Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

MAYAHUDI WAIPINGA QUR_ANI TAKATIFU

0 Voti 00.0 / 5

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI

MAYAHUDI HAWAISADIKI QUR_ANI TAKATIFU2

MAYAHUDI HAWAISADIKI QUR_ANI TAKATIFU WALA HAWAMSADIKI MTUME (S.A.W.W).

Katika makala iliyopita tulielezea vipi Mayahudi walimkanusha Mtume Muhammad (s.a.w.w) na kitabu chake, katika makala hii basi tutaendelea na mada yetu hiyo na kutupilia macho mitihani ambayo Mwenyeezi Mungu anawapa waja wake.

Basi Mwenyeezi mungu anawajibu Mayahudi kwa kusema hivi:-

وَاتَّبَعُواْ مَا تَتْلُواْ الشَّيَاطِينُ عَلـٰي مُلْكِ سُلَيْمَانَ وَمَا كَفَرَ سُلَيْمَانُ وَلَـكِنَّ الشَّيْاطِينَ كَفَرُواْ يُعَلِّمُونَ النَّاسَ السِّحْرَ وَمَا اُنزِلَ عَلـٰي الْمَلَكَيْنِ بِبَابِلَ هَارُوتَ وَمَارُوتَ وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ اَحَدٍ حَتَّي يَقُولاَ إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ فَلاَ تَكْفُرْ فَيَتَعَلَّمُونَ مِنْهُمَا مَا يُفَرِّقُونَ بِهِ بَيْنَ الْمَرْءِ وَزَوْجِهِ وَمَا هُم بِضَآرِّينَ بِهِ مِنْ اَحَدٍ إِلاَّ بِإِذْنِ اللهِ وَيَتَعَلَّمُونَ مَا يَضُرُّهُمْ وَلاَ يَنفَعُهُمْ وَلَقَدْ عَلِمُواْ لَمَنِ اشْتَرَاهُ مَا لَهُ فِى الآخِرَةِ مِنْ خَلاَقٍ وَلَبِئْسَ مَا شَرَوْاْ بِهِ اَنفُسَهُمْ لَوْ كَانُواْ يَعْلَمُونَ[1]

Tarjuma:

Na wakafuata yale waliyo zua mashet'ani kuuzulia ufalme wa Su leiman. Na wala Suleiman hakukufuru, bali mashet'ani ndio walio kufuru, wakiwafundisha watu uchawi, na yaliyo teremshwa kwa Malaika wawili, Haaruta na Maaruta katika Baabil. Wala hao hawakumfundisha yeyote mpaka wamwambie: Hakika sisi ni mtihani; basi usikufuru. Wakajifunza kwa hao wawili yale ya kumfarikisha mtu na mkewe. Wala hawawezi kumdhuru mtu ila kwa kutaka Mwenyezi Mungu. Na wanajifunza yatayo wadhuru wala hayawanufaishi. Na hakika wanajua kwamba aliye khiari haya hatakuwa na fungu lolote katika Akhera. Na hakika ni kiovu mno walicho jiuzia nafsi zao laiti wangelijua.

Maelezo kuhusiana na Aya ya 102 Suratul baqara

Suleimani aliyetajwa hapa ni Nabii suleimani. Mayahudi wanamwitakidi nabii Suleimani kuwa ni Mfalme aliyepata ufalme wa uchawi, si Mtume,basi na hawa wachawi wa kiislamu humnasibisha nabii Suleimani hizo elimu zao za uchawi, basi Mwenyeezi Mungu anamkanushia haya, na Aya hii inaonesha wazi kuwa:-

a) uchawi ni amali ya ukafiri.

b)kuwa mchawi hawezi kumdhuru mtu ila kwa idhini ya Mwenyeezi Mungu.

c)kuwa mchawi anadhurika mwenyewe kwa uchawi wake.

Na anataja hapa Mwenyeezi Mungu kuwa nyuma huko kabisa katika zama za ufalme mkubwa na ustaarabu mkubwa wa Mababiloni, (wakaazi wa Iraqi wa zamani kabisa). Mwenyeezi Mungu aliwaletea Malaika wawili – Harut wa Marut – kwa sura ya kibinaadamu, na wakiwaambia watu kuwa wao wanajua uchawi wa kila namna – wa kuweka na kuondoa – wa kufarikisha na wakuungamanisha na wa mengine, lakini wakiwaambia vile vile hapana ruhusa kujifundisha, atakayekubali tumfundishe atakuwa kafiri; huu ni mtihani mnaofanyiwa na Mwenyeezi Mungu. Kama mlivyofanyiwa mtihani wa kupewa matamanio ya nafsi na mtihani wa kushindana na iblisi na kama hii, basi huu mtihani. Yazuilieni matamanio yenu msijifundishe. Lakini wapi! Walijifundisha.

Basi huu mchawi ulioko mpaka sasa ni pepesi za uchawi huo. Mwenyeezi Mungu anawafanyia viumbe vyake mitihani namna kwa namna ili wadhihiri wema na wajulikane wabaya.[2]

وَلَنَبْلُوَنَّكُمْ بِشَيْءٍ مِّنَ الْخَوفْ وَالْجُوعِ وَنَقْصٍ مِّنَ الاَمَوَالِ وَالانفُسِ وَالثَّمَرَاتِ وَبَشِّرِ الصَّابِرِينَ[3]

Hapana shaka tutakujaribuni kwa chembe ya khofu, na njaa, na upungufu wa mali na watu na matunda. Na wabashirie wanao subiri.

فَلَمَّا فَصَلَ طَالُوتُ بِالْجُنُودِ قَالَ إِنَّ اللّهَ مُبْتَلِيكُم بِنَهَرٍ فَمَن شَرِبَ مِنْهُ فَلَيْسَ مِنِّى وَمَن لَّمْ يَطْعَمْهُ فَإِنَّهُ مِنِّى إِلاَّ مَنِ اغْتَرَفَ غُرْفَةً بِيَدِهِ فَشَرِبُواْ مِنْهُ إِلاَّ قَلِيلاً مِّنْهُمْ فَلَمَّا جَاوَزَهُ هُوَ وَالَّذِينَ آمَنُواْ مَعَهُ قَالُواْ لاَ طَاقَةَ لَنَا الْيَوْمَ بِجَالُوتَ وَجُنودِهِ قَالَ الَّذِينَ يَظُنُّونَ اَنَّهُم مُّلاَقُو اللهِ كَم مِّن فِئَةٍ قَلِيلَةٍ غَلَبَتْ فِئَةً كَثِيرَةً بِإِذْنِ اللهِ وَاللّهُ مَعَ الصَّابِرِينَ[4]

Basi Taluti alipo ondoka na majeshi alisema: Mwenyezi Mungu atakujaribuni kwa mto. Atakaye kunywa humo si pamoja nami, na asiye kunywa atakuwa pamoja nami: ila atakaye teka kiasi ya kitanga cha mkono wake. Lakini walikunywa humo isipo kuwa wachache tu miongoni mwao. Alipo vuka mto yeye na wale walio amini pamoja naye, walisema: Leo hatumwezi Jaluti (Goliati) na majeshi yake. Wakasema wale wenye yakini ya kukutana na Mwenyezi Mungu: Makundi mangapi madogo yameshinda makundi makubwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu yu pamoja na wenye kusubiri.

 Maelezo kuhusiana na Aya ya 249 suratul Baqarah:

Kutii (taa) ni kitu kikubwa kabisa katika kutengenea mambo ya watu, watu wasiokuwa na taa ya kutii mambo yao huharibikiwa tu, na hapa anatoka mfalme huyu, taluti na jeshi kubwa wala halijui utiifu wake, basi Mwenyeezi Mungu ndiyo akamwambia awafanyie mtihani huu wa kutokunywa mpaka kukata kiu, wasiotii asiwachukue kwenda huko kwenye midani ya vita wasije wakakhalifu watakayoambiwa.

وَمَا اَصَابَكُمْ يَوْمَ الْتَقَي الْجَمْعَانِ فَبِإِذْنِ اللهِ وَلِيَعْلَمَ الْمُؤْمِنِينَ[5]

Na yaliyo kusibuni siku yalipo pambana majeshi mawili yalikuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na ili awajue Waumini.

يَا اَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ لَيَبْلُوَنَّكُمُ اللّهُ بِشَيْءٍ مِّنَ الصَّيْدِ تَنَالُهُ اَيْدِيكُمْ وَرِمَاحُكُمْ لِيَعْلَمَ اللّهُ مَن يَخَافُهُ بِالْغَيْبِ فَمَنِ اعْتَدَي بَعْدَ ذٰلِكَ فَلَهُ عَذَابٌ اَلِيمٌ[6]

Enyi mlio amini! Mwenyezi Mungu atakujaribuni kidogo kwa wanyama wa kuwinda inayo wafikia mikono yenu na mikuki yenu, ili Mwenyezi Mungu amjue nani anaye mkhofu kwa ghaibu. Basi atakaye ruka mipaka baada ya hayo atapata adhabu kali.

Maelezo kuhusiana na Aya ya 94 ya Suratul-Maidah.

Mwenyeezi Mungu huwafanyia mtihani waja Wake kwa lolote lile atakalo aonyeshe walikuwa waja hawa wametii, wamefuata waliyoambiwa, au hawakutii.

Nyuma huko alilifanyia mtihani jeshi alilokuwamo Nabii Daudi kuwa litashikwa na kiu kali kabisa, na litakutana na mto wa maji mengi mazuri lakini halina ruhusa kunywa na kukata kiu katika mto huo, ruhusa aliyopewa kila mmoja katika hao ni kuteka maji funda tu katika mkono wake anywe lile lile tu basi, likimkata kiu lisimkate, basi wengi katika hao walikhalifu amri hiyo wakayapapia kweli kweli.

Basi Nabii Muhammad katika mwaka wa saba Alhijra alipotoka na jeshi lake la watu elfu wa khamsumia wanakwenda kufanya umra, Mwenyeezi Mungu aliwaharamishia kuwinda kinyama chochote cha barani, na akawaambia kuwa atawafanyia mtihani wa kuwawekea chekwa wanyama hao katika kila njia watakayopita. Watakuwa chekwa kila upande na wengi kabisa wa kuweza kwa urahisi kupigwa kwa mikuki bali na kukamatwa kwa mkono pia. Lakini wakaambiwa hawana ruhusa kuwagusa.

Basi waliwanyia haya wakayakuta hayo waliyoambiwa, lakini wote walivuka salama, hakuna asiyekhalifu hata mmoja.

 

[1] Suratul baqara aya ya 102

[2] Tazama Aya ya 155na 249 katika surat baqara, 166 Al-imrani, 94Almaida na nyenginezo

[3] Suratul baqara aya ya 155

[4] Suratul baqara aya ya 249

[5] Surat Al-imrani Aya ya 166

[6] Surat Maidah Aya ya 94

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini