TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 20317
Pakua: 2430


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 20317 / Pakua: 2430
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

وَإِذْ يَتَحَاجُّونَ فِي النَّارِ فَيَقُولُ الضُّعَفَاءُ لِلَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا إِنَّا كُنَّا لَكُمْ تَبَعًا فَهَلْ أَنتُم مُّغْنُونَ عَنَّا نَصِيبًا مِّنَ النَّارِ ﴿٤٧﴾

47. Na watapohojiana huko Motoni, wanyonge watawaambia wale waliotakabari: Hakika sisi tulikuwa wafuasi wenu, basi je, mtatuondolea sehemu ya huu Moto?

قَالَ الَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا إِنَّا كُلٌّ فِيهَا إِنَّ اللَّـهَ قَدْ حَكَمَ بَيْنَ الْعِبَادِ ﴿٤٨﴾

48. Watasema waliotakabari: Hakika sote sisi tumo humo humo! Hakika Mwenyezi Mungu ameshahukumu baina ya waja!

وَقَالَ الَّذِينَ فِي النَّارِ لِخَزَنَةِ جَهَنَّمَ ادْعُوا رَبَّكُمْ يُخَفِّفْ عَنَّا يَوْمًا مِّنَ الْعَذَابِ ﴿٤٩﴾

49. Na walio Motoni watawaambia walinzi wa Jahannamu: Mwombeni Mola wenu atupunguzie siku moja ya adhabu.

قَالُوا أَوَلَمْ تَكُ تَأْتِيكُمْ رُسُلُكُم بِالْبَيِّنَاتِ قَالُوا بَلَىٰ قَالُوا فَادْعُوا وَمَا دُعَاءُ الْكَافِرِينَ إِلَّا فِي ضَلَالٍ ﴿٥٠﴾

50. Watasema: Je! Hawakuwa wakiwafikia Mitume wenu kwa hoja zilio wazi? Watasema: Kwani? Watasema: Basi ombeni! Na maombi ya makafiri hayawi ila ni kupotea bure.

إِنَّا لَنَنصُرُ رُسُلَنَا وَالَّذِينَ آمَنُوا فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَيَوْمَ يَقُومُ الْأَشْهَادُ ﴿٥١﴾

51. Hakika tunawanusuru Mitume wetu na wale ambao wameamini katika uhai wa duniani na siku wataposimama mashahidi.

يَوْمَ لَا يَنفَعُ الظَّالِمِينَ مَعْذِرَتُهُمْ وَلَهُمُ اللَّعْنَةُ وَلَهُمْ سُوءُ الدَّارِ ﴿٥٢﴾

52. Siku ambayo hautawafaa madhalimu udhuru wao, nao watapata laana, na watapata makazi mabaya.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَى الْهُدَىٰ وَأَوْرَثْنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ الْكِتَابَ ﴿٥٣﴾

53. Na kwa hakika tulimpa Musa uwongofu, na tukawarithisha Wana wa Israili Kitabu.

هُدًى وَذِكْرَىٰ لِأُولِي الْأَلْبَابِ ﴿٥٤﴾

54. Ni Uwongofu na Ukumbusho kwa wenye akili.

فَاصْبِرْ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ وَاسْتَغْفِرْ لِذَنبِكَ وَسَبِّحْ بِحَمْدِ رَبِّكَ بِالْعَشِيِّ وَالْإِبْكَارِ ﴿٥٥﴾

55. Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli. Na, omba maghufira kwa dhambi zako na umsabihi Mola wako kwa kumhimidi jioni na asubuhi.

WANAHOJIANA MOTONI

Aya 47 – 55

MAANA

Aya hizi zimekwishatangulia kimaneno na kimaana. Kwa hiyo tutazifasiri kwa kupitia tu na tutaashiria Aya zilizotangulia zilipo:Na watapohojiana huko Motoni, wanyonge – yaani wafuasi –watawaambia wale waliotakabari: - yaani waliofuatwa -Hakika sisi tulikuwa wafuasi wenu, basi je, mtatuondolea sehemu ya huu Moto?

Mtu huko Akhera atakuwa pamoja na aliyempenda duniani na akamtii. Mwenye kuwapenda waongofu hapa duniani, atakuwa pamoja nao katika neema ya Pepo na atawashukuru kwa kupata uwongofu kwenye njia ya amani na uwokofu.

Lakini yule atakayewafuata mataghuti, basi atawalaani kesho na atawaambia nyinyi ndio sababu ya uovu wangu, sasa je, mtanipunguzia adhabu ninayoipata.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (14:21).

Watasema waliotakabari: Hakika sote sisi tumo humo humo! Hakika Mwenyezi Mungu amekwishahukumu baina ya waja!

Waliofuatwa watawajibu wale waliowasikiza na kuwatii: Leo hapana mjadala wala maneno. Mwenyezi Mungu amekwishaihukumu kila nafsi kwa kila ilichokichuma, na amekwishatuhukumia sisi na wale waliotufuata kwenda motoni

Na walio Motoni watawaambia walinzi wa Jahannamu: Mwombeni Mola wenu atupunguzie siku moja ya adhabu.

Wanafikiria adhabu ya Jahannam ni kama jela ya duniani, wafungwa wanavyopata mapumziko nje ya jela. Hapo wataomba wafanyiwe motoni kama wanavyofanyiwa katika jela ya duniani.

Watasema: Je! Hawakuwa wakiwafikia Mitume wenu kwa hoja zilio wazi? Watasema: Kwani? Watasema: Basi ombeni! Na maombi ya makafiri hayawi ila ni kupotea bure.

Walinzi watawajibu kuwa Mwenyezi Mungu amekwishamaliza udhuru kwenu, kupitia mitume yake; kama mlivyokiri wenyewe. Kwa hiyo hakuna lawama ikiwa hatajibu maombi yenu ila mjilaumu wenyewe tu. Umetangulia mfano wake katika Juzuu hii tuliyo nayo (39:71) na kwa upana zaidi kwenye Juz. 7 (7:50-53).

Hakika tunawanusuru Mitume wetu na wale ambao wameamini katika uhai wa duniani na siku wataposimama mashahidi.

Siku ya mashahidi ni Siku ya Kiyama ambapo wakasofu watatolewa ushahidi na malaika maulama wanaofikisha na hata viungo vya mkosaji:

حَتَّىٰ إِذَا مَا جَاءُوهَا شَهِدَ عَلَيْهِمْ سَمْعُهُمْ وَأَبْصَارُهُمْ وَجُلُودُهُم بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٢٠﴾

“Hata watakapoufikia Moto yatawashuhudia masikio yao, na macho yao na ngozi zao kwa waliyokuwa wakiyatenda.” (41:20).

Aya hii inafahamisha, kwa uwazi, kuwa Mwenyezi Mungu anawanusuru mitume na waumini wenye ikhlasi kuwa washindi duniani na Akhera. Ushindi wa Akhera uko wazi, lakini ushindi wa duniani una sura mbali mbali.

Unaweza ukawa ni nguvu ya kumshinda adui au kuenea itikadi na misingi au hata kuinuka jina na kuwa na shani daima. Kuna baadhi ya mashahidi, makaburi yao yamekuwa kama Al-Ka’aba, yanatembelewa na mamilioni. Historia ni shahidi wa hayo.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22: 38-41) kifungu cha ‘Mwenyezi Mungu huwakinga walioamini.’

Siku ambayo hautawafaa madhalimu udhuru wao, nao watapata laana, na watapata makazi mabaya, pasipokuwa na wa kuwakinga wala udhuru utakaowafaa waasi. Kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekata nyudhuru zote. Na mwema ni yule asiyetaka udhuru kwa kufanya matendo mema.

Na kwa hakika tulimpa Musa uwongofu, na tukawarithisha Wana wa Israili Kitabu, ni Uwongofu na Ukumbusho kwa wenye akili.

Makusudio ya uwongofu hapa ni miujiza inayofahamisha utume wa Musa(a.s ) na yale aliyopewa wahyi, ya halali na haramu. Makusudio ya Kitabu ni Tawrat ya kweli.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja kuwa anawanusuru mitume na waumini, hapa anaashiria Musa na wale waliokuwa na ikhlasi katika wana wa Israil. Kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwanusuru na Firauni na watu wake.

Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w. w ) , akiamrishwa kuvumilia, kama walivyovumilia mitume ulul-azm na kuashiria ahadi Yake aliyoieleza katika kauli yake:

هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُونَ ﴿٣٣﴾

“Yeye ndiye aliyemtuma Mtume wake kwa uongofu na dini ya haki ili ipate kushinda dini zote, ijapokwa washirikina wamechukia.” Juz. 10 (9:33).

Ahadi ya Mwenyezi Mungu haiwezi kuachwa.

Na omba maghufira kwa dhambi zako.

Amri ya kuomba msamaha wa dhambi haimaanishi kuwa kuna dhambi. Mtume alimuomba Mola wake ahukumu kwa haki, ingawaje anajua kuwa hahukumu isipokuwa haki:

قَالَ رَبِّ احْكُم بِالْحَقِّ ﴿١١٢﴾

“Akasema: Mola wangu! Hukumu kwa haki.” Juz. 17 (21:112).

Unaweza kuuliza : Kuna faida gani basi ya kufanya istighfari ya dhambi?Jibu : Hakuna isipokuwa ibada; kama amri ya tahalili, takbira na tasbih, kama alivyosema:

Na umsabihi Mola wako kwa kumhimidi jioni na asubuhi.

Neno jioni limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu ibkar lenye maana ya kuanzia kupinduka jua hadi usiku. Na asubuhi kutoka Ashiyy lenye maana ya kuanzia Alfajiri hadi mchana.

Zaidi ya hayo ni kuwa kuamrishwa Mtume kuomba msamaha na hali hana dhambi, kunafahamisha kuwa kutubia wenye dhambi ni bora zaidi.

Aina hii ya maneno inaitwa kuuashiria mlengwa. Kwa sababu anayesikiliza atatambua kuwa hukumu inayothibiti kwa anayeatamkiwa inathibiti kwa aliyenyamaziwa vile vile, kwa kiasi cha kusikia tu.

MWENYEZI MUNGU NA WAISRAIL

Katika Juz. 1 (2:40-46) tulisema kuwa maana ya neno Israil ni Abdallah (mtumishi wa Mwenyezi Mungu), kwa kutegemea wafasiri, akiwemo Tabariy, Razi na mwenye Majmaul-bayan.

Lakini tulipoanza Juzuu hii tuliyo nayo, tukaona kuwa kauli hii inahitaji uthibitisho na kwamba haikufaa kutegemea kauli za wafasiri, au angalau tungelitegemeza kauli kwa msemaji (kusema kuwa Fulani ndiye aliyesema hivi); kama inavyotakikana katika mantiki ya elimu. Lakini kuwategemea wajuzi hasa waliotangulia, lilikuwa na linaendelea kuwa ni tatizo la waaandishi na watunzi na hata wapokezi wa Hadith.

Basi nikawa natafuta kitabu Talmud, lakini sikupata, badala yake nikapata kitabu: Treasure provision in the rules of the Talmud na Kamusi ya Kitabu (Bible Dictionary), nikavinunua. Waliochangia kutengeneza kamusi hii ni wasomi wa kikiristo 28, wakiwemo makasisi 17, na wengine ni madokta, mashemasi na waalimu. Humo kuna nukuu hii: "Israil: Maana ya neno hili ni yule anayepigana jihadi na Mwenyezi Mungu au aliyepigana miereka na Mwenyezi Mungu. Hilo ni jina la Yakobo alilopewa na Mungu aliyepigana naye hadi alfajiri" (Biblia Mwanzo 32:28).

Kwa hiyo maana ya Israil ni yule anayepigana miereka na Mwenyezi Mungu, kwa nukuu ya Tawrat. Kuna tofauti kubwa baina ya mja au mtu- mishi na mpiganaji. Kwa sababu mpiganaji anapigana na yule aliyefanana naye, lakini mtumishi anakuwa mnyonge.

Hii inatubainikia kuwa Tawrat ya sasa sio ile aliyoiashiria Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliposema: 'Na tukawarithisha wana wa Israil Kitabu ni uwongofu na ukumbusho' kwa sababu Tawrat ya sasa ni ya matamanio na upofu, kwa vile inasema kuwa Ya'qub alipigana na Mungu mpaka Alfajiri, Lut alilala na mabinti zake mpaka akazaa nao na Daud naye aliwapora wake za watu na kuwaua waume zao.

Watafiti wamekongamana kuwa Tawrat iliyoko sasa, iliandikwa baada ya Musa kwa muda mrefu. Tazama Qamusul-kitabul-muqaddasa (kamusi ya kitabu kitakatifu ya kiarabu), ukurasa 763 na 1120 chapa ya Al-injilya ya Beirut 1964. Vile vile Al-asfarul-muqaddasa,' (Vitabu vitakatifu) cha Abdul-wahid Wafi, ukurasa 16 chapa ya kwanza 1964.

Vile vile imetubainikia kuwa wana wa Israil wa mwanzo waliorithishwa Kitabu, wako mbali sana kinasabu na kushabihiana na dola ya Israil, kambi mpya ya ukoloni mashariki ya kati.

Jarida la A-Majalla la Misr la mwezi January 1970, limechapisha makala yenye kurasa 20, kwa anuani ya 'Tawrat ya Mayahudi' ya mwandishi Hussein Dhul-fiqar Sabri.

Ndani ya makala hiyo kuna mahali anamnukuu Mzayuni Stehr, kwamba Mungu wa Israil, kama inavyoona fikra ya Kiyahudi, ana mfungano na historia ya wana wa israil. Ikiondoka Israil, basi dalili za kufahamisha kuweko Mungu nazo zitakuwa zimeondoka. Kwa hiyo inamlazimu kila myahudi apamabane na dhati hiyo isiyojulikana - yaani Mwenyezi Mungu - mpaka alfajiri, kama alivyofanya Ya'qub, iwe mapambano haya ni ya kushindwa au kushinda.

Vile vile mwandishi amemnukuu mzayuni, Popper, kwamba maana yaliyo katika akili za mayahudi wengi ni kuwa Ya'qub alikuwa na nguvu kuliko Mwenyezi Mungu.

Mwisho, baada ya utafiti wa kina wa mwandishi huyu, akatoka na natija aliyoipata kutoka Tawrat na vitabu vingine vya kiyahudi na pia kutoka katika kauli za wanafikra wa kizayuni, kwamba kiini cha itikadi ya kiza- yuni ni kuweko Israil na kupambana na tishio lolote, hata kama chimbuko la tishio hilo ni Mungu. Na kwamba Tawrat ya sasa ni uchambuzi tu wa uyahudi na kupingana na Mwenyezi Mungu. Yeye yuko pamoja nao na wakati huohuo yuko dhidi yao, katika Tawrat yao Mungu amechanganyika: hatakikani, lakini pia ni mwenye huruma.

Huu ndio Uzayuni. Itikadi yake ni kuwa kuna watu wana nguvu zaidi ya Mwenyezi Mungu, na kwamba kuweko Mungu kunategemea kuweko Israil. Ikiondoka Israil Mungu naye ameondoka.

Ndio maana Uzayuni ukajiunga na ukoloni wa kimataifa, dhidi ya mataifa mengine, dini na ubinadamu kwa ujumla. Matokeo ya muungano huu yakawa ni kupatikana Israil, ndani ya ardhi ya Palestina. Lakini Alhamdulillah, roho ya uadui dhidi ya ukoloni na uzayuni imeenea kwenye miji yote ya kiarabu. Dalili kubwa ya hilo ni mapambano ya Wapalestina na kukubaliana waarabu kuisaidia Palestina. Kwa uweza wa Mwenyezi Mungu, matunda yatapatikana, kama si leo ni kesho.

إِنَّ الَّذِينَ يُجَادِلُونَ فِي آيَاتِ اللَّـهِ بِغَيْرِ سُلْطَانٍ أَتَاهُمْ إِن فِي صُدُورِهِمْ إِلَّا كِبْرٌ مَّا هُم بِبَالِغِيهِ فَاسْتَعِذْ بِاللَّـهِ إِنَّهُ هُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ ﴿٥٦﴾

56. Hakika wale ambao wanabishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya dalili yoyote iliyowafika, hawana vifuani mwao ila kutaka ukubwa tu, na wala hawaufikii. Basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu; hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

لَخَلْقُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَكْبَرُ مِنْ خَلْقِ النَّاسِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٧﴾

57. Hakika umbo la mbingu na ardhi ni kubwa zaidi kuliko umbo la watu. Lakini watu wengi hawajui.

وَمَا يَسْتَوِي الْأَعْمَىٰ وَالْبَصِيرُ وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ وَلَا الْمُسِيءُ قَلِيلًا مَّا تَتَذَكَّرُونَ ﴿٥٨﴾

58. Na kipofu na mwenye kuona hawawi sawa; na walioamini na watendao mema hawawi sawa na muovu. Ni machache mnayoyakumbuka.

إِنَّ السَّاعَةَ لَآتِيَةٌ لَّا رَيْبَ فِيهَا وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يُؤْمِنُونَ ﴿٥٩﴾

59. Hakika Saa, itafika, haina shaka, lakini watu wengi hawaamini.

وَقَالَ رَبُّكُمُ ادْعُونِي أَسْتَجِبْ لَكُمْ إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِي سَيَدْخُلُونَ جَهَنَّمَ دَاخِرِينَ ﴿٦٠﴾

60. Na Mola wenu amesema: Niombeni nitawaitikia. Kwa hakika wale ambao wanajivuna kufanya ibada yangu wataingia Jahannamu wadhalilike.

اللَّـهُ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ اللَّيْلَ لِتَسْكُنُوا فِيهِ وَالنَّهَارَ مُبْصِرًا إِنَّ اللَّـهَ لَذُو فَضْلٍ عَلَى النَّاسِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَشْكُرُونَ ﴿٦١﴾

61. Mwenyezi Mungu ambaye amewafanyia usiku ili mpate kutulia humo, na mchana wa kuonea. Hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mwenye fadhila juu ya watu, lakini watu wengi hawashukuru.

ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ فَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ ﴿٦٢﴾

62. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu, Muumba wa kila kitu. Hapana mungu ila Yeye; basi mnageuzwa wapi?

كَذَٰلِكَ يُؤْفَكُ الَّذِينَ كَانُوا بِآيَاتِ اللَّـهِ يَجْحَدُونَ ﴿٦٣﴾

63. Hivyo ndivyo walivyogeuzwa wale ambao walikuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu.

KUUMBA MBINGU NA ARDHI

Aya 56 – 63

MAANA

Katika Hakika wale ambao wanabishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya dalili yoyote iliyowafika, hawana vifuani mwao ila kutaka ukubwa tu, na wala hawaufikii.

Makusudio ya wanaobishana hapa ni wapenda anasa. Kwani wao wanapinga kitu kikiwa hakikubaliani na ukubwa wao. Ushahidi wa hilo ni kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘ila kutaka ukubwa tu’ Yaani kwa sababu ya kiburi chao na kujikuza, hawaikubali haki na wanabishana. Ingelikwa bora kama wangelitubia na kukubali makosa.

Basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu na kiburi na mwisho mbaya.

Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona, kiburi chao wana- choking’ang’ania kwa sababu ya jaha na utajiri wao. Katika Nhajul-bal- agha, imesemwa: “Jikingeni kwa Mwenyezi Mungu na majivuno kama mnavyojikinga na majanga.”

Hakika umbo la mbingu na ardhi ni kubwa zaidi kuliko umbo la watu. Lakini watu wengi hawajui.

Kila elimu inavyoendelea, ndio maana ya Qur’ani nayo yanavyozidi kwa nguvu kufunguka kwenye akili. Wataalamu wa zamani walisema: Mtu ndiye kiumbe wa ajabu ardhini na katika anga za juu na kwamba ardhi ndio kituo cha ulimwengu. Kisha ikaja elektroni na ala nyingine za elimu ya kisasa, ili ziseme:

Hapana! Mtu sio kiumbe wa ajabu wala ardhi zio kituo cha ulimwengu. Kwani ulimwengu una mamailio ya vituo na kila kituo kina mamlioni ya nyota, na kwamba hakuna yoyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayejua au anayeweza kujua idadi ya vituo hivyo au idadi ya nyota na vinginevyo vilviyomo kwenye kila kituo; na ardhi katika ulimwengu ni kama chembe tu.

Hapa ndio tunapata tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Hakika umbo la mbingu na ardhi ni kubwa zaidi kuliko umbo la watu.’ Ndio! Lakini ndani ya binadamu kuna ulimwengu wa ajabu, jinsi alivyo, hakika yake, mapendeleo yake hisia zake na matamanio yake.

Na kipofu na mwenye kuona hawawi sawa; na walioamini na watendao mema hawawi sawa na muovu. Ni machache mnayoyakumbuka.

Tofuti ni kubwa sana baina mjuzi na mjinga baina ya mwema na mfisadi na baina mwenye kufanya mazuri na mwenye kufanya maovu. Hapana! Hawawi sawa mbele ya Mwenyezi Mungu wala mbele ya watu wenye insafu mwamko. Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:50), Juz. 13 (13:16) na Juz. 22 (35:19).

Hakika Saa ya Kiyamaitafika, haina shaka, na itatupelekea kusimama mbele za mwenye uwezo aliye mjuzi, batilil zitaondoka, uhakika utathibiti na visababu vyote vitakatika.

Lakini watu wengi hawaamini kwamba wao watafufuliwa siku itakayokuwa kubwa na wataulizwa waliyokuwa wakiyafanya.

Na Mola wenu amesema: Niombeni nitawaitikia.

Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa maana yake ni niabuduni nitawalipa. Wametoa dalili kuwa Qur’an inatumia neno dua kwa maana ya ibada kwa Aya ya isemayo:

إِن يَدْعُونَ مِن دُونِهِ إِلَّا إِنَاثًا ﴿١١٧﴾

“Huwamuombi asiyekuwa yeye isipokuwa (masanamu) ya kike.” Juz. 5 (4:117).

Sisi tuko pamoja na wanaosema kauli hii; hasa katika Aya hii, ambapo mfumo wa maneno unarudia kwenye maana hii, pale aliposema moja kwa moja:

Kwa hakika wale ambao wanajivuna kufanya ibada yangu wataingia Jahannamu wadhalilike.

Kwa hiyo kusema kwake: ‘ambao wanajivuna na ibada yangu,’ ni tafsiri na ubanifu wa kauli yake: ‘niombeni.’ Kwa vyovyote iwavyo, ni kuwa Uislamu ni dini ya matendo sio dini ya maneno. Na Mwenyezi Mungu humruzuku mwenye kufanya juhudi na akawa na subira:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَرْضَ ذَلُولًا ﴿١٥﴾

“Yeye ndiye aliyeifanya ardhi mororo kwa ajili yenu” (67:15).

Tumezungumzia kuhusu dua (mombi) katika Juz. 2 (2: 186).

Mwenyezi Mungu ambaye amewafanyia usiku ili mpate kutulia humo, na mchana wa kuonea. Hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mwenye fadhila juu ya watu, lakini watu wengi hawashukuru.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 11 (10:67).

Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu, Muumba wa kila kitu. Hapana mungu ila Yeye; basi mnageuzwa wapi?

Vipi mnageuzwa kumtii Mwenyezi Mungu na kumwabudu na hali Yeye peke yake ndiye Muumba na Mwenye kuruzuku? Makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Amewafanyia, Mwenye fadhila na Muumba wa kila kitu,’ ni kubainisha kuwa Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekusanya sifa zote za uungu za ukamilifu na kwamba sifa hizo zote ziko wazi kwa mwenye macho na akili nzuri, lakini watu wengi wameghafilika na yale wanayotakiwa kuyafanya na yanayolengwa kwao.

Hivyo ndivyo walivyogeuzwa wale ambao walikuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu.

Kila mwenye kughafilika na kupuuza dalili zinazofahamisha ukuu wa Mwenyezi Mungu, lazima awe anaachana na ibada ya Mwenyezi Mungu na twaa yake. Kwa sababu watu ni maadui wa yale wasiyoyajua.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

اللَّـهُ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَرْضَ قَرَارًا وَالسَّمَاءَ بِنَاءً وَصَوَّرَكُمْ فَأَحْسَنَ صُوَرَكُمْ وَرَزَقَكُم مِّنَ الطَّيِّبَاتِ ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ فَتَبَارَكَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٦٤﴾

64. Ni Mwenyezi Mungu aliyewafanyia ardhi kuwa ni pahala pa kukaa, na mbingu kuwa jengo. Na akawatia sura, na akazifanya nzuri sura zenu, na akawaruzuku vizuri. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu. Basi amekuwa na baraka Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu wote.

هُوَ الْحَيُّ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ فَادْعُوهُ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ الْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٦٥﴾

65. Yeye yuko hai - hapana mungu isipokuwa Yeye. Basi muabuduni Yeye mkimsafia Dini Yeye. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

قُلْ إِنِّي نُهِيتُ أَنْ أَعْبُدَ الَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ لَمَّا جَاءَنِيَ الْبَيِّنَاتُ مِن رَّبِّي وَأُمِرْتُ أَنْ أُسْلِمَ لِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٦٦﴾

66. Sema: Hakika nimekatazwa kuwaabudu wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu, ziliponijia hoja zilizo wazi kutokana na Mola wangu. Na nimeamrishwa nisilimu kwa Mola wa walimwengu wote.

هُوَ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ مِنْ عَلَقَةٍ ثُمَّ يُخْرِجُكُمْ طِفْلًا ثُمَّ لِتَبْلُغُوا أَشُدَّكُمْ ثُمَّ لِتَكُونُوا شُيُوخًا وَمِنكُم مَّن يُتَوَفَّىٰ مِن قَبْلُ وَلِتَبْلُغُوا أَجَلًا مُّسَمًّى وَلَعَلَّكُمْ تَعْقِلُونَ ﴿٦٧﴾

67. Yeye ndiye ambaye amewaumba kwa udongo, kisha kwa tone, kisha kwa pande la damu, kisha akawatoa katika hali ya mtoto mchanga, kisha mpate kufikia utu uzima, kisha mpate kuwa wazee. Na kati yenu wapo wanaokufa kabla, na ili mfikie muda uliokwishawekwa, na ili mpate kutia akili.

هُوَ الَّذِي يُحْيِي وَيُمِيتُ فَإِذَا قَضَىٰ أَمْرًا فَإِنَّمَا يَقُولُ لَهُ كُن فَيَكُونُ ﴿٦٨﴾

Yeye ndiye ambaye anahuisha na anafisha. Akihukumu jambo liwe, basi huliambia: Kuwa! Likawa.

AMEWATIA SURA NA AKAZIFANYA NZURI

Aya 64 – 68

MAANA

Ni Mwenyezi Mungu aliyewafanyia ardhi kuwa ni pahala pa kukaa, na mbingu kuwa jengo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t), hapa, ameisifu ardhi kuwa ni mahali pa kukaa, mahali pengine ameipa sifa ya tandiko na pengine kitanda. Maana yote hayo ni mamoja. Na ameisifu mbingu hapa kuwa ni jengo na mahali pengine kuwa ni sakafu na yenye buruji na yenye mpangilio.

Makusudio ya sakafu ni kufananisha, kwa sababu inaonekana kama hivyo kwenye macho. Kundi la wafasiri limesema kuwa makusudio ya buruji ni nyota na mpangilio. ni njia. Ama makusudio ya jengo ni kuwa aliiumba kwa mpangilio mzuri na akaipamba kwa pambo la nyota; kama ilivyo katika Juz. 23 (37:6).

Na akawatia sura, na akazifanya nzuri sura zenu, na akawaruzuku vizuri. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu. Basi amekuwa na baraka Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu wote.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemuumba mtu, akalifanya vizuri umbile lake, kimo na viungo, kwa mpangilio wa hali ya juu; kuongezea ubainifu, utambuzi, na mengineyo, kama vile utambuzi n.k. Hali hii ya uwiano wa ajabu baina ya mtu na ulimwengu; kiasi ambacho muundo wake umekuja kwa namna ambayo mtu anaweza kutumia nishati na heri zote zilizo ulimwenguni kulingana na haja na masilahi yake, huenda ndiyo inayomfanya mtu awe kiumbe wa aina yake.

Lau kusingelikuwa na dalili yoyote inayofahamisha kuweko Mwenyezi Mungu, isipokuwa kiumbe huyu wa ajabu (mtu), basi ingelitosha. Hapa ndio tunapokuta tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na katika ardhi zimo Ishara na katika nafsi zenu, je hamuoni?” (51:20-21). Tumeyazungumzia hayo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 15 (17:70).

Yeye yuko hai - hapana mungu isipo kuwa Yeye. Basi muabuduni Yeye mkimsafia Dini Yeye. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

Yeye yuko hai kwa sababu Ndiye anayetoa uhai na ni Mmoja wa peke Yake kwa sababu ni Mungu. Kwani uungu unapelekea kuwa wa pekee mmoja tu. Maana ya kumsafia dini ni kumwamini na kumwelekea Yeye tu peke Yake, katika kauli zote na vitendo vyote. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:29) na Aya ya 14 ya sura hii tuliyo nayo.

Baada ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kusema kuwa Yeye ndiye aliyewatia sura, anaashiria kuwa inatakikana mtu amshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema yake ya kuumba na kuruzuku.

Sema: Hakika nimekatazwa kuwaabudu wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu, ziliponijia hoja zilizo wazi kutokana kwa Mola wangu. Na nimeamrishwa nisilimu kwa Mola wa walimwengu wote.

Huu ni mfumo mzuri wa kujadili na kudadisi. Washirikina walipomwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : abudu masanamu tunayoyaabudu, ndipo Mwenyezi Mungu akamwambia Mtume wake waambie kuwa vipi niabudu masanamu na hali Mwenyezi Mungu amenikataza kuyaabudu na akaniamuru kusalimu amri Kwake Yeye peke yake.

Pia amenifahamisha dalili za kutosha kwamba mnavyoviabudu hav- istahiki kuabudiwa kabisa, kwa sababu ni mawe tu, yasiyodhuru wala kunufaisha. Umetangulia mfano wake katika Aya 41 ya sura hii tuliyo nayo.

Yeye ndiye ambaye amewaumba kwa udongo, kisha kwa tone, kisha kwa pande la damu, kisha akawatoa katika hali ya mtoto mchanga, kisha mpate kufikilia utu uzima, kisha mpate kuwa wazee. Na kati yenu wapo wanaokufa kabla, na ili mfikie muda uliokwishawekwa, na ili mpate kutia akili

Umetangulia mfano wake katika Juz. 14 (16:70), Juz. 17 (22:70), Juz. 18 (23:14) na Juz. 22 (35:11).

MWANAFALSAFA RUSSEL NA MUDA ULIOWEKWA

Yeye ndiye ambaye anahuisha na anafisha. Akihukumu jambo liwe, basi huliambia: Kuwa! Likawa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye anayeleta mauti na uhai katika vitu vya asili ya maumbile na Ndiye aliyeleta maumbile yote, zikiwemo sayari zake, kwa neno ‘kuwa’ kutokana na kutokuweko chochote. Sio kutokana na ukungu; wala mengineyo. Kama muulizaji atauliza: Ni nani basi aliyemuumba Mwenyezi Mungu? Tutajibu: maana ya neno Allah (Mwenyezi Mungu) ni kuwa Yeye ni muumba asiyeumbwa na kwamba dhati yake inapelekea kupatikana wala haihitaji mwenye kuipatisha.

Akisema mara ya pili kuwa hayo ni madai tu yanyohitaji uthibitisho, na kwamba huo ukungu huuhitaji mwenye kuupatisha, tutamjibu hivi: Maisha haya na nidhamu hii haiwezi kufasiriwa na ukungu wala na kitu chochote kisichokuwa na uhai wala utambuzi. Kwa sababu asiyenacho haiwezi kuitoa.

Kwa hiyo basi haitabakia kwa mwenye akili kufasiri uhai na nidhamu katika maumbile isipokuwa kukubali kuweko Mwenye uwezo, Mpangiliaji aliyemuumba wa kila kitu na asiyehitajia chochote. Makadirio yoyote yasiyokuwa haya hayakubaliki kiakili.

Na mwenye kupinga basi na alete lililo bora kuliko hili na amwachie mtu kufuata atakalo nasi tutakuwa pamoja naye.

Kwa ufupi ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemumba mtu katika umbile zuri, akamgurisha kutoka hali moja hadi nyingine mpaka kufikia muda wake uliowekwa. Ikiwa hatujamuona muumba basi tumeona athari na dalili zinazofahamisha kuwa Yeye ni Mkuu katika uumbaji Wake.

Kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘na ili mfikie muda uliokwishawekwa, na ili mpate kufahamu.’ Tunakumbuka tukio lililomtokea mwanafalsafa mkubwa Bretrand Russel, alipokuwa na umri wa miaka 76.

Mnamo mwaka 1948, alisafiri kwa ndege kutoka Oslow hadi London. Ndege ilipokuwa inakurubia ufukwe wa Norway, mhudumu mmoja wa ndege alimuuliza kama ni lazima avute sigara? Alikuwa amekaa kwenye viti vya mbele, akamjibu: “Nisipovuta nitakufa.”

Basi akamuonyesha viti vya nyuma aende akakae huko, ataruhusiwa kuvuta sigara. Mara tu baada ya kukaa, ndege ikaanguka baharini, watu waliokuwa viti vya mbele wakafariki na waliokuwa vya nyuma wakapona.

Hatuwezi kupata tafsiri ya hili ispokuwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘na ili mfikie muda uliokwishawekwa, na ili mpate kufahamu.’ Mwenyezi Mungu ametanabisha kufika muda uliowekwa na kufahamu, ili awaeleze walahidi wanaofasiri tukio kama hili na mfano wake kuwa ni sadfa.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ يُجَادِلُونَ فِي آيَاتِ اللَّـهِ أَنَّىٰ يُصْرَفُونَ ﴿٦٩﴾

69. Je, Huwaoni wale ambao wanabishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu wanageuziwa wapi?

الَّذِينَ كَذَّبُوا بِالْكِتَابِ وَبِمَا أَرْسَلْنَا بِهِ رُسُلَنَا فَسَوْفَ يَعْلَمُونَ ﴿٧٠﴾

70. Ambao wamekadhibisha Kitabu na yale tuliyowatuma nayo Mitume wetu. Basi watakuja jua.

إِذِ الْأَغْلَالُ فِي أَعْنَاقِهِمْ وَالسَّلَاسِلُ يُسْحَبُونَ ﴿٧١﴾

71. Zitakapokuwa pingu shingoni mwao na minyororo, huku wanabururwa.

فِي الْحَمِيمِ ثُمَّ فِي النَّارِ يُسْجَرُونَ ﴿٧٢﴾

72. Katika maji ya moto, kisha wataunguzwa Motoni.

ثُمَّ قِيلَ لَهُمْ أَيْنَ مَا كُنتُمْ تُشْرِكُونَ ﴿٧٣﴾

73. Tena wataambiwa: Wako wapi mliokuwa mkiwashirikisha.

مِن دُونِ اللَّـهِ قَالُوا ضَلُّوا عَنَّا بَل لَّمْ نَكُن نَّدْعُو مِن قَبْلُ شَيْئًا كَذَٰلِكَ يُضِلُّ اللَّـهُ الْكَافِرِينَ ﴿٧٤﴾

74. Badala ya Mwenyezi Mungu Watasema: Wametupotea, bali tangu zamani hatukuwa tukiomba kitu! Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu huwapoteza makafiri.

ذَٰلِكُم بِمَا كُنتُمْ تَفْرَحُونَ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَبِمَا كُنتُمْ تَمْرَحُونَ ﴿٧٥﴾

75. Haya ni kwa sababu mlikuwa mkifurahi katika ardhi pasipo haki, na kwa sababu mlikuwa mkijishaua.

ادْخُلُوا أَبْوَابَ جَهَنَّمَ خَالِدِينَ فِيهَا فَبِئْسَ مَثْوَى الْمُتَكَبِّرِينَ ﴿٧٦﴾

76. Ingieni kwenye milango ya Jahannamu, mdumu humo. Basi ni maovu yaliyoje makazi ya wanaotakabari!

فَاصْبِرْ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ فَإِمَّا نُرِيَنَّكَ بَعْضَ الَّذِي نَعِدُهُمْ أَوْ نَتَوَفَّيَنَّكَ فَإِلَيْنَا يُرْجَعُونَ ﴿٧٧﴾

77. Basi subiri, hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli. Na ama tukikuonyesha baadhi ya yale tuliyowaahidi au tukikufisha, lakini wao watarudishwa kwetu tu.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا رُسُلًا مِّن قَبْلِكَ مِنْهُم مَّن قَصَصْنَا عَلَيْكَ وَمِنْهُم مَّن لَّمْ نَقْصُصْ عَلَيْكَ وَمَا كَانَ لِرَسُولٍ أَن يَأْتِيَ بِآيَةٍ إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ فَإِذَا جَاءَ أَمْرُ اللَّـهِ قُضِيَ بِالْحَقِّ وَخَسِرَ هُنَالِكَ الْمُبْطِلُونَ ﴿٧٨﴾

78. Na kwa hakika tuliwatuma Mitume kabla yako. Wengine katika hao tumekusimulia na wengine hatukukusimulia. Na haiwi Mtume alete Ishara yoyote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Basi ikija amri ya Mwenyezi Mungu huhukumiwa kwa haki, na hapo wapotofu watapata hasara.

MLIKUWA MKIFURAHI

Aya 69 – 78

MAANA

Je, Huwaoni wale ambao wanabishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu wanageuziwa wapi?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu akipinga ubishi wa kibatili wa washirikina, kuwa umeona ewe Muhammad jinsi washirikina na wapenda anasa wanavyozifumbia macho hoja mkataa na ubainifu ulio wazi juu ya ukuu wa Mwenyezi Mungu na utume wako? Na pia vile wanavyoikimbia haki na kwenda kwenye ujinga na upotevu wa kuabudu mawe?

