Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

MCHANGO WA HIJA KATIKA SUALA LA UMOJA

0 Voti 00.0 / 5

BISMILLAHIR-RAHMAANIR-RAHIIM

MCHANGO WA HIJA KATIKA SUALA LA UMOJA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa moja ya haja za dharura za kipindi cha sasa ni kutilia maanani umoja na mshikamano wa Kiislamu. Ayatullah Ali Khamenei ameyasema hayo katika hadhara ya wafanyakazi wa sekta ya utamaduni na wasimamizi wa misafara ya hija ya mwaka huu ya Iran. Amesisitiza kuwa ibada ya hija inapaswa kuwa dhihirisho la azma kubwa ya umma wa Kiislamu mkabala wa hatua zozote za kuzusha mfarakano na zinazopinga umoja na maendeleo ya dunia ya Kiislamu.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa hija ni fursa adhimu na yenye thamani kubwa na akaongeza kuwa fursa ya kuwa kando ya msikiti mtakatifu wa Makka, msikiti wa Mtume, haram za Maimamu watoharifu na masahaba wa Mtume inapaswa kutumiwa kwa ajili ya kuzidisha rasilimali ya imani, masuala ya kiroho na unyenyekevu mbele ya Mola Mlezi. Amesema kuwa mahujaji wanapaswa kuwa macho ili fursa hiyo ya thamani isitumike katika kazi zisizokuwa na thamani za kidunia.

Ayatullah Khamenei amesema moja kati ya sifa makhsusi za fursa hiyo adhimu ni kukutana na Waislamu kuoka pembe mbalimbali za za dunia na akaongeza kuwa hujaji wa Kiirani anaweza kuarifisha Uislamu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa mahujaji wengine kwa mwenendo, harakati na tabia za Kiislamu.

Amesema kuwa moja ya tabia na adabu bora za Kiislamu na malezi ya Qur'ani ni kuhudhuria katika Sala za jamaa katika Masjidul Haram na Masjidun Nabii na akaongeza kuwa, Imam Khomeini Mwenyezi Mungu amrehemu ambaye alikuwa mtu aliyepevuka, daima alikuwa akiwahimiza mahujaji wa nyumba ya Mwenyezi Mungu kushiriki katika Sala za jamaa kwa sababu kuhudhuria kwenye Sala hizo ni moja ya vielelezo vya kivitendo vya umoja wa Kiislamu. Ayatullah Khamenei amesema, vikao vya kusoma dua ya Kumail na shughuli ya kujibari na kujiweka mbali na washirikina ni ulinganiaji mkubwa wakati wa ibada ya hija. Amesema kuwa hija ndiyo dhihirisho la tauhidi na kumpekesha Mwenyezi Mungu, kwani ndani ya ibada hiyo kuna kuthibitisha utawala wa Mwenyezi Mungu na kukana mamlaka yasiyokuwa yake Yeye; na hiyo ndiyo ibada ya kujiweka mbali na washirikina.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza juu ya umuhimu wa umoja na mshikamano wa Kiislamu katika kipindi cha sasa na akasema: "Vitendo vya umwagaji damu vinavyofanyika katika baadhi ya nchi za Kiislamu ikiwemo Iraq, Pakistan na katika baadhi ya maeneo hapa nchini vinafanyika kwa lengo la kuzusha hitilafu na mfarakano kati ya Waislamu wa Kishia na Kisuni; kwa msingi huo suala la umoja kati ya Waislamu linapaswa kupewa kipaumbele. Ayatullah Ali Khamenei amesema kuwa watu anaotekeleza mashambulio hayo ya kigaidi na ya kumwaga damu za watu ni vibaraka wa wageni moja kwa moja au kwa njia isiyokuwa ya moja kwa moja.

Ayatullah Khamenei amesema, mahujaji wa nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu al Kaaba hawawezi kupuuza yanayojiri katika ulimwengu wa Kiislamu hususan huko Iraq, Afghanistan, Palestina na sehemu ya Pakistan. Amesisitiza kuwa wakati wa ibada ya hija Waislamu wanapaswa kuonyesha msimamo wao kuhusu mambo yanayokinzana na umoja wa Kiislamu au njama zinazofanywa dhidi bendera ya dunia ya Kiislamu ambayo kwa sasa inapepea nchini Iran.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekosoa dharau na mwenendo mbaya unaofanywa dhidi ya Waislamu wa Kishia na hata kuvunjiwa heshima katika eneo la Baqii au katika Masjidul Haram na Masjidun Nabii. Amesema kuwa hatua kama hizo ni dhidi ya umoja na zinahudumia malengo na matakwa ya Marekani na mashirika ya ujasusi ya nchi za kigeni. Ameongeza kuwa serikali ya Saudi Arabia inapaswa kutekeleza wadhifa wake wa kukabiliana na vitendo kama hivo.

Mwishoni mwa hotuba yake, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewashuruku wasimamizi wa misafara ya hija ya Iran hususan Hujjatul Islam Walmuslimin Muhammadi Reyshahry na Mawaziri wa Wizara ya Utamaduni na Muongozo wa Kiislamu katika miaka ya hivi karibuni na akasema: "Mipango na ratiba za masuala ya kiutamaduni, kisiasa na usimamizi wa misafara ya hija inapaswa kubuniwa kwa mijibu wa mahitaji ya kila zama.

Kabla ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kiongozi wa misafara ya hija ya Iran Hujjatul Islam Walmuslimin Muhammadi Reyshahri alitoa ripoti fupi kuhusu utafiti na hatua zilizochukuliwa katika uwanja wa utamaduni hususan kutoa mafunzo kwa wasimamizi wa hija, wanazuoni na mahujaji na akasema kuwa kaulimbiu ya mwaka huu ya msafara wa hija wa Iran ni "Hija na Kusibiri Imam wa Zama"

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini