TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN12%

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 42553 / Pakua: 4762
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

4

5

6

16

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA SHAMS (JUA) (NA. 91)

INA AYA 15

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu

وَالشَّمْسِ وَضُحَاهَا ﴿١﴾

1. Naapa kwa jua na mwanga wake.

وَالْقَمَرِ إِذَا تَلَاهَا ﴿٢﴾

2. Na (kwa) mwezi unapoliandamana.

وَالنَّهَارِ إِذَا جَلَّاهَا ﴿٣﴾

3. Na (kwa) mchana unapoifunia.

وَاللَّيْلِ إِذَا يَغْشَاهَا ﴿٤﴾

4. Na (kwa) usiku unapoifunika.

وَالسَّمَاءِ وَمَا بَنَاهَا ﴿٥﴾

5. Na (kwa) mbingu na aliyeziweka.

وَالْأَرْضِ وَمَا طَحَاهَا ﴿٦﴾

6. Na (kwa) ardhi na aliyeitandika.

وَنَفْسٍ وَمَا سَوَّاهَا ﴿٧﴾

7. Na (kwa) nafsi na aliyelingamanisha.

فَأَلْهَمَهَا فُجُورَهَا وَتَقْوَاهَا ﴿٨﴾

8. Akaifahamisha maasia yake na twaa yake.

قَدْ أَفْلَحَ مَن زَكَّاهَا ﴿٩﴾

9. Hakika amefaulu mwenye kuitakasa.

وَقَدْ خَابَ مَن دَسَّاهَا ﴿١٠﴾

10. Na hakika amepata hasara mwenye kuitweza.

كَذَّبَتْ ثَمُودُ بِطَغْوَاهَا ﴿١١﴾

11. Ilikadhibisha (kabila ya) thamud kwa kupetuka mipaka.

إِذِ انبَعَثَ أَشْقَاهَا ﴿١٢﴾

12. Wakati walipomshakiza mwovu wao (kumuua ngamia).

فَقَالَ لَهُمْ رَسُولُ اللَّـهِ نَاقَةَ اللَّـهِ وَسُقْيَاهَا ﴿١٣﴾

13. Akawaambia Mtume wa Allah, (tahadharini na) ngamia wa Allah na maji yake.

فَكَذَّبُوهُ فَعَقَرُوهَا فَدَمْدَمَ عَلَيْهِمْ رَبُّهُم بِذَنبِهِمْ فَسَوَّاهَا ﴿١٤﴾

14. Wakamkadhibisha (na) wakamchinja. Mola wao akaeneza (adhabu) kwa sababu ya madhambi yao, na akaifanya sawa.

وَلَا يَخَافُ عُقْبَاهَا ﴿١٥﴾

15. Wala haogopi matokeo yake.

UBAINIFU

Sura inataja kwamba kufaulu kwa mtu ni kuitakasa nafsi yake na kuikuza makuzi mema kwa kuipamba na takua na kuitakasa na uovu. Na kupata hasara na kuzuiliwa wema ni kwa mwenye kuitweza. Yanatolea ushahidi hilo yale yaliyowapitia kabila la Thamud walipong'olewa na adhabu pale walipomkadhibisha Mtume was Saleh na kumchinja ngamia. Hilo ni kuwaonyesha watu wa Makka. Sura imeshuka Makka kwa ushahidi wa mpangilio wake wa maneno.

Aya Na 1

Maana ya neno Dhuhaa ni kukunjuka jua na kuenea mchana na neno hilo limetumiwa kwa wakati. Katika aya hii kuna kiapo kwa jua na kuangaza kwake juu ya Ardhi.

Aya Na 2

Inaungana na Aya Na kwanza na nikuapa kwa mwezi hali yakuwa unaandamia jua. Makusudio ya kuandamia ikiwa inamaanisha kule kupata mwezi nuru yake kutoka kwa jua, basi itakuwa ni kuapa kwa wakati wote wa mwezi. Na ikiwa ni kuchimbuka kwa mwezi baada ya kutua jua, basi itakuwa kuapa ni tangu kuwa mwezi mchanga mpaka kuwa mpevu.

Aya Na 3

Maana ya neno Jallaha ni kudhihirisha na dhamir ni ya Ardhi kwa maana ya kuwa: ninaapa kwa mchana unapoidhirisha ardhi kwa macho. Inasemekana kuwa dhamir ya (mtendaji) ni ya mchana na dhamir ya (mtendwa) ni ya jua, kwa maana ya kuwa, ninaapa kwa mchana wakati Mwenyezi Mungu anapolidhihirisha jua, na hiyo ni njia iliyo mbali.

Aya Na 4: Yaani unapoifunika ardhi, dhamir ni ya ardhi kama katika aya iliyotangulia. Na inasemekana kuwa ni ya jua na hiyo pia ni njia iliyo mbali, kwa sababu usiku haufuniki jua isipokuwa unafunika ardhi na vilivyo juu yake. Ibara ya kufunika ardhi imekuja kwa (kitendo cha sasa) kinyume cha aya zilizotangulia ambapo ibara zake zimekuja kwa kitendo cha muda uliopita. Hiyo ni kufahamisha kufunika uovu wa ardhi kwa wakati uliopo ambao ndio mwanzo wa kudhihiri mlingano (mwito) wa Kiislamu, kutokana na yaliyotangulia kuwa kuna muungano kati ya kuapa na mwenye kuapiwa.

Aya Na 5-6

Herufi Maa katika neno Maabanaaha na Maatwahaaha ni kiwakilishi yaani na ambaye ameziweka na kuitandika ni Mwenyezi Mungu. Kuleta ibara bila ya kumtaja Mwenyezi Mungu ni athari ya kuficha kunakofahamisha ukubwa na ajabu, kwa maana ya kuwa; Ninaapa kwa mbingu na kitu chenye nguvu cha ajabu kilichoziweka. Na ninaapa kwa ardhi na kitu chenye nguvu cha ajabu kilichoitandika. Imesemwa kuwa Maa ni kiarifa chenye kutumika kama jina kwa maana ninaapa kwa mbingu na kuziweka kwake. Na ardhi na kuitandika kwake, lakini mpangilio wa maneno katika Sura kama vile aya inayofuatia haulisaidii hilo.

Aya Na 7

Yaani ninaapa kwa nafsi na kitu chenye uwezo, ujuzi na hekima ambacho kimeilingamanisha, kuipanga umbo lake na viungo vyake na kuilingamanisha sawa nguvu yake. Makusudio na nafsi ni nafsi ya mtu yoyote. Imesemwa kuwa makusudio ni nafsi na Nabii Adam(a.s) , lakini mpangilio wa maneno hauafikiani na hilo hasa Aya Na tisa na kumi.

Aya Na 8

Neno Fujuur kama alivyotaja Raghib ni kupasua sitara ya dini. Makatazo ya Mungu ya kufanya au kuacha, ni sitara iliyowekwa kati ya binadamu na Mwenyezi Mungu na kufanya yaliyokatazwa ni kupasua sitara hiyo. Neno Taqwa kama alivyotaja Raghib ni kuifanya nafsi katika kinga ya yanayohifiwa. Makusudio ya Taqwa kwa kuilinganisha na aya inayofuatia ni kujiepusha na maovu na kujilinda na yaliyo katazwa. Imefasiriwa katika hadith kwamba ni kujichunga ya yaliyoharamishwa.

Kuifunga silika (Ilham) juu ya anuani mbili za uovu wa nafsi na takua yake, ni kwa ajili ya kufahamisha kwamba makusudio ni kwamba Mwenyezi Mungu anamfahamisha mtu sifa ya kitendo chake kuwa ni kizuri au kibaya, baada ya kumfahamisha kitendo chenyewe hasa, kwa kuangalia asili yake ya mwenzo, ambapo kitendo kinaweza kuwa ni kizuri na kibaya wakati mmoja. Kwa mfano kula mali ya yatima ambako ni kuovu na kula mali yake mwenyewe ambako ni kitendo kizuri au kuvaana na mwanamke ambako kunashirikiana kati ya zina ambayo ni uovu na ndoa ambayo ni takua. Kwa ujumla makusudio na kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemfahamisha mtu kuwa kitendo anachokifanya ama kitakuwa cha uovu au cha takua na akampambanulia takua na uovu.

Kuifuatisha silika juu ya usawa katika kauli yake: "na mwenye kuilingamanisha. Akaifahamisha." ni kuashiria kuwa (mtu) kufahamu uovu na heri - ambapo ndiyo akili ya kimatendo - ndiyo kusawazisha nafsi. Na hiyo ni miongoni mwa sifa za umbile la hiyo nafsi; kama alvyosema Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Basi uelekeze uso wako katika dini iliyo sawasawa ndiyo umbile Allah alilowaumbia watu; hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe vya Allah. Hiyo ndiyo dini iliyo haki " (30:30).

Kutegemeza uovu na takua kwenye dhamir na nafsi ni kuonyesha kwamba makusudio ya uovu na takua zinafahamishwa hapa ni uovu na wema kuhusika na hii nafsi iliyoelezewa ya mtu na zile za majini kama ilivyodhihiri katika Qur'an tukufu kuwa wao ni wenye kukalifiwa na imani na kutenda amali njema.

Aya Na 9 -10

Kufaulu ni kushinda matakwa na kupata matakwa, kinyume chake ni kupata hasara. Kutakata ni kukua kwa makuzi mema yenye baraka. Na kutweza ni kuingiza kitu katika kitu chengine, makusudio yake kwa kukutanisha na aya, inayokabiliana na kutakasa, ni kuikuza nafsi katika misingi inayohitalifiana na tabia yake na kuipandanisha nayo. Aya hizo mbili ni jawabu la kiapo na Aya Na pili inaungana na ya kwanza. Kuleta ibara ya kutengenea nafsi na kuharibika kwake kwa neno kutakasa na kutweza ni udhihirisho wa inavyofahamisha kauli yake Mwenyezi Mungu. Akaifahamisha maasi yake na twaa yake, kwamba ni katika ukamilifu wa nafsi ya kiutu kwamba hiyo nafsi kimaumbile inapambanua uovu kutokana na twaa, yaani dini ya Kiislamu ni dini ambayo Mwenyezi Mungu anaikusudia kwa maumbile ya mtu, kwa hiyo kuipamba nafsi kwa twaa ni kuitakasa.

Aya Na 11

Aya hii na zinazofuatia mpaka mwisho wa Sura ni ushuhuda na uthibitisho wa yaliyotangulia katika kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hakika amefaulu mwenye kuitakasa ".

Aya Na 12

Makusudio ya mwovu wa Thamud ni yule aliyemchinja ngamia. Jina lake kutokana na yaliyo katika riwaya ni Qidar bin Salif. Na kushakiza kulikuwa na kushakiza kwa watu kama zinavyofahamisha aya zinazofuatia kutokana na dhamir zake za wingi.

Aya Na 13

Makusudio ya Mtume wa Mwenyezi Mungu hapa ni Saleh(a.s) Mtume wa Thamud. Maana yake: akawaambia Mtume Saleh kwa ujumbe utokao kwa Mwenyezi Mungu: "Tahadharini na ngamia wa Allah na maji yake wala msimtaaradhi kuwa kutaka kumuua au kumzuwia na zamu yake ya kunywa maji ." Mwenyezi Mungu amekifafanua kisa hiki katika Sura ya II (Hud) na nyenginezo.

Aya Na 14

Kusema kwake akaifanya sawa, kwa dhahiri dhamir ni ya Thamud kwa kuzingatia kuwa ni kabila yaani akalifanya sawa na ardhi hilo kabila au ni kufanya sawa kwa maana ya kuitandaza hiyo ardhi. Inasemekana kuwa dhamir ni ya neno kueneza kwa maana ya kuwa akawaeneza adhabu na akaifanya sawa kwa wote hila ya kuangalia mwenye nguvu, wala myonge au mkubwa wala mdogo.

Aya Na 15

Dhamir ni ya kueneza au kufanya sawa yaani Mola wao haogopi mwisho wa kueneza adhabu na kuifanya sawa, kama wanavyoogopa wafalme na wenye nguvu mwisho wa mateso kwa maadui zao; kwa sababu mwisho wa mambo ni vile anavyotaka yeye Mwenyezi Mungu na kuafikiana na anavyoidhinisha. Aya hii iko karibu katika maana na aya inayosema: "Haulizwi anayoyafanya, lakini wao wataulizwa " (21:23).

Inasemekana kuwa dhamir ya neno haogopi ni ya mwovu kwa maana ya kuwa haogopi mchinjaji ngamia mwisho wa aliofanya. Na pia imesemekana kuwa dhamir ya haogopi ni ya Saleh na dhamir ya mwisho wake ni ya kueneza adhabu kwa kutegemea kuokoka. Udhaifu wa njia zote hizo mbili uko wazi.

Utafiti Wa Hadith Katka Tafsiri ya Qummi kuhusu Aya Na saba amesema: Akaiumba na kuitia Sura. Katika Majmau amepokea Zurarah na Hamran, na Muhammad bin Muslim kutoka kwa Abu Jaffar na Abu Abdillah(a.s) katika kauli yake Mwenyezi Mungu: Akaifahamisha maasis yake na twaa yake, ni kuwa ameibanisha yale ya kufanya na ya kuwacha. Na katika kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hakika amefaulu mwenye kuitakasa". Amesema: "Hakika amefaulu mwenye kutwii" Na kuhusu na hakika amepata hasara mwenye kuitweza. Amesema: "Hakika amepata hasara mwenye kuasi".

Katika Durril Manthur ametoa Ahmad, Muslim, Ibn Jariyr, Ibn Mundhir, Ibn Murdawayh kutoka kwa Amran bin Haswiyn kwamba mtu mmoja alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu unaona wanayoyafanya watu leo wanajitahidi katika jambo ambalo limekwisha hukumuliwa na kupitishwa katika kadar iliyotangulia? Au katika ambayo wanamkubalia Mtume wao"? Akasema: "Bali ni jambo lililokwisha pitishwa.' Akasema huyo mtu kwa nini wanafanya basi? Akasema Mtume: "Ambaye Mwenyezi Mungu amemuumbia kwa moja ya daraja mbili humuandalia kuifanya. Na ukweli wa hayo ni katika kitabu cha Mwenyezi Mungu: "Na (kwa) nafsi na aliyelingamanisha akaifahamisha maasia yake na twaa yake ."

Ufafanuzi Wa Hadith Hiyo Aliposema au katika wanayomkubalia Mtume wao, inaungana na sehemu ya kwanza kama swali yaani, Je, katika kumtii Mtume wao kumepitishwa na kukadiriwa tayari? Aliposema: "Kwa nini wanafanya basi, yaani nini maana ya amali yao na kutugemezwa kitendo kwao"? Na aliposema; "Ambaye Mwenyezi Mungu amemuandalia " Maana yake ni kuwa: Matokeo ya kutenda wema au uovu yanatokana na wao pamoja na kuangalia kuwa yamekwishapitishwa na kukadiriwa; huko hakukanushi kutokea kwake kwa kumwangalia mtu na hiyari yake. Na hayo yamefafanuliwa mara nyingi. Katika utafiti uliotangulia katika kitabu hiki.

Katika hiyo Durril Manthur, ametoa Ibn Abu Hatim,Abu Shakh, Ibn Murdawayah na Addilami kutoka kwa Juwaybir naye kutoka Adh-dhahak naye kutoka kwa Ibn Abbas amesema: Nimemsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akisema: "Hakika amefaulu mwenye kuitakasa". Imefaulu nafsi aliyoitakasa Mwenyezi Mungu na imepata hasara nafsi aliyoihasirisha Mwenyezi Mungu na kila heri".

Kunasibisha utakaso na hasara kwa Mwenyezi Mungu S.W.T. ni kwa njia ambayo haikanushi kunasababishwa twaa na maasi kwa mtu. Na hakika hunasababishwa upotevu kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa njia ya fumbo; kaa S.W.T. kwa njia ya fumbo; kama alivyosema Mwenyezi Mungu "Na hamwachii yoyote kupotea kwa mfano huo isipokuwa wale wavunjao amri zake (mafasiki) " (2:26).

Katika Majmau anasema: " Imesihi riwaya kwa kutegemeza Uthman bin Suhaib naye kutoka kwa baba yake amesema" "Mtume(s.a.w.w) alisema kuumuliza Ali bin Abu Twalib: ni nani mwovu zaidi wa watu wa mwanzo?" Akasema: " aliyemchinja ngamia". Mtume akasema, "umepata". "Na nani mwovu wa watu wa mwisho?" Akasema "sijuwi ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu." Akasema Mtume: "Ambaye atakupiga kwenye huu (akaonyesha utosi wake)". Na imepokewa hadith nyengine kwa maana haya haya kutoka kwa Ammar bin Yassir. Katika Tafsiri ya Burhan amepokea Thalaabi ne Wahidi kwa kutegemezwa kwao, kutoka kwa Ammar na kutoka kwa Athman Bin Suhaib na kutoka kwa Adh-dhahhak.

Na amepokea Ibn Murdawayh kutoka kwa Jabir bin Samra; na kutoka kwa Ammar kutoka kwa Ibn Adi na amepokea Attabari na Muswili. Amepokea Ahmad kutoka kwa Adh- dhahhak naye kutoka kwa Ammar kwamba yeye amesema: Amesema Mtume(s.a.w.w) : "Ewe Ali mwovu zaidi wa kwanza ni mchinja ngamia na mwovu zaidi wa mwisho ni muuaji wako ".

17

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA LAYL (USIKU) (NA. 92)

INA AYA 21

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

وَاللَّيْلِ إِذَا يَغْشَىٰ ﴿١﴾

1. Naapa kwa usiku unapofunika

وَالنَّهَارِ إِذَا تَجَلَّىٰ ﴿٢﴾

2. Na (kwa) mchana unapofunuka.

وَمَا خَلَقَ الذَّكَرَ وَالْأُنثَىٰ ﴿٣﴾

3. Na (kwa) mwenye kuumba kiume na kike.

إِنَّ سَعْيَكُمْ لَشَتَّىٰ ﴿٤﴾

4. Hakika matendo yenu ni mbali mbali.

فَأَمَّا مَنْ أَعْطَىٰ وَاتَّقَىٰ ﴿٥﴾

5. Ama mwenye kutoa akamcha (Mwenyezi Mungu).

وَصَدَّقَ بِالْحُسْنَىٰ ﴿٦﴾

6. Akalisadiki jambo jema.

فَسَنُيَسِّرُهُ لِلْيُسْرَىٰ ﴿٧﴾

7. Tutamsahilishia njia ya wepesi.

وَأَمَّا مَن بَخِلَ وَاسْتَغْنَىٰ ﴿٨﴾

8. Ama mwenye kufanya ubakhili akajiona hana haja.

وَكَذَّبَ بِالْحُسْنَىٰ ﴿٩﴾

9. Akalikadhibisha jambo jema.

فَسَنُيَسِّرُهُ لِلْعُسْرَىٰ ﴿١٠﴾

10. Tutamfanyia nyepesi njia ya uzito.

وَمَا يُغْنِي عَنْهُ مَالُهُ إِذَا تَرَدَّىٰ ﴿١١﴾

11. Hayatamfaa mali yake atakapopomoka.

إِنَّ عَلَيْنَا لَلْـهُدَىٰ ﴿١٢﴾

12. Hakika na juu yetu kuongoza.

وَإِنَّ لَنَا لَلْآخِرَةَ وَالْأُولَىٰ ﴿١٣﴾

13. Na hakika ni yetu sisi akhera na ulimwengu.

فَأَنذَرْتُكُمْ نَارًا تَلَظَّىٰ ﴿١٤﴾

14. Basi ninawahadharisha na moto unaowaka kwa nguvu.

لَا يَصْلَاهَا إِلَّا الْأَشْقَى ﴿١٥﴾

15. Hatauingia ila mwovu mno!

الَّذِي كَذَّبَ وَتَوَلَّىٰ ﴿١٦﴾

16. Ambaye amekadhibisha akapa mgongo.

وَسَيُجَنَّبُهَا الْأَتْقَى ﴿١٧﴾

17. Na ataepushwa nao mwenye kucha (Mungu).

الَّذِي يُؤْتِي مَالَهُ يَتَزَكَّىٰ ﴿١٨﴾

18. Ambaye hutoa mali yake kwa (kutaka) kujitakasa.

وَمَا لِأَحَدٍ عِندَهُ مِن نِّعْمَةٍ تُجْزَىٰ ﴿١٩﴾

19. Na hali ya kuwa hakuna yoyote aliyemfanyia hisani ili awe anamlipa.

إِلَّا ابْتِغَاءَ وَجْهِ رَبِّهِ الْأَعْلَىٰ ﴿٢٠﴾

20. Isipokuwa ni kwa kutaka radhi ya Mola wake aliye Mtukufu mno.

وَلَسَوْفَ يَرْضَىٰ ﴿٢١﴾

21. Basi hapo ataridhia.

UBAINIFU

Lengo la Sura hii ni kuonya. Inaelezea huko kuonya kwa kufuata njia ya kuonyesha tofauti ya matendo ya watu: Kwamba katika wao, mwenye kutoa, akamcha Mwenyezi Mungu na akalisadiki jambo jema, basi Mwenyezi Mungu atammanikisha katika maisha mema ya milele. Na katika wao mwenye kufanya ubakhili, akajiona hana haja na akalikadhibisha jambo jema, basi Mwenyezi Mungu atamwelekeza kwenye uovu. Sura hii inatilia umuhimu zaidi jambo la kutoa mali. Kulingana na mpangilio wake inawezekana kuwa imeshuka Makka au Madina.

Aya Na 1

Mwenyezi Mungu anaapa kwa usiku unapofunika mchana; kama alivyosema: "Huufunika usiku kwa mchana " (7:54). Inawezekana kuwa makusudio yake ni kufunika ardhi au jua.

Aya Na 2

Inaungana na Aya Na (1). Maana ya neno Tajallaa ni kudhihiri kitu baada ya kujificha. Amesema katika Majmau ni kudhihiri huo mchana kutoka katika giza. Hili ni neema kubwa, kwani lau wakati wote ungekuwa ni giza, basi watu wasingeweza kutafuta maisha.

Aya Na 3

Pia inaungana na aya iliyotangulia herufi Maa ni kiwakilishi na makusudio yake ni Mwenyezi Mungu Mtukufu. Imekuja ibara hiyo bila ya kumtaja Mwenyezi Mungu kwa kutambulisha utukufu wake; Maana yake; ninaapa kwa kitu cha ajabu ambacho kimeleta kiume na kike ambavyo ni namna moja, lakini vimetofautina. Imesemwa kuwa herufi Maa ni kiarifa chenye kutumika kama jina; Maana yake ni ninaapa kwa kuumba kiume na kike lakini njia hii ni dhaifu. Mukusudio ya kiume na kike hapa ni aina yoyote ya kiume na kike. Imesemwa kuwa ni mtu mume na mke na pia imesemwa kuwa ni Adam na mkewe Hawa, lakini njia iliyo na nguvu zaidi, ni hiyo ya kwanza.

Aya Na 4

Neno Saa'ya lina maana ya kwenda haraka, na makusudio yake hapa ni ketendo kwa vile mtu anajihimu nacho, nalo liko katika maana ya wingi. Jumla hiyo ni jawabu la kiapo na maana yake; Ninaapa kwa vitu hivi vyenye kutofautiana kwa umbo na athari, hakika matendo yenu ni yenye kutofautiana hayo yenyewe na athari zake. Kuna katika hayo ni ya kutoa, kumcha Mwenyezi Mungu na kusadikisha, yana athari inayohusika nayo. Na kuna katika hayo ni ya ubakhili, kujitosheleza na kukadhibisha nayo yana athari inayohusika nayo.

Aya Na 5-6

Ni ufafanuzi wa kutofautiana matendo yao na kutofautiana athari yake. Makusudio ya kutoa ni kutoa mali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kinyume chake ni ubakhili wa kujizuia kutoa mali. Na kusema kwake: "Hayatamfaa mali yake atakapopomoka." Na kusema kwake : "Na akamcha Allah" ni kama anafasiri kutoa, makusudio yake ni kutoa kwa njia ya (taqwa) uchaji Mungu. "Jambo jema" ni sifa yenye kusimama mahali pa chenye kusufiwa, kwa dhahiri kukadiriya kwake ni maandalizi mema ambayo ameyatolea ahadi Mwenyezi Mungu Katika thawabu ya kutoa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) Na huko kutoa ni kusadikisha ufufuo na kuamini Mwenyezi Mungu na kulazimisha imani kwa umoja wake Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika ubwana na kuuamini utume. Hiyo ndiyo njia ya kufikia yale aliyoyatolea ahadi Mwenyezi Mungu kupitia kwenye ulimi wa Mtume wake.

Aya Na 7

Makusudio ya kumsahilishia njia ya wepesi ni kumwafikisha kwa mali njema kwa kuzifanya nyepesi bila ya uzito wowote. Au kumfanya ni mwenye kujiandaa kwa maisha mema mbele ya Mola wake na kuingia peponi kwa sababu ya amali njema anazozifanya. Hii njia ya pili ni karibu na iko wazi zaidi kutokana na yale yaliyotolewa ahadi katika viaga vya Qur'an.

Aya Na 8 -10

Ubakhili ni kunyume cha kutoa. Makusudio ya kukadhibisha jambo jema ni kukanusha mambo mema na thawabu za Mwenyezi Mungu ambazo wamezielezea Mitume. Na hayo yanarudia kukanusha ufufuo. Makusudio ya 'kusahilishiwa uzito' ni kutofanikiwa kwake kwa kukosa kuwafikishwa kwenye amali njema, kwa kuwa nzito na kukosa kukunjuliwa moyo wake na imani au ni kuandaliwa adhabu.

Aya Na 11

Herufi Maa ni swali yaani mali yake itamfaa namna gani atakapokufa na kuangamia. Au ni ya kukanusha, yaani haitamfaa mali yake atakapoangamia.

Aya Na 12-13

Ni sababu ya yaliyotangulia katika kuzungumzia wepesi na uzito Au nikuelezea kwa ufafanuzi zaidi kwamba hakika sisi tunafanya huu wepesi au tunaubainisha ubainifu huu, kwa sababu unatokana na uongofu na ni juu yetu kuongoza na wala hakituzuii kitu chochote. Kwa hivyo kusema kwake "Hakika ni juu yetu kuongoza", kunamaanisha kwamba kuongoza watu alikokupitisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) amejiwabisha mwenyewe kwa mujibu wa hekima, na hilo ni kwamba yeye amewaumba ili wamwabudu; kama alivyosema: "Sikuumba majini na watu ila waniabudu ". (51:56).

Kwa hiyo amefanya kumwabudu ndiyo lengo la kuumbwa kwao na akaifanya hiyo ibada ni njia yenye kunyooka ya kumwendea yeye; kama alivyosema: "Hakika Allah ni Mola wangu na ni Mola wenu, basi mwabuduni hii ndiyo njio iliyonyooka " (3:51) "Hakika wewe unaongoza njia iliyonyooka " (42:52).

Mwenyezi Mungu amejihukumilia kuwabainishia watu njia yake na kuwaongoza kwake, kwa maana ya kuwaonyeshea njia, ikiwa wataifuata au wataiwacha, kama alivyosema: "Na Allah ndiye anayesema kweli, naye kuongoa njia (ya uongofu) (33:4). Amesema tena: "Hakika sisi tumemuongoa njia, basi ama atakuwa mwenye kushukuru au kukufuru ". (76:3).

Hayo yote hayapingi kuwa mtu mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu kuweza kusimamia jambo hili kwa idhini yake Mwenyezi Mungu, kama vile mitume; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Hakika wewe (Muhammad) unaongoza njia iliyonyooka " (42:52). Amesema tena: "Sema, hii ndiyo njia yangu ninailingania kwa Allah kwa ujuzi wa kweli, mimi (ninafanya hivi) na wanaonifuata " (12:108)

Hayo ni ikiwa uongozi ni kwa maana ya kuonyesha njia. Ama ikiwa uongozi ni kwa maana ya kufikisha kwenye matakwa - na matakwa ni athari nzuri ambazo zinafuatana na kuongoka kwa uongofu wa Mwenyezi Mungu kama maisha mema ya dunia na ya akhera ya milele - basi kwa ubainifu zaidi itakuwa ni kwa upande wa kutengeneza na kupatisha ambako anahusika nako Mwenyezi Mungu (s.w.t) Hayo ni katika yale aliyoyahukumilia Mwenyezi Mungu na kujiwajibishia na kuyasajili kwa kiaga chake cha haki; Mwenyezi Mungu anasema: "Basi atakayeufuata uongofu wangu hatapotea wala hatataabika ." (20:123).

"Mwenye kufanya mema miongoni mwa wanaume au wanawake na hali ya kuwa yeye ni muu'min tutamuhuyisha maisha mema na tutawapa ujira wao mkubwa kwa sababu ya yale mema waliyokuwa wakiyatenda ." (16:97).

Amesema tena: "Na wale waliomaini na wakatenda njema tutawaingiza katika mabustani yapitayo mito chini yake watakaa humo milele. Ndiyo ahadi ya Allah iliyokweli. Na ninani mkweli zaidi kwa usemi kuliko Allah ? (4:122). Kunasibishiwa uongozi mtu mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kwa kuingia kati huyo mtu na hayo yanayonasibishwa kwa Mwenyezi Mungu. Hii ikiwa ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Hivyo Mwenyezi Mungu atakuwa ndiyo asili ya uongozi, na mtu huyo ni mfuasi. Maana ya aya, ikiwa makusudio ya uongofu ni kuonyesha njia, ni: hakika sisi tunawabainisha yale tunayoyabainisha, kwa sababu ni juu yetu kuonyesha njia ya kuabudu. Ikiwa ni kwa makusudio ya kufikisha kwenye matakwa, ni: hakika tunawasahilishia hawa wepesi wa amali njema, au na maisha mepesi ya milele na kuingia peponi; kwa sababu hilo ni katika kuvifikisha vitu kwenye lengo lake, na hilo ni juu yetu. Ama kusahilishia njia ya uzito ni kuzuilika na kupata wepesi, "Ili Allah apate kuwapambanua walio wabaya na walio wazuri na kuwaweka wabaya juu ya wabaya wengine na kuwarundika wote pamoja na kuwatupa katika Jahanam ". (8:37).

Mwenyezi Mungu amekwishasema: "Na tunateremsha katika Qur'an (Hayo mafundisho yake) ambayo ni ponyo na rehema kwa wanaoamini wala hayawazidishi (mafundisho hayo) madhalimu ila hasara tu! (kwani hawakubali kufuata) ." (17:82).

Inawezekana kuwa maana ya ungozi hapa - kwa vile tamko 'uongozi' halikutegemezewa sharti yeyote - ni kwamba huu uongozi, pasi na kutajwa katika jambo gani, una maana mapana zaidi kuliko uongozi uliotajwa kama katika mazingatio ya sheria n.k. - kwa hiyo Mwenyezi Mungu ni wake uongozi wa kiuhakika kama alivyosema: "ambaye amekipa kila kitu umbo lake kisha akakiongoza ." (20:50).

Na ni wake uongofu wa kimazingatio, kama alivyosema: "Hakika sisi tumemuongoa (tumembainishia) njia (ya kheri nay a shari) , basi (mwenyewe tena) atakuwa mwenye kushukuru au kukufuru .(76:3).

Kuhusu Aya Na (13) ni ulimwengu wa mwanzo na ulimwengu wa kurudi; kila kinachohisabika ni kitu basi ni milki yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa milki ya uhakika ambayo inasimamia kupatikana kwa kiti hicho, kisha ndipo inakuja milki wa kimazingatio ambayo katika athari zake ni kujuzu kukifanya lolote.

Kwa hiyo yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamiliki kila kitu kwa kila upande hakuna mpinzani anayempinga wala mzuwiyaji atakayemzuwiya, wala hakuna kitu kinachomshinda, kama alivyosema: "Na Allah huhukumu hakuna wa kupinga hukumu yake "(13:41).

Na amesema tena: "Na Allah hufanya apendavyo." (14:27).

Na amesema tena: "Na Allah ndiye mwenye kushinda juu ya jambo lake (alitakalo lazima liwe) ." (12:21).

Aya Na 14-16

Ni mtiririko wa yaliyotangulia; yaani ikiwa uongofu ni juu yetu, basi ninawatahadharisha na moto wa Jahannam. Na kwa hilo anauelekeza msemo katika kauli yake (ninawatahadharisha) kutoka katika wenye kusema wengi kwenda kwa mwenye kusema mmoja pekee, yaani ikiwa uongofu ni wenye kupitishwa, basi muhadharishaji wa asili ni Mwenyezi Mungu ijapokuwa ni kupitia kwa ulimi wa Mtume wake. Makusudio ya moto uwakao ni Jahannam kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Lakini wapi! Kwa hakika huo ni moto uwakao ". (70:15).

Makusudio ya mwovu mno ni kafiri yeyote ambaye anakufuru kwa kukadhibisha na kupa mgongo. Kwani yeye ni mwovu zaidi ya waovu wengine. Mwenye kuwa na balaa katika mwili wake amepata uovu, mwenye kupatwa na balaa katika mali yake au mtoto wake pia amepata uovu na mwenye kupata hasara katika mambo yake ya akhera amekuwa mwovu, lakini huyu ni mwovu zaidi ya wengine kwa vile uovu wake ni wa milele hakuna tamaa ya kuepukana nao. Kinyume cha uovu wa mambo ya kidunia, kwa sababu uovu unakatika na ni wenye kutarajiwa kuondoka haraka.

Kwa hiyo makusudio ya mwovu mno hapa ni kafiri mwenye kukadhibisha mlingano wa haki, kama alivyomwelezea Mwenyezi Mungu kwa kusema: "Ambaye amekadhibisha na akapa mgongo." Ama kusema muovu zaidi ni kwa maana ya muovu wa watu wote ni jambo ambalo halisaidiwi kabia na mpangilio wa maneno. Makusudio ya neno Yaswlaaha ni kuufuata huo moto na kulazimiana nao (kuwa nao) kwa hiyo inafahamisha kudumu kwenye huo moto. Hayo ni katika aliyoyahukumilia Mwenyezi Mungu katika haki ya kafiri, kama alivyosema: "Na wale ambao wamekufuru na wakayakadhibisha maneno yetu hao ni watu wa motoni, watakaa milele humo ." (2:39).

Hilo basi linapinga yale yaliyosemwa kwamba maana ya neno: "Hatauingia ila mwovu mno" kwamba mafasiki katika waislamu hawataingia motoni, isipokuwa inaonyesha kuwa asiyekuwa kafiri hatadumu , lakini atauingia.

Aya Na 17-19

Makusudio ya neno Atqaa ni yule mwenye kumcha Mungu zaidi: Wako watu hucha kupotea nafsi kama kwa kifo au kuuawa, na wengine hucha kuharibika mali na wengine hucha ufakiri, kwa hiyo wanajizuia kutoa mali. Na wengine humcha Mwenyezi Mungu tu; kwa hiyo wanatoa mali. Basi huyu ndiye mwenye kucha zaidi ya wote, anatoa mali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Ukipenda unaweza kusema: hucha hasara ya akhera , kwa hiyo anajitakasa kwa kutoa. Yule ambaye hachi kwa kutoa mali anashindwa na huyo anayetoa mali, ijapokuwa hucha mambo ya kidunia au humcha Mungu kwa baadhi ya matendo mema.

Ayah ii inaenea kwa wote na sio mahsusi kwa mtu, kulingana na inavyofahamisha, na kunafahamisha hilo, kumsifu mwenye kucha zaidi kwa aya inayofuatia. "Ambayo hutoa mali yake" hiyo ni sifa ya yeyote yule amayetoa, lakini hili halikanushi kuwa aya au Sura yote imeshuka kwa sababu mahsusi kama ilivyopokewa katika sababu za kushuka. Ama kumuhusisha mbora zaidi mmoja tu! Juu ya watu wote, wabaya au wema katika wote au katika kila zama na iwe maana ni "ataepushwa nao mwenye kucha zaidi ya watu wote, na hatauingia ila mwovu zaidi ya watu wote", ni jambo ambalo halisaidiwi na mpangilio wa aya za mwanzo wa Sura vile vile hakuna maana ya kusema "Ninawahadharisha nyote na moto ambao hatadumu ndani yake ila mmoja katika nyinyi na hataokoka ila mmoja katika nyinyi".

Aya Na (18) ni sifa ya yule mwenye kumcha zaidi yaani ambaye anatoa mali yake hali ya kutaka kwa hilo ziada njema.

Aya Na (19) ni ya kuthibitisha madhumuni ya aya iliyotangulia yaani hana yoyote mbele zake ihsani itakayolipa hiyo ihsani yake isipokuwa anatoa kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu. HAya Na natiliwa nguvu na aya inayofuatia.

Aya Na 20

Maana yake ni lakini yeye anatoa mali yake hali ya kutaka radhi ya Mola wake Mtukufu. Maelezo zaidi ya Mola Mtukufu yako katika Sura ya 87.

Aya Na 21

Yaani huyu mchaji zaidi ataridhia yale anayopewa na Mola wake Mtukufu kutokana na malipo mema yaliyo mazuri. Kutaja sifa mbili za Mola na Utukufu, ni kufahamisha kwamba yale malipo anayopewa ni malipo ya neema zaidi na ya utukufu zaidi (juu zaidi) nayo ni yenye kunasibiana na Uungu na Utukufu.

Utafiti Wa Hadith Katika Kafi kutoka kwa Muhammad bin Muslim amesema: "Nilimuuliza Abu jaffar(a.s) kuhusu maneno ya Mwenyezi Mungu: "Naapa kwa usiku unapofunika, na naapa kwa nyota zinapoanguka (zinapokuchwa) " na mifano ya hayo. Akaniambia: "Hakika Mwenyezi Mungu anaweza kuapia chochote anachotaka katika viumbe vyake, lakini viumbe haviwezi kumwapia asiyekuwa Yeye (Mwenyezi Mungu). Imepokewa katika Faqih kutoka kwa Ali bin Mahziyar kutoka kwa Abu Jaffar wa pili(a.s) na katika Tafsiri ya Qummi kuhusu Aya Na kwanza anasema: Ni wakati unapofunikwa mchana, na hicho ni kiapo. Kutoka kwa Humayri naye kutoka kwa Ahmad bin Muhammad naye kutoka kwa Ahmad bin Muhammad bin Abu nasr naye kutoka kwa Abul-Hassan Arridhaa(a.s) kuhusu tafsiri ya Sura ya Al-layl anasema:

"Hakika mtu mmoja alikuwa na mtende katika ukuta wa Mtu mwengine na huyo mwenye mtende alikuwa akimdhuru huyo mwengine; akamshtakia Mtume akaitwa yule mwenye na Mtume akamwambia nipe mtende wako kwa mtende wa peponi, akakataa. Na kulikuwepo mtu mwengine anayeitwa Abu Dahdaah aliyesikia hayo akamwendea mwenye mtende akamwambia niuzie mtende wako kwa ukuta wangu akamuuzia. Abu Dahdaah akwamwendea Mtume akamwambia nimeununua mtende fulani: kwa ukuta wangu. Mtume akamwambia "utapata badala yake mtende katika peponi ndipo akateremsha Mwenyezi Mungu: "Na mwenye kuumba kike na kiume. Hakika matendo yenu ni mbalimbali. Ama mwenye kutoa (yaani mtende) na akamcha Allah na akalisadiki jambo jema (yaani lililo mbele ya Mtume(s.a.w.w) mpaka Aya Na 11.

Katika Tafsiri ya Qummi mwenye kucha Mwenyezi Mungu zaidi ni Abu Dahdaah. Hayo ni kwa upande wa Shia kutokana na Maimamu wa Ahlul Bait. Kwa upande wa Ahli Sunna amepokea Tabrasi katika Majmau kwamba kisa hicho kimepokewa kwa Wahidi naye kutoka kwa Akrama naye kutoka kwa Ibn Abbas kwamba Ansari mmoja alipiga bei na mwenye mtende akaununua kwa mitende arubaini, kisha akampa Mtume naye Mtume akampa mwenye nyumba. Amepokea Tabrasi kutoka kwa Ata kwamba jina la huyo mtu ni Abu Dahdaah. Na amepokea Assuyuti katika Durril Manthur kisa hicho kutoka kwa Ibn Abu Hatim naye kutoka kwa Ibn Abbas, lakini ameifanya dhaifu riwaya hiyo.

Imepokewa tena, katika njia ya Ahli Sunna kwamba Sura hii ilishuka kwa Abu Bakr. Amesema Arrazi katika Tafsiri Kabir: "Wamekongamana wafasiri katika sisi kwamba makusudio katika aya ni Abu Bakr. Anaendelea kusema Arrazi: "Jua kwamba Mashia wote wanakanusha riwaya hii, wanasema imeshuka katika haki ya Ali bin Abu Twalib na dalili juu ya hilo ni juu ya aya inayosema: "Na hutoa zaka na hali yakua wao wanaswali " (5:55).

Kwa hiyo neno lake Mwenyezi Mungu: "Mwenye kumcha (Mungu) zaidi ambaye hutoa mali yake kwa kujitakasa " linaishiria kwenye aya hiyo (5:55).

Ama yale yaliyonasibishwa kwa Mashia wote, yenye kutegemewa katika njia zao ni Sahihi ya Al-Himyariyy iliyotangulia kueleza yaliyo katika riwAya Na nayofahamisha kushuka aya kwa Abu-Dahdaah El- Ansari.

Ndio, imekuja riwaya dhaifu kutoka kwa Barqi naye kutoka kwa Ismail bin Mahraan naye kutoka kwa Ayman bin Muhriz naye kutoka kwa Abu Basiyr naye kutoka kwa Abu Abdillah amesema: Ama kauli yake: Na ataepushwa nao mwenye kumcha (Mungu) zaidi, mwenye kumcha (Mungu) zaidi ni Mtume(s.a.w.w) na wafuasi wake na Ambaye hutoa mali yake kwa (kutaka) kujitakasa, huyo ni Amiirul-Mui'miniin Ali(a.s) na ndiyo kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na wanatoa zaka na hali wao ni wenye kuswali ." (5:55).

Na kuhusu aya "Na hali ya kuwa hakuna yoyote aliyemfanyia hisani ili awe anamlipa " huyo ni Mtume(s.a.w.w) ambaye hana yoyote wa kumlipa hisani na hali hisani zake ni zenye kuenea kwa watu wote.

Riwaya hiyo ni dhaifu kwa upande wa mapitio yake na kufuatilia kwake bila ya kuangalia tafsir. Dalili iliyowazi ya udhaifu wake ni vile kufuatilia kwake kuwa mwenye kusifiwa ni Mtume na sifa iwe juu ya Ali(a.s) kisha aya inayofuatia tena juu ya Mtume. Na kama hilo lingekuwa katika tafsiri ingeliharibika nidhamu yake kabisa. Na huyo Ayman bin Muhriz hajulikani.

Imepokjewa kutoka kwa Al Himyariyy kutoka kwa Ahmad bin Muhammad bin Abu Nasr naye kutoka kwa Abul hassan Arridha(a.s) amesema: Niliulizwa kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Hakika Allah humwongoza anayemtaka na kumpoteza anayetaka. Nikamwambia: Mwenyezi Mungu akufanye uwe mwema "Hakika watu katika watu wetu wanadai mwamba maarifa ni yenye kuchumwa na kwamba wao wakiangalia vizuri wanapata heri". Akakanusha hilo na akasema: "Hawa watu hawachumi heri wao wenyewe, hakuna yeyote katika watu isipokuwa ni wajibu kuwa heri inatokana na yule ambaye heri inatoka kwake.

Ama uongofu ambao makusudio yake ni kufikisha kwenye matakwa, huo ni wa Mwenyezi Mungu kwa sababu ni katika mambo ya Mungu. Ama upotevu ambao makusudio yake ni kupoteza kwa upande wa njia na wala sio kupoteza kwa kuanzia ambako hakuegemezwi kwa Mwenyezi Mungu, ni kwa Mwenyezi Mungu pia, kwa kuwa yeye ni mwenye kuzuwiya kushusha rehema na kukosekana uongofu. Ikiwa uongofu unatokana naye basi kuzuilika nako pia kunatokana naye.

18

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA ADHUHAA (DHUHA)(NA. 93)

INA AYA 11

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu.

وَالضُّحَىٰ ﴿١﴾

1. Naapa kwa mwanzo wa mchana.

وَاللَّيْلِ إِذَا سَجَىٰ ﴿٢﴾

2. Na kwa usiku unapotuwa.

مَا وَدَّعَكَ رَبُّكَ وَمَا قَلَىٰ ﴿٣﴾

3. Hakukuacha Mola wako wala hakukukasirikia.

وَلَلْآخِرَةُ خَيْرٌ لَّكَ مِنَ الْأُولَىٰ ﴿٤﴾

4. Hakika akhera ni bora kwako kuliko ulimwengu.

وَلَسَوْفَ يُعْطِيكَ رَبُّكَ فَتَرْضَىٰ ﴿٥﴾

5. Na atakupa Mola wako utaridhia.

أَلَمْ يَجِدْكَ يَتِيمًا فَآوَىٰ ﴿٦﴾

6. Je, hakukuta ni yatima akakuhifadhi?

وَوَجَدَكَ ضَالًّا فَهَدَىٰ ﴿٧﴾

7. Akakukuta umedangana akakuongoza?

وَوَجَدَكَ عَائِلًا فَأَغْنَىٰ ﴿٨﴾

8. Akakukuta ufakiri akakutajirisha.

فَأَمَّا الْيَتِيمَ فَلَا تَقْهَرْ ﴿٩﴾

9. Basi yatima usimdhalilishe.

وَأَمَّا السَّائِلَ فَلَا تَنْهَرْ ﴿١٠﴾

10. Na mwenye kuoma usimkaripie.

وَأَمَّا بِنِعْمَةِ رَبِّكَ فَحَدِّثْ ﴿١١﴾

11. Na neema ya Mola wako, izungumze.

UBAINIFU

Inasemekana kuwa Mtume(s.a.w.w) alikatikiwa na wahyi kwa siku kadhaa mpaka watu wakawa wanasema: "Hakika Mola wake amemwachilia mbali". Basi ndio akateremsha Mwenyezi Mungu Sura hii kuituliza nafsi yake. Sura hii inawezekana kuwa imeshuka Makka au Madina.

Aya Na 1-2

Maana ya neno Dhuhaa ni kuangaza jua na kuenea mchana na neno Sajaa nikutulia yaani kuingia giza.

Aya Na 3

Ni jawabu la kiapo. Mnasaba wa nuru ya mchana na giza la usiku kwa kushuka wahyi na kukatika kwake uko dhahiri.

Aya Na 4

Maana yake kutokana na inavyofahamisha aya iliyotangulia ni kama vile anaambiwa Mtume: Yale uliyonayo miongoni mwa fadhila na rehema ni muda wa kuwa uko hai katika dunia na uhai wako wa akhera ni bora kwako kuliko maisha yako ya dunia.

Aya Na 5

Ni uthibitisho wa aya iliyotangulia na imekusanya kiaga cha kutoa kutakakofuatiwa na kuridhia. Imesemwa aya hii inaangalia pande zote mbili (maisha ya dunia na akhera) na wala sio akhera tu!

Aya Na 6

Inaishiria baadhi ya neema zake Mwenyezi Mungu kwa Mtume; alifiwa na baba yake akiwa tumboni mwa mama yake, kisha akafa mama yake akiwa na miaka miwili, tena akafa (mlezi wake) babu yake naye akiwa na miaka minane, basi ndio akachukuliwa na ami yake kumlea. Inasemekana makusudio ya yatima hapa ni yule mtu aliye peke yake. Kwa hiyo maana inakuwa; Je hakukuta peke yako kati ya watu, akawakusanya watu kwako?

Aya Na 7

Makusudio ya neno Dhwallan ni kudangana kukosa ungofu na makusudio ya kudangana kwake Mtume(s.a.w.w) ni ila hali ya kukatikiwa na ungofu wake Mwenyezi Mungu Mtukufu na hapana uongofu kwa Mtume(s.a.w.w) wala kwa yoyote katika viumbe ila kwa msaada wa Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo nafsi yake ilikuwa imedangana, ijapokuwa uongofu wa Mwenyezi Mungu ni wenye kulazimiana naye. Aya hii iko katika maana na aya inayosema: "Ulikuwa hujui kitabu nini wala imani " (42:52).

Vile vile iko katika maana ya neno la Musa, kama anavyosimulia Mwenyezi Mungu katika Qur'an. "nimeyafanya hayo nilipokuwa miongoni mwa waliodangana ." (26:20) yaani wakati bado sijapata uongofu wa utume.

Yanakurubia maana hayo na yale yaliyosemwa kuwa makusudio ya Dhwallan ni kuondokewa na elimu (kutokujua) kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu."..ili kama mmoja wao akipotea, mmoja wao amkumbushe mwengine " (2:282).

Hayo yanatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu: "na hakika ulikuwa kabla ya haya ni miongoni mwa wasio na habari hizi ." (12:3).

Imesemwa maana yake ni akakukuta umepotea kati ya watu hawajui haki yako akawaongoza kwako na akawajulisha kuhusu wewe.

Imesemwa ni ishira ya kupotea njia ya Makka alipokuwa mdogo. Pia imesemwa ni ishara ya kupotea kwake ndani ya msafara wa Maysara mtumishi wa Khadija, wakati alipokwenda Sham pamoja na ami yake, Abu Twalib. Na yamesemwa zaidi ya hayo ni hizo zote ni njia dhaifu.

Aya Na 8

Fukara ni yule ambaye hana mali. Alikuwa Mtume(s.a.w.w) ni fukara akatajirishwa na Mwenyezi Mungu baada ya kumuoa Bibi Khadija ambaye alikuwa na mali nyingi akampa Mtume.

Aya Na 9-11

Aya zote hizi tatu zinatokana na aya zilizotangulia na zinataja wema wake Mwenyezi Mungu (s.w.t), ni kama anasema: "Umeyapata yale yanayompata yatima katika udhalili na upweke kwa hiyo basi usimdhalilishe yatima kwa kuidhalilisha nafsi yake au mali yake." Na mara nyingi umeipata haja ya mwenye kupotea vile anavyohitajia uongofu na fakiri anavyohitajia utajiri, basi usimkaripie mwenye kuomba kuondolewa haja yake ya uongofu au maisha. Vile vile umeona kuwa neema ulizonazo amekuneemesha Mola wako kwa ukarimu wake, basi ishukuru neema yake kwa kuizungumza wala usiifiche. Maamrisho yote haya ni kwa watu wote ingawaje yanaelekezwa kwa Mtume.

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu neno la Mwenyezi Mungu Dhuhaa anasema ni wakati wa kupanda jua na Sajaa anasema ni wakati wa giza. Na kuhusu neno la Mwenyezi Mungu Maqalaa anasema ni "hakukukasirikia". Katika Durril Manthur kuhusu Aya Na tano, ametoa Ibn Abu Shayba kutoka kwa Ibn Masud amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) "Sisi Ahlul Bait Mwenyezi Mungu ametuchagulia akhera kuliko dunia ."

Katika hiyo hiyo Durril Manthur ametoa Askary katika Mawaidh, Ibn Laali na Ibn Najjar kutoka kwa Jabir bin Abdillahi amesema; "Mtume(s.a.w.w) aliingia kwa Fatima akiwa anatwanga kwa jiwe huku amevaa nguo za sufu za ngamia". Alipomwangalia akasema: "Ewe Fatima fanya haraka umeze uchungu wa dunia kwa neema na akhera kesho." Akateremsha Mwenyezi Mungu aya hiyo ya tano. Riwaya hii inachukulia kuwa aya hiyo ilishuka peke yake baada ya kushuka aya zilizo kabla yake katika Sura hii kisha kuunganishwa. Kuna uwezekano wa Aya hiyo kushuka peke yake kwa mara nyingi.

Katika hiyo hiyo Durril Manthur ametoa Ibn El Mundhir,Ibn Murdawayh na Abu naim katika Hilyat kutoka katika njia ya Harb bin Sharih amesema:"Nilimwambia Abu jaffar Muhammad bin Ali bin Hussein(a.s) unaonaje hii Shafaa (uombezi) wanayoizungumzia watu wa Iraq ni kweli? Akasema: "Kabisa Wallah". Alinizungumzia Ami yangu Muhammad bin El-Hanafiya kutoka kwa Ali kwamba Mtume(s.a.w.w) alisema: "nitauombea shafaa umati wangu mpaka Mola wangu anisemeshe: Umeridhika ewe Muhammad? Na nisema: Ndio ewe Mola wangu nimeridhika." Kisha akanikabili na kuniambia: "Hakika nyinyi watu wa Iraq mnasema: Hakika aya yenye kutarajiwa zaidi katika kitabu cha Mwenyezi Mungu ni ile inayosema: "Sema, enyi waja wangu mliojidhulumu nafsi zenu! Msikate tamaa na Rehema ya Allah; Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote " (39:53). Nikasema ndio sisi tunasema hivyo. Akasema: Basi sote sisi Ahlul Bait tunasema: "Hakika aya inayotarajiwa zaidi katika kitabu cha Mwenyezi Mungu ni ile inayosema: "Na atakupa Mola wako nawe utaridhia". Yaani uombezi. (Aya Na tano katika Sura hii).

Katika Tafsiri ya Burhan kutoka kwa Baabwayh kwa isnadi ya Ibn Jaham kutoka kwa Ridhaa(a.s) katika kikao pamoja ya Maamun alisema huyo Ridhaa; "Anasema Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumwambia Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) . "Je hakukuta ni yatima akakuhifadhi?" Anasema: "Je hakukuta peke yako akakusanyia watu? Na akakukuta umedangana yaani mbele ya watu wako "akakuongoa" yaani akawongoa watu wakakufahamu. Na akakukuta ufakiri akakutajirisha". Anasema "akakutajirisha kwa kujaalia dua yako ni yenye kutakabaliwa?" Akasema Maamun: "Mwenyezi Mungu akubarikie ewe mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu".

Katika hiyo hiyo Tafsiri ya Burhan kutoka kwa Barqi kwa isnadi yake kutoka kwa Amru bin Abu Nasr amesema: Alinizungumzia mtu mmoja katika watu wa Basra akasema: "Nilimuona Hussein bin Ali(a.s) na Abdallah bin Umar wanatufu Al-Kaaba. Nikamuuliza Ibn Umar: Kuhusu neno lake Mwenyezi Mungu "Na neema ya Mola wako izungumze", Akasema : "Ni kuzungumza aliyoneemesha Mwenyezi Mungu." Kisha nikamuuliza Hussein bin Ali(a.s) akasema: "Nikuzungumza aliyoneemesha Mwenyezi Mungu katika dini yake." Katika Durril Manthur kutoka kwa Bayhaqi naye kutoka kwa Hassan bin Ali kuhusu ayay hiyo ya 11 akasema: "Ukipata heri wazungumzie ndugu zako".

Katika hiyo Durril Manthur ametoa Abu Dawud kutoka kwa Jabir bin Abdillahi kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) amesema: "Mwenye kujaribiwa kwa kupewa misukosuko akaizungumza, hakika huyo amemshukuru Mwenyezi Mungu, na mwenye kuficha atakuwa amemkanusha (uweza) wa Mwenyezi Mungu. Na mwenye kujinasibishia asilokuwa nalo, hakika yeye ni kama amevaa nguo za uzushi.

11

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA TARIQ (CHENYE KUJA USIKU) (NA. 86)

INA AYA 17

Kwa Jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu.

وَالسَّمَاءِ وَالطَّارِقِ ﴿١﴾

1. Naapa kwa mbingu na chenye kuja usiku.

وَمَا أَدْرَاكَ مَا الطَّارِقُ ﴿٢﴾

2. Na lipi la kukujulisha ni nini chenye kuja siku.

النَّجْمُ الثَّاقِبُ ﴿٣﴾

3. Ni nyota inayong'ara usiku.

إِن كُلُّ نَفْسٍ لَّمَّا عَلَيْهَا حَافِظٌ ﴿٤﴾

4. Hakuna nafsi isipokuwa kuna mwenye kuitunza.

فَلْيَنظُرِ الْإِنسَانُ مِمَّ خُلِقَ ﴿٥﴾

5. Basi mtu na ajitazame ameumbwa kwa kitu gani..

خُلِقَ مِن مَّاءٍ دَافِقٍ ﴿٦﴾

6. Ameumbwa kwa maji yanayotoka kwa nguvu.

يَخْرُجُ مِن بَيْنِ الصُّلْبِ وَالتَّرَائِبِ ﴿٧﴾

7. Yanayotoka baina ya uti wa mgongo na mifupa ya kifua.

إِنَّهُ عَلَىٰ رَجْعِهِ لَقَادِرٌ ﴿٨﴾

8. Hakika yeye ni mweza wa kumrejeza.

يَوْمَ تُبْلَى السَّرَائِرُ ﴿٩﴾

9. Siku zaitakapofunuliwa siri.

فَمَا لَهُ مِن قُوَّةٍ وَلَا نَاصِرٍ ﴿١٠﴾

10. Basi hatakuwa na nguvu wala wa kumnusuru.

وَالسَّمَاءِ ذَاتِ الرَّجْعِ ﴿١١﴾

11. Naapa kwa mbingu yenye kurudi.

وَالْأَرْضِ ذَاتِ الصَّدْعِ ﴿١٢﴾

12. Na ardhi yenye mipasuko.

إِنَّهُ لَقَوْلٌ فَصْلٌ ﴿١٣﴾

13. Hakika hii (Qur'an) ni kauli yenye kupambanua.

وَمَا هُوَ بِالْهَزْلِ ﴿١٤﴾

14. Wala si upuuzi.

إِنَّهُمْ يَكِيدُونَ كَيْدًا ﴿١٥﴾

15. Hakika wao wanakuchimbia vitimbi.

وَأَكِيدُ كَيْدًا ﴿١٦﴾

16. Nami (pia) ninawachimbia vitimbi.

فَمَهِّلِ الْكَافِرِينَ أَمْهِلْهُمْ رُوَيْدًا ﴿١٧﴾

17. Basi wape muhula makafiri wape muhula kidogo.

UBAINIFU

Katika Sura hii kuna maonyo kwa marejeo ya akhera na kufufuliwa. Na hayo yanafamisha uwezo wake Mwenyezi Mungu. Na inamalizia Sura kwa kueleza kiaga cha makafiri. Sura hii imeshuka Makka bila ya ubishi.

Aya 1-3

Neno Twariq asili yake- kama ilivyosemwa- ni kugonga kiasi cha kutoa sauti, miongoni mwao, ni nyundo na lina maana njia. Njia imeitwa hivyo kwa vile mpita njia anaigonga kwa nyayo zake. Kywa hivyo likaenea neno hilo kutumiwa kwa njia, kisha likahusishwa na kuja usiku, kwa sababu mwenye kuja usiku aghlabu hukuta milango imefungwa, kwa hiyo hugonga, kisha likaenea hilo neno kwa kila chenye kuhidhiri usiku. Makusudio ya neno hilo katika aya ni nyota yenye kutokeza usiku. Neno Thaqb asili yake ni kupasua; kisha likawa ni nuru yenye kuangaza, kwa sababu inapasua giza, na linakuja kwa maana ya kuwa juu kama kusema: imepaa juu ndege, nikama vile inapasua anga kwa kuruka kwake. Kwa hivyo makusudio ya Aya Na kwanza ni kuapa kwa mbingu na nyota inayotokeza usiku. Na Aya Na pili ni kwa ajili ya kulikuza jambo la chenye kuapiwa ambacho ni hicho chenye kutokeza usiku. Aya Na tatu ni ubainifu wa hicho chenye kutokeza usiku. Jumla hiyo ni jawabu ya swali.

Aya Na 4

Ni jawabu la kiapo. Herufi Lamma ni kwa maana ya illa (isipokuwa). Makusidio ya kutunza hapa ni kuandika matendo yake mema na maovu, ili yaweze kuhisabiwa siku ya Kiyama na kulipwa. Kwa hivyo mtunzaji ni malaika na chenye kutunzwa ni matendo, kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na hakika mna wenye kuwatunza watukufu wenye kuandika ." (82:10-11).

Sio mbali kuwa makusudio ni kutunza nafsi dhati yake na vitendo vyake, kwa hiyo inafahamisha kuwa nafsi ni zenye kutunzwa hazimaliziki kwa mauti wala haziharibiki mpaka Mwenyezi Mungu atakapovifufua viwiliviwili, atavirudisha nafsi na atakuwa mtu kama alivyokuwa mtu wa duniani kwa dhati yake; kisha alipwe kwa mujibu wa vitendo vyake vyenye kuchungwa, vikiwa ni kheri au shari. Hilo linatiliwa nguvu na aya nyingi zinazofahamisha juu ya kutunzwa vitu, kama vile kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Sema atawaua Malaika wa mauti aliye wakilishwa kwenu kisha mtarejeshwa kwa Mola wenu. " (32:11).

"Allah huzichukua roha wakati wa mauti yake na zile zisizokufa katika usingizi wao. Basi huzizuwiya zile alizozihukumia mauti. ." (39:42).

Hayo hayakanushi dhahiri ya Aya Na Sura ya (82:10).

kuwa kutunza kwa Malaika ni kuandika, kwa sababu kuitunza nafsi pia kutokana na kuandika kama anavyofahamisha Mwenyezi Mungu kwa kusema: "Hakika sisi tulikuwa tukiandika yale aliyokuwa mkiyatenda ." (45:29).

Kwa njia hii kunabatilika kutia makosa juu ya yale yanayofahamisha juu ya marejeo ya Kiyama katika kuenea Kudura, kwamba kumrusisha mtu kwa dhati yake ni muhali kwa sababu mtu ataumbwa tena mara ya pili mfano wa yule mtu wa duniani aliyeumbwa kwanza, lakini si yule yule na mfano wa kitu sio kitu chenyewe. Njia ya kubatilisha hoja hiyo ni kwamba: utu wa mtu unatokana na mtu kwa nafsi yake sio kwa kiwilikiwili chake na nafsi ni yenye kihifadhiwa kwa hivyo akiumba kiwilikiwili na kukifungamanisha na nafsi atakuwa ndiya yule yule mtu wa duniani kwa utu wake, ijapokuwa sio dhati yake.

Aya Na 5

Yaani aangalie nini mwanzo wa umbile lake? Na ni kitu gani ambacho Mwenyezi Mungu amekifanya kuwa mtu? Jumla hii ni mtiririko wa aya iliyotangulia. Maana yanavyofahamisha kutokana na mpangilio wake, ni kwamba, ikiwa kila nafsi ni yenye kuhifadhiwa kwa dhati yake na vitendo vyake, bila ya kwisha hiyo nafsi na kusahauliwa vitendo vyake basi akubali mtu ukweli kwamba yeye atarudi kwa Mola wake na kulipwa aliyoyatenda, wala hilo asilihisabu kuwa ni mbali. Naangalie ukweli huu kwenye asili ya umbile lake na akumbuke kwamba yeye ameumbwa kwa maji yanayoka kwa nguvu yanayotoka baina ya uti wa mgongo na mifupa ya kifua. Basi yule aliyeanza kumuumba kutokana na maji haya anaweza kumrudisha na kumuhuisha baada ya mauti.

Aya Na 6

Maji yenye kutoka kwa kuruka ni manii. Jumla hiyo iko katika jawabu la swali.

Aya Na 7

Neno Sulb lina maana ya mgongo na Taraib ni mifupa wa kifua. Wamehitalifiana kiajabu kwenye matamko yao katika aya hii na iliyo kabla yake. Kwa dhahiri makusudio yake ni sehemu iliyokatikati ya uti wa mgongo na mifupa ya kifua.

Aya Na 8

Yaani ambaye amemuumba mtu kutokana na maji, sifa yake ni hiyo hiyo, ni mwenye kuweza kumrudisha na kumuhuisha baada ya mauti.

Aya Na 9: Ni siku yatakayofichuka yale alioyoyaficha mtu na kuyafanya siri katika itikadi na matendo ya kheri au ya shari. Aya hii iko katika maana ya aya inayosema "Na mkidhihirisha yaliyomo katika nyoyo zenu au mkiyafichua, Allah atawataka hisabu ya (yote) hayo ." (2:284)

Aya Na 10

Hana uwezo katika nafsi yake utakaomzuia na adhabu ya Mwenyezi Mungu wala hana wa kumnusuru atakayemkinga na adhabu yaani hakutakuwa na uwezo wowote utakaomkinga na shari kutoka kwake au kwa mtu mwengine.

Aya Na 11

Kiapo baadha ya kiapo, ni kwa ajili ya kutilia mkazo jambo la Kiyama na kurejea kwa Mungu. Makusudio ya kurudi ni kuhisi kwenda kwake kwa kuchimbuka nyota na kutua. Imesemwa kuwa makusudio yake ni mvua. Makusudio ya kupasuka ni kupasuka kwa ajili ya mimea.

Aya Na 12-13

Maana ya neno Fasl ni kupambanua kati ya vitu viwili. Aya hizi mbili ni jawabu la kiapo kwa maana; ninaapa kwa hivyo nilivyoviapia hakika Qur'an ni neno lenye kupambanua kati ya haki na batili na sio maneno yasiyokuwa na maana. Yale inayoyahakikisha ni haki isiyokuwa na shaka na yale inayoya batilisha ni batili isiyokuwa na shaka. Kwa hiyo yale iliyoyatolea habari katika ufufuo na marejeo ni haki isiyokuwa na shaka ndani yake. Imesemekana kuwa dhamiri katika neno Innahu ni ya hayo yaliyotangulia kuelezwa katika habari ya marejeo lakini tuliyoyaeleza mwanzo ndiyo yanayoelekea zaidi.

Aya Na 15

Yaani makafiri wanaichimba vitimbi wakikusudia kuizima nuru ya Mwenyezi Mungu na kubatilisha mlingano wako.

Aya Na 16

Ikiwa wao wanavyo vitimbi na mimi ninavyo vitimbi. Na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kushinda juu ya jambo lake, kwa hivyo wangojee tu; wala usifanye haraka, ngoja kidogo tu! Yatawajia yale waliyoahidiwa, na kila linalokuja liko karibu.

Utafiti Wa Hadithi Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu "Hakika kila nafsi ina mwenye kuichunga" amesema ni Malaika. Na kuhusu "Ameumbwa kwa maji yanayotoka kwa nguvu" amesema ni manii ambayo hutoka kwa nguvu". Kuhusu "yanayotoka kati ya uti wa mgongo na mifupa ya kifua" amesema uti wa mgongo ni mwanaume na mifupa ya kifua ni mwanamke. Katika Majmau imepokewa hadith marfuu kutoka kwa Abu Dardai amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) :Amedhamini Mwenyezi Mungu kuumba kwake vitu vine: Swala, Zaka, Kufunga Ramdhan na kuoga janaba na hizo ndizo siri alizozisema Mwenyezi Mungu "Siku itakayofunuliwa siri ."

Huenda ikawa maana ya hadithi hiyo ni kutaja baadhi ya mambo ya ukweli, kama inavyotilia nguvu hilo hadithi inayofuata. Katika hiyo hiyo Majmau kutoka kwa Muadh bin Jabal amesema: "Nilimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu: ni siri zipi ambazo Mwenyezi Mungu atawafunuliwa waja katika akhera? Akasema siri zenu ni matendo yeno ya swala, kufunga, zaka, udhu, kuoga janaba na kila lenye kufaradhiwa, kwa sababu matendo yote ni siri yenye kufichamana, mtu akitaka anaweza kusema ameswali na asiwe ameswali au aseme ametawadha kumbe hakutawadha. Basi ndiyo kusema kwake Mwenyezi Mungu "siku itakayofunuliwa siri."

Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kauli yake Mwenyezi Mungu: "Basi hatakuwa na nguvu wala wa kumnusuru." Amesema: hatakuwa na nguvu yoyote kwa muumba wake wala wa kumnusuru kama Mwenyezi Mungu akimtakia uovu. Katika hiyo Tafsiri ya Qummi amesema kuhusu neno Raj'n amesema ni mvua na ardhi yenye mipasuko ni ardhi yenye mimea. Katika Majmau kuhusu : "hakika hii Qur'an ni kauli ya haki" amesema "Hakika Qur'an inapambanua kati ya haki na batili kwa kuibainisha kila moja. Hayo yamepokewa kutoka kwa Imam Assadiq(a.s) .

