MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)50%

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S) Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Imam Husein (A.S)

  • Anza
  • Iliyopita
  • 7 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9564 / Pakua: 3881
Kiwango Kiwango Kiwango
MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

Mwandishi:
Swahili

,MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN(A.S)

KIMEANDIKWA NA: SAYYID ABDUL HUSAIN SHARAFUDDIN

MTARJUMI: MUSABBAH SHABAN

Mtukufu Mtume(s.a.w.w) Amesema:

1. "Ee Allah! Hawa (Ali, Fatima, Hasan na Husain) ndio AhlulBait wangu, basi watoharishe kwa tohari kamili."

2. "Husain anatokana na mimi na mimi ninatokana na Husain..."

3. "Hao (Hasan na Husain) ni maua yangu katika dunia."

4. "Ewe Mwanangu (Husain)! Mwili wako ni mwili wangu na damu yako ni damu yangu;"

5. (Ewe Husain), wewe u Sayyid, mwana wa Sayyid, na ndugu wa Sayyid; wewe u uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu) mwana wa uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu) na ndugu wa uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu); na baba wa uthibitisho tisa ambao wa tisa wao ni Qaim wao ambaye atakuwa al-Mahdi.

6. "Hasan na Husain ni Masayidi wa Vijana wa Peponi."

7. "Ewe Mola wangu! Mpende yule ampendae Husain."

8. "Adhabu atakayoipewa yule mwuaji wa Husain huko Motoni itakuwa sawa na nusu (nzima) ya adhabu yote watakayoipewa wenye dhambi waulimwengu."

9. " Allah hujirafikisha na wale wajirafikishao na Husain yu adui wa wale walio maadui zake."

DIBAJI

Ahlul-Bayt(a.s) Assembly ya Tanzania (ABATA) ina furaha kutoa kitabu kama hicho cha Majlis kwa watu wazungumzao Kiswahili. Allamah Sayyid Saeed Akhtar Rizvi, Mwenyekiti wa ABATA, amekichagua kwa ajili ya madhumuni hiyo kitabu kiitwacho "Muqaddamah al-Majalis al-Fakhirah fi Ma'atim al-Itrah at Tahirah" kilichoandikwa na mwanachuoni mashuhuri wa dini na mtunzi, marehemu Allamah Sayyid Abdul Husain Sharafud-din al-Musawi, wa Jabal Amil (Lebanon).

Shaykh Musabah Shaban Mapinda, wa Dar-es-Salaam, kwa ushauri wa Mwenyekiti wa ABATA amefanya tarjuma ya kitabu hiki kutoka Kiarabu kwenda kwenye Kiswahili, knachoitwa "Maombolezo ya Kifo cha Imam Husain(a.s) ."

Hiki ni kitabu cha pili ambacho kinatolewa na Ahlul-Bayt(a.s) Assembly ya Tanzania; na tunayo furaha kubwa kwa kutoa kitabu cha Majlis ambacho ni cha kwanza katika lugha ya Kiswahili.

Allah Subhanahu wa Ta'ala atoe malipo yake kwa mtunzi, mfasir na wale wote ambao wamesaidia katika uchapishaji wake kwa njia yoyote.

Wa ma Tawfeeqi illa Billah

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN(A.S)

KIMEANDIKWA NA: SAYYID ABDUL HUSAIN SHARAFUDDIN

MAJLIS YA KWANZA

RUHUSA YA KULIA

Hapana shaka kwamba kuwalilia wafu Waumini ni jambo linalofaa katika Uislamu kutokana na dalili ya kitendo cha Mtume(s.a.w.w) kuhusu jambo hilo.

Mtume kulitenda tendo hili kumekaririka mara nyingi na pahala pengi kama ifuatavyo: Mara ya kwanza ni siku alipofariki ami yake na mlezi wake Bwana Abu Talib. Ya pili ni siku alipouawa kishahidi ami yake Mtume Bwana Hamza katika vita ya Uhud. Ya tatu siku alipopata Shahada (kuuawa) Bwana Jaafar Bin Abi Talib na Bwana Zaid Bin Harith na Bwana Abdallah Bin Ruwah, wote hawa waliuawa katika vita ya Muuta. Mara ya pile, ni siku alipofariki Bwana Ibrahim ambaye ni mtoto wake mwenyewe Mtume(s.a.w.w) .

Mtume(s.a.w.w) alimlilia mwanawe huyu kiasi ambacho kilimfanya Bwana Abdurahman bin Auf amwambie Mtume(s.a.w.w) : "Na wewe unalia Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu "?

Bwana Mtume(s.a.w.w) akasema: "Ewe mwana wa Auf hiyo ni alama ya huruma ".

Kisha Mtume akaendelea kulia na akasema: "Hakika jicho Iinatoa machozi na moyo unahuzinika, wala hatusemi isipokuwa yale anayoyaridhia Mola wetu, na hakika sisi kutengana nawe ewe Ibrahim Wallahi tunahuzunika . "

Na mara ya tano, ni siku Mtume(s.a.w.w) alipozuru kaburi Ia mama yake Bibi Amina, alilia kiasi cha kuwaliza watu waliokuwa karibu yake.

Vitabu vinavyoashiria juu ya Mtume kuwalilia wafu ni vingi mno idadi yake siyo rahisi kuidhibiti.

Kadhalika mapokezi ya kauli ya Mtume(s.a.w.w) na kukiri kwake juu ya kufaa kulia kwa ajili ya wafu ni mengi. Mojawapo ni siku alipopata Shahada Bwana Jaafar bin Abi Talib (At-Tayyaar), Mtume(s.a.w.w) alikwenda kwa mkewe (Jaafar) Bibi Asmaa bint Umais ili kumpa faraja, naye Bibi Fatma aliingia pahala hapo huku analia na kusema: "Ewe Ami yangu". Basi Mtume(s.a.w.w) akasema:

"Na walie wenye kulia kuwalilia mashujaa mfano wa Jaafar ."

Siku nyingine aliyowakubalia watu kuwalilia wafu ni siku alipofariki Ruqaiya binti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , wanawake wakawa wanamlilia (Ruqaiya), basi Omar bin Al-Khatab akawa anawapiga kwa bakora yake, pamoja na kwamba Mtume alikwishawakubalia kulia, basi Mtume(s.a.w.w) akamwambia Omari: "Waache walie " kisha Mtume akasema: "Vyovyote iwavyo, huzuni itokayo Moyoni na jicho kulia, hayo ni kwa ajili ya huruma, ameyaweka Mwenyezi Mungu ".

Pia kuna siku lilipitishwa jeneza mbele ya Mtume(s.a.w.w) ili-hali kuna wanawake wanalia, Omar akawakemea, Mtume akamwambia Omar: "Waache walie ewe Omar kwani nafsi huhuzunika na jicho hutoa machozi ".

Mapokezi ya hadithi kuhusu jambo hili yako mengi kiasi ambacho hatuna nafasi ya kuyakamilisha yote, lakini itoshe kwamba Nabii Yaaqub bin Is-haq bin Ibrahim alimlilia mwanawe Yusufu pale Mwenyezi Mungu alipomuondosha Yusuf machoni pake na akasema (alipokuwa akilia): "Oh majonzi yangu kwa Yusufu! Na macho yake yakawa meupe kwa huzuni naye alikuwa amejawa na huzuni ." Qur'an 12:84.

Kutokana na kilio cha Yaaqub imefikia hadi kusemwa kwamba, "Hayakukauka macho yake (kwa kulia) tangu alipotengana na Yusuf(a.s) mpaka alipokuja kukutana naye, ukiwa umepita muda wa miaka themanini. [1]

Basi je palikuwa na nani aIiyebora mbele ya Mwenyezi Mungu katika zama hizo kuliko Nabii Yaaqub?

Imepokewa kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kwamba yeye Mtume alimuuliza Jibril(a.s) yalifikia kiasi gani majonzi ya Yaquub alipokuwa akimlilia mwanae"? Jibril akaseama: Yalifikia kiasi cha majonzi ya wanawake sabini waliopotelewa na watoto wao.

Mtume akasema: "Je alipata malipo kiasi gani?" Jibril akasema: "Alipata ujira wa mashahidi mia moja.. " [2]

Mimi nasema: "Basi ni mtu gani atakayechukizwa na madhehebu yetu sisi (Shia Ithnashari) katika suala Ia kulia tokana na huzuni, baada ya kuwa jambo hili limethibiti toka kwa Manabii. Ni nani anayechukizwa na mila ya Ibrahim? Hakuna, Isipokuwa yule anayeitia nafsi yake katika upumbavu. Qur'an, 2:130.

Kwa hakika sera ya Maimamu juu ya maombolezo na kulia iliendelea zama baada ya zama, na wakawaamuru wafuasi wao kudumisha mikusanyiko ya huzuni juu ya Imam Husein(a.s) .

Amesema Imam Jaafar As-Sadiq(a.s) : "Hakika Ali bin Husein(a.s) alimlilia baba yake maisha yake yote, hapakuwekwa chakula mbele yake ila hulia, na wala hakuletewa kinywaji isipokuwa hulia.

Kutokana na kulia kwake huko, mmoja wa wafuasi wake alimwambia: "Mimi niwefidia kwako, acha kulia hakika nachelea kwamba utakuwa miaongoni mwa wenye kuangamia kwa kulia sana".

Imam Ali bin Husein (Zainul Abidina) akajibu: "Hapana jambo lolote (linaloniliza sana) isipokuwa mimi nashitakia huzuni zangu kwa Mwenyezi Mungu nami nayajua yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ambayo ninyi hamuyajui ".

Na katika mapokezi mengine Imam Ali bin Husein alisema kumwambia mmoja katika wafuasi wake, "Ole wako hakika Yaaqub(a.s) alikuwa na watoto kumi na wawili, macho yake yalibadilika na kuwa meupe kwa ajili ya kulia sana (kumlilia Yusuf) na mgongo wake ulipinda kutokana na huzuni nyingi, hali yakuwa mwanawe yu hai hapa duniani, lakini mimi nalia sana kiasi hiki kwa sababu niliwaona na kuwashuhudia, baba yangu (Imam Husein), ndugu zangu, ami zangu na watu kumi na saba miongoni mwa watu wa nyumba yangu wakiwa wamenizunguka hali wamechinjwa!"

Pia Imam Ali bin Husein alikuwa kila anapochukuwa chombo ili anywe maji, hulia mpaka chombo kile akakijaza damu.

Akiulizwa kuhusu bali hiyo hujibu: "Basi ni kwa nini nisilie wakati ambapo baba yangu alinyimwa maji ambayo yalikuwa hayana kizuwizi chochote kwa wanyama.........?

Na imepokewa hadithi toka kwa Bwana Rayaan bin Shubaib amesema: "Nilingia nyumbani kwa Imam Ar-Ridha(a.s) katika siku ya kwanza ya Muharram, Imam akaniambia: "Ewe mwana wa Shubaib, hakika Mwezi wa Muharram (Mfungo nne) ni mwezi ambao watu wa zama za Jahiliya (kabla kuja Uislamu) walikuwa wakiharamisha dhulma na mauaji kutokana na utukufu wa Mwezi huu lakini watu wa Ummah huu (wa Kiislamu) hawakuheshimu Utukufu wa Mwezi huu wala heshima ya Mtume wao(s.a.w.w) , kwani walikiua kizazi chake ndani ya Mwezi wa Muharram, na wakawateka wanawake wa kizazi cha Mtume wao, na wakapora vyombo vyao, Ewe mwana wa Shubaib, ikiwa wewe utakuwa ni mwenye kulia, basi mlilie Husein(a.s) kwani yeye alichinjwa kama anayavyochinjwa kondoo, na aliuawa yeye pamoja na watu kumi na nane katika watu wa nyumba yake, ambao hawalinganishwi na ye yote hapa duniani kwa ubora, na kwa hakika Mbingu Saba zililia kwa kuuawa Husein".

Imepokewa hadithi toka kwa Abu Ammarah Al-Munshid amesema: "Hakutajwa Imam Husein(a.s) mbele ya Abu Abdillah As-Sadiq(a.s) katika siku yoyote isipokuwa (siku hiyo) hakuonekana kuwa na furaha mpaka usiku".

Na amesema Abu Ammarah, "Abu Abdillah as-Sadiq alikuwa akisema: Mauaji aliyouliwa Husein(a.s) ni jambo Ia kumpa mazingatio kila Muumini.

Na imepokewa kutoka kwa Imam Jaafar As-Sadiq(a.s) amesema: "Imam Husein(a.s) alisema, mimi nitauawa ili yapatikane mazingatio kutokana na mauaji hayo, hatanikumbuka (kwa kunitaja) Muumini yeyote bali atapata mazingatio.

MAJLIS YA PILl

RUHUSA YA KUOMBOLEZA

Hapana shaka kwamba ipo ruhusa ya kuomboleza vifo vya Waumini, na kwamba jambo hilo ni halali, na hapana dalili iliyo kinyume cha hivi.

Kwa hakika baba yetu Nabii Adam(a.s) aliomboleza kifo cha mwanawe Habil, na maombolezo yakawa yanaendelea mpaka leo kila inapotokea jambo la kifo katika kizazi cha wanaadamu bila upinzani.

Ama Mtume Muhammad(s.a.w.w) aliwaruhusu Masahaba wake kufanya maombolezo kwa wingi kutokana na huzuni, na pia aliruhusu kutaja mema ya waliofariki na kutoa sifa zao katika tabia nzuri na matendo mazuri.

Na wakati Mtume(s.a.w.w) alipofariki, Masahaba walishindana katika kutaja sifa zake walipokuwa wakiomboleza kifo chake.

Katika kifo hicho cha Mtume(s.a.w.w) Bibi Fatma bint wa Mtume(s.a.w.w) pia aliomboleza wazi wazi na kuonesha huzuni yake kwa kusoma beti za Kishairi. [3]

Kadhalika kifo cha Bwana Mtume kiliombolezwa na shangazi yake Mtume(s.a.w.w) Bibi Safia kama inavyoonesha katika Istiiab cha Ibnu Abdil-Bari. Pia lbnu ami yake Mtume Bwana Abu Sufian bin Harith Bin Abdil-Mutalib na Bwana Abu-Dhuarib AlHadh-li, Bwana Abul-Haithami At-Taihani, Ummu Ra-Ala AlQushairiyya na Bwana Amir bin At-Tufail na wengineo wote waliomboleza.[4]

Pamoja na maelezo haya, ili kumkinaisha mtu kuhusu suala la maombolezo yafaa sana kukiangalia na kukisoma kitabu kiitwacho Al Istiiab na pia At-Tabaqat cha Ibn Saad na Usudul Ghaaba na al-Isaba, kwani humo atakuta mambo mengi yanayohusu maomboIezo yaliyofanywa na Masahaba.

Katika Masahaba walioomboleza sana-sana kutokana na vifo ni Sahaba wa Kike Bibi Al-Khinsaa, ambaye aliomboleza vifo vya nduguze wawili, Mabwana Sakhr na Muawiya ambao walikuwa makafiri.

Bibi huyu alikuwa miongoni mwa watu wachamungu kiasi kwamba alitoa wanawe kwa ajili ya kutumikia Uislamu, na wote waliuawa katika njia ya kutumikia Uislamu, kitu ambacho Bibi huyu alikifurahia.

Lakini pamoja na yote hayo hakuacha kuomboleza mauti ya nduguze mpaka alipofariki na wala hakutokea mtu wa kumkemea kwa tendo hilo.

Kwa kifupi suala la kuomboleza ni mashuhuri katika kila zama na kila mahali baina ya Waislamu na wala hawapingani katika hilo.

Sisi tunatosheka na dalili ya kuhalalisha maombolezo yetu tuyafanyayo kama walivyopokea wapokezi wetu kutoka kwa Bwana Zaidi bin As-Shuhaam amesema: "Tulikuwa mbele ya Abu Abdullahi Al-Sadiq(a.s) huku tukiwa na kundi la watu kutoka Al-Kufah, mara akaingia Jaafar bin Af-Fan basi Imam Al- Sadiq akamkaribisha na akamsogeza karibu yake kisha akasema: "Ewe Jaafar nimepata habari kwamba wewe unasoma mashairi juu ya Imam Husein na unayasema vizuri, Jaafar bin Af-Fan akasema: "Ndiyo", Imam Jaafar akasema: "Hebu soma mashairi hayo, nikasoma".

Baada ya Mashairi hayo kusomwa katika hali ya kuomboleza mauaji ya Imam Husein(a.s) , Imam Jaafar Al-Sadiq(a.s) alilia na wakalia watu waliokuwa wamemzunguka kiasi ambacho machozi yalimtiririka usoni mwake hadi kwenye ndevu, kisha Imam akasema: "Ewe Jaafar WalIah wamekushuhudia Malaika Watukufu na wao wanasikiliza maneno yako unapoomboleza kwa ajili ya Imam Husein(a.s) , na kwa hakika wamelia kama tulivyolia sisi na zaidi ya hapo, na Mwenyezi Mungu Mtukufu amefaradhisha kwako Pepo katika muda huu na amekusamehe".

Kisha Imam Jaafar Al-Sadiq akasema kumwambia Jaafar bin Af-Fan, "Je. nikuongezee ubora kwa wenye kuomboleza mauaji ya Imam Husein(a.s) ", akasema Jaafar bin Afan: "Ndiyo Ewe Bwana wangu".

Akasema Imam Jaafar(a.s) : "Hapana yeyote yule atakayesoma Shairi la maombolezo ya Imam Husein(a.s) , na kwa maombolezo hayo akalia na akawaliza wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu atamsamehe na kumuwajibishia kupata Pepo".

Imam Muhammad bin Idris As-Shafii (Imam Shafii) ni miongoni mwa watu waliombeleza mauaji ya Imam Husein(a.s) aliposoma mashairi ambayo tafsiri yake ni kama ifuatavyo:

Ulimwengu ulitingishika kwa ajili ya kuuawa kizazi cha Mtume Muhammad(s.a.w.w) , Milima migumu ilikuwa karibu kuyeyuka kwa ajili ya kuuawa kizazi cha Mtume Muhammad(s.a.w.w) , Milima migumu ilikuwa karibu kuyeyuka kwa ajili ya kuwahuzunikia wao (kizazi cha Mtume), Basi nani atanifikishia barua ya huzuni kwa Husein? Nitaomboleza kifo cha Husein japo nafsi za watu na nyoyo zitachukia. [5]

MAJLIS YA TATU YAH:

KUSOMWA HABARI ZA WALIOKWISHA PITA HAPO KALE

Hapana shaka kuwa, upo mkazo na umuhimu mkubwa kusoma na kueleza habari na sifa za Waumini waliokwisha fariki zamani, na pia kutaja matatizo na misiba iliyowafika katika maisha yao ya kueneza Uislamu. Kwani kuyataja mambo yao huwa sawa kama kuwataja wao katika hali ya uhai wao.

Ummah hunufaika kutokana na utukufu walioupata zinapotajwa sifa zao, pia tabia njema walizokuwa nazo na vitendo vyao vizuri huunufaisha Ummah wa Kiislamu.

Iwapo Ummah utatoa umuhimu wa kusimulia historia ya viongozi wao walio wema ndiyo nafasi bora ya kulinda Utukufu wake na huwa ni muongozo mzuri kwa kizazi kitakachofuata.

Kwa hakika mwendo wa vizazi vya tangu hapo zamani na vile vilivofuatia baadaye, upo katika mtiririko wa kutaja na kukumbuka ubora wa watu waliokufa na misiba iliyowafika kwa njia mbali-mbali, ikiwa ni pamoja na kuyakumbuka hayo kwa njia za uandishi, khutba na utunzi wa mashairi.

Maamuzi sahihi ya akili pamoja na mapokezi sahihi ni vitu ambavyo kimsingi vinatoa mwelekeo wa kuboresha hifadhi ya masimulizi ya watu waliopita.

Kadhalika misingi ya maendeleo na maarifa inalazimisha kuweko kumbukumbu za athari za zamani zenye manufaa kwa jamii.

Ukweli ulivyo ni kwamba uhifadhi wa athari hizo huzifanya roho za watu watukufu ziendelee kuwa hai, na kutokana na kumbukumbu zao hutokea mashindano kwa walio hai ili kujaribu kuzifikia sifa zao na wema wao (Hakika katika kutaja habari za watu waliopita kuna kumbukumbu yenye mazingatio kwa wenye akili). Qur'an 12:111

Angalia kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wake(s.a.w.w) vimeweka wazi sifa za Manabii na matatizo yaliowapata. Pia vimeonyesha bayana jinsi maadui was Mwenyezi Mungu na Manabii wake walivyofedheheka.

Na lau kama si Qur'an na Sunna ya Mtume tusingefahamu Utukufu wa Manabii wa Mwenyezi Mungu, wala tusingejua uovu wa maadui wa Mwenyezi Mungu.

Basi ni vipi hatufahamu kwamba, lau si Qur'an na Sunna kusimamia maelezo ya mafunzo na miongozo ya Mwenyezi Mungu kwa Manabii na waja wa Mwenyezi Mungu, na pia mafunzo ya kuwausia subira kutokana na kero na usumbufu walioupata katika kupigania haki, tungejuaje vituko vya kina Namruda dhidi ya Nabii Ibrahim, na Firaun dhidi ya Musa na wengineo?

Ifahamike wazi kwamba kauli zitolewazo kuharamisha kusomwa na kutajwa ubora wa watu watukufu, na kutaja matatizo yao na misiba iliyowafika ni lazima ziende sambamba na kuharamisha Qur'an na Sunna ya Mtume visisomwe.

Kadhalika ni lazima kauli hizo kama zitakubalika, basi hakutakuwa tena na haja ya somo la historia wala (Ilmu-R-rijal).

Na hakuna mwenye kuridhia upumbavu huu katika nafsi yake akachagua upofu wakati anatambua haki iko wapi.

(Tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na ujinga uliopita kiasi).

Ili kuthibitisha kwamba kuyataja mema ya waliopita ni tendo lililoanza tangu hapo kabla, tunasoma ndani ya vitabu vya historia juu ya matokeo ya mwaka wa arobaini Hijriya kama ifuatavyo:

Alipofariki Imam Ali(a.s) alisimama mwanawe Imam Hasan(a.s) akasema: "Hakika leo mumemuuwa mtu ambaye hajakuweko kabl yake wakumfananisha naye miongoni mwenu, na hatapatikana ye yote baadaye wa kufananishwa naye .[6]

MAJLIS YA NNE

VIKAO KWA AJILI YA KUHUZUNIKIA WAFU

Hapana shaka kwamba Mtume(s.a.w.w) alihuzunika huzuni nyingi kwa ajili ya kufiwa na Ami yake Bwana Abu Talib na Bibi Khadija Ummul-Muuminina(a.s) , kwani wawili hawa walifariki ndani ya mwaka mmoja, na Mutume akauita mwaka huo kuwa ni mwaka wa "huzuni".

Kipindi hiki cha msiba huu mkubwa, Bwana Mtume(s.a.w.w) alipunguza kutoka, ikawa muda mrefu hukaa nyumbani, na ikawa Maquraishi wanapomhujumu huomboleza kwa kusema: "Ewe Ammi yangu imekuwa mapema mno kukukosa ." [7]

Na zimethibiti habari kwamba Mtume alifanya kikao ndani ya Msikiti kwa ajili ya kuwahuzunikia Ibn Ammi yake Jaafar na Zaid pamoja na ibn Ruwaha waliouawa katika vita ya Muuta.

Vile vile imethibiti kuwa yeye Bwana Mtume alihuzunika sana na haikuonekana huzuni namna hiyo kwa Mtume baada ya kuuawa wasomaji wake wa Qur'an, na alifanya Qunut kuwaombea msamaha kwa muda wa mwezi mmoja, na pia akawa huwaapiza katika Qunut hiyo waliowauwa.

Kwa hiyo basi kutokana na dalili hizi utakuta zinatoa maamuzi ya kutia nguvu kuwekwa vikao kwa ajili ya kuonesha huzuni kwa kuwakosa watu wema na wenye kumbukumbu nzuri na ukarimu.

Kwani katika kuwapambanua na makundi mengine, huwa na sababu ya kuwahamasisha watu ili waweze kutokea miongoni mwao wenye mfano kama huo. Pia jambo hilo dhahiri yake ni kuwapa haki yao wanayostahiki baada ya kufa kwao, na hupelekea kuwapata watu wengi watakaoiga mienendo yao.

Ama tukija upande wa kufanya vikao kwa ajili ya kumbukumbu ya Masaibu yaliyowapata Maimamu katika njia ya kuleta amani na sul-hu kwa Ummah, jambo hili hufanya nafsi kuwa na imani na uongofu na kuzifanya nyoyo kuwafuata Maimamu, japo zimekwisha kupita siku nyingi na matukio hayo yalitokea sehemu za mbali.

Na maneno ya wanaolaumu mambo haya, wakasema kwamba haifal kufanya vikao kwa ajili ya kuhuzunikia maiti hasa unapokuwa umepita muda mrefu, hayana maana tunapoizingatia misiba iliyotupata kutokana na mambo waliyofanyiwa watu wa nyumba ya Mtume(s.a.w.w) , kiasi ambacho ukweli maneno yao hayaturudishi nyuma katika kuwahuzunikia watu wa nyumba ya Mtume japo ni muda mrefu umepita, na wala hayaondoi huzuni iliyotokana na misiba hiyo, na wala hayazimi joto la huzuni muda wote.

Je hawaioni hadithi iliyoandikwa na Imam Ahmad bin Hambal katika Musnad yake kwamba, Imam Ali(a.s) alipokuwa akienda Siffin, alipofika Nainawa akawa anasema: "Kuwa na subira Ee Abu Abdillah kuwa na subira Ee Abu Abdillah katika kingo za mto Furat ".

