TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 27001
Pakua: 2872


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 27001 / Pakua: 2872
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

Mwandishi:
Swahili

16

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Sura Ya Hamsini Na Mbili: Surat At-Tur. Imeshuka Makka. Ina Aya 49.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

وَالطُّورِ ﴿١﴾

1. Naapa kwa Mlima,

وَكِتَابٍ مَّسْطُورٍ ﴿٢﴾

2. Na kitabu kilichoandikwa

فِي رَقٍّ مَّنشُورٍ ﴿٣﴾

3. Katika waraka wa ngozi iliyo kunjuliwa,

وَالْبَيْتِ الْمَعْمُورِ ﴿٤﴾

4. Na kwa Nyumba iliyojengwa,

وَالسَّقْفِ الْمَرْفُوعِ ﴿٥﴾

5. Na kwa sakafu iliyonyanyuliwa,

وَالْبَحْرِ الْمَسْجُورِ ﴿٦﴾

6. Na kwa bahari iliyojazwa.

إِنَّ عَذَابَ رَبِّكَ لَوَاقِعٌ ﴿٧﴾

7. Hakika adhabu ya Mola wako hapana shaka itatokea.

مَّا لَهُ مِن دَافِعٍ ﴿٨﴾

8. Hapana wa kuizuia.

يَوْمَ تَمُورُ السَّمَاءُ مَوْرًا ﴿٩﴾

9. Siku zitakapotikisika mbingu kwa mtikiso,

وَتَسِيرُ الْجِبَالُ سَيْرًا ﴿١٠﴾

10. Na milima iwe inakwenda kwa mwendo mkubwa.

فَوَيْلٌ يَوْمَئِذٍ لِّلْمُكَذِّبِينَ ﴿١١﴾

11. Basi ole wao siku hiyo wanaokadhibisha,

الَّذِينَ هُمْ فِي خَوْضٍ يَلْعَبُونَ ﴿١٢﴾

12. Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi.

يَوْمَ يُدَعُّونَ إِلَىٰ نَارِ جَهَنَّمَ دَعًّا ﴿١٣﴾

13. Siku wataposukumwa kwenye Moto kwa msukumo wa nguvu.

هَـٰذِهِ النَّارُ الَّتِي كُنتُم بِهَا تُكَذِّبُونَ ﴿١٤﴾

14. Huu ndio ule Moto mliokuwa mkiukadhibisha!

أَفَسِحْرٌ هَـٰذَا أَمْ أَنتُمْ لَا تُبْصِرُونَ ﴿١٥﴾

15. Je, huu ni uchawi, au hamuoni?

اصْلَوْهَا فَاصْبِرُوا أَوْ لَا تَصْبِرُوا سَوَاءٌ عَلَيْكُمْ إِنَّمَا تُجْزَوْنَ مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿١٦﴾

16. Uingieni, mkistahamili au msistahamili - ni mamoja kwenu. Hakika mnalipwa kwa mliyokuwa mkiyatenda.

NAAPA KWA MLIMA

Aya 1 – 16

LUGHA

Anasema Fayruzi Abad katika Kamusi yake Al-Muhit: Neno Tur linatumika kwa maana ya uga wa nyumba, kila mlima na mlima ulio karibu na Ayla unaoitwa mlima Sinai. Pia hutumika kwa milima miwili, mmoja uko Qudus na mwingine ulioko Raasul-ayn. Vile vile mlima ulioko Tiberias.

MAANA

Naapa kwa Mlima, na kitabu kilichoandikwa katika waraka wa ngozi iliyo kunjuliwa, na kwa Nyumba iliyojengwa, na kwa sakafu iliyonyanyuliwa, na kwa bahari iliyojazwa.

Mlima hapa ni ule mlima Sinai aliozungumza Mwenyezi Mungu na Musa. Pia Mwenyezi Mungu ameapa na mlima huu katika (95:2).

Makusudio ya kitabu chenye kuandikwa ni kila kitabu cha mbinguni. Kwa sababu neno kitabu hapa limekuja kwa kuenea kwenye jinsia yake (nakra). Kulihusisha neno hilo na kitabu maalum kutahitajia maunganishao. Kule kutajwa mlima sinai tu, hakutoshi kuwa makusuidio yawe ni Tawrat.

Makusudio ya kusema kilichoandikwa katika waraka, ni kuwa Mwenyezi Mungu hakuteremsha kitabu ila alikifanya kitumike mikononi mwa watu na kila mtu aweze kukifikia na kukijua kwa ukamilifu. Imam Aliy(a.s ) anasema:

“Nashuhudia kuwa Muhammad ni mja wake na ni Mtume wake aliyemtuma kwa dini liliyo mashuhuri na kitabu kilichoandikwa.”

Nyumba iliyojengwa ni Al-Kaa’ba. Mwenyezi Mungu anasema:

وَإِذْ يَرْفَعُ إِبْرَاهِيمُ الْقَوَاعِدَ مِنَ الْبَيْتِ ﴿١٢٧﴾

“Na Ibrahim alipoinua misingi ya ile nyumba.” Juz. 1 (2:127).

Sakafu iliyonyanyuliwa ni mbingu:

وَجَعَلْنَا السَّمَاءَ سَقْفًا ﴿٣٢﴾

“Na tukaifanya mbingu kuwa sakafu.” Juz. 17 (21:32).

Yani iko kama sakafu katika jicho la mwenye kutazama. Bahari iliyojazwa ni kujaa maji:

وَإِذَا الْبِحَارُ سُجِّرَتْ ﴿٦﴾

“Na bahari zitakapojazwa.” (81:6).

Mwenyezi Mungu ameapa na vitu hivi vitano kuashiria uweza wake. Tazama Juz. 23 (37:1) kifungu cha: ‘Mwenyezi Mungu na kuapa na viumbe vyake.’

Hakika adhabu ya Mola wako hapana shaka itatokea kwa wakosefu. Jumla hii ni jawabu la kiapo. Hapana wa kuizuia; kama yalivyo mauti hakuna wa kuyarudisha ila yule mwenye kuleta uhai na mauti.

Siku zitakapotikisika mbingu kwa mtikiso.

Yaani kani mvutano itaondoka, uzani baina ya sayari utaharibika na kutokea mparaganyo utakaoenea.

