Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

VISIMAMO VYA SIKU YA KIAMA

0 Voti 00.0 / 5

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI
KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

VISIMAMO VYA SIKU YA KIYAMA

IDADI YA VISIMAMO VYA SIKU YA KIYAMA NA KIPINDI CHA ZAMA ZAKE.

* Walimwengu watapitia hatua gani itakapofika siku ya Kiyama?
* Hatua hizo zitapitwa namna gani?.
Mazungumzo au maelezo yanayohusiana na visimamo vya siku ya Kiama maelezo ambayo yanamtoa mwanaadamu katika pumbuazi na kughafilika alikonako, mwanaadamu anaposikia na kutambua maelezo yanayohusiana na visimamo hivyo huingiwa na hofu fulani katika moyo wake, hofu hiyo huwaingia wale ambao watatahayari baada ya kudhihirika uhakika huo, Qur-ani kariym inabainisha
visimamo hivyo kwa kusema (fazaa kubwa), basi fazaa hiyo itawakuwa wale ambao walioishi duniani kwa kutenda maovu na kumuasi Mola Mtakatifu, ama kwa wale ambao ni waja wema waliotenda amali njema zinazomridhisha Allah (s.w) kwa hakika hawatakuwa na hofu yoyote ya visimamo hivyo vya siku ya Kiyama, watu hao ni wale waliokuwa na nafsi zilizotakasika, basi ni watu wa aina hiyo ndio watakaoweza kupita kwa urahisi katika visimamo hivyo, waumini hao wenye imani na taquwa walijikinga na kuwa mbali na aina yoyote ile ya shirki au kumshirikisha Mwenyeezi Mungu, hawakuwa ni wenyekufanya ria wala hawakuwa wanafiki, nyoyo zao zilijaa nuru ya imani ya Mwenyeezi Mungu, na waliwafuata na kuwatii Mitume na Ahlulbayt (a.s) pamoja na viongozi waadhamu walio watukufu na Masalihi wa dini yake Allah (s.w), basi Mwenyeezi Mungu atawaondolea watu hao hofu, na ghamu katika nyoyo zao. Kwa kuzingatia Aya takatifu za Qur-ani tunaweza kuvigawa visimamo vya siku ya Kiyama katika hatua tatu zifuatazo:-

  *Hatua ya kwanza:

Kukusanywa kwa vitu na viumbe vyote duniani. Allah (s.w) anasema:

وَتَرَكْنَا بَعْضَهُمْ يَوْمَئِذٍ يَمُوجُ فِى بَعْضٍ وَنُفِخَ فِى الصُّورِ فَجَمَعْنَاهُمْ جَمْعاً[1]

Na siku hiyo tutawaacha wakisongana wao kwa wao. Na baragumu litapulizwa, na wote watakusanywa pamoja.   

 * Hatua ya pili:

Viumbe kufanya harakati kuelekea katika vituo vya hesabu na kuulizwa masuala. Mwenyeezi Mungu Mtukufu anasema:-

وَجَاءتْ كُلُّ نَفْسٍ مَّعَهَا سَائِقٌ وَشَهِيدٌ[2]

Na kila nafsi itakuja na pamoja nayo mchungaji na shahidi.

* Hatua ya tatu.

Kufanya harakati kuelekea katika uwanja wa malipo na jazaa. Allah (s.w) anasema:-

وَسِيقَ الَّذِينَ كَفَرُوا إِلَي جَهَنَّمَ زُمَراً حَتَّي إِذَا جَاؤُوهَا فُتِحَتْ اَبْوَابُهَا وَقَالَ لَهُمْ خَزَنَتُهَا اَلَمْ يَاْتِكُمْ رُسُلٌ مِّنكُمْ يَتْلُونَ عَلَيْكُمْ آيَاتِ رَبِّكُمْ وَيُنذِرُونَكُمْ لِقَاء يَوْمِكُمْ هَذَا قَالُوا بَلَي وَلَكِنْ حَقَّتْ كَلِمَةُ الْعَذَابِ عَلـٰي الْكَافِرِينَ[3]

Na waliokufuru watapelekwa katika jahanamu makundi- makundi mpaka watakapoifikia itafunguliwa milango yake; na walinzi wake watawaambia: “Jee! hawakukujieni Mitume miongoni mwenu wakikusomeeni Aya za Mola wenu na kukuonyeni makutano ya siku yenu hii?”. watasema: Kwa nini? (wametujia)! Lakini limethubuti neno la adhabu juu ya wale waliowakanusha. (Nao ndio sisi).”

Maelezo kuhusiana na Aya:

Basi natutengenee kabla ya kusimangwa kwa Aya hii na nyenginezo. Aliyeonya, Hana Lawama Akitesa, na Mwenyeezi Mungu ametuonya kweli kweli.
Na kuhusiana na watu waumini na wacha Mungu tunasoma hivi:

وَسِيقَ الَّذِينَ اتَّقَوْا رَبَّهُمْ إِلَي الْجَنَّةِ زُمَراً حَتَّي إِذَا جَاؤُوهَا وَفُتِحَتْ اَبْوَابُهَا وَقَالَ لَهُمْ خَزَنَتُهَا سَلاَمٌ عَلَيْكُمْ طِبْتُمْ فَادْخُلُوهَا خَالِدِينَ[4]
Na waliomcha Mola wao watapelekwa peponi makundi- makundi; mpaka watakapofikia (wataingia tu na wataikuta) milango yake imekwishafunguliwa; na walinzi wake watawaambia: “Amani juu yenu, furahini,
ingieni humu make milele.”
Hatua hizo tatu zina vituo vilivyoenea tabu na mashaka, na watu watasimama katika vitua hivyo kwa muda mrefu mrefu sana, katika qur-ani tunasoma:-

يُدَبِّرُ الاَمْرَ مِنَ السَّمَاءِ إِلَي الاَرْضِ ثُمَّ يَعْرُجُ إِلَيْهِ فِى يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ اَلْفَ سَنَةٍ مِّمَّا تَعُدُّونَ[5]

Anapitisha mambo yote yalio baina mbingu na ardhi, kisha yanapanda kwake kwa siku ambayo kipimo chake ni miaka elfu kwa mnavyo hisabu nyinyi.
Watu waovu na waliomuasi Mwenyeezi Mungu kwa kutenda maovu siku ya Kiyama watakuwa katika hali mbaya iliyo na tabu, kiasi ya kwamba kusubiri kwa muda mrefu katika vituo hivyo kutawafanya wao wajisikie wako adhabubi kwa muda usiopungua miaka elfu hamsini. kama tunavyosoma katika Aya hii takatifu:-

تَعْرُجُ الْمَلاَئِكَةُ وَالرُّوحُ إِلَيْهِ فِى يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ خَمْسِينَ اَلْفَ سَنَةٍ[6]

Malaika na Roho hupanda kwendea kwake katika siku ambayo kadiri yake ni miaka khamsini elfu! Riwaya ya Imamu sadiqi (a.s) inasisitiza maana hiyo, Yeye amesema:-

"الا فحاسبوا انفسکم قبل ان تحاسبوا فان فی القیامة خمسین موقفا کل موقف مثل الف سنة مما تعدون[7] ثم تلا هذه الایة " فِى يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ خَمْسِينَ اَلْفَ سَنَةٍ

Zingatieni! fuatilieni hesabu zenu kabla hazijafuatiliwa hesabu zenu, kwa hakika siku ya Kiyama kuna visimamo hamsini, kila kisimamo kimoja ni mfano wa miaka elfu ya ile miaka mnayohesabu nyinyi, Baadae
Imamu akasoma Aya hiyo,katika siku ambayo kadiri yake ni miaka khamsini elfu! Ama siku ya Kiyama Waumini hawataona tabu yoyote isipokuwa wepesi, (na muda wote huo) kwa Waumini na wacha Mungu ni kipindi kifupi tu, katika Qur-ani tunasoma:-

فَاَمَّا مَنْ اُوتِيَ كِتَابَهُ بِيَمِينِهِ. فَسَوْفَ يُحَاسَبُ حِسَاباً يَسِيرا[8]

Ama atakaye pewa daftari lake kwa mkono wa kulia, Basi huyo atahisabiwa hisabu nyepesi.

Maelezo kuhusiana na Aya ya 7.

Siku ya hesabu kila mtu atapewa daftari lake kama ilivyotaja Aya ya kumi ya Surat Takwiyr, basi kuna watakaopewa kwa upande wa kulia; na hao ndio watu wema, na kuna watakaopewa kwa upande wa kushoto na kwa nyuma ya migongo yao, na hao ndio watu waovu.

Maelezo kuhusiana na Aya ya 8

Watu, kuna watakaohisabiwa pasi na kuhojiwa, kwa kila walilolitenda, bali watatajiwa mema yao na maovu yao, kisha watasamehewa yale maovu walipwe kwa mema, Hao ndio watu wema, na hiyo ndiyo “Hisabu Nyepesi.” kuna na wengine watahisabiwa pamoja na kuhojiwa kwa kila walilolitenda moja moja, hao ndio watu waovu, na hiyo ndiyo hisabu nzito. Kulingana na kiwango cha imani na matendo ya wanaadamu, Mwenyeezi Mungu huwalipa waja wake malipo yao, kwa wale ambao imani zao zilikuwa khalisi na safi basi Mwenyeezi Mungu atawapa watu hao ujira mkubwa na kuwapa mafanikio mema waliyoyapata kupitia amali zao hizo, basi watu hao watabakia katika utulivu wa milele. Basi Mitume ya Mwenyeezi Mungu na Ahlulbayt (a.s) hawatakuwa katika mabalaa wala adhabu zozote zile.

فَوَقَاهُمُ اللهُ شَرَّ ذٰلِكَ الْيَوْمِ وَلَقَّاهُمْ نَضْرَةً وَسُرُوراً[9]

Basi Mwenyezi Mungu atawalinda na shari ya siku hiyo, na atawakutanisha na raha na furaha.

[1] Surat Alkahf Aya ya 99

[2] Surat Qaf Aya ya 21

[3] Surat Zumar Aya ya 71

[4] Surat Zumar Aya ya 73

[5] Surat As-sajdah Aya ya 5.

[6] Surat Al-Maarij Aya ya 4

[7] Kitabu Kafi, juzuu ya ,8

[8] Surat Inshiqaaq Aya ya 7-8.

[9] Surat Al-Insan Aya ya11

 


 

 

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini