TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 20324
Pakua: 2432


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 20324 / Pakua: 2432
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Sura Ya Arubaini Na Mmoja: Surat Fussilat. Imeshuka Makka, ina Aya 54.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu

حم ﴿١﴾

1. Haa Mim.

تَنزِيلٌ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ ﴿٢﴾

2. Ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

كِتَابٌ فُصِّلَتْ آيَاتُهُ قُرْآنًا عَرَبِيًّا لِّقَوْمٍ يَعْلَمُونَ ﴿٣﴾

3. Ni Kitabu kilichopambanuliwa Aya zake. Qur’an ya Kiarabu kwa watu wanaojua.

بَشِيرًا وَنَذِيرًا فَأَعْرَضَ أَكْثَرُهُمْ فَهُمْ لَا يَسْمَعُونَ ﴿٤﴾

4. Inayotoa bishara, na inayoonya. Lakini wengi wao wamepuuza; kwa hiyo hawasikii.

وَقَالُوا قُلُوبُنَا فِي أَكِنَّةٍ مِّمَّا تَدْعُونَا إِلَيْهِ وَفِي آذَانِنَا وَقْرٌ وَمِن بَيْنِنَا وَبَيْنِكَ حِجَابٌ فَاعْمَلْ إِنَّنَا عَامِلُونَ ﴿٥﴾

5. Na wakasema: Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayotuitia, na masikio yetu yana uziwi, na baina yetu na wewe kuna pazia. Basi wewe tenda, nasi tunatenda.

قُلْ إِنَّمَا أَنَا بَشَرٌ مِّثْلُكُمْ يُوحَىٰ إِلَيَّ أَنَّمَا إِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ فَاسْتَقِيمُوا إِلَيْهِ وَاسْتَغْفِرُوهُ وَوَيْلٌ لِّلْمُشْرِكِينَ ﴿٦﴾

6. Sema: Hakika mimi ni mtu kama nyinyi; ninapewa wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake maghufira. Na ole wao wanaomshirikisha.

الَّذِينَ لَا يُؤْتُونَ الزَّكَاةَ وَهُم بِالْآخِرَةِ هُمْ كَافِرُونَ ﴿٧﴾

Ambao hawatoi Zaka nao ndio wanaoikataa Akhera

إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَهُمْ أَجْرٌ غَيْرُ مَمْنُونٍ ﴿٨﴾

8. Hakika wale ambao wameamini na wakatenda mema watakuwa na ujira usiosimbuliwa.

KITABU KILICHOPAMBANULIWA

Aya 1 – 8

MAANA

Haa Mim.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1). Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ameianza sura hii kwa kuitaja Qur’ani na kuisifu kwa sifa zifuatazo:

1.Ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

Qur’ani imetoka kwa Mwingi wa kurehemu Mwenye kurehemu, nayo ni rehema kwa walimwengu. Pia aliyeshuka nayo kuileta kwa Muhammad(s.a.w. w ) ni rehema, kwa sababu yeye ni roho mwaminifu. Na Mwenyezi Mungu amemtolea ushahidi Mtume wake mtukufu kuwa yeye “anawahangaikia sana; kwa waumini ni mpole mwenye huruma” Juz. 11 (9:128)

Kwa hiyo basi Qur’ani ni rehema, aliyetumwa kuifikisha kwa Mtume ni rehema, Mtume ni rehema na Yule ambaye ameiteremsha ndiye msingi na chimbuko la rehema. Basi natija ya uhakika ya rehema (huruma) hizi nne ni kuwa mwenye kushikamana na Qur’ani na akaitumia, hushukiwa na mmiminiko wa rehema, na mwenye kuachana nayo, atakuwa ameidhulumu nafsi yake na ameichagulia maangamizi na balaa.

2.Ni Kitabu kilichopambanuliwa Aya zake.

Zinazobainisha halali ya Mwenyezi Mungu, haramu yake, nasaha zake na mawaidha yake, wala hazikumwachia udhuru mwenye kutafuta udhuru na visababu.

3.Qur’ani ya Kiarabu kwa watu wanaojua.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameiteremsha Qur’ani kwa Kiarabu, kwa vile hamtumi Mtume ispokuwa kwa lugha ya watu wake, ili waweze kumfahamu. Ilikuwa hivyo kwa Ibrahim, Tawrat ya Musa na Injil ya Isa(a.s) .

Nabii Muhammad(s.a.w. w ) alimwandikia Kisra, Kaizari, viongozi na wafalme wengineo wasiokuwa wa kiarabu, kwa lugha ya kiarabu, akiwaita kwenye Uislamu. Yametangulia maneno kuhusiana na hilo katika Juz. 12 (12:2) na Juz. 22 (36:1-12) kifungu ‘Mdundo wa ndani katika Qur’ani’.

Vyovyote iwavyo ni kuwa siri ya ukuu wa Qur’ani haiwi kwenye lugha na mfumo peke yake; bali inakuwa katika maana yake na malengo yake ya kudumu yasiyokuwa na mipaka ya kibaguzi, kizazi wala wakati.

4.Inayotoa bishara, na inayoonya.

Qur’ani inampa mtiifu habari njema ya rehema za Mwenyezi Mungu na pepo yake, na inamuonya muasi kwa adhabu ya Mwenyezi Mungu na hasira yake.

Lakini wengi wao wamepuuza; kwa hiyo hawasikii.

Wamepuuza haki kwa ujinga na kung’ang’ania kuiga mababa au tamaa ya manufaa ya haraka haraka; hata kama ni njozi na mawazo tu.

Na wakasema: Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayotuitia, na masikio yetu yana uziwi, na baina yetu na wewe kuna pazia. Basi wewe tenda, nasi tunatenda.”

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) aliwapa, wapenda anasa wakishirikina mwito wa kumwamini Mwenyezi Mungu peke yake na kutumia Kitabu chake, lakini jawabu lao lilikuwa nyoyo zetu zina kizuizi na wewe, na masikio yetu hayakusikilizi na sisi na wewe tuko mbali mbali. Jitahidi utakavyo na utoe vitisho sisi hatutishiki.

Hivi ndivyo yafanyavyo matamanio – yanaua moyo na kupofusha macho na yanatoa uhuru wa ujinga na upotevu.

Sema: Hakika mimi ni mtu kama nyinyi; ninapewa wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake maghufira.

Mataghuti walimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuwa baina yetu na wewe kuna kizuizi, Mwenyezi Mungu akamwamuru Nabii wake mtukufu awaambia, kizuizi hiki na nyinyi kimetokea wapi?

Kwani mimi si ni mtu tu kama nyinyi, kiroho na kimwili, nikifanya manayoyafanya? Je, wahyi ulionijia kuwa mimi na nyinyi tumwamini Mungu mmoja na tusimshirikishe na yeyote, tutubie kwake na twende sawa kwenye njia ya haki na uadilifu, ndio unaniweka mbali na nyinyi? Au hiyo ndio ingekuwa njia bora ya kutuunganisha kwenye heri na takua? Lakini nyinyi mmekataaa ispokuwa upofu tu na upotevu.

Na ole wao wanaomshirikisha ambao hawatoi Zaka nao ndio wanaoikataa Akhera.

Katika tafsir Albahrul-muhit imeelezwa kuwa sura hii imeshuka Makka na sharia ya zaka ya mali ilishuka Madina, kwa hiyo hapa hapana budi kuifasiri zaka kwa maana ya kutoa tu kwa aina yoyote ya heri au kuifasiri kwa maana ya kuitwaharisha nafsi na ushirikina.

Sisi tunaitilia nguvu tafsiri ya kwanza, kwa sababu kama tukifasiri kwa maana ya kutwaharika nafsi na washirikiana tayari wanajulikana kuwa haawakutwaharika na shirk, itakuwa ni kama kufasiri maji kwa maana ya maji. Kwa hiyo maana yanakuwa washirikina wamekusanya mambo mabaya matatu: Ushirikina, kupinga Akhera na ubakhili.

Hakika wale ambao wameamini na wakatenda mema watakuwa na ujira usiosimbuliwa.

Yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawalipa na kuwapa thawabu bila ya kuwasimbulia kwa sababu wao wanastahiki kila ukarimu. Neno kusimbulia tumelifasiri kutokana na neno mann ambalo pia hufasiriwa kwa maana ya kukatika. Kuifasiri Aya kwa maana yoyote kati ya hayo mawili inafaa, lakini tunaona ya kwanza iko karibu zaidi.

قُلْ أَئِنَّكُمْ لَتَكْفُرُونَ بِالَّذِي خَلَقَ الْأَرْضَ فِي يَوْمَيْنِ وَتَجْعَلُونَ لَهُ أَندَادًا ذَٰلِكَ رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٩﴾

9. Sema: Hivyo nyinyi mnamkataa aliyeumba ardhi katika siku mbili, na mnamfanyia washirika? Huyo ndiye Mola wa walimwengu wote.

وَجَعَلَ فِيهَا رَوَاسِيَ مِن فَوْقِهَا وَبَارَكَ فِيهَا وَقَدَّرَ فِيهَا أَقْوَاتَهَا فِي أَرْبَعَةِ أَيَّامٍ سَوَاءً لِّلسَّائِلِينَ ﴿١٠﴾

10. Na akaweka humo milima juu yake na akabarikia humo na akakadiria humo chakula chake katika siku nne. Ni sawa kwa wanaouliza.

ثُمَّ اسْتَوَىٰ إِلَى السَّمَاءِ وَهِيَ دُخَانٌ فَقَالَ لَهَا وَلِلْأَرْضِ ائْتِيَا طَوْعًا أَوْ كَرْهًا قَالَتَا أَتَيْنَا طَائِعِينَ ﴿١١﴾

11. Kisha akaielekea mbingu, na ilikuwa moshi, akaiambia hiyo na ardhi: Njooni, kwa hiari au kwa nguvu! Vyote viwili vikasema: Tumekuja nasi ni watiifu.

فَقَضَاهُنَّ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ فِي يَوْمَيْنِ وَأَوْحَىٰ فِي كُلِّ سَمَاءٍ أَمْرَهَا وَزَيَّنَّا السَّمَاءَ الدُّنْيَا بِمَصَابِيحَ وَحِفْظًا ذَٰلِكَ تَقْدِيرُ الْعَزِيزِ الْعَلِيمِ ﴿١٢﴾

12. Basi akazifanya mbingu saba kwa siku mbili, na akaipangia kila mbingu mambo yake. Na tukaipamba mbingu ya dunia kwa mataa na kwa ulinzi. Hayo ndio makadirio ya Mwenyezi nguvu Mwenye Kujua.

MWENYEZI MUNGU AMEUMBA ARDHI

Aya 9 – 12

MAANA

Sema: Hivyo nyinyi mnamkataa aliyeumba ardhi katika siku mbili, na mnamfanyia washirika? Huyo ndiye Mola wa walimwengu wote.

Kabla ya kuumbwa ulimwengu hakukuwa na wakati wala mahali. Hakukuwa na kitu chochote ispokuwa Mwenyezi Mungu tu mmoja mwenye nguvu.

Kwa hiyo basi makusudio ya siku mbili yatakuwa ni mikupuo miwili au nyakati mbili, kama ilivyosemekana. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:53). Kutokana na haya, tunataja waliyosema baadhi ya wafasiri: “Hakika mfumo wa Qur’ani unatofautiana na mifumo yote.

Inapoashiria suala lolote la kielimu hailionyeshi kama wanavyolionyesha wataalamu wa sayansi kwa ulinganishi na ufafanuzi; huwa mara nyingine hulileta kwa ishara, au alama za siri (code) au kwa kudokeza kwa neno ambalo huenda likampita anayelisikia wakati ule. Lakini inajua kuwa historia na mustakbali utalifafanua neno hilo na kulithibisha kwa uwazi.”

Hakika hii ilikuja mdomoni mwa Ibn Abbas tangu karne 14 zilizopita, pale aliposema: “Msifasiri Qur’ani, zama zitaifasiri” yaani msizame sana katika Aya za kilimwengu (kisayansi), kwa sababu maendeleo ya elimu itafichua siri zake.

Na akaweka humo milima juu yake.

Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَأَلْقَىٰ فِي الْأَرْضِ رَوَاسِيَ أَن تَمِيدَ بِكُمْ ﴿١٥﴾

“Na akaweka katika ardhi milima ili isiyumbe nanyi.” Juz. 14 (16:15)

Na akabarikia humo na akakadiria humo chakula chake katika siku nne. Ni sawa kwa wanaouliza.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alibariki humo mimea, petroli n.k. Makusudio ya kukadiria chakula chake ni kuwa vyote vilivyo katika ardhi viko kwa kiasi cha mahitaji ya waliohai wote, kadiri idadi yao itakavyokuwa.

Kundi la wafasiri wamesema kuwa siku mbili zilizotajwa mwanzo ni kati- ka jumla ya siku nne; yaani kuumbwa ardhi na kukadiriwa chakula chake kulitimia ndani ya siku nne katika siku za Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya wenye kuuliza hapa ni kila mwenye kuhitajia chakula. Na usawa ni kuwa Mwenyezi Mungu hakujaalia manufaa ya ardhi kwa jinsia fulani au taifa fulani tu; bali viumbe wote wako sawa katika riziki yake na fadhila yake. Akipatikana mwenye njaa basi ni kwa dhulma ya mwenye nguvu dhidi ya mnyonge. Tazama Juz. 8 (7:54-56) kifungu ‘Mwenyezi Mungu ameitengeneza ardhi na binadamu akaiharibu’

NINI UFUMBUZI WA TATIZO LA NJAA?

Kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘na akakadiria humo chakula chake,’ tutaashiria kauli ya wale waliosema kuwa sababu ya kwanza ya tatizo la njaa ulimwenguni ni wingi wa watu wanaozidi siku baada ya siku kufikia kutotosha chakula cha ardhi na heri zake; na kwamba hakiendani na ongezeko la uzazi. Kisha wakatofautiana kuhusu njia ya kutatua tatizo hili.

Kuna waliosema ufumbuzi ni vita vya maangamizi vitavyowaua watu wengi ili upatikane uwiano wa idadi ya watu na uzalishaji wa chakula. Fikra hii wameiunga mkono wenye viwanda vya silaha na walanguzi wa vyakula wanaotafuta utajiri kwa kukandamiza mailioni ya watu.

Wengine nao wakasema, kama sio vita basi kuwe na maradhi ya kuambukiza. Kisha ikaenea rai ya tatu ya kupanga uzazi. Hakuna neno kwa rai hii, kwa sababu kupanga uzazi ni haki ya kimaumbile na kisharia kwa kila mtu, kwa sharti ya kupanga kabla ya kupatikana uzazi; yaani kabla ya tone la manii halijatua kwenye mfuko wa uzazi kwa ajili ya kutengeneza mtoto.

Ama ile rai ya kwanza, inatosha tu kuwa haifai kutokana na walioitoa – wafanya biashara ya silaha na wenye mashirika ya kilanguzi kwenye mataifa masikini.

Sababu kubwa ya tatizo la njaa, inatokana na nguvu ya shari kwenye kheri za ardhi na kuzihodhi, anasa za wachache zinazotokana na kuwakandamiza wengi, kuangamiza mazao kwa ajli ya kulinda soko la kupandisha bidhaa, kutupa maelfu ya tani ya kemikali kwenye vijiji na mashamba ya Vietnam na kwengineko na kuielekeza elimu kwenye uzalishaji wa silaha.

Lau elimu ingeelekezwa kwenye uzalishaji wa usalama tu, ingelitosha kuzidi heri za ardhi kwa watu na riziki zingelikuwa kama mchanga. Jarida la UNESCO linaandika utafiti uliosema: Gharama za kombora moja tu kubwa inatosha kujenga Hospitali 75, kila hospitali moja ikiwa na vitanda 100, vikiwa na mahitaji yake yote. Au kutosha kununua majembe 50,000 ya kukokotwa, yanayoweza kulima mamilioni ya heka badala ya kulima makombora ya kuangamiza. Serikali ya Marekani imetumia $ 400, Bilioni kwenye vita vya Vietnam kabla ya kumalizika[3] .

Je, mabilioni yote haya si katika heri za ardhi na baraka zake? Lau yangelitumika katika kilimo si yangelitosha kulima mapori yote na hata bahari na kwenye sayari nyingine? Watu wote ardhini wangeliishi maisha ya raha.

Zaidi ya hayo, lau ingelikuwa kweli kauli ya aliyesema kuwa watu wamezidi mahitaji yao ardhini, maana yake ingelikuwa Mwenyezi Mungu hakupangilia vizuri makadirio na makisio, na kwamba Yeye anakosea mahisabu ya wakazi wa ardhini kila wakati unavyozidi kupita au kuwa Yeye anakosea kukadiria mahitaji ya chakula! Mwenyezi Mungu Mtukufu ametukuka na ametakata na wayasemayo wajinga.

Tatizo la njaa duniani haliwezi kutatuka kwa vita, maradhi ya kuambukiza wala kwa kupanga uzazi. Kutakua na faida gani ya yote haya ikiwa katika watu kuna dhalimu na mwenye kudhulumiwa na mlaji na mwenye kuliwa?

Ufumbuzi pekee wa tatizo hili ni kuondoa vikwazo baina ya mtu na nyenzo za maisha, kuitumia vizuri ardhi kuzalisha chakula na mavazi na kukidhi mahitaji ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kisha akaielekea mbingu, na ilikuwa moshi, akaiambia hiyo na ardhi: Njooni, kwa hiari au kwa nguvu! Vyote viwili vikasema: Tumekuja nasi ni watiifu.

Kusema ‘tumekuja nasi ni watiifu’ ni kinaya cha uweza wa Mwenyezi Mungu na jinsi ulimwengu unavyofuata amri yake. Aya inaashiria kuwa anga kabla ya kuumbwa nyota ilikuwa na kitu kama moshi.

Basi akazifanya mbingu saba kwa siku mbili.

Mbingu saba ni anga za aina saba za ulimwengu na wala sio nyota saba Tazama Juz. 18 (23:12-17). Kifungu ‘maana ya mbingu saba.’ Ama kuhusu siku mbili ni mikupuo miwili au nyakati mbili, kama ilivyosemekana.

Na akaipangia kila mbingu mambo yake.

Yaani ameumba katika kila mbingu nyota na vinginevyo ambavyo anayevijua ni Yeye ti.

Na tukaipamba mbingu ya dunia kwa mataa.

Ambayo ni sayari zinazoangaza kama taa.

Na kwa ulinzi.

Mwenyezi Mungu anazihifadhi sayari katika kuendelea kwake na mfumo mmoja.

Hayo ndio makadirio ya Mwenyezi nguvu, Mwenye Kujua.

‘Hayo’ ni hayo yaliyotangulia ya kuumbwa ardhi na manufaa yake, kuumbwa mbingu na kupambwa kwake na kuhifadhiwa kwake. Hayo hayawi ispokuwa kutoka kwa mwenye uweza anayepangilia vizuri mambo na mwenye ujuzi.

Haya ndio tuliyo nayo katika fahamu na elimu ya kufasiri Aya hizi. Tunayataja kwa kujichunga tukiwa na imani na Mwenyezi Mungu na uweza wake na kwa kila ghaibu aliyoiashiria katika Kitabu chake kwa tamko tusilolijua maana yake kwenye njia yake wala kutambua uhakika wa siri yake.

Kama tukitaka ziada ya maarifa hatupati ispokuwa kunakili kutoka katika vitabu vya wataalamu, ambapo wao hawaleti dalili za kuthibitisha au kukanusha ispokuwa mara chache.

Anayetaka maelezo zaidi ya kauli zao na arejee kwenye kitabu Alkawnul-a’jib (ulimwengu wa ajabu) cha Hafidh Twawqan, Maallah fis samai (Pamoja na Mwenyezi Mungu katika mbingu) cha Ahmad Zakiy na vinginevyo.

10

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

فَإِنْ أَعْرَضُوا فَقُلْ أَنذَرْتُكُمْ صَاعِقَةً مِّثْلَ صَاعِقَةِ عَادٍ وَثَمُودَ ﴿١٣﴾

13. Basi wakipuuza, sema: Nawahadharisha ukelele mfano ukelele wa A’di na Thamudi.

إِذْ جَاءَتْهُمُ الرُّسُلُ مِن بَيْنِ أَيْدِيهِمْ وَمِنْ خَلْفِهِمْ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا اللَّـهَ قَالُوا لَوْ شَاءَ رَبُّنَا لَأَنزَلَ مَلَائِكَةً فَإِنَّا بِمَا أُرْسِلْتُم بِهِ كَافِرُونَ ﴿١٤﴾

14. Walipowafikia Mitume mbele yao na nyuma yao wakawaambia: Msimuabudu ila Mwenyezi Mungu! Wakasema: Angelitaka Mola wetu bila ya shaka angeliwateremsha Malaika. Basi sisi hakika tunayakataa hayo mliyotumwa.

فَأَمَّا عَادٌ فَاسْتَكْبَرُوا فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَقَالُوا مَنْ أَشَدُّ مِنَّا قُوَّةً أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّ اللَّـهَ الَّذِي خَلَقَهُمْ هُوَ أَشَدُّ مِنْهُمْ قُوَّةً وَكَانُوا بِآيَاتِنَا يَجْحَدُونَ ﴿١٥﴾

15. Ama kinaA’di walitakabari katika ardhi bila ya haki, na wakasema: Nani aliye na nguvu zaidi kuliko sisi? Kwani wao hawakuona kwamba Mwenyezi Mungu ambaye amewaumba ni Mwenye nguvu zaidi kuliko wao? Na wao wakawa wanazikataa Ishara zetu!

فَأَرْسَلْنَا عَلَيْهِمْ رِيحًا صَرْصَرًا فِي أَيَّامٍ نَّحِسَاتٍ لِّنُذِيقَهُمْ عَذَابَ الْخِزْيِ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَلَعَذَابُ الْآخِرَةِ أَخْزَىٰ وَهُمْ لَا يُنصَرُونَ ﴿١٦﴾

16. Basi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku za nuhusi, ili tuwaonjeshe adhabu ya kuwahizi katika uhai wa duniani, na bila ya shaka adhabu ya Akhera ina hizaya zaidi, na wala wao hawatanusuriwa.

وَأَمَّا ثَمُودُ فَهَدَيْنَاهُمْ فَاسْتَحَبُّوا الْعَمَىٰ عَلَى الْهُدَىٰ فَأَخَذَتْهُمْ صَاعِقَةُ الْعَذَابِ الْهُونِ بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ ﴿١٧﴾

17. Na ama Thamudi tuliwaongoza, lakini walistahabu upofu kuliko uwongofu. Basi uliwachukua ukelele wa adhabu ya kuwafedhehi kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma

وَنَجَّيْنَا الَّذِينَ آمَنُوا وَكَانُوا يَتَّقُونَ ﴿١٨﴾

18. Na tukawaokoa wale ambao wameamini na wakawa na takua.

NAWAHADHARISHA UKELELE

Aya 13 – 18

MAANA

Basi wakipuuza, sema: Nawahadharisha ukelele mfano ukelele wa A’di na Thamudi. Walipowafikia Mitume mbele yao na nyuma yao wakawaambia: Msimuabudu ila Mwenyezi Mungu!

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) kuhusiana na washirikina wa kiarabu. Mbele yao na nyuma yao ni kinaya cha msisitizo wa mitume na jitihadi zao katika kubashiria na kuonya, na kwamba wao walifuata kila njia kwa ajili ya kuwaongoza wao, lakini shetani akawapambia na akawaingizia dhana yake, pale aliposema:

ثُمَّ لَآتِيَنَّهُم مِّن بَيْنِ أَيْدِيهِمْ وَمِنْ خَلْفِهِمْ وَعَنْ أَيْمَانِهِمْ وَعَن شَمَائِلِهِمْ وَلَا تَجِدُ أَكْثَرَهُمْ شَاكِرِينَ ﴿١٧﴾

“Kisha hakika nitawaendea kwa mbele yao na nyuma yao na kuumeni kwao na kushotoni kwao; wengi katika wao hutawakuta wenye kushukuru.” Juz. 8 (7:17).

Maana ni kuwa, sema ewe Muhammad kumwambia yule anayekukanusha wewe na risala yako kuwa A’d na Thamud waliwakadhibisha waliowalingania kama haya ninayoyalingania – Tawhid, na wakatoa juhudi zao kwa ajili ya uongofu wao.

Lakini walipong’ang’nia kwenye upotevu, Mwenyezi Mungu aliwakamata kwa adhabu ya dunia na Akhera na kwam- ba mimi nawaonya yasije yakawasibu yale yaliyowasibu wao.

Wakasema: Angelitaka Mola wetu bila ya shaka angeliwateremsha Malaika. Basi sisi hakika tunayakataa hayo mliyotumwa.

A’d na Thamud waliwajibu mitume kwa kuwakadhibisha kwa sababu Mwenyezi Mungu, kwa madai yao, hatumi ispokuwa Malaika. Kauli yao hii tumeipinga katika kufasiri Juz. 7 (6:9).

Ama kina A’di walitakabari katika ardhi bila ya haki.

Kauli yake Mwenyezi Mungu: bila ya haki ni katika upande wa kufafanua na kusiitiza tu. Kwa sababu hakuna kiburi cha haki; hasa ikiwa ni kumfanyia kiburi Mwenyezi Mungu.

A’di walifanya kiburi wakawadharau wanyonge na wakasema hakuna yoyote anayetuweza.

Na wakasema: Nani aliye na nguvu zaidi kuliko sisi? Kwani wao hawakuona kwamba Mwenyezi Mungu ambaye amewaumba ni Mwenye nguvu zaidi kuliko wao?

Hili ni wazi, halihitaji dalili. Imam Aliy(a.s) anasema:“Kila mtukufu asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni dhalili, na kila mwenye nguvu asiyekua yeye Mungu ni dhaifu, na kila mfalme asiyekua Yeye ni mmilikiwa, na kila mjuzi asiyekua yeye ni mwanafunzi na kila muweza asiyekua Yeye ni dhaifu.

Na wao wakawa wanazikataa Ishara zetu!

Walizikana dalili za ulimwengu zinazofahamisha umoja wa Mwenyezi Mungu na ukuu wake. Wakasema kila kilichomo ulimwenguni pamoja na mpangilio wake na nidhamu ni kazi ya maumbile.

Basi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku za nuhusi, ili tuwaonjeshe adhabu ya kuwahizi katika uhai wa duniani, na bila ya shaka adhabu ya Akhera ina hizaya zaidi, na wala wao hawatanusuriwa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwadhibu duniani kwa upepo uliokuja na baridi katika siku za mkosi na hizaya, kisha watakamilisha adhabu kali zaidi na ya kufedhehesha huko Akhera kuliko adhabu ya duniani.

Na ama Thamudi tuliwaongoza, lakini walistahabu upofu kuliko uwongofu. Basi uliwachukua ukelele wa adhabu ya kuwafedhehi kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma.

Aya hii ni dalili wazi kwamba mtu ana hiyari wala halazimishwi, kwa sababu inasema Mwenyezi Mungu aliwaongoza Thamud kwenye njia ya uokovu, akawaamrisha kuifuata na akawakataza maasi, akawabainishia njia ya maangamizi akawakataza na kuwahadharisha na mwisho mbaya kama wataifuata, lakini wakaathirika nayo kuliko ya uokovu; ikawa malipo yao ni balaa na hasara.

