MSINGI WA KUIFAHAMU QUR_ANI

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI 

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

UTANGULIZI

MSINGI WA KUFAHAMU QUR_ANI – 1-

Tunamshukuru Mwenyeezi Mungu aliyesema katika Qur-ani yake kuwa “imekujieni – kutoka kwa Mwenyeezi Mungu – nuru (kubwa) na kitabu (kitukufu) kinachobainisha (kila linalohitajiwa)”. Na Rehema Zake na Amani zake zimwendee Mtume wake bwana Muhammad (s.a.w.w) , Mwisho wa Mitume wote na ziwaendee Ahli bayt wake (a.s).

Vitabu vutote tunavyosoma tunaona ndani yake kuwa kila yanayotajwa humo – katika maelezo, fikra na hoja – yanahusika na jambo makhsusi, na kwa mpango wa utungaji makhsusi na kwa kuendeleza hayo anayoyataka huyo mtungaji.

Basi kwa ajili ya kuzoea haya yule anayeanza kuvisoma,akaona kuwa kitakuwa kama hivyo- yamekwisha kupangwa mbali mbali makusudio yake, na yametengwa katika milango mbali mbali, ili aisome kila khabari mahala pake, na anadhani kuwa ataona kila jambo katika mambo yanayohusiana na uhai wa binaadamu limepangwa peke yake kwa mfuatano wake.

Lakini akianza kuisoma Qur-ani kwa kuzingatia ataona kinyume cha alivyodhani. Ataona mambo yaliyohusiana na itikadi, na mambo yaliyohusiana na Akhlaqi (tabia njema), na mambo yaliyohusiana na sharia ya ulinganio wa dini na nasaha, mazingatio na kutoa makosa ya kulaumu na kuhofisha, kupendezesha, ya hoja na dalili ya visa ya mambo yaliyopita na ya ishara zinazopatikana kwa kutazama alivyoumba Mwenyeezi Mungu kwenye mbingu na ardhi, ataviona vyote hivi kunakaririka kubainishwa kwake mara kwa mara na huanzwa- na hurejezwa – utajo wake kwa namna mbali mbali.

Utaona Qur-ani inataja kitu mara – hiyo – imezukia kitu chengine, na wakati mwengine kwa mzukio wa ghafla. Baasi hutokea ikawacha dhamiri nyenginezo au mpango mwengineo.

Ama kugaiwa Qur-ani katika mambo makhsusi, na milango makhsusi, hili halimo kabisa.

Yakitajwa mambo ya Tarikhi, na yakitajwa mambo ya Philosophy, nature study au Logic na mengineyo hayatajwi kwa lafdhi zinazotumiwa humo, na yakitajwa mambo yanayohusika na wanaadamu, siasa au uchumi, kanuni na hukumu, haitaji kwa lafdhi hizo, na ikitaja habari ya ikhlaqi na mwenenzo mzuri hutumia mpango ambao sio uliozoewa kutumiwa.

Basi msomaji Qur-ani ili  aijue ndani yake akiona hivi,- ambavyo sivyo alivyozoea kuona katika vitabu vyengine, hushituka akaona kuwa  kitabu hiki kimekosa mpango mzuri, na maelezo yake yameparaganyika ovyo katika vifungu visivyokuwa na mfuatano.

Basi anayeisoma hii Qur-ani, na hali ya kuwa hataki kuiamini, ila anataka kupinga tu na kuleta matatizo, anapata fursa nzuri ya kutolea pumzi zake hizo, lakini kwa yule ambaye anaisoma hali ya kuwa anaiamini na anainyenyekea, humvuta kabisa hiyo migeuko yake ya mara kwa mara.

Mara akawacha matakwa haya, mara akatulia moyo wake kwa hayo, mara akapata natija nyengine nzuri kwa yale. Hata huwa kama kila Aya imejitenga na mwenziwe kwa namna ya peke yake wenyew, nzuri kabisa kama ile ya mwenziwe, mambo mapya mapya yanamzukia.

Akitaka mtu kukijua kitabu chochote kile kilivyo, lazima kwanza ajue nini makusudio ya kitabu hicho, na nini hasa matakwa yake mahsusi katika kitabu hicho, na ajue vile vile mbinu za mwandiko wake na namna ya lugha yake inavyotumiwa, na ajue undani wake, na vitabu vingi tunavyovisoma hatupati tabu katika kutambua haya.

Lakini katika Qur-ani hatuwezi kuyapata haya kwa upesi tuliouzowea, kwa hiyo mtu akiisoma hii Qur-ani kama anavyovisoma vitabu vyengine hawezi kupata makusudio yake kwa upeo wa jambo lake, na anaustaajabia mpango wake na usimuliaji wake, na hajui kwa nini ikawa hivyo. Juu ya kuwa anapata hikima tukufu kabisa zilizomo katika hii Qur-ani, lakini hapati undani wake, ingawa anapata anayoyapata.

Bali kuna watu wengine wametatizika kwa kusoma hii Qur-ani bila ya ujuzi wa kawaida zake za kuifahamia, wakababaika kwa ile mimeremeto yake inavyomeremeta huku, pasi na kutambua sababu ya kumeremeta kwa aya hizo.

Kwa hiyo inataka mtu ajue hii Qur-ani mpango wake ni vipi kwa mkabala wa vitabu vyengine, vipi imeteremka, na kwa nini ikaja kwa mpango huu, na inasema juu ya habari gani, na yepi hasa mambo muhimu, akiyajua mtu haya kwanza atasalimika na kuteleza njiani, na zitamfunukia njia nyengine za kuifahamu.

MWISHO