TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 10634
Pakua: 1298

Maelezo zaidi:

Juzuu 9
Juzuu 1
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 10634 / Pakua: 1298
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

Mwandishi:
Swahili

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

وَالَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا سَنَسْتَدْرِجُهُم مِّنْ حَيْثُ لَا يَعْلَمُونَ ﴿١٨٢﴾

182. Na wale waliokadhibisha ishara zetu, tutawavuta kidogo kidogo kidogo kwa namna wasiyoijua.

وَأُمْلِي لَهُمْ إِنَّ كَيْدِي مَتِينٌ ﴿١٨٣﴾

183. Nami nitawapa muda, hakika hila yangu ni madhubuti.

أَوَلَمْ يَتَفَكَّرُوا مَا بِصَاحِبِهِم مِّن جِنَّةٍ إِنْ هُوَ إِلَّا نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿١٨٤﴾

184. Je,hawafikiri kuwa mwenzao hana wazimu? Hakuwa yeye ila ni mwonyaji aliye dhahiri.

أَوَلَمْ يَنظُرُوا فِي مَلَكُوتِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا خَلَقَ اللَّـهُ مِن شَيْءٍ وَأَنْ عَسَىٰ أَن يَكُونَ قَدِ اقْتَرَبَ أَجَلُهُمْ فَبِأَيِّ حَدِيثٍ بَعْدَهُ يُؤْمِنُونَ ﴿١٨٥﴾

185. Je, hawatazami ufalme wa mbingu na ardhi na alivyoviumba Mwenyezi Mungu. Na kuwa pengine ajali yao imekwisha karibia. Basi ni mazungumzo gani baada yake watakayoyaamini?

مَن يُضْلِلِ اللَّـهُ فَلَا هَادِيَ لَهُ وَيَذَرُهُمْ فِي طُغْيَانِهِمْ يَعْمَهُونَ ﴿١٨٦﴾

186. Ambaye Mwenyezi Mungu humpoteza hana wa kumwongoza, Na anawaacha katika upotofu wao wakimangamanga.

WALIOKADHIBISHA AYA ZETU

Aya 182 – 186

MAANA

Na wale waliokadhibisha ishara zetu, tutawavuta kidogo kidogo kwa namna wasiyojua.

Huwa zikafululiza neema kwa mtu, naye akaendelea kupetuka mipaka kwa kuhadalika na wingi wake na utajiri huku akisahau yaliyofichikana na yajayo ghafla, mpaka watu wakisema kheri zote ni zake, basi humjia ghafla kuharibikiwa.

Abu Sufyan alihadaika siku ya Uhud akasema: “Leo tumewalipizia siku ya Badr”, lakini ulipokuja msaada wa Mwenyezi Mungu na ushindi, alisilimu akiwa mnyonge.

Imam Ali(a.s) anasema:“Ni wangapi wanachukuliwa kidogo kidogo kufanyiwa hisani, na wanaohadaliwa kwa kusitiriwa, na wanaofitiniwa kwa kuambiwa maneno mazuri. Na hakujaribiwa yeyote na Mwenyezi Mungu mfano wa kupewa muda.”

Nami nitawapa muda, hakika hila yangu ni madhubuti.

Makusudio ya hila ya Mwenyezi Mungu ni kwamba yeye atawaacha wahadaike na hisani yake ya dhahir, mpaka wakielemea, basi huwachukua bila ya kujua.

أَيَحْسَبُونَ أَنَّمَا نُمِدُّهُم بِهِ مِن مَّالٍ وَبَنِينَ ﴿٥٥﴾ نُسَارِعُ لَهُمْ فِي الْخَيْرَاتِ بَل لَّا يَشْعُرُونَ ﴿٥٦﴾

“Je, wanadhani ya kuwa kwa vile tunavyowapa mali na watoto ndio tunawahimizia kheri? Bali hawatambui” (23:55 – 56).

Je,hawafikiri kuwa mwenzao hana wazimu? Hakuwa yeye ila ni mwonyaji aliye dhahiri.

Hivi ndivyo wezi, wauaji wanavyoeneza propaganda zao dhidi ya kila mwenye ikhlas, kila wakati na kila mahali. Nabii Muhammad(s.a.w.w) ni mwenda wazimu, mchawi na mwongo, Kwa nini? Kwa vile tu yeye anakataa uongo na upotevu na kuupiga vita wizi na unyang’anyi.

Makureish walimzulia Nabii Muhammad(s.a.w.w) wakiwa wanamjua tangu utoto wake mpaka kufikia miaka arubaini katika umri wake mtukufu. Wanamjua akili aliyo nayo, ukweli na uaminifu. Lakini Vilevile wanajua kuwa ujumbe wa Nabii Muhammad(s.a.w.w) ndio hatari kubwa juu ya utawala wa Kikuraish. Ni kwa ajili hii pekee ndio wakasema yeye ni mwenda wazimu, ili angalau wahadaike wale wanaowatawala na kuwanyonya.

Ndipo Qur’an ikawalingania kwenye kufikiri na kuzingatia jambo la Nabii Muhammad(s.a.w.w) , naye ni mwenzao na jamaa yao waliyempima, wafikiri, je, wamempata na lawama yoyote au wamepata katika akili yake na hulka yake tuhuma yeyote?

Hakuwa yeye ila ni muonyaji aliye dhahiri anayebainisha haki na kumwonya anayemhalifu, Hili ndilo kosa pekee kwao.

Je, hawatazami ufalme wa mbingu na ardhi na alivyoviumba Mwenyezi Mungu.

Yaani mbingu na ardhi na vyote vilivyomo vinanyenyekea ufalme wake na kufahamisha umoja wake, na kwamba hakuna yeyote mwenye akili atakayeangalia vitu hivi vilivyopo, bila ya kuwa na lengo jingine lolote, ila atamwamini Mwenyezi Mungu, vitabu vyake na Mitume yake.

Ama ambaye hafikirii isipokuwa maslahi yake tu, haongoki wala hataongoka kwa Mwenyezi Mungu wala kwa kitu chochote cha kheri.

Na kuwa pengine ajali yao imekwisha karibia.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuwataka wafikiri kuzingatia maumbile ya ulimwengu na vitu vyake sasa, anawazindua kwenye mauti, mvunja starehe na mtawanyaji makundi, na kwamba hayo mauti huenda yakawajia ghafla hivi karibuni na wao wakiwa wanaendelea katika upotevu wao. Amezindua hivi, huenda wao wakatubu na kuelekea kwenye uongofu.

Basi ni mazungumzo gani baada yake watakayoyaamini?

Dhamir ya yake inarudia Qur’an, Hakuna ubainifu wa kutosheleza baada ya Qur’an wala dalili yenye nguvu zaidi yake. Ambaye hakinaishwi na dalili za Mwenyezi Mungu basi hakinaishwi na chochote.

Ambaye Mwenyezi Mungu humpoteza hana wa kumwongoza.

Tumetaja maana yake punde tu katika kufasiri Aya 178 ya Sura hii.

Na anawaacha katika upotofu wao wakimangamanga.

Yaani Mwenyezi Mungu atawaacha wakitangatanga ovyo katika upotevu na kuwapa muda kisha awalipe yale waliyoyafanya nyuma, Wala kuwapuuza huko sio dhulma. Kwa sababu kumekuja baada ya ubainifu na hadhari, na baada ya kukata tamaa ya kuwakemea na kuwaongoza.

يَسْأَلُونَكَ عَنِ السَّاعَةِ أَيَّانَ مُرْسَاهَا قُلْ إِنَّمَا عِلْمُهَا عِندَ رَبِّي لَا يُجَلِّيهَا لِوَقْتِهَا إِلَّا هُوَ ثَقُلَتْ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ لَا تَأْتِيكُمْ إِلَّا بَغْتَةً يَسْأَلُونَكَ كَأَنَّكَ حَفِيٌّ عَنْهَا قُلْ إِنَّمَا عِلْمُهَا عِندَ اللَّـهِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿١٨٧﴾

187. Wanauliza hiyo saa (Kiyama) kutokea kwake kutakuwa lini? Sema: Ujuzi wake uko kwa Mola wangu. Hakuna wa kuidhihirisha kwa wakati wake ila yeye tu. Ni nzito katika mbingu na ardhi. Haitawafikia ila kwa ghafla tu. Wanakuuliza kama kwamba unaidadisi. Sema, Ujuzi wake uko kwa Mwenyezi Mungu tu, Lakini watu wengi hawajui.

قُل لَّا أَمْلِكُ لِنَفْسِي نَفْعًا وَلَا ضَرًّا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّـهُ وَلَوْ كُنتُ أَعْلَمُ الْغَيْبَ لَاسْتَكْثَرْتُ مِنَ الْخَيْرِ وَمَا مَسَّنِيَ السُّوءُ إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ ﴿١٨٨﴾

188. Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara ila apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kama ningelijua ghaibu ningelijizidishia kheri nyingi, wala isingelinigusa dhara. Mimi si chochote ila ni mwonyaji na mtoaji bishara kwa watu wanaoamini.

WANAKUULIZA SAA (KIYAMA)

Aya 187 – 188

MAANA

Wanauliza hiyo saa (Kiyama) kutokea kwake kutakuwa lini? Sema: Ujuzi wake uko kwa Mola wangu. Hakuna wa kuidhihirisha kwa wakati wake ila yeye tu.

Makusudio ya saa ni utakapokwisha ulimwengu na kufa viumbe.

Dhahiri ya Aya inafahamisha kwamba, jamaa walimwuliza Mtume Muhammad(s.a.w.w) : “Kiyama kitakuwa lini.” Mwenyezi Mungu akamwamrisha awaambie kwamba hiyo ni katika mambo ambayo hayako chini ya uwezo wa mtu katika kuyajua, na kwamba ujuzi wake unahusika na Mwenyezi Mungu tu peke yake, yeye ndiye atakayeidhihirisha wakati wake uliopangwa.

Ni nzito katika mbingu na ardhi.

Yaani ni nzito kutokea kwake kwa watu wa mbingu na ardhi kwa ukuu wake na ukali wake.

Haitawafikia ila kwa ghafla tu, bila ya kutangaza mapema.

Wanakuuliza kama kwamba unaidadisi.

Yaani kama kwamba wewe unapupa sana kujua saa itakuwa lini. Mtume (s.a.w.) hakuwa akijishighulisha na kujua Kiyama kitakuwa lini; isipokuwa alikuwa akijishughulisha na kuifanyia amali saa hiyo ya kiyama, kuonya watu na kuunganisha kati ya kuokoka na vituko vyake na kufanya amali njema. Kwa ajili hii ndio hakumuliza Mola wake kuhusu saa hiyo.

Imesemekana kuwa bedui mmoja alimwuliza Mtume(s.a.w.w) : “Ni lini itakuwa hiyo saa? Akamjibu: “Umeiandalia nini?” Kwa jibu hili anakusudia kumfahamisha kuwa ubora kwako ni kuuliza kitakachokuokoa wakati huo itakapofika na si kujua wakati wake na picha yake. Mwenye akili akipatwa na ugonjwa haulizi namna ya kufa na ugonjwa huo, isipokuwa anauliza ni lipi litakalomponesha na ugonjwa huo.

Tena amerudia Mwenyezi Mungu kusema:Sema, Ujuzi wake uko kwa Mwenyezi Mungu tu, kwa kutilia mkazo kuwa ujuzi wa hiyo saa uko kwa Mwenyezi Mungu peke yake, na pia ni utangulizi wa kauli yake,Lakini watu wengi hawajui kwamba ujuzi wa saa uko kwa aliyeiumba wala hajui mwengine yoyote.

MTUME NA ELIMU YA GHAIB

Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara ila apendavyo Mwenyezi Mungu.

