MUAMALA WA MTUME

BISMILLAHIR-RAHMAANIR-RAHIIM

MUAMALA WA MTUME

Muamala wa Mtume na Jinsi ya kulingania Ukweli Makala hii iliyoko mbele yako inahusiana na tabia njema na muamala wa Mtume Mtukufu (SAW) katika kualika watu kwenye ukweli. Kwa kuitalii kwa makini utatambua kwamba, kinyume na inavyodaiwa na watu wenye chuki na maslahi binafsi ya siri, Uislamu ulienea kutokana na mantiki yake ya nguvu na sio jambo jingine lolote.
Kwa maelezo hayo wale watu wanaodai kwamba Uislamu ulienea na kusambaa kwa ncha ya upanga na mabavu ni waongo wakubwa walio na agenda ya siri kuhusiana na suala hilo. Tunamualika sasa msomi mpenzi kusoma kwa makini yaliyomo humu kwa faida yake mwenyewe na faida ya Waislamu wenzake. Mwenyezi Mungu amemuarifisha Mtume mtukufu (SAW) kwa maneno na ibara maalumu kwa kusema: 'Ewe Mjumbe wa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Kwa yakini Sisi tumekutuma, (tumekuleta uwe) shahidi na mtoaji wa habari nzuri na muonyaji. Na uwe muitaji (wa watu) kwa Mwenyezi Mungu, kwa idhini yake, na (uwe) taa itoayo nuru' (33:45-46).
Kuhusiana na aya hii, moja ya majukumu muhimu ya Mtume Mtukufu wa Uislamu (SAW) lilikuwa ni kuwaita watu kwa Mwenyezi Mungu. Bila shaka jukumu hili zito lilihitajia kuwepo kwa mbinu na njia maalumu ya kufikiwa lengo hilo. Kuna njia tatu muhimu ambazo zimetajwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kufikiwa lengo hilo nazo ni hekima, ushauri mzuri na mawaidha au majadiliano mema: 'Waite (watu) katika njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora' 916:125). Kwa kutegemea ayah ii, njia ya kwanza ya kualika na kuita watu kwa Mwenyezi Mungu ni kutumia hekima na busara, mantiki na hoja zilizo thabiti na madhubuti.
Kutokana na kuwa ujumbe na jukumu kubwa la Mtume Mtukufu ni kuamsha fikra na kufanya hazina ya kifikra kunawiri, njia bora zaidi ya kufikai lengo hilo ni kutumia mbinu ya mantiki, hoja yenye nguvu na iliyo wazi. Hatua ya pili kuhusiana na suala hili ni kutumia nyaadhi na mawaidha mema ambayo kwa kawaida huwa na athari kubwa nay a moja kwa moja kwa watu wanayoyasikiliza mawaidha hayo. Kwa kawaida mawaidha huwa na natija na athari ya moja kwa moja yanapotolewa kwa nia njema na kwa lengo la kuwaongoza walengwa. La sivyo, iwapo mawaidha hayo yatatolewa kwa madhumuni ya kukejeli na kuudunisha upande wa pili au mtoa mawaidha kuhisi kwamba ni mmbora zaidi kuliko upande unaotolewa mawaidha hayo bila shaka mawaidha hayo hayatakuwa na natija iliyokusudiwa. Hali huwa mbaya zaidi na kutoa natija hasi iwapo mawaidha yataandamana na vitendo vya ghasia na utumiaji nguvu ili kufikisha ujumbe unaokusudiwa kwa walengwa.
Hatua ya tatu ya kuita kwa Mwenyezi Mungu ni kutumia mijadala na majadiliano bora na yaliyo na njema njema. Hii ina maana kwamba mjadala kama huo unapasa kufanyika kwa madhumuni ya kutaka kufikia ukweli, uadilifu, hakika na uaminifu ulio mbali na batili. Kwa kutilia maanani kwamba Mwenyezi Mungu aliye juu ndiye aliye na hoja ya mwisho na iliyokamilika, ni wazi kuwa ujumbe aliomtuma nao Mtume wake (SAW) unapasa pia kuwa mkamilifu kihoja ili kuuwezesha umma wake pia unafaike na hoja hoja hizo na upendo wa wazi. Kutokana na kuwa msingi wa ujume wa Mtume (SAW) ilisimama juu ya msingi wa majadiliano mema na hoja timilifu, Mwenyezi Mungu alimpa hoja nyingi ambazo mmara nyingine zilitimia katika sura ya hekima na hoja za kielimu, waadhi na mawaidha na wakati mwingi kupitia mijadala muhimu iliyoandaliwa kwa nia njema. Kuita kwa Mwenyezi Mungu kupitia hekima, mawaidha na mijadala mizuri hutimia kwa njia busara na kuona mbali. Kwa maelezo hayo Mwenyezi Mungu anamuhutubu Mtume wake kwa kusema: 'Sema: Hii ndiyo njia yangu; ninaita (ninalingania) kwa Mwenyezi Mungu kwa ujuzi wa kweli; mimi na (kila) wanaonifuata' (12:108).
Kwa mujibu wa aya hii, kila mtu anayemfuata Mtume (SAW) anapasa kulingania na kuita watu kwa Mwenyezi maneneo na matendo yao mema.
Ushahidi na kualika katika Tauhidi Moja ya njia zinazotumika katika kualika waitu kwenye Tauhidi ni kwa kutumia ushahidi au uthibitisho (hoja). Hata hivyo maana ya hoja iliyotumika katika kitabu kitakatiifu cha Qur'ani ni pana na kubwa zaidi kuliko maana inayotumika katika falsafa kwa kuzingatia madhihirisho na maonyesho ya maana ya neno hilo katika sehemu mbili hizi. Kwa vyovyote vile maana ni moja kwa kuzingatia kuwa humuelimisha mwanadamu na kumuongezea maarifa.

MWISHO