Na milima iwe inakwenda kwa mwendo mkubwa. Itakapotikisika mbigu ardhi itatetemeka na milima itaondoka sehemu zake.

Aya mbili hizi zinaashiria kusimama kiyama na kuharibika ulimwengu, ambapo viumbe watakusnywa kwa ajili ya hisabu.

Basi ole wao siku hiyo wanaokadhibisha. Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi.

Waliichezea dunia nayo ikawachezea, lakini hawakuiweza, kwa hiyo ikawapiga mweleka na ikawapeleka haraka kwenye Jahannam ambayo ni makazi mabaya.

Siku wataposukumwa kwenye Moto kwa msukumo wa nguvu.

Watasukumwa kwa nguvu na Malaika wa adhabu watawaambia: Huu ndio ule Moto mlio kuwa mkiukadhibisha! “Ionjeni adhabu iunguzayo. Hayo ni kwa sababu ya yale yaliyokwishatangulizwa na mikono yenu. Na hakika Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.” Juz. 10 (8:50-51).

Je, huu ni uchawi, au hamuoni.

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) aliwahofisha na Moto wa Jahannam wakamwambia wewe ni mchawi. Siku ya malipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawafanya ni kuni za Jahannam na awaambie, je mmeona sasa? Je, Muhammad ni mchawi? Je, adhabu ya kuungua ni uchawi? Uingieni, mkistahamili au msistahamili - ni mamoja kwenu, adhabu ni hiyo hiyo haipungui wala haiishi. Hakika mnalipwa kwa mliyokuwa mkiyatenda ya dhulma na ufisadi.

إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَنَعِيمٍ ﴿١٧﴾

17. Hakika wenye takua watakua katika Mabustani na neema,

فَاكِهِينَ بِمَا آتَاهُمْ رَبُّهُمْ وَوَقَاهُمْ رَبُّهُمْ عَذَابَ الْجَحِيمِ ﴿١٨﴾

18. Wakifurahi kwa yale aliyowapa Mola wao. Na Mola wao atawalinda na adhabu ya Motoni.

كُلُوا وَاشْرَبُوا هَنِيئًا بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿١٩﴾

19. Kuleni na kunyweni kwa raha kwa sababu ya mliyokuwa mkiyatenda.

مُتَّكِئِينَ عَلَىٰ سُرُرٍ مَّصْفُوفَةٍ وَزَوَّجْنَاهُم بِحُورٍ عِينٍ ﴿٢٠﴾

20. Wakiegema viti vya fahari vilivyopangwa safu. Na tutawaoza mahurulaini.

وَالَّذِينَ آمَنُوا وَاتَّبَعَتْهُمْ ذُرِّيَّتُهُم بِإِيمَانٍ أَلْحَقْنَا بِهِمْ ذُرِّيَّتَهُمْ وَمَا أَلَتْنَاهُم مِّنْ عَمَلِهِم مِّن شَيْءٍ كُلُّ امْرِئٍ بِمَا كَسَبَ رَهِينٌ ﴿٢١﴾

21. Na walioamini na dhuriya zao wakawafuata kwa Imani tutawakutanisha nao dhuriya zao, na wala hatutawapunja kitu katika vitendo vyao kila mtu ni rehani wa alichokichuma.

وَأَمْدَدْنَاهُم بِفَاكِهَةٍ وَلَحْمٍ مِّمَّا يَشْتَهُونَ ﴿٢٢﴾

22. Na tutawapa matunda, na nyama kama watavyopenda.

يَتَنَازَعُونَ فِيهَا كَأْسًا لَّا لَغْوٌ فِيهَا وَلَا تَأْثِيمٌ ﴿٢٣﴾

23. Watapeana humo bilauri zisio na (vinywaji) vya upuuzi wala dhambi.

وَيَطُوفُ عَلَيْهِمْ غِلْمَانٌ لَّهُمْ كَأَنَّهُمْ لُؤْلُؤٌ مَّكْنُونٌ ﴿٢٤﴾

24. Na watawapitia watumishi wao kama kwamba ni lulu zilizofichwa.

وَأَقْبَلَ بَعْضُهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ يَتَسَاءَلُونَ ﴿٢٥﴾

25. Wataelekeana wakiulizana.

قَالُوا إِنَّا كُنَّا قَبْلُ فِي أَهْلِنَا مُشْفِقِينَ ﴿٢٦﴾

26. Waseme: Tulikuwa zamani pamoja na ahali zetu tukiogopa.

فَمَنَّ اللَّـهُ عَلَيْنَا وَوَقَانَا عَذَابَ السَّمُومِ ﴿٢٧﴾

27. Basi MwenyeziMungu akatufanyia hisani na akatulinda na adhabu ya upepo wa Moto.

إِنَّا كُنَّا مِن قَبْلُ نَدْعُوهُ إِنَّهُ هُوَ الْبَرُّ الرَّحِيمُ ﴿٢٨﴾

28. Hakika sisi zamani tulikuwa tukimwomba Yeye. Hakika Yeye ndiye Mwema Mwenye kurehemu.

WATU WA PEPONI

Aya 17 – 28

MAANA

Hakika wenye takua watakua katika Mabustani na neema, Wakifurahi kwa yale aliyowapa Mola wao. Na Mola wao atawalinda na adhabu ya Motoni.

Neno ‘wakifurahia’ tumelifasiri kutokana na neno fakihina ambalo pia lina maana ya kuwa njema nafsi. Maana zote mbili zinaendana na Pepo na neema. Lakini maana ya kufurahia inaafikiana zaidi na kauli yake Mwenyezi Mungu inayofuatia: Kuleni na kunyweni kwa raha.

Maana ni kuwa walimcha Mwenyezi Mungu duniani, naye amewakinga na adhabu ya Moto na amewafanyia Pepo kuwa ndio malipo yao.

Kuleni na kunyweni kwa raha kwa sababu ya mliyokuwa mkiyatenda.

Nyinyi wacha Mungu, mna haki zaidi ya neema hii, kwa sababu mlifanya kwa ikhlasi. Aya inafahamisha kuwa hakuna heshima yoyote mbele ya Mwenyezi Mungu kwa kiumbe isipokuwa kwa kufanya amali. Ama vyeo nasaba na mali si chochote, ila zikiwa ni nyenzo za heri na masilahi ya umma.