Hii ndiyo itikadi ya Waislamu kwa Mtume wao Muhammad(s.a.w.w) mtukufu wa viumbe vyote vya Mwenyezi Mungu, Yeye mwenyewe hajimilikii nafsi yake sikwambii kummilikia mwingine. Na itikadi hii kwa Nabii Muhammad ni natija ya itikadi ya Tawhid.

Na lau kama ningelijua ghaibu ningelijizidishia kheri nyingi, wala isingelinigusa dhara.

Neno ghaibu halifahamishi maana yake tu, bali vilevile linafahamisha kuwa ghaibu ni ya Mwenyezi Mungu peke yake.

Zaidi ya dalili hii ni kwamba aliye karibu zaidi na Mola wake kuliko yey ote, anawatangazia watu kuwa yeye mbele ya ghaibu ni mtu wa kawaida tu, hana tofauti na watu wengine. Kisha hatosheki na tangazo hili, bali analitolea dalili hilo kwa hisia na dhamiri, kuwa lau kama yeye angelijua ghaibu basi angelijua mwisho wa mambo, hapo angefanya lile ambalo mwisho wake ni wema na kuliacha lile ambalo mwisho wake ni shari na yasingempata yale anayoyachukia kumpata katika maisha haya.

Na ili mtu asije akasema: Itakuwaje Nabii Muhammad(s.a.w.w) hajui ghaibu naye ni Mtume mwenye kukurubishwa kwa Mwenyezi Mungu, ndio Nabii Muhammad akasema:

Mimi si chochote ila ni mwonyaji na mtoaji bishara kwa watu wanaoamini.

Yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka, lakini umuhimu wa Mtume unathibitika kwa kufikishia watu ujumbe wa Mola wao na kumwonya kwa adhabu yule mwenye kutii. Ama elimu ya ghaibu, kunufaisha na kudhuru, hayo yako mikononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake.

Amewahusisha waumini kwa bishara na maonyo, pamoja na kuwa yanawahusu watu wote, kuishiria kwamba anayenufaika na hayo ni yule tu anayeitaka haki na imani, ama mwenye kiburi halimfai yeye jambo lolote.

Utauliza : Yamekuja maelezo katika sera ya Mtume na vitabu vya Hadith kwamba Nabii Muhammad(s.a.w.w) ametolea habari mambo mengi ya ghaibu, kama vile kuwa waislamu baadaye watawashinda warumi na wafursi, na kwamba Salman Farsy atavishwa taji la Kisra kichwani kwake, na ikawa.

Vilevile alitoa habari ya mauti ya Najash, na kufa shahid Zaid bin Harith, Jafar bin Abu Talib na Abdallah bin Rawaha, na pia kuhusu mbweko wa mbwa wa Hawab kwa Aisha kupigana na Ali bin Abu Twalib na wavunja ahadi waliokengeuka, na Khawarij, kufa shahid kwa mjukuu wake, Husein bin Ali na mengine mengi. Sasa itakuwaje hayo na kauli yake, Lau ningelijua ghaibu.

Jibu : Ghaib za Mwenyezi Mungu hazina mpaka wala idadi, Na ghaibu ziko aina nyingi.

Kuna aina anayoificha Mwenyezi Mungu na wala hamfichulii yeyote katika waja wake vyovyote walivyo, kama vile kuja saa ya Kiyama.

Aina nyingine humfichulia anayemridhia katika waja wake, Hayo ameyashiria katika Aya isemayo:

عَالِمُ الْغَيْبِ فَلَا يُظْهِرُ عَلَىٰ غَيْبِهِ أَحَدًا ﴿٢٦﴾ إِلَّا مَنِ ارْتَضَىٰ مِن رَّسُولٍ ﴿٢٧﴾

“Yeye ndiye mjuzi wa ghaibu wala hamdhihirishii ghaibu yake yoyote, isipokuwa Mtume wake aliyemridhia.” (72: 26 – 27).

Na pia Aya isemayo:

وَمَا كَانَ اللَّـهُ لِيُطْلِعَكُمْ عَلَى الْغَيْبِ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يَجْتَبِي مِن رُّسُلِهِ مَن يَشَاءُ فَآمِنُوا بِاللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَإِن تُؤْمِنُوا وَتَتَّقُوا فَلَكُمْ أَجْرٌ عَظِيمٌ ﴿١٧٩﴾

“Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwafunulia mambo ya ghaibu, lakini Mwenyezi Mungu humchagua amtakaye katika Mitume yake. Basi mwaminini Mwenyezi Mungu na Mitume Yake.” Juz.4 (3:179).

Na kuna aina nyingine anawafichulia watu wote, kama vile ufufuo, pepo na moto.

Makusudio ya kuwa ghaibu ni ya Mwenyezi Mungu na iko kwa Mwenyezi Mungu, ni kuwa hakuna njia ya kuijua kwa majaribio, akili wala kwa kitu chochote isipokuwa kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu mtukufu.

Naye humpa wahyi kwa sehemu ndogo ya ghaibu yake kulingana na heki- ma inavyotaka na haja ya watu. Na Mtume naye kwa nafasi yake hii huwapa watu habari ya ghaibu hiyo; kama alivyoipokea kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Kwa hiyo basi hakuwi kutolea habari kwa Mtume kuwa ni kujua ghaibu, bali ni kunakili kutoka kwa mwenye ujuzi wa ghaibu. Na tofauti ni kubwa baina ya chimbuko la ujuzi na yule anayenukuu kutoka kwenye chimbuko hilo. Kwa sababu, wa kwanza ni shina na wapili ni tawi. Vilevile kuna tofauti baina ya anayenukuu kutoka kwenye shina moja kwa moja na yule anaye nukuu kwa mnukuu huyu.

قَالُوا سُبْحَانَكَ لَا عِلْمَ لَنَا إِلَّا مَا عَلَّمْتَنَا إِنَّكَ أَنتَ الْعَلِيمُ الْحَكِيمُ ﴿٣٢﴾

“Wakasema: Utakatifu ni wako hatuna elimu isipokuwa ile uliyotufundisha; hakika wewe ndiwe mjuzi, mwenye hekima.” Juz.1 (2:32)

Aya hizi ni dalili mkataa juu ya kubatilika wanayoyasema masufi kwamba nafsi ya mtu kwa upande wa mazoezi ya kiroho inageukea kwenye mambo ya ghaibu na mgeuko huu wameuita elimu ya kimungu.

Sijui masufi wanachanganya vipi itikadi hii ya elimu ya kimungu na kumwamini Mwenyezi Mungu na Utume wa Nabii Muhammad(s.a.w.w) ?

Ya kushangaza zaidi ni yale aliyoyasema Ibn Al-Araby, katika Kitab Futuhatil – Makkiyya Juz.3 mlango wa 311, kwamba mwenye kumpenda Mwenyezi Mungu kwa mapenzi halisi anaweza kuigeuza nafsi yake kwenye kitu chochote anachotaka, iwe mnyama, mti, jiwe au maji.

Na kuwa hayo yametokea; Kwamba mmoja wa wapenzi wa Twariqa hii, yaani ya kisufi aliingia kwa Sheikh akajigeuza mbele yake kuwa ukufi wa maji. Sheikh alipoulizwa, fulani ameingia kwako na hakutoka, yuko wapi? Akawaambia: “Haya maji ndiye yeye!”

هُوَ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَجَعَلَ مِنْهَا زَوْجَهَا لِيَسْكُنَ إِلَيْهَا فَلَمَّا تَغَشَّاهَا حَمَلَتْ حَمْلًا خَفِيفًا فَمَرَّتْ بِهِ فَلَمَّا أَثْقَلَت دَّعَوَا اللَّـهَ رَبَّهُمَا لَئِنْ آتَيْتَنَا صَالِحًا لَّنَكُونَنَّ مِنَ الشَّاكِرِينَ ﴿١٨٩﴾

189. Yeye ndiye aliyewaumba katika nafsi moja, na katika hiyo akamjaalia mkewe ili apate utulivu kwake Alipomkurubia alishika mimba nyepesi na kutembea nayo. Hata alipokuwa mzito, wote wawili walimwomba Mola wao, kama ukitupa mwema tutakuwa miongoni mwa wanaoshukuru.

فَلَمَّا آتَاهُمَا صَالِحًا جَعَلَا لَهُ شُرَكَاءَ فِيمَا آتَاهُمَا فَتَعَالَى اللَّـهُ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿١٩٠﴾

190. Basi alipowapa mwema walimfanyia washirika katika kile alichowapa. Basi ametukuka Mwenyezi Mungu na hao wanaowashirikisha.

ALIYEWAUMBA KATIKA NAFSI MOJA

Aya 189 – 190

MAANA

Aya mbili hizi sio masimulizi ya tukio lililotokea baina ya mtu na mkewe, kama inavyoonyesha dhahiri ya matamshi, isipokuwa ni kuzungumzia hali ya mtu alivyo, bila ya kuangalia mtu maalum.

Kwa ufupi masimulizi ya hali hiyo au tamthilia hiyo ni kuwa mtu akipatwa na machukivu au akitaka kupata ayatakayo hukimbilia kwa Mwenyezi Mungu akimwomba na kunyenyekea huku akiweka ahadi kwamba Mwenyezi Mungu akimpatia anayoyataka basi atamshukuru na kumtii, lakini akimpatia yale anayoyataka, hana habari tena na ahadi zake.

Baada ya utangulizi huu, inatakikana kufahamiwa misingi ya Aya hizi tunayoifafanua kama ifuatavyo.

Yeye ndiye aliyewaumba katika nafsi moja, na katika hiyo akamjaalia mkewe ili apate utulivu kwake.

Maneno katika ‘Aliyewaumba’ yanaelekezwa kwa watu wote. Maana ni kuwa. Enyi watu wote nyinyi ni kitu kimoja, kwa kwa jinsia, maumbile na rangi. Hakuna tofauti kabisa baina ya wa mashariki na wa magharibi, mwarabu na mwajemi, mweusi na mweupe wala baina ya mwanamume na mwanamke.

Suala la jinsia linahusu vitu vyote, Mwenyezi Mungu anasema:

وَمِن كُلِّ شَيْءٍ خَلَقْنَا زَوْجَيْنِ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ ﴿٤٩﴾

“Na katika kila kitu tumeumba dume na jike ili mpate kujua” (51:49)

Lengo katika hilo linajulikana, nalo ni kuchunga aina. Kuongezea lengo hilo ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemuumba mtu mke katika jinsi yake ili kila mmoja kati ya wawili hao apate utulivu kwa mwenzake na kuweko mapenzi na kuhurumiana baina ya wawili hao.

Alipomkurubia alishika mimba nyepesi na kutembea nayo. Hata alipokuwa mzito, wote wawili walimwomba Mola wao, kama ukitupa mwema tutakuwa miongoni mwa wanaoshukuru.

Kumkurubia, ni kumwingilia, kutembea nayo, ni kuendelea mimba bila ya kutoka, na kuwa mzito, ni kukaribia wakati wa kuzaa. Wakati huu ndipo baba na mama huelekea kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) na kumnyenyekea awaruzuku mtoto mwema; yaani aliye sawa kimaumbile na kihulka. Na kama Mwenyezi Mungu akiwatakabalia basi watashukuru neema hii kwa ukamilifu.

Basi alipowapa mwema walimfanyia washirika katika kile alichowapa.

Dhamir ya walifanya, ni ya mume na mke. Makusudio ya alichowapa ni mtoto waliyemtaka. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu alipowapa mtoto, walisema, kuwa fadhila na baraka ni za masanamu na wakamsahau Mwenyezi Mungu na yale waliyomwahidi.

Basi ametukuka Mwenyezi Mungu na hao wanaowashirikisha.

Yaani wanashirikisha makafiri wakiwemo hawa wawili mke na mume. Kwa mara nyingine tena tunasema kuwa lengo la masimulizi ni hali ya mtu alivyo, sio tukio maalum.

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

أَيُشْرِكُونَ مَا لَا يَخْلُقُ شَيْئًا وَهُمْ يُخْلَقُونَ ﴿١٩١﴾

191. Je, wanawashirikisha wale ambao hawaumbi kitu, hali wao wameumbwa?

وَلَا يَسْتَطِيعُونَ لَهُمْ نَصْرًا وَلَا أَنفُسَهُمْ يَنصُرُونَ ﴿١٩٢﴾

192. Wala hawawezi kuwasaidia wala kujisaidia wenyewe.

وَإِن تَدْعُوهُمْ إِلَى الْهُدَىٰ لَا يَتَّبِعُوكُمْ سَوَاءٌ عَلَيْكُمْ أَدَعَوْتُمُوهُمْ أَمْ أَنتُمْ صَامِتُونَ ﴿١٩٣﴾

193. Na kama mkiwaita kwenye uwongofu hawatawafuata, Ni sawa ikiwa mtawaita au mtanyamaza.

إِنَّ الَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ عِبَادٌ أَمْثَالُكُمْ فَادْعُوهُمْ فَلْيَسْتَجِيبُوا لَكُمْ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿١٩٤﴾

194. Hakika hao mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni waja mfano wenu, Hebu waombeni nao wawaitikie ikiwa nyinyi mnasema kweli.

أَلَهُمْ أَرْجُلٌ يَمْشُونَ بِهَا أَمْ لَهُمْ أَيْدٍ يَبْطِشُونَ بِهَا أَمْ لَهُمْ أَعْيُنٌ يُبْصِرُونَ بِهَا أَمْ لَهُمْ آذَانٌ يَسْمَعُونَ بِهَا قُلِ ادْعُوا شُرَكَاءَكُمْ ثُمَّ كِيدُونِ فَلَا تُنظِرُونِ ﴿١٩٥﴾

195. Je, wao wanayo miguu ya kuendea? Au wanayo mikono ya kushika? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio ya kusikiliza? Sema: Waiteni hao mnaowashirikisha kisha nifanyieni vitimbi wala msinipe muda.

إِنَّ وَلِيِّيَ اللَّـهُ الَّذِي نَزَّلَ الْكِتَابَ وَهُوَ يَتَوَلَّى الصَّالِحِينَ ﴿١٩٦﴾

196. Hakika mlinzi wangu ni Mwenyezi Mungu aliyeteremsha Kitab naye ndiye awalindaye wafanyao mema.

وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ لَا يَسْتَطِيعُونَ نَصْرَكُمْ وَلَا أَنفُسَهُمْ يَنصُرُونَ ﴿١٩٧﴾

197. Na wale mnaowaabudu badala yake hawawezi kuwasaidia wala kujisaidia wenyewe.

وَإِن تَدْعُوهُمْ إِلَى الْهُدَىٰ لَا يَسْمَعُوا وَتَرَاهُمْ يَنظُرُونَ إِلَيْكَ وَهُمْ لَا يُبْصِرُونَ ﴿١٩٨﴾

198. Na kama mkiwaita kwenye uongofu hawatasikia, Na unawaona wanakutizama, nao hawaoni.

JE, WANAWASHIRIKISHA WASIOUMBA KITU?

Aya 191 – 198

MAANA

Je, wanawashirikisha wale ambao hawaumbi kitu, hali wao wameumbwa?

Kuumba na amri ni ya Mwenyezi Mungu tu ndiye ambaye kukiambia kitu kuwa kikawa. Yoyote asiyekuwa Yeye, yakiwemo masanamu, anamhitajia Yeye katika asili ya kupatikana kwake na katika kuendelea kuweko kwake.

Wala hawawezi kuwasaidia wala kujisaidia wenyewe.

Usaidizi, ushindi, utukuzaji na udhalilishaji, yote hayo yako chini ya uwezo wa Mwenyezi Mungu. Masanamu yanayokojolewa na paka na mbwa hayawezi kusaidia wala kujisaidia.

Na kama mkiwaita kwenye uwongofu hawatawafuata, Ni sawa ikiwa mtawaita au mtanyamaza.

Haya masanamu hayaumbi, hayasaidii wala hayajisaidii, hayaongoki wala hayaongozi, hayamwiti yeyote wala hayaitikii mwito wa yeyote. Pamoja na yote haya yanaabudiwa!

Hakika hao mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni waja mfano wenu, Hebu waombeni nao wawaitikie ikiwa nyinyi mnasema kweli.

Mmedai nyinyi washirikina kwamba masanamu ni miungu; na Mungu hunufaisha na kudhuru, hutoa na kuzuia, basi waombeni ili tuone kuwa je, wataitikia maombi yenu?

Je, wao wanayo miguu ya kuendea? Au wanayo mikono ya kushika? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio ya kusikiliza?.

Huku ni kuamshwa na kuzinduliwa washirikina kwamba wao ni bora kuliko masanamu wanayoyaabudu. Kwa sababu wao wana akili za utambuzi, macho ya kuona, masikio ya kusikia, miguu ya kutembelea, mikono ya kushika na ndimi za kutamka.

Lakini masanamu hayana chochote katika hayo, Sasa imekuaje aliye duni ndiye anayeabudiwa badala ya aliye mkamilifu?

Sema: Waiteni hao mnaowashirikisha kisha nifanyieni vitimbi wala msinipe muda.

Anaambiwa Nabii Muhammad(s.a.w.w) awaambie washirikina, ikiwa masanamu yenu yana kitu, kama mnavyodai, basi mimi ninayadharau pamoja na nyinyi, basi kama mnaweza shindaneni wala msingoje.

Hakika mtawala wangu ni Mwenyezi Mungu aliyeteremsha Kitab naye ndiye awalindaye wafanyao mema.

Baada ya Mtume(s.a.w.w) kuwakana washirikina na miungu yao aliwaam- bia kuwa nyinyi mnawatawalisha masanamu na mimi ninatawalisha Mungu aliyeniteremshia Qur’an iliyo na ubainifu wa kila kitu yake, Yeye vilevile anasimamia hifadhi yangu nani mlinzi wangu.

Je, masananu yenu yana kitabu? Je,yanawalinda? Natija ikawa, kama wanavyojua wote, ni kudhalilika washirikina na kutukuka Uislam na waislamu.

Na wale mnaowaabudu badala yake hawawezi kuwasaidia wala kuji- saidia wenyewe.

Imetangulia punde katika Aya 192. Kumekuja kukaririka kwa sababu Mtume(s.a.w.w) alishindana na masanamu, kuwa yampe madhara, ndipo ikanasibu kuishiria kwamba hayo hayawezi hata kujisaidia yenyewe.

Na kama mkiwaita kwenye uongofu hawatasikia.

Vilevile imetangulia katika Aya 193, kukiwa kukaririka ni kwa lengo hilo hilo.

Na unawaona wanakutizama,nao hawaoni.

Inafahamisha nasi hii kwamba masanamu yalikuwa sawa na masanamu haya yaliyomo makanisani. Na kwamba Waarabu walikuwa ni wasanii wa kuchonga. Kwani wao waliyafanya masanamu yao yaonekane kama yanaona ukiyatazama haraka haraka.

Utauliza : Kwa nini Mwenyezi Mungu amerudiarudia katika Aya zinazo fanana kwamba masanamu hayadhuru wala hayanufaishi, hayasaidii wala hayajisaidii na kwamba hayana mikono wala miguu wala macho, mpaka kufikia Aya tisa ambapo ingeotosha tu kusema hayo ni mawe?

Jibu : Fikra ya kuabudu mizimu na masanamu ilitawala sana katika akili za waarabu na ikachanganyika na roho zao na damu zao kwa vizazi na karne. Imani yao hii ilikuwa na nguvu kuliko kumwamini Mwenyezi Mungu waliyemfanya ni mshirika wa masanamu.

Kwa hiyo haikuwa rahisi kubadili itikadi yao hii. Wao walikuwa wakijitolea kwa pumzi zao zote, kama ikitajwa kwa ubaya imani yao hiyo.

Ndipo ikalazimika kukaririka huko na kusisitiza na kufananua. Hebu tufaradhie mtu mmoja wa kanisa ajaribu kuondoa picha na sanamu ndani ya kanisa. Je, itatosha aseme tu, hizi ni karatasi na mawe au itabidi atoe hotuba ndefu na pana?

خُذِ الْعَفْوَ وَأْمُرْ بِالْعُرْفِ وَأَعْرِضْ عَنِ الْجَاهِلِينَ ﴿١٩٩﴾

199. Shika usamehevu na amrisha mema na achana na wajinga.

وَإِمَّا يَنزَغَنَّكَ مِنَ الشَّيْطَانِ نَزْغٌ فَاسْتَعِذْ بِاللَّـهِ إِنَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ ﴿٢٠٠﴾

200. Na kama uchochezi wa shetani ukikuchochea, basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu; hakika yeye ndiye asikiaye na ajuaye.

إِنَّ الَّذِينَ اتَّقَوْا إِذَا مَسَّهُمْ طَائِفٌ مِّنَ الشَّيْطَانِ تَذَكَّرُوا فَإِذَا هُم مُّبْصِرُونَ ﴿٢٠١﴾

201. Hakika wale wanye takuwa zinapowagusa pepesi za shetani huzinduka.

وَإِخْوَانُهُمْ يَمُدُّونَهُمْ فِي الْغَيِّ ثُمَّ لَا يُقْصِرُونَ ﴿٢٠٢﴾

202. Na ndugu zao wanawavutia katika upotofu kisha wao hawaachi.

وَإِذَا لَمْ تَأْتِهِم بِآيَةٍ قَالُوا لَوْلَا اجْتَبَيْتَهَا قُلْ إِنَّمَا أَتَّبِعُ مَا يُوحَىٰ إِلَيَّ مِن رَّبِّي هَـٰذَا بَصَائِرُ مِن رَّبِّكُمْ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ ﴿٢٠٣﴾

203. Na usipowaletea ishara, husema: "Kwa nini hukuibuni?" Sema: Hakika nafuata niliyopewa wahyi kutoka kwa Mola wangu tu. Hizi ni busara zitokazo kwa Mola wenu na ni uwongofu na rehema kwa watu wanaoamini.

SHIKA USAMEHEVU

Aya 199 – 203

MAANA

Shika usamehevu na amrisha mema na achana na wajinga.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimfunza tabia njema Mtume wake Nabii Muhammad(s.a.w.w) , naye alikuwa akisema katika dua yake: “Ewe Mwenyezi mungu nifanye mzuri wa maumbile na tabia na niepushe na tabia mbaya.” Alimwitikia dua yake na akamtimizia tabia njema kisha akamtuma kutimiza tabia njema kwa watu wote.

Aya hii ni miongoni mwa mafunzo ya Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake mtukufu(s.a.w.w) . nayo imekusanya misingi mitatu ya sharia na adabu.

USAMEHEVU

Nao ni kuchukulia upole bila uzito wala mashaka. Nako kunakua katika vitendo na hulka. Na katika mali ni ile iliyozidi haja.

Mwenyezi Mungu amemwamrisha Mtume wake kutowatia kwenye uzito na mashaka katika anayowaamrisha na kuwakataza. Na kuchukua Zaka ya mali yao katika kinachozidi haja zao. Huu ni msingi katika misingi ya sharia.

وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ ﴿٧٨﴾

“Wala hakuweka juu yenu uzito katika dini” (22:78)

Na pia alimwamrisha kutowakalifisha hulka; kama kumwamrisha mmoja wao asamehe deni lake au asichukue kisasi.

KUAMRISHA MEMA

Ni kheri inayojulikana na iliyo wazi anayoijua mtu kwa umbile lake.

NA ACHANA NA WAJINGA

Wale ambao hakutarajiwi kuongoka kwao kwa hoja na dalili wala kwa mawaidha na uongozi. Huenda ikawa kuwapuuza na kuachana nao ni vizuri kuliko kuwaongoza.

Amesema Sheikh Maraghi katika tafsir ya Aya hii: “Imepokewa kutoka kwa Jafar As-Sadiq (r.a) kwamba yeye amesema: “Hakuna katika Qur’an Aya inayokusanya maadili mema kama hii.”

Na kama uchochezi wa shetani ukikuchochea, basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu; hakika yeye ndiye asikiaye na ajuaye.

Mtume hukasirika, hilo halina shaka, lakini yeye anakasirika kwa ajili ya Mwenyezi Mungu; hata kukasirika kwa nafsi yake ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Huenda akakasirikia ujinga wa mjinga katika alioamrishwa kuachana nao na kutaka kumkabili kwa neno litakalomstahiki.

Ndipo Mwenyezi Mungu mtukufu akamwambia kwa kumfundisha: Ikisadifu kukutokea mfano wa hali hii, basi ghadhabu isiondoe upole wako, vumilia na mtake hifadhi Mwenyezi Mungu, kwani yeye anakusikia na kukuitikia na anajua yanayokupata kutoka kwa wajinga.

Hapana budi kuishiria kuwa kauli yake hii Mwenyezi Mungu ni kiasi cha kukadiria tu, kutokana na neno ‘kama’ sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

لَئِنْ أَشْرَكْتَ لَيَحْبَطَنَّ عَمَلُكَ وَلَتَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٦٥﴾

”Kama ukishirikisha, hakika amali zako zitapomoka na utakuwa miongoni mwa wenye hasara. (39:65).

Kimsingi ni kwamba kukadiri muhali sio muhali. Katika Juz.3 (3:60) kifungu ‘Mtume na Isma’, tumebainisha kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaweza kuwakataza maasi Mitume wake walio maasum; Kwa sababu kukataza kwake kunatoka juu kuja chini; na wala haijuzu kwa yeyote, asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kuwaamrisha au kuwakataza.

Hakika wale wenye takuwa zinapowagusa pepesi za shetani huzinduka.

Hakuna mtu asiyeshindana na misukumo ya kibinafsi, baadhi yake ni ya tamaa ya moyo, mingine ni ya akili na pia ya kidini.

Mara nyingi dini na akili hushindwa na msukumo wa moyo. Kwa sababu unachimbuka katika dhati ya mtu, na unakuwa naye tangu yuko tumboni mwa mama yake.

Na akili inakuja baadae, nayo hukua kwa mafunzo na majaribio. Ama dini imeletwa kuuzoeza msukumo wa moyo na kuufunga hatamu.

Nayo utendaji kazi wake ni dhaifu, isipokuwa tu kwa mtu aliyekinai kwa nafsi yake na dhati yake, kwa namna ambayo haoni wema, isipokuwa wa dini na kufanya amali kulingana na hukumu zake.

Aina hii ya wanadini ndio wale ambao dini yao inashinda mapondokeo yao. Ndio wanokusudiwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: “Zinapowagusa pepesi za shetani huzinduka” Yaani shetani akiwahadaa kwa maasia ya Mwenyezi Mungu au akiwapa wasiwasi wa nafsi inayoamrisha uovu, basi hukumbuka aliyowaamrisha Mwenyezi Mungu na aliyowakataza. Mara wao hutambua vitimbi vya shetani na wasiwasi wa nafsi, basi hujizuia na maasi na dini yao hushinda hawa zao.

Na ndugu zao wanawavutia katika upotofu kisha wao hawaachi.

Makusudio ya ndugu hapa ni mashetani. Dhamir ya ndugu zao inarudia kwa washirikina ambao wametajwa. Makusudio ya hawaachi, ni kuwa shetani haachi kuwapoteza washirikina na kuwaharibu. Kwa ufupi ni kwamba mashetani ndio ndugu wa washirikina hawaachi kuwapoteza.

Na usipowaletea ishara, husema: Kwa nini hukuibuni?

Washirikina walikuwa wamemtaka Mtume miujiza maalum kwa njia ya inadi. Kama hakuwaletea muujiza huo husema: Kwani huwezi kuufanya mwenyewe, kwani wewe si ni Mtume?

Sema: Hakika nafuata niliyopewa wahyi kutoka kwa Mola wangu tu.

Yaani sema ewe Muhammad kuwaambia hawa wenye inadi: Ndio mimi ni Mtume, lakini Mtume hatengenezi muujiza wala haonyeshi ishara yoyote au kuipendekeza kwa Mwenyezi Mungu; bali anangoja wahyi na kuufik- isha kwa waja wake.

Hii ni busara zitokazo kwa Mola wenu na ni uwongofu na rehema kwa watu wanaoamini.

Hii ni ishara ya Qur’an na busara ni hoja na dalili ambazo mwenye akili anapata busara kwazo.

Baada ya Mtume(s.a.w.w) kuwaambia washirikina kuwa nafuata niliyope- wa wahyi kutoka kwa Mola wangu, aliwaambia, na Mwenyezi Mungu amenipa wahyi hii Qur’an ambayo ina dalili wazi za utume wangu. Nayo ni uwongofu na rehema kwa anayetaka kuamini haki kwa njia ya haki.

Mkiwa mwaitafuta haki, kama mnavyodai, basi acheni shirk na msilimu. Vinginevyo basi nyinyi ni watafutaji manufaa na watu wa malengo yenu tu.

وَإِذَا قُرِئَ الْقُرْآنُ فَاسْتَمِعُوا لَهُ وَأَنصِتُوا لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ ﴿٢٠٤﴾

204. Na isomwapo Qur’an isikilizeni na mnyamaze ili mpate kurehemiwa.

وَاذْكُر رَّبَّكَ فِي نَفْسِكَ تَضَرُّعًا وَخِيفَةً وَدُونَ الْجَهْرِ مِنَ الْقَوْلِ بِالْغُدُوِّ وَالْآصَالِ وَلَا تَكُن مِّنَ الْغَافِلِينَ ﴿٢٠٥﴾

205. Na mtaje Mola wako nafsini mwako kwa unyenyekevu na hofu na bila ya kupiga kelele kwa kauli, asubuhi na jioni, Wala usiwe miongoni mwa walioghafilika.

إِنَّ الَّذِينَ عِندَ رَبِّكَ لَا يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِهِ وَيُسَبِّحُونَهُ وَلَهُ يَسْجُدُونَ ۩﴿٢٠٦﴾

Hakika wale walioko kwa Mola wako hawajivuni wakaacha kumwabudu na wanamtakasa na wanaumsujudia.

ISOMWAPO QUR’AN ISIKILIZENI

Aya 204 – 206

MAANA

Na isomwapo Quar’an isikilizeni na mnyamaze ili mpate kurehemiwa.

Alipotaja Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya iliyotangulia kwamba hii Qur’an ni busara na uwongofu na rehema, anaamrisha katika, Aya hii, kuisikiliza na kunyamaza ili kuzingatia uwongofu na dalili zilizomo. Hapana shaka kwamba mwenye kuizingatia vyema Qur’an na akawaidhika nayo, basi yeye anastahiki rehema ya Mwenyezi Mungu na radhi zake.

Wameafikiana mafakihi, isipokuwa wa madhebu ya Dhahiriya, kwamba kuinyamazia Qur’an ni sunna na wala sio wajibu kwa asiyekuwa Maamuma anayeswali nyuma ya Imam.

Wamehitalifiana kuhusu Maamuma, kuwa je, ni wajibu asikilize na amnyamazie Imam akiwa anasoma Qur’an? Kuna kundi lililosema kuwa ni wajibu na wengine wakasema si wajibu.

Kwa hali yoyote iwavyo, ni kwamba amri katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

‘Isikilizeni’ na nyamazeni’ ni ya kupendekeza sio ya wajibu. Kwa sababu amri hii hukumu yake ni kama hukumu ya Aya inyofuatia (Na mtaje Mola wako moyoni mwako…) Kwa sababu, zote mbili zimekuja katika mfumo mmoja. Na amri ya kutaja ni ya sunna, kwa hiyo pia amri ya kusikiliza na kunyamaza.

Zaidi ya hayo ni kwamba kumnyamazia kila msomaji ni jambo zito na lenye mashaka; hasa hivi sasa ambapo kusomwa Qur’an katika vipaza sauti ni kama mchezo na nyimbo; watu hupaaza sauti kukiwa na tukio na hata kama hakuna.

Na mtaje Mola wako nafsini mwako kwa unyenyekevu na hofu na bila ya kupiga kelele kwa kauli, asubuhi na jioni.

Msemo katika ‘Mtaje’ unaelekezwa kwa Nabii Muhammad na makusudio ni kwa wote. ‘Bila ya kupiga kelele’ maana yake ni mtaje Mola wako kwa sauti ya katikati baina ya sauti kubwa na ndogo. Na asubuhi na jioni ni fumbo la kudumu kumtaja na kumkumbuka.

Kauli yake Mwenyezi Mungu ‘Bila ya kupiga kelele’ inafahamisha wazi kwamba mtu anayeinua sauti yake kwa kusoma Qur’an basi ameacha mapendekezo na kufanya kinyume; hasa ikiwa ni kwa kuwasumbua wali- olala.

Wala usiwe miongoni mwa walioghafilika na kumtaja Mwenyezi Mungu katika nafsi yako.

Kwa sababu kumtaja kwa ulimi tu, kunafanana na maneno matupu yasiyo kuwa na maana. Maana ya kumtaja Mwenyezi Mungu mtukufu katika nafsi ni kujua kwamba Mwenyezi Mungu peke yake ndiye muumba mwenye kuruzuku mwenye kutoa uhai na mwenye kufisha na mwenye kuanzisha na kurud- isha.

Kumtaja kuliko bora ni kuogopa mtu kumfanyia ubaya ndugu yake binadamu kwa kuhofia mateso ya Mwenyezi Mungu; na bora zaidi kwake ni kumfanyia wema kwa kutaraji thawabu za Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Tunasema bila ya kusita kuwa; haya ndiyo makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَلَذِكْرُ اللَّـهِ أَكْبَرُ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ مَا تَصْنَعُونَ ﴿٤٥﴾

“Na kwa hakika kumbuko la Mwenyezi Mungu ni (jambo) kubwa kabisa, Na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyatenda” (29:45)

Kauli yake: “anajua mnayoyatenda” baada ya kusema “na kumbuko la Mwenyezi Mungu ni kubwa”, kunatilia nguvu kuwa kumtaja na kumkumbuka Mwenyezi Mungu ni kuwafanyia wema waja wa Mwenyezi Mungu.

Na mwenye hasara zaidi katika watu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule anayefanya Tahlili na takbira, na huku anafanya ufisadi katika nchi kwa kudanganya na hadaa na kuwasaidia mataghuti na wakoloni dhidi ya waja wanyonge wa Mwenyezi Mungu wasio na hatia.

Hakika wale walioko kwa Mola wako hawajivuni wakaacha kumwabudu na wanamtakasa na wanamsujudia.

Wafasiri wanasema kuwa Mwenyezi Mungu amewakusudia Malaika,Wametoa dalili ya neno walioko kwa Mola wako. Kwa sababu walioko kwa Mwenyezi Mungu ni Malaika.

Lakini inawezekana kwamba makusudio ni kila mwenye nafasi na jaha mbele ya Mwenyezi Mungu; ni sawa awe ni Malaika au mwanadamu.

Wametofautiana mafakihi, kuwa je ni wajibu, kusujudu wakati wa kusomwa Aya iliyo na neno

‘Wanasujudi’, kama hii?

Amenukuu Tabrasi kauli kutoka kwa Hanafi kuwa ni wajib na kutoka kwa Shafii na Shia Imamiya kuwa ni sunna yenye kutiliwa mkazo.

Ikumbukwe kuwa Shia Imamia wamewajibisha kusujudi msomaji na msikilizaji zinaposomwa Aya zilizo katika Sura nne: 32, 41, 53 na 96.

MWISHO WA SURA YA SABA