TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA Juzuu 11

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 9737
Pakua: 1411

Maelezo zaidi:

Juzuu 11
Juzuu 1
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9737 / Pakua: 1411
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA Juzuu 11

Mwandishi:
Swahili

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA

خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا وَصَلِّ عَلَيْهِمْ إِنَّ صَلَاتَكَ سَكَنٌ لَّهُمْ وَاللَّـهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ ﴿١٠٣﴾

103. Chukua sadaka katika mali zao uwasafishe na uwatakase kwayo. Na uwaombee rehema, Hakika maombi yako ni utulivu kwao. Na Mwenyezi Mungu ni Msikizi, Mjuzi.

أَلَمْ يَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ هُوَ يَقْبَلُ التَّوْبَةَ عَنْ عِبَادِهِ وَيَأْخُذُ الصَّدَقَاتِ وَأَنَّ اللَّـهَ هُوَ التَّوَّابُ الرَّحِيمُ ﴿١٠٤﴾

104. Je, hawajui kwamba Mwenyezi Mungu ndiye anayekubali tob aya waja wake na kuzipokea sadaka. Na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kukubali toba, Mwenye kurehemu?

وَقُلِ اعْمَلُوا فَسَيَرَى اللَّـهُ عَمَلَكُمْ وَرَسُولُهُ وَالْمُؤْمِنُونَ وَسَتُرَدُّونَ إِلَىٰ عَالِمِ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿١٠٥﴾

105. Na sema: Tendeni vitendo Mwenyezi Mungu na Mtume wake na waumini wataviona vitendo vyenu na mtarudishwa kwa Mjuzi wa ghaibu na dhahiri, naye awaambie mliyokuwa mkiyatenda.

وَآخَرُونَ مُرْجَوْنَ لِأَمْرِ اللَّـهِ إِمَّا يُعَذِّبُهُمْ وَإِمَّا يَتُوبُ عَلَيْهِمْ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ ﴿١٠٦﴾

106. Nawengine wanangojea amri ya Mwenyezi Mungu, ama atawaadhibu au awakubalie toba, Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

CHUKUA SADAKA KATIKA MALI ZAO

Aya 103 – 106

MAANA

Chukua sadaka katika mali zao uwasafishe na uwatakase kwayo.

Wameafikiana kuwa dhamir katika ‘kwayo’ ni ya sadaka, na wakahitalifiana katika dhamir ya mali zao. Ikasemwa kuwa inawarudia wale waliochanganya amali njema na mbaya Ikasemwa kuwa inawarudia matajiri wote kwa sababu Aya imeshuka katika zaka ya wajibu. Kauli hii iko karibu na maana.

Kwa hiyo maana yatakuwa ni chukua ewe Mtume! Zaka katika mali za matajiri, kwani zinawatakasa na ubakhili kwa haki ya Mwenyezi Mungu. Tumezungumzia zaka katika kufasiri Aya 60 ya Sura hii, na Juz. 3 (2: 274)

Na uwaombee rehema, Hakika maombi yako ni utulivu kwao.

Yaani muombee baraka na maghufira mwenye kutoa zaka, kwani hupata furaha na raha ya nafsi kwa dua yao.

Na Mwenyezi Mungu ni Msikizi, Mjuzi.

Anasikia na ataitikia maombi yako kwa watoaji zaka, na anajua nia ya anayetoa zaka kwa roho safi, kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu peke yake.

Je, hawajui kwamba Mwenyezi Mungu ndiye anayekubali toba ya waja wake na kuzipokea sadaka?

Mfumo unaashiria kwamba toba imetajwa hapa kwa kuashiria kuwa mwenye kuzuia zaka, kisha akatubia na akaitoa, basi Mwenyezi Mungu ataikubali toba yake na kupokea sadaka yake. Maana ya kukubali ni kwamba Mweneyezi Mungu, ambaye limetukuka neno lake atailipa thawabu. Kuna Hadith isemayo: “Hakika sadaka inaingia mkononi mwa Mwingi wa rehema kabla ya kuingia katika mkono wa mwombaji.” Mkono wa Mwingi wa rehema ni fumbo la kukubali.

Na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kukubali toba, Mwenye kurehemu?

Yaani anakubali toba na kuwarehemu wenye kutubia.

Na sema: Tendeni vitendo Mwenyezi Mungu na Mtume wake na Waumini wataviona vitendo vyenu.

Katika kitabu Futuhatul-Makkiyaa J4, ameitaja Muhyiddin bin Al-arabi, Aya hii na kuifafanua kuwa maana ya kuona yanatofautiana kulingana na mwonaji. Kwa hiyo maana ya kuona kwa Mwenyezi Mungu ni kukijua kitu kwa pande zake zote. Maana yake kwa Mtume(s.a.w.w) ni kujua kitu kwa njia ya wahyi uliomshukia. Maana yake kwa na mumin mwenye maarifa, ni kujua kwa kadiri ya alivyojua na kufahamu kutokana na wahyi ulioteremshiwa Mtume(s.a.w.w) .

Kwa hiyo basi, mwenye kufanya amali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu anajua hakika ya amali yake na kuiridhia; Mtume naye anajua kuwa amali hii imeridhiwa kwa Mwenyezi Mungu, na mumin pia anajua kuwa ni mwenye kuridhiwa na Mtume. Natija ya mwisho ni kuwa mwenye kufanya amali njema anaridhiwa na Mwenyezi Mungu, Mtume na waumini.

Na wengine wanangojea amri ya Mwenyezi Mungu, ama atawaadhibu au awakubalie toba.

Katika Aya ya 100 na inayofuatia, Mwenyezi Mungu (s.w.t), ametaja aina nne ya watu: Waliotangulia kuhama na waliotangulia kusaidia, waliowa- fuatia hao kwa wema, wanafiki na wenye kukiri dhambi zao.

Katika Aya hii ameashiria watu ambao hakuwapa sifa maalum, kama alivyofanya kwa aina hizo nne, wala hakuweka wazi hukumu yao; isipokuwa amesema kuwa wao wanangojea adhabu ya Mwenyezi Mungu au msamaha wake; yaani jambo lao liko Kwake Yeye Peke Yake, amewaficha. Huenda hekima ya hivi ni kuwa wawe baina ya kuhofia na kutarajia, wasiwe na tamaa wala kukata tamaa.

Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

Ni Mjuzi, wa yanayowafaa hawa na wengineo, na ni mwenye hekima kati- ka kufanya wangojee hukumu yao na katika kila analolifanya.