Wakiegema viti vya fahari vilivyopangwa safu.

Kuegema viti pamoja na kuwa faragha, kunafahamisha kutokuwa na matatizo ya maisha na tabu zake.

Na tutawaoza mahurulaini, wanovutia akili na macho kwa uzuri wao na ukamilifu wao. Neema iliyoje!

Na walioamini na dhuriya zao wakawafuata kwa Imani tutawakutanisha nao dhuriya zao.

Hakuna mwenye shaka kwamba watoto wadogo hawataadhibiwa kwa hali yoyote ile; ni sawa wazazi wao wawe wema au waovu, kwa sababu hakuna adhabu bila ya uasi, wala hakuna uasi bila taklifa. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemwondolea kalamu mtoto mdogo mpaka abaleghe.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekariri katika Aya kadhaa kauli yake: “Wala mbebaji hatabeba mzigo wa mwingine.” Juz. 8 (6:164).

Ama kauli ya anayesema kuwa mtoto wa kafiri ataingia motoni, kwa vile kama angeliishi basi angelifuata dini ya baba, kuali hii imeachwa, kwa sababu Mwenyezi Mungu humuhisabu mtu kwa aliyoyatenda, wala hamuhisabu kwa ambayo angeliyatenda.

Unaweza kuuliza : Je, watoto wadogo watafufuliwa na kuingia Peponi?

Jibu : Hakuna njia ya kujua hilo isipokuwa Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Nabii wake. Akili hapa haina nafasi ya kuhukumu; wala hakuna katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu au Hadith mutawatir kwamba watoto wa makafiri watafufuliwa.

Kuna Hadith isemayo: “Hakika waumini wataongozwa kwa baba zao wenye takua siku ya kiyama.” Wafasiri wengi wamesema kuwa watoto wakubwa wa waumini katika kizazi cha wanaomcha Mwenyezi Mungu watakutanishwa na daraja za juu za mababa zao Peponi, hata kama amali zao njema ziko chini, ili wazazi waburudike nao. Wameitolea dalili kauli yao hiyo kwa kauli yake Mwenyezi Mungu:

Na wala hatutawapunja kitu katika vitendo vyao; yaani tutawazidisha karama mababa wala hatutawapunguzia mababa kitu chochote katika thawabu zao na daraja zao.

Shia Imamia, Hanafi, Shafii na Hambali wamesema kuwa mtoto atahukumiwa kuwa ni Mwislamu kutokana na mmoja wa wazazi wake. Akiwa mmoja ni mwislamu na mwingine ni kafiri, basi mtoto atahukumiwa kuwa ni Mwislamu, bila ya kuangalia aliye kafiri ni baba au mama. Lakini Malik wamesema unaozingatiwa ni Uislamu wa baba tu, lakini mama hana athari yoyote ya Uislamu kwa mtoto wake.

Kila mtu ni rehani wa alichokichuma. Yeye peke yake atafuatwa na matendo yake na kwayo ndio atakubaliwa nayo kesho kwa Mungu wala hataulizwa aliyotenda mwingine.

Na tutawapa matunda, na nyama kama watavyopenda.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehusisha kutaja matunda na nyama, kwa sababu ndio vyakula vikuu.

Watapeana humo bilauri zisio na (vinywaji) vya upuuzi wala dhambi.

Watakunywa vinywaji vya kuchangamsha, lakini visivyokuwa na ulevi au vurugu wala kusababisha dhambi na kuchukuliana maneno.

Na watawapitia watumishi wao kama kwamba ni lulu zilizofichwa.

Kusema kwake Mwenyezi Mungu ‘watumishi wao’ ni ishara yakuwa wao watafuata amri zao na makatazo yao.

Wataelekeana wakiulizana.

Wataulizana ilivyokuwa duniani, Vipi wamestahiki heshima hii kutoka kwa Mwenyezi Mungu?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 23 (37:50).

Waseme: Tulikuwa zamani pamoja na ahali zetu tukiogopa.

Tulimwogopa Mwenyezi Mungu duniani kwa kuhofia ghadhabu yake na kutumai thawabu zake,Basi Mwenyezi Mungu akatufanyia hisani kwa rehema yake, akatuhusisha na neema yakena akatulinda na adhabu ya upepo wa Moto unaoambua ngozi na kuunguza nyuso.

Hakika sisi zamani tulikuwa tukimwomba Yeye. Hakika Yeye ndiye Mwema Mwenye kurehemu.

Duniani tulikuwa wema wenye huruma, na Mwenyezi Mungu huku Akhera amekuwa mwema kwetu na Mwenye huruma.

17

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

فَذَكِّرْ فَمَا أَنتَ بِنِعْمَتِ رَبِّكَ بِكَاهِنٍ وَلَا مَجْنُونٍ ﴿٢٩﴾

29. Basi kumbusha! na wewe, kwa neema ya Mola wako, si kuhani wala mwendawazimu.

أَمْ يَقُولُونَ شَاعِرٌ نَّتَرَبَّصُ بِهِ رَيْبَ الْمَنُونِ ﴿٣٠﴾

30. Au wanasema: mshairi, tunamtazamia kupatilizwa na dahari.

قُلْ تَرَبَّصُوا فَإِنِّي مَعَكُم مِّنَ الْمُتَرَبِّصِينَ ﴿٣١﴾

31. Sema: tazamieni, na mimi pia ni pamoja nanyi katika wanaotazamia.

أَمْ تَأْمُرُهُمْ أَحْلَامُهُم بِهَـٰذَا أَمْ هُمْ قَوْمٌ طَاغُونَ ﴿٣٢﴾

32. Au akili zao ndio zinawaamrisha haya, au wao ni watu waasi?

أَمْ يَقُولُونَ تَقَوَّلَهُ بَل لَّا يُؤْمِنُونَ ﴿٣٣﴾

33. Au wanasema: Ameitunga? Bali hawaamini tu.

فَلْيَأْتُوا بِحَدِيثٍ مِّثْلِهِ إِن كَانُوا صَادِقِينَ ﴿٣٤﴾

34. Basi na walete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli.

أَمْ خُلِقُوا مِنْ غَيْرِ شَيْءٍ أَمْ هُمُ الْخَالِقُونَ ﴿٣٥﴾

35. Au wao wameumbwa pasipo kutokana na chochote Au wao ndio waumbaji?

أَمْ خَلَقُوا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ بَل لَّا يُوقِنُونَ ﴿٣٦﴾

36. Au wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana yakini.

أَمْ عِندَهُمْ خَزَائِنُ رَبِّكَ أَمْ هُمُ الْمُصَيْطِرُونَ ﴿٣٧﴾

37. Au wanazo hazina za Mola wako, au wao ndio wenye madaraka?

أَمْ لَهُمْ سُلَّمٌ يَسْتَمِعُونَ فِيهِ فَلْيَأْتِ مُسْتَمِعُهُم بِسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿٣٨﴾

38. Au wanayo ngazi ya kusikilizia? Basi huyo msikilizaji wao na alete hoja iliyo wazi!

أَمْ لَهُ الْبَنَاتُ وَلَكُمُ الْبَنُونَ ﴿٣٩﴾

39. Au Yeye Mwenyezi Mungu ana wasichana, na nyinyi mna wavulana?

أَمْ تَسْأَلُهُمْ أَجْرًا فَهُم مِّن مَّغْرَمٍ مُّثْقَلُونَ ﴿٤٠﴾

40. Au wewe unawaomba ujira, kwa hiyo wanaelemewa na gharama?

أَمْ عِندَهُمُ الْغَيْبُ فَهُمْ يَكْتُبُونَ ﴿٤١﴾

41. Au wanayo ilimu ya ghaibu, nao wanaandika?

أَمْ يُرِيدُونَ كَيْدًا فَالَّذِينَ كَفَرُوا هُمُ الْمَكِيدُونَ ﴿٤٢﴾

42. Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini waliokufuru ndio watakaotegeka.

أَمْ لَهُمْ إِلَـٰهٌ غَيْرُ اللَّـهِ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٤٣﴾

43. Au wanaye mungu asiye kuwa Mwenyezi Mungu? Ametakasika Mwenyezi Mungu na hao wanaowashirikisha naye.

وَإِن يَرَوْا كِسْفًا مِّنَ السَّمَاءِ سَاقِطًا يَقُولُوا سَحَابٌ مَّرْكُومٌ ﴿٤٤﴾

44. Na hata wangeona pande linatoka mbinguni linaanguka wangesema: Ni mawingu yaliyobebana.

HANA UDHURU MWENYE KUUKANA UTUME WA MUHAMAD

Aya 29 – 44

MAANA

Aya hizi zinaashiria hali ya Mtume(s.a.w. w ) pamoja na washirikina pale alipowapa mwito wa Tawhid na kutupilia mbali ushirikina.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alianza kumwambia Mtume wake mtukufu kwa namna zifuatazo:-

1.Basi kumbusha! na wewe, kwa neema ya Mola wako, si kuhani wala mwendawazimu.

Endela na kazi yako ya kulingania kwa Mwenyezi Mungu na kuhadharisha adhabu yake; wala usijali na wayasemayo baadhi ya wapinzani kuwa wewe ni kuhani unayedai kujua ghaibu na wengine wakisema kuwa wewe ni mwendawazimu. Wewe kwa fadhila za Mwenyezi Mungu uko mbali kabisa na madai yao na urongo wao. Utakuwaje kuhani au mwendawazimu na hali Mwenyezi Mungu amekujaalia kuwa ni mwaminifu kwa wahyi wake na akakuchagua kwa risala yake?

2.Au wanasema: mshairi, tunamtazamia kupatilizwa na dahari kwa mauti.

Wengine wakisema ni mshairi anayezungumza kutokana na mawazo. Sema: tazamieni, na mimi pia ni pamoja nanyi katika wanaotazamia. Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume wake kuwaambia kuwa ngojeni na mimi ninangoja, mtajua nani atakayefikwa na adhabu ifedheheshayo na kuwa katika wanaojuta.

3.Au akili zao ndio zinawaamrisha haya ya uzushi na uwongo?

Makusudio ya ya akili zao, neno liliofasiriwa kutoka ‘Ahlam’ yenye maana ya noto, ni matamanio yao ya hadaa.

4.Au wao ni watu waasi?

Wao wanajua fika kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu wa haki na ukweli, lakini wanaikana haki kwa uasi, inadi na kupupia vyeo vyao na chumo lao.

5.Au wanasema: Ameitunga hiyo Qur’an! Bali hawaamini tu haki wala hawajizuii na batili!

Basi na walete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli kuwa Qur’an ni ushairi au ukuhani. Wanao washairi wengi na makuhani.

6.Au wao wameumbwa pasipo kutokana na chochote kwa sadfa tu, hakuna muumbaji wala mpangiliaji, hakuna lengo wala majukumu? Je hakuna chochote kabisa sawa na wanavyopatikana wadudu kwenye uvundo na uchafu?

7.Au wao ndio waumbaji waliojiumba wenyewe kwa uweza wao?

8.Au wameziumba mbingu na ardhi?

Unaweza kuuliza : washirikina hawadai kwamba wao wamejiumba wala kuumba wengine; bali Qur’an imenukuu kukiri kwao kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba na akaumba mbingu na ardhi. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَهُمْ لَيَقُولُنَّ اللَّـهُ ﴿٨٧﴾

“Na ukiwauliza ni nani aliyewaumba? Bila ya shaka watasema: Mwenyezi Mungu!”

Juz. 25 (43:87).

Pia amesema:

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَسَخَّرَ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ لَيَقُولُنَّ اللَّـهُ ﴿٦١﴾

“Na ukiwauliza ni nani aliyeumba mbingu na ardhi na akalitiisha jua na mwezi, bila shaka watasema ni Mwenyezi Mungu.” Juz. 21 (29:61).

Sasa je, kuna utetezi gani wa kauli yake Mwenyezi Mungu: “Au wao ndio waumbaji au wameziumba mbingu na ardhi?”

Jibu : wao kwa upande wa nadharia wanakubali kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu, lakini kwa upande wa kimatendo wanafanya kama anavyofanya asiyemwamini Mungu wala kukubali kuwa yuko. Bali matendo yao yanajulisha kuwa wao wanadai ni waumbaji na miungu. Haya ameyadokeza Mwenyezi Mungu kwa kauli yake:

Bali hawana yakini. Wasifu huu unawahusu wengi hivi sasa wanaodai kumwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho.

9.Au wanazo hazina za Mola wako.

Ikiwa wanakubali kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, je, basi wanadai kuwa Mungu amewaachia idara ya milki yake, kuchagua manabii wake, kugawanya riziki na umri kwa waja? Umetangulia mfano wake katika Juz. 25 (44:32).

10.Au wao ndio wenye madaraka kwa viumbe wote, atake Mwenyezi Mungu au asitake?

11.Au wanayo ngazi ya kusikilizia?

Ikiwa wao hawadai kitu katika hayo je, basi wanadai kuwa wamepanda kwa Mwenyezi Mungu na wakamsikia akisema kuwa Muhammad ni mwongo?

Basi huyo msikilizaji wao na alete hoja ilio wazi!

Haya ndio mantiki ya haki na uadilifu na ukomo wa kumfanyia haki hasimu. Kila mtu anaweza kudai anavyotaka, hata ilimu ya ghaibu, lakini kwa sharti ya kuleta ushahidi wazi wa madai yake; vinginevyo atakuwa ni mzushi mrongo.

12. Au Yeye Mwenyezi Mungu ana wasichana, na nyinyi mna wavu- lana?

Hakuna tofauti kabisa baina ya kusema kwao Muhammad ni mshairi, kuhani, mwendawazimu na kusema kwao kuwa Mwenyzi Mungu ana wasichana na wao wana wavulana. Uzushi kwa Mtume hauishilii tu kwa kusema kuwa yeye ni mwendawazimu wala kwa kumnasibishia Mwenyzi Mungu washirika au watoto; bali kila mwenye kuhalalisha haramu au aka- haramisha halali atakuwa amemzulia Mwenyezi Mungu na Mtume.

13. Au wewe unawaomba ujira, kwa hiyo wanalemewa na gharama?

Kwanini wamemkadhibisha Mtume wa Mwenyezi Mungu? Je amewalazimisha gharama inayowashinda kuitekeleza?

14.Au wanayo ilimu ya ghaibu, nao wanaandika?

Je, wao ni waandishi wa wahyi mbele ya Mwenyezi Mungu wakisajili riziki na umri na yule watakayemchagua katika manabii, kwa hiyo Mwenyezi Mungu hakuwapa jina la Muhammad kulisajili?

15.Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini walio kufuru ndio watakaotegeka.

Hii ndio hakika yao. Wao hawataki chochote isipokuwa vitimbi na uovu kwa Muhammad(s.a.w.w) , lakini vitimbi vitawarudia wao wenyewe, kwa sababu: “vitimbi viovu havimpati ilia mwenyewe” Juz. 22 (35:43)

16.Au wanaye mungu asiye kuwa Mwenyezi Mungu? Ametaksika Mwenyezi Mungu na hao wanaowashirikisha naye.

Ni nani huyo na yuko wapi huyo mungu ambaye atawaepusha na adhabu ya Mwenyezi Mungu itakapowashukia. Mwenyezi Mungu ametakata kabisa kuwa na mfano na mapinzani.

Na hata wangeona pande linatoka mbinguni linaanguka wangesema: Ni mawingu yaliyobebana.

Hata wangeiona adhabu, ana kwa ana, wangelifanya kiburi na kusema haya ni mawingu na sarabi tu. Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَلَوْ فَتَحْنَا عَلَيْهِم بَابًا مِّنَ السَّمَاءِ فَظَلُّوا فِيهِ يَعْرُجُونَ ﴿١٤﴾ لَقَالُوا إِنَّمَا سُكِّرَتْ أَبْصَارُنَا بَلْ نَحْنُ قَوْمٌ مَّسْحُورُونَ ﴿١٥﴾

“Na lau tungeliwafungulia mlango wa mbingu wakawa wanapanda. Basi wangelisema: Macho yetu yamelevywa; bali sisi ni watu waliorogwa.” Juz. 14 (15:14-15).

Kwa ufupi ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakumwachia udhuru wowote yule mwenye kukadhibisha au kuukadhibisha utume wa Muhammad(s.a.w.w) , ila akane kuweko Mwenyezi Mungu kabisa.

فَذَرْهُمْ حَتَّىٰ يُلَاقُوا يَوْمَهُمُ الَّذِي فِيهِ يُصْعَقُونَ ﴿٤٥﴾

45. Basi waache mpaka wakutane na siku yao watakaangamizwa.

يَوْمَ لَا يُغْنِي عَنْهُمْ كَيْدُهُمْ شَيْئًا وَلَا هُمْ يُنصَرُونَ ﴿٤٦﴾

46. Siku ambayo hila zao hazitawafaa kitu, wala wao hawatanusuriwa.

وَإِنَّ لِلَّذِينَ ظَلَمُوا عَذَابًا دُونَ ذَٰلِكَ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٤٧﴾

47. Na hakika waliodhulumu watapata adhabu nyengine isiyokuwa hiyo, lakini wengi wao hawajui.

وَاصْبِرْ لِحُكْمِ رَبِّكَ فَإِنَّكَ بِأَعْيُنِنَا وَسَبِّحْ بِحَمْدِ رَبِّكَ حِينَ تَقُومُ ﴿٤٨﴾

48. Na ingojee hukumu ya Mola wako. Kwani wewe hakika uko machoni mwetu. Na mtakase kwa kumsifu Mola wako unaposimama.

وَمِنَ اللَّيْلِ فَسَبِّحْهُ وَإِدْبَارَ النُّجُومِ ﴿٤٩﴾

49. Na usiku pia msabihi, na zinapokuchwa nyota.

BASI WAACHE MPAKA WAKUTANE NA SIKU YAO

Aya 45 – 49

MAANA

Basi waache mpaka wakutane na siku yao watakaangamizwa.

Bado maneno yanendelea kuhusiana na waliomkadhibisha Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) . Maana ni kuwa usijali ewe Muhammad na ukadhibishaji wao na inadi yao, kwani watafikiwa na siku isiyokuwa na kimbilio la kuepuka maangamizi na adhabu chungu.

Siku ambayo hila zao hazitawafaa kitu, wala wao hawatanusuriwa.

Yaani hakutakuwa na hila ya kujikinga siku hiyo wala hakutakuwa na usaidizi.

Na hakika waliodhulumu watapata adhabu nyengine isiyokuwa hiyo.

Yaani wataadhibiwa adhabu nyingine kabla ya siku ya kiyama. Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa hiyo ni adhabu ya kaburi. Wengine wakasema ni yaliyowapata siku ya vita vya Badr. Ama sisi tunayanyamazia aliyoyanya- mazia Mwenyezi Mungu.

Lakini wengi wao hawajui kuwa madhalimu wataadhibiwa kabla ya siku ya Kiyama na ndani ya Siku ya Kiyama.

Na ingojee hukumu ya Mola wako. Kwani wewe hakika uko machoni mwetu.

Makusudio ya hukumu ya Mwenyezi Mungu hapa ni kuwapa muda madhalimu mpaka siku yao waliyoagwa. Machoni mwetu ni kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) , yuko katika hifadhi ya adha ya maadui na vitimbi vyao.

Na msabihi kwa kumsifu Mola wako unaposimama na usiku pia msabihi, na zinapokuchwa nyota.

Mdhukuru Mwenyezi Mungu katika hali zote kwani kumdhukuru yeye ndio dhikri nzuri. Na amewahidi wenye kumdhukuru ahadi ya ukweli.

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA MBILI: SURAT AT-TUR

18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Sura Ya Hamsini Na Tatu: Surat An-Najm. Imeshuka Makka. Ina Aya 62.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

وَالنَّجْمِ إِذَا هَوَىٰ ﴿١﴾

1. Naapa kwa nyota inapoanguka,

مَا ضَلَّ صَاحِبُكُمْ وَمَا غَوَىٰ ﴿٢﴾

2. Mwenzenu hakupotea, wala hakukosea.

وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾

3. Wala hatamki kwa matamanio.

إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ ﴿٤﴾

4. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliotolewa;

عَلَّمَهُ شَدِيدُ الْقُوَىٰ ﴿٥﴾

5. Amemfundisha mwenye nguvu sana,

ذُو مِرَّةٍ فَاسْتَوَىٰ ﴿٦﴾

6. Mwenye umbo la sura, akatulia,

وَهُوَ بِالْأُفُقِ الْأَعْلَىٰ ﴿٧﴾

7. Naye yuko upeo wa juu kabisa.

ثُمَّ دَنَا فَتَدَلَّىٰ ﴿٨﴾

8. Kisha akakaribia na akateremka.

فَكَانَ قَابَ قَوْسَيْنِ أَوْ أَدْنَىٰ ﴿٩﴾

9. Akawa umbali wa pinde mbili, au karibu zaidi.

فَأَوْحَىٰ إِلَىٰ عَبْدِهِ مَا أَوْحَىٰ ﴿١٠﴾

10. Akampa wahyi mja wake alichompa wahyi.

مَا كَذَبَ الْفُؤَادُ مَا رَأَىٰ ﴿١١﴾

11. Moyo haukusema uwongo uliyoyaona.

أَفَتُمَارُونَهُ عَلَىٰ مَا يَرَىٰ ﴿١٢﴾

12. Je, mnabishana naye juu ya aliyoyaona?

وَلَقَدْ رَآهُ نَزْلَةً أُخْرَىٰ ﴿١٣﴾

13. Na alimuona mara nyingine,

عِندَ سِدْرَةِ الْمُنتَهَىٰ ﴿١٤﴾

14. Penye Mkunazi wa mwisho.

عِندَهَا جَنَّةُ الْمَأْوَىٰ ﴿١٥﴾

15. Karibu yake pana Bustani ya makazi.

إِذْ يَغْشَى السِّدْرَةَ مَا يَغْشَىٰ ﴿١٦﴾

16. Kilipoufunika huo Mkunazi kilichoufunuika.

مَا زَاغَ الْبَصَرُ وَمَا طَغَىٰ ﴿١٧﴾

17. Jicho halikuhangaika wala halikupetuka mpaka.

لَقَدْ رَأَىٰ مِنْ آيَاتِ رَبِّهِ الْكُبْرَىٰ ﴿١٨﴾

18. Hakika aliona katika Ishara kubwa kabisa za Mola wake.

ALIMWONA KWENYE MKUNAZI WA MWISHO MAANA

Aya 1 – 18

MAANA

Naapa kwa nyota inapoanguka.

Mwenye tafsir Al-Bahrul-muhit ametaja kauli kumi kuhusiana na Aya hii. Iliyo karibu zaidi ni ile isemayo kuwa Makusudio ya nyota ni nyota yoyote, kwa sababu Alif na laam iliyoko katika neno hilo ni za jinsia. Na kwamba maana ya kuanguka nyota ni kuwa zitaanguka na kutawanyika katika anga siku ya kiyama, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na nyota zitakapotawanyika.” (82:1). Kwa sababu Qur’an inajitafsiri yenyewe. Katika kiapo hiki kuna ishara kuwa mwenye kumkana Muhammad(s.a.w.w) atapata malipo yake Siku ya Kiyama.

Mwenzenu hakupotea, wala hakukosea, wala hatamki kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliotolewa.

Mwenzenu, ndiye anayeapiwa, ambaye ni Muhammad(s.a.w.w) anatamka na kutenda kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, si kwa shaka wala kwa kutojua, au kupotea wala kwa msukumuo wa matamanio yake. Vipi asitamke na kutenda kulingana na wahyi na hali yeye amekuja kutengeneza na kumaliza ufisadi na tamaa?

UMBALI WA PANDE MBILI

Aya hizi kuanzia 5 – 18, zinaashiria tukio maalum lisiloweza kujulikana isipokuwa kwa njia ya wahyi. Kwa sababu maudhui yake ni kujitokeza Jibril kwa Mtume mara mbili kwa sura yake halisi aliyomuumba nayo Mwenyezi Mungu na sio sura aliyozoea kuiona Mtume pale anapomletea wahyi.

Maneno yamekuwa mengi sana kuhusiana na Aya hizi; mpaka wengine wakathubutu kutaja wasifu wa Jibril na mbawa zake bila ya hoja wala dalili. Sisi tutafupiliza yale yanayofahamiushwa na dhahiri ya Aya na yanoingia akilini, bila ya kujilazimisha na kauli ya mfasiri au mpokezi; na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuombwa msaada:

1.Amemfundisha mwenye nguvu sana.

Kumfundisha Maana yake ni kumfikishia; yaani Jibril alimfikishia Muhammad(s.a.w.w) . Makusudio ya nguvu hapa ni sifa zinazomwandaa Jibril(a.s) kuufikisha wahyi; kama vile kuhifadhi, uaminifu na uhakika; kama kwamba Nabii anausikia moja kwa moja kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Dalili ya hilo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na hakika hiyo ni uteremsho wa Mola wa walimwengu wote. Ameiteremsha Roho mwaminifu.” Juz. 19 (26:192-193). Vile vile neno ‘amemfundisha,’ linaashiria hivyo.

Kwa hiyo Maana ni kuwa Jibril mwenye nguvu na mwaminifu, alimfkishia Muhammad(s.a.w.w) wahyi kwa uhakika wake kama ulivyo katika ilimu ya Mwenyezi Mungu.

2.Mwenye umbo la sura, akatulia.

Hiyo ni sifa ya Jibril; yaani alimtokea Mtume(s.a.w.w) sawasawa kama alivyoumbwa.

3.Naye yuko upeo wa juu kabisa.

Ni huyo huyo Jibril. Yaani alimpomtokezea Mtume kwa sura yake alikuwa amenyooka juu ya anga. Wafasiri wanasema: Upeo wa juu ni mawiyo ya jua; yaani mashariki na upeo wa chini ni magharibi. Kwa hali yoyote iwayo ni kuwa Makusudio yake ni kueleza kuwa Jibril sura yake ilitanda angani; wala si muhimu kuwa anga hiyo ilikuwa mashariki au magharibi.

4.Kisha akakaribia na akateremka. Akawa umbali wa pinde mbili, au karibu zaidi.

Hapa kuna maneno ya kutangulizwa; yaani aliteremka akakaribia. Maana ni kuwa Jibri baada ya kumdhirikia Mtume kama alivyoumbwa na Mwenyezi Mungu na umbo lake kupanda hadi juu, alirudi kwenye sura aliyokuwa akikutana nayo Mtume wakati akimpa wahyi na akamkurubia mpaka akawa kiasi cha umbali wa pinde mbili au chini yake. Ni maarufu kuwa Jibril alikuwa akimjia Mtume kwa sura ya Dahiya Al-Kalbiy

5.Akampa wahyi mja wake alichompa wahyi .

Aliyetoa wahyi ni Mwenyezi Mungu na mja ni Muhammad(s.a.w.w) . Maana ni kuwa Jibril baada ya kurudia sura yake aliyokuwa akikutana na Mtume na kumkurubia, Mwenyezi Mungu alimpa wahyi Muhammad(s.a.w.w) mambo muhimu kupitia kwa Jibril.

6.Moyo haukusema uwongo uliyoyaona.

Yaani Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alimuona Jibril kwa macho yake, kama alivyomuumba; jicho halikukosea lilichokiona wala moyo hakutuia shaka kilichoonwa na jicho; bali alikuwa na yakini na akasadiki.

Je, mnabishana naye juu ya aliyoyaona?

Wanaambiwa washirikina kuwa je, mnamkadhibisha Muhammad na kubishana naye kwa aliyoyaona kwa macho yake na kuyaamini kwa moyo wake na akili yake; na hali nyinyi mumeujua ukweli wake, uaminifu wake, akili yake na usawa wake?

7.Na alimuona mara nyingine, penye Mkunazi wa mwisho. Karibu yake pana Bustani ya makazi.

Mtume alimuona Jibril mara nyingine. Makusudio ya Mkunazi wa mwisho ni mahali pa mwisho na ukomo wanapopafikia viumbe; hata Malaika. Kundi la wafasiri wamesema kuwa katika mbingu ya saba kuna mti ulio kuume mwa Arshi unaoitwa, Mkunazi wa mwisho!

Kauli hii inahitajia dalili. Vyovyote iwavyo sisi hatuna majukumu ya kuu- jua hasa maadamu Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameunyamazia kuufafanua. Tunavyofahamu kutokana na Aya pamoja na maelezo yaliyokuja kwenye Juz.15 (17:1), ni kuwa Jibril alimchukua Mtume(s.a.w.w) usiku wa Miraji na kuzunguka naye mbinguni mpaka akafikia umbali aliouita Mwenyezi Mungu Mkunazi wa mwisho. Hapo akasimama na hakuendelea.

Ama kuhusu Bustani ya makazi, kauli zimegongana katika tafsiri yake. Lakini dhahiri ni kuwa ni Pepo ya milele aliyoijaalia Mwenyezi Mungu kuwa ni malipo ya wale wanaomcha, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na ama yule mwenye kuogopa kusimama mbele ya Mola wake, na akaikataza nafsi na matamanio, basi hakika Pepo ndio makazi.” (79:40-41). Kwani Qur’an inajifasiri yenyewe.

Maana yanayopatikana ni kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alimuona Jibril mara mbili kwa umbo lake, kama alivyo. Mara ya kwanza ni ile iliyoashiriwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Naye yuko upeo wa juu kabisa;” na mara ya pili ni katika usiku wa Miraji pale alipozunguka naye mpaka akafika mahali pasipovukwa.

Haya ndiyo yote yaliyojulishwa na dhahiri ya Aya, au tuliyoyafahamu sisi kutokana na dhahiri ya Aya. Zaidi ya hapo – kwa maoni yetu – ni katika mambo ya ghaibu, yaliyofichwa.

Kilipoufunika huo Mkunazi kilichoufunuika.

Neno kufunika tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu yaghsha ambalo pia lina maana ya kuja. Inafaa kufasiri Aya kwa maana zote mbili, kwa sababu makusudio yake ni kuwa kwenye Mkunazi wa mwisho kunapatikana maajabu ya athari ya uweza Mwenyezi Mungu na ukuu wake yasiyokuwa na kipimo wala kudhibitiwa na akili, ndio maana Mwenyezi Mungu akayafumba na kuacha kuyafafanua.

Jicho halikuhangaika wala halikupetuka mpaka.

Kabisa! Jicho la Mtume halikuepuka hali halisi. Kila aliloliona kwa Jibril na mbinguni usiku wa Miraji ni haki na kweli.

Hakika aliona katika Ishara kubwa kabisa za Mola wake.

Kuona ishara alizozishuhudia Mtume katika miraji ziko zaidi ya mahisabu yote na wakati na mahali pote, ni muhali kuziona binadamu isipokuwa kwa uweza wa Mwenyezi Mungu na matakwa yake. Tumezungumzia Israi na Miraji katika Juz. 15 (17:1) kifungu cha: “Israi kwa roho na mwili.’

أَفَرَأَيْتُمُ اللَّاتَ وَالْعُزَّىٰ ﴿١٩﴾

19. Je, mmemuona Lata na Uzza?

وَمَنَاةَ الثَّالِثَةَ الْأُخْرَىٰ ﴿٢٠﴾

20. Na Manata, mwingine wa tatu?

أَلَكُمُ الذَّكَرُ وَلَهُ الْأُنثَىٰ ﴿٢١﴾

21. Je, nyinyi mnao watoto wa kiume na Yeye ndio awe na watoto wa kike?

تِلْكَ إِذًا قِسْمَةٌ ضِيزَىٰ ﴿٢٢﴾

22. Huo ni mgawanyo wa dhulma!

إِنْ هِيَ إِلَّا أَسْمَاءٌ سَمَّيْتُمُوهَا أَنتُمْ وَآبَاؤُكُم مَّا أَنزَلَ اللَّـهُ بِهَا مِن سُلْطَانٍ إِن يَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ وَمَا تَهْوَى الْأَنفُسُ وَلَقَدْ جَاءَهُم مِّن رَّبِّهِمُ الْهُدَىٰ ﴿٢٣﴾

23. Hayo hayakuwa ila ni majina mliyowapa nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuteremsha dalili yoyote juu ya hayo. Hawafuati ila dhana tu na kipendacho nafsi. Na kwa hakika uwongofu ulikwishawafikia kutoka kwa Mola wao.

أَمْ لِلْإِنسَانِ مَا تَمَنَّىٰ ﴿٢٤﴾

24. Je, mtu anakipata kila anachokitamani?

فَلِلَّـهِ الْآخِرَةُ وَالْأُولَىٰ ﴿٢٥﴾

25. Ni wa Mwenyezi Mungu mwisho na mwanzo.

وَكَم مِّن مَّلَكٍ فِي السَّمَاوَاتِ لَا تُغْنِي شَفَاعَتُهُمْ شَيْئًا إِلَّا مِن بَعْدِ أَن يَأْذَنَ اللَّـهُ لِمَن يَشَاءُ وَيَرْضَىٰ ﴿٢٦﴾

26. Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia.

LATA NA UZZA

Aya 19 – 26

MAANA

Je, mmemuona Lata na Uzza? Na Manata, mwingine wa tatu?

Wanaambiwa washirikina wa kikuraishi waliokuwa wakiabudu masanamu haya na kuyaita ni mabinti wa Mungu, kwa hiyo ndio wakayapa majina yenye ishara ya kike ya herufi ta na alif.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alizikejeli akili zao kwa kusema:

Je, nyinyi mnao watoto wa kiume na Yeye ndio awe na watoto wa kike? Huo ni mgawanyo wa dhulma!

Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na wamemfanyia Mwenyezi Mungu yale wanayoyachukia.” Juz. 14 (16:62).

Hayo hayakuwa ila ni majina mliyowapa nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuteremsha dalili yoyote juu ya hayo, kwa sababu hayo ni mawe tu hayadhuru wala hayanufaishi.

Yametangulia mazungumzo kuhusu masanamu na ibada yake katika makumi ya Aya. Inatosha kuwa ni kuwarudi wanaoyaabudu na kuyatukuza, kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Hakika wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu hawatoumba nzi wajapojumuika kwa hilo. Na nzi akiwapokonya kitu hawawezi kukipata kwake. Amedhoofika atakaye na anayetakiwa.” Juz. 17 (22:73).

Mwanafasihi mmoja anasema: “Akikunyang’anya nzi maisha yako kwa kukuletea maradhi, ni nani anayeweza kukurudishia uhai huo? Na ikikutoka chembe moja tu ya chakula chako inayogeuka sukari katika matumbo yako, je wakemia wakikusanyika wote wataweza kukurudishia chembe yako?

Hawafuati ila dhana tu na kipendacho nafsi.

Makusudio ya dhana hapa ni ujinga. Mtu anayadhibiti matamanio yake kwa akili yake na ilimu yake. Akiwa ni mjinga au dhaifu wa akili, matamanio yake yatamhukumu na kumwongoza kwenye maangamizi.

Na kwa hakika uwongofu ulikwishawafikia kutoka kwa Mola wao, wakasema nyoyo zetu zimefunikwa na katika masikio yetu mna uziwi. Basi neno la adhabu likawathibitikia.

Je, mtu anakipata kila anachokitamani?

Washirikina walitamani shafaa ya masanamu, ndio Mwenyezi Mungu akawarudi kwa kuwauliza, je, mtu anaweza kupata kila anachotamani? Kwa maneno mengine ni kuwa waabudu masanamu walichanganya ujinga na matamanio yanayopofusha na kutia uziwi, basi ujinga ukapanda juu ya ujinga mwingine.

Ni wa Mwenyezi Mungu mwisho na mwanzo. Ufalme na amri ni yake peke yake duniani na akhera.

Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia.

Walisema kuwa sisi tunaabudu masanamu ili yatuombee kwa Mungu! Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawaambia kuwa Malaika wa mbinguni pamoja na ukubwa na utukufu wao nao hawataombea isipokuwa kwa idhini yake, vipi mawe yenye uziwi yaweze kuwaombea?

Tumezungumzia kuhusu shafaa katika Juz.1 (2:48) kifungu cha: ‘Shafaa.’