WADHIFA WA WANADINI WAISLAMU

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI
KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
WADHIFA WA WANADINI WAISLAMU
Wanadini wote mahasusi Waislamu inawawajibikia kukabiliana na vile vitengo vya wahakiki ambavyo malengo yao ni kuiharibu dini au kuitawala jamii.

Kwa upande mwengine Waislamu ni lazima wawe na elimu ya kutosha katika kuwapatia wahakiki majibu ya masula yao, majibu ambayo yatamtoa muhakiki katika shaka na kumridhisha kiakili na kiakida, hatimae kuelewa na kutambua haki na uhakika wa dini.

Ni wadhifa wa kila Muislamu kupokea suala, tata, au mapingaji yoyote yale yanayotolewa na wahakiki bila ya kudharau nadharia au mitazamo ya wanahakiki, kutafiti tata na masuala ambayo yanatolewa na wahakiki na kuyapatia ufumbuzi wake.

Ni wadhifa wa Waislamu kupokea tata za wahakiki kwa nia moja, na malengo mamoja ya kuzitafutia ufumbuzi wa kielimu tata hizo, na sio kuzitoa maana tata au masuala mbali mbali yanayoulizwa na wahakiki, kwa sababu kufanya hivyo hakutapelekea faida yoyote katika jamii na dini ya Kiislamu, kwani malengo makuu ya dini ya Kiislamu na Waislamu kwa ujumla ni kuitangaza dini hiyo tukufu ili kuenea katika pande zote za dunia, kwani dini hiyo ndio dini ya haki inayohitajiwa na kila mwanaadamu katika kuendeleza na kupata saada njema ya maisha yake ya duniani na Akhera.

10. Wahakiki wa dini katika hatua ya mwanzo ni lazima kufahamu na kutambua uhakika wa dini kupitia udhahiri wa matini za kidini, na katika hatua ya pili baada ya kufahamu kwa uzuri dhahiri ya dini basi anaweza akafanya jitihada katika kufahamu batini ya dini, lakini ni lazima azingatie kuwa analazimika kutumia dhahiri ya dini kwa ajili ya kufahamu batini ya dini, na sio kutoka nje ya dini, kwa sababu kile anachokifahamu katika undani wa dini ni ule ufahamu wa yale aliyoyakubali katika udhahiri wa dini. Kwa hiyo uhakiki wa kweli hauwezi kukubalika kwa kuhakiki katika njia za logical Politivism, kutafsiri kwa kutumia njia yaTaawiyl ( kutafsiri kwa njia ya dhahiri shahiri), au kuhakiki kwa njia ya Hermenutics. Katika paragrafu hii tutazielezea njia hizo kwa undani zaidi, kwani inawezekana baadhi ya watu wasielewe makusudio ya njia hizo ni nini.

 a) Logical Politivism: Ni kitu ambacho kinaweza kufanyiwa majaribio na tajriba. Kwa maana nyengine tunaweza kusema hivi:-

Ni sentensi, mada,au tungo yoyote ile ya sheria ya kidini, jamii, serikali, ni lazima iwe na uwezo wa kuiingiza katika maabara na kutafutiwa utafiti na majaribio ambayo yataweza kuonyesha kwa kina uhakika wake, kwa mfano kama inadaiwa kuwa siku ya kiama kuna Pepo kwa watu wema, na kuna jahanamu (moto) kwa watu wabaya, basi ni lazima pafanyiwe utafiti utakaoonyesha ukweli wa Pepo na Jahanamu hiyo, na ikiwa kutokana na uhakiki au utafiti utakaofanywa hakukupatikana uhakika wala ufumbuzi wowote utakaothibitisha kuwepo kwa vitu hivyo, basi madai hayo ya kuwa kuna Pepo na moto hayatakubalika.

b)Taawili (tafsiri ya dhahiri shahiri) ni tafsiri yenye kumurika maneno kupitia darubini ya udhahiri wa mambo, na maana dhahiri za maneno zilivyo.

Taawili ni kufasiri na kutafuta maana za maneno kupitia darubini ya nguvu za kiakili zenye uwezo wa kujua maana dhahiri na kuilenga ile maana halisi iliyojificha ndani ya maneno. Kwa hiyo kwa msingi huo tunaweza kusema kuwa tafsiri ya dhahiri shahiri ni tafsiri ya wazi yenye kuonekana dhahiri shahiri bila ya mashaka yoyote.

Taawili ni tafsiri mficho ambayo maana yake ni lazima itafutwe huko mafichoni iliko, tafsiri mficho ni yenye kuyasaka na kuyatafuta maneno yaliyo mafichoni, (yaani maneno yaliyo batini, yaani maneno yaliyojificha ndani ya ibara, au sentensi). Kwa mfano:-

Mwenye kufasiri Qur-ani kwa njia ya dhahiri anatumia akili yake kwa kiwango kidogo tu, wala hatakiwi kutafakari kwa kiwango kikubwa, ama kwa yule mfasiri ambaye anaifasiri Qur-ani kwa ubatini wake, basi mfasiri huyo atakuwa anatumia akili na kiwango kikubwa cha kutafakari. Natuzingatie mfano huu wa Aya unaoonyesha tafsiri ya dhahiri na tafsiri ya batini, Allah (s.w) anasema:-

إِنَّ الَّذِينَ يُبَايِعُونَكَ إِنَّمَا يُبَايِعُونَ اللهَ يَدُ اللهِ فَوْقَ اَيْدِيهِمْ فَمَن نَّكَثَ فَإِنَّمَا يَنكُثُ عَلـٰي نَفْسِهِ وَمَنْ اَوْفَي بِمَا عَاهَدَ عَلَيْهُ اللهَ فَسَيُؤْتِيهِ اَجْراً عَظِيماً[1]

Bila ya shaka wanao fungamana nawe, kwa hakika wanafungamana na Mwenyezi Mungu. Mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao. Basi avunjaye ahadi hizi anavunja kwa kuidhuru nafsi yake; na anaye tekeleza aliyo muahadi Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu atamlipa ujira mkubwa.

Na katika Aya nyenginea anasema:-

وَقَالَتِ الْيَهُودُ يَدُ اللهِ مَغْلُولَةٌ غُلَّتْ اَيْدِيهِمْ وَلُعِنُواْ بِمَا قَالُواْ بَلْ يَدَاهُ مَبْسُوطَتَانِ يُنفِقُ كَيْفَ يَشَاءُ وَلَيَزِيدَنَّ كَثِيراً مِّنْهُم مَّا اُنزِلَ إِلَيْكَ مِن رَّبِّكَ طُغْيَاناً وَكُفْراً وَاَلْقَيْنَا بَيْنَهُمُ الْعَدَاوَةَ وَالْبَغْضَاء إِلَي يَوْمِ الْقِيَامَةِ كُلَّمَا اَوْقَدُواْ نَاراً لِّلْحَرْبِ اَطْفَاَهَا اللّهُ وَيَسْعَوْنَ فِى الاَرْضِ فَسَاداً وَاللّهُ لاَ يُحِبُّ الْمُفْسِدِينَ[2]

Na Mayahudi walisema: Mkono wa Mwenyezi Mungu umefumba. Mikono yao ndiyo iliyo fumba, na wamelaaniwa kwa sababu ya waliyo yasema. Bali mikono yake iwazi. Hutoa apendavyo. Kwa yakini yaliyo teremshwa kwako kutoka kwa Mola wako Mlezi yatawazidisha wengi katika wao uasi na kufuru. Na Sisi tumewatilia uadui na chuki baina yao mpaka Siku ya Kiyama. Kila mara wanapo washa moto wa vita, Mwenyezi Mungu anauzima. Na wanajitahidi kuleta uharibifu katika ardhi. Na Mwenyezi Mungu hawapendi waharibifu.

 Maelezo kuhusiana na Aya:

Katika Aya hiyo unaonekana moto wa Mayahudi unavyowaka na kuzimika mara kwa mara, na mwisho utazimika kabisa, Mwenyeezi Mungu kasema Mayahudi hawatapata ukubwa ulimwenguni ila kwa sharti mbili:-

a) Washikamane na mwenendo mzuri aliyouweka Mwenyeezi Mungu, au

b) Wawe wanapata msaada kwa dola nyenginezo; kama tunavyoona hivi sasa lakini wenyewe Mayahudi tu peke yao hawataweza kuwa chochote maishani mwao.

c) Mayahudi eti wanamtia mori Mwenyeezi Mungu azidi kuwapa kwa kusema:-

“Siku hizi mkono wa Mwenyeezi Mungu hautoi sana”.

Mwenye kufasiri aya hizo kutokana na udhahiri wake atafasiri kuwa Mwenyeezi Mungu ana mikono, kutokana na neno “yad” lililokuja katika Aya hizo, likiwa na maana ya mkono, basi inawezekana kwa mfasiri atakayefasiri kwa udhahiri wake akasema kuwa mkono wa Mwenyeezi Mungu uko juu ya mikono yao, hali ya kwamba katika Qur-ani takatifu kuna Aya zinazopinga kuwa Allah (s.w) ana mkono, kwa sababu Yeye Allah (s.w) anasema kuwa Yeye hajafanana na kitu chochote pale aliposema:-

فَاطِرُ السَّمَاوَاتِ وَالاَرْضِ جَعَلَ لَكُم مِّنْ اَنفُسِكُمْ اَزْوَاجاً وَمِنَ الاَنْعَامِ اَزْوَاجاً يَذْرَؤُكُمْ فِيهِ لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ وَهُوَ السَّمِيعُ البَصِيرُ[3]

Yeye ndiye Muumba mbingu na ardhi, amekujaalieni mke na mume katika nafsi zenu, na katika nyama hoa dume na jike, anakuzidishieni namna hii. Hapana kitu kama mfano wake. Naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona.

Na katika Aya nyengine anasema:-

قُلْ هُوَ اللهُ اَحَدٌ . اللهُ الصَّمَدُ . َمْ يَلِدْ وَلَمْ يُولَدْ . وَلَمْ يَكُن لَّهُ كُفُواً اَحَد[4].

Sema: Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee. Mwenyezi Mungu Mkusudiwa

Hakuzaa wala hakuzaliwa. Wala hana anaye fanana naye hata mmoja.

Kwa upande mwengine yule mfasiri atakayeifasiri Qur-ani kwa undani wake atapinga kauli hiyo (ya kuwa Mwenyeezi Mungu ana mkono), kwa kuzingatia na kupekua Aya mbali mbali zinazothibitisha kuwa Mwenyeezi Mungu hafananizwi na kitu basi hatuwezi kumfananiza Mwenyeezi Mungu na binaadamu au kitu chochote kwa uthibitisho wa Aya hizo tulizibainisha hapo juu, na Aya nyengine nyingi zilizomo ndani ya Qur-ani.

  Basi kutokana na Aya hizo tumefahamu kuwa kwa wale watu wanaofasiri qur-ani kwa kutegemea udhahiri wake tu hawawezi kuifahamu Qur-ani kwa maana zake za ndani, na kwa wale wanaofasiri kwa kuzingatia maana za ndani za Qur-ani hutumia Aya nyengine kama ni kisaidizi tu kinachosaidia kufahamu maana zilizo mafichoni.

[1] Surat Al-Fat-h Aya ya 10.


[2] Surat Al-Maidah Aya ya 64.


[3] Surat Ash-Shuura Aya ya 11


[4] Surat Ikhlas Aya 1-4