TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 10617
Pakua: 1288

Maelezo zaidi:

Juzuu 9
Juzuu 1
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 10617 / Pakua: 1288
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

وَقَطَّعْنَاهُمْ فِي الْأَرْضِ أُمَمًا مِّنْهُمُ الصَّالِحُونَ وَمِنْهُمْ دُونَ ذَٰلِكَ وَبَلَوْنَاهُم بِالْحَسَنَاتِ وَالسَّيِّئَاتِ لَعَلَّهُمْ يَرْجِعُونَ ﴿١٦٨﴾

168. Na tukawafarikisha katika ardhi makundi makundi, Miongoni mwao wako walio wema na wengine kinyume cha hivyo. Na tukawajaribu kwa mema na mabaya ili wapate kurejea.

فَخَلَفَ مِن بَعْدِهِمْ خَلْفٌ وَرِثُوا الْكِتَابَ يَأْخُذُونَ عَرَضَ هَـٰذَا الْأَدْنَىٰ وَيَقُولُونَ سَيُغْفَرُ لَنَا وَإِن يَأْتِهِمْ عَرَضٌ مِّثْلُهُ يَأْخُذُوهُ أَلَمْ يُؤْخَذْ عَلَيْهِم مِّيثَاقُ الْكِتَابِ أَن لَّا يَقُولُوا عَلَى اللَّـهِ إِلَّا الْحَقَّ وَدَرَسُوا مَا فِيهِ وَالدَّارُ الْآخِرَةُ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ يَتَّقُونَ أَفَلَا تَعْقِلُونَ ﴿١٦٩﴾

169. Na wakafuatia baada yao wabaya waliorithi Kitab wanachukua vitu vya maisha haya duni na wakasema: Tutasamehewa! Na vikiwajia vingine mfano wake, watavichukua, Je, hawakuchukua ahadi katika Kitab kuwa hawatasema juu ya Mwenyezi Mungu ila haki? Nao wamekwishasoma yaliyomo humo, Na nyumba ya Akhera ni bora kwa wale wenye takuwa Basi je, hamtii akilini?

وَالَّذِينَ يُمَسِّكُونَ بِالْكِتَابِ وَأَقَامُوا الصَّلَاةَ إِنَّا لَا نُضِيعُ أَجْرَ الْمُصْلِحِينَ ﴿١٧٠﴾

170. Na wale wanaoshikamana na Kitab na wakasimamisha Swala, hakika sisi hatupotezi ujira wa watendao mema.

وَإِذْ نَتَقْنَا الْجَبَلَ فَوْقَهُمْ كَأَنَّهُ ظُلَّةٌ وَظَنُّوا أَنَّهُ وَاقِعٌ بِهِمْ خُذُوا مَا آتَيْنَاكُم بِقُوَّةٍ وَاذْكُرُوا مَا فِيهِ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ ﴿١٧١﴾

171. Na tulipouinua mlima ukawa juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawaangukia. Tukawaambia: shikeni kwa nguvu tuliyowapa na yakumbukeni yaliyomo ndani yake ili mpate kuwa na takua.

TUKAWAJARIBU KWA MEMA NA MABAYA

Aya 168-171

MAANA

Na tukawafarikisha katika ardhi makundi makundi.

Mwenyezi Mwenye aliwatawanya Waisraili makundi na vipote mbalimbali, hawana nchi inayowaweka pamoja wala dola inayowalinda.

Uzayuni umejaribu kuwawekea dola kutoka mto Naili hadi Furat kwa kunyang’anya kimabavu. Wanafikiria kuwa uadui wa Israil utapata unayoyataka, wakisahau kuwa dola ya Israili ni ya kupandikizwa tu na kwamba iko siku litawatokea la kuwatokea na mambo yote ya viumbe yako mikononi mwa Mwenyezi Mungu, sio mikononi mwa uzayuni na ukoloni.

Miongini mwao wako walio wema na wengine kinyume cha hivyo.

Kwa dhahir ni kuwa makusudio ya wema hapa ni imani na kinyume cha hivyo ni wasiokuwa waumini. Umetangulia mfano wake katika Aya 159 ya Sura hii.

Na tukawajaribu kwa mema na mabaya ili wapate kurejea.

Makusudio ya mema ni afya na raha, na mabaya ni kinyume chake. Lengo la kupewa mema na mabaya ni kulipwa uongofu wao na kutubia kwa Mola wao.

Na wakafuatia baada yao wabaya waliorithi Kitab wanachukua vitu vya maisha haya duni na wakasema: Tutasamehewa! Na vikiwajia vingine mfano wake, watavichukua.

Makusudio ya maisha haya duni, ni dunia na vitu vya maisha duni; kama riba na rushwa.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja kwamba wakati wa Nabii Musa(a.s) kulikuwa na watu wema miongoni mwa wana wa Israil na wengine wasiokuwa wema, aliendelea kusema kuwa wote hao wameacha kizazi kilichojua halali ya Tawrat na haramu yake, lakini wakawa wanahalalisha haramu na wakiharamisha halali, huku wakisema: Mwenyezi Mungu atatughufria wala hatatuadhibu na kitu chochote. Kwa sababu sisi ni watoto wake wapenzi na ni taifa lake teule.

Unaweza kuuliza : Kwanini Mwenyezi Mungu amesema: “Wanachukua vitu vya maisha haya” tena akasema: “Vikiwajia mfano wake, wanachukua?” pamoja na kuwa kauli mbili ziko kwenye maana moja? Je, kuna lengo gani la kukaririka huku?

Lengo ni kuwakanya kwa vile wao wanang’ang’ania madhambi makubwa na kuyarudia mara kwa mara bila ya kujali na huku wakisema kuwa Mungu atatusamehe. Ikiwa kuendelea na madhambi madogo yanageuka kuwa makubwa, je kuendelea na makubwa itakuwaje?

Je, hawakuchukua ahadi katika Kitab kuwa hawatasema juu ya Mwenyezi Mungu ila haki? Nao wamekwishasoma yaliyomo humo.

Hili ni kemeo la pili kwao. Anawakemea kwa madai yao kuwa wao wana- iamini Tawrat na kwamba wameisoma na kuyafahamu yaliyomo. Na katika yaliyokuja katika Tawrat ni kwamba Mwenyezi Mungu anamsamehe mwenye kutubia na akayang’oa madhambi yake. Ama mwenye kung’ang’ania basi yeye ni katika walioangamia.

Vilevile Tawrat imechukua ahadi kuwa kila mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu na hiyo Tawrat, basi asimzulie Mungu uwongo. Na waasi hao wanajua hakika hii, lakini bado wanaendelea na madhambi makubwa huku wakisema: “Mungu atatusamehe.” Huku ni kuvunja ahadi na kumzulia Mungu.

Na nyumba ya Akhera ni bora kwa wale wenye takua hawarukii maisha ya dunia hii wala hawasemi uwongo na uzushi kuwa Mungu atatusamehe.

Basi je, hamtii akilini?

Vipi atatia akilini ambaye akili yake imetekwa na matamanio yake na moyo wake ukatiwa maradhi na hawaa yake?

Na wale wanaoshikamana na Kitab na wakasimamisha Swala, hakika sisi hatupotezi ujira wa watendao mema.

Wanoshikamana na kitabu ni wale wanaotenda kulingana nacho. Anayeshikamana na kitu hasa ni yule anayetenda, kwa sababu anahisi uthabiti na azma ya kufanya.

Ameunganisha kushikamana na Kitab na kusimamisha Swala katika hali ya kuungania mahsus kwenye ujumla, kwa sababu ya siri iliyowajibisha mahsus.

Aya inawataaradhi Mayahudi ambao wameamini Tawrat na wasitumie hukumu zake. Vilevile kumtaaradhi kila mwenye kunasibika kwenye dini na akapuuza hukumu zake; hasa Swala ambayo ndiyo nguzo ya dini, lakini vijana wa sasa wameiweka pembeni.

Na tulipouinua mlima ukawa juu yao kama kwamba ni kiwingu kilichowafunika na wakadhani kuwa utawangukia. Tukawaambia: Shikeni kwa nguvu tuliyowapa na yakumbukeni yaliyomo ndani yake ili mpate kuwa na takua.

Mwenyezi Mungu aliwainulia wana wa Israil mlima ukawa kama kiwingu kilichowafunika, kuwahofisha ili wamche Mungu, lakini Waisraili ni Waisraili tu… Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:63).

وَإِذْ أَخَذَ رَبُّكَ مِن بَنِي آدَمَ مِن ظُهُورِهِمْ ذُرِّيَّتَهُمْ وَأَشْهَدَهُمْ عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ أَلَسْتُ بِرَبِّكُمْ قَالُوا بَلَىٰ شَهِدْنَا أَن تَقُولُوا يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّا كُنَّا عَنْ هَـٰذَا غَافِلِينَ ﴿١٧٢﴾

172. Na Mola wako alipowaleta katika wanadamu kutoka miongoni mwa kizazi chao, na akawashuhudiza juu ya nafsi zao. Je, mimi si Mola wenu? Wakasema: Kwa nini! Tumeshuhudia, Msije mkasema siku ya Kiyama kuwa sisi tulikuwa tumeghafilika na haya.

أَوْ تَقُولُوا إِنَّمَا أَشْرَكَ آبَاؤُنَا مِن قَبْلُ وَكُنَّا ذُرِّيَّةً مِّن بَعْدِهِمْ أَفَتُهْلِكُنَا بِمَا فَعَلَ الْمُبْطِلُونَ ﴿١٧٣﴾

173. Au mkasema, baba zetu ndio walioshirikisha zamani, nasi tulikuwa kizazi nyuma yao, basi utatuangamiza kwa waliyofanya wabatilifu.

وَكَذَٰلِكَ نُفَصِّلُ الْآيَاتِ وَلَعَلَّهُمْ يَرْجِعُونَ ﴿١٧٤﴾

174. Na kama hivyo tunazipambanua ishara, kwa kutaraji kuwa watarejea.

JE MIMI SI MOLA WENU?

Aya 172 –174

MAANA

ULIMWENGU WA CHEMBE CHEMBE

Na Mola wako walipowaleta katika wanadamu kutoka migongoni mwa kizazi chao, na akawashuhudiza juu ya nafsi zao. Je, mimi si Mola wenu? Wakasema: Kwanini! Tunashuhudia” Msije mkasema siku ya Kiyama kuwa sisi tulikuwa tumeghafilika na haya.

Katika Waislamu kuna kikundi kinachoamini ulimwengu wa chembe chembe. Maana yake, kinasema, ni kuwa baada ya Mwenyezi Mungu kumuumba Adam, alitoa mgongoni kwake kila mwanaume na mwanamke watakaozaliwa baadaye kuanzia Adam wa kwanza mpaka mwisho wa ulimwengu. Akawakusanya wote pamoja wakiwa na umbo la chembe chembe, kisha akawaambia. Je, mimi si Mola wenu? Wakasema ndiye Mola wetu. Baada ya kukiri hivi akawarudishia mgongoni mwa Adam.

Sisi tuko tayari kuwaunga mkono wale wanaoamini ulimwengui wa chem- be iwapo watatujibu maswali haya yafuatayo:

Je, ni wapi alikusanya Mwenyezi Mungu chembe chembe hizi, Ni katika ardhi hii au nyingine? Je, ardhi hii iliwatosha kwa sababu walikuwa kwenye umbo la chembe. Je, Adam alikuwa mkubwa kiasi cha kuweza kuchukua kila atakayetoka kwake moja kwa moja na kupitia wengine mpaka siku ya ufufuo?

Kisha je, katika rundo hilo linalozidi idadi ya mchanga anaweza kukum-buka mmoja tu maneno hayo na ahadi hiyo aliyompa Mwenyezi Mungu kwa mdomo? Ikiwa ameisahau kwa sababu ya muda mrefu. Je, Mwenyezi Mungu atakuwa na hoja kwake kwa kitu asichokikumbuka?

Haya ni katika upande wa akili, yaani baadhi ya yanayozunguka akilini. Ama katika upande wa

Aya, ni kwamba inafahamisha kinyume na ulimwengu wa chembe chembe, uliochukuliwa kutoka katika mgongo wa Adam wa kwanza. Kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema: Mola wako alipowaleta katika wanadamu, na wala hakusema katika Adam. Na ilivyo ni kuwa mwanadamu anaweza kuitwa Adam, lakini Nabii Adam wa kwanza hawezi kuitwa mwanadamu.

Vilevile Mwenyezi Mungu anasema kutoka migongoni mwao na hakuse- ma kutoka mgongoni mwake. Akasema , kizazi chao na hakusaema kizazi chake. Zaidi ya haya ni kwamba Mwenyezi Mungu anasema katika Aya ya pili kwamba amefanya hivi ili asiwe na hoja yeyote ya shirk ya mababa, ambapo mshirikina wa kwanza hawezi kutoa hoja ya ushirikina wa baba yake.

Ikiwa haya yote yanafahamisha kitu, basi kitu chenyewe ni kwamba ahadi ilichukuliwa kwa kila mmoja peke yake baada ya kupatikana kwake, bali na baada ya kuongoka na kutambua kwake.

Sisi hatujui maana nyingine ya ahadi hii, inayochukuliwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu kutuoka kwa mwanadamu, zaidi ya maumbile na silika ya maandalizi ambayo Mwenyezi Mungu ameipa kila akili, na ambayo lau mtu anakusudia kufahamu, hupambanua baina ya uongofu na upotevu na baina ya haki na batili. Na kwa silika hiyo huongoka kwenye imani ya Mwenyezi Mungu na dini yake ya haki.

Kwa maneno mengine ni kwamba kila mtu ni lazima afikirie ishara za Mwenyezi Mungu na dalili zake.

Wameafikiana Waislamu wote kwa kauli moja kwamba Hadith za Mtume ni tafsir na ubainifu wa Aya za Qur’an. Imethibiti Hadith Mutawatir inayosema: “Kila anayezaliwa huzaliwa katika umbile (safi). Wazazi wake ndio watakaomfanya Myahudi au Mnaswara (Mkristo) au Mmajusi.” Na ile isemayo: “Mwenyezi Mungu anasema: Hakika mimi nimewaumba waja wangu wakiwa wameachana na upotofu, kisha huwajia mashetani na kuwaepusha na dini yao.”

Na akawashuhudiza juu ya nafsi zao, Je, mimi sio Mola wenu? Wakasema: Kwanini! Tumeshuhudia.

Swali na jawabu yako mpaka leo ni hayo hayo mpaka siku ya mwisho. Kwa sababu ni lugha ya hali na matukio, sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَقَالَ لَهَا وَلِلْأَرْضِ ائْتِيَا طَوْعًا أَوْ كَرْهًا قَالَتَا أَتَيْنَا طَائِعِينَ ﴿١١﴾

“Akaiambia (mbingu) na ardhi: Njooni kwa hiyari au kwa nguvu! Zikasema: Tumekujia hali ya kuwa watiifu” (41:11).

Msije mkasema siku ya Kiyama kuwa sisi tulikuwa tumeghafilika na haya.

Haya, ni Tawhid inayofahamishwa na kauli yake: “Je, mimi si Mola wenu?” Hakuna sababu wala udhuru, si katika maisha haya wala ya akhera, kwa aliyepewa na Mwenyezi Mungu maanadalizi kamili ya kufahamu dalili na hoja juu ya umoja wa Mwenyezi Mungu na ukuu wake, kisha akakufuru na akashirikisha.

Au mkasema: Hakika baba zetu ndio walioshirikisha zamani, nasi tulikuwa kizazi nyuma yao, basi utatuangamiza kwa waliofanya wabatilifu?

Mtu hufuata vitu ambavyo anahitaji kujihusisha navyo na kumaliza miaka kadhaa ya kusoma; kama vile udaktari, uhandisi n.k. Ama utambuzi wa kimaumbile ambao haukalifishi mtu zaidi ya kuzinduka na kuamka, kama vile kuwako Mwenyezi Mungu na umoja wake, yote hayo yako sawa.

Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesimamisha dalili zenye kutosheleza juu ya umoja wake, na akaipa kila akili maandalizi ya kuufahamu kwa wepesi.

Kwa hiyo haikubaki udhuru wa mwenye kusema kuwa yeye amekanusha au kushirikisha kwa kuwafuata wengine wabatilifu. Wala hakuna tofauti kabisa katika mtazamo wa akili baina ya anayefanya bila elimu yake kwa makusudi na yule anayefuata batili kwa ujinga bila ya kukusudia, lakini ana uwezo wa kujua na kupambanua.

Na kama hivyo tunazipambanua ishara, kwa kutaraji kuwa watarejea kwenye akili zao ambazo, kwa vyovyote zikisaidiwa na dalili, zitawapeleka kwenye itikadi ya Tawhid.

Angalia Juz, 7 (6:41) kifungu ‘Mwenyezi Mungu na maumbile.

وَاتْلُ عَلَيْهِمْ نَبَأَ الَّذِي آتَيْنَاهُ آيَاتِنَا فَانسَلَخَ مِنْهَا فَأَتْبَعَهُ الشَّيْطَانُ فَكَانَ مِنَ الْغَاوِينَ ﴿١٧٥﴾

175. Na wasomee habari za yule tuliyempa ishara zetu, kisha akajivua nazo na shetani akamwandama akawa miongoni mwa waliopotea.

وَلَوْ شِئْنَا لَرَفَعْنَاهُ بِهَا وَلَـٰكِنَّهُ أَخْلَدَ إِلَى الْأَرْضِ وَاتَّبَعَ هَوَاهُ فَمَثَلُهُ كَمَثَلِ الْكَلْبِ إِن تَحْمِلْ عَلَيْهِ يَلْهَثْ أَوْ تَتْرُكْهُ يَلْهَث ذَّٰلِكَ مَثَلُ الْقَوْمِ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا فَاقْصُصِ الْقَصَصَ لَعَلَّهُمْ يَتَفَكَّرُونَ ﴿١٧٦﴾

176. Na kama tungelitaka tungelimuinua kwazo. Lakini yeye akashikilia ardhi na akafuata hawaa yake. Basi mfano wake ni kama wa mbwa, ukimhujumu hutweta na ukimwacha pia hutweta. Huo ni mfano wa watu waliozikadhibisha ishara zetu, Basi simulia visa, huenda wakatafakari.

سَاءَ مَثَلًا الْقَوْمُ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا وَأَنفُسَهُمْ كَانُوا يَظْلِمُونَ ﴿١٧٧﴾

177. Huu ni mfano muovu kabisa wa watu wanaokadhibisha ishara zetu na wakajidhulumu nafsi zao.

TUMEMPA AYA ZETU AKAJIVUA

Aya 175 – 177

MAANA

Na wasomee habari za yule tuliyempa ishara zetu, kisha akajivua nazo na shetani akamwandama akawa miongoni mwa waliopotea.

Maneno hapa anaambiwa Mtume Muhammad(s.a.w.w) , Wanaosomewa ni Mayahudi. Ama yule ambaye Mwenyezi Mungu amempa ishara akajivua nazo, hatumjui ni nani, nasi hatujiingizi katika kitu kisichokuwa katika Qur’an wala Hadith Mutawatir, lakini wasimulizi wa visa na wafasiri wengi wanasema kuwa mtu huyo alikuwa akiitwa Balam Bin Baur, na kwamba yeye alikuwa kwenye dini ya Nabii Musa na mjuzi wa hukumu zake, kisha akartadi.

Sisi tunaangalia nukuu hii na nyingine kwa hadhari, wala hautulii moyo ila kwa nukuu ya Qur’an. Na nukuu hii inafahamisha tu, kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume awape habari Mayahudi juu ya Kisa cha mtu ambaye alikuwa akijua dini ya Mwenyezi Mungu na ishara zake, kisha akahadaliwa na shetani akaacha ilimu yake na dini, akashikamana na upotevu, akawa miongoni mwa wapotevu walioangamia. Kama kawaida maulama wa kiyahudi walikuwa wakimjua mtu huyu.

Na kama tungelitaka tungelimuinua kwazo.

Yaani kwa aliyompa Mwenyezi Mungu kujua ishara zake, Lakini Mwenyezi Mungu hakutaka kumlazimisha kuzitumia ishara zake. Kwa sababu Mwenyezi Mungu mtukufu hawapeleki watu kwa matakwa ya kuumba ambayo ni kukiambia kitu kuwa kikawa. Isipokuwa huwapeleka kwa matakwa ya nasaha na mwongozo yanayoitwa amri zake na makatazo yake. Kwa hiyo akamwachia yule aliyejivua na ishara zake, uhuru na hiyari, akachagua dunia kuliko akhera.

Lakini yeye akashikilia ardhi na akafuata hawaa yake.

Makusudio ya ardhi hapa ni starehe za maisha ya dunia, kwa sababu ardhi ndio chimbuko lake. Maisha yenyewe ni pamoja na starehe na anasa. Maaana ni kuwa huyu aliyejivua amemwasi Mola wake akatii hawaa yake akiwa ameishikilia haiachi.

Razi anasema kuwa Aya hii ni kali zaidi kwa mwenye elimu. Mtume wa Mwenyezi Mungu anasema: “Mwenye kuzidi elimu, lakini asizidi uongofu hatazidi kwa Mwenyezi Mungu ila kuwa umbali.”

Basi mfano wake ni kama wa mbwa, ukimhujumu hutweta na ukimwacha pia hutweta.

Mbwa anayepumua kwa nguvu na kutoa ulimi kwa kiu au kuchoka (kuhaha) anaendelea tu, ukimkemea au ukimwacha yeye ataendelea hivyo hivyo.

Vilevile mwenye kushikilia hawaa yake huendelea katika upotevu wake umwonye au umwache yeye hupotea tu.

Huo ni mfano wa watu waliozikadhibisha ishara zetu.

Yaani hiyo ndiyo hali ya kila mwenye kuendelea na maasi, daima hanufaiki na ishara wala hazingatii mawaidha. Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa mwenye kupumua na kutoa ulimi na mwasi mwenye kuendelea kwa kuishiria uduni wake.

Basi simulia visa, huenda wakatafakari.

Yaani “Ewe Nabii Muhammad(s.a.w.w) wasimulie mayahudi kuhusu wakale wao na yaliyowafikia, kama watu wa kijiji kilichokuwa ufukweni mwa bahari na huyu aliyejivua ili yawe ni mazingatio kwao na kuwakanya kukadhibisha utume wako.

Huu ni mfano muovu kabisa wa watu wanaokadhibisha ishara zetu na wakajidhulumu nafsi zao.

Kumzulia Mwenyezi Mungu uwongo na kuzikadhibisha ishara zake, yote hayo ni uzushi, Hali ya kwanza inathibitisha katika dini yasiyokuwamo.

Ya pili inakanusha yaliyomo, na huo ndio uzushi (bid’a) hasa, na kila uzushi ni upotevu, na kila upotevu ni katika moto. Kwa hiyo mwenye kuzua ameidhulumu nafsi yake kuiingiza kwenye adhabu na maangamizi.

Utauliza : mwenye kuipindua haki kwa kuhofia nafsi yake na dhalimu, je, anahisabiwa kuwa mzushi?

Jibu : Ndio, ni mzushi anayestahiki adhabu, hilo halina shaka. Kwa sababu ni juu yake kuhofia ghadhabu ya Mwenyezi Mungu kwa kuipindua haki sio ghadhabu ya dhalimu kwa kuithibitisha haki.

Inawezekana mtu kuacha kufanya haki kwa kujikinga na madhara, lakini kuipindua dini kwa kumzulia Mwenyezi Mungu uwongo, hakuna sababu yoyote, vyovyote itakavyokuwa.

مَن يَهْدِ اللَّـهُ فَهُوَ الْمُهْتَدِي وَمَن يُضْلِلْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْخَاسِرُونَ ﴿١٧٨﴾

178. Atakayeongozwa na Mwenyezi Mungu ndiye aongokaye, na atakayepotezwa, basi hao ndio watakaopata hasara.

وَلَقَدْ ذَرَأْنَا لِجَهَنَّمَ كَثِيرًا مِّنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ لَهُمْ قُلُوبٌ لَّا يَفْقَهُونَ بِهَا وَلَهُمْ أَعْيُنٌ لَّا يُبْصِرُونَ بِهَا وَلَهُمْ آذَانٌ لَّا يَسْمَعُونَ بِهَا أُولَـٰئِكَ كَالْأَنْعَامِ بَلْ هُمْ أَضَلُّ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْغَافِلُونَ ﴿١٧٩﴾

179. Na hakika tumewaumbia Jahannam majini wengi na watu. Wana nyonyo, lakini hawafahamu kwazo, na wana macho, lakini hawaoni kwayo, na wanayo masikio, lakini hawasikii kwayo. Hao ni kama wanyama bali wao ni wapotevu zaidi, Hao ndio walioghafilika.

وَلِلَّـهِ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَىٰ فَادْعُوهُ بِهَا وَذَرُوا الَّذِينَ يُلْحِدُونَ فِي أَسْمَائِهِ سَيُجْزَوْنَ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٨٠﴾

180. Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri, Basi mwombeni kwayo, Na waacheni wale wanaoharibu utakatifu wa majina yake, watalipwa waliyokuwa wakiyatenda.

وَمِمَّنْ خَلَقْنَا أُمَّةٌ يَهْدُونَ بِالْحَقِّ وَبِهِ يَعْدِلُونَ ﴿١٨١﴾

181. Na miongoni mwa tuliowaumba wako watu wanaoongoza kwa haki na kwayo wafanya uadilifu.

ATAKAOWAONGOZA MUNGU NDIO WATAKAOONGOKA

Aya 178 – 181

MAANA

Atakayeongozwa na Mwenyezi Mungu ndiye aongokaye, na atakayepotezwa, basi hao ndio watakaopata hasara.

Makusudio sio kuwa yule aliyeumbiwa kuongoka ndiye atakayeongoka na kwamba aliyeumbiwa kupotea ndiye mpotevu. Hapana si hivyo! Maana haya yanakataliwa na maumbile na hali ilivyo; Kwa sababu Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.

Vilevile inakataliwa na nukuu ya Qur’an:

فَمَنِ اهْتَدَىٰ فَإِنَّمَا يَهْتَدِي لِنَفْسِهِ وَمَن ضَلَّ فَإِنَّمَا يَضِلُّ عَلَيْهَا ﴿١٠٨﴾

“…Basi anayeongoka anaongoka yeye mwenyewe na anayepotea hupotea yeye mwenyewe…” (10:108).

Vipi Mwenyezi Mungu awe na sifa ya uadilifu na wakati huo huo awe ni mpotezaji. Mpotezaji ni shetani:

قَالَ هَـٰذَا مِنْ عَمَلِ الشَّيْطَانِ إِنَّهُ عَدُوٌّ مُّضِلٌّ مُّبِينٌ ﴿١٥﴾

“Akasema hii ni kazi ya shetani, hakika yeye ni adui mpotezaji aliye wazi” (28:15).

Tuanavyo sisi ni kuwa makusudio ya Aya ni kuwa mwenye kuongoka hasa ni yule aliyeongoka mbele ya Mwenyezi Mungu, hata kama mbele ya watu ni mpotevu.

Hakuna mwenye shaka kwamba mtu hawezi kuwa ni muongofu katika mizani ya Mungu ila akiamini na kutenda mema:

إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ يَهْدِيهِمْ رَبُّهُم بِإِيمَانِهِمْ ﴿٩﴾

“Hakika wale walioamini na wakatenda mema, Mola wao atawaongoa kwa sababu ya imani yao” (10:9).

وَالَّذِينَ جَاهَدُوا فِينَا لَنَهْدِيَنَّهُمْ سُبُلَنَا ﴿٦٩﴾

“Na wanaofanya juhudi kwa ajili yetu, tutawaongoa kwenye njia yetu” (29:69)

Vilevile mpotevu ni yule aliyepotea kwa Mwenyezi Mungu sio kwa watu. Kwa maneno mengine ni kwamba Aya inapinga maana ya kuwa basi amefanywa hivyo na Mwenyezi Mungu; kama alivyosema Imam Ali(a.s) :“Utajiri na ufukara ni baada ya kuonekana kwa Mwenyezi Mungu.”

Na hakika tumewauumbia Jahannam majini wengi na watu.

Mwenyezi Mungu hakuumba wala hataumba yeyote kwa ajili ya kumwadhibu. Vipi iwe hivyo? Kwani Mwenyezi Mungu anaona raha kuwaadhibu wanyonge ambao hawana hila yoyote na wala hawanyookewi.

Katika baadhi ya mambo niliyoyasoma, ni kwamba wamarekani walikuwa wanapotaka kujistarehesha, humleta mmoja asiyekuwa mweupe, wanamzunguka na kumiminia mvua ya risasi za bastola zao. Anapoanguka chini akiwa amelowa damu, wao hucheka sana.

Na kwamba Mwenyezi Mungu hatamwunguza mtu katika moto wake akiwa ana jinsia ya kimarekani au Kizayuni, Ametakata Mwenyezi Mungu na wanavyomsifu.

Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemuumba mwanadamu kwa ajili ya kupata elimu yenye manufaa amali njema, na akampa maandalizi yote ya hayo.

Akampa akili yenye kupambanua baina ya uongofu na upotevu, akampelekea Mitume wa kumzindua na kumwongoza, na akamwachia hiyari ya kufuata njia anayoitaka. Kwa sababu uhuru ndio msimamo wa hakika ya mtu. Lau asingempa uhuru angelikuwa sawa na mawe.

Kwa hiyo basi, akichagua njia ya uongofu itampeleka kwenye radhi ya Mwenyezi Mungu na thawabu zake; na akifuata njia ya upotevu basi mwisho wake ni Jahannam, ni marejeo mabaya. Kwa hali hiyo herufi Laam ni ya umwisho; kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَالْتَقَطَهُ آلُ فِرْعَوْنَ لِيَكُونَ لَهُمْ عَدُوًّا وَحَزَنًا ﴿٨﴾

“Basi wakamwokota watu na Firauni ili awe adui kwao na huzuni.” (28:8).

Yaani mwisho wake alikuwa adui yao. Utauliza: Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesema:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ ﴿٥٦﴾

“Sikuumba majini na watu ila waniabudu” (51:56)

Na wewe unasema kuwa mtu ameumbwa kwa ajili ya elimu yenye manufaa na amali njema, sasa ni vipi?

Jibu : Elimu yenye manufaa na amali njema ni katika twa’a bora zaidi. Imekuja riwaya isemayo: “Mwanachuoni mmoja ni bora kuliko wenye kuabudu elfu na wenye zuhudi elfu.” Riwaya nyingine inasema: “Mwanachuoni anayepatiwa manufaa kwa elimu yake ni bora kuliko wenye kuabudu elfu sabini.”

Wana nyonyo, lakini hawafahamu kwazo, na wana macho, lakini hawaoni kwayo, na wanayo masikio, lakini hawasikii kwayo.

Kitu chochote ambacho hakitekelezi lengo linalotakiwa basi kuweko kwake na kutokuwepo ni sawa. Na katika malengo yaliyokusudiwa moyo ni kufungukia dalili za haki, macho yaone dalili hizi na masikio yasikie. Kama vifaa hivi vitatu ukiviepusha na hayo na wala visinufaike kwa chochote katika dalili ya haki, basi kuweko kwake ni sawa na kutokuwepo. Mwenyezi Mungu anasema:

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَذِكْرَىٰ لِمَن كَانَ لَهُ قَلْبٌ أَوْ أَلْقَى السَّمْعَ وَهُوَ شَهِيدٌ ﴿٣٧﴾

“Kwa hakika katika hayo upo ukumbusho kwa mwenye moyo au ategaye sikio naye yupo” (50:37)

Moyo upo na masikio yapo, lakini inafaa kusema haupo ikiwa umeghafilika na haki na dalili zake.

Hao ni kama wanyama

Wana nyoyo, macho na masikio, lakini nyoyo zao hazifungukii haki, macho yao hayaoni dalili za haki na masikio yao hayasikii, basi wakawa kama wanyama.

Bali wao ni wapotevu zaidi.

Kwa sababu wanyama wanatekeleza lengo wanalotakiwa kwa njia ya ukamilifu kwa vile wanashindwa kufikia ukamilifu, na wala hawahisabiwi au kuadhibiwa; na tena mnyama hulijua umbile lake la asili. Makafiri hawatekelezi wanayotakiwa kuyafanya, wanaweza kufikia ukamilifu laki- ni hawafanyi, nao watahisabiwa na kuadhibiwa.

Hao ndio walioghafilika na dalili za Mwenyezi Mungu zilimo katika nafsi zao na pambizoni mwao. Pia wameghafilika na mwisho wao na yale yatakayowapata huko akhera katika hizaya na adhabu.

JE, MAJINA YA MWENYEZI MUNGU NI HAYOHAYO AU YANA KIASI

Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri.

Majina yote ya Mwenyezi Mungu ni mazuri, kwa sababu yana maana mazuri na makamilifu, na yote yako sawa katika uzuri. Kwani Mwenyezi Mungu hana hali mbalimbali wala sifa zenye kugeuka; hata kwa wale wasemao kuwa sifa yake sio dhati yake, wala pia hana vitendo vinavyotofautiana. Kuumba bawa la mbu na kuumba ulimwengu wote ni sawa kwake. Vyote hupatikana kwa neno “Kuwa na Ikawa.”

Basi mwombeni kwayo.

Yaani mtajeni Mwenyezi Mungu na mwombeni kwa jina lolote mnalolita- ka katika majina yake. Yote hayo ni matamko yanaelezea utakatifu wake na ukuu wake kwa kipimo kimoja; wala Mwenyezi Mungu hana jina kubwa na jina lisilokuwa kubwa.

Kwa ajili hiyo, sisi hatusemi kama wale wanaosema kuwa Mwenyezi Mungu ana jina mahsus ambalo ni katika majina matukufu (Ism A’dham), na kwamba mwenye kulijua atamiminikiwa na kheri nyingi na kuwa na miujiza.

Pia imesemekana kuwa Mwenyezi Mungu ana majina tisini na tisa, na kwamba mwenye kuyajua ataingia peponi; kama kwamba pepo imeumbi- wa watungaji kamusi za lugha na sio wacha Mungu.

Na waacheni wale wanaoharibu utakatifu wa majina yake, watalipwa waliyokuwa wakiyatenda.

Kuharibu ni kuacha lengo lililokusudiwa. Maana ya ujumla ni kukataza kabisa tamko lolote linalotambulisha Uungu kwa mwingne; awe Mtume, nyota, sanamu au kitu chochote kingine. Vilevile haijuzu kabisa kutumia tamko litakalofahamisha usiokuwa Ungu, kama vile baba na mwana.

Wametofautiana maulamaa wa Tawhid kuhusu majina ya Mwenyezi Mungu mtukufu, kuwa je, ni hayo hayo au yana kiasi. Maana ya kuwa ni hayo hayo ni kusimama katika majina yake yaliyotajwa kwenye Qur’an na Hadith; kiasi ambacho haijuzu kabisa jina lolote isipokuwa liwe limetokana na nukuu ya Aya au Hadith.

Maana ya kuwa yana kiasi ni kuwa jina loloate ambalo maana yake yanathibiti katika haki yake Mwenyezi Mungu, basi inajuzu kulitumia, ni sawa liwe limenukuliwa au la.

Maulama wengi wamesema kuwa majina ya Mwenyezi Mungu ni hayo hayo tu. Ama sisi tunaona kuwa inafaa kumwita au kumwomba MwenyeziMungu kwa jina lolote linalofahamisha utukatifu na utukufu wake; ni sawa liwe limenukuliwa kwenye Qur’an na Hadith au la.

Hatujizui ila lile lilozuiwa na Mwenyezi. Tunasema hivyo kwa kutegemea msingi wa: “Kila kitu ni halali mpaka kielezwe kukatazwa kwake.”

Haya ndiyo yanayopitishwa na elimu ya misingi ya kidini; kuongezea kongamano (Ijma’i) la umma, zamani na sasa, kuwa wasiokuwa waarabu wanaweza kuitaja dhati ya Mwenyezi Mungu, sifa zake na vitendo vyake kwa lugha zao.

Na miongoni mwa tuliowaumba wako watu wanaoongoza kwa haki na wafanyao uadilifu.

Katika watu kuna Muumin na kafiri na mwema na mwovu, wote wanajua hakika hii, sasa kuna makusudio gani kubainisha?

Jibu : Katika Aya iliyotangulia, Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesema kuwa wengi katika majini na watu mwisho wao ni Jahannam, kwa hiyo ikanasi- bu hapa kusema kuwa miongoni mwao mwisho wake ni pepo, hata ingawaje ni wachache kuliko wale; kama lilivyofahamisha neno miongoni. Amewaita watu wa peponi kwa ibara ya wanaoongoza kwa haki na kufanya uadilifu kuishiria kuwa sababu inayowajibisha kuingia kwao peponi ni uongofu na uadilifu.