TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 10665
Pakua: 1310

Maelezo zaidi:

Juzuu 9
Juzuu 1
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 10665 / Pakua: 1310
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA Juzuu 9

Mwandishi:
Swahili

11

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا لَقِيتُمُ الَّذِينَ كَفَرُوا زَحْفًا فَلَا تُوَلُّوهُمُ الْأَدْبَارَ ﴿١٥﴾

15. Enyi mlioamini! Mnapokutana vitani na wale waliokufuru, basi msiwageuzie migongo.

وَمَن يُوَلِّهِمْ يَوْمَئِذٍ دُبُرَهُ إِلَّا مُتَحَرِّفًا لِّقِتَالٍ أَوْ مُتَحَيِّزًا إِلَىٰ فِئَةٍ فَقَدْ بَاءَ بِغَضَبٍ مِّنَ اللَّـهِ وَمَأْوَاهُ جَهَنَّمُ وَبِئْسَ الْمَصِيرُ ﴿١٦﴾

16. Na atakayewageuzia mgongo wake siku hiyo – isipokuwa kwa mbinu za vita au kuungana na kikosi - hakika amestahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu; na makazi yake ni Jahannam, napo ni mwishilio muovu.

فَلَمْ تَقْتُلُوهُمْ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ قَتَلَهُمْ وَمَا رَمَيْتَ إِذْ رَمَيْتَ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ رَمَىٰ وَلِيُبْلِيَ الْمُؤْمِنِينَ مِنْهُ بَلَاءً حَسَنًا إِنَّ اللَّـهَ سَمِيعٌ عَلِيمٌ ﴿١٧﴾

17. Hamkuwaua nyinyi, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaua, Na hukutupa wewe ulipotupa, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyetupa, Ili awajaribu waumini majaribu mazuri, Hakika Mweyezi Mungu ni Msikizi, Mjuzi.

ذَٰلِكُمْ وَأَنَّ اللَّـهَ مُوهِنُ كَيْدِ الْكَافِرِينَ ﴿١٨﴾

18. Ndiyo hivyo! Na hakika Mwenyezi Mungu ndiye adhoofishaye vitimbi vyamakafiri.

إِن تَسْتَفْتِحُوا فَقَدْ جَاءَكُمُ الْفَتْحُ وَإِن تَنتَهُوا فَهُوَ خَيْرٌ لَّكُمْ وَإِن تَعُودُوا نَعُدْ وَلَن تُغْنِيَ عَنكُمْ فِئَتُكُمْ شَيْئًا وَلَوْ كَثُرَتْ وَأَنَّ اللَّـهَ مَعَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٩﴾

19. Kama mnataka ushindi, basi ushindi umekwishawajia, na kama mkiacha, basi itakuwa kheri kwenu; na kama mtarudia sisi pia tutarudia; na jeshi lenu halitawafaa chochote hata likiwa kubwa. Na kwa hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na waumini.

KUKIMBIA VITA

Aya 15 – 19

MAANA

Enyi mlioamini! Mnapokutana vitani na wale waliokufuru, basi msi- wageuzie migongo.

Yametangulia maelezo kuwa washirikina walitoka Makka kuja kupambana na waislamu. Aya hii ni katika mafunzo ya vita, Inamaanisha waislamu wawe imara kumkabili adui wala wasikimbie wanapokutana vitani. Kwa sababu kukimbia ni unyonge katika dini na udhalili kwa waislamu.

Na atayewageuzia mgongo wake siku hiyo - isipokuwa kwa mbinu za vita au kuungana na kikosi - hakika amestahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu; na kimbilio lake ni Jahannam, napo ni mwisho muovu.

Mbinu za vita, ni kama kuacha mahali pake na kwenda mahali pazuri zaidi. Na kuungana na kikosi, ni kuungana na kikosi kingine kinachomhitajia au anachokihitajia.

Maana ni kuwa: Enyi waislamu! Mjizatiti na adui yenu katika vita wala msimkimbie ila ikiwa ni kuchagua sehemu nzuri au kupanga mpango mzuri kwa kuungana; na kwamba mwenye kukimbia adui bila ya sababu za msingi basi amestahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na marejeo yake ni Jahannam.

Mafakihi wametoa fatwa kuwa ni haramu kukimbia vita ila ikiwa idadi ya jeshi la adui ni kubwa kuliko jeshi la waislamu.

Tuanavyo sisi ni kuwa mafakihi hawawezi kuwa na fatwa hapa ya wajibu wa kubaki au kujuzu kukimbia; isipokuwa amri katika hilo ni lazima aachiwe kamanda mwaminifu mwenye majukumu ya vita na wala sio mafakihi. Kwa hiyo ni wajibu yeye aachiwe kupanga wajibu wa kubaki au kukimbia.

Anaweza akaonelea kuwa wabakie licha ya kuzidi idadi ya adui mara tatu zaidi, na anaweza akaona lazima wakimbie na kujiondoa vitani hata kama idadi ya waislamu ni maradufu ya maradufu. Kwa sababu kubaki ni tendo la kujiua. Na, katika hali zote ni wajibu kuchukua kauli yake sio kauli ya mafakihi wanayofutu wenyewe wakiwa wamelalia mito.

Zaidi ya hayo ni kwamba kauli ya mafakihi imepitwa na wakati, ambapo nguvu zilikuwa zikipimwa na idadi sio kwa aina, na kwa idadi ya jeshi sio kwa maandalizi yake ya silaha za kisasa.

Hamkuwaua nyinyi, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaua.

Waislamu waliwashinda washirikina Badr; wakawauwa na kuwateka. Sababu ya ushindi huu ni uimara wa waislamu na uvumilivu. Ama sababu ya uimara huu na uvumilivu ni ile iliyoashiriwa na Aya iliyotangulia kuwa Mwenyezi Mungu alizikazanisha nyoyo za waislamu, akaimarisha nyayo zao, akawasaidia kwa Malaika na akaondoa hofu katika nyoyo zao na kuitia katika nyoyo za washirikina.

Kwa hali hiyo inafaa kunasibisha kwa waislamu kuuwa washirikina, kwa sababu ilikuwa ni kwa mikono yao na ni kwa sababu ya uimara na subira yao. Vilevile itafaa kunasibisha kwa Mwenyezi Mungu mtukufu kwa sababu yeye ndiye aliyewaandalia uimara na subira hiyo, Zaidi ya hayo yeye ndiye sababu ya sababu zote.

Imesimuliwa kwamba baadhi ya waislamu walisema siku ya Badr: “Mimi nimemuuwa fulani”, mwengine naye akasema, Ndipo Mwenyezi Mungu akateremsha kauli yake hiyo.

Na hukutupa wewe ulipotupa, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyetupa.

Ndio Mwenyezi Mungu ndiye aliyetupa, lakini yeye alichagua kiganja cha kutupa cha Nabii Muhammad(s.a.w.w) ambaye amemfadhilisha juu ya viumbe vyote; akamhusisha na ujumbe wake ambao rehma yake imewaenea walimwengu wote.

Imepokewa kuwa Mtume alichukua gao la changarawe au mchanga, akawatupia washirikina, akasema: “Na zihizike nyuso”, hilo likafuatiwa na kushindwa kwao. Sio mbali kuwa riwaya hii ni sahih. Vilevile sio mbali kuwa makusudio ya kutupa ni kupanga mambo.

Vyovyote itakavyokuwa ni kwamba matakwa ya Mwenyezi Mungu ndiyo sababu ya sababu. Kwani sababu yoyote ya tukio lolote iwe ya moja kwa moja au si ya moja kwa moja, basi itaishia kwenye nguvu kuu iliyopatikana bila ya mpatishaji. Vinginevyo basi neno kupatikana lisingekuwa na maana.

Ili awajaribu waumini majaribu mazuri.

Majaribu (mtihani) yanaweza kuwa ya neema ili kudhihirisha shukrani na yanaweza kuwa ni misukosuko ili kudhihirisha uvumilivu. Pia maana yake yanakuwa ni kupewa, Hayo ndio maana yaliyokusudiwa katika Aya hii.

Ama makusudio ya mazur ni ushindi na ngawira; yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaamrisha waislamu kuwa imara, wavumilivu na kuacha kukimbia vita; na akawaandalia wao njia ya hilo, ili awatimizie neema yake ya ushindi na ngawira.

Hakika Mweyezi Mungu ni Msikizi, Mjuzi.

Amesikia maombi ya msaada na akawaitikia, kwa vile alijua usafi wao wa nia na usahihi wa azma.

Ndiyo hivyo! Na hakika Mwenyezi Mungu ndiye adhoofishaye hila za Makafiri.

Hakuna neema kubwa na adhimu kuliko kudhoofishwa adui na kubatilishwa hila zake.

Kama mnataka ushindi, basi ushindi umekwishawajia, na kama mkiacha, basi itakuwa kheri kwenu; na kama mtarudia sisi pia tutarudia; na jeshi lenu halitawafa chochote hata likiwa kubwa. Na kwa hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na waumini.

Maneno yote wanaambiwa washirikina kwa kuangalia mfumo wa maneno na kutimia maana.

Imepokewa kuwa Washirikina walipotoka Makka kuelekea Badr waliishika nguo inayofunika Al-Kaaba, wakamtaka nusura ya ushindi Mwenyezi Mungu, wakasema: “Ewe Mwenyezi Mungu lipe ushindi jeshi lililo juu na lililo tukufu kati ya majeshi mawili.”

Ndipo Mwenyezi Mungu akawajibu: Kama mnataka ushindi; yaani mkitaka ushindi kwa jeshi lililo juu na lililo na uongofu basi amekwisha lipa ushindi. Na kama mkiacha kupigana na waislamu na kumpinga Mwenyezi Mungu na Mtume, basi itakuwa ni bora kwenu baada ya kuonja kipigo cha kuuawa na kutekwa. Na kama mkirudia vita yatawafika tena yale yaliyowafika mwanzo.

Ama wingi ambao mnajitukuza nao, mmeuona haufai kitu, hauwazuilii kuuliwa, kutekwa na kushindwa. Kwani Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kutoa ushindi, naye yuko pamoja na waumini.

Ikiwa mnataka ushindi wa kweli basi acheni shirk na mumuami Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَطِيعُوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَلَا تَوَلَّوْا عَنْهُ وَأَنتُمْ تَسْمَعُونَ ﴿٢٠﴾

20. Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msijiepushe naye hali mnasikia.

وَلَا تَكُونُوا كَالَّذِينَ قَالُوا سَمِعْنَا وَهُمْ لَا يَسْمَعُونَ ﴿٢١﴾

21. Wala msiwe kama wale wanaosema: Tumesikia; na kumbe hawasikii.

إِنَّ شَرَّ الدَّوَابِّ عِندَ اللَّـهِ الصُّمُّ الْبُكْمُ الَّذِينَ لَا يَعْقِلُونَ ﴿٢٢﴾

22. Hakika wanyama waovu mbele ya Mwenyezi Mungu ni viziwi, mabubu ambao hawatumii akili.

وَلَوْ عَلِمَ اللَّـهُ فِيهِمْ خَيْرًا لَّأَسْمَعَهُمْ وَلَوْ أَسْمَعَهُمْ لَتَوَلَّوا وَّهُم مُّعْرِضُونَ ﴿٢٣﴾

23. Na kama Mwenyezi Mungu angelijua wema wowote kwao angeliwasikilizisha;na kama angeliwasikilizisha, wangeligeuka wakipuuza.

KUMTII MWENYEZI MUNGU NA MTUME

Aya 20 – 23

MAANA

Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msi- jiepushe naye hali mnasikia.

Mwito huu umekuja baada ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na kwa hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na waumin.” Lengo lake ni kumuelezea Mumini ambaye atapewa ushindi na Mwenyezi Mungu na atakayekuwa naye Mwenyezi Mungu popote alipo.

Huyo ni yule ambaye anamtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake katika wanayomwamrisha na wanayomkataza na kwamba mwenye kumhalifu na kuasi; basi amestahiki adhabu na hizaya kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Wala msiwe kama wale wanaosema: Tumesikia; na kumbe hawasikii.

Mara nyingi kusikia kutumiwa kwa maana ya kukubali; kama vile mtu kusema: Mimi sikuzikilizi; yaani sikukubalii. Au kama vile kusema: Wenye kusikia sana uwongo; yaani wenye kuukubali

Haya ndiyo maana yaliyokusudiwa katika Aya hii, Yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawakataza waumini kuwa kama wanafiki wakidhihirisha kumkubalia Mtume na kutii amri yake na huku wakificha uhalifu na uasi.

Hakika wanyama waovu mbele ya Mwenyezi Mungu ni viziwi, mabubu ambao hawatumii akili.

Kiziwi hasikii na bubu hasemi. Wanyama wana masikio ya kusikia, lakini hawafahamu maneno wanayoyasikia na wana ndimi lakini hawasemi, Kwa hiyo hawafahamu wala hawafahamiwi.

Mwenye kusikia maneno ya Mwenyezi Mungu na Mtume kisha asiongoke kwayo, basi mfano wake ni kama mfano wa mnyama kiziwi aliye bubu, husikia maneno, lakini hanufaiki nayo.

MWENYE KUTAFUTA HAKI NA MWENYE KUTAFUTA WINDO

Na kama Mwenyezi Mungu angelijua wema wowote kwao angeliwasikilizisha; na kama angeliwasikilizisha wangeligeuka wakipuuza.

Watu ni aina mbili:

1. Ni yule mwenye kuitafuta akiwa hana lengo lolote. Huyu hawezi kuamini msingi wala kuona rai yoyote ila baada ya utafiti na kutilia manani dalili kisha hujenga rai yake juu ya dalili hizo.

2. Ni mwenye kutafuta windo fulani. Haamini isipokuwa dhati yake na maslahi yake. Hukaribisha yale yanayoafikiana na maslahi yake, hata kama ni batili na hukataa yale yanayopingana nayo, hata kama ni haki.

Mwenyezi Mungu huwasikilizisha mwito wa haki wote wawili kwa njia ya sawa sawa, kuweka hoja. Anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَمَا كُنَّا مُعَذِّبِينَ حَتَّىٰ نَبْعَثَ رَسُولًا ﴿١٥﴾

Na hatukuwa ni wenye kuadhibu mpaka tumpeleke Mtume. (17:15).

Baada ya ubainifu unaotumiza hoja kwa wote, Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anazidisha nasaha na mwongozo kwa wale wanaoitikia na kunufaika nao

وَالَّذِينَ اهْتَدَوْا زَادَهُمْ هُدًى وَآتَاهُمْ تَقْوَاهُمْ ﴿١٧﴾

“Na wale wanaokubali kuongoka huwazidishia uongofu.” (47:17).

Ama wale ambao hawaitikii isipokuwa manufaa yao ya kidhati, basi Mwenyezi Mungu huachana nao, maadamu nasiha haziwafai chochote. Haya ndiyo makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na kama angejua wema wowote angeliwasikilizisha.”

Hilo linafahamika kutokana na kauli yake moja kwa moja bila ya kuingia kati kitu kingine: “Na kama angewasikilizisha wangeligeuka wakipuuza.” Yaani lau angeliwasikilizisha haki, wangeliachana nayo, kwani haikubaliani na hawaa zao.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اسْتَجِيبُوا لِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُمْ لِمَا يُحْيِيكُمْ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ يَحُولُ بَيْنَ الْمَرْءِ وَقَلْبِهِ وَأَنَّهُ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ ﴿٢٤﴾

24. Enyi mlioamini! Mwitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapowaita kwenye lile litakalowapa uhai. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba mtakusanywa kwake.

DINI NA MAISHA

Aya 24

MAANA

Mwenye kuujua vilivyo Uislamu atakuta kila asili ya itikadi yake na kila tawi la sharia yake inasimamia kwa uwazi au kuwa na madhumuni ya kufanya kazi kwa ajili ya uhai (maisha).

Kumwamini Mungu ni imani iliyo na mwito wa kujikomboa na utumwa, isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu mmoja peke yake, na kwamba hakuna utawala kwa sababu ya mali wala jaha au jinsi au kitu chochote kile isipokuwa kwa haki na uadilifu.

Kimsingi ni kwamba maisha mema yenye nguvu hayapatikani na ni muhali kupatikana ila kwa kushikamana na msingi huu na kuufuatilia.

Ama kuamini Utume wa Muhammad(s.a.w.w) kwenyewe ni kuamini sharia ya udugu na usawa, uhuru wa mtu na himaya yake na kila msingi ambao unampa binadamu kheri njema. Hilo ni kwa vile utume wa Muhammad unalenga kwenye uongofu wa mtu na wema wake na kueneza uadilifu baina ya watu.

Kuamini siku ya mwisho ni kuamini kuwa mtu hataachwa bure na kwamba yeye ataulizwa kila dogo na kubwa katika amali zake. Atahisabiwa na kulipwa; ikiwa ni kheri basi atalipwa kheri, na ikiwa ni shari basi atalipwa shari. Imani hii, kama unavyoona, inafanana na serikali kuu, au mhimizaji wa matendo yanayowajibisha kumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume.

Hayo ni katika yale yanayohusiana na misingi ya itikadi. Ama matawi ya dini, yaani yale yanayofaa kufanywa na yasiyofaa katika sharia ya kiislamu, huwa yanasimamia misingi ya binadamu, iliyoashiriwa na kauli yake Imam Jafar As-Sadiq(a.s) :“Kila lililo na masilahi kwa watu kwa upande fulani basi linajuzu, na kila lililo na ufisadi kwa upande fulani basi halijuzu.

Huu ndio mwito wa Mwenyezi Mungu na Mtume ulioelezwa na Qur’an waziwazi:

Mwitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapowaita kwenye lile litakalowapa uhai.

Tukiinganisha Aya hii na ile isemayo:

قُلْ أَطِيعُوا اللَّـهَ وَالرَّسُولَ فَإِن تَوَلَّوْا فَإِنَّ اللَّـهَ لَا يُحِبُّ الْكَافِرِينَ ﴿٣٢﴾

“Sema mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume. Na kama wakikata, basi hakika Mwenyezi Mungu hawapendi Makafiri” Juz.3 (3:32),

Tutapata picha hii ya makisio ya kimantiki kuwa: Mungu na Mtume wametoa mwito kwa ajili ya maisha na akahukumu ukafiri wa kila anayepinga mwito huu. Kwa hiyo natija ni kuwa asiyetenda kwa ajili ya maisha basi ni kafiri[2] .

Kwa hali hiyo basi inatubainikia kuwa Uislamu unakwenda sambamba na maisha, na kwamba kila ambalo liko mbali na maisha basi si Uislamu chochote.

Kila mtu, vyovyote awavyo, akilingania kwenye maisha yasiyokuwa na unyanyasaji, dhulma au matatizo, basi mwito wake huo unakutana na mwito wa Mwenyezi Mungu na Mtume, apende asipende.

Na yule anayeikingamia njia ya maisha na maendeleo yake, basi huyo ni adui wa Mwenyezi Mungu na Mtume, hata akiswali usiku na kufunga mchana.

Ama vikundi vilivyojitokeza siku hizi ambavyo vimeiuza dini yake kwa uzayuni na ukoloni, huku vikijificha kwa jina la dini, tumevielezea kaatika Juz. 4 (3:142).

Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake na kwamba mtakusanywa kwake.

Moyo ndio mahali pa imani, ukafiri, ikhlas na unafiki. Pia ni mahali pa pendo na chuki. Kwenye moyo hutokea matendo mema na mbaya, Lau si moyo mtu asingekuwa mtu.

Inatosha kuwa moyo ni kitu kikubwa, kauli yake Mwenyezi Mungu katika Hadith Qudsi: “Haikunipanua ardhi yangu wala mbingu yangu, lakini umenipanua moyo wa mja wangu muu’min.” Hakuna mwenye shaka kwamba kinachompanua aliyeshindwa kupanuliwa na mbingu na ardhi, kuwa ni kikubwa zaidi ya ardhi na mbingu.

Utauliza : vipi kiungo hiki kidogo kiweze kupanua aliyeshindikana na ardhi na mbingu? Tena, kwa nini Mwenyezi Mungu mtukufu amehusisha moyo wa Mumini na wala sio wa kafiri?

Jibu : Makusudio ya upana katika Hadith Qudsi hii, sio upana wa mahali. Kwa sababu Mwenyezi Mungu hana mahali isipokuwa makusudio ni kumfahamu Mwenyezi Mungu, na kwamba moyo wa mumini unamfahamu Mwenyezi Mungu mtukufu kwa namna isiyoweza mbingu na ardhi kufahamu.

Vilevile moyo wa kafiri, haufahamu chochote kuhusu Mwenyezi Mungu, kwa vile uko katika kifuniko cha upotevu na ufisadi. Mwenyezi Mungu mtukufu, anasema:

وَقَالُوا قُلُوبُنَا فِي أَكِنَّةٍ مِّمَّا تَدْعُونَا إِلَيْهِ وَفِي آذَانِنَا وَقْرٌ وَمِن بَيْنِنَا وَبَيْنِكَ حِجَابٌ ﴿٥﴾

“Na wakasema: Nyoyo zetu ziko katika vifuniko kwa yale unayotulingania, na katika masikio yetu mna uzito, na baina yetu na baina yako kuna pazia” (41:5).

Kwa hivyo basi inatubainikia kuwa makusudio ya mtu ambaye Mwenyezi Mungu huingia kati yake na moyo wake, ni yule ambaye amepofushwa na hawaa zake na upotevu. Hivyo Aya hii inakuwa na maana ya Aya isemayo: “Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao; na juu ya macho yao pana kifuniko,”

Yaani hawanufaiki kwa nyoyo zao kwa sababu ya kutu za upotevu zilizo juu yake, mpaka ikawa kama kwamba Mwenyezi Mungu amepiga sili au amekaa kati yake na mwenye moyo huo.

Hivyo anakuwa kunasibisha muhuri na kuzuia kwake Mwenyezi Mungu mtukufu ni kimajazi sio kihakika.

Kundi la wafasirii wamesema kuwa maana ya kuingia kati ya mtu na moyo wake ni kwamba moyo unashikwa na Mwenyezi Mungu akiugeuza vile anavyotaka, hubadilisha ukumbusho ukawa usahaulivu na usahaulivu ukawa ukumbusho, hofu kuwa amani na amani kuwa hofu. Lakini tafsiri zote hizo ni za kudhania tu.

12

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA TISA

وَاتَّقُوا فِتْنَةً لَّا تُصِيبَنَّ الَّذِينَ ظَلَمُوا مِنكُمْ خَاصَّةً وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٢٥﴾

25. Na jikingeni na fitna ambayo haitawasibu wale waliodhulumu miongoni mwenu peke yao, na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

وَاذْكُرُوا إِذْ أَنتُمْ قَلِيلٌ مُّسْتَضْعَفُونَ فِي الْأَرْضِ تَخَافُونَ أَن يَتَخَطَّفَكُمُ النَّاسُ فَآوَاكُمْ وَأَيَّدَكُم بِنَصْرِهِ وَرَزَقَكُم مِّنَ الطَّيِّبَاتِ لَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿٢٦﴾

26. Nakumbukeni mlipokuwa wachache, mkionekana wadhaifu katika nchi; mkawa mnaogopa watu wasiwanyakue; akawapa makao na akawatia nguvu kwa nusura yake na akawapa riziki njema ili mpate kushukuru.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَخُونُوا اللَّـهَ وَالرَّسُولَ وَتَخُونُوا أَمَانَاتِكُمْ وَأَنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿٢٧﴾

27. Enyi mlioamini! Msimfanyie hiyana Mwenyezi Mungu na Mtume na mkahini amana zenu na hali mnajua.

وَاعْلَمُوا أَنَّمَا أَمْوَالُكُمْ وَأَوْلَادُكُمْ فِتْنَةٌ وَأَنَّ اللَّـهَ عِندَهُ أَجْرٌ عَظِيمٌ ﴿٢٨﴾

28. Na jueni kwamba mali zenu na watoto wenu ni fitna. Na hakika kwa Mwenyezi Mungu yako malipo makubwa.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِن تَتَّقُوا اللَّـهَ يَجْعَل لَّكُمْ فُرْقَانًا وَيُكَفِّرْ عَنكُمْ سَيِّئَاتِكُمْ وَيَغْفِرْ لَكُمْ وَاللَّـهُ ذُو الْفَضْلِ الْعَظِيمِ ﴿٢٩﴾

29. Enyi mlioamini! Mkimcha Mwenyezi Mungu atawajaalia upaambanuzi, na atawafutia makosa yenu na atawasamehe; na Mwenyezi Mungu ni mwenye fadhila kuu.

OGOPENI ADHABU

Aya 25 – 29

LUGHA

Neno Fitna lina maana nyingi, miongoni mwa maana hizo ni adhabu ambayo ndiyo makusudio yake katika Aya hii ya 25. Ama katika Aya 28, makusudio yake ni mapenzi na hawaa zinazozuia haki. Makusudio ya upambanuzi ni mwongozo.

MAANA

Na jikingeni na fitna ambayo haitawasibu wale waliodhulumu mion- goni mwenu peke yao, na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

Ni tahadhari inayotoka kwake Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kila mfitini anayeharibu nchi; hasa wale wanaoeneza farakano na kuvuruga amani na kuwachokoza wanyonge. Hadhari ni kwamba ubaya wa adhabu hautaishia kwa madhalimu tu, bali utaenea katika jamii yote na kumwenea mwema na mwovu.

Imeelezwa katika Tafsir Tabari akimnukuu Sadiy, ambaye ni mfasiri mkubwa, kwamba Aya hii inafungamana na watu wa (Vita vya Jamal) ngamia ambao walimpiga vita Ali bin Abu Talib.

Ametaja Razi katika kufasiri Aya hii: “Zubeir siku moja alikuwa akibarizi na Mtume(s.a.w.w) mara akatokea Ali (r.a), Zubeir akamcheka. Mtume wa Mwenyezi Mungu akamwambia: “Vipi unavyompenda Ali?” Akajibu “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu ninapenda kama ninavyompenda mwanangu au zaidi. Mtume akamwambia:‘’Utakuwaje ukienda kupigana naye?

Vilevile imeelezwa katika Tafsiru Tabari: “Zubeir bin Al-a’wam alisema: “Tumesoma Aya hii zama zilizopita, lakini hatukuwaona wanaohusika nayo, mara sisi ndio tunahusika nayo”.

Na kumbukeni mlipokuwa wachache, mkionekana wadhaifu katika nchi; mkawa mnaogopa watu wasiwanyakue; akawapa makao na akawatia nguvu kwa nusura yake na akawapa riziki njema ili mpate kushukuru.

Maneno wanaambiwa Maswahaba wa Mtume(s.a.w.w) . Mwenyezi Mungu mtukufu anawakumbusha udhaifu na hofu waliyokuwa nayo kabla ya Uislamu. Vilevile udhalili na ufukara, na jinsi alivyowapa amani utajiri na utukufu baada ya Uislamu, kwa vile wao wameitikia mwito wa maisha waliyopewa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Lengo la ukumbusho huu ni kuwa waendelee na utiifu na kuitikia mwito wa uhai, ili waishi wakiwa wenye nguvu na heshima. Na kwamba wao pindi tu wakikengeuka na kuasi watarudia unyonge na udhalili waliokuwa nao wenzao, kama ilivyo hali ya waislamu leo, hasa waarabu.

Enyi mlioamini! Msimfanyie hiyana Mwenyezi Mungu na Mtume.

Kumfanyia hiyana Mwenyezi Mungu sio kuacha kufunga na kuswali tu; isipokuwa hiyana kubwa ni kuufanyia hiyana umma na nchi, kwa kuwatawalisha mataghuti kwenye sehemu za uongozi wakatawala nchi na huku tunawavumilia na kuwanyamazia bila ya kuwapiga vita.

Na mkahini amana zenu.

Yaani wala msihini amana zenu, Wafasiri wengi wamesema kuwa ukatazo huu ni wa hiyana ya amana ya mangiliano ya kimali baina ya watu. Hakuna mwenye shaka kwamba kurudisha amana ni wajibu na kuifanyia hiyana ni haramu, lakini hiyana kubwa ni kuacha kusaidiana na wanyonge kurudisha haki zao kutoka kwa wenye nguvu walio madhalimu.

Na hali mnajua.

Hakuna mjeuri zaidi kwa Mwenyezi Mungu kuliko yule anayemuasi Mwenyezi Mungu kwa makusudi hali anajua.

Jueni kwamba mali zenu na watoto wenu ni fitna.

Imekuja Aya hii baada ya makatazo ya hiyana ili kumzindua Mumini kwamba haitakikani mali na watoto wamzuie kutekeleza wajibu wake kwa umma na nchi mbele ya Mungu. Makusudio ya fitna hapa ni mapenzi yanayozuia haki na kheri.

Imepokewa Hadith kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) amesema: “Mtoto ni tunda la moyo. Na yeye ni mahali pa woga, ubahili na huzuni” Sawa na mali ambayo ni matunda ya jasho na mkono.

Ni woga kwa sababu, mwenye nayo huhofia kusema haki na kufanya kwa kuihofia; kama ambavyo anahofia juu ya mtoto wake.

Ni ubahili, kwa sababu mwenye kuimiliki anakuwa na pupa nayo na uchoyo; kama anavyokuwa na pupa na mtoto wake.

Nayo ni huzuni kwa sababu mwenye kuikusanya huhuzunika ikipatwa na jambo; kama anavyohuzunika likipatwa na jambo tunda la moyo wake.

Maneno mazuri niliyosoma kuhusu maudhui haya ni shairi la bedui mmoja akisema:

• Alikuwa fukara

• Akatajirika akapenda mali uchu ukamshika

• Akitaka kutumia huhuzunika

Na hakika kwa Mwenyezi Mungu yako malipo makubwa.

Mwenye akili hupendelea malipo haya na kuyahangaikia kwa juhudi na amali njema; wala haathiriki na mali inayokwisha na mtoto asiyebakia.

Enyi mlioamini! Mkimcha Mwenyezi Mungu atawajalia upaambanuzi.

Mara nyingi sana mtu anakuwa mateka wa matamanio. Humgeuzia zuri likawa baya na baya likawa zuri. Mara nyingi hilo huwa katika mambo yanayohusiana na mali na watoto ambapo matamanio hufikia kilele chake.

Kwa ajili hii ameamrisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) takuwa baada ya kuhadharisha fitna ya mali na watoto. Ama upambanzi, yaani mwongozo, anaowapa Mwenyezi Mungu wenye kumcha ili wapambanue haki na batili, ni natija ya kujikomboa na hawa na matamanio.

Kwa sababu, matamanio hupofusha na hutia uziwi.

Kunasibisha mwongozo kwa Mwenyezi Mungu ni kuwa yeye ndiye aliyeuwekea dalili. Mwenye kuzichunguza vizuri, akiwa hana malengo mengine yoyote isipokuwa kutafuta mwongozo wa haki, basi ataifikia tu.

Na atawafutia makosa yenu na atawasamehe; na Mwenyezi Mungu ni mwenye fadhila kuu.

Wafasiri wanasema kuwa makusudio ya kufutiwa makosa ni kusitiriwa duniani; na kusamehewa ni kusamehewa akhera, Wamesema hivi kukimbia kukaririka.

Ama sisi hatukimbii kukarika Qur’an na tumebainisha njia yake katika Juz.1 Maana ya Aya yote ni kuwa mwenye kumcha Mwenyezi Mungu atampa mwongozo, msamaha na thawabu.

Hilo kwa Mwenyezi Mungu si kubwa. Kwa sababu ni mkuu wa fadhila na kutoa kwake ni sahali kunamfikia kila mwenye kutafuta na kutaka radhi zake.

وَإِذْ يَمْكُرُ بِكَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِيُثْبِتُوكَ أَوْ يَقْتُلُوكَ أَوْ يُخْرِجُوكَ وَيَمْكُرُونَ وَيَمْكُرُ اللَّـهُ وَاللَّـهُ خَيْرُ الْمَاكِرِينَ ﴿٣٠﴾

30. Na walipokupangia njama wale waliokufuru ili wakufunge au wakuue au wakutoe. Na wakapanga njama na Mwenyezi Mungu akapanga njama. Na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa kupanga njama.

وَإِذَا تُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ آيَاتُنَا قَالُوا قَدْ سَمِعْنَا لَوْ نَشَاءُ لَقُلْنَا مِثْلَ هَـٰذَا إِنْ هَـٰذَا إِلَّا أَسَاطِيرُ الْأَوَّلِينَ ﴿٣١﴾

31. Na wanaposomewa Aya zetu, husema: Tumekwishasikia, na lau tungependa tungelisema kama haya. Haya si chochote ila ni ngano tu za watu wa kale.

وَإِذْ قَالُوا اللَّـهُمَّ إِن كَانَ هَـٰذَا هُوَ الْحَقَّ مِنْ عِندِكَ فَأَمْطِرْ عَلَيْنَا حِجَارَةً مِّنَ السَّمَاءِ أَوِ ائْتِنَا بِعَذَابٍ أَلِيمٍ ﴿٣٢﴾

32. Na waliposema: Ewe Mwenyezi Mungu! Ikiwa haya ni haki itokayo kwako, basi tupige mvua ya mawe kutoka mbinguni au tuletee adhabu iumizayo.

وَمَا كَانَ اللَّـهُ لِيُعَذِّبَهُمْ وَأَنتَ فِيهِمْ وَمَا كَانَ اللَّـهُ مُعَذِّبَهُمْ وَهُمْ يَسْتَغْفِرُونَ ﴿٣٣﴾

33. Na Mwenyezi Mungu hakuwa ni mwenye kuwaadhibu maadamu wewe umo pamoja nao. Wala hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaadhibu hali wanaomba msamaha.

وَمَا لَهُمْ أَلَّا يُعَذِّبَهُمُ اللَّـهُ وَهُمْ يَصُدُّونَ عَنِ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَمَا كَانُوا أَوْلِيَاءَهُ إِنْ أَوْلِيَاؤُهُ إِلَّا الْمُتَّقُونَ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٣٤﴾

34. Na wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu; hali wao wanazuilia (watu) msikiti mtakatifu? Wala wao hawakuwa ndio walinzi wake. Hawakuwa walinzi wake isipokuwa wenye takuwa tu, lakini wengi wao hawajui.

وَمَا كَانَ صَلَاتُهُمْ عِندَ الْبَيْتِ إِلَّا مُكَاءً وَتَصْدِيَةً فَذُوقُوا الْعَذَابَ بِمَا كُنتُمْ تَكْفُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Na haikuwa Swala yao kwenye hiyo nyumba ila miluzi (kupiga mbinja) na makofi. Basi onjeni adhabu kwa sababu ya yale mliyokuwa mkikufuru.

WALIPOKUFANYIA VITIMBI

Aya 30 – 35

LUGHA

Njama ikinasibishwa kwa mtu maana yake ni hila na hadaa. Na ikinasibishwa kwa Mwenyezi Mungu maana yake ni kuvunja njama.

MAANA

Na walipokupangia njama wale waliokufuru ili wakufunge au wakuue au wakutoe.

Katika Aya iliyotangulia (26) Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewakumbusha Waislamu neema yake juu yao. Katika Aya hii anamkumbusha Mtume(s.a.w.w) neema yake juu yake ambapo Washirikina wa Kiquraish walikubaliana kummaliza Nabii Muhammad(s.a.w.w) , Wakatofautiana katika njia ya kummaliza, Mmoja akasema tumfunge, mwingine akasema tumtoe Makka.

Kisha wakaafikiana wachague mtu katika kila ukoo na waivamie nyumba yake akiwa amelala kitandani wampige kwa panga zao pigo moja. Hapo damu yake itakuwa kwa koo zote, na Bani Hashim watashindwa kupigana na waarabu wote.

Wafasiri wanasema, akiwemo Tabari, Razi, na Abul Hayaan Al-Andalusi, kwamba; Mwenyezi Mungu alimpa wahyi Mtume wake kumjulisha hilo. Akamwamrisha atoke kuelekea Madina na akamwamrisha Ali bin Abu Talib alale kitandani kwake. Ali akalala kitandani kwake na kujifinika shuka yake. Walipovamia kitanda chake walimwona Ali, wakapigwa na mshangao. Pia Mtume alimwusia Ali kurudisha amana za watu walizoziweka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu.

Na wakapanga njama na Mwenyezi Mungu akapanga njama na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa kupanga njama.

Njama ya Maquraish ni ile mipango yao ya kumuua Nabii Muhammad kwa namna ambayo ukoo wa Hashim utashindwa kulipizia kisasi. Ama njama ya Mwenyezi Mungu ni kupangua njama yao kwa kupanga Mwenyezi Mungu (s.w.t) Mtume atoke, na Ali alale kitandani kwake, Yametangulia maelezo kuhusu hayo katika kufasiri Juz.3 (3:54).

Na wanaposomewa Aya zetu, husema: Tumekwishasikia. Na lau tungependa tungelisema kama haya. Haya si chochote ila ni ngano tu za watu wa kale.

Maquraish walisema kuwa Qur’an ni ngano za watu wa kale, na kwamba wao wakitaka wanaweza kusema mfano wake. Walisema hivi wakiwa wanajua fika kwamba hiyo inatoka kwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu wao na watu wote walishindwa kuleta mfano wa hata Sura moja tu.

Maquraish wameshindwa ndio maana wanakimbilia uzushi, kuficha kushindwa kwao na upotevu wao; sawa na kila anayeshindwa kuikabili haki kwa hoja na mantiki.

Na waliposema: Ewe Mwenyezi Mungu! Ikiwa haya ni haki itokayo kwako, basi tupige mvua ya mawe kutoka mbinguni au tuletee adhabu iumizayo.

Baadhi ya watu wanaweza kung’angania dhambi kwa kiburi chao; sawa na wanavong’ang’ania dini au zaidi; mpaka wanafikia kuwa tayari kufa kuliko kukubali kushindwa, hata kama upande wa pili ni haki.

Wako tayari kuangamia na kuadhibiwa kuliko kuacha mafunzo yao na mila zao. Historia imetaja mifano mingi ya watu wa aina hiyo. Qur’an imetaja Firauni, watu wa Nuh, n.k.

Maquraish walipoitwa na Mtume kwenye Uislamu walisema: “Kama Muhammad ni mkweli basi itupige mvua ya mawe.” Yaani wanaona afadhali kuangamia kwa kupigwa mawe kuliko kumfuata Muhammad, hata kama ni Nabii.

Basi Mwenyezi Mungu akawajibu kwamba adhabu bado iko mbele yao na kwamba mlango bado uko wazi; na aliwapa muda kwa sababu moja aliy oiashiria kwa kauli yake:

Na Mwenyezi Mungu hakuwa ni mwenye kuwaadhibu maadamu wewe umo ndani yao.

Yaani Mwenyezi Mungu mtukufu hawaadhibu watu wa Makka maadamu Nabii Muhammad yuko. Hii ikiwa ni kumtukuza na kumwadhimisha.

Wala hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaadhibu hali wanaomba msamaha.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kusema kuwa hatawaadhibu Maquraish maadam Nabii Muhammad yuko kwao, anasema kuwa, vilevile, hatawaadhibu wakiamini, ni sawa Nabii Muhammad awe nao au asiwe nao. Kauli yake hii Mwenyezi Mungu ni sawa na kauli yake nyingine:

مَّا يَفْعَلُ اللَّـهُ بِعَذَابِكُمْ إِن شَكَرْتُمْ وَآمَنتُمْ ﴿١٤٧﴾

“Mwenyezi Mungu ana haja gani ya kuwaadhibu kama mtashukuru na mtaamini” Juz.5 (4:147).

Makusudio ya maana haya yanafahamika kutokana na kusema kwake moja kwa moja.

Na wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu?

Na pia kauli yake akiwaambia Maquraish:

Basi onjeni adhabu kwa sababu ya yale mliyokuwa mkikufuru.

Kwa ufasaha zaidi ni kuwa maana ya Aya ni kwamba, Yeye Mwenyezi Mungu hatawadhibu ikiwa Nabii Muhammad yuko kwao, Vilevile hatawaadhibu wakisilimu.

Ametumia neno msamaha kwa maana ya kusilimu, kwa sababu msamaha ni katika mambo yanayolazimiana na Uislamu, Kwa ufafanuzi huu, inatubainikia kuwa hakuna haja ya taawili walizozitaja wafasiri, tena zinamwacha msomaji gizani.

Na wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu: hali wao wanazuilia (watu) msikiti mtakatifu?

Hilo ni swali lenye maana ya kukanusha; yaani hakuna chochote katika dini au tabia kitakachowazuia kuadhibiwa kwao. Kwani wao kwa upande wa ushirikina wao wanazuia waislamu kumwabudu Mwenyezi Mungu katika nyumba yake takatifu.

Mwislamu yeyote, hata Mtume(s.a.w.w) alipokuwa Makka, hakuwa akiweza kuswali ndani ya Masjudil-Haram bila ya kupata udhia na mateso. Waliafikiana wamzuie Mtume kwa nguvu asifanye umra mwaka wa Hudaybiya.

Wala wao hawakuwa ndio walinzi wake.

Yaani washirikina si walinzi wa Masjidul Haram wala si watu wa nyumba hiyo, bali ni maadui wa Mwenyezi Mungu na maadui wa nyumba yake. Kwa hiyo ni wajibu kuwafukuza na kuwazuia, kwa vile wanauchafua kwa najisi zao na uchafu wao. Kwa ajili hii, Uislamu ulipopata nguvu, walizuiliwa kuukurubia:

إِنَّمَا الْمُشْرِكُونَ نَجَسٌ فَلَا يَقْرَبُوا الْمَسْجِدَ الْحَرَامَ بَعْدَ عَامِهِمْ هَـٰذَا ﴿٢٨﴾

“Hakika washirikina ni najisi, kwa hiyo wasiukaribie Msikiti mtakatifu baada ya mwaka wao huu” (9:28).

Hawakuwa walinzi wake isipokuwa wenye takuwa tu.

Yaani hatastahiki yeyote, vyovyote alivyo; kuusimamia Msikiti mtakatifu (Masjidul Haram) ila akiwa ni mwema mwenye kumcha Mungu akiwa Mwislamu aliyepiga shahada, Je, itakuwaje mshirikina na mwenye kupinga?

Ingawaje maudhui ya Aya yanahusika na msikiti mtakatifu, lakini takuwa ni sharti ya kila anayesimamia misikiti au sehemu za kidini. Kwa vile sababu ya hilo ni utwahara wa mahali na utakatifu wake. La kushangaza ni kwamba wengi wanaosimamia mambo haya ni wale viumbe waovu ambao ni mabingwa wa fani ya hila na wizi.

Lakini wengi wao hawajui kwamba mwenye kusimamia msikiti na sehemu takatifu ni lazima awe mwema, mcha Mungu; na kwamba hakuna usimamizi kwa fasiki.

Utauliza : kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu” inafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu aliwaadhibu Maquraish, ambapo inajulikana kuwa hayakuwapitia kama yaliyowapitia watu wa Mitume waliotangulia, kama vile Ad, Thamud, watu wa Nuh, wa Lut n.k.?

Jibu : Wale waliomuudhi Mtume na waislamu, Mwenyezi Mungu aliwaua siku ya Badr kwa mikono ya waislamu wenyewe. Miongoni mwa waliouwawa ni Abu Jahl, Uqba bin Abu Mui’t, Nadhr bin Al-Harith, Umayya bin Khalaf na wengineo katika vigogo vya Maquraish ambao walikuwa wamezidi mno kuwaudhi waislamu.

Kwa mfano Umayya bin Khalaf alikuwa akimmiliki Bilal mwadhini wa Mtume(s.a.w.w) . Alikuwa akimwadhibu kwenye mchanga ulio moto sana na kumpa adhabu za kila aina. Siku ya Badr Umayya alitoka pamoja na washirikina, na Bilal naye akatoka pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu.

Mara tu, Bilal alipomwona Umayya alipiga ukelele: “Huyu kiongozi wa ukafiri, ama zake ama zangu.” Wakakusanyika baadhi ya wanyonge waliokuwa wakiteswa na huyu Umayya wakamshika; Bilal naye akampiga Umayya kwa upanga mpaka akamuua.

Akakichukua kichwa chake akakitungika kwenye upanga wake na huku akicheza kwa furaha.

Na haikuwa swala yao kwenye hiyo nyumba ila miluzi (kupiga mbinja) na makofi.

Kama kwamba mwulizaji anauliza: Maquraish walikuwa wakiswali katika msikiti mtukufu, sasa vipi wamestahiki adhabu? Akajibu Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa swala yao ilikuwa ni vurugu tu, haina unyenyekevu.

Kwa sababu ilikuwa ni miluzi (mbinja) ya mdomoni na makofi ya mikononi.

Basi onjeni adhabu iliyowafikia siku ya Badr.

Na adhabu ya akhera ni kali zaidi.

Kwa sababu ya yale mliyokuwa mkikufuru.

Lau mngesilimu mngelisalimika na adhabu ya duniani na akhera.

إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا يُنفِقُونَ أَمْوَالَهُمْ لِيَصُدُّوا عَن سَبِيلِ اللَّـهِ فَسَيُنفِقُونَهَا ثُمَّ تَكُونُ عَلَيْهِمْ حَسْرَةً ثُمَّ يُغْلَبُونَ وَالَّذِينَ كَفَرُوا إِلَىٰ جَهَنَّمَ يُحْشَرُونَ ﴿٣٦﴾

36. Hakika wale waliokufuru hutoa mali zao ili kuzuilia njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watazitoa, kisha zitakuwa majuto juu yao, kisha watashindwa. Na wale waliokufuru watakusanywa kwenye Jahanamu.

لِيَمِيزَ اللَّـهُ الْخَبِيثَ مِنَ الطَّيِّبِ وَيَجْعَلَ الْخَبِيثَ بَعْضَهُ عَلَىٰ بَعْضٍ فَيَرْكُمَهُ جَمِيعًا فَيَجْعَلَهُ فِي جَهَنَّمَ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْخَاسِرُونَ ﴿٣٧﴾

37. Ili Mwenyezi Mungu apate kuwapambanua walio wabaya na walio wazuri na kuwaweka wabaya juu ya wabaya wengine na kuwarundika wote pamoja na kuwatupa katika Jahanamu, Hao ndio waliohasirika.

قُل لِّلَّذِينَ كَفَرُوا إِن يَنتَهُوا يُغْفَرْ لَهُم مَّا قَدْ سَلَفَ وَإِن يَعُودُوا فَقَدْ مَضَتْ سُنَّتُ الْأَوَّلِينَ ﴿٣٨﴾

38. Waambie wale waliokufuru, kama watakoma, watasamehewa yaliyopita. Na wakirudia basi imekwishapita desturi ya watu wa zamani.

وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ كُلُّهُ لِلَّـهِ فَإِنِ انتَهَوْا فَإِنَّ اللَّـهَ بِمَا يَعْمَلُونَ بَصِيرٌ ﴿٣٩﴾

39. Na piganeni nao mpaka kusiwe na fitna na dini yote iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Wakikoma, basi hakika Mwenyezi Mungu anayaona wanayotenda.

وَإِن تَوَلَّوْا فَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ مَوْلَاكُمْ نِعْمَ الْمَوْلَىٰ وَنِعْمَ النَّصِيرُ ﴿٤٠﴾

40. Na wakigeuka, basi jueni kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Mola wenu, ni Mola mwema na msaidizi mwema.

WALIOKUFURU HUTOA MALI ZAO

Aya 36 – 40

MAANA

Hakika wale waliokufuru hutoa mali zao ili kuzuilia njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watazitoa, kisha zitakuwa majuto juu yao, kisha watashindwa. Na wale waliokufuru watakusanywa kwenye Jahanamu.

Washirikina walikuwa wakitoa mali zao katika kupigana na waislamu na kuzuilia watu Uslamu.

Ndipo Mwenyezi Mungu akabainisha, katika Aya hii, kwamba mali hizo zitawarudishia majuto, udhalili duniani na adhabu kali huko akhera. Kwa sababu mwisho ushindi utakuwa wa dini ya Mwenyezi Mungu na watu wake.

Ili Mwenyezi Mungu apate kuwapambanua walio wabaya na walio wazuri.

Hii ni sababu na kubainisha sababu yenye kuwajibisha majuto ya Washirikina na udhalili wao. Nayo ni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mwadilifu na mwenye hekima.

Miongoni mwa uadilifu wake ni kutokuwa sawa mbele yake mwema na mwovu na Mu’min na kafiri, bali atampambanua kila mmoja na kumfanyia anayostahiki.

Kwa ajili hii, atampa thawabu mwema na kumwinua huko akhera. Na pengine humchanganyia malipo ya dunia na akhera. Na atamdhalilisha mwovu na kumwadhibu huko akhera kwenye nyumba ya hisabu na malipo. Pengine humpa aina fulani ya adhabu katika dunia kwa kadiri hekima yake inavyotaka.

Na kuwaweka wabaya juu ya wabaya wengine na kuwarundika wote pamoja na kuwatupa katika Jahanamu.

Makusudio ni jinsi ya wabaya; yaani wanaofungamana na jina hilo. Kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu.

Hao ndio waliohasirika.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu kesho atawakusanya wabaya wakiwa mrundo kisha awatupe katika Jahanamu, kama anavyofanya mtafuta kuni akizikusanya pamoja na kuzitia motoni. Mwenyezi Mungu anasema:

وَأَمَّا الْقَاسِطُونَ فَكَانُوا لِجَهَنَّمَ حَطَبًا ﴿١٥﴾

“Na ama wanaokengeuka (kuiacha haki) watakuwa kuni za Jahanamu.” (72:15).

Hao ndio waliohasirika.

Kuna hasara gani kubwa zaidi ya kuwa mtu na nyama zake na damu yake ni kuni za moto alioukoka Mwenyezi Mungu kwa ghadhabu yake juu ya aliyemfanyia hiyana Mola wake na dhamir yake!

“Ewe Mwenyezi Mungu! Hakika sisi tunaihofia adhabu yako, Na tunakimbilia kwako, Wewe ni mkarimu humfukuzi mwenye kutaka hifadhi ya ukarimu wako na kukimbilia rehema yako.”

Waambie wale waliokufuru, kama watakoma, watasamehewa yaliyopita.

Maneno haya anaambiwa Mtume(s.a.w.w) . Mwenyezi Mungu anamwamrisha kuwapa mawaidha makafiri na kuwaambia mlango wa toba uko wazi mbele yao, na kwamba wamepewa fursa ya kuacha ukafiri na uadui kwa Mwenyezi Mungu na Mtume, wakitubia basi Mwenyezi Mungu atawakubalia toba.

Kwa sababu Uislamu unakata yaliyokuwa kabla yake; kama ilivyoelezwa katika Hadith.

Na wakirudia basi imekwishapita desturi ya watu wa zamani.

Mfano wale waliokadhibisha Mitume na kuwapiga vita. Makusudio ya desturi ya Mwenyezi Mungu kwa waliopita – ni kuangamizwa makafiri, na Mitume kuwa washindi.

Mwenyezi Mungu amekwishandika: Hakika nitashinda mimi na Mitume wangu.

إِنَّ اللَّـهَ قَوِيٌّ عَزِيزٌ ﴿٢١﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye nguvu, mwenye kushinda.” (58:21).

Na piganeni nao mpaka kusiwe na fitna na dini yote iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Wakikoma, basi hakika Mwenyezi Mungu anayaona wanayotenda.

Makusudio ya Fitna hapa ni ukafiri. Aya imetangulia na tafsiri yake katika Juz.2 (2:193).

Na wakigeuka, basi jueni kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Mola wenu, ni Mola mwema na msaidizi mwema.

Yaani kama washirikina wakipingana na ubainifu wa Mtume na amani yake, basi mjiizatiti enyi Waislamu wala msiwaogope. Kwani Mwenyezi Mungu atawasaidia na atawalinda; naye ni mbora wa walinzi na wasaidizi.

SHARTI YA KUCHAPA

Sharti ya kuchapa au kusambaza ni kutaja rejeo hili. haki zote zimehifadhiwa na Taasisi ya Al-Hasanain Taasisi ya Imamu Husein(a.s)

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini(a.s) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini.

MWISHO WA JUZUU YA TISA