Ufafanuzi zaidi wa Aya hii na ufupisho wake ni kauli ya Imam Ali(a.s) :“Mwenye kukithirisha mzozo wake kwa ujinga hudumu upofu wake na haki.”

Ambao wamekadhibisha Kitabu yaani Qur’anina yale tuliyowatuma nayo Mitume wetu. Basi watakuja jua.

Siku hiyo uhakika utadhihirika na wakosefu wataiona adhabu yao,zitakapokuwa pingu shingoni mwao na minyororo, huku wanabururwa katika maji ya moto, kisha wataunguzwa Motoni.

Wataburuzwa kupelekwa motoni wakiwa wamefungwa minyororo, kinywaji chao kitakuwa maji ya moto na mikono itafungwa shingoni na utosi utakutanishwa na nyayo:

يُعْرَفُ الْمُجْرِمُونَ بِسِيمَاهُمْ فَيُؤْخَذُ بِالنَّوَاصِي وَالْأَقْدَامِ ﴿٤١﴾

“Watajulikana wakosefu kwa alama zao, watakamatwa kwa nywele za utosi na kwa miguu” (55-41).

Tena wataambiwa: Wako wapi mliokuwa mkiwashirikisha badala ya Mwenyezi Mungu na mkiwaweka akiba ya wakati wa shida? Basi waiteni wawaitikie ikiwa nyinyi ni wakweli.

Watasema: Wametupotea, wala hatuwaoni hata athari yao.bali tangu zamani hatukuwa tukiomba kitu! Kumbe walikuwa ni mangati tu.

Hivyo ndivyo Mwenyezi huwapoteza makafiri, kwa sababu wameamua kufuata njia mbaya kwa hiyari yao, baada ya kukatazwa na wakafa kwenye uovu na kufuru na hali wameamriwa kutubia na kurejea kwa Mwingi wa maghufira Mwenye kurehemu. Mwenye kuingia mlango wa uovu, ajilaumu mwenyewe tu.

TUNATAFUTA DUNIA KWA DINI

Haya ni kwa sababu mlikuwa mkifurahi katika ardhi pasipo haki, na kwa sababu mlikuwa mkijishaua.

Wakifurahi kwa mambo duni ya dunia yanayoisha wala hawatilii umuhimu neema za daima za akhera zinazowapita. Lakini wasifa huu hauwahusu washirikina tu; bali unatuhusu sisi pia. Tofauti ni kuwa wao wanaikabili dunia wakiwa wanikana Akhera waziwazi na kwa ndani, lakini sisi tunaikabili dunia na kuipupia kwa kutumia imani ya Mwenyezi Mungu na Siku ya mwisho. Sasa ni lipi kati haya mawili linastahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu?

Ingieni kwenye milango ya Jahannamu, mdumu humo. Basi ni maovu yaliyoje makazi ya wanaotakabari!

Ataambiwa haya mwenye kutakabari na kila mwenye kuitumia dini na nchi kujinufaisha na akachezea akili za watu wasio na hatia; ni sawa ameyafanya hayo kwa makusudi au kutojua hakika na hali halisi. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

قُلْ هَلْ نُنَبِّئُكُم بِالْأَخْسَرِينَ أَعْمَالًا ﴿١٠٣﴾ الَّذِينَ ضَلَّ سَعْيُهُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَهُمْ يَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ يُحْسِنُونَ صُنْعًا ﴿١٠٤﴾

“Sema je, tuwaambie wale wenye hasara mno ya vitendo? Ambao juhudi yao katika maisha ya dunia imepotea bure, nao wanadhani kuwa wanafanya kazi nzuri? Juz. 16 (18:103 – 104).

Ulama wameafikana kwa kauli moja kwamba mjinga (asiyejua) kwa uzembe hana udhuru mbele ya Mwenyezi Mungu.

Basi subiri, hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli.

Imetangulia kwa herufi zake katika Aya 55 katika sura hii tuliyo nayo.

Na ama tukikuonyesha baadhi ya yale tuliyowaahidi au tukikufisha, lakini wao watarudishwa kwetu tu.

Maneno yanelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) kuhusiana na washirikina. Maana ni kuwa tunaweza tukawaadhibu duniani wale wanaokukadhibisha na kukuudhi wewe ukiwaona na tunaweza tukakuhitari ukaja kwetu kabla ya hayo. Katika hali zote hizo, marejeo ni kwa Mwenyezi Mungu peke yake.

Aya inashiria kwamba mumin wa kweli anatakikana afurahi kwa yale yanayomridhisha Mwenyezi Mungu, awe na yakini na dini yake na afanye juhudi kadiri atakavyoweza kupiga vita ubatilifu na upotevu, kisha malipo amwachie Mwenyezi Mungu:

وَمَا رَبُّكَ بِغَافِلٍ عَمَّا يَعْمَلُونَ ﴿١٣٢﴾

“Na Mola wako si mwenye kughafilika na yale wanayoyatenda” Juz. 8 (6:132)

Na kwa hakika tuliwatuma Mitume kabla yako. Wengine katika hao tumekusimulia na wengine hatukukusimulia.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 6 (4:164). Tazama kifungu ‘Je, mitume wote ni wa mashariki?

Na haiwi Mtume alete Ishara yoyote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya ishara hapa ni muujiza. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hudhihirisha muujiza mikononi mwa mitume, kulingana na inavyotaka hekima na masilahi; sio kama wanavyotaka wenye kiburi na inadi.

Basi ikija amri ya Mwenyezi Mungu huhukumiwa kwa haki, na hapo wapotofu watapata hasara.

Hapo ni hapo Siku ya Kiyama; nayo ni siku mbaya sana kwa wabatilifu na siku njema sana kwa wenye haki.

اللَّـهُ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَنْعَامَ لِتَرْكَبُوا مِنْهَا وَمِنْهَا تَأْكُلُونَ ﴿٧٩﴾

79. Mwenyezi Mungu ndiye ambaye amewajaalia wanyamahowa ili muwapande baadhi yao na wengine muwale.

وَلَكُمْ فِيهَا مَنَافِعُ وَلِتَبْلُغُوا عَلَيْهَا حَاجَةً فِي صُدُورِكُمْ وَعَلَيْهَا وَعَلَى الْفُلْكِ تُحْمَلُونَ ﴿٨٠﴾

80. Na katika hao mna manufaa Na manapata kwao haja zilizo vifuani mwenu; Na mnachukuliwa juu yao na juu ya majahazi.

وَيُرِيكُمْ آيَاتِهِ فَأَيَّ آيَاتِ اللَّـهِ تُنكِرُونَ ﴿٨١﴾

81. Na anawaonyesha ishara zake, basi ni ipi katika ishara za Mwenyezi Mungu mtaikataa?

أَفَلَمْ يَسِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَيَنظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ كَانُوا أَكْثَرَ مِنْهُمْ وَأَشَدَّ قُوَّةً وَآثَارًا فِي الْأَرْضِ فَمَا أَغْنَىٰ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَكْسِبُونَ ﴿٨٢﴾

82. Je, hawatembei katika ardhi wakaona ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Walikuwa wenye nguvu zaidi kuliko wao na wakilima ardhi, lakini hayakuwafaa waliyokuwa wakiyachuma.

فَلَمَّا جَاءَتْهُمْ رُسُلُهُم بِالْبَيِّنَاتِ فَرِحُوا بِمَا عِندَهُم مِّنَ الْعِلْمِ وَحَاقَ بِهِم مَّا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٨٣﴾

83. Basi walipowajia Mitume wao kwa dalili zilizo wazi walifurahia elimu waliyokuwa nayo na yakawazunguka waliyokuwa wakiyafanyia sti- hzai.

فَلَمَّا رَأَوْا بَأْسَنَا قَالُوا آمَنَّا بِاللَّـهِ وَحْدَهُ وَكَفَرْنَا بِمَا كُنَّا بِهِ مُشْرِكِينَ ﴿٨٤﴾

84. Walipoiona adhabu yetu wakasema: Tumemwamini Mwenyezi Mungu peke yake na tumekataa tuliyokuwa tukimshirikisha naye.

فَلَمْ يَكُ يَنفَعُهُمْ إِيمَانُهُمْ لَمَّا رَأَوْا بَأْسَنَا سُنَّتَ اللَّـهِ الَّتِي قَدْ خَلَتْ فِي عِبَادِهِ وَخَسِرَ هُنَالِكَ الْكَافِرُونَ ﴿٨٥﴾

85. Lakini imani yao haikuwa ni yenye kuwafaa walipoiona adhabu yetu. Ni desturi ya Mwenyezi Mungu iliyopita kwa waja wake. Na hapo waliokufuru watapata hasara.

MWENYEZI MUNGU AMEWAJAALIA WANYAMAHOWA

Aya 79 – 85

MAANA

Mwenyezi Mungu ndiye ambaye amewajaalia wanyamahowa ili muwapande baadhi yao na wengine muwale.

Wanyamahowa ni ngamia, ng’ombe, mbuzi na kondoo. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewatumikisha kwa ajili ya manufaa ya binadamu; kama vile kula na kupanda.

Amewahusu kuwataja, pamoja na kuwa neema zake hazina idadi, kwa kuungana kwake na maisha ya waarabu wakati huo, na mpaka sasa bado wana mahitaji mengi sana katika baadhi ya miji.

Na katika hao mna manufaa mengine; kama vile kunufaika na manyoya yake na ngozi zake. Na manapata kwao haja zilizo vifuani mwenu; kama vile kubeba mizigo mizito na bidhaa mbalimbali kutoka mji mmoja hadi mwingine.Na mnachukuliwa juu yao na juu ya majahazi.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (6:142) na Juz. 14 (16:66).

Na anawaonyesha ishara zake, basi ni ipi katika ishara za Mwenyezi Mungu mtaikataa?

Yaani mtaikataa pamoja na hoja na dalili? Ndio walikata kwa vitendo ishara za Mwenyezi Mungu na hukumu zake. Kwa sababu mema kwao ni maovu na maovu kwao ni mema.

Je, hawatembei katika ardhi wakaona ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Walikuwa wenye nguvu zaidi kuliko wao na wakilima ardhi.

Historia ya watu wa ardhi imejaa mazingatio na mawaidha kwa mwenye kuzingatia na kupata somo. Ni uma ngapi zilifikia ukomo wa starehe na maendeleo, lakini walipopetuka mipaka, Mwenyezi Mungu aliwakamata kwa dhulma zao kwa mshiko wa Mwenye nguvu na uweza.Basi hayakufaa waliyokuwa wakiyachuma; kama vile utawala, mali na makasri na ngome walizozijenga. Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (12:109), Juz. 17 (22:46) na Juz 21 (30:9).

Basi walipowajia Mitume wao kwa dalili zilizo wazi wakifurahia elimu waliyokuwa nayo.

Makusudio ya furaha hapa ni kughurika. Na makusudio ya elimu ni sababu za utajiri, yaani elimu ya kuzalisha chakula na mavazi. Hilo linaashiriwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘Walikuwa wenye nguvu zaidi kuliko wao na wakilima ardhi.’ Qarun naye alipoambiwa: “Na utafute kwa aliyokupa Mwenyezi Mungu makazi ya Akhera” Alijibu: “Nimepewa haya kwa sababu ya elimu” Juz 20 (28:77-78)

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu aliwatuma mitume, kwa hoja mkataa, wakati uliopita kwenye umma zilizokuwa na utajiri; kama vile viwanda n.k. Wakaghurika kwa sababu hizi au kwa elimu na wakawafanyia maskhara manabii wa Mwenyezi Mungu na vitabu; sawa na mashirika ya leo yanayohodhi kila kitu ambayo yanaikataa haki na ubinadamu na kudharau thamani yake na amani ya mataifa

Na yakawazunguka waliyokuwa wakiyafanyia stihzai.

Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa kupituka kwao mipaka na yakawasibu yale waliyokuwa wakiyadharau. Huu ndio mwisho wa kila mwenye kupituka mipaka na kuasi, hata kama muda utarefuka kiasi gani.

Walipoiona adhabu yetu wakasema: Tumemwamini Mwenyezi Mungu peke yake na tumekataa tuliyokuwa tukimshirikisha naye.

Walipokuwa katika amani ya Mwenyezi Mungu walimkufuru, lakini walipoiona adhabu yetu wakasema tumeamini,lakini imani yao haikuwa ni yenye kuwafaa walipoiona adhabu yetu. Kwa sababu hii sio imani yoyote ispokuwa ni kukimbia adhabu, lakini watakimbia wapi?

Ni desturi ya Mwenyezi Mungu iliyopita kwa waja wake, ambayo ni kuwa Mwenyezi Mungu anasikiliza toba na kuzikubali katika nyumba ya taklifa na matendo sio katika nyumba ya hisabu na malipo.

Na hapo waliokufuru watapata hasara.

Kila mkosefu ni mwenye hasara na mtupu.

MWISHO WA SURA YA ARUBAINI: SURAT AL-GHAAFIR