Wafasiri wengi wanasema kuwa Aya hii iliwashukia jamaa katika waislam waliobaki nyuma katika vita vya Tabuk, kisha wakajuta.

Lakini Aya 118, imeeleza kuwa masahaba watatu walibaki nyuma katika vita ya Tabuk, kisha wakatubia na kwamba Mwenyezi Mungu aliwatakabalia toba yao na akatangaza kukubali kwake, wala hakuwacha baina ya kuhofia na kukata tamaa.

Haya ndiyo yaliyotudhihirikia katiaka kufasiri Aya hii tuliyo nayo: hatujui tutapata maana gani tutakapofikia Aya hiyo ya 118, Tuonane huko.

وَالَّذِينَ اتَّخَذُوا مَسْجِدًا ضِرَارًا وَكُفْرًا وَتَفْرِيقًا بَيْنَ الْمُؤْمِنِينَ وَإِرْصَادًا لِّمَنْ حَارَبَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ مِن قَبْلُ وَلَيَحْلِفُنَّ إِنْ أَرَدْنَا إِلَّا الْحُسْنَىٰ وَاللَّـهُ يَشْهَدُ إِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿١٠٧﴾

107. Na wale waliotengeza msikiti kwa ajili ya kudhuru na ukafiri na kuwafarikisha waumini na mahali pa kuvizia kwa yule aliyempiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume hapo kabla. Na bila shaka wataapa kwamba hutakukusudia ila wema; na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo.

لَا تَقُمْ فِيهِ أَبَدًا لَّمَسْجِدٌ أُسِّسَ عَلَى التَّقْوَىٰ مِنْ أَوَّلِ يَوْمٍ أَحَقُّ أَن تَقُومَ فِيهِ فِيهِ رِجَالٌ يُحِبُّونَ أَن يَتَطَهَّرُوا وَاللَّـهُ يُحِبُّ الْمُطَّهِّرِينَ ﴿١٠٨﴾

108. Usisimame humo kabisa, Msikiti uliojengwa juu ya msingi wa takua tangu siku ya mwanzo, unastahiki zaidi wewe usimame humo. Humo mna watu wanopenda kuji takasa; na Mwenyezi Mungu anawapenda wanaojitakasa.

أَفَمَنْ أَسَّسَ بُنْيَانَهُ عَلَىٰ تَقْوَىٰ مِنَ اللَّـهِ وَرِضْوَانٍ خَيْرٌ أَم مَّنْ أَسَّسَ بُنْيَانَهُ عَلَىٰ شَفَا جُرُفٍ هَارٍ فَانْهَارَ بِهِ فِي نَارِ جَهَنَّمَ وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠٩﴾

109. Je, aliyeweka msingi wa jengo lake juu ya kumcha Mwenyezi Mungu na radhi (zake) ni bora au aliyeweka msingi jingo lake juu ukingo wa shimo linalomomonyoka, na likamomonyoka likaanguka pamoja naye katika moto wa Jahannamu na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

لَا يَزَالُ بُنْيَانُهُمُ الَّذِي بَنَوْا رِيبَةً فِي قُلُوبِهِمْ إِلَّا أَن تَقَطَّعَ قُلُوبُهُمْ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ ﴿١١٠﴾

110. Jengo lao hilo walilolijenga litaendelea kuwa ni sababu ya kutiwa wasiwasi nyoyoni mwao, isipokuwa nyoyo zao zikikatikakatika. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

MSIKITI WA MADHARA

Aya 107 –110

MAANA

Aya zilizotangulia zimeonyesha aina mbali mbali za unafiki wa wanafiki. Aya hii inaonyesha aina nyingine ya unafiki wao na hila yao.

Jamaa fulani katika wanafiki wa Madina waliona njia nzuri ya kuufanyia vitimbi Uislam na Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) ni kujenga msikiti chini ya sitara ya kujumuika kumwabudu Mwenyezi Mungu na kunadi kuwa Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Nyuma ya nembo hii watakuwa wamemkufuru Mwenyezi Mungu na Mtume wake, kuudhuru Uislamu na waislam na kuwagawanya.

Naam walijenga msikiti huu vizuri sana na kuutolea mapesa. Baada ya kuukamilisha walimwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu wakamwambia: Nyumba zetu ziko mbali na msikiti wako inakuwa vigumu kwetu kuhudhuria na tunachukia kuswali swala isiyokuwa ya Jamaa; nasi tumejenga msikiti kwa lengo hili na kwa ajili ya wanyonge na vilema. Kama utaswali humo basi itakuwa ni vizuri na tutabaruku kuswali mahali utakaposwali.

Hivi ndivyo walivyo wanafiki na wahaini kila wakati, wanabeba nembo za kutengeneza kumbe wanataka kubomoa. Lakini mara moja inafichuka aibu yao na kufedheheka mbele ya watu wote; kama walivyofedheheka wenye msikiti wa madhara, pale Mwenyezi Mungu alipomfahamisha Mtume wake hakika yao, kwa kusema:

Na wapo waliotengeza msikiti kwa ajili ya kudhuru na ukafiri na kuwafarikisha waumini na mahali pa kuvizia kwa yule aliyempiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume hapo kabla.

Aya tukufu inasema kuwa waliojenga msikit wa madhara wana malengo manne:

1. Kuwadhuru waislamu.

2. Kumkufuru Mwenyezi Mungu na kumtia ila Mtume wake.

3. Kuwagawanya waislamu na kuwaweka mbali na Mtume wa Mwenyezi Mungu.

4. Kuufanya msikiti ni maficho ya yule aliyempiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake zamani.

Wameafikiana wafasiri na waandishi wa sera ya Mtume kwamba makusudio ya adui aliyempiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake ni mtu mmoja katika Khazraji anyeitwa Abu Amir Arrahib[2] .

Alikuwa ameingia ukiristo, mwenye cheo katika watu wake, Mtume(s.a.w.w) alipofika Madina alipambana kiuadui na mlanifu huyu ambaye Mtume alikuwa akimwita fasiki.

Alipoona Mtume anazidi kupata nguvu, alikimbilia Makka kuwachochea Maquraish dhidi ya Mtume, Baada ya ushindi wa Makka alikimbilia Taif.

Watu wa Taif waliposilimu alikimbilia Sham. Huko aliwaandikia wafuasi wake wamjengee msikiti kwa sababu yeye atakuja na jeshi la Kaizari kumpiga vita Muhammad(s.a.w.w) .

Iliposhuka Aya hii, Mtume(s.a.w.w) akiwambia baadhi ya masahaba zake: “Nendeni kwenye msikiti huu wa watu madhalimu muuvunje.”

Wakafanya hivyo na Mtume(s.a.w.w) akaamrisha pale mahali pawe ni jaa. Baadhi ya mapokezi yameelezea kufananishwa msikiti wa madhara na ndama aliyeabudiwa na Waisrail na Musa akiwa hai. Kama ambavyo Nabii Musa aliamrishwa na Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumvunjavunja ndama, vile vile Mtume aliamrishwa auvunje mskiti wa madhara.

Na, msikiti wowote, taasisi au klabu yoyote inayoundwa kwa sababu ya njama dhidi ya waumini basi hiyo ni ndama wa waisrail na ni msiki wa madhara, ni wajibu kuuvunja na kuufanya jaa.

Tangu yalipopatikana mafuta katika miji ya Kiarabu, mashirika ya nje ya kusimamia mafuta yalikuja na maamia ya misikiti ya madhara kwa sura mbali mbali. Miongoni mwa sura hizo ni kama hizi zifuatazo: Ile iliyobandikwa jina la sehemu ya kuabudia au vyuo, yenye jina la ofisi kuu au taasisi za kidini na yenye majina ya maendeleo ya kijamii au vilabu vya michezo.

Mingine ni ile iliyojitokeza kwa sura ya kitab, gazeti au mhadhara unao tangazwa kwenye idhaa kwa jina la dini au la nchi na mengineyo mengi ambayo dhahiri yake ni rehema na ndani yake ni adhabu. Yote hayo lengo lake ni kuharibu dini na nchi.

Tumezungumzia kuhusu nembo za kidini katika Juz 4 (3:142)

Na bila shaka wataapa kwamba hutakukusudia ila wema; na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo.

Yaani hawa wanafiki waliapa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kwamba lengo la kujenga msikiti huu ni ibada tu na manufaa kwa waislamu; na Mwenyezi Mungu anajua kuwa wao hawakujenga msikiti ila kwa kutaka kuwadhuru waislamu, kumkufuru Mwenyezi Mungu, kuwatenganisha Waumini na maficho ya anayempiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Usisimame humo kabisa.

Maneno anaambiwa Mtume, lakini makatazo ni kwa wote; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

أَقِمِ الصَّلَاةَ لِدُلُوكِ الشَّمْسِ ﴿٧٨﴾

“Simamisha Swala jua linapopenduka” (17:78)

Wafasiri wamesema kuwa makusudio ya usisimame, hapa, ni usiswali. Lakini kwa dhahiri hapa, kusimama ni ujumla, kunachanganya swala na mengineyo.

Kwa vyovyote ilivyo, kauli yake Mwenyezi Mungu usisimame humo kabisa ni dalili mkataa ya kutosihi swala katika msikiti uliojengwa kuwadhuru waislamu na kuwatenganisha na kwamba mwenye kuswali humo, basi swala yake ni batil, ni lazima airudie mahali pengine, Kwa sababu ukatazo katika ibada unafahamisha kuharibika.

Msikiti uliojengwa juu ya msingi wa takua tangu siku ya mwanzo, unastahiki zaidi wewe usimame humo.

Imesemekana kuwa makusudio ni msikiti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kwa sababu ndio uliojengwa siku ya kwanza Madina. Na ikasemekana kuwa ni Msikiti Quba ambao waliujenga Bani Amr bin Auf. Kwa dhahiri ni kwamba makusudio ni kila msikiti uliojengwa kwa ajili ya kumcha mungu, Kwa sababu neno Msikiti limekuja kiujumla (nak`ra).

Na kauli yake:‘Tangu siku ya mwanzo, ’ maana yake ni kuwa umejengwa kwa lengo la uislamu tangu siku ya kuanza kujengwa kwake. Kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Unastahiki zaidi,’ maana yake ni kwa uhakika, na wala sio kuwa huu ni bora zaidi kuliko wa madhara. Kwa sababu msikiti wa Madhara sio bora hata kidogo na haifai kuswali ndani yake kwa vyovyote vile.

Humo mna watu wanopenda kujitakasa; na Mwenyezi Mungu anawapenda wanaojitakasa.

Yaani, msikiti huu ambao umeasisiwa kwa msingi wa takua, wenye ikhlasi wanaukusudia kwa swala na ibada ya Mwenyezi Mungu tu, si kwa unafiki na njama dhidi ya uislamu na Mtume; kama walivyofanya wenye msikiti wa madhara.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameleta ibara ya swala hapa kwa neno kuji- takasa, kwa sababu swala inamtakasa mtu na madhambi. Kuna Hadith isemayo: “Hakika swala ni kama mto unaopita, mwenye kuoga humo mara tano kila siku hatabakiwa na uchafu; vile vile mwenye kuswali mara tano kila siku hatabakiwa na dhambi.

Haya ndiyo tuliyoyafahamu katika Aya hii, pamoja na kukiri kuwa hakuna mfasiri yeyote aliyefasiri kutakata kwa maana ya swala, kama tunavyojua; na kwamba wengi wao wamefasiri kwa maana ya kutakasa uchafu kwa maji.

Je, aliyeweka msingi wa jengo lake juu ya kumcha Mwenyezi Mungu na radhi (zake) ni bora au aliyeweka msingi jengo lake juu ya ukingo wa shimo linalomomonyoka, na likamomonyoka likaanguka pamoja naye katika moto wa Jahannamu na Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

Makusudio ya Aya ni kutofautisha baina ya msikiti wa Takua na msikiti wa madhara. Kwani wa madhara hauna uthabiti na unaweza ukaanguka kwenye moto mara moja; sawa na ambaye amejenga ukingoni mwa mto au kwenye mto. Ama jengo la msikiti wa takua ni thabiti lenye msingi imara usiotingishwa na chochote; na watu wake wako katika amani. Aya hii ni mfano wa Aya isemayo:

لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿٢٠﴾

“Hawalingani sawa watu wa motoni na watu wa peponi. Watu wa peponi ndio wenye kufuzu” (59:20).

La kushangaza ni kauli ya baadhi ya wafasiri kwamba kauli ya ‘moto wa Jahanamu’ ni ishara ya yaliyotukia duniani kuwa moto ulitoka kwenye mskiti wa madhara na moshi wake ukabakia hadi zama za Abu jafar Al-Mansuru.

Jengo lao hilo walilolijenga litaendelea kuwa ni sababu ya kutiwa wasiwasi nyoyoni mwao, isipokuwa nyoyo zao zikikatikakatika. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

Makusudio ya wasiwasi hapa, ni kwamba wanafiki hawakuamini utume wa Muhammad(s.a.w.w) . Kukatika nyoyo ni fumbo la kufa. Maana ni kuwa wao walijenga msikiti wakiwa na shaka bila ya kumwamini Muhammad(s.a.w.w) , watabaki na shaka hiyo hadi kufa.

إِنَّ اللَّـهَ اشْتَرَىٰ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ أَنفُسَهُمْ وَأَمْوَالَهُم بِأَنَّ لَهُمُ الْجَنَّةَ يُقَاتِلُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَيَقْتُلُونَ وَيُقْتَلُونَ وَعْدًا عَلَيْهِ حَقًّا فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ وَالْقُرْآنِ وَمَنْ أَوْفَىٰ بِعَهْدِهِ مِنَ اللَّـهِ فَاسْتَبْشِرُوا بِبَيْعِكُمُ الَّذِي بَايَعْتُم بِهِ وَذَٰلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿١١١﴾

111. Hakika Mwenyezi Mungu amenunua kwa Waumini nafsi zao na mali zao kwamba wao wapate Pepo, wanapi gana katika njia ya Mwenyezi Mungu, kwa hiyo wanaua na kuuawa. Ni ahadi aliyojilazimisha kwa haki katika Tawrat na Injil na Qur’ani. Na ni nani atekelezaye zaidi ahadi kuliko Mwenyezi Mungu? Basi furahini kwa biashara yenu mliofanya naye, Na huko ndiko kufuzu kukubwa.

التَّائِبُونَ الْعَابِدُونَ الْحَامِدُونَ السَّائِحُونَ الرَّاكِعُونَ السَّاجِدُونَ الْآمِرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَالنَّاهُونَ عَنِ الْمُنكَرِ وَالْحَافِظُونَ لِحُدُودِ اللَّـهِ وَبَشِّرِ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١١٢﴾

112. Wanaotubia, wanaoabudu wanaohangaika, wanaorukuu, wanaosujudu, wanaoamrisha mema na wanaokataza maovu na wanaohifadhi mipaka ya Mwenyezi Mungu, Na wape bishara Waumini.

MUNGU HUUZA NA KUNUNUA

Aya 111 – 112

MAANA

Hakika Mwenyezi Mungu amenunua kwa Waumini nafsi zao na mali zao kwamba wao wapate Pepo, wanapigana katika njia ya Mwenyezi Mungu, kwa hiyo wanaua na kuuawa.

Mnunuzi ni Mwenyezi Mungu (s.w.t) muuzaji ni mumin, bidhaa ni nafsi na mali, cha kununuliwa ni pepo, na madalali ni Mitume. Bei yenyewe ni ya mkopo; kwamba muuzaji akabidhi bidhaa kwa mnunuzi atakapoitaka, lakini thamani yake atalipwa baadaye; na Mwenyezi Mungu ndiye mdhamini; na hakuna mwenye kutekeleza ahadi na tajiri zaidi ya Yeye.

Utauliza : Mungu ni muumbaji wa nafsi na Mwenye kuruzuku mali, sasa vipi mwenye kumiliki kitu akinunue.

Jibu : Huku siko kununua kunakojulikana; isipokuwa ni kuhimiza twaa. Mwenyezi Mungu ameleta ibara ya kununua kwa mambo mawili:

Kwanza : mtiifu ategemee malipo na thawabu ya twaa yake; sawa na anavyotegemea muuzaji thamani badala ya bidhaa yake.

Pili : kuzindua kuwa imani sio tu maneno ya mdomoni, picha za akilini au matamanio yanayohisiwa katika nyoyo; isipokuwa ni kujitolea mhanga kwa nafsi na mali, kutafuta thawabu za Mwenyezi Mungu ambazo ni ghali zisizokwisha; sawa na anavyotoa mnunuzi milki yake katika bidhaa ambayo anaiona ina manufaa na yenye kufaa.

Kitu kikubwa kwa binadamu ni uhai wake na nafsi yake. Ama kupenda kwake mali ni kwa kuwa hiyo ni nyenzo ya kuhifadhi uhai na kutekeleza matakwa yake na hawaa zake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawatahini wanaodai wana imani kwa vitu wanavyovipenda ili ampabanue mkweli wa imani na mwongo; wala hataweza kutoa hoja kesho kwa saumu yake na swali yake akiwa amefanya ubakhili na kujizuia kujitolea kwa nafsi yake na mali yake.

Ni ahadi aliyojilazimisha kwa haki.

Hii ni sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

كَتَبَ عَلَىٰ نَفْسِهِ الرَّحْمَةَ ﴿١٢﴾

Amejilazimisha rehema Juz.7 (6:12)

Yaani yeye mwenyewe ndiye aliyejiwajibshia, Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaahidi wapigania jihadi Pepo ikawa ni haki yao kutokana na ahadi hii;

hasa baada ya kuisajilikatika Tawrat na Injil na Qur’ani. Na ni nani atekelezaye zaidi ahadi kuliko Mwenyezi Mungu?

Lengo la usisitizo huu ni kuwa wapigania jihadi wawe na uhakika wa malipo na thawabu adhimu; mpaka wawe kama walioyaona kwa macho, wafurahi na wapate bishara.

Basi furahini kwa biashara yenu mliyofanya naye, Na huko ndiko kufuzu kukubwa.

Huu ni usisitizo mwingine wa ahadi ya malipo mema. Watalamu wa elimu ya Tawhidi wanasema kuwa Mwenyezi Mungu akiahidi thawabu, basi atatekeleza aliyoahidi, na akiahidi adhabu basi ana hiyari, akiadhhibu ni kwa uadilifu wake na akasamehe ni kwa fadhila zake; na Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.

Tumeizungumzia thamani ya Pepo katika kufasiri Juz. 2 (2:155).

Kisha Mwenyezi Mungu akawasifu wale waliouza nafsi zao na mali zao kwa Pepo yake, kwa sifa hizi zifuatazo:

Wanaotubia kwa kila wanalolikosea; hata kama ni la makruh.

Wanaoabudu . Yaani wenye ikhlasi katika matendo yao yote.

Wanaohimidi Mwenyezi Mungu katika raha na dhiki.

Wanaohangaika katika ardhi kutafuta elimu au riziki ya halali.

Wanaorukuu, wanaosujudu, Yaani wanaoswali.

Wanaoamrisha mema na wanaokataza maovu. yaani wanaoneza mwito wa Mwenyezi Mungu na twaa yake na kupamba na kila anayechezea haki yoyote miongoni mwa haki za Mungu na haki za waja wake.

Na wanaohifadhi mipaka ya Mwenyezi Mungu . Mipaka yake ni halali yake na haramu yake

Na wape bishara Waumini walio na sifa hizi, kuwa wao wana fadhila kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA MOJA

مَا كَانَ لِلنَّبِيِّ وَالَّذِينَ آمَنُوا أَن يَسْتَغْفِرُوا لِلْمُشْرِكِينَ وَلَوْ كَانُوا أُولِي قُرْبَىٰ مِن بَعْدِ مَا تَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُمْ أَصْحَابُ الْجَحِيمِ ﴿١١٣﴾

113. Haimfalii Mtume na wale walioamini kuwatakia msamaha washirikina ijapokuwa ni jamaa. Baada ya kuwabainikia kuwa wao ni watu wa motoni.

وَمَا كَانَ اسْتِغْفَارُ إِبْرَاهِيمَ لِأَبِيهِ إِلَّا عَن مَّوْعِدَةٍ وَعَدَهَا إِيَّاهُ فَلَمَّا تَبَيَّنَ لَهُ أَنَّهُ عَدُوٌّ لِّلَّـهِ تَبَرَّأَ مِنْهُ إِنَّ إِبْرَاهِيمَ لَأَوَّاهٌ حَلِيمٌ ﴿١١٤﴾

114. Na haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila ni kwa sababu ya ahadi aliyofanya naye, lakini ilipom pambanukia kuwa yeye ni adui wa Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye. Hakika Ibrahim alikuwa Mpole sana wa moyo mvumilivu.

ABU TWALIB NA KUWATAKIA MSAMAHA WASHIRIKINA

Aya 113 – 114

KUSHUKA AYA

Watu wamesema mengi kuhusu Uislamu wa Abu Twalib, ami yake Mtume(s.a.w.w) . Kauli zimetofautiana na viko vitabu vya zamani na karibuni kuhusu suala hilo. Vile vile maudhui haya yaliwahi kutolewa katika kurasa za gazeti la Majallatul-Arabi Na 108 na 110.

Wanaosema kuwa alisilimu, wametoa dalili kwa yale aliyopambana nayo kutoka kwa vigogo vya maquraish na kauli zake katika kumsifu Mtume kishairi n.k. Ama wale waliosema kuwa alikuwa mshirikina, walitoa dalili kwa riwaya inayosema kuwa Aya mbili hizi zilishuka kuhusiana na Abu Twalib.

Nilipofika hapa kufasiri, nilifuatilia riwaya na kauli katika vitabu vya zamani na vya sasa kuhusu sababu za kushuka Aya mbili hizi, nikatoka na natija kuwa wapokezi na wafasiri wametofautiana kwenye kauli tatu kuhusu sababu za kushuka Aya hizi.

KAULI YA KWANZA

Kuwa jamaa katika Waumini walisema, tuwatakie msamaha wafu wetu washirikina; kama alivyomtakia msamaha Ibrahim baba yake, ndipo zikashuka Aya mbili hizi.

Haya yametajwa na Tabari, Razi na Abu Hayan Al-andalusi. Vile vile mwenye Tafsiri Al-manar na wengineo.

Kauli hii ina nguvu kuliko kauli nyingine, kwa sababu katika Aya hizo kuna matamko yanayofahamisha hivyo; kama vile kauli yake Mwenyezi Mungu “…na wale walioamini kuwatakia msamaha washirikina ijapokuwa jamaa …”

Kwa hiyo kukatazwa waumini kuwatakia msamaha jamaa zao, washirikina, kunatambulisha kuwa wao walikuwa wakiwatakia msamah au walijaribu kufanya hivyo.

Vile vile kauli isemayo:“Na haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake …”

Hilo ni jawabu la kauli ya waumini waliposema: Kama alivyomtakia msamaha Ibrahim baba yake.

KAULI YA PILI

Kwamba Mtume(s.a.w.w) alikwenda kwenye kaburi la mama yake akalia, na kumtaka idhini Mola wake amwombee msamaha, ndipo zikashuka Aya mbili hizo. Kauli hii wameitaja wale tuliowanukuu kwenye kauli ya kwanza.

Kauli hii inaizidi ile isemayo kuwa zilishuka wakati wa kufa Ami yake Abu Twalib. Kwa sababu Abu Twalib alikufa Makka katika mwaka wa huzuni miaka mitatu kabla ya Hijra, na Sura ya Tawba yenye Aya hizo mbili ilishu- ka Madina mwaka wa 9 Hijra – miaka 12 tangu kufa AbuTwalib.

KAULI YA TATU

Kwamba Aya mbili hizi zilishuka kwa Abu Twalib kwa madai ya kwamba Mtume alimwambia Ami yake, AbuTwalib akiwa karibu ya kukata roho: “Ewe Ami sema: “Lailaha illa llah” lakini hakusema, Mtume akasema: “Nitakuombea msamaha kwa Mwenyezi Mungu maadamu sijakatazwa”

Kauli hii imejibiwa na kundi la maulama kwa kauli mbili:

Kwanza : kuwa Aya mbili, kama tulivyodokeza, zilishuka baada ya kufa Abu Twalib.

Pili : kwamba Abu Twalib alikufa baada ya kusilimu na kuufanyia ikhlasi Uislamu wake, Tazama kitabu Al-Ghadiri cha Aminiy J7 Uk 369 chapa ya mwaka 1967.

HALI HALISI

Kama tukiachana na kauli za wafasiri na wapokezi, tukaiweka itikadi ya Abu Twalib kutegemea alivyokuwa, kulingana na mambo yalivyo, basi natija itakuwa kwamba Abu Twalib alikuwa akiamini utume wa Muhammad(s.a.w.w) katika kauli zake zote na vitendo vyake, Na huo ndio Uislamu hasa.

Mtume aliinukia akiwa ni yatima wa baba na mama – Baba yake alikufa akiwa yuko tumboni na inasemekana kuwa alikuwa mtoto mchanga. Mama yake akafa akiwa na miaka sita, Akabaki katika malezi ya babu yake, Abdul Muttwalib, kiasi cha miaka minane.

Babu yake alipofikiwa na mauti alimkabidhi kwa Abu Twalib. Abu Twalib hakuwa ndiye mtoto mkubwa wa Abdul Mutwalib, wala hakuwa na mali nyingi isipokuwa alikuwa ndiye mwenye heshima, mwenye hulka nzuri na mkarimu sana kuliko ndugu zake wote.

Kwa hiyo Abu Twalib akamlea vizuri; akampenda sana kuliko watoto wake; alitunga kasida ndefu na fupi kumsifu; alikuwa akitabaruku naye na akimtegemea wakati wa balaa kutokana na karama zilizodhihiri kwake.

Imepokewa kutoka kwa Ibn Asakir, kwamba watu wa Makka walipatwa na kahati; akatoka Abu Twalib na Muhammad akiwa ni kijana akaomba mvua kwa uso wake. Ikabubujika mvua na ardhi ikarutubika.

Ismail Haqqi anasema katika Rawhilbayaan katika kufasiri (12:45): “Abu Twalib alimlea na kumhami Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na kumtetea katika uhai wake”.

Ilivyo ni kwamba yeye ni miongoni mwa waliokuwa na imani kama ilivyotangulia kuelezwa.

JE, KUNA SIRI GANI?

Ikiwa Abu Twalib anampenda Muhammad, anajitolea kwa nafsi yake na kuwa tayari kufa ili amsaidie, kutegemea ukweli wake na msimamo wake, naye aliona aliyoyaona katika karama zake, kabla ya utume na baada ya utume, kwa nini basi asiamini utume wake?

Ikiwa ni kweli madai ya kuwa Abu Twalib si Mwislamu basi itabidi kuweko na siri iiyomzuia kuwa Mwislamuu Je, ni siri gani hiyo? Je, Abu Twalib, aliyekuwa akimjua kiuhakika Muhammad, alimwona na mambo yanayopingana na Utume? Hapana! Mwenye kudai hivyo si Mwislamu kabisa!

Kisha itakuwaje Muhammad(s.a.w.w) aweze kuwakinaisha wachunga ngamia na wale waliokuwa hawajui chochote zamani, lakini ashindwe kumkinaisha ami yake, Abu Twalib ambaye alikuwa akimjua chimbuko lake?

Je, Abu Twalib alikuwa na akili ndogo kuliko Bedui wa jangwani, au alikuw ana tamaa iliyomzuia kusilimu, kama walivyozuilika wenye tamaa? Matamanio ambayo yangeweza kumzuia Abu Twalib kuingia Uislamu ni moja kati ya mambo mawili: Ama kuhofia mali yake na utajiri wake, na ilivyo ni kwamba Abu Twalib aliishi maisha ya kifukara na alikufa fukara. Au itakuwa ni kuhofia kuondokewa na uongozi katika nyumba ya Hashim nk, na ni kinyume cha hivyo.

Ikiwa sababu hizo mbili hazipo, na tukiunganisha kukosekana sababu na mambo yanayoelekeza Uislamu wake, ambayo ni kumpenda kwake Muhammad na kujua uhakika wake, basi natija ni kwamba Abu Twalib sio tu kuwa alisilimu bali ni katika waislamu wa mwanzo.

Vile vile ikiwa itabatilika kauli kuwa Aya mbili zilimshukia Abu Twalib na haikuthibitika riwaya sahihi kwamba zilishuka kwa sababu ya mama wa Mtume, basi itabakia kauli ya kwanza, kwamba ziliwashukiwa watu waliokuwa au waliojaribu kuwaombea msamaha watu wao; na dhahiri ya Aya mbili inaliweka wazi hilo.

MAANA

Haimfalii Mtume na wale walioamini kuwatakia msamaha washirikina ijapokuwa ni jamaa.

Imeelezwa katika Tafsir Tabari haya yafuatayo; ninanukuu: “Watu katika maswahaba wa Mtume(s.a.w.w) walisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Katika mababa zetu wako waliokuwa na ujirani mwema, wakiunga udugu, wakisadia na kutekeleza madeni; je, tuwatakie msamaha? Akasema: Kwa nini isiwe hivyo, nami nitamtakia msamaha baba yangu, kama Ibrahim alivyomtakia msamaha baba yake, Ndipo Mwenyezi Mungu akateremsha Aya hiyo.”

Utauliza : kuwa itakuwaje Mtume(s.a.w.w) atoe idhini kwa masahaba zake kuwatakia maghufira baba zao washirki na ikiwa ni haramu?

Jibu : Kila kitu ni halali mpaka kikatazwe; na wakati Mtume alipotoa idhini kuombea msamaha hakukuwa kumekatazwa; baada ya kukatazwa, aliwakataza.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha sababu za kukataza kwa kusema:

Baada ya kuwabainikia kuwa wao ni watu wa motoni.

Aya hii inatufahamisha kuwa mtu anahukumia ukafiri wake na imani yake kutokana na dhahiri ya hali yake, na kwamba ambaye dhahiri yake ni ukafiri basi haifai kumtakia msamaha wala kumrehemu.

Utauliza : Ikiwa kuwaombea msamaha washirikina ni haramu, kwanini Mtume aliwaombea msamaha watu wake walipomvunja meno na wakamchana uso wake? Imethibitika kwamba yeye alisema: “Ewe Mola Wangu! Wasamehe watu wangu, kwani wao hawajui.”

Wafasiri wengi wamelijibu swali hii kwamba Aya imekataza kutakiwa msamaha washirikina waliokufa, sio waliohai wanaotarajiwa imani yao.

Jibu : tunaloliona ni kwamba kutaka msamaha kwa Mtume(s.a.w.w) kulikuwa ni kusamehe haki yake ya kibinadamu, sio kusamehe haki ya Mwenyezi Mungu na maghufira kwa ushirikina.

Na, hakuna mwenye shaka kwamba inafaa kwa mtu kusamehe haki yake, inayomhusu yeye tu, kwa mwislamu na kafiri.

Swali la pili : Ibrahim alikuwa akimlingania baba yake kwenye imani na kumhimiza na kumwahidi kumtakia msamaha; kama asemavyo Mwenyezi Mungu:

إِلَّا قَوْلَ إِبْرَاهِيمَ لِأَبِيهِ لَأَسْتَغْفِرَنَّ لَكَ وَمَا أَمْلِكُ لَكَ مِنَ اللَّـهِ مِن شَيْءٍ ﴿٤﴾

“… Ila kauli ya Ibrahim kumwambia baba yake: Hakika nitakuombea msamaha, wala similiki chochote kwa ajili yako mbele za Mwenyezi Mungu…”(60:4)

Naye alitekeleza ahadi yake hii na akamwombea msamaha kwa kusema:

رَبَّنَا اغْفِرْ لِي وَلِوَالِدَيَّ وَلِلْمُؤْمِنِينَ يَوْمَ يَقُومُ الْحِسَابُ ﴿٤١﴾

“Ewe Mola wetu! Unighufirie mimi na wazazi wangu wawili na waumini, siku ya kusimama hisabu.” (14:41)

Sasa vipi Ibrahim(a.s) alimtakia msamaha baba yake, ambapo kumtakia msama mshirikina hakufai? Mwenyezi Mungu (s.w.t) amejibu swali hilo kwa kusema:

Na haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila ni kwa sababu ya ahadi aliyofanya naye, lakini ilipompambanukia kuwa yeye ni adui wa Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye.

Yaani Ibrahim(a.s) alimtakia msamaha baba yake kwa vile tu, alimwahidi kuwa atamwamini Mungu. Alipovunja ahadi na kumbainikia kuwa yeye ni adui wa Mwenyezi Mungu alijiepusha naye.

Sio mbali kuwa dua ya Ibrahim(a.s) kwa baba yake, ni sawa na dua ya Muhammad(s.a.w.w) kwa watu wake washirikina; yaani kusamehe haki yake ya kibinadamu, sio haki ya Mwenyezi Mungu na kutakia msamaha ushirikina.

Hilo linatambulika kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu mtukufu.

Hakika Ibrahim alikuwa Mpole sana wa moyo mvumilivu.

Mpole wa moyo ni yule mnyenyekevu na mvumilivu ni yale anayesamehe akiwa na uwezo. Na, Ibrahim alisamehe kauli ya baba yake:

لَئِن لَّمْ تَنتَهِ لَأَرْجُمَنَّكَ وَاهْجُرْنِي مَلِيًّا ﴿٤٦﴾

“Usipokoma nitakupiga mawe, na niondokelee mbali kwa muda mhache” (19:46)

وَمَا كَانَ اللَّـهُ لِيُضِلَّ قَوْمًا بَعْدَ إِذْ هَدَاهُمْ حَتَّىٰ يُبَيِّنَ لَهُم مَّا يَتَّقُونَ إِنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿١١٥﴾

115. Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwapoteza watu baada ya kuwaongoza; mpaka awabainishie ya kujiepusha nayo Hakika Mwenyezi Mungu anajua kila kitu.

إِنَّ اللَّـهَ لَهُ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ يُحْيِي وَيُمِيتُ وَمَا لَكُم مِّن دُونِ اللَّـهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا نَصِيرٍ ﴿١١٦﴾

116. Hakika Mwenyezi Mungu ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, huhuisha na hufisha; nanyi hamna mlinzi wala msaidizi isipokuwa Mwenyezi Mungu.

MWENYEZI MUNGU HAWAPOTEZI WATU

Aya 115 –116

MAANA

Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwapoteza watu baada ya kuwaongoza.

Makusudio ya kuwapoteza ni kuwahisabu na kuwachukulia kuwa wamepotea. Na makusudio ya watu ni waumini tu; kwa dalili ya kauli yake, ‘baada ya kuwaongoza.’

Maana ni kuwa waumini wakifanya kitu chochote wasichokijua kuwa ni halali au haramu; kama vile kuwaombea msamaha au kuwarehemu washirikina kwa kutojua uharamu, basi Mwenyezi Mungu (s.w.t) hatawaadhibu, mpaka awabainishie ya kujiepusha nayo kwa ubainifu ulio wazi wa kiasi. Baada ya ubainifu, wakifanya uasi,hapo watastahiki adhabu.

Tafsiri bora ya Aya hii ni kauli ya Mtume mtukufu(s.a.w.w) : “Mtu yoyote aliyefanya jambo kwa kutojua hana neno.” Na kauli ya Imam Ja’far Asswadiq(a.s) : “Kila kitu ni halali mpaka kikatazwe.”

Hakika Mwenyezi Mungu ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, huhuisha na hufisha, nanyi hamna mlinzi wala msaidizi isipokuwa Mwenyezi Mungu.

Aya ikowazi na mfano wake umekwishapita mara nyingi na utaendelea kuja. Lengo ni kuwa binadamu daima awe pamoja na Mungu na kuukumbuka ukuu wake; na kwamba yeye peke yake ndiye bwana wake, ili asiweze kupetuka mpaka wowote katika mipaka yake.

لَّقَد تَّابَ اللَّـهُ عَلَى النَّبِيِّ وَالْمُهَاجِرِينَ وَالْأَنصَارِ الَّذِينَ اتَّبَعُوهُ فِي سَاعَةِ الْعُسْرَةِ مِن بَعْدِ مَا كَادَ يَزِيغُ قُلُوبُ فَرِيقٍ مِّنْهُمْ ثُمَّ تَابَ عَلَيْهِمْ إِنَّهُ بِهِمْ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ﴿١١٧﴾

117. Hakika Mwenyezi Mungu amekwisha pokea toba ya Mtume na wahajiri na Answar waliomfuata saa ya dhiki. Baada ya nyoyo za baadhi yao kukurubia kugeuka, Kisha akawakubalia toba. Hakika yeye kwao ni Mpole Mwenye kurehemu.

وَعَلَى الثَّلَاثَةِ الَّذِينَ خُلِّفُوا حَتَّىٰ إِذَا ضَاقَتْ عَلَيْهِمُ الْأَرْضُ بِمَا رَحُبَتْ وَضَاقَتْ عَلَيْهِمْ أَنفُسُهُمْ وَظَنُّوا أَن لَّا مَلْجَأَ مِنَ اللَّـهِ إِلَّا إِلَيْهِ ثُمَّ تَابَ عَلَيْهِمْ لِيَتُوبُوا إِنَّ اللَّـهَ هُوَ التَّوَّابُ الرَّحِيمُ ﴿١١٨﴾

118. Na pia wale watatu walioachwa nyuma, mpaka ardhi ikawa finyu juu yao pamoja na wasaa wake; na nafsi zao zikadhikika juu yao, na wakayakinisha kuwa hakuna kwa kumkimbia Mwenyezi Mungu isipokuwa kwake. Kisha akawakubalia toba ili wapate kutubu. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwingi wa kukubali toba Mwenye kurehemu.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَكُونُوا مَعَ الصَّادِقِينَ ﴿١١٩﴾

119. Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu na kuweni pamoja na wa kweli.

MWENYEZI MUNGU AMEMKUBALIA TOBA MTUME

Aya 117 – 119

MAANA

Bado maelezo ni ya vita vya Tabuk na matukio yake, Vita hivi vina mambo yake mahsusi yasiyokuwa katika vita vingine.

Miongoni mwa mambo hayo au yaliyo muhimu ni kuwa jeshi lilikuwa katika joto, njaa, kiu na uchache wa vipando, Ndio maana jeshi hili likaitwa ‘Jeshi gumu.’

Wapokezi wanasema kuwa kikundi fulani cha jeshi la Waislamu walikuwa wakipokezeana kupanda ngamia mmoja; chakula chao kilikuwa ni shayiri yenye wadudu na tende yenye mabuu, Mmoja wao alikuwa anaweza kufyonza tende akipata ladha yake, humpa mwenzake. Kuhusu maji walikuwa wanapochinja ngamia wanakamua mavi yaliyo katika utumbo wake na kurambisha ndimi zao.

Wanafiki walirudi nyuma kwenye vita hivi, Yamekishatangulia maelezo kuwahusu wao, Ama Waumini, ambao walimfuata Mtume(s.a.w.w) katika vita vya Tabuk, Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewashiria kwa kusema:

Hakika Mwenyezi Mungu amekwisha pokea toba ya Mtume na wahajiri na Answar waliomfuata saa ya dhiki.

Ikisemwa kuwa fulani ametubia basi hufahamika kuwa alikuwa na dhambi, kisha akatubia, na ikisemwa kuwa Mwenyezi Mungu amepokea toba hufahamika kuwa amemkubalia toba yake. Lakini vile vile ina maana ya kuelekezwa rehema ya Mwenyezi Mungu na radhi yake kulingana na jumla ilivyo.

Maana ya kukubaliwa toba ndiyo yaliokusudiwa kwa wale watatu. Na maana ya rehema na radhi ndiyo yaliyokusudiwa kwa Mtume na swahaba waliomfuata katika saa ya dhiki. Hii inatokana na hali halisi ilivyo ya isma ya Mtume(s.a.w.w) na utiifu wa waliomfuata katika saa ya dhiki.

Baada ya nyoyo za baadhi yao kukurubia kugeuka.

Waliorudi nyuma walirudi nyuma, na Waumini katika wahajiri na Answari wakamfuata, lakini kikundi katika hawa walipozidiwa na shida na ugumu wa safari walilegea na kukusudia kuachana na Mtume, lakini Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapa uthabiti na kuwalinda. Hivyo wakavumilia na kujitolea.

Kisha akawakubalia toba kutokana na vile walivyoazimia kumwacha Mtume.

Makusudio ya kuwakubalia toba hapa ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwachukulia kuwa hawakudhamiria dhambi, Kwa sababu mwenye kud- hamiria dhambi kisha asilitende, haandikiwi kitu.

Hakika yeye kwao ni Mpole, Mwenye kurehemu.

Kwa vile yeye alijua kwao ukweli katika imani yao na ikhlasi katika nia yao na kwamba dhamira yao ilikuwa ni jambo lililozuka tu na kuondoka bila ya kuacha athari yoyote.

Na pia wale watatu walioachwa nyuma, mpaka ardhi ikawa finyu juu yao pamoja na wasaa wake; na nafsi zao zikadhikika juu yao, na wakayakinisha kuwa hakuna kwa kumkimbia Mwenyezi Mungu isipokuwa kwake.

Wameafikiana wafasiri na wapokezi kwamba watatu hao ni katika waumini wa Kianswari, waliobaki nyuma katika vita vya Tabuk kwa uvivu na kupuuza, sio kwa unafiki na inadi. Hao ni Kaab bin Malik, Mar’wan bin Rabii na Hilal bin Umayya Al-waqif.

Masimulizi ya hao tunamwamchia Twaha Hussein aliyeleta Muhtasari wa yale waliyoyoafikiana wote na yanayofahamika katika Aya, Anasema katika Kitab mir-atul-islam:

“Watatu hawa walikuwa na imani kubwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wenye mapenzi ya ukweli kwake yaliyowafanya wasiongezee kosa la uwongo baada ya lile la kubaki nyuma. Kwa sababu ya ukweli na kuhofia Mwenyezi Mungu kuwafedhehesha waongo, walikiri makosa yao; na Mtume akawasikia na kutangaza kuwa wao ni wakweli, lakini pamoja na hayo hakuwasamehe; akaamrisha waumini wasiwasemeshe. wakawa wametengwa wakiwa mbali kabisa na watu; wakawa katika hali ambayo, jela ilikuwa bora kuliko hali hiyo.

Siku moja Mtume akatuma ujumbe wa kuwaaamuru watengane na wake zao. Hilo sio ajabu, kwa sababu wake zao ni waumini; na amri imetoka kuwa waumini wote watengane nao.

Baada ya kupita siku hamsini wakiwa wamejuta sana, Mwenyezi Mungu aliteremsha Aya kuwatakabalia toba yao. Waumini wote wakalifurahi hilo wakawa wanawapongeza hawa watatu kwa kutakabaliwa toba. Kaab, alifurahi sana; akadhamiria kutoa sadaka mali yake yote, lakini Mtume akamwamuru atoe sehemu tu, Kaab akaahidi kutosema uwongo mpaka kufa.

Kisha akawakubalia toba ili wapate kutubu. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye mwingi wa kukubali toba Mwenye kurehemu.

Utauliza : kuwa dhahiri ya kukubaliwa toba ni kuwa walitubu na wakakubaliwa toba; na dhahiri ya ili wapate kutubu ni kuwa hawajatubia bado; sasa je, kuna wajihi gani?

Swali hilo limejibiwa kwa majibu mengi . Lenye nguvu zaidi ni lile lise- malo kuwa makusudio ya kukukabaliwa toba ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwakubalia toba ili watubu na wasiendelee na dhambi na waseme lau Mwenyezi Mungu atatukubalia toba yetu, basi tutatubu kabisa. Hiyo inafanana na mtu unayempenda akikufanyia uovu nawe unataka kumsamehe, ukamfundisha msamaha ili aombe, nawe umsamehe.

Tumeweka mlango maalum wa toba katika Juz.4 (4: 17).

Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu na kuweni pamoja na wa kweli.

Wakweli ni Mitume na wale ambao Mwenyezi Mungu amewaondolea uchafu na kuwatakasa kabisa kabisa. Kwa maneno mengine, makusudio ya ukweli hapa sio kutosema uwongo tu katika mazungumzo, kwa sababu wako watu wasiosema uwongo lakini haifai kuwafuata katika kila jambo; isipokuwa makusudio ni ukweli katika kauli vitendo na elimu ambavyo vitamwandaa mwenye navyo kuweza kufuatwa.