HEKIMA YA KUVAA HIJABU

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
HEKIMA NA MALENGO YA KUVAA HIJABU

Katika makala hii tutaelezea baadhi ya hekima na malengo machache tu ya kuvaa hijabu, na katika makala ijayo tutaendelea kuelezea hekima hizo.

 Dada mpendwa wewe uliuliza kwamba una malengo gani mpaka uvae hijabu, na usivae nguo za zinazokwenda na wakati na kujipamba?

JAWABU: Mimi nna uhakika kwamba kama utakaa na kufikiri kwa makini kuhusu suala hilo basi ni lazima utafahamu malengo ya kuvaa hijabu.

Kwa maoni yangu mimi mwanamke yoyote atakaesoma maelezo hayo ataelewa umuhimu na malengo ya kuvaa hijabu.

 1. KUDHIHIRISHA URAFIKI KATIKA KUMPENDA MOLA

Hakuna shaka wewe ushashuhudia baadhi ya watu walio karibu nawe, inawezekana rafiki, au mtu mwengine yoyote mkawa mmekinaiana na akatumia lugha mbali mbali za kukuonesha wewe kwamba anakujali na ni rafiki wake wa karibu sana, ikatokea siku ukawa na shida na ukamfata mmoja wa rafiki zako hao na kumuomba akusaidie kiasi fulani cha pesa, lakini akakujibu kwamba yeye pia anahitaji kusaidiwa pesa na wewe, siku nyengine ukamwambia akuazime kitabu akakujibu kwamba yeye vile vile anataka kusoma, fikiria kila unapokuwa na shida anakuzungusha huku na huku kuonesha kwamba hataki kukusaidia, wewe unaweza kumfikiria nini mtu kama huyo.

Bila ya shaka utasema ni rafiki gani huyu anaenipoza kwa maneno tu?

Sasa fikiria uhusiano ulionao wewe na Mola wako, sisi binaadamu kila siku tunajionesha kwamba ni wapenzi wa Mola wetu, ama mambo tunayoyafanya hayamridhishi.

Basi malengo bora kwako wewe kuhusu masuala ya kuvaa hijabu ni kumtaka mola wako ambae anakupa rizki na kila mahitaji ambayo unayataka, nayeye ni rafiki bora zaidi miongoni mwa rafiki zako, basi kwa nini usikubali na kuyatekeleza yale ambayo ameyaamrisha na anayaridhia? Ili kuonesha kwamba na wewe umeridhika kuwa na urafiki nay eye?

 2.KUMSHUKURU MWENYEENZI MUNGU KWA NEEMA AMBAZO AMEKUJAALIA

 Binaadamu wakati anapokwenda kuwaangalia wagonjwa hospitali atashuhudia vijana wengi wamelala vitandani, na pengine hawawezi kuinuka mpaka kwa kusaidiwa, hawana neema ya uzima, wanaomba Mungu awaondoshee maradhi hayo ili waweze kuinuka kwa miguu yao, hapo mwanaadamu anaweza kufahamu kwamba Mola wake amempa neema ya uzima lakini yeye hazingatii wala hafikirii, uzima na uzuri ni moja ya neema kubwa ambazo Mwenyeenzi Mungu amewakirimu waja wake, basi binaadamu hatuna budi kushukuru neema hizo, basi tuwe tayari kufuata yale ambayo ameyaridhia Allah (s.w) na tusimuasi Mola wetu.

Dada mpendwa wakati unapojiangalia katika kioo zingatia kwa makini neema ambazo amekujaalia Mola wako, angalia macho yako kama ungelikuwa huna macho ungelikuwa na tofauti kiasi gani na wenye macho, basi hivi kweli inaelekea kutokana na neema ambazo ametujaalia Mola wetu tumuasi yeye na tumfuate shaitani?.

Dada mpendwa nakuomba uyaangalie maelezo haya kwa makini, itokee siku unatembea na mwanao njiani  ukiwa na matunda mkononi na uwakute watoto wanacheza, uwagaie matunda hayo watoto hao, na baadae wasikushukuru, wale matunda hayo na yatakayobakia wampige nayo mtoto wako wewe utawafanya nini au utasema nini juu ya watoto hao?

Mwenyeenzi Mungu hana mtoto, lakini binaadamu ni waja wake, basi akitokea mwanamke ambae Mola amempa neema ya uzuri na uzima, na kwa kutumia neema hizo akamkufuru Mola wake kwa kufanya yale asioyaamrisha Mola mwanamke huyo atakuwa na tofauti gani na watoto hao?

Ndio, kushukuru neema ambazo ametujaalia Mola mfano wa uzuri na uzima, ni sababu muhimu ambayo itakufanya uwelewe lengo na umuhimu wa kuvaa hijabu.

 3.KUMPOKONYA SILAHA SHETANI

 Adui mkubwa wa mwanaadamu ni shetani, naye ameapa kwamba ni lazima ampotoshe binaadamu. Na ndio maana utaona sehemu zenye kitega uchumi na pesa nyingi watu wengi hughilibiwa na shetani, kwa sababu sehemu kama hizo shetani ndipo anapopata nafasi ya kuharibu amani ya mwanaadamu, sasa ikawa sisi ndio sababu inayomfanya afanikiwe na tusiyakubali yale ambayo Mola ametuamrisha na tukamfata shetani.

Hakuna shaka kwamba kutokuvaa hijabu kwa wanawake na kujipamba ndio sababu kubwa inayomfanya mwanamme aghilibiwe na shetani, kuna wanume wangapi ambao walikuwa ni wacha Mungu lakini baada ya shetani kuwaghilibu kwa kupitia wanawake wamekuwa ni wenye kumuasi Mola wao, na baada ya kuwa walikuwa ni watu wa peponi , wamejipalilia moto wenyewe na wamekuwa ni watu wa motoni.

 Mtume wetu Muhammad (s.a.w) anasema “Kuwaangalia wanawake kwa matamanio ni sawa na mshale wa sumu unaotoka kwa bilisi.

 Yaani ikiwa muwindaji hatoweza kuwinda paa, na kwa kutumia mshale akampiga paa huyo mguuni na kumfanya asiweze kutembea, baadae akaharakia kwenda kumchukua paa huyo.

 Basi kwa kuzingatia mfano huo shetani nae anapotaka kumghilibu mwanamke au mwanamme kwanza humtia wasi wasi mpaka amuone tayari keshamughilibu, ndipo humdhoofisha amani yake na kidogo kidogo humvuatia upande wake.

 Basi kutokana na maelezo hayo tumeelewa kwamba moja katika madhumuni ya kuvaa hijabu ni kwamba kila mwanamke muislamu awe na itikadi ya kupigana na shetani ili asiweze kumughilibu, na asikubali kutumiwa na shetani ili kumkufuru Mola wake.

MWISHO