TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 7731
Pakua: 2258


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 7731 / Pakua: 2258
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

كَذَّبَتْ ثَمُودُ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٤١﴾

141. Thamud waliwakadhibisha mitume.

إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ صَالِحٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٤٢﴾

142. Alipowaambia ndugu yao Swaleh: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٤٣﴾

143. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٤٤﴾

144. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٤٥﴾

145. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

أَتُتْرَكُونَ فِي مَا هَاهُنَا آمِنِينَ ﴿١٤٦﴾

146. Je, mtaachwa salama katika haya yaliyopo hapa?

فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٤٧﴾

147. Katika mabustani na chem- chem?

وَزُرُوعٍ وَنَخْلٍ طَلْعُهَا هَضِيمٌ ﴿١٤٨﴾

148. Na mimea na mitende yenye makole yalioiva?

وَتَنْحِتُونَ مِنَ الْجِبَالِ بُيُوتًا فَارِهِينَ ﴿١٤٩﴾

149. Na mnachonga majumba mlimani kwa ustadi

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٥٠﴾

150. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَلَا تُطِيعُوا أَمْرَ الْمُسْرِفِينَ ﴿١٥١﴾

151. Wala msitii amri za waliopituka mipaka.

الَّذِينَ يُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ وَلَا يُصْلِحُونَ ﴿١٥٢﴾

152. Ambao wanafanya ufisadi katika ardhi wala hawaiten- genezi.

قَالُوا إِنَّمَا أَنتَ مِنَ الْمُسَحَّرِينَ ﴿١٥٣﴾

153. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.

مَا أَنتَ إِلَّا بَشَرٌ مِّثْلُنَا فَأْتِ بِآيَةٍ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿١٥٤﴾

154. Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi. Basi lete ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

قَالَ هَـٰذِهِ نَاقَةٌ لَّهَا شِرْبٌ وَلَكُمْ شِرْبُ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿١٥٥﴾

155. Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalum.

وَلَا تَمَسُّوهَا بِسُوءٍ فَيَأْخُذَكُمْ عَذَابُ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٥٦﴾

156. Wala msimguse kwa ubaya isije ikawashika adhabu ya siku kubwa.

فَعَقَرُوهَا فَأَصْبَحُوا نَادِمِينَ ﴿١٥٧﴾

157. Lakini wakamuua wakawa wenye kujuta.

فَأَخَذَهُمُ الْعَذَابُ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٥٨﴾

158. Basi ikawashika adhabu. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٥٩﴾

159. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

SWALEH

Aya 141 – 159

MAANA

Kisa cha Swaleh kimetangulia katika Juz. 8 (7: 73 – 79) na Juz. 12 (11: 61 -68).

Thamud waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Swaleh: Je, hamna takua? Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Zimetangulia Aya hizi kwa herufi zake katika sura hii Aya 105 – 110, na pia katika sehemu iliyopita bila ya mabadiliko yoyote isipokuwa jina tu la Thamud na Swaleh. Tumesema huko kuwa siri ya hilo ni kuwa risala ya mitume wote ni moja.

Je, mtaacha salama katika haya yaliyopo hapa katika mabustani na chemchem na mimea na mitende yenye makole yalioiva? Na mna chonga majumba mlimani kwa ustadi

Kabila la Thamud lilizama katika anasa na strehe – matunda, mito, makasri, wanyama n.k. Wakiwa wameghafilika na kila kitu isipokuwa matamanio yao na ladha zao. Ndipo ndugu yao Swaleh akawaonya na mwisho mbaya na akawaambia, Je, mmemsahau Mwenyezi Mungu na yeye hajawasahau? Je, mmejiaminisha na matukio ya ghafla?

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na nitiini wala msitii amri za waliopituka mipaka ambao wanafanya ufisadi katika ardhi wala hawaitengenezi.

Makusudio ya waliopituka mipaka, walio wafisadi, ni viongozi ambao ndio chimbuko la balaa zote; isipokuwa wachache sana. Hakuna dini wala misimamo, katika ufahamu wao, isipokuwa masilahi yao na masilahi ya jamaa zao.

Wafisadi hawa, katika kaumu ya Swaleh, walikuwa tisa; kama ilivyoelezwa katika Aya nyingine: kwenye juzuu hii. “Na walikuwako mjini watu tisa wakifanya ufisadi katika ardhi wala hawafanyi la masilahi” (25:48).

Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.

Umerogwa na mchawi mpaka umekuwa hujui unalolisema. Hivi ndivyo wasemavyo vijana wengi wa kileo wanapoambiwa swalini na fungeni.

Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, unakula chakula na kutembea sokoni, sasa vipi unateremshiwa wahyi zaidi yetu sisi?

Basi lete ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

Walisema haya wakiwa wameazimia kuendelea na ukafiri wao na inadi yao, hata kama wataletewa dalili elfu na moja; vinginevyo maombi yao yangelikuwa ya haki na ya sawa.

Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalum. Wala msimguse kwa ubaya isije ikawashika adhabu ya siku kubwa.

Walimuomba awaletee muujiza unaofahamisha utume wake, akawaletea ngamia kwa njia isiyo ya kawaida na akawawekea sharti la maji kwa zamu; siku moja yao na siku moja ya ngamia na kwamba wasimdhuru isije ikawafikia adhabu,

lakini wakamuua wakawa wenye kujuta, Basi ikawashika adhabu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7: 77 – 78).

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

كَذَّبَتْ قَوْمُ لُوطٍ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٦٠﴾

160. Kaumu ya Lut waliwakadhibisha mitume.

إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ لُوطٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٦١﴾

161. Alipowaambia ndugu yao Lut: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٦٢﴾

162. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٦٣﴾

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٤﴾

164. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

أَتَأْتُونَ الذُّكْرَانَ مِنَ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٥﴾

165. Je, katika viumbe wote mnawaendea wanaume?

وَتَذَرُونَ مَا خَلَقَ لَكُمْ رَبُّكُم مِّنْ أَزْوَاجِكُم بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ عَادُونَ ﴿١٦٦﴾

166. Na mnaacha alichowaumbia Mwenyezi Mungu katika wake zenu? Bali nyinyi ni watu mnaoruka mipaka.

قَالُوا لَئِن لَّمْ تَنتَهِ يَا لُوطُ لَتَكُونَنَّ مِنَ الْمُخْرَجِينَ ﴿١٦٧﴾

167. Wakasema: Kama hutakoma ewe Lut bila shaka utakuwa miongoni mwa wanaotolewa.

قَالَ إِنِّي لِعَمَلِكُم مِّنَ الْقَالِينَ ﴿١٦٨﴾

168. Akasema: Hakika mimi ni katika wanaokichukia hiki kitendo chenu.

رَبِّ نَجِّنِي وَأَهْلِي مِمَّا يَعْمَلُونَ ﴿١٦٩﴾

Mola wangu! Niokoe na ahli zangu kwa wayatendao.

فَنَجَّيْنَاهُ وَأَهْلَهُ أَجْمَعِينَ ﴿١٧٠﴾

Basi tukamuokoa na ahli zake wote.

إِلَّا عَجُوزًا فِي الْغَابِرِينَ ﴿١٧١﴾

171. Isipokuwa kikongwe katika waliokaa nyuma.

ثُمَّ دَمَّرْنَا الْآخَرِينَ ﴿١٧٢﴾

Kisha tukwaangamiza wale wengine.

وَأَمْطَرْنَا عَلَيْهِم مَّطَرًا فَسَاءَ مَطَرُ الْمُنذَرِينَ ﴿١٧٣﴾

173. Na tukawanyesheza mvua, basi ni uovu mno wa mvua ya waliyoonywa.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٧٤﴾

174. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٧٥﴾

175. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

LUT

Aya 160-175

MAANA

Kisa cha Lut kimetangulia katika Juz. 8 (7:80 –84) na Juz. 12 (11:82– 87).

Kaumu ya Lut waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Lut: Je, hamna takua?

Ni ndugu yao katika kuwa pamoja na makazi; si katika dini wala nasabu. Kwa kuwa yeye alikuja hapo na ami yake, Ibrahim(a.s) kutoka Babel (Babylon) kupitia Misr hadi Palestina. Lut alikaa katika bonde la Jordan na Ibrahim akakaa katika nyanda za juu kaskazini. Hapo ilikuwa ni karne kumi na tisa kabla ya kuzaliwa Nabii Isa (19 B.C.)

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya sura hii na pia sehemu iliyopita.

“Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Lut alianza kama alivyoanza Nuh, Hud na Swaleh(a.s ) . Kwa sababu risala ya wote ni moja. Soma katika sura hii Aya zinazomzungumzia kila mmoja katika wao.

Je, katika viumbe wote mnawaendea wanaume?

Mnafanya kitendo hiki cha fedheha kwa wanaume katika wanadamu?

Na mnaacha alichowaumbia Mwenyezi Mungu katika wake zenu?

Kwa hiyo mnahalifu hukumu ya maumbile na kanuni, tabia na lengo la kumbwa mume na mke.

Tendo lenu halikubaliwi hata na wanyama na wadudu. Lakini bunge la Uingereza limeruhusu ulawiti. Hiyo ni dalili kuwa Uingereza ni duni zaidi kuliko wanyama katika hulka yake na thamani yake. Sio mbali kuwa hii ni natija ya historia yake ndefu ya ukoloni unaochukiwa. Kwa sababu utaghuti na uadui una mwisho mbaya.

Bali nyinyi ni watu mnaoruka mipaka.

Mmepituka mipaka yote kwa hawa, usafihi, uasi na ujeuri wenu.

Wakasema: Kama hutakoma ewe Lut bila shaka utakuwa miongoni mwa wanaotolewa.

Umetangulia mfano wake katika Aya 116 ya Sura hii.

Akasema: Hakika mimi ni katika wanaokichukia hiki kitendo chenu.

Katika maana yake ni; Aya 216 ya sura hii! “Na ikiwa watakuasi basi sema mimi ninajitenga mbali na hayo mnayo yatenda.”

Mola wangu! Niokoe na ahli zangu kwa wayatendao. Basi tukamuokoa na ahli zake wote. Isipokuwa kikongwe katika waliokaa nyuma. Kisha tukwaangamiza wale wengine. Na tukawanyesheza mvua, basi ni uovu mno wa mvua ya waliyoonywa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:83 – 84) na Juz. 14 (15:59 – 60).

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.

كَذَّبَ أَصْحَابُ الْأَيْكَةِ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٧٦﴾

176. Watu wa mwituni waliwakadhibisha mitume.

إِذْ قَالَ لَهُمْ شُعَيْبٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٧٧﴾

177. Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٧٨﴾

178. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٧٩﴾

179. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٨٠﴾

180. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

أَوْفُوا الْكَيْلَ وَلَا تَكُونُوا مِنَ الْمُخْسِرِينَ ﴿١٨١﴾

181. Timizeni kipimo sawasawa wala msiwe miongoni mwa wanaopunja.

وَزِنُوا بِالْقِسْطَاسِ الْمُسْتَقِيمِ ﴿١٨٢﴾

182. Na pimeni kwa mizani iliyo sawa.

وَلَا تَبْخَسُوا النَّاسَ أَشْيَاءَهُمْ وَلَا تَعْثَوْا فِي الْأَرْضِ مُفْسِدِينَ ﴿١٨٣﴾

183. Wala msiwapunguzie watu vitu vyao, Wala msifanye ufisadi katika nchi mkafanya vurugu.

وَاتَّقُوا الَّذِي خَلَقَكُمْ وَالْجِبِلَّةَ الْأَوَّلِينَ ﴿١٨٤﴾

184. Na mcheni aliyewaumba nyinyi na vizazi vilivyotangulia.

قَالُوا إِنَّمَا أَنتَ مِنَ الْمُسَحَّرِينَ ﴿١٨٥﴾

185. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.

وَمَا أَنتَ إِلَّا بَشَرٌ مِّثْلُنَا وَإِن نَّظُنُّكَ لَمِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿١٨٦﴾

186. Na wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, na kwa hakika tunakuona ni katika waongo.

فَأَسْقِطْ عَلَيْنَا كِسَفًا مِّنَ السَّمَاءِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿١٨٧﴾

187. Basi tuangushie kipande cha mbingu, ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

قَالَ رَبِّي أَعْلَمُ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٨٨﴾

188. Akasema: Mola wangu anajua zaidi mnayoyatenda.

فَكَذَّبُوهُ فَأَخَذَهُمْ عَذَابُ يَوْمِ الظُّلَّةِ إِنَّهُ كَانَ عَذَابَ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٨٩﴾

189. Basi wakamkadhibisha, ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٩٠﴾

190. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٩١﴾

191. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

SHUA’YB

Aya 176 – 191

MAANA

Kisa cha Shua’yb kimetangulia katika Juz. 8 (7: 85) na Juz. 12 (11:84 – 95).

Watu wa mwituni waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?

Wafasiri wamesema kuwa watu wa mwituni ni watu waliokuwa karibu na Madyan kwenye miti mingi.

Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakusema ndugu yao Shua’yb, kama alivyosema ndugu yao Hud, Swaleh na Lut, kwa sababu Shua’yb si mtu wa hapo kinasabu wala hana uhusiano wowote na watu wa mwituni, isipokuwa ujirani. Mwenyezi Mungu alimtuma kwao; kama alivyomtuma kwa watu wake wa Madyan.

Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Aya hizi zimetanguliwa kwa herufi zake kupitia mdomoni mwa Nuh, Hud, Swaleh na Lut. Hayo ni maneno ya kila Nabii.

Timizeni kipimo sawasawa wala msiwe miongoni mwa wanaopunja. Na pimeni kwa mizani iliyo sawa. Wala msiwapunguzie watu vitu vyao, Wala msifanye ufisadi katika nchi mkafanya vurugu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7: 85) na Juz. 12 (11:84)

Na mcheni aliyewaumba nyinyi na vizazi vilivyotangulia.

Yaani mhofie adhabu ya Mwenyezi Mungu aliyewaumba nyinyi na wale waliotangulia.

Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.

Imetangulia kwa herufi zake katika Aya 153 ya sura hii.

Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, na kwa hakika tunakuona ni katika waongo.

Yaani wewe unakusudia uwongo katika madai yako ya utume, kwa dalili ya kuwa wewe ni mtu unayekula chakula na kutembea sokoni. Lau wahyi ungeliwashukia watu basi watu wote wangelikuwa Mitume.

Ibn Hisham katika kitabu Al-Mughni, katika kuelezea watu wasiofaliwa na maneno yoyote, anasema: “Mtu mmoja alimwambia mwengine: ‘Baba yako amemfanyaje punda wako?’ Akasema: ‘Amemuuzo’ akiwa na maana amemuuza. Yule muulizaji akasema kwa mshangao: kwa nini umeweka o kwenye herufi ya mwisho? yule akajibu: si wewe umeweka o kwenye herufi ya mwisho!” Mtu wa namna hii utamwambiaje?

Basi tuangushie kipande cha mbingu, ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

Aliwahadharisha na adhabu wakamdharau na wakasema iko wapi hiyo adhabu unayotutisha nayo, basi teremsha kipande cha mbingu kiwe ni adhabu, ukiwa ni mkweli wa madai yako.

Akasema: Mola wangu anajua zaidi mnayoyatenda na amri ni yake peke yake, akitaka ataileta haraka au ataicheleweshwa. Basi wakamkadhibisha, ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakubainisha kivuli hicho. Wafasiri wanasema ni mawingu waliyoyafanya kivuli kutokana na joto lililowapata, kisha yakawanyeshea mvua ya moto iliyowaunguza wote.

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَإِنَّهُ لَتَنزِيلُ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٩٢﴾

192. Na hakika hiyo ni uteremsho wa Mola wa walimwengu wote.

نَزَلَ بِهِ الرُّوحُ الْأَمِينُ ﴿١٩٣﴾

193. Ameiteremsha Roho mwaminifu.

عَلَىٰ قَلْبِكَ لِتَكُونَ مِنَ الْمُنذِرِينَ ﴿١٩٤﴾

194. Juu ya moyo wako, ili uwe katika waonyaji.

بِلِسَانٍ عَرَبِيٍّ مُّبِينٍ ﴿١٩٥﴾

195. Kwa ulimi wa kiarabu ulio wazi.

وَإِنَّهُ لَفِي زُبُرِ الْأَوَّلِينَ ﴿١٩٦﴾

197. Na hakika hiyo iko katika vitabu vya kale.

أَوَلَمْ يَكُن لَّهُمْ آيَةً أَن يَعْلَمَهُ عُلَمَاءُ بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿١٩٧﴾

198. Je haikuwa kwao ni ishara kwamba wanayajua haya maulama wa wana wa Israil?

وَلَوْ نَزَّلْنَاهُ عَلَىٰ بَعْضِ الْأَعْجَمِينَ ﴿١٩٨﴾

198. Lau tungeliitermsha juu ya mmoja wa wasiokuwa waarabu.

فَقَرَأَهُ عَلَيْهِم مَّا كَانُوا بِهِ مُؤْمِنِينَ ﴿١٩٩﴾

199. Na akawasomea wasingelikuwa wenye kuiamini.

كَذَٰلِكَ سَلَكْنَاهُ فِي قُلُوبِ الْمُجْرِمِينَ ﴿٢٠٠﴾

200. Namna hivi tunaingiza katika nyoyo za wakosefu.

لَا يُؤْمِنُونَ بِهِ حَتَّىٰ يَرَوُا الْعَذَابَ الْأَلِيمَ ﴿٢٠١﴾

201. Hawataiamini mpaka waione adhabu chungu.

فَيَأْتِيَهُم بَغْتَةً وَهُمْ لَا يَشْعُرُونَ ﴿٢٠٢﴾

202. Basi itawafikia ghafla na hali hawaitambui.

فَيَقُولُوا هَلْ نَحْنُ مُنظَرُونَ ﴿٢٠٣﴾

203. Na watasema: Je sisi tutapewa muda?

أَفَبِعَذَابِنَا يَسْتَعْجِلُونَ ﴿٢٠٤﴾

204. Basi je wanahimiza adhabu yetu?

أَفَرَأَيْتَ إِن مَّتَّعْنَاهُمْ سِنِينَ ﴿٢٠٥﴾

205. Unaonaje, kama tukiwastarehesha kwa miaka.

ثُمَّ جَاءَهُم مَّا كَانُوا يُوعَدُونَ ﴿٢٠٦﴾

206. Kisha yawafikie waliyokuwa wakiahidiwa.

مَا أَغْنَىٰ عَنْهُم مَّا كَانُوا يُمَتَّعُونَ ﴿٢٠٧﴾

207. Hayatawafaa yale waliyostareheshewa.

وَمَا أَهْلَكْنَا مِن قَرْيَةٍ إِلَّا لَهَا مُنذِرُونَ ﴿٢٠٨﴾

208. Wala hatukuuangamiza mji wowote ila ulikuwa na waonyaji.

ذِكْرَىٰ وَمَا كُنَّا ظَالِمِينَ ﴿٢٠٩﴾

209. Kuwa ni ukumbusho wala hatukuwa sisi ni wenye kudhulumu.

وَمَا تَنَزَّلَتْ بِهِ الشَّيَاطِينُ ﴿٢١٠﴾

210. Wala mashetani hawakuteremka nayo.

وَمَا يَنبَغِي لَهُمْ وَمَا يَسْتَطِيعُونَ ﴿٢١١﴾

211. Wala haiwapasi wala hawaiwezi.

إِنَّهُمْ عَنِ السَّمْعِ لَمَعْزُولُونَ ﴿٢١٢﴾

121. Hakika wao wametengwa na kusikia.

AMEITERMSHA ROHO MWAMINIFU

Aya 192 – 212

MAANA

Na hakika hiyo ni uteremsho wa Mola wa walimwengu wote. Ameiteremsha Roho mwaminifu juu ya moyo wako, ili uwe katika waonyaji.

Hiyo ni Qur’an. Roho mwaminifu ni Jibril(a.s) na maneno yanelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) .

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja visa vya mitume katika Aya zilizotangulia, sasa anamtaja Muhammad na Qur’an na kwamba Jibril ameitermsha kwa Mtume mtukufu ili apambane na makafiri na wapinzani kwa Aya zake na ubainifu wake. Jibril ameitwa roho kwa sababu ameiteremsha Qur’an ambayo ni uongofu na ponyo kwa roho:

هُوَ لِلَّذِينَ آمَنُوا هُدًى وَشِفَاءٌ ﴿٤٤﴾

“Hiyo ni uwongofu na ponyo kwa wenye kuamini.” (41:44).

Na ameitwa mwaminifu kwa sababu ni mtiifu kwa Mwenyezi Mungu, akiwa na biidii ya kuufikisha ujumbe wake kwa mitume, kama ulivyo. Yeye vile vile anaujua huo ujumbe na malengo yake.

Kwa ulimi wa kiarabu ulio wazi.

Katika Juz. 12 (12:2) tumebainisha sababu za kushuka Qur’an kwa lugha ya kiarabu, tazama huko.

Na hakika hiyo iko katika vitabu vya kale.

Yaani vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyotangulia, vilimbashiria Muhammad(s.a.w.w) na Qur’an. Huko nyuma tulithibitisha dalili za kiakili na kinakili kwamba Qur’an ni wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Katika dalili za kiakili ni kwamba Qur’an iliwashinda wapinzani hata kuleta mfano mmoja tu wa Sura zake. Walijaribu wakashindwa. Na kwamba inatolea habari mambo ya ghaibu na yakatokea. Pia hiyo Qur’an inachukua njia nyingi za tafsiri. Wala hakuna siri ya hili ila ni kwa kuwa inatoka kwa ambaye amekizunguka kila kitu kwa ujuzi. Tazama Juz. 1 (2: 23) Juz. 5 (4:53 na 82) na Juz. 18 (24:55).

Ama dalili za kinukuu, miongoni mwazo ni Tawrat na Injili za asili, zilizoleta bishara ya Muhammad. Tazama Juz. 9 (7: 157). Vile vile vitabu vingine vya mbinguni vilitoa habari ya kuja Muhammad. Tazama Juz. 1 (2:46).

Je, Haikuwa kwao ni ishara kwamba wanayajua haya maulama wa wana wa Israil?

Maulama wa kiyahudi, kabla ya kutumwa Mtume(s.a.w.w) , walikuwa wakimbashiria Muhammad; wakiwazungumzia waarabu kuhusiana naye na kutaja sifa zake kwa makuraishi na wengineo. Alipokuja wakasilimu baadhi ya Mayahudi waliokuwa wakimzungumzia; kama vile Abdallah bin Salaam na wenzake. Vile vile wakasilimu jamaa katika waarabu na wakampinga mayahudi wengine na vigogo katika makuraishi.

Aya hii inawaambia wale waliomkadhibisha Muhammad(s.a.w.w) baada ya kusikia hadith ya mayahudi kumhusu. Inawaambia, vipi mnamkadhibisha na hali mmewasikia maulama wa kiyahudi kabla, wakimtolea habari, wakikiri kuwa ametajwa katika Tawrat? Ushahidi wao huo hauwatoshi kuwa ni dalili ya ukweli wa Muhammad(s.a.w.w) ?

Hakuna mwenye shaka kwamba dalili hii ni tosha kwa mwenye kuitafuta haki kwa njia ya haki, lakini vigogo ambao walipinga utume wa Muhammad(s.a.w.w) walifanya hivyo kwa sababu ya masilahi yao; sio kwa sababu ya udhaifu wa hoja na dalili:

وَمَا تُغْنِي الْآيَاتُ وَالنُّذُرُ عَن قَوْمٍ لَّا يُؤْمِنُونَ ﴿١٠١﴾

“Na dalili na maonyo hayawafai watu wasioamini.” Juz. 11 (10:101).

Lau tungeliiteremsha juu ya mmoja wa wasiokuwa waarabu na akawasomea, wasingelikuwa wenye kuiamini.

Wao hawaiamini haki na ubainifu wake, iwe imekuja na mwarabu au asiyekuwa mwarabu. Kwa sababu haki na elimu kwao ni masilahi; vinginevyo si chochote kwao. Tumelikariri hilo mara nyingi pamoja na uwazi wake.

Namna hivi tunaingiza katika nyoyo za wakosefu.

Yaani wakosefu wanapoisikia haki au Qur’an wanaipinga na kuikanusha. Kwa maneno mengine ni kuwa mbengu inaota vizuri kwenye ardhi iliyo na rutuba, lakini ikiwa ardhi si nzuri, basi uotaji wake utakuwa hauna manufaa:

وَالْبَلَدُ الطَّيِّبُ يَخْرُجُ نَبَاتُهُ بِإِذْنِ رَبِّهِ وَالَّذِي خَبُثَ لَا يَخْرُجُ إِلَّا نَكِدًا ﴿٥٨﴾

“Na mji mzuri hutoa mimea yake kwa idhini ya Mola wake. Na ule ulio mbaya hautoi ila kwa taabu tu.” Juz. 8 (7:58).

Kadhalika haki inaleta matunda na athari ikisadifu kuwa kwenye nafsi safi na haileti chochote ikiwa kwenye nafsi chafu. Maana ni kuwa Qur’an haina athari yoyote katika nafsi zao isipokuwa upinzani na kukadhibisha.

Hawataiamini mpaka waione adhabu chungu. Basi itawafikia ghafla na hali hawaitambui.

Wakosefu hawaiamini Qur’an. Yaani wao hawaiamini haki hata ikiwa na dalili kiasi gani ila ikiwafikia adhabu kwa ghafla. Na wakionywa kabla wanaifanyia masihara. Ilivyo ni kwa kunyenyekea wakati wa kuona adhabu ni unafiki na ni kulazimishwa sio hiyari.

Na watasema: Je sisi tutapewa muda?

Waliiharakia adhabu kabla ya kuiona na wakamwambia Mtume wao ilete ukiwa ni katika wakweli. Walipoiona kwa macho walijuta na wakatamani lau wangelipewa muda ili waamini na watii. Ndivyo alivyo mpotevu; anatamani kurudi au kupewa muda baada ya kupita wakati.

Basi je wanahimiza adhabu yetu?

Haya ni maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwajibu wale waliomwambia Mtume wao. Tuangushie kipande cha mbingu na tuletee yale uliyotuahidi. Maana yake ni kuwa vipi mnaiharakia adhabu na ikiwafikia hamuiwezi wala kuikwepa.

Unaonaje, kama tukiwastarehesha kwa miaka, kisha yawafikie waliyokuwa wakiahidiwa, hayatawafaa yale waliyostareheshewa?

Wakosefu watatamaani kupewa muda watakapoiona adhabu, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawajibu kwamba kupewa muda hakufai kitu hata kama muda utakuwa mrefu kiasi gani. Bali kila muda unavyokuwa mrefu ndio madhambi yanazidi na kuongezeka na kuzidi adhabu yao.

Wala hatukuuangamiza mji wowote ila ulikuwa na waonyaji.

Aya hii iko katika maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَمَا كُنَّا مُعَذِّبِينَ حَتَّىٰ نَبْعَثَ رَسُولًا ﴿١٥﴾

“Wala sisi hatuadhibu mpaka tupeleke Mtume.” Juz. 15 (17:15).

Kuwa ni ukumbusho wala hatukuwa sisi ni wenye kudhulumu katika kuangamiza miji, wakati ambapo tulituma waonyaji wa hiyo adhabu, na wakumbushaji wa twaa ya Mwenyezi Mungu wakiwa na dalili. Wakawakadhibisha ndio ikastahiki adhabu.

Wala mashetani hawakuteremka nayo wala haiwapasi wala hawaiwezi.

Watu wa wakati wa ujahili walikuwa wakiitakidi ukuhani; kwamba kila kuhani ana shetani wake anayemletea habari za ghaibu. Iliposhuka Qur’an wakasema kuwa inatoka kwa shetani kwenda kwa makuhani ambao nao wanampelekea Muhammad(s.a.w.w) ; au yeye mwenyewe ni kuhani anayeteremkiwa na shetani.

Ndipo Mwenyezi Mungu akayajibu madai haya, kuwa Qur’an ni uongofu, mwanga na ni ubainifu ulio wazi. Ni wapi na wapi ukuhani na ushetani kulinganisha na uongofu na ubainifu? Wao ni dhaifu na ni duni zaidi. Zaidi ya hayo ni kuwa hakika wao wametengwa na kusikia.

Wamezuiliwa kusikia Qur’an pale Mwenyezi Mungu anapompa Jibril kuileta kwa Muhammad(s.a.w.w) . Ikiwa mashetani wameshindwa kuleta hata Aya moja mfano wake na pia kusikiliza japo tamko moja, basi watainukuu vipi kwa makuhani na kuitolea habari?

فَلَا تَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ فَتَكُونَ مِنَ الْمُعَذَّبِينَ ﴿٢١٣﴾

213. Basi usimwombe Mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu ukawa miongoni mwa watakaoadhibiwa.

وَأَنذِرْ عَشِيرَتَكَ الْأَقْرَبِينَ ﴿٢١٤﴾

214. Na uwonye jamaa zako walio karibu.

وَاخْفِضْ جَنَاحَكَ لِمَنِ اتَّبَعَكَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٢١٥﴾

215. Na inamisha bawa lako kwa wanokufuata katika waumini.

فَإِنْ عَصَوْكَ فَقُلْ إِنِّي بَرِيءٌ مِّمَّا تَعْمَلُونَ ﴿٢١٦﴾

216. Na ikiwa watakuasi basi sema: Mimi ninajitenga mbali na hayo mnayoyafanya.

وَتَوَكَّلْ عَلَى الْعَزِيزِ الرَّحِيمِ ﴿٢١٧﴾

217. Na mtegemee Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

الَّذِي يَرَاكَ حِينَ تَقُومُ ﴿٢١٨﴾

218. Ambaye anakuona unaposimama.

وَتَقَلُّبَكَ فِي السَّاجِدِينَ ﴿٢١٩﴾

219. Na mageuko yako katika wale wanaosujudu.

إِنَّهُ هُوَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴿٢٢٠﴾

220. Hakika yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.

WAONYE JAMAA ZAKO WA KARIBU

Aya 213 – 220

MAANA

Basi usimwombe Mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu ukawa miongoni mwa watakaoadhibiwa.

Dhahiri ya mfumo wa maneno inaonyesha yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , lakini makusudio ni kutoa habari kuwa kila atakayemuomba Mungu mwingine zaidi ya Mwenyezi Mungu basi atakuwa ni mwenye kuadhibiwa kwa hali yoyote atakayokuwa.

Na uwonye jamaa zako walio karibu.

Mtume(s.a.w.w) ni mwenye kuamrishwa kuwaonya watu wote:

يَا أَيُّهَا الْمُدَّثِّرُ ﴿١﴾ قُمْ فَأَنذِرْ ﴿٢﴾

“Ewe uliyejigubika! Simama uonye.” (74:1 – 2),

عَجَبًا أَنْ أَوْحَيْنَا إِلَىٰ رَجُلٍ مِّنْهُمْ أَنْ أَنذِرِ النَّاسَ وَبَشِّرِ الَّذِينَ آمَنُوا ﴿٢﴾

“Kwamba tumempa wahyi mmoja wao, kuwa uwaonye watu na uwape bishara wale walioamini.” Juz. 11 (10:2).

Amehusisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja jamaa wa Mtume(s.a.w.w) , kwa sababu mwenye kutaka kutengeneza kwanza anajianza yeye mwenyewe, kisha jamaa zake, ndio wafuatie wengine. Jamaa zake wakimsadiki na kumwamini watamsaidia kueneza mwito wake.

Maneno ya Waislamu yamekuwa mengi kuhusiana na Aya hii. Jamaa katika Sunni wamesema kuwa iliposhuka Aya hii Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alisema: “Ewe Fatima bint Muhammad! Ewe Swafiya bint Abdul Muttwalib! Enyi wana wa Abdillah! Fanyeni amali, kwani mimi siwatoshelezei chochote kwa Mwenyezi Mungu.

Shia na jamaa wengie wa kisunni; akiwemo: Ahmad bin Hambal, An-Nasai, As-Suyutwi, Abu Na’im Al-Baghwi, Atha’alabi, mwenye kitabu Assiratul-halabiya, mwenye kitabu Kanzul-u’mmal na wengineo, wamesema kuwa, iliposhuka Aya hii, Mtume(s.a.w.w) aliwaita watu wa ukoo wa Abdul-Muttwalib. Wakati huo walikuwa ni watu arobaini, wakiwemo maami zake: Abu Twalib, Hamza, Abbas na Abu Lahab.

Alikuwa amewaandalia karamu. Baada ya kula na kunywa, akasema: “Enyi wana wa Abdul-Muttwalib! Nimewaletea kheri ya duniani na Akhera na Mwenyezi Mungu ameniamrisha nitoe mwito wa hilo. Basi ni nani atakayenisaidia kwenye jambo hili, awe ndugu yangu, wasii wangu na khalifa wangu kwenu?”

Wakanyamaza wote, isipokuwa Ali(a.s) akasema:“Mimi ewe Nabii wa Mwenyezi Mungu.” Basi akamshika shingoni na akasema: “Hakika huyu ni ndugu yangu, wasii wangu na khalifa wangu kwenu. Basi msikilizeni na mumtii [1]

Tukio hili alilitaja Muhammad Haykal katika kitabu chake Hayatu Muhammad, chapa ya kwanza na akaliondoa katika chapa ya pili.

Abu Hayyan Al-Andalusi katika Bahrul-muhit, anasema: “Zimepokewa Hadith kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuhusiana na hilo.” Anaashiria Hadith zilizomtaja Imam Ali na zile ambazo hazikumtaja. Wala hakuna kupingana baina ya Hadith hizi.

Kwa sababu kuzichanganya pamoja ni jambo linalowezekana na la karibu sana. Mtume(s.a.w.w) aliwaandalia chakula watu arobaini katika jamaa zake na kuwaambia ni nani atakayenisaidia … kisha pia akawaambia mimi siwatoshelezi lolote kwa Mwenyezi Mungu.

Na inamisha bawa lako kwa wanokufuata katika waumini.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 14 (15:88).

Na ikiwa watakuasi basi sema: Mimi ninajitenga mbali na hayo mnayoyafanya.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , awaambie wale jamaa zake aliowaonya. ‘Aliye karibu na Mwenyezi Mungu na Mtume wake ni yule aliyekurubishwa na takua. Na aliye mbali na Mwenyezi Mungu na Mtume wake ni yule aliyewekwa mbali na maasi, kwa namna yoyote atakavyokuwa’

Na mtegemee Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu na uachane nao wakikuasi; wala roho isikutoke juu yao, na uelekee kwa Mwenyezi Mungu peke yake katika mambo yako yote.

Ambaye anakuona unaposimama kwenye tahajjud (Swala za usiku wa manane)na mageuko yako katika wale wanaosujudu.

Shia Imamiyya wanasema kuwa mababa wote wa Mtume walikuwa wakimpwekesha Mwenyezi Mungu. Miongoni mwa dalili zao katika hilo ni Aya hii; walipofasiri mgeuko kwa maana ya mgeuko wake katika migongo ya wanaompwekesha Mungu; yaani kupitia mifupani mwao.

Tamko la Aya linakubaliana na maana haya na pia linakubaliana na tafsiri ya anayesema kuwa Mungu anakuona ukiwa pamoja na wanaoswali. Dhahiri ya mfumo wa maneno inafahamisha tafsiri hii zaidi kuliko ile.

Hakika yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.

Anasikia kauli na anajua siri na vitendo vyote na kuvilipa. Vikiwa ni kheri basi ni kheri na vikiwa ni shari basi ni shari.

هَلْ أُنَبِّئُكُمْ عَلَىٰ مَن تَنَزَّلُ الشَّيَاطِينُ ﴿٢٢١﴾

221. Je niwaambie ambao mashetani wanawashukia?

تَنَزَّلُ عَلَىٰ كُلِّ أَفَّاكٍ أَثِيمٍ ﴿٢٢٢﴾

222. Wanamshukia kila mzushi mkubwa, mwingi wa dhambi.

يُلْقُونَ السَّمْعَ وَأَكْثَرُهُمْ كَاذِبُونَ ﴿٢٢٣﴾

223. Wanawapa masikio na wengi wao ni waongo.

وَالشُّعَرَاءُ يَتَّبِعُهُمُ الْغَاوُونَ ﴿٢٢٤﴾

224. Na washairi ni wapotofu ndio wanaowafuata.

أَلَمْ تَرَ أَنَّهُمْ فِي كُلِّ وَادٍ يَهِيمُونَ ﴿٢٢٥﴾

225. Je huwaoni kwamba wao wanatangatanga katika kila bonde?

وَأَنَّهُمْ يَقُولُونَ مَا لَا يَفْعَلُونَ ﴿٢٢٦﴾

226. Na kwamba wao wanasema wasiyoyatenda?

إِلَّا الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ وَذَكَرُوا اللَّـهَ كَثِيرًا وَانتَصَرُوا مِن بَعْدِ مَا ظُلِمُوا وَسَيَعْلَمُ الَّذِينَ ظَلَمُوا أَيَّ مُنقَلَبٍ يَنقَلِبُونَ ﴿٢٢٧﴾

227. Isipokuwa wale ambao wameaamini na wakatenda mema na wakamtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi na wakajitetea wanapodhulumiwa. Na punde watajua waliodhulumu ni mgeuko gani watakaogeuka.

WASHAIRI WANAFUATWA NA WAPOTOFU

Aya 221 – 227

MAANA

Qur’an inawapiga vita wabatilifu, lakini kabla ya chochote, kwanza inawapiga vita kwa mantiki ya kiakili iliyo salama na inawajadili kwa njia nzuri, huku ikiwalingania kwenye haki kwa hekima na mawaidha mazuri; ikifafanua kwa kila aina ya mfumo na kuwaomba, kwa upole na ulaini kabisa, walete hoja zao:

لَّوْلَا يَأْتُونَ عَلَيْهِم بِسُلْطَانٍ بَيِّنٍ ﴿١٥﴾

“Kwa nini hawawaletei dalili bayana?” Juz. 15 (18:15).

Wanapoleta hoja dhaifu, Qur’an huibatilisha na kubainisha udhaifu uliopo. Washirikina na watu wengi wanaojali masilahi yao tu, wamesema mengi kuhusiana na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) . Miongoni mwa madai yao ni kuwa Qur’an inatokana na shetani na pia kudai kuwa Muhammad(s.a.w.w) ni mshairi. Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawajibu kwa haya yafuatayo:

Je niwaambie ambao mashetani wanawashukia? Wanamshukia kila mzushi mkubwa, mwingi wa dhambi.

Hili ni jibu la kauli yao kuwa Qur’an ni katika wahyi wa shetani. Njia ya kujibu ni kuwa shetani anaingiza wasiwasi na ubatilifu kwa waongo na wenye madhambi mfano wao: “Mashetani watu na majini. Baadhi yao wanawapa wenzao maneno ya kupambapamba kuwahadaa.” Juz. 8 (6:112).

Shetani hana njia kwa wa kweli na waaminifu, kama vile mitume na viongozi wema. Zaidi ya hayo ni kuwa ni kuwa Qur’an ni haki na kheri na mawazo ya shetani ni shari na uzushi.

Wanawapa masikio na wengi wao ni waongo.

Makusudio ya kuwapa masikio hapa ni kuwasikiliza. Wanaosikilizwa ni makafiri. Maana ni kuwa wale ambao wanawasikiliza mashetani na kuchukua kutoka kwao uwongo na ubatilifu ndio makafiri. Na makafiri wengi ni waongo katika mazungumzo yao na kauli zao. Muhammad(s.a.w.w) ni mkweli katika kauli zake zote na vitendo vyake vyote; vipi aambiwe amesikiliza na kupokea kutoka kwa shetani?

Na washairi ni wapotofu ndio wanaowafuata. Je huwaoni kwamba wao wanatangatanga katika kila bonde na kwamba wao wanasema wasiyoyatenda?

Hii ni kuwajibu washirikina waliosema kuwa Muhammad ni mshairi. Njia ya kubainisha ni kuwa kuna tofauti kubwa baina ya washairi na Muhammad kwa njia hizi zifuatazo:

Kwanza : wale waliomfuata Muhammad(s.a.w.w) walimfuata kwa kumwamini na kumwadhimisha. Na pia kumwamini Mwenyezi Mungu wakitarajia biashara isiyofilisika.

Ndio maana walimfidia kwa roho zao na wakapigana na mababa zao na watoto wao kwa ajili yake. Lakini washairi wao wanaishi katika njozi na kufikirika tu. Wakale walisema: “ushairi ni njozi ” wala hakuna anayewafuata hawa isipokuwa wale wanaoelekeana nao.

Pili : washairi wengi hapo zamani walikuwa wakiwasaidia viongozi madhalimu. Mshairi alikuwa akitumia kipawa chake na akili yake kutunga shairi au nyimbo itakayoimbwa mbele ya viongozi madhalimu. Sasa hili ni wapi na wapi na risala ya Muhammad(s.a.w.w) ambayo hiyo yenyewe ni mapinduzi dhidi ya dhulma na ufisadi?

Tatu, kwamba washairi wengi wanasema sana na kutenda kidogo, wala hakiwapi umuhimu kitu isipokuwa hawa na malengo yao tu ndio yanayowapa msukumo yakiwalekeza popote yanapoelekea. Lakini Muhammad(s.a.w.w) yeye hatamki kwa hawa yake wala hafuati isipokuwa wahyi kutoka kwa Mola wake. Sasa vipi ataambiwa ni mshairi:

وَمَا عَلَّمْنَاهُ الشِّعْرَ وَمَا يَنبَغِي لَهُ إِنْ هُوَ إِلَّا ذِكْرٌ وَقُرْآنٌ مُّبِينٌ ﴿٦٩﴾

“Wala hatukumfundisha mashairi, wala hayatakikani kwake. Haukuwa huu ila ni ukumbusho na Qur’an inayobainisha.” (36:69).

Unaweza kuuliza : Je hii haifahamishi kuwa Uislamu unapiga vita mashairi, kutokana na Qur’an kuyashutumu?

Jibu : Hapana! Qur’an haikushutumu shairi kama shairi au washairi kama washairi; isipokuwa imewashutumu washairi wanaoipinga haki na kufuata kombokombo. Ama washairi wanaoelezea matumaini ya wanyonge na kuwa pamoja na wanaodhulumiwa, kuusaidia uadilifu na uhuru wa binadamu na kupinga utaghuti, ujinga na kurudi nyuma, hawa wako katika safu ya wapigania jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu.

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliulizwa unasemaje kuhusu washairi? Akasema: “Hakika muumini ni mpigania jihadi kwa upanga wake na ulimi wake. Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mikononi mwake, wao ni kama kwamba wanarusha mikuki.”

Aina ya mashairi ambayo ni mikuki katika nyoyo za madhalimu ndiyo aliyoikusudia Mtume(s.a.w.w) katika kauli yake: “Hakika katika shairi kuna hekima.” Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Amemfundisha ubainifu.” (55:4).

Hakuna mwenye shaka kuwa ushairi ni fani ya hali ya juu ya ubainifu na fasihi, kama ambavyo ni utajiri wa lugha na hazina yake yenye thamani.

Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawavua washairi wema na wapigania jihadi kwa kusema:

Isipokuwa wale ambao wameaamini na wakatenda mema na wakamtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi na wakajitetea wanapodhulumiwa.

Yaani washairi wakiitetea haki na na watu wake kutokana na wachokozi na maadui na wakautetea uhuru wa ubinadamu na heshima yake.

Hii ni nukuu iliyo wazi kutoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwamba shairi la kimapinduzi dhidi ya dhulma na uonevu ni katika umuhimu wa dini, imani na matendo mema.

Katika maana ya Aya hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t):

لَّا يُحِبُّ اللَّـهُ الْجَهْرَ بِالسُّوءِ مِنَ الْقَوْلِ إِلَّا مَن ظُلِمَ ﴿١٤٨﴾

“Hapendi Mwenyezi Mungu maneno ya kutangaza uovu ila kwa mwenye kudhulumiwa.”

Juz. 6 (4:148).

Na punde watajua waliodhulumu ni mgeuko gani watakaogeuka.

Huu ni ukemeo na kiaga cha mwisho mbaya kwa kila mwenye kudhlumu na kuonea.

Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote na rehema na amani zimshukie Muhammad na kizazi chake kitakatifu.