Katika Durril Manthur ametoa Ibn Abi Shayba, Addarami, Tirmdhi, Muhammad bin nasr na Ibn el- Ambari katika Masahif kutoka kwa Harith el-Aa'war amesema: Niliingia msikitini mara watu wakaingia katika mazungumzo. Nikamwendea Ali nikampa habari; akasema: "Je wamekwishafanya? Mimemsikia Mtume(s.a.w.w) akisema: "Kutatokea fitna. Nikasema: Ni kitu gani cha kutokea katika fitna hiyo Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Je ni sawa hapa? Akasema:kitabu cha Mwenyezi Mungu kina habari za kabla yenu baada yenu na kimekwisha wahukumia, ni upambanuzi na sio upuuzi, mwenye kukiacha Mwenyezi Mungu kumuangamiza, mwenye kukusudia pengine Mwenyezi Mungu humpoteza .

Ni kamba madhubuti, mauidha yenye hekima na njia yenye kunyooka. Ni ambachi hakipotezi wala hawashibi nacho wanavyuoni, hazitatiziki nacho ndimi wala haiishi ajabu yake. Ndicha ambacho majini waliposikia walisema: " Hakika tumesikia Qur'an ya ajabu inaongoza kwenye uongofu." Mwenye kusema kwacho huwa mkweli, mwenye kuhukumu kwacho amefanya uadilifu na mwenye kuganya amali kwacho amepata thawabu, na mwenye kulingania kwenye kitabu hicho ameongoka katika njia iliyonyooka. Amepokea karibu na maana hayo Muadh bin Jabal kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

12

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA A'ALAA (MTUKUFU) (NA. 87)

INA AYA 19

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu.

سَبِّحِ اسْمَ رَبِّكَ الْأَعْلَى ﴿١﴾

1. Litakase jina la Mola wako aliye Mtukufu.

الَّذِي خَلَقَ فَسَوَّىٰ ﴿٢﴾

2. Ambaye ameumba (kila kitu) akakiweka sawa.

وَالَّذِي قَدَّرَ فَهَدَىٰ ﴿٣﴾

3. Na ambaye amekadiria (kila kitu) na akakiongoza.

وَالَّذِي أَخْرَجَ الْمَرْعَىٰ ﴿٤﴾

4. Na ambaye ameotesha malisho.

فَجَعَلَهُ غُثَاءً أَحْوَىٰ ﴿٥﴾

5. Kisha akayafanya makavu yenye kupiga weusi.

سَنُقْرِئُكَ فَلَا تَنسَىٰ ﴿٦﴾

6. Tutakusomesha wala hutasahau.

إِلَّا مَا شَاءَ اللَّـهُ إِنَّهُ يَعْلَمُ الْجَهْرَ وَمَا يَخْفَىٰ ﴿٧﴾

7. Ila anachopenda Allah. Hakika yeye anayajua yaliyowazi na yaliyofichika.

وَنُيَسِّرُكَ لِلْيُسْرَىٰ ﴿٨﴾

8. Tutakusahilishia njia nyepesi.

فَذَكِّرْ إِن نَّفَعَتِ الذِّكْرَىٰ ﴿٩﴾

9. Basi waidhisha ikiwa utafaa waadhi.

سَيَذَّكَّرُ مَن يَخْشَىٰ ﴿١٠﴾

10. Atawaidhika nao mcha (Mungu).

وَيَتَجَنَّبُهَا الْأَشْقَى ﴿١١﴾

11. Na atajiepusha nao asiyemcha.

الَّذِي يَصْلَى النَّارَ الْكُبْرَىٰ ﴿١٢﴾

12. Ambaye atauingia moto mkubwa..

ثُمَّ لَا يَمُوتُ فِيهَا وَلَا يَحْيَىٰ ﴿١٣﴾

13. Kisha humo hatakufa wala hatokuwa hai.

قَدْ أَفْلَحَ مَن تَزَكَّىٰ ﴿١٤﴾

14. Hakika amekwishafaulu mwenye kujitakasa.

وَذَكَرَ اسْمَ رَبِّهِ فَصَلَّىٰ ﴿١٥﴾

15. Akakumbuka jina la Mola wake na akaswali.

بَلْ تُؤْثِرُونَ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا ﴿١٦﴾

16. Lakini nyinyi mnapenda zaidi maisha ya ulimwengu.

وَالْآخِرَةُ خَيْرٌ وَأَبْقَىٰ ﴿١٧﴾

17. Hali akhera ni bora na yenye kubaki.

إِنَّ هَـٰذَا لَفِي الصُّحُفِ الْأُولَىٰ ﴿١٨﴾

18. Hakika hAya Na mo katika vitabu vya kwanza.

صُحُفِ إِبْرَاهِيمَ وَمُوسَىٰ ﴿١٩﴾

19. Vitabu vya Ibrahim na Musa.

UBAINIFU

Ni amri ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu juu ya yale yanayoelekeana na upande wake Mtukufu na kuitakasa dhati yake tukufu na kutaja pamoja na jina lake Mtu mwengine au kutegemeza kwa mwengine yale yanayopasa kutegemezwa kwake, kama kuumba kuangalia vizuri mambo na kuruzuku. Na nikiaga chake kwa Mtume kwa kumpa nguvu kwa elmu, hifadhi na kummakinisha katika njia ambayo ni nyepesi kwa tabligh na inayonasibiana zaidi na mlingano. Mpangilio wa aya katika mwanzo wa Sura ni mpangilio wa ki Makka. Ama mwisho wake yaani kuanzia Aya Na 14 mpaka mwisho wa Sura, imepokewa katika njia ya Maimamu wa Ahlul Bait vile vile katika njia ya Ahli Sunnah kwamba, makusudio yake ni zaka ya fitr, na swala ya Idd, na ni maalum kuwa saumu na yanayofuatia saumu miongoni mwa zaka ya fitr na swala ya Idd ilianzishwa Madina baada ya Hijra. Hivyo zitakuwa aya za mwisho zimeshuka Madina. Katika hiyo Sura mwanzo wake ni Makka na mwisho wake ni Madina, wala hayo hayakanushi yale yaliyokuja kuwa Sura imeshuka Makka, kwani ilivyo nikuwa haikataliki kuchukulia hivyo mwanzo wa Sura.

Aya Na 1

Ni amri ya kulitakasa jina lake Mwenyezi Mungu S.W.T. na kulitukuza. Na kwa vile hapa kutakaswa Mwenyezi Mungu kumefungamanishwa na jina yake, basi huko kumtakasha kunamaanisha asitajwe yeyote ambaye yeye Mwenyezi Mungu ametakata naye. Kwa sababu jina linatokea katika kusema. Hivyo isitajwe pamoja na jina lake miungu wengine washirikina, waombozi na kuwanasibishia uungu. Na vile vile kama kutaja baadhi ya yanayohusika naye Mwenyezi Mungu (s.w.t) kama kuumba kupatisha, kuruzuku, kuhuisha na kufisha na mfano wake kwa kuyanasibisha kwa asiyekuwa yeye Mwenyezi Mungu Au kama kutaja baadhi ya yasiyofanana na upande wa utakatifu wake, katika vitendo kama kushindwa, ujinga, dhuluma, mghafala na mfano wake katika sifa za upungufu na aibu kwa kuyanasibisha kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t).

Kwa ujumla kulitakasa jina lake ni kuepuka kauli na kutaja yasiyonasibiana kuyataja kwake na jina lake Mwenyezi Mungu (s.w.t), na huko ni kumtakasa katika kiwango cha kauli kwenye kuafikiana na kumtakasa kwake katika kiwango cha kitendo. Hiyo inalazimisha Tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu) iliyo kamili kwa kukanusha kumshirikisha Mwenyezi Mungu kuliko waziwazi; kama ilivyo katika kusema kwake Mwenyezi Mungu:

"Na anapotajwa Allah peke yake nyoyo za wale wasioamini akhera, huchukiwa na wanapotajwa wale walio kinyume naye, mara wanafurahi ". (39:45).

Na pia kusema kwake: "Na unapomtaja Mola wako katika Qu'ran peke yake, basi wao hugeuza migongo yao kwa kuchukia ." (17:46).

Kutegemeza jina Mola kwa dhamiri ya mwenye kusemeshwa (jina la Mola wako) ni kutilia nguvu yale tuliyotangulia kuyataja, kwani maana ni litakase jina la Mola wako ambaye umemfanya ni Mola na wewe unalingania kuwa yeye ni Mola wa waungu, basi isitokee katika maneno yako pamoja na kutaja jina lake kwa uungu wake na kutaja mwengine, kwa kiasi ambacho kitakanusha kumwita Mungu kama alivyojijulisha kwako.

Kusemwa kwake: Mtukufu ni ambaye yuko juu ya aliye juu na kushinda kila kitu, hiyo ni sifa ya Mola wako yaani litakase jina lake kwa sababu yeye ni Mtukufu zaidi. Imesemwa kuwa maana ya aya hii ni kusema "Subhana rabial aala" hayo ni kutoka kwa Ibn Abbas, pia amesema, ni kuswali. Imesemwa makusudio ni jina vile, anavyoitwa yaani mtakase Mwenyezi Mungu S.W.T. na kila sifa na vitendo visivyofanana naye. Imesemwa kuwa makusudio ni kuyatakasa majina yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) na yale yasiyofanana naye wala haitwi asiyekuwa yeye na jina linalomhusu yeye Mwenyezi Mungu, wala halitamkwi katika mahali pasipo nasibiana naye kama chooni n.k. Yale tuliyotanguliza kuyataja katika maana ndiyo mapana zaidi na yenye kukusanya zaidi maana na ndiyo yanayonasibiana zaidi na aya inayosema "tutakusomesha wala hutasahau" na "tutakusahilishia njia nyepesi". Kwa sababu mpangilio ni wa kupewa utume mpaka kwenye ukumbusho na tabligh. Hivyo ikaanzwa kwa maneno yake Mtume(s.a.w.w) ya kumtakasa na kila linalo tambulisha shirika kwa uwazi au kwa undani. Akamwahidi mara ya pili kumsomesha kiasi ambacho hataweza kusahau chochote katika yale aliyopewa Wahyi na kusahilishiwa njia ya Tabligh.

Aya Na 2

Kuumba kitu ni kukusanya mafungu yake na kuyapanga sawasawa kiasi ambacho huwekwa kila kitu mahali pake panapo nasibiana napo na kukipa haki yake, kama kuweka kila kiungo katika viungo vya binadamu mahali panapo nasibu. Ayah ii mpaka mwisho wa Aya Na nne zinasifu mipangilio mizuri, ya Mungu na hayo ni dalili ya uungu wake Mwenyezi Mungu (s.w.t)

Aya Na 3

Yaani ni kuvifanya vitu alivyoviuumba juu ya kiasi mahususi na mipaka yenye kuonyesha dhati zake na sifa zake na vitendo vyake visivyozidi kipimo chake na akaviandaa na yale yanayonasibiana na yaliyokadiriwa. Kwa hiyo kila mmoja anafuata upande wa yale yaliyokadiriwa kwake, kwa uongozi wa Mungu, kama mtoto kuendea titi la mama yake, kifaranga kutegemea riziki ya mama yake, mwanamume kwa mwanamke na mifano ya hayo. Mwenyezi Mungu anasema:"Na hakuna kitu chcochote ila hazina yake iko kwetu wala hatukukiteremsha ila kwa kipimo maalum ." (15:21).

Amesema tena: "Kisha akamfanyis nyepesi njia " (80:20). Amesema tena: "Kila mmoja ana mwelekeo wake wa kuelekea ." (2:148).

Aya Na 4 -5

Kutoa malisho kwa ajili ya chakula kisha kuyafanya makavu meusi ni katika usadikisho wa mipangilio ya Mungu na dalili zake; kama ilivyo katika kuumba, kulinganisha sawa, kukadiri na uongozi.

Aya Na 6-7

Amesema katika Mufradati: "Kusoma ni kukusanya herufi na matamko pamoja katika kusoma, lakini sio mkusanyiko wowote ni kusoma, huwezi kusema umewasoma watu, kama ukiwakusanya." Hiyo inafahamisha kuwa hakuwezi kuitwa kusoma kwa herufi moja. Katika Majmau anasema kusomesha ni kuchukua kisomo kwa msomaji kwa kumsikiliza ili usahihishe makosa.

Kumsomesha kwake Mtume, sio kama vile tunavyosemeshana sisi kwa kumsikiliza msomaji kisha kumsahihisha anayoyakosa. Haikuwa kwa Mtume kusoma chochote katika Qur'an akakikosea au asahau wahyi kisha asome ndipo arekebishwe la, bali makusudio yake ni kumwezesha Mtume (SAWW) kuisoma Qur'an kama ilivyoteremsha bila ya kuibadilisha, kwa kuzidisha kitu au kupunguza au kuifanya kombo kwa sababu ya kusahau. Kwa hivyo kauli yake Mwenyezi Mungu tutakusomesha hutasahau ni kiaga kitokacho kwake Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kumuwezesha kuijua Qur'an na kuifikisha kama ilivyoteremshwa, kiasi ambacho hataisahau. Huo ni msingi wa kufikisha wahyi (ufunuo) kama iluvyofunuliwa. Kusema kwake "Ila anachopenda Allah, ni kuvua kunakofahamisha uwezo wa Mungu ulio huru na kwamba kipawa hiki cha kutosahau sio kuwa Mungu amelazimika macho. Yeye anao uwezo wa kukusahaulisha kama akitaka.

Ayah ii kwa mpangilio wake, haiepukani kuwa inatilia nguvu yale yaliosemwa kwamba Mitume(s.a.w.w) alipokuwa akiletewa wahyi (ufunuo) na Jibril humsomea kwa kuogopa kusahau, ikawa Jibril akimaliza tu naye huanza. Basi iliposhuka ayah ii hakusahau kitu baadaye. Inakurubia kuzingatia kuwa ayah ii tutakusomesha hutosahau ilishuka kwanza ndipo ikashuka aya inayosema: "Usiutikise ulimi wako kwa (kuufanyia haraka) wahyi kwa hakika ni juu yetu kuukusanya na kuusomesha. Wakati tunapokusomea, basi fuata kusomwa kwake, kisha ni juu yetu kuubainisha ". (75:17-19).

Kisha aya inayosema: Usiifanyie haraka (hii) Qur'an kabla haujamalizika wahyi (ufunuo) wake, Na (uombe) useme. Mola wangu nizidishie elimu" (20:114).

Kusema kwake "Hakika anajua yaliyowazi na yaliofichika" kuwa wazi ni kwa kuona au kusikia kama Qur'an inavyosema: "Wakasema tuonyeshe Mungu waziwazi ". (4:153).

"Hakika yeye anajua kauli iliyo dhahiri ". (21:110) Jumla ya aya iko katika mahali pa sababu kwa maana tutakufanyia uzuri katika kupokea wahyi (ufunuo) na kuuhifadhi kwa sababu sisi tunajua dhahiri na ndani ya hali yako na vile unavyojihimu katika jambo la wahyi na unavyopupia twaa katika yale uliyoamrishwa.

Aya Na 8

Wepesi ni sifa yenye kusimama mahali pa msifiwa yaani njia nyepesi, kwa maana ya kuwa daima tutakufanyia njia ya tabligh ni nyepesi kwa maneno na vitendo utaongoza watu na itatimia hoja kwa wengine na utafanya subira juu ya maudhi yao.

Aya Na 9

Ni mtiririko wa amri iliyotangulia ya kulitakasa jina la Mola wake kuahidiwa kwake kusomeshwa wahyi kiasi ambacho hatasahau, na kusahilishiwa njia nyepesi, hizo ni sharti za kidharura ambazo zinaweza kuzuwia kufaulu mlinganio wa kidini. Maana ni kuwa ukitimiza amri ya kufuata yale tuliyokuamrisha, kukusomesha hutosahau na kukusahilishia njia ya wepesi, basi waidhisha ikiwa utafaa (huo) waadhi.

Imeshartiwa kuwa waadhi uwe wenye kunufaisha. Na hilo ni sharti juu ya uhakika wake. Kwani ikiwa waadhi hautanufaisha basi itakuwa ni upuuzi, naye Mwenyezi Mungu ametakata na kuamrisha upuuzi. Kwa hiyo kumwadhia mwenye kumcha Mwenyezi Mungu kwanza kunafahamisha kupondokea haki na hayo ndio manufaa yake (huo waadhi), vile vile kuwaidhika kama alivyosema: "Atawaidhika anayemcha (Mungu). Na kumwaidhia muovu ambaye haogopi katika moyo wake, kwanza kunafahamisha kutimia hoja juu yake na ndio manufaa yake (huo waadhi) na kunalazimisha kuejiepusha kwake, na kuikataa kwake haki kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na atajiepusha nayo muovu". Waadhi baada wa waadhi haunufaishi na chochote kwa hiyo kukaamriwa kuachana naye. Mwenyezi Mungu amesema: "Basi jiepushe na wale wanaoupa mgongo ukumbusho wetu huu na wala hawataki ila maisha ya dunia ." (53:29)

Imesemekana kuwa sharti ni sharti la kisura tu! Sio la kihakika, kwamba ni kutolea habari kuwa waadhi ni wenye kunufaisha katika kuzidisha twaa na kukoma na maasi, kama inavyosemwa: Muulize inafaa kumuuliza, kwa hiyo ndio baadhi yao wakasema: "Herufi In katika aya ni kwa maana ya (Qad) hakika". Na imesemwa kuwa maneno ni ya mkato kwa kuondoa maneno mengine, kukadiria kwake ni "Basi waidhisha ikiwa utafaa waadhi na hata ukitofaa". Hilo ni kwamba yeye Mtume(s.a.w.w) amepelekwa kwa waadhi na kuonya. Kwa hiyo ni juu yake kuonya na kutoa waadhi uwe una manufaa au usiwe na manufaa; Kwa hiyo aya inaelekeana na aya inayosema: "Na amewafanyia kanzu zinazowakinga na joto (na baridi) ". (16:81).

Imesemwa kuna ishara ya kuweka mbali manufaa ya hawa wenye kutajwa; Ni kama vile imesemwa: Fanya unayoamrishwa hata kama hayatanufaisha.

Aya Na 10

Yaani atawaidhika na Qur'an yule ambaye moyoni mwake mna kitu cha kumwogopa Mwenyezi Mungu na kuogopa mateso yake.

Aya Na 11

Dhamiri ni ya mawaidha. Makusudio ya neno Ashqa kwa kulinganisha na aya iliyotangulia, ni yule asiyemwogopa Mwenyezi Mungu.

Aya Na 12

Mto mkubwa ni moto wa Jahanam, ni mkubwa kulinganisha na wa dunia. Imesemwa makusudio yake ni daraja ya chini ya Jahanam ambayo ina adhabu kali zaidi.

Aya Na 13

Makusudio ya kutokufa wala kuwa hai, ni kutookoka kabisa kwa maana ya kuwa adhabu haitakwisha wala maisha hayatabadilika kuwa mazuri. Kwa hiyo makusudio ya uhai ni maisha mema; kama alivyosema katika Ardhi; "Si hai wakutarajiwa wala si maiti wakusahauliwa".

Aya Na 14 -15

Makusudio ya kujitakasa hapa, ni kujitakasa na uchafu wenye kufungamana na dunia kwa dalili ya kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Lakini nyinyi mnapendelea zaidi uhai wa kilimwengu." Kurejea kwa Mwenyezi Mungu kwa kumuelekea yeye Mwenyezi Mungu ni kujitakasa. Kutoa katika njia ya Mwenyezi Mungu ni kujitakasa na uchafu unaofungamna na mali. Hata udhu wa swala ni mfano wa kujitakasa na yale yaliyochumwa na nyuso, mikono na miguu. Kusema kwake: Akalikumbuka jina la Mola wake akaswali, makusudio yake kwa dhahiri ni kumtaja Mwenyezi Mungu kwa kutamka, na kuswali ni swala ya kawaida ya Kiislamu. Aya mbili hizi kwa dhahiri ufahamisho wake ni kuenea a kila kitu, lakini imepokewa kutoka kwa Maimamu wa Ahlul Bait(a.s) kuwa aya hizo zinahusu zaka ya fitri na swala ya Idd. Vile vile hayo yamepokewa katika Ahli Sunnah.

Aya Na 16

Msemo huo unaelekezwa kwa watu juu ya tabia yao ya kiutu inayopelekea kufungamana kabisa na dunia na kujishughulisha na kuiamirisha. Imesemwa kuwa msemo unawaelekea makafiri tu. Kwa hali yoyote maneno ni yenye kuelekezwa kwenye lawama.

Aya Na 17

Imehisabiwa akhera ni yenye kubakia kulinganisha na dunia, pamoja na kuwa yenyewe akhera ni yenye kubaki milele, kwa sababu ya kupima kati ya dunia na akhera.

Aya Na 18-19

Neno haya "Linaonyesha yale yaliyobainishwa kuanzia aya 14 mpaka 17. Imesemwa kuwa ni hAya Na kuwa akhera ni bora na ni yenye kubaki. Imesemwa kuwa kusema vitabu vya kwanza tu. Kisha kuvibainisha kuwa ni vitabu vya Ibrahim na Musa ni kwa ajili ya kutukuza na kukuza jambo.

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Iyashi kutoka kwa Uqba bin Amir El-Jahaniy amesema iliposhuka aya inayosema: "Litakase jina la Mola wako aliye mkuu" Mtume(s.a.w.w) alisema ifanyeni katika kurukui kwenu. Na iliposhuka "Litakase jina la Mola wako aliye Mtukufu akasema": Ifanyeni katika kusujudi kwenu. Hadith hiyo pia imepokewa katika Durril Manthur kutoka kwa Ahmad, Abu Dawud, Ibn Maja Ibn El-Mundhir na Ibn Murdawayh nao wamepokea kutoka ka Uqba naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu Aya Na kwanza amesema: "utakata ni kwa Mola wangu aliye Mtukufu". Kuhusu na ambaye ameumba akakamilisha na ambaye makadirio ya mwanzo kisha akaviongoza.

Katika Durril Manthur ametoa Ibn Murdawayh kutoka kwa Ibn Abbas amesema: "Mtume(s.a.w.w) alikuwa anajikumbusha Qur'an kwa kuhofia kusahau akaambiwa tumekutoshea na hilo", na ikashuka aya Tutakusomesha wala hutasahau. Katika Faqih aliulizwa Imam As Sadiq(a.s) kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) "Hakika amefaulu mwenye kuitakasa " Akasema: "Ni mwenye kutoa zaka ya fitr". Akaulizwa: na akamkumbuka Mola wake, akaswali? Akasema ni aliyetoa uwanjani akaswali. Amepokea hadith kwa maana hii Hammad, naye kutoka kwa Jarir naye kutoka kwa Abu Baswir na Zurarah kutoka kwake Imam Jaffar As Sadiq(a.s) . Katika Durril Manthur ametoa Ibn Murdawayh kutoka kwa Abu Said Al-Khudri amesema: Mtume(s.a.w.w) alikuwa akisema: "Hakika amefaulu mwenye kujitakasa na akamkumbuka Mola wake akaswali " Kisha hugawanya zaka ya fitr kabla ya kwenda kwenye mswala siku ya Idd-ul-fitr.

Vile vile kumepokewa kushuka aya mbili hizo katika zaka ya fitri na swala ya Idd kwa njia mbili kutoka kwa Abu Said, vile vile kwa njia mbili kutoka kwa Ibn Umar kwa njia moja kutoka kwa Naila bin Al-Asqa, kwa njia mbili kutoka kwa Abu Aliya na kwa njia moja kutoka kwa Atau. Vile vile kwa njia moja kutoka kwa Muhammad bin Sirin, kwa njia moja kutoka kwa Ibrahim Annakhyi na kutoka kwa Amru bin Awf naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Katika Khiswali imepokewa kutoka kwa Utbah bin Amru Allaythi naye kutoka kwa Abu Dharr katika hadith inayosema: "Nilimuuliza Mtume(s.a.w.w) ni kitu gani katika dunia alichokuteremshia Mwenyezi Mungu kilichokuwa katika vitabu vya Ibrahim na Musa? Akasema, Ewe Abu Dharr, soma: hakika amefaulu mwenye kujitakasa akalikumbuka jina la Mola wake akaswali. Lakini nyinyi mnapendelea zaidi uhai wa kilimwengu. Hali akhera ni bora na yenye kubaki. Hakika hayo yamo katika vitabu vya kwanza vitabu vya Ibrahim na Musa. Hadithi inatilia nguvu kuwa ishara na neno "haya" ni mkusanyiko wa aya nne kama ilivyotangulia. Katika Baswir kwa isnadi yake kutoka kwa Abu Baswir amesema Abu Abdillah: Tunazo suhuf alizozitaja Mwenyezi Mungu katika Aya Na 19: Nikamwambia ni mbao? Akasema ndio. Amepokea vile vile kwa njia nyengine Abu Baswir kutoka kwake Abu Abdillah(a.s) . Kwa dhahiri ni kwamba makusudio ya kuwa Suhuf ni mbao nikuwa ni Taurat yenye kuelezewa katika Qur'an kama mbao; kama alivyosema Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Na ukamwandikia katika mbao kila kitu ." (7:145).

Na pia kusema kwake Mwenyezi Mungu:'na akazitupa mbao .." (7:150). Na kusema kwake "aliziokota zile mbao " (7:154).

Katika Majmau imepokewa kwa Abu Dharr, yeye amesema: "Nilimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu ni Mitume wangapi? Akasema: Ni laki moja na ishirini na nne elfu (124,000) nikamuuliza ni wangapi walio Mursaal katika wao? Akasema mia tatu na kumi na tatu (313). Nikasema Adam alikuwa Mtume. Akasema ndio Mwenyezi Mungu alimsemesha na amemuumba kwa mkono wake. Ewe Abu Dharr, Mitume waarabu ni Hud, Saleh, Shuayb na Mtume wako.

Nikasema tena: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu ameteremsha vitabu vingapi? Akasema mia moja na nne (104). Kwa Adam mbao kumi, kwa Shiyth hamsini kwa Ukhnun ambaye ni Idris thelathini naye ndiye wa kwanza kuandika kwa kalamu, Ibrahim kumi na Taurat, Injil, Zabur na Qur'an. Yamepokewa hayo katika Durril Manthur kutoka kwa Abd bin Hamid, Ibn Murdawayh na Ibn Asakir nao kutoka kwa Abu Dharr isipokuwa hazikutajwa mbao za Adam na zimetajwa mbao kumi za Musa kabla ya Taurat.

13

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA GHASHIYA (KIYAMA) (NA. 88)

INA AYA 26

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwnye kurehemu

هَلْ أَتَاكَ حَدِيثُ الْغَاشِيَةِ ﴿١﴾

1. Je, imekujia habari ya Kiyama?

وُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ خَاشِعَةٌ ﴿٢﴾

2. Nyuso siku hiyo zitadhalilika.

عَامِلَةٌ نَّاصِبَةٌ ﴿٣﴾

3. Zitatumika na kutaabika.

تَصْلَىٰ نَارًا حَامِيَةً ﴿٤﴾

4. Zitaingia katika moto mkali.

تُسْقَىٰ مِنْ عَيْنٍ آنِيَةٍ ﴿٥﴾

5. Zitanyweshwa maji ya chemshemi ichemkayo.

لَّيْسَ لَهُمْ طَعَامٌ إِلَّا مِن ضَرِيعٍ ﴿٦﴾

6. Hawatakuwa na chakula isipokuwa cha miba.

لَّا يُسْمِنُ وَلَا يُغْنِي مِن جُوعٍ ﴿٧﴾

7. Hakinenepeshi wala hakiondoi njaa.

وُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ نَّاعِمَةٌ ﴿٨﴾

8. Nyuso siku hiyo zitanawiri.

لِّسَعْيِهَا رَاضِيَةٌ ﴿٩﴾

9. Zitakuwa radhi kwa amali yake.

فِي جَنَّةٍ عَالِيَةٍ ﴿١٠﴾

10. (Zitakuwa) katika pepo iliyo tukufu.

لَّا تَسْمَعُ فِيهَا لَاغِيَةً ﴿١١﴾

11. Hazitasikia humo upuuzi.

فِيهَا عَيْنٌ جَارِيَةٌ ﴿١٢﴾

12. Humo mna chemichemi inayotiririka.

فِيهَا سُرُرٌ مَّرْفُوعَةٌ ﴿١٣﴾

13. Mna malili yaliyotukuzwa.

وَأَكْوَابٌ مَّوْضُوعَةٌ ﴿١٤﴾

14. Na vikombe vilivyowekwa.

وَنَمَارِقُ مَصْفُوفَةٌ ﴿١٥﴾

15. Na mito iliyopangwa.

وَزَرَابِيُّ مَبْثُوثَةٌ ﴿١٦﴾

16. Na mazulia yaliyotandikwa.

أَفَلَا يَنظُرُونَ إِلَى الْإِبِلِ كَيْفَ خُلِقَتْ ﴿١٧﴾

17. Je, hawamtazami ngamia namna gani alivyoumbwa.

وَإِلَى السَّمَاءِ كَيْفَ رُفِعَتْ ﴿١٨﴾

18. Na mbingu namna gani zilivyoinuliwa?

وَإِلَى الْجِبَالِ كَيْفَ نُصِبَتْ ﴿١٩﴾

19. Na majabali namna gani yalivyo simamishwa.

وَإِلَى الْأَرْضِ كَيْفَ سُطِحَتْ ﴿٢٠﴾

20. Na ardhi namna gani ilivyotandikwa.

فَذَكِّرْ إِنَّمَا أَنتَ مُذَكِّرٌ ﴿٢١﴾

21. Basi kumbusha, hakika wewe ni mkubushaji tu!

لَّسْتَ عَلَيْهِم بِمُصَيْطِرٍ ﴿٢٢﴾

22. Wewe si mtenza nguvu.

إِلَّا مَن تَوَلَّىٰ وَكَفَرَ ﴿٢٣﴾

23. Lakini mwenye kupa mgongo akakufuru.

فَيُعَذِّبُهُ اللَّـهُ الْعَذَابَ الْأَكْبَرَ ﴿٢٤﴾

24. Allah atamwadhibu adhabu kubwa mno!

إِنَّ إِلَيْنَا إِيَابَهُمْ ﴿٢٥﴾

25. Hakika ni kwetu sisi marejeo yao.

ثُمَّ إِنَّ عَلَيْنَا حِسَابَهُم ﴿٢٦﴾

26. Kisha ni juu yetu sisi hesabu yao.

UBAINIFU

Ni Sura ya maonyo na biashara. Inasifu Kiyama kwa hali ambayo watu watakuwa nayo ya kugawanyika makundi mawili: Wema na waovu, na kutua kwao katika sehemu walizoandaliwa miongoni mwa pepo na moto. Inamalizia kwa kumwamrisha Mtume(s.a.w.w) kuwakumbusha watu fani za mazingatio ya Mungu katika ulimwengu zenye kufahamisha juu ya uungu wake, na kurudi kwao kwake kwa ajili ya kuhisabiwa. Sura imeshuka Makka kwa ushahidi wa mpangilio wa aya zake.

Aya Na 1

Ni swali linalopelekea kukuza mambo. Limetumiwa neno kufudikiza (Ghashiya) kwa maana ya Kiyama, kwa sababu kitawafudikiza watu na kitawazingira kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na tutawafufua wala hatutamwacha hata mmoja katika wao ." (18:47). Au kimeitwa hivyo kwa kuwa kitafudikiza nyuso za makafiri kwa adhabu.

Aya Na 2

Yaani nyuso ni zenye kudhalilika kwa ghamu na adhabu itayozifunika. Kudhalilika kutawapata wenye nyuso, lakini hapa kumenasabishwa kwenye nyuso, kwa sababu kunadhihiri katika uso.

Aya Na 3

Makusudio yake kwa kulinganisha na aya inayokabiliana nayo katika sifa ya watu wa peponi inayosema "Zitakuwa radhi kwa mali yake" ni kuwa kutumika kwake ni katika dunia na kutaabika kwake ni katika akhera. Hakika mtu anafanya anayoyafanya katika dunia ili atengenekewe, na apate matakwa, lakini amali zao ni bure tu; Hazitawafaa na chochote, kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na tutayaendea yale waliyoyatenda katika amali tuyafanye kama mavumbi yaliyitawanywa ". (25:23).

Kwa hiyo hakirudi chochote katika waliyoyafanya isipokuwa taabu, kinyume cha watu wa peponi, kwani hakika wao mahangaiko yao waliyohangaika katika dunia ni kibali kitakachowapeleka katika pepo siku ya Kiyama. Imesemwa makusudio yake ni kutumika katika dunia kwa maasi na kutaabika katika moto siku ya Kiyama.

Aya Na 4

Yaani ni moto katika ukomo ya joto.

Aya Na 5

Yaani ni yenye joto kali.

Aya Na 6

Dhwarii ni aina ya miba ambayo watu wa Hijazi wanaita hivyo inapokauka. Na chakula kibaya sana, hawawalishi hata wanyama wao. Huenda hiyo ya motoni imeitwa hivyo, kwa kufanana.

Aya Na 7

Kunawiri ni fumbo la furaha inayodhihiri usoni kama ilivyosemwa: "utaona katika nyuso zao mng'ao wa kunawiri ." (83:24). Au itakuwa kwa maana ya kuneemeka. Imesemwa haikuwekwa herufi za kuunganisha kwa kuonyesha ubainifu kamili kati ya hali za makundi mawili.

Aya Na 8

Makusudio ya amali njema yaani imeridhia amali yake njema kwa kulipwa malipo mema.

Aya Na 9-16

Ni utukufu wa daraja yake, kwani katika hiyo pepo kuna maisha yasiyokuwa na kifo, ladha isiyokuwa na machungu yoyote, na furaha isiyokuwa na huzuni. Kusema kwake "Hazitasikia humo upuuzi" yaani hizo nyuso hazitasikia tamko lolote lisilokuwa na faida. Kuhusu chemchemi makusudio yake ni jinsi yake, na amezihesabu Mwenyezi Mungu chemchemi katika hiyo pepo katika maneno kama Salsabil Kinywaji kitakatifu nk.

Aya Na 17

Baada ya kumaliza kukisifu Kiyama na kubainisha hali za makundi mawili wa waumini na makafiri, amefuatishia kuishiria kijumla mipangilio mizuri ya Mungu ambayo inabainisha uungu wake, inayohukumilia kumwabudu kwake, na hilo likafuatiwa na hisabu ya matendo na malipo ya muumin kwa imani yake na kafiri kwa kufuru yake. Wakati wake hayo ni siku ya Kiyama. Kwanza amewaambia kuangalia ngamia vile alivyoumbwa. Vipi alivyoitia sura Mwenyezi Mungu ardhi isiyokuwa na uhai wala hisia, kwa Sura hii ya ajabu katika viungo vyake, nguvu zake na vitendo vyake. Akaitiisha kwao ili wanufaike nayo kwa kuipanda, uchukuzi, nyama yake, maziwa yake, ngozi yake na sufu yake. Na hata mkojo wake na kinyesi chake. Je, yote hAya Na mezuka tu kwa bahati bila ya kupangwa? Kuhusisha kutaja ngamia ni kwa njia kuwa Sura imeshuka Makka na ngamia alikuwa ndio nguzo ya maisha ya waarabu.

Aya Na 18

Imepambwa hiyo mbingu kwa jua, mwezi na sayari nyenginezo kwa manufaa ya watu wa dunia; na amejaalia hewa ambayo wanalazimika wanyama kuivuta.

Aya Na 19

Majabali ndio vigingi vya ardhi vinavyoizuia ardhi isitetemeke na hazina ya maji ambapo mito na chemchem hububujika kutoka huko na ni hifadhi za madini.

Aya Na 20

Yaani imatendikwa ili mwanadamu aweze kukaa na kumsahilikia kuguru hapa na pale na matumizi mengine ya kiufundi. Basi mipangilio yote hii imetegemezwa kwa Mwenyezi Mungu bila ya wasiwasi wowote. Yeye ni Mola wa mbingu ardhi na vilivyo ndani yake. Yeye ni Bwana wa ulimwengu wa kibinadamu, niwajibu kwao kumfanya ndiye Mola, kumpwekesha na kumwabudu na mbele yao kuna Kiyama ndiyo siku ya hesabu ya malipo.

Aya Na 21

Ni sehemu ya yaliotangulia maana yake ikiwa Mwenyezi Mungu ndiye Mola na hakuna Mola asiyekuwa yeye na mbele yao kuna siku ya hesabu na malipo kwa aliyeamini katika wao au aliyekufuru, basi wakumbushe hilo. Kusema kwake "Hakika wewe ni mkumbushaji tu " ni ubainifu wa kuwa kazi ya Mtume ni kukumbusha tu kwa kutarajia kuitikiwa na kuaminiwa bila ya kulazimisha.

Aya Na 22

Ni ubainifu na tafsiri ya aya iliyotangulia.

Aya Na 23

Hapo anavuliwa na ukumbusho yule mwenye kupa mgongo na kukufuru. Ilivyo ni kuwa kukanusha kumekuja baada ya ukumbusho; kukanusha kwa kuvua, ni ukumbusho baada ya ukumbusho. Ni kama vile imesemwa wakumbushe na udumishe ukumbusho isipokuwa yule ambaye umemkumbusha akapa mgongo na kukufuru. Kwa hiyo huna haja ya kudumisha kumkumbusha bali achana naye. Mwenyezi Mungu atamwadhibu adhabu kubwa. Aya Na 21 - 24 katika Sura hii zinalingana na Aya Na 9 -12 ya Sura ya Al-A'laa (87). Imesemekana kuwa sio kuvuliwa na ukumbusho bali nikuvuliwa kutenza nguvu, na maana ni wewe simtenza nguvu isipokuwa juu ya yule mwenye kupa mgongo akakufuru ndio Mwenyezi Mungu anakusaliti naye na kukuamrisha kufanya jihadi; utapigana naye na kumuua. Na imesemwa kuvua hapa ni kwa kukataa tu, Kwa maana; wewe si mtenza nguvu, lakini mwenye kupa mgongo akakufuru katika wao hataachwa bure. Atamwadhibu Mwenyezi Mungu adhabu kubwa. Tuliyoyatanguliza kuyataja yako karibu na yenye nguvu zaidi.

Aya Na 24-25

Imetangulizwa "ni kwetu sisi" kwa sababu ya kutilia mkazo. Na aya hiyo iko katika mahali pa illa (sababu) ya kuadhibu kulikotajwa katika aya iliyotangulia.

Utafiti Wa Hadith Katika Majmau imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) Dhwarii ni kitu katika moto kinafanana na mwiba kichungu kuliko shubiri. Kinanuka uvundo kuliko mzoga na ni kikali kuliko moto. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kwake Mwenyezi Mungu "Hawatasikia humo upuzi" ni upuuzi na uwongo." Kuhusu Aya Na 22 amesema yaani sio mwenye kuwachunga. Katika Durril Manthur ametoa Ibn Jariyr, Hakim, Ibn Murdawayh na Bayhaqi kutoka kwa Jabir amesema: 'Amesema Mtume(s.a.w.w) : "Nimeamrishwa kupigana na watu mpaka waseme: "La ilaha illa llahu" wakisema, damu yao na mali zao zitakuwa zimesalimika isipokuwa kwa haki yake, na hisabu yao iko juu ya Mwenyezi Mungu, kisha akasoma aya "Basi kumbusha hakika wewe ni mkumbushaji wewe si mtenza nguvu ". Hakuna dalili yoyote kwamba kuvua kunatokana na dhamiri ya wao na hilo ni dhahiri.

Katika hiyo Durril Manthur katika hadith iliyopokewa kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Lakini mwenye kupa mgongo na akakufuru" anakusudia yule asiyewaidhika, na asiyesadiki akakanusha uungu na akakufuru neema. "Atamwadhibu Allah adhabu kubwa mno!" anakusudia adhabu nzito ya milele. "Hakika ni kwetu sisi marejeo yao" anakusudia mwisho wao "kisha hakika ni juu yetu sisi hesabu yao" anakusudia malipo yao. Katika Nahj aliulizwa Ali(a.s) vipi atawahisabu Mwenyezi Mungu watu na wingi wao huo? Akasema: Kama vile anvyowaruzuku na wingi wao. Kukaulizwa vipi atawahisabu na hawamuoni? Akasema kama anavyowaruzuku na hawamwoni.

Katika hiyo hiyo Nahj amesema As Sadiq, kila Umma utahisabiwa na Imam wa zama zake. Na wanawajua maimam marafiki zao na maadui zao kwa alama zao na ndio maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na juu ya mahali hapo palipoinuka watakuaweko watu hao watakaowafahamu wote kwa alama zao ". (7:46). Imepokewa hadith kwa maana haya katika Baswir kutoka kwa Sadiq, katika Kafi kutoka kwa Baqir na Kadhim(a.s) na katika Faqih kutoka kwa Hadi(a.s) .


9

10

11

12

13

14

15

16