Na tukawaokoa wale ambao wameamini na wakawa na takua.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaokoa kwa sababu walifuata njia ya uokovu. Yametangulia mazungumzo kuhusu A’di katika Juz.12 (11:50) na kuhusu Thamud katika Juzuu hiyo hiyo na sura hiyo Aya 50.

وَيَوْمَ يُحْشَرُ أَعْدَاءُ اللَّـهِ إِلَى النَّارِ فَهُمْ يُوزَعُونَ ﴿١٩﴾

19. Na siku watakapokusanywa maadui wa Mwenyezi Mungu kwenye Moto, nao watazuiliwa.

حَتَّىٰ إِذَا مَا جَاءُوهَا شَهِدَ عَلَيْهِمْ سَمْعُهُمْ وَأَبْصَارُهُمْ وَجُلُودُهُم بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٢٠﴾

20. Hata watakapoufikia Moto yatawashuhudia masikio yao, na macho yao na ngozi zao kwa waliyokuwa wakiyatenda.

وَقَالُوا لِجُلُودِهِمْ لِمَ شَهِدتُّمْ عَلَيْنَا قَالُوا أَنطَقَنَا اللَّـهُ الَّذِي أَنطَقَ كُلَّ شَيْءٍ وَهُوَ خَلَقَكُمْ أَوَّلَ مَرَّةٍ وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿٢١﴾

21. Na wataziambia ngozi zao: Kwa nini mmetushuhudilia? Zitasema: Ametutamkisha Mwenyezi Mungu ambaye ametamkisha kila kitu! Na Yeye ndiye aliyewaumba mara ya kwanza, na kwake Yeye mtarejeshwa.

وَمَا كُنتُمْ تَسْتَتِرُونَ أَن يَشْهَدَ عَلَيْكُمْ سَمْعُكُمْ وَلَا أَبْصَارُكُمْ وَلَا جُلُودُكُمْ وَلَـٰكِن ظَنَنتُمْ أَنَّ اللَّـهَ لَا يَعْلَمُ كَثِيرًا مِّمَّا تَعْمَلُونَ ﴿٢٢﴾

22. Na hamkuwa wenye kujificha hata masikio yenu, na macho yenu, na ngozi zenu, zisiwashuhudie. Lakini mlidhani kwamba Mwenyezi Mungu hayajui mengi katika mliyokuwa mkiyatenda.

وَذَٰلِكُمْ ظَنُّكُمُ الَّذِي ظَنَنتُم بِرَبِّكُمْ أَرْدَاكُمْ فَأَصْبَحْتُم مِّنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٢٣﴾

23. Na hiyo dhana yenu mliyokuwa mkimdhania Mola wenu, imewaangamiza; na mmekuwa miongoni mwa waliopata hasara.

وَذَٰلِكُمْ ظَنُّكُمُ الَّذِي ظَنَنتُم بِرَبِّكُمْ أَرْدَاكُمْ فَأَصْبَحْتُم مِّنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٢٣﴾

23. Basi wakisubiri Moto ndio makazi yao. Na wakitoa udhuru hawakubaliwi.

MASIKIO YAO NA MACHO YAO YATAWASHUHUDIA

Aya 19 – 24

MAANA

Na siku watakapokusanywa maadui wa Mwenyezi Mungu kwenye Moto, nao watazuiliwa.

Aya hizi tulizo nazo zinaungana na Aya iliyopita inayosema: ‘Basi wakipuuza, sema: nawahadharisha ukelele mfano ukulele wa A’di na Thamudi.’ Yaani pia waambie ewe Muhammad kuwa Malaika wa adhabu watawapeleka wakosefu kwenye Jahannam kwa nidhamu.

Atakayechelewa watamkemea na atakayejaribu kukimbia watamzuia. Makusudio ni kuwa hawana pakukimbia.

Hata watakapoufikia Moto yatawashuhudia masikio yao, na macho yao na ngozi zao kwa waliyokuwa wakiyatenda.

Hakuna kitu Siku ya Mwisho ispokuwa hisabu na malipo. Baadhi ya Aya za Qur’ani, ikiwemo hii tuliyo nayo,zinafahamisha kwamba Mwenyezi Mungu hatamwaadhibu mkosefu siku hiyo mpaka amkinaishe kuwa ana dhambi na anastahili adhabu.

Hii ni miongoni mwa tofauti zilizoko baina ya hakimu wa duniani anayetoa hukumu yake kwa hali yoyote iwayo; awe mwenye kuhukumiwa amekinai kuwa kweli amekosea au la, na hukumu ya Mwenyezi Mungu huko Akhera; ambapo Mwenyezi Mungu kesho hatatoa hukumu mpaka mhukumiwa akinai kuwa anastahili adhabu.

Kwa ajili hii ndio kutakuwa na ushahidi mwingi dhidi ya mkosefu. Wachukuzi wa dini watashuhudia kuwa walimfikishia halali ya Mwenyezi Mungu na haramu yake, Malaika watatoa ushahidi kua aliasi na akafanya jeuri na kitabu cha matendo yake kitasajili kila kauli na kitendo. Ikiwa hatatosheka, ngozi yake itashuhudia kuwa iligusa haramu, kama zina na utangulizi wake, masikio yatatoa ushahidi kuwa yalisikia haki na yakaikataa na macho nayo yatatoa ushahidi kuwa yaliona dalili za umoja wa Mungu yakazikataa na mengineyo.

Aya inaashiria maana ya ndani yakuwa sharti la shahidi ni kutopendelea. Pengine mkosefu anaweza akatuhumu kwamba wafikisha dini na Malaika wanaweza kuwa upande wa Mwenyezi Mungu kwa vile wanafanya mambo kwa amri yake. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t) akaleta ushahidi wa mtu mwenyewe binafsi ili kuondoa tuhuma hii hata kama si ya kweli.

Kuna Hadith isemayo kuwa mja kesho atamwambia Mola wake: Je, hukunikataza dhulma? Atajibiwa: ndio! Basi atasema: Mimi sitakubaliana na ushahidi ispokuwa ushahidi wa nafsi yangu. Basi hapo Mwenyezi Mungu Mtukufu ataviamuru viungo vitoe ushahidi. Mja mwenye dhambi atasema: Potoleeni mbali! Mara ngapi nimewapinga!

Na wataziambia ngozi zao: Kwa nini mmetushuhudilia?

Kauli yao hii inaonyesha kuwa baadhi wa wakosefu hawatakubali ushahidi wa wafikishaji dini na wa Malaika na kwamba wao watafikiria kuwa kukataa kwao huku kutawafaa, lau si Mwenyezi Mungu kuwawekea ushahidi wao wenyewe.

Zitasema: Ametutamkisha Mwenyezi Mungu ambaye ametamkisha kila kitu! Na Yeye ndiye aliyewaumba mara ya kwanza, na kwake Yeye mtarejeshwa.

Viungo vyao duniani vinatamka kwa lugha ya kihali na kushuhudi hekima na mpangilio uliomo duniani kwamba Mwenyezi Mungu ndiye mwanzilishi na mrejeshaji. Na akhera vitatamka hivyo hivyo kwa uwazi kabisa. Wametofautiana wafasiri katika namna ya ushahidi wa viungo kesho.

Kuna wanaosema kuwa kutajitokeza alama za kuonyesha makosa yaliyofanyika. Wengine wakasema kuwa Mwenyezi Mungu atavitamkisha hasa kiuhakika. Hii ndio kauli iliyo wazi, kwa sababu dhahiri ya Aya inaonyesha hivyo, na akili hailikatai hilo.

Na hamkuwa wenye kujificha hata masikio yenu, na macho yenu, na ngozi zenu, zisiwashuhudie. Lakini mlidhani kwamba Mwenyezi Mungu hayajui mengi katika mliyokuwa mkiyatenda.

Makusudio ya kudhani hapa ni kuitakidi. Yaani mliamini enyi wakosefu kuwa mnafanya makosa kujificha mkihofia watu na sio kumhofia Mwenyezi Mungu, kwamba hajui mnayoyafanya kwa kujificha, na kwamba viungo vyenu havitawafichua siku ya hisabu.

Na hiyo dhana yenu mliyokuwa mkimdhania Mola wenu, ime- waangamiza; na mmekuwa miongoni mwa waliopata hasara.

Itikadi ya ubatilifu ndiyo iliyowapeleka kwenye Jahannam na ni mrejeo mabaya. Hii vile vile inalingana na wale wanaoiamini Akhera kinadharia na kuikana kimatendo; pale wanapojificha na watu na hawajifichi na Mwenyezi Mungu.

Bali hawa ni wabaya zaidi kuliko wale wanaopinga ufufuo na uweza wa Mwenyezi Mungu, kwa sababu wamemuasi Mwenyezi Mungu wakiwa na uhakika kuwa yuko nao akisikia na kuona; na kwamba hakifichiki kwake chochote katika mbingu na ardhi.

Basi wakisubiri Moto ndio makazi yao. Na wakitoa udhuru hawakubaliwi.

Wakivumilia moto wakosefu basi ndio sawa na ndio makazi yao wala hawataokoka. Na wakiomba radhi kwa Mwenyezi Mungu hawaridhii.” Na wakiomba msaada watapewa maji kama mafuta yaliyotibuka yanayobabua nyuso. Kinywaji kibaya kilioje na mahali pabaya palioje pa kupumzika!” Juz. 15 (18:29).

وَقَيَّضْنَا لَهُمْ قُرَنَاءَ فَزَيَّنُوا لَهُم مَّا بَيْنَ أَيْدِيهِمْ وَمَا خَلْفَهُمْ وَحَقَّ عَلَيْهِمُ الْقَوْلُ فِي أُمَمٍ قَدْ خَلَتْ مِن قَبْلِهِم مِّنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ إِنَّهُمْ كَانُوا خَاسِرِينَ ﴿٢٥﴾

25. Na tukawawekea marafiki, na wakawapambia yaliyo mbele yao na nyuma yao. na ikawathibitikia kauli wawe pamoja na uma zilizopita kabla yao, miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa ni wenye kuhasirika.

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَا تَسْمَعُوا لِهَـٰذَا الْقُرْآنِ وَالْغَوْا فِيهِ لَعَلَّكُمْ تَغْلِبُونَ ﴿٢٦﴾

26. Na wale ambao wamekufuru walisema: Msiisikilize Qur’ani hii, na timueni zogo, huenda mkashinda.

فَلَنُذِيقَنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا عَذَابًا شَدِيدًا وَلَنَجْزِيَنَّهُمْ أَسْوَأَ الَّذِي كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٢٧﴾

27. Basi wale ambao wamekufuru hapana shaka tutawaonjesha adhabu kali, na hapana shaka tutawalipa malipo ya mabaya zaidi waliyokuwa wakiyafanya.

ذَٰلِكَ جَزَاءُ أَعْدَاءِ اللَّـهِ النَّارُ لَهُمْ فِيهَا دَارُ الْخُلْدِ جَزَاءً بِمَا كَانُوا بِآيَاتِنَا يَجْحَدُونَ ﴿٢٨﴾

28. Hayo ndiyo malipo ya maadui wa Mwenyezi Mungu - Moto! Humo watakuwa na nyumba ya kudumu, ndiyo malipo yao kwa sababu walikuwa wakizikataa Ishara zetu.

