatu ni kuwa: matakwa ya Mwenyezi Mungu yamehukumia kumpa mtu akili, ukumbusho kupita utume, uwezo wa kufanya kheri na shari na kumwachia hiyari na kumjaribu kwa matamanio na hadaa ana- zoshawishiwa na Iblis na majeshi yake; ili kumpambanua mwema na mwovu na mwenye ikhlas na mwenye khiyana.

Kwa maelezo zaidi angalia Juz.7 (5:94) kifungu ‘Maana ya mtihani wa Mwenyezi Mungu.’

5 UKWELI WA USHIA

KUYAJENGEA MAKABURI

FUADI : Ewe Jaafar, je unaniruhusu nikuulize kuhusiana na maudhui ya Shia na Sunni?[13]

JAAFAR : Uliza kwani nina penda sana kila mtu awe ni mwenye kufahamu mambo, mwenye elimu na anae fahamu mambo kutokana na utafiti na kwa kupata yakinina hawi ni mwenye msimamo legelege na mwenye kufuata kila akisikiacho na kipepeacho angani, au kila sauti ijitokezayo na kutangaa anganibila ya kufahamu usahihi wake na ubatilifu wake au ufisadi wake.

FUADI : Je maneno yangu utayaamini ikithibitika kuwa sisi (Ahli sunna) ndio wenye haki?

JAAFAR : Kwa hakika mimi niko msitari wa mbele kati ya wale wenye kuamini mambo ya kweli haraka pale wanapo yafahamu, na mimi sikushikamana na ushia isipokuwa ni baada ya kuuona kuwa ni haki na wewe unafahamu ya kuwa baba yangu na mama yangu na ndugu zangu na watu wa kabila langu wote ni masunni na kati yao hakuna Shia hata mmoja, na mimi sikufuata Ushia isipokuwa ni kwa ajili ya ukweli nilio uona na kuukuta ndani ya madhehebu hayo.. na lau nitafahamu usahihi wa maneno yako mimi ni wa mwanzo kuyaamini.

FUAD : Nyie Mashia mnayajengea makaburi ya Manabii, Maimamu, Maulamaa na watu wemamajengo makubwa, mnasali kwenye makaburi, wakati jambo hilo ni shirki, kama washirikina wanavyo abudu masanamu nanyi Mashia mnaaabudu majengo ya makaburi ya mawalii.

JAAFAR : Ni wajibu sisi tuwe wakweli na tunao kwenda sambamba na uhakika wa mambo, tusiwe ni watu wachukuao maganda na kuacha kiini, tusiangalie yasemwayo na fulani au fulani, bali tuangalie ukweli ulio wazi katika kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wake(s.a.w.w) , na mwenendo wa watu wema walio tangulia.

FUAD : Ndio, nami ni hivyo hivyo, ninapenda kufahamu ukweli wa mambo kupitia njia za kielimu na ufahamu sahihi, si kufuata mambo ufuataji wa kipofu.

JAAFAR : Kwanza kabisa: Sio sisi Mashia pekee tuhusikao na suala la kuyajengea makaburi, kwani waislaam wote wanayajengea makaburi ya Manabii na Maimam na wanazuoni wakubwa au viongozi wao, na ifuatayo ni mifano juu ya hayo: Kaburi la Mtume(s.a.w.w) na makaburi ya makhalifa wawili bado hadi hivi sasa yamejengewa kwa jengo kubwa na yenye kuba kubwa na ya hali ya juu kabisa.

Makaburi ya Mitume kadhaa, kama vile kaburi la Nabii Ibrahim(a.s) lililoko Jodan katika mji wa (Al-khaliil) makaburi hayo yana dharihi (yamejengewa) na juu yake kuna kuba na majengo makubwa. Kaburi la Nabi Mussa(a.s) lililoko Jodan kati ya mji wa (Qudsi) na (Omman) lina jengo kubwa. Kaburi la Abi Hanifa lililoko Baghdad hadi leo bado limejengewa kwa jengo kubwa, na juu yake kuna kuba. Kaburi la Abi Hurairah katika (Misri) hufanyiwa ziara na limejengewa na juu yake kuna kuba. Kaburi la Abdul-qaadir lililoko (Baghdaad) kaburi hilo lina uwanja mkubwa na dharihi na juu yake kuna kuba.

Na makaburi mengine ya Mitume, na makaburi ya Maimamu na wanazuoni wakubwa wa madhehebu, yote hayo yana majengo na juu yake kuna kuba, na yana waqfu maalum ambapo waqfu hizo faida zake hutumika kuyaimarisha na kuyakarabati makaburi hayo na kuyalinda yasiharibike.

Na Miji ya kiislaam imejawa na majengo kama hayo.. na Waislaam wote pamoja na tofauti za madhehebu yao tangu siku ya kwanza hadi leo huyapenda mambo hayo, na huwaamrisha watu kuyatekeleza hayo, na hawakukataza kufanya hivyo hata siku moja, kwa hivyo si sisi Mashia pekee tuhusikao na hukumu hii, bali wanakubaliana nasi na kuwafikiana nasi Waislaam wengine wote, na wao pia huyajengea makaburi ya maimamu wao na wakati wote huyatembelea.

Pili: Sisi- Mashia- au waislaam wengine wakati tunapo Sali pembezoni mwa makaburi ya mawali, hatusali kwa ajili ya mawalii hao bali tunasali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu pekee. Na liwezalo kukujulisha hilo ni kuwa sisi tunapokuwa katika sala huelekea kibla na wala hatuyaelekei makaburi hayo, na lau kama tunge kuwa tukiyasalia makaburi yale, na kuelekea kwenye ibada zatu kwenye dharihi zile (majengo yale ya makaburi), ingewajibika kuyaelekea, na tusinge elekea kwenye kibla.

FUAD : Kwa nini mnasali nyuma ya makaburi hayo, mpaka mkayafanya kuwa ni kibla chenu?

JAAFAR : Hakika sisi wakati tunapo Sali nyuma ya makaburi, tunaelekea kibla na wala hatuyaelekei makaburi, bali makaburi yale-imetokea tu- yakawa mbele yetu, bila ya sisi kukusudia kuyaelekea.

Na hili halitokei isipokuwa kwa mtu anae Sali akiwa ameelekea kibla katika sehemu fulani na ikatokea kwa mfano kukawa na jengo kubwa mbele yake, je kusali katika sehemu hiyo kunamaanisha kuwa mwenye kusali anaabudu jengo hilo?! Na zaidi ya hayo Maulamaa wote wa Waislaam wanasema kuwa: Inajuzu kusalia katika majumba ya ibada za washirikina hali ya kuwa umeelekea kibla hata kama mbele ya mwenye kusali kutakuwa na sanamu lenye kuabudiwa kinyume cha Mwenyezi Mungu, Kwani mwenye kusali humuelekea Mwenyezi Mungu na wala halielekei sanamu. Je hii inamaana kuwa mwenye kusali analiabudu sanamu lile?

FUAD : Ikiwa kuyajengea makaburi si shirki- kama unavyo sema- na waislam wote wanasema ya kuwa inajuzu kufanya hivyo, ilikuwaje wakavunja madharihi (majengo ya makaburi) na makuba yaliyo jengwa juu ya makaburi ya maimamu na wengineo, kwa hoja ya kuwa kufanya hivyo ni shirki na ni kumuabudu asie kuwa Mwenyezi Mungu, na maulamaa wa Hijazi wakatoa fat'wa ya kufanya hivyo?

JAAFAR : Kwa hakika ni baadhi tu walio toa fat'wa kama hiyo kati ya maulamaa wa Hijazi katika zama zile, kwani kuna baadhi ya Mashekhe waishio katika mji wa Madina walio nihadithia na kunisimulia kwa kusema: Kwa hakika wakati huo walipo toa amri ya kubomoa makuba na majengo ya makaburi, maulamaa wenyewe wa Hijazi walipinga amri hiyo, wakitoa hoja kuwa hilo si shirki bali vitu kama hivyo ni sunna katika sheria ya kiislaam, kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:jambo lililo pelekea kufukuzwa kwa maulamaa wale, na kuwauz ulu wengine katika nyadhifa zao na kuwatenga. Kwa hivyo basi: Fat'wa hiyo haikutolewa isipokuwa na baadhi tu ya maulamaa wa Hijaz.

FUAD: Kwa hakika mimi nilikuwa nikifikiria na kujiuliza ya kuwa: Ikiwa kujenga madharihi na makuba ni haram na shirki, kwa nini maulamaa wa Waislaam hawakuzinduka na kuliona hilo tangu zama za Mtume(s.a.w.w) hadi leo, na kwanini hawakuzuwia kufanya hivyo? Na ilikuwaje Waislaam wasilifahamu hilo kwa muda wa karne kumi na tatu?

JAAFAR: Nitakuongezea elimu na maarifa: Hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alikiri na kukubali kujengea makaburi, madharihi na makuba na hakukataza kufanya hivyo. Kwa mfano hili ni jengo la hijri Ismail mahala alipo zikwa Nabi (Ismail) na sehemu alipo zikiwa mama yake Haajar. Na haya hapa makaburi ya Manabii wengine-kama Ibrahim Musa na wengineo- walio zikiwa pembezoni mwa baytul-maqdas, yalikuwa ni yenye majengo makubwa katika zama za Mtume(s.a.w.w) na hadi zama zetu hizi, na wala hakuzuwia yeyote si Mtume Mwenyewe (s.a.w) wala mmoja wapo kati ya makhalifa wake.

Na lau kama tendo hilo linge kuwa haram au linge kuwa ni shirki basi Mtume ange amuru kuvunjwa na kubomolewa kwa majengo na makuba hayo, na ange kataza kufanya hivyo. Na kutokana na ukweli kuwa hakufanya hivyo tunafahamu na kuwa na yakini ya kuwa mfano wa vitu kama hivyo au kufanya hivyo ni kitu kinacho juzu na kinafaa.

Hivyo hivyo baada ya kufariki Mtume(s.a.w.w) , kwani Mtume wa Mwenyezi Mungu alipo chukuliwa roho yake alizikwa katika chumba chake, na mlango wa chumba kufungwa, na kaburi lake likawa katikati ya chumba kilicho jengewa kuta na dari, na lau kama sahaba yeyote ange sikia kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kuwa tendo kama hilo ni haram basi wasinge thubutu kumzika Mtume katika chumba hicho kilicho jengewa, na lau kama ingelazimika kumzika chumbani mwake basi ingekuwa wajibu kubomoa chumba hicho ili kaburi hilo lisiwe na jengo au lisiwe ni lenye kujengewa.

Na kutokana na kutofanya kwao hivyo, tukafahamu ya kuwa kujenga juu ya makaburi si haram, sasa vipi itakuwa ni shirki?.

FUAD: Ninakushukuru kwa wema wako kwani umeniongoza kwenye ukweli (haki), na kunijulisha ya kuwa kujenga juu ya makaburi si haram wala shirki, na kwamba wale ambao wanaharamisha jambo hilo hawana dalili yoyote katika sheria wawezayo kuitegemeza kwayo kauli yao.Na kwa hakika mimi nitakushukuru daima juu ya hili.

JAAFAR: Nami ninakushukuru kwa kukubali kwako ukweli na haki baada ya kuifahamu, na kuufuata kwako uongofu pale ulipo uona, kwani wewe ni mwenye kufuata muongozo wa akili na mantiki sahihi, kwa hivyo basi ninapenda kukuzidishia maarifa zaidi kuhusiana na haki na ukweli, na kukupatia maarifa mbali mbali katika dini, je unawakati zaidi ili niweze kuzungumza na wewe?

FUAD: Kwa hakika mimi ninapenda sana maneno ya kweli, zungumza ulitakalo, hakika mimi niko tayari kukusikiliza na kuyajaza masikio yangu kwa maarifa.

JAAFAR: Kutokana na mazungumzo yetu yaliyo pita imethibiti kuwa kujenga juu ya makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu ni jambo linalo faa na inajuzu kufanya hivyo, na jambo hilo si haram.

FUAD: Ndio.. nami niko pamoja nawe katika hilo.

JAAFAR : Hivi sasa nataka kusema hivi: Hakika kujenga juu ya makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu na kuweka madharihi juu yake na kujenga makuba.. yote hayo ni sunna, hupewa thawabu mwenye kuyafanya hayo yote, si tu kwamba inajuzu.

FUAD : Vipi inakuwa sunna?

JAAFAR : Mwenyezi Mungu mtukufu amesema:( Na anayeziheshimu alama za Mwenyeezi Mungu basi hayo ni katika unyenyekevu wa nyoyo). Kwa hivyo kila kitu ambacho huzing atiwa na kuhesabiwa kuwa ni katika shiari za Mwenyezi Mungu kukitukuza ni sunna katika Uislaam.

FUAD: Ndio..lakini vipi itakuwa kujenga juu ya makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu ni katika shiari za Mwenyezi Mungu?

JAAFAR: Shiari ni vitu ambavyo huitukuza dini katika mtizamo wa ulimwengu bila kuwepo dalili juu ya uharamu wake.

FUAD: Je dini hutukuzwa kwa majengo na makuba hayo?

JAAFAR : Ndio.

FUAD: Ki vipi?

JAFAAR: Kujengea makaburi ya maulamaa na viongozi watukufu wa kiislaam, na kujenga makuba juu yake, na kuyahifadhi yasiharibike na yasibomoke, ni kuwatukuza watukufu hao bila shaka yoyote. Kwa mfano: Akijitokeza mtu fulani na kupanda uwa waridi kwenye kaburi la mtu alie kufa, je mtu huyu haonekani kuwa amemtukuza maiti yule, na kuwa amemuenzi?

FUAD : Ni sahihi.

JAAFAR : Vipi ikiwa atajenga juu ya kaburi lake jengo kubwa na kuweka kuba juu yake, hakika kufanya hivyo ni kumtukuza na kumuenzi maiti huyo bila shaka yoyote. Na kuwatukuza viongozi na maulamaa wa kiislaam pia maimamu na mawalii.. ni kuutukuza Uislaam, na kuitukuza na kuienzi dini ambayo watu hawa walikuwa wakiilingania, na wakiwaelekeza watu kwenye dini hiyo. Je mtu fulani anapo mtukuza Raisi wa chama fulani, au walinganiaji wa itikadi za chama hichohuzingatiwa kuwa ni mwenye kukitukuza chama kile na itikadi ile au laa?

FUAD: Ndio ni kama usemavyo.

JAAFAR: Kwa hivyo basi kuyajengea makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu ni kuwatukuza wao na kumtukuza Mwenyezi Mungu, na ni kuuinua na kuutukuza Uislamm, na kila kitu ambacho kukifanya kutakuwa ni kumtukuza Mwenyezi Mungu na ndani yake kuna kuuinua Uislaam, kitu hicho ni katika shiari za Mwenyezi Mungu ambazo anahimiza kuzifanya, kwani anasema:Suratul- haji aya 32.

FUAD: Kwa hivyo..kuvunja na kubomoa maka buri ya mawalii na Mitume na maimam, inakuwa ni kuidhalilisha dini, na kuutia dosari utukufu wa kiislaam.. kwani kuyabomoa ni kuwadharau viongozi wetu, na ni kuwahini wao.. na kuwahini wao ni kuihini dini, na kuutia dosari utukufu wao ni kuutia dosari utukufu wa Uisalaam.

JAAFAR: Na mimi pia nimekuwa Shia, na nimefuata madhehebu ya Ahlil-bayti (a.s) na nimebadilisha jina kutoka jina la Waliid na kuwa Jaafarkwa sababu hii hii? Kwa hakika mimi wakati nilipo kuwa nikifuata rai za watu wengine sikuwa nikidha nia ya kuwa hakuna alie kwenye haki kinyume changu mimi, lakini nimeitafuta haki na kuifuata hadi kuifikia. Na mtu wakati wote anapo acha nyuma na kuzitupilia mbali asabia za madhehebu, na kukifungua kifua chake kwa ajili ya kuikubali haki, na kuitafuta haki.. hapana budi ataifikia haki hiyo na kuipata.

FUAD: Mimi, na baada ya msimamo na mawkifu haya, nitakuwa makini katika mambo mbali mbali, na nitakuwa ni mwenye kuitafuta haki, mpaka niweze kuifuata haki kokote nitako ikuta. Na kwa hakika nitakushukuru kwa muda wote.. Basi niruhusu nende zangu kwani nina ahadi na mtu fulani.

JAAFAR: Nenda, Mwenyezi Mungu akulinde.

FUAD : Fii amani llahi.

JAAFAR : Uwe katika amani ya Mwenyezi Mungu.

Abu haatam Ar-raziy katika kitabu chake (Az-ziinah) anasema: Kwa hakika jina la kwanza lililo dhihiri katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu ni Shia, na jina hili ndilo lililo kuwa jina mashuhuri (Laqab) la masahaba wane nao ni: Abu Dharri Salman Miqdaad na Ammar.

Na Shekh Mohammad Husein Kaashiful-Ghitaa katika kitabu chake kiitwacho (Aslush-shia wa Usuuliha) anasema: Hakika mbegu ya mwanzo ya Ushia iliwekwa na kupandikizwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) tangu zama za mwanzo kuanza kueneza Uislaam bila ya kutofautisha kati ya vitu viwili hivyo na vikiwa sawa.

Na ushahidi ni hadithi zake tukufu si kupitia njia za Mashia na upokezi wa wapokezi wa Kishia Imamiyyah pekee bali ni hadithi za maulamaa wa kisunni na wanazuoni wao na kupitia njia zao wanazo ziamini ambazo hazidhaniwi kuwa zina chembe ya uongo, na katika hadithi hizo ni hadithi iliyo pokelewa na Suyuut katika kitabu chake (Ad-durrul-manthuur fii tafsiri kitabillahi bil-ma'athur) katika kuitafsiri kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu:(Hao ndio viumbe bora) (suratul bayyinah aya 7). Ame sema: Ametoa hadithi Ibn Asakir kutoka kwa Jaabir bin Abdillahi amesema: Tulikuwa kwa Mtume(s.a.w.w) mara akatokea Ali na kuingia na Mtume(s.a.w.w) akasema: Nina apa kwa haki ya yule ambae nafsi yangu iko mikononi mwake hakika huyu na wafuasi (Mashia) wake ndio walio faulu na kufuzu siku ya kiama. Na hapo ikatelemka aya isemayo:(Hakika wale ambao waliamini na kufanya matendo mema hao ndio viumbe bora). (Suratul-bayyinah aya 7). Ibnu Hisham katika Siir atun-nabawiyyah anasema:Hakika umma wa kiarabu uligawanyika katika makundi mawili Masunni na Mashia tangu siku ya Sakifa.

Muhammad Abu Zuhra anasema katika kitabu chake kiitwacho Taarikhul-madhaahibil-islaamiyyah:(Ushia ni madhehebu ya kiislaam ya kisiasa ya tangu muda mrefu na Mashia walidhihiri na madhehbu yao hayo tangu mwishoni mwa zama za Uthuman na kukua na kupata nguvu katika zama za ukhalifa wa Ali, kwani kila alipo pata nafasi ya kuchanganyika na watu walizidi kupendezewa na kuvutiwa kutokana na kipawa chake na kutokana na nguvu ya Imani yake ya dini na elimu yake).

Ibnu Abil-hadiid anasema katika kitabu chake Sharhu Nahjul-balagha:(Hakika Mashia katika zama za dola na utawala wa Muawia walikuwa wakifadhilisha kuitwa Al-kitabiy na wasiitwe Shia. Kwani Ushia anwani yake na shiari yake ni kushikamana na Ahlul-bayti na kufuata elimu yao na kujiepusha na watu wa Bidaa (Uzushi) na kushikamana na kizazi kitwaharifu na kilicho pambika na tabia njema na bora kabisa) (Rejea kitabu Taarikhul-firaqil-islaamiyyah cha Shekh Muhammad Khaliil Az-zayni ukurasa wa 108-109).

Neno Sunnah: Lenye shadda, asili ya neno hilo ni njia, na neno hilo limepanuka maana yake katika makundi tofauti, na linapo tumika huwa lina maana ya aliyo yafanya Mtume (s.a.w) kama kauli vitendo au aliyo yakataza na kuyakemea, na hutumika katika maana hizo kupitia ndimi za wanazuoni na hadithi za Mtume(s.a.w.w) . Na katika zama za hivi karibuni neno Sunnah limekuwa likitumika katika mukabala wa neno Shia, na Husemwa: As-sunnatu wal-jamaah katika mukabala wa watu maalum, na katika ufahamu wa Shekh wa madhehebu ya Hanbali Ibnu Taimiyyah: Neno Sunnah: lina maana ya kumpenda Ali Uthmani na kumtanguliza Abubakar na Omar kwa wawili hao walio tangulia.

Na madhehebu yalipokithiri na makundi kuwa mengi, baadhi wakashikamana na rai isemayo kuwa tamko Sunni lilikuwa likitumika kwa mtu ambae anafuata dini kwa kuwapenda na kuwatawalisha mashekhe wawili, (Abubakar na Omar), na ilikuwa ikisemwa Sunaatul-umariyyh) Rejea kitabu Tariikhul-firaqil-islaamiyyah ukurasa 44-45).

6 UKWELI WA USHIA

KUPAMBWA KWA MAKABURI YA MAIMAM

KHALID : Salaamun alaykum.

BAAQIR : Wa alaykumus-salaam warahmatullahi wabarakatuhu.KHALID : Umefanya vizuri umekuja lini?

BAAQIR : Nimekuja kumtembelea mtoto wa ami yangu anaishi hapa.KHALID : Nakuomba leo hii ukaribie nyumbani kwetu.

BAAQIR : Kwa hakika ninakazi nyingi nilizo ziacha kwa ajili ya kuwatembelea ndugu (kuunga udugu) na kuomba unisamehe sana kwa wito huo.

KHALID : Haiwezekani..marafiki wawili baada ya kutengana kwa muda wa miaka kumi wanakutana kisha wasibakie na kufuatana walau kwa muda wa saa moja. Hakika mimi -pia nina haki ya udugu wa kiislaam. Kisha kulitokea mazungumzo kati yangu na ndugu yangu mmoja muumini kuhusiana na maudhui ya Shia na Sunna na kutokana na kuwa mimi ninamatumaini na imani na wewe ninataka na ninakusudia kufanya mazungumzo na wewe kuhusu maudhui hayo ili niweze kuelewa ukweli na uhaki katika maudhui hayo.

BAAQIR : Hakuna shaka. Walifuatana pamoja hadi nyumbani kwa Khalid, na kufika nyumbani kwake, na kila mmoja akaketi pembezoni mwa mwenziwe. Na baada ya kuzungumza kuhusiana na mambo yanayo wahusu na yaliyo maalum kwa ajili yao wawili, Baaqir akamuwahi mwenzie kwa kumuuliza swali na kusema: Ni mazungumzo gani yaliyo fanyika kati yenu?

KHALID : Mazungumzo yalikuwa yakihusiana na kuyapamba makaburi ya Manabii, maimam, maulamaa, waumini na watu wema na mfano wa hao, kwa Dhahabu na Fedha na mapambo mengineyo.

BAAQIR : Ni tatizo gani lililopo kuhusiana na jambo hilo?

KHALID : Je kufanya hivyo si haram?

BAAQIR : Kwanini iwe haram?

KHALID : Je maiti anafaidika na mapambo hayo?

BAAQIR : Hapana, hafaidiki nayo.

KHALID : Kwa hivyo, hayo yote ni Israfu na matumizi mabaya, na Mwenyezi Mungu anasemaWala usitawanye (mali yako) kwa ubadhirifu. Hakika watumiao kwa ubadhirifu ni ndugu za mashetani. suratul- israai aya 26-27.

BAAQIR : Unasemaje kuhusiana na nguo ifunikwayo juu ya Kaaba na mapambo yake, na Dhahabu Fedha na vitu ambavyo vipo juu ya Kaaba na ndani ya Kaabah?

KHALID: Sijui.

BAAQIR : Ndio, Kaaba ina nguo ambayo hufunikwa juu yake, na kuna Dhahabu nyingi, ambayo watu huitoa zawadi kwa ajili ya Kaaba kutoka sehemu tofauti za Dunia tangu zama za ujahilia hadi katika zama zetu hizi. Ibnu Khaladuni[14] anasema katika utangulizi wa kitabu chake:

[15] Kwa hakika tangu zama za Ujahilia kaumu mbali mbali walikuwa wakiitukuza Kaaba, na wafalme walikuwa wakituma mali na vitu vya thamani kwenye nyumba hiyo kama vile Kisraa na wengineo, Na kisa cha mapanga na nguo zilizo fumwa kwa dhahabu, vitu ambavyo Abdulmutwalib alivikuta chini alipo chimba kisima cha Zamzam ni maarufu sana).

Na Mtume(s.a.w.w) alipo ikomboa Makka alikuta katika kisima kirefu kukiwa na Awqiyah sabini elfu za Dhahabu vitu ambavyo wafalme walikuwa wakizitoa zawadi kwa ajili ya nyumba ya Allah. Na kulikuwa na dinari milioni moja, yaani zenye uzito wa Kintwari milioni mbili. Na Ali(a.s) alisema kumwambia Mtume: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu unaonaje ukitumia mali hii ikakusaidia katika vita vyako? Mtume hakufanya hivyo. Kisha akamwambia Abubakar nae hakuzitoa. (hadi akasema)

(Amesema Abu waail): Niliketi kwa Shaibah bin Othuman nae akasema Aliketi kwa Omar bin Khattab, akasema: Niliazimia nisibakishe katika nyumba hiyo chembe yoyote ya Dhahabu wala Fedha isipokuwa nitaigawa kati ya Waislaam. Nikasema Hutafanya hivyo?

Akasema: Kwanini nisifanye hivyo?

Nikasema: Sahiba wako hakufanya hivyo.

Akasema: Hao wawili ndio ambao hufuatwa nyendo zao.[16]

Je Kaabah ilikuwa ikifaidika na Dhahabu na Fedha hizo ewe Khalid?

Au -Mwenyezi Mungu -ametakasika na hili- alikuwa akifaidika na vitu hivyo viwili?

KHALID : Hapana.

BAAQIR : Pamoja na hayo Mtume(s.a.w.w) hakuunyoosha mkono wake kwenye mali hiyo iliyo kuwa imelimbikizana, wala hakutumia hata chembe moja ya mali hiyo, pamoja na kuwa wakati ule Uislaam ulikuwa ukihitajia sana mali na pesa nyingi wakati ambapo hazina ilikuwa imejaa, kwa ajili ya kuimarisha nguzo zake katika miji na nchi mbali mbali. Kwa nini hakufanya hivyo? Ni kwa sababu mali hiyo nyingi ilikuwa ni mali ya Kaabah na huiongezea Kaabah utukufu na heba yake machoni mwa watu, japokuwa utukufu na daraja yake ya kweli iko kwa Mwenyezi Mungu mtukufu, utukufu ambao haupungui wala kuongezeka, sawa iwe na mali zote za dunia, au isiwe na chochote.

Na maneno ni hayo hayo kuhusiana na makuba ya Dhahabu, na milango ya Dhahabu na Fedha, na nguo ifunikwayo juu yake na mapambo yatolewayo zawadi na kupambwa nayo makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu mtukufu kama vile: Amirul-muuminiin, Imam hasan na Imam Husein, Imam Ridhaa na wengineo juu yao rehma na amani. Watu hawa cheo na daraja yao ya kweli waliyo pewa na Mwenyezi Mungu haipungui wala kuzidi kwa kuwepo madini hayo ya thamani kwenye makaburi yao, na wala haipungui ikiwa hayakuwepo, kwa mfano Imam Hasan bin Ali(a.s) ni bora kuliko nduguye Husein(a.s) japokuwa kaburi la Imam Hasan(a.s) hupigwa na jua katika jangwa la Bakii'i likiwa halikujengewa juu yake au juu yake kukiwa hakuna jengo lolote, na likiwa halikupambwa na pambo la aina yoyote, na kaburi la Imam Husein(a.s) lilikuwa na majengo makubwa makubwa ya dhahabu halisi iangazayo angani na kuyaondoa mawingu.

Lakini tumeyafanya hayo kwa ajili yao, na kutoa zawadi ya mapambo ya Dhahabu kwenye makaburi yao, na makuba ya makaburi yao kuyatia dhahabu na mengineyo, yote hayo kwa ajili ya kuwaenzi na kuwatukuza wao.

KHALID : Je vitu hivi vinawapatia hawa utukufu katika macho ya watu?BAAQIR : Ndio. Na hivi sasa nitakufanya ukiri jambo hilo. Kwa mfano ukienda kwa Mayahudi na kuyaona makaburi ya maulamaa wao yakiwa yameharibika, yakipigwa na jua, hakuna kizuizi chochote juu yake au chumba ambacho mwenye kuyatembelea anaweza kujikinga jua kwenye kivuli chake. Kisha ukenda kwa Wakiristo, na ukakuta makaburi ya maulamaa wao yakiwa yamejengewa vizuri na kuhifadhika, yakiwa yamejengewa makuba na yakiwa yamepambwa kwa dhahabu na fedha, na mapambo mengine ya madini mbali mbali. Je ni maulamaa gani utakao waona kuwa ni wenye utukufu, ni maulamaa wa Mayahudi au Wakiristo, pamoja na kuwa unafahamu ya kuwa wewe ni Muislaam na unafahamu ya kuwa wote wawili wako kwenye batili?

KHALID : Bila shaka kutokana na mandhari ya makaburi ya pande mbili niliyo yaona nitachukua picha fulani ya utukufu wa maulamaa wa Wakiristo, na picha ya udhalili wa maulamaa wa Mayahudi.

BAAQIR : Kwa hivyo basi wayafanyayo Mashia na Masunni kwa kujenga madharihi juu ya makaburi, na kujenga haram na makuba na mengineyo juu ya makaburi ya maimamu na Mitume.. ni kwa ajili ya kuwatukuza wao na kuwaenzi, kwa sababu hiyo huyapamba kwa Dhahabu Fedha na mapambo mengine ya madini mbali mbali.

KHALID : Yote hayo ni sahihi lakini je jambo hilo linakitoa kitendo hicho kwenye sifa ya israfu na matumizi mabaya na yasiyo ya lazima?.BAAQIR : Ndio, na zaidi ya hapo. Ikiwa itathibiti kuwa matendo haya ni kuwatukuza mawalii wa Mwenyezi Mungu, wakati huohuo ni kuutukuza Uislaam, kwani kuwatukuza viongozi na watukufu wa Uislaam ni kuutukuza Uislaam, na kila kitu ambacho ndani yake kuna kuutukuza Uislaam basi kitu hicho ni katika shiari za Mwenyezi Mungu ambazo Mwenyezi Mungu amesema kuhusiana nazo:Kwa hivyo basi kuyapamba makaburi ya mawalii wa Mwenyezi Mungu ni katika shiari za Mwenyezi Mungu ambazo ni sunna kuzifanya na kufanya kazi kwa ajili yake, na mtu mwenye kufanya hivyo hupewa thawabu kwa matendo yake hayo. KHALID : Nakuomba samah ani, kwa kuchukua kiasi hiki cha wakati wako lakini mbele ya Mwenyezi Mungu ni mwenye malipo, kwani umenitoa kwenye kiza cha ujinga na kuniweka kwenye nuru ya elimu na ufahamu, ni kwa kiasi gani nilikuwa nikifikiria kuhusiana na upambaji huu wa makaburi na nisielewe siri yake na faida yake na usahihi wake, kwa hakika hivi leo-wewe- umenitia nuru kwa elimu yako hii, na umenifikisha niliko kuwa nikipakusudia.

BAAQIR : Sasa shaka yote uliyo kuwa nayo kuhusiana na kupamba makaburi imetoweka?

KHALID : Ndio.. hakuna shaka yoyote niliyo bakia nayo kwani kufanya hivyo ni sunna na jambo lililo himizwa na Qur'ani tukufu kwa kauli yake Mwenyezi Mungu:

BAAQIR : Alaa ayyi hal (Kwa hali yoyote ele):Hakika mimi niko tayari kufahamiana nawe katika maudhui kama haya ili niweze kufaidika, au wewe pia ufaidike, na wote kwa pamoja tuwe ni wenye kuyafahamu mambo kwa ufahamu mzuri na wenye mazingatio.

KHALID : Ninakushukuru sana sana, na ninamuomba Mwenyezi Mungu mtukufu akuwafikishe kwa yale ayaridhiayo.

7 UKWELI WA USHIA

KUBUSU MADHARIHI (MAKABURI)

MAALIK: Ewe Swaadiq ni sababu gani iwafanyayo kubusu Dharihi ya kaburi la Mtume na maimam na kutoacha kitendo hicho?

SWAADIQ: Je kuna tatizo (ishkali) lolote kufanya hivyo?

MAALIK: Inasemekana kuwa kufanya hivyo ni miongoni mwa matendo ya shirki.

SWADIQ: Nani asemae kuwa kufanya hivyo ni shirki?

MAALIK: Waislaam ndio wasemao hivyo.

SWADIQ: Ajabu! Basi ni watu gani ambao wanabusu madharihi?MAALIK: Inasemekana kuwa ni kikundi kidogo cha Mashia.

SWADIQ: Je umewahi kwenda hija?

MAALIK: Ninamshukuru Mwenyezi Mungu.. ndio nimefanikiwa kwenda hija.

SWADIQ: Je umelitembelea kaburi la Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w) katika mji wa Madinah?

MAALIK: Ninamshukuru Mwenyezi Mungu nimefanikiwa kulitembelea.SWAADIQ: Je hukuwaona maelfu ya waislaam wa madhehebu ya sunni wakikusudia na kutaka kulibusu dharihi la kaburi la Mtume wa Mwenyezi Mungu na huku wakipigwa na walinzi wa kikundi cha (Hay'atu amri bil-maarufi)?!!

MAALIK: Ndio..

SWAADIQ: Kwa maana hiyo si sisi Mashia pekee tunao busu madharihi ya Mitume wa Mwenyezi Mungu, bali waislaam wote huyabusu.

MAALIK: Sasa kwanini baadhi wanasema kuwa kufanya hivyo ni haram, na kwamba kufanya hivyo ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu mtukufu?

SWAADIQ: Hawa ni watu wachache wa kikundi fulani kati ya makundi ya waislaam, wajionao kuwa wao ndio wenye haki, na kwamba wao ndio waislam wa kweli na wanawaona waislaam wengine kuwa ni makafiri na washirikina wanamuabudu asie kuwa Mwenyezi Mungu, na hawawaoni watu wengine kuwa ni waislaam walio kosea, kwa hivyo ndio maana huwaona wakiyakufurisha madhehebu (makundi) mengine yote ya kiislaam. Je hukuona ile kamati ya (Al-amri bil-maarufi)!! katika nchi ya Hijazi wakimpiga anaekusudia na kutaka kubusu dharihi la kaburi la Mtume(s.a.w.w) na kumwambia:Ewe kafiri! Ewe mshirikina! Ewe zindiki! Ewe nguruwe! Ewe mbwa! Na mengineyo kati ya aina mbali mbali za matusi na tuhuma zilizo mbaya kabisa.

Na matusi hayo humuelekea kila mtu: Sawa awe Shia, Hanafiy, Maalikiy, Shafiiy, Hanbaliy, Zaydiah, na waislaam wengine..[17]

MAALIK: Ndio.. yote hayo nimeyaona, na yaliyo mabaya zaidi kuliko hayo: Kwa hakika mimi niliwaona wakimpiga kichwani mtu mmoja alie ng'ang'ania kufanya hivyo kwa fimbo kiasi kwamba huenda pigo hilo lilipelekea kumpasua na kutoka damu, na wakati mwingine huwapiga kwa mikono yao-kwa nguvu- na wakiwapiga vifuani waislaam walio kuja kufanya ziara mapigo ambayo huwaumiza na kuwadhuru vifua vyao na kuwasababishia maumuvu na maradhi miili yao! Na ni kwa kiwango gani niliumia kwa kuyao mambo hayo na vitendo hivyo!!.

Hija ambayo Mwenyezi Mungu ameifanya kuwa ni kongamano la waislaam wote ulimwenguni ili waweze kuzungumza katika kongamano hilo kuhusu mambo yao mbali mbali, hivi leo imekuwa ni mahala pa kutia tofauti kati ya waislaam kutokana na matendo ya kikundi hicho kidogo kinacho jiita kuwa ni (hay'atul-amri bil-maaruf wannahyi anil-munkar)!!!.SWAADIQ: Ala ayyi hal, ewe Maalik.. je wewe unambusu mwanao?MAALIK: Ndio!

SWADIQ: Je unamshirikisha Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kumbusu mwanao?

MAALIK: Hapana, hapana.. kamwe simshirikishi Mwenyezi Mungu.SWADIQ: Vipi usimshirikishe Mwenyezi Mungu kwa kumbusu mwanao?MAALIK: Kwa hakika mimi ninambusu mwanangu kwa ajili ya mapenzi yangu kwake, na hilo si shirki.

SWADIQ: Je wewe unaibusu Qur'ani?

MAALIK: Ndio.

SWADIQ: Je kwa kufanya kwako hivyo humshirikishi Mwenyezi Mungu?

MAALIK: Hapana.

SWADIQ: Je jalada la Qur'ani unalo libusu si ngozi ya mnyama?MAALIK: Ndio.

SWADIQ: Kwa hivyo wewe unamshirikisha Mwenyezi Mungu, na unaifanya ngozi ya mnyama kuwa ni mshirika wa Mwenyezi Mungu.. ametakasika Mwenyezi Mungu na hilo.

MAALIK: Si hivyo. Kwa hakika mimi ninaibusu Qur'ani kwa sababu imekusanya maneno ya Mwenyezi Mungu, kutokana na mapenzi ya maneno ya Mwenyezi Mungu ndio maana ninalibusu jalada lililo ifunika Qur'ani hiyo, na hii ni kutokana na mapenzi mengi, na wingi wa shauku yangu kwa Qur'ani, ni tofauti iliyoje kati ya kitendo hiki na kumshirikisha Mwenyezi Mungu?

Kisha ninapo ibusu Qur'ani ninapata thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kufanya hivyo, kwa sababu kuibusu Qur'ani ni kuitukuza na kuienzi na kuiinua daraja yake, na kuitukuza Qur'ani kuna thawabu na malipo mbele ya Mwenyezi Mungu, kwa hivyo ni tofauti iliyoje iliyopo kati ya tendo hili na kumshirikisha Mwenyezi Mungu?

SWADIQ: Kwa nini maneno kama hayo usiyasema katika kubusu dharihi la Mtume(s.a.w.w) na madharihi ya maimam(a.s) [18] au unadai ya kuwa wale ambao wanabusu madharihi huvifanya vyuma hivyo kuwa ni washiriki wa Mwenyezi Mungu mtukufu?! Ikiwa ni hivyo kwanini hawabusu vyuma mbali mbali vilivyoko huku na kule katika ardhi? Lakini..kutokana na ukweli kuwa dharihi hilo limefunika kaburi la Mtume(s.a.w.w) au kaburi la mmoja wapo kati ya maimamu(a.s) , kutokana na mapenzi ya Mtume(s.a.w.w) na maimamu na kutokana na shauku yao kwao ndio maana wanalibusu dharihi la kaburi lake kwa sababu wao hawawezi kumfikia Mtume na imamu mwenyewe(a.s).

Pamoja na kufanya kwao hivyo hakika wao hupata malipo kwa Mwenyezi Mungu mtukufu, na hupawa thawabu kwa kufanya hivyo, kwani kulibusu dharihi la mtu fulani ni kumtukuza mtu yule. Na kumtukuza Mtume(s.a.w.w) au mmoja wapo kati ya maimamu(a.s) , ni kuutukuza Uislaam ambao huyu alikuwa ni Mtume wake(s.a.w.w) au alikuwa ni imamu wake alie kuwa akilingania watu kwenye Uislaam huo.

Na jambo lolote litakapo kuwa na sura ya kuutukuza Uislaam basi jambo hilo ni katika shiari za Mwenyezi Mungu ambazo amezizungumzia kwa kusema:suratul-haji aya 32.

MAALIK: Ikiwa ukweli ni huo basi kwanini baadhi ya watu wanasema kuwa nyinyi ni wenye kumshirikisha Mwenye zi Mungu?

SWAADIQ: Imepokelewa katika Hadithi tukufu kama ifuatavyo:(Kwa hakika matendo hufanyika kutokana na Nia) [19] ikiwa mtu yeyote anabusu dharihi na katika kubusu kwake huko anakusudia kumshirikisha Mwenyezi Mungu bila shaka mtu huyo ni mwenye kumshirikisha Mwenyezi Mungu (mshirikina). Na ikiwa kubusu huku kunatokana na mapenzi mengi, na kwa ajili ya kupata thawabu kwa ajili ya kuadhimisha na kutukuza shiari za Mwenyezi Mungu kwa kufanya hivyo, basi hupewa thawabu yule mwenye kuyatekeleza matendo hayo. Na wewe waulize wote wale ambao wanayabusu madharihi kati ya Mashia na Masunni kama ifuatavyo: Kwa nini mnabusu madharihi?

Hata kujibu yeyote kati yao isipokuwa kwa kusema tunafanya hivyo kutokana na mapenzi makubwa na shauku kubwa tuliyo nayo na kwa ajili ya kupata thawabu, na huwezi kumsikia yeyote kamwe-bila shaka yoyote- akisema ya kuwa anabusu dharihi kwa ajili ya jambo lingine tofauti na hili tulilo litaja.

MAALIK: Ni kweli, maneno yako ni sahihi.

SWADIQ: Na ikiwa kubusu peke yake bila kukusudia kumshirikisha Mwenyezi Mungu kunamfanya mtu kuwa mshirikina, bila shaka huwezi kumpata mwanadamu yeyote asie mshirikina, kwani waislaam imma wanabusu madharihi, au wanabusu Qur'ani.. kwa msingi wa hali mbili hizi wao-wote-ni washirikina. Sasa ikiwa hali ni kama hiyo Muislaam ni nani?

MAALIK: Ninakushukuru sana, na kwa hakika mimi nitafanya mazungumzo na majadiliano na baba yangu alie kuwa akinilisha na kunifundisha mambo kama haya ya asabia yasiyo na maana yoyote, na sinto sikiliza maneno ya mtu yeyote wa madhehebu mengine, kwa hakika nimefahamu ya kuwa haki na ukweli uko pamoja nanyi-nyinyi Mashia- na wewe unahaki juu yangu milele, kwa sababu umenionyesha njia, si katika jambo hili tu bali katika mambo yote, ili nisifuate kila kinifikiacho masikioni mwangu, bila ya kufikiria kuhusu usahihi wake na ubatilifu wake.


4

5

6

7

8

9