Akaulizwa Imam Ali(a.s) maana ya kusema hivyo, naye akajibu kwa kusema: "Siku moja niliingia kwa Mtume(s.a.w.w) nikamkuta analia, basi nikamuuliza sababu ya kulia kwake akasema: "Hivi punde Jibril alisimama mbele yangu akaniambia kwamba hakika Husein atauawa katika kingo za mto wa Furat, akasema Jibril: Je nikunusishe udongo wa sehemu hiyo? Nikamwambia ndiyo, basi akanyoosha mkono wake akachota gao moja la udongo akanipa ". [8]

Na imepokewa kutoka kwa Bibi Aisha UmmuI-Muuminina kwamba siku moja Husein bin Ali(a.s) aliingia nyumbani kwa Mtume(s.a.w.w) hali ya kuwa Mtume anapokeya Wahyi, basi Jibril akasema: "Hakika Ummah wako wataingia katika fitna baada yako na watamuuwa mwanao huyu (Husein a.s), na (Jibril a.s) akanyoosha mkono wake akachukua udongo mweupe na akasema katika ardhi ya udongo huu atauawa mwanao ."

Basi Jibril alipoondoka Mtume wa Mwenyezi Mungu alitoka nje hadi kwa Sahaba zake wakiwemo Abubakar na Umar and Ali na Hudhaifa, Ammar na Abudhar, hali ya kuwa analia, basi wote wakamwambia: "Kitu gani kinakuliza Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu?"

Mtume akasema: "JibriI ameniambia kwamba mwanangu Husein atauawa katika ardhi ya AT-TAF na ameniletea udongo huu akasema kuwa, katika udongo huu ndipo yatakapokuwa malazi yake".

Basi mtu wa kwanza kumlilia Imam Husein katika Ummah huu na wa kwanza kupewa udongo wa malazi ya Imam Husein(a.s) na wa kwanza kuunusa na wa kwanza kuwasomea watu mauaji ya Imam Husein(a.s) katika ardhi ya AT-TAF ni Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) .

Na ni yeye Mtume(s.a.w.w) ndiye wa kwanza aliyewasikilizisha masahaba zake hadith ya mauaji ya Imam Husein(a.s) .

Basi hapana shaka kwamba Masahaba walimliwaza Mtume(s.a.w.w) kutokana na huzuni hiyo na kilio chake (Hakika mnacho kiigizo chema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa yule anayemtaraji Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, na yeyote mwenye kupinga basi hakika Mwenyezi Mungu ni mkwasi Mtukufu). Qur'an 33:21

MAJLIS YA TANO

KUMTOLEA SADAKA MAITI

Hapana shaka kwamba, ni jambo zuri kuwatolea sadaka maiti wa Waumini kwani jambo hilo alilifanya Mtume(s.a.w.w) na akaamuru lifanywe.

Ndani ya sahihi mbili (Bukhari na Muslim) imepokewa toka kwa Bibi Aisha amesema: "Sikupata kumuonea wivu mwanamke ye yote miongoni mwa wakeze Mtume kuliko nilivyomuonea wivu Bibi Khadija ambaye hata sikuwahi kumuona, lakini Mtume alikuwa akimtaja sana (Khadija) na wakati mwingine alikuwa akichinja kondoo na kumkatakata vipande vipande kisha huvipeleka kwa jamaa za Khadija kuwa ni sadaka, basi wakati mwingine nilimuambia Mtume(s.a.w.w) , "Kama kwamba katika Dunia hii hakupata kuweko mwanamke isipokuwa Khadija, basi Mtume husema hakika alikuwa ni mwanamke wa pekee bora (katika wake nilioowa) na wala hajakuwepo wa mfano wake na kwake yeye Khadija nilipata watoto". [9]

Hadithi hii inatuonyesha kwamba ni jambo zuri kutowa sadaka kwa marafiki au jamaa wa maiti.

Naye Imam Muslim ameandika kwamba, mtu mmoja alifika kwa Mtume(s.a.w.w) akasema: "Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu hakika mama yangu amefariki na wala hakuacha usia, je, atapata malipo iwapo nitamtolea sadaka? Mtume akasema: "Ndiyo ". [10]

KUZALIWA KWA AL-IMAM HUSEIN BIN ALI(A.S)

Al-Imam Husein(a.s) amezaliwa tarehe tano Mwezi wa Shaaban Mwaka wa nne Hijiriyah.

Baada ya kuzaliwa kwake alishuka Jibril(a.s) akiwa na kundi la Malaika wapatao Elfu Moja, wakampongeza Mtume(s.a.w.w) .

Mtume(s.a.w.w) alifurahi sana kwa kuzaliwa kijana huyu, na akawa amempa jina Ia Husein.

Imepokewa kutoka kwa Ummul-Fadhl mkewe Bwana Abbas Bin Abdil-Mutalib amesema; "Niliota ndoto kabla Husein hajazaliwa, nikaona kama kwamba kipande cha nyama ya mwili wa Mtume kimewekwa mapajani mwangu basi nikamsimulia jambo hilo Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mtume akasema: "Naona kuna kheri iwapo ndoto yako itakuwa ya kweli, kwani Fatma atazaa mtoto wa kiume nami nitakupa wewe umlee".

Anaendelea kusimulia Ummul-Fadhli anasema: "Basi mambo yakawa kama alivyosema Mtume(s.a.w.w) na akanipa Husein nimlee".

Siku moja nikaja naye kwa Mtume(s.a.w.w) , wakati Mtume(s.a.w.w) akiwa anambusu Husein, alikojoa na likaruka tone la mkojo kwenye nguo ya Mtume(s.a.w.w) nikamshika Husein (a.s) ili kuepusha asizikojolee nguo za Mtume(s.a.w.w) , Husein(a.s) akalia, Mtume akasema katika hali ya kama mwenye kukemea, "Tulia ewe Ummul-Fadhli, nguo yangu itafuliwa lakini umemuumiza mwanangu ."

Ummul-Fadlili anasema: "Nikamuacha Husein mapajani kwa Mtume na nikasimama kwenda kumletea Mtume(s.a.w.w) maji aisafishe nguo yake.

Basi nikaleta maji na nikamkuta Mtume(s.a.w.w) analia, nikamwambia unalia nini ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu?

Mtume(s.a.w.w) akasema: "Hakika Jibril amenijia na kuniambia kwamba Ummati wangu watamuuwa mwanangu huyu basi ole wao, Mwenyezi Mungu asiwafikishie shufaa (maombezi) yangu siku ya Qiyama watu watakaomuuwa ."

Al-Imam Husein(a.s) alipotimiza mwaka mmoja tangu kuzaliwa kwake, walimshukia Mtume(s.a.w.w) Malaika kumi na wawili, nyuso zao nyekundu huku wanalia na wakawa wanamuambia Mtume(s.a.w.w) kwamba: "Hakika mwanao yatampata masaibu yaIiyompata Habil kutoka kwa Qabil, na kwa ajili hiyo atapewa malipo mema kama alivyopewa Habil, na atakayemuuwa atakuwa na dhambi sawa na dhambi za Qabil.

Hapakubakia Malaika huko Mbinguni ila wote walikuwa wakishuka na kuja kumpa pole na kumuomba awe mvumilivu na pia walikuwa wanamfahamisha malipo atakayolipwa Imam Husein(a.s) , si hivyo tu, bali walikuwa wanamuonyesha udongo wa mahali atakapouawa, na Mtume(s.a.w.w) akawa husema: "Ewe Mwenyezi Mungu mpinge atakayempinga na Umlaani atakaye muuwa... "

Alipotimia Imam Husein umri wa miaka miwili Mtume alitoka kufanya safari na katika safari yake hiyo alisimama mahali fulani, basi aliamua kutoendelea na safari yake na mara macho yake yakawa yanabubujika machozi, akaulizwa sababu gani iliyomfanya alie. Mtume(s.a.w.w) akasema: "Jibril ananieleza kuhusu ardhi iliyoko kando ya mto Furat iitwayo "KARBALA" mahala ambapo atauawa mwanangu Husein, sasa hivi ni kama nauona uwanja wa mapambano baina yake na adui zake, pia kama kwamba napaona mahala atapozikwa.

Kisha baadaye Bwana Mtume(s.a.w.w) aliamua kurudi hali ya kuwa mwenye huzuni na majonzi, akapanda katika Mimbari na akatoa khutba huku Hasan na Husein(a.s) wakiwa mikononi mwake.

Alipoteremka kwenye Mimbari akaweka mkono wake wa kulia juu ya kichwa cha Imam Hasan na nikono wa kushoto akauweka kichwani kwa Imam Husein(a.s) akanyanyua kichwa chake mbinguni akasema: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi Muhammad Mja wako na ni Nabii wako na hawa wawili (Hasan na Husein) ni watu bora katika familia yangu na ni wabora katika kizazi changu na atakuwa mbora mtu atakayewafuata hawa katika Ummati wangu, na hakika Jibril ameniambia kwamba mwanangu huyu atapingwa na atauawa. Ewe Mola mpe baraka nyingi atakapouawa na umfanye awe miongoni mwa Mabwana wa Mashahidi. Ewe Mwenyezi Mungu usimbariki atakayemuuwa na atakayempinga."

Basi baada ya maneno hayo watu wakaangua kilio Msikitini, kisha Mtume akatoa tena khutba nyingine fupi hali yakuwa rangi imembadilika na macho yake yanatoka machozi akasema, "Enyi watu hakika mimi ninawaachia vizito viwili, Kitabu cha Mwenyezi Mungu Mtukufu na Kizazi changu watu wa Nyumba yangu, na hakika viwili hivyo havitatengana mpaka vinifikie katika Haudh, fahamuni kwamba hakika mimi ninavisubiri viwili hivyo, na kwa hakika siwatakeni jambo lolote isipokuwa ni lile aliloniamuru Mola wangu. "Muwapende jamaa zangu". (Kizazi Changu).

Mtume akaendelea kusema: "Fahamuni ya kwamba (siku ya Qiyama) yatanijia makundi matatu katika Ummah huu.

Kundi Ia kwanza litakuwa Ia watu weusi sana, wamezingirwa na Malaika, kisha watasimama mbele yangu nami nitasema: "Ni kina nani nyie"?

"Watashindwa kunitambua, nao watasema: "Sisi ni watu wa Tauhidi mongoni mwa Waarabu.

Basi mimi nitawaambia, "Mimi ndiye Ahmad Nabii wa Waarabu na wasio Waarabu".

Kisha wao watasema: "Sisi ni katika ummati wako".

Nami nitawaambia: "Basi ni vipi mulinifuata katika kizazi changu na katika Kitabu cha Mola Wangu".

Watanijibu: "Ama kitabu tulikipuuza na kizazi chako tulikiangamiza kwa kuwauwa".

Basi nitageuza uso wangu, nao watarudi wakiwa na kiu kali hali ya kuwa nyuso zao ni nyeusi.

Kisha litanijia kundi jingine jeusi mao kuliko lile la mwanzo nami nitawaambia: "Vipi mulinifuata katika vizito viwili, kile kikubwa na kile kidogo, yaani Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Kizazi changu"?

Basi hao watasema: "Ama kile kikubwa (Qur'an) tulikipinga, na ama kile kidogo tulikinyanyasa na kukitawanya ovyo ovyo".

Basi nitawaambia niondokeeni mbele yangu hapo wataondoka hali wakiwa na kiu kali makoo yamewakauka na nyuso zao nyeusi.

Baadaye litanijia kundi jingine Ia watu ambao nyuso zao zinangara kwa nuru.

Basi nami nitawauliza, "Ni kina nani ninyi?"

Watasema: "Sisi ndiyo watu wa neno Ia Tauhidi na Uchamungu, sisi ni Ummati wa Muhammad Mteule, nasi ndiyo bora katika watu wa haki, tulikilinda vema Kitabu cha Mola wetu, tukaihalalisha halali iliyohalalishwa na Kitabu na tukaiharamisha haramu iliyoharamishwa na Kitabu, na tuliwapenda kizazi cha Nabii wetu".

Basi nitawaambia: "Furahini hakika mimi ndiye Nabii wenu Muhammad(s.a.w.w) na hakika ninyi duniani muliishi kama hivyo mlivyontajia."

Basi hapo nitawanywesha maji kutoka ndani ya Haudhi langu (alilonipa Mwenyezi Mungu) nao watarejea bali ya kuwa kiu imewakatika tena watakuwa na furaha, na baadaye wataingia peponi waishi humo milele na milele.

KUTHIBITI UIMAM KWA HUSEIN(A.S)

Ulithibiti Uimamu kwa Imam Husein(a.s) baada ya kufariki kwa nduguye Al-Imam Hasan bin Ali bin Abi Talib(a.s) na hapo ikawa ni faradhi kwa viumbe wote kumtii Imam Husein(a.s) .

Na Uimamu wake ulikuwa ni kwa mujibu wa kauli ya baba yake na babu yake(a.s) na pia usia wa nduguye Imam Hasan(a.s) .

Imam Hasan na Imam Husein(a.s) wao ni Mabwana wa vijana wa peponi kwa mujibu wa Mwenyewe Mtume wa Mwenyezi Mungu ambaye ni babu yao.

Miongoni mwa ubora waliokuwa nao Imam Hasan na Imam Husein(a.s) , baada ya kuwa ni wajukuu wa Mtume(s.a.w.w) na vipenzi vyake katika watu wa nyumba yake, pia ni miongoni mwa watu aliotokanao kwenda kuapizana na wakristo wa Najran pale iliposhuka aya ya 61 Sura ya Tatu:

"Basi watakaokuhoji kuhusu Nabii Issa, baada ya kukufikia ujuzi (wa-jambo hili) basi waambie njooni tuwaite watoto wetu na watoto wenu na wanawake wetu na wanawake wenu na sisi wenyewe na ninyi, kisha tuapizane tuombe laana ya Mwenyezi Mungu iwashukie waongo ".

Aya hii inaitwa aya ya Mubahala, na sababu ya kushuka kwake, ni pale viongozi wa Kikristo kutoka Najran walipokuja Madina katika mwaka wa tisa Hijiriya kumjadili Bwana Mtume(s.a.w.w) kuhusu Nabii Isa(a.s) Mtume akawajibu kwamba; "Hakika mfano wa Isa mbele ya Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa Adam ".

Wakristo hao waliendelea kumjadili Mtume(s.a.w.w) hata baada ya jibu hili, ndipo Mwenyezi Mungu aliposhusha aya hii ya 61 Sura ya Tatu, Mtume akaambiwa kama wataendelea kumhoji, basi awaambie waje waapizane kama ilivyoashiria aya hiyo.

Kutokana na uzito wa suala la kuapizana baina ya Mtume(s.a.w.w) na Wakristo hao, ilibidi Bwana Mtume(s.a.w.w) kwa upande wa Waislamu atoke na watu ambao pia watakuwa na uzito wa kukabili maapizano hayo.

Ndipo alipowachukua Hasan na Husein kama wawakilishi wa watoto wa Kiislamu, na Bi Fatma(a.s) kama muwakilishi upande wa wanawake wa Kiislamu na yeye Mtume(s.a.w.w) na Imam Ali(a.s) wakawa ndiyo nafsi za Waislamu.

Kwa mujibu wa uwakilishi wa Imam Hasan na Imam Husein(a.s) katika tukio hili unadhihiri ubora na utukufu wa vijana hawa wawili ndani ya Uislamu, na inamuwajibikia kila Muislamu kuitambua heshima yao na daraja waliyopewa na Mwenyezi Mungu, kama ambavyo Kiongozi Mkuu wa Wakristo hao kutoka Najran alivyokiri ubora na utukufu uliomo ndani ya nyumba ya Mtume(s.a.w.w) siku hiyo ya mapinzano akasema: Hakika mimi naziona nyuso za watu ambao lau watamuomba Mwenyezi Mungu auondoe mlima mahala ulipo atauondoa, hivyo basi musiapizane nao mtaangmia na hatabakia Mkristo yeyote ulimwenguni baada ya leo".

Pia miongoni mwa hoja zilizowazi kuhusiana na utukufu walio kuwa nao Imam Hasan na Imam Husein ni kuteremka aya zinazothibitisha kuwa wao ni katika watu watakaoingia Peponi hali ya kuwa bado wakiwa ni vijana wadogo, na jambo hili linapatikana katika Surat Ad-Dahr kuanzia aya ya saba mpaka aya ya kumi na mbili.

Kabla ya kuzitaja aya hizo ni bora kukisimulia kisa cha kushuka aya hizo japo kwa mukhtasar.

Imepokewa kwa Ibn Abbas kwamba, Hasan na Husein(a.s) waliugua. Basi Mtume na baadhi ya watu wakenda kuwaona, watu hao wakamwambia Imam Ali(a.s) "Lau utaweka nadhiri itakuwa bora ".

Imam Ali, Bi Fatma(a.s) na Mjakazi wao aliyekuwa akiitwa Fiza, wakaweka nadhiri ya kufunga siku tatu ikiwa Hasan na Husein watapona.

Vijana hawa wawili walipona na ikawa kipindi cha kutekeleza ile nadhiri kimefika, lakini ndani ya Nyumba hamkuwa na kitu.

Hivyo Imam Ali(a.s) alikwenda kwa Myahudi mmoja aliyekuwa akiitwa Sham-uun na akakopa vibaba vitatu vya shayiri.

Bi Fatma(a.s) akaisaga shayiri hiyo na akaoka mikate mitano kwa ajili ya kufuturu kulingana na idadi yao katika nyumba yao.

Chakula hicho kilipowekwa ili waanze kula, alibisha hodi mgeni na akawatolea salam akasema:

"Asalaam Alaikum enyi watu wa Nyumba ya Mtume, mimi ni Masikini wa Kiislamu naomba munipe chakula, nanyi Mwenyezi Mungu atakulisheni chakula cha Peponi ".[11]

Basi wakamuonea huruma wakampa chakula chote, nao wakanywa maji kisha wakalala.

Asubuhi wakaamka na saumu na jioni mwana Fatma aliandaa tena mikate na ilipowekwa tayari kufuturu alibisha hodi yatima na kuomba chakula, wakampa na wao wakanywa maji kisha wakalala.

Asubuhi waliamka na saumu, kisha jioni Bi Fatma alioka tena mikate mitano kwa ajili ya kufuturu.

Walipoketi kufuturu alibisha hodi mtu aliyekuwa mateka akaomba chakula wakampa mikate yote kisha wakanywa maji wakalala.

Kwa ajili ya wao kujinyima kwa muda huo wa siku tatu mfulululizo ndipo ziliposhuka aya zifuatazo katika Sura Ad-Dahr "Wanaotekeleza nadhiri (zao) wanaiogopa siku ambayo shari yake itaenea na wanawalisha chakula masikini na yatima na mateka hali wao pia wanakitaka chakula hicho. (nao husema watoapo chakula hicho) tunakulisheni kwa ajili ya kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, hatutaki kwenu malipo wala shukurani. Hakika tunaogopa kwa Mola wetu siku hiyo yenye taabu na shida. Basi Mwenyezi Mungu atawalinda na shari ya siku hiyo na kuwakutanisha na neema na furaha. Na atawalipa kwa kuwapa Bustani (Pepo) na (Mavazi) ya hariri kutokana na kusubiri kwao.

Zaidi ya hayo ni kwamba Bwana Mtume(s.a.w.w) alidhihirisha wazi Uimamu wao kwa Ummah wake pale aliposema: "Wanangu hawa (Hasan na Husein) ni Maimamu wawe wima au wawe wamekaa ".

Mlolongo wa uimamu wa Maimamu wetu umekuja kwa kila mmoja kumbainisha atakayechukua nafasi ya Imam anayeondoka.

Na jambo hili Ia kubainisha Imamu anayefuata IiIianzia kwa mwenyewe Bwana Mtume(s.a.w.w) kumbainisha Imam Ali(a.s) katika bonde Ia Khum pale alipokuwa akitoka katika Hija ya mwisho. (Mwenye kutaka ziada kuhusu jambo la Uimamu wa Ali bin Abi Talib(a.s) atizame vitabu vya hadithi za Mtume na vitabu vya Historia vinavyotegemewa usahihi wake atalikuta liko wazi). Naye Imam Ali(a.s) alimbainisha Imam Hasan kuwa ndiye atakaye chukua nafasi yake, naye Imam Hasan alimbainisha nduguye Husein(a.s) kuwa ndiyo Imam wa haki baada yake.

Lakini kwa bahati mbaya sana siyo Imam Ali wala Imam Hasan na Husein(a.s) aliyepata fursa ya kuongoza Ummah kama ilivyotarajiwa.

Na hii ilitokana na hali iliyowasibu watukufu hawa baada ya Mtume kuondoka.

Tukimuangalia Imam Husein unakuta matatizo yaliyomkuta ni kama yale yaliyomkuta baba yake hata akasema lmamu Ali kama ifuatavyo: "Nikawa nafikiri baina ya kuwa niupate (Ukhalifa) kwa kuuvuta kwa nguvu au nivumilie uvumilivu wa vipofu wasiojua kitu" Mpaka alifikia kusema, "Basi nikaamua kuvumilia hali ya kuwa jichoni mwangu mna mchanga, na katika koo langu mna dukuduku, nauona urithi wangu umechukuliwa kwa nguvu".

Kwa mwendo kama huu, ndivyo alivyofanya Imam Hasan(a.s) katika siku za uhasama wa Bani Umayya, pindi Mu'awiya bin Abi Sufiyan alipotwaa madaraka ya Ukhalifa kwa nguvu.

Lakini ifahamike wazi sera ya Maimamu wetu kuwa ni sera ya Mtume(s.a.w.w) kwani taabu ilimpata Mtume mwanzo wa kubashiria Uislamu, hakupata utulivu kila alipokuwa akiwaita watu kwenye Uislamu.

Kwa hiyo hali ya Mawasii wake baada yake ni kama ilivyokuwa kwake Mtume(s.a.w.w) hasa itakapokumbukwa kwamba, Maquraishi walipata kumtenga Bwana Mtume(s.a.w.w) na baadaye akalazimika kujificha pangoni wakati akihama Makkah kwenda Madina.

Hali ya matatizo na usumbufu, kama ilivyowapata Manabii ndivyo ilivyokuwa kwa Maimamu.

Muawiyyah bin Abi Sufiyani alipofariki na hali ya vita ikawa imemalizika, hali ambayo ilikuwa ikimzuia Imam Husein(a.s)

kujitangaza Uimamu wake wazi wazi, kipindi hiki walitokea watu wa kumsaidia Imam Husein(a.s) katika kufikisha Ujumbe wa Mwenyezi Mungu, Imam Husein(a.s) alisimama na kujiandaa kufikisha na kusimamia Dini ya Mwenyezi Mungu (s.w.t).

Ili kuanza utekelezaji wa kazi hii, ilimbidi Imam Husein asafiri kutoka Madina kwenda Makkah na hatimaye aelekee Iraq kutokana na wito wa watu wa Al-Kufa waliomtaka aende huko ili akawasaidie na kuwaokoa dhidi ya watawala dhalimu.

Kabla yeye Imam Husein(a.s) kuelekea huko, alimtanguliza Ibn ammi yake Bwana Muslim Bin Aqiil ili akaanze kuwalingania

Dini ya Mwenyezi Mungu na kuchukua kwao baia (kiapo cha utii) kwa niaba ya Imamu Husein(a.s) kwamba watakuwa naye katika Jihadi ya kutetea neno Ia Mwenyezi Mungu, na kuiokoa Dini na Waislamu kutokana na wanafiki waliokuwa wamewakalia Waislainu kwa mabavu.

Muslim Bin Aqiil alipofika huko, watu hao walimpokea na kumuahidi kumsaidia. Lakini haukupita muda mrefu watu hao wakatangua kiapo chao kwa Muslim Bin Aqiil na wakamuacha akauawa mbele yao kifo cha dhulma akiwa ugenini, lakini pia alikufa akiwa ni shahidi.

Na wao hao hao waliomuita Imam Husein wakatoka hapo Al-Kufa kumfuata Imam Husein kwenda kumpiga vita, na wakamtendea mambo ambayo hawakuyatenda Khawarij (Kundi lililomuasi Imamu Ali(a.s) .

Wahinsonga Imam Husein(a.s) , wakamzuia asirudi Makkah wala Madina, wakaweka vizuizi baina yake na maji ya mto Furat mpaka wakamuua hali akiwa na kiu, na wakamdhulumu hali akiwa katika Jihadi, mwenye subira akitaraji radhi za Mola wake.

Hakika ilitenguliwa baia yake na heshima yake ilivunjwa na wala ahadi alizoahidiwa hazikutekelezwa na wakapora mali zake, wakawashika mateka familia yake, wakakidhulumu kizazi cha Mtume(s.a.w.w) hali ya kuwa kimekosa ni mahali gani kitakwenda, njia zote zimefungua.

Kizazi cha Mtume(s.a.w.w) kikawa na huzuni isiyokifani.

1

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN(A.S)

SAFARI YA IMAM HUSEIN(A.S) TOKA MADINA HADI MAKKA

Baada ya Imam Hasan(a.s) kufariki. Mashia waliokuwa Iraq walimuandikia Imam Husein kumjulisha kwamba wao waniempa baia na wako tayari kumnusuru.

Imam(a.s) aliwajibu kwa kusema: "Baina yetu ma Muawiya upo mkataba kuhusu jambo hili, hivyo haifai kuuvunja mkataba huo ".

Katikati ya mwezi wa Rajab mwaka wa Sitini Hijiriyah Muawiyyah Bin Abi Sufian alikufa na Yazid mwanawe Muawiyyah akachukua mahali pa baba yake, na ile ahadi na makubaliano aliyoyafanya Imam Hasan na Muawiyyah yakavunjwa, kwani usia wa Muawiyyah ulitaka Yazid ndiyo awe Khalifa kinyume na makubaliano kwamba atakapokufa Muawiyyah ukhalifa urudishwe katika nyumba ya Mtume(s.a.w.w) .

Basi ilikuwaje alipochukua Ukhalifa Yazid yule mlevi asiyejali utu wake, mcheza na mbwa, hana akijuacho katika dini kama alivyokiri yeye mwenyewe ndani ya ibara ziftuatazo baada ya kukalia Ukhalifa akasema: "...na kwa hakika nimetawazwa baada yake (Muawiyyah) na wala sitowi udhuru (wa kuacha jambo hili) kutokana na ujinga (nilionao) na wala sijisumbui kutafuta elimu ".[12]

Kitabu hiki kinatolewa na Wizara ya Elimu ya Saud Arabia kwa ajili ya shule za kati kwa wasichana ndani ya sahi ya tatu."[13]

Jambo aliloona kwamba ndiyo maslahi kwake yeye Yazid, ni kuandika barua kumpelekea lbn Ami yake Walid bin Utba ambaye alikuwa ndiyo Gavana wa Madina siku hizo, akamuamuru achukue baia kutoka kwa watu wote na kutoka kwa Imam Husein(a.s) kwa niaba yake yeye Yazid, akasema katika barua hiyo "Iwapo Husein(a.s) atakataa kutoa baia basi muuwe na uniletee kichwa chake".

Walid bin Utba alipoipata barua hiyo alimtaka ushauri Marwan.

Marwan akamwambia Walid "Hakika Husein(a.s) hawezi kumbai Yazid, lakini Iau mimi ningekuwa na cheo kama chako ningemuua."

Baadaye Walid alimwita Imam Husein(a.s) , naye akaja kwa Walid akiwa na watu thelathini miongoni mwao wakiwa ni watu wa nyumba yake na wafuasi wake.

Imam Husein(a.s) alipofika mbele ya Walid, yeye Walid akamjulisha Imam(a.s) juu ya kifo cha Muawiyyah na pia akawa anamlazimisha ampe baia Yazid.

Imam Husein(a.s) akamwambia "Hakika kiapo cha utii (baia) siyo jambo la siri, basi kesho waite watu nasi pia tuite (tutafanya hiyo baia).

Marwan akasema kumwambia Walid "Ewe Amir usikubali udhuru wake, kama ni baia atowe sasa hivi au sivyo muuwe."

Imam Husein(a.s) akakasirishwa na maneno ya Marwan akamwambia "Ewe mwana wa Zarqaa unaniuwa wewe au yeye? Hakika wewe ni muongo tena umefanya jambo Ia uovu (Kutamka hivyo)". Kisha Imam akamgeukia Walid akasema: "Kwa yakini sisi ndiyo watu wa Nyumba ya Mtume(s.a.w.w) , na kwetu ndiyo kwenye kituo cha Ujumbe (wa Mwenyezi Mungu) na Mwenyezi Mungu alileta nusra kupitia kwetu sisi na akaukamilisha Ujumbe wake kwa Ulimwengu kwetu sisi, na huyu Yazid ni mtu mlevi, muuwaji wa nafsi bila sababu, anafanya maovu wazi wazi, kwa hiyo basi watu kama mimi hawawezi kumpa baia mtu kama yeye". Kisha Imam Husein(a.s) alitoka mahala hapo akaenda zake.

Marwan akamwambia Walid: "Unaona ulipinga ushauri wangu". (Sasa Husein amekukatalia wazi wazi) Walid akamkemea Marwan akasema: "Kefule!!! Ulilokuwa umenishauri ni jambo la kuniharibia Dunia yangu na Akhera yangu, Wallahi sipendi kuona Dunia yote inakuwa yangu wakati nitakuwa nimemuuwa Husein eti kwa sababu amesema hatombai Yazid, walasidhani kama ye yote atakayemuuwa Husein kwamba atakutana na Mwenyezi Mungu akasalimika, bali mtu huyo atajikuta siku ya Qiyama mizani yake ni nyepesi (hana chochote) na Mwenyezi Mungu hatomtazama mtu huyo wala hatamtakasa na atapata adhabu kali". (kwa kumuuwa Husein).

Basi Imam Husein alikaa Nyumbani kwake usiku huo ambao ulikuwa ni usiku wa kuamkia Jumamosi tarehe 27 Rajab mwaka wa Sitini.

Kulipokucha akatoka ili apate kujua habari zilizoko mjini, mara akakutana na Marwan, kisha Marwan akasema: "Ewe Abu Abdillah (Imam Husein) mimi ninayo nasaha kwa ajili yako tafadhali nitii kwa nitakayokuambia utafanikiwa".

Imam Husein(a.s) akasema: "Ni nasaha gani hiyo sema niisikie"?

Marwan akasema: "Hakika mimi nakuamuru umtii Yazid kwani jambo halo ni bora kwako na ni bora katika Dini yako na Dunia yako".

Imam Husein(a.s) akasema: "Hakika sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na hakika sisi kwake tutarejea, Eti mimi kumtii Yazid ndiyo itakuwa ni amani kwa Uislamu? Hakika Ummah umepata mtihani mkubwa kwa kuwa na kiongozi mfano wa Yazid".

Mazungumzo baina yao yalikuwa mengi kiasi ambacho Marwan aliondoka il-hali kachukia.

Jioni ya Jumamosi Walid alituma watu waende kwa Imam Husein(a.s) ili aje afanye baia.

Imam Husein akawaambia: "Ngojeni kutapokucha kesho kisha mtaona ni lipi la kufanya, nasi pia tutaona la kuamua". Wakanyamaza wala hawakuendelea kumlazimisha afanye baia.

Basi Imam Husein alitoka usiku wa kuamkia Jumapili tarehe 28 Rajab kuelekea Makkah, pamoja na wanawe na ndugu zake na kikundi cha watu wa nyumba yake, akaondoka Madina hali anasoma Aya ya Qur'an isemayo: "Akatoka katika mji huo hali anakhofu, anangoja (lipi litamfika) akasema: "Mola wangu niokowe kutokana na watu madhalimu ". Sura Al-Qasas: 21.

Alipita njia kuu iliyo mashuhuri, akaombwa abadili njia kukwepa kufuatwa na adui kama alivyofanya Ibnuz-Zubair, akakataa kufanya hivyo na akasema: "Sitaiacha njia hii mpaka Mwenyezi Mungu aamuwe chochote atakachoniamulia".

Imam Husein(a.s) alifika Makkah usiku wa kuamkia Ijumaa tarehe tatu Shaaban, na aliingia Makkah huku akisoma Aya ifuatayo:

"Na alipoelekea upande wa Madiyan alisema: Huenda Mola wangu ataniongoza njia iliyo sawa ". Sura Al-Qasas Aya 22.

Alikaa hapo Makka kuanzia Mwezi huo wa Shaaban mpaka mfungo pili na siku nane za Mwezi wa mfungo tatu, kisha aliona usalama wake pale Makka in mdogo.

Kwa hiyo Imam Husein hakuwa na utulivu tena wa kumuwezesha kukamilisha Ibada yake ya Hija kwa kuhofia kukamatwa na majasusi ambao wangemkamata hapo Makka na kumpeleka kwa Yazid Bin Muawiyyah.

Hivyo basi akafungua Ihram yake na akaifanya kuwa ni Umra.

Imam Husein(a.s) akautoka Mji wa Makka ambao in Mji wa Mwenyezi Mungu uliotukuka, katika Mji huo ndege na wanyama wanapewa amani waingiapo, basi vipi kwa mjukuu wa Mtume(s.a.w.w) kutishiwa amani yake?

Alitoka Makka kama alivyo uacha mji Mtukufu wa Madina mji wa babu yake ambaye in Mtume wa Mwenyezi Mungu, hali anakhofu mwenye kungojea lipi litamtokea.

MAJLISI YA SITA

YALIYOTOKEA MAKKA BAADA YA IMAM HUSEIN(A.S) KUFIKA HAPO

Ilipofahamika kwa wakazi wa Makkah kwamba, Imam Husein(a.s) yupo Mjini hapo, wakazi wa Mji huo walianza kumtembelea kwa wingi.

Miongoni mwa watu waliofika kwake ni pamoja na wageni kutoka sehemu mbalimbali waliokuja Makka kufanya Umra.

Ikawa watu wanapishana, hawa wanatoka na wengine wanaingia. Pia Abdallah Bin Abbas na Talha Bin Zubair nao walifika kumuona Imam Husein(a.s) .

Wawili hawa walimtaka Imam Husein(a.s) akae hapo Makkah na anyamaze. (Asijihusishe na mambo ya Ukhaiifa).

Imam aliwajibu akasema, "Hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu aliniamuru jambo ambalo mimi nitalitekeleza ".

Vile vile Abdallah bin Omar bin Khatab alifika kwa Imam Husein(a.s) na kumtaka afanye mapatano na Yazid bin Muawiya bin Abi Sufiyan.

Imam(a.s) alijibu akasema, "Ewe Baba Abdur-Rahman, unafahamu kwamba Dunia hii kwa uovu uliyomo ni pamoja na kuvinyanyasa viumbe vitukufu vya Mwenyezi Mungu, na elewa pia kwamba kichwa cha Mtume Yahya bin Zakariya kilitolewa na kuwa kama zawadi kwa mtu muovu miongoni mwa watu waovu wa Kiban-Israil?" Akaendelea Imam(a.s) kusema, "Je unafahamu kwamba, wana wa Israil walikuwa wakiwauwa manabii sabini katika kipindi cha kuchomoza Al-fajiri na kutoka jua, kisha baada ya kufanya tendo hili, huenda wakakaa sokoni na kufanya biashara zao za kununua na kuuza kama kwamba hawakutenda chochote cha uovu? Lakini Mwenyezi Mungu hakufanya haraka kuwaadhibu kutokana na maovu yao bali baadaye aliwaadhibu adhabu kali, basi muogope Mwenyezi Mungu ewe baba Abdur-Rahman na wala usiache kunisaidia".

Katika mji wa Al-Kufah, habari za kifo cha Muawiyya zilipowafikia watu wa Mji huo pia kutawazwa kwa Yazid kuwa ndiyo Khalifa wao hawakupendezwa.

Na waIipofahamu kuwa Imam Husein amekataa kumpa baia Yazid na kwamba yuko Makkah, Mashia walikusanyika katika nyumba ya bwana Suleiman bin Surd AI-Khuzai.

Walipokamilika Bwana Sulaiman alisimama akasema, "Kwa hakika Muawiyya amekufa na Husein amekataa kuwatii waliotwaa madaraka na ameondoka Madina sasa yuko Makkah, nanyi ndiyo wafuasi wa baba yake basi ikiwa mnajua kwamba mnaowajibu wa kumsaidia na kumpiga adui yake na kuziangamiza nafsi zetu kwa ajili yake muandikieni barua aje, na kama mtaogopa kushindwa basi musimuite mtu huyu".

Wakajibu kwa kusema; "Sisi tuko tayari kutoa nafsi zetu kwa ajili yake na tutampiga adui yake".

Sulaiman akasema, "Basi muandikieni". Wakamuandikia Imam Husein(a.s) .

BISMILLAAH RAHMAN RAHIM

Barua kwa Husein bin Ali(a.s) kutoka kwa Sulaiman bin Surd na Musayib bin Najiya na Rifaat Shadad na Habib bin Mudhhir na Mashia wake Waumini Waislam katika watu wa Al-Kufah.

Amani iwe juu yake, hakika tunamtukuza Mwenyezi Mungu ambaye hapana Mola ila yeye.

Ama Baad:

Sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu ambaye amemuangamiza adui yako aliyekuwa jeuri na mpinzani wa haki huku anaijua.

Adui huyo aliukandamiza Umma huu kwa nguvu, akapora mali za Umma, akautawala Umma hali yakuwa hautaki kutawaliwa naye, kisha akawa anauwa watu wema katika Umma huu na kubakisha watu waovu mali ya Mwenyezi Mungu akaifanya ni ya kutumiwa na matajiri na wakatili, basi na alaaniwe kama walivyolaaniwa watu wa Thamud.

Kwa hakika sisi hatuna kiongozi wa kutuongoza, basi njoo ili Mwenyezi Mungu apate kutuunganisha katika haki kwako wewe.

Na huyu Nuuman (Gavana wa Muawiyya hapo al-Kufah) sisi hatushirikiani naye kwenye Ibaada ya Ijumaa wala hatutoki pamoja naye kwenye sala ya Idi.

Iwapo tutafahamu tu kwamba tayari umeshafika mjini hapa, basi tutamtoa tumrudishe Shamu Insha-Aallah.

Amani iwe juu yako ewe mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na pia amani imshukie Baba yako, wala hapana hila wala nguvu isipokuwa vitoke kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu."

Kisha barua hiyo wakapewa Mabwana Abdallah bin Masmaa Al-Hamadani na Abdallah bin Wail waipeleke Makkah na wakawaamuru kwenda mwendo wa haraka.

Baada ya siku mbili kupita tangu walipotuma barua yao, watu wa Mji wa Al-Kufah waliwatuma Mabwana wafuatao.

1. Qais bin Mas-har As-Saidawi

2. Abdalla na Abdur-Rahman watoto wa Shadad Al-ar-habi.

3. Ammarah bin Abdallah Al-Saluli

Waliwapatia barua zisizopungua mia tano kila mtu.

Baada ya siku mbili tena wakawatuma Mabwana Hani bin Haniy As-Subai na Said bin Abdallah Al-Hanafi waende kwa Imam Husein(a.s) kumpelekea barua iliyokuwa na maneno yafuatayo.

BISMILLAHI RAHMAN RAHIM

Kwa Husein bin Ali(a.s) barua kutoka kwa wafuasi wake miongoni mwa Waumini na Waislamu.

Ama baada salaam:

Njoo haraka, kwa hakika watu wanakusubiri, hawana rai nyingine ila kukusubiri wewe.

Basi fanya haraka tena haraka sana"

Barua kwenda kwa Imam Husein(a.s) zilifuatana mfululizo kiasi cha kufikia barua kumi na mbili alfu.

Pamoja na wingi wa barua na kuhimizwa kote alikohimizwa ndani ya barua hizo, Imam Husein(a.s) alikuwa mzito kuwajibu watu hao.

Siku moja ilitokea zikamfikia barua mia sita wajumbe waliotumwa wote wakakutana kwa Imam Husein katika kipindi hicho hicho.

Imam Husein(a.s) akawauliza kuhusu hali ya watu ilivyo huko watokako, kisha akawaambia mabwana Hani na Said bin Abdallah al-Hanafi, "Hebu niambieni ni kina nani hasa waliojumuika kuniandikia barua hii?

Mabwana hawa wakamfahamisha Imam Husein hali halisi ya watu wa Al-Kufah ilivyo na wakamtajia pia watu wenye msimamo na rai ya kumwita yeye Imam(a.s) .

Basi baada ya kutoshelezwa na maelezo ya mabwana hawa, Imam(a.s) alisimama akaswali rakaa mbili halafu akaandika barua ifuatayo.

BISMILLAAH RAHMAN RAHIM

Barua toka kwa Husein Bin Ali, kwenda kwa Watukufu Waumini na Waislamu.

Ama baad, hakika Hani na Said wamenifikia wakiwa na barua zenu, nao ni watu waliofika mwisho miongoni mwa wajumbe wenu niliowatuma.

Kwa kweli niineyafahamu yote mliyoyaeleza, na jambo muhimu mlilozungumza ni kwamba, "Hakika sisi hatuna kiongozi, basi njoo huenda Mwenyezi Mungu akatuimarisha kwenye haki na uongofu kupitia kwako".

Mimi ninanituma ndugu yangu na ibn ammi yangu naye ni miongoni mwa watu wa nyumba yangu (Muslim bin Aqiil) aje huko. Basi iwapo ataniandikia kuniarifu kuwa rai za viongozi wenu na watu bora miongoni mwenu zimeafikiana kama ambavyo wajumbe wenu walivyonijulisha, na nilivyosoma barua zenu, basi mimi nitakuja huko haraka apendapo Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Kwa Yaqin naapa, "Hawi mtu ni Imam (kiongozi wa haki) ila yule anayehukumu kwa mujibu wa Qur'an, mwenye kusimamia haki, anayeishi kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya haki (Uislamu) mwenye kuifunga nafsi yake katika dhati ya Mwenyezi Mungu.

Wasalaam.

Baada ya kuandika barua hiyo, Imam Husein(a.s) alimwita nduguye Bwana Muslim bin Aqiil na akamtuma aende Al-Kufah, afuatane na mabwana Qais bin Mas-har As-Saidawi, Ammaarah bin Abdallah na Abdallah na Abdur-Rahman watoto wa Shadad Al-Arhabi.

Imam(a.s) akamuusia nduguye kumcha Mwenyezi Mungu na awe mpole pia asizungumze sababu za yeye kwenda huko.

Mwisho alimtaka afanye haraka kwenda, kwani yaonesha watu wameshikamana pamoja juu ya kumtaka Imam Husein(a.s) kwenda huko.

Muslim bin Aqiil aliondoka kuelekea AI-Kufah kupitia Madina, mahala ambapo alipofika, aliingia katika Msikiti wa Mtume(s.a.w.w) akaswali kisha aliwaaga watu wa nyombani kwake na wangine aliopenda kuwaaga. Baada ya hapo aliondoka mpaka Al-Kufah na akafikia katika nyumba ya bwana Mukhtar bin Ubaid At-Thaqafi. Mashia wa Al-Kufah walipopata habari za kuwasili kwa Muslim bin Aqiil, wakawa wanapishana katika nyumba ya Mukhtar ili waonane naye, na kila wakikusanyika kikundi huwasomea barua ya Imam Husein, kitu ambacho kilikuwa kikiwafanya walie.

Wakampa baia Muslim bin Aqiil watu wapatao elfu kumi na nane.

Muslim bin Aqiil alipoiona hali hiyo kutoka kwa watu wa Al-Kufah, alimuandikia Imam Husein(a.s) kumjulisha na kumtaka aende huko.

Mashia waliendelea kumtembelea Muslim bin Aqiil, mpaka Nuuman bin Bashir aliyekuwa Gavana wa Al-Kufah wakati wa Muawiyya na baadaye katika kipindi cha Yazid, akautambua mkusanyiko huo. Pamoja na kutambua hali hiyo, Nuuman bin Bashiri hakumfanyia lolote Ia ubaya Muslim bin Aqiil.

Lakini baada ya muda kupita, Abdallah bin Muslim bin Rabia Al-Hadhrami ambaye alikuwa mfuasi mkubwa wa bani Ummaya, akamuendea Nuuman bin Bashir akamwambia, "Hakika yote uyaonayo yanatendeka hapa hayana mafanikio kwako ila utapoteza madaraka, na msimamo unaouonyesha baina yako na adui yako ni msimamo wa watu wanyonge".

Kisha huyu Abdallah alimuandikia barua Yazid na akamuambia "Hakika Muslim bin Aqiil amefika hapa Al-Kufah, na watu wamempa baia kwa niyaba ya Husein, basi iwapo wewe unaitaka nchi hii ibaki mikononi mwako, mlete mtu imara atakayesimamia maslahi yako, na atafanya vile ambavyo wewe unamfanyia adni yako, kwani Nuuman ni mtu dhaifu au pengine anajifanya dhaifu."

Nao kina Ammarah bin Uqba na Omar bin Saad, kila mmoja alimuandikia Yazid barua mfano wa ile aliyoandika Abdallah.

Barua hizi zilipomfikia Yazid, mara moja akamuandikia Ubaidullah bin Ziyad aliyekuwa Gavana wa Basra akamjulisha kwamba, kuanzia sasa yeye ni Gavana wa al-Kufah na amemkabidhi nchi hiyo.

Kisha Yazid alimjulisha lbn Ziyad Khabari za Muslim bin Aqiil na akamsisitiza kumkamata na hatimaye amuuwe.

Ubaidullahi bin Ziyad aliyelaaniwa, aliondoka haraka kutoka Basra kuelekea Al-Kufah na akamkabidhi madaraka ya hapo Basra nduguye aliyekuwa akiitwa Athuman.

Ubaidullahi aliingia Al-Kufah usiku, na watu wakadhani kuwa ni Imam(a.s) , wakafurahia na kumsogelea. Walipotambua kwamba kumbe ni lbn Ziyad walitawanyika na kumuacha, naye akaenda hadi kwenye jumba la utawala wa bani Umayya akalala mpaka asubuhi.

Kulipokucha alitoka akaanza kutishia na kuonya kwa ukali wale wanaomuunga mkono Muslim bin Aqiil. Muslim bin Aqiil aliposikia habari za vitisho vya Ibn Ziyad akachelea usalama wake na akaenda nyumbani kwa Bwana Hani bin Urwa mahali ambapo alipewa hifadhi.

Baada ya vitisho na maonyo ya ibn Ziyad hali iligeuka ikawa mbaya sana, kiasi cha kuwafanya watu waliokuwa wamempa baia Muslim bin Aqiil wahitilafiane na wakavunja baia yao, wala hawakuthubutu tena kujitokeza kumtetea Muslim bin Aqiil na ahadi yao ya kumsaidia wakashindwa kuitimiza.

Kwa hakika kilikuwa kipindi kigumu kwa Muslim bin Aqiil, kipindi chenye mateso na tishio la kuuawa. Ni wakati mgumu kwa kuwa waliokuwa wamemuahidi kumsaidia na kumhifadhi walimtelekeza. Kutelekezwa alikotelekezwa Muslim bin Aqiil kulitoa nafasi kwa adui yake kuzidisha uovu wake dhidi yake na ikafikia Muslim bin Aqiil kuwa anasakwa kila mahali na kuzinngirwa barabara katika kila upande hali ya kuwa mpweke hana wakumsaidia.

Muslim bin Aqiil alipata mtihani unaowafika watu wema na alivumilia kungoja matokeo kutokana na vitisho vya panga za maadui zake.

MAJLISI YA SABA

YALIYOTOKEA AL-KUFAH BAADA YA IBN ZIYAD KUFIKA HAPO

Ibn Ziyad alipokwisha wasili katika mji wa AI-Kufah, alijiimarisha kwa kutawanya majasusi kufuatilia nyendo za Muslim bin Aqiil. Matokeo ya ujasusi huo yalimfanya yeye lbn Ziyad afahamu kuwa Muslim bin Aqiil yuko katika nyumba ya Bwana Hani.

Kwa hiyo lbn Ziyad aliwaita mabwana Muhammad bin Al Ashath na Hasan bin Asma bin Kharijah na Amru bin Al-Hajaaj akawaambia, "Ni kitu gani kinamfanya Hani asije kwetu (kutusalimia)?"

Wao wakamjibu, "Hatujui lakini inasemekana ni mgonjwa". lbn Ziyad akasema "Habari hizo nazifahamu, lakini pia nafahamu kwamba kesha pona na kwamba yeye mara kwa mara anaonekana mlangoni kwake amekaa, na lau ningefahamu kuwa bado anaumwa bila shaka ningelimtembelea kumjua hali".

Ibn Ziyad aliendelea kuwaambia, "Nendeni mkamwambie asiache kufanya wajibu wake juu ya haki yetu, (kutoa baia) hakika mimi sipendi kuuona ufisadi mbele yangu unaotokana na mtu mtukufu miongoni mwa Waarabu mfano wake yeye Hani".

Ilipokuwa jioni, mabwana hawa wakaenda nyumbani kwa Bwana Hani na wakasimama mbele ya mlango wa nyumba yake wakamwambia, "Ni kitu gani kinachokuzuia usikutane na Amiri (lbn Ziyad) kwani yeye amekutaja na amesema lau ningefahamu kwamba (Hani) anaumwa ningelimtembelea kumjua hali".

Hani akasema, "Ni maradhi ndiyo yanayonizuia nisiende kukutana naye".

Wale mabwana wakasema kumwambia Hani, "Hakika zimeshamfikia habari kwamba wewe kila jioni unakaa mlangoni nyunbani kwako, naye anakuvumilia kwa hilo, na fahamu kuwa mtawala hawezi kuendelea kuwavumilia watu mfano wako, kwani wewe ni kiongozi wa watu wako, nasi tunakuapia ukweli ulivyo twende pamoja mpaka kwa Ibn Ziyad".

Waliendelea kujadiliana naye mpaka wakamshinda, kisha aliagiza mavazi yake akavaa na hatimaye akaomba aletewe nyumbu wake akapanda na wakaondoka. Walipolisogelea jumba Ia Ibn Ziyad Hani alihisi kutatokea mambo ambayo si mazuri kwake kama ambavyo tangu mwanzo alikuwa akihisi hivyo. Hani akamwambia Hasan bin Asma bin Kharijah, "Ewe mtoto wa ndugu yangu, kwa kweli mimi ninayohofu kubwa juu ya mtu huyu wewe unaonaje"?

Ibn Kharijah akasema, "Ewe ami yangu mimi siogopi chochote juu yako, usianze kutoa nafasi ya mashaka kwa nafsi yako".

Kwa bahati mbaya Hasan alikuwa hakufahamu dhamira na lengo la Ibn Ziyad dhidi ya Bwana Hani. Basi Hani (Mwenyezi Mungu amrehemu) akaja pamoja na jamaa hao mpaka wote wakaingia kwa lbn Ziyad. lbn Ziyad alipomuona Hani akasema, "Muhaini kaletwa na miguu yake mwenyewe".

Hani akasema, "Unakusudia nini kusema hivyo ewe Amir".

Mjadala baina yao ulipokuwa mrefu, na Hani hakukubali madai dhidi yake, lbn Ziyad alimwita Ma-Aqal ambaye alipata kuwa mtumwa wake, akaja akasimama mbele yake.

Huyu Ma-Aqal alikuwa jasusi wa ibn Ziyad na alikuwa akipeleleza nyendo zote za kina Hani na Muslim bin Aqiil hali ya kuwa wao hawana habari kwamba yule ni jasusi, kutokana kuwa akidhihirisha upendo na nia njema kwa kizazi cha Mtume(s.a.w.w) , hivyo basi alifahamu mengi kuwahusu wao.

Hani alipomuona mtu huyo, ndipo alipotambua kwamba alikuwa nijasusi la ibn Ziyad na kuwa mambo yao yote amekwisha yafikisha hapo, na amefaulu kumtumbukiza mikononi mwa ibn Ziyad.

Hali ilivyokuwa hivyo, Hani akasema kumwambia lbn Ziyad, "Mwenyezi Mungu amfanye mwema Amir, naapa kwa jina la Mwenyezi Mwigu kwamba, Muslim bin Aqiil sikumwita mimi lakini alinifikia bali ya kuwa anaomba ulinzi wangu nikamkubalia kumlinda, na niliona haya kumkatalia, na niliingiwa na utu ambao ulimlazimisha kumkaribisha, na sasa hebu nipe nafasi ili nirudi nikamuamuru atoke nyumbani mwangu aende apendako ili nijitoe kuwa mimi ni mdhamini wake, na kisha nitarudi nije nikupe kiapo changu cha utii."

lbn Ziyad akasema, "Wallahi hutoki hapa isipokuwa uniletee huyo Muslim Bin Aqiil". Hani akasema, "Wallahi sitakuletea wataka nikuletee mgeni wangu kisha umuuwe"?

lbn Ziyad akasema, "Wallahi naapa kuwa lazima utaniletea mtu huyo."

Hani naye akajibu, "Wallahi sikuletei hata kidogo".

Majibizano baina ya wawili hawa yalipozidi, bwana mmoja aitwaye Muslim bin Amri Al-Baahili akasema, "Mwenyezi Munga na amfanye mwema Amir, (Amir) hebu niachie nafasi mimi na yeye nizungumze naye. Akasimama yeye na Hani sehemu fulani humo ndani, kiasi kwamba Ibn Ziyad anawaona na anasikia wanachokisema.

Wakati mazungumzo yao yanaendelea, mara sauti zao zikapanda juu zaidi, kisha Bwana Al-Baahili akasema, "Nakuapia Mwenyezi Mungu ewe Hani usijiuwe mwenyewe, na wala usilete balaa kwa jamaa zako, Wallahi hakika mimi nakuona ni mtu muhimu sipendi kuona unanawa, mtoe huyu (Muslim bin Aqiil) uwape watawala, kwani jambo hilo la kumtoa siyo unyonge wala aibu bali unamtoa kwa mtawala (ataamua Ia kumfanya)".

Hani akajibu, "Wallahi kumtoa Muslim bin Aqiil kwangu mimi ni dalili za unyonge na aibu, nimtoe mgeni wangu na isitoshe ni Mjumbe wa mjukuu wa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu hali nikiwa ni mzima mwenye nguvu na ninao wasaidizi wengi, Wallahi naapa japo hata ningekuwa peke yangu sina wakunisaidia nisingemtoa (Muslim bin Aqiil) mpaka nife kwa ajili yake".

Al-Baahili akawa anamsisitiza Hani amkabidhi Muslim kwa lbn Ziyad, lakini Hani hujibu, "Wallahi simtoi kamwe".

lbn Ziyad akawa ameyasikia hayo akasema, "Msogezeni hapa karibu yangu", Hani akasogezwa kisha lbn Ziyad akasema kumwambia Hani, "Wallahi lazima uniletee huyo Muslim vinginevyo nitaikata shingo yako".

Hani akasema, "Kama utaniua fahamu wazi utakuwa umewasha moto wa fitna nyumbani kwako".

Akasema: Ooo! Ole wako nakuonea huruma, unanitishia hiyo fitna"?

Kipindi hicho Hani alikuwa akidhani kwamba nduguze na jamaa zake watamsaidia.

Baada ya lbn Ziyad kutamka maneno yale akasema, "Msogezeni kwangu" akasogezwa, kisha lbn Ziyad akatoa fimbo ambayo alianza kumpiga Hani puani na usoni mpaka pua ya Hani ikakatika na nyama za usoni mwake zikachanakanchanika, damu zikawa zinamvuja na kutiririka kwenye nguo zake, na wala hakuacha kumpiga mpaka ile fimbo ikavunjika.

Naye Hani baada ya kutendewa haya, alinyoosha mkono akikusudia kuuchukua upanga wa askari moja aliyekuwa kasimama hapo, yule Askari akauvuta upanga wake kuusalimisha.

Alipoona hivyo lbn Ziyad alipiga kelele akasema "Mshikeni mara moja". Basi Hani akakamatwa na kukokotwa hadi katika moja ya nyumba akafungiwa humo na kuwekewa mlinzi.

Hasan bin Asma bin Kharijah akasimama na kumwambia lbn Ziyad, "Hatujapata kuwa wajumbe wenye khiyana isipokuwa leo ewe Amir, umetuagiza kwa mtu huyu na ukatuamru tumlete kwako, na tulipokuwa tumekuletea umeuchanachana uso wake na umeimwaga damu yake na bado unadai kwamba utamuua".

Maneno haya yakamchukiza Ibn Ziyad, akakasirika sana akasema kumwambia Hasan, "Nawewe uko hapa (kumtetea Hani)"?

Kisha akatoa amri Hasan apigwe, akapigwa na baadaye akafungwa kamba na akatupwa Gerezani. Hapo Hasan akawa anaomboleza kwa kusema "Hakika sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na kwake tutarudi, ewe Hani kwa nafsi yangu ninakusikitikia".

Khabari za tukio hili zikamfikia Bwana Amri bin Al-Hajaaj, na kwamba Hani amekwisha kuuawa.

Bwana Hani alikuwa ni mkwe wa huyu Al-Hajaaj kwa binti yake aliyekuwa akiitwa "Ruwaihah". Hivyo basi Amri bin al-Hajaaj akafika hapo Al-Kufah akiwa na jamaa zake, wakalizunguka jumba Ia Ibn Ziyad, kisha Amri alizungumza kwa sauti kubwa akasema, "Mimi ni Amri bin Al-Hajaaj na hawa nilionao ndiyo viongozi wa jamii ya Madh-haj, nao hawajatoka katika utii wala kupinga umoja, lakini habari zimetufikia kwamba mwenzetu (Hani) kauawa".

Basi Qadhi Shuraih akaja kutoka ndani alimokuwa yeye na Ibn Ziyad na anayaona yote yaliyomfika Hani akamwambia ya kwamba Hani yu katika amani. Basi wakaridhika na kuondoka kurejea kwao.

MAJLISI YA NANE

MAAFA YALIYOMPATA MUSLIM BIN AQIL

Muslim Bin Aqiil zilipomfikia habari za matendo aliyoyatenda Ibn Ziyad kumtendea Hani, alitoka yeye pamoja na watu waliokuwa wakimtii kwenda kumsaidia Hani na kumuokoa, pia kupigana na Ibn Ziyad.

Ibn Ziyad alipogundua jambo hilo alijificha katika jumba hilo la utawala wa Bani Umayya, ikawa wafuasi wake ndiyo wanapigana na watu wa Muslim bin Aqiil.

Wafuasi wa Ibn Ziyad waliokuwa pamoja naye wakawa wanachungulia na kuwatahadharisha wafuasi wa Muslim bin Aqil na wakawaonya kuwa litakuja Jeshi kutoka Sham kwa Yazid nalo litawashambulia.

Waliendelea kufanya hivyo mpaka usiku ukaingia, hapo ndipo wafuasi wa Muslim bin Aqiil walipoanza kutawanyika kumkimbia Muslim, na wakawa wanaambiaana, "Ni kitendo gani tukifanyacho kwa kuikimbilia fitna, inatupasa kujificha majumbani wetu tuwaache hawa jamaa mpaka hapo Mwenyezi Mungu atakapoleta upatanishi baina yao."

Waliendelea kutawanyika mpaka ilipofika jioni, Muslim bin Aqill aliswali Maghrib akiwa na watu thelathini tu ndani ya msikiti. Alipoiona hali hiyo alitoka kuelekea milango ya upande wa Kindah, na hakufika hapo ila alikuwa kabaki peke yake watu wote walikwisha kumtoroka.

Kisha Muslim alitoka kupitia mlangoni, lakini ghafla akajikuta hana mtu wa kumuongoza njia, kumbe alikuwa kabaki peke yake watu wote walikwisha kumtoroka.

Muslim bin Aqiil akaendelea mbele hali ya kuwa akipita katika vichochoro vya mji wa Al-Kufah, hajuwi la kufanya wala hafahamu aendako. Alitembea mpaka akafika kwenye mlango wa nyumba ya mama mmoja aliyekuwa akiitwa "Taua" ambaye alipata kuwa mjakazi wa Ash-Ath bin Qais, alipomuacha huru akaolewa na Usaid Al-Hadhrami akamzalia mtoto aliyeitwa "Bilal".

Huyu Bilal wakati Muslim bin Aqiil anafika kwenye nyumba ya mama yake, alikuwa katoka pamoja na watu fulani, hivyo basi mama yake alikuwa akimngojea pale mlangoni.

Muslim bin Aqiil akamtolea salamu mama yule "akaitikia", kisha akamuomba maji ya kunywa "Akapewa". Yule mama aliporejesha ndani kile chombo cha maji, alitoka na kumkuta Muslim akiwa ameketi chini akamuuliza, "Je, hujanywa maji?" akajibu, "Nimekunywa".

Mama yule akaendelea kumsemesha Muslim, lakini akawa hakujibu, mwisho yule mama akasema "Sub-hana Llah!!'. Ewa mja wa Mwenyezi Mungu simama uende kwenu, haifai wewe kuendelea kukaa mlangoni kwangu wala siwezi kukuruhusu ukae hapa".

Muslim bin Aqiil akasimama na akasema, "Ewe mtumwa wa Mwenyezi Mungu, katika mji huu sina makazi wala ndugu, je wapenda kupata ujira mwema na malipo mazuri, ili nami hapo baadaye nikulipe kwa wema wako baada ya siku hii ya leo?"

Yule mama akasema "Nini makusudio yako Ewe mtumwa wa Mwenyezi Mungu?"

Akajibu "Mimi ni Muslim bin Aqiil, watu wa Mji huu wamenidanganya na wamenihadaa, na sasa wamenifukuza."

Yule mama akasema, "Wewe ndiwe Muslim"?

Akasema "Ndiyo".

Yule mama akasema "Ingia ndani".

Muslim akaingia ndani ya nyumba miongoni mwa nyumba za mama yule isiyokuwa ile anayoishi mwenyewe, na yule mama akamtayarishia Muslim mahali pa kulala, na akamletea chakula ambacho Muslim hakukila.

Mtoto wa yule mama aliporudi na akawa amemtambua Muslim basi haraka alipeleka habari kwa Ibn Ziyad kumjulisha mahali alipo Muslim bin Aqiil.

Ibn Ziyad akamleta Muhammad bin AI-Ash-ath na akamtuma pamoja naye Ubaidullah bin Abbas As-Sulami wakiwa na watu sabini wa Kabila Ia Qais mpaka kwenye nyumba aliyoko Muslim.

Basi Muslim aliposikia sauti ya kwato za farasi na sauti za watu, akafahamu kwamba amefuatwa yeye. Akawatokea akiwa na upanga wake, nao wakamvamia ndani ya nyumba kabla hajatoka, akawashambulia kwa upanga mpaka akawatoa nje. Kisha walimrudia tena naye akawashambulia vikali, na ikatokea mashambulizi yakawa baina ya Muslim na Bakru bin Hamran Al-Ahmari, basi huyo Bakru "Mwenyezi Mungu amlaani" alimpiga Muslim dhoruba Ia Upanga akamkata mdomo wa juu, na akafanya haraka kumkata mdomo wa chini pia, meno ya chini ya Muslim yakabomoka.

Naye Muslim pamoja na hali hiyo alimpiga Bakru dhoruba kali ya kichwani, akamfuatisha nyingine katika sehemu iliyo kati ya shingo na bega, dhoruba ambayo ilikaribia kuingia ndani kabisa ya mwili wa Bakru.

Muslim pamoja na maumivu aliyokwisha yapata, aliendelea kuwashambulia watu wa ibn Ziyad mpaka akafaulu kuwauwa kikundi miongoni mwao.

Walipoona hali ya ushujaa wa Muslim, walianza kumshambulia wakiwa juu ya nyumba kwa kumtupia mawe, na wakawasha vijinga vya moto kisha wakawa wanamrushia kutoka katika paa la nyumba.

Muslim hakukata tamaa bali aliwatokea hali ya kuwa ameutoa upanga wake tayari kwa kupambana nao.

Muhammad bin AI-Ash-ath akawa anamwambia Muslim "Jisalimishe usiiue nafsi yako".

Muslim alimjibu Muhammad AI-Ash-ath hali ya kuwa akiwashambulia akasema: "Nimeapa, siuawi ila niwe katika hali ya uhuru, japokuwa mauti nayaona kuwa ni jambo gumu, nachukia kuhadaiwa au kudanganywa, nitakupigeni wala siogopi madhara".

Ibn Al-Ash-ath akapiga ukelele aksema, "Hakika wewe hudanganywi wala kuhadaiwa".

Lakini kufikia kipindi hiki Muslim akawa ameshehenezwa kwa mawe na akashindwa kuendelea na mapambano, basi akauegemeza mgongo wake ukutani.

lbn Al-Ash-ath akamwambia tena Muslim, "Jisalimishe".

Muslim akajibu, "Mimi nimekwisha salimika".

Akasema ibn Ash-ath, "Vema".

Kisha Muslim akawaambia jamaa waliokuwa wakimshambulia, "Je ninayo amani?"

Wakasema, "Ndiyo".

Akasema "Japo msinipe amani lakini siwezi kuweka mkono wangu mikononi mwenu" (Siwezi kuwatii).

Hapo wakamletea nyumbu, wakampandisha kisha wakamzunguka na wakamnyang'anya panga lake, ikawa kama kwamba Muslim katika kipindi hicho anaihuzunikia nafsi yake, basi ghafla akaaza kujawa machozi machoni mwake akasema: "Huu ndiyo mwanzo wa kuvunja ahadi, uko wapi basi uaminifu wenu?" Hapa Muslim akawa analia.

Ubaidullah As-Sulami akasema kumwambia Muslim bin Aqiil, "Hakika yeyote mwenye kutafuta mambo kama haya uyatafutayo, pindi anapofikwa na hali kama hii ihyokufika wewe hana haja ya kulia".

Muslim akajibu, "Hakika mimi Wallahi silii kwa ajili ya nafsi yangu, wala nafsi yangu siihuzunikii kutokana na kifo, japokuwa siipendelei nafsi yangu kuangamia, lakini (fahamu kwamba) nawalilia jamaa zangu wanaokuja kunifuata mimi, namlilia Husein na watu wa Husein (a.s.)."

Kisha Muslim akamuelekea Ibn Al-Ash-ath akasema: "Hakika wewe utashindwa kunipa amani, basi je kwako kuna wema wowote (unitendee)? Unaweza ukatuma mtu kutoka kwako kwa niyaba yangu akamfahamishe Husein(a.s) , kwani mimi simuoni Husein ila atakuwa leo ametoka au atatoka leo pamoja na watu wa nyumba yake basi akamwambie kwamba "Hakika mwana wa Aqiil amenituma kwako, hali ya kuwa yeye ni mateka mikononi mwa watu (wa Al-Kufah) haoni nafasi yoyote ila jioni atakuwa kisha uawa, naye anasema rudi, wewe na watu wa nyumba yako, baba yangu na mama yangu (nawatoa) iwe fidia kwako na wala wasikudanganye watu wa Al-Kufah, hakika wao ndiyo wale wale watu (waliojidai kushirikiana na) baba yako, ni wao ambao alikuwa akitamani (Baba yako) kutengana nao ima kwa mauti (ya kawaida) au kuuawa, hakika hawa watu wa Al-Kufah wamekudanganya na mwenye kudanganywa huwa hana rai".

lbn Ash-ath akamchukua Muslim mpaka kwenye mlango wa jumba la utawala, akaingia ndani na kumpa khabari zote Ibn Ziyad.

Muslim kiu kali ikawa imemsonga, na hapo kwenye mlango wa jumba hilo kuna watu wengi wanasubiri kupewa ruhusa (kuingia). Mara ghafla likaletwa jagi la maji ya baridi, Muslim akasema "Ninywesheni maji haya".

Muslim bin Amri Al-Baahili akasema, "Wayaonaje, ubaridi ulioje wa maji haya!, Wallahi hutaonja japo tone moja kabisa, mpaka kwaza uonje joto kali liliilomo katika moto wa Jahannam."

Muslim bin Aqiil akamjibu Muslim bin Amri akasema;

"Mama yako kapata hasara (kuzaa mtoto kama wewe) unauovu kiasi gani na moyo mbaya kadiri gani (bali muovu mno) ewe mwana wa Baahilah, wewe ndiyo unastahiki mno kulipata joto hilo kali na pia kuishi milele ndani ya moto wa Jahannam".

Kisha Muslim bin Aqiil akaegemea ukutani.

Bwana Amri bin Huraith akaja na kile chombo kilichokuwa na maji, juu yake kuna kitambaa, pia alikuwa na jagi ambalo alilitia maji yale na akamwambia Muslim bin Aqiil "Kunywa maji", ikawa kila anapotaka kuyanywa maji, basi lile jagi hujaa damu yake inayobubujika kutoka mdomoni mwake.

Akajaribu mara mbili kuyanywa maji hayo bila mafanikio, na alipokusudia kwa mara ya tatu kunywa, meno yake mawili ya mbele yakabomoka na kutumbukia ndani ya jagi la maji.

Muslim bin Aqiil akasema, "Al-hamdulillah (Sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu) lau ningekuwa nayo riziki iliyogawiwa kwangu (kwenye maji haya) ningeyanywa".

Baadaye akaingizwa ndani kwa ibn Ziyad, Muslim hakumtolea salam lbn Ziyad.

Mlinzi wa Ibn Ziyad akamwambia Muslim, "Mtolee salaam Amir (kiongozi)".

Muslim akasema, "Ole wako nyamaza, Wallahi kwangu mimi (huyu) siyo Amiri."

Ibn Ziyad akasema kumwambia Muslim, "Ewe mwana wa Aqiil uliwakuta watu (hapa AI-Kufah) wakiwa pamoja, ukawatenganisha na kuwatawanya (wasikubaliane), pia ukawafanya wagombane wao kwa wao".

Muslim akasema, "Sivyo kabisa, mimi sikuja hapa kwa ajili hiyo, lakini watu wa Mji huu walidai kwamba Baba yako (Muawiyya) amewauwa watu wema (miongoni mwa wenyeji wa hapa) na amemwaga damu zao, na akawatendea matendo ya (Wafalme Kisra ha Kaisar, basi sisi tukawafikia (hapa) ili tuamrishe uadilifu na tuwaite (wote) kwenye hukumu ya kitabu (Qur'an)".

Ibn Ziyad akasema, "Tangu lini nawe (Muslim) ukafaa kuwa (kiongozi) wa hayo uliyoyasema? Kisha lbn Ziyad mwenye kulaaniwa akaendelea kusema kumwambia Muslim "Ewe muovu hakika nafsi yako inakutamanisha jambo ambalo Mwenyezi Mungu kisha kumpa mwingine, na haikukuonyesha mwenye kustahiki".

Muslim akasema, "Basi nani atastahiki jambo hilo (Ia uongozi wa Umma) endapo sisi (tutaonekana) hatufai?"

Ibn Ziyad akajibu akasema, "Mwenye kustahiki jambo Ia (uongozi) ni Amirul Muuminina Yazid".

Muslim aksema, "Kwa kila hali Mwenyezi Mungu ashukuriwe, sisi tumeridhia na tunaridhia kwamba Mwenyezi Mungu ndiye atakayetoa uamuzi baina yetu na ninyi".

Ibn Ziyad akasema, "Mwenyezi Mungu anilaani iwapo sitakuuwa, tena kwa uwaji baya ambalo hajapata mtu kuuliwa katika Uislam".

Muslim akasema, "Ama ilivyo kweli na hakika wewe ni mtu uliyezusha katika Uislamu mambo ambayo hapo kabla hayakuwapo, na kwa tabia yako hutaacha kufanya mauaji ya kinyama, na hutoacha kuwa ni mfano mbaya, mwenye niya mbaya, na kijicho kwa yule mwenye kustahiki mno kwa jambo hili kuliko wewe"

lbn Ziyad akamuelekea Muslim kwa ulimi wa matusi kumtukana yeye na kamtukana Husein na Ali(a.s) pia Aqiil (baba yake Muslim) akamtukana.

Muslim akanyamaza asimsemeshe kitu Ibn Ziyad, bali aliwaangalia watu waliokuwa pamoja na lbn Ziyad, akamuona Omar bin Saad akiwa ni miongoni mwao, akasema kumwambia Omar bin Saad "Ewe Omar bila shaka baina yangu mimi na wewe kuna udugu, basi mimi ninayo haja fulani kwako, na itakupasa wewe ufanikishe haja yangu hiyo, lakini ni siri baina yangu na wewe".

Omar bin Saad (mwenye kulaaniwa) akakataa kumsikiliza Muslim, lakini Ubaidullahi bin Ziyad akamuamuru Omar asikilize ombi Ia Muslim.

Basi wakajitenga wawili hao upande fulani hali ya kuwa Ibn Ziyad anawaona, Muslim akasema, "Hakika kuna baadhi ya watu wa Al-Kufah wananidai Dir-ham miasaba, basi kauze upanga wangu na deraya yangu kisha ulipe deni hilo, na nitakapokuwa nimeuawa uchukue mwili wangu na uusitiri (uuzike) na pia mtume mtu aende kwa Husein amwambie arudi (asije hapa Al-Kufah) bila shaka mimi nilimuandikia kwamba watu wanamuunga mkono (kumbe wamegeuka) nami namuona kuwa anakuja".

Ibn Saad akasema kumwambia ibn Ziyad, "Je wafahamu anasema nini (Muslim) ewe Amiri? hakika anasema kadha kadha". (Akasema yote aliyomwambia Muslim) "Ibn Ziyad akasema kumwambia Muslim bila shaka mtu mwaminifu hawezi kukufanyia khiyana lakini wewe umemuamini mtu mwenye khiyana".

Kisha huyu Ibnu Ziyad "Mwenyezi Mungu amlaani" akaamuru Muslim apandishwejuu ya paa la jumba hilo na akatwe shingo yake huko juu, na itakapoanguka wakitupe kiwiliwili chini kuifuata shingo itakayokuwa imeporomoka chini pamoja na kichwa. lbn Ziyad akamwita Bakru bin Hamran akamwambia "Panda juu ukamkate shingo yake". Akapanda.

Wakati Muslim akipandishwa juu ili akauawe, alikuwa akisoma Takbira na kuomba msamaha kwa Mwenyezi Mungu na akimsalia Bwana Mtume(s.a.w.w) na pia akawa husema, "Ewe Mwenyezi Mungu hukumu baina yetu na wale waliotudanganya na wametutweza, basi ghafla akainamishwa chini kisha shingo yake ikakatwa ikadondoka chini na mwili wake pia ukafuatishwa mpaka chini (Muslim bin Aqiil akawa ameuawa kishahidi, ewe Mola iteremshie amani na Rehema roho yake nasi tujaalie vifo vya kishahidi katika kukutumikia - Amin).

Baada ya kuuawa Muslim bin Aqiil, pale pale Ibn Ziyad akaamuru Hani atolewe (alikuwa bado kafungwa) akasema "Mtoeni mumpeleke sokoni kisha muikate shingo yake". Hani akatolewa ilhali mikono yake imefungwa na akawa anasema "Ee!!! jamaa zangu, leo sina jamaa yeyote, wako wapi jamaa zangu"?

Alipoona kwamba hakuna ye yote wa kumsaidia aliutoa kwa nguvu mkono wake katika kifungo alichofungiwa, kisha akasema, "Je hakuna fimbo au kisu au jiwe ambalo mtu anaweza kujilinda nafsi yake"?

Askari wa Ibn Ziyad wakamrukia na wakamfunga barabara na hapo hapo wakamwambia "Nyoosha shingo yako".

Hani akasema, "Sijawa mkarimu kiasi hicho kuwanyooshea shingo yangu, na pia siwezi kuwasaidieni katika kuiua nafsi yangu."

Mturuki ambaye alipata kuwa mtumwa wa lbn Ziyad akaachia dhoruba ya upanga kumkata Hani, lakini dhoruba hiyo haikumfanya kitu Hani.

Hapo Hani aksema, "Kwa Mwenyezi Mungu ndiko kwenye marejeo, Ewe Mola narudi kwenye huruma zako na radhi zako".

Yule mturuki akarudia mara ya pili kumkata Hani akafaulu kumuuwa, hivyo Hani akafa akiwa shahidi kwa kutaraji rehema za Mola wake.


3

4