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا رَبَّنَا أَرِنَا اللَّذَيْنِ أَضَلَّانَا مِنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ نَجْعَلْهُمَا تَحْتَ أَقْدَامِنَا لِيَكُونَا مِنَ الْأَسْفَلِينَ ﴿٢٩﴾

29. Na wale ambao wamekufuru watasema: Mola wetu! Tuonyeshe waliotupoteza miongoni mwa majini na tuwaweke chini ya miguu yetu, wapate kuwa miongoni mwa walio chini kabisa.

WALIOKUFURU WALISEMA MSISIKILIZE QUR’ANI

Aya 25 – 29

MAANA

Na tukawawekea marafiki, na wakawapambia yaliyo mbele yao na nyuma yao.

Makusudio ya yaliyo mbele yao ni dunia na balaa yake, na ya nyuma yao ni Akhera ambayo kwa wapinzani ni uzushi. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaandalia mataghuti marafiki wabaya wanaowavutia na maovu na kuwaweka mbali na mema.

Unaweza kuuliza : ikiwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyewapangia watakaowahadaa kwenye upotevu na maasi, basi si itakuwa ni dhulma kuwaadhibu na kusema: ‘Basi ikiwathibitikia kauli;’ yaani adhabu.

Jibu : Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewafanyia hivyo baada ya wao wenyewe, kwa uchaguzi wao mbaya, kufuata njia ya upotevu. Hilo amelifafanua Mwenyezi Mungu (s.w.t.) aliposema:

وَمَن يَعْشُ عَن ذِكْرِ الرَّحْمَـٰنِ نُقَيِّضْ لَهُ شَيْطَانًا فَهُوَ لَهُ قَرِينٌ ﴿٣٦﴾

”Anayeyafanyia upofu maneno ya Mwingi wa rehema tunamwekea Shetani kuwa ndiye rafiki yake.” (43:36)

Pia akasema:

فَلَمَّا زَاغُوا أَزَاغَ اللَّـهُ قُلُوبَهُمْ ﴿٥﴾

“Walipopotoka Mwenyezi Mungu alizipotosha nyoyo zao” (61:5).

Hayo yamekwishaelezwa huko nyuma mara kadhaa.

Na ikawathibitikia kauli wawe pamoja na uma zilizopita kabla yao, miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa ni wenye kuhasirika.

Waliasi na wakafanya uovu, wakastahili adhabu, sawa na walivyostahili mfano wao katika umma zilizopita. Aya hii inafahamisha kuwa majini wana umma na vizazi, wana mitume na manabii; na miongoni mwao kuna wema na wengine waovu, sawa na watu.

Na wale ambao wamekufuru walisema: Msiisikilize Qur’ani hii, na timueni zogo, huenda mkashinda.

Mataghuti walishangaa walipoona athari ya Qur’ani na inavyoatwala kwenye nafsi za watu; wakawa wamedangana hawajui wafanye nini baada ya kushindwa kukabili hoja kwa hoja. Kisha wakaafikiana waipige vita kwa mambo yasiyosawa – waipe sifa ya uchawi na vigano na waifanyie vurugu. Wakaona kuwa hiyo ndiyo njia iliyobaki ya kuishinda.

Hii ya kufanya vurugu inafahamisha kukubali kwao kushindwa, na kwamba Qur’ani ni ngome ya Mwenyezi Mungu iliyoshinda fikra zote za bianadamu, wakati wote.

Basi wale ambao wamekufuru hapana shaka tutawaonjesha adhabu kali, na hapana shaka tutawalipa malipo ya mabaya zaidi waliyokuwa wakiyafanya.

Makosa yanagawanyika sehemu mbili: Kuna yale mabaya na yale yaliyo mabaya zaidi. Vile vile malipo kwa sababu:

مَنْ عَمِلَ سَيِّئَةً فَلَا يُجْزَىٰ إِلَّا مِثْلَهَا ﴿٤٠﴾

“Mwenye kutenda uovu hatalipwa ila sawa na huo,” (40:40).

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja mabaya zaidi waliyoyafanya ili kubainisha kuwa malipo nayo yatakuwa mabaya zaidi, sawa na matendo yao.

Hayo ndiyo malipo ya maadui wa Mwenyezi Mungu - Moto! Humo watakuwa na nyumba ya kudumu, ndiyo malipo yao kwa sababu walikuwa wakizikataa Ishara zetu.

Hayo ni ishara ya hayo malipo ya mtendo mabaya zaidi ambayo ni kudumu katika moto wa Jahannam. Kudumu huku, Mwenyezi Mungu amekufanya ni malipo ya kila mpinzani mwenye inadi na mshirikina, mambo ambayo hayana udhuru wowote kabisa.

Ujinga unaweza kuwa ni udhuru, lakini sio katika shirki na kupinga. Kwa sababu dalili za umoja wa Mwenyezi Mungu na utukufu wake hazikujificha, ziko waziwazi. Kuzijua kunahitaji kuangalia kusikokuwa kwa kuiga au kufuata mapenzi ya moyo.

Na wale ambao wamekufuru katika wadhaifuwatasema: Mola wetu! Tuonyeshe waliotupoteza miongoni mwa majini na watu katika wale waliofuatwa,tuwaweke chini ya miguu yetu, wapate kuwa miongoni mwa walio chini kabisa.

Walimuomba Mwenyezi Mungu awaletee wale waliowapoteza katika mashetani watu na majini ili wawakanyage na wawe sehemu ya ndani kabisa ya Jahannam, lakini Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekwishawafanyia mabaya na mabaya zaidi.pale alipomkamata kila mmoja kwa